Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 8 2020-01-30

Name

Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Primary Question

MHE. DKT. STEPHEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa niweze kumuuliza Mheshimiwa Wazir Mkuu swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kuwa Serikali yetu ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais wetu mpendwa Dkt. John Pombe Magufuli imejinasibu kuhamasisha ujenzi wa viwanda vikiwemo viwanda vya kuchakata nyama na mazao mengine yanayotokana na mifugo.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba wafugaji wanatengewa maeneo ya malisho na malisho hayo yanaendelezwa kwa kujenga na kukarabati mabwawa, kuchimba visima vya maji na kuwekewa miundombinu mingine muhimu ili kuboresha afya ya mifugo ili waweze kukidhi haja ya hivi viwanda kwa ajili ya ng’ombe hawa wanapokuwa wameongezewa thamani, wafugaji watapata bei yenye tija? Ahsante sana.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Kiruswa Mbunge wa Longido kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli, kama ambavyo nimesema awali kwamba Serikali yetu imejikita katika kuhamasisha ujenzi wa viwanda kwa lengo la kukuza uchumi wetu; na nimeeleza vizuri sana mwanzo manufaa ya viwanda ikiwemo na kuendeleza sekta yenyewe. Kwa kiwanda cha nyama kuwepo kwake Wilayani Longido tuna uhakika wafugaji wetu watapata faida kubwa kwa kufuga kisasa, kwa kupata masoko ya uhakika lakini pia na sisi tutanufaika kwa kupata nyama iliyopitia kiwandani yenye ubora ambao na sisi tumeuona kwamba ni ubora uliohakikiwa na taasisi yetu.

Kwahiyo, uwepo wa kiwanda kile na mwekezaji huyo, Wizara yetu ya Mifugo na Uvuvi imeweka utaratibu mzuri sana sasa; kwamba wale wote waliowekeza viwanda tumewaunganisha na taasisi yetu ya NARCO kwa kuwapa maeneo yaliyotengwa kama ni maeneo ya malisho, kwa kuwapa eneo la kuhifadhia ng’ombe wao, kuwakuza ng’ombe wao na zile taratibu zote zile za mifugo ili ziweze kukamilika kabla hajaingia ndani ya kiwanda kwa lengo la kutoa nyama iliyo bora kwa ajili ya chakula kama ambavyo tumetaka iwe.

Kwa hiyo tumebaini kwamba ranchi zetu zote nchini au maeneo yote ya malisho nchini. Hawa tumewapa maeneo hayo kwanza wale wenye viwanda lakini pili wafugaji wakubwa na tatu tumewatambua pia na wafugaji wadogo ambao wana ng’ombe kuanzia 100 na kuendelea, ambao tumesema tusiruhusu kuwa na ng’ombe 100 vijijini kwa sababu kunakuwa na migogoro mingi ya mifugo kula mazao, mifugo kuharibu miundombinu mingine. Kwa hiyo tumewatengea maeneo kwenye hizo Rachi zetu au kwenye maeneo hayo ya malisho.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa utaratibu huu tumetambua jitihada za wafugaji na kuboresha namna ya ufagaji wao na mahali pa kuuzia, kwa maana ya soko kwenye kiwanda. Mwekezaji naye sasa naona lengo la nchi la kumlinda mwekezaji wetu kwa kumpa maeneo ya kuhifadhia ng’ombe wake halafu awapeleke viwandani. Tunatarajia kuendelea kutenga maeneo mengi zaidi ya malisho na kutoa fursa nyingi zaidi kwa wafugaji wetu wa ngazi zote; wakubwa, wa kati na wadogo ili waendeshe shughuli zao za mifugo vizuri.

Mheshimiwa Spika, Waziri wetu pamoja na Naibu Waziri wake na Makatibu Wakuu wa Wizara hii wanafanya kazi hiyo kila siku, unawaona hata kwenye vyombo vya habari wakiendelea kuratibu maeneo haya ya malisho kwa lengo la kuboresha ufugaji nchini na pia kwa lengo la kukuza sekta ya nyama, kwa maana ya kuwa na viwanda vinavyotengeneza nyama hizi, zinazo-process nyama hizi kwa ajili ya chakula cha ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge aendelee kuhamasisha na kuhakikishia wapiga kura wake kwamba Serikali yetu imejikita katika kuhifadhi na kulinda wafugaji wetu wote na kuhakikisha kwamba tunawatengenezea fursa za kupata pia na masoko yake. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister