Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 7 2021-02-11

Name

Esther Nicholus Matiko

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, natambua Serikali ina mamlaka ya kutoa ardhi kutoka kwa wananchi kwa ajili ya matumizi mbadala kama vile ya uwekezaji au matumizi mbalimbali kwa taasisi za umma na binafsi kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu. Sheria ya Ardhi ya mwaka 1999, Sheria Na.4 Kifungu cha 3(i) na (g) kinatamka bayana kwamba pale mtwaaji anapochukua ardhi kutoka kwa wananchi lazima ahakikishe amefanya uthamini wa haki na ukamilifu, lakini zaidi ahakikishe analipa fidia kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na haya mazoea ya kufanya uthamini lakini inachukua muda mrefu sana kulipa fidia katika maeneo haya ambayo Watanzania wamechukuliwa ardhi zao, ili waweze kwenda sehemu zingine na kuweza kuanzisha makazi na kufanya shughuli za kijamii na uchumi:-

Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujua, ni nini hatua ya Serikali kuhakikisha kwamba pale tathmini inapofanyika basi hawa wananchi wanalipwa fidia zao kwa wakati ili waweze kwenda kuendelea na shughuli za kiuchumi? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Mkoa wa Mara, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli tunayo Sheria ya Ardhi na imetoa maelekezo kwa watumiaji wote. Kwa sera ya Serikali yetu nchini, ardhi ni mali ya Serikali na ni tofauti sana na maeneo mengine na kila mtumiaji wa ardhi hii ni lazima apate kibali, sisi tunaita hati, ile hati ni kibali cha matumizi ya ardhi ambacho kinaeleza umepewa ardhi hiyo kwa ajili ya nini? Mfano, kujenga nyumba; kiwanda au shamba, kile ni kibali cha Serikali kwa mtumiaji. Huo ndiyo utaratibu ambao tunao na ndiyo maana tunasisitiza kila aliyejenga nyumba, mwenye shamba, anataka kufanya biashara ya kiwanda, lazima apate hati, yaani apate kibali kutoka Serikalini.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ardhi hii ni ya Serikali, inaweza kuwa na mahitaji ya uendelezaji kwenye eneo ambalo tayari watu wapo, wanafanya kazi zao za kilimo yaani wanaendelea na maisha yao ya kawaida. Pale ambapo tunahitaji ardhi hiyo na hapo pana watu wanafanya shughuli zao, ili kuwatoa tunafanya uthamini. Katika zoezi la uthamini ni lazima uende kujua eneo hilo la ukubwa huo ambako mwananchi huyo yupo; kama alipanda mazao; mazao yote yamewekwa bei maalum ya uthamini; lakini pia kama amejenga nyumba, inafanyiwa uthamini na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali inapotaka kufanya jambo hilo, au yeyote anapotaka kutumia eneo hilo ambalo mwananchi yupo, suala la uthamini limezungumzwa pia na limesisitizwa na hili lazima lizingatiwe kwamba mtu anapotolewa eneo moja kupelekwa eneo lingine kwa lengo la kutumia eneo hilo iwe ni kwa uwekezaji au kufanya kazi nyingine, ni lazima uthamini uwepo. Najua yapo matatizo kadhaa katika maeneo mbalimbali, wengine huchukua ardhi bila fidia, wakati mwingine kunaweza kuwa na makubaliano, wakati mwingine wananchi wenyewe wanaamua kutoa ardhi ili shughuli muhimu ifanywe.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge kama analo eneo ambalo kuna malalamiko na yanahitaji wananchi wa eneo hilo kupata haki yao stahiki, bado una fursa ya kuonana na viongozi wa eneo hilo waanze utaratibu wa kwenda kufanya uthaminishaji ili wananchi wote waweze kulipwa fidia yao kulingana na ukubwa wa ardhi na thamani ya mali zilizopo.

Kwa hiyo, hili limesisitizwa na linasimamiwa maeneo yote ili kila mmoja apate haki yake kulingana na ukubwa wa eneo lililoachwa kwa ajili ya shughuli hiyo mpya. Huo ndiyo utaratibu tulionao ndani ya Serikali. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister