Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2021-09-02

Name

Sophia Hebron Mwakagenda

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nami nimepata nafasi ya kuuliza swali.

Mheshimiwa Spika, maeneo makubwa sana hasa yaliyomilikiwa na makanisa zaidi ya miaka 50 walishindwa kuyaendeleza na wananchi wakaingia kufanya shughuli za kilimo. Kwa sasa wameanza kuwaondoa wananchi hao ambao wamelima zaidi ya miaka 50. Serikali itasaidia nini wananchi hawa waweze japo basi kugaiwa kidogo waweze kuendeleza shughuli zao za kilimo maana kwa miaka mingi wamekuwa wakiishi mahali hapo? Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Unaweza ukatoa mfano?

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ndiyo. Pia Waziri Mkuu alifika eneo la Ilolo Katika Kata ya Kiwira, Wilaya ya Rungwe, Mkoa wa Mbeya, anafahamu tulilizungumzia suala hilo.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakagenda, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, upo ukweli kwamba taasisi zetu za kidini nyingi ziliweza kumudu kuchukua maeneo makubwa sana kwa ajili ya kujenga nyumba zetu za ibada kwenye maeneo hayo. Maeneo kama haya wamemudu kujenga eneo dogo na maeneo makubwa yamebaki, tukiwa tunazungukwa na vijiji na wananchi wanahitaji kutumia na maeneo mengi pia wananchi wameingia humo kutumia.

Mheshimiwa Spika, bado hatuwezi kuacha kufuata Kanuni za Ardhi kwamba unapokuwa na ardhi lazima upate Hati, unapokuwa na Hati unakuwa na kibali cha umiliki wa eneo hilo. Yeyote ambaye atakuja hawezi kupata hati nyingine juu ya hati; na kama atafanya kazi hapo, ajue kwamba eneo hilo siyo lake, bali ni la yule mwenye hati.

Mheshimiwa Spika, mgogoro mkubwa uliokuwepo kwenye maeneo mengi ni huo ukubwa wake na matamanio ya watu kuingia. Mbali ya ziara yangu niliyofanya Mkoani Mbeya Kiwira, lakini nilikuwa Dar es Salaam eneo la Temeke, kuna Kanisa huko la Anglikana, lina eneo kubwa kabisa, Halmashauri wamehangaika kutafuta eneo la kujenga kituo cha mabasi hawana, wameenda.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme, kwanza zipo Taasisi za Kidini zinatambua mahitaji ya ardhi kwa wananchi wanaowazunguka na wanachofanya wanapima uwezo wao hata wa kuendeleza wanawagawia wananchi kidogo kidogo na wanawapa vibali vya muda lakini pia baadaye huko tunaona nia thabiti ya baadhi ya Taasisi za Kidini zikiruhusu wananchi kuwakatia eneo hilo na wapate Hati na kuwaachia kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, yapo maeneo yanamilikiwa bado na taasisi hizo. Wizara ya Ardhi inayo Sera yake ya maeneo haya, namna ya kuishi na hawa watu, lakini kutambua kwamba sasa hivi tuna ongezeko kubwa la wananchi na wanahitaji kupata huduma ya maeneo ya kilimo ili waweze kujikimu.

Mheshimiwa Spika, tunaendelea kufuatilia mwenendo wa sheria zetu, tunaendelea kushauri wale waliochukua maeneo makubwa wapunguze maeneo hayo ili tuwaruhusu wananchi; na kwa busara za viongozi wetu wa kidini, wanakubali, wanatoa maeneo yale na kuwaruhusu wananchi waweze kulima na baadaye pia hata kurasimisha wao waweze kuchukua maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ambacho tunakifanya sasa ni Mamlaka zetu za Mitaa kule Halmashauri, wanakaa na hao ambao wamechukua maeneo makubwa na hayatumiki kwa miaka mingi ili wakubali kuyaachia na jamii iweze kunufaika. Kwa hiyo, tunaendelea kuzungumza nao ili waweze kuachia, lakini pale ambapo tutakuja kuimarisha na kusimamia sheria zetu, tutakuja kuimarisha, lakini kwanza kwa haki yake ya msingi aliyonayo, basi lazima kwanza tushauriane naye ili apunguze maeneo na hiyo inatokea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tutaendelea kuzungumza na wenye maeneo makubwa, hasa Taasisi za Kidini lakini kwa hao wengine ambao waliita ni wawekezaji, tukakubaliana kwamba katika kipindi fulani atakuwa ameshalima, ameendeleza na hajafanya hivyo kwa miaka mingi, hao sasa Mheshimiwa Rais anatumia nafasi yake kuchukua ardhi hiyo na kuwagawia wananchi ili waweze kutumia kwa manufaa yao.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaendelea na busara zote mbili hasa kwenye maeneo ya kidini kuweza kushauriana nao viongozi wa kidini na kwa bahati nzuri wanatuelewa. Kwa hiyo, huo ndiyo utaratibu ambao tunautumia kwa sasa. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister