Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 38 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 7 2021-05-27

Name

Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Primary Question

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kumwuliza Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo unafahamu mwaka huu nchi yetu ilivamiwa na nzige wa jangwani na ikanipelekea kupenda kufahamu mkakati wa Serikali katika kupambana au kudhibiti majanga yanayoweza kuathiri usalama wa chakula na mazao mengine ya kiuchumi katika nchi yetu ikiwemo mifugo. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Kiruswa, Mbunge wa Longido, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anataka kujua mkakati wa Serikali wa namna ya kukabiliana na majanga. Amezungumzia chakula, lakini majanga yapo mengi. Mkakati huo upo ndani ya Serikali, pale ambapo Ofisi ya Waziri Mkuu kimeanzishwa Kitengo cha Maafa. Kitengo hiki ambacho kipo Ofisi ya Waziri Mkuu, tumekishusha pia kipo ngazi ya Mkoa, kiko Kamati ya Maafa; ngazi ya Wilaya tuna Kamati ya Maafa na pia ngazi ya Tarafa ina Kamati ya Maafa.

Mheshimiwa Spika, wajibu wetu ni kuhakikisha kwamba tunaepusha utokeaji wa majanga haya. Wakati mwingine huwezi kuyaepusha, ila ni kushughulikia majanga haya yanapojitokeza. Kwa hiyo, eneo la chakula nako pia linapotokea janga ambalo linapoteza vyakula ambavyo wananchi walikuwa wanavitegemea, nayo pia tunashughulikia.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dkt. Kiruswa atakumbuka siku za hivi karibuni kule Longido na maeneo mengine tulivamiwa na nzige, nami niliwenda pale, nikaenda mpaka Monduli kwenda kuona hali ya nzige. Ndiyo majanga hayo, wadudu wamekuja kutoka huko, wameruka wanakuja kushambulia chakula, lakini tulikabiliana nao kabla hawajaanza kushughulikia chakula chetu. Kwa hiyo, hiyo ndiyo njia mojawapo ambayo tunaitumia kukabiliana na majanga. Tulienda kuwakabili kabla hawajaanza kula chakula chetu na tukamudu kuwapoteza wote.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumeimarisha kitengo hiki kwa kuweka vifaa, watalaam na pia pamoja na utaalam huo tumeendelea kushusha elimu hii kwa wananchi wenyewe waanze kushughulikia majanga pindi tu inapotokea majanga haya. Vile vitengo husika na vyenyewe vikikaa na kuratibu, vinashughulikia, lakini pale wanaposhindwa ngazi ya Kata, wanajulisha Wilaya, janga linapokuwa kubwa zaidi ya ngazi ya Wilaya wanajulisha Mkoa na Mkoa unaposhughulikia janga hilo likionekana limeshindikana, wanajulishwa Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Waziri Mkuu imekuwa ikifanya kazi hiyo vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwahakikishie Watanzania kuwa na uhakika na Serikali yao na kuiamini kwamba pia tumejipanga kwenye eneo hilo la kupambana na majanga mbalimbali ili kuhakikisha kwamba shughuli zote za Watanzania zinaenda vizuri na tuweze kuwa na akiba ya kutosha kwenye chakula na pia usalama wa maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister