Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 16 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2019-04-25

Name

Pascal Yohana Haonga

Gender

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mbozi

Primary Question

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Suala la vitambulisho kwa wajasiriamali wadogo wadogo imekuwa ni kero kubwa sana katika maeneo mbalimbali nchini na limekuwa ni kero kubwa zaidi kwa wajasiriamali wale wanaouza mboga mboga kama mchicha, nyanya, tembere, maandazi na vitumbua. Kibaya zaidi, maeneo mengine hata wale wanaotoka shambani, amechuma mchicha wake, anaambiwa naye ni Mjasiriamali aweze kutoa shilingi 20,000/= apewe kitambulisho.

Mheshimiwa Spika, suala hili kwa mtazamo wangu mimi naona kama vile halijatafsiriwa vizuri kule chini hasa wale wanaolitekeleza kwa sababu maeneo mengine pia hata wapiga debe na walimu maeneo mengine wanaambiwa kwamba ni wajasiriamali waweze kulipia vitambulisho vya shilingi 20,000/=.

Mheshimiwa Waziri Mkuu sasa swali langu: Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka hili jambo lingeweza kusitishwa kwanza ili tuweze kufanya tathmini na kupanga vizuri kwamba hasa ni watu gani ambao wamelengwa na wenye mitaji ya namna gani? Kwa sababu kuna wengine wana mitaji ya shilingi 1,000/= wengine shilingi 2,000/=, lakini wanaambiwa walipe shilingi 20,000/= kwa ajili ya vitambulisho vya ujasiriamali?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwalimu Haonga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali imeweka utaratibu mzuri sana wa kuwafanya wajasiriamali wadogo kuweza kuchangia pato la Taifa; na Mheshimiwa Rais alibuni njia nzuri ambayo inawatambulisha hawa wajasiriamali. Hata hivyo, wajasiriamali hawa tumewaweka kwenye madaraja yao. Wako wale wadogo, wako wafanyabiashara wa kati na wale wajasiriamali wakubwa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais aliwalenga Serikali imewalenga hawa wadogo ambao kipato chao kutokana na kazi wanayoifanya hakizidi zaidi ya shilingi milioni nne kwa mwaka ili nao wapate nafasi ya kuweza kuchangia pato la Taifa lakini kuwaondolea usumbufu kwenye maeneo wanayofanya biashara kwa kutozwa kodi kila siku ambayo pia na yenyewe inasaidia kupunguza mapato wanayopata kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, sasa vitambulisho vile vilipotolewa kwa Wakuu wa Wilaya, tambua kwamba kuna maeneo mengine utekelezaji wake siyo mzuri, kwa sababu wako wengine wanalazimisha watu badala ya kuwaelimisha namna ya kupata vitambulisho hivyo. Yako maeneo wanapewa hata wale wajasiriamali wakubwa wenye pato la zaidi ya shilingi milioni nne, linawafanya na wao wanashindwa kuchangia kulingana na biashara wanazozifanya kwa sababu wao kwa category yao wanachangia TRA moja kwa moja, lakini wale wadogo hupitia vile vitambulisho.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, maelekezo ambayo tumeyatoa tena baada ya kuwa tumepata malalamiko kutoka kwenu Waheshimiwa Wabunge, ni kwamba Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya, Wakuu wa Mikoa watumie muda wao kuelimisha nani anapaswa kuwa na kitambulisho badala ya kutumia wakati mwingine nguvu au kwenda kulazimisha au kuwapa wajasiriamali wakubwa wenye mapato zaidi ya shilingi milioni nne na kuondoa maana ya uwepo wa vitambulisho? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kupitia Mheshimiwa Mbunge Serikali tumeipokea hiyo. Tunaendelea kutoa maelekezo kwa Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya watumie nafasi hiyo kuelimisha zaidi kuliko kulazimisha, ni nani wanatakiwa wapate kitambulisho hicho ili kuwaondolea usumbufu wa kuwa wanatozwa fedha tena shilingi 200/=, shilingi 500/= kila siku anapoendelea kufanya biashara yake ya mchicha, maandazi, wale wanaokimbiza mahindi vituo vya mabasi.

Mheshimiwa Spika, watu wa namna hii ndio ambao Mheshimiwa Rais aliwalenga ili nao waone uchangiaji wa uchumi, pato la nchi ni sehemu yao lakini pia waendelee kufanya biashara yao bila kusumbuliwa ndani ya mwaka kwenye Halmashauri zao. Kwa hiyo, niseme tu, tumeipokea tena hiyo na tutaifanyia kazi zaidi ili kuleta utendaji ulio sahihi na wajasiriamali waweze kujitoa kuchangia kwenye nchi yao.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri Mkuu katika swali lake amesema pia kwamba walimu wanalazimishwa wapewe vitambulisho vya wajasiriamali. Sijui hilo nalo unasemaje Mheshimiwa Waziri Mkuu?

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Sawasawa, hilo limetokea Jimboni kwangu.

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la swali la Mhehsimiwa Mwalimu Haonga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, inawezekana pia uko utekelezaji usio sahihi. Mwalimu kama Mwalimu ni miongoni mwa watu wenye pato la zaidi ya shilingi milioni nne kwa mwaka. Kwa hiyo, mwalimu anapofanya biashara, ile biashara anayoifanya kama yenyewe haimfikishi kwenye pato hilo, Mkuu wa Wilaya ambaye yuko kwenye eneo hilo, anajua mwenedno wa pato la huyo mtu ambaye yuko pale.

Mheshimiwa Spika, sasa suala la mwalimu na mfanyakazi mwingine, muhimu zaidi ni ile biashara anayoifanya, lakini pia namna ambavyo anaweza pia akachangia pato kupitia biashara hii anayoifanya ambayo uzalishaji wake haifikii kiwango hicho cha shilingi milioni nne kwa mwaka.

Additional Question(s) to Prime Minister