Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 39 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2017-06-01

Name

Devotha Methew Minja

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kuwa ni sera ya Serikali kuboresha kilimo hapa nchini, ikizingatiwa kwamba kilimo kinatoa ajira kwa Watanzania kwa zaidi ya asilimia 80 na kilimo kimekuwa kikihudumia Watanzania kwa maana ya kujitosheleza kwa chakula, lakini kwa kuwa pia ni sera Serikali iliamua kuja na mikakati ya kuboresha sekta ya kilimo ikiwa ni pamoja na kutoa majukumu kwa mawakala wa pembejeo hapa nchini ili waweze kutoa huduma hizo za pembejeo kwa wakulima wetu hapa nchini.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, mawakala wa pembejeo wamefanya kazi yao kwa uadilifu mkubwa toka mwaka 2014/2015; 2015/2016 lakini mpaka sasa hivi mawakala hao hawajalipwa fedha zao.

Je, Mheshimiwa Waziri Mkuu ni sera ya Serikali kuwarusha mawakala ambao wamefanya kazi yao vizuri?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaanza kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, naomba nitumie nafasi hii kutoa pole kwa Watanzania, pia kwa Kambi ya Upinzani inayoongozwa na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani, Mheshimiwa Freeman Aikael Mbowe, kwa kifo cha kiongozi wetu wa kisiasa toka Kambi ya Upinzani toka Chama cha CHADEMA Mheshimiwa Philemon Ndesamburo ambaye jana alitangulia mbele za haki, nitoe pole pia kwa mke na watoto wa marehemu, nitoe pole pia kwa Wabunge wenzangu kwa sababu Mheshimiwa Marehemu Ndesamburo tulikuwa naye hapa ndani ya Bunge. Nitoe pole pia kwa Watanzania wote kwa sababu tumempoteza kiongozi ambaye alionesha uwezo mkubwa wa kulitetea Taifa, alionesha uwezo mkubwa wa kusemea Watanzania kwa ujumla wake. Sote kwa pamoja tumuombe marehemu Mzee wetu Ndesamburo ili Mwenyezi Mungu aweze kuiweka roho yake mahala pema.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nianze kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Minja, Mbunge wa Morogoro kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba sera ya Serikali, moja kati ya mambo muhimu ni kuboresha kilimo na Serikali za awamu zote zimeendelea kufanya vizuri kwenye eneo hili kwa kusisitiza kilimo na Serikali tunatambua kwa asilimia zaidi ya 80 ya Watanzania tunategemea kilimo. Hata mpango wetu wa sasa wa Tanzania ya viwanda na uchumi wa viwanda unategemea kilimo zaidi ili kuendesha viwanda vyetu. Nikiri kile ambacho umesema Mheshimiwa Mbunge kwamba tunapata msaada sana na Watanzania ambao wanajitoa katika kuunga mkono jitihada za Serikali kwa usambazaji wa pembejeo, kufanya kazi mbalimbali za kilimo na namna ambavyo wanajitahidi kuwa wavumilivu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakiri kwamba ni kweli wanatudai, lakini katika hili nataka niseme ukweli kwamba tulipoanza mfumo wa utoaji wa pembejeo kwa njia ya vocha na kuwatumia hawa mawakala kutupelekea pembejeo hizi kwa wakulima kule vijijini, zipo dosari kadhaa ambazo tumeziona. Moja ya dosari kubwa ambayo tumeiona ni kwamba baadhi ya mawakala, wachache wamekuwa siyo waaminifu sana. Kwamba walikuwa wanashirikiana na watendaji wetu wa vijiji kule katika kuorodhesha majina ya wakulima ambao si wakulima na hawapo, wamewapa mbolea, madawa na kudai fedha nyingi sana ambazo hazipo na tukajikuta tuna deni ya zaidi ya shilingi bilioni 65. Ninazo kumbukumbu kwa sababu hao mawakala wote nimekutana nao, tumekaa nao hapa tumejadili namna nzuri lakini tuliwaambia dosari hii kwa wachache wao na kwamba tumewahakikishia Serikali itawalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nataka tufanye jambo moja lazima tujiridhishe tuende kwenye vijiji kupitia watendaji ambao ni waaminifu kufanya uhakiki wa kama kweli pembejeo hizi ziliwafikia wakulima ili tueze kujua deni halisi. Nataka nikuhakikishie baada ya kuwa tumeanza uhakiki huo maana yake tumeshafanya uhakiki awamu ya kwanza. Kati ya shilingi bilioni 35 zilizoonekana kwenye orodha ya madeni ya awali tulipata shilingi bilioni sita tu ambazo Serikali inadaiwa. Lakini bado tuna shilingi bilioni 30 nyingine ambazo sasa na kwa mujibu wa mazungumzo yangu na mawakala wote ambao walikuja hapa wiki mbili zilizopita tumekubaliana. Kimsingi kwanza, tumewasihi waendelee kuwa wavumilivu pia tumeshukuru kwamba wamekuwa wavumilivu kwa kiasi hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni muhimu tufanye huo uhakiki ili tujue Serikali hasa inadaiwa kiasi gani ili tuweze kuwalipa. Nataka nikuhakikishie kwamba kazi hiyo inaendelea na tuko kwenye hatua za mwisho na tutawalipa madeni yote. Kila aliyefanya kazi vizuri kwa uaminifu, deni lake atalipwa kwa sababu hiyo ni stahili yake na kweli umefanya kazi nzuri ya kufikisha pembejeo kwa wakulima na tunatambua mchango wao na tutaendelea kuheshimu mchango wao. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister

Name

Devotha Methew Minja

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Question 1

MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, umekiri kwamba ni kweli Serikali inadaiwa, lakini umesema kwamba kuna dosari ambazo zimejitokeza katika uhakiki wa zoezi hilo na toka mwaka 2014/2015 – 2015/2016 ni muda mrefu. Serikali kwa nini haiwezi kuona kwamba kuna haja sasa ya kuharakisha zoezi hilo kama watu wanastahiki zao wakalipwa kwa maana hivi sasa ninavyozungumza ziko taarifa kwamba kuna baadhi ya mawakala hivi sasa wameuziwa nyumba zao, kuna baadhi ambao hivi sasa wanashindwa kusomesha watoto wao shule na kuna baadhi ya mawakala ambao wamefariki kwa mshituko baada ya kuona nyumba zao zinauzwa na mabenki. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kazi hii kama hawa watu mmewatambua na wamefanya kazi yao kwa uadilifi. Serikali kwenye hii Kamati ya kuandaa mawakala ilijumuisha Serikali wakiwemo wa TAKUKURU, Polisi, Wakurugenzi, Wakuu wa Wilaya. Sioni ni kwa nini uhakiki wa namna hii na ucheleweshaji wa namna hii kwa hawa watu ambao wamefanya kazi yao kwa uadilifu. Mheshimiwa Waziri Mkuu umetoa commitment kwa mawakala hawa kwa siku….

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Devotha Minja muda wako unakwisha naomba uulize swali sasa ili uweze kujibiwa.

MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Waziri Mkuu ulitoa siku 25 kwamba zoezi hili la uhakiki liwe limefanyika Tanzania nzima kwa mawakala zaidi ya 940. Ni kwa nini mpaka sasa kwa miaka hiyo toka mwaka 2014 watu hawa Serikali haitaki kuwalipa haki yao ya msingi?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kupitia mazungumzo yetu kwa pamoja na mawakala wote tulitoa muda ambao tumejipanga kufanya uhakiki wa madeni yaliyobaki ili tuweke utaratibu wa kulipa na tarehe hiyo imeishia jana tarehe 31. Kwa hiyo, sasa nasubiri taarifa kutoka Halmashauri za Wilaya zote zitakazokusanywa kwenye ngazi ya Mikoa na Mikoa itatuletea takwimu na baada ya kupeleka Wizara ya Kilimo ikishapitia watapeleka Wizara ya Fedha na malipo hayo yatalipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba baadhi ya mawakala kwa mujibu wa mazungumzo yetu walieleza adha
hiyo ambayo wanaipata, lakini kupitia kauli hii wanasikia pia hata wale wadai kwamba, wale wote ambao watakuwa na madeni sahihi baada ya kuhakikiwa ni watu wema na ndio ambao pia tunajua tunatakiwa tuwalipe. Kwa hiyo, hakuna umuhimu wa kuharakisha kunyang’anya nyumba, na kufanya vitu vingine ni jambo la kuona kwamba taratibu hizi tunazozitumia ni taratibu ambazo zinaleta tija kwa Watanzania, zinaleta tija kwa Serikali kwa sababu tungeweza kupoteza mabilioni ya fedha ambayo yangeweza pia kusaidia kwenye miundombinu nyingine, lakini sasa tumebaini kwamba hayakuwa ya ukweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natumia nafasi hii kutoa wito kwa watumishi wa Serikali wote ambao wamehusika katika hili ambao pia tutawabaini kwamba wao walihusika kwenye wizi, ubadhirifu na udanganyifu huo wote tutawachukulia hatua kali, hilo moja.

Pili, wale wote ambao wameshiriki katika hili, nirudie tena kuwahakikishia kwamba madeni hayo yakishathibitishwa kwamba fulani anadai kiasi fulani tutawalipa kama ambavyo tumetangaza, ahsante sana.