Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Hasna Sudi Katunda Mwilima (44 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naitwa Hasna Sudi Katunda Mwilima, Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kusini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza na mimi niungane na wengine waliotangulia kusema kukupa pole na mtihani mzito uliokukuta tangu tukupitishe huna hata siku tatu humu Bungeni. Lakini mimi nishauri vyombo vya ulinzi na usalama hali hii ilionekana kwa muda mrefu tumeiachia kwa muda mrefu, na kilichonisikitisha kwa sababu nimekuwa Mkuu wa Wilaya karibuni miaka kumi, ni pale ambapo na vyombo vyetu vya dola vilipoingia humu ndani vikaanza ku-negotiate muda wote waliosimama tunajiuliza hivi wanafanya nini pale wakati kitu umeshatoa amri. Mimi niombe sana tukiendelea kufanya hivi wenzetu hawa watadharau na vyombo vya dola, yaani imeniumiza sana nimeona hili niliseme kabla sijachangia kitu chochote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nizungumzie sekta ya viwanda, kwenye Jimbo langu la Kigoma Kusini tunalima michikichi, michikichi ndiyo inaleta mafuta ya mawese, lakini kinachosikitisha kwenye hii hotuba ya Mheshimiwa Rais anazungumzia dhamira yake ya kuanzisha viwanda kwenye ukurasa wa 15.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wamalaysia walikuja Kigoma kwa ajili ya kuchukua mbegu, leo Wamalaysia ndiyo wanaoongoza kuzalisha mafuta ya mawese lakini Kigoma kama Kigoma mpaka leo tumebaki kwamba tumetoa mbegu na mbegu zimekwenda Malaysia hata kama na wao walikuwa na michikichi yao walitambua fika kwamba mbegu ya Kigoma ndiyo mbegu bora, wakaipeleka Malaysia na kwenye takwimu zao wanakuambia mwaka 2011 Pato la Taifa Malaysia zao la mchikichi lilikuwa ni kama zao la nne kuwaingizia mapato, income ile ya Taifa, na wanakwambia walipata kwenye ile ringgit pesa yao ile wanaita ringgit, ringgit bilioni 53 sawa na dola bilioni 16,000.8.
Lakini sisi Kigoma mpaka sasa hivi mawese yanatengenezwa na wanawake wale wa kijijini na tunatengeneza kwa ile teknolojia ya kizamani ya asili, tunachukua masufuria makubwa tunachukua katika ule mti wa mchikichi ukishatoa ngazi kuna yale yanayobaki yale ndiyo tunakoka moto, tunaweka masufuria makubwa au mapipa tunachemsha ngazi, tukimaliza tukamua, ndiyo haya mawese mnayoyaona kwenye soko la Kariakoo pale Dar es Salaam. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha sana mimi inaniuma sana nilikuwa nimeingia kwenye website inayozungumza masuala ya palm oil, nikaona kwamba Tanzania yaani sisi tumejiweka kabisa kwamba Tanzania siyo nchi ambayo iko tayari ku-produce mafuta ya mawese. Inasikitisha kwa sababu moja, sisi pale tuna Lake Tanganyika, Congo DRC, lakini hata Congo Brazzaville, Burundi, Rwanda, Zambia tuna uwezo pia wa kuwapelekea mawese, kwa sasa tu kwa teknolojia yetu hiyo ya kizamani lakini bado tunayatoa mawese Kigoma, tunayapeleka Burundi, tunayapeleka Rwanda, tunayapeleka Congo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niombe sana hii dhamira ya Mheshimiwa Rais wetu, hebu tuombe Wizara husika ione namna ya kutuletea wawekezaji kwenye Mkoa wa Kigoma watuanzishie basi kiwanda cha mawese. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika mchikichi hili ni zao la mchikichi tunatoa pia sabuni, wengi mnazifahamu zile sabuni za rangi mbili ambayo ina rangi nyeupe na blue, zile sabuni zinatengenezwa kwa mise. Mise ni ile mbegu ya mchikichi tukishatoa mawese tunabaki na ile mbegu ya ndani ndiyo inayotengeneza sabuni. Sasa mimi niombe viwanda vya sabuni inawezekana kabisa tukavitumia pale Kigoma na angalau uchumi wa wanawake, hasa wanawake wa Kigoma ukaendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile huwezi kuzungumzia viwanda bila kilimo, hapa wajumbe wengi wamezungumzia kilimo cha tumbaku. Kilichonisikitisha ni kama vile tumbaku inalimwa tu Tabora, jamani tunalima tumbaku Wilaya ya Uvinza na ndiyo maana Tarafa ya Nguruka pale taasisi ya kifedha hii ya CRDB imeona umuhimu kuja kufungua benki pale hawafungui hivi hivi. Kama wangekuwa hawapati faida wasingekuja kufungua branch ya CRDB pale Nguruka, wamefungua kwa sababu wanajua zao la tumbaku ndiyo zao ambalo pia linatuingizia sisi Halmashauri ya Uvinza kipato.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka Disemba Halmashauri ya Uvinza, tumepata shilingi milioni 800 kwenye zao la tumbaku, ndiyo Halmashauri inayoongoza kupata ile own source kupitia zao la tumbaku. Kwa hiyo, mimi niombe Mheshimiwa Waziri Mwigulu anapokuja asisahau kulifuatilia na hili zao la tumbaku hata kama hatuna Chama Kikuu ndani ya Mkoa wetu wa Kigoma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie reli. Kwenye ukurasa wa 12 Mheshimiwa Rais amezungumzia umuhimu wa kujenga reli kwa maana ya kuboresha inayotoka Dar es Salaam, Tabora, Mwanza na Kigoma. Lakini vilevile amegusa reli ya Uvinza, kwa maana ya kutoka Uvinza, Msongati, Burundi, Isaka, Kigali, Rwanda.
Mimi niombe sana Wizara husika tusiwe tunazungumza tu maneno ambayo hayatekelezeki, niombe kweli kweli Uvinza siyo ile mnayoifahamu, maana tatizo ukisema wewe Mbunge wa Kigoma Kusini, watu wakikumbuka Mbunge aliyepita alikuwa maneno mengi humu Bungeni wanadhani tuna hali nzuri, tuna hali mbaya sana Jimbo la Kigoma Kusini. Hatuna maji, barabara hatuna, umeme wenyewe umewashwa wiki tatu zilizopita tangu uhuru, umeme kwenye Jimbo la Kigoma Kusini tulikuwa hatuna umeme. Tumewashiwa umeme kwenye Kata tatu, Kata ya Kandaga, Kata ya Kazuramimba, Kata ya Uvinza na kwa kupambana mimi kuongea na Mkurugenzi wa TANESCO Ndugu Mramba na namshukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maneno mengi hatuna maendeleo yoyote katika Jimbo la Kigoma Kusini, niombe sana Serikali iliangalie Jimbo la Kigoma Kusini kwa jicho la huruma, safari hii wananchi wa Jimbo la Kigoma Kusini wamepata Mbunge, wamempata Mbunge wa vijijini, hawajapata Mbunge wa Mataifa. (Makofi/Vigelegele)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Kigoma Kusini na niwaambie ule upotevu na maneno mengi ya propaganda yanayoenezwa kule Jimboni, mimi ndiyo Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kusini. (Makofi)
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana nitawatumikia na tumeshaanza kazi nzuri, sasa hivi tunajenga zahanati karibu vijijini 20; tunaongeza madarasa kwenye shule ambazo miaka kumi shule ina darasa moja hapa mtu alikuwepo anajiita eti Mbunge wa Mataifa, Mbunge wa Dunia, Mbunge wa Dunia kwa wananchi waliokupa kura. Mimi niwaombe sana wananchi wa Jimbo langu la Kigoma Kusini kwamba niko imara nachapa kazi propaganda zinazoendelea Jimboni msizisikilize Mbunge wenu niko hapa, nitawafanyia kazi na Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi itaniunga mkono kuhakikisha tunatekeleza ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie na suala moja lililozungumzwa hapa nadhani alikuwa Msigwa maana wote tumemsikia, tusiwa-criticize ma-RC na ma-DC. Bila ma-RC na ma-DC amani na utulivu kwenye maeneo yetu…
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana naunga mkono hoja hotuba ya Rais. (Makofi/Vigelegele)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri anazofanya za kutekeleza Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi 2015 – 2020. Pia nimpongeze Waziri wa TAMISEMI, Naibu Mawaziri, Katibu Mkuu pamoja na Naibu Katibu Mkuu. Vilevile nimpongeze ndugu yangu Mheshimiwa Mkuchika, Waziri wa Utumishi na Utawala Bora, pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri wanazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti baada ya pongezi, nitoe shukrani kwa Serikali, naishukuru Serikali kwa kutupatia shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali yetu ya Wilaya pale Lugufu. Naishukuru pia Wizara hii ya TAMISEMI kwa kutupatia shilingi milioni 800 kwa maana shilingi milioni 400 kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Kalya na shilingi milioni 400 kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Uvinza. Mheshimiwa Waziri nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambasamba hilo, bado nina ombi kwenye sekta hii ya afya. Tuna ahadi alipokuja Waziri Mkuu, tarehe 29 Julai, 2019, alituahidi kwamba TAMISEMI mtatupatia shilingi milioni 800 kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Kazuramimba na Kituo cha Afya cha Kabeba. Mheshimiwa Waziri natambua kwamba mahitaji ni makubwa ndani ya nchi lakini unaweza ukatupatia nusu yake, unaweza ukatupa shilingi milioni 400 tukazigawanya shilingi milioni 200 zikaenda Kituo cha Afya cha Kabeba na shilingi milioni 200 nyingine zikaenda Kituo cha Afya cha Kazuramimba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishukuru pia Serikali, nakumbuka nilichangia hapa kuhusiana na maboma, kilio chetu mmekisia kwenye zile shilingi bilioni 253 sisi kama Halmashauri ya Uvinza tumepokea shilingi milioni 375 kwenye shule kumi za sekondari. Tunakushukuru sana Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Rais kwa sababu makusanyo yanakusanywa na ndiyo maana miradi ya maendeleo inaweza kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niende sasa kwenye ukurasa wa 125(ix) katika kitabu cha Mheshimiwa Waziri. Mheshimiwa Waziri umezungumzia kuhusu ununuzi wa magari kwamba magari kumi yatanunuliwa kwenda kwenye Halmashauri za Nyang’hwale, Buhigwe na nyinginezo. Mheshimiwa Waziri umefanya ziara kwenye Jimbo langu kwenye ile Timu iliyoteuliwa na Mheshimiwa Rais kwenda kuangalia migogoro ya ardhi na mipaka na umeona Jimbo langu ni kubwa sana na ulikuwa shahidi na Mawaziri wenzako, Mheshimiwa Dkt. Hussein Mwinyi, Mheshimiwa Lukuvi mliona ni jinsi gani mama natawala Jimbo ambalo hata ninyi wanaume limewagusa. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nashangaa kuona kwenye ukurasa huu wa 125, Halmashauri yangu ya Uvinza hamjatenga ipatiwe gari. Mkurugenzi na Wakuu wa Idara hawana magari na hizi Halmashauri ulizozizungumza ukurasa wa 125 ni Halmashauri mpya ambazo ndiyo mnatakiwa muwapelekee Wakurugenzi magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Bajeti kwenye Vote 21 ya Hazina wametenga shilingi bilioni 20 kwa ajili ya ununuzi wa haya magari, magari ya Wakurugenzi, Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya. Nimelizungumza jambo hili na Waziri wa Fedha, Naibu Waziri na yuko hapa, Katibu Mkuu (Ndugu Doto), Naibu Katibu Mkuu pia na mwanamke mwenzangu Kamishna wa Bajeti ili kwenye hii shilingi bilioni 20 mliyoitenga ya ununuzi wa magari, naomba gari la Halmashauri ya Uvinza kaka yangu Mheshimiwa Jafo tulipate kwenye hizi pesa, usiponiletea mimi nitaona kuna upendeleo. Namtambua kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mpango amezaliwa kule Buhigwe lakini walianzaanza Uvinza ndiyo wakaenda kuhamia Buhigwe basi na mimi Uvinza niletewe gari la Mkurugenzi, kaka yangu Mheshimiwa Jafo naomba hilo ulipokee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye ukurasa wa 19 – 24, Mheshimiwa Waziri amezungumzia pia kuhusu majengo ya utawala ya Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi. Nimwombe pia kaka yangu Mheshimiwa Jafo, hivi kuna nini, mbona Uvinza haijazungumzwa na unajua fika kwamba tunayo majengo yanayosimamiwa na TBA lakini kwenye bajeti hii ya 2019/2020 tumeomba shilingi milioni 550 kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya Buhigwe, Uvinza na Kasulu lakini kwenye ukurasa huu wa 19 – 24, nasikitika Uvinza haijazungumzwa. Kaka yangu Mheshimiwa Jafo, naomba upokee, najua utanisikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA, ukurasa wa 83, nimeona kwenye bajeti ya 2018/2019 tuliidhinisha shilingi bilioni 243.29 lakini hadi mwaka huu Februari TARURA wamepokea shilingi bilioni 136.02 sawa na asilimia 56. Kwenye hili naomba nizungumzie kwenye barabara zangu, mtandao wangu wa barabara ni Km.1230. Bajeti tuliyopangiwa mwaka jana ni shilingi milioni 490, bajeti ya ukomo tuliyopangiwa kwenye TARURA mwaka huu ni shilingi milioni 490, mtandao wa barabara ni Km.1230, nimwombe kaka yangu Mheshimiwa Jafo hebu mtuongezee pesa TARURA ili tuweze kuchapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba nizungumzie kidogo mapato ya Halmashauri. Nilikuwa naangalia ukurasa wa 139, Halmashauri ya Uvinza ilipangiwa kukusanya shilingi bilioni 1.709 kwa bajeti inayoishia tarehe 30, tumekusanya shilingi milioni 850, tatizo ni nini, naomba nizungumzie kidogo vitambulisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivu vitambulisho vya wajasiriamali naviunga mkono, utaratibu ni mzuri, lakini kwenye utekelezaji kuna shida. Vitambulisho wamepewa Wakuu wa Wilaya ambao siyo Maafisa Masuuli, Maafisa Masuuli ni Wakurugenzi. Hebu sisi tushauri kama Wabunge, kule chini hivi vitambulisho tumeuliza, mimi niko Kamati ya Bajeti, tumemuuliza Waziri, hivi hizi pesa zinazokusanywa zinakwenda wapi? Tukaambiwa zinaingizwa kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa haya mapato mnayachukua kwa wale wajasiriamali wadogowadogo ndani ya Halmashauri zetu, kwa nini hizi pesa zisiingie kwenye mapato ya ndani ya Halmashauri zetu? Kwa nini hizi pesa ziende kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali wakati mkitambua fika kwamba hiki ni chanzo cha mapato cha Halmashauri. Tunaomba Mheshimiwa Waziri mkae chini na Wizara ya Fedha mlizungumzie hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kidogo kwenye suala la watumishi wetu. Watumishi wengi hawajapandishwa madaraja kwa sababu wamekaimu miaka tisa, wanatakiwa wawe Wakuu wa Idara, wanashindwa kupandishwa vyeo kwa sababu wanaambiwa sio Maafisa Waandamizi. Hebu mliangalie hili, muwaruhusu wapandishwe vyeo yaani wathibitishwe kwenye nafasi za Ukuu wa Idara huku bado hawajawa Maafisa Waandamizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambasamba na hili, naomba nizungumzie suala la watumishi ambao walikuwa Kigoma Vijijini wakahamia Uvinza hawajalipwa pesa zao mpaka leo. Niliona kwenye Fungu la Hazina kuna kama shilingi bilioni 350 kwa ajili ya kulipa madeni ya watumishi mbalimbali. Naomba na watumishi wangu wa Uvinza waweze kufikiriwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya ndani ya nchi yetu. Leo mdogo Mheshimiwa Heche alizungumza kwamba kwenye Jimbo lake afya, elimu hali ni mbaya, lakini mimi kwa taarifa nilizonazo Serikali hii inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli imepeleka shilingi milioni 400 kwenye Kituo cha Afya cha Mkende kwenye Jimbo la Mheshimiwa Heche, imepeleka shilingi milioni 400 kwenye Kituo cha Sirari, imepeleka pesa za ujenzi wa jengo la Halmashauri kwenye Jimbo la mdogo wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nikamsikia kaka yangu Japhary anazungumzia kwamba, unajua ninyi mnaweza mkaenda huku na sisi tukaenda huku, hivi mnazungumzia utawala bora, utawala bora kweli mnaufahamu ndugu zangu Wapinzani? Tumeona juzi Maalim Seif amehama CUF ameenda ACT, anaangalia tumbo lake haangalii chama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona humu ndani tulikuwa na CUF A na CUF B, leo nimemsikia Bwege anasema wote ni CUF moja. Sasa najiuliza huo ni utawala bora upi? Mlikuwa CUF A na B, kwa nini msiende ACT? Kwa hiyo, nini kinachoonekana hapa ni kwamba mmebaki CUF hii hii ya Lipumba kwa ajili ya matumbo yenu. Sasa mnapokuwa mnaisema Serikali ya Chama cha Mapinduzi muwe mnajiangalia na ninyi. (Makofi)

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. HASNA S.K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la utawala bora...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Hasna, muda wako umemalizika. (Makofi)

MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. HASNA S. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba na mimi nichangie kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Jimbo langu Kigoma Kusini lina jumla ya shule za msingi 119; lakini kati ya hizo tuna shule nne zina darasa moja na zingine zina madarasa mawili. Kwa kweli hali ya shule hizi inatisha; nyumba za walimu hakuna, nimwombe Mheshimiwa Waziri, aliangalie Jimbo la Kigoma Kusini kwa jicho la huruma ukizingatia miundombinu ya barabara kuwafikisha walimu kutoka wanakopanga nyumba hadi kwenye shule ni mibovu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Waziri ahakikishe bajeti ya Halmashauri ya Uvinza inakuja bila kukosa kwa mwaka wa fedha wa 2016/2017. Wilaya ya Uvinza tuna shule mbili za A-level na O-level za Lugufu Boys na Lugufu Girls; nimuombe Mheshimiwa atusaidie kuzisajili kuwa ya bweni ili ziweze kupata mgao wa chakula kwani tangu zianze zimekuwa ni za bweni ilhali zilisajiliwa kama za kutwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe pia Mheshimiwa Waziri, atusaidie kusajili shule mbili mpya za sekondari za kata za Mloakiziga na Basanza. Kwani wanafunzi wa kata hizi mbili wanatembea zaidi ya kilometa 15 kufuata sekondari za kata za jirani. Kwa kuwa hizi ni nguvu za wananchi tuiombe Wizara ijitahidi kuzisajili japo kuwa hazijakuwa na miundombinu yote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie pia uhaba wa vyoo. Kwenye shule zangu za Jimbo la Kigoma Kusini niombe pesa za ujenzi na ukarabati zielekezwe kama tulivyoomba kwenye bajeti ya Halmashauri ya Wilaya kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia uhaba wa nyumba za walimu ni tatizo kubwa ndani ya Jimbo langu. Sambamba na haya niombe Wizara ituletee walimu kwani Halmashauri ya Wilaya, bado ina uhaba wa walimu hususani walimu wa sayansi na walimu wa kike.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nitoe pongezi kwa dada yangu Mheshimiwa Waziri Profesa Joyce Ndalichako, kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais, kuteuliwa kuwa Mbunge na kupewa dhamana ya kuiendesha Wizara hii nyeti ya kufuta ujinga kwa watoto wetu. Nizidi kukuombea afya na achape kazi kwani wanawake tukipewa nafasi tunaweza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa pongezi kwa namna unavyoliongoza Bunge. Naomba kuchangia Wizara ya Viwanda na Biashara kwa maandishi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Kigoma Kusini liko Wilaya ya Uvinza, Mkoa wa Kigoma na ni Jimbo ambalo wananchi wake wanajishughulisha na kilimo cha michikichi pia ni wavuvi. Naomba Waziri aone namna ya kuwapatia wananchi wa uvinza miche ya michikichi ya kisasa inayozaa kwa muda mfupi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema haya kwa kuwa Mheshimiwa Waziri amesema wawekezaji wako tayari kuja kuanzisha viwanda vya mawese Uvinza. Namwahidi Mheshimiwa Waziri kama Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kusini, niko tayari kuhamasisha wakulima wa zao la michikichi, kulima zao hili kwa nguvu zote na mimi pia nitakuwa mfano wa kulima zao hili la michikichi. Hivyo, namwomba Mheshimiwa Waziri atupe kipaumbele kutuletea mbegu ya michikichi ya muda mfupi ili na sisi wananchi wa Uvinza tuweze kupata wawekezaji wa kuja kuanzisha viwanda. Pia nampongeza sana Waziri kwa mipango yake mizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie viwanda vya uvuvi. Wananchi wa Uvinza pia ni wavuvi wa samaki na dagaa, hivyo, kwa kuwaanzishia viwanda itawasaidia wavuvi kupandisha thamani mazao haya ya uvuvi. Hivyo naomba Mheshimiwa Waziri, mipango yako hii mizuri izingatie kuwaletea wananchi wa Jimbo la Kigoma Kusini viwanda vya Mawese na Viwanda vya Uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuwapongeza Waziri na Naibu Waziri kwa kazi kubwa na nzito wanayokabiliana nayo. Niwatie moyo kuwa mnaweza na muendelee kuchapa kazi na kutatua kero zilizopo ndani ya Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuzungumzia hifadhi ambazo zipo karibu ya makazi ya wananchi na kwa miaka mingi hifadhi hizo haziendelezwi badala yake hifadhi hizo zimekuwa mapori. Mfano, Hifadhi ya Lukunda Pachambi, msitu huu unaingia kwenye kata tatu; Kata ya Mtego wa Noti, Kata ya Mganza na Kata ya Nguruka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hifadhi kama hizi za Lukunda Pachambi na Tandala Ilunde ziwekewe mikakati maalum ikiwezekana baadhi ya maeneo yatengwe kwa ajili ya wafugaji ili kutatua migogoro ya wakulima na wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie migogoro ya baadhi ya vijiji na hifadhi zetu. Naona Mheshimiwa Waziri kwenye kitabu hiki cha bajeti kazungumzia tatizo hili la migogoro ya hifadhi na vijiji (ukurasa wa 61) kuwa timu iliundwa ya kutatua migogoro ya wafugaji na wakulima na ilifanya kazi kwenye mikoa mitano. Kamati ilihusisha Wizara ya Maliasili na Utalii, TAMISEMI, Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Makazi na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hapa nizungumzie mgogoro wa Hifadhi ya Mahale na vijiji vya Sibwesa, Kalilani, Lubilisi na vijiji vingine vilivyopo karibu na hii Hifadhi ya Mahale. Mgogoro wa Hifadhi ya Mahale na vijiji viwili kati ya hivyo hapo juu, kijiji cha Kalilani na kijiji cha Sibwesa una miaka zaidi ya 30 na vijiji hivi vimesajiliwa kwa mujibu wa sheria. Natambua zoezi la uwekaji wa beacons ni agizo la
Mheshimiwa Waziri Mkuu lakini vijiji hivi vilitangazwa kwa mujibu wa sheria na Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumshauri Mheshimiwa Waziri kwa nini suala hili la vijiji viwili vya Sibwesa na Kalilani ambapo mgogoro wake umedumu kwa takribani miaka 30; kwa nini basi usuluhishi usifanywe na Wizara ya Maliasili, wananchi kwa maana ya Serikali za Vijiji vya Sibwesa na Serikali ya Kijiji cha Kalilani, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Makazi na TAMISEMI?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri hili ili mazungumzo yafanyike kwa utaratibu wa Serikali na siyo hivi sasa Hifadhi ya Mahale inavamia na kuweka beacons pasipo ushirikishi wa Serikali za Vijiji na TAMISEMI, kwa sababu GN za vijiji zinaingiliwa na beacons hizi. Namuomba sana Mheshimiwa Waziri, natambua ni mtu sikivu sana na muelewa kwa miaka mingi sana. Hivyo, tuombe haki ya wananchi hawa wa vijiji hivi ilindwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuishukuru TANAPA kwa kutoa shilingi bilioni 1.6 za kujengwa madaraja matatu. Daraja la Rukoma, Daraja la Lagosa na sasa wanaendelea kujenga daraja la mwisho. Kwa niaba ya wananchi wa huu Ukanda wa Ziwa Tanganyika tunaishukuru sana TANAPA kwa msaada huo na bado tunaomba msaada wa ujenzi wa barabara inayokwenda Mahale kilometa 30.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. HASNA S.K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nichangie Wizara hii ya Maliasili na Utalii. Kwanza, nimshukuru Mwenyezi Mungu, niwashukuru pia na wapiga kura wangu wa Jimbo la Kigoma Kusini kwa dua na maombi yao yaliyowezesha kesi iliyokuwa na mvuto mkubwa zaidi ya miezi sita hatimaye tarehe 17 Mahakama imeweza kutupilia mbali shauri la Ndugu David Kafulila. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nami nijikite kwenye hoja iliyopo mbele yetu. Kwenye Wilaya yangu ya Uvinza tuna matatizo katika baadhi ya maeneo kwa mfano kwenye Kata ya Uvinza kuna Kitongoji cha Tandala. Kile kitongoji kimesajiliwa kwa mujibu wa sheria na wananchi wanaishi pale, lakini tatizo kubwa ambalo liko pale wananchi hawawezi kufanya shughuli yoyote ya maendeleo kwa sababu wanaambiwa pale ni eneo la hifadhi. Sasa unajiuliza inakuwaje eneo la hifadhi ambalo wananchi wanaishi zaidi ya miaka 35.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, nimeona kwenye hotuba yake ameonesha kwamba kwenye Halmashauri za Wilaya ana hekta karibu milioni 3.1, lakini kuna maeneo mengine yapo tayari yanakaliwa na wakaazi, tungeomba maeneo kama hayo yaweze kuachiwa na hatimaye yatumiwe na wananchi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, hicho Kitongoji cha Tandala hawana shule, wanasoma kwenye kibanda. Nimeweza kuwasaidia vitabu, nimewasaidia vifaa mbalimbali vya kujifundishia, kuna mzee mmoja amejitolea pale kufundisha watoto, watoto hawawezi kutembea kutoka pale mpaka kwenye Kijiji cha Chakuru kwenda kutafuta elimu. Kwa hiyo, ningeomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha hapa hoja yake, basi aweze kuangalia maeneo kama hayo, Wizara iweze kuachia tuendelee na masuala ya wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalo vilevile tatizo kama hilo kwenye Kata ya Nguruka, Kitongoji cha Nyangabo. Tunalo eneo la hifadhi linaitwa Rukunda Kachambi, nimeenda kutembelea pale, unakuta nyumba ya mkaazi hii hapa na GN iko nyuma ya choo. Wananchi wamebanwa kabisa, hawawezi kulima na hawawezi kufanya shughuli zozote za maendeleo. Kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Waziri washirikiane na Wizara ya TAMISEMI kama ikiwezekana zile GN zisogezwe ili wananchi wapate maeneo ya kulima na kufanya shughuli zao za kimaendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye Kata ya Itebula tuna eneo linaitwa Ipuguru. Eneo la Ipuguru ni hifadhi lakini kwa bahati nzuri hakuna wanyama wowote mle kwa zaidi ya miaka 20. Sasa kwenye maeneo kama hayo tungeomba basi hata wakulima waruhusiwe, lakini hata wafugaji pia waruhusiwe kutumia maeneo hayo. Wafugaji wamekuwa wanahangaika, wanaingiza mifugo yao kwenye mashamba, wanaingiza mifugo yao kwenye maeneo mbalimbali kwa sababu hakuna maeneo halisi ya kuchungia mifugo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tuna eneo la Kurora, nadhani Mheshimiwa Waziri analifahamu. Hili eneo lilitengwa kwa ajili ya matumizi bora ya ufugaji, lakini kwa bahati mbaya wakulima wamevamia na kusababisha wafugaji watoe mifugo yao na ianze kuhangaika kwenye mashamba. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha ajaribu kuangalia kwenye Wizara yake kuna maeneo mengi yanaitwa kama hifadhi lakini kwa bahati mbaya wananchi wameshavamia na vijiji vimeshasajiliwa kwa mujibu wa sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa namsikia Mheshimiwa Magdalena Sakaya hapa anazungumza kwamba Tabora wana zaidi ya vijiji 50 vimesajiliwa kisheria ndani ya hifadhi. Tatizo hilo Mheshimiwa Waziri na sisi pia tunalo. Kwa mfano, sisi tuna ile Hifadhi ya Mahale ambayo ipo kwenye Kijiji cha Kalilani lakini Waziri anafahamu kuna mgogoro wa zaidi ya miaka 20 baina ya wananchi wa Kalilani na watu wa hifadhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, huu mgogoro unapelekea mpaka watu wa hifadhi hata zile shughuli za kijamii za kuwachangia wananchi wa Kijiji cha Kalilani wanakuwa hawatekelezi na badala yake wanakwenda kusaidia vijiji vingine ambavyo havipakani na ile Hifadhi ya Mahale. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri aliangalie suala hili, ni mgogoro ambao uko ofisini kwa Mheshimiwa Waziri akiuliza ataambiwa. Katibu Mkuu wa CCM, Ndugu Kinana alipokuja tulimwambia na tulimkabidhi documents zote kwamba mgogoro baina ya wananchi wa Kijiji cha Kalilani na watu wa Hifadhi ya Mahale, tunaomba Mheshimiwa Waziri auangalie ili utatuliwe waweze kukaa kwa amani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, naomba pia nitoe shukrani kwa watu wa TANAPA kwa sababu sisi kwenye ile Hifadhi ya Mahale watalii wanapokuja wanatumia usafiri wa boti kwa sababu barabara hakuna. Tunazo kilometa kama 30 ambazo mtu hawezi kupita kwa gari na tuna mito kama mitatu ambayo inahitajika ijengewe madaraja.
Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru watu wa TANAPA kwenye bajeti hii ya 2016/20167, wameweza kututengea shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kutengeneza barabara ile na tulipitisha kwenye kikao chetu cha barabara cha Mkoa wa Kigoma. Kwa hiyo, nimeona pia nitoe shukrani zangu za dhati maana wangeweza kupeleka sehemu nyingine, lakini wameona waje kusaidia ili watalii nao waweze kupita bila tatizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe pia Mheshimiwa Waziri aangalie sana kama inawezekana kuboresha zile speed boat za Mahale kwa sababu kwenye Ziwa Tanganyika tuna kitu kinaitwa Rukuga, ni upepo mkali sana, unapokuwa mkali hata meli ya Liemba haiwezi kupita. Hata kama sikuangalia kwenye bajeti kama wametenga namna yoyote ya kuboresha usafiri maeneo yale, naomba waone umuhimu wa kuwaongezea watu wa Mahale speed boat nyingine kwa ajili ya kubeba watalii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nichangie kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, ukurasa wa 32. Asubuhi mdogo wangu Mheshimiwa Doto alichangia kuhusiana na masuala ya unyanyasaji wa wafugaji kwenye hifadhi. Mimi nilikuwa Mkuu wa Wilaya ya Mbogwe, Mbogwe ilizaliwa kutoka Bukombe, Mkoa mpya wa Geita. Matatizo hayo kwenye Hifadhi ya Kigosi wakati yametokea kwenye ile Operesheni Tokomeza, nilikuwa Mkuu wa Wilaya pale. Kwa kweli kabisa alichosema mdogo wangu ni kweli, unyanyasaji ni mkubwa sana. Wanapowakamata, hawawakamati tu kwamba wafuate sheria, sheria imewekwa kwamba watu wanapokamatwa wameingiza mifugo kwenye hifadhi wachukuliwe hatua gani. Wale maaskari badala ya kufanya hivyo wanawa-harass wale wananchi na wanawapiga risasi ng‟ombe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge kwamba tuko hapa leo kuipitisha bajeti ya Wizara hii ya Maliasili na Utalii, tunatambua fika kwamba Mheshimiwa Waziri ndiyo kwanza amepewa dhamana kwenye hii Wizara na hii ndiyo bajeti yake ya kwanza. Kwa hiyo, badala ya kumshambulia au kum-attack moja kwa moja tumpe ushauri ili aweze kupokea, aangalie upungufu uliojitokeza kwenye Wizara yake siku za nyuma na aweze kuyafanyia kazi. Huu ndiyo ushauri ambao napenda kuutoa. Namfahamu Mheshimiwa Maghembe, najua ni mchapakazi na msikivu, yote haya tunayoyasema hapa atayasikia, atayapokea na atayafanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee tu kumtakia kila la kheri Mheshimiwa Waziri na nimwambie kwamba aangalie sana sekta ya wanyama pori. Wale maaskari wanaolinda hifadhi hizi wamekuwa ni shida kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niombe Mheshimiwa Waziri wa Maliasili kuna mambo mengine wawasiliane pia na Waziri wa Kilimo. Kwa mfano, haya matatizo ya mifugo kuvamia hifadhi na wakati Uvinza tunazo ranch za Serikali kama tatu lakini zile ranch inaonekana siku za nyuma walipewa watu ambao hawako tayari kuzitumia na badala yake wanazikodisha kwa pesa nyingi. Kwa hiyo, kwenye matatizo kama haya wakae chini Wizara na Wizara, kwa mfano Wizara ya TAMISEMI na Wizara hii waone matatizo hayo ya GN ambazo zimeingia mpaka kwa wananchi walikojenga waweze kusogeza ili kutatua migogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. HASNA S.K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba na mimi nichangie kwenye Kamati hizi mbili ambazo zimewasilishwa leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wangu, nitazungumzia sana suala la watumishi. Kwenye Halmashauri yetu ya Uvinza tuna tatizo kubwa sana la watumishi. Hivi karibuni tulipokea barua kutoka Wizara ya TAMISEMI ikimtaka Mkurugenzi kuwasimamisha kazi watumishi wote ambao walikuwa wanafanya kazi kama vibarua ili wakae pembeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mbunge mwenzangu hapa kutoka Lushoto alikuwa anatolea mfano kwamba wao Halmashauri yao wanatumia shilingi milioni 28 kwenye own source kwa ajili ya kuwalipa watumishi ambao hawana vibali. Sasa nikawa najiuliza maswali, kwa nini Halmashauri zingine ziruhusiwe kuendelea kufanya kazi na wale watumishi ambao hawana vibali na Halmashauri zingine tuletewe barua ya kuwasimamisha watumishi ambao wameshafanya kazi zaidi ya miaka minne. Zaidi ya miaka minne mtu anafanya kazi, anaitumikia Serikali halafu ghafla tunawaweka pembeni tunasema kwamba ninyi ni vibarua hamna ajira rasmi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niliona hili nilizungumzie kwa sababu Halmashauri hizi mpya zilizoanzishwa 2012 zina uhaba mkubwa sana wa watumishi. Kwa hiyo, tutaomba Mheshimiwa Waziri husika, wa Utumishi na Waziri wa TAMISEMI waone namna ya kuliangalia hili. Tunaweza tukaendelea kutumia own source yetu kama ambavyo wenzetu wa Lushoto wanavyotumia ili tuwalipe hawa watumishi waendelee kutekeleza majukumu ya Halmashauri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna tatizo pia kubwa la watendaji wa vijiji na leo kupitia wenzangu waliochangia nimejifunza kitu. Kwenye Halmashauri ya Uvinza Watendaji wa Vijiji 75% ni Walimu Wakuu wa Shule za Sekondari na Walimu Wakuu wa Shule za Msingi. Leo tunasema watoto wanafeli kwenye shule za msingi, leo tunasema watoto wamefeli, matokeo sio mazuri kidato cha nne. Itakosaje kuwa matokeo mabaya wakati Walimu Wakuu hao hao kwenye baadhi ya Halmashauri ndiyo tunawatumia kama Makaimu Watendaji wa Kata na Makaimu Watendaji wa Vijiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe tu Wizara husika, Wizara ya TAMISEMI iliangalie hili ili ikitoa waraka, natambua kwamba kuna waraka mbalimbali huwa zinatolewa Serikalini, ili wakae chini wachunguze ni Halmashauri zipi zinazotumia Walimu Wakuu wa shule kama Watendaji wa Vijiji na Halmashauri zipi zinazotumia Watendaji wa Vijiji kupitia jamii zetu. Kwa nini tusitumie tu jamii? Kwa sababu kama kwenye kijiji mimi ninavyofahamu unaitishwa Mkutano Mkuu wa Kijiji wanaulizana nani miongoni mwetu anastahili kukaimu nafasi ya Mtendaji wa Kijiji? Then wanapiga kura yule aliyechaguliwa anakaimu kuliko kama sisi wengine Walimu hao hao ni wachache, hatuna watumishi lakini na hao hao wanafanya na majukumu ya kijiji. Kwa hiyo, niliona hili nilizungumzie kwa namna hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ni uhaba wa watumishi kwenye sekta ya elimu na afya. Halmashauri yetu tumejitahidi sana kuhamasisha, tuna vijiji 61, tunazo zahanati 33, lakini tumehamasisha hadi sasa tuna takriban zahanati 15 zimejengwa lakini hakuna watumishi. Kwa hiyo, unakuta tuna zahanati ambazo tayari tungeweza kuzianzisha lakini kwa uhaba wa watumishi wa afya tunashindwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na wenzangu waliochangia kusema kwamba zoezi la uhakiki wa watumishi limeshachukua takriban mwaka mzima, limekwenda vizuri na sisi tunampongeza sana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Utumishi, lakini sasa waone ni namna gani wanaweza wakatoa ajira mpya ili sasa vijana wetu waliomaliza vyuo mbalimbali waajiriwe, huu uhaba wa watumishi kwenye sekta za afya, elimu na kilimo uweze kuondoka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ambalo nataka kulizungumzia ni ugumu wa miundombinu na mazingira katika Halmashauri mpya. Na-declare interest kwamba nimekuwa DC siku za nyuma, tulikuwa tunaona kutoka Wizara ya TAMISEMI, wale wanaoshughulika na masuala ya Local Government wanatembelea zile Halmashauri mpya kuangalia changamoto ambazo wanazo na kuona ni jinsi gani wazisaidie ili ziweze kusonga mbele. Sasa Halmashauri ya Uvinza, tunatumia majengo yaliyoachwa na kambi zile za wakimbizi. Takriban four years tuko pale! Tunaishukuru Serikali juzi kupitia hii bajeti tunayomaliza 2016/2017 tumepata shilingi bilioni 1.1 kwa ajili ya kujenga jengo la Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tangu Halmashauri ile ianzishwe hatuna magari ya kuwasababisha Wakuu wa Idara na Mkurugenzi waweze ku-move kwenye vijiji wasimamie miradi ya maendeleo. Sasa naomba Serikali iweze kuangalia Halmashauri hizi maana unasikia Halmashauri kongwe zina miaka 20 bado zinapelekewa magari mapya lakini zile Halmashauri ambazo ni changa wala hazifikiriwi kupelekewa magari ili waweze kufanya kazi zao za kila siku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Waziri wa TAMISEMI aangalie Halmashauri hii ya Uvinza kwa jicho la huruma. Nashukuru sana tumepata Mkurugenzi, ni mpya lakini anajua majukumu yake ya utendaji wa Halmashauri. Kwa hiyo, tunaomba sana Mheshimiwa Waziri tuangalie namna ya kuwezesha Halmashauri ya Uvinza ili tuweze kusonga mbele katika kutekeleza majukumu yetu ya maendeleo….
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi pia naomba niungane kuchangia kwenye hii kamati ya Bajeti. Kwanza nililokuwa nataka nichangie baada ya kupitia hii taarifa nimeona tumejikita sana kuzungumzia robo ya kwanza ya bajeti ya mwaka 2016/2017, lakini sote tunatambua kwamba pesa za maendeleo zimechelewa sana huko vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, ninaangalia kwenye bajeti yetu ya mwaka 2016/2017 tulipanga shilingi bilioni tisa kutekeleza miradi ya maendeleo kwenye Halmashauri yetu ya Uvinza, lakini hadi sasa tunavyoongea mwaka jana mwezi Disemba tumepokea shilingi bilioni mbili, sawa na asilimia 22. Sasa ninajiuliza maswali, hivi kweli tutatekeleza vipi hii miradi ya maendeleo maana sasa tumeinga mwaka wa pili tangu tuchaguliwe huko na tuliahidi mambo mengi. Kwa hiyo, ninaomba kwenye Kamati hii ya Bajeti nimeona imeshauri sana, lakini haijafikia makubaliano na Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, nilikuwa naangalia ukurasa wa 10. Ukiangalia ukurasa wa 10, Fungu Namba 49, Wizara ya Maji na Umwagiliaji unaona kabisa kwamba kulikuwa na hoja ya kuongeza tozo kwa kila lita ya mafuta, petroli na dizeli, kuongeza 50 ili ifike 100. Lakini lengo la Kamati ilikuwa ni kwamba fedha hizi zipelekwe kwenye Mfuko wa Miradi ya Maendeleo ya Maji Vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia matokeo ya ushauriano Kamati inasema haijafikia makubaliano na Serikali. Sasa naanza kujiuliza kama hatujafikia makubaliano na Serikali, hii miradi ya maji ambayo mingi imeanzishwa tangu kwenye bajeti ya mwaka 2012/2013 mpaka leo miradi ya maji haijafikia hata asilimia 50.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa pia, ninaangalia kwenye ukurasa huohuo, tunazungumzia kwamba, ujenzi wa zahanati na vituo vya afya kwa mwaka 2016/2020. Ukienda kwenye hoja Kamati ilipendekeza shilingi bilioni 30 ziende kwenye utekelezaji wa ujenzi wa zahanati na ujenzi wa vituo vya afya, lakini hadi sasa Serikali inasema bado haijapata itatumia shilingi ngapi katika utekelezaji wa hiyo miradi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana tumepitisha bajeti na tunaendelea na mwaka huu tena tutapitisha bajeti. Sasa hivi tunavyoongea tuko kwenye robo ya tatu ya bajeti ya mwaka 2016/2017, pesa kule chini zinaenda kwa asilimia ndogo sana. Kwa hiyo, tuombe Serikali iwe sikivu na tunafahamu Serikali yetu ni sikivu, Serikali ya Chama cha Mapinduzi iweze kusikia na kuona ni jinsi gani tunapeleka pesa za maendeleo huko chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia, nizungumzie zile milioni 50 kupeleka kule vijijini. Ukiangalia kwenye ukurasa wa 11 unaona kwamba Kamati imeshauriana na kukubaliana na majibu wa Serikali kuwa imeridhia shilingi bilioni 59.5 sawa na asilimia 45 ili iweze kutumika katika kupeleka vijijini na kutafuta zile pilot area. Sasa mimi nikawa naangalia hii pilot program hivi ni Wilaya zipi ambazo zimekuwa specifically kwamba zimekuwa ni pilot area kwa ajili ya utekelezaji wa hizi shilingi milioni 50!
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nilikuwa ninaomba, najua kabisa tuna changamoto nyingi, lakini pia nimeona ukusanyaji wa mapato umekwenda kwa kasi. Ukiangalia kuna Mbunge mmoja amezungumzia kwamba, hata polisi imeingilia kwenye upande wa makusanyo. Polisi ina haki ya kuingilia upande wa makusanyo kwa sababu yale makosa yanayofanyika barabarani, polisi ikikusanya ndiyo pesa zinaingia huko katika miradi ya maendeleo mbalimbali nchini. Kwa hiyo, hatuwezi kubeza jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali yetu, hususan kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani kwa Polisi kukusanya kodi mbalimbali za makosa. Kwa hiyo, niwatie moyo polisi, nimtie moyo IGP, nimtie moyo pia Waziri wa Mambo ya Ndani kwamba aendelee na ukusanyaji huo wa kodi ili tuweze kufanya maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la kilimo; mwenzangu aliyekaa amesema zaidi ya asilimia 73, mimi ninavyofahamu ni asilimia 82 inajihusisha na suala la kilimo Tanzania, lakini pembejeo zimechelewa huko vijijini. Watu wamelima, watu wamepanda, pembejeo hazijafika. Ukipita vijijini ni malalamiko. Sasa tunajiuliza kama pembejeo zinachelewa, wakulima wataweza kuvuna vipi? Makusanyo ya Halmashauri nyingi nchini zinapata makusanyo yake kupitia mazao mbalimbali yanayolimwa kule vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba sana kwenye bajeti hii inayokuja tuweze kutenga pesa nyingi kwenye Wizara ya Kilimo. Wizara ya Kilimo ni Wizara nyeti, tunalima tumbaku, tunalima pamba, tunalima alizeti, lakini tunahitaji pembejeo za kutosha. Tunahitaji ruzuku iongezwe zaidi kama mwenzangu alivyosema kwenye mbegu.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia nchi ya viwanda, lakini hali ya umeme ni mbaya sana. Kwa mfano, mimi naongelea Jimbo langu, katika vijiji 61 nina vijiji vitatu tu vyenye umeme, lakini Wilaya ile ndiyo tunaozalisha michikichi. Tunazungumzia hapa tuanzishe viwanda vya mawese, tunaanzishaje viwanda wakati umeme wenyewe hakuna. Tunafaya sensitization kwa wananchi waone umuhimu wa kulima zao la mchikichi, umuhimu wa kulima mazao mbalimbali ili tuweze kupata raw materials ya kuweza ku-maintain hivi viwanda. Ninaomba pia kwenye mradi, kama alivyozungumza mwenzangu, lile deni la TANESCO lilipwe, tulipe deni la TANESCO ili miradi ya umeme vijijini iendelee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo pia, tuiombe Wizara husika iweze kupunguza bei. Wananchi wengi walioko vijijini hawana uwezo wa kulipia umeme kama ambavyo sasa hivi wanavyotaka hiyo pesa tuilipie. Naomba Wizara yenye dhamana ione ni jinsi gani itaweza kupunguza bei ya umeme ili basi wananchi waweze kukidhi haja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba pia kuchangia kwenye miradi ya barabara, hali ya huko vijijini tunatofautiana, sisi miundombinu yetu ni mibaya sana. Niombe katika bajeti tuweze basi zile pesa zilizotengwa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya barabara mbalimbali vijijini ziweze kupelekwa ili miradi hii iweze kutekelezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nizungumzie suala la TRA (ukusanyaji wa mapato). Najua dhamira ya Serikali ni njema, hali huko chini sio nzuri sana, unakuta mfanyabiashara kwa mujibu wa Sheria ya TRA wanasema ile turn over ya mwaka kama ni less than 14 million hautakiwi kuwa na ile mashine ya kukatia risiti wateja. Lakini kwenye maeneo mengine kama Dar es Salaam unakuta mfanyabiashara ameshafanyiwa assessment na akaambiwa kwamba labda biashara yako ni milioni tisa ndiyo turn over kwa mwaka, lakini bado baada ya miezi miwili wanarudi wanamwambia tukiiangalia biashara yako kwa macho, tunaona kwamba wewe unatakiwa uwe na risiti, aahhaa! Sasa umeshafanya, umemkadiria, umeona kwamba yuko less than 14 million. Kwa nini tena urudi umwambie kwa macho tu…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Kamati ya Bajeti kwa Taarifa yao nzuri, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema ya kuweza kusimama hapa kuchangia kwenye Wizara hizi mbili; kwenye mwelekeo wa bajeti inayokuja mwaka 2017/2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na Wizara ya TAMISEMI. Kumekuwa na changamoto kubwa sana kwenye Wilaya 19 zilizoanzishwa hapa nchini ikiwemo Wilaya ya Uvinza. Ninavyoongea, tangu Wilaya ya Uvinza ianzishwe, haina Hospitali ya Wilaya. Tunatambua kabisa kwamba Wizara ya TAMISEMI ni Wizara mtambuka, ndiyo inayosimamia masula yote ya Halmashauri zote nchini. Sasa namwomba sana Mheshimiwa
sana Waziri, akiungana na Naibu wake waone ni jinsi gani wanaweza kutupitishia maombi. Tumeleta barua ya maombi kwenye maombi maalum, shilingi bilioni mbili; tunaomba hizo shilingi bilioni mbili tupewe ili tuweze kujenga hospitali na tayari tumetenga eneo la ujenzi, ekari 30.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, ukipitia kwenye taarifa ya Mheshimiwa Waziri, ya mwelekeo ya mapato na matumizi ya bajeti ya 2017/2018, ukurasa wa 103 utaona kwamba kwenye Mfuko wa Pamoja wa Afya, Halmashauri ya Uvinza haijapangiwa hata shilingi moja. Tuna Halmashauri takriban tisa, lakini tuna Majimbo manane. Kati ya Majimbo hayo, ni Jimbo moja tu ndilo linaloongozwa na mwanamke.
Sasa ninaanza kupata shida na msemaji mmoja aliongea juzi ndugu yangu Mheshimiwa Chikambo kwamba Wizara inaongozwa na wanaume. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mwanamke, yaani Halmashauri zote zitengewe pesa kwenye Mfuko wa Pamoja wa Afya, Halimashauri yangu ya Uvinza isitengewe hata thumni, kulikoni? Mheshimiwa Waziri nazungumzia kwenye pesa zile za nje za forex; sina hata thumni, nimejisikia vibaya sana. Nimeangalia kwenye ule ukurasa, nikanyong’onyea, nikasema kulikoni? Ila sina mashaka, Mheshimiwa Simbachawene ni jirani yangu, nadhani utaliangalia hili na utarekebisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kwenye ukurasa huo huo kwenye pesa za lishe na ulinzi wa mtoto, sina hata thumni. Wakati Halmashauri yangu ya Mkoa wa Kigoma inapitisha bajeti, Hazina ilikubali kututengea pesa; nasi tuna watoto 86,388 ambao wapo chini ya umri wa miaka mitano. Sasa ninashangaa, Hazina wamekubali kutuwekea shilingi 86,388,000 lakini kwenye hiki kitabu hakuna hata shilingi. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri, nakuomba sana, kulikoni? Maana yake ukiona mwanamke amepita kwenye Jimbo, ujue alipambana kweli kweli, siyo mambo ya ki-sport sport! Hatukuwa na mambo ya ki-sport sport mpaka tukaingia hapa. Sasa tunaomba Mheshimiwa Waziri unisaidie kama ambavyo Majimbo mengine yalivyopata pesa, basi nami naomba unifikirie. Utakapokuja kufanya majumuisho hapa, uniambie utanisaidiaje
kwenye huo Mfuko wa Pamoja wa Afya pamoja na lishe na ulinzi wa mtoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, naomba nizungumzie Kituo cha Afya cha Nguruka. Tarafa ya Nguruka ina Kata nne na hiki kituo kinahudumia wananchi zaidi ya 100,000 na kitu na wanahudumia vilevile Kata ya Usinge kutoka Wilaya ya Kaliua. Sasa tumekuwa tunaomba mara kwa mara kupewa pesa ya kuweza kukipanua hiki Kituo cha Afya ili kiweze kuwa na huduma zinazostahili sambamba na
kuongeza wodi ya wanaume na wodi ya wanawake. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI aweze pia kutuangalia katika suala la Kituo chetu cha Afya cha Nguruka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumzia hayo, naomba pia nizungumzie Mfuko wa Barabara. Mfuko wa Barabara kwa bajeti hii tunayokwenda kumaliza tarehe 30 Juni, tuliidhinishiwa shilingi milioni 695, lakini hadi sasa tumepokea asilimia 45 tu. Sasa kwenye hii coming budget tunayotarajia ambayo itaanza tarehe 01 Julai, tumepitishiwa shilingi milioni 495 tu na sisi kwenye Jimbo letu, kwenye Halmashauri hii, hakuna barabara yoyote yenye lami. Mtandao wa barabara ambazo zina changarawe ni kilometa 44 tu na siyo zaidi ya hapo. Kwa hiyo, naomba hebu tuwe tunaangalia hizi Halmashauri mpya, tuwe tunazipa kipaumbele zaidi kuliko zile Halmashauri ambazo zimeanzishwa
miaka mingi. Niliona hilo nalo nilizungumzie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nizungumzie suala la uanziswaji wa Mamlaka ya Mji Mdogo wa Nguruka. Tumekuwa tunaleta barua kwenye Wizara hii ya TAMISEMI na huko nyuma tuliambiwa kwamba hakuna shida, Mamlaka ya Mji Mdogo inaweza ikaanzishwa, lakini changamoto ambayo tunayo ni nini? Kata ya Nguruka ina vijiji viwili; Kata ya Itebula ina vijiji viwili; Kata ya Mganza ina vijiji sita; na Kata ya Mteguanoti ina vijiji vine. Sasa unaangalia kwamba kama hatuwezi kuongeza, maana yake hizi Kata ni kubwa mno. Tunachoomba Wizara ya TAMISEMI mmesema hamna mpango wowote wa kuongeza Kata, wala vijiji, lakini kuna Majimbo mengine ni makubwa mno, lazima mfikirie namna ya kutuongezea kugawanya Kata na vijiji ambavyo ni vikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, Jimbo langu mimi lina square meters 10,178. Dada yangu Mheshimiwa Anne alikuwa anaongelea hapa, kwamba Same ina square meters 5,000, nikashtuka; kwangu ni 10,000. Kijiji kimoja mpaka ukimalize, unatakiwa ufanye ziara kwa siku mbili. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri uone namna ya kutukubalia maombi yetu pale tutakapoyaleta ili tuweze kuongeza vijiji kwenye
Kata ya Nguruka, Kata ya Itebula ili uanzishwaji wa Mamlaka ya Mji Mdogo wa Nguruka utakapokuwa unaanza, basi tuweze kuwa na vijiji vya kutosha mamlaka hiyo iweze kuendeshwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie migogoro baina ya vijiji na hifadhi. Kwenye Kijiji changu cha Sibwesa na Kalilani wamekuwa wana mgogoro zaidi ya miaka 30 na Hifadhi ya Mahale, lakini cha kushangaza, tunatambua kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu hivi karibuni alitoa tamko kwamba kila taasisi za Serikali zihakiki mipaka yao. Ninavyofahamu, unapotaka kufanya uhakiki wa mipaka, wewe kama ni Wizara fulani kwa mfano ya Maliasili, maana yake nazungumzia Hifadhi ya Mahale, lazima ushirikishe na Wizara ya TAMISEMI. Kwa sababu hivi vijiji
vimewekwa kwa mujibu wa sheria na aliyetangaza tangazo kabla ya kutangaza hivi vijiji ni Waziri Mkuu; ni Ofisi hiyo hiyo ya Waziri Mkuu. Sasa iweje leo Mkurugenzi wa Mahale anakwenda kuweka alama (beacons) kwamba hapa ndiyo sisi Mahale tunatakiwa mipaka yetu iishie; anaingilia mpaka zile GN za Serikali ambazo zimewekwa kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri mambo haya yakafanyika kwa mashirikiano. Nimewahi kuwa DC pale Arumeru, migogoro yote ya Arumeru tulikuwa tunafanya kwa ushirikishwaji. Unahusisha Wizara ya Ardhi, unahusisha Wizara ya TAMISEMI na kama kuna hifadhi, unahusisha pia na Wizara ya Maliasili. Sasa tatizo ambalo tunalo, tuna Wakuu wa Wilaya wengine ambao hawaelewi watatue matatizo ya wananchi kwa namna gani. Napenda kumuelimisha ana… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. HASNA S.K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono, hoja japo m da ni mdogo, nilitaka niseme
zaidi ya hapo. Ahsante sana.

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi kwa niaba ya wananchi wa Jimbo langu la Kigoma Kusini naomba nichangie Wizara hii nyeti yenye masuala ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwanza niipongeze Wizara hii chini ya uongozi wa Mheshimiwa Waziri Profesa Mbarawa pamoja na Naibu wake, lakini pia niwapongeze watendaji wote wa Wizara hii, kwa kweli kwa Jimbo langu mimi la Kigoma Kusini Wizara hii imetutendea mema mengi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nianze kuzungumzia barabara ya Simbo – Kalya. Barabara hii ya Simbo – Kalya kwa muda mrefu sasa inatengenezwa kwa kiwango cha changarawe. Sasa tulikuwa tuna ombi, kwanini Wizara isifike sasa mahali ikaona namna gani inaweza ili ikafanya kutengeneza barabara hii kwa kiwango cha lami ili kuondoa usumbufu wa kufanya maintenance ya mara kwa mara?
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba pia nizungumzie kipande cha barabara kutoka Uvinza kwenda Malagarasi kilometa 51.1. Barabara hii ina muda mrefu sana, hawamalizii kile kiwango cha lami kinachokwenda kuunga mpaka Malagarasi. Nimeona kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri anazungumzia kwamba tunatarajia pesa za wafadhili kama mfuko wa Abudhabi na mifuko mingine. Sasa nimuombe Mheshimiwa Waziri aone namna ya kutusaidia wananchi wa Uvinza kumalizia hizi kilometa 51.1, na ikizingatiwa kamba barabara hii ni barabara kubwa inayopita Ma-semi trailer yanayobeba mizigo ya kwenda Congo na kwenda Burundi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie vile vile kipande cha kilometa 40 kinachotoka Chagu hadi Kazilambwa. Kipande hiki ni korofi sana wakati wa mvua, na tumekuwa tunaomba hapa, hata bajeti iliyopita nilimuomba sana Mheshimiwa Waziri aone ni jinsi gani wanaweza wakatafuta namna ya kumalizia hizi kilometa 40. Kwa hiyo ninaomba sana Mheshimiwa Waziri utusaidie wana Uvinza namna ya kutumalizia kipande hiki cha Chagu – Kazilambwa Wilaya ya Kaliua.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie vile vile barabara ya kutoka Uvinza kwenda Mpanda ambayo tuna kilometa kama 60 zinazokwenda Mishamo. Sisi tunacho kijiji kinaitwa kijiji cha Ubanda. Wananchi wa kijiji cha Ubanda wanatoka kata ya Kalya hawawezi kusafiri kwa njia yoyote zaidi ya kutumia hii barabara ya Mpanda. Kwa hiyo, tunamuomba sana Mheshimiwa Waziri aone namna ya kuangalia hizi barabara za vijijini, hali ya huko vijijini si nzuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba atumalizie hicho kipande cha kilometa 60, na ikiwezekana basi waweze kuanza ujenzi wa hizi kilometa 35 kama alivyotenga kwenye kitabu chake, kwenye taarifa yake hii ya bajeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nizungumzie masuala ya uchukuzi. Jimbo langu nina vijiji kama 33 viko Ukanda wa Ziwa Tanganyika. Nimeona kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri amezungumzia ujenzi wa gati tatu; gati ya Sibwesa, gati ya Lagosa na gati ya Kalya; na amesema kwamba gati ya Sibwesa na gati ya Lagosa ujenzi umekemilika kwa asilimia 50. Mheshimiwa Waziri mimi nikuombe sana, nimeshaomba sana hapa, nimeomba kwenye bajeti iliyopita lakini nimeomba pia katika maswali ya nyongeza. Wananchi wa Ukanda huu wa Ziwa Tanganyika wanapata tabu mno. Usafiri wanaotumia ni meli ya Liemba, hatuna gati hata moja inayofanya kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna gati ambayo ilitakiwa ijengwe, hiyo ya Kalya, Sibwesa, gati ya Mgambo, gati ya Lagosa na gati ya Kirando, hakuna iliyokamilika hata moja tangu uhuru, miaka 56. Tunaomba Mheshimiwa Waziri, nilikuwa napitia kwenye kitabu chako nimeona baadhi ya maeneo wana magati matatu, wana magati manne; nini tatizo kwenye Jimbo la Kigoma Kusini kutupa hata gati tatu zikamilike ili meli ya Liemba iweze kupata maeneo ya kuegesha na abiria wapate kutoka kwenye usumbufu?
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nizungumzie Daraja la Ilagala. Tumekuwa tunapata shida sana na Daraja la Ilagala na Mheshimiwa Waziri umetuahidi kwamba Wizara yako inafanya mkakati wa kutujengea daraja la muda mfupi ili wananchi pamoja na magari waweze kuvuka.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile mimi ni mkazi wa Kigamboni. Sambamba na daraja langu la Ilagala naomba pia nizungumzie Daraja la Nyerere – Kigamboni. Tuna kilometa
3.8 kutoka Tungi kwenda Kibada; hivi karibuni tumekwama pale siku tatu tunashindwa kufika kwenye daraja kwa sababu ya mvua nyingi zinazonyesha pale Kigamboni. Kwa hiyo, ninaomba Mheshimiwa Waziri, maadamu umezungumzia kwamba kuna pesa zimetengwa za kujenga hizi kilometa 3.8 kutoka Tungi kwenda Kibada tunaomba basi uweze kutekeleza.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nitoe pongezi kwa Serikali kwa ujenzi wa meli mpya ambayo inatarajia kuanza hivi karibuni, ambayo itakuwa inabeba abiria pamoja na mizigo kwenye Ziwa Tanganyika; natoa pongezi sana, lakini pia natoa pongezi kwa ukarabati wa meli ya Liemba ambapo wote tunajua hii meli ya Liemba kihistoria ni meli ya Wajerumani na nimeona kwamba Mheshimiwa Waziri anasema wanataraji kusaini mkataba hivi karibuni ili maintenance hiyo iweze kufanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo naomba pia nitoe pongezi kwa Serikali kwa ununuzi wa ndege mbili. Wananchi wa Kigoma tulikuwa tunapata taabu sana na usafiri, lakini tangu Mheshimiwa Rais, amenunua hizo ndege mbili kwa kweli wananchi wa Kigoma tunamshukuru sana tena sana kwa kuturahisishia usafiri wa Kigoma.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo naomba pia nizungumzie ujenzi au upanuzi wa uwanja wa ndege wa Kigoma. Mheshimiwa Waziri unakumbuka mwaka jana kulikuwa na mvutano wa wananchi wa Kibirizi na wananchi wa maeneo ya jirani ya uwanja wa ndege. Sasa tulikuwa tunaomba basi upanuzi uanze mara moja ili kuondoa ile kizungumkuti, kulikoni Serikali imelipa fidia wananchi lakini hakuna lolote linaloendelea la kupanua uwanja wa ndege wa Kigoma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nizungumzie reli. Kwa sababu ujenzi wa reli hii ya standard gauge inapita pia kwenye Jimbo langu kwa maana Uvinza kwenda Msongati, Mpanda mpaka Karema. Hizo kilometa 150 ambazo mpo katika hatua ya kufanya upembuzi yakinifu, Mheshimiwa Waziri mimi nipongeze sana kwa jitihada hizo. Lakini pia nipongeze jitihada za reli yetu ya kati ambayo inatoka Kaliua
- Mpanda - Tabora – Kigoma kilometa 411; nipongeze pia kwani hiyo pia ni jitihada nzuri kwa sisi wananchi tunaotumia reli ya kati.
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: ahsante sana.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niombe kuchangia kwa maandishi kama ifuatavyo:-
Mheshimwia Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja asilimia 100. Pili nitoe shukrani zangu za dhati kwa Wizara hii hususan Mheshimiwa Waziri Ummy Mwalimu na Naibu wake kwa msaada mkubwa walioutoa kwenye vituo vya afya viwili; kituo cha Bulungu kupewa ambulance na kituo cha afya cha Nguruka nacho kilipatiwa ambulance. Tunaishukuru sana Wizara kwa msaada huo na tuiombe Wizara pale ambapo ambulance zinapatikana basi nitaomba kukiombea kituo cha afya cha Kalya ambacho kiko kilometa 270 kutoka Makao Makuu ya Halmashauri ya Lugufu. Wakina mama wajawazito wanapata taabu sana tena sana pindi wapatapo shida ya kujifungua kwa kupasuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe pia Wizara itupitishie ombi letu maalum la shilingi bilioni mbili kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya, tayari tumetenga eneo la hekari 30 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Uvinza ina jumla ya zahanati 33, kati ya vijiji 61 tunavyo vituo vya afya vitano katika ya kata 16 hivyo tuna upungufu wa vituo vya afya 11. Kwa sasa tunaendelea na ujenzi wa vituo vya kata za Kazura Mimba, Basanza pamoja na Mwakizega. Hivyo Mheshimiwa Waziri utaona ni jinsi gani hali ya afya bado haijaimarika ndani ya Wilaya ya Uvinza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaendelea na ujenzi wa zahanati zifuatazo; katika kijiji cha Mazugwe ujenzi umekamilika. Kuna jitihada ya uanzishwaji kupitia Mfuko wa Jimbo na Halmashauri na kumalizia; zahanati za Lufubu, Ikubuvu, Kalilani, Msiezi, Kajije, Katenta, Malagarasi, Humule. Zahanati zote hizi tisa zinajengwa kwa nguvu ya Mfuko wa Jimbo na nguvu za wananchi. Tunaiomba Wizara kutuletea pesa kwa wakati ili tuweze kuunga mkono jitihada hizi za mimi Mbunge wao pamoja na nguvu za wananchi. Sambamba na jitihada za ujenzi wa zahanati tuiombe Serikali kutupa upendeleo kituo cha afya cha Nguruka kwani kinahudumia wakazi wapatao 80,000 ndani ya kata nne na kata moja ya jirani, kata ya Usinge Wilaya ya Kaliua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya vifaa tiba si nzuri kabisa. Kuna zahanati hazina vitanda wala magodoro, tunaiomba Wizara itusaidie vitanda, magodoro pamoja na vifaa tiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna upungufu mkubwa sana wa watumishi wa sekta ya afya kwa asilimia 70. Tunaiomba Wizara itakapoanza kuajiri basi Wilaya ya Uvinza iangaliwe kwa jicho la huruma, hali inatisha. Tuna mtumishi wa zahanati ya Mwakizega anaitwa Zainabu Hassan Salim, hivi karibuni nchi nzima ilishuhudia jinsi wananchi walivyoandamana kupinga nurse huyo kuhamishwa. Hebu Wizara iwe na utaratibu wa kutoa motisha kwa watumishi kama huyo; na kwa kuanzia si vibaya wakaanza na nurse Zainabu Hassan Salim wa zahanati ya Mwakizega.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuchangia haya naomba kumpongeza tena Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na Katibu Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri kwa Mheshimiwa Waziri Ummy kwenye maeneo kama ya Jimbo langu, si vibaya kuwa na ambulance za speed boat ili kuokoa vifo vya mama na mtoto kwenye Ukanda wa Ziwa Tanganyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa mara nyingine niunge mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niungane na wachangiaji wenzangu kwa kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, kwa kuchapa kazi ya kusimamia Wizara hii na kupunguza migogoro ya ardhi nchini na migogoro ya wakulima na wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuzungumzia migogoro ya mipaka ya vijiji na hifadhi, natambua Mheshimiwa Waziri ni mzoefu wa kupunguza migogoro ya ardhi na kwa kuwa migogoro ya hifadhi na vijiji vilivyosajiliwa vinamgusa kwenye Wizara yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana tena sana Mheshimiwa Waziri Lukuvi tushirikiane kwa ukamilifu sana na Wizara ya Maliasili na Utalii na TAMISEMI ili basi mgogoro wa hifadhi na Vijiji vya Sibwesa na Kalilani, unaweza kutatuliwa na kwisha ili basi wananchi na hifadhi wenyewe waweze kufanya shughuli za kimaendeleo na kufanya mahusiano ya kijamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa watumishi wa ardhi; niombe kwa Mheshimiwa Waziri akipata watumishi wa ardhi, basi atukumbuke Halmashauri ya Uvinza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nizungumzie suala la NHC, kwanza nimpongeze Mtendaji Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa Tanzania (NHC). Kwa kuchapa kazi na kwa kasi kubwa anayofanya ya kuwajengea Watanzania nyumba za bei ya kati ambayo Watanzania wengine wamemudu kununua. Rai yangu katika hili tuombe NHC nao waweze kutoa fursa kwa Watanzania kulipa asilimia 10 na baadaye walipe kila mwezi hadi hapo mkataba utapokwisha ndio wapewe Hatimiliki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ya kulipa asilimia 10 halafu zilizobaki mtu alipe ndani ya miezi mitatu kwa kweli inatunyima fursa Watanzania wengi kuweza kununua nyumba hizi na wadau ni wengi, mtu anaweza kuwa na nyumba Dar es Salaam akapenda kuwa na nyumba pia Arusha, lakini kwa utaratibu wa kulipa 10% halafu miezi mitatu awe amemaliza kwa kuchukua mkopo Benki, hili ni gumu. Sababu ni kwamba, wapo Watanzania tayari wana mikopo mingine benki ya biashara, sasa akichukua mkopo benki kwa ajili ya kununulia nyumba mikopo inakuwa mingi inamzidia. Hivyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri, aone namna ya kuchukua mfumo wa NSSF mtu analipa downpayment ya miezi mitatu kisha kila mwezi analipa pango hadi amalize.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe pia Mheshimiwa Waziri, NHC waje Uvinza kutujengea nyumba za bei za kati na bei za nafuu katika ukanda wa Ziwa Tanganyika. Ziwa hili lina mandhari nzuri sana na viwanja tunavyo. Sambamba na hili tunaomba pia waje kujenga Uvinza, viwanja vikubwa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba hizi tunavyo na huku kwa vile ni Wilaya mpya watumishi wengi wa Serikali na Taasisi mbalimbali hawana nyumba za kuishi, hivyo tunawakaribisha NHC kuja kujenga nyumba za bei nafuu na kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayoifanya kwenye Wizara. Naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Spika, naomba kuchangia kwa maandishi Wizara hii. Kwanza nianze kwa kutoa pole kwa familia ya watoto na Walimu pamoja na dereva wa basi lililopata ajali Wilayani Karatu, Mkoa wa Arusha. Nitoe pole za dhati ya moyo wangu kwa kweli inasikitisha sana tena sana na kutia uchungu, kikubwa kazi ya Mungu haina makosa. Tuombe roho za marehemu ziwekwe mahala pema peponi amina.

Mheshimiwa Spika, pili nimpe pongezi mzee wangu Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe kwa kuendelea kuaminiwa na Mheshimiwa Rais kupewa Wizara hii ya Michezo, Habari na Utamaduni.

Mheshimiwa Spika, wilaya nyingi nchini hazina viwanja vya michezo ya football, netball, basketball na kadhalika, lakini kuna mikoa hapa nchini ina historia ya kutoa wachezaji bora na wasanii bora kama Mkoa wa Kigoma ninaotokea mimi.

Mheshimiwa Spika, cha kunishangaza ni kuona TFF wanajenga viwanja Mwanza na kuacha kuboresha viwanja vya Lake Tanganyika na Wilaya ya Kigoma ili kuwaenzi wachezaji wa zamani kama kina Sande Manara, Katwila, kina Mambo sasa, Kitwana Manara na wengine na hata kina Mizani Khalfan kina Juma Kaseja na wengine wengi.

Mheshimiwa Spika, pia kuhusu suala la wasanii wa muziki wa kizazi kipya kama kina Diamond, Ali Kiba, Omari Dimpozi, Banana Zoro, Maunda Zoro, Juma Nature na kadhalika wote hawa wanatoka Kigoma.

Mheshimiwa Spika, inaashiria kuwa Mkoa wa Kigoma ni mkoa unaotoa vipaji vya kila aina. Tunachoomba Serikali ni kuona namna ya kuwasaidia wasanii hawa kuwa na hati miliki ili waweze kunufaika na vipaji vyao vya asili kuliko kama ilivyo sasa msanii anatunga yeye, anaimba yeye, anayenufaika ni mwingine.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo nizungumzie suala la utamaduni; tuombe Serikali kupitia Wizara hii kurudisha ngoma za asili mashuleni ili basi tuweze kuenzi ngoma zetu za asili. Kupitia mashuleni sherehe mbalimbali za kitaifa, sherehe za mikoani na wilayani kuwa na utaratibu wa kualika ngoma za asili ili kutunza tamaduni zetu za Tanzania.

Mheshimiwa Spika, nichangie pia kukuza michezo mashuleni kwa kurejesha kwa nguvu kubwa michezo ya UMISETA ili kuanza kuibua michezo mashuleni na hatimaye watoto wakue na vipaji vyao.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie pia suala la TBC; hali ya huko vijijini TBC haisikiki kabisa tuombe Serikali kupitia Wizara hii ione namna gani ya kuboresha vitendea kazi ili waweze kufanya kazi yao ya kutoa huduma kwa watanzania wote hususan kwa wananchi wa vijijini.

Mheshimiwa Spika, niongelee pia suala la mchezo wa kuogelea kuna tatizo la mchezo wa kuogelea pale ambapo tunaacha kwenda kuibua vipaji kwenye wilaya zenye maziwa kama vile Ziwa Tanganyika, Ziwa Nyasa na Ziwa Victoria, hebu tushauri Serikali kuibua vipaji kwenye maeneo hayo kwani watoto wengi hujua kuogelea vizuri. Tukiwapa mafunzo ya kuogelea kwenye swimming pool wanaweza kufanya vizuri na kuiletea ushindi nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, mwisho nizungumzie lugha ya Kiswahili; kuna tatizo kubwa la nchi za nje kama USA, Holland, UK, na kadhalika watu wa DRC na Kenya ndio wanaofundisha Kiswahili kwenye vyuo vikuu vya nchi mbalimbali, kwa nini Serikali isiwaandae Walimu wa Kitanzania wanaochukua somo la Kiswahili na Kiingereza ili wawe na degree ya lugha tu na waweze kuthubutu kwenda nje kufundisha lugha ya Kiswahili.

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi naomba kuchangia hotuba ya bajeti hii ya Elimu, Sayansi na Teknolojia; binafsi nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Joyce Ndalichako, dada yangu kwa kumudu Wizara hii na sote tunaona namna anavyochapa kazi. Namuombea asirudi nyuma, azidi kusonga mbele ili kuhakikisha anatatua changamoto za elimu, ukosefu wa nyumba za walimu, ukosefu wa vyoo, ukosefu wa madarasa, ukosefu wa maabara na vifa vya kufundishia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi nijielekeze kwenye changamoto mbalimbali zinazoikabili Halmashauri yetu ya Uvinza.

Mhesimiwa Mwenyekiti, moja; tunazo shule ambazo zinajengwa na wananchi na kumaliziwa na Halmashauri na pia Mfuko wa Jimbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano shule ya sekondari Mwakizego; shule hii imepokea hadi walimu wa Serikali na ina jumla ya madarasa kumi. Imejengwa ili kupunguza umbali wa watoto wetu kutembea hadi Ilagala sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe dada yetu Mheshimiwa Joyce Ndalichako mambo mawili; kwanza, kuisajili shule hii kabla ya mwaka wa bajeti tarehe 30 Juni, 2018. Pili, nimuombe aje atembelee shule hii ili aone jitihada za wananchi wa Mwakizega.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walimu hawa wapya inakaribia miaka miwili hawalipwi pesa zao za uhamisho hadi leo. Sambamba na hili walimu wengi wana malalamiko ya kutolipwa pesa zao za stahiki zao mbalimbali ikiwemo na kucheleweshewa kupandishwa vyeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu shule mbili za Lugofu Girls High School na Lugofu Boys; shule hizi ziko kwenye majengo yaliyoachwa na UN (Kambi ya Wakimbizi).

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule hizi pia Serikali imezisahau, kwa nini wasipewe pesa kwa ajili ya kujenga mabweni mazuri ya kisasa na vyoo? Kwa nini vyoo wanavyotumia haviko kwenye hali nzuri kabisa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo shule za msingi nyingi ziko kwenye hali mbaya sana, tunayo shule ya msingi Anzerani ina madarasa mawili zaidi ya miaka minane na nyumba ya walimu two in one, imepaliliwa lakini hakuna pesa za kuimalizia.

Tunaomba Wizara itupatie upendeleo wa fedha za ujenzi wa madarasa ili tuweze kujenga madarasa kwenye shule zote zenye uhaba wa madarasa. Kwa mfano shule ya msingi Msimba ina darasa moja kwa zaidi ya miaka 10. Sambamba na haya tunao uhaba mkubwa wa walimu wa shule za msingi, hali ya miundo mbinu ni mbaya, vyoo na nyumba za walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Uvinza hatuna Chuo cha VETA na wanafunzi wanaomaliza shule ya msingi na sekondari wengi hawapati ufaulu wa kuendelea na shule za sekondari na high school; kwa nini Serikali isianzishe Chuo cha VETA Ilagala ili kunusuru vijana hawa?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wote kwa pamoja kwa uchapakazi wake katika kuhakikisha Wizara hii nyeti yenye kuwagusa wananchi kwenye masuala ya kilimo, uvuvi na ushirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuzungumzia suala la tumbaku. Tumbaku ni zao linaloingizia sana kipato Taifa letu, ukizingatia hata wanunuzi hununua na pesa ya kigeni yaani dola, lakini tumekuwa na tatizo kubwa na middleman wanaokaa katikati ya mkulima na mnunuzi, hawa wamekuwa wakisababisha wakulima kupata bei za chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushirika. Tunaomba Wizara iimarishe vyama vya ushirika vya kilimo na mazao. Nashauri pia, sambamba na hili nizungumzie pia mikopo ya pembejeo. Sote tunatambua vyama vya ushirika wa mazao kama vile, mazao ya tumbaku, pamba, korosho, kahawa, michikichi na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua jitihada za Serikali za kuanzisha Benki ya Kilimo. Kwa nini sasa Serikali isione umuhimu wa kuweka matawi kwenye Kanda zote nchini ili basi wakulima wetu huko Majimboni waweze kupata fursa ya kukopa na kuendeleza mashamba yao. Uimarishaji wa mazao baada ya mavuno na kuongeza upatikanaji wa masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie kuhusu uvuvi. Zao la uvuvi ni zao ambalo likifanyiwa kazi na kuwekewa mkakati wa kuwakopesha wavuvi zana za uvuvi kama maboti, mashine, nyavu za kisasa na kadhalika, lingeingizia Taifa letu kipato kikubwa. Mfano, nimeona ukurasa wa 18 Mheshimiwa Waziri kaonesha idadi ya samaki waliopo kwenye Ziwa ya Victoria, tani 2,451,296 Ziwa Tanganyika tani 295,000 na Ziwa Nyasa tani 168,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tuna tani zote hizi tungeweka mikakati ya makusudi ya kuvua samaki hawa na kuuza nje ya nchi tungepata kipato kikubwa cha Taifa, lakini nijuavyo mimi idadi hii ya samaki waliopo Ziwa Tanganyika ya 295,000 siyo ya kweli. Tuombe Serikali ifanye utafiti wa kina wa kujua idadi kamili na siyo kubuni tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko nyuma walikuja watafiti kutoka China na walifanya utafiti na kugundua Ziwa Tanganyika lina samaki wengi na lina aina ya samaki zaidi ya 250. Iweje leo utafiti uoneshe idadi hiyo ya 290,000. Tuombe utafiti ufanyike na kumbukumbu stahiki ziwekwe kwa faida ya nchi na faida ya vizazi vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie zao la uvuvi kwenye tozo. Wavuvi wamekuwa wakitozwa tozo kubwa na nyingi, tuiombe Wizara ione namna ya kutoa maelekezo (Waraka) kwenye Halmashauri zetu ambako Maafisa Uvuvi ndiyo wako huko. Tuombe pia, Wizara iangalie zao la michikichi, zao hili lina faida kubwa na Kigoma ndiyo mkoa unaoongoza kulima zao hili. Zao hili lina faida kubwa, zao hili linatoa mafuta ya mawese (palm oil) na mbegu zake zinatoa mafuta ya Korea na pia linatoa sabuni za miche na sabuni za maji. Naamini utafiti ukifanyika wanaweza kupata faida nyingine nyingi tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Waziri aone namna ya kutoa miche bora ya michikichi ya muda mfupi wa miaka mitatu kwa bei nafuu kwani bei wanayouziwa wakulima, mche mmoja Sh.5,000/=. Eka moja inahitajika miche 50, swali ni wakulima wangapi wana uwezo wa kununua miche hiyo bora? Kuna ulazima wa kupata ruzuku ya miche hii ili wakulima wang’oe miche ya zamani na kupanda miche bora inayokua kwa miaka mitatu kama wenzetu wa zao la korosho wanavyoweza kupanda miche bora ya muda mfupi na leo zao la korosho limeingizia wakulima pato kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie migogoro ya wakulima na wafugaji kwenye Jimbo langu la Kigoma Kusini, Wilaya ya Uvinza. Mheshimiwa Waziri Wilaya ya Uvinza tunavyo vitalu vingi sana kwenye ranchi ya Uvinza. Vitalu hivi vingegawiwa kwa wafugaji wa Uvinza au wenyeji wa Uvinza, lakini cha ajabu vitalu vyote vimegawiwa kwa wageni toka mikoa mingine wakati Mheshimiwa Waziri Mkuu hivi karibuni aliwahi kutoa tamko vitalu vyote kwenye ranchi viangaliwe na vigawiwe kwa wenyeji wa maeneo hayo ili kupunguza migogoro ya wakulima na wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Waziri akija kuhitimisha aniambie waliopewa vitalu kwenye ranchi ya Uvinza na je, kuna vitalu vilivyobaki ili basi mimi kama mwakilishi wa wananchi wa Uvinza nijue na mwisho Waziri atakuwa tayari kunipa majina ya wamiliki waliogawiwa hivyo vitalu na maeneo yaliyobaki ili basi niweze kushauri jinsi ya kuvigawa vilivyobaki ili kupunguza migogoro ukanda wa reli na ukanda wa Ziwa Tanganyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kuipongeza Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa kutimiza azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kuifanya Tanzania yenye viwanda kutimia. Pia kupongeza kauli ya Serikali iliyotolewa jana na Mheshimiwa Waziri Mkuu kuhusu mafuta. Hali iliyopo nje kwa wapiga kura wetu ni mbaya, kwanza mafuta yamepotea, pili mafuta yamepandishwa bei sana. Tuzidi kuiomba Serikali kutatua sintofahamu zilizopo baina ya wafanyabiashara, TRA na Wizara ili mwezi wa mfungo wa Ramadhani mafuta yapatikane na kwa bei ya chini kama ilivyokuwa hapo awali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili nizungumzie pia hali ya upoteaji wa sukari na upandaji bei. Kumekuwa na tabia ya wafanyabiashara kuficha mafuta, sukari na bidhaa nyingine za chakula na ifikapo mwezi Mtukufu wa Ramadhani wanaviachia na kuvipandisha bei na kuwasababishia Waislamu wanaofanya ibada hii muhimu kupata adha kubwa ya kupata mahitaji yao muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la makontena yaliyozuiliwa bandarini kwa kigezo cha kulipia kodi, hii ni hatari sana. Tende hizi zinatumiwa na Waislamu kipindi cha mfungo wa Ramadhani kwa mujibu wa kalenda yetu tunatarajia mfungo kuanza tarehe 17 Mei, 2018 na tende hizi ni kifungua kinywa muhimu sana kwa mwezi huu wa Ramadhani. Tuombe Serikali iliangalie hili suala ili basi TRA waweze kuruhusu makontena hayo na hatimaye Waislamu waanze mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda katika Mkoa wa Kigoma; Mkoa wa Kigoma tunalima zao la michikichi, tuliomba kupitia bajeti iliyopita kwa nini Wizara wasitoe ruzuku kwenye zao la michikichi ili kuwawezesha wakulima wengi ndani ya Mkoa wa Kigoma kulima zao hili kwa wingi tofauti na ilivyo sasa kuna mzungu, raia wa kigeni anavyo vitalu vya michikichi anauza kila mche mmoja shilingi 5,000 na ekari moja inahitajika michikichi 40 hadi 45.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo wakulima wengi wanaendelea kutumia michikichi yao ya asili tangu babu zao. Kwa kufanya hivyo hawapati mafuta ya kutosha, lakini wangepata miche ya ruzuku ya michikichi ya kisasa wangeweza kupata mafuta mengi ya kukidhi mahitaji ya walaji na pia kipato chao kingeongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wawekezaji wengi toka nje ya nchi wako tayari kuingia ubia na Watanzania kwenye viwanda vya kuunganisha pikipiki (bodaboda). Tatizo kubwa linalowakuta Watanzania ni kukosa Government Guarantee, kuwapa assurance wawekezaji kuingia ubia na Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niiombe Serikali kupeleka umeme Wilaya ya Uvinza ili kuwawezesha wananchi kuanzisha viwanda vidogo vidogo vya mafuta ya mawese, mafuta ya mise na utengenezaji wa sabuni sambamba na viwanda vya kuongeza thamani ya mazao ya Ziwa Tanganyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kutoa pongezi za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia kuhusu miradi ya maji mikubwa miwili; mradi wa Rukoma na mradi wa Kandaga. Miradi hii ilianza bajeti ya 2012/2013 hadi bajeti hii ya 2017/2018 haina mwelekeo wowote wa kukamilishwa. Tatizo la miradi hii ni mgawanyo wa Halmashauri ya Wilaya mbili yaani kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma Vijijini na kuzaliwa Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza na miradi hii ikabaki Halmashauri mama ya Wilaya ya Kigoma Vijijini na miradi mingine mikubwa kama Uvinza, Nguruka, Ilagala na Kalya ilihamishiwa Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza na inaendelea vizuri.

Mhshimiwa Naibu Spika, niombe Wizara isiache kutupia macho miradi ya Kandaga na Rukoma ili Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma Vijijini watumalizie na kutukabidhi kwenye Halmashauri ya Uvinza.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi hii minne inayotekelezwa na Halmashauri ya Uvinza kwa maana ya Mradi wa Nguruka, kiasi kilichobaki ni Sh.1,865,024,153; Mradi wa Ilagala kiasi kilichobaki ni Sh.491,628,240; Mradi wa Uvinza thamani ya pesa zilizobaki ili mradi ukamilike ni Sh.1,040,943,442 na Mradi wa Kalya kiasi kilichobaki ni Sh.185,170,935. Jumla tunahitaji Sh.3,582,766,770 ili tukamilishe miradi hii minne.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kitabu cha bajeti cha Mheshimiwa Waziri, bajeti ya miundombinu ya maji kwa mwaka wa fedha 2017/2018 ni Sh.1,723,135,000. Utaona ni kwa namna gani miradi hii iliyoanza tangu bajeti ya 2012/ 2013 haitakamilika na kusababisha wananchi wa maeneo husika kukosa maji safi na salama na ikizingatiwa kati ya vijiji 61 ni vijiji vitano tu ndivyo vinavyopata maji safi na salama tena ya visima vifupi. Tuombe Wizara ione namna ya kutuongezea fedha pale ambapo wakandarasi watakapokuwa wamelipwa hizi 1.7 bilioni na wakawa wameleta certificate zao kwa ajili ya malipo ili basi miradi hii iweze kukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe pia masikitiko yangu kwa Wizara ya Fedha na Mipango kupunguza bajeti ya maendeleo ya miradi ya maji kutoka shilingi bilioni 900 kwenye bajeti ya 2016/2017 hadi shilingi bilioni 600 kwa bajeti ya mwaka huu wa bajeti 2017/2018 unaoanza tarehe 1/07/ 2017. Inasikitisha sana tena sana na kwa mpango huu wa upunguzaji wa bajeti ya maendeleo ya miradi ya maji inaonesha jinsi gani Serikali haina dhamira ya dhati ya kumaliza miradi ya maji inayoendelea kwenye majimbo yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza tunavyo visima virefu na vifupi kama cha Mganza, kisima cha Shule ya Msingi Mliyabibi, kisima cha Sanuka na maeneo mengine havijafanyiwa marekebisho kwa miaka mingi sana na kusababisha visima hivi kutotoa maji na badala yake wananchi wa maeneo haya wanabaki kuona visima ambavyo hawana faida navyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua bajeti ya mwaka 2017/2018 ni finyu ila tuombe Wizara iliangalie Jimbo la Kigoma Kusini kwa jicho la huruma kwani hali ya upatikanaji wa maji safi na salama ni mbaya sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe kuzungumzia suala la umwagiliaji. Mheshimiwa Waziri anatambua fika Jimbo langu ndiko Mto Malagarasi ulipo na mto huu unapita takribani vijiji 22 na mradi wa maji safi na salama wa Mto Malagarasi unahusisha Miji ya Urambo, Kaliua na Nguruka.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na uchambuzi yakinifu unaoendelea kwenye mradi huu mkubwa lakini pia tunalo Bonde la Mto Malagarasi kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji hasa kilimo cha mpunga. Tumwombe Mheshimiwa Waziri pale panapokuwa na fursa ya kusaidia wakazi wa Tarafa hii ya Nguruka ili waweze kuendeleza kilimo cha umwagiliaji na ukizingatia Tarafa hii inalima sana mpunga.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nami nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Katibu Mkuu, Mkuu wa Majeshi na timu yote chini ya Wizara hii kwa utendaji wao mahiri na makini ndani ya Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua umuhimu wa Wizara hii, tatizo ninaloliona ni kuwa tunapitisha bajeti lakini mwisho wa mwaka hawapelekewi fedha zote. Wizara hii ina mambo mengi muhimu sana kwa mustakabali wa nchi yetu. Hivyo lazima Hazina waone umuhimu wa kuwapelekea fedha zote za bajeti tunazopitisha. Nasema hivi kwani binafsi nilikuwa kwenye Kamati hii ya Ulinzi na Usalama (KUU).

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitembelea eneo la karakana ya JWTZ iliyoko Kibaha, tatizo kubwa ni uchakavu wa mitambo ya kijeshi ndani ya nchi yetu. Tunatambua kwa kuboresha karakana hizi, ikizingatiwa kazi kubwa ya jeshi letu ni kulinda mipaka ya nchi zetu, amani tuliyonayo italindwa kwa asilimia kubwa na Jeshi letu au majeshi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba mafunzo ya JKT kwa vijana wetu yaongezwe hususani kwa wale waliomaliza Kidato cha Sita, ambao hawakupata nafasi ya kujiunga na hivyo kumaliza Chuo Kikuu bila kupata mafunzo haya ya JKT.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, nashauri Bajeti ya JKT iheshimiwe na kupelekwa yote na ikiwezekana kila mwaka bajeti iongezwe ili kutoa fursa kwa vijana wengi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. HASNA S. MWILIMA: Mheshimiwa Spika, nami naomba niungane na wenzangu kuchangia mapendekezo ya bajeti ya 2017/2018 yaliyowasilishwa na Mheshimiwa Waziri kaka yangu Mpango. Kwanza kabisa nimpongeze sana kaka kwa umahiri mkubwa na utulivu aliotumia siku ya kuwasilisha taarifa hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama alivyotangulia kusema Mbunge mwenzangu Mheshimiwa Shabiby kwamba wengi walikuwa wanasema hasikii, hachukui mapendekezo, amechukua mapendekezo na ametuleta taarifa ya mapendekezo ya bajeti yenye tija, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, pia nimpongeze Mheshimiwa Rais, nami niseme jamani, niliwahi kusema siku za nyuma, suala la madini linatuhusu watu wote lakini siku Wizara ya Madini inawasilisha hapa chini ya Waziri wa Viwanda na Biashara, aliyesoma taarifa ya Kambi ya Upinzani mdogo wangu Mnyika, alionesha kabisa kwamba Rais ameanza kutatua tatizo dogo badala ya kutatua tatizo kubwa la mikataba.

Mheshimiwa Spika, nami nikasema, anawezaje kuanza na hilo bila kuchunguza na kuona hivi kweli nikivamia mikataba hawa watu ni kweli wanaiba madini? Akaunda Tume ya kwanza, ikatupa taarifa. Tume ya pili, imetupa taarifa na wote tumesikia tangu 1998 mpaka 2017 tumepoteza shilingi trilioni 108. Ukienda kwenye bajeti yetu ya mwaka huu tunayotarajia ianze tarehe Mosi Julai, ni mara tatu ya bajeti tunayokwenda kuipitisha ya trilioni 31.7. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashangaa, ninachokiona mimi kisiasa kwa sababu wenzetu walikuwa hawaoneshi kuunga mkono kazi anayofanya Rais ya kupambana na wizi wa rasilimali kwenye madini yanayotoroshwa, sasa wanatafuta kick kwa wananchi. Mimi niseme, wananchi ni waelewa, jana kwenye vyombo vya habari nilivyokuwa nasikia wapo wanachama wengi tu wa Vyama vya Upinzani wameamua kuachiaachia nyadhifa mbalimbali ili waweze sasa kumuunga mkono Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka niseme hivi ndugu zagu, haya mambo mazuri ambayo Mheshimiwa Rais anayafanya, hata kama msipotaka kuyaunga mkono, hata kama mtayapekuapekua mnavyotaka kupekua ninyi ili wananchi waone kwamba ninyi ndiyo bora na Rais wa Chama cha Mapinduzi siyo bora, nasema hamuwezi kupata tija katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nizungumzie dhamira njema ya bajeti hii kwenye suala la viwanda. Tunafahamu kabisa kwamba Kigoma tuna kiwanda kimoja tu cha Uvinza Salt Mine. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, kuna tatizo la wafanyakazi ambao walikuwa wanafanya kazi siku za nyuma, tangu 1994 wakaachishwa bila kulipwa mafao yao.

Mheshimiwa Spika, tatizo hili ni la muda mrefu lakini lilifanyiwa kazi na Serikali na ikataka kujiridhisha ni kweli wafanyakazi wale wana haki za kulipwa? Suala hili likapelekwa mpaka kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye naye akalifanyia kazi, akalipekua kisheria akaona kwamba wafanyakazi hawa wana haki kabisa za kisheria kulipwa mafao yao.

Mheshimiwa Spika, suala hili lipo mezani Ofisi ya Wizara ya Fedha na Mipango, lina muda mrefu, lipo kwenye meza ya Katibu Mkuu. Nimwombe Mheshimiwa Waziri kaka yangu Mpango, alifanyie kazi ili wafanyakazi hawa walipwe. Wapo ambao wameshatangulia mbele ya haki, familia zao zipo, wajane na watoto wapo, watapokea ile haki ambayo wazazi wao walikuwa wapokee.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hilo hilo la viwanda niseme pia tunapotaka tuwe na Serikali ya Viwanda na Nchi ya Viwanda, tusiangalie tu baadhi ya Ukanda ndiyo uwe na viwanda na Ukanda mwingine tusiwe na viwanda. Kwa hiyo, ninachoomba, tunatambua kabisa Kibondo pale tuna miwa mingi sana, tunaweza tukaanzisha Kiwanda cha Sukari. Uvinza tunaweza tukaanzisha Kiwanda cha kutengeneza Mafuta ya Mawese na mafuta ya mawese yanalika sana ulimwenguni.

Mheshimiwa Spika, ukienda Marekani kwenye super market zile unakuta palm oil ziko pale na ni very expensive, lakini sasa Serikali kama Serikali bado haijaweka jitihada za makusudi kuongeza tija kuanzisha viwanda katika Mkoa wetu wa Kigoma.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la ujenzi wa reli ya kati na ujenzi wa reli kwa kiwango cha standard gauge. Kwanza niipongeze sana Serikali kwa hatua hii ya ujenzi huu lakini niombe, naona kila mkizungumza ujenzi wa reli mnazungumzia itatoka Tabora itaenda Mwanza. Sasa sisi Kigoma kama alivyosema Kaka yangu Mheshimiwa Nsanzugwako tunapakana na Zambia, DRC – Kongo na Burundi na mizigo mingi sana inatoka huko. Ukienda railway kwenye department ya transportation ukiwauliza watakwambia mabehewa mengi yanayokodishwa yanapeleka mizigo Kongo na Burundi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tuombe, katika ujenzi wa reli ya kati, mtakapokuwa mmepata mkandarasi wa kuanzia Tabora kwenda Mwanza basi tupate mkandarasi mwingine wa kuanzia Tabora kwenda Kigoma. Tunafahamu kwamba sisi wananchi wa Kigoma huu ndiyo usafiri ambao tunauamini zaidi kuliko usafiri mwingine. Kwa hiyo, tunaomba mtufikirie katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hili, reli inayojengwa kwa kiwango cha standard gauge inapita kwenye Jimbo langu la Uvinza. Niombe, tusiwe na mambo ya kushtukizana, pale ambapo mmeshapanga kabisa ifanyike feasibility study ya kujua reli hiyo itapita kwenye maeneo gani basi mtuambie mapema ili wananchi nao wawe na utayari wa kuipokea hii reli inayojengwa kwa kiwango cha standard gauge.

Mheshimiwa Spika, naomba niunge mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2017/2018
MHE. HASNA S. MWILIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi kwa niaba ya wananchi wangu wa Jimbo la Kigoma Kusini nishukuru kwa kunapata nafasi ya kuchangia Wizara hii nyeti, Wizara ya Nishati na Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze sana kwanza kwa kumpongeza Waziri aliyewasilisha makadario ya bajeti ya Wizara hii kwa kushirikiana na Mheshimiwa Naibu Waziri. Natambua kwamba uwezo wanao na wanaweza kufanya kazi vizuri katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaanza kuzungumzia suala la Jimboni kwangu, naomba nimpongeze sana Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli, kwa hatua nzuri aliyochukua ya kuunda Tume. Leo tumesikia hapa taarifa ya upande wa pili unaonesha masikitiko kwamba Rais ameanza kwa kazi ndogo walitaka aanze na mikataba lakini tarehe 29/03/2017 sote tunatambua kwamba Mheshimiwa Rais aliunda Tume na ikafanya kazi yake chini ya Profesa Mruma.

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania wote ni mashahidi, Mheshimiwa Rais alitumia uwazi, akaitoa ile taarifa kwa uwazi kwenye vyombo vya habari, wananchi walioko vijijini, wanaotumia redio walisikia, wenye kuona luninga waliona na akasoma taarifa. Kwa mfano kwenye yale makontena 277 kwa taarifa aliyoitoa Mheshimiwa Rais wetu ilionyesha kwamba Watanzania kupitia hayo makontena 277 tunapoteza takribani bilioni 676. Halafu leo tunasema hii ni kitu kidogo wakati pesa hizi zinazopotea tungezipeleka kwenye majimbo yetu, Serikali ingeelekeza kwenye kujenga hospitali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo kwenye makontena hayo wakati Mheshimiwa Rais anatoa taarifa imeonekana pia tuna upotevu wa copper na sulphur. Kwa mfano, nilikuwa naangalia kwenye taarifa ya copper inaonesha kwamba kwenye kila kontena tuna tani 20 za copper zinazopotea. Ukijumlisha yale makontena yote 277 unapata tani 1440.4 zenye thamani ya jumla ya shilingi bilioni
17.9. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachonishangaza sisi wote tunafahamu wakati sisi wageni hatujaingia Bungeni siku za nyuma tulikuwa tukiangalia Bunge tunawasikia wapinzani wanaisema Serikali ya Chama cha Mapinduzi inakumbatia mafisadi na wanasema Serikali ya Chama cha Mapinduzi inaachia rasilimali za nchi zinaibiwa. Leo Mheshimiwa Rais amewasikia kwamba wapinzani walikuwa na vidonda sasa anajaribu kuona ni jinsi gani anaponyesha vile vidonda walivyokuwa navyo siku za nyuma. Raha ya donda, ukiwa na kidonda chochote lazima kipate dawa, iwe ni dawa ya kizungu, iwe ni dawa ya kienyeji lakini lazima kipate dawa. Mheshimiwa Rais analeta dawa kwa kuanza na haya makontena 277 lakini tunasema kwamba angeanza na mikataba, angeanza na mikataba wapinzani hao hao wangesema Rais kakurupuka, anaanzaje na mikataba kabla ya kufanya uchunguzi. Sasa ameanzia makontena ndugu zangu ili kubaini hivi kweli huu mchanga unapopelekwa nje tunaibiwa au hatuibiwi? Kamati imetueleza kuwa tunaibiwa na Mheshimiwa Rais ametuambia anajiandaa kutoa taarifa ya pili kwa nini jamani tusimpe muda tukaisikiliza na ile taarifa ya pili ili tuweze kuona inatuletea nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka siku za nyuma wakati wa makelele ya ufisadi, tunaibiwa rasilimali zetu, Baba Askofu, Mwadhama Kadinali Pengo wa Jimbo la Dar es Salaam Katoliki aliwahi kuhoji, hivi hawa wanaopiga kelele kwamba Watanzania wanaibiwa rasilimali zao zinatoroshwa, wanaongea kwa uchungu wa dhati au wanaongea kwa sababu wamekosa fursa na wao ya kuiba? Mimi nilifikiri kwenye suala hili tusimame kama Watanzania, tusimame kama nchi, tuache itikadi zetu, tumpe moyo Rais. Kama hatumpi moyo atafikia wapi kuwaza kuichambua na mikataba, kutoa fursa ili Bunge nalo tuletewe hiyo mikataba tuipitie na tumsaidie Rais kubadilisha yale ambayo tunaona ni upungufu?

Kwa hiyo, naomba sana tuwe na subira ndugu zangu, mambo mazuri hayahitaji haraka. Tume imetoa taarifa ya kwanza tusubiri taarifa ya pili na nina imani Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ni mtu makini na atatupa taarifa ya pili na kwa taarifa zilizoko huko nje ni kwamba Watanzania wamefurahi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siku ile Rais anatoa taarifa kaka yangu Mheshimiwa Tundu Lissu hapa alihojiwa na waandishi wa habari akasema wao kama Upinzani wamekuwa wanapiga kelele siku nyingi sana lakini Serikali haichukui hatua, leo Serikali inachukua hatua tunasema nini sasa, si tuipongeze? Halafu jamani ndugu zangu tujenge utamaduni wa kupongeza au kukosoa Serikali pale ambapo inapostahili, sio kila kitu tupinge. Hata nyumbani kwako inawezekana kabisa ukirudi mke unamnunia lakini siku akikupikia chakula kizuri si ni lazima umsifie, umwambie kwamba leo mke wangu umenipikia chakula kizuri ili kesho apate nafasi ya kwenda kununua zaidi na aweze kukupikia zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kumpongeza Rais na hiyo jitihada aliyofanya, naomba sasa niende kwenye Jimbo langu. Jimbo langu lina vijiji 61 tuna umeme kwenye vijiji kumi tu.

Kwenye REA Awamu ya Pili tulipata vijiji kumi vya Kandaga, Mlela, Kazuramimba, Kalenge, Uvinza na Mwamila lakini kwenye Awamu hii ya Tatu ya REA pia tumepangiwa vijiji kama 11. Rai yangu, naomba Waziri ambaye amewasilisha hapa waweze kushirikiana na Naibu Waziri na Mkurugenzi wa REA Tanzania Ndugu Msofe waone ni jinsi gani wanatusaidia wananchi wa Uvinza ili basi tuweze kuongezewa vijiji. Ni jambo la aibu kuona tangu uhuru vijiji 61 tuna umeme kwenye vijiji kumi tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nawapongeza kwanza wametufikiria kwa mara ya kwanza tunapata umeme mpaka Kijiji cha Malagarasi kwenye Kata ya Mganza. Najua huu ni mwanzo mwema ndiyo hatua sasa ya kupeleka umeme kwenye Tarafa yangu ya Nguruka. Kwa maana utoke pale Malagarasi uende Mlyabibi, Bweru mpaka Nguruka. Nina imani kwa sababu Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi ni sikivu itayapokea haya na kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HASNA S.K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya. Binafsi sina shaka kabisa kwamba 2020 Serikali ya Chama cha Mapinduzi itaendelea kuongoza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kama Kiongozi Mkuu wa shughuli zote za Serikali. Nianze sasa kuzungumzia changamoto mbalimbali zinazoikabili Halmashauri yangu ya Uvinza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la umeme, ukurasa wa 21 tunao mradi wa REA awamu ya pili kwenye Vijiji vya Kabeba, Mwakizega, Ilagala, Mkandarasi aliyekuwa akitekeleza mradi huu kasimamishwa kuendeleza mradi, wakati mradi huu ulitakiwa uwe umezinduliwa tangu Machi, 2017. Leo hii wananchi wamebaki kuziangalia nguzo na transfoma badala ya kuwasha umeme kwenye nyumba zao. Niombe Serikali ituletee Mkandarasi mwingine atakayemalizia mradi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili, hadi tarehe ya leo hatma ya mradi wa REA awamu ya tatu wananchi wa Jimbo la Kigoma Kusini hawajui lini mradi huu utaanza rasmi, niombe Serikali kutangaza tender mara moja ili na mradi huu wa REA awamu ya tatu uanze mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Uvinza inayo miradi sita (6) mikubwa ya maji. Mradi wa maji wa Nguruka, mradi wa maji wa Uvinza, mradi wa maji wa Kandaga, mradi huu wa Kandaga hadi leo Halmashauri ya Uvinza hawajui utekelezaji, kwa kuwa mradi huu unatekelezwa na Halmashauri ya Kigoma Vijijini pamoja na mradi wa maji wa Rukoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na tabia ya kupeleka Viongozi wa Kitaifa upande mmoja wa Wilaya au upande mmoja wa Jimbo la Kigoma Kusini, mfano. Jimbo hili la Kigoma Kusini lina Kata 16 na Vijiji 61 ndani ya square meter za mraba 10,178 na Kanda mbili (2). Ukanda wa Reli una kata nane, Kata ya Kandaga inayopakana na Kidahwe Mbili, Kata ya Kazuramimba, Kata ya Basanza inapakana na Kasulu, Kata ya Uvinza, Kata ya Mganza, Kata ya Itabula inapakana na Urambo, Kata ya Nguruka, Kata ya Mtego wa Noti inapakana na Kibondo na Upande wa Kaliua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukanda wa Ziwa Tanganyika, Kata ya Mwakizega inapakana na Simbo. Kata ya Ilagala kwenye Gereza la Ilagala, Kata ya Sunuka, Kata ya Sigunga, Kata ya Herembe, Kata ya Igalula inayopakana na Mwesa Mkoa wa Katavi, Kata ya Bohingu kwenye Hifadhi ya Mahale, Kata ya Kalya inapakana na Mpanda. Naelezea haya yote ili Mheshimiwa Waziri Mkuu aone umuhimu wa Viongozi wa Kitaifa wanapokuja kufanya ziara wajue kuwa ukanda huu pia una kata nane (8) na vijiji 34 na una miradi mikubwa ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi wa maji mkubwa wa Kalya na wananchi wameishaanza kunywa maji na Mkandarasi anajipanga kuukabidhi mradi huu Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza. Tunao mradi wa maji Ilagala tayari maji yanatoka, tunaomba mradi wa Mwalo wa Samaki na Dagaa Muyobaozi, Kata ya Mwakizega, lakini cha kusikitisha kila kiongozi anayekuja wanaishia kumpeleka ukanda huu wa Lake Tanganyika na badala yake wote wanaishia kuwapeleka ukanda wa Reli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri Mkuu atakapokuja kufanya ziara ya Wilaya ya Uvinza aje kuzindua kati ya miradi ifuatayo: Mradi wa maji Kalya, mradi wa maji Ilagala au mradi wa Mwalo wa samaki Mwakizega sambamba na mradi wa shule ya sekondari ya Mwakizega.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho Mheshimiwa Waziri Mkuu atakapofanya ziara ukanda huu wa maji ndiyo ataona umuhimu wa kuligawa Jimbo, tayari utaratibu wote ulishafanyika kugawa Majimbo mawili (2) Jimbo la Uvinza na Jimbo la Kigoma Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa na nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Spika, na mimi nianze kuchangia Wizara hii muhimu sana tena sana kwa mustakabali wa nchi yetu na wananchi wetu kwa jumla. Jimbo la Kigoma Kusini lina vijiji 61, kati ya hivyo vijiji 34 viko kwenye Ziwa Tanganyika, wavuvi wanategemea uvuvi ndio wamudu maisha yao. Lakini tuna tatizo kubwa sana tena sana, Idara ya Uvuvi Mkoa wa Kigoma tuna mwanamama pale ambaye ni Afisa Uvuvi Mkoa amekuwa kikwazo kikubwa sana kwa wavuvi. Kwanza hatoi ushirikiano wowote kwa wavuvi, pili amekuwa ni mtu wa kuwakwamisha wavuvi kwa kuwatoza pesa ili wamtetemekee, wanaokataa wanachukuliwa hatua kwa visingizio vya kukosea sheria za uvuvi.

Mheshimiwa Spika, ninao mfano wa Taasisi ya Tuungane iliyopo Kata ya Buhingu, Kijiji cha Mgambo. Taasisi hii haijulikani ina vibali gani kwa kusimamia masuala ya uvuvi ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza wamekuwa ni kero kubwa kwa wananchi maeneo yote yenye dagaa na samaki wa kutosha, wao ndio wanayachukua na kuvua, lakini ukiwauliza wanadai wanalinda samaki wadogo ili wasivuliwe mapema.

Mheshimiwa Spika, tunae mdau namba moja anaitwa Amadi Saidi, ni Mtanzania wa kuzaliwa. Yeye na wazazi wake pale Buhingu na mimi pia nina undugu naye, lakini alichukua uraia wa Abu Dhabi, lakini ni mvuvi mkubwa. Tuombe Wizara imsaidie kumpatia vibali vya uvuvi vyote kwani kufanya kwake kazi ya uvuvi katika Kata ya Buhingu kuna manufaa makubwa sana, amejenga Kituo cha Polisi, amejenga madarasa, amenunua madawati ya shule za Kata ya Buhingu.

Mheshimiwa Spika, nimuombe Mheshimiwa Waziri aliangalie hili. Mheshimiwa Naibu Waziri alikuja/alitembelea na kuona kazi kubwa anayofanya Ndugu Amadi Said. Naomba pia Wizara itupatie nyavu za ruzuku, mashine za maboti za ruzuku na ikiwezekana tupatiwe na maboti ya kuvulia samaki au kama Wizara inatoa mikopo ya wavuvi basi, sisi tupatiwe.

Mheshimiwa Spika, mwisho, tunao mwalo umejengwa Kata ya Mwakizega, Kitongoji cha Muyobozi ili wavuvi waongeze thamani ya mazao yao ya uvuvi, nimuombe Mheshimiwa Waziri amshawishi Mheshimiwa Waziri Mkuu ili atakapokuja kufanya ziara Mkoa wa Kigoma mwezi wa Julai, 2018 basi huu mradi wa mwalo ufunguliwe rasmi kwani mwaka umekamilika.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema, maana ninyi wote ni mashahidi, nimetembelea magongo hapa karibu miezi sita; lakini kwa vile Mheshimiwa Rais aliona kwamba afya yangu inatakiwa iimarike ili niweze kuwatumikia vyema wananchi wa Jimbo langu la Kigoma Kusini, akanipa kibali cha kwenda tena kupata matibabu nje ya nchi na hatimaye leo namshukuru Mwenyezi Mungu naweza kutembea bila kutumia magongo yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona nishukuru hivi kwa sababu mambo yalikuwa mengi, wako waliofikiri sasa nitakufa na Jimbo litabaki wazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, anayepanga maradhi ni Mwenyezi Mungu. Unaweza ukamwona leo huyu ni wa kufa kesho na asife na wewe ambaye ni mzima ukafa ukamwacha yule mgonjwa anaendelea kuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naomba pia nimshukuru Mheshimiwa Rais, juzi wote tumeona kupitia Mfuko wa Falme za Kiarabu Mfuko wa Abu Dhabi tumepata karibu shilingi bilioni 33 kwa ajili ya ujenzi wa kilometa 51.1 kutoka Uvinza mpaka Malagarasi. Barabara hii siyo tu itakuwa ni faida kwa wananchi wa Jimbo la Kigoma Kusini bali pia itakuwa faida kwa Tanzania nzima kwa sababu malori yanayosafiri kuleta bidhaa kwenda Kongo na Burundi yanatumia barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa haraka haraka pia nichangie kuhusu elimu ya msingi na sekondari. Tumepokea shilingi milioni 144 nashukuru sana Wizara ya TAMISEMI kwa kutupatia pesa hizo ambazo zitatusaidia kumalizia majengo yanayojengwa na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna upungufu mkubwa sana wa Walimu. Sisi kwenye mgao tumepokea Walimu 32. Walimu 20 wanaume na Walimu 12 wa kike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo lile ni kubwa, Halmashauri ile ni kubwa sana, ina mita za mraba 10,178 zaidi ya Mkoa wa Kilimanjaro. Mnapofanya mgao kwa Walimu, naiomba Serikali iangalie Halmashauri ya Uvinza tofauti na Halmashauri nyingine, kwa sababu jiografia ni mbaya, kuna barabara ambazo hazipitiki. Kwa mfano, sasa hivi tuna mvua nyingi, Walimu hata wanapokuwa na mahitaji muhimu hawawezi kusafiri mpaka msimu huu wa mvua uishe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunayo majengo ya maabara kwa muda mrefu yamesimama kwa ukosefu wa pesa. Kwa hiyo, naomba Wizara husika ituangalie kwa jicho la huruma ili tusirudishe nyuma jitihada za wananchi wetu wa Jimbo la Kigoma Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Idara ya afya. Naishukuru sana Serikali kwa bajeti hii, tumetengewa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya uanzishwaji wa ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Kwa niaba ya wananchi wangu, natoa shukrani za dhati, lakini tunatambua hivi karibuni Serikali mmetuambia mtatuletea ramani ya ujenzi wa hospitali. Tunaomba mharakishe ili basi ujenzi huo tuweze kuuanza mara moja baada ya kupitisha bajeti hapa Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina vituo viwili vya afya; Kituo cha Kalya na Buhingu. Leo kumeulizwa swali hapa, Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI akajibu kwamba tulete barua ili waweze kutupatia Madaktari. Sisi tumepeleka barua tangu bajeti ya mwaka 2017/2018 kwamba tuna upungufu mkubwa wa Watumishi Idara ya Afya na Idara ya Elimu Msingi na Sekondari. Cha kusikitisha, mpaka leo hatuna Daktari kwenye Kituo cha Afya cha Buhingu, hatuna Daktari kwenye cha Kalya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI leo hii naomba, naona anatembelea halmashauri mbalimbali, namkaribisha Halmashauri ya Uvinza. Aje atufungulie rasmi Kituo chetu cha Afya cha Kalya ili yeye mwenyewe ajionee kilometa 250 wananchi wanatembea kutoka Kalya mpaka Kigoma Mjini. Hali ni mbaya kwa kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tumeona juzi, kwanza tumshukuru Mheshimiwa Waziri wa Utumishi kwa kutupa ufafanuzi kwa wale Watendaji wa Vijiji na Watumishi ambao wamewekwa pembeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vibali hivi mnavyovitoa, mnatupa vibali kuajiri Watendaji wa Vijiji watano au sita au kumi, wakati tuna upungufu karibu wa Watendaji wa Vijiji 30. Tunaomba Wizara ya Utumishi iliangalie hilo tupate vibali ili tuweze kuajiri Watendaji wa Vijiji, Watendaji wa Kata na watumishi wa kada nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado naishauri Serikali. Watendaji wa Vijiji wapo waliofanya kazi zaidi ya miaka 20 mpaka 30, leo wamewasimamisha kazi. Kule vijijini wanaojua mazingira ya vijiji ni wale wananchi husika wa maeneo husika. Tunapotangaza ajira, wanakuja watu wa kutoka Kagera, Mwanza na kadhalika. Mazingira ya kule ni mabovu, badala yake wanaingia kwenye masuala ya rushwa na hawafanyi kazi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wawaangalie sana wale Watendaji ambao wamefanya kazi zaidi ya miaka 20 ili wamalizie kazi na hatimaye waweze kustaafu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie mfuko wa
TARURA. Ni jambo jema…

TAARIFA . . .

MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nalipokea lakini nilikuwa naliangalia kwa mapana zaidi na nilishashukuru kwenye hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusiana na barabara. Jimbo langu hali ya barabara ni mbaya sana. Kwenye bajeti ya mwaka huu tumetengewa shilingi milioni
400. Hivi shilingi milioni 400 tunafanya kazi gani katika mtandao wa barabara wa Halmashauri ya Uvinza? Naomba TARURA waongezewe pesa ili tuweze kujenga barabara zetu za Jimbo la Kigoma Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona vile vile kwenye taarifa ya Mheshimiwa Waziri amezungumizia namna ambavyo tunaendeleza miji kwa maana ya miji 161 iko kwenye hatua mbalimbali ya kufanywa iwe miji midogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Nguruka kuwa Mamlaka ya Mji Mdogo, takribani sasa miaka 10 tumeomba mamlaka ya Nguruka iwe Mamlaka ya Mji Mdogo lakini hadi leo utekelezaji unakuwa mgumu kwa sababu Kata ya Nguruka ina vijiji viwili, Kata ya Itebula ina vijiji viwili,
tunawezaje kuunda Mamlaka ya Mji Mdogo wakati kuna wakazi zaidi ya 50,000 kwenye eneo moja? Naiomba sana TAMISEMI iliangalie hili jambo ili ituruhusu tuweze kuongeza kata na vijiji ili Mamlaka ya Mji Mdogo wa Nguruka uweze kuundwa na hatimaye shughuli za wananchi ziweze kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda, nimalizie tu kwa kusema, naishukuru sana Serikali kwa mambo mbalimbali hususan miradi ya maji. Miradi ya maji ya Nguruka, Uvinza, Ilaghala, Kalya na Kandaga inaenda vizuri, watu wanakunywa maji. Mradi wa maji wa Rukoma ndiyo utekelezaji haujulikani, sasa ni zaidi ya miaka mitatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia Wizara hii muhimu sana. Kabla sijaanza kuchangia nitoe tu ushauri wa jumla, tunapozungumza hapa kwa hisia kali kumkosoa Rais, tunashauriwa sisi Wabunge wa CCM mwambieni Rais awe anakosolewa. Ndugu zangu, hata kwenye familia zetu kuna wakuu wa familia, hivi huwa tunawatukana wale wakuu wa koo zetu? Tukitaka kuzungumza na wale wakuu wa koo zetu au wakuu wa familia zetu, huwa tunawajibu tunawatukana? Tunaongea nao taratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ndugu zangu, naomba nishauri kwa nia njema kabisa; Rais ni Rais tu, ni mamlaka ambayo amepewa kwa mujibu wa Katiba, kwa hiyo lazima tumheshimu, lazima tufahamu kwamba waligombea wengi lakini Mungu alimpanga yeye awe Rais wa Tanzania. Kwa hiyo, tunapokuwa tunasimama jazba zetu kidogo tuwe tunazishusha chini halafu tunajua huyu ndiye Rais wetu, tupende tusipende tayari Mungu ameshamtukuza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba sasa nianze kuchangia. Kwanza nimpongeze sana ndugu yangu Mheshimiwa Mwigulu kwa kazi kubwa na nzuri anayofanya katika Wizara hii, lakini pia nimpongeze ndugu yangu IGP kwa kazi nzuri anazofanya, kwenye mazuri hapakosi kasoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nizizungumze kasoro, hususani katika Jimbo langu la Kigoma Kusini, Idara ya Polisi, Vote 28, nilikuwa naangalia kwenye Vote hii 28 naona mikoa mingine imetengewa pesa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za maaskari wa ofisi za ma-OCD, lakini nimwombe sana Mheshimiwa Waziri; amekuja Kigoma ameona hali halisi ya maaskari, niombe sana kwa nini hawatoi upendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Uvinza ni wilaya mpya, ina miaka sita sasa lakini OCD hana nyumba, OCD hana ofisi, hana gari, katika mazingira kama yale anafanyaje kazi? Naomba sana, nimeona wametenga magari lakini hakuna gari hata moja kwenye wilaya, gari ambalo tumepewa Halmashauri ya Uvinza ni gari lililokuwa linatumika kwenye Ofisi ya RPC. Hata hivyo, tunavyoongea leo hii hata pakitokea matukio ya ujambazi OCD lazima aombe gari mkoani ndiyo afanye kazi katika eneo lake la kazi. Niombe sana hebu wajaribu kumwangalia OCD.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba za maaskari; maaskari wetu wanaishi uraiani, tunawatuma waende wakakamate wahalifu; wanakamata vipi wahalifu wakati wanaishi nao uraiani? Kwa hiyo, kwenye bajeti ijayo wajaribu kuangalia watenge pesa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za maaskari jamani, wana maisha magumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, naomba nichangie kuhusu Magereza, tunalo Gereza la Ilagala, gereza hili limechukua maeneo makubwa ya wananchi wa eneo la Ilagala. Mheshimiwa Waziri alikuja tukafanya kikao akatoa maelekezo tuhakiki mipaka ya wananchi na mipaka ya gereza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhakiki ule umeonesha ni dhahiri kabisa kwamba gereza wamehodhi maeneo ya wananchi. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, hebu tufikie mwisho. Wamechukua eneo kubwa karibu ekari 5,000, kwa nini wasitoe hata ekari 2,500 zirudi kwa wananchi na zile 2,500 tuwaachie wao waendeleze na masuala mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakwenda kwa harakaharaka kwa sababu nataka nisimame sana kwenye Uhamiaji. Katika uhamiaji tuna kero kubwa sana na uhamiaji ndani ya Mkoa wa Kigoma. Katika Tanzania hii sio Kigoma peke yake ambayo inapakana na nchi za jirani, hata Arusha wanapakana na Kenya, ukienda Mtwara wanapakana na Msumbiji, lakini ukienda Kagera wanapakana na Rwanda. Leo wananchi wa Kigoma hatuishi na amani, kutwa kucha tunaitwa Banyamurenge, tunaitwa Wakongo, tunaitwa Warundi, roho zinatuuma sana sisi watu wa Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, roho zinatuuma kwa sababu unaposikia wananchi wanavamiwa saa nane za usiku, hivi tujiulize, saa nane za usiku operesheni za kwenda kuvunja milango kwenda kukamata raia. Nane usiku wote tunafahamu sisi wanawake humu ndani, mwanamke saa nane usiku ndio anatafuta namna ya kujaza nyumba. Leo saa nane usiku watu wanabomolewa milango, inauma, naongea kama mwanamke, inaniuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapigiwa simu Mheshimiwa Mbunge tunavamiwa saa tisa, sasa hawa watu wakiwavamiavamia mwisho jamani wanaume wetu wale watashindwa kusimamisha mambo vizuri. Hii haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naongea kwa uchungu. Operesheni zinazofanywa ndani ya Mkoa wa Kigoma sio sahihi, ile Kigoma ni Tanzania, wananchi waliopo ndani ya Wilaya za Kigoma ni Watanzania, leo tukisimama hapa tumechaguliwa kwa sababu ni Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuombe, najua kwamba Mkurugenzi wa Uhamiaji ni mwanamke, hali ya uhamiaji ndani ya Mkoa wa Kigoma ni mbaya ndugu zangu, lazima ifike mahali tuambiane ukweli. Abiria wa kutoka Mkoa wa Kigoma wanapanda basi saa 11.30 alfajiri, wakifika Uvinza mabasi yanasimamishwa wanateremshwa wote wanaanza kuambiwa wewe shuka tuone uraia wako, mbona maeneo mengine hawafanyi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshalalamika, nimeshaongea mpaka na Mkurugenzi wa Uhamiaji. Kwenye bajeti ya mwaka jana nilimwomba Mkurugenzi wa Uhamiaji pale nje kwamba hali ya operesheni zisizokuwa na ubinadamu hatuzitaki ndani ya Mkoa wa Kigoma. Mkoa wa Kigoma ni wa Tanzania, kama tunaongea lugha moja na Warundi isiwe sababu, ule ni Mkoa wa Waha, ni Mkoa wa Wamanyema lakini sio mkoa wa kusema sio wa Tanzania; nimeongea kwa jazba kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, NIDA, zoezi la vitambulisho vya uraia Tanzania linaendelea katika Mkoa wa Kigoma, lakini cha kunisikitisha, wanaambiwa watoe pesa Sh.15,000 ndiyo waweze kuandikishwa. Hivi hili zoezi la nchi nzima mbona hatukusikia watu wanaambiwa watoe hela; kwa nini sisi kule wanaambiwa watoe hela?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna mambo yanayoendelea ndani ya Mkoa wa Kigoma, kama sisi tusipowasemea hawana mtu mwingine wa kuwasemea. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri, hebu ajaribu kuwasiliana na idara husika, huu uonevu unaofanyika katika Mkoa wa Kigoma hatuwezi kukubaliana nao; tunajua yeye ni mchapakazi, tunajua ni msikivu na mimi binafsi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu Kitila na watendaji wake. Mnyonge nyongeni lakini haki yake mpeni, Mheshimiwa Waziri na timu yake inafanya kazi kubwa sana kuhakikisha wanamtua mwanamke ndoo kichwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo kubwa walilokumbana nalo Wizara hii ni ukosefu wa fedha za kutekeleza bajeti za Wizara tunazopitisha. Natambua kuna fedha tulitakiwa kupokea mkopo wa dola za Kimarekani bilioni 500 toka Exim Bank ya India ili kutekeleza miradi mbalimbali ya maji nchini. Tatizo kubwa ni Wizara ya Fedha kuwataka walipie VAT mkopo huo. Tuombe sheria iletwe ili kumpa mamlaka Waziri wa Fedha kutoa msamaha wa kodi ili tupokee mkopo huo kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji. Sambamba na hili tuongeze tozo ya shilingi 50 ili ifike shilingi 100 kuwezesha miradi mbalimbali ya maji kutekelezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie upande wa miradi ya maji Jimboni kwangu, moja ni Mradi wa Kalya. Naishukuru sana tena sana Serikali kwa kuuwezesha mradi wa maji wa Kalya kukamilika kwa asilimia 95 na tayari maji yanatoka. Nimuombe Mheshimiwa Waziri kuongezewa pesa ili maji haya yanayotoka katika Vijiji vya Tambisho na Kalya yaende hadi Kijiji cha Kashaguru. Pia nimuombe Waziri yeye binafsi tuambatane hadi Kalya kuona jitihada kubwa sana za Serikali ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Mradi wa Rukoma, nitoe masikitiko yangu kwenye mradi huu kwani tenki limejengwa lakini takribani miaka minne sasa hakuna chochote kinachoendelea. Tumeomba zaidi ya mara 20 mradi huu na wa Kandaga kuhamishiwa utekelezaji wake kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza, lakini hadi leo Halmashauri ya Kigoma Vijijini wamegoma kuileta miradi hii Halmashauri ya Uvinza. Tatizo kubwa ni Mhandisi wa Maji Mkoa kwani anatambua fika hii miradi iko kwenye Hamashauri ya Wilaya ya Uvinza. Pamoja na barua za Wizara kuelekeza miradi hii irudi Uvinza lakini yeye amekuwa ni sehemu ya kukwamisha Halmashauri ya Kigoma Vijijini kutoukabidhi Halmashauri ya Uvinza. Nimuombe Waziri wakati akija Kalya tupite na kukagua miradi hii miwili ya Rukoma na Kandaga.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Ilagala; kutokana na ukaribu wa kutoka Ilagala kwenda Mwakizega naomba Wizara itufikirie kuongeza mtandao wa maji kuelekea Vijiji vya Kabeba na Mwakizega.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Uvinza unaenda vizuri. Tunaiomba Serikali kuleta fedha kwa wakati ili mradi huu ukamilike.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Nguruka ulikuwa ukamilike tangu Desemba, 2017 lakini bado haujakamilika. Najua kuwa tuliomba Mheshimiwa Waziri utuongezee mtandao wa maji toka Nguruka hadi Miyabibi. Tunaishukuru Serikali kwa kukubali ombi letu la kupatiwa maji Kijiji cha Miyabibi.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine ni vijiji vya Bweru na Itabula. Nimuombe Mheshimiwa Waziri aangalie uwezekano wa vijiji hivi viwili vya Bweru na Itabula vipate maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe Mheshimiwa Waziri atuangalie kwenye visima hali ni mbaya sana Halmashauri yetu ya Uvinza. Sambamba na hili tuombe suala la bomba la Maragalasi kuwa ni kitovu cha kilimo cha umwagiliaji. Nataka kujua kwa nini huu Mradi wa Kitaifa wa Ziwa Tanganyika usiwanufaishe na wananchi wa Vijiji vya Kalilani, Lufubu, Mgambo, Katumbi, Sigunga, Herembe, Igalula, Kaparamsenga, Kanawena, Kahama, Mkonkwa, Lyabusanda, Msiezi, Sunuka, Karago na kadhalika ili wananchi wanaoishi kando ya Ziwa Tanganyika wanufaike na mradi huu?

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya haya niendelee kuwapa pongezi Wizara hii kwa utendaji wao mzuri. Ili utendaji huu mzuri uendelee lazima Serikali iwe inapeleka fedha za miradi ya maendeleo tunazopitisha hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizo, nianze sasa kuchangia Wizara hii. Kwanza nitoe shukrani za dhati kwa Mheshimiwa Waziri kwa kunipatia ambulance mbili Kata ya Buhingu, kwenye kituo cha afya na ya pili Kituo cha Afya Kata ya Uvinza. Sambamba na shukrani hizi bado tuna changamoto kubwa kwenye Kituo cha Afya Kalya, kina umbali wa kilometa 250. Mheshimiwa Waziri alipofanya ziara alituahidi ambulance ya Kituo cha Kalya, tunaomba tuletewe hiyo ambulance.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunavyo vituo vya afya vinne vinavyojengwa ndani ya Jimbo langu. Vituo vitatu Ukanda wa Ziwa Tanganyika na kituo kimoja ukanda wa reli. Vituo hivyo ni hivi vifuatavyo: Kituo cha Afya Kabeba, Kituo cha Afya Kazuramimba na Kituo cha Afya Igalula (Rukoma). Tunazo pia zahanati mbalimbali zinazojengwa kwa jitihada za wananchi na kupitia Mfuko wa Jimbo. Mheshimiwa Waziri akiona inampendeza atusaidie fedha kwa ajili ya kumalizia maboma haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaishukuru Serikali kwa kutupatia shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Ujenzi umeshaanza, tunaendelea. Tunaomba kwenye bajeti hii tutengewe fedha nyingine kwa ajili ya kuendeleza hospitali hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, majengo hayawezi kwisha bila vifaa na watumishi. Hivyo, tunaomba Mheshimiwa Waziri kwenye mgao wa watumishi, Uvinza iangaliwe kwa jicho la huruma, kwani jimbo ni kubwa na watumishi ni wachache sana. Sambamba na watumishi, tunaomba pia vitendeakazi, kwa mfano Ukanda wa Ziwa Tanganyika na Kituo cha Nguruka wapate vifaatiba kama X-Ray, Ultrasound na vifaa vingine, kwani wagonjwa ni wengi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua fika Halmashauri ya Uvinza ilianzishwa tarehe 18 Mei, 2012 lakini hakuna idara hata moja iliyo na gari. Hii inasababisha Wakuu wa Idara kupata taabu sana kwenye kufanya ufuatiliaji wa utekelezaji wa fedha zinazopelekwa huko chini kwenye kata, vijiji na vitongoji. Namuomba Mheshimiwa Ummy atupatie gari moja, Land Cruiser ya watumishi kufuatilia miradi na utendaji kazi wa watumishi kwani malalamiko ya wananchi ni mengi, ni vyema gari ikapatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, nimkumbushe Mheshimiwa Ummy Mwalimu ahadi yake ya kumpongeza Nesi Zainabu, anayefanya kazi kwenye Zahanati ya Mwakizega kwa kazi nzuri hadi wananchi wakaandamana kumlilia Nesi Zainabu. Maana tangu mwaka 2017 hakuna motisha yoyote aliyopewa kwenye Halmashauri ya Uvinza.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, niendelee kumpongeza mdogo wangu, Mheshimiwa Ummy Mwalimu, kwani ataacha kumbukumbu muhimu sana kwenye hii Wizara. Sote ni mashahidi, anafanya kazi yenye tija na kuridhisha sana. Baada ya pongezi naomba kuunga mkono hoja hii asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshiwa Mwenyekiti, naomba nichangie Wizara hii muhimu sana na ndiyo uti wa mgongo wa Taifa kwani ni zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania ni wakulima na ndiyo wanapata kipato chao. Wizara hii inategemewa sana tumaini la viwanda vya Tanzania vinavyotarajia kupata malighafi za kuendeshea viwanda vyao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pembejeo imekuwa ni tatizo kubwa sana kuna mikoa yenye misimu miwili na mikoa yenye msimu mmoja. Lakini sote tunatambua kuwa wakulima wengi wanaanza kuandaa mashamba mwisho wa mwezi wa nane au mwazo wa mwezi wa tisa. Lakini pembejeo hadi wakulima wamemaliza mashamba na mazao yameanza kuota hakuna pembejeo iliyopelekwa. Niombe Serikali chonde chonde tupelekeeni pembejeo kwa wakati ili wakulima wapate pembejeo za kupandia na kukuzia kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mbegu za ruzuku, huko nyuma tulikuwa na utaratibu wa kutoa mbegu za ruzuku mfano, mahindi, mpunga alizeti, choroko, kunde na kadhalika. Leo hii mbegu hizo za ruzuku hazipatikani, niombe sana kwa Mheshimiwa Rais anataka viwanda vya mafuta vya ndani kwa nini sasa tutoe ruzuku msimu wa 2018/2019 kwa mbegu zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, alizeti, ufuta, michikichi, michikichi, niombe Serikali kwa kuwa Malaysia ilikuja kuchukua miche ya michikichi kutoka Kigoma. Kwa nini Serikali sasa isiombe Serikali ya Malaysia irudishe mbegu, miche ya michikichi ili basi na wakulima wa Mkoa wa Kigoma wanufaike na mbegu hizo kutoka Malaysia. Sambamba na hilo, tunaweza pia kuchukua mbegu za michikichi kutoka Burundi ili basi tuwe na aina tatu za aina ya michikichi ya kutoka Naliendele, Burundi, Malaysia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa na tatizo kubwa sana kwenye zao la tumbaku kwa wakulima wa Tarafa ya Nguruka, Kata ya Basanga, Itebila, Mganza na Nguruka, mfano kucheleweshwa, kutokana kwa makisio ya uzalishaji wa kilo na makampuni waliyoingia mkataba na wakulima, kwa mujibu wa sheria ya makisio yanatoka mwezi wa tatu na mwezi wa nne, hadi leo bado tunasikia makisio hayo ya kutoka mwezi wa Septemba, 2018. Kwa kuchelewesha makisio hayo kutasababisha mambo yafuatayo:-

Kwanza, kuchelewa kuagiza pembejeo, makisio hayo kutolewa mapema ndiyo benki wanajua wamekopesha wakulima kiasi gani, kwa kuchelewa kuna sababisha mkulima kulima chini ya kiwango cha makisio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la masoko, wakulima wamelima mazao mengi, mahindi, maharage, mbaazi mpunga na kadhalika. Tatizo kubwa ni soko, tuombe Serikali iwaruhusu wakulima kuuza mazao yao nje. Tanzania iko kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa nini sasa wakulima wasiruhusiwe kuuza mazao nje ya nchi hususani ndani ya nchi ndani ya nchi za Shirikisho la Afrika Mashariki. Kitendo cha kuwazuia wananchi kuuza mazao yao nje ni kosa kubwa wakulima hawa wanasomesha watoto wao, watoto hawapewi pesa wakati na Serikali mmekataza mazao yasiuzwe nje ya nchi hii ni tatizo kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niombe kumshauri Mheshimiwa Waziri sisi Wabunge wa Majimbo ndiyo wawakilishi wao, anapofanya ziara kwenye majimbo yetu tunapomtafuta tunahitaji kumpa changamoto zaidi za wakulima wetu, sasa anaacha kutupa taarifa za ziara zake ndani ya majimbo na kuacha kuwasiliana na sisi, matokeo yake anasema ya kwake na kupokea changamoto chache, changamoto kubwa za wananchi walio wengi hazipokei, tunaomba sana, atambue umuhimu wa Wabunge wenzake wa Majimbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. HASNA S.K. MWILIMA: Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kuchangia kwa maandishi. Kwanza niwapongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri pamoja na Watendaji wote wa Wizara. Zao la michikichi ni zao linalolimwa Mkoa wa Kigoma na ndiyo asili ya zao hili, japo kwa siku za hivi karibuni, mikoa mingine ya Tanzania nayo inalima zao hili la michikichi. Zao hili linatupa mafuta ya mawese, tunapata mafuta ya mise, tunapata chakula cha mifugo, tunapata na sabuni. Mheshimiwa Waziri Mkuu ameamua kwa makusudi kulisimamia zao hili, binafsi nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa namna ambavyo amewekea mkazo zao hili la michikichi.

Mheshimiwa Spika, ombi kwa Serikali, naomba Wizara isituletee pesa bali itununulie miche ya michikichi ya miaka mitatu ili wananchi wapewe miche na kuanza kupandikiza miche hii ya muda mfupi.

Mheshimiwa Spika, ombi la pili kwa Serikali kupitia Wizara hii ya kilimo, tunaomba mbege kwa kuwa wakulima wa zao hili hawana pesa, wala hawana namna ya kupata hizo mbegu, miche ya michikichi.

Mheshimiwa Spika, ombi la tatu, mashine za kuchakata mafuta ya mawese, kwani kwa sasa wanatumia magogo kukaa watu wanne na kuzunguka hadi jasho jembamba kuwatoka ndiyo wapate mafuta ya mawese. Natambua SIDO wanazo machine za kuchakata mafuta, ni bora wapewe machine kwa mkopo watarejesha pindi watakapopata pesa kwa kuuza mafuta yao. Sambamba na mashine za kukamua mafuta safi na salama ya mise pamoja na machine za kuchakata sabuni, kwa kufanya hivyo Tanzania ya viwanda itakuwa imekamilika.

Mheshimiwa Spika, Tarafa ya Nguruka ni Tarafa yenye wakulima wengi wa za la tumbaku lakini zao hili limekuwa na changamoto nyingi sana, ikiwepo changamoto ya wakulima kubambikiziwa madeni na vyama vya msingi kuwalazimisha wakulima kuchukua mikopo hata kama hawataki siku bank wakiendelea kumdai aliyekopa wanawafilisi wote hata wale wasiokopa.

Kwa hoja, hiyo niombe Waziri au Naibu Mawaziri kupanga ziara ya kuja Uvinza na kusikiliza kilio cha wakulima wa tumbaku, pamoja na changamoto ya kukosa mbolea, mbegu na madawa ya viuatilifu ya kuulia wadudu. Natambua hivi karibuni Wizara ya Muungano chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais imepiga marufuku mifuko ya plastic ifikapo 1/7/2019, Kigoma tunalima mihogo Mkoa wote. Tunaomba Wizara ituletee mbegu ili basi wananchi walime mihogo kwa wingi, kuwezesha viwanda vya kutengeneza karatasi vifunguliwe kwa wingi kwani malighafi zitapatikana.

Mheshimiwa Spika, Uvinza tunalima alizeti, kahawa na ufuta lakini tatizo ni mbegu na pembejeo zote kwa ujumla. Niiombe Wizara ya Kilimo kutuletea mbegu za alizeti, ufuta, kahawa na mpunga tunayo mabonde mengi yanayolimika mwaka mzima hata kama hakuna mvua. Sambamba na ombi la pembejeo na mbegu, tunatambua Wizara ina mpango wa ASDP unaowezesha kujenga maghala, tunaomba Halmashauri ya Uvinza tupatiwe maghala Vijiji vya Kashagulu, Mgambazi, Nguruka, Mganza, Basanza na Ilagala.

Mheshimiwa Spika, baada ya mchango wangu huu, naomba kuunga mkono hoja.
Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Spika, na mimi niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, sambamba na kutoa pongezi lakini kuna tatizo kubwa la TFS na Jeshi la Wanyamapori. Wilaya ya Uvinza ina Hifadhi za Ilunde, Mahale pamoja na Ipuguru. Vilevile ina Msitu wa Pakunda Pachambi na Msitu wa Masanza.

Mheshimiwa Spika, nianze na Hifadhi ya Mahale, hifadhi hii imepakana na vijiji viwili, Kijiji cha Simbwesa na Kijiji cha Kalilani. Kijiji cha Kalilani kilisajiliwa tangu mwaka 1995 kwa Namba 244 na Kijiji cha Simbwesa kimesajiliwa kisheria tangu mwaka 1967.

Mheshimiwa Spika, tumekuwa na tatizo kubwa na DC wa Uvinza kwa kushirikiana na mhifadhi pamoja na watumishi wa Hifadhi ya Mahale. Mheshimiwa DC alienda Kalilani na kuwafokea wazee kama watoto wadogo. Naye Mheshimiwa DC wa Kigoma Mjini Ndugu Hanga alikwenda Kijiji cha Simbwesa akawatukana wanakijiji na kuwatishia kuwa Serikali hii ya Awamu ya Tano haitaki mchezo na mtu na kutoa amri kwa askari na askari wa hifadhi kuwa waweka vigingi ndani ya Kijiji cha Simbwesa na kuwatishia kuwaweka Serikali ya kijiji ndani.

Mheshimiwa Spika, ninavyoona mimi kama mwakilishi wa wananchi hawa wa Vijiji vya Kalilani na Simbwesa sina mahusiano kabisa na Hifadhi ya Mahale kwa kuwa hata wakiwa na suala na vijiji hivi wanatakiwa kunishirikisha mimi, mimi kama mwakilishi wa wananchi badala yake wanatoa hongo kwa viongozi wa Wilaya. Niwe wazi Mheshimiwa DC Mwanamvua Mlindoko ni kero, kero, kero kubwa kwenye suala la utatuzi wa migogoro.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa vijiji hivi viwili vya Kalilani na Simbwesa vimesajiliwa kwa mujibu wa sheria, kwa nini hifadhi walazimishe kuweka vigingi ndani ya eneo la vijiji? Nimuombe Mheshimiwa Waziri watoe vigingi ndani ya vijiji hivi ili wananchi waweze kupata maeneo ya kulima na kufanya shughuli zao za kimaendeleo. Kwa kuwa kuna Kamati ya Waziri Mkuu hivi vijiji vya Kalilani na Simbwesa vimo niombe basi kauli ya Serikali itolewe kuwaachia wananchi maeneo yao. Mgogoro huu una zaidi ya miaka 46.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Msitu wa Masito, tunao msitu huu ambao umekwisha kabisa na hauna wanyama wala miti. Tulipata fedha za ujenzi wa barabara ya Basanza – Lugofu Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza.

Tangu tupewe fedha za ujenzi wa barabara hii inayopita ndani ya Msitu wa Masito ni miezi 12 sasa tunashindwa kuijenga barabara hii kwa kigezo cha kuzuiliwa na Mkuu wa TFS wa Uvinza.

Mheshimiwa Spika, ni barabara ngapi zinapita ndani ya hifadhi za Selous, Ngorongoro Serengeti na kadhalika? Kwa nini sisi Uvinza tusiruhusiwe kuijenga hii barabara ambayo ni muhimu sana kwa wananchi wa Kata ya Basanza? Niombe Mheshimiwa Waziri tupewe kibali kabla pesa hazijarudi Hazina.

Mheshimiwa Spika, Msitu wa Pakunda Pachambi, msitu huu uko chini ya Halmashauri ya Wilaya, lakini changamoto tuliyonayo ni watu wa maliasili kuweka vigingi hadi kwenye vyoo vya wananchi na kusababisha wananchi wa Kata ya Nguruka, Kitongoji cha Humula na Kitongoji cha Reli Mpya kukosa maeneo ya kulima, kujenga zahanati pamoja na kujenga taasisi muhimu za Serikali. Tuombe pia kibali cha kugaiwa ekari kadhaa kwa vitongoji hivi pamoja na Vijiji vya Chagu, Mganza nan Nyangabo ili wapate maeneo ya kulima na kujenga mahitaji yao muhimu.

Mheshimiwa Spika, tuiombe Serikali itupe pesa za kujenga barabara ya kutoka Rukoma hadi Kalilani ili kukuza utalii. Watalii wanapata shida sana ya kutumia boti wakati wa upepo mkali. Tuna vita Rukuga, ni lazima barabara hii ijengwe na TANAPA. Tunaishukuru TANAPA kwa kujenga madaraja mawili, lakini madaraja haya hayana tija kama barabara haitojengwa.

Mheshimiwa Spika, mwisho nitoe shukrani za dhati kwa Mheshimiwa Waziri kwa kutupa Msitu wa Masito – Ugala kwani kwa kupata msitu huu Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza itaongeza mapato. Pia niombe Mheshimiwa Waziri atusaidie gari kwa ajili ya Idara ya Maliasili kwa ajili ya kuijengea ufanisi idara hii. Baada ya kuchangia haya niendelee kumpongeza Waziri na Naibu Waziri.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Madini
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Spika, na mimi nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibau Waziri, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa Wizara. Leo mimi nitajikita kuzungumzia minerals (industries). Madini ya viwandani kama gypsum, lime stone, coltan nakadhalika. Madini ya viwandani yana soko zuri nje ya nchi hasa Afrika Mashariki. Kwa mfano limestone unaweza kusafirisha kwa kuiponda kuwa kokoto au ambayo imekuwa processes au wengine wanachoma zile kokoto na kusafirisha kwenye viloba.

Mheshimiwa Spika, tatizo ambalo wachimbaji wangine wanapata hasa wachimbaji wadogo ni pale wanapohitaji vibali vya kusafirisha madini ya viwandani inawawia vigumu. Kwa mfano wachimbaji wa Kigoma, Katavi na Rukwa, ili wapate vibali lazima wasafiri kuja Dodoma na inaweza kuchukua hata miezi 6 hadi mwaka bila kupata kibali.

Mheshimiwa Spika, natambua Serikali inapenda madini haya ya viwandani yauzwe hapa hapa nchini, lakini tatizo ni bei. Kwa mfano kokoto za limestone zinanunuliwa na wenye viwanda vya saruji na wanalipa 25,000 hadi 35,000 kwa tani ilhali ukipeleka nje ya nchi, kwa mfano Burundi na Rwanda unalipwa USD 150 per tone. Sasa unaweza kuona ni jinsi gani wafanyabiashara wakubwa wa viwanda wanavyowalilia wafanyabiashara wadogo. Tunaomba Wizara iweke kanda za kutoa vibali vya kusafirisha madini ili kurahisisha wafanyabiashara wa madini ya viwandani wasafirishe kwa wakati

Mheshimiwa Spika, la pili ni kuhusu uingizaji wa vifaa vya viwandani kama crusher machines, Grinding machines, processing machines etc. Tunaomba Serikali itoe exemption ili wachimbaji wadogo waweze kuingiza mashine hizi na kuchimba kwa kisasa zaidi kuliko ilivyo sasa, ambapo wanagonga mawe ili yawe kokoto ndipo wapange kumi kwa ajili ya kuchoma. Mkitoa vibali vya kuingiza hizi mashine utapunguza wachimbaji wadogo kuharibu mazingira kwa kukata miti.

Mheshimiwa Spika, mwisho ni kuhusu suala la grants najua kuna mikopo ya wachimbaji wadogo niombe Wizara iangalie na wachimbaji wa Kigoma kwani Jimbo langu lina wachimbaji wengi wa chokaa. Kwa leo mchango wangu ni huo.

Mheshimiwa Spika, mwisho niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri Doto Biteko na Naibu wake Mheshimiwa Nyongo kwa kazi kubwa wanayoifanya kwenye Wizara hii naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Nishati
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia Wizara hii muhimu sana kwenye majimbo yetu. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na watendaji wao wote ndani ya Wizara hii ya Nishati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo langu lina vijiji 61 lakini vijiji ambavyo vina umeme mpaka sasa ni 6 tu. Wengine wakisimama hapa wanasema wamebakisha vijiji 10, 5, tumuombe Mheshimiwa Waziri wakati mnapopanga mradi huu wa Awamu ya III wa REA tukuletea umeme, hebu sisi ambao hatuna umeme kabisa tuwe kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliuliza hapa swali la nyongeza, kwa bahati mbaya ukachanganya Nguruka na Uvinza, ukasema kwamba mimi na wewe tuliambatana Nguruka kwenda kuwasha umeme. Mheshimiwa Waziri mimi na wewe tuliambata Uvinza kwenda kuwasha umeme. Umenichonganisha na wananchi wangu wa Nguruka. Sasa Mheshimiwa Waziri ili kuninasua na wananchi wangu wa Nguruka, naomba sana tuletewe umeme kwenye Vijiji vya Chagu, Ilalanguru, Mganza, Nyangabo, Nguruka, Itegula, Kasisi, Amriabibi na Mpeta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataja vijiji hivi kwa sababu kuna sintofahamu huko, kwamba Mheshimiwa Mbunge mbona Waziri amesema mliambatana kuja kutuwashia umeme Nguruka. Sasa hivi vijiji nilivyovitaja viko kwenye Tarafa ya Nguruka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri aniletee umeme kwa sababu, umeme wa Gridi ya Taifa unaotoka Kaliua umekuja mpaka kwenye Kata ya mwisho ya Usinge. Nachomuomba Mheshimiwa Waziri watuongezee pale substation ya kutoka Urambo ifungwe Kaliua na substation nyingine iletwe Uvinza. Kwa kuyafanya haya, ina maana tutarahisisha sasa umeme wa kutoka Kaliua wa Gridi ya Taifa uweze kuingia katika hivi vijiji nilivyovitaja. Kwa kuingiza umeme kupitia Uvinza, itakuwa rahisi kuupeleka kwenye Vijiji vya Basanza na hatimaye kuingia kwenye Jimbo la Kasulu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe pia kuzungumzia REA awamu ya II. Tunavyo Vijiji vya Kabeba, Mwakizega na Ilagara. Vijiji hivi umeme umeshamalizika kwa maana ya nguzo, transfoma na kila kitu lakini kutokana na mvutano baina ya Wizara ya Nishati na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi mkandarasi aliyekuwa anatekeleza mradi ule kwa maana ya Mkoa wa Kigoma na Katavi na Rukwa alisimamishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali yangu kwa Waziri atakapokuja hapa kuhitimisha bajeti yake anieleze au awaeleze wananchi wa Jimbo la Kigoma Kusini, hivi Vijiji vya Mwakizega, Kabeba na Ilagara, mradi wa REA mkandarasi ataendelea na taratibu zilizobaki kwenye mradi ule wa REA wa Awamu ya II? Kwa sababu tunapata kigugumizi, kama mkandarasi huyu tayari amefutiwa mkataba na hataendelea tena, nani anayeendeleza mradi ule wa REA katika Kata zangu hizi mbili za Mwakizega na Ilagara? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie umeme kuingia Kata ya Kalia. Nimuombe Mheshimiwa Waziri kwa kuwa kutoka Mwese mpaka Kijiji cha Lugufu kwenda Vijjiji vya Kashaguru, Chambusha, Kalia na hatimaye kumalizia Sibwesa ni karibu sana na Mwese kuliko kutoka kule kuja Ilagara. Sasa nimwombe Mheshmiwa Waziri hebu huu umeme ambao uko Mpanda unaelekea Mwese ndiyo mtuweke kwenye progamu ya REA Awamu ya III utoke Mwese, uingie katika hivi vijiji ndani ya Kata ya Kalia. Namuomba kwa unyenyekevu mkubwa na ndiyo maana leo wala siongei kwa jazba, natambua kwamba Waziri ni msikivu, Naibu Waziri ni msikivu lakini ndugu yangu Maganga naye ni msikivu, atanisikia na kwa faida ya wananchi wa Jimbo langu la Kigoma Kusini, wananchi wa Kalia nao watapata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze kwanza Wizara kwa kuona umuhimu wa kuongeza megawatts 45 kutoka Malagarasi hadi Kidahwe. Nipongeze jitihada hizi ni nzuri, najua kwamba mradi huu mkubwa wa Malagarasi ukitekelezwa na njia ile ikijengwa ya kutoka Malagarasi kilomita 53 hadi kufika Kidahwe wananchi watanufaika na kupata umeme wa uhakika. Kwa sasa tunatumia majenereta, uendeshaji wa majenereta jamani ni mkubwa mno na hawa wenzetu TANESCO kama walivyoongea Waheshimiwa Wabunge mbalimbali, uwezo wao umekuwa wa chini mno ukilinganisha na siku za nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie TANESCO. Umeme kwenye vijiji sita kwa maana ya Vijiji vya Mlela, Kandaga, Uvinza, Kazoramimba na Mwamila umeishia barabarani na ukiwauliza REA wanakwambia wenye mamlaka ya kuuchukua ule umeme na kuuingiza kwenye vijiji vya ndani ni TANESCO. Sasa hao TANESCO ambao tunawasema leo tangu mradi wa REA wa Awamu ya II umekamilika, hakuna TANESCO walichokifanya kutoa nguzo barabarani na kuwapelekea wananchi wa Kandaga na Nyanganga. (Makofi)

Mheshmiwia Mwenyekiti, nimuombe sana Waziri, hawa TANESCO mbona wamebaki tu kama jina? Yaani tumebaki na TANESCO kama jina. Kama inaonekana TANESCO imefika mahali imekufa kabisa basi Serikali ituambie ili tusiwe tunasimama hapa kupiga kelele za TANESCO.

TAARIFA . . .

MHE. HASNA S. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tuko hapa kuishauri Serikali, hayo mambo ya mikataba na nini mimi sitaki kujiingiza sana huko. Ndiyo maana tunaishauri Serikali ikae chini ione ni jinsi gani ya kuiwezesha TANESCO. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu, taasisi nyingi ndani ya jimbo langu hazijapata umeme. Kwa mfano, tunayo Shule ya Lugufu Boys na Lugufu Girls lakini tunazo zahanati na vituo vya afya vinashindwa kupata umeme. Mimi niliongea na Meneja wa TANESCO, akaniambia nguzo wanazo nadhani mia moja na kitu lakini hawana pesa ya kuwapa mafundi ili waweze kuchukua zile nguzo na vifaa ambavyo wanavyo wawapelekee wananchi umeme kwenye maeneo ambayo hatujapata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe sana Waziri, Naibu Waziri na Mkurugenzi na pia niungane na wenzangu, huyu Kaimu Mkurugenzi wa REA, Ndugu Maganga jamani athibitishwe kama anaonekane anafaa. Kwa sababu unapokuwa unakaimu, mimi naelewa maana ya kukaimu,
nimefanya kazi Serikalini, ukikaimu unakuwa huna mamlaka, ukikaimu unakuwa huna sauti. Sasa tunabaki kusema mambo mengine akitaka kuyatolea maamuzi anashindwa kwa sababu bado yeye ni Kaimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nimeona wakati Spika anawatambulisha kila aliyesimamishwa pale ni Kaimu. Sasa mtu anapokuwa Kaimu hapati ile confidence ya kufanya kazi yake inavyotakiwa. Kwa hiyo, tuombe Mheshimiwa Waziri umshauri Mheshimiwa Rais ili hawa wanaokaimu kama wamekidhi vigezo waweze kuthibitishwa na hatimaye tuweze kusonga mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na nawapongeza zaidi hawa Mawaziri kwa kweli wanafanya kazi.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nami nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake kwa kuwasilisha bajeti yenye matumaini kwa Watanzania. Hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Waziri kwa sababu mimi niko kwenye Kamati ya Bajeti kwa kusikiliza Wajumbe wa Kamati na kuweza kufanyia marekebisho mambo mbalimbali. Hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na ukurasa wa mapendekezo ya bajeti, ukurasa wa 29 unaosema kwamba, kutoa kipaumbele kwa ukamilishaji wa miradi iliyoanzishwa na wananchi. Nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, tulikuwa tupokee shilingi bilioni 251 kwa ajili ya miradi ya afya na elimu, lakini kwa bahati mbaya mpaka sasa pesa zile bado hazijafika kwenye maeneo yetu. Waziri anafahamu kwamba Waziri wa TAMISEMI aliwaita Wakurugenzi wakakubaliana kwamba ni miradi gani ya kimkakati ambayo wanapendekeza kwenye Halmashauri zao na wakataja ile miradi. Kwa hiyo, tumuombe sana Mheshimiwa Waziri suala la afya na elimu ya msingi na sekondari ni muhimu sana katika majimbo yetu.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu wananchi tumewahamasisha, wamejenga madarasa, wamejenga zahanati, wamejenga vituo vya afya, wanategemea Serikali watakwenda kumalizia kupaua na taratibu zingine ili madarasa haya yaweze kutumika. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba ajitahidi kama anaweza atupatie ile shilingi bilioni 251 ili Waheshimiwa Wabunge wote wakitoka humu waweze kuwa na jambo la kuzungumza kwa wananchi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji ni uhai, sisi wote tunafahamu bila maji hakuna uhai. Waislamu huwa tunafunga na leo bado watu wanaendelea kwenye sita, akifungua kitu cha kwanza anakimbilia maji. Sasa tunazungumzia miradi ya maji, hali ya miradi hiyo siyo nzuri. Tunamwomba Mheshimiwa Waziri atukubalie kwenye mapendekezo ya Finance Bill tuone ni jinsi gani tunaweza tukapenyeza hapo ile Sh.50 kwa ajili ya kwenda kwenye Mfuko wa Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili linawezekana, hata kama Wabunge wengi waliosimama hapa hawakusema lakini kila mmoja ukimuuliza hapa ni wangapi wanapendekeza ile Sh.50 iongezwe ili iende kwenye Mfuko wa Maji, wote watasema ndiyo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri tunaomba kwenye Finance Bill aweze kuliangalia hili na sisi tuko kwenye Kamati ya Bajeti tunaendelea kutoa mapendekezo nadhani na hili tutalileta kwako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nizungumzie kilimo. Uvinza ni wakulima wa tumbaku lakini zao hili wakulima wamefika mahala wamelikatia kabisa tamaa na chanzo kikuu wanachokitegemea halmashauri ni zao hili. Tunaomba sana Wizara ya Kilimo iangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa Mikoa ya Kusini wanaomba zile shilingi bilioni 81, lakini na mimi pia nazisemea zile shilingi bilioni 81 kwa sababu asilimia 65 kwa mujibu wa sheria inatakiwa iende kwa wakulima wa korosho, tunaomba ziende. Kwa nini nasema hivi Mheshimiwa Waziri? Waziri ni mzaliwa wa Kigoma, Naliendele wametuletea miche ya mikorosho, tumepokea miche ya mikorosho, tumehamasisha, wananchi wa Uvinza wamepanda korosho kwa mara ya kwanza. Sasa wakisikia korosho imekufa Ukanda wa Kusini na wenyewe watakata tamaa. Kwa hiyo, tunaomba ile asilimia 65 ipelekwe ili na mikoa mingine kama Tabora, Kigoma, Dodoma ambao tumeitikia kulima hili zao la korosho basi tuweze kupata motisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie miundombinu. Tunapitisha bajeti za Wizara hapa lakini hatimaye inafika tarehe 30 Juni, utekelezaji hakuna. Natambua kwamba sisi tumepata pesa ya Daraja la Ilagala, nimwombe Mheshimiwa Waziri atuletee hiyo pesa ya kujenga Daraja la Ilagala. Wananchi watakuwa wameokoka na vifo vya wamama wajawazito na watoto vitapungua. Wanapopata uchungu wakifika kwenye ferry, SUMATRA wametuambia saa 12.00 jioni ndiyo mwisho wa kivuko kutumika. Daraja la Ilagala likijengwa wale wanawake wa kata sita watakuwa wanavuka wanaenda kwenye Kituo cha Afya cha Ilagala wanajifungua kwa wakati bila madhara yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia hili suala la Electronic Tax. Hili suala siyo baya, tunachosema sisi tunaomba yale mapendekezo ya Mwenyekiti waKamati ya Bajeti yapokelewe na yazingatiwe. Kwa sababu huyu mtu kwa muda wa mwaka mmoja atakuwa amerudisha hela yake na faida juu. Tunapompa mkataba wa miaka mitano tunaonesha ni jinsi gani ataondoka ametajirika kwa pesa za walalahoi. Kwa nini nasema za walalahoi? Tukitumia huu mfumo kwa kampuni hiyo tuliyoipendekeza wanaokwenda kuathirika ni walaji, mfano, wanywaji wa soda, bia na maji na wavutaji sigara. Kwa hiyo, hatulikatai hili lakini kwa nini basi tusitoe kipaumbele kwenye kampuni za wazawa? Kwa hiyo, hili suala liangaliwe tusilirukie sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nizungumzie ukurasa wa 72. Wilaya ya Uvinza ni wadau wa chumvi. Tunashukuru kwamba Mheshimiwa Waziri ameona umuhimu wa kutoa tozo mbalimbali. Kwenye hii tozo ya kwanza ukurasa wa 73(a), kufuta ushuru wa mazao ya chumvi unaotozwa na halmashauri, Mheshimiwa Waziri ametuua. Halmashauri ya Uvinza tunategemea tumbaku na chumvi, hii 0.03 tunaomba atuachie. Leo tulikuwa na mmiliki wa kile kiwanda yeye mwenyewe ameona kwamba hii 0.03 isifutwe, iendelee kuwepo ili na sisi halmashauri tuweze kupata hapo kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Waziri, tunayo madini ya chokaa. Madini haya hapa Tanzania hatuna viwanda vikubwa tuna viwanda...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba suala hili la kwenye chumvi liende pia na kwenye chokaa ili wanaochimba chokaa waweze kunufaika na mimi pia ni mdau wa suala hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na mimi kwa kupata nafasi ya kuchangia kamati hizi mbili, hasa Kamati yangu ya Bajeti kwa sababu mimi ni Mjumbe kwenye hiyo kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuchangia, leo asubuhi nilimsikia mdogo wangu Mheshimiwa Ester Bulaya anasema tuongee kama Taifa tusiongee kama Wabunge wa vyama tofauti, lakini Mchungaji Msigwa hapa ametuambia kama tunawatukana donors tutapataje ile asilimia 40 kuiingiza kwenye bajeti yetu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi napata mashaka kidogo. Juzi tukiwa kwenye kamati Mheshimiwa Waziri wa Fedha alituambia kwamba Serikali ya Ubelgiji imesema haiwezi kutupa misaada kwa ajili hatuungi mkono masuala ya ushoga.

Sasa najiuliza maswali kama tunazungumza kama Taifa, yeye leo ameambiwa na Mheshimiwa Jacqueline hapa kuhusiana na suruali, ameomba Mwongozo, ina maana hapendezwi na hayo masuala. Tunawezaje kukubaliana na donors ambao wanataka vizazi vyetu ambavyo tumevizaa huko baadaye vije kuwa ni vizazi vya asilimia 80 vya ushoga, haiwezekani. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pilipili usiyoila inakuwashaje?

KUHUSU UTARATIBU

MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lema ni mdogo wangu, lakini kama pilipili usiyoila huwezi kujua muwasho wake ukoje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme hivi, kwamba sisi kama Serikali ya Chama cha Mapinduzi tunatekeleza miradi mbalimbali kwa pesa zetu za ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hii imejionesha. Leo kuna mtu alisema kwamba, huwezi kuweka tozo kwamba ni sehemu ya revenue, lakini kwenye taarifa ya REA, kwenye taarifa ya maji, waliyoleta Waheshimiwa Naibu Mawaziri wameonesha ni jinsi gani Wizara ya Fedha imepeleka tozo zote zilizotolewa na miradi imetekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hiyo bilioni 67 point something iliyopelekwa kwenye miradi ya maji imetokana na nini? Imetokana na revenue ya tozo ya lita ya mafuta shilingi 50, petroli na dizeli. Kwa hiyo, pesa zetu za ndani zinatusukuma na miradi, lakini wale wafadhili ambao wanaona hawataki kutuletea masharti yasiyokuwa na msingi na taifa letu wanaendelea kuisaidia Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi. Kwa hiyo tuache upotoshaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijikite kwenye taarifa yetu ya bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kwamba tuna ile miradi ya mkakati, naomba unilindie muda wangu maana Mheshimiwa Lema aliniharibia muda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua tuna ule mkakati wa miradi ya kimkakati kama vile SGR pamoja na mradi wa Mchuchuma na Liganga. Niishauri Serikali, hebu iangalie hii miradi kwa sababu, deni letu la Taifa ni himilivu tuone ni jinsi gani tunaweza tukakopa tukaangalia miradi mikubwa miwili kama SGR, Liganga na Mchuchuma, ili tuwe na uhakika wa kuongeza kipato katika makusanyo yetu ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema hivi kwa sababu Mradi wa SGR tumeuanza kwa pesa zetu za ndani, lakini tuangalie matawi ambayo yana umuhimu zaidi kiuchumi kuliko kuangalia tawi linalokwenda Isaka mpaka Mwanza huku tunaacha kutoka Tabora kwenda Kigoma kama alivyosema mdogo wangu Mheshimiwa Bashe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tuangalie vilevile njia ya kutoka Isaka kuelekea Kigali, ili tuweze kupata mapato zaidi na hatimaye Taifa letu litekeleze miradi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwe mkweli, mnyonge mnyongeni haki yake mpeni. Mheshimiwa Rais ana miaka mitatu, leo ameingiza ndege sita, tunakosa kumpongeza! Hizi ndege, tunayo Dreamliner moja, Airbus mbili, tukitoa direct flight, Dar es Salaam to Guangzhou, Dar es Salaam to New Delhi, hatuwezi kuingiza mapato? Watalii watakuja direct kwa kutumia ATCL. Sasa tusikashifu hapa as if kwamba hizi ndege zilizonunuliwa hazina thamani yoyote ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana tuache upotoshaji, Serikali inafanya kazi. Mheshimiwa Rais ameshasema, hata wewe nyumbani kwako ukitaka ukiwa na maisha mazuri, lazima ujibane. Tutaendelea kujibana ili Taifa lisonge mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naunga mkono hoja Kamati yetu ya Bajeti pamoja na hiyo Kamati nyingine.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru nami kwa kupata nafasi ya kuchangia Wizara hizi tatu; kwa maana ya Mambo ya Ndani, Ulinzi na Usalama, pamoja na Nishati na Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kikao chake alichofanya tarehe 22 pale Dar es Salaam, kuitisha wachimbaji wadogo na kusikiliza kero zao. Ni jambo zuri na kwa kweli wachimbaji wote Tanzania nzima wamempongeza Mheshimiwa Rais pamoja na Waziri na Naibu Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze na Wizara ya Mambo ya Ndani. Ukurasa wa 11, Kamati imezungumzia kuhusu migogoro mbalimbali baina ya wananchi pamoja na Jeshi la Polisi na Magereza. Naomba nizungumzie kuhusu suala la migogoro ya wananchi pamoja Magereza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pale Ilagala tunalo Gereza, lakini ni miaka mingi sana wananchi wa Ilagala wamekuwa wakipiga kelele kwamba Gereza limehodhi maeneo yao na Ofisi ya DC pamoja na Mkurugenzi waliunda Kamati na ikabaini kwamba ni kweli Gereza lilihodhi maeneo ya wananchi bila kufuata utaratibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua nia njema ya Serikali na Wizara kwamba wanahitaji Magereza wawe na maeneo kwa ajili ya kulima kutosheleza chakula cha wafungwa; lakini kwa kuwa Magereza wamechukua karibu ekari 10,000 na kitu, tunaomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hapa, awaambie wananchi wa Ilagala: Je, wameamua ni ekari ngapi zitarejeshwa kwa wananchi ili na wananchi wapate maeneo ya kulima?

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hilo, nitajikita sana kwenye suala la madini. Nimeona hapa Sekta ya Madini inachangia asilimia 4.8 tu kwenye Pato la Taifa. Hii ilinishawishi niingie kwenye mtandao kuangalia kwenye East Africa nchi nyingine zinafanyaje especially kwa wachimbaji wadogo? Nikaangalia kwa mfano, wenzetu Kenya wanazungumzia tu kwenye Kijiji cha Usiri. Kijiji hiki ile revenue per year kwenye local economy tu, kinaingiza Dola za Kimarekani 1.9 million.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiacha hivyo, Migori District, kwenye madini ya dhahabu tu; nataka tu kutoa mfano, madini ya dhahabu tu, Migori wanaingiza 37 Million USD per year. Ukienda Rwanda ambayo ni nchi ndogo sana, unaona kwamba wachimbaji ambao wamewa-formalized pamoja wanaingiza 39.5 million per year, lakini wanakwambia kwa mwaka mzima kusafirisha madini nje kwenye nchi ya Rwanda ni sawasawa na asilimia 20 inaingiza mapato ya Serikali ya Rwanda kwa maana ya hii foreign exchange. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nilitaka nizungumzie suala la madini. Tuliwasikia wachimbaji wakati wanaongea na Rais, walimwomba Mheshimiwa Rais Wizara ya Madini isijikite tu kwenye masuala ya dhahabu, tanzanite na gemstones, wajikite vilevile kwenye industry minerals kama vile gypsum, chokaa na madini mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi, kwa sababu gani? Wachimbaji hawa wanaochimba madini ya ujenzi, Serikali kupitia Wizara ya Madini wangeweza kuwaangalia vizuri, kuwasimamia ili wajiunge wawe na utaratibu mzuri, Serikali ingepata mapato mengi sana kwenye madini ya ujenzi, tofauti kama wanavyong’ang’ania dhahabu na madini mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikizungumzia hivyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, hata ile withholding tax ile 5%, mimi nipo kwenye Kamati ya Bajeti, tuliomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha aweze kuitoa ile kuishusha iende mpaka 3%. Naona Kamati kwenye ukurasa wa 32 nao wamependekeza hivyo hivyo, withholding tax itoke 5% iende mpaka 3%.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata Mheshimiwa Rais wakati anaongea na wachimbaji alionesha kwamba anaridhia na alitoa tamko kwamba Wizara ya Fedha na Wizara ya Madini ikae chini na ione namna gani ya kupunguza hii withholding tax pamoja na tozo nyingine mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, madini ya chokaa yana namna mbili; tuna namna ile kwamba madini yameshakuwa processed kwa maana ya ile lime powder ambayo unaweza ukauza hapa hapa nchini, lakini tuna ile limestones ambayo tunasafirisha nje. Sasa ukienda ukurasa wa 33, mimi naungana kabisa na Kamati kwamba Wizara itoe vibali vya kusafirisha madini nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaposema madini yasitoke nje, madini yanatofautiana. Tanzanite sawa utai- process hapa utaipeleka nje lakini limestone tunasafirisha. Mimi ni mdau, tunasafirisha ikiwa imepondwapondwa kama kokoto, tunapeleka kwa tons tunazisafirisha nje kwa maana ya Kongo, Burundi, Rwanda na nchi nyingine. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, hebu haya mapendekezo ya ukurasa wa 33 tunaomba ayafanyie kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile wachimbaji wadogo wanachajiwa ekari moja Sh.80,000/=. Ni mchimbaji gani anaweza? Unakuta mchimbaji ana-own ekari 30, anatakiwa alipie Sh.80,000/= kwa ekari. Naona Kamati nayo imetoa mapendekezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la NEMC, wachimbaji wadogo wanatakiwa walipe shilingi milioni moja na nusu, wachimbaji wakubwa ndiyo shilingi milioni 4.5. Sasa namwomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atoe tamko zuri ili tuweze kuelewa Serikali yetu na kama Rais wetu alivyo na nia njema katika kuhakikisha hii Sekta ya Madini inakua.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikizungumzia NEMC; wachimbaji wa chokaa wao wanachoma kwa kutumia kuni, sasa hivi wanajipanga kuchukua makaa ya mawe ambayo wanayatoa Mpanda. Wananunua tani moja shilingi 145,000 na kule Mpanda hawaruhusiwi kununua tani moja mpaka waanzie tani tano. Kwa hiyo, unakuta shilingi 145,000 mara hiyo tani tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa kusema hivi, wachimbaji wa chokaa mfuko mmoja wa chokaa ambayo imeshakuwa processed wanailipa Halmashauri shilingi 500 kwa mfuko. Tunaomba Mheshimiwa Waziri, hilo aliangalie. Wanailipa Wizara ya Madini, kwa maana ya Ofisi ile ya Madini shilingi 150.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wanaomba angalau hiyo shilingi 500 kwa mfuko iteremke mpaka kwenye shilingi 250 ili waweze kukidhi na angalau Serikali muweze kupata mapato zaidi kuliko kuweka kiwango kikubwa ambacho mnawasababishia watafute njia za panya kutorosha chokaa zao badala ya kuilipa Serikali na Serikali iweze kupata mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naishukuru sana Serikali, lakini nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuwajali wachimbaji wadogo wadogo wa Tanzania. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ya kusimamia utekelezaji wa Ilani yetu ya CCM ya 2015-2020, sambamba na Waheshimiwa Mawaziri Mheshimiwa Jenista na Manaibu wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze kwanza kwenye hoja ya uwekezaji. Tunatambua Mheshimiwa Waziri Mkuu ameanzisha kampeni ya kufufua zao la michikichi katika Mkoa wa Kigoma, Tabora, Katavi, Rukwa Mbeya Wilaya ya Kyela. Zao hili la michikichi asili yake hapa Tanzania ni Mkoa wa Kigoma na sote tunatambua kuwa zao hili ndilo linalowapa kipato wananchi wa Kigoma likifuatiwa na zao la muhogo na maharage.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka ya nyuma nchi ya Malaysia walikuja kuchukua miche na kupeleka kwao, leo hii Malaysia ndiyo nchi inayoongoza duniani kwa uzalishaji wa palm oil. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoa tamko la kuwa Chuo cha Kihinga kuwa kituo cha uzalishaji mbegu au miche, tunaomba bajeti itengwe kwa ajili ya uzalishaji na ununuzi wa miche ili basi Serikali iweze kuwapa wananchi wake ili dhamira ya kuwa na viwanda vya mafuta ya mawese iweze kutimia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwa kuwa Mheshimiwa Waziri Mkuu alikutana na wadau mbalimbali tarehe 28 Julai, 2018 akaja na Bank ya TIB na TADB, tuiombe Serikali masharti yawe mepesi ili wakulima wengi wa zao la michikichi wapewe mikopo kununua miche ya michikichi. Tumuombe pia Mheshimiwa Waziri Mkuu atuletee wawekezaji wa kununua mazao hayo na kuanzisha viwanda vya mafuta haya ya mawese ili kununua zao hili la michikichi. Nimezungumzia sana zao la michikichi kwa sababu ni zao muhimu sana Tanzania na ulimwenguni kote wanatumia palm oil.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie zao la muhogo. Tunatambua hivi karibuni Serikali ilipokea wawekezaji wanaotoka China wanaohitaji kununua mihogo tani kwa tani kupitia Wizara ya Kilimo. Tunacho Chuo cha Naliendelea kina mbegu nzuri sana za mihogo, swali langu wananchi wanaotoka kwenye mikoa inayolima zao hili wanapataje mbegu ili wawekezaji waweze kununua mihogo yenye tija?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili, Wizara ya Uwekezaji isimamie uanzishwaji wa viwanda vya kutengeneza karatasi na mifuko ya karatasi ili tuondokane na uharibifu wa mifuko ya plastic inayotuchafulia mazingira yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie uwekezaji wa kwenye sekta ya uvuvi. Sekta hii tumeiacha sana lakini kama tutaiangalia vizuri inaweza kutuingizia pato kubwa katika taifa letu. Mfano tunaweza kununua meli za uvuvi katika maziwa yetu ya Victoria, Nyasa, Tanganyika na kadhalika. Kwenye bajeti ya 2018/2019, Mheshimiwa Waziri wa Fedha alionyesha kuweka fedha za ununuzi wa meli za uvuvi, hata bajeti ya mwaka huu 2019/2020 kwenye mpango wa maendeleo tumeendelea kuonyesha kuwa Serikali imepanga kununua meli hizo za uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku za nyuma Mkoa wa Kigoma tuliwahi kupata mwekezaji toka Ugiriki alikuwa na meli ya uvuvi iliyoitwa YOROGWE. Meli hii ilikuwa inavua samaki wengi sana. Kigoma watu wengi wanajua tuna samaki aitwae mgebuka lakini tunao samaki aina nyingi kwa utafiti uliofanywa na Wachina wakagundua tunao aina za samaki 250. Kwa mfano, ninaowajua mimi na kuwala ni mgebuka, kohe, ngenge, sangara, monzi, singa, karongwe, mbaga, mneke, kabare, mbisu, mrombo ndubu na kadhalika. Natambua sekta ya uvuvi, mifugo na kilimo inachangia zaidi ya asilimia 40 ya pato la Taifa. Hivyo ni wakati muafaka sasa Serikali yetu ikajikita kwenye sekta ya uvuvi, kilimo na mifugo ili pato letu la Taifa likue zaidi kwa sekta hizi tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mchango wangu huo, naomba niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anayofanya kwenye Taifa hili. Sote tunamuona jinsi anavyofanya ziara mikoani na ndani ya wilaya zote kufuatilia utekelezaji wa Ilani ya CCM ya 2015- 2020 inatekelezwa ipasavyo. Nimpongeze Waziri, Mheshimiwa Jenista, Waziri, Mheshimiwa Kairuki na Manaibu wote wawili kwa kufanya kazi nzuri ya kumsaidia Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu bila kumsahau Mkurugenzi wa TEA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyuo vya VETA ni mkombozi wa vijana wetu hususan wale waliomaliza darasa la saba na kidato cha nne ambao hawakubahatika kuendelea na masomo. Nchi yetu ina Halmashauri 185, ni muhimu Halmashauri zote nchini ziwe na vyuo hivi ili basi vijana wetu wapate elimu itakayowasaidia kujiajiri na kupunguza vijana wetu kujiingiza kwenye vishawishi vya kuingia kwenye wizi na vitendo visivyokuwa na maadili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi, nashauri Wizara iweke mpango mkakati wa kuanzisha vyuo katika Halmashauri zote nchini. Kwa kuanzia naomba Wizara itoe kipaumbele kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza, kwani tunayo misitu mingi inayoweza kuwasaidia vijana kuvuna mbao na kutengeneza samani mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kushauri Serikali kuangalia namna ya kusaidia Halmashauri mpya kupata vyombo vya usafiri. Halmashauri ya Uvinza haina gari na tunazo shule 122 za msingi, 119 zimesajiliwa na shule tatu (3) ziko kwenye hatua za kusajiliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya kutokuwa na gari kunasababisha wakaguzi kushindwa kutimiza majukumu yao ya ukaguzi wa shule na ukaguzi wa ubora wa elimu inayotolewa. Niendelee kumuomba Mheshimiwa Waziri, dada yangu mpendwa Mheshimiwa Prof. Joyce Ndalichako kutupatia gari angalau tatu; moja ya Ukaguzi na gari mbili, DEO Msingi na DEO Sekondari. Jiografia ya Jimbo la Uvinza ni ngumu sana tena sana na hivyo kusababisha watumishi wa idara hizi kushindwa kutimiza majukumu yao ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ya watu wazima, ukurasa wa 15. Naishauri Serikali kuanzisha vituo hivi kwenye kila Kata ikiwezekana huku baadaye kila kijiji ili elimu hii ya watu wazima iwe mkombozi kwa wote wale wenye mahitaji maalum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ya sekondari, kwanza nitoe shukrani zangu kwa Mheshimiwa Waziri kwa namna alivyosikia kilio cha wananchi wa kata zangu mbili, Kata za Basanza na Mwakizega. Shule hizi zilizojengwa kwa nguvu ya wananchi na Mfuko wa Jimbo sasa zimesajiliwa, nasema ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, ninazo shule mbili za Kata ya Sigunga, Ukanda wa Ziwa Tanganyika na Shule Kata ya Nguruka. Shule hizi mbili zimeshajengwa madarasa sita, vyoo na darasa moja kama jengo la utawala kwa kuanzia. Namuomba Mheshimiwa Waziri aone namna ya kutusaidia kuzisajili shule hizi kwani hadi leo hii tunao wanafunzi 250 Kata ya Nguruka hawajapata nafasi na wengine 780 wameachwa kwenye shule mbalimbali ndani ya Halmashauri ya Wilaya yangu ya Uvinza. Nimuombe Mheshimiwa Waziri atusaidie fedha kwa ajili ya kusaidia shule hizi mbili za Nguruka Sekondari na Sekondari ya Sigunga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kidato cha sita, tunayo Shule ya Lugufu Boys na Girls. Shule hizi zilianzishwa kwenye majengo ya wakimbizi. Miundombinu yake ni chakavu sana na ina mazingira ambayo siyo rafiki, hakuna maji wala umeme. Tuiombe Wizara kuona namna ya kutenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa majengo sambamba na kuwapatia visima ili wapate maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo shule ya walemavu Kata ya Uvinza. Shule hii ni ya msingi, mazingira yake siyo rafiki kabisa, tunaomba msaada kwa ajili ya watoto hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maslahi ya walimu. Hali ya makazi ya nyumba za walimu ni tete, shule nyingi za msingi, sekondari hakuna nyumba na zile ambazo zina nyumba basi ni chakavu hata vyoo hakuna. Tuiombe Serikali kutuletea fedha za ujenzi wa nyumba za walimu pamoja na matundu ya vyoo kwenye shule za msingi na sekondari kwa wanafunzi na walimu, hali ni tete.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kwa kuzungumzia maslahi ya walimu wa shule za msingi na sekondari. Walimu wangu wengi wanayo madai mengi wanadai na hawalipwi. Niombe Wizara ya Elimu pamoja na Wizara ya TAMISEMI ione namna ya kuwalipa walimu wanaodai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo changamoto ya walimu wapya kucheleweshewa kulipwa posho zao za kujikimu kwa mujibu wa sheria pamoja na kuwekwa hadi miezi sita bila kupata posho wala mishahara. Tutoe rai kwa Serikali kujipanga kwani wanatambua fika ni lini watawaajiri walimu. Kwa nini pindi wakitoa tangazo la ajira wasipange na fedha zao kwenye Halmashauri zote nchini ili ajira zinapotoka na fedha ziwe tayari kwenye Halmashauri za Wilaya ili kupunguza usumbufu wanaopata walimu wetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ajira za walimu. Hivi karibuni tumeona tangazo la ajira za walimu na tumesikia walioomba ni zaidi ya 80,000. Ombi langu katika hili, Wizara itupe Halmashauri ambazo zina upungufu mkubwa wa walimu kama vile Halmashauri yangu ya Uvinza. Sambamba na hayo, niombe pia Waziri aje kutembelea Jimboni ili apate muda wa kusikiliza matatizo ya walimu wangu wa Jimbo la Kigoma Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikopo ya elimu ya juu. Nimuombe Mheshimiwa Waziri aangalie Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu kwani wanafunzi wengi wanayo malalamiko makubwa ya kukoswa mikopo hasa watoto wa watu maskini. Nimuombe Waziri atupie macho Bodi hii waache kuwaonea watoto wa maskini hasa wanaotoka vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuchangia hayo, niendelee kumpongeza Waziri na timu yake yote kwa namna wanamsaidia Mheshimiwa Rais kutelekeza Ilani ya CCM kutoa elimu bure sambamba na kuiendeleza elimu Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwakupata hii fursa uya kuchangia Wizara muhimu sana, Wizara ya Maji, maana bila maji hakuna uhai. Nianze kwa kumpongeza Profesa, Mheshimiwa Waziri maana yake juzi nililia kidogo kuhusiana na mradi wangu wa Nguruka Mheshimiwa Waziri na Katibu Mkuu wamenisaidia lita 2,000 za mafuta. Nawashukuru sanaMheshimiwa Waziri pamoja na Katibu Mkuu kwa namna ambavyo walivyoweza kuwasaidia akinamama wa Tarafa yangu ya Nguruka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba sasa nizungumzie suala la miradi yangu ya maji iliyoko jimboni. Naomba nizungumzie Mradi huo wa Nguruka, namwomba Mheshimiwa Waziri, natambua kwamba ule mradi ni wamuda mrefu na kiasi fulani umekamilika, lakini bado ile extension ya kutoka pale Nguruka kwenda Kijiji cha Bweru na Kijiji cha Mlyabibi haijaanza kutekelezwa. Kwa hiyo namwomba Mheshimiwa Waziri,kwa sababu waliahidi wenyewe kama Wizara kwamba mradi ule chanzo chake cha maji kinatosha kupeleka maji yale mpaka Mlyabibi lakini sio tu Mlyabibi na Kijiji cha Bweru. Sambamba na hilo nimwombe tu Mheshimiwa Waziri ajaribu kumwomba Mkandarasi aweze kumaliza basi hayo maeneo mawili kwa maana ya Bweru, pamoja na Mlyabibi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili naomba nizungumzie Mradi wangu wa Kandaga. Ninao Mradi waKandagaambao utekelezaji wake ulikuwa ni bajeti 2013/ 2014, lakini hadi leo hii Mheshimiwa Waziri ni shahidi tulifanya naye ziara, tulienda pale, maji yanatoka kiasi, lakini wananchi bado hawajapata maji. DP zimewekwa, tanki lipo, maji yanatoka, lakini wananchi hawajapata maji, kwa hiyo wananchi wa Kijiji cha Kandaga wamenituma, wanasema wanaomba sana kama mama niko hapa, waliniamini na wanataka waniamini tena hapo baadaye, kwa hiyo naomba Mradi ule wa Kandaga uweze kutoa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu naomba nizungumzie Mradi wangu waKijiji cha Rukoma. Tunao mradi mkubwa katika Kijiji cha Rukoma lakini kwa bahati mbaya mradi ule una chanzo kikubwa cha maji, chanzo chake ni Mto Luegele, mto huu una maji mengi sana kiasi kwamba hata wenzetu wa Wizara ya Nishati wanatarajia kufua umeme kupitia chanzo hiki. Sasa ombi la kwanza naomba aidha niMheshimiwa Waziri au ni Mheshimiwa Naibu Waziri watafute siku tuambatane waende wakashuhudie ule Mradi wa Rukoma lakini wakashuhudie hicho chanzo cha maji. Chanzo kipo, tatizo ni utekelezaji wa ule mradi umesimama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo naomba nizungumzie Mradi wa Ilagala, tunao Mradi mkubwa wa Ilagala lakini mradi ule unaonekana kwamba ulitekelezwa chini ya viwango. Kwa hiyo Ilagala sio mbali Mheshimiwa Waziri atakapokuja kwenda Rukoma nitaomba pia tuambatane twende Ilagalailiaweze kuona tunafanyaje hapo kuwasaidia wananchi wa Vijiji vya Ilagala na vitongoji vyake kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri amezungumzia kwenye kitabu chake ni jinsi gani Wizara wanajipanga kutekeleza Mradi wa Usambazaji Maji kutoka kwenye Maziwa Makuu kwa maana ya Ziwa Nyasa, Ziwa Victoria pamoja na Ziwa Tanganyika. Mimi najiuliza maswali sipati majibu, Ziwa Tanganyika maji yake ni baridi, ni kama tu maji haya ya Kilimanjaro na maji mengine, kwa nini hakuna mkakati maalum wa kuvisaidia vijiji 34 ambavyo vinapakana na Ziwa Tanganyika. Ukiangalia wananchi wale wanakaa karibu na Ziwa lakini hawana maji safi na salama. Kwa hiyo nimwombe sana Mheshimiwa Waziri watakapokuwa na mkakati wa makusudi, naomba basi watambue kwamba Jimbo langu lina vijiji 34 vinavyopakana na Ziwa Tanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na mpango mkakati wa Wizara ya Maji na Wizara ya Kilimo by that time, kwamba wanataka kutekeleza mradi mkubwa wa Mto Malagarasi. Sasa sijajua Mheshimiwa Waziri mradi ule umefikia wapi? Labda Jumatatu akija hapa kuhitimisha atuambie ule mpango mkakati wa Mradi huu mkubwa wa Mto Malagarasi umefikia wapi, kwa sababu kama sisi watu wa Kigoma tukiweza kupata Mradi kutoka Ziwa Tanganyika pamoja na wenzetu wa Katavi na Rukwa, lakini tukapata pia Mradi wa Mto Malagarasi hata wenzetu wa Kaliuwa, wenzetu wa Urambo pia watapata maji safi na salama kupitia katika Mradi huu mkubwa wa Mto Malagarasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, niiombe sana Serikali iangalie namna ya kuwaongezea pesa wenzetu hawa wa Wizara ya Maji. Nasema hivi kwa sababu kwenye bajeti ya 2018/2019, Wizara hii ilipangiwa takribani shilingi bilioni 697 na ushee, lakini kwenye bajeti hii Wizara imepangiwa pungufu ya shilingi bilioni 66. Sasa niiombe sana Wizara ya Fedha, najua kwamba Mheshimiwa Naibu Waziri yupo hapa, hii Wizara ni Wizara nyeti sana, wengi wameongea kila mtu ameongea kwa hisia zake kwa sababu sisi Serikali yetu kupitia Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi tunasema kwamba tutamtua mwanamke ndoo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante kwa mchango mzuri Mheshimiwa.

MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwakuunga mkono hoja nakuzidi kuwapongeza Mawaziri pamoja na Katibu Mkuu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru nianze kwa kumpongeza Waziri, pamoja na Manaibu wake Mawaziri na Watendaji wote wa Wizara hii muhimu sana katika majimbo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kuzungumzia madaraja, jimbo langu lina eneo moja korofi sana tunaita kwenye kivuko cha Malagarasi kwenye ukurasa wa 167 nimeona mmeelezea kujenga daraja la Mto Malagarasi sasa nilikuwa nataka ufafanuzi Mheshimiwa Waziri atakapokuja, hapa nione je, hili daraja la Mto Malagarasi mnalenga daraja gani, Kwenye ukurasa wa 167? Ndiyo daraja la Ilagala kwa sababu linapita pale kwenye Mto Malagarasi au mnalenga daraja lipi? Kwa sababu nilipomwuliza Mheshimiwa Waziri aliniambia niangalie ukurasa wa 340. Ukurasa wa 340 mnazungumzia kujenga daraja kwenye Mto Rwegere. Mto Rwegere upo kwenye Kijiji cha Mgambazi, unakwenda mpaka kwenye Kijiji cha Rukoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naona hapa kuna contradiction ambayo ningependa Mheshimiwa Waziri na Naibu Mawaziri mliangalie vizuri, kama mtakuwa mnalenga Ilagala, basi nadhani ni hili daraja la Mto Malagarasi. Kwa hiyo, naomba kwa faida ya wananchi wa ukanda huo, basi Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha ataweza kunifafanulia vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili nizungumzie suala la gati. Tunazo gati mbili kubwa zinazojengwa; gati ya Sibwesa na gati ya Mgambo. Naomba tu gati ile ya Sibwesa sasa ikamilike kwa sababu imekuwa ni muda mrefu sana. Gati ile mara kwenye kitabu mmendika ukamilishaji asilimia 91. Bajeti ya mwaka 2018 mlisema ukamilishaji asilimia 90. Sasa kila mwaka mnapokuja hapa mnaongeza asilimia fulani ya ukamilishaji. Naomba mnisaidie kukamilisha bandari ile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nizungumzie suala la SGR. Nimeangalia kwenye ukurasa wa 212, ule mtandao wa SGR mnazungumzia tu Dar es Salaam mpaka Tabora, Tabora – Isaka, Isaka – Mwanza. Tumekuwa tunalia hapa Bungeni mbona hamwoneshi ule mtandao wa kutoka Tabora mpaka Kigoma? Hata kama itachukua miaka mitatu, miaka minne kukamilika lakini tunaomba kwa sababu mpango unatambua huu mtandao wa kwenda Tabora, basi tunaomba Mheshimiwa Waziri aweze kuzingatia kuonyesha na ule mtandao wa kutoka Tabora kwenda Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie barabara ukurasa wa 164. Ninayo barabara yangu ya Uvinza mpaka Malagarasi kilometa 51.1 na kilometa 36 kutoka Chagu mpaka Kazilangwa. Ninajua kwamba kwenye Mfuko ule wa Maendeleo ya Abudhabi Mheshimiwa Waziri wa Fedha alishatia saini kupokea pesa takribani miaka miwili iliyopita. Sasa ninachoomba ni utekelezaji. Ni lini Serikali itatangaza tenda kwa ajili ya Mkandarasi kuanza ujenzi wa barabara hiyo ya kutoka Uvinza - Malagarasi na hicho kipande cha Chagu mpaka Kazilambwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, tunayo hii barabara yetu hii ya kutoka Simbo mpaka Kalya ina kilometa 250. Kila mwaka mnaitengea fedha shilingi bilioni 1.9, shilingi bilioni 1.8 lakini tusipoteze hizi fedha za Serikali, tunatenga pesa nyingi kwa ajili ya kujenga barabara kiwango cha udongo na changarawe, sasa kwa nini tusiende kwenye kiwango cha lami? Hii barabara tangu mmeanza kuijenga ni takribani miaka zaidi ya 20. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri aangalie namna ya kupandisha hadhi barabara hii iweze basi kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie bandari ya Kigoma. Asubuhi nilimsikia Mheshimiwa Zitto anaongelea bandari. Bandari hii ni kwa faida ya Wabunge wote na wananchi wote ndani ya Mkoa wa Kigoma. Leo ninavyoongea, tunao Mkutano mkubwa pale Kigoma ambao ulikuwa Mheshimiwa Makamu wa Rais awe Mgeni Rasmi, lakini amemtuma Mheshimiwa Kandege kumwakilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna wafanyabiashara kutoka Zambia, tuna wafanyabiashara kutoka Burundi, tuna wafanyabiashara kutoka Congo na Rwanda; wameanzia jana, wako kwenye mkutano mkubwa wa wafanyabiashara wanaozunguka Ziwa Tanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naiomba Serikali waone umuhimu wa bandari ya Kigoma. Bandari hii ina umuhimu sana. Tunafanya biashara na watu wa Zambia, Congo na Burundi, wanachukua mizigo yao Dar es Salaam wanaipeleka Congo, Zambia na Burundi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa bandari hii, kwa sababu Benki ya Afrika iko tayari kutusaidia fedha, tunaomba Serikali iangalie kwa jicho la huruma ili basi bandari hii na itaiingizia fedha Serikali, ni chanzo cha mapato, yaani...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Hasna muda wako umekwisha.

MHE. HASNA S.K. MWILIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na mimi kuchangia mpango wetu huu wa maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa mpongeza Mheshimiwa Waziri kwa namna anavyosimamia Wizara hii, Wizara nyeti na Wizara ambayo ndiyo inatupa mustakabali wa Taifa letu la Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niko Kamati ya Bajeti, Kamati ya Bajeti wasiwasi wetu mkubwa ilikuwa ni kuona utekelezaji wa mipango tunayoipanga. Mfano nizungumzie ile miradi ya vielelezo, mradi kama ule wa SGR, mradi kama huu wa Liganga na Mchuchuma, mradi wa uwekezaji Bagamoyo lakini pia mradi wa maeneo ya uwekezaji kama vile Kurasini. Tunachokiona hapa kwa mfano kwenye SGR Serikali inatumia pesa zake za ndani, kwa kutumia pesa zake za ndani mradi huu utachukua muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tuko kutokea Morogoro kwenda Makutupora, tutoke Makutupora tuje mpaka Dodoma, tuendelee mpaka Isaka, Isaka – Mwanza, Mwanza – Isaka – Tabora na Tabora – Kigoma. Sasa mimi nikawa nafikiri dhamira ya Serikali ni mradi huu wa SGR ukamilike ili Serikali ianze kukusanya mapato. Sasa nikawa najiuliza kwa nini Serikali kama inakopesheka isione namna ya kukopa pesa ili huu mradi wa SGR uweze kukamilika kwa muda mfupi na tuweze kuona matunda yake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nizungumzie kuhusiana na mabehewa reli ya kati. Serikali imeweka mkakati wa kununua mabehewa 200 na wanasema hadi sasa wamenunua mabehewa 70. Nilifikiri kwamba tungejikita kununua haya mabehewa yote 200 ili tuanze kuchukua mizigo inayotoka Dar-es-Salaam badala ya kusafirishwa na magari isafirishwe na treni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukianza sasa hivi tunakuwa tumejihakikishia kwamba SGR itakapokamilika tutakuwa na mzigo wa kutosha ili wafanyabiashara waanze kuona sasa kumbe badala ya kutumia magari tuna uwezo wa kutumia reli kupeleka mizigo yetu Mwanza, Isaka, Tabora na Kigoma. Ukiangalia tayari Serikali ina mkakati maalum wa kuweka bandari ya nchi kavu pale Kibaha lakini pia ina mkakati maalum kuweka bandari ya nchi kavu pale Kigoma. Sasa tukiboresha reli ya kati pamoja na mabehewa nadhani tunaweza tukafanya vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nilitaka nizumgumzie hii miradi ya elimu. Miradi ya elimu Serikali imefanya vizuri lakini bado kuna changamoto kwenye maboma. Ukisoma kwenye Mpango wanasema wananchi wahamasishwe kuchangia maendeleo yao. Wananchi wamehamasishwa, wamechangia madarasa, vyoo na nyumba za walimu, tatizo kubwa ni katika umaliziaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha aliangalie hilo, lakini dada yangu Mheshimiwa Joyce Ndalichako kazi nzuri anayoifanya na yeye aangalie ni mkakati upi ndani ya hii miezi sita iliyobaki tunaweza tukamalizia maboma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano pale kwangu Nguruka ninayo shule mpya imejengwa, mkandarasi anadai kama shilingi milioni 76. Serikali inaweza ikafumba macho ikatuletea hela hizo, tumeshajenga vyumba sita, tunataka kama shilingi milioni 76 ili vile vyumba vikamilike na shule iweze kuanza. Watoto wanasoma kwenye maabara za Shule ya Sekondari ya Nguruka. Kwa hiyo, mnaweza mkaona mnafanyaje kutupa pesa ili tuweze kukamilisha ujenzi wa shule ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nizungumzie hali ya miradi ya maji. Tunayo miradi mingi ya maji ambayo haijakamilika. Mfano pale kwangu tunao Mradi wa Rukoma. Serikali katika miradi hii mikubwa ya vielelezo, sawa mmeweka kujenga Mradi ule wa Ziwa Viktoria, lakini hata hii miradi ambayo ilishaanzishwa kwa sababu ipo ndani ya mpango ni vema tukajipanga namna ya kuimalizia ili wananchi waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hii miradi mikubwa ya vielelezo, hivi tumewezaje kuanzisha Mradi wa Ziwa Victoria unaotoka Mwanza unaenda Tabora, Igunga, Uyui mpaka Nzega, kwa nini hatuweki mkakati wa makusudi wa kutoa pia mradi wa maji kutoka Ziwa Tanganyika. Maji ya Ziwa Tanganyika ni baridi unaweza tu ukachota ukayanywa, kwa hiyo nafikiri katika mpango ujao wa miaka mitano tunaweza pia tukaanza kuweka maandalizi ya kuweka huu Mradi wa Maji wa Ziwa Tanganyika ambao utasaidia karibu mikoa mitatu Mkoa wa Kigoma, Mkoa wa Katavi na Mkoa wa Rukwa Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili nimpongeze Mheshimiwa Rais juzi na mimi nilipata fursa ya kupokea ile Dreamliner ya pili, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais amejiwekea mipango yake na ameweza kuitekeleza. Hii ni changamoto kwa Waheshimiwa Mawaziri kwamba Rais amesema lazima ninunue ndege, lazima nifufue ATCL na amefanya hivyo, sasa haya mambo na Mawaziri kila mmoja aangalie kwenye Wizara yake na yeye anatimizaje ahadi ambazo ameziweka katika huu Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri huku tunanunua ndege, tuweke pia na mkakati madhubuti wa kuboresha viwanja vyetu vya ndege. Kiwanja cha Kigoma, Kiwanja cha Tabora, Kiwanja cha Mwanza, Kiwanja cha Mbeya, hii mikoa mikubwa mikubwa kiwanja cha Arusha pale Mjini tunao Kilimanjaro lakini tunayo Arusha Airport, hebu tuboreshe. Hapa nataka nitanie kidogo tu, hizi ndege zetu ni nzuri na zinafanya vizuri, lakini mle ndani nako tunaowaajiri wale ma- air hostess hebu tuangalie ambao hata wakiitwa mle kwenye ndege unamwita air hostess akigeuka hivi abiria anaona kweli tuna ma-air hostess humu ndani, lakini naangalia kama vile, mtanisamehe ndiyo maana nimesema hili nilizungumze jamani, unakuta air hostess, sijui mnatumia vigezo gani, mfupi hana mvuto wa kuifanya ndege yetu ya Air Tanzania ionekane. Leo mimi Hasna hapa nimezeeka nina miaka hamsini na kitu, lakini ukiniweka..

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hasna, kuna taarifa ya Musukuma tusikilize

MHE. HASNA S. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Musukuma ananiharibia.

T A A R I F A

MHE. KASHEKU J. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa kuhusu utaratibu Mheshimiwa Hasna kwamba huu ubaguzi anaoutaka sisi binadamu tunatofautiana, wengine tunazaa watoto hawana hizo shepu ambazo anazitaka, lakini tunazaa wafupi, tunazaa weusi, sasa tutakuwa na mizigo ambayo tumeisomesha halafu kwenye ajira kunakuwa na ubaguzi. Ni hayo tu.

MWENYEKITI: Ahsante. Hiyo taarifa nzuri wafupi pia wazuri Mheshimiwa Hasna.

MHE. HASNA S. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sifa ya air hostess lazima awe mrefu aliyenyooka, akiwa mvulana, akiwa msichana, awe mrefu aliyenyooka. Tunaomba hilo lizingatiwe, ndege zetu zinafanya kazi nzuri, tunataka na ma- air hostess pale wawe na mvuto ili abiria wanaposafiri waweze kuona tofauti na ilivyo sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie na bandari, naomba katika mpango Mheshimiwa Waziri amezungumzia kuendeleza Bandari ya Kigoma, Bandari ya Kalema, kwa ajili ya kuteka soko la Kalemi lakini vis-a-vis na ununuzi wa meli ya mizigo na meli ya abiria. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri Mpango hebu tujitahidi kuhakikisha kwamba meli ya mizigo inanunuliwa katika Ziwa Tanganyika, meli ya abiria inanunuliwa katika ziwa Tanganyika, lakini sambamba na kuitengeneza meli ya Mv Lihemba, watu wa Kigoma wanauliza Mv Lihemba itakamilika lini? Sasa hivi hakuna usafiri wowote ule wa meli kubwa ndani ya Ziwa Tanganyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naunga mkono Mpango, ni mzuri na nampongeza sana Mheshimiwa Rais na niwaombe Watanzania wote, tunapoenda kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa jamani Rais kafanyakazi Chama cha Mapinduzi kimefanya kazi, twendeni tukaonyeshe mfano, tarehe 24 Novemba tupige kura kumwonyesha Rais kweli Chama cha Mapinduzi kimefanya kazi katika miaka yake hii minne. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru nami kupata hizi dakika tano za kuchangia taarifa hizi za Kamati mbili, lakini nitajikita zaidi kwenye taarifa ya Kamati moja ya Miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kwamba Serikali imefanya kazi nzuri sana ya kuboresha Bandari mfano, Mwanza, vilevile kuboresha gati kwa zile bandari ndogo ndogo kama ambavyo taarifa inavyojieleza hapa. Pia kama ambavyo taarifa inavyojieleza kumekuwa na ahadi ya Serikali ya kujenga meli mpya kwenye Maziwa Makuu mfano, Ziwa Victoria, Ziwa Nyasa na Ziwa Tanganyika. Tumeona kwenye Ziwa Victoria baadhi ya meli mpya zimeweza kuwasili, lakini pia ukarabati uliofanywa kwenye meli mbalimbali zilizopo ndani ya Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu tu kwa Serikali, kwa kuwa ndani ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliowekwa wa mwaka mmoja na miaka mitano wamepanga kutengeneza meli kubwa ndani ya Ziwa Tanganyika ya kubeba abiria lakini meli pia kwa ajili ya mizigo. Tuwaombe tu Serikali waone umuhimu wa kufanya hivyo kwa sababu ndani ya Ziwa Tanganyika tumepakana na nchi jirani ya DRC na nchi jirani ya Zambia. Kwa kufanya hivyo tutaweza kufanya biashara ya kutoka Tanzania na kuelekea Congo vis-a-vis Zambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikigusa uchukuzi naomba pia niguse suala la miundombinu kwa maana ya sekta ya barabara. Kwenye Jimbo langu Serikali ilipokea pesa kiasi cha shilingi bilioni 35 kutoka kwenye Mfuko wa Maendeleo ya Abu Dhabi kwa ajili ya kujenda barabara yenye urefu wa kilomita 51.1 kutoka Uvinza hadi Malagarasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu Serikali ipokee pesa hizo leo tunavyoongea ni mwaka wa tatu utekelezaji hakuna, niombe tu Serikali sasa hivi hali ya mvua ile barabara imeharibika sana, kila wakati tunapofanya maintenance bila kujenga barabara kwa kiwango cha lami inakuwa haitusaidii na badala yake tunapoteza pesa za Serikali. Kwa hiyo niombe Wizara ione ni namna gani itatangaza tenda ili hii barabara ya Uvinza hadi Malagarasi iweze kujengwa pamoja na kile kipande cha Chagu hadi Kazilambwa chenye zaidi ya kilomita 48. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu muda ni mfupi naomba nizungumzie kidogo kuhusu NIDA. Natambua kwamba dhamira ya Serikali ni njema katika kusitisha wale wote ambao hawajasajili simu zao kwa alama ya vidole, lakini hii nchi ni kubwa na miundombinu yake sio rafiki. Hivi ninavyoongea katika Jimbo langu hata asilimia 20 haijafika, kwa hiyo niiombe sana Wizara niiombe Serikali wanapokuwa wanatupa taarifa Wabunge watambue kwamba hata wale Maafisa wa NIDA hawapo site.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano ndani ya Wilaya ya Uvinza Maafisa wa NIDA hawapo, wananchi wamezimiwa simu zao, mawasiliano yao, wazazi wana watoto wao Dar es Salaam, wana watoto wao Dodoma wanatumiwa pesa kwa kutumia simu zao. Niombe tu Serikali ije na mkakati maalum waone ni jinsi gani waweze hata kuwasajili kwa vitambulisho hivi vya wapiga kura, kwa sababu Watanzania wengi wana vile vitambulisho vya kupigia kura, lakini hivi vitambulisho vya uraia kwa masharti ambayo Serikali imeweka kwa kweli itakuwa na wakati mgumu sana, tunaweza tukamaliza mwaka bado Watanzania hawa walioandikwa humu milioni 15 wakawa bado hawajasajili simu zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niunge mkono hoja na nishukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii muhimu sana, Wizara inayoshughulika na masuala ya uvuvi pamoja na mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jimbo langu mimi asilimia kama 70 hivi au 65 wanajihusisha na masuala ya uvuvi; lakini hapo hapo tena asilimia hiyo hiyo au zaidi wanajihusisha na masuala ya mifugo. Kwa hiyo nitachangia mambo yote mawili; lakini kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri na timu yake yote ya Wizara kwa namna ambavyo wameweza kuwasilisha taarifa ambayo inatupa matumaini. Nina imani wavuvi na wafugaji wanaweza wakaona mwanga mpya unaotaka kuja katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la uvuvi. Kulifanyika operesheni kwenye Ziwa Tanganyika, wavuvi wetu wakatupigia simu Wabunge na mimi nikamuona Waziri pamoja na Naibu Waziri. Nitoe shukrani zangu za dhati kwamba jana walitupa nafasi ya kuwasikiliza wavuvi zaidi 35 kutoka Ziwa Tanganyika, na tatizo kubwa ilikuwa ni uvuvi kwa kutumia ring net.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru kwamba jana tulimaliza mazungumzo salama, lakini bado wale wavuvi wanahitaji kurudishiwa nyavu zao saba ambazo zilishapimwa kwenye ile operesheni ya kwanza na zikaonekana zinafaa. Nashukuru kwamba Mkurugenzi amewaita kesho asubuhi saa mbili ili aweze kukutana nao. Sasa naomba nyavu zao zirudishwe, mashine zao zirejeshwe kwa sababu ndicho wanachokitegemea kupata kipato kwa dhana hizo zilizoshikiliwa nje ya utaratibu na nje ya Sheria ya Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimzungumzie, Mheshimiwa mwenzangu amesema siyo vizuri kumtaja mtu mimi naomba nimtaje. Namtaja kwa sababu Mheshimiwa Tizeba aliyekuwa anamlenga ni yuleyule mama anayeitwa Judith ambaye leo mmetuletea kwenye Mkoa wetu wa Kigoma. Wabunge wote hapa nyuma, Mbunge wa Ukerewe, Mbunge wa sengerema, Mbunge wa wapi sijui wote wanazungumza kuhusiana na huyu Mama Judith. Huyu mama anaripoti kila mwezi TAKUKURU kutokana na madudu aliyoyafanya Mwanza. Leo mtu anayeripoti TAKUKURU kwa madudu aliyoyafanya Mwanza mnatuletea Kigoma kuja kuua uvuvi na wanachi wanategemea hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri mimi nakufahamu, wewe ni msikivu na ndiyo maana ulitupa nafasi ya kutusikia pale Wizarani jana; huyu mama tafuta pa kumpeleka siyo Kigoma, Kigoma hatumtaki. Kama alitoka Mwanza akaletwa Kigoma na Kigoma hatumtaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu gani, anakamata hizo ring net…..

MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Heche.

T A A R I F A

MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa dada yangu Hasna taarifa hivi ule utaalam wa Kigoma siku hizi hawatumii mpaka…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hasna umemsikia? Taarifa yako haijasikika Mheshimiwa Hasna endelea.

MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Heche huwa anapenda kila nikisimama kunipa taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wangu hizo dakika kidogo naomba zilindwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu mama ametumwa kutekeleza kazi kwa mujibu wa sheria lakini amefika kule anaharibu utaratibu mzima wa uvuvi kwenye ziwa lote la Tanganyika, kwa maana ya Kigoma, Katavi na eneo kidogo la Rukwa. Jana amewaita baadhi ya wavuvi wa Kigoma Mjini wakiongozwa na mtu anaitwa Francis Kabure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu Francis ni Mrundi, mimi nimepiga simu Kigoma nikauliza huyu mtu ni Mtanzania, wananiambia ameshaomba uraia zaidi ya mara tatu bado hajapewa uraia. Mheshimiwa Waziri swali langu hivi Sheria ya uvuvi inasemaje kuhusiana na mtu ambaye si raia na anapewa cheo cha kupambatizwa kwamba yeye ndiye Mwenyekiti wa Wavuvi Mkoa wa Kigoma kachaguliwa na Judith kwa maslahi yapi? na amemleta mpaka Dodoma na ushahidi tunao na jana amekaa kikao na Mkurugenzi wa Uvuvi. Japo Mkurugenzi ni haki yake kuwasilikiza hilo mimi siwezi kuhoji, lakini je, ana maslahi gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri huyu mama hatumtaki tunaomba utuondolee pale Kigoma, tafuta pa kumpeleka. Kwanza hana sifa ya kuendelea kuwa msimamizi iwe Nyasa, iwe Victoria iwe Tanganyika kwa sababu tayari anashutuma za rushwa ndani yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili niendelee kuishukuru pia Wizara. Jana tulikuwa tunazungumzia masuala ya tozo; suala hili la uvuvi linatozo nyingi sana. Naomba Mheshimiwa Waziri kwenye mabadiliko ya kanuni ujaribu kuangalia kidogo hizi tozo mvuvi analipa, mtumbwi unalipwa, akisafirisha dagaa analipa. Jaribu kuziweka iwe ni win situation, Serikali mpate na sisi pia tupate.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie mifugo kwa haraka haraka kabla kengele nyingine haijapigwa. Kuna suala hile…..

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hasna kengele ya pili hiyo nakuachia kidogo umalizie, hii ni ya pili.

MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru naomba suala moja tu la Mwanduhu Bantu. Nimeona hapa Mheshimiwa anaonesha Uvinza kuna ekari kama 49 kwa ajili ya kugaiwa wafugaji. Mheshimiwa Waziri ulikuja ukatoa maelekezo eneo la Mwanduhu Bantu umeriridhia tuendelee nalo kama halmashauri tugawe vitalu, wafugaji wagawiwe na wakulima wagawiwe. Naomba utakapokuja kuwasilisha kesho uweze kutupa tamko rasmi, ni lini sasa umeturuhusu ili tuweze kupata mapato haya na wewe pia Wizara yako itapata mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya naendelea kumpongeza Waziri, Naibu Waziri, Makatibu Wakuu wote pamoja na Mkurugenzi wa Idara hii ya Uvuvi, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi. Kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na timu yote ya Wizara kwa kazi kubwa wanayoifanya. Natambua kwamba hawalali wanafanya kazi lakini sisi kama wawakilishi wa wananchi tunapoona wanapita huko mikoani lakini umeme hauwashwi kwenye vijiji lazima tuseme tunapopata nafasi hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mheshimiwa Waziri umeme kwenye Kijiji cha Nyanganga wameshawasha na wananchi wanashukuru sana kwa jitihada alizozifanya. Hata hivyo, tuna tatizo kubwa katika Mkoa wa Kigoma, nguzo na vitendea kazi vingine bado havijawasili katika mkoa wetu. Sasa tunashindwa kufahamu, ni lini wakandarasi hawa wataanza kupeleka nguzo Nguruka ili vijiji vyangu vya Chagu, Kijiji cha Mganza, Kijii cha Mtegowanoti, Kijiji cha Nyangabo, Kijiji cha Nguruka, Kijiji cha Bweru, Itebula, Mganza, Kasisi, Mlyabibi, Mpeta na kuendelea, lini watapelekewa nguzo ili angalau umeme sasa uweze kuwafikia wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri anatambua kwamba jiografia ya Jimbo langu ni mbaya, wananchi wa Ukanda wa Ziwa Tanganyika kwa maana ya Kata ya Mwakizeja, kuna vijiji kama viwili havijapelekewa umeme, lakini Kata ya Ilagala. Tatizo langu mimi kama mwakilishi wao, tangu survey ile ya kwanza waliyoifanya mpaka leo hakuna kinachoendelea. Sasa ninawiwa kwenye kushika shilingi na naomba kabisa niwekwe kwenye list ya kushika shilingi ili niweze kuambiwa ni lini vifaa vitapelekwa kwenye vijiji vyangu 24 ili sasa kazi ya kupeleka umeme iweze kuanza mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri afanye ufuatiliaji wa kina kwa mfano, tunacho Kitongoji cha Muyobozi na Kijiji cha Kabeba. Tangu mwaka jana mwezi wa Saba (7) wenzao wamewashiwa umeme, wao waliwashiwa siku moja, siku ya pili wakabeba transformer wakazipeleka Kigoma Mjini. Sasa swali langu, tangu nimelia kwa Waziri kwamba Muyobozi na Kabeba wawashiwe umeme hawajawashiwa umeme, basi waende wakang’oe nguzo. Wakang’oe nguzo, wakang’oe nyaya ili wananchi waache kuonga nyaya na nguzo kwa mwaka mzima, umeme hawawashiwi, tatizo liko wapi? Nimeshalalamika sana kwa Mheshimiwa Waziri, safari hii nitashika shilingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia kwenye vijiji vyangu vya Kata ya Kalya, tulikubaliana vizuri REA awamu ya tatu kwamba Kijiji cha Ubanda, Lufubu, Kashaguru, Tambusha, Kalya na Sibwesa watapata umeme kutoka Ikola au kutoka Mwese. Nimwombe Mheshimiwa Waziri, hadi leo ninavyoongea hakuna survey yoyote iliyofanywa kwenye hivi vijiji sita, sasa wananchi wamenituma niulize, hii ndiyo bajeti ya mwisho. Bajeti hii tunalialia hapa kwa sababu bajeti inayokuja tunakwenda kwenye uchaguzi, sasa Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa kuhitimisha nataka nijue hivi vijiji sita ndani ya Kata ya Kalya vinapata lini umeme kutoka Ikola au Mwese ili tujue way forward.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa Hasna, ahsante sana kwa mchango wako.

MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na mimi kwa kupata nafasi ya kuchangia bajeti hii ya Serikali.

Kwanza nianze kwa kumpongeza kaka yangu Dkt. Mpango pamoja na Naibu Waziri pamoja na Katibu Mkuu na watendaji wote wa wizara hii. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Bajeti naona ni namna gani taarifa hii ya Mheshimiwa Waziri ilivyozingatia maoni mbalimbali ya wajumbe wa Kamati ya Bajeti. Mheshimiwa Waziri hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie hali halisi ya reli ya kati; sote tunafahamu kwamba reli ya kati ni reli ambayo inasaidia sana wafayabiashara wanaopeleka mizigo Congo, Burundi na Zambia. Lakini leo hii kuna tatizo kubwa la upungufu wa mabehewa kwenye Mpango wa Serikali wa Miaka Mitano na Mpango wa Mwaka Mmoja wameonesha kwamba wanajipanga kununua mabehewa mapya na wanajipanga kununua vichwa vya treni.

Mimi naomba tu niiishauri Serikali hebu tuharakishe haraka kununua mabehewa, kwa nini nasema hivi; juzi tu hapa mimi ni mdau katika kufanya biashara kidogo tumelipa shilingi 54,195,000 kwa ajili ya mabehewa 13 kusafirisha tani 520 kwenda Kalemi. Kwa bahati mbaya tunaambiwa kwamba mmelipa hizi pesa, lakini mabehewa mtayapata baada ya miezi mitatu au miezi sita. Sasa wafanyabiashara wanashindwa kuendelea kufanya biashara na Wakongo kwa sababu unachukua tender kwa Wakongo, unawaahidi kwamba ndani ya wiki tatu au mwezi utakuwa umewafikishia mizigo yao Kigoma ili waweze kupakia kwenye meli kupeleka Kalemi au kupeleka Burundi matokeo yake wenzetu wa TRL hawana mabehewa ya kutosha kwa ajili ya kubeba mizigo.

Kwa hiyo, mimi niliomba nijikite kwenye hili ili Mheshimiwa Waziri kwa sababu mmeonesha kwenye bajeti ya Wizara ya Miundombinu kwamba wana bajeti yao ya kununua mabehewa mapya na vichwa mimi naomba pesa ile ipelekwe ili waweze kununua mabehewa mapya, wafanyabiashara waweze kubeba mizigo kupeleka Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hili reli inakwenda na bandari. Mheshimiwa Waziri unafahamu kwamba Bandari ya Kigoma mnaendelea kidogo kidogo kuiboresha. Tunaomba kasi ile ya kuboresha iongezeke zaidi, lakini huku tukiboresha bandari nimeona katika mpango na katika bajeti ya mwaka 2019/2020 mmeonesha kwamba kuna ununuzi wa meli mpya kwa ajili ya mizigo kwenye Ziwa Tanganyika, lakini kuna ununuzi wa meli mpya kwa ajili ya abiria. Mimi niombe Mheshimiwa Waziri utusaidie meli hiyo iweze kununuliwa kwenye mwaka wa fedha ujao kama ambavyo mlivyopanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie SGR; nimeona kwenye Kamati ya Bajeti hapa ule mtandao wa ujenzi wa SGR kwa maana ya kutoka Dar es Salaam mpaka Isaka; Isaka - Mwanza halafu ndio iende Tabora - Kigoma; Kigoma - Kalema, na hatimaye Uvinza huko Songati mpaka Kigali. Mimi niiombe Serikali natambua kwa sasa hivi tumejipanga ku-concentrate na huu mtandao wa kutoka Dar es Salaam mpaka Isaka; Isaka - Mwanza lakini wakati tunakwenda Mwanza tuangalie nah ii route ya kwenda Tabora; Tabora - Kigoma tukifanya hivyo tutawezesha sasa kupokea mizigo inayokwenda Kongo lakini pia mizigo inayotoka Kongo inayoingia Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa taarifa nilizonazo Rais Mstaafu Kabila wa DRC ameshasimamia kule Kalemi bandari imekamilika, wamekamilisha na meli kubwa ya kubeba mizigo na target yao ni nini? Target yao ni kuchukua yale madini ya kolta kuyatoa Kalemi na kuyaleta Dar es Salaam na tayari wameona kwamba Mheshimiwa Rais wetu ameanzisha masoko ya madini kitu ambacho Wakongomani kimewafurahisha sana. Sasa wanajipanga kuwa wanatoa dhahabu, wanatoa yale madini ya kolta kutoka kule kuyaleta Dar es Salaam. Sasa tukuombe Mheshimiwa Waziri hivi katika huu mtandao wa SGR tuweke mkazo na kutoka Isaka - Tabora - Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hili nizungumzie kiwanja cha ndege cha Kigoma. Hivi karibuni tulimpokea Spika wa Bunge la Burundi pamoja na Wabunge walisafiri kutoka Burundi kwa magari mpaka Kigoma, wakapanda ndege pale mpaka Dar es Salaam, Dar es Salaam ndio wakapanda tena ndege kuja Dodoma, lakini wanachosikitika wao ni kwamba hakuna yaani ile airport pale ikiboreshwa wao wanaweza wakawa wanasafiri kwenda nje ya nchi kwa kutumia kiwanja kile kile ili mradi tu connection ziweze kuimarishwa vizuri. Sasa kile kiwanja cha Kigoma tulishawalipa fidia wananchi, wananchi hawadai tena fidia.

Sasa najiuliza swali kigugumizi ni nini katika kuendeleza kile kiwanja cha Kigoma? Tukiendeleze kiwanja cha Kigoma ili tuwe na route ya kwenda Kalemi tuwe sasa hivi tuna route ya kwenda Bujumbura tunataka sasa tuwe na route ya kwenda Kalemi, tuwe na route ya kwenda Lubumbashi, tufungue mipaka zaidi ya kibiashara, wafanyabiashara kutoka nchi hizi jirani waweze kuingia Kigoma wafanye biashara zao na hatimaye warudi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo sasa nizungumzie masuala ya jimboni kwangu. Tunafahamu kwamba vyanzo vingi vya Halmashauri vimechukuliwa na Serikali kuu na sasa hivi hali ya Halmashauri zetu Wakurugenzi wanashindwa kuwalipa Waheshimiwa Madiwani hata posho za vikao. Sasa nilifikiri katika hii Finance Bill labda vile vyanzo tulivyovichukua vya Halmashauri ilikuwa sasa ni wakati muafaka kuvirejesha kwenye Halmashauri zetu. Kwa nini nasema hivyo; tuone kwenye makusanyo ya majengo, kodi ya majengo tulimuuliza DG wa TRA kwamba ninyi target yenu mlikuwa ni kukusanya kiasi gani wanasema ilikuwa ni kukusanya Halmashauri zote 180; lakini mmekusanya kiasi gani? Tumekusanya kwenye Halmashauri 30 tu.

Sasa unajiuliza tuna Halmashauri 180 TRA wameweza kukusanya Halmashauri 30 peke yake; kwa nini hivi vyanzo sasa kama vimeshindikana Serikali Kuu tusivirudishe kule halmashauri ili Wakurugenzi waendelee kusimamia. Nilikuwa namuomba sana Mheshimiwa Waziri kwa sababu hali za Halmashauri zetu ni mbaya sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie miradi ya maendeleo. Tunayo miradi ya maji, imekuwa ni hadithi. Tuna miraji ya maji ambayo inashindwa kukamilika zaidi ya miaka 15 tangu awamu ya Mheshimiwa Mkapa, awamu ya Mheshimiwa Jakaya na sasa tuko awamu ya Mheshimiwa Magufuli tunayo miradi ya maji ambayo haikamiliki. Mfano peke yake mimi jimboni kwangu nina mradi mkubwa kule Rukoma na mradi mkubwa pale Kandaga...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Hasna sekunde 30 malizia sentensi muda wako umeisha.

MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru niombe tu Serikali labda tufunge macho, tujaribu kumaliza miradi yote ile ya maji iliyokuwa huko nyuma halafu ndio tuendelee na miradi mipya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya naomba kuunga mkono na nampongeza sana kaka yangu Mpango. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi, wa Mwaka 2016
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nishukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia hii Miswada miwili kwa maana ya Muswada wa mambo ya uvuvi lakini pia na Muswada wa masuala ya kilimo. Naomba nijikite kwenye huu Muswada wa Uvuvi kwa sababu kwenye Jimbo langu tunalo Ziwa Tanganyika na limekuwa maarufu sana kwa kutoa samaki anayeitwa mgebuka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kwenye hii taarifa yake aliyotoa, kwenye mambo muhimu ya Muswada huu kuna kipengele hapa kinasema kuweka utaratibu na kumbana mtafiti anaposhindwa kuwasilisha taarifa ya mwisho ya utafiti. Siku za nyuma tulikuwa na Kampuni ya Wagiriki iitwayo YOROGWE ilifanya kazi ya utafiti na ilikuwa inavua samaki kwa kutumia meli zile kubwa. Ziwa Tanganyika lina kina kirefu sana duniani lakini ninachojaribu kusema…
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kigoma wale ambao wamezungukwa na ziwa hili kwa maana ya Jimbo la Kigoma Kaskazini, Jimbo la Kigoma Kusini na Jimbo la Kigoma Mjini wanashindwa kuvua samaki walio wengi kwa sababu zana zao za uvuvi haziwafai kwenda chini zaidi. Hii Kampuni ya Wagiriki ambayo ilikuwa inatwa YOROGWE wakati inavua Kigoma wale samaki walikuwa hawaishi kwa sababu walikuwa wanatumia zana zenye hadhi ya kuvua samaki kwenye Ziwa Tanganyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema kwamba tunaweka sheria hii na na-support kwamba utafiti wa kina uweze kufanywa, lakini Wizara iwe inahakikisha hawa watu wanapofanya utafiti wawe wanatoa taarifa pia kwenye Halmashauri husika zinazozunguka hilo Ziwa Tanganyika. Kwa mfano, kwenye miaka ya 2000 tumekuwa na wenzetu hawa wa FAO ambao waliwahi kufanya utafiti na wakatoa taarifa kwamba Ziwa Tanganyika lina aina ya samaki zaidi ya 250.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tuulizane ukizungumzia Ziwa Victoria unazungumzia sato na sangara lakini sangara ametolewa Ziwa Tanganyika. Walifanya utafiti, wakamchukua sangara kutoka Ziwa Tanganyika wakampeleka Ziwa Victoria na hatimaye ndiyo wakampa jina la sangara. Sangara ni jamii ya singa na nonzi kutoka Ziwa Tanganyika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali ikilitumia vizuri Ziwa Tanganyika kupitia Wizara ya Kilimo na Mifugo tunaweza kuingiza kipato cha Taifa kwa kuvua samaki wengi walioko kwenye ziwa hili. Hata hivyo, kinachoonekana bado Wizara haijajipanga vizuri kutumia mazao haya ya uvuvi kwenye Ziwa Tanganyika ili kuiingizia kipato Serikali yetu. Kwa hiyo, tunapitisha Muswada huu mzuri lakini pia tuweke taratibu za kuwabana watafiti watakaofanya utafiti kwenye maziwa yetu haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo maana nikitaja tu samaki tunaowavua kwenye Ziwa Tanganyika kwa kutumia zana zetu hizo hizo ambazo siyo bora, tuna samaki ambaye anaitwa babukubwa, kuhe, nonzi, sangara, singa, kibonde, kavugwe, kuku maji, mibanga, jamani tuna zaidi ya samaki 30 wanavuliwa na wavuvi wa Kigoma kwa kutumia zana ambazo hazina tija. Je, Serikali ikiweka nguvu, ikawapa wavuvi zana ambazo zina tija tutavua samaki wangapi kwenye Ziwa Tanganyika? Tutaingiza shilingi ngapi katika Taifa letu? Sisi tumepakana na Zambia, Burundi na Kongo na mazao haya ya samaki na dagaa tunakwenda kuuza Kongo, Burundi, Rwanda na Zambia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nilimsikia mchangiaji mmoja kama sikosei Mheshimiwa Haonga alikuwa anazungumzia namna ambavyo dagaa wa Ziwa Viktoria wanavyopelekwa Kongo. Sasa fikiria mpaka dagaa wa Ziwa Viktoria wanaenda Kongo. Kwa hiyo, ninachojaribu kuomba hapa ndugu zangu ni kwamba tuweke akili yetu yote kwenye mazao ya uvuvi. Nimepitia taarifa ya Kamati nimeona imejikita kwenye Muswada wa Kilimo tu haijajikita kwenye Muswada wa Uvuvi. Sasa nikapata shida, hivi kilimo ndiyo kinaingiza zaidi mapato kushinda zao la uvuvi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kusema ni kwamba katika utafiti huu tusijikite tu kwenye utafiti wa kilimo tujikite pia na kwenye utafiti wa zao la uvuvi. Kwa mfano, sisi watu wa Kigoma tunao mwalo pale Mwakizega. Tumejenga mwalo mzuri na Halmashauri sasa hivi inaendelea kuumalizia japo wavuvi wameshaanza kuutumia ili angalau kupandisha hadhi mazao yao ya dagaa na samaki waweze kupata kipato zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunachoomba Serikali itupie jicho la huruma kwenye majimbo haya matatu, Jimbo la Kigoma Kusini, Kaskazini na Mjini ili kuwawezesha wavuvi wetu kwa zana zenye ubora zaidi ili waweze kuzitumia kuvua samaki wengi na kuongeza kipato cha Halmashauri zetu lakini pia kipato cha nchi maana tunawatoza ushuru. Kwa mfano, gunia moja la dagaa, wavuvi wanalipa Sh.3,000 mara wavuvi waliopo ni shilingi ngapi, ni pesa nyingi. Hizi ni own source zinazoingia kwenye Halmashauri zetu na sisi tunazielekeza kwenye miradi mbalimbali ya maendeleo ndani ya majimbo yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili nichangie pia kwenye upande wa Muswada wa Kilimo. Niunge mkono taarifa ya Kamati ya kutoa pendekezo lao la uanzishwaji wa Mfuko Maalum wa Utafiti wa Kilimo. Nimekuwa Mkuu wa Wilaya ya Tandahimba, Newala na Mtwara, Naliendele hawana tu uwezo wa kutafiti zao la korosho bali wanafanya utafiti wa mazao yote, lakini tatizo kubwa hapatengwi pesa za kutosheleza ili hizi tafiti ziweze kufanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa aweze kutuambia pendekezo hili la Kamati la kuanzishwa Mfuko Maalum wa Utafiti wa Kilimo amelichukuliaje ili kuwezesha upatikanaji wa fedha zaidi za utafiti. Kwa sababu Naliendele na taasisi zote za utafiti Tanzania zikiweza kutengewa pesa zitafanya kazi kubwa na nzuri ya kufanya utafiti wa mazao mbalimbali nchini ili wakulima wetu waweze kunufaika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia pale Kilimanjaro Hai, tunayo TACRI ambao ni watafiti la zao la kahawa. Nikiwa pale kama Mkuu wa Wilaya nilichojifunza Serikali haitengi pesa ya kutosha kuipa taasisi hii ya utafiti ya TACRI. TACRI inategemea ufadhili wa European Union, ukiwa pale unakuta unapokea Mabalozi wa European Union wanakuja kuangalia uendelezaji wa TACRI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najiuliza, hivi hawa European Union wakitoa mkono wakasema kwamba hawasaidii tena ile TACRI itaendelea? Kwa hiyo, ninachojaribu kuomba taasisi hizi za utafiti zitengewe pesa zisiwe zinatupwa au zinawekwa pembeni. Wizara inapokuja hapa kwenye bajeti ijayo iweze kuona namna ya kuwezesha taasisi zetu hizi za utafiti ili ziweze kufanya kazi vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru pale Kigoma tunao hawa TAFIRI na wanaendelea na utafiti wao wa kuonesha tuna idadi ngapi ya samaki kati ya wale 250. Hata hivyo, TAFIRI hawa wamekuwa wanafanya kazi Kigoma Mjini, tuombe basi Wizara ione namna ya kujenga hata chuo kimoja cha utafiti ndani ya Mkoa wa Kigoma hata kama ni branch ya utafiti kwenye zao la uvuvi ili vijana wetu waweze kujifunza zaidi masuala ya uvuvi, waachane na uvuvi haramu na wafanye uvuvi halali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, niseme Miswada hii miwili wa Uvuvi na wa Kilimo ni mizuri na naunga mkono hoja. Ahsante sana.