Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2020-02-06

Name

Julius Kalanga Laizer

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Monduli

Primary Question

MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kumuuliza Waziri Mkuu swali:-

Mheshimiwa Waziri Mkuu, pamoja na mpango mzuri wa Serikali wa kuhakikisha kwamba, kila kijiji kinapelekewa umeme katika nchi yetu. na kwa kuwa, Serikali imejitahidi sana kupeleka nguzo nyingi na nyaya katika maeneo mengi ya nchi yetu, lakini bado nguzo hizo zimeendelea kulala chini na nyingine hazijafungiwa umeme. Na kwa kuwa mpango wa REA Awamu hii ya Tatu ni kwamba, lazima uishe mwezi wa sita, lakini katika mwenendo wa utekelezaji wa mradi wenyewe inaonekana mpaka mwezi wa sita kuna miradi ambayo itakuwa haijakamilika.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kwamba, mradi huu wa utekelezaji wa REA katika vijiji vyetu unakamilika mwezi wa sita kama ambavyo Serikali ilipanga?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Julius Kalanga Laizer, Mbunge wa Monduli, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo miradi hii ya REA ambayo inapeleka umeme vijijini ambayo kwa kweli kazi zinaendelea vizuri. Tumeenda maeneo mengi; na sasa tumefikia zaidi ya asilimia 60 na kitu katika kuweka umeme kwenye vijiji vyetu vingi ambavyo vimekusudiwa. Mkakati huu unalenga kila kijiji huko kwenye maeneo yetu tunakotoka. Wizara ya Nishati imejipanga vizuri, imeshasambaza wakandarasi kila halmashauri, wakandarasi ambao wamesaini mkataba kukamilisha kazi hiyo kwa muda na kwa kuweka umeme katika kila kijiji kwa awamu hii ya tatu, awamu ya kwanza na kwenye awamu ya tatu kuna awamu ya kwanza na ya pili na zote hizi zitatekelezwa, ili kuhakikisha kwamba, umeme unapelekwa kwenye ngazi ya vijiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hiyo ambayo nimeeleza kwamba inaendelea na ni nzuri inaanza sasa kupeleka umeme kwenye vijiji vyetu vingi; na vijiji vyote vilivyobaki viendelee kuwa na uhakika kwamba, umeme utafikishwa. Sasa suala la kufika mwezi wa Juni inategemea hapa katikati kama kunaweza kuwa na jambo lolote lile linaloweza kumfanya mkandarasi akashindwa kukamilisha kazi yake vizuri. Sisi ndani ya Serikali tunahakikisha mtiririko wa fedha za malipo kwa mkandarasi unakwenda, tunahakikisha kwamba, vifaa anavipata.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa bahati nzuri sasa vifaa vya kutengenezea kazi hizo vinapatikana hapahapa nchini. Nguzo zinapatikana nchini, transformer zinapatikana hapa nchini, nyaya zinapatikana hapa nchini. Kwa hiyo tuna matumaini kwamba, tunaweza kukamilisha kazi hiyo kwa kipindi ambacho tunatarajia, na kwa kuwa, wakandarasi wako kazini na tumetoa pia mamlaka kwa TANESCO zetu maana TANESCO na REA ni taasisi mbili zilizo kwenye Wizara moja, ili TANESCO sasa wasimamie kazi za REA kuwa zinakamilika kwenye maeneo ambayo wanayasimamia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni matumini yangu kwamba kazi za uwekaji umeme kwenye vijiji itakamilika. Mheshimiwa Waziri wa Nishati ameelza hapa, kwamba sasa tunakwenda mbali zaidi mpaka kwenye vitongoji vikubwa navyo tunapeleka umeme. Kwa hiyo wananchi wawe na matumaini na wajiandae sasa kutumia fursa ya kuwa na umeme kwenye maeneo yao kwa ajili ya kuendesha shughuli mbalimbali zinazohitaji umeme, asante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister