Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 34 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 8 2019-05-23

Name

Pauline Philipo Gekul

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Babati Mjini

Primary Question

MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa fursa niulize swali kwa Waziri Mkuu, ni azma ya Serikali yetu na ni Sera ya Serikali yetu kuwapatia wananchi maji safi na salama lakini kwa bei nafuu. Nafahamu pia mchakato wa Serikali kupandisha bili za maji kupitia mamlaka za maji kufanya public hearing na mwisho EWURA waweze kufanya maamuzi ya bili hizo.

Mheshimiwa Spika, EWURA wamemaliza mchakato bahati mbaya sana maoni ya wananchi hayajazingatiwa, bili hizi za maji kote nchini zimepanda kwa zaidi ya asilimia 80. Mfano, mtumiaji wa maji nyumbani alikuwa analipa unit 1 kwa shilingi 1,195 imepanda kuanzia hapo mpaka 1,800. Naomba nifahamu kauli ya Serikali juu ya ongezeko hili la zaidi ya asilimia 80 ya bili za maji nchini wakati wananchi waliomba kwamba bili hizi zisipande?(Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gekul, Mbunge wa Babati Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, azma ya Serikali katika kutoa huduma mbalimbali nchini bado ni njema na inawaangalia uwezo wa Watanzania mpaka yule mwananchi wa chini wanaweza kumudu kugharamia gharama hizo kwa uwezo wake wa kifedha. Umeeleza upo mchakato unaendelea na umeishia mahali ambapo gharama zimepanda kwa asilimia 80. Sisi Serikali tumetoa mamlaka kwenye hizi wakala ili kufanya mapitio na mapitio hayo lazima yaangalie uwezo wa wananchi wenyewe nchini ili wawezeshe wananchi kupata huduma hiyo kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nimepata taarifa kwamba EWURA na Wizara ya Maji kupitia wakala wamekaa vikao vyao na sasa wameshatoa taarifa ya mwisho ya gharama hizo na zimefikia kwa kiwango ulichokitaja ambacho kimepanda kwa asilimia 80 lakini utaratibu Serikalini ni kwamba baada ya kuwa maazimio hayo yamefanywa, wanatoa taarifa Serikalini. Nashukuru kwamba umetuambia hilo na tumepata taarifa kwamba hata wadau hawakuweza kupata fursa ya kusikilizwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni jukumu la Serikali sasa baada ya kupata matokeo yale, baada ya wao mjadala wao wataleta Serikalini tuone kwamba je, viwango walivyotoa vinawezesha Watanzania kupata huduma hiyo? Na tutakapogundua kwamba hawawezeshwi kupata huduma hiyo, basi Serikali itafanya maamuzi mengine dhidi ya hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nikutake ufanye subira, EWURA walete matokeo ya vikao vyao na mapendekezo yao, Serikali tutafanya maamuzi kwa kushirikiana na Wizara ya Maji. Tukishawapa taarifa hiyo ya mwisho ndiyo itakuwa ndiyo bei ambazo zitakuwa zinatumika na mamlaka hiyo, ahsante. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister