Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2021-02-11

Name

Khatib Said Haji

Gender

Male

Party

CUF

Constituent

Konde

Primary Question

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, miongoni mwa ahadi zilizopo katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi na kupitia kauli za Mheshimiwa Rais, ni juu ya uboreshwaji wa maslahi ya wafanyakazi Tanzania. Wafanyakazi wa Tanzania wameendelea kuwa wavumilivu, wastahimilivu na wakijenga matumaini juu ya ahadi hii muhimu sana kwa maisha yao:-

Je, Serikali inatoa kauli gani, ni lini wafanyakazi wa Tanzania watapandishiwa mishahara yao na kuboreshewa maslahi yao? Ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Khatib, Mbunge kutoka Pemba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inayo dhamira na inaendelea na dhamira hiyo ya kuboresha maslahi ya watumishi wa umma. Tunalo eneo la mishahara, upandishaji wa madaraja na maeneo mengine pia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Tano ilipoingia madarakani ilijifunza kwamba wakati wote tunapotangaza hadharani kupandishwa kwa mishahara kumekuwa kunatengeneza gharama kubwa kwenye masoko yetu na kusababisha ugumu wa maisha ya watu wengine. Unajua tunao wafanyakazi, lakini tuna wakulima, wafugaji, wavuvi; hayo ni makundi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa eneo la wafanyakazi peke yake ukitangaza hadharani kwamba tumepandisha mishahara kwenye masoko yetu, vituo vya mabasi na huduma nyingine zote zinapanda lakini wanapandisha hii kwa sababu ya maslahi ya kundi moja tu, tukiwa tuna makundi mengine hatuna forum za kupandisha maslahi yao. Kwa hiyo tumeona kwenye eneo hili tutumie njia ambayo si lazima twende hadharani, lakini tunaboresha maslahi ya wafanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maslahi ya wafanyakazi hayapo kwenye mishahara tu; kwa kuwapandisha daraja, tunawapandisha, kupunguza kiwango cha kodi nacho pia na namna mbalimbali za kumfanya mtumishi aweze kuboreshewa maslahi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba wafanyakazi wengi wanasubiri kusikia kupanda kwa mishahara, lakini ukifanya hilo tayari unatengeneza ugumu wa maisha kwa sababu ya kupanda kwa vitu mbalimbali. Bado Serikali inaendelea kutafuta njia nzuri ya kuongeza maslahi ya mtumishi ambayo pia mengine yanakuwa zaidi hata ya mshahara.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais amesema mara kadhaa kupitia sherehe za wafanyakazi kwamba kupandisha mshahara kwa Sh.20,000 au Sh.30,000 haina tija, lakini mara nyingi ukiamua kupunguza kodi ambayo mfanyakazi analipa kutoka kwenye double digit kuja kwenye single digit, hilo ongezeko linaweza kuwa kubwa zaidi kuliko hata hili la kupandisha mshahara kwa Sh.10,000 na kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado Mheshimiwa Rais ameendelea kuahidi na Serikali hii imeendelea kuahidi kuboresha maslahi ya watumishi wa umma. Bado Serikali ipo na imeingia madarakani, tunatambua mchango mzuri sana unaotolewa na watumishi wa umma na Serikali yao inatambua na ndiyo Serikali sasa inapata mafanikio kwa sababu ya mchango wao mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nitoe wito kwa watumishi wa umma, wasikate tamaa wakidhani kutangaza mshahara hadharani ndiyo kunaweza kutatua matatizo. Muhimu zaidi kupitia Mabaraza ya Wafanyakazi ambayo tunakaa nayo mara kwa mara kujadiliana namna nzuri ya kuongeza maslahi, tunaendelea kukaa na zile taasisi/jumuiya za wafanyakazi kuweza kutafuta njia nzuri ya kuboresha maslahi ya wafanyakazi. Kwa hiyo wafanyakazi wetu waendelee kufanya kazi, tuendelee kuiamini Serikali na tuendelee kutumia vyombo vyetu kwa maana ya jumuiya zetu za wafanyakazi ili kuendelea kuzungumza maeneo ambayo tunahitaji kuyafanyia kazi, kwa lengo la kuleta maslahi kwa wafanyakazi.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister