Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Prof. Anna Kajumulo Tibaijuka (1 total)

MHE. MENDRAD L. KIGOLA (K.n.y. MHE. PROF. ANNA K. TIBAIJUKA) aliuliza:-
Halmashauri ya Wilaya ya Muleba in shule 39 za sekondari za kata na kati ya hizo, shule 31 hazina walimu wa vipindi muhimu na nyingine zina walimu wa ziada wasio na kazi; mfano shule 12 hazina walimu wa hesabu kabisa, shule tisa baiolojia, shule nane kemia, shule 18 walimu wa fizikia na shule 10 hazina kabisa walimu wa uraia.
(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kukabiliana na tatizo hilo na kuliondoa ili kuokoa kizazi cha vijana watakaoishi katika karne ya 21 bila kusoma masomo ya sayansi?
(b) Je, kuhusu walimu wa ziada takribani 213 wasiohitajika kwenye sekondari kwa sasa hivi, Serikali itaruhusu Halmashauri iwapange kufundisha kwenye shule za msingi ambapo kuna upungufu mkubwa kuliko kuingia gharama kuwahamisha na kuwarejesha tena wakihitajika kwa sababu shule za sekondari zinaendelea kupanuka?
(c) Je, Serikali itasaidiaje Halmashauri ya Muleba kutengeneza programu maalum ya mafunzo kwa walimu wa ziada kujifunza kufundisha masomo mengine ambayo walimu wake hawatoshi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Profesa Anna Kajumulo Tibaijuka, Mbunge wa Muleba Kusini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeanza kuwapanga walimu wa sayansi moja kwa moja katika shule badala ya Halmashauri kama ilivyokuwa hapo awali ili kuleta uwiano sawa mashuleni. Vilevile Serikali imeandaa mkakati wa kuwaajiri wahitimu wa Shahada za Sayansi ambazo sio za Ualimu baada ya kuwapa mafunzo ya muda mfupi kuhusu mbinu za ufundishaji na maadili ya ualimu. Tayari kibali kimeombwa katika Ofisi ya Rais - Utumishi kwa ajili ya utekelezaji.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inafanya tathmini ya mahitaji ya Walimu wa masomo ya sanaa kwa kila Halmashauri ili kubaini maeneo yenye ziada na yenye upungufu ili kusawazisha ikama. Mpango wa Serikali uliopo ni kuwahamisha Walimu wa ziada wa masomo ya sanaa kwenda kufundisha katika shule za msingi ndani ya Halmashauri husika. Kabla ya kuanza utekelezaji wa mabadiliko haya, Serikali itatoa waraka maalum kwenda katika Halmashauri zote.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, katika utaratibu wa mafunzo ya walimu, Halmashauri moja haiwezi kuwa na mfumo wa pekee wa wa kuandaa walimu kwa sababu ni vigumu kudhibiti ubora wa mafunzo hayo kwa walimu. Pamoja na nia nzuri, lakini ni vigumu kwa walimu hao wa ziada ambao ni wa masomo ya sanaa, mfano ni wa Kiswahili, Kiingereza au Uraia kupewa mafunzo maalum kufundisha masomo ya Hisabati, Kemia au Fizikia kwa sababu wengi hawana kabisa msingi wa uelewa wa masomo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa Serikali itaendelea kuongeza udahili wa walimu wa sayansi katika vituo vya ualimu kadiri iwezekanavyo ili kukidhi mahitaji. Mpango wa muda mfupi ni kuwatumia wahitimu wa shahada za masomo ya sayansi kwa kuwapatia mafunzo ya muda mfupi kama ilivyoelezwa katika sehemu (a) ya jibu langu. (Makofi)