Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 7 2020-01-30

Name

Cosato David Chumi

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mafinga Mjini

Primary Question

MHE. CASATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata nafasi ili niweze kumuhuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali, katika siku za karibuni dunia imekumbana na majanga makubwa mawili; la kwanza ni ule ugonjwa ambao uko rafiki ya China unausababishwa na virus wa aina ya corona.

Mheshimiwa Spika, la pili ni baa la Nzige ambao tayari wameshafika katika baadhi ya nchi jirani na hasa za Afrika Mashariki. Nilikuwa napenda kufahamu, Serikali imejipangaje katika kukabiliana na kudhibiti masuala haya mawili ambayo kwa namna moja ama nyingine yasipodhibitiwa yanaweza yakaadhiri ukuaji wa maendeleo ya taifa letu na wananchi wetu na hasa ukizingatia kwamba kuna biashara kubwa kati ya nchi yetu na China?

Vilevile ukizingatia kwamba kupitia Jumuiya ya Afrika Mashariki wenzetu jirani wameshakubwa na baa la Nzige?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Chumi Mbunge wa Mafinga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba nchini China kuna ugonjwa unaosababishwa na virusi vya corona ambao unapoteza maisha ya watu; na sasa tumeanza kuona hata nchi za jirani yake nazo pia zimepata maambukizi hayo. Lakini pia hili la pili la nzige tumepata taarifa kupitia mitandao na vyombo vya habari kwamba hapa nchi jirani ya Kenya mazao yao yanashambuliwa na hao nzige.

Mheshimiwa Spika, sasa tuanze na hili la corona, corona iliyopo nchini China, China ni nchi rafiki na Tanzania, Watanzania wengi wapo China, lakini pia wapo wachina walioko nchini Tanzania. Tunayo maingiliano mengi kati ya Tanzania na China. Wakati huu wa uongonjwa huu, kwanza tumewahakikishia Watanzania kwamba Tanzania haina tatizo hilo la corona; na jana Waziri wa afya pamoja na Naibu Waziri wa afya wametoa taarifa kwa Watanzania, na nimeona leo kwenye gazeti limetoka hili, sasa jukumu letu ni kuwa na taadhari tusije tukapata tatizo hilo.

Mheshimiwa Spika, sasa kwenye tahadhari Serikali imejipanga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, moja tumeimarisha mawasiliano na Balozi yetu iliyoko China kujua hali huko China inaendeleaje; na Mheshimiwa Mbelwa Kairuki anafanya kazi hiyo ya kutupa mrejesho kila siku na hali iliyoko kule. Baalozi Mbelwa anaendelea kazi nzuri ya kuendelea kutoa elimu kwa Watanzania kwanza ametafuta madaktari wa Kitanzania ambao wamejifunza ugonjwa huo na kuendelea kuwaelimisha Watanzania walioko nchini China namna ya kujikinga.

Mheshimiwa Spika, na balozi kule kwa Tanzania walioko China amewakanya watanzania wasiwe na mizunguko mingi sana kwa sababu ugonjwa huo maambukizi yake ni pale ambapo watu wanakutana. Hiyo moja.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tumewataka Watanzania wale wanapohitaji labda kurudi Tanzania, na kwa sababu watatakiwa kusafiri kwenye ma treni, mabasi wafanye mawasiliano na Balozi juu ya namna nzuri ya kusafiri. Wasisafiri kwenda ubalozini Beijing ulipo Ubalozi na badala yake watumie mawasiliano ya kimtandao kupata ridhaa hiyo na kuambiwa hali ikoje ili wapate vibali vya kurudi.

Ndugu Watanzania tunatambua kuna wazazi wana watoto wetu wanasoma nchini China, na wengine wamesharudi likizo. Tunawasihi watoto hawa wasiende kwanza nchini China mpaka hapo tutakapopata taarifa za kidiplomasia.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Mambo ya Nje Tanzania inaendelea kufanya mawasiliano na Balozi zote mbili, Balozi ya China Nchini Tanzania na Balozi Tanzania Nchini China kuona mwenendo wa ugonjwa huo. Pale ambapo Serikali itaridhika kwamba kule hali imepungua tutatoa tamko kwa Watanzania walioko likizo hapa kurudi nchini China kuendelea na masomo, na vinginevyo ikiendelea sana basi Serikali itatafuta utaratibu mwingine.

Mheshimiwa Spika, kwahiyo, nitowe wito kwa Watanzania kama ambavyo Wizara imetoa kwamba kila Mtanzania awe makini na wageni wanaoingia mpakani na hasa wale wote ambao tumewaweka mpakani kuhakiki wanaongia nchini kupitia vifaa vyetu ambavyo vinaweza kutambua magonjwa mbalimbali kuvitumia vifaa hivyo kikamilifu ili kubaini hao ambao wana dalili ya magonjwa hayo ili kudhibiti kuingizwa ugonjwa huu wa corona hapa nchini Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la nzige, kama ambavyo nimesema majirani zetu mazao yanaharibiwa. Nzige ni wadudu hatari sana, wakiingia hapa watamaliza mazao yetu. Tumechukuwa taadhari, Wizara yetu ya Kilimo inaendelea kuwasiliana na Wizara ya Kilimo nchini Kenya kuona mwenendo na ukuwaji wa tatizo hilo, na sisi huku tunajipanga kwa namna ambavyo tunaweza kushiriki kikamilifu; lakini Serikali yetu inashiriki pia kusaidia nchini Kenya kupoteza wadudu hao ili wasiongezeke tatizo hili likawa kubwa nchini Kenya lakini pia lisije likaamia huku nchini kwetu.

Mheshimiwa Spika, sasa bado nitowe wito kwa mikoa na wilaya na vijiji vilivyoko mpakani kuwa makini na hao wadudu nzige.Pale ambapo watawaona wakiingia watowe taarifa haraka sana kwenye mamlaka zao ili hatua kamili iweze kuchukuliwa.

Sisi tumejipanga kudhibiti hali hiyo na tutaendelea kudhibiti hali hiyo ili tusije tukapata tatizo hilo la kuwa na nzige hapa nchini kwetu. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister