Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2019-09-12

Name

Mariamu Nassoro Kisangi

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, katika miezi ya karibuni katika Mikoa mbalimbali ya nchi yetu kumekuwa na changamoto kubwa ya kupanda kwa gharama za maji bila kuzingatia uasilia, kuletewa bili zisizo sahihi, kukatiwa maji bila utaratibu na kukosa maji kwa muda mrefu kisha unaletewa bili kubwa. Kero hiyo imejitokeza katika Mikoa mbalimbali katika nchi yetu ikiwemo Mikoa ya Dar es Salaam, Manyara, Dodoma, Tanga, Mwanza na Mikoa mingine mingi na hasa katika maeneo ya Mijini.

Je, Serikali inatoa kauli gani kwa wananchi wake waliokumbwa na kero hiyo?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Kisangi, Mbunge wa Mkoa wa Dar es Salaam, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, alichosema Mheshimiwa Mbunge, yako maeneo yanajitokeza kwamba mamlaka tulizozipa mamlaka hiyo ya kusimamia maji kwenye maeneo yao, tunazo mamlaka ambazo tunazianzisha sasa za RUWA za vijijini na kwenye ngazi za Wilaya, lakini zipo mamlaka ambazo zimechukua maeneo makubwa kwenye ngazi za Mikoa, pia tuna Kamati za Maji ambazo zinasimamia miradi hii kwenye maeneo ya vijiji na maeneo mengine yote.

Mheshimiwa Spika, kumejitokeza wimbi la mabadiliko ya bei. Ni kweli upo utaratibu ndani ya Serikali kwamba mamlaka hizo zinapoona zinahitaji kuboresha huduma zinaweza kufanya mapitio ya bei zao. Lakini kinachotokea sasa ni kwamba zipo mamlaka zinapita zaidi ya kiasi.

Mheshimiwa Spika, nimefanya ziara Mkoani Simiyu na hapa karibuni nilikuwa kwenye Wilaya ya Maswa, moja kati ya malalamiko niliyoyapokea kwa wananchi pale ni kupanda kwa bei kutoka shilingi 5,000 wanayoilipa kwa mwezi mpaka shilingi 28,000. Sasa bei hizi hazina uhalisia, hakuna sababu ya mamlaka kutoza fedha yote hiyo na kuwafanya wananchi wakose maji.

Mheshimiwa Spika, Serikali ndiyo inatekeleza hii miradi na inatoa fedha kwa lengo la kuwapa huduma wananchi ili wapate huduma ya maji. Mamlaka tumewapa jukumu la kusimamia mradi huo na kuhakikisha kwamba angalau wanaweza kufanya marekebisho, matengenezo pale ambapo kunatokea uharibifu. Kwa hiyo, gharama haziwezi kuwa kubwa kiasi hicho na wala wao hawapaswi kutoza wananchi ili kurudisha gharama za mradi kwa sababu Serikali haijadai gharama ya kuendesha mradi huo kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa bahati nzuri jana nilikuwa na Waziri wa Maji nikimwambia hili la kwamba lazima afuatilie Mamlaka ya EWURA ambayo ina mamlaka ya kukaa na hizo mamlaka zetu za maji kufanya mapitio ya bei. Bei zinazotakiwa kuwekwa ni zile ambazo mwananchi wa kule kijijini anaweza kuzimudu lakini siyo kwa kupandisha bei kutoka shilingi 5,000 mpaka shilingi 28,000, jambo ambalo halina uhalisia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote na Watanzania kwa ujumla, tutaendelea kusimamia Mamlaka zote za Maji, lakini Serikali itaendelea kutoa huduma za maji, nataka tujiridhishe kila Mtanzania anapata maji kwenye maeneo yake kwa usimamizi wa mamlaka hizi, lakini hatutaruhusu na hatutakubali kuona Mtanzania anatozwa gharama kubwa za maji kiasi hicho. Huku tukiwa tunatoa wito kwamba lazima tuchangie maji ili tuweze kuendesha miradi hii pale ambapo tunatakiwa kununua diesel, tunatakiwa tununue tepu ya kufungulia maji au bomba linapopasuka, lazima mamlaka zile ziweze kufanya ukarabati huo, lakini siyo kwa kutoza fedha kiasi hicho.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, masharti ambayo yapo mnapotaka kuongeza bei ni kwamba mamlaka hizo zinapodhamiria jambo hilo ni lazima kwanza zitoe taarifa EWURA, mbili kwenye vikao hivyo lazima Kamati za Maji zihusike, Kamati ambazo zinaundwa na wananchi wenyewe, tatu ni lazima wahusishe wadau, wadau ni wale watumia maji. Kwa hiyo, wote wakikubaliana sasa kwa viwango ambavyo wananchi wake wanaweza kuvimudu ndipo mnaweza kupandisha. lakini msipandishe wenyewe na mkawaumiza wananchi na miradi yenyewe imetekelezwa na Serikali, Serikali inayotaka wananchi wapate maji halafu mnataka kuwakwaza wananchi wasipate maji waanze kuilalamikia Serikali yao. Hatutakubaliana na hili na kwa hiyo mamlaka ziwe makini, Wizara ya Maji iendelee na utaratibu na maagizo ambayo nimewapa jana.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister