Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2021-09-02

Name

Janejelly Ntate James

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kumekuwa na usumbufu mkubwa katika mafao ya watumishi mara wanapostaafu, kukiambatana na kuchukua muda mrefu. Je, ni nini tamko la Serikali juu ya kuwawezesha hawa wastaafu wetu ambao wamelitumikia Taifa kwa juhudi kupata mafao yao kwa wakati?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la mafao ya wafanyakazi nataka niwahakikishe wafanyakazi tumeendelea kuliratibu ndani ya Serikali kupitia Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii na wote mnatambua tulikuwa na Mifuko mingi ikaleta usumbufu mkubwa sana. Nini tumekifanya? Tumekusanya Mifuko yote ya Hifadhi tumeunda Mfuko mmoja PSSSF ambao upo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, Mfuko huu umeendelea kuratibu kwanza idadi ya wafanyakazi wote waliokuwa wanalipwa na mifuko ile mbalimbali na kuweka utaratibu wa wale waliostaafu ambao walikuwa hawajalipwa kuanza kuwalipa na wale ambao wanastaafu kuendelea kadiri tunavyopata fedha na wale ambao watastaafu siku za karibuni wote wanaratibiwa vizuri ili tuondoe usumbufu uliokuwepo.

Mheshimiwa Spika, nikiri kwamba bado kuna wachache hawajapata mafao yao kwa muda, lakini Serikali inaendelea kulipa wastaafu kadri inavyoweza kupata fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siku za karibuni hapa nilikuwa nazungumza na wafanyakazi wa TALGWU, wa Serikali za Mitaa na hiyo ilikuwa ni moja kati ya jambo ambalo wao walitaka kulijua na mimi niliwahakikishia kwamba Serikali inaendelea na mwezi wa Nne tumelipa zaidi ya bilioni 172 wastaafu na tunaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuwalipa wastaafu. Pia Mfuko huu umerahisisha namna ya wafanyakazi waliostaafu kuufikia; tumefungua Ofisi ya PSSSF kila Mkoa ili wastaafu waweze kufika pale mkoani.

Mheshimiwa Spika, tumeanzisha pia mfumo wa kielekroniki wa mawasiliano kati ya wastaafu na makao makuu. Kwa hiyo, mstaafu huko alipo anaweza kuwasiliana na makao makuu kupata taarifa mbalimbali. Tutaimarisha elimu kwenye hili ili kila anayestaafu aweze kujua na aweze kulipa kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, huo ndio mkakati ambao tunaendelea nao, tunajitahidi sana na narudia tena tunatambua kwamba wapo wastaafu ambao bado hawajafikiwa kulipwa fedha zao, lakini nataka niwahakikishie tutawalipa haki yao. Huo ndio msisitizo ambao tumewasisitiza waajiri watunze kumbukumbu za watumishi wao kutoka wanapowaajiri mpaka wanapomaliza ajira zao.

Mheshimiwa Spika, huu Mfuko tumeendelea kuusimamia hata Waziri wa Nchi wiki moja iliyopita amekaa kikao na wale watumishi wa Mfuko ule kwa kujiridhisha kama je mambo yanaenda sawasawa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaendelea kulipa mafao tunatambua wengine bado hawajalipwa lakini tutawalipa. Kwa hiyo, naomba nitumie nafasi hii kuwahakikishia wastaafu kwamba kila aliyestaafu atalipwa fedha yake ya mizigo kurudi nyumbani na vile vile ile pensheni ambayo ilipaswa kulipwa wakati wote anapokuwa kwenye ustaafu. Hayo ndio malengo ya Serikali. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister