Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2021-09-02

Name

Deus Clement Sangu

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kwela

Primary Question

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii niulize swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, baadhi ya mikoa hapa nchini hasa Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini wanategemea zao la mahindi kama chanzo kikuu cha mapato. Hata hivyo, kwa miaka mitatu mfululizo zao hili limekumbwa na mdororo wa bei na masoko.

Je, Serikali mmejipanga vipi kuiwezesha Taasisi za Serikali hasa NFRA ili waweze kupunguza mlundikano wa mahindi huko sehemu zenye shida?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Kwela, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mikoa yetu ile saba/nane ya Nyanda za Juu Kusini inazalisha sana zao la mahindi na ndiyo tunalitegemea kwa chakula hapa nchini. Pia mwaka huu, msimu uliopita wamezalisha na ziada; na biashara ya mahindi haijaenda vizuri msimu huu kwa sababu bei imeshuka sana.

Mheshimiwa Spika, pamoja na ruhusa iliyotolewa na Wizara ya Kilimo ya kuruhusu watu watafute masoko popote ndani na nje ya nchi, lakini bado uzalishaji ni mkubwa sana kwa sababu pia hata hizo nchi za jirani nazo zimezalisha pia zao hili.

Mheshimiwa Spika, tulichokifanya ni kuimarisha kuboresha Hifadhi yetu ya Taifa (NFRA) ambapo sasa tumeipa fedha za kwenda kununua angalau kwa bei inayoweza kumkidhi mkulima kujiandaa kwa msimu ujao. Uwezo siyo mkubwa sana lakini tumetoa fedha. Hata juzi wamepewa tena fedha zaidi ya shilingi bilioni 15 ili waende kwenye mikoa ile kwa ajili ya ununuzi huo.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa Mkoani Katavi siku nne zilizopita, hilo nimelisikia na nimeshuhudia mlundikano wa mahindi kule. Nilikutana pia na watu wa NFRA kuona kama je, ununuzi wao pale upo na wananunua kwa kiasi gani? Bado uwezo wa kununua ni mdogo, lakini Serikali itaendelea kuwapa fedha kadiri siku zinavyokwenda ili pia waweze kununua. Pamoja na malalamiko ya wananchi wa Mkoa wa Katavi ambayo waliniambia kwamba kituo cha kununulia kipo mbali, sasa tumeamua angalau tupeleke kwenye kila Halmashauri kituo kimoja ili kiweze kukusanya mahindi kwa ukaribu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hili tutajitahidi. Tunajua Mkoa wa Ruvuma, Njombe, Mbeya, Songwe, Rukwa na Mikoa ya Iringa na sasa Tabora kidogo inazalisha sana. Kwa hiyo, tutajitahidi kukusanya mahindi hayo kupitia NFRA pamoja na Bodi ya Mazao Mchanganyiko ambayo pia tumeipa dhamana ya kununua, nao wanasaga wenyewe kupitia vinu vyao. Kwa hiyo, mashirika yetu haya mawili au taasisi hizi mbili tunazipa fedha halafu zinakwenda kununua.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge, na Waheshimiwa Wabunge wote mnaotoka kwenye mikoa inayozalisha sana zao la mahindi, Serikali inaendelea kuwawezesha NFRA pamoja na Bodi ya Mazao Mchanganyiko kwenda kununua mahindi kwa kiwango hicho. Najua mahindi ni mengi, lakini bado tumefungua milango, yeyote ambaye anaona soko lipo Zambia, Congo, Burundi, Rwanda, Kenya na maeneo mengine kama Malawi na Msumbiji, aende. Bado ruhusa imetolewa ili mradi unaripoti kwamba nina tani hizi, nazipeleka Zambia ili viongozi wa eneo lile waratibu tuweze kujua tumeweza kuingiza fedha kiasi gani za kigeni kwa mazao yetu kupelekwa huko nje?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hiyo ndiyo taarifa ambayo kwa sasa tunayo na Wizara inaendelea na uratibu wa taasisi hizi mbili kununua mahindi kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister