Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 39 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2017-06-01

Name

Amina Saleh Athuman Mollel

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali kwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, baadhi ya walimu wenye ulemavu kutegemeana na ulemavu walionao wanahitaji vifaa maalum vya kujifunzia na kufundishia katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. Vifaa hivyo ni pamoja na mashine za maandishi ya nukta nundu, shime sekio pamoja na vifaa vingine. Natambua kazi nzuri iliyofanywa ofisi yako pia Wizara ya Elimu kwa kutoa vifaa kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum. Bado tatizo lipo kwa walimu hasa kwa kuzingatia kwamba sio walimu wote wenye ulemavu wanaopangiwa kwenye shule zenye mahitaji maalum ambazo shule hizo zina vifaa hivi.

Je, wewe kama Baba na hasa kwa kuzingatia masuala haya ya watu wenye ulemavu yako chini ya ofisi yako, nini kauli yako ili kuhakikisha kwamba walimu hawa wanatekelezewa mahitaji yao na kutimiza majukumu yao pasipo matatizo yoyote?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina uratibu mzuri sana wa kuhahakisha kwamba Watanzania wenzetu wenye mahitaji maalum wanapata huduma stahiki ili waweze kukamilisha shughuli zao za siku katika nyanja mbalimbali. Moja kati ya ushahidi kwamba jambo hili limeratibiwa vizuri Serikali zote zilizopita pamoja na hii ya Awamu ya Tano tumeweza kutenga Wizara inayoshughulikia Watanzania wenzetu ambao wana mahitaji maalum. Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo mimi mwenyewe nipo, ndio hasa Wizara ambayo inashughulikia kwa ujumla wake, lakini tuna Wizara ya Elimu na Ofisi ya Rais (TAMISEMI) zote hizi zinaratibu kwa namna ambavyo tumepanga utaratibu wa kufikisha huduma hii mahali hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hawa wote ambao wana mahitaji maalum, tunatambua kwamba wakati wote wanahitaji kujielimisha, kupitia taasisi na shule mbalimbali na kule wako waelimishaji ambao wanafanya kazi hiyo kila siku. Sisi tuna utaratibu kwenye maeneo haya ya vyuo, taasisi na shule mpango wa kwanza tumepeleka fedha za kuwahudumia pale ambapo wanahitaji huduma kulingana na mahitaji yake. Wako wale ambao hawana usikivu mzuri, uono hafifu, ulemavu wa viungo, wote hawa tumewaandalia utaratibu kwa kupeleka fedha kwenye Halmashauri ili waweze kuhudumiwa. Pia walimu ambao wanatoa elimu hii nao pia tumeweza kuwawezesha kwa kuwapa vifaa vya kufundishia na kujifunzia kulingana na aina ya mahitaji ambayo tunayo.

Pia walimu hawa tunawapeleka semina mara nyingi kuhakikisha kwamba na wao pia wanapata elimu ya kisasa zaidi ili kuweza kuwahudumia vizuri hawa wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni lini Serikali itajiimarisha katika kutoa huduma hii ni kwamba Serikali imeandaa kituo cha Msimbazi Center kuwa ni eneo la kukusanyia vifaa ambavyo tunavisambaza kwenye shule na taasisi zote ili viweze kutumika katika kufundishia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikuhakikishie pia Jumanne wiki ijayo napokea vifaa vingi sana vya elimu kule Dar es Salaam ambavyo vimeletwa kwa ajili ya kupeleka kwenye shule zetu za msingi. Miongoni mwa vifaa ambavyo pia tutakabidhiwa siku ya Jumanne ni pamoja na vifaa vya Watanzania wenzetu walioko vyuoni, kwenye shule ambao wana mahitaji maalum.

Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Amina Mollel na tunajua jitihada zako za kusemea sana eneo hili kwamba Serikali iko pamoja, Serikali inaendelea kuratibu vizuri na niendelee kukuhakikishia kwamba Serikali itaendelea kuratibu na kuhakikisha kwamba vifaa vya kujifunzia na kufundishia vitapatikana na hawa waelimishaji wanapata elimu ya mara kwa mara ili waweze kuwasaidia hawa wenzetu ambao wana mahitaji maalum. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister

Name

Amina Saleh Athuman Mollel

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Question 1

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, vilevile naishukuru sana Serikali yangu inayoongozwa na Chama cha Mapinduzi, nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa majibu mazuri yenye kutia moyo na faraja kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina swali dogo la nyongeza na swali hili ni kwa mujibu wa Mwongozo wa Huduma kwa Watumishi wa Umma Wenye Ulemavu ambao katika kifungu cha 3 (12) chenye vipengele vya (a), (b), (c) na (d) vinatambua na vinasisitiza na kusema kwamba, nitanukuu kidogo; “kutambua kuwa ni haki ya watumishi wenye ulemavu kupatiwa mahitaji yao muhimu kama vile vifaa vya kuwaongezea uwezo, fedha kwa ajili ya matibabu na ukarabati wa afya zao (rehabilitation), nyenzo na vifaa hivi vitolewe na waajiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ninataka kupata kauli yako Mheshimiwa Waziri Mkuu, baadhi ya waajiri hawatekelezi majukumu haya kwa watumishi wa umma wenye ulemavu. Kama baba mwenye dhamana, nini kauli yako kwa waajiri wasiotimiza wajibu wao kama Mwongozo wa Utumishi wa Umma unavyowataka kutekeleza mahitaji hayo kwa watumishi wa umma wenye ulemavu? Ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo ameeleza kwamba, uko mwongozo wa Serikali juu ya Watumishi wa Umma wanaofanya kazi kwenye taasisi zetu za Serikali, lakini pia sio Serikali tu, hata taasisi zisizokuwa za kiserikali, unawataka waajiri wote wanapowaajiri wenzetu ambao wana mahitaji maalum lazima watekelezewe mahitaji yao ili kuwawezesha kufanya kazi yao vizuri. Kwa maana hiyo, kwa upande wa Serikali Wizara zote ziko hapa, Mawaziri wako hapa, Makatibu Wakuu wanaisikia kauli hii na kwamba lazima sasa watekeleze mahitaji na matakwa ya Serikali ya kuwahudumia hawa watumishi wenye mahitaji maalum kulingana na sekta zao. Kama yeye yuko upande wa ukarani, basi wahakikishe ana vifaa vya kutosha kumwezesha kufanya kazi hiyo vizuri na hivyo kila sekta lazima apate huduma hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatoa wito kwa sekta binafsi kutoa nafasi zaidi za ajira kama ambavyo Serikali tunawaajiri wenye mahitaji maalum. Hakuna sababu ya kukwepa kuwaajiri ati kwa sababu unatakiwa kuwahudumia. Wote ni Watanzania na wote wana uwezo na tumethibitisha uwezo wao, pia hata Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, kuthibitisha kwamba sera hii ni yetu ndani ya Serikali ametoa ajira, ameteuwa watumishi ambao wana mahitaji maalum na hawa wote mahali pao pa kazi wanawezeshwa kwa vifaa vitakavyowawezesha kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikuhakikishie tutaendelea kuajiri ndani ya Serikali na ninatoa wito kwa sekta binafsi ziajiri Watanzania wenzetu wenye mahitaji maalum wote ambao tunaajiri, wenye mamlaka ya kuajiri, na
Mwenyekiti wa Tume ya Ajira yuko hapa wa Chama cha Waajiri yuko hapa, asikie ili awaelekeze wenzake kwamba, ni wajibu wa kila muajiri kuwawezesha wenye mahitaji maalum kufanya kazi zao baada tu ya kuajiri, kama ambavyo Sera ya Serikali inahitaji kufanya hivyo. Ahsante.