Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2017-11-09

Name

Munde Abdallah Tambwe

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MUNDE A. TAMBWE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuuliza swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu umekuwa mfuatiliaji mzuri wa mazao ya wakulima huko mikoani ili waweze kupata tija. Umekuja Tabora mara kadhaa, umetoa maelekezo kadhaa kuhusu suala zima na kero za tumbaku, lakini agizo kubwa ulilolitoa la kuhakikisha tumbaku iliyopo ndani ya wakulima na kwenye magodauni ya msimu uliopita inunuliwe, ambayo mpaka leo hii ninavyoongea tumbaku hiyo bado haijanunuliwa. Hii imesababisha adha kubwa kwa wakulima wa tumbaku wa Mkoa wa Tabora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ni msimu wa kulima tumbaku nyingine lakini tumbaku iliyopo ni ya mwaka wa jana na haijanunuliwa; na tumbaku hii ikikaa kwa muda mrefu inashuka grade ambapo ubora wa tumbaku unapungua na inateremka uzito. Mpaka sasa ma-godown mengi yanavuja na tumbaku hiyo kuvujiwa na kusababisha hasara kubwa na tahaluki kubwa kwa wakulima wa tumbaku Mkoa wa Tabora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Tabora wana imani kubwa na Serikali ya Awamu ya Tano na leo wanakuomba sana, wanakusihi wapo chini ya miguu yako wameniagiza; wanaomba utoe tamko.

Je, Serikali inatoa tamko gani leo kuhusu kununua tumbaku ya msimu uliopita ambayo bado haijanunuliwa, iliyopo kwenye magodauni ya wakulima wa Mkoa wa Tabora?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Munde, Mbunge wa Tabora kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, suala la zao la tumbaku ni jambo ambalo Serikali tumelifanyia kazi kweli kweli, na zao la tumbaku ni miongoni mwa mazao ambayo tunataka sasa yapate mabadiliko ya kilimo chake, lakini pia na masoko yake. Moja kati ya tatizo ambalo lipo sasa ni lile aliloeleza mheshimiwa Mbunge la masoko ya tumbaku na Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote wanaotoka kwenye maeneo ya tumbaku wanajua jitihada za Serikali zilizofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la tumbaku upo utamaduni wa kila mwaka wa wakulima wetu na makampuni yanayonunua kufunga mikataba ya kiwango cha tumbaku kitakachonunuliwa na makampuni na ndicho kiwango ambacho wakulima wanapaswa kulima.

Mheshimiwa Spika, jambo lililojitokeza mwaka huu ni kwamba wakulima wamelima zaidi ya kiwango kilichowekewa mikataba ya kununuliwa kwenye msimu. Kwa hiyo, tumbaku ambayo imebaki sasa ni ile ya ziada ya msimu ya bajeti ambayo makampuni yanayonunua yalitaka yanunue tumbaku. Ile tumbaku yote ambayo ilikuwa kwenye bajeti ilishanunuliwa, hii ni ile ya ziada.

Mheshimiwa Spika, Serikali ziada hii hatujaiacha kama ambavyo tunaona sasa, ni kwamba makampuni yenyewe tumekaa nayo, tumeyasihi yaweze kununua tumbaku. Wameeleza kwamba walikuwa nje ya bajeti na walikuwa wanaendelea kuzungumza na vyanzo vyao vya fedha ili waje kununua tumbaku yote iliyobaki. Mjadala huo umeendelea na sasa upo mjadala wa bei kwa kuwa sasa imekuwa ni ziada ya mahitaji yao wao wanalazimisha na wanataka wanunue kwa kiwango cha chini, lakini Serikali tunataka wanunue angalau kwa bei dira ya zao lile.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo bado tumeendelea na jitihada za kutafuta nchi mbalimbali zinazoweza kununua tumbaku. Tumeenda Indonesia, China, Misri na Iran na nchi zote hizi zimeonyesha nia ya kuinunua tumbaku iliyopo sasa kwenye maghala yetu. Nchi ya Indonesia imefikia hatua nzuri, wanajadili kiwango cha tumbaku watakachochukua na sasa wanajadili kwenye eneo la bei. Watakapokamilisha mjadala wa kujua kiwango gani watanunua, Serikali sasa itaridhia.

Interest yetu Serikali ni kuona kwamba mwananchi ananufaika kwa kuuza tumbaku yake kwa bei nzuri ili sasa kila mkulima aweze kuendelea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nawasihi sasa Waheshimiwa Wabunge wenzangu, lakini pia wakulima wote wa zao la tumbaku, jana nimeona pia kwenye TBC tumbaku ipo pale Kaliua, nimemwona Mwenyekiti wa Halmashauri akieleza madhara yanayojitokeza kama ambavyo umeeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka tu nieleze kwamba jitihada za kilimo zitakapokamilika tutawapa taarifa ya hatua nzuri tuliyoifikia na hatua nzuri kwetu ni kutaka kununua tu hiyo tumbaku iliyobaki. Kwa hiyo, tunaendelea na bei tutawapa taarifa.

Additional Question(s) to Prime Minister