Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2020-01-30

Name

Albert Ntabaliba Obama

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Primary Question

MHE. ALBERT O. NTABALIBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kunipa fursa hii niweze kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali. Mheshimiwa Waziri Mkuu natambua na ninapongeza juhudi za Serikali juu ya upatikanaji wa vitambulisho vya NIDA. Vilevile natambua na ninajua faida za vitambulisho vya NIDA kwa kutambua mtu mmoja mmoja kama Mtanzania na sababu za kiusalama. Hata hivyo kwa sasa hivi kumekuwa na changamoto kubwa ya upatikanaji wa namba hizo za NIDA kwenye vijiji na miji. Nini kauli ya Serikali kwasababu wananchi sasa wanapata mkanganyiko speedna upatikanaji nini kauli ya Serikali?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika,naomba kujibu swali la Mheshimiwa Obama Mbunge wa Buhigwe kama ifuatavyo:-

Upo ukweli kwamba Watanzania wengi tulikuwa hatujawafikia kuwapa vitambulisho maarufu vya NIDA mpaka ngazi ya vijiji na kule vitongojini; jambo hili Serikali imelifanyia kazi. Kwanza tumeongeza idadi ya watumishi kwenye ngazi za halmashauri ili kuwezesha kufika mpaka kwenye vijiji na vitongoji na kufanya kazi hiyo.

Mbili, tumeongeza pia na mitambo ya kufanyia kazi ili baadaye tuweze kupata vitambulisho; na idadi hii ya watumishi hawa ambao tumeongeza nimpaka Makao Makuu, ili kuweza kuharakisha kutoa vile vitambulisho vyao.

Mheshimiwa Spika, tunachokifanya sasa, ili Watanzania waweze kupata huduma yeyote ile inayohitaji kitambulisho cha NIDA Serikali imeridhia kila yeyote anayetaka kitambulisho cha NIDA kwa mwananchi; na kama mwananchi atakuwa hajapata kitambulisho cha NIDA basi atumie namba aliyopewa ili kuweza kuhalalisha kupata huduma yeyote ile ambayo inahitaji kitambulisho huku akiwa hana kitambulisho. Hiyo ni njia ya kwanza ambayo tumeitumia kurahisisha kuwafikia Watanzania.

Mheshimiwa Spika, lakini mbili, inawezekana pia namba hii ni ngumu kwa mwananchi huyo aliyeko kijiji kuipata. Tumetoa maelekezo kwa watendaji wetu wa NIDA walioko kule kwenye ngazi ya halmashauri kwamba sasa watoe orodha ya wale wote waliowaandikisha kwenye vituo vyao na namba zao ili angalau mwananchi aweze kufika pale kwenye kituo aone orodha na namba yake sasa imuwezeshe mwananchi huyu kupata huduma popote panapohitaji kitambulisho cha NIDA kwa kupeleka namba tu; hiyo ndiyo njia ambayo tumeirahisisha ili kuwafikia Watanzania wote mpaka vijijini na kuhakikisha kwamba sasa uzalishaji wa vitambulisho makao makuu kule Kibaha iende kwa haraka na vitambulisho vipelekwe mpaka vijijini kwa haraka ili kila Mtanzania aweze kupata vitambulisho.

Mheshimiwa Spika, lakini natambua kwenye eneo hili, naomba nizungumze jambo moja, kwamba yapo maeneo tumeongeza umakini mkubwa, na hasa maeneo ya mipakani, kwa lengo la kuzuia wananchi wa nchi jirani kujipatia kitambulisho cha NIDA nchini Tanzania halafu akafanya mambo yake huku ndani kupitia kitambulisho cha nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwahiyo mtaona kunaweza kuwa kuna ucheleweshaji huko kwenye miji iliyoko mipakani na nchi jirani za Tanzania. Kwasababu tunafanya zoezi hili kwa umakini kwa lengo la kutoa kitambulisho kwa Mtanzania tu. Na nitoe wito kwa Watanzania mtusaidie kuwatambua ambao siyo wakazi wa nchi wanaokuja kuchukua vitambulisho vyetu kwa lengo la kudhibiti hali ya ulinzi na usalama ndani ya nchi. Kwahiyo kama kunaweza kuwa kuna kuchelewa maeneo kadhaa hasa mipakani; natambua Mheshimiwa Mbunge unatoka Buhigwe. Buhigwe iko karibu na nchi ya Burundi, kwahiyo pale tumeongeza umakini sana pale ili tusiweze kutoa vitambulisho kwa ndugu zetu wa nchi jirani.

Additional Question(s) to Prime Minister