Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Joseph Anania Tadayo (38 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia kuwa sehemu ya Bunge lako hili la Kumi na Mbili kwa mara ya kwanza.

Mheshimiwa Spika, la pili, nikishukuru sana chama changu Cha Mapinduzi chini ya Mwenyekiti wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuniamini niweze kupeperusha bendera ya Chama Cha Mapinduzi katika uchaguzi uliopita. Niwashukuru sana wananchi wa Mwanga kwa ushindi mkubwa walionipa wa kura za kishindo.

Mheshimiwa Spika, namwomba sana Mwenyezi Mungu anijaalie mimi lakini atujalize sisi sote tuweze kuwatumikia wananchi ipasavyo kwa kuwa utendaji wa Serikali hii ya Awamu ya Tano kwa kipindi cha miaka mitano ya kwanza pamoja na ushindi huu wa kishindo umeamsha shauku kubwa sana ya wananchi na matarajio makubwa ambayo wanayo. Kwa hiyo Mungu atujaalie tuweze kuyatimiza.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja hii ya hotuba ya Mheshimiwa Rais na sababu kubwa ni kwamba hotuba hii ni mwendelezo wa hotuba ya 2015 ambayo ilitekelezwa ikatutoa na kutupeleka kwenye uchumi wa kati. Ni dhahiri kwamba tukitekeleza hotuba hii mafanikio yatakayopatikana ni makubwa mno na yatatupeleka mbele sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeitazama hotuba hii nikaona pamoja na mambo mengine lakini kwakweli inatusababishia kwenye kushusha chini yale mafanikio makubwa ambayo yalipatikana kwenye miradi mikubwa ya kitaifa yaende yawaguse wananchi na kugusa uchumi wa mtu mmoja mmoja, jambo ambalo ndilo hasa wananchi wanalolitamani na kulitarajia. Naipongeza sana Serikali kwa sababu imeshaanza kutekeleza. Kwenye Jimbo langu la Mwanga tulikuwa na tatizo sugu la maji ambalo matumaini ya kuliondoa yalikuwa yanafifishwa na utendaji ambao ulikuwa hauridhishi wa mkandarasi ambaye kimsingi alikimbia site kwenye ule mradi mkubwa wa maji. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Maji kwa maana alisikia kilio chetu akachukua hatua za haraka za kuweza kusaidia na ule mradi sasahivi unaendelea vizuri.

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa Serikali ni kwamba iwajali wale wafanyakazi waliokuwa chini ya mradi ule kwa sababu baada ya mkandarasi yule kuususa au ku- repudiateule mkataba na kuondoka wako wafanyakazi ambao stahiki zao hazijalipwa. Naamini kabisa kwamba kwa sababu mkandarasi amekimbia basi endapo kuna chochote anachodai Serikali inayo mamlaka ya kumkata na kuwalipa wale wafanyakazi nahata kama hakuna anachodai bado Serikali inaweza ikawalipa wafanyakazi pamoja na watu wengine waliokuwa wana mikataba na mkandarasi yule na ziko taratibu za kisheria za Serikali ku-recover fedha hizo.

Mheshimiwa Spika, naomba sana kwamba kwa kasi hiyo hiyo ambayo imeonekana kwenye miradi hii, basi miradi mingine ambayo iliahidiwa wakati wa kampeni ambayo wananchi wa Mwanga wameiomba sana itekelezwe. Kwa mfano, liko suala la mradi wa hospitali ya wilaya ambayo Mheshimiwa Rais alituahidi, kiwanja kipo tayari hekari 54, kwa hiyo tunaiomba Wizara husika basi iweze kulitekeleza jambo hilo kwa sababu litakidhi kiu na matamanio makubwa sana ya wananchi wa Mwanga. Pili, iko miradi ya umaliziaji wa vituo vya afya hasa Kituo cha Afya cha Kigonigoni ambacho kwa kweli kiko kwenye mkwamo. Tunaomba Wizara husika ilitazame suala hili.

Mheshimiwa Spika, tunashukuru Wizara ya Ujenzi kwa niaba ya Serikali kwamba kasi ya ujenzi wa barabara katika Jimbo la Mwanga inaendelea vizuri lakini bado ziko barabara, iko barabara ya Lembeni – Kilomeni mpaka Lomwe kilometa 31 ambayo tayari iko chini ya TANROADS tunaomba sasa barabara hiyo nayo itazamwe. Iko barabara ya Kisangara – Ngujini – Shingatini kilometa 25.9 na barabara ya Mgagao – Pangaro – Toroha kilometa 35 ambazo katika ngazi ya road board na RCC zimeshaombewa kuingia TANROADS. Tunamwomba Mheshimiwa Waziri husika basi atusaidie barabara hizi ziingie TANROADS ili pia ziweze kupata matengenezo kama barabara zingine.

Mheshimiwa Spika, ukienda ukurasa wa 15 wa hotuba ya Mheshimiwa Rais amezungumzia mkazo juu ya uwekezaji katika sekta ya nyama. Jimbo la Mwanga ni wadau wakubwa pia wa sekta hii ya nyama kwa sababu tunayo mifugo mingi na pia eneo letu location yetu iko mahali pazuri kwa ajili ya viwanda vya nyama kwa sababu kuna Bandari ya Tanga iko karibu, kuna Uwanja wa Ndege wa KIA na pia tuko mpakani. Nafahamu kabisa kwamba nyama ya Tanzania hasa nyama ya mbuzi ina soko kubwa sana middle east huko na nafahamu kabisa kwamba ziko nchi za jirani ambazo huwa zinachukua mbuzi wetu na kuwachinjia kwao na kutoa certificate of origin wale mbuzi waonekane wanatoka kwao, lakini ukweli wa mambo wale mbuzi wanatoka Tanzania na wanapata soko zuri nje kwa sababu ya ladha yake. Kwa hiyo, tunaomba Waziri anayehusika kutukumbuka katika uwekezaji kwenye sekta hii ya nyama hasa katika eneo la Kata ya Mgagao ambapo tayari kuna mnada mkubwa unaovuta watu kutoka hata nchi za jirani.

Mheshimiwa Spika, pamoja na ombi hili, ningependa pia niseme kwamba wafugaji katika Jimbo langu kwa sababu wako wanapakana na Mbuga ya Mkomazi wanakabiliwa na changamoto zinazokabili wafugaji wengi wanaopakana na maeneo ya hifadhi. Ni vizuri Serikali ikahakikisha kwamba mipaka kati ya maeneo ya wafugaji na hizi mbuga inaeleweka na wafugaji wapewe elimu inayotosheleza na kwa kweli ni vizuri wakaongezewa maeneo ya kulisha mifugo yao. Ziko faini ambazo wanatozwa pale ambapo mifugo yao imekosea ikaingia kwenye maeneo ya hifadhi. Zile faini ni kubwa mno na kwa kweli zinakuwa ni kama zinawakomoa hawa wafugaji. Wafugaji wanaishi maisha ya mashaka sana katika mipaka na hifadhi ikiwa ni pamoja na wafugaji wa Jimbo langu la Mwanga.

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru Wizara ya Maliasili na Utalii kwa niaba ya Serikali kwa jinsi ambavyo imeweza kudhibiti suala la…

Mheshimiwa Spika, nasikia kengele imelia. Nakushukuru kwa nafasi hii.

SPIKA: Hapana ni kengele ya kwanza.

MHE. JOSEPH A. TADAYO:Ni kengele ya kwanza, ahsante.

Mheshimiwa Spika, basi kwa haraka nizungumze tu kwamba suala la kudhibiti uwindaji haramu limefanikiwa katika kipindi cha miaka mitano. Hii imesaidia wanyamapori kuongezeka, lakini baraka hii ya wanyamapori kwa baadhi ya maeneo imesumbua sana.

Mheshimiwa Spika, tunalo tatizo kubwa sana la tembo ambalo limefanya maeneo ya karibu kata tano za jimbo langu yawe magumu sana au yasifae kabisa kwa masuala ya kilimo. Nilimsikia Mheshimiwa Waziri Mkuu akizungumzia juu ya kuweka kambi za hawa Askari wa Wanyamapori katika maeneo ya changamoto kama hizo. Naomba hilo liharakishwe kwa sababu ziko kata tano za jimbo langu ambazo kwa sasa hivi maisha ni magumu na wako watu kadhaa ambao wameshapoteza maisha kwa ajili ya wanyama hawa tembo.

Mheshimiwa Spika, naomba kurudia kwamba naunga mkono hoja kwa dhati kabisa na tuko pamoja katika kutekeleza haya yaliyomo humuna kuisukuma mbele nchi yetu kwenda kwenye uchumi wa kati wa juu sasa. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii ya kuwa mchangiaji wa kwanza kwa mchana huu. Nitachangia kwenye taarifa ya Kamati ya LAAC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naishukuru kwanza Serikali yetu chini ya Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo imeendelea kutuongoza vizuri na kuwapelekea wananchi wetu huduma mbalimbali ikiwa ni za kiuchumi, za kijamii na kadhalika. Hivi ninavyozungumza, jimboni kwangu tulikuwa tunakabiliwa sana na tatizo la chakula, lakini leo hii kuna chakula cha bei nafuu ambacho kinashushwa kupitia NFRA. Naishukuru Serikali, na kipekee namshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, nilimlilia sana na hata kuomba kuongezewa kwa sababu ya hali ilivyo. Kwa hiyo, Serikali inafanya kazi nzuri kiuchumi, kijamii na pia kuwahudumia wananchi pale panapokuwa na majanga.

Mheshimiwa mwenyekiti, shughuli zote hizi, wasimamizi wakuu ni Mamlaka za Serikali za Mitaa ambazo nazizungumzia leo kwenye taarifa hii ya LAAC. Sote ni mashahidi kwamba miradi mingi inatekelezwa na mamlaka hizi. Nikitoa tu mfano kwenye Jimbo langu la Mwanga, Halmashauri ya Mwanga inasimamia vizuri ujenzi wa Hospitali ya Wilaya, kazi inakwenda vizuri; Halmashauri imesimamia vizuri ujenzi wa Vituo vya Afya, na sasa wanamalizia Kitua cha Afya cha tatu cha kimkakati, shule na kadhalika. Kwa hiyo, kwa kweli wanafanya kazi nzuri, nawapongeza Halmashauri yangu ya Mwanga, Viongozi wote pamoja na Baraza la Madiwani kwa kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi hizi wanazoendelea kuzifanya sasa, ili waendelee kuzimudu vizuri, yapo mambo ambayo Serikali pia inahitaji kuendelea kuyafanya kwenye Halmashauri zetu. La kwanza hasa ni kuwajengea uwezo kwenye eneo la Bajeti. Halmashauri yangu ya Mwanga kwa hesabu hizi tulizozizungumzia za mwaka 2021, ilipokea 33% tu ya bajeti iliyotengwa. Sasa hili ni tatizo kubwa sana kutegemea utekelezaji wa miradi kwa asilimia kubwa kwa kiwango cha bajeti ni tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ipo changamoto pia ya watumishi. Nikitolea mfano hapo hapo kwenye Malmashauri yangu ya Mwanga, mahitaji ya jumla ya watumishi ni 3,117 lakini halisi tulionao ni 1,861, kuna upungufu wa 1,256, upungufu huu ni mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukija kwenye sekta mbili nyeti sensitive; Afya mahitaji ni watumishi 786, lakini halisi ni 336 tu, kuna upungufu wa 400. Ukija kwenye elimu; elimu msingi mahitaji ni 1,274, lakini actual tulionao ni 674, na upungufu ni 450. Ukija kwenye elimu ya sekondari, mahitaji ni 683, halisi ni 583, kwa hiyo kuna upungufu wa
100. Kwa hiyo, pamoja na yote hayo tunayozungumza, lakini ni vema tukawajengea uwezo wa kibajeti, pia suala la watumishi na kuwajengea uwezo katika mifumo ambayo inafanya kazi kule, hasa mifumo hii ya kielektroniki ambapo imeonekana wazi kwamba ziko halmashauri nyingi ambazo zina upungufu wa watu wenye uwezo wa ku-manage mifumo hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kutupitisha juzi kwenye mfumo huu wa TAUSI, sisi tumeuelewa kidogo, lakini tungependa kuuelewa zaidi. Sasa kama wenzetu kule hawatajengewa uwezo wa kutosha ambao ndio watumiaji wakuu wa mfumo huu, kutakuwa kuna tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo linahitaji kujengewa uwezo ni juu masuala ya mikataba na manunuzi. Sasa pamoja na mafanikio haya na haya yote ambayo nimeomba kwamba wawezeshwe, bado katika mchakato wa kazi hii tuliyoifanya kwenye Kamati, yako mambo ambayo bado wangeweza kuyatimiza lakini hawajayatimiza, nami nitazungumzia maeneo kama manne tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza, zipo kesi nyingi sana Mahakamani zinazoendelea na zilizokwisha. Kuna ambazo halmashauri zetu zinashtakiwa na kuna ambazo halmashauri zetu zinashtaki. Nikizungumzia zile ambazo tunashtakiwa, ziko ambazo nyingi tumeshindwa, lakini tukumbuke kwamba halmashauri haipelekwi Mahakamani kabla haijapewa notice ya siku 90.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wito wangu kwa halmashauri ni kwamba kwa kesi zile ambazo wanaona kabisa kwamba hapa mtu ali-supply kitu chake, kuna delivery note, kuna invoice na kila kitu, wanapopewa ile notice ya siku 90 watumie huo muda ku-settle hizi kesi kuliko kuacha ziende Mahakamani tushindwe halafu tuingie gharama kubwa ya kuja kulipa riba na gharama na kadhalika. Pale ambapo tumeshindwa, na kuna sababu za kukata rufaa, ni vizuri rufaa ikakatwa ndani ya muda ili tusiendelee kupoteza muda halafu tukaingia hasara kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko settlement ambazo zimefanyika nje ya Mahakama, ni vizuri halmashauri zikafuata utaratibu wa kusajili zile settlement Mahakamani ili tusije tukaingia shida wakati wa utekelezaji wa hukumu tukashindwa kupata kile ambacho tunatakiwa kupata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni masuala ya mikataba. Halmashauri zetu zinaingia kwenye mikataba mingi sana, ipo mingine mizuri na mingine mibovu; lakini upo udhaifu ambao ningependa kuuzungumzia. Udhaifu wa kwanza ni kutokufuata mikataba inavyotaka. Tumekutana na maeneo mengi sana ambapo mkataba wa ujenzi unasema kabisa kwamba kabla mkandarasi hajalipwa yale malipo ya awali (advance payment) lazima alete advance payment guarantee, lakini yapo maeneo ambako mkandarasi amelipwa bila advance payment guarantee, amefika mahali sasa ameshindwa, tunashindwa kupata zile fedha na hao wenzetu wakiulizwa huko, hawana maelezo kwamba kwa nini hamkuchukua advance payment guarantee?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sidhani kama Wanasheria wetu kule kwenye halmashauri au Maafisa Mipango au Wakurugenzi wanashindwa kusoma mikataba kwa mambo mepesi kama hayo. Kwa hiyo, hili ni eneo ambalo wanatakiwa kulikazia kuhakikisha kwamba wanafuata mikataba inavyosema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna baadhi mikataba ambayo kwa kweli ni dhaifu. Yapo matukio ambayo tumekuta halmashauri tatu zimepewa dhamana moja kwa ajili ya mradi fulani, yaani mkataba unataka kwamba kabla yule mzabuni hajapewa ile tenda, basi alete dhamana. Sasa mtu anakuja ameshinda tender kwenye Halmashauri ‘A’ analeta hati, anaweka pale, labda inapigwa copy hapo, kinyume kabisa na utaratibu, anaondoka nayo, anaenda kuchukua tender ya Halmashauri ‘B’ na Halmashauri ‘C’, sasa amefika mahali ame-default kote, wanashindwa ku-recover kwa sababu hati ni ile ile moja, kila mtu anaing’ang’ania na licha ya hivyo, utakuta thamani yake ni ndogo zaidi. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika eneo kama hili, suala la kuchukua dhamana ni suala ambalo linafanyika na mabenki au na makampuni ya insurance, ambao wakishachukua ile dhamana, wao wanaisajili ile dhamana, halafu wanatoa guarantee kwa Halmashauri ili iendelee kumpa kazi yule mzabuni ambaye amepata. Wao wana uwezo wa kuchukua hata dhamana moja kwa halmashauri tatu kwa sababu wanazitengeneza kwa uratatibu wa Pari-Passu ambao unasajiliwa, na pale kunakuwa na default, kila mtu pale anapata haki yake, kwa sababu wanaangalia thamani ya ile dhamana, thamani ya mikataba ambayo inatakiwa kutoa dhamana ile, wanaitoa kwa utaratibu wa sheria na kunakuwa hakuna matatizo. Ila halmashauri zinapochukua kienyeji, ndiyo matokeo yake unakuta hati moja imedhamini halmashauri tatu tofauti na default inatokea, wote wanashindwa ku-recover. Tumelikuta hili sana kwenye halmashauri, tunaomba lizingatiwe kwa nguvu sana, lirekebishwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala la kukabiliana na vitendo vya ubadhirifu, wizi, kughushi, matumizi mabaya ya madaraka na kadhalika. Hivi vitendo vinajitokeza kwa wingi kwenye halmashauri zetu, lakini imekuwa kama dini sasa kwamba likitokea tatizo, TAKUKURU; mtu anadaiwa deni, peleka TAKUKURU; mtu amekimbia na hela za POS, amekusanya amekimbia nazo, peleka TAKUKURU; Mkandarasi hajamaliza ujenzi wake, peleka TAKUKURU. Sasa tunawajazia TAKUKURU mzigo wa mambo ambayo hata uwezo wao siyo mkubwa kiasi hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi sote Waheshimiwa Wabunge, tuangalie kwenye majimbo yetu tuone Ofisi za TAKUKURU zina wafanyakazi wangapi; zina magari mangapi; zina resources kiasi gani za kukabiliana na haya mambo? Mengine ni mambo ya wizi yanayotakiwa yapelekwe Polisi yashughulikiwe na mambo mengine ni ya utakatishaji fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kuna halmashauri ambayo fedha za TANESCO za kwenda kufidia watu ambao zile waya za high tension zimepita kwake, zimekuwa diverted zikapelekwa kwenye vijiji, kutoka kule zikapigwa kwenye account za watu binafsi wakagawana, lakini mwisho wa siku unaambiwa Watendaji wa Vijiji wamepelekwa TAKUKURU, lakini wale wakubwa, huyu kahamishiwa huku na huyu kahamishiwa huku. Tunaipa mzigo TAKUKURU bure, tutailaumu wakati ambapo kwa kweli haya mambo wakati mwingine hayako ndani ya mamlaka yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachosisitiza ni kwamba tusibebeshe TAKUKURU kila mzigo. Haya mambo yaende kwenye kila taasisi kwenye vyombo vyetu vya ulinzi na usalama ambavyo vina mamlaka ya kisheria na uwezo wa kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ambalo nimeliona lina-shout, yaani linaonekana kila mara, ni udhaifu unaotokana na matumizi ya force account hasa kwenye miradi ya ujenzi. Utaratibu wa ujenzi uko wazi sana, kwamba mradi wa ujenzi unaanza na msanifu (architect) anachora, halafu unakwenda kwa mkadiriaji wa ujenzi (quantity surveyor) anakadiria kwamba gharama ni kiasi gani, halafu kunakuwa na yule mjenzi; na mjenzi kuna contractor yule aneyejenga na kuna structural engineer; na kila mmoja hapa ana majukumu yake kisheria na yote ndiyo yanayopelekea kwenye kupata value for money.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo utaratibu sasa ambao tunaukuta kule, unaenda unakuta mchoraji, yaani msanifu, Tadayo; mjenzi, Tadayo; sijui consultant ni huyo huyo. Kwa hiyo, hata zile certificate ni yeye mwenyewe anangalia, anajikadiria, anasema hapa nilipwe kiasi fulani. Tukiendelea hivi, hatutapata value for money. Tutapata product ambayo ni dhaifu na tusije tukalaumu sana hawa wakurugenzi au wale watu wanaosimamia ambao wengine ni walimu, lakini hao watu walioweka utaratibu kwamba miradi ya ujenzi iende na wataalamu wa fani mbalimbali walikuwa na maana kabisa kwamba bila hivyo hatuwezi kupata value for money. Sasa hiki ndicho kinachoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukikuta namna hiyo, utakapoenda kusoma lile bango la ujenzi, utakuta hata building permit hakuna, kwa sababu huwezi kupata building permit kama huja-involve hizi taaluma zote ambazo nimezitaja hapa. Kwa hiyo, hili jambo nadhani tunahitaji kuwa serious. Kama hatuna hao wataalam, tujaribu kutumia hata wataalam kutoka maeneo mengine ili tu kuhakikisha kwamba tunapata value for money. Hela inayokwenda kwenye halmashauri zetu kwa kweli ni kubwa, ni lazima tuitendee haki kwa kuhakikisha kwamba kazi inayifanyika inakidhi viwango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, siyo mwisho kwa umuhimu, mimi binafsi katika mchakato wa kazi yetu ya kamati, nawiwa kabisa kuishukuru sana Ofisi ya CAG kwa kazi ambayo wamefanya. Ofisi ya CAG imekuwa mwalimu, imekuwa mlezi na imekuwa na umuhimu mkubwa sana katika hizi halmashauri zetu. Watakaofuata ushauri wao, watapona, lakini ambao hawataufuata watatuletea matatizo na hatutakubali kuendelea kuwa na matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, naunga mkono hoja ya Kamati kama ilivyoletwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi hii ya kuchangia Mpango huu. Nianze kwanza kuipongeza Serikali yetu chini ya Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa ajili ya kutuletea Mpango huu mzuri. Naipongeza pia Wizara kwa kazi nzuri ambayo wamefanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku moja nilikuwa nasoma journal moja ambayo imeandikwa na Royal Irish Academy ikizungumzia juu ya vyama vikongwe kubakia madarakani. Walifanya uchambuzi mzuri sana, walipofika kwenye CCM wakaeleza kwamba CCM ipo madarakani na ina uwezo wa kuendelea kuwa madarakani kwa sababu baada ya uchaguzi huwa wana-stick kwenye kutekeleza Ilani, hawafanyi manipulations na kufanya mambo mengine mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipokuwa nasoma Mpango huu, kikubwa nilichokuwa najaribu kukitazama ni hicho kwamba umeendana vipi na ilani yetu? Mimi nimeridhika kabisa kwamba Mpango ulioletwa uko sambamba na Ilani na kwa hiyo, kama ilivyo kawaida kwamba kwenye Mfumo wa Vyama Vingi, chama kinachoshinda kwenye uchaguzi Ilani yake inageuka kuwa sera, basi tuungane kwa pamoja tutekeleze Mpango huu, tuutungie sheria, bajeti ikija tupitishe mafungu tukatekeleze kwa pamoja na kwa umoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri tu mambo machache. Suala la kwanza ni elimu. Endapo kweli tutataka kama ambavyo tunataka kwamba vijana wetu washiriki katika uchumi wa viwanda na waweze kufaidi matunda ya nchi kufikia katika uchumi wa kati, basi suala la VETA ni lazima tulitilie mkazo sana kama ambavyo imezungumzwa kwenye Mpango. Vipo Vyuo vya VETA ambavyo vilianzishwa na wananchi kwa kushirikiana na marafiki na wafadhili mbalimbali; kwenye Jimbo langu viko viwili; kuna kimoja kiko Tarafa ya Usangi na kingine kiko Tarafa ya Ugweno, ni muhimu hivi vikafufuliwa viweze kufanya kazi kwa sababu huduma yake bado inahitajika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunahitaji Vyuo vya VETA katika kila wilaya ambavyo vitaendena na uchumi wa eneo husika. Kwa mfano, Kanda ya Kaskazini tuko kwenye utalii na madini; basi Vyuo vyetu vya VETA viendane na kutengeneza vijana watakaoshiriki kwenye uchumi huo. Halikadhalika, Kanda ya Ziwa kama kuna uvuvi na madini, basi twende hivyo hivyo ili tuhakikishe kweli vyuo vyetu vinawafaidisha vijana wa maeneo yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunahitaji kuendelea kutilia mkazo elimu ya juu. Dhana kwamba kwa sasa hivi elimu ya juu imeanza kuwa irrelevant, hiyo mimi sikubaliani nayo kabisa, kwa sababu mbili. Kwanza, huwezi kupigana vita ukawa na Askari wa chini peke yao bila Majenerali. Halikadhalika, liko suala kwamba dunia imekuwa kijiji, tunahitaji ku-export hata grains. Kama tunavyopeleka wachezaji akina Mbwana Samatta wakacheze nje huko, pia tunahitaji wasomi wetu waende wakafanye kazi za kibingwa huko nje. Wako wengi mpaka sasa hivi ambao wanafanya kazi hiyo, hata waliotoka kwenye Jimbo langu, lakini tunahitaji succession plan kwamba hawa wanapostaafu, wapatikane wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mweyekiti, kwa hiyo, tutilie mkazo pia elimu ya juu, kwenye Jimbo langu tuna ardhi kubwa sana, kwa hiyo, ninaalika kabisa Serikali ije kuwekeza hata kwenye vyuo vikuu. Tuna ardhi ya kutosha, tufanye kazi hiyo, pamoja na Vyuo vya VETA lakini pia tuendelee kutengeneza akili kubwa kwa ajili ya kuingia kwenye Soko la Dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotakiwa ni kwamba wataalam wetu wa elimu watutengenezee mitaala ambayo itawafanya wahitimu wasiabudu vyeti. Kuna nchi jirani tu hapa, kuna kijana ame-graduate International Relations and Diplomacy lakini akaenda kuanzisha car wash. Sasa yeye kwa sababu amefikia level hiyo, anaenda kwa Mabalozi na Mashirika ya Kimataifa, anasaini mikataba ya kuwaoshea magari, analipwa dola. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kijana mwingine atakuja akuambie naomba mtaji wa kuanzisha car wash shilingi milioni tano, sijui nitanunua hoover na hiki na hiki; akishaanzisha car wash anakaa hapo anasubiri wateja wamfuate, yeye anaongea habari ya Arsenal na nini akisubiri wateja waje, badala ya kwenda kuwagongea mlango. Bora hata angezungumza Simba na Yanga maana ni za kwetu. Kwa upande wa elimu napenda nisema hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa kilimo, naungana na wote ambao wamesema kabisa kwamba kilimo ni moja ya vitu ambavyo vitatutoa kiuchumi, lakini lazima twende kwenye kilimo cha umwagiliaji. Nchi yetu ina vyanzo vingi sana vya umwagiliaji kiasi ambacho hata suala la greenhouse linaweza likaja kama second option.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu kwa sababu kengele imelia, ipo miradi kwa mfano kwenye Jimbo langu, naishukuru Serikali kwamba…

(Hapa kengele ya pili ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi hii ya kufunga dimba la uchangiaji jioni hii. Awali ya yote kama ambavyo wachangiaji wenzangu waliotangulia walivyosema mimi kwa kweli naishukuru sana Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kazi nzuri na kubwa wanayoifanya ya kumsaidia Mheshimiwa Rais katika utekelezaji wa majukumu haya ambayo tumemtwisha ya kuiongoza nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi yote hii inayotekelezwa pamoja na kazi nyingine ambazo Mheshimiwa Rais anatuongoza vizuri, uratibu wake unafanywa na Ofisi ya Waziri Mkuu, kwa hiyo tuna kila sababu ya kumpongeza na hata kwenye taarifa yake tumeona jinsi ambavyo miradi hii ya SGR, Bwawa la Mwalimu Nyerere, ATCL, Bomba la Mafuta, madaraja makubwa na kadhalika yanavyokwenda ni chini ya uratibu wake, anaziratibu hizi Wizara anazosimamia, kwa hiyo lazima tumpongeze kwa kazi nzuri na pia tumemuona akitembea huko na huko akikerwa na kutoa maelekezo mbalimbali juu ya miradi inayosinziasinzia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa miradi hii unachangia pia katika kuongeza mzunguko wa fedha katika nchi yetu, ndiyo maana kuna umuhimu wa kuhakikisha kwamba miradi hii inatekelezwa mpaka ifikie mwisho ndiyo kazi kubwa iliyoko mbele sasa hivi ya kuhakikisha kwamba miradi hii inakamilishwa. Pamoja na kukamilishwa vilevile tuwe mstari wa mbele katika kusimamia haya makandokando yanayojitokeza kama haya yanayotokea kwenye ripoti ya CAG yanayotusumbua sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata kama basi kweli muda wa kikanuni haujafika wa kujadili lakini nadhani wakati mwingine tunaiogopa hii taarifa kwa kudhani kwamba labda taarifa ya CAG ni kitu hasi, tuichukulie positively, ni kitu chanya kwamba angalau sasa tuna mifumo ambayo inaweza ikatuambia nini kimetokea, sasa unapotuambia nini kimetokea na kinajadiliwa mitaani hatuwezi kufumba midomo kabisa. Lazima tufike mahali tutaje na zipo namna nyingi za ku-justify mjadala huu katika kipindi hiki hatuwezi kukaa jambo linajadiliwa na wananchi huko sisi tukakaa hapo kimya kana kwamba siyo sehemu ya nchi hii, hilo nadhani tuwekane huru kuligusia wakati tunachangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee kuhusu Jimbo langu la Mwanga. Wananchi wa Mwanga wanaishukuru sana Serikali ya CCM chini ya Mama Samia Suluhu Hassan, miradi mingi sana imetekelezwa kuanzia miradi ile ambayo tulikubaliana kama Mwanga kwamba ni miradi ya kimkakati, kama ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ambao unakwenda vizuri kabisa kwa kasi, ujenzi wa barabara bypass kilometa 13.9 tutakayoita Msuya, ujenzii wa chuo cha VETA, ujenzi wa jengo la utawala la Halmashauri, pamoja na ahadi ya Mheshimiwa Rais ya stendi ya kisasa ambayo hii kwa kweli haijafikia mahali pa kuridhisha na ndiyo maana nahitaji hapa kuwakumbusha wanaohusika kwamba Mheshimiwa Rais aliwaahidi wananchi wa Mwanga kwamba watapata stendi ya kisasa na utekelezaji ulianza katika maana ya kutakiwa kupeleka andiko na michoro, yote haya yalifanyika lakini kuna mahali pamekwama ambapo ningeomba sana kwamba pakwamuliwe ili mradi ule utekelezwe.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, specifically kwa mradi unaowagusa wananchi kama mradi wa hospitali ya Wilaya tunaomba sasa tupatiwe zile fedha zilizobakia Shilingi Bilioni 1.3 na Watendaji wangu, Wataalam wangu wa Halmashauri na Baraza langu la Madiwani ambao kila siku namuombea Mungu awabariki na kuwalinda, wameniahidi kabisa kwamba wakipata fedha hizo za mwisho bilioni 1.3 ukifika mwisho wa mwaka huu tutaanza kuomba vifaa ili tuweze kutoa huduma zile za msingi pale za OPD na baadhi ya huduma za kulaza. Tuko kwenye jengo la mionzi sasa hivi tunaomba Wizara husika isituangushe kwa fedha zilizobakia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa vituo vya afya tumeendelea vizuri. Tuna vituo vya afya vya kimkakati vipya vitatu na vile vya zamani ni vitatu jumla vituo vya afya Sita. Vituo vyote vinakabiliwa na changamoto inayofanana ya watumishi wa afya pamoja na vifaatiba. Nilipochangia mara ya mwisho kwenye ripoti ya LAAC nilitoa takwimu ya mapungufu tuliyonayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie Kituo cha Afya cha Kata ya Lang’ata ambacho kwa kweli kimechakaa sana, tunaomba kituo hiki kikarabatiwe ili kiweze kutoa huduma katika viwango vya vituo vya afya vilivyokusudiwa kwa sasa hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti hii tulipaswa kupata vituo viwili vya afya vya kisasa, kimoja tumepata kwenye Kata ya Kirya ambacho ni Kituo cha Afya cha kisasa kabisa, kinahudumia mpaka watu wa kutoka kwa rafiki yangu Senior Brother hapa Mheshimiwa Ole-Sendeka kule Simanjiro pia kutoka Same wanapata huduma pale. Pia kile kituo kingine ambacho kilipaswa kujengwa bado hakijapata fedha tunaomba tupate fedha kwa ajili ya kituo hiki cha afya cha pili ili mpango ule na ahadi ile iweze kukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu miradi ya elimu, tuliahidiwa kupata shule mbili kwenye Kata zile mbili ambazo zilikuwa hazina shule. Bado Kata moja ya Toroha haijapata shule yake pamoja na kwamba tulifikia mahali kabisa mpaka pa kuwa requested bank account ili fedha ziingie lakini hapo palipokwama sasa tunaomba pakwamuke ili fedha ziweze kupelekwa wale wananchi wangu ambao wengi wao ni jamii ya wafugaji waweze kupata shule. Shule ambayo tumeipata moja ya Kivisini imekamilika vizuri na tumekusudia kuifanya moja kati ya shule zetu bora kama ilivyo shule ya Dkt. Asha Rose Migiro, Shule ya Kamwala na Shule ya Usangi ‘A’ ambazo ni moja ya shule bora Kimkoa na Kitaifa zinazotokea pale Wilayani kwetu Mwanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna tatizo kubwa la Walimu. Suala la ajira ya Walimu ni tatizo kubwa sana. Juma lililopita tulikuwa tunafanya tathmini ya kila Mwalimu jinsi ambavyo ame-perform na alivyofaulisha kwenye somo lake, wako Walimu wa kujitolea ambao hawalipwi chochote lakini wameongoza katika kufaulisha masomo yao. Walimu kama hawa zawadi pekee ya kuwapa ni kuwajiri kwa kweli katika shule hizi. Vinginevyo wapo ambao wamejitolea muda mrefu ninaogopa wanaweza wakafikia umri wa kustaafu kabla hawajaajiriwa halafu wakapoteza kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la maji. Ipo miradi mingi lakini kwa kweli kasi ya miradi ya maji haijaridhisha bado. Mheshimiwa Waziri wa Maji juzi alikuja nilimweleza hili jambo, kubwa kuliko yote ni shukrani kubwa sana kwa Serikali kwa ajili ya mradi mkubwa wa maji wa Same - Mwanga - Korogwe ambao utalisha maji katika Wilaya ya Mwanga eneo lote la tambarare Same mpaka Korogwe, huu ni mradi mkubwa sana wa Shilingi Bilioni 262. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais mradi huu ulikwama kwa muda mrefu lakini mwezi uliopita alikuja Mheshimiwa Waziri wa Maji akakwamua mradi ule tukasaini restatement agreement na kuahidiwa kwamba ndani ya miezi 14 maji yatatoka, tunaomba ahadi hii ambayo watu wameichukua kwa thamani sana kwa sababu ni ahadi ya Mheshimiwa Rais ikamilike kama ambavyo imeelezwa pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la barabara linaendelea vizuri lakini kipekee niishukuru Serikali kwa ajili ya usanifu unaoendelea wa barabara inayotoka Kisangara kwenda Nyumba ya Mungu kilometa 17 kwa kiwango cha lami. Barabara hii ni muhimu kwa sababu eneo lile lina miradi mikubwa ya Kitaifa, huku mradi wa umeme ambapo tunachangia kwenye Grid ya Taifa na miradi mingine mingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kengele imegonga niseme moja la mwisho iko barabara nyingine ya kutoka Kifaru kutokea kituo cha Ng’ombe kilometa 75, hiyo ni barabara ya mpakani. Kwa hiyo kwa ajili ya umuhimu wake, kwa ajili ya mambo ya usalama na miradi mikubwa ambayo inaendelea katika eneo hili, hii ni barabara inayounganisha Tarafa Tano tunaomba iwe upgraded kufikia kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna tatizo kubwa sana la vyanzo vya mapato, vyanzo vyetu viwili vimetelekezwa. Kimoja ni Bwawa letu la Lang’ata ambalo lilikuwa likitoa Samaki na mapato makubwa sana, tunaomba kauli ya Serikali tatizo ni Samaki wamedumaa au tatizo ni mbegu isiyofaa? Mpaka sasa hivi hakuna kauli ya Serikali juu ya bwawa lile tunaomba lifanyiwe kazi pamoja na suala la magugu maji katika Ziwa. Naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii ya kuchangia Wizara hii muhimu. Awali ya yote kwa vile Wizara hii iko chini ya Ofisi ya Rais mwenyewe, nichukue nafasi hii kumpongeza sana na kumshukuru kwa ajili ya kazi kubwa, mageuzi makubwa yanayofanyika katika sekta hii ya utumishi na hata sekta ya utawala bora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakuna anayebisha kwamba yako mageuzi makubwa ambayo yamefanyika ndani ya muda mfupi katika maeneo hayo yote mawili. Watanzania wanaona na hata dunia nzima inaona. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwapongeze Waheshimiwa hawa nikianza na Mheshimiwa George Simbachawene pamoja na Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete kwa kuaminiwa kuongoza Wizara hii nyeti. Ni wanasheria na mawakili wabobezi lakini nakwepa kuwaita wasomi kwa sababu historia inaonyesha kwamba suala hili la wanasheria kuitwa wasomi ilitengenezwa kwa ajili ya mahakamani ili kutawala zile nyongo zao na nini na kuheshimiana wakati mambo yanapokuwa makali kwenye mabishano. Sasa mnapotuita wasomi huku nje kuna kaujanja hapa mnataka kututenga na mambo fulani fulani mazuri, tumeshtuka tunaanza kukataa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la utumishi changamoto ambazo Waheshimiwa Wabunge wenzangu wamezizungumza katika maeneo yao pia zipo katika Jimbo letu la Mwanga hasa katika sekta ya elimu na afya. Upungufu ni mkubwa na changamoto zote zilizozungumzwa zipo. Naungana na wale ambao wameshauri kwamba pamoja na vigezo vizuri ambavyo TAMISEMI imeviweka katika kuajiri kama vilivyozungumzwa na Mheshimiwa Waziri katika Bunge hili, bado kile kigezo cha wanaojitolea ni kigezo cha muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, unaweza ukakuta hizi kazi za ualimu hasa ualimu na afya pamoja na kwamba ni kazi za mshahara lakini ni kazi za wito. Mtu anaweza akawa alimaliza 2015 akaomba ajira, alipoikosa akaenda kufanya shughuli zake. Leo 2022 nafasi zimetoka anaomba, tunasema kwa vile ni wa 2015 tumpe lakini yuko mwingine ambaye amehitimu 2018 akakosa ajira lakini akajitolea mpaka leo. Kwangu mimi huyu ndiye mwalimu au mhudumu wa afya mwenye wito kwa hiyo apewe kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, liko suala la ATCL ambalo nimeona kwamba kamati imeshauri kwamba Serikali iiondolee mzigo Wakala wa Ndege za Serikali mzigo wa kumiliki hizi ndege za biashara ambazo zinaendeshwa na ATCL. Wazo hilo ni zuri lakini naamini kabisa kwamba utekelezaji wake ni wa kiufundi sana ambao unahitaji makamati makubwa makubwa ya wataalamu waliobobea katika fani mbalimbali. Nachangia kwenye eneo hilo kama kuchochea tu kufikiri ili Serikali ione umuhimu wa kulikabili jambo hili kwa utaalamu wa hali ya juu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama kumbukumbu zangu ziko sawa, nikikumubuka Hotuba ya aliyekuwa Waziri wa sekta hiyo, Dkt. Harrison Mwakyembe kipindi fulani ambapo aliwashambulia sana watu walioingiza fedha kwenye akaunti ya ATCL ilihali wakijua kwamba kuna madeni. Nadhani utaratibu huu wa kuzinunua hizi ndege kupitia wakala wa ndege za Serikali umesaidia katika kutibu hili jambo kwamba ATCL imepata muda wa kupumua kuweka mambo yake sawa kabla haijaingia kwenye biashara hii nyeti ya kumiliki na kuendesha ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa jambo hili limetuokoa katika madeni ya ATCL hasa yale ya ndani kwa sababu sheria yetu hairuhusu kukamata mali za Serikali katika kutekeleza hukumu.

Mheshimiwa Spika, sasa katika madeni haya ya nje hasa yanayotokana na maamuzi ya mahakama za kimataifa imeonekana kwamba sasa ndiyo tumeizamisha huko ndiyo maana baadhi ya ndege zetu kwa taarifa zinazokuja ni kwamba zimekamatwa na pia hatujui kwamba na hizi ambazo hazijakamatwa ziko salama au ziko namna gani kwa sababu suala la kushtakiwa na kuwa na hukumu ambazo ni dhidi yetu ni suala la kawaida tu kwa sababu kama nchi inakuwa inaingia kwenye mikataba inafanya mambo makubwa haiwezekani ikakaa tu bila kukabiliana na majanga kama hayo ya kesi. Kwa hiyo, hatuwezi kukwepa, dawa yake ni kuangalia jinsi ya kulinda mali zetu katika matatizo kama hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tufanye nini? Mimi ushauri wangu, muundo wa ATCL mpango wake wa uwekezaji pamoja na masuala ya madeni yapitiwe upya kitaalamu. Ikiwezekana tufanye, sasa naomba kutumia lugha ya Kingereza, tufanye restructuring ya madeni yake kwa kupitia benki. Baada ya kufanya hivyo, yatakayoonekana kwamba bado ni madeni au ni fedha ambazo tunahitaji kwa uwekezaji tukope kwenye benki. Tunaweza kutumia benki yetu kama TIB. Tukope kwenye benki halafu tu-charge assets zote za ATCL kwenye benki katika maana kwamba tuweke rehani assets zote kwenye benki. Tukifika hapo maana yake ni kwamba hizi assets zitakuwa zinamilikiwa na benki. Kwa hiyo, hakuna anayezidai wa ndani wala wa nje wala anyeidai Serikali ambaye anaweza akagusa mali hizi kwa sababu zitakuwa zinamilikiwa na benki.

Mheshimiwa Spika, nadhani hii ni njia mojawapo ambayo ikifanyiwa kazi kitaalam inaweza ikatufikisha katika utatuzi wa tatizo hili la ATCL ambalo tumelia nalo kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nimejaribu kuangalia mashirika mengine ya ndege, umiliki wake uko namna gani. Kenya Airways kwa takwimu zilizoko kwenye mitandao na tovuti zao za 2022, za mwaka jana, 48.9% ndiyo inayomilikiwa na Serikali na katika hizi 48.9%, 38.1% inamilikiwa na fungamano (consortium) ya mabenki ambayo yameikopesha KQ. Kwa hiyo, utakuta zaidi ya 51% haimilikiwi na Serikali. Ukija South African Airways, 51% inashikiliwa na fungamano la makampuni (consortium) inayoitwa TAKATSO, 51%.

Mheshimiwa Spika, Rwanda airways yeye alikuwa anamilikiwa na Serikali lakini mwaka jana kuna mazungumzo yalikuwa yanaendelea, sijapata matokeo yake ya mwisho, walikuwa wanakusidia kuuza asilimia 49 kwa Qatar airways.

Mheshimiwa Spika, British Airways wakongwe wenyewe wanamilikiwa na Parent Company inaitwa International Airline Group, asillimia 25.1 hii Parent Company inamilikiwa na Qatar Airways. Ninachosema ni nini? tukitoa asilimia 51 ya hisa za ATCL ikawa haimilikiwi na Serikali ina maana kampuni hii haitakuwa ya Serikali kwa sababu majority share…

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, private, kwa hiyo hii itasaidia…

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. JOSEPH A. TADAYO:… hakuna atakayeweza kuikamata ndege zetu kwa ajili ya madeni ya Serikali kwa sababu mmiliki hatakuwa Serikali katika maana ya majority shareholding. Na suala la kumiliki…

SPIKA: Mheshimiwa Tadayo kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Halima Mdee.

TAARIFA

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, taarifa kuchagiza tu kidogo, Indian Airways ambayo imebeba jina la nchi inamilikiwa kwa asilimia 100 na Kampuni binafsi ya TATA, kwa hiyo nakubaliana na wewe kwamba haya mambo lazima tuyafikirie na kuyachakata. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Tadayo unapokea taarifa hiyo.

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa hiyo mimi nilizozifanyia utafiti Indian Airways haikuwa mojawapo lakini mimi ninaona fahari kwamba airline yetu imefufuliwa in the National Carrier. Wakati ulikuwa ukisafiri kwenda hata Nairobi au Ethiopia ukiangalia ndege zao zimepangwa pale National Carrier kama ng’ombe wa Mmasai halafu sisi tulikuwa hatuna ndege ilikuwa ni jambo la kusikitisha. Kwa hiyo huu ni mchakato ni mzuri, nakubaliana na hiyo taarifa; lakini tuendelee kufanya mchakato wa kulinda na kuokoa ndege zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata suala zima la kumilikiwa hizi ndege na Wakala wa Serikali nadhani kuna benefit zingine ambazo tulikosa. Kwa mfano kuna taasisi inaitwa International Civil Aviation Organization (ICAO) ambayo inashughulikia mambo ya kufanya tathmini zinapotokea ajali za ndege, mambo ya bima na vitu vingine vingi sana. Sasa sidhani kama ile taasisi inaweza ika-admit ndege ambazo zinamilikiwa na Serikali kwa sababu ile ni purely kwenye mambo ya biashara.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa muda wangu nafikiri bado dakika chache naomba tu nizungumzie suala moja tu juu ya sekta ya utoaji haki. Naipongeza sana Serikali kwa uwekezaji mkubwa katika sekta ya utoaji haki hasa kwa mfano katika eneo la Idara ya Mahakama.

Mheshimiwa Spika, majengo haya mazuri na facility zingine bado hazitaweza kutufikisha tunapotaka, kama sheria zetu za procedure hatujazibadilisha. Mwalimu wangu Marehemu Dkt. Lamwai Mungu amlaze mahali pema, aliwahi kuniambia kwamba kila mtu anajua haki yake lakini jinsi ya kuipata ndio ambayo watu hawafahamu. Kwa hiyo tusiporahisisha sheria zetu hizi katika kupata haki mbalimbali bado sheria zitakuwepo pale zinatupa haki lakini jinsi ya kuifikia inakuwa changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naona kengele imegonga nisiendelee sana kwenye hilo naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii muhimu sana. Awali ya yote nimpongeze Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambayo anaendelea kulifanyia Taifa letu na mojawapo ya sehemu ya kazi nzuri ni kututeulia viongozi makini kama Waziri wetu wa Mambo ya Ndani pamoja na Naibu wake na timu yake nzima kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kazi inakwenda vizuri kwenye Wizara hii mchango wangu utakuwa mfupi. Nimetazama majukumu ya Wizara hii chini ya Government Notice ile namba 383 na namba 385 ya mwaka 2021 kama ambavyo imeboreshwa na Government Notice namba 334 ya Julai, 2021. Majukumu ya Wizara hii ni mapana sana, lakini yako summarized pale kwamba ni utekelezaji wa sera za usalama wa umma (implementation of policies on public safety).

