Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 1 Energy and Minerals Wizara ya Madini 14 2021-02-02

Name

Anton Albert Mwantona

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Rungwe

Primary Question

MHE. ANTON A. MWANTONA Aliuliza:-

Je, ni lini ahadi ya Mheshimiwa Rais ya mwaka 2019 ya kufufua mradi wa uzalishaji wa makaa ya mawe Kiwira itatekelezwa?

Name

Prof. Shukrani Elisha Manya

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nami kwa vile nasimama kwa mara ya kwanza mbele ya Bunge lako Tukufu, nimshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia Mheshimiwa Rais kwa imani aliyonipatia kutumika katika utumishi huu mtukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anton Albert Mwantona, Mbunge wa Jimbo la Rungwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mgodi wa Makaa ya Mawe Kiwira ulikabidhiwa Serikalini kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) mwaka 2013 kwa lengo la kuuendeleza. Katika jitihada za kuuendeleza mgodi huo ambao ni wa chini ya ardhi, STAMICO, kwa kushirikiana na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) wanaendelea na mpango wa pamoja wa muda mrefu wa kuzalisha umeme zaidi ya MW 200 kutoka katika mgodi huo. Makubaliano ya Ushirikiano (MoU) yako hatua za mwisho kukamilika kabla ya kuwasilishwa kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa mapitio.

Mheshimiwa Spika, tayari timu ya wataalamu wa STAMICO na TANESCO wametembelea eneo la mradi kwa lengo la kutambua mahitaji halisi ya uendelezaji wa mradi huo. Aidha, maandalizi ya kuhuisha taarifa ya upembuzi yakinifu ya mradi ya mwaka 2007 yanaendelea. Katika taarifa hiyo, tathmini ya awali inaonesha kwamba jumla ya mashapo yanayokadiriwa tani milioni 93 yapo katika eneo hilo na gharama zinakadiriwa ni jumla ya Dola za Kimarekani milioni 480 ambazo zitahusisha kuchimba makaa ya mawe, kujenga mtambo wa kuzalisha umeme na kujenga njia ya kusafirisha umeme kutoka eneo la mradi yenye urefu wa kilometa 100.

Mheshimiwa Spika, malengo ya muda mfupi ni kuendelea na uchimbaji wa makaa ya mawe kwa matumizi ya viwanda vya ndani na nje ya nchi. Kwa sasa uchimbaji huo unaofanywa na STAMICO unaendelea katika eneo la Kabulo ambapo tangu mwaka 2017 uchimbaji ulipoanza hadi kufikia Desemba, 2020 Shirika limezalisha tani 50,949 za makaa ya mawe na kuuza tani 29,686.56 zenye thamani ya shilingi 2,264,472,998.70. Baadhi ya makaa hayo yameuzwa kwenye viwanda vya simenti nchini vikiwemo viwanda vya Mbeya Cement, Lake Cement pamoja na kampuni ya Sanflag ya Jijini Arusha.

Mheshimiwa Spika, Shirika limefanya tathmini ya ukarabati wa miundombinu ya mgodi wa chini wa Kiwira kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa makaa ya mawe ili kuendelea kuvipatia viwanda malighafi hiyo, lakini pia ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya uzalishaji mkubwa kwa ajili ya mitambo ya kuzalisha umeme pindi makabuliano na TANESCO yatakapokamilika. Aidha, shirika liko katika maandalizi ya mwisho ya kuanza ukarabati wa miundombinu hiyo. Ahsante.

Additional Question(s) to Prime Minister

Name

Anton Albert Mwantona

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Rungwe

Question 1

MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Spika, nadhani kila mtu anajua faida ya mradi wa makaa ya mawe pale Kiwira Coal Mine. Kwanza huu mradi ulikuwa unazalisha ajira zaidi ya 2,500 kabla haujaisha na mara kwa mara suala hili limejadiliwa hapa kwenye Bunge lako tukufu. Mwaka 2006 iliahidiwa na Wizara hii kwamba huu mradi utaanza mara moja, chini ya Naibu Waziri kipindi kile, Mheshimiwa Dkt. Medard Kalemani; mwaka 2018 pia ikajadiliwa hivyo kwamba mradi utaanza mara moja, sasa hivi tunaambiwa tena kwamba wako katika hatua za mwisho.

Je, ni lini ukarabati wa mgodi huu wa mawe utakamilika na tunategemea kuajiri watu wangapi? Kwa sasa hivi katika sehemu hii ndogo tumeajiri watu 28 tu lakini capacity ya kwanza ilikuwa ni watu 2,500.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni lini Serikali itatoa ahadi ya uhakika kwa sababu 2016 tumeahidiwa, 2018 tumeahidiwa, sasa hivi tunaambiwa tena mradi utaanza; ni lini Serikali itatoa ahadi ya uhakika ambapo sasa tutapata ajira za kutosha kwa wananchi lakini pia tutapata za huduma za kiuchumi kwa Wilaya za Rungwe, Kyela pamoja na Ileje? Ahsante. (Makofi)

Name

Prof. Shukrani Elisha Manya

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyotoa majibu katika swali la msingi, ni kweli kwamba Shirika liko katika maongezi na TANESCO ili kukamilisha hatua za mwanzo kwa ajili ya uchimbaji kuanza. Napenda Mheshimiwa Mbunge ajue kwamba taratibu za uchimbaji zinahusisha upembuzi yakinifu kwa sababu unapokuja kuwekeza unawekeza fedha nyingi. Kwa hiyo, tunapokuwa tunasema kwamba upembuzi yakinifu unafanyika, lengo ni kwamba tunapoingia katika uchimbaji tuweze kuingia kwa namna ambayo tunajua kile kilichopo, fedha inayoingizwa na hatimaye kupata faida.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu tuko katika maongezi na kuhitimisha hatua hizi, nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hili litafanyika baada ya kuhitimisha hatua hizi za mwanzo. Ajira zinazotarajiwa kupatikana tunaweza tukazipata baadaye baada ya kuwa tumemaliza upembuzi wote yakinifu kwa ajili ya mradi.

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa majibu hayo.