Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 6 2017-11-16

Name

John Peter Kadutu

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Primary Question

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kunipa fursa hii.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, hivi karibuni na ni muda mrefu sasa kumekuwa na migogoro ya hifadhi na maisha ya wananchi wetu kwenye majimbo mbalimbali Na hivi karibuni kumekuwa na matangazo ya kuwakataza wananchi wetu wasiendelee na shughuli za uzalishaji na waweze kuondoka kwenye maeneo hayo. Je, Serikali inatamka nini juu ya maeneo ambayo asilimia kubwa ni hifadhi, lakini vijiji vyake vimeandikishwa kwa maana vina GN? Ahsante sana.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kadutu, Mbunge wa Ulyankulu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nchi yetu tuna mapori ambayo tumeyahifadhi kisheria na yana mipaka yake rasmi kwa mujibu wa ramani zilizochorwa zinzolindwa na sheria hizo. Mapori haya yako katika kila eneo na ni budi kila Mtanzania kushiriki kuyahifadhi. Sasa kumetokea uvamizi ambao unafanywa na walio jirani kwenye maeneo hayo, lakini mbili, maeneo hayo yamekuwa na migogoro mingi kati ya mapori


yetu na vijiji, kati ya mapori na wananchi ambao wanapeleka kufanya shughuli za kijamii huko ndani ambako pia, haturuhusu kufanya shughuli za kijamii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kutokana na migogoro hii ya muda mrefu nilitoa agizo kwa Wizara ya Maliasili na Utalii kufanya mapitio ya mipaka hiyo na kuweka alama kwenye mipaka ya mapori yote, lakini tumekuja kugundua kwamba, pia kwenye mapori hayo viko vijiji vimesajiliwa na ni Serikali tumesajili.

Mheshimiwa Spika, pia kulianza migogoro pale ambapo wale wataalam wanapita kuweka mipaka ile ili kutambua mipaka, tulichowasihi wananchi walio kwenye vijiji vilivyosajiliwa hata kama viko kule ndani kwenye misitu ile kwamba, wawaache wataalam wafanye mapitio na waweke alama hizo zinazobainisha mipaka hiyo kwa mujibu wa ramani.

Baada ya hapo tutakuja kuona ni kijiji gani kiko ndani na je, pale palipo kijiji malengo yetu ya uhifadhi yamefikiwa na bado ni mahitaji sahihi? Ili baadaye tuje tufanye maamuzi ya au kupunguza maeneo ambayo tunaona kwa sasa kwa uhifadhi huo hauna tija kwenye maeneo hayo, ili kuondoa migogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kazi hiyo inaendelea na nimewaagiza kufikia mwezi wa 12 tarehe 30 wawe wamekamilisha mapori ambayo bado. Baada ya hapo sasa tutakwenda kuona ni vijiji vingapi vilisajiliwa na Serikali viko kwenye hifadhi hiyo na kama vijiji hivyo, bado viko kwenye maeneo ambayo yana tija kwa malengo ya uhifadhi au hayana tija kwa malengo ya uhifadhi, tufanye maamuzi mengineyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka nitoe wito kwa wananchi wote ambao wako kwenye hifadhi ambazo zimetambuliwa baada ya kuwa wanaweka alama hizi, wawaache wataalam wetu waweke zile beacons, wamalize zoezi hilo hata kama kijiji hicho kimejikuta kiko ndani ya
beacon hizo, wawaache watulie wafanye kazi zao. Baada ya kazi hiyo tutakuja kufanya mapitio katika vijiji hivyo, ili sasa tufanye maamuzi na tutafanya maamuzi kwa maslahi ya nchi. Inaweza kuwa labda kufuta kijiji au kukiacha na kubadilisha mipaka na kuchora ramani mpya. Kuanzia hapo sasa tutakuwa tunaenda vizuri na wananchi watashiriki pia katika kuhifadhi misitu hiyo. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister