Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 7 2021-09-02

Name

Abubakar Damian Asenga

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kilombero

Primary Question

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nami naomba kumwuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba kumekuwa na ucheleweshwaji mkubwa sana wa vitambulisho vya Taifa kwa baadhi ya maeneo ya nchi yetu; na jambo hili limekuwa likitokana na kutokuwepo na mtiririko mzuri unaoridhisha wa taarifa za wananchi:-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuunganisha Taasisi ya Serikali ya RITA, NIDA na labda Uhamiaji kidigitali ili mtoto anapozaliwa taarifa zake zianze kutunzwa na kupatiwa kitambulisho kimoja cha Taifa kitakachotumika kama cha kuzaliwa na cha Taifa? Ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abubakari, Mbunge wa Kilombero, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza ameeleza usumbufu wa upatikanaji wa Vitambulisho vya Taifa na pia ametaka kujua kama je, tunaweza kuunganisha NIDA na RITA au Uhamiaji ili kurahisisha kuwa na chombo kimoja chenye taarifa zote?

Mheshimiwa Spika, hivi vyombo vyote vina majukumu tofauti. NIDA wanatoa Kitambulisho cha Taifa ambacho ndiyo kinachomtambulisha Mtanzania kuwa huyu ni Mtanzania. Kitambulisho hiki hakitolewi kwa yeyote ambaye sio Mtanzania. Suala la Kitambulisho hiki cha Utanzania kinaangalia mambo mengi sana hasa maslahi ya Mtanzania.

Mheshimiwa Spika, RITA ni chombo kinachotoa cheti cha kuzaliwa kwamba wewe umezaliwa tarehe na eneo fulani. RITA hiyo hiyo kazi yake ni kusajili vifo. Unaweza kuzaliwa leo; wale wana utaratibu wa kuweka takwimu za waliozaliwa Tanzania, lakini pia wanatoa na vyeti vya vifo kama mtu akifariki. Kama ulisajiliwa kuzaliwa na huku umepata cheti cha kifo, maana yake wanaondoa ile, maana yake unakuwa haupo kwenye takwimu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, chombo hiki cha RITA kinaweza kutoa vitambulisho cha kuzaliwa hata kama siyo Mtanzania. Hilo nalo pia lijulikane kwamba RITA inaweza kutoa vitambulisho kwa yoyote anayezaliwa Tanzania hata kama sio Mtanzania, lakini Kitambulisho cha Taifa, hiki ni kwa ajili ya Mtanzania tu. Kwa hiyo, hayo ndiyo majukumu tofauti.

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Uhamiaji ni katika kutoa vibali vya kuingia na kutoka nchini na majukumu kadhaa ambayo wamepewa. Sasa kuunganisha kwa wakati mmoja, yapo maeneo huwezi kuunganisha kama ambavyo tunafikiria, lakini wanaweza kupeana taarifa pale ambapo chombo kimoja kinahitaji taarifa upande wa pili. Hiyo inawezekana pia. Kwa hiyo, vyombo hivi viwili vinafanya kazi kwa utaratibu huo.

Mheshimiwa Spika, usumbufu ambao unazungumzwa hapa, nilipokuwa nafanya ziara hasa kwenye Mikoa ya pembezoni; nimefanya ziara Mkoani Kagera, Kigoma na Mtwara. Mikoa yote hii inapakana na nchi jirani na tumeanza kuona pia wimbi la wenzetu kutoka jirani kupenda kuishi Tanzania na wangependa kupata Kitambulisho cha Taifa.

Mheshimiwa Spika, haiwezekani kwa sababu wao sio Watanzania, lakini akiwa hapa hata kama ameingia kwa kutoroka na amekaa hapa na mke wake ana miezi, miaka akazaa mtoto, kitambulisho cha kuzaliwa anachokipata kwenye hospitali zetu pale alipozalia, siyo cha Utaifa. Kitambulisho cha NIDA ni cha Utaifa zaidi kuliko kuzaliwa. Kwa hiyo, huo ndiyo utofauti wa vyombo hivi.

Mheshimiwa Spika, sasa kwenye mikoa hii niliyopita, upo urasimu unazungumzwa kwamba wanachelewa sana kutoa vitambulisho vya NIDA. Ni kweli kwa sababu utoaji wa Kitambulisho cha Utaifa, hii inajikita zaidi kwenye usalama wa nchi. Huwezi kumtambua yeyote anayekuja hapa nchini bila kujiridhisha kwamba ni Mtanzania ukampa Kitambulisho cha Utaifa bila kujua kama yeye ni Mtanzania au la.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kuchelewa kwetu kwenye mikoa ya pembezoni ambako kunaitwa kama urasimu, sisi tumeweka utaratibu mzuri wa kufanya questionnaire au maswali yanayoweza kubainisha kama huyu ni Mtanzania au sio Mtanzania? Kwa hiyo, lazima kutakuwa kuna kuchelewa kidogo. Kama kuna urasimu, ni wa aina hiyo, wa kujiridhisha kama je, huyu aliyeomba ni Mtanzania au ni mtu kutoka nje? Maamuzi yafanyike. Kwa hiyo, huo siyo urasimu, bali ni kuhakiki kwa kina ili cheti cha NIDA kitolewe kwa Watanzania tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimepata nafasi ya kuwaeleza wananchi kwenye maeneo hayo na kuwataka wafanye Subira. Acha chombo chetu cha NIDA kijiridhishe kama huyu ni Mtanzania au la. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie tu kwamba yeyote Mtanzania mwenye baba na mama Mtanzania atappata Kitambulisho cha Utanzania. Kwa hiyo, nao waendelee kuwa na subira ili wataalam wetu wajiridhishe. Huku tumejaribu kurahisisha kidogo, tumeongeza mitambo ya uchapishaji wa vitambulisho, tumeongeza pia mfumo wa vitambulisho kufika mpaka vijijini, tumeongeza idadi ya wafanyakazi kwenye NIDA ili kurahisisha upatikanaji hasa wale ambao tayari wamehakikiwa na wanapaswa kupata kitambulisho. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister