Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 38 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2021-05-27

Name

Aida Joseph Khenani

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Nkasi Kaskazini

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi nami niweze kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, miongoni mwa magonjwa sugu ambayo yanakuja kwa kasi ni pamoja na ugonjwa wa Kisukari. Madaktari bingwa wanapatikana kuanzia Hospitali za Mikoa, Kanda pamoja na Taifa kulingana na Sera yetu ya Afya; na wagonjwa hawa wa Kisukari wapo maeneo yote nchini:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujua, kwa kuwa wagonjwa hao wa vijijini, wengi wanashindwa kujua kwamba wana ugonjwa huo na hawana uwezo wa kutoka vijijini na kwenda mpaka Hospitali ya Mkoa; Serikali ina mkakati gani wa ziada kulingana na uzito wa tatizo hili hivi sasa kuweza kutoa huduma kwenye Hospitali za Wilaya pamoja na ngazi ya Kata?

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida, Mbunge wa Nkasi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nami naungana naye kwamba tunayo magonjwa mengi nchini na ambayo tunaendelea kutafuta tiba sahihi ili Watanzania waendelee kuwa na afya njema zitakazowawezesha kufanya shughuli zao za maendeleo. Ugonjwa wa Kisukari ni miongoni mwa magonjwa ambayo kwa sasa yamesambaa sana nchini. Kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge, ni kweli mengine yapo mpaka kwenye Vitongoji.

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu imepanua wigo wa utoaji huduma za afya. Wigo huu umeanzia kwenye ngazi ya huko huko vijijini ambapo kuna zahanati. Vile vile katika ngazi ya Kata kama rufaa ya zahanati, tuna vituo vya afya vinavyotoa huduma nzuri sana sasa hivi na tumejenga vituo vya afya vingi sana na tunaendelea kuvijenga. Pia tuna Hospitali za Wilaya, Mkoa na Rufaa mpaka zile za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ugonjwa wa Kisukari ni miongoni mwa magonjwa ambayo sasa tunatoa huduma mpaka kule kwenye zahanati. Kwenye Sera yetu imeelekeza zahanati na zenyewe zinunue madawa ya Kisukari ili wawe wanapata huduma kule. Pale ambapo anaweza kupimwa kwenye Hospitali ya Kata ambayo ipo kwenye maeneo hayo hayo, lakini upatikanaji wa dawa sasa unakwenda mpaka kwenye zahanati.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni jukumu la zahanati na nataka niagize Halmashauri ambazo ndiyo zinasimamia zahanati kuhakikisha kwamba wanaagiza dawa za Kisukari na ziende katika zahanati, kwenye kituo cha afya na kwenye kila ngazi ya kutoa huduma ili wale Watanzania walioko kule kijijini kabisa wapate huduma hiyo bila usumbufu wa kusafiri na kulipa nauli kwenda mahali pengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kupitia Mheshimiwa Aida, nikuhakikishie kwamba Serikali tumejipanga vizuri kwenye sekta ya utoaji huduma kwenye ngazi zote na bado tunaendelea na maboresho ya utoaji huduma kwa magonjwa yote. Mkakati wetu sasa ni kuhakikisha tunapunguza ukali wa magonjwa haya ili Watanzania wawe na afya njema na kila Mtanzania afanye kazi yake vizuri. Tunataka tuone tija ikipatikana kwa Watanzania kuwa na fya njema.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister