Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Peter Joseph Serukamba (6 total)

MHE. PETER J. SERUKAMBA aliuliza:-
Maji ni tatizo kubwa kwenye Jimbo la Kigoma Kaskazini:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Peter Joseph Serukamba, Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekwishaanza utatuzi wa tatizo la maji katika Jimbo la Kigoma Kaskazini kupitia miradi ya maji inayotekelezwa chini ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji. Utekelezaji wa miradi hiyo umefikia hatua mbalimbali kama ifuatavyo:-
Mradi wa Maji wa Nyarubanda, Kagongo na Nkungwe inayohudumia wananchi wapatao 13,757 imekamilika. Taratibu za kumpata Mkandarasi atakayejenga mradi wa maji wa Kalinzi zimekamilika. Fedha zikipatikana Mkataba utasainiwa ili mkandarasi aanze kazi mapema iwezekanavyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha Serikali inaendelea kutatua kero ya maji katika Jimbo la Kigoma Kaskazini, Halmashauri ya Kigoma imepanga kutekeleza miradi mbalimbali katika Awamu ya Pili ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji kuanzia mwaka wa fedha 2016/2017. Vijiji vilivyowekwa kwenye mpango huo ni Mwandiga, Kibingo, Kiganza, Kaseke, Nyamoli, Mkigo, Matendo, Pamila, Matyazo, Mkabogo, Kiziba, Kidahwe, Kigalye, Kalinzi, Kalalangabo, Mtanga, Bugamba, Nyamhoza, Kizenga, Mgaraganza, Mahembe, Samwa, Bubango, Chankele, Kagunga, Zashe, Bitale, Mwamgongo, Machazo na Mkongoro.
Ujenzi wa Soko la Kimataifa Mpaka wa Kagunga

Je, ni lini Serikali itajenga soko la Kimataifa Kagunga mpakani mwa Tanzania na Burundi?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Peter Joseph Serukamba, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mpango wa kujenga soko la kisasa la Kimataifa la Kagunga jirani na Mpaka wa nchi yetu na Burundi lenye ukubwa wa hekta 1.5. Tayari Manispaa ya Kigoma imetenga shilingi milioni 250 kwa bajeti yake ya mwaka 2015/2016 kwa ajili ya ujenzi wa soko hilo, juhudi za kumpata mzabuni wa kujenga soko hilo zinaendelea. Pamoja na jitihada hizo, mwekezaji kutoka United Nations Capital Development Fund pia ameonyesha nia ya kuwekeza kwenye miundombinu ya masoko, ameanza ujenzi na anajiandaa kwa ajili ya ujenzi wa soko hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na soko hilo, Serikali kupitia mamlaka ya EPZ, imetenga eneo la hekta 20,000 kwa ajili ya uwekezaji yakiwa ni maeneo ya viwanda, makazi, biashara pamoja na Mkoa wa Kigoma (Kigoma Special Economic Zone).Hadi sasa hekta 700 zimepimwa na wananchi 369 kati ya 360 wamelipwa fidia ya maeneo yao, jumla ya shilingi bilioni 1.03 ambayo ni sawa na asilimia 61 imetumika.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, upimaji na uandaaji wa michoro ya matumizi unaendelea na utengaji wa maeneo hayo karibu na miji utasaidia kasi ya kuleta maendeleo na ushindani kuinua uchumi wa wananchi wa Kigoma.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kutoa wito kwa Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wengine, kuhamasisha wawekezaji na wadau wa maendeleo kufanikisha ujenzi wa masoko ya mipakani kwani ujenzi wa masoko hayo unahitaji sana nyongeza na nguvu za wananchi kuongeza jitihada za Serikali.
MHE. PETER J. SERUKAMBA aliuliza:-
Mheshimiwa Rais alipokuja kwenye kampeni Jimbo la Kigoma Kaskazini aliahidi kuwalipa fidia wahanga wa Barabara ya Mwandiga – Manyovu.
Je, ni lini jambo hilo litatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Peter Joseph Serukamba, Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Mwandiga - Manyovu, yenye urefu wa kilometa 56.26 ulianza mwaka 2009 na kukamilika mwaka 2011.
Mheshimiwa Spika, wakati wa utekelezaji wa ujenzi wa barabara hii wananchi wa Mwandiga hadi Manyovu walilalamika kwa kuvunja nyumba zao wenyewe bila kulipwa fidia kwa agizo la Serikali. Mwaka 2010 Serikali iliunda tume ya kuchunguza malalamiko hayo na kugundua kuwa wananchi hao walivunja nyumba hizo kwa kuwa zilikuwa ndani ya eneo la hifadhi ya barabara kinyume na Sheria ya Barabara ya mwaka 2007 pamoja na kanuni zake, hivyo wananchi hao hawakusatahili kulipwa fidia.
MHE. PETER J. SERUKAMBA aliuliza:-
Mheshimiwa Rais alipokuja kwenye kampeni aliahidi kuanza ujenzi wa barabara ya Mwandiga – Chankele – Kagunga.
Je, ni lini ujenzi wa barabara hiyo utaanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Peter Joseph Serukamba, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ya Mwandiga – Chankele - Kagunga yenye urefu wa kilometa 55.76 ipo katika eneo la mwambao wa Ziwa Tanganyika. Tayari upembuzi yakinifu umefanyika na kubaini kuwa zinahitajika shilingi bilioni saba kuweza kujenga barabara hiyo.
Mheshimiwa Spika, kutokana na uwezo mdogo wa Halmashauri, ilikubalika kupitia Kikao cha Bodi ya Barabara cha Mkoa wa Kigoma, iweze kuhudumiwa na Wakala wa Barabara Mkoa (TANROADS). Maombi hayo yamewasilishwa kwa Waziri mwenye dhamana na ujenzi kwa ajili ya kupata kibali.
MHE. STANSLAUS S. MABULA (K.n.y MHE. PETER J. SERUKAMBA) aliuliza:-
Bei ya kahawa ni ndogo ikilinganishwa na gharama za uzalishaji.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kupandisha bei ya zao la kahawa?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wakulima kwa kuwapatia ruzuku?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Peter Joseph Serukamba, Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kaskazini, lene sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, bei ya kahawa duniani ikiwa ni pamoja na kahawa ya Tanzania hutegemea bei katika masoko mawili ya rejea duniani ambayo ni Soko la Bidhaa la New York (New York Commodities Market) kwa kahawa ya Arabica na Soko la London International Financial Futures and Options Exchange kwa kahawa ya Robusta.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwenendo wa bei katika masoko hayo huathiri moja kwa moja bei kwa nchi zote wazalishaji wa kahawa ambapo mwenendo huo pia huathiri bei katika soko la mnada wa kahawa na bei ya wakulima Tanzania. Bei ya kahawa katika masoko ya rejea pia hutokana na kiasi kilichopo na mahitaji (demand and supply) ya kahawa duniani kwa wakati husika. Aidha, kwa kuwa wanunuzi hununua kahawa kwa bei ya mwali pwani (FOB) ambayo hujumuisha bei ya mkulima na gharama, zao za ununuzi kwa hivyo bei ya kahawa haizingatii kabisa gharama za uzalishaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, zao la kahawa pia hukabiliwa na ada na tozo mbalimbali ambazo huongeza gharama za kufanya biashara na hivyo kusababisha wanunuzi wengi kwenda kununua kahawa katika nchi jirani ambako hakuna ada na tozo nyingi na hivyo kutoa bei nzuri ukilinganisha na bei za ndani. Hali hiyo husababisha wakulima kutorosha kahawa nje ya nchi ili waweze kupata bei nzuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali haiwezi kupandisha bei ya kahawa kwa kuwa bei hiyo hutokana na masoko rejea ya dunia. Hata hivyo, Serikali inatekeleza mikakati mbalimbali ya kuwaongeza kipato wakulima. Mikakati hiyo ni pamoja na kufuta ada na tozo zipatazo 17 katika sekta ya kahawa ili kumpunguzia mkulima mzigo wa malipo ambayo wanunuzi huweka kwenye gharama zao za ununuzi; kuongeza ushindani katika mnada kwa kuwaondoa wanunuzi wa kahawa vijijini ili wakanunue kahawa mnadani kwa ushindani, kuimarisha, kufufua na kuanzisha Vyama Vikuu vya Ushirika katika kila Mkoa unaolima kahawa na Vyama vya Msingi kwa maana ya AMCOS katika kila kijiji ili kukusanya kahawa ya wakulima, wanachama na kuipeleka mnadani. Aidha, AMCOS zimehamasishwa kuanzishwa viwanda vya kuchakata kahawa ili kupata kahawa bora na yenye bei nzuri na kuimarisha usimamizi kwa zao la kahawa katika ngazi na hatua zote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali huwapatia wa kahawa ruzuku kwa kupunguza bei ya miche bora ya kahawa inayozalishwa na Taasisi ya Utafiti wa Kahawa Tanzania, vilevile Mamlala za Serikali za Mitaa zinazolima kahawa nchini zimeagizwa zote kuanzisha bustani za kuzalisha miche bora kulingana na mahitaji ya wakulima wao na kuigawa bure na pia kuhakikisha inapandwa na kutunzwa. (Makofi)
MHE. PETER J. SERUKAMBA aliuliza:-
Jimbo la Kigoma Kaskazini katika Kata ya Ziwani kuna tatizo kubwa la mawasiliano ya simu hasa katika vijiji vya Kalalangobo, Rubabara, Kigalye, Mtanga, Nyantole na Kazinga. Je, ni lini wananchi watapatiwa mawasiliano hayo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Peter Joseph Serukamba, Mbunge wa Kigoma Kaskazini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote umeviainisha vijiji vya Kata ya Ziwani vikiwemo vijiji vya Kalalangobo, Kigalye, Manga, Rubabara, Nyantole na Kazinga na kuviingiza katika miradi ya kufikisha huduma ya mawasiliano vijijini kwa kadri ya upatikanaji wa fedha za utekelezaji wa miradi.