Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Richard Phillip Mbogo (18 total)

MHE. JOHN P. KADUTU (k.n.y. MHE. RICHARD P. MBOGO) aliuliza:-
Mwaka 2009 Serikali iliwapa uraia wakimbizi toka Burundi walioingia nchini mwaka 1992 na wengine waliozaliana katika makambi ya wakimbizi ya Katumba, Mushamo na Ulyankulu:-
(a) Je, ni lini Serikali itakamilisha ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kuwapa wakimbizi waliosalia?
(b) Ili kuondoa hali ya sintofahamu katika Sheria ya Wakimbizi Na. 20 inayokataza mikusanyiko zaidi ya watu watano, je, ni lini Serikali itafuta hadhi ya makambi ya wakimbizi katika maeneo ya Katumba?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, napenda kurekebisha swali hilo kwamba ni kweli mwaka 2009 Serikali iliwapa uraia wakimbizi toka Burundi walioingia nchini mwaka 1972 na siyo mwaka 1992. Pia hakuna Sheria ya Wakimbizi Na. 20 bali ipo Sheria ya Wakimbizi Na. 9 ya mwaka 1998. Vilevile maeneo aliyoyataja Mheshimiwa Mbunge ni makazi ya wakimbizi na siyo makambi ya wakimbizi na hakuna mkimbizi aliyepo kambini aliyepewa uraia.
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la kushughulikia Wakimbizi (UNHCR) ipo katika hatua za mwisho kufanya uhakiki kamili kwa wakimbizi walengwa ili kutoa uraia kwa wanaostahili, kama Mheshimiwa Rais alivyoahidi. Tunategemea hadi kufikia mwisho wa mwaka huu kazi hii itakuwa imekamilika ili taratibu za kutoa uraia kwa mujibu wa sheria ziweze kufanyika.
Mheshimiwa Spika, Kifungu cha 20 cha Sheria ya Wakimbizi Na. 9 ya mwaka 1998 kinahusu wakimbizi na hasa kililengwa kwa wakimbizi waliopo makambini katika makazi ya Katumba, Ulyankulu na Mishamo. Wengi wa wakazi wake sasa ni raia, sio wakimbizi. Kwa hiyo, kifungu hicho hakiwahusu kwa kuwa sasa wakazi wengi wa Katumba, Ulyankulu na Mishamo wameshapewa uraia. Wizara yangu kwa kushirikiana na TAMISEMI inaandaa utaratibu wa kufuta utengefu wa maeneo haya ili viwe vijiji vya kawaida kwa mujibu wa sheria.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza: -
Chaguzi za Madiwani zilifanyika katika kambi ya wakimbizi Katumba wa 2015:-
Je, ni lini Serikali itapeleka fedha ili kukamilisha chaguzi za Serikali za Vijiji na Mtaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Katumba, Vijiji ambavyo havijafanya uchaguzi wa Vviongozi wa Serikali za Mitaa kwa mwaka 2014 ni 14 na vitongoji 51. Uchaguzi ulishindwa kufanyika kwa sababu Kata hiyo ilikuwa ni kambi ya wakimbizi ambao walikuwa hawajapata uraia wa Tanzania kwa mujibu wa sheria za nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Serikali kuwapa uraia wananchi wa maeneo hayo, Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo inaendelea na maandalizi ya kufanya uchaguzi mdogo katika vijiji na vitongoji hivyo na tayari katika bajeti ijayo ya mwaka 2016/2017 zimetengwa sh. 3,300,000 ili kuwezesha zoezi hilo.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-
Licha ya kwamba chanzo cha maji yanayotumika katika Manispaa ya Mpanda kipo katika Kijiji cha Ikolongo, Kata ya Mtapenda na Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo, lakini wananchi wa maeneo haya hawapati maji:-
(a) Je, kwa nini Serikali katika bajeti ya mwaka 2016/2017 isitenge fedha ya miradi ya maji ili wananchi wa viiji jirani vya Kata za Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo ambazo ni Kapalala, Itenka, Machimboni, Sitalike, Kanoge na Katumba wapate maji?
(b) Kwa kuwa Mto Ugalla ni chanzo kizuri cha maji: Je, Serikali itaondoa lini kero ya maji katika Kata ya Ugalla na jirani ya Litapunga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Serikali katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017, imetenga shilingi milioni 757.4 kwa ajili ya miradi ya maji katika Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo. Miradi iliyopangwa kutekelezwa ni pamoja na upanuzi wa mradi wa Nduwi Station katika Kata ya Ntumba, kujenga mradi wa maji katika Kijiji cha Katisunga, kujenga mradi wa maji katika Kijiji cha Songambele, Kata ya Kapalala pamoja na uchimbaji wa visima virefu sita.
(b) Mheshimiwa Spika, kulingana na tathmini iliyofanywa na Mkoa kupitia Mamlaka ya Maji, Mkoa wa Katavi mwezi Desemba, 2015, chanzo cha Mto Ugalla kimeonekana kuwa siyo cha uhakika kutokana na kupungua kwa maji wakati wa kiangazi. Serikali ina mpango wa kutumia Ziwa Tanganyika ambacho ni chanzo cha uhakika kwa ajili ya kupeleka maji katika Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo na Mpanda.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-
Halmashauri ya Nsimbo imekuwa ikipokea wahamiaji toka mikoa mbalimbali ambao ni wakulima na wafugaji na kusababisha kukosa maeneo yenye rutuba.
Je, ni lini Serikali itaongeza maeneo ya vijiji vilivyotangazwa mwaka 1974?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vyote vilivyoanzishwa mwaka 1974 katika Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo, vinapakana na Hifadhi ya Taifa ya Katavi na Msitu wa Hifadhi wa Msaginya, Mulele Hills na Mpanda North East. Misitu hii pamoja na Mbuga ya Katavi iko chini ya usimamizi wa Wizara ya Maliasili na Utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi za Taifa zipo kwa mujibu wa Sheria kwa maslahi mapana ya Taifa zima na hairuhusiwi kuendesha shughuli za kilimo na ufugaji katika maeneo hayo yaliyohifadhiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, endapo kuna hoja ya kuongeza eneo la kijiji kwa kumega eneo la hifadhi, kijiji kinatakiwa kwanza kuanza mpango wa matumizi bora ya ardhi kwa kuainisha takwimu za msingi za idadi ya watu, idadi ya kaya, ukubwa wa eneo lililopo na mahitaji ya ardhi ya ziada.
Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vyenye mahitaji ya ardhi kutoka kwenye hifadhi vinatakiwa kujadili suala hili katika Mikutano Mikuu ya Vijiji, Kamati ya Maendeleo ya Kata, Kamati ya Ushauri ya Mkoa na hatimaye maombi hayo kuwasilishwa Wizara yenye dhamana na kuwasilishwa kwa maamuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kutoa wito kwa viongozi wa Vijiji, Wilaya na Mkoa, kuweka utaratibu wa kudhibiti wahamiaji haramu katika maeneo ya mipakani wakiwemo wafugaji wanaoingiza mifugo katika Hifadhi za Taifa.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-
Vifo vya mama na mtoto vinachangiwa na huduma hafifu ikiwemo ukosefu wa usafiri hasa gari la kubebea wagonjwa (ambulance).
Je, ni lini Serikali itatoa gari la wagonjwa kwa Jimbo la Nsimbo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo ina jumla ya vituo vya afya vitatu. Kituo cha Afya cha Katumba, Kituo cha Afya cha Kanoge na Kituo cha Afya cha Mtisi vinavyohudumiwa na gari moja la wagonjwa. Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo ina upungufu wa magari mawili. Kwa kuzingatia changamoto hiyo, Halmashauri imetenga jumla ya shilingi milioni 220 katika mwaka wa fedha 2017/2018 kwa ajili ya ununuzi wa gari la wagonjwa ili kuharakisha huduma za rufaa na kupunguza vifo vya akina mama na watoto.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-
Electronic Fiscal Device (EFD) risiti hazidumu kwa muda mrefu kwani zinafutika maandishi ndani ya muda mfupi.
Je, TRA wataridhika na maelezo ya mlipakodi bila ushahidi wa risiti?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango napenda kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo awali kulikuwa na tatizo la matumizi ya risiti za EFD bila maelekezo ya Mamlaka ya Mapato Tanzania. Hali hiyo ilisababisha baadhi ya wafanyabiashara kutumia risiti ambazo zinafutika au zinadumu kwa muda mfupi. Hata hivyo, baada ya kubaini tatizo hilo, TRA ilitoa maelekezo kwa watumiaji wote wa mashine za EFD kununua na kutumia karatasi zilizoidhinishwa na Mamlaka ambazo hudumu kwa muda mrefu, takribani miaka mitano. Pili, TRA imeidhinisha waagizaji wa karatasi zenye sifa ili kuondokana na tatizo la karatasi zisizo na kiwango.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na changamoto tunayokabiliana nayo ya baadhi ya wafanyabiashara kutumia karatasi zinazofutika au kudumu kwa muda mfupi, TRA inaweza kufuatilia na kubaini kumbukumbu za mteja kutoka kwenye server iliyopo TRA na hivyo kurahisisha uhakiki wa stakabadhi, ama iliyofutika au kupotea. Hivyo basi, endapo risiti ya mtumiaji wa mashine za EFD itafutika au kupotea, ushahidi wa muamala uliofanywa na mteja kwa kutumia mashine za EFD utapatikana kwenye server kuu iliyopo TRA.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-
Katika mpango wa matumizi bora ya ardhi kwa Mkoa wa Katavi uliofanywa na Halmashauri ya Mpanda mwaka 2004 kwa kushirikisha ngazi ya Mkoa na ngazi ya Wizara, zililipwa sehemu za Hifadhi za Misitu North East Mpanda (JB94) na Msanginia (JB215) na ramani mbalimbali kuidhinishwa ikiwemo 48870, 48893 na 40250.
Je, ni lini Serikali itabadili mipaka hiyo kwa mujibu wa Sheria ya Misitu ya 2002 (Namba 14) Kifungu cha 28?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu naomba nichukue nafasi hii kwanza kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na kuniwezesha kufika siku hii ya leo. Pili, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kuniamini na kuniteua katika nafasi hii. Tatu, nimshukuru Mheshimiwa Spika pamoja na uongozi mzima wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Wenyeviti wa Kamati nilizokuwa Mjumbe kwa malezi yao ambayo wameyatoa kwangu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Misitu wa hifadhi wa Mpanda North East na Msangimya ni misitu ya Serikali inayosimamiwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania. Msitu wa North East Mpanda umehifadhiwa kwa tangazo la Serikali Na. 296 la mwaka 1949. Aidha, Msitu wa Msangimya umehifadhiwa kwa Tangazo la Serikali Na. 447 la mwaka 1954 na inasimamiwa kwa mujibu wa Sheria ya Misitu Na. 14 ya mwaka 2002 Sura ya 323.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda ilipima maeneo ya Hifadhi ya Msitu wa Mpanda North East na Msangimya kupitia ufadhili wa Shirika la Africare chini ya mradi wa Ugalla Ecosystem ili kuanzisha maeneo ya usimamizi wa Wanyamapori (Wildlife Management Area- WMA) na makazi pamoja na kuandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi ya vijiji. Baada ya upimaji huo ramani 48870, 48893 na 40250 zilichorwa na Halmashauri husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya nia njema iliyokuwepo ya kuwapatia wananchi makazi yaliyopimwa kwa mujibu wa sheria na uanzishwaji wa maeneo ya usimamizi wa wanyamapori (WMA) na kuandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi ya kijiji, utaratibu huu haukuzingatia Sheria ya Misitu Na. 14 ya mwaka 2002 pamoja na Sheria ya Wanyamapori Na. 5 ya mwaka 2009. Kwa mujibu wa kifungu cha 31(1) cha Sheria ya Wanyamapori, WMA zote zinaanzishwa kwenye misitu iliyoko kwenye ardhi ya kijiji au ardhi ya ujumla na siyo kwenye misitu ya Hifadhi ya Serikali Kuu. Aidha, mpango wa matumizi bora ya ardhi ya kijiji inafanyika kwenye ardhi ya kijiji husika na siyo kwenye misitu iliyohifadhiwa kisheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili ardhi ya msitu wa hifadhi uweze kutumika kwa matumizi mengine, Sheria ya Misitu Na. 14 ya mwaka 2002 katika kifungu cha 29 inatoa utaratibu wa kisheria wa kufuta hadhi ya msitu wa hifadhi ambapo Waziri wa Maliasili na Utalii anaweza kufuta sehemu ya msitu au msitu wote wa hifadhi baada ya kujiridhisha kuna umuhimu ya kufanya hivyo. Mara baada ya mchakato huu kukamilika ndipo ardhi ya msitu itatumika kwa matumizi na shughuli zingine za kibinadamu mbali na uhifadhi. Aidha, Waziri wa Maliasili na Utalii atatoa maamuzi hayo baada ya kushauriana na Kamati ya Taifa ya Ushauri wa Misitu (National Forestry Advisory Committee) ambayo inatajwa katika Sheria ya Misitu Na. 14 ya mwaka 2002 katika Kifungu cha 10.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mchakato wa kupima sehemu ya misitu ya hifadhi niliyoeleza hapo juu umefanyika kinyume cha sheria na taratibu zilizopo, hadhi ya misitu hiyo ya hifadhi inaendelea kubaki kisheria kama ilivyoainishwa kwa mujibu wa matangazo ya Serikali niliyoyataja hapo juu. Aidha, Serikali itaangalia kama kunaweza kuwa na uwezekano wa maeneo hayo kutolewa kwa ajili ya matumizi mengine kwa mujibu wa sheria, lakini ikiweka kipaumbele kwanza kitatolewa kwa maslahi mapana ya Taifa na kwa kufuata ushauri utakaotolewa na Kamati ya Taifa ya Ushauri ya Misitu.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-
Zao la tumbaku lina tozo nyingi ambazo ni mzigo kwa wakulima.
(a) Je, ni lini Serikali itapunguza tozo hizo?
(b) Je, kama itapunguza, itaanza kupunguza tozo ngapi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Jimbo la Nsimbo lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua changamoto mbalimbali katika uzalishaji wa mazao ya biashara nchini ikiwemo zao la tumbaku. Changamoto hizo ni pamoja na kuwepo ada na tozo mbalimbali zinazotozwa kwa wakulima na wadau wengine wanaojishughulisha na mnyororo wa thamani wa zao hilo ambazo zimekuwa na athari katika mapato ya wakulima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2017/2018 imefuta, ada na tozo zipatazo 80 kati ya tozo na ada 139 zilizokuwa zinatozwa katika mazao ya kilimo nchini ambazo zilibainika kutokuwa na tija kwa wakulima. Kutokana na maamuzi hayo kwenye tasnia ya tumbaku, jumla ya tozo 10 zilifutwa na tozo mbili zilipunguzwa viwango na tasnia ya kahawa jumla ya tozo 17 zilifutwa na tozo moja ilipunguzwa kiwango, tasnia ya sukari jumla tozo 16 zilifutwa, tasnia ya pamba tozo mbili zilifutwa, tasnia ya korosho tozo mbili zilifutwa, tasnia ya mbegu tozo saba zilifutwa, tasnia ya mbolea tozo tatu zilifutwa na tozo moja ilipunguzwa kiwango. Aidha, tozo 20 zilikuwa zinatozwa na Vyama vya Ushirika katika ngazi mbalimbali nazo zilifutwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika orodha ya tozo ambazo zilitamkwa kufutwa katika tasnia ya tumbaku kwenye Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Kilimo ya mwaka 2017/2018 ni pamoja na mchango kwa Chama cha Ushirika cha Msingi kiasi cha USD 0.072 kwa kilo na mchango wa Chama cha Ushirika cha Mkoa kiasi cha USD 0.030 kwa kilo.
Hata hivyo, baada ya majadiliano ya wadau katika tasnia ya tumbaku, tozo hizo zilirejeshwa kutokana na umuhimu wake katika kuwezesha usimamizi unaofanywa na Vyama vya Ushirika katika tasnia ya tumbaku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mukhtadha huo, ada na tozo zilifutwa katika tasnia ya tumbaku ni pamoja na ada ya fomu ya maombi ya leseni za kununua tumbaku, ada ya leseni ya kununua tumbaku kavu, ada ya leseni ya kuuza tumbaku nje ya nchi, ada ya leseni ya kununua tumbaku mbichi kiwandani, tozo ya leseni ya kununua tumbaku mbichi kwa kila Wilaya, tozo ya Baraza la Tumbaku (Tobacco Council) na tozo ya dhamana ya Benki Kuu ya Tanzania kwa ajili ya mikopo.
Aidha, mpango wa Serikali ni kuhakikisha tozo na ada mbalimbali ambazo ni kero kwa wakulima wa tumbaku zinafutwa na kubakia zile ambazo zina mahusiano na uendelezaji wa zao husika.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-
Electronic Fiscal Device (EFD) risiti hazidumu kwa muda mrefu kwani zinafutika maandishi ndani ya muda mfupi.
Je, TRA wataridhika na maelezo ya mlipakodi bila ushahidi wa risiti?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango napenda kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo awali kulikuwa na tatizo la matumizi ya risiti za EFD bila maelekezo ya Mamlaka ya Mapato Tanzania. Hali hiyo ilisababisha baadhi ya wafanyabiashara kutumia risiti ambazo zinafutika au zinadumu kwa muda mfupi. Hata hivyo, baada ya kubaini tatizo hilo, TRA ilitoa maelekezo kwa watumiaji wote wa mashine za EFD kununua na kutumia karatasi zilizoidhinishwa na Mamlaka ambazo hudumu kwa muda mrefu, takribani miaka mitano. Pili, TRA imeidhinisha waagizaji wa karatasi zenye sifa ili kuondokana na tatizo la karatasi zisizo na kiwango.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na changamoto tunayokabiliana nayo ya baadhi ya wafanyabiashara kutumia karatasi zinazofutika au kudumu kwa muda mfupi, TRA inaweza kufuatilia na kubaini kumbukumbu za mteja kutoka kwenye server iliyopo TRA na hivyo kurahisisha uhakiki wa stakabadhi, ama iliyofutika au kupotea. Hivyo basi, endapo risiti ya mtumiaji wa mashine za EFD itafutika au kupotea, ushahidi wa muamala uliofanywa na mteja kwa kutumia mashine za EFD utapatikana kwenye server kuu iliyopo TRA.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-
Serikali imeendelea na juhudi mbalimbali za kulinda Nyara za Serikali:-
Je, vitalu vya uwindaji vinachangia kiasi gani katika upotevu wa Nyara za Serikali?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, uwindaji wa kitalii ni sehemu ya matumizi endelevu ya wanyamapori na unafanyika kwa mujibu wa Sera ya Wanyamapori ya Mwaka 2007, Sheria ya Kuhifadhi Wanyamapori, Sura 283 na Kanuni za Uwindaji wa Kitalii za Mwaka 2015 zikisomwa kwa pamoja, pamoja na marekebisho yake ya mwaka 2017. Ili uwindaji uweze kufanyika, kampuni iliyopewa kitalu huomba na kupatiwa mgao wa wanyamapori (quota) watakaowindwa katika msimu husika. Mgao wa wanyamapori huandaliwa na Kamati ya Ushauri wa Mgao wa Wanyamapori (Quota Allocation Advisory Committee).
Mheshimiwa Mwenyekiti, vigezo vinavyotumika kutoa mgao ni pamoja na; moja, idadi ya wanyamapori (population status) kulingana na sensa; pili, taarifa kutoka kwa Maafisa Wanyamapori wa maeneo yanayohusika; tatu, mafanikio katika matumizi ya mgao wa wanyamapori (offtake levels); nne, ukubwa wa nyara zinazopatikana mwaka hadi mwaka (trend of trophy size) na tano, matakwa ya Mikataba ya Kimataifa kama vile CITEs.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara imeweka udhibiti wa kutosha ili kuzuia uwezekano wa kupotea nyara wakati wa uwindaji. Udhibiti huo unaanzia kwenye kutoa vibali ambavyo ni vya kielektroniki, usimamizi porini wakati wa uwindaji ili kuhakikisha aina na idadi ya wanyamapori wanaowindwa waliotolewa kwenye kibali inazingatiwa, umilikishwaji wa nyara zilizowindwa na ukaguzi wa nyara kabla ya kusafirishwa kwenda nje ya nchi. Aidha, pale inapotokea ukiukwaji wa sheria na kanuni wahusika hufikishwa mbele ya sheria na adhabu stahiki hutolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu imeendelea kuongeza udhibiti katika usimamizi wa uwindaji wa kitalii kwa kutumia sheria na kanuni ambazo wanyamapori huwindwa kwa kuzingatia jinsi, umri na ukubwa wa nyara. Udhibiti huo umesaidia kupunguza uwezekano wa wanyamapori kupungua kutokana na kuwindwa na pia kumesaidia kupatikana kwa mapato yatokanayo na uwindaji wa kitalii. Hivyo basi, vitalu vya uwindaji husaidia katika kulinda na kuhifadhi nyara na kutoa mchango katika uchumi wa nchi, hasa kwa kuchangia fedha za kigeni, kutoa ajira kwa wananchi na kuchangia maendeleo ya jamii.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-
TEHAMA imekuwa kichocheo cha maendeleo na hivyo kurahisisha ulipaji wa gharama (bills) mbalimbali kupitia miamala kwa njia ya simu. Mathalani, muda wa maongezi, ving’amuzi, umeme, kodi na laini mbalimbali.
Je, mlipaji aweke ushahidi wa aina gani katika kumbukumbu ngumu (hard paper) ili wakaguzi wa TRA waone au TRA itaridhika kwa kumbukumbu ya muamala?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango napenda kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa matakwa ya kifungu cha 35(1)(2), cha Sheria ya Usimamizi wa kodi ya mwaka 2015, kila mlipa kodi au mtu yeyote anayetakiwa kulipa kodi ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anatakiwa kutunza kumbukumbu za miamala katika mfumo wa kumbukumbu ngumu au mfumo wa kielektroniki. Aidha, kifungu cha 35(3) kinamtaka mlipa kodi kutunza kumbukumbu zake kwa muda wa miaka mitano kuanzia tarehe ambayo muamala umefanya au kwa muda zaidi kulingana na matakwa ya sheria.
Mheshimiwa Spika, sambamba na Sheria ya Usimamizi wa Kodi kifungu cha 69(3)(b) cha Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (The Value Added Tax Act, 2014) kinamtaka mlipa kodi aliyesajiliwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania katika mfumo wa malipo ya Kodi ya Ongezeko la Thamani kuwa na risiti ya EFD au ankara ya kodi (tax invoice) wakati akiwasilisha taarifa zake za mwezi (VAT return).
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-
Novemba, 2016 Serikali ilivunja mabanio (vizibo) vya maji katika Mto Katuma, Mto Mpanda na Mto Mafunsi ambayo yalikuwa yanasaidia wakulima wa zao la mpunga na mengineyo katika Mkoa wa Katavi.
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga mabanio (vizibo)ili matumizi ya maji yawe haki kwa kila kiumbe kama sheria hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji; naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa Rasilimali za Maji Na. 11 ya mwaka 2009 kifungu namba 43 kinamtaka mtu yeyote anayetaka kuchepusha au kuchukua maji kutoka chanzo chochote cha maji ikiwemo mito, maziwa, mabwawa au maji chini ya ardhi lazima awe na kibali na awe kibali cha kutumia maji kutoka Bodi ya Maji ya Bonde husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Novemba, 2016 Serikali ilivunja miundombinu ya umwagiliaji (mabanio) iliyopo katika Mito ya Katuma, Mpanda na Mifunsi kutokana na miundombinu hiyo kujengwa bila kuwa na vibali vya kutumia maji kama sheria inavyoelekeza, hivyo kusababisha Mbuga ya Katavi na Vijiji ambavyo viko chini kukosa maji. Mwezi Agosti, 2017 Wizara kupitia Bodi ya Maji Bonde la Ziwa Rukwa kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Katavi na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mpanda iliainisha maeneo nane yanayofaa kujengwa miundombinu ya umwagiliaji katika Mito ya Katuma, Mpanda na Mafunsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka 2018/2019 Serikali ilitenga shilingi bilioni 2.750 kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu wa ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo katika Mito ya Katuma, Mpanda na Mafunsi.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-

Upatikanaji wa maji safi na salama katika Jimbo la Nsimbo ni asilimia 40 chini ya wastani wa kitaifa vijijini wa asilimia 61.1 ili kufikia wastani huo inahitajika fedha kiasi cha bilioni 15:-

Je, Serikali ipo tayari kuitengea Halmashauri ya Nsimbo angalau bilioni tatu kila mwaka wa fedha?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Jimbo la Nsimbo, kama ifuatvyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2018/2019 imeitengea Halmshauri ya Wilaya ya Nsimbo kisi cha shilingi bilioni 1.413 ikiwa ni fedha kwa ajili ya ujenzi wa miradi ya maji inayoendelea kutelezwa katika vijiji vya Sitalike, Igongwe, Itenka, Nduwi pamoja na ufungaji wa pampu za mkono katika vijiji vya Kashelami, Kapanda, Wenyeji, Imilamate, Kambuzi Halt, Ofisi ya DED - Nsimbo, Katambike, Kabuga, Kituo cha Afya Katumba, Buremo, Ikondamoyo na Ndurumo A.

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha wananchi wote wananufaika na huduma ya maji wakiwemo wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo Serikali imejiwekea lengo la kuhakikisha huduma ya maji inafikia asilimia 85 upande wa maji vijijini na asilimia 95 miji ya mikoa ifikapo 2020. Hivyo, Serikali itaendelea kutenga fedha mwaka hadi mwaka kwa ajili ya utekelezaji wa miradi maji nchi kote ili kuweza kufikia malengo hayo.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-

Mabadiliko ya Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa Sura 290 yameleta nafuu sana kwa wakulima, lakini wakati huo huo Halmashauri za Wilaya zenye wakulima wadogo zimeathirika kimapato na kusababisha kushindwa kutatua kero za wananchi kwa wakati.

(a) Je, Serikali inaweza kuangalia upya suala la utaoji ruzuku za maendeleo?

(b) Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo imeathirika kwa kiwango kikubwa: Je, Serikali ipo tayari kuipatia ruzuku ili kutoa huduma za elimu na afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, Sura ya 290 imefanyiwa marekebisho na Bunge Mwezi Juni, 2017 kwa kupunguza kiwango cha ushuru wa mazao kutoka asilimia tano hadi asilimia tatu kwa mazao ya chakula na biashara. Hata hivyo, Mamlaka za Serikali za Mitaa zimeendelea kubuni vyanzo vipya vya mapato na kuimarisha makusanyo katika vyanzo vilivyopo ili kuongeza mapato na kuboresha utaoji huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na mikakati hiyo, mapato ya ndani ya Halmashauri yameendelea kuongezeka kila mwaka. Mfano, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Halmashauri ziliidhinishiwa kukusanya shilingi bilioni 687 na zilikusanya shilingi bilioni 553.39 sawa na asilimia 81. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, Halmashauri zimeidhinishiwa kukusanya shilingi bilioni 735.58 hadi Februari, 2019 zimekusanywa shilingi bilioni 401 sawa na asilimia 55. Aidha, katika mwaka wa fedha 2019/2020, Halmashauri zimekadiria kukusanya shilingi bilioni 765.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali halisi kwa ujumla inaonyesha makusanyo ya Halmashauri yameendelea kuongezeka pamoja na kupungua kwa ushuru wa mazao kutokana na Halmashauri kubuni vyanzo mbalimbali vya mapato na vyanzo mbadala. Ofisi ya Rais, TAMISEMI itaendelea kuzisimamia Halmashauri katika ukusanyaji wa mapato ya ndani ili kuimarisha makusanyo na kupunguza utegemezi kutoka Serikali kuu.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi mwaka 2019, Serikali imepeleka kiasi cha shilingi milioni 416 kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo kwa ajili ya kugharamia Elimu Msingi Bila Malipo, shilingi milioni 250 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma 20 ya shule za sekondari na shilingi 411 kwa ajili ya ununuzi wa dawa, vitendanishi na vifaa tiba. Serikali itaendelea kuongeza utoaji wa ruzuku kwa mamlaka ya Serikali za Mitaa kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Ahsante.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-

(a) Je, ni lini Serikali italeta mbegu bora ya tumbaku kama inayolimwa katika nchi nyingine Kusini mwa Jangwa la Sahara?

(b) “Produce cess” ilishushwa kutoka asilimia tano mpaka asilimia tatu ili mkulima afaidike kwenye bei ya kuuza lakini hakuna utekelezaji kwa Makampuni ya Kununua Tumbaku na kwenye Halmashauri mapato yameshuka. Je, Serikali inaweza kupitia upya Sheria hiyo na kurudisha kama awali?

(c) Je, ni lini Serikali itakaribisha Kampuni nyingine za kununua Tumbaku ili kuongeza ushindani na kuondoa hofu kwa wakulima?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, uhitaji wa aina ya tumbaku hutofautiana kati ya mteja na mteja. Tumbaku inayozalishwa nchini kwa sasa inatokana na mbegu zinazopendwa na wanunuzi waliopo. Wizara imepokea maombi kutoka Nchi ya China ya kuuziwa aina ya tumbaku inayotokana na mbegu zinazolimwa katika Nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara. Utaratibu wa kupate mbegu za tumbaku aina za PVH 2254 na KRK 26 kutoka Malawi na aina ya MHW 86 kutoka Zambia umeanza ili mbegu hizo ziweze kuzalisha tumbaku inayokidhi soko la China kuanzia msimu wa 2020/2021.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Serikali ilipunguza ushuru wa mazao ya biashara katika mwaka wa fedha 2017/2018, kutoka asilimia tano hadi asilimia tatu ili kuongeza kipato cha wakulima. Utekelezaji wa Sheria hiyo umefanyika kwa mwaka mmoja tu wa fedha wa 2018/2019, hivyo Serikali itafanya tathmini ya utekelezaji wa sheria hiyo na kama itabainika utekelezaji wake katika tasnia ya tumbaku hauna tija kwenye mapato ya Halmashauri na kipato cha mkulima, Serikali haitasita kuchukua hatua na kupitia upya sheria hiyo.

(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kupunguza ukiritimba wa Kampuni zinazonunua Tumbaku nchini, Serikali inaendelea kuweka mazingira wezeshi ili kuzivutia kampuni nyingine zaidi na kuleta ushindani. Kufuatia jitihada hizo, Serikali imefanikiwa kupata kampuni zingine za kununua tumbaku ikiwemo Kampuni ya British-American Tobacco (BAT) ambayo imeonesha nia ya kununua tumbaku yetu moja kwa moja kutoa kwa wakulima. Taratibu za kufanikisha mpango huo zinafanyika ili Kampuni hiyo iweze kununua tumbaku ya wakulima kwa msimu wa Mwaka 2019/2020. Aidha, katika hatua nyingine, Serikali inakamilisha taratibu za kulipata soko la China kwa kutumia mbegu za tumbaku zinazozalishwa katika nchi zilizopo Kusini mwa Jangwa la Sahara.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-

Huduma za matibabu ya madaktari bingwa zipo katika kanda zote isipokuwa kanda za Magharibi na Kusini:-

Je, ni lini Serikali itapeleka huduma hizo Mkoani Katavi ili kusaidia wananchi wa Kanda ya Magharibi?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo Mbunge wa Nsimbo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Mkoa wa Katavi kuna uhitaji wa Madaktari bingwa 24 kulingana na ikama na kwa sasa kuna Madaktari Bingwa wawili. Madaktari hao ni Madaktari bingwa wa Watoto na Wanawake. Ili kukabiliana na changamoto hii, Serikali imepanua wigo wa mafunzo kwa ajili ya Madaktari bingwa. Lengo la Serikali ni kuwa na Madaktari bingwa angalau wawili wawili katika fani za magonjwa ya kina mama, watoto, magonjwa ya dharura, mifupa, usingizi na upasuaji. Wataalamu hawa watakapomaliza mafunzo watapangiwa katika Hospitali za Rufaa za Mikoa ikiwa ni pamoja na Katavi.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali ina kusudio la kujenga Hospitali ya Kanda ya Magharibi Mkoani Tabora ambayo inategemewa kuhudumia wakazi wa Mikoa ya Rukwa, Katavi, Tabora pamoja na Kigoma.
MHE. RICHARD P. MBOGO Aliuliza:-

Mabadiliko ya Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa Sura 290 yameleta nafuu sana kwa wakulima, lakini wakati huo huo Halmashauri za Wilaya zenye wakulima zenye wakulima wadogo zimeathirika kimapato na kusababisha kushindwa kutatua kero za wananchi kwa wakati:-

(a) Je, Serikali inaweza kuangalia upya suala la utoaji Ruzuku za maendeleo?

(b) Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo imeathirika kiwango kikubwa: Je, Serikali ipo tayari kuipatia ruzuku ili kutoa huduma za Elimu na Afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITAIRA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa ruhusa yako kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Richard Mbogo, naomba uniruhusu niwatakie heri vijana wetu, watoto wetu wa Darasa la Saba ambao leo na kesho wanafanya mitihani yao ya kumaliza Darasa la Saba na wanafunzi hao wapo takribani 947,221 wa kawaida na wale wenye mahitaji maalumu.

Nawaomba watu wote ambao wanahusika na zoezi hili la mitihani, wazingatie taratibu na kanuni na miongozo na kamwe wasijihusishe na udanganyifu kwa namna yoyote ile ili matokeo yawe yawe mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba sasa kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI nijibu swali la Mheshimiwa Richard Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali ilifanya mabadiliko ya Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa Sura 290 kwa kuondoa kodi ambazo zilikuwa ni kero hasa kwa wakulima wadogo. Takwimu za jumla zinaonesha makusanyo ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa yamekuwa yakiongezeka kila mwaka. Mwaka wa fedha 2016/2017 Halmashauri zilipanga kukusanya shilingi bilioni 665.4 na zikakusanya shilingi bilioni 544.8; mwaka wa fedha 2017/2018 Halmashauri zilipanga kukusanya shilingi milioni 687.3 na zikakusanya kiasi cha shilingi bilioni 553.4.

Mheshimiwa Mwenyekiti, samahani hizi zisomeke bilioni, siyo milioni. Mwaka wa fedha 2018/2019 Halmashauri zilipanga kukusanya shilingi bilioni 723.7 na zimekusanya shilingi bilioni 661.36. Hivyo, kwa tathmini ya jumla, inaonesha kuwa uamuzi wa kuondoa kodi kero haujaathiri ukusanyaji wa mapato kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye sekta ya afya katika kipindi cha Mwaka 2017/2018 na 2018/2019, Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo shilingi bilioni moja kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya vya Kamoge na Katumba na shilingi milioni 220 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba. Vilevile katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Nsimbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa sekta ya elimu, mwaka wa Fedha 2018/2019, Serikali imeipelekea Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo kiasi cha shilingi milioni 250 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya madarasa 20 ya shule za sekondari. Vilevile katika Mwaka wa Fedha 2018/2019 kupitia Programu ya EP4R Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo kiasi cha shilingi milioni 205.7 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa manne, ukamilishaji ma maboma ya madarasa saba na ujenzi wa matundu ya vyoo 12 katika shule za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kupitia EP4R, Serikali imeipatia Halmashauri ya Nsimbo kiasi cha shilingi milioni 100.6 kwa ajili ya ujenzi wa maabara na matundu sita ya vyoo shule za sekondari. Aidha, kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020, Serikali imeitengea Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo kiasi cha shilingi milioni 421 kwa ajili ya elimu msingi bila malipo.Ahsante.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-

(a) Je, kuna miongozo ya fedha mingapi inayoitaka Halmashauri kutenga fedha za ndani kwa ajili ya matumizi ya kawaida na maendeleo?

(b) Je, ni halali kuwepo miongozo zaidi ya mmoja ukizingatia kuwa sasa Halmashauri hazina ruzuku?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, usimamizi wa fedha kwenye Halmashauri unafanyika kwa kuzingatia Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, Sura 290. Kifungu cha 37 na Kifungu cha 68 vinampa mamlaka Waziri mwenye dhamana na Serikali za Mitaa kutoa miongozo ya usimamizi wa fedha katika Serikali za Mitaa.

(b) Mwongozo wa mgawanyo wa mapato ya ndani kwa ajili ya Miradi ya Maendeleo na Matumizi ya Kawaida umezingatia uwezo wa Halmashauri kukusanya mapato ambapo Halmashauri zenye mapato makubwa zinachangia asilimia 60 ya mapato yake kwa ajii ya Miradi ya Maendeleo na Halmashauri zenye mapato kidogo zinachangia asilimia 40 ya mapato yake kwa ajili ya Miradi ya Maendeleo.