Mheshimiwa Mwenyekiti, jukumu hili si jukumu dogo kwa sababu ni jukumu ambalo wateja wake kuanzia mwanzo mpaka mwisho ni binanadamu. Kama ambavyo watu wanasema kazi ya kuongoza binadamu siyo kazi ndogo, wakati mwingine kuongoza vitu ambavyo havina utashi au haviko hai ni rahisi zaidi kuliko kuongoza binadamu. Kwa hiyo taasisi zote hizi ukianzia Polisi, Magereza, Uhamiaji, Zimamoto zote zinashughulikia binadamu, tena binadamu wenye changamoto au binadamu walioko katika changamoto za matukio mbalimbali. Kwa hiyo si jambo ambalo ni rahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tukubali kwamba juhudi zote hizi za uchumi za kukuza uchumi na ustawi wa jamii ambazo Serikali inaendelea nazo bila Wizara hii kukaa sawa sawa hatutaweza kufaidi matunda yake. Tutaomba madarasa yatajengwa lakini vibaka watakuja wataiba madirisha ya kisasa. Tutaomba dawa zitakuja wezi wataiba, mateja wa madawa ya kulevya watavuruga Nchi. Kwa hiyo, Wizara hii ina umuhimu mkubwa sana tofauti ambavyo tunadhani kwamba labda kazi yao ni kukamata na kuachia watu. Mambo yote ya msingi haki za binadamu zinaanzia Wizara hii, haki jinai zinaanzia Wizara hii. Sijui kufanya siasa, hata sisi kufanya si lazima Wizara hii ikae sawa sawa ili tuweze kufanya siasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata mpira, Yanga wasingecheza vizuri jana kama kungekuwa hakuna usimamizi wa Wizara hii. Tuende mbele hata suala la sovereignty, uhuru wa Nchi ambaye inakupa right to govern na responsibility to protect (haki ya kutawala na wajibu wa kulinda). Bila kuwa na Wizara hii makini ikalinda watu wako huwezi ukahesabiwa kama ni nchi huru kama watu wanakufa na kuuwawa kila siku kama kuku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa la kujiuliza hapa ni kwamba hawa tunaowakabidhi dhamana kubwa nanma hii hali yao ikoje? Hali yao kibajeti kwa mfano iko namna gani? Kamati imeeleza hapa kwamba ukienda kwenye miradi ya Wizara hii stress ni msongo wa akili imeeleza taarifa ya Kamati kwamba tumekwenda Handeni kule kwenye kile chuo cha pale Chogo kwa kweli kinatia msongo. Hali siyo nzuri kwa sababu hakuna kinachoendelea pamoja na bajeti kutengwa. Ukienda kituo pale ofisi za uhamiaji pale Babati hakuna kinachoendelea, ukienda kile kituo cha uhamiaji kule Kichakamiba halafu kina nafuu kidogo lakini bado, ukienda Chuo chetu cha Polisi Moshi bado, ukienda gereza kule Kilosa bado, hata ukija kwenye Gereza la Jimbo langu la Mwanga bado hali hairidhishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi ninachokiomba sana ni kwamba fedha zinazotengwa za miardi ya maendeleo kwa Wizara hii ziende tena ziende kwa wakati, vinginevyo tunajiingiza kwenye mazingira ambayo sio mazuri. Hali ikoje kimaslahi, malalamiko juu ya stahiki za askari yamekuwa mengi sana, kila siku wapo kwenye maswali na majibu tunayaona. Hili suala linahitaji kutazamwa sana kwamba tusibaki tubakakia na askari wetu ambao wanaishi kwenye malalamiko kila siku. Suala lingine ambalo ni la muhimu katika taasisi za Wizara hii ni suala la mafunzo na vifaa, taasisi zilizoko chini ya Wizara hii kama nilivyosema zina-deal na wahalifu zina-deal na wageni zina-deal na majanga. Sasa ili uweze kushughulika na mambo kama haya na bado utimize sheria lazima mafunzo na vifaa uwe navyo vya hali ya juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais ameweka umuhimu mkubwa sana katika suala la haki jinai ndiyo maana akaunda na Tume ambayo ina wabobezi inazunguka kufanya kazi nzuri, lakini masuala yote yanaanzia kwenye Wizara hii. Mahakama haziwezi kufanya vizuri kwenye mambo ya uhalifu kama Wizara ya Mambo ya Ndani haifanyi vizuri. Tutaweka watu ndani, Magereza watatoka bado majambazi kama suala la urekebu halifanyiki vizuri. Kwa hiyo, tunapokuja kwenye suala la bajeti katika Wizara hii kwa kweli ni vizuri tukatilia kipaumbele kama ambavyo tunatilia kipaumbele Wizara zingine ambazo labda matokeo yao yanaonekana kwa macho, maana ukisema kilimo utaona mashamba kwa macho na chakula utakiona, ukisema madini utaona madini yanachimbwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa wanashughulika na jambo ambalo pengine halionekani kwa macho lakini lina umuhimu mkubwa sana ili hao mengine yaweze kufanyika. Liko suala ambalo limesumbua, Tanzania tu lakini limesumbua hata Dunia hasa Nchi za Afrika na Afrika Mashariki kwa sasa. Ni juu ya suala la hizi taasisi za dini pamoja na NGOs ambayo zinafanya mambo ambayo kwa lugha ya mtaani tunasema ni ya hovyo, lakini tuseme ni mambo ambayo ni kinyume cha sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo pamoja na mengine ambayo yapo lakini tatizo moja wapo ni suala zima la kuchuja hizi taasisi wakati wa usajili. Tunafahamu kwamba sheria inataka kabla taasisi haijasajiliwa idhaminiwe na taasisi nyingine ambayo tayari iko inafanya kazi. Sasa udhamini huu uko wa namna gani, siyo suala tu la kusaini form tu ambalo nadhani ndiyo linalofanyika. Umefika wakati sasa udhamini huu uende na uwajibikaji kwamba wacha niitolee mfano dini yangu mimi ili ni rahisi zaidi. Kama mimi nakuja nataka kusajili taasisi ya kikristo, nafikiri umefika wakati sasa Wizara ku-rank zile taasisi za kikristo ambazo tayari zipo, zile ambazo zimeshadumu miaka mingi na zina sifa ya kudhamini taasisi mpya ndiyo zipewe wajibu huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, udhamini unakuaje? Lazima kusaini form ya kusema mimi so and so wa taasisi fulani nimesoma Katiba ya mwombaji na mafundisho yake, Constitution and Doctrines, nimeridhika kwamba kwa Katiba hii na kwa mafundisho haya huyu mwombaji anaweza akaendesha taasisi au kanisa whatever la Kikristo. Sasa akishasaini hivyo tukakubaliana siku naye akianza kuficha watu porini tutamuuliza, atakuwa ni sehemu ya kutusaidia katika ushahidi na katika kuiwajibisha hii taasisi kwamba mbona wewe katiba yako ilisema unafanya haya na haya, haya ya kupeleka watu porini ya kushindisha watu njaa, mbona yalikuwa hayapo katika katiba yako wala kwenye doctrines zako. Usipofika hapo tutaendelea kupata shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina fahamu kwamba utaratibu huu unafuata katika maana ya udhamini lakini hauendi deep kwenye kuhakikisha kwamba yule anayedhamini ni nani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wakati tunaingia Council of Legal Education tuwe Mawakili ilikuwa lazima upate referee, lazima upate udhamini wa Wakili lakini siyo kila Wakili, ni Wakili ambaye amefikia level fulani ya seniority ambayo Mahakama inamuani kwamba huyu akituambia huyu kijana anafaa mruhusuni afanye mtihani wa uwakili anaweza, siyo kila mtu tu. Kwa hiyo, hili tunahitaji kuliangalia kwa makini sana lisije likatuvurugia Nchi kama ambavyo tumeona sehemu zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yote hayo lakini nisisahahu kupongeza taasisi zilizoko chini ya Wizara hii. Nikianzia Jimboni kwangu Mwanga, Polisi pale Mwanga jengo lao wamelikarabati kwa kuchanga kutoka kwenye mishahara yao na kuwakamata wadau wengine kama sisi, lakini wamelikarabati vizuri. Wananchi wa Jimbo la Mwanga hasa Tarafa ya Usangi wameungana wakajenga Kituo cha Polisi cha kisasa kabisa na hili nikuombe sana Mheshimiwa Waziri kwamba baada ya kukupitishia bajeti yako twende ukakitazame kile kituo ili tujenge na vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho pia niwapongeze Idara ya Uhamiaji, mradi mmojawapo ambao unafanya vizuri ni kile Chuo pale cha Kichakamiba taarifa ni kwamba walianza kwa kukatana mishahara wachange wao wenyewe kutoka mishahara yao kuanza kujenga na ndiyo maana ile taasisi iko vizuri sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naunga mkono hoja na nawapongeza kwa kazi nzuri wanayofanya. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kupata nafasi hii. Awali ya yote nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Pindi Chana, Waziri pamoja na timu yake yote ikiwa ni pamoja na Naibu Waziri kwa dhamana kubwa hii ambayo Mheshimiwa Rais amewapa ya kuongoza Wizara hii ambayo kwanza inabeba uchumi wa nchi, lakini pia inabeba taswira ya nchi yetu. Mheshimiwa Pindi Chana kwa kiasi kikubwa nakufahamu tumefanya kazi pamoja kwenye Halmashauri Kuu ya Taifa, mzigo huu ni size yako kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mary Masanja dada yangu tulikuwa wote kwenye mapambano ya tembo kule kwenye Jimbo langu yalipoanza pamoja na kwamba yanaendelea nitakueleza, lakini niliona uwezo wako, mzigo huu wa kumsaidia Mheshimiwa Pindi Chana ni size yako kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaongelea maeneo mawili; moja kuhusiana na Jimbo langu lakini la pili nitazungumza juu ya habari ya Royal Tour. Jimbo langu linapakana na mbuga za wanyama mbili moja, ni Tsavo ya Kenya halafu na Hifadhi ya Mkomazi ya hapa kwetu Tanzania. Tumekuwa na changamoto kubwa sana ya tembo na kwa kweli kwa juhudi ambazo Wizara imeshafanya mimi nawapongeza. Lakini mimi kwa kweli sasa hivi kilio changu kikubwa ni kwamba linapotokea janga kama hili watafiti wetu tunawasikiliza wanasema nini? Vyuo Vikuu vyetu vinasemaje juu ya janga hili ambalo limekaa muda mrefu kiasi hiki? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama basi tumefikia hapa, mimi ningeshauri Wizara kwa kweli labda mtangaze package kama iliyotangazwa na Wizara ya Elimu juzi kwamba, atakayeweza kutoa chapisho likaenda kwenye majarida fulani mashuhuri atapata fifty million shillings basi na hapa nadhani mngetangaza boom ili watafiti wetu waingie kazini kwa sababu hali haifurahishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikwenda na Mheshimiwa Naibu Waziri kule hali haikuwa nzuri, lakini pia yako mambo ambayo tuliwaahidi wananchi wa Jimbo la Mwanga ambayo pia kwa namna fulani yangesaidia kupunguza kasi ya tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na suala la lango la Kaskazini la Mbuga ya Mkomazi ile ahadi mpaka leo haijatimizwa pamoja na kwamba iliingia katika utaratibu wa bajeti ya mwaka uliopita. Tunaomba ile ahadi itimizwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na ahadi ya bweni la wavulana katika shule ya sekondari Kigonigoni, ili kuwapunguzia kutembea umbali mrefu kwa sababu ya tembo kwenye eneo lile. Pia kulikuwa na ahadi ya shule ya msingi ya Mbigili kwa sababu hiyo hiyo. Ahadi hizi bado hazijatekelezwa ninawashukuru wenzetu wa TANAPA, juzi juzi wamenitumia taarifa ya kuonesha kwamba zimeingia kwenye taratibu zao za bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu yangu Mwakilema anatoa ushirikiano sana hasa kwenye upande wa mawasiliano namshukuru, kwa hiyo naomba sasa, ahadi zitekelezwe ili kuendelea kuwapunguzia wananchi hawa machungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kuna suala la kifuta machozi kwa waliopoteza maisha na fidia kwa waliopoteza mazao. Hilo pia bado halijakamilika, tunaomba hayo yatimie, ili tuendelee kupata ushirikiano wa wananchi wa Mwanga katika janga hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende kwenye suala la Royal Tour. Royal Tour pamoja na yote mema yaliyozungumzwa lakini ningependa kurudi kwenye historia yake kidogo kwamba ile ni series ambayo huwa inafanyika ikiongozwa na yule ndugu yetu Peter Greenberg ambaye ni mtu mwenye nishani nyingi sana za kimataifa katika eneo hili na ile inatolewa kwanza kwa nchi ambayo ina vivutio mahususi vya utalii na pili nchi ambayo inakiongozi ambaye, amethibitisha kuwa na uwezo mkubwa wa kushawishi katika masuala ya kukuza uchumi. (Makofi)

Kwa hiyo, kwa Royal Tour ile kufanyika hapa ni kwamba tume-qualify kuwa na nchi yenye vivutio hivyo na pia kuwa na Rais ambaye amethibitika kidunia kwamba anaushawishi mkubwa katika kusukuma uchumi wa nchi yake. Kwa hilo, lazima tumpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa ku-qualify kufikia hapo na hii Royal Tour huwa inaongozwa na wakuu wa nchi, najaribu kusema hivyo kwa sababu kuna watu wanapata shida kwamba kwa nini tusingetumia sijui ma-star wa dunia? Ma-star wa dunia u-star huwa unakwisha, lakini fikiria mpaka leo kuna mahali unakwenda unauliza unatoka nchi gani? Tanzania ni country of Nyerere? Mpaka leo Nyerere bado wanamkumbuka. (Makofi)

Sasa tunajaribu kujenga legacy nyingine ambayo itaendeleza pale ambapo pamebaki ili kuweza kuendelea kukuza uchumi wa nchi yetu. Ilipofanyika Israel aliiongoza mwenyewe Benjamin Netanyahu - Waziri Mkuu, ilipofanyika Poland aliiongoza Waziri Mkuu - Mateus, ilipofanyika Ecuador aliiongoza Rais mwenyewe Raphael Korea, ilipofanyika Mexico aliiongoza Rais Philippe na Rwanda aliiongoza Paul Kagame mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ni suala ambalo linaongozwa na Wakuu wa nchi sio kila mtu hapa Mbunge wa Mwanga niende nikaongoze Royal Tour hilo haliwezekani. Nilikuwa najaribu kujibu hilo swali na katika nchi zote hizi ambazo Royal Tour hii imefanyika kwa kuongozwa na wakuu wa nchi uchumi wa nchi zile ulikua sana. Hakuna ubishi kwamba Israel pamoja na kwamba ni nchi ndogo na yenye migogoro mingi, lakini inaongoza katika uchumi na teknolojia. Rwanda hapa katika nchi za Afrika tunaingalia kabisa kwa jicho kwamba ni nchi ambayo inaongoza. Ecuador kuna programu moja imeanza pale inaitwa Four Worlds in One Place, ambapo waliigawanya ile nchi katika Zone nne tu za climate tu, Amazon, Andes, Coast na vile Visiwa vya Galapagos. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vinailetea watalii wengi na uchumi umekua kwa ajili hiyo tu. Sasa Tanzania tuna uwezo wa kugawa hata dunia 40 ndani ya nchi yetu. Ukienda kwenye culture peke yake inatosha kabisa kuvutia utalii, kuna sehemu Pwani huko, ukienda kwetu huko Kaskazini culture ziko tofauti ile peke yake ni kivutio. Hata chakula for that matter, rafiki yangu Musukuma bila ugali kwake hakuna chakula ukimletea ndizi anasema hii ni mboga. Ukienda kwa Mheshimiwa Mwigulu kule wanakula kuku wa kienyeji, lakini ukienda kwa ndugu zangu Wamasai wanasema hawa ndege sisi hatuli na kadhalika. Kwa hiyo, diversity peke yake ya culture ni kitu kikubwa sana ambacho kinauwezo wa kutuletea utalii mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nenda Zanzibar tulikwenda kule kwenye ile misitu ya Jozani, tukakuta wale nyani wekundu ambao dunia nzima unawakuta pale Zanzibar. (Makofi)

Kwa hiyo, sisi hata faru tunao wengi mpaka tuna Faru John na faru wa kila aina na sasa hivi nimeona kuna nyati weupe wamezuka. Kwa hiyo, kwa kweli kwa kutumia sasa hii Royal Tour ambayo imetufikisha hapo, tuna uwezo wa kuipeleka hii nchi next level kwa namna ambayo ni rahisi kabisa. (Makofi)

Ndugu zangu ukisoma kwenye vitabu wafalme wa zamani walitangulia wenyewe vitani, lakini wakitangulia vitani walikuwa wanakwenda pamoja na watu wao. Sasa Rais ametutangulia katika vita hii ya kufufua uchumi wetu kwa njia nyingi ambazo tumeziona hata za miundombinu na sasa ya Royal Tour, lakini sasa tunapaswa kwenda naye, tusiseme tu kwamba ameupiga mwingi sasa akishaupiga mwingi nani atafunga goli? Ameupiga mwingi watalii wamekuja je, Uhamiaji wako tayari pale airport ili kuwapitisha watalii haraka haraka tusianze kupata lawama? Ameupiga mwingi kwenye mahoteli amezungumza mchangiaji mmoja customer service yetu iko namna gani? Ameupiga mwingi watalii wamekuja, barabarani vizuizi vyetu hivi kilometa 100 vizuizi sita tunafikaje hapo? (Makofi)

Kwa hiyo, yako mambo ambayo kwa kweli tukitaka tupate faida ya hii Royal Tour inakuwa ni jukumu letu sisi sote, hasa sisi Wabunge ambao tunapita huko tukiwaona tuseme tupige kelele na Serikali iitikie ifanye kazi yake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa yako mambo kama hili nilizungumza la ripoti ya CAG ambapo imezungumzia juu ya vitalu ambavyo tayari vilishagawanywa lakini watu hawajapewa. Hiyo inaweza ikatupeleka kushtakiwa bure, tukajikuta tunalipa mamilioni kumbe tu kuna mtu mmoja ambaye baada ya mwingi kule kupigwa ameshindwa kupokea tukafunga goli. (Makofi)

Kwa hiyo, vitu kama hivyo na hata hivi vitalu bado ukiangalia ukilinganisha kwa kweli bei zake bado ni kubwa na muda ambao watu wanapewa mwaka mmoja ni mfupi sana. Ni vyema tungefikiria hata kumpa mtu miaka mitatu mpaka mitano wakati anapowekeza pale ajue anawekeza mahali ambapo kesho na kesho bado atakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia utaratibu wa kuondoka na zile trophies kwa wale wawindaji, wakati mwingine unakuwa mgumu sana tunaona hayo malalamiko katika maeneo mengi. Kwa hiyo, mimi wito wangu ni kwamba pamoja na mama kuupiga mwingi na tukapata hii boom sasa ya watalii ambayo inakuja na sekta zingine kwa sababu Royal Tour haikuzi utalii peke yake, kwenye nchi zote ambazo ilifanyika imekuza uchumi wote kwa ujumla. Sasa ni lazima tujiandae kila sekta kuhakikisha kwamba hili linalokuja tunalipokea na kuweza kufunga yale magoli ambayo yamekusudiwa, isije ikawa timu nyingine ile ya watani wako ambayo magoli kwao kidogo inakuwa shida shida na inakuwa ya kubahatisha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naunga mkono hoja sana na ninaomba tuunge mkono hoja hii, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi hii ya kuchangia hoja hii muhimu. Awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake kwanza kwa kuaminiwa kuongoza Wizara hii nyeti, lakini pia kwa kazi nzuri ambayo wameifanya na hasa kwa kuleta bajeti ya matumaini makubwa kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, bajeti hii kwa maoni yangu ni kweli kabisa imezingatia lile azimio la nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki kwamba tuwe na bajeti ambazo zinachochea kukua kwa uchumi wa nchi na kuwapunguzia wananchi ugumu wa maisha. Naiona sura hiyo katika bajeti yetu kwa kiasi kikubwa. Hii ni bajeti shirikishi ambayo imeanzia chini kabisa kwenye halmashauri zetu, ikapanda ikatufikia huku juu, kwa hiyo ni rahisi hata utekelezaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona jinsi ambavyo bajeti hii imesisitiza juu ya kuongeza pato la Taifa kwa kuweka msisitizo mkubwa katika sekta ya kilimo, madini na hata sekta ya utalii na pia kuongeza mzunguko wa fedha kwa kutenga fedha za kulipa madeni hasa ya wakandarasi na wazabuni wengine na pia fedha kwa ajili ya miradi mikubwa ya kimkakati iliyokuwa inaendelea. Hii itainufaisha sana nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, pia yako marekebisho ya sheria na baadhi ya tozo ambazo zimeondolewa na nini zote zikielekezwa katika kuchochea sekta binafsi ambayo ni muhimu sana kwa ajili ya uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, pia suala zima la kusisitiza juu ya value for money yaani thamani ya kazi kwa fedha zinazotolewa. Nimeona kwa namna pekee kabisa, Ofisi ya CAG inaongezewa wataalam wa fani zingine ili kuipa nguvu zaidi katika kuhakikisha kwamba miradi inakaguliwa kwa uhakika zaidi na kwamba tuendelee kupata thamani halisi ya fedha ambazo tunatoa. Nimewahi kulisema hili katika Bunge hili kwamba hata matumizi yetu ya force account kwenye halmashauri zetu na maeneo mengine yanahitaji sana kupelekewa wataalam wa fani zote ili kwamba tunapofanya kazi hasa za ujenzi tuweze kupata kitu ambacho ni cha uhakika zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, iko hofu ambayo inaendelea duniani kote juu ya hili suala la inflation na mdororo wa uchumi. Ukiangalia sana kinacholeta hofu hii ni vita ya Ukraine na Urusi, lakini nasema vita ya Ukraine na Urusi, risasi hazifiki huku, kinachofika huku ni madhara yanayotokana na bei za mafuta na suala zima la chakula. Kwa upande wa bei za mafuta naweza nikasema ni changamoto, lakini upande wa chakula kwetu inaweza ikawa fursa vilevile.

Mheshimiwa Spika, nasema hivyo kwa sababu tukijikita kwenye kilimo kwa nguvu zote ikawa kama vita, kuhakikisha kwamba kila ardhi inayofaa kulimwa, inalimwa na inalimwa mazao ambayo kitaalam yamekubalika kwamba yatatuletea tija, tutafika mahali pazuri. Hata ardhi ya mtu ambaye hajaitumia, kama hailimi sasa either ikodishwe alipwe rent ilimwe au apewe hisa kwa mwekezaji ambaye ataingia pale ili ardhi yote inayofaa kulimwa, ilimike.

Mheshimiwa Spika, mwaka 45 yuko mpiga kura wangu mmoja wa enzi hizo kabla sijawa Mbunge alikuwa anaitwa Reverent Silas Msangi alitunga ule wimbo unaosema Tanzania, Tanzania nakupenda kwa moyo wote. Akaelezea jinsi ambavyo watu watakuja kukimbilia Tanzania ili waweze kupigana kwa ajili ya kupata uhuru kwao. Unabii huo unaweza ukatimia tena na hilo lilitimia kwa sababu ule wimbo ule ulitungwa mwaka 45 ikaja kutimia mpaka kesho asubuhi. Hata sasa hivi tukijikita vizuri kwenye sekta ya kilimo watu watakuja kufatuta chakula kwetu na nchi hii itaendelea kukimbiliwa na watu kama sehemu pekee ambayo itakuwa inapatikana chakula kwa sababu kama ni ardhi tunayo kubwa kuliko ya Ukraine, kama ni hali ya hewa, ni nzuri na hatuna uhaba wa wataalam, watu wamesoma vizuri na uwezo wa kufanya kazi wanao.

Mheshimiwa Spika, nashauri, tujikite kwenye sekta ya kilimo kwa nguvu kama ambavyo tuliingia kwenye sekta ya miundombinu tukaanzisha miradi ambayo ilikuwa ni ya kufikirika na ikatimia. Kwa hiyo, tukiingia kwenye sekta ya kilimo kwa nguvu kwa kiasi hicho tunaweza tukafika mahali pazuri sana. Tusiende tu kwenye hali ile ya kusema, tumetenga fedha nyingi lakini tunaziingiza kwenye miradi kama, sisemi vibaya lakini kilimo kwanza labda na nini ambayo tunaishia kuongeza matrekta ambayo yanaharibika siku mbili. Twende kwenye hali halisi, mazao gani yanafaa hapa, ardhi kiasi gani ipo, yalimwe, yasimamiwe ili tuweze kutoka sisi na kuitoa East Africa yote katika matatizo haya ya chakula.

Mheshimiwa Spika, tunakushukuru sana jana ulituletea wataalam kutoka Benki Kuu pamoja na Taasisi za Fedha, wakatoa mawasilisho yao. Ukiangalia yale mawasilisho yao yameendana kabisa na review ya PricewaterhouseCoopers wanaofanya juu ya bajeti hii. Jambo kubwa sana la msingi lililojitokeza ni juu ya ukweli kwamba inflation kwa sisi Tanzania tuko vizuri kuliko Nchi zote za Afrika Mashariki pamoja na SADC. Wataalam hawa wasingeweza kudanganya. Jambo hili si jambo la kuchuliwa kwa mchezo mchezo, ni jambo ambalo ni la muhimu sana, tukianzia hapa tunaweza kufika mbali.

Mheshimiwa Spika, sasa ukiacha hapa tulipofikia, pamoja na changamoto za corona na za vita vya Ukraine, bado taarifa zinakuja kwamba hoteli zetu na booking zetu za utalii zimejaa na hii itakuwa endelevu kwa sababu ya royal tour. Tukiipokea hii vizuri, Tanzania itapaa na ikipaa tusitegemee mazuri tu, tutegemee na maadui pia wa kiuchumi. Tumeona hapa kiongozi mkubwa wa nchi moja jirani wa cheo cha Senator anatoa kauli za kashfa kashfa za kuingilia suala la ndani ya nchi yetu. Inasemekana basi kama taarifa za kwenye mtandao ni za kutegemea sana, kwamba nchi yetu imepelekwa ICJ. Siamini kwa sababu sioni kwamba lililotokea linaweza kupelekwa ICJ kwa sababu ICJ ina mamlaka za aina mbili. Kwanza, ni juu ya contentious matters ambazo ni ugomvi wa mipaka, ambayo ni magomvi kati ya nchi nan chi, ambalo sasa sio hilo. Lingine labda ni kwenda kutafuta ushauri tu.

Mheshimiwa Spika, ukweli ni kwamba jambo hilo linachochewa na nchi nyingine, inaonesha kabisa kwamba hii ni vita ya kiuchumi ambayo inatokana na hali hii tunayoisema, Tanzania hii tunayoijua ambayo watu wamekuwa wakiitazama kwa jicho kama vile sisi sio watu wa kupiga hatua sana, lakini leo hii tukiambiwa kwamba inflation yetu ipo chini kuliko Nchi zote za Afrika Mashariki na SADC, lazima wajitokeza maadui. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nadhani Vyuo Vikuu vilipoanza hapa Afrika Mashariki, Kitivo cha kwanza kilikuwa ni cha Sheria, kwa hiyo naamini kimejizatiti, hata wakienda ICJ twendeni, nina hakika tutajieleza vizuri na tutashinda na tutaendelea kukuza uchumi wetu kwa njia hizo za utalii, kilimo, madini na hata sekta zingine kama za ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, amezungumza vizuri Mheshimiwa Shamsi Vuai Nahodha juu ya ubora wa barabara zetu na kadhalika na kadhalika. Ukweli tumekuwa tukisema Serikali iwape kipaumbele wakandarasi wazalendo, lakini pia na wao ni vizuri wakaji-link na juhudi kubwa za innovation ambazo zinafanyika katika sekta ya ujenzi duniani ambazo zinahusisha makundi matatu. Kundi la kwanza, ni watengenezaji wa materials za ujenzi na kundi la pili ni wateja pamoja na wajenzi. Teknolojia imepanda sana, hata kama tutajaribu kuwa-favour watu wetu kwa kuwapa mitaji na kadhalika lakini kama watakuwa hawajaweza kuifahamu teknolojia iliyopo sasa, bado wanapokuja watu wa nje kwenye miradi wataonekana bei zao zipo chini na wataweza kupata miradi na miradi yao itakuwa bora zaidi kwa sababu ya teknolojia.

Mheshimiwa Spika, nilitaka kusema hayo, kusisitiza kwamba tunahitaji kwenda na teknolojia ya dunia na sasa hivi tunaishukuru Serikali, nimeona kwenye bajeti ya Waziri wa Fedha amezunguma juu ya suala la kuzingatia masuala ya TEHAMA katika kuendesha nchi, atatupunguzia gharama na atatuongezea na ubora wa kazi.

Mheshimiwa Spika, lingine ni hili la ku-take advantage ya hali ya uchumi ilivyo sasa hivi, tunataka tuvuke kwenda mbele lakini tujipange pia kuwa maadui watakuwepo hasa kwa hili ambalo limejitokeza. Nimeona kabisa kwamba hili limejitokeza kwenye sekta ya utalii, sijiingizi kusema kwamba nani yuko sahihi na wapi, lakini suala zima la kuingiliwa na nchi ya nje katika mipango ya utekelezaji wa sheria zetu za ndani sio sahihi.

Mheshimiwa Spika, nilipata kusoma mahali kwamba masuala kama haya ya Loliondo na Ngorongoro mradi tu yanafanyika kwa mujibu wa sheria zetu, hakuna matatizo yoyote, ni jambo la kawaida ambalo linafanyika kila wakati katika maeneo mbalimbali ya Tanzania, wala halina sura ya ukabila wala ya uonevu, lakini sasa anayeingilia kutoka nje hapo ndiyo inabidi tujipange kwamba kwa kweli hii sasa ni vita. Mara nyingi mti ambao hauna matunda huwa haupigwi jiwe hata na mtoto mdogo, kwa hiyo ukiona mawe yameanza ujue mti wetu una matunda.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja na naomba Wabunge wenzangu waunge mkono hoja hii. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata nafasi hii. Nami pia kwa nafasi yangu kama Mbunge na Mjumbe wa Kamati iliyoleta hoja, naunga mkono hoja ambayo imeletwa kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulipewa kazi hii na wewe ili kuwapa haki wenzetu hawa ambao kwa mujibu wa kanuni tunawaita mashahidi, kuwapa ile haki yao ya kikatiba ya kuwasikiliza. Tuliwasikiliza chini ya kiapo na wakakubali kwamba kweli hizi kauli ni wao walizitoa. Inakuja sasa kuangalia juu ya uhalali wa kauli hizi kisheria kama ambavyo ripoti imezungumza kwamba unasimama, unasema kwamba viongozi wamepewa fedha ili kuruhusu chanjo ambayo si salama iingie. Kwamba kila anayetetea chanjo, kila anayechanjwa ikiwa ni pamoja na mimi kwamba ni hela, ni hela, ni hela. Halafu unafika mahali unajigamba kuwa juu ya kila mtu, kuwa juu ya Bunge, kuwa juu ya Spika kwamba mimi naweza nikafyatua mtu ndani ya Bunge, naweza nikafyatua mtu nje.

Mheshimiwa Spika, sasa ni wazi kabisa kwamba hata bila kusoma sheria, kila mtu anapaswa kuthibitisha yale mambo ambayo anayasema dhidi ya wenzake, kwa sababu kila mtu anastahili jina lake liwe safi kama lilivyo. Kwa maana ya kwamba mimi nimeajiriwa, nafanya kazi ni Waziri wa Sekta au nafasi yeyote ile. Kazi yangu naifanya kwa mujibu wa sheria, sasa kama unasema kwamba mimi nimepewa hela ili nifanye hivi, basi unao wajibu wa kuthibitisha jambo ambalo shahidi wa kwanza, Mheshimiwa Gwajima alishindwa kabisa kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, hali kadhalika kwa shahidi wa shauri la pili, Mheshimiwa Jerry Silaa, dai lake kubwa kwamba mishahara ya Wabunge haikatwi kodi. Sasa waraka wa msingi, primary document ya kuthibitisha mshahara wa mtu huwa ni salary slip ile ambayo inatumika kukulipa wewe mshahara. Mmiliki wa ile document ni yule anayekulipa, sasa Mhasibu Mkuu wa Bunge ameshakuja, ameshatoa ile, ametenga ile salary slip ni hii hapa, inakatwa kodi na amesema inakatwa kodi na ametueleza kwamba hata wakusanyaji kodi wenyewe waliwahi kuja wakatazama hili jambo, wakaridhika nalo. Hata hivyo, bado mtu unasisitiza kwamba upo sahihi. Maana yake sasa huu kwa kweli ni uvunjaji sheria wa makusudi tu ambao ndiyo maana Kamati ikafikia hapo kutoa adhabu hizi ambazo mimi naziunga mkono kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni vizuri sisi Wabunge tukakumbuka kwamba baada ya kuchaguliwa tuliapa kuilinda, kuitetea na kuhifadhi Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Katiba hii ndiyo iliyoweka hii mihimili ambayo tunazungumzia habari ya kuigonganisha na kuidhalilisha. Katiba hii ndio inayogawa mamlaka na madaraka ya watu kufanya kazi. Pia Katiba hii imetupa nafasi hasa sisi Waheshimiwa Wabunge namna ya kuhoji au namna ya kurekebisha mambo ambayo tunafikiri hayaendi sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Ibara ya 63, kwamba tunayo mamlaka ya kumhoji Waziri yeyote juu ya suala lolote lile ambalo tunaona haliendi sawa. Sasa endapo basi tunadhani kwamba Serikali inakwenda ndivyo sivyo hatuna mamlaka ya kwenda kuwahojia huko kwenye maeneo yetu, kwenye vikundi vyetu vya ngoma au kwenye Makanisa au mahali pengine popote pale. Sheria inatuongoza na kutupa wajibu kabisa wa kuja kuihoji mahali ambapo ni stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hali kadhalika, endapo basi mtu ameona kwamba sheria inayotulipa sisi mishahara kama ilivyo kwenye kifungu cha 20 cha ile National Assembly (Administration) Act, haipo sawasawa, basi unataka kuanzisha mchakato wa marekebisho, basi sidhani kama mchakato unaanzishwa hivyo. Sisi ni Wabunge, tunafahamu utaratibu wa kuanzisha mchakato wa marekebisho ya Katiba ili hata ile posho ya mafuta ambayo ukienda kununua mafuta tayari kodi imeshakatwa, kama unataka na yenyewe ikatwe tena sijui mara ya ngapi, basi mchakato wa kisheria upo wa kufanya hivyo, sio kwenda kuchochea wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sasa hivi, hizi kauli za wenzetu hawa wote wawili effect yake pia ni kuwachochea wananchi kuichukia Serikali. Kwa sababu kwa upande mmoja ya Mheshimiwa Gwajima ni kwamba anawachochea wananchi waone kwamba Serikali haijali afya zao, Serikali haijali usalama wao. Kwa hiyo watu wanapokea tu fedha huko wanaleta machanjo ambayo sio sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii nyingine ni kwamba Serikali ina upendeleo kwamba wengine wanakatwa kodi, wengine hawakatwi kodi. Kwa hiyo kauli zote hizi mbili zinakwenda zaidi hata ya makosa yetu ya kikanuni, kuna uchochezi hapa pia. Kwa hiyo ni vizuri kabisa Azimio hili la Bunge likapita kama ambavyo Kamati imelileta. Naliunga mkono, twende hivyo, turekebishane ili tuweze kwenda sawasawa katika kuwatumia wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja kwa mara ya pili. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kupata nafasi hii ya mwisho kuchangia. Mchango wangu ni mfupi sana.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote niungane na wote ambao wamepongeza kazi nzuri iliyofanywa na Wizara hii pamoja na changamoto nyingi ambazo tunazifahamu zinazoikabili Wizara hii lakini kwa kweli kazi ni nzuri na hata ukisoma takwimu crime rate yetu sio mbaya kama nchi zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili niungane pia na wote waliozungumza juu ya suala la hali mbaya ya miundombinu ya vitendeakazi na majengo ya polisi hata Jimboni kwangu Mwanga tuna tatizo hilo kiasi ambacho askari wetu wakati mwingine, nilipita siku moja pale kituoni nikakuta wanachangishana kupiga rangi kwenye jengo la polisi jambo ambalo lina moyo mzuri kwa kweli nawapongeza lakini tunahitaji kuwasaidia kwasabbau kimsingi sio kazi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine nishauri sasa kuhusu masuala yote yanayohusiana na ujenzi katika majeshi yetu. Kwa bahati ni kwamba Wizara hii ina nafasi ya kuwa na nguvukazi yenye ujuzi mbalimbali ambao ni wenzetu wale wafungwa. Iko teknolojia ya matofali haya ya hydra form ambayo National Housing wanafanya vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, nina hakika kabisa tukiipeleka hii teknolojia kwenye maeneo ya megereza yetu na kwa ujumla kwenye majeshi mbalimbali ambayo iko chini ya Wizara hii wana uwezo wa kutengeneza matofali na tukamaliza kabisa tatizo la ujenzi wa nyumba za askari pamoja na maeneo mbalimbali ya maofisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo pengine hata sisi tunaweza tukashirikiana ni kwamba hata tunapozungumzia hizi fedha za CSR kwenye wawekezaji mbalimbali ni vizuri pia tukakumbuka vituop vyetu vya polisi kwenye mambo ya furniture n.k. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo nilipenda kuzungumzia ni juu ya suala la majanga ya moto. Mwishoni mwa mwaka jana Jimbo langu lilipata tatizo la kuunguliwa na shule inaitwa Nyerere Sekondari, moto ambao ulitokea karibu mara tatu mfululizo ukaunguza mabweni mawili kwa kiasi kikubwa sana. Vyombo vyetu vya ulinzi na usalama viliitikia kwa haraka sana, navipongeza. Lakini nadhani tunahitaki kwenda mbele kidogo kwenye tatizo hili iwe ni sehemu ya kuwaelimisha wanafunzi wetu shuleni na kuwapatia vifaa vya kuzimia moto. Endapo wale wanafuzni wangekuwa na elimu ya kutosha ya kupambana na moto halafu wakawa na vifaa vya kisasa, nina hakika majanga haya yangeweza yakadhibitiwa kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama tuliweza kukimbia mchaka mchaka kila asubuhi tukiwa wanafuzni sidhani kama leo tukiamua kwamba kila Jumamosi tuna zoezi la kudhibiti moto, la kuzima moto kwa wanafunzi wetu sidhani kama itashindikana. Naamini itawezekana na tutaweza kuzuia haya majanga kwa sababu hata tungekuwa na magari mengi bado janga linapotokea ni vizuri wasije kuzima moto ila moto udhibitiwe, usitokee au usiendelee pale ambapo umeanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu ni mfupi tu. Naomba kuunga mkono hoja ya Wizara hii. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kupata nafasi hii. Awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na timu yake kwa kazi nzuri ambayo wamekuwa wakiifanya na majukumu mengi ambayo wanayabeba kwa umahiri na weledi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina hakika kabisa kwamba timu hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ikiendana sasa na kauli mbiu mpya ya kazi iendelee chini ya mama yetu mama Samia Suluhu Hassan ambaye tunamuombea sana Mungu amjaalie hekima na maisha marefu, nina hakika tutakwenda vizuri watatufikisha salama tunapotakiwa kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitachangia maeneo matatu. Eneo la kwanza ni juu ya suala zima la hifadhi ya jamii. Niipongeze Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii kwa muda mrefu imetufanyia kazi nzuri hasa maeneo ambayo wamekuwa mabingwa zaidi wa kuwekeza la real estate. Eneo hili ni eneo ambalo ni stable kwenye uchumi, huwa haliyumbi sana, hata likiyumba huwa linarudi sawasawa, kwa hiyo nawapongeza wamefanya kazi nzuri, wamesaidia sana suala la kuongeza makazi bora. Tunafahamu kwamba nadhani mwaka 2018 urbanization rate ilikuwa asilimia 32.6 bila kuwa na juhudi za kupata makazi bora tunaweza kuishia kukaa kwenye slums. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza na-declare interest kwamba niko kwenye Kamati ya Katiba na Sheria, kwa hiyo tulipata fursa ya kutembelea miradi ya ujenzi ya NSSF ya Dungu, Toangoma na Mtoni Kijichi. Miradi ile ni mizuri na ilibeba maono makubwa. Hata hivyo, tukiangalia hatua ambazo ile miradi mbalimbali imefikia, mbele bado ni parefu na nadhani iko haja ya Serikali kufanya intervention kusaidia ile miradi. Ushauri wangu ni kwamba kwa vile ziko fedha nyingi za kukopesha watu katika mambo ya mortgages hasa kupitia TMRC na benki zinazo hiyo fursa ya kukopesha lakini zinashindwa kwa kukosa wateja kwa sababu ya masharti kuwa makali. Ningeshauri katika hatua hii Serikali iandae stimulus package kwa ajili ya mabenki ambayo yako tayari kuwakopesha watu kununua zile nyumba. Tusipoweza kukopesha watu wakanunua zile nyumba nadhani ile miradi haitakwenda vizuri, haitatimiza makusudi yale ambayo yalikuwa yamelengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la stimulus package ni la kawaida kabisa kwenye uchumi mahali popote pale kunapokuwa na kamgogoro/kamyumbo fulani. Kwa hali hii iliyotokea tunahitaji kuziwezesha benki zetu zikopeshe watu kwa chini ya asilimia 10 ya riba ili waweze kunua zile nyumba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo ningependa kuchangia ni juu ya suala la Mahakama. Tumezunguka kama Kamati tumeona maboresho kwenye Idara ya Mahakama kwakweli upande wa majengo na TEHAMA wanafanya vizuri sana, lakini liko eneo moja ambalo labda hapo kabla sijaenda nishukuru kwamba hata katika Jimbo langu la Mwanga pia tumepata jengo la Mahakama zuri, mkandarasi anasubiriwa tu kuingia site, lakini tayari mkataba umeshasainiwa. Hata hivyo kiko kipande kimoja ambacho naona kimeachwa pembeni kwa sababu tu ya sheria na pengine kitakuja kutusumbua mbele ya safari.

Mheshimiwa Naibu Spika, iliamuliwa hapo awali kwamba, Mabaraza ya Ardhi yatolewe nje ya Mfumo wa mahakama. Kwa kweli, uamuzi huu pamoja na kwamba, umefanyika lakini haujawa na tija sana. Kwanza mabaraza haya yako machache, kuna wilaya nyingi ambazo hazina mabaraza ya ardhi ikiwa ni pamoja na wilaya yangu ya Mwanga. Ushauri wangu ni kwamba, Mabaraza ya Ardhi haya yarudishwe chini ya mahakama, ili yasiachwe nje ya haya maboresho ambayo yanafanyika yakaja kuachwa nyuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati hayo yanaendelea ni jambo ambalo linawezekana kabisa tu kwa kutumia circular la Mheshimiwa Jaji Mkuu, mahakimu wale wa mahakama za wilaya wakapewa mamlaka ya kuendelea kusikiliza masuala ya ardhi. Kama mahakama kuu imewezekana hilo hata hizi mahakama za chini inawezekana, migogoro ya ardhi ni moja ya sehemu kubwa sana inayozisumbua jamii zetu na hasa kwangu. Sisi ni wapare tunapenda na tunaweza kesi, tunahitaji baraza la ardhi pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la mwisho limeshazungumziwa na baadhi ya watu hapa, ni eneo la maafa. Yako maeneo ambayo kila mwaka yanakumbwa na maafa. Mojawapo ya maeneo hayo ni kata ambayo ipo kwenye Jimbo langu la Mwanga, Kata ya Kileo. Yako mafuriko ambayo huwa yanaanzia Mto Hona, kila mwaka wananchi wale wanapata mafuriko wanakuwa ni watu wa kusaidiwa nguo na chakula.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka huu tulifanya jitihada za kwenda kutembea mguu kwa mguu na viongozi wale madiwani wa kata ile ya Kileo pamoja na viongozi wa kata ya Jirani kwa Mheshimiwa Dkt. Kimei, Kata ya Kahe Mashariki. Tukatembea mguu kwa mguu pamoja na wataalamu kutoka Mamlaka ya Uendelezaji wa Bonde la Mto Pangani ambayo nayo ni Mamlaka inayofanya vizuri sana, tunaipongeza. Tulibaini kwamba, eneo linalohitaji kudabuliwa pale ili tuondokane na shida hii ni kilometa 1.72 ili mto ule uweze kupitisha maji mafuriko yale yakome.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka tunavyozungumza hatujaweza bado kupata grader la kufanya hiyo kazi. Wako wafadhili binafsi ambao wametusaidia tukadabua sehemu kubwa ndio ambayo mpaka sasa hivi inafanya mvua zilizonyesha tusipate mafuriko. Lakini nilikuwa naongea na Mheshimiwa diwani wa pale anasema Mheshimiwa Mbunge tuko kwenye dilemma, tuombe Mungu alete mvua au aache kwasababu, ikija tutapata mafuriko ikikosa tutakosa chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitoe mwito kwamba, maeneo kama haya yatazamwe ili maafa haya yasiwe ni suala la kila mwaka kwamba, ikifika mvua zikikaribia watu wanajijua kabisa kwamba, wanakaribia kulala nje na kupoteza vyakula. Kwa hiyo, huo ndio wito wangu kwa eneo hili ambalo liko ndani, maafa haya ambayo yanatokea kwenye Jimbo la Mwanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii. Naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia zote. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii. Awali ya yote, nampongeza sana Waziri Mheshimiwa Ummy pamoja na timu yake siyo tu kwa kuwasilisha bajeti yao vizuri sana, maana yake kwa kweli wamewasilisha vizuri, lakini pia hata kwa kazi ambazo tumeshawaona wakizifanya ndani ya muda mfupi toka wameingia kwenye nafasi hizo, nikiwatazama hawa naona matumaini kama ninavyoitazama timu yangu ya Simba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naungana na wote waliozungumza juu ya kuongezea nguvu TARURA, suala la dawa kwenye Hospitali zetu, watumishi mbalimbali na kuwaongezea uwezo pia Madiwani wetu, hayo yote nayaunga mkono kwa asillimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikija kwenye Jimbo langu la Mwanga, naomba kusema kwamba ipo ahadi ya Hospitali ya Wilaya iliyotolewa na Mheshimiwa Rais wakati wa Kampeni. Kama alivyosema Mheshimiwa Rais, Mama Samia, yeye na Mheshimiwa Hayati Dkt. Magufuli ni kitu kimoja, kwa hiyo, kwa vile Mheshimiwa Dkt. Magufuli alitoa hiyo ahadi, basi ahadi hii ni ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan na tunaiomba itekelezwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Mwanga walirukaruka sana baada ya kupewa ahadi hiyo kwa sababu ilikuwa ni kilio cha muda mrefu, wakaibana Halmashauri yao, ikatenga ekari 54 za ardhi ambazo zipo tayari kwa ajili ya mradi huo. Namkaribisha Mheshimiwa Waziri pamoja na Manaibu watuletee huo mradi.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili juu ya sekta ya afya, ni Kituo cha Afya cha Kigonigoni ambacho ni moja kati ya vituo vya mkakati. Serikali ilileta kwanza shilingi milioni 400 kikajengwa kikafikia hatua iliyofikiwa, lakini tangu hapo kimesimama. Yale majengo na vitu vingine vyote vilivyojengwa vinazidi kuharibika. Tusipomalizia kile kituo cha afya tutazidi kupata hasara na wananchi wa Kata ya Kigonigoni na maeneo yote ya ile Tarafa ya Jipendea watateseka kwa sababu walikuwa na matumaini makubwa ya kituo hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo mawili ya Jimbo langu la Mwanga, yapo mengi, lakini mengine ninaamini Mheshimiwa Waziri na timu yake watakuja kuyaona na mengine tutazungumza, nizungumze moja tu la Kitaifa. Nina imani kabisa hili suala la matumizi ya force account yanaweza yakatupeleka mbali, lakini tukitaka mafanikio makubwa kwenye suala hili ni vizuri basi Halmashauri zetu zikawa na jopo zima linalohusika na ujenzi. Lazima Halmashauri ziwe na ma-architect, ma-quantity surveyors na ma-engineer. Bila hivyo miradi hii itakuja kutupa shida baadaye.

Mheshimiwa Spika, tungependa majengo haya yanayojengwa wajukuu zetu wayakute, lakini kwa mfumo huu wa kumwachia engineer peke yake au pengine hata engineer hakuna, asimamie mradi ya shilingi bilioni moja, kwa kweli hatuwezi kufika vizuri. Wataalam wa ujenzi walitengeneza mfumo wa jopo linaloweza kusimamia kazi ya ujenzi hata mikataba ambayo inatumika kwa nchi nzima; mikataba ya FIDIC na NCC yote inazingatia kwamba lazima kuwe na jopo la hao wataalam ili kazi iende vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati tunasubiri kupata wataalam hao, Serikali inaweza kuamua kutumia bodi mbalimbali za wataalam wa hizi fani kama CRB, AQRB, ERB hizo zote zinaweza zikaratibu kwa kutumia wataalam waliopo kwenye zone mbalimbali ili kuhakikisha miradi hii inasimamiwa vizuri ili tuweze kupata value for money.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, Wizara hii ni moyo wa maendeleo, yapo mengi ambayo tunaweza tukasema, lakini kwa timu hii ambayo Serikali imetupatia, tunaamini watakuja huko kuyaona ili tuweze kufanya mambo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 –Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi hii ya kuchangia hoja ya Wizara ya Katiba na Sheria. Nianze kwa kuishukuru na kuipongeza sana Wizara kwa wasilisho zuri, nina imani kabisa kwamba mwalimu wangu, Mheshimiwa Prof. Kabudi, pamoja na timu yake, watakwenda vizuri katika kuiendesha Wizara hii ambayo inabeba sehemu kubwa sana ya maisha ya kila siku ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipongeze pia Wizara ya Katiba na Sheria kwa ajili ya maboresho mbalimbali ambayo yamefanyika ya kutenganisha ile Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Mwendesha Mashtaka. Naamini kabisa kwamba hatua hii italeta ufanisi mkubwa sana kwa sababu itakuwa imepunguza mzigo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nipongeze pia maboresho ya miundombinu ya Mahakama, hasa suala la majengo. Nadhani tumemaliza wakati ule sasa wa kuona kwamba Mahakama lazima zikae kwenye majengo machakavu na yaliyochoka, sasa yanajengwa majengo mazuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru hata katika Jimbo langu la Mwanga ujenzi wa Mahakama ya Wilaya umeanza, tunasubiri sasa kama ambavyo wenzetu wa Kamati ya Bajeti wameomba kwamba sasa Mahakama za Mwanzo ziboreshwe kwa sababu ndiyo zipo karibu zaidi na wananchi. Hivi sasa kwa vile Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo wanapelekwa wale wenye shahada, naamini kabisa mambo sasa yatakwenda vizuri na Mawakili watakwenda, haki itatendeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini bado ziko changamoto na malalamiko mengi sana juu ya suala zima la utoaji haki, hasa katika maeneo haya ambayo yamekuwa yakilalamikiwa ya watu kuwa na kesi ambazo hazina dhamana na hizi kesi za utakatishaji fedha ambazo watu wengi wanazilalamikia. Mara nyingi malalamiko haya yanapotokea watu wanalaumu kwamba sheria ni mbovu lakini kuna wakati fulani Mheshimiwa Jaji Mkuu Mstaafu, Mheshimiwa Barnabas Samatta, aliwahi kusema kwamba tunahitaji zaidi Mahakama imara kuliko sheria kali. Sheria zinaweza zikawa kali sana lakini kama hatuna Mahakama ambayo iko thabiti ikatusumbua.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mahakama yetu ni nzuri, ina uwezo mkubwa sana na mimi nimefanya nao kazi muda mrefu lakini hapa katikati Mahakama yetu imeingiwa na katatizo fulani, Mahakama yetu imeishiwa na wivu. Nasema hivyo kwa sababu wote waliosoma sheria wanafahamu iko kanuni moja inayotumika katika sheria inasema kwamba The Court must be jealous of its jurisdiction (Mahakama lazima iwe na wivu na mamlaka yake). Hata hivyo, hapa katikati Mahakama imekosa wivu na mamlaka yake, imeachia mamlaka yake ifanywe na watu wengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, utakuta shauri linakuja Mahakamani, ile Sheria ya Utakatishaji Fedha inasema kabisa kwamba lazima kuwe na kosa la msingi halafu ndiyo la money laundering lifuate. Hata hivyo, shtaka la money laundering linakuja, Mahakama inaona kabisa kwamba hapa siyo sahihi na wale washtakiwa wanalia na kuomba kwamba jamani mbona hapa hakuna kesi ya money laundering, lakini zinaendelea na zinaendelea kuumiza watu. Ukweli wa mambo ni kwamba Mahakama hapa inatakiwa ikae kwenye sehemu yake ili twende mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Ibara ya 107A ya Katiba ya Jmahuri ya Muungano wa Tanzania, imeipa mamlaka Mahakama kuwa ndiyo yenye kauli ya mwisho pale ambapo kunakuwa na jambo lolote linalolalamikiwa. Sasa Mahakama irudi kwenye nafasi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo suala hili kwa mfano la certificate ya DPP inayozuia dhamana. Mahakama inafahamu kabisa kwamba mkija Mahakamani watu wawili, mmoja ni DPP ambaye ni mshtaki na mshatakiwa, hawa watu wote wawili wako sawa mbele ya Mahakama ili iwaamulie shauri lao. Sasa mmoja anatoa wapi mamlaka ya kumzuia mwenzake asipate dhamana kwa certificate? Yule analalamika kwamba jamani huyu mwenzangu ni party, yaani amekuja mbele ya Mahakama kama mimi; anapata wapi yeye mamlaka ya kunizuia mimi dhamana kwa certificate? Sheria kweli inaweza ikawa inampa mamlaka lakini sheria inayompa mamlaka haizidi Katiba, Mahakama bado ina uwezo kabisa wa kuingilia kati na kusimama kwenye nafasi yake na kuweza kutenda haki. Sisemi kwamba lazima wapewe dhamana, lakini kama wananyimwa wanyimwe na Mahakama.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tadayo.

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, naam.

NAIBU SPIKA: Kaa kidogo.

Waheshimiwa Wabunge, napata changamoto kidogo na mchango wako maana unauzungumzia Mhimili wa Mahakama na kwamba kuna mambo mhimili ule haufanyi sawasawa. Sasa kwa taratibu tulizonazo humu ndani, Serikali huwa inasemwa kwa sababu inao hapa watu wa kuisemea, sasa tukiingia huko kwenye kuisema Mahakama kwa namna ambavyo unachangia, ni tofauti na kama ungekuwa unatoa ushauri kwamba kuna jambo fulani labda unaona liko hivi.

Kwa sababu ikiwa kuna watu ambao wameonewa na Mahakama wote tunafahamu utaratibu; unakata rufaa kulekule Mahakamani. Kwa sababu ukiileta kesi ambayo iko kule, mtu hakutendewa haki kule, ukaileta hapa Bungeni, hapa Bungeni siyo chombo ambacho Kikatiba kimewekwa kusikiliza mashauri ambayo Mahakama haijafanya sawasawa.

Sisi wenyewe tumeapa hapa kuilinda Katiba, kwa hiyo, kama ambavyo sisi Wabunge hatutegemewi huko nje tukaanze kujadiliwa kwa namna fulani hivi, ni vilevile mihimili mingine pia haiyumkiniki. Kama sheria ina shida, ni kazi yetu sisi kubadilisha sheria, siyo kazi ya Mahakama, ni kazi yetu sisi.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Tadayo, mwanasheria mbobezi kabisa, hebu jielekeze mchango wako kwa mipaka ile ambayo tunawekewa na Katiba yetu.

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa maelekezo yako na nayapokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo napenda kulizungumzia, nilishawahi kulitaja tena hapa Bungeni ni juu ya suala la Wizara mbili kuzungumza, Wizara ya Sheria na Wizara ya Ardhi ili Mabaraza yale ya Ardhi yaweze kurudi chini ya Mhimili wa Mahakama. Nasema hivyo kwa sababu ukienda Mahakama Kuu, pamoja na kwamba kuna Kitengo cha Ardhi ambacho kilianzishwa lakini pia Mahakama Kuu hii ya kawaida inapokea mashauri ya ardhi. Sasa tunapata changamoto kwenye zile Wilaya ambazo hazina Mabaraza ya Ardhi ambazo ni nyingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu ni kwamba Wizara hizi mbili zizungumze ili mashauri ya ardhi yaweze kusikilizwa kwenye Mahakama za kawaida kupunguza mzigo mkubwa wa mashauri ya ardhi ambayo ndiyo yanayoleta matatizo na changamoto nyingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikifika hapo naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja; ahsante sana kwa nafasi hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru kwa kupata nafasi hii ya kuchangia na hasa kupata nafasi ya kuzungumza baada ya Mheshimiwa Mchafu kuzungumza ili tu uniruhusu nimpe kataarifa kidogo kwamba tutakapocheza Simba na Arsenal tutawafunga sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa wasilisho zuri lakini niipongeze zaidi Kamati kwa sababu wasilisho lao limesaidia hata uchangiaji wetu kwenda vizuri. Wamefanya kazi nzuri sana. Amesema mambo mazuri sana katika hoja ya Wizara hii. Nizungumze machache sana nikianzia hasa yanayohusiana na Jimbo langu la Mwanga. Sehemu ya ninachotaka kuzungumza, kimeguswa juu ya mawasiliano katika maeneo ya mipakani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Mwanga lina Kata 20 na katika hizo, Kata 6 ziko kwenye maeneo ya mipakani na pengine kwa kumbukumbu nikizitaja tu. Kuna Kata ya Kileo, Kivisini, Jipe, Kigonigoni, Kwakoa na Kata ya Toloha. Zaidi ya nusu ya maeneo haya ukiingia na simu yako ya mkono kuna mahali unafika unaambiwa karibu Safaricom, sasa Safaricom na haya ma-bundle ya vijana wetu akifika kule hapati mawasiliano. Ni kijana wa bodaboda alikuwa kule, mteja wake anamtafuta hampati, wanapoteza income. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani wenzetu wa TCRA wanapotoa leseni pia wana jukumu la kufuatilia mambo ya udhibiti ubora. Wasiachie haya makampuni yanawekeza kule halafu hawajali juu ya ubora wa huduma zao wanazozitoa kule wanaendelea kutuumiza. Hili jambo nashukuru kwamba Mheshimiwa Ndugulile alishaanza kunong’ona na sisi Wabunge ambao tunatoka kwenye maeneo ya mipaka naamini kabisa kwamba atalitilia mkazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko kata nyingine ya Mlimani ambayo kuna mnara wa Halotel lakini ule mnara unatumia solar, sasa kule kwetu ni kama Uswisi. Wakati mwingine hatuoni jua kutwa nzima. Kwa hiyo, siku kama hakuna jua basi na mawasiliano hakuna. Mimi sidhani kampuni kubwa kama ile inasubiri umeme wa REA, wavute nguzo ziende pale ili mawasiliano yaweze kupatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi tu baada ya hapo nije tu kwenye hoja moja ya Kitaifa ya TTCL ambayo imezungumzwa sana na ninasema hivyo kwa sababu ilani yetu ya Chama Cha Mapinduzi ukurasa wa 96 imezungumzia juu ya kuwekeza kwenye shirika hili la mawasiliano. Shirika hili tunapozungumzia juu ya kulifufua, kupata National Telecom, nafikiri ni sawasawa na tulipokuwa tukizungumzia habari ya kupata National Carrier ATCL, kwamba ni jambo la muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda katika nchi nyingi, mashirika haya, hizi National Telecoms ni mashirika makubwa sana ukianzia Egypt Telecom ni shirika kubwa tu, ukienda BOTNET Botswana ni shirika kubwa, China Telecom ndiyo usiseme na Ethio Telecom ya Ethiopia, turnover yake kwa taarifa za 2020 ilikuwa ni dolla bilioni 1.35. walipoelekea tu kutaka kutoa asilimia 45 ya hisa wawekezaji walifoleni pale kwa sababu ni shirika ambalo lina tija kubwa sana. TTCL, halikadhalika tukiwekeza kwa ile miundombinu ya msingi ambayo tayari ilikuwepo, tukiwekeza na kuiboresha inaweza ikawa kampuni kubwa, ikaleta ajira nyingi na ikaleta kodi nyingi ukiacha faida nyingine nyingi ambazo zimezungumzwa hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulizungumza kidogo hapa, kuna watu walitaja juu ya uwekezaji kwenye Sekta hii ya Mawasiliano. Hawa watu walionunua TIGO na ZANTEL, Exim nilisoma kwenye gazeti la East African, lazima nikiri hii ni taarifa ya kwenye gazeti wana mpango wa kuwekeza mbali na fedha walizonunulia, wanawekeza dola milioni 400 ndani ya miaka mitano kufufua haya mashirika. Kwa hiyo, ni dhahiri kwamba sisi tukizungumzia uwekezaji mdogo mdogo tutaendelea kucheza hapa hili shirika halitafufuka na tutaendelea kupata hasara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema mchango wangu ni mfupi kwa sababu mengi yamezungumzwa. Naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi hii, awali ya yote nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Dada yetu Balozi Liberata Mulamula, Naibu Waziri, Balozi Mbarouk Nassor pamoja na wajina wangu, Katibu Mkuu Balozi Joseph Sokoine na timu nzima ya Wizara kwa kazi nzuri ambayo kwa muda mfupi toka wameaminiwa wameifanya na tumeiona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pongezi hizi lazima zitanguliwe na pongezi na shukrani kubwa kwa Mheshimiwa Rais Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo wameonesha uwezo mkubwa sana na nia ya kushungulikia masuala ya kidiplomasia na kukuza diplomasia ya nchi yetu. Hata uteuzi wa mabalozi uliofanyika hivi karibuni ni ishara tosha kwa sababu uteuzi huu umefurahisha watu wengi kutokana na jinsi ambavyo umefanyika kwa umakini na kwa wigo mpana wa kuwagusa watu wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu kwa miaka mingi imekuwa na sauti kubwa sana kwenye mambo ya kimataifa hasa upande huu wa Kusini mwa Afrika kutokana na mambo mawili; kwanza, historia yetu na pili msimamo wetu ambao tumekuwa nao katika mambo yanayohusiana na haki na mambo mengine ya kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi ni waasisi wa SADC ambayo ilianzia kwenye Umoja wa Nchi Tano za Mstari wa Mbele, sisi ni waasisi wa African Union ulioanzia kwenye OAU pamoja na East Africa na hata katika masuala ya Pan Africanism umajumui Afrika nchi yetu ilikuwa mstari wa mbele na tumeaminika na kuheshimika kwa hilo. Tunaiomba Wizara iendelee kuratibu ushiriki wetu katika jumuiya hizi ili sauti yetu iendelee kuwa pale pale na sasa hivi tuna nguvu kubwa zaidi kwa sababu tuko katika uchumi wa kati, kundi ambalo najumuisha karibu asilimia 75 ya population ya dunia tunapokuwa pale na sauti yetu tunakuwa na nguvu zaidi kuliko hata ambayo tulikuwa nayo mwanzoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi na uteuzi mzuri wa mabalozi ambao unafanyika ingawa bado hawajapelekwa kwenye nchi mbalimbali, lakini tuendelee tu kusisitiza vigezo na masharti kwamba mabalozi wetu wanakokwenda huko ni muhimu wakazingatia kwamba either huko waliko watuletee wawekezaji au watuletee masoko au fursa za elimu au ajira zote za chini na za kibigwa pia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu si kila balozi ataleta wawekezaji kwa sababu pengine nchi halioko haina wawekezaji wengi ambao tunawahitaji, lakini kutakuwa na masoko, kutakuwa kuna ajira au kutakuwa na fursa za elimu nina amini kabisa nchi yetu haiwezi ikafungua ubalozi mahali ambapo hakuna fursa, tunachohitaji ni kwamba mabalozi wetu watutangulie katika kuhakikisha kwamba fursa hizo tunazipata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tusiwe watu tunasisitiza tu kwamba tutowe permit haraka haraka kwa watu wafanye kazi kwetu, lakini je, sisi kwenda kufanya kazi kwenye maeneo mengine. Uniruhusu nitaje tu kwamba mimi binafsi nafurahishwa sana na utendaji wa balozi wetu alioko China, tunaona jinsi ambavyo anashughulika na matokeo tunayaona, naamini kabisa mfumo huo ukienda namna hiyo tutaendelea kufaidi Zaidi katika diplomasia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu ni mfupi ninzungumze moja tu la mwisho juu ya Chuo chetu cha Diplomasia. Tunafahamu kwamba chuo kile kilikuwa hakidahili sana wanafunzi kutoka nje kilikuwa ni zaidi ya kukuza uwezo wa ndani, lakini hivi karibuni kimekuwa kikidahili wanafunzi wengi hata vijana wanaotoka Jimbo langu la Mwanga wengi wanasoma pale na wengine wameshasoma pale tayari. Kwa hiyo, ipo haya ya kukiongezea nguvu ya miundombinu pamoja na walimu na rasilimali zingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo Lingine ambalo linasumbua kidogo kwenye chuo kile ni kwamba vijana wanapokwenda field kuna tatizo kubwa sana ya kupata nafasi sehemu ambazo ni relevant.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu taratibu za ki-protocol ambazo zinafanya vijana hawa wasipokelewe kwenye balozi kufanya field, lakini mimi ningeshauri Wizara au Serikali i-negotiate na hizi balozi ili vijana wetu waweze kwenda kufanya field katika hizi balozi ili waweze kupata hasa uzoefu wa kile ambacho wanakisomea, si lazima tuanze na balozi zote tunaweza tukaanza na balozi chache kama za East Africa Community au za SADC ili vijana wetu wanaposoma waweze kutoka vizuri zaidi kwa kufanya mazoe katika mambo ambayo wanayasomea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naunga mkono sana hoja ya Wizara hii na nasisitiza kama walivyosema wenzangu kwamba Serikali itoe fedha kama ambavyo zimeombwa na zitakavyopitishwa kwenye bajeti ili Wizara iweze kutekeleza majukumu yake, ahsante sana na naunga mkono hoja (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JOSEPH A. THADAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kupata nafasi hii la kwanza niungane na wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri Katibu Mkuu pamoja na timu nzima ya Wizara kwa dhamana kubwa hii ambayo wamekabidhiwa ya Wizara hii nyeti kwa ajili ya mapato ya nchi yetu ajira na kuitangaza nchi yetu nje. Wanafanya kazi nzuri na kwa kweli tuna kila sababu ya kuwapongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu ya Awamu ya Tano na ya Sita imetumia nguvu nyingi sana katika kutangaza utalii jambo ambalo hapo kale pengine halikuwahi kufanyika sawasawa na kwa sasa naamini kabisa kwamba duniani hakuna asiyejua kwamba Kilimanjaro iko Tanzania, Olduvai Gorge iko Tanzania na Fukwe za Zanzibar zenye Dolphins wengi ziko Tanzania, pamoja na Serengeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili pia tuipongeze Bodi ya Utalii chini ya Mheshimiwa Jaji Mstaafu Thomas Mihayo, walionekana kabisa kuwa kutumia nguvu ya ziada kwenye hili, tunawapongeza sana. Juhudi hizi zisipunguzwe kwa sababu washindani wetu bado wako kazini. Hii ni sawasawa tu na vita ya kiuchumi, kwa hiyo tuendelee kujitangaza kwa nguvu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nisiache kuzungumzia suala la tembo kwa sababu Jimbo langu la Mwanga liko katika mazingira magumu zaidi kwa sababu liko katikakati ya mbuga mbili, upande mmoja kuna Mbuga ya Tsavo ya Kenya na upande wa pili kuna Mbuga ya Mkomazi. Naishukuru sana Wizara, Naibu Waziri alitutembelea. Alifanya kazi nzuri sana na kwa kweli niwashukuru wananchi wangu wa Mwanga pamoja na viongozi wote wa Chama na Serikali, walijitokeza kwa wingi na kimsingi wananchi wa Mwanga wamekubaliana na wito wa kuwa wadau wakubwa sana wa hifadhi na kazi inaendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yako mambo matatu ambayo wananchi wa Mwanga wanayatarajia. La kwanza, ni kuongezewa idadi ya Askari wa Wanyamapori ili angalau waweze kuvuna vile walivyovipanda na pia watoto waweze kwendaa shule, ahadi hiyo ilitolewa na tunaamini itatekelezwa. La pili, ni kufungua lile lango la la Kaskazini kwenye Mbuga ya Mkomazi kwenye maeneo ya Kata ya Toloha, ambayo kwa kweli wananchi wa Mwanga wanaisubiri kwa hamu na wameshajiandaa kwa ajili ya fursa za biashara zitakazotokana na lango lile la pale. La tatu, ni kwamba bado wananchi wa Mwanga wanaona kwamba watafiti wetu, Vyuo Vikuu vyetu pamoja na wataalam bado wanacho cha kutuambia juu ya tatizo hili la tembo.

Mheshimiwa Naibu Spika, yako mambo ambayo Serikali imefanikiwa tu, kwa mfano; tatizo lile la majani yaliyokuwa yanaota kwenye mbuga ambayo siyo mazuri, yalimalizwa kitaalam na kitafiti na hali inaendelea vizuri sana. Sasa kwa vile tumeshajua kwamba kinachowatoa kule tembo ni nini kuwaleta huku, basi tuwajengee mazingira ili waendele waweze kuendelea kukaa kule. Kama yako aina ya malisho ambayo inawafanya watoke kule, naamini yanaweza yakapandikizwa huko huko kwenye mbuga ili waendelee kukaa kule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia liko suala la matumizi ya electronic fence ambacho taarifa nilizonazo ni kwamba pale Tsavo National Park wenzetu wameweka electronic fence upande unaoelekea kwenye maeneo ambayo hawataki tembo waende, ndiyo maana wanakuja kwa wingi huku. Hata ukienda Amboseli National Park kuna maeneo mawili wametumia electronic fence moja linaitwa Namelok, ambalo limefanikiwa sana na fence nyingine inaitwa Kinama bado inachangamoto, lakini inaendelea kufanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachoamini ni kwamba watafiti wetu; Vyuo vikuu vyetu na wataalam wetu, wakiingia kazini sawasawa, bado tunao uwezo mkubwa sana wa kuweza kupata suluhisho la kudumu kuliko kutegemea hizi measures ambazo ni kama za dharura za kushughulikia jambo kama hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nasoma utafiti wa Cambridge University kwenye journal yao moja online, wanasema hata suala la kutumia nyuki bado lina changamoto, tena walifanyia utafiti mwaka 2018 kwenye Hifadhi ya Udzungwa, bado lina changamoto. Kwa hiyo nadhani, watafiti wetu wanapaswa kuingia kazini zaidi ili kusaidia juhudi hizi za Serikali nazo zifanywe katika kuzuia hili tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sina zaidi ya hapo, naunga mkono hoja, Wizara inafanya kazi nzuri, Serikali iwape fedha walizoomba ili waweze kutekeleza majukumu yao. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Pili wa Bunge
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kupata nafasi hii ya mwisho ya kufunga jamvi la uchangiaji. Awali ya yote niishukuru na kuipongeza sana Serikali kwa jinsi ambavyo imeendelea kuziongezea nguvu Mamlaka za Serikali za Mitaa na bajeti hii inashuhudia hayo, kwa hiyo, kwa hilo nipende kuwapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kuongezea nguvu Serikali za Mitaa ni pamoja na suala hili la by-laws ambazo tunazizungumzia leo, kwa hiyo niwapongeze sana Kamati husika, wasilisho lao limekuwa zuri na ambalo nadhani pia limerahisisha uchangiaji wetu kwa siku hii ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni wazi kabisa kwamba taarifa ya Kamati imeonyesha umuhimu mkubwa sana wa kuziongezea uwezo mamlaka zinazohusika na utungaji wa hizi wa hizi by- laws na kwa sababu Mwanasheria Mkuu wa Serikali yupo hapa na amesikia na hili niseme kwa nidhamu kwa sababu kwa taratibu zetu huyu ndiye wakili namba moja au msomi namba katika nchi, kwa hiyo, sisi wote tukimkuta huwa tunampisha kiti kwanza, naamini kwa vile yupo hapa na amesikia basi hiyo kazi itafanyika. Sheria ndogo ni muhimu siyo kwa uchumi wa nchi tu, lakini hata katika kulinda utulivu wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo la sheria ndogo lipo kwenye kukinzana na sheria mama, lakini pia kupatikana kwa ule murua na sheria zingine zinazohusika, ile harmonization. Nitoe mfano, kwenye Jimbo langu la Mwanga sisi tunategemea sana mapato kwenye chanzo kimoja kinachoitwa madini ya ujenzi hasa mchanga. Ilitungwa ile Sheria Ndogo ya Ada na Ushuru ya Halmashauri ya Wilaya ya Mwanga ya mwaka 2019 ambayo ilizipa halmashauri mamlaka ya kukusanya mauzo pamoja na ushuru kwenye hivi vyanzo vya madini haya ya ujenzi na hilo linaendelea kufanyika. Sasa hilo limefanyika bila kuangalia upande mwingine wa sheria ya madini ambapo Kamishna wa Madini anayo mamlaka ya kutoa hizi primary mining licenses kwa watu binafsi hata kwa mamlaka hata kwa vijiji.

Kwa hiyo, utakuta kweli Halmashauri ina mamlaka hayo chini ya by-law, lakini wapo watu ambao wanazo primary mining licenses kwenye maeneo yao. Kwa hiyo, hapo sasa kunakuwa na mgongano kwamba mimi nina leseni mbona wewe unakuja kukusanya hapa. Kwa hiyo, hilo linahitaji sana kutazamwa tusitazame tu zile sheria mama, lakini pia tutazame pia hizi sheria zingine ambazo zinahusika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, limesemwa vizuri hapa suala la rumbesa, kwa tatizo la rumbesa linatoka wapi! Tatizo la rumbesa linatokana na Sheria ya Vipimo (Weights and Measures), rafiki yangu, Mheshimiwa Shangazi atakubali kule kwake wanalima viazi sana, by-laws inasema rumbesa hapana, lakini ile Sheria ya Vipimo yenyewe inazungumzia juu ya uzito kwamba kilo 100 bila kujali imejaa mpaka wapi as long as ni kilo 100 imetimiza sheria. Sasa swali linakuja kwamba hivi gunia ni kipimo au ni kifungashio? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hawa wengine sasa huko kwenye barriers sasa/kwenye vizuizi vya barabarani, ndio wanachukua sasa faida hapo wakifika hapo wanaweza kukubabaisha. Kwa sababu upande mmoja anaweza akasimama na by-laws, upande mwingine akasimama na Sheria ya Vipimo. Sasa wewe hapo katikati ndio unakuwa uko katikati ya nyundo na msumari unaendelea kuumia.

Mheshimiwa Spika, nikirudi nyuma kidogo ni kwamba hizi by-laws zinapotoa mamlaka fulani, lazima pia ziende kubana hizi Halmashauri kwenye suala la matumizi; kwa mfano kabla ya mwaka 2019 kwenye Jimbo langu vijiji vilikuwa vinakusanya mapato na ushuru wa mchanga kwenye vijiji kule, sasa ikachukuliwa na Halmashauri, lakini bado suala la kuzibana halmashauri kuhakikisha kwamba, ile asilimia 40 inarudi kwenye shughuli za maendeleo za maeneo husika yanayoonekana, sio tu tusikie sikie tu kwamba hapa sijui kuna gharama fulani ilitumika, no. vitu ambavyo vinaonekana na vitu tangible hilo bado halijafanyika vizuri. (Makofi)

Sasa hilo linaleta ile resistance kwamba watu wanaona kama vile wamenyang’anywa mapato yao, lakini kwa sababu hawaoni kile kinachorudi wazi. Kwa hiyo, nadhani nguvu inayotumika kwenye kukusanya, pia itumike katika kuhakikisha kwamba ule wajibu wa kurudisha yale mapato nyuma kwa wale wananchi unatekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi kama mchangiaji wa mwisho siwezi kuwa na mengi sana ya kusema, labda tu nimalizie kwa kusema kwamba yapo mambo mengine ya kisera ambayo yanatakiwa yatangulie kwanza kabla ya by-law. Kwa mfano, tuna tatizo la kutenga maeneo ya malisho, ya mifugo na maeneo ya wakulima. Leo hii ukitunga by-law kabla ya sera ya matumizi bora ya ardhi ile by-law lazima italeta mgogoro tu. Kwa hiyo, zitangulie kwanza hizi sera husika ziweze kupitia katika michakato na zikubalike halafu, ndio twende kwenye by-law hapo zitatekelezwa vizuri. Suala la kutimiza sheria bila shuruti tutaliona kwa vizuri zaidi, kuliko sasa hivi ambapo inaonekana wakati mwingine kama ni vita kati ya wananchi na mamlaka zetu husika. Vinginevyo kwa kweli mimi niendelee kushukuru kwamba hasa katika bajeti hii mamlaka hizi za Halmashauri zimepewa nguvu ya kutosha. Kwa hiyo, sisi kama sehemu ya Mabaraza ya Madiwani tukitimiza wajibu wetu, nina hakika tutakwenda vizuri na wananchi wataona faida ya ushuru na tozo mbalimbali ambazo wanalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Tatu wa Bunge na Mkutano wa Nne wa Bunge pamoja na Kanuni za Uvuvi za Mwaka 2009
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii. Awali ya yote niipongeze sana Kamati, kwa kweli taarifa ya Kamati ni nzuri sana, imeturahisishia kazi na imetufungulia vizuri jinsi ya kuchangia. Kamati imefanya kazi nzuri, tunaipongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo napenda kusema ni kwamba sheria ndogo ni sheria kama sheria nyingine. Kwa bahati zenyewe zinagusa zaidi maisha ya kila siku ya wananchi. Kwa hiyo tunapozungumzia juu ya utungaji wa sheria ndogo nadhani tunahitaji kuwa makini sana kwa sababu zina umuhimu kwa vile zinagusa maisha ya kila siku ya wananchi. Kwa hiyo hata tunapozungumza suala la utawala wa sheria, ambayo katika hiyo pia nataka kutumia nafasi hii kuipongeza Serikali, suala la sheria ndogo ni sehemu ya sheria kwa hiyo utungwaji wa sheria ndogo nzuri na usimamizi wake unachangia sana katika suala la utawala wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema naipongeza Serikali kwa sababu ukiona utulivu mitaani, haiwezi kuwa asilimia 100 ya utulivu, lakini ukiona hali ya utulivu mitaani, ukiona haya mambo ya kukua kwa uchumi na mambo mengine yote, hayo yote yanatokana pia na kuwepo kwa utawala wa sheria kwa sababu kila jambo ambalo linafanyika linapaswa lifanyike kwa mujibu wa sheria. Sasa ni sheria za namna gani, ndiyo hili ambalo tunalizungumza kwamba lazima ziwe ni sheria bora ambazo zimezingatia viwango katika utungaji wake na zinaweza kusimamiwa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama nilivyosema, kwamba Kamati imezungumza mambo mengi mazuri na wachangiaji wamezungumza vizuri, nizungumzie labda mambo matatu tu. La kwanza ni jambo ambalo limesisitizwa juu ya hizi sheria ndogo kuzingatia sheria mama na kuzingatia Katiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli yako mambo mengine ambayo ukiyatazama unaweza ukafikiri ni madogo, lakini yanatisha kidogo. Kwa mfano hili suala la ombaomba ambalo kumekuwa na utaratibu wa kusema haya, wamekamatwa warudisheni kwao. Sasa unajiuliza kwao ni wapi? Maana Katiba ya Nchi inasema una haki ya kuishi mahali popote ilimradi huvunji sheria. Sasa nikivunja sheria hapa Dodoma nitahukumiwa tu, lakini sitaambiwa nirudi kwetu. Sasa hii ya kusema warudi kwao, najiuliza hivi kwao ni wapi? Kwa hiyo nadhani hizi sheria ndogo kuna haja ya kuzipitia kila wakati kuhakikisha kwamba hazivurugi mambo katika misingi kama hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni kuzingatia uhalisia pamoja na utafiti. Kwa mfano, kwenye Jimbo la Mwanga, kuna Bwawa la Nyumba ya Mungu pale; sheria na hata ukisoma kwenye leseni zao wanasema kwamba huruhusiwi kuvua samaki ambaye ukubwa wake ni chini ya inchi tatu. Sasa kwa miaka karibu 20 pale sasa hivi samaki wa pale hawavuki inchi tatu, wako hivyohivyo, wanataga mayai, wanajukuu hivyohivyo wakiwa wadogo. Kwa hiyo ina maana ukiamua kufuatisha hiyo sheria ni kwamba pale mahali hapatavuliwa kabisa na ukiifuatisha matokeo yake kila siku tutakamata wavuvi haramu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wavuvi haramu nasema kwenye inverted commas kwa sababu nashindwa kusema ni haramu wakati ambapo huwezi kupata halali kwa vile samaki hawavuki kile kiwango. Ndiyo maana nikasisitiza kuangalia uhalisia na utafiti, kwamba sasa hapa tumefika mahali ambapo hatuwezi kupata hao samaki ambao umewaweka kwenye leseni.

Kwa hiyo, ni lazima kuwe na exemption kwa sababu haiwezekani sheria hiyohiyo ika-apply Ziwa Victoria, iende Ziwa Tanganyika, bado iende kwenye kabwawa kadogo kama kale ka kwangu ka Nyumba ya Mungu. Kwa hiyo kuzingatia uhalisia na pia utafiti wa mara kwa mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu; ni vizuri by-laws zetu nyingi zikawa zinazingatia kwenye kuwezesha kuliko kuzuia. Nitoe tu mfano, hapa katikati kulikuwa na shida kubwa sana kwamba mtu alikuwa anakatazwa hata kukata mti ambao aliupanda yeye mwenyewe. Sasa unarudi kwenye Katiba ya Nchi, kwamba mtu ana haki ya kupata kipato halali kutokana na kazi halali aliyoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mtu amepanda mti wake ili ukiiva auvune apeleke mtoto wake shule, siku ya kuukata unamkataza kwa sababu ya sheria. Nadhani sheria zingekuwa zimesisitiza zaidi kwenye kuwezesha upandaji wa miti ili tusije kugombana na mtu anayekata kamti kake kamoja shambani wakati kuna maeka na maeka ya maeneo ambayo haya miti ambayo yangeweza yakawekewa sheria yakapandwa miti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani tukizingatia hayo; kwanza tukizingatia huo uandishi bora uliozungumzwa na Kamati, tuzingatie kwamba hizi by-laws zifuate sheria mama, zifuate Katiba; pili, utafiti pamoja na uhalisia; na tatu, kwenda kwenye uwezeshaji zaidi kuliko kuzia, nadhani tutakwenda vizuri na faida ya sheria ndogo tutaiona na utulivu wa nchi utaendelea kuwa vizuri na watu wataendelea kufaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ya kwangu ni hayo mafupi, nashukuru kwa nafasi. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Naungana na wenzangu kuwapongeza Wenyeviti wa Kamati zetu pamoja na Waheshimiwa Mawaziri, wataalam na wadau wote ambao tumeshirikiana nao kwenye Kamati zote kufanya hii kazi, pia kipekee na kwa upendeleo, wale ambao wanaangukia kwenye Kamati yangu ya Katiba na Sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jambo ambalo liko wazi kwamba pamoja na majanga yote ya kidunia na nini lakini uchumi wa nchi yetu umeendelea kukua na Mheshimiwa Raisi Mama Samia Suluhu Hassan katika Awamu yake ya Sita amekuja na kauli moja ya kusema kwamba tunaifungua nchi yetu kwa ajili ya kukuza uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli hii sio kauli ndogo, ni kauli kubwa sana; na mimi ninachofurahia juu ya Wizara na wadau wote wanaoingia kwenye Kamati ya Katiba na Sheria ni kwamba wamejitahidi kufanya kazi kubwa sana katika kupata mambo mawili; jambo la kwanza kujenga mazingira katika kuifungamanisha nchi yetu na dunia kwa sababu ndiko teknolojia na mitaji iliko, lakini pili kujenga mazingira ya sisi wenyewe Watanzania kwenda na hiyo hali mpya ya kujifungamanisha na dunia. Kwa sababu unajua unapofungua dirisha hewa iingie hata papasi na panzi huwa wanaingia kwa hiyo lazima pia ndani ujipange, ukishajifungamanisha na dunia yako mengi yanayoingia kwa hiyo lazima ujipange kwenda nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hapa nazungumzia mfano wa taasisi zetu za usalama kazini; OSHA na Workers Compensation pamoja na hifadhi ya jamii (pension). Taasisi hizi zimefanya kazi nzuri na hata ukizipima kwenye vigezo vya blue prints wametekeleza kwa kiwango kikubwa sana na ndio maana kama taasisi ya OSHA imeweza kujifikisha kwenye viwango vya kimataifa kiasi cha kuweza kupata dawati katika mambo ya usalama kazini pale SADC, hii ni hatua kubwa ambayo kwa kweli tunapaswa kuiona kwamba taasisi imetuwakilisha vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, OSHA ikifanya kazi yake vizuri, majanga yakapungua mahali pa kazi, mzigo unapungua Workers Compensation kwenye fidia, kwa sababu kunakuwa hakuna ajali ajali. Mzigo ukipungua kule wale wanapata nafasi ya kuwekeza na kwa ajili ya kukuza uchumi wetu. Hali kadhalika watu wa pension wakifanya kazi zao vizuri inaongeza ufanisi kwenye kazi na inapunguza hata matatizo ya rushwa kwa sababu wakati mwengine ufanisi na mambo ya kudaidai rushwa pia yanatokana na hofu ya kustaafu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu anajiuliza fine nafanya kazi leo nna mshahara mzuri lakini nikishaafu kesho itakuwaje. Kwa hiyo kama kuna taasisi hizi za hifadhi za jamii ambazo zipo stable hiyo pia zinatusaidia hata katika mambo kama haya ya kupunguza rushwa na kuongeza ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa kweli kwa kipindi hiki cha mwaka mmoja ambapo tumepata fursa ya kuziangalia taasisi hizi, kazi imefanyika vizuri na tunazipongeza na tunadhani kwa viwango vya blue print na viwango vingine wanapaswa kuigwa kwa ufanisi mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa sekta wa utoaji haki; Mahakama, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu pamoja na DPP pia wamefanya kazi nzuri, zipo changamoto za upungufu wa watumishi pamoja na masuala ya kibajeti, hali hiyo sasa ni jukumu letu kushirikiana nao kwamba wakati wa bajeti ikija tuwapitishie bajeti nzuri kwa sababu wameshaonyesha uwezo wa kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata sheria ambazo tumezipitia, tumeangalia jumla ya Miswada sita ambayo inarekebisha sheria 58 almost. Hizi zote zimekaa kimkakati wa kuisaidia nchi yeti katika kupiga hatua za kiuchumi, kwa sababu tuseme yote lakini uchumi ndio kila kitu, hali ya nchi itakuwa nzuri uchumi ukiwa vizuri. Kwa hiyo, zipo sheria kubwa ambazo zimezungumzwa hapa na wenzangu kama mabo yale ya nolle prosequi na mambo mengine ya kukamilisha upelelezi kabla ya kupeleka watu Mahakamani ni mambo mazuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ziko sheria nyengine ambazo sio rahisi kuzi-note lakini bado zina-impact sana katika masuala ya uchumi wa nchi. Kwa mfano marekebisho ya Sheria ya Makampuni ambayo tuliyapitisha. Ooh! Naona kengele imelia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Malizia sentensi yako.

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Basi labda tu niseme kwamba sheria zote ambazo zimepitishwa kwa kweli nimekuwa nimejiandaa kuzitaja zote zimekaa kimkakati kusaidia nchi yetu kuweza kujifungamanisha na dunia na kurahusisha mambo ya biashara za kimataifa, lakini pia kulinda haya mafanikio yanayokuja na kuwalinda Watanzania katika mchakato huu unaokuja wa uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo na kwa ajili ya muda basi nuinge mkono hoja kwa asilimia zote ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Mkataba wa Umoja wa Nchi Huru za Afrika wa Kuzuia na Kupambana na Ugaidi ya Mwaka 2004
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kupata nafasi hii ya kuwa mchangiaji wa mwisho kwa upande wa Wabunge. Awali ya yote ninawashukuru Wakuu wa nchi zetu za Afrika kwa sababu iliwapendeza miaka hiyo ya nyuma ya 2004 kuandaa Itifaki hii. Ni jambo la kimapinduzi na la kipekee kwa sababu tumezoea kuwa na Itifaki za Umoja wa Mataifa au Taasisi zake kubwa za Kimataifa, lakini tunapofikia sasa mahali pa kuanza kuwa na Itifaki ambazo zinatokana na Afrika kwa ajili ya Afrika ni jambo linalofurahisha sana kwamba AU sasa inarejea katika kazi yake ile ya msingi. Mwanzoni ilikuwa ni mambo ya ukombozi lakini baadaye ikaendelea kuwa sasa masuala ya uchumi, usalama na ustawi wa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunafahamu kwamba huwezi ukaitaja AU au OAU bila kuitaja Tanzania. Mwalimu Nyerere pamoja na wenzake waliokuwepo enzi hizo ndio waliokuwa waanzilishi na mbegu ile ndiyo inayomea mpaka sasa hivi. Kwa hiyo, kipekee kabisa kwa kweli leo tunaporidhia Itifaki hii tunapaswa kabisa kutambua, kupongeza na kushukuru juhudi za Mheshimiwa Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa jinsi ambavyo ameendelea kufanya juhudi za kutufanya tubaki pale turudi kwenye nafasi yetu, katika Itifaki ya Afrika na ya Kimataifa na katika mambo ya Kidiplomasia ya Afrika na ya Kimataifa hasa katika maeneo yanayohusu maslahi ya Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pengine hiyo ni sehemu ya jibu kwamba kwa nini tunaridhia Itifaki hiyo leo, Itifaki ya mwaka 2004, hizi ni zama sasa za kutokuchelewesha mambo ya Kimataifa ni zama sasa ya kuyatekeleza, tumpongeze sana Mheshimiwa Rais na kwa kuridhia Itifaki hii leo tunaunga mkono hizo juhudi zake ambazo dunia nzima imeshaziona tayari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri nikataja kidogo juu ya hii tarehe kwa nini tunaridhia leo tusiwe wanyonge sana kwamba ni kuanzia 2004. Ukienda Ibara ya 10 ya Itifaki hii utaona imeelekeza kwamba mpaka nchi 15 zitakapokuwa zimesaini na ku-deposit (zimeridhia) ndipo ile Itifaki itaanza kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nchi hizi 15 zilifikiwa mwaka 2014 miaka 10 baada ya ile Itifaki. Kwa hiyo, leo hii tusiseme kwamba tunafanya kazi ya mwaka 2004 hapana, hata tungeifanya hivyo isingekuwa hatujafanya kazi yoyote bila nchi 15 ambazo zilifikiwa mwaka 2014.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ugaidi kama ambavyo wengi wamesema ni uhalifu wa Kimataifa na unaovuka mipaka, ni tofauti na uhalifu mwingine. Tunayo Sheria ile ya Kuzuia Ugaidi Sura ya 19 ambayo kwa kweli inatuwezesha zaidi kupambana na ugaidi wa ndani (Domestic Terrorism) lakini haitoshi tunapokwenda kwenye ugaidi wa Kimataifa, kwa sababu, ugaidi wa Kimataifa sasa hivi unaweza ukapigwa hapa na mtu aliyepo kilometa 10,000 kutoka hapo ulipo au mtu anaweza akapiga hapa lakini baada ya nusu saa ameshatoka nje ya nchi hii. Kwa hiyo, ni muhimu kuridhia Itifaki kama hizi ambazo zinapanua wigo wa kuweza kushughulika na jambo kama hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunayo Sheria nyingine inaitwa Mutual Assistants in Criminal Matters Act Cap. 254 ambayo inasaidia katika kuchukua ushahidi katika kupekua na kukamata vitu ambavyo vimepatikana katika upelelezi na katika kukamata watu wanaokimbia ambayo inatumika kwa nchi mbalimbali, lakini bado hata yenyewe hiyo inashughulika na makosa yote siyo kama hii ambayo ni maalum kwa ajili ya ugaidi. Kwa hiyo, pamoja na Sheria hiyo lakini bado tumeendelea kupata changamoto kwenye suala la ugaidi kutokana na upekee wake. Kwa hiyo, kutokana na upekee wake ni lazima tuingie kwenye Itifaki kama hii ambayo itatusaidia kupambana na hili jambo kwa kushirikiana na wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ugaidi hata usipotokea hapa Tanzania ukatokea nchi nyingine bado unaweza kutuathiri sisi. Kwa mfano, naamini kabisa magaidi walivyopiga pale Westgate Kenya siyo Wakenya peke yao ambao walidhurika na kufa ni watu wa Mataifa mbalimbali inawezekana hata Watanzania. Hata kule Chuo Kikuu - Garisa pia siyo Wakenya peke yao nakumbuka kabisa kwamba katika watu waliokamatwa kupanga na kutekeleza ile njama, sisemi kupatikana na hatia mimi nazungumzia kukamatwa kama walipatikana na hatia hiyo ni baadaye, lakini mmojawapo alikuwa ni kijana wa Kitanzania. Kwa hiyo, maafa haya yanakwenda kila mahali hata Septemba 11 kule Marekani iligusa watu wengi duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili la ugaidi pia linagusa haki ya kuishi (right to life) ambayo ndiyo Mama wa haki zote kwa hiyo, kwa kuridhia Itifaki hii pia tunatekeleza matakwa ya Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania juu ya kulinda haki ya msingi ya kuishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo machache labda ninashauri tu mambo mawili. Jambo la kwanza kwenye utekelezaji wa Itifaki hii hasa kwa upande wa mambo ya movement ya finances (fedha) ni vizuri tukawa waangalifu sana, kuna watu wengine huwa wanatumia tusiwe Wakatoliki kuliko Papa mwenyewe. Tusije tukaitekeleza hii Sheria kwa ukali mpaka tukazuia vijana wetu ambao wanataka kuibukia katika biashara za Kimataifa sasa. Tuwe na uchunguzi wa kina kabla hatujachukua hatua kwenye haya mambo ya fedha kwa sababu yanaweza yakatumika pia kufifisha juhudi zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kama Mbunge ninayetoka Jimbo la Mpakani ninazo taarifa kwenye baadhi ya maeneo ambapo sisi tumekuwa wakali mpaka kuzuia biashara kwa upande wetu lakini wenzetu kule wakalegeza wakafanya biashara. Kwa hiyo, tuwe makini kidogo kwenye hilo kwamba tusije tukajiumiza wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhusu elimu sahihi juu ya ugaidi ni kitu gani na gaidi ni nani ili tusije tukaingia kwenye mtego wa kushabihisha ugaidi na kabila fulani na Taifa fulani na dini Fulani, jambo ambalo ni la hatari sana. Ni vizuri tu tukajua kwamba ugaidi ni uhalifu wa Kimataifa ambao unalenga tu maeneo yenye udhaifu either kwa kukosekana kwa haki kwenye uchumi au kukosekana kwa haki kwenye siasa na mambo ya uongozi, basi wanapenyea hapo hapo na kuingiza mambo ya ugaidi lakini hauna msingi wowote katika kabila lolote, hauna msingi wowote katika dini yoyote wala katika katika Taifa lolote lile. Elimu ni muhimu sana katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumaliza tu nirudi kuipongeza Serikali kwa kuleta Itifaki hii sasa hivi, pia Kamati kwa kweli mimi binafsi, kwa sababu sitoki kwenye Kamati husika wameni-impress sana kuanzia taarifa yao na Wajumbe wa Kamati walivyochangia, kwa kweli wameonesha umahiri mkubwa wa kuelewa Itifaki hii ambayo wameileta, wametufungulia hata sisi ambao siyo Wajumbe wa Kamati na hatujawahi kuchangia kwenye Kamati kupata ukereketwa wa kutaka kuchangia kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru naunga mkono na ninaomba Bunge lako Tukufu liunge mkono hoja hii. Ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Kuongeza Mamlaka ya Mahakama ya Afrika Mashariki
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kupata fursa hii kuchangia. Awali ya yote naipongeza sana Serikali kwa hatua ambayo wamefikia sasa kutuletea itifaki hii kwa ajili ya kuiridhia. Kipekee pia nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Sheria pamoja na timu yake kwa kazi nzuri ambayo wameifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hii tunalolijadili leo lina umuhimu mkubwa sana katika kuhakikisha kwamba Jumuiya hii ya Afrika Mashariki inaendelea na haitakutana tena na madhila kama yale yaliyoipata ile iliyotangulia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia historia utakuta kwamba suala la umoja wa forodha katika nchi hizi ya Afrika Mashariki, lilianza hata kabla nchi hizi hazijapata uhuru; lilianza wakati wa mkoloni, likianza na Kenya na Uganda na baadaye Tanzania. Kwa hiyo, hata Jumuiya ya Afrika Mashariki ilipoundwa mara ya kwanza mwaka 1967 jambo kubwa ambalo lilikuwa linazingatiwa ni hapo kwenye masuala ya forodha, lakini baada ya miaka 10 ile jumuiya ikawa imeshindwa kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma sababu za kuanguka kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa miaka ile, zinatajwa nyingi, lakini mojawapo wanazungumzia habari za tofauti za mifumo ya kiuchumi katika nchi wanachama. Sasa mimi ukiniuliza nitasema, katika ushirikiano wa aina yoyote ile, tofauti na mifumo ya kiuchumi au kisiasa hazipaswi kuwa sababu ya kuanguka kwa jumuiya. Kuanguka kwa jumuiya kunatokana na kukosekana kwa mikakati ya kuweza kuzisawazisha zile tofauti ili nchi zikaenda kwa pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani ndicho tunachokizungumza hapa kwamba kwa kuwa madhumuni makubwa ya hizi jumuiya ni uchumi; tunazungumzia sawa siasa, jamii na nini, lakini kama jumuiya yoyote, hizi Reginal Integration, kama hai-address suala la uchumi lazima itaanguka. Kwa hiyo, masuala haya ya uchumi yasipowekewa mfumo mzuri wa kuyaendesha na kuyadhibiti, basi lazima anguko lake litakuwa karibu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana utakuta mwaka 1999 tulipounda tena jumuiya mpya kama walivyoeleza waliotangulia kwamba hatua ya kwanza ikawa ni masuala ya Umoja wa Forodha mwaka 2005, ni suala la uchumi hilo; ikaja Soko Huria 2010, ni uchumi sasa tunaangalia mambo ya Sarafu ya Pamoja, ni uchumi pia, ndiyo sasa tuanze kuota hiyo ndoto ya Political Federation huko baadaye, lakini mpaka haya yakae stable kwanza ndiyo unaweza kufikiria hilo la kisiasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chombo ambacho kina-balance au kina- harmonize haya mambo huwa ni Mahakama. Mahali popote pale ukitaka mambo yaende bila migogoro, lazima uwe na Mahakama, kwa sababu vinginevyo basi unaachia watu waamue kwa kutumia mapanga. Sasa Mahakama tuliyonayo sasa hivi ambayo inaundwa na Ibara ya 23 na 27 ya Mkataba huu wa Afrika wa Mashariki, inashughulikia zaidi mambo ya tafsiri ya mkataba waliovunjwa ule mkataba; iwe ni nchi au ni watu binafsi, mamlaka hiyo iko ndani ya Mahakama hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, mamlaka hii haiendi katika kutoa maamuzi ambayo yana nguvu ya kisheria, ni binding kwa lugha ya kisheria, ni maamuzi ambayo ni matamko (declamatory) au ni ya kushauri tu (advisory). Sasa haya yanaweza yakaendelea kwenye upande wa siasa na jamii na haki za binadamu na kadhalika; lakini ukija kwenye uchumi, lazima kuwe na maamuzi ambayo ni binding, yaani yanaweza yakafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ibara ya 27 inaruhusu kwamba mahakama ile itakuja kuongezewa mamlaka kama ambavyo council itaamua na nadhani ndiyo kinachofanyika hapa. Kwa hiyo tunachokifanya hapa kiko ndani kabisa ya ule Mkataba wa East Africa kwamba mahakama sasa iongezewe uwezo katika mambo haya ya kiuchumi; Umoja wa Forodha, umoja wa hii mambo ya fedha ili kuweza kutoa maamuzi ambayo yanaweza kutiliwa nguvu ya kisheria yakafanyika. Kwa hiyo, nadhani kuridhia hili ni jambo la muhimu sana katika kufanya jumuiya hii isikubwe tena na madhila ya kuyumba au kuanguka kama hapo nyuma ilivyotokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hakuna jambo jema ambalo halina changamoto zake au halina tahadhari za kujiandaa. Naona hili ni jambo jema sana, lakini sisi kama nchi tunahitaji kutia nguvu zaidi kwenye uzalendo wetu. Unapoingia kwenye mambo ya mashirikiano na watu wengine suala la uzalendo linatakiwa liwe na kipaumbele sana. Kwa hiyo moja, tunahitaji sana kujenga nguvu kubwa zaidi ya uchumi wetu, yaani tujenge nguvu ya ushindani kwenye uchumi ili hata tunaposema Umoja wa Forodha na sisi tuwe na mambo ya kwenda kufanya kule kwa wenzetu. Isije ikawa ni Umoja wa Forodha wenzetu wakawa wanakuja kufanya kwetu, sisi hatuna access ya kwenda kule. Siyo access kwa sababu ya sheria, ila access kwa sababu ya uwezo, kwa hiyo tuwajengee wafanyabiashara wetu uwezo wa kushiriki katika uchumi katika biashara zinazokwenda nje ya mipaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuwajengea uwezo Watanzania kujua fursa zilizopo katika nchi za wenzetu. Ni kweli tunatakiwa kufanya jitihada sana wawekezaji waje kwetu, lakini pia na sisi tunahitaji kwenda kuwekeza kwenye nchi za wenzetu. Sasa hapa tunahitaji kuwajengea uwezo Watanzania, vijana wanaoinukia kwenye biashara ili wawekeze hapa na watoke pia nje wawekeze. Ni mabenki mangapi ya Tanzania ambayo yamefungua matawi nje ya nchi. Pengine wala siyo uwezo, baadhi ya benki zetu zinao, lakini ile kuona iko fursa pale inaweza ikawa ni tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunakwenda kwenye mahakama, mahakama ni sehemu muhimu sana ya biashara, kwa hiyo mtu akipata kesi yake anataka akawakilishwe na mtu ambaye atashinda, whether ana kosa au hana, anachotaka yeye ni kushinda kesi. Kwa hiyo uwezo pia wa Wanasheria wetu na Mawakili wetu ni jambo muhimu sana. Hili ni eneo maalum, siyo kesi za kawaida zile ambazo tumezoea kufanya, kwa hiyo Chama cha Wanasheria Tanganyika na hasa hasa Wizara ya Katiba na Sheria iratibu mafunzo na kuwajengea uwezo Wanasheria wetu ili waweze kushiriki katika mahakama hii, vinginevyo watatokea wafanyabiasha wataenda kutafuta Wanasheria nje, kwa sababu mfanyabiashara anachotaka yeye ni kushinda kesi, siyo mambo mengine ya wema wema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, basi nishukuru kwa kupata nafasi hii, kama nilivyosema nitachangia kwa ufupi, naunga mkono hoja kwa tahadhari hizo ambazo nimejaribu kuzitoa. Nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii awali ya yote nianze kwa kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupata nafasi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nianze kwa kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Rais na Mwenyekiti wa CCM, Mama Samia Suluhu Hassan. Kwa kumpongeza yeye naamini kabisa nimewapongeza pia wateule wake wote pamoja na Watendaji na Wataalam wanaomsaidia kazi, hasa ukizingatia kwamba Wizara hii tunayoijadili ni ofisi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi nzuri inafanyika Tanzania, Watanzania wanaona na dunia inaona. Jimboni kwangu Mwanga pia kazi inafanyika vizuri. Mimi Mbunge wa Mwanga ninaiona kazi na wananchi wangu wa Mwanga pia wanaona kazi nzuri inayofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mwanga siyo Wilaya changa sana, ina umri wa takribani miaka 44 sasa, lakini kwa mara ya kwanza sasa tumepata jengo la utawala la Halmashauri ambalo tulikuwa hatujapata siku zote. Tumepata katika maana ya kwamba tumetengewa fedha Shilingi Bilioni Moja. Tumetengewa pia Shilingi Bilioni Moja kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya. Kwa haya yote mawili naishukuru Serikali pia ninatoa wito kwamba kule tumeshaanza kazi tayari ya maandalizi, kiwanja kipo, tunaanza kusafisha na kukusanya vifaa.

Kwa hiyo, tunaomba Wizara isituangushe, tupate hizo fedha kwa wakati ili tuweze kukamilisha hii miradi kama ambavyo wananchi wanaitarajia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwanga kuna changamoto ya vyanzo vya mapato. Kwa ajili hiyo tuliamua kubuni miradi ya kimkakati ili kuweza kuongeza mapato. Mradi wa kwanza ni stendi na kwa bahati nzuri sana tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwa sababu alipokuja Kilimanjaro tulizungumzia suala hilo na akalibariki, kwa hiyo ile ni ahadi ya Rais. Tunaomba tupatiwe stendi ya kisasa Mwanga kama ambavyo Mheshimiwa Rais ameahidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa pili wa kimkakati ni soko la samaki. Kwa kutumia mapato ya ndani tumekarabati jengo la chakula barafu na kujenga mialo kama 24 hivi. Alipokuja kututembelea aliyekuwa Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Ummy Mwalimu, alivutiwa na ule mradi na akatuahidi barabara ya kufika kwenye lile eneo. Tunaomba ahadi hii kwa sababu ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri na alikuwa na timu ya wataalam ni ahadi ya Serikali, tunaomba itekelezwe ili Mheshimiwa Waziri tutakapokukaribisha kuelekea mwishoni mwa mwaka huu kuja kufungua huo mradi usipate shida ya kufika barabara iweze kukufikisha vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliomba shule za Kata kwenye Kata mbili ambazo hazikuwa na shule. Tumepata Kata moja ya Kivisini, tunaomba Kata ya Toloha ipate shule kwa sababu ni Kata yenye changamoto za wanyama tembo na wanaoishi kule ni ndugu zetu wa jamii ya kifugaji. Tunatamani shule isogee ili waweze kupata huduma hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo changamoto ya shule chakavu kama maeneo mengine yalivyo lakini kipekee naomba niiseme shule moja, Shule ya Msingi ya Ndorwe ambayo ilianguka baada ya kutokea tukio la landslide. Wananchi wamejitahidi wametafuta kiwanja kingine wamesafisha uwanja na wameanza kuweka vifaa. Tuliomba fedha kwenye mfuko wa maafa, tunaomba sana tusaidiwe fedha hizi ili tuweze kukamilisha kwa sababu watoto wanatembea umbali mrefu sana kufuata huduma ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vituo vya afya tuliomba vituo viwili vya kimkakati, tumepata kimoja, tunaomba sana kwamba na hiki kingine tukipate kwa sababu ni changamoto kubwa sana, vituo vya afya ni vichache. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia nizungumzie suala la ajira. Kwanza nishukuru kwamba tumepata ahadi hiyo ya ajira nyingi katika sekta za elimu na afya. Mwanga tuna Walimu wanaojitolea, upande wa sekondari wako walimu 55 na upande wa shule za msingi walimu 83.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba walimu wale wangeajiriwa palepale, ingetupunguzia mambo kama mawili. Jambo la kwanza, ingetupunguzia gharama za kuwapeleka huko mbali ambako pengine watapata ajira, lakini jambo la pili, hata wao maisha yao yatakwenda vizuri kwa sababu pale wana nyumba hata wakiwa nacho kipato kinaweza kikatosheleza. Kwa hiyo, ninaomba katika kufikiriwa ajira za walimu, wale walimu wanaojitolea Mwanga waajiriwe palepale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu kwamba iko sera ya ajira na nini, labda tunazungumzia mambo ya umoja na kadhalika kwamba waende huko na huko, lakini hili sasa ni janga kwa sababu kuna watu wamemaliza chuo mwaka 2015 mpaka leo hawajapata kazi. Wasije wakafikia umri wa kustaafu kabla hawajapata kazi. Tulichukulie kama janga, hawa watu waajiriwe ili waweze kutumia elimu yao ambayo wameipata kwa gharama kubwa kwa ajili ya faida ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme hayo tu kwa leo kwa sababu ya muda nisiseme mengi. Nakushukuru sana kwa nafasi hii, ninaunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kupata nafasi ya kuchangia hotuba hii ya bajeti ya Wizara ambayo mimi nasema ni wizara nyeti sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu tumeanza kuchangia jana mpaka leo imetolewa michango mingi yenye umahiri na weledi mkubwa sana hasa kwa upande wa masuala ya utumishi. Na katika michango hiyo pamoja na hotuba ya Mheshimiwa Waziri tumebaini jinsi ambavyo kazi kubwa imefanyika katika kurekebisha suala zima la utumishi wa umma na kuwajengea watumishi mazingira mazuri ya kazi na matumaini ya kuendelea kufanya kazi katika mazingira mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo katika hili nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake, kazi waliofanya ni kubwa na Watanzania wameiona. Lakini kipekee kabisa nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa sababu wizara hii iko chini ya ofisi yake, kwa hiyo haya yote yaliyofanyika yana m-reflect yeye mwenyewe, jinsi ambavyo amekuwa mtu wa kujali na jinsi ambavyo amekuwa mtu mwenye nia ya kuifikisha nchi yetu mahali pazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nichangie upande wa utawala bora kwa sababu ni jambo ambalo ni cross cutting, linakwenda kila Wizara. Hawa watumishi tunaowazungumzia popote pale walipo wana wajibu wa kutumika kwa kuzingatia misingi ya utawala bora na hakuna taasisi wala idara yeyote ambayo inaweza ikafanya kazi nje ya mfumo wa utawala bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili kwanza nitambue jinsi ambavyo tumefanya vizuri, na si kwa viwango vyetu sisi, tumesoma kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kwamba tumepanda ngazi katika kiwango cha Corruption Perception Index na hata kwenye Rule of Law Index tumepanda. Sasa tathmini hizi ambazo zinafanywa na mashirika ya kimataifa yaani hakuna namna ya kusema kuna mtu amejipendelea hapo, zimefanyika kwa viwango vya kitaaluma na kitaalam, kwa hiyo tunastahili kuipongeza Serikali kwa hilo na pia sisi wenyewe kujivunia kwamba tunakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utawala bora katika nchi ambayo ina katiba iliyoandikwa (written constitution) unaanzia na kuishia kwenye utawala wa sheria; yaani utawala ambao kila mtu, ikiwa ni pamoja na dola yenyewe, inapaswa kutenda kazi zake kwa mujibu wa sheria na kwa kutii sheria, hakuna aliye juu ya sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia sheria si kila sheria ni sheria, kwamba hata zile za wakati wa Idi Amin anaamka kule kwake anasema leo weka watu hawa kwenye karandinga tukawatupe baharini nayo ni sheria hapana. Sheria inayozungumziwa katika utawala wa sheria ni ile sheria ambayo imetungwa na chombo halali kama sheria zetu ambazo zinatungwa na Bunge hili, na imetungwa kwa mfumo wa uwazi ambao inashirikisha hata wadau kupata maoni ya wadau na kadhalika kwa mfumo ambao ni shirikishi, na ni sheria ambayo inaweza kutumika kwa ajili na dhidi ya mtu yeyote yule hata dola yenyewe kama ambavyo nimekuwa nikizungumza; na pia ni sheria ambazo zinaendana na misingi ya haki za binadamu, ile misingi ya kimataifa; na katika hili bado tumefanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili bado tumefanya vizuri kwa nini nasema tumefanya vizuri. Mwaka 1984 Bill of Rights ule mkataba wa Haki za Binadamu uliingizwa katika Katiba yetu, baada ya hapo ikatokea kipindi karibu cha miaka 10 ambapo Idara mbalimbali zilianza kurekebisha Sheria zao ili ziendane na Bill of Rights na pale ambapo hawakufanya hivyo wananchi binafsi waliweza kufanya hivyo kupitia Mahakama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtakumbuka kesi kama ya Daudi Pete ambayo ilifanya marekebisho kwenye Sheria ya Dhamana, mtakumbuka Sheria ile ya Government Proceedings Act ambayo ilikuwa inakataza wananchi kuishitaki Serikali mpaka wapate kibali cha Waziri wa Sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1992 kuna mtu mmoja ni Mwalimu anaitwa Peter Ng’omango alikwenda Mahakamani wakaifuta ile Sheria. Ilipofika mwaka 1994, Bunge hili likaona sasa tuwarahisishie zaidi wananchi kazi kwamba wanapotaka kurekebisha sheria siyo lazima waende wakaishambulie ile Sheria Mahakamani kwamba inakiuka Katiba, ikatungwa ile Sheria ya Basic Rights and Duties Enforcement Act, ambayo kwa mujibu ya Sheria ile ya Mwaka 1984 nafikiri ni Sheria Na. 33, mtu yeyote ambaye haki yake imenyimwa au anaona kwamba haki yake itanyimwa ana haki ya kwenda Mahakamani na akaipinga ile Sheria na ile Sheria ikafutwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Sheria hii imetumika kurekebisha Sheria nyingi sana ambazo watu walikuwa wanaona zinawanyima haki na hata juzi juzi kesi ambayo bado nadhani iko kwenye mawazo ya watu ni kesi ya Ndugu Rebecca ambapo alikwenda Mahakamani kupinga vile vifungu vya Sheria ya Ndoa ambayo ilikuwa inaruhusu watoto wa kike kuolewa chini ya umri na ile sheria Mahakama ikaitamka kwamba inakiuka Katiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kusema ni kwamba Katiba yetu, Sheria zetu na mifumo yetu iko ambayo inatuwezesha kupata haki zetu kwa mujibu wa Katiba, lakini tatizo linakuwa wapi? Tatizo ninakuwa uelewa tu ndiyo tatizo. Kwa hiyo, tunapopanga bajeti zetu na kuleta hapa Bungeni ni vizuri sana tukazingatia suala la training na kujenga uelewa kwa upande wa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya zile bajeti zinazopita kwenye Kamati yetu ya Katiba na Sheria kwa kweli tuling’ang’ana sana na walioleta bajeti kwamba jamani bajeti ya training ni ndogo, bajeti ya mafunzo ni ndogo mambo ya kujenga uelewa, wakati ule tunaambiwa ni ukomo wa bajeti, nafikiri sasa ukakomoe maeneo mengine tusikomoe suala la training ambalo kwa kweli ni muhimu sana. Unaweza ukawa na sheria nzuri, unaweza ukawa na Katiba nzuri lakini kama watu hawaifahamu na hawaifahamu jinsi ya kuitumia kufikia haki zao inakuwa unafanya kazi bure, unakuwa na karatasi za bure. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata Waheshimiwa Wabunge ni vizuri tukajengewa uwezo kwenye maeneo ya kimkakati ili tunapokwenda kwenye mikutano ya hadhara tuweze kuwaelimisha watu wetu ili waweze kujua jinsi ya kufikia haki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mambo madogo mdogo ambayo yanawakerakera wananchi ambayo kama tu mafunzo yangekuwa yanafanyika kwa wananchi wenyewe na kwa wale Watendaji tusingekuwa na tatizo. Kwa mfano, mtu anakwenda anataka dhamana ana kitambulisho cha Taifa cha NIDA ambacho kimepatikana kwa mifumo ya hali ya juu lakini anaambiwa kalete barua ya Mtendaji. Sasa anakwenda kufuata barua ya Mtendaji anakuta Mtendaji siku hiyo kafiwa kaenda mazikoni, anarudi anakuta OCS ameshaondoka, mtu analala ndani bila sababu wakati kitambulisho cha Taifa kimejitosheleza kufanya hiyo kazi. Wengine wanaofanya hivyo ni kuelewa awaelewi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la dhamana unaambiwa kalete barua ya mtu ambaye ameajiriwa Serikalini. Sasa upo pale umekamatwa, uende ukatafute mfanyakazi wa Serikali, by the time unarudi muda umeisha mtu anakosa dhamana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Jimbo langu pale kuna jambo moja lilitokea hapo ni la kuchekesha tu ambalo ni lakusikitisha kwa kweli, kwenye Kata ambazo zilishambuliwa na Tembo, Kata ambazo zina matatizo ya Tembo Kata ya Kwakoa, Kigoligoli na Toloa walikwenda watu kulipwa kifuta jasho, sasa anakuja mtu anakitambulisho kimeandikwa kwa mfano Zaituni Athumani Mbarouk, sasa lile jina lilivyochapwa huko Wizarani kuletwa kwake limeandikwa Zaituni Athumani Mbaraka anaambiwa sasa nenda kaape Mahakamni kubadilisha hii Mbarouk na Mbaraka ili upate hela yako, wanakwenda kuapa Mahakamani anarudi tayari watu wameshaondoka na mpaka leo hawajarudi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mambo mengine ni uelewa tu wa hawa tu ambao kwa kweli kama wangepewa mafunzo, wakajengewa uwezo, nadhani kwamba tusingefika hapa, haya matatizo madogo madogo tungeyaondoa, tunaweza tukawekeza kwenye haya makubwa tuka-shine tukapata na sifa, lakini haya madogo ni muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. JOSEPH A. THADAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kupata nafasi hii ya kuchangia Wizara hii nyeti ya Katiba na Sheria. Awali ya yote niipongeze sana Serikali na Wizara, hasa Wizara ya Katiba na Sheria pamoja na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu kwa ajili ya kazi nzuri ambayo wamefanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria; kwa hiyo chini ya Kanuni ya 117 ya Kanuni za Kudumu za Bunge za mwaka 2020 nilipata fursa ya kutembea pamoja na kamati kuangalia miradi mbalimbali ya maendeleo ya Mahakama, iliyoko chini ya Wizara hii. Na kwa kweli, lazima nikiri kwamba, tumeona maendeleo makubwa sana katika uboreshaji wa sekta ya utoaji haki. Tumeona majengo ya kisasa kama ambavyo wenzangu wameeleza, tumeona uboreshaji mkubwa sana wa mifumo ya TEHAMA, pamoja na vitu vya kisasa kama hii Call Centre ambayo inawasaidia wananchi kupeleka kero zao.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tumeona ushirikishwaji wa wadau wengine. Kwa mfano kitendo cha kuwa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kupewa ofisi ndani ya Jengo la Mahakama, ili watu wote wanaohitaji msaada wa kisheria waweze kuupata palepale, hayo ni mapinduzi makubwa sana yanayodhihirisha kwamba Serikali ya Awamu ya Sita haifanyi maigizo kwenye suala zima la utoaji haki. Wako serious kwamba, tunataka nchi iende kwa mujibu wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na nadhani ni jambo ambalo linaeleweka tu kwamba, umuhimu wa sekta ya utoaji haji katika kukua kwa uchumi na utulivu wa nchi. Pamoja na kwamba, Mahakama haiuzi na kununua, lakini wanaouza na kununua hawataweza kuuza na kununua kama Mahakama na sekta ya utoaji haki kwa ujumla haifanyi kazi zake vizuri.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mambo hayo mazuri tunaendelea kushauri tu kwamba, Serikali iendelee kuwekeza katika sekta ya utoaji haki. Kwa mfano, tumekwenda vizuri katika hivi vituo jumuishi ambavyo ni Mahakama Kuu na Mahakama za Wilaya, lakini bado hatujafika vizuri kwenye Mahakama za mwanzo.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, katika Jimbo langu la Mwanga tumepata jingo la Mahakama la kisasa ambalo liko katika hatua za mwisho kabisa za umaliziaji, lakini kwenye kata 20 ambazo tunazo tuna Mahakama za mwanzo tano tu. Sasa wananchi wengi ni wanufaika zaidi wa Mahakama za mwanzo kuliko hizi Mahakama nyingine huku. Na bahati mbaya kwa utaratibu wa sheria ni kwamba, hata kama Mahakama ya Wilaya au Mahakama Kuu iko ukumbini mwako, lakini kama shauri lako inabidi lianzie Mahakama ya Mwanzo lazima ukaanzie kule. Kwa hiyo, pamoja na kuwa na hizi Mahakama nzuri za katika ngazi ya wilaya na Mahakama Kuu, lakini kuna umuhimu sana wa kuwekeza katika Mahakama za Mwanzo ambako ndiko wengi waliko.

Mheshimiwa Spika, na huku kwenye Mahakama za Mwanzo, au tuseme mahitaji ya watu wengi zaidi yanayoleta kero kubwa yako zaidi kwenye masuala ya ardhi na haya masuala ya familia, kama vile ndoa, talaka, mirathi, n.k.

Mheshimiwa Spika, sasa yako mambo mawili hapa ambayo ningependa kusema. La kwanza ni kwamba, hata tunapokwenda kuwekeza kwenye Mahakama za Mwanzo tuangalie pia kuwajengea uwezo mahakimu walio kwenye Mahakama za Mwanzo juu ya suala zima la sheria za ardhi pamoja na hizi sheria zinazohusiana na mambo ya mirathi na ndoa, n.k. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na suala la sheria zinazohusiana na mambo ya mirathi na (family law), tatizo kubwa kwa kweli, liko kwenye sheria za kimila ambazo hasa ndizo ambazo zinasumbua watu wengi kule chini. Na bahati mbaya ni kwamba, utaratibu wa marekebisho wa zile sheria haupo kupitia Bunge, ila uko kupitia kwenye Halmashauri za wilaya kwa kupitia ile sheria inayoitwa Judicature and Application of Laws ACT, Kifungu cha 12. Ni vizuri hilo eneo likafanyiwa kazi kwa sababu, tunaweza tukawa na miundombinu mizuri sana ya Mahakama, n.k., lakini watu wanatumia sheria za kimila kufanya mambo yao huko na kwa hiyo mateso yataendelea huko chini wakati sisi huku tunabakia na facilities zetu ambazo ni nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili ni kuhusu suala hili la Mahakama za Ardhi. Tunaweza kuwa na Mahakama za Wilaya nzuri sana, lakini bahati mbaya ni kwamba, katika level ile ya chini ya wilaya ukiwa na shauri la ardhi lazima uende Mahakama ya ardhi kwanza. Sasa Mahakama za ardhi ziko chache sana, mimi nashukuru Napata Mahakama nzuri ya Wilaya, lakini bado ukiwa na tatizo la ardhi lazima uende Same kwa sababu Mahakama ya ardhi pale haipo. Ni vizuri ikafanyika kama ilivyofanyika kwenye Mahakama Kuu.

Mheshimiwa Spika, hapo awali ilikuwa hata ukiwa kwenye Mahakama Kuu ilikuwa lazima uende kwenye Mahakama Kuu, Kitengo cha Ardhi, lakini nafikiri mwaka 2010 Mheshimiwa Jaji Mkuu alipitisha circular, tena namshukuru sana kwa hilo, kuzipa Mahakama Kuu mamlaka ya kusikiliza mashauri ya ardhi, Mahakama kuu zote, Kitengo cha Ardhi pamoja nah ii Mahakama Kuu ya kawaida. Kwa hiyo, nadhani tunahitaji kulifanya hilo katika ngazi ya wilaya pia, ili wananchi waweze kutumia huu uboreshaji ambao unafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine la muhimu ni kwamba, tunaweza tukaboresha Mahakama sana lakini tusipoboresha wale washiriki na wadau wa hii sekta ya utoaji wa sheria kama magereza na polisi, bado matatizo yatakuwa palepale. Na kwa bahati mbaya sana lawama huwa zinaenda kwa Mahakama tu wakati ambapo Mahakama mwisho wa siku naweza nikasema ni kama computer kwa hiyo, lazima ulete ui-feed, iweze ku-process na kutoa matokeo. Sasa hayo yanafanyika kwa hawa wadau wengine kama polisi, n.k. Kwa hiyo, ni vizuri maboresho haya yanapofanyika kwenye Mahakama yaende pia kwenye maeneo mengine.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JOSEPH A. THADAYO: Mheshimiwa Spika, hivi ni kengele ya kwanza au ya pili? Ya kwanza, ahsante.

Mheshimiwa Spika, sasa nilikuwa nasisitiza hilo kwamba, ni vizuri maboresho haya yanapokwenda kwenye Mahakama yaende pia kwa hawa wadau wengine. Ukienda kwenye baadhi ya magereza, kama Gereza la Kirumi lililoko katika jimbo langu kwa kweli hali ni ya kusikitisha. Jengo lenyewe ni dogo na ardhi ni ndogo pia, hawana hata mahali pa kupanuka au hata pa kuendesha shughuli kilimo, lakini pia hawana magari na vitu vingine. Kwa hiyo tusipoboresha hawa wadau ni kwamba hata Mahakama zenyewe zitakuwa haziwezi kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Spika, la mwisho nizungumzie kuhusu suala la utoaji wa elimu kwa wananchi juu ya matumizi ya haki zao kwenye Katiba na Sheria nyingine.

Mheshimiwa Spika, naona kengele imelia; niombe tu kuunga mkono hoja pamoja na kwamba, nilikuwa na hoja ya muhimu kidogo kwenye eneo hilo. Ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuimarisha demokrasia nchini na kukuza diplomasia ya uchumi
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nami nashukuru sana kupata fursa hii ya kuchangia azimio hili muhimu. Historia inajieleza kwamba nchi yetu toka ipate uhuru imekuwa mstari wa mbele katika kusimamia ajenda zilizoko mezani mwa Afrika na dunia kwa ujumla katika maeneo ya uchumi, siasa na maeneo ya kijamii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunamshukuru Mungu kwamba katika awamu hii ya sita tumepata kiongozi ambaye anayatambua haya na yuko tayari kuyaishi. Sote ni mashahidi kama mtoa hoja alivyozungumza kwamba Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanya juhudi za makusudi kuhakikisha kwamba demokrasia na utawala bora vinastawi katika nchi yetu. Sasa hii ni muhimu katika kuleta utengamano na amani ndani ya nchi, lakini pia katika kukuza uchumi.

Mheshimiwa Spika, hakuna nchi ambayo inaweza ikakua kiuchumi kama hakuna demokrasia na utawala bora kama ambavyo sasa hivi hapa Tanzania tulivyo. Tunao ushahidi kabisa wa nchi nyingi ambazo zina uchumi mkubwa sana wa maliasili na kila kitu, lakini kwa sababu hakuna amani na utulivu, uchumi ule na zile mali haziwafai kitu chochote kw kuwa amani na utulivu unakuja pale ambapo kuna demokrasia, utawala bora na haki. Kwa hiyo, kwa hilo lazima tumpongeze sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa diplomasia ya kiuchumi, kwanza pamoja na maana zake nyingine nyingi, lakini diplomasia ya uchumi ni zile hatua za makusudi ambazo Taifa linazichukua ili kuonesha mahusiano mazuri na dunia na pia kukuza uchumi na ajira za wananchi wake bila kujali kama kuna gharama zozote za kisiasa ambazo zinaingia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika nchi yetu tumeona faida kubwa sana ya diplomasia ya kiuchumi ambayo Mheshimiwa Rais ameisimamia. Majimboni kwetu kote kuanzia Jimboni kwangu Mwanga na Waheshimia Wabunge wote wanashuhudia kwamba iko miradi mikubwa ambayo inaendelea kuliko kipindi kingine chochote ambacho kimewahi kuwepo katika historia ya nchi yetu. Hii miradi inaendelea, mingine kutaokana na fedha ambazo zinatoka nje na pia hali ya uchumi inaimarika kutokana na utawala bora na hali ya demokrasia ambayo tunayo katika nchi.

Mheshimiwa Spika, kubwa la kumpongeza Mheshimiwa Rais ni kwamba amesisitiza kabisa masuala haya ya demokrasia, utawala bora na haki za binadamu kwamba yatafanyika kwa kuzingatia mila na desturi zetu sisi Watanzania. Hatuingii katika masuala haya kwa lugha za mitaani kusema kichwa kichwa, bila kuangalia kwamba sisi Watanzania tumetoka wapi na historia yetu imetoka wapi? Kwa hiyo, Mheshimiwa Rais anatuongoza vizuri kwamba tuingie kwenye mambo haya ambayo ni muhimu katika dunia, lakini kwa kuzingatia mila zetu na desturi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni rahisi sana watu kusema kwamba aah, mbona haya mambo tayari yapo kwenye Katiba! Ni sahihi, yapo kwenye Katiba, hata hivyo zipo nchi nyingi ambazo mambo yapo kwenye Katiba za nchi zao lakini wanakosa viongozi ambao wana utashi wa kuyatekeleza na kuyasimamia, na hiyo hasa ndiyo sababu ya kumpongeza Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa uchache tu kwa kweli niungane mkono na mtoa hoja pamoja na Waheshimiwa Wabunge wenzangu na kuomba kwamba tumuunge mkono Mheshimiwa Rais katika hili na Tanzania kwa ujumla katika hatua hizi za utekelezaji wa sera hizi za kidemokrasia, utawala bora na diplomasia ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kupata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii nyeti, nianze kwa kusema kabisa kwamba naunga mkono hoja hii ya Wizara ya Katiba na Sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nipongeze na kuishukuru Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa jinsi ambavyo imefanya kazi kubwa, imefanya uwekezaji mkubwa katika Sekta ya utoaji haki. Kwetu sisi ambao tulikaa kaa kidogo kwenye hii sekta kwa muda mrefu tunaona kabisa kama ni mapinduzi makubwa kwa sababu ni sekta ambayo ilikuwa kama imesahauliwa, majengo yalikuwa yamechakaa hata karatasi za kuandikia zilikuwa wakati mwingine ni shida unapoingia mahakamani asubuhi lakini kwa hali ilivyo sasa hivi kwa kweli tunashukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri Mheshimiwa Rais amegundua kabisa kwamba hapo ndiyo mahali ambapo akifanya uwekezaji hata nchi yetu itaheshimika duniani kote kwa sababu ya utoaji haki ulio katika viwango bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze pia viongozi wa Wizara hii, ndugu yangu na rafiki yangu Dkt. Damas Ndumbaro, Waziri na Dada yangu Dada Pauline Gekul pamoja na wengine wote ambao ni wadau katika kuongoza sekta hii muhimu ya utoaji haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Hotuba ya Mheshimiwa Waziri amesisitiza juu ya suala la utoaji elimu. Nadhani hakuna jambo muhimu kama hili kwa sasa na elimu hii iende katika sehemu mbili; kwanza iende kwa wananchi lakini pia iende kwa watumishi katika sekta hii ya utoaji haki. Nikianza na mahakama kwa mfano ni vizuri watu wakaelewa sheria, wananchi wakaelewa sheria wakaelewa na jinsi ya kupata haki zao kwa kutumia sheria lakini pia watumishi wa mahakama wakapata mafunzo ili wananchi wanapokwenda mahakamani waone mahakama kama mahali rafiki, wasione mahakama kama ni mahali ambapo ni pa kuogopwa au ni mahali ambapo ni pa mabavu na kadhalika. Kwa hiyo, elimu ni muhimu katika sekta hizo zote mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri elimu ingetolewa sawa sawa hata malalamiko kama baadhi ya yaliyoletwa hapa juu ng’ombe waliokamatwa ambao ni suala la kukaza hukumu ya mahakama siyo suala la kuja kwa Waziri Ndumbaro tena. Nafikiri hata hayo tusingepata tabu kwa sababu hukumu ikishapatikana uko utaratibu wa kui-execute wa kuikaza kwa Kiswahili wanasema kwa hiyo hayo yote yanaashiria kwamba tuna changamoto juu ya watu ya kuelewa mfumo jinsi ya kupata haki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata suala la katiba mpya for that matter lisipotanguliwa au kwenda sambamba na elimu ya kutosha halitaleta tija yoyote. Tutakuwa na katiba imekaa hapo nzuri, hata kama iliyopo na kama hii ambayo iko hapa sasa hivi ambayo ina haki karibu zote lakini iko kabatini watu hawana uwezo wa kuitumia wala kuweza kupata zile haki zao ambazo ziko ndani ya katiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri mambo machache sana. Nimeona katika ukurasa wa 36 wa ripoti ya kamati imetoa ushauri kwa Tume ya Kurekebisha Sheria juu ya kufanya mambo mbalimbali. Ningependa kuongeza yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, wametaja pale kwamba Tume ya Kurekebisha Sheria ishauriwe juu ya masuala ya Sheria za Ardhi. Tumejenga mahakama nzuri sana maeneo mengi ikiwa ni pamoja na Jimboni kwangu Mwanga lakini bado ukiwa na suala la ardhi utatakiwa kwenda Baraza la Kata ambalo kazi yake ni kutoa ushauri tu kusuluhisha kama vile masuala ya kusuluhisha ndoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitoka hapo lazima uende Mahakama ya Ardhi ambayo pale Mwanga haipo. Mahakama za Ardhi ziko chache tena haziko chini ya Judiciary, chini ya mahakama ziko chini ya Wizara ya Ardhi. Kwa hiyo hiyo inaleta changamoto kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama iliwezekana kwa Mahakama Kuu kuwa na mamlaka ya kushughulikia mashauri ya ardhi na mashauri mengine ya kawaida sioni kwanini sijapata maelezo ya kutosha kutoka kwa Wizara kwamba ni kwa nini sheria isirekebishwe, mahakama za wilaya na mahakama za mahakimu wakazi zikaweza pia kushughulikia mashauri ya ardhi kama iliwezekana High Court naamini hata huko inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo linahitaji marekebisho ni juu ya hizi Sheria za Mienendo, procedure ambazo nilipata kusema hapa kwamba zinanyima haki sana watu kutokana na procedure zenyewe kuwa mzigo. Kasuala kadogo kanatokea mtu amekamatiwa mizigo yake alikuwa anapeleka sokoni labda ni vitu vya kuharibika nyanya sijui na mihogo lakini kama imekamatwa na mamlaka ya Serikali akitaka kwenda mahakamani lazima atoe notisi ya siku 90. Nyanya zinaharibika ndani ya siku 90 na mihogo inaharibika. Kwa hiyo, analazimika tu kufuata kile anachoambiwa afanye hata kama anaona hakuna haki yake lakini afanye nini hawezi kufuata hiyo procedure ambayo ni mzigo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu hata kwenye mizani pale, mtu amekamatwa kwenye jambo ambalo ana hakika kabisa haki yake ipo lakini saa ngapi aende mahakamani aanze kutoa notisi ya siku 90 wakati mzigo ule ameubeba na fedha ya mkopo benki ambayo mwisho wa mwezi kuna marejesho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tusipohangaika na hizi Sheria zetu za Mienendo zikarahisisha mienendo kwa baadhi ya mambo hata kwenye zile haki za msingi ambazo ziko ndani ya katiba. Nitoe tu mfano kwa mfano juzi hapa kule Mkoa wa Kilimanjaro wameandamana watu kupinga haya mambo ya ushoga. Nawapongeza wamefanya kitu kizuri sana lakini nafikiria tu kwamba angetokea mtu asiyejua haki za watu akawanyima kibali cha maandamano, wangefanyaje. Wangetakiwa kwenda ku-challenge ile. Sasa ku-challenge unatoa notisi ya siku 90 wakati watu wanaangamia na ushoga uko wapi na wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tufike mahali turekebishe Sheria zetu za Mienendo zirahisishe jinsi ya kupata haki mbalimbali katika maeneo ambayo ni ya muhimu. Asilimia 90 mimi nasema ya haki katika katiba yetu na katika sheria zetu, zipo zinaweza zikapatikana, tatizo ni namna ya kuzipata ule mlolongo wa kuzipata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu ni mfupi tu kwa kumalizia tu imetamkwa hapa Bungeni kwamba Serikali imeshindwa kukusanya fedha zile za Plea Bargaining. Naheshimu sana huo mchango lakini nalazimika kutoa na maoni yangu. Wote tunafahamu kwamba mambo yale ya Plea Bargaining yalifanyika ilikuwa inafanyika na watu ambao wako ndani wako, jela. Mtu ameshakaa miaka miwili na kule hata mawakili, mimi nilikuwa wakili wakati ule, mawakili tulikuwa tunakatazwa kushiriki kwenye ule mchakato. Kwa hiyo, yalikuwa ni mambo ya kulazimisha, yalikuwa ni mambo ya kuumiza watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika kipindi hiki ambacho tunataka kurekebisha mambo yaliyotokea nyuma ambayo yalitesa watu sidhani kama kuna haja ya kuanza kufikiria kuanza kuwakamata tena watu katika mambo haya ambayo katika spirit ya maridhiano tulishaona kwamba hayafai. Plea Bargaining maana yake ni bargaining, mnakaa mnapatana kwa hiari kama unaona haifai mnakubalina. Ku-bargain ni kama mnavyo-bargain bei na machinga kule ilimradi maslahi ya pande zote mbili yazingatiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile iliyokuwa inafanyika kama kuwekewa pistol hapa mtu yuko ndani miaka miwili analazimika kuchangiwa kuuza vitu kufanya nini halafu leo hii tumeshapata reliefs sasa tunaanza kuweka mambo sawasawa ili twende mbele, tunaanza kusema kwamba tuanze kukamata tena watu. Nafikiri hii siyo sahihi, ipo haja ndiyo ya kupitia baadhi ya zile kesi lakini nyingi kati ya zile kesi ile Plea Bargaining haikufanyika katika utaratibu ambao unakubalika kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sishauri hilo ambalo mwenzangu ameshauri, mimi naomba kutofautiana naye na kushauri Serikali kwamba utaratibu huo hautafaa. Yale yaliyolipwa bila utaratibu fine yamelipwa, tuangalie utaratibu mwingine lakini…

MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante sana.

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi ya kuwa mchangiaji wa kwanza mchana huu. Kwanza kabisa niipongeze na kuishukuru Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi chini ya Rais wetu na Mama yetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi unaendelea vizuri, wananchi hasa wa Jimbo langu la Mwanga wanafurahia kazi za maendeleo zinazoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu kwa dhamana kubwa hii waliyopewa, hotuba ya Mheshimiwa Waziri toka jana asubuhi ilileta hamasa kubwa sana na hatuna sababu kwa nini tusipitishe bajeti yake. Naunga mkono hoja kwa sababu nataka kuona hiyo hamasa aliyotupa ikiingia kwenye vitendo.

Mheshimiwa Spika, niliangalia kwa haraka tu jukumu la Wizara hii. Pamoja na mambo mengine, lakini kuna statement pale kwamba ni kusimamia na kuendeleza Sekta ya Mifugo na Uvuvi kwa ujumla, kukuza uchumi na kupunguza umaskini na kuyafikia malengo ya millennium. Katika upana huo ni kwamba Wizara hii inagusa maisha ya kila mtu ya kila siku. Naamini kabisa zaidi ya asilimia 90 ya Watanzania aidha wanakula nyama au samaki, mayai au maziwa na ikibidi sana basi hata wanatumia mbolea kulima mchicha na kula mazao ambayo yanatokana na mbolea za mifugo hii. Kwa hiyo ni sekta ambayo imegusa maisha ya kila siku ya watu. Kwa hiyo usimamizi wake ni jambo ambalo ni la muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo langu la Mwanga tuna ufugaji wa aina mbili ukizungumzia habari ya ng’ombe na mbuzi. Maeneo ya milimani wanafugia ndani zero grazing, tunazalisha zaidi maziwa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri alipokuwa Naibu niliwahi kumvuta koti siku moja, nikamwambia kwamba kule kwetu tunahitaji sana masuala ya kukusanya maziwa pamoja na uhamilishaji. Sasa amekuwa full Waziri tunaomba atukumbuke hasa kwenye Miradi yake ya Heifer ili tuendelee kuzalisha maziwa kule milimani.

Mheshimiwa Spika, katika maeneo ya tambarare karibu kata kumi, zote zina ufugaji huu wa huria wa kuchunga. Ni jamii za Wamasai pamoja na makabila mengine, lakini kwa kweli tumesahaulika sana kwenye upande wa miundombinu ya ufugaji kama majosho, malambo na hata madawa ya mifugo. Kama sio Shirika la WWF kutukumbuka mara kwa mara nadhani wale wafugaji wangu Mwanga wangekuwa wameshakimbia. Kwa hiyo, tunaomba Wizara itukumbuke katika huduma hizo.

Mheshimiwa Spika, pia tuna mnada wa kimataifa pale wa mifugo kwenye Kata ya Mgagao. Katika mnada ule wanakuja watu kutoka Mombasa na Comoro kuja kuchukua mifugo pale, lakini miundombinu ya mnada ule bado sio rafiki. Kwa hiyo, tunaomba Serikali iwekeze katika mnada ule wa Kimataifa wa Mgagao. Pia eneo hili la Mgagao linafaa sana kwa Kiwanda cha Kusindika Nyama, kwa sababu tuko katikati tunapokea mifugo kutoka Mwanga yenyewe, Simanjiro na hata kutoka maeneo ya Mkoa wa Tanga na airport ya KIA haiko mbali, Bandari ya Tanga iko karibu pia, pamoja na mpaka wa Kenya pale kwa ajili ya biashara. Kwa hiyo, ni eneo la kimkakati, tunaomba pia tukumbukwe.

Mheshimiwa Spika, tukija kwenye Sekta ya Uvuvi, Jimbo la Mwanga lina rasilimali kubwa mbili za uvuvi. Kwanza ni Ziwa Jipe ambalo liko mpaka mwa Kenya. Ziwa hili kwa muda mrefu sana uvuvi sasa unakaribia kufa kwa sababu ya suala la magugu maji. Serikali karibu miaka 20 sasa imekuwa ikitoa ahadi ya kuondoa magugu maji pale. Mara ya mwisho mwaka 2021 alikuja Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira akatuahidi pale kwamba fedha zipo na kwamba magugu maji yataondolewa, lakini mpaka leo hakuna kitu na nimeendelea kufuatilia kila siku lakini inaonekana ahadi hii haitimii wakati ilitolewa mbele ya wananchi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba Mheshimiwa Waziri ni upande wa mifugo lakini ukiangalia jukumu la Wizara yake ni pamoja na kusimamia hivi vyanzo. Kwa hiyo, tunaomba kauli ya Serikali kwamba wanaliachaachaje Ziwa lile la Jipe life wakati ambapo lina uvuvi mzuri wa samaki aina ya tilapia na liko mpakani mwa Kenya? Tunaomba Ziwa lile liangaliwe kwa umakini sana.

Mheshimiwa Spika, ukija chanzo kingine ni Bwawa la Nyumba ya Mungu. Bwawa hili asilimia 61 iko upande wa Mwanga na asilimia zinazobakia ni Simanjiro na Moshi Vijijini. Watu wa pale wanategemea uvuvi peke yake kama njia yao ya Maisha, kwa sababu lile eneo halina hata mvua ya kutosha, hivyo, hakuna kilimo pale. Hata hivyo, kwa muda mrefu sasa uvuvi wa pale hauendi vizuri, samaki wale hawakui na kwa sababu samaki hawakui kila Mvuvi sasa anaonekana ni mvuvi haramu. Serikali imepambana sana na uvuvi haramu lakini bado mambo pale ni magumu.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi kuna taarifa kwamba Wakuu wetu wa Wilaya hizi tatu wameandika barua Wizarani kuomba kufunga lile bwawa. Sasa kufunga bwawa tafsiri yake ni kwamba uvuvi haramu ndio pekee unaosababisha kutokukua kwa wale samaki. Sasa nilizungumza na mtaalam mmoja ambaye hata Wizara inamtambua kwa umahiri wake akaniambia wale samaki aina ya tilapia wameumbiwa namna ya kujilinda wasipotee.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, panapokuwa na tishio fulani hivi la kimazingira kama ni mabomu ya uvuvi haramu au ni maji kupungua au ni maji kuchafuka huwa wana mature ghafla ili wasipotee wanaishia hapo hapo walipo. Kwa hiyo, ndio maana wote wanakuwa wadogo. Nilipokwenda jimboni mara ya mwisho kwenye weekend hii ya Mei Mosi, watu wananinonesha wanasema Mheshimiwa angalia hawa samaki ni wadogo lakini wana mayai, tena wana watoto na wajukuu tayari lakini ndio wamefikia hapo. Ndio maana kila mvuvi pale anaonekana kuwa ni mvuvi haramu.

Mheshimiwa Spika, sasa nasema kwa vile hatujaona kama wenzetu wa Lake Tanganyika, hatujapata taarifa kwamba kwa nini Serikali inaona ni uvuvi haramu tu na sio sababu zingine za kimazingira zinazofanya wale samaki wengine wasikue? Basi kama ni hivyo ina maana huu ufungaji ni ufungaji wa majaribio (experimental closure). Sasa kama ni experimental closure, tunaomba basi wale wananchi wapatiwe mbadala.

Mheshimiwa Spika, tumesikia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kuna fedha nyingi kwa ajili ya ufugaji wa samaki. Naomba wakati tunafikiria kufunga Bwawa la Nyumba ya Mungu, basi wale wananchi wapatiwe hii miradi ya ufugaji wa samaki. Halmashauri ya Mwanga imewekeza ikajenga Soko la Samaki lenye mpaka jengo la chakula barafu. Sasa hatuwezi kuacha ile facility ikakaa hivi hivi, tufuge samaki ili tuendelee kutumia.

Mheshimiwa Spika, lengo letu kujenga lile Soko la Samaki na jengo la chakula barafu ni kwamba samaki wauziwe mahali pamoja ili tuweze ku-control vizuri masuala ya afya, masuala ya ushuru wa Serikali na yule mtu atakayekuja sokoni na samaki wake wasiuzike aweze kuwaweka kwenye chakula barafu wawe fresh kesho asubuhi. Pia yule anayetaka kusafirisha basi tunamtengenezea wanakaa kwenye temperature inayofaa ili aweze kusafirisha. Kwa hiyo hatutarajii kabisa na wala hatutamani tuone kabisa lile bwawa linafungwa na wale watu wakose chakula, wakose ajira halafu na hii facility kubwa ambayo tumeweka isipate matumizi.

Mheshimiwa Spika, naomba kumalizia kwa kumwomba Mheshimiwa Waziri, baada ya Bajeti hii twende akaangalie eneo lile la Lang’ata jinsi ambavyo halmashauri imewekeza kujenga hizi facility na jinsi ambavyo watu wote wanategemea maisha yao pale kwenye bwawa, halafu ndio atuambie kwamba tunalifunga kwa utaratibu gani.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. Nashukuru sana. (Makofi)
Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kupata fursa hii ya kuwa mchangiaji wa pili katika hoja hii muhimu sana iliyoko mbele ya Bunge lako.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote niishukuru sana Serikali yetu chini ya Mheshimiwa Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa ajili ya kuendelea kupambana kutafuta majibu ya maswali magumu yanayosumbua uchumi na ukuaji wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bandari ni moja kati ya masuala magumu ambayo yana umuhimu mkubwa katika uchumi wa nchi yetu, kwa hiyo kitendo cha kuendelea kuhangaika kutafuta ufumbuzi juu ya suala hili ni jambo ambalo tunapaswa kuliunga mkono na kulipongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo muwasilishaji hoja pamoja na mchangiaji aliyetangulia alivyosema hoja hii imekuja mbele ya Bunge lako chini ya Ibara ya 63(3)(e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ajili ya kujadiliwa na kuridhiwa na Bunge lako hili mwaka 2017 lilishapitisha mwongozo wa jinsi ya kujadili ambao umezingatiwa, Kamati imefanya kazi yake vizuri na tumeona taarifa yake na tunaipongeza kwa taarifa nzuri katika hoja hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili kama alivyozungumza mchangiaji wa kwanza suala hili limeleta taharuki, limeleta hofu katika jamii yetu ya Tanzania moja kwa mambo ambayo pengine ni ya kisiasa yanayoenezwa na watu mbalimbali lakini hofu nyingine tu ni hofu ya kawaida ya hofu ya kitu kipya, hofu ya kitu usichokijua (fear of unknown). (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii inatokana tu na kwamba tumekaa na bandari yetu kwa miaka 60 tumekuwa tukiitumia wenyewe, tunapanda, tunashuka, tunakwenda, tunarudi miaka 60 siyo muda mchache, sasa ghafla unaposikia kwamba uendelezaji wake unachukua mfumo mwingine lazima kunakuwa na hofu ambayo sisi kama Wabunge tunalo jukumu la kuelewa na kuwaelewesha Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nitaangalia zaidi maeneo ambayo huwa yanahojiwa kwenye mkataba. Ukipewa mkataba uuchambue au utoe opinion mojawapo ya mambo ya kwanza kwanza kabisa kujiuliza ni wahusika wa mkataba (parties) kwamba hivi ni nani hawa wanaosaini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkataba huu uko wazi kwamba umesainiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo hiyo hatuna hofu yoyote ya kuifahamu kwa sababu tunaijua ni Serikali yetu, lakini pia pale kwenye preamble imesainiwa na nchi inaitwa The Emirates of Dubai. Sasa the Emirates of Dubai ni sehemu ya Umoja wa Falme ya Nchi za Kiarabu au UAE United Arabs Emirates ambayo ni dola ya Kifalme inayoongozwa na Katiba, it is the constitutional monarchy.

Mheshimiwa Spika, Katiba yake ya mwaka 1971 kama ambavyo imerekebishwa mara nyingi mpka 2004 ndio toleo ambalo lipo sasa hivi inaunda shirikisho lenye hizi Emirates lenye hizi nchi saba ambayo ni Dubai tunayoizungumzia Sharjah, Abu Dhabi, Dubai, Ajman, Umm Al-Quwain, kuna Ras Al Khaimah na Fujairah. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hizi nchi ambazo zinaunda hili shirikisho, shirikisho lina bendera linaundwa Taifa, lakini hizi nchi shiriki zinazounda hili shirikisho pia zina bendera zake na mamlaka yake. Ibara ya 120 ya Katiba ya UAE inataja masuala ya Muungano (union matters) za UAE, inataja masuala ya Muungano ambayo yako 19 katika masuala hayo suala la uwekezaji si sehemu ya masuala ya Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la uwekezaji ni sehemu ya mamlaka ambayo imeachiwa hizi nchi moja moja hizi Emirates. Kwa hiyo, Mkataba wetu huu umesainiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwakilishwa na Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, Waziri wetu wa Miundombinu kwa idhini ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na upande wa The Emirates of Dubai imesainiwa kwa idhini ya Mfalme wa Dubai. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, twende mbali kidogo, Dubai ni absolute monarchy yaani ni nchi ya Kifalme per see ambapo Mfalme akishasaini under seal chini ya ile lakiri yao huo ni mkataba ambao ni halali kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimelizungumza hili kwa sababu mojawapo ya hofu zinazoendelea ni kwamba mbona hapa Rais wetu amesaini na Waziri lakini kule amesaini mkuu wa ile port ni kwa sababu ile ni absolute monarchy na tayari Mfalme yule ameshasaini pale kwenye ule mkataba, ameshatoa idhini yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndivyo ambavyo wenzetu hawa wamekuwa wakiishi mpaka wakageuza jangwa likawa sehemu ambayo dunia nzima inaitamani. Wamenaishi hivyo na wameweza kufikia hatua hiyo katika nchi hiyo katika nchi hii I mean katika dunia hii. Kwa hiyo uwekezaji haupo chini ya yale mambo ya Muungano isipokuwa article 117 ya Katiba hiyo ya UAE inatoa mamlaka kwa kila nchi kushughulikia mambo ya ukuaji wa uchumi na biashara wa nchi zao ili waweze kuchangia kule kwenye union yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo sasa niendelee tu kusema kwamba haya ni makubaliano, makubaliano pia unaweza ukayaita mkataba, lakini haya ninayosema ni makubaliano ya uendelezaji wa bandari zetu chini ya Ibara ya 5(3) cha Mkataba huu, hizi taasisi mbili maana kama ilivyosema Tanzania inamiliki TPA na Dubai inamiliki DP World na hakuna mahali kwenye mkataba huu ambapo DP World imesaini ni hizi Serikali mbili zimesaini ili kujenga mazingira sasa ya haya makampuni yake mawili kushirikiana na chini ya ile Ibara ya 5(3) ya mkataba huu kila panapokuwa na project ambayo TPA na DP World wataingia mkataba kutakuwa na presentation na uwasilishi ambao utaletwa na DP World, TPA italipitia na kulijadili na kusaini mkataba tofauti kwa kila mradi ambao utakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, cha kushauri tu kama ambavyo mwenzangu Profesa Mkumbo alizungumza ni kwamba tunahitaji umakini mkubwa tu wakati wa kusaini hii mikataba mmoja mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimemsikia Mheshimiwa Waziri akieleza mambo ambayo Serikali ime-undertake kuzingatia wakati wa kusaini huo mkataba. Mimi nakubaliana na yale mambo ambayo ameyaorodhesha ikiwa ni pamoja na suala la land right ambalo lipo huku, kwamba kama ambavyio mkataba huu unazungumzia kwamba land right ni juu possession na access na siyo ownership basi hilo liendelee kuzingatiwa hivyo hivyo kama ambavyo mkataba huu kubwa umeweza kusema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mkataba huu unaruhusu marekebisho yaani amendment, unaruhusu termination na Ibara ya 21 inaruhusu matumizi ya sheria za Tanzania katika ile mikataba mmoja mmoja ambayo tutakwenda kuingia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo mimi naunga mkono hoja, na ninawashawishi Wabunge wenzangu tuuridhie mkataba huu, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kupata nafasi hii ya kuchangia bajeti hii muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote ninaishukuru sana Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi chini ya Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na mambo mengi sana ambayo hatuwezi kuyataja yote lakini utekelezaji mzuri wa bajeti ya mwaka 2022/2023 ambayo imetuwezesha sasa kuingia kwenye bajeti hii ya 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi katika Jimbo langu la Mwanga ni mingi ambayo imetekelezwa lakini tunaomba kusisitiza juu ya ukamilishaji wa miradi muhimu ambayo bado inaendelea. Mradi wa kwanza ni Hospitali ya Wilaya ambapo tulitengewa bilioni 3.3 mpaka sasa hivi tumepata bilioni mbili tunaomba hiyo bilioni 1.3 ili tumalizie ile kazi iliyobakia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo mradi mkubwa wa Maji wa Same, Mwanga - Korogwe, tunaishukuru sana Serikali imekwamua mradi huu ambao ulikuwa umekwama tumeahidiwa kukamilika ndani ya miezi 14 na nikuambie tu kwamba kuna mama mmoja aliniita kwenye eneo lile la mradi, amepigilia vijiti 14 kwenye ukuta wake kila mwezi ukipita anang’oa kimoja ananiambia Mheshimiwa Mbunge vinavyozidi kupungua hivi vijiti ndiyo mimi nategemea maji yanywewe. Kwa hiyo, kuna siku atakapong’oa cha mwisho kama maji hayajanywewa tutapata shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Mwanga wana imani kubwa sana kwamba miradi hii itakamilika na sababu kubwa ni mbili, sababu ya kwanza ni kwamba wanamuona Mheshimiwa Rais jinsi ambavyo ameendeleza mahusiano katika diplomasia ya uchumi kiasi ambacho tunaendelea kupata fedha za maendeleo. Pili, kinachowapa imani kubwa ni bajeti hii ambayo kwanza imepanua wigo wa kodi lakini pili imeweka commitment ya kutumia utaratibu wa PPP na pia kufufua Ofisi ya Tax Ombudsman ambayo nayo itatuharakishia fedha kuingia kwenye mzuguko, kodi kulipwa kwa wakati na mambo kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo imani ya watu wa Mwanga ni kwamba kwa sababu hiyo basi, miradi yao itaendelea kutekelezwa vizuri. Wito wangu ni kwamba Serikali iendelee ku-negotiate vizuri mikataba ya PPP, tui-negotiate kibingwa ili tuweze kupata faida tunayostahili sisi kama wananchi wa Tanzania. Ile mikataba inayofanya vizuri tuendelee kuiheshimu kama mkataba wa SONGAS kwa mfano, ni moja kati ya PPP ambazo kwa ufahamu wangu zimetuletea heshima kubwa sana kama nchi tujifunze kwamba tulifanya nini hawa SONGAS wakatufanikisha kiasi hicho tuendelee kuutunza mkataba huu lakini pia tuendelee kuingia mikataba mingine mizuri kama huu wa SONGAS ambao unaendelea vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipo kilio kikubwa sana ambacho kinasumbua katika nchi hii kwa sasa hivi, nacho ni suala la wakandarasi wazalendo na malimbikizo ya madai yao katika miradi ambayo wanaifanya. Wako wakandarasi wengi sana ambao wanashikilia certificate sasa hivi zaidi ya miezi tisa na hawajalipwa na wameanza kukata tamaa, wameanza kufilisiwa na mabenki kwa dhamana zao kuuzwa, lakini kikubwa pia ni kwamba pamoja na kwamba wakati mwingine tunapata hasara ya kulipa interest lakini ile interest ile riba haisaidii chochote kwao, kwa sababu wamekopa benki kwa riba kubwa za asilimia 20 halafu fedha zikichelewa ile riba inazidi kukusanyika wakati wao huku riba wanayolipwa ni kidogo sana kwa mujibu wa Mkataba. Kwa hiyo, wanaendelea kwenda chini na pia iko hatari ya mabenki kufikia mahali kuona kwamba miradi hii ya Serikali ni miradi hatarishi jambo ambalo si jema na wala halifai kwa afya ya uchumi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais amekuwa akisisitiza mara nyingi kwamba walipwe kwa wakati ili tuweze kukwepa riba hizi ambazo Serikali upande mmoja inapata hasara lakini pia wakandarasi wetu wanazidi kupata hasara kwa sababu riba ile ni ndogo ukilinganisha na riba ambayo wanalipa kwenye mabenki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nishauri tu juu suala la Tax Ombudsman ambalo nimelizungumza, nimejaribu kuangalia kanuni zilizotengenezwa mwaka jana kwa bahati mbaya zinaleta mlolongo mrefu kidogo wa jambo kuamuliwa mbele ya ile Ofisi ya Tax Ombudsman. Ukiangalia zile notice zinavyokwenda ni karibu siku 154 kwa shauri moja kuamuliwa, hiyo inaweza iturudishe kulekule ambako kulikuwa na mlolongo wa kwenda kwa Kamishna halafu uende TRAB, uende TRAT uende Mahakama ya Rufaa unatumia karibu miaka mitano. Nchi jirani hapo mwaka 2016/2017 Ofisi ya Tax Ombudsman ilishugulikia masuala ya malalamiko 92,000 na ikafanikiwa kuamua 77,000 na hiyo ni kwa sababu regulation zao kidogo zinachukua muda mfupi kukamilisha malalamiko ambayo yamepelekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vinginevyo mimi kwa kweli ninaunga mkono bajeti hii kwa asilimia zote, nikitarajia kabisa kwamba kasi ya miradi iliyokuwa ikienda katika Majimbo yetu hasa Jimbo langu la Mwanga itaendelea kama vile ambavyo imekuwa ikiendelea na pengine kwa kasi zaidi kutokana na jinsi ambavyo bajeti hii imeleta matumaini makubwa. Mheshimiwa Waziri tukupongeze na tukushukuru unatuwakilisha vizuri katika sekta yako na kwa kweli tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kukuamini kama ambavyo sisi tumeweza pia kukuamini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru sana kupata nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, niungane na wenzangu wote kumpongeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoendelea kufanya kwa ajili ya nchi yetu. Tanzania inaona na dunia inaona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake, kazi yao ni nzuri na wametuletea bajeti yenye matumaini makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yuko mdau mmoja wa mambo ya uchumi alikuwa akizungumza juzi juzi kwamba utajiri uliyoko juu ya ardhi ni mkubwa kuliko ulioko chini ya ardhi. Utajiri ulioko juu ya ardhi ni katika maana ya kilimo na ulioko chini ya ardhi katika maana ya madini. Kinachokosekana tu ni uwekezaji. Kwa uchumi kama wa kwetu ambao unategemea wakulima wadogo, kilichokuwa kinakosekama ni kile ambacho kipo kwenye ukurasa wa 14 wa Hotuba ya Bajeti ya Waziri kuongeza nguvu kwenye utafiti, kuongeza nguvu kwenye ugani, umwagiliaji na ubora wa mbegu. Yakitekelezwa haya kama Mheshimiwa Waziri alivyotuletea, basi nadhani maneno haya ya mdau huyu yatatimia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo langu la Mwanga maeneo yote ya milimani yalikuwa yakitegemea zaidi uchumi wa kahawa ambao hapo katika ulidorora kidogo kutokana na matatizo haya ya ugani pengine na masoko, lakini sasa hivi ari kubwa ya kahawa imerudi. Tunachoiomba Serikali ni kupatiwa mbegu tu, yaani miche ambayo inahimili hali ya kule milimani ambayo pia haihitaji dawa nyingi kwa ajili ya kukua na kustawi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninazo skimu tatu kubwa za umwagiliaji. Kwanza ni Skimu ya Kirya ambayo nashukuru sana kwamba tulipata fedha inaendelea. Potential ya ile skimu ni hekta 1,600, lakini Mkandarasi aliyeko site akikamilisha tutaweza kutumia hekta 950. Tunashukuru na tunaamini tutaendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, skimu ya pili ni ya Kivulini Kileo ambayo ina potential ya hekta 1,550, lakini zinazotumika ni hekta 712. Tunaomba tupatiwe fedha ya kumalizia ili skimu hii ifanye kazi kwa asilimia 100. Pia tupatiwe maghala na mashine za kukaushia mpunga. Kwa sasa hivi wanaanika nje, hali ambayo haileti ubora mzuri wa mpunga.

Mheshimiwa Naibu Spika, skimu yetu ya tatu ni Skimu ya Kigonigoni. Mheshimiwa Waziri nakushukuru, ulipokuwa Naibu Waziri ulikuja Kilimanjaro ukanipa breakfast pale Kili Wanders, nami sikulipa, ni wewe ulilipa, nakushukuru sana. Ukanishauri juu ya Skimu hii ya Kigonigoni kwamba tutafute fedha tufanye upembuzi yakinifu. Tulifanya hivyo na hiyo kazi imefanyika, sasa hivi wako kwenye designing. Ile skimu ina potential kubwa sana ya hekta 2,300.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachoomba Mheshimiwa Waziri ni kwamba tutakapokamilisha upembuzi yakinifu hivi karibuni, basi tusaidiwe fedha kupitia kwa wadau wa maendeleo kama IDF na JICA tusije tukasubiri tena bajeti ijayo. Naamini kabisa tutakamilisha upembuzi yakinifu ndani ya muda kwa sababu umetupa kijana mzuri sana, Eng. Said pale Mkoa wa Kilimanjaro. Tunachoomba tu ni kwamba aongezewe nguvu hasa manpower kwa sababu wataalam pale ni wachache na wanakimbiza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ajili ya muda, naomba nimalizie mchango wangu hapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, naunga mkono hoja.
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa Duniani na kupewa Tuzo ya mafanikio ya ujenzi wa miundombinu
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata nafasi hii. Nami niungane na wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya heshima kubwa ambayo ameiletea nchi yetu. Tuzo hii ya Babacar N’Diaye, 2022 imetolewa kwa mtu mashuhuri. Nilikuwa naangalia tofauti kati ya mashuhuri na maarufu. Mashuhuri ni mtu ambaye amejulikana kwa jambo jema, maarufu anaweza akawa hata maarufu kwa mambo mabaya. Kwa hiyo, sasa tuna Rais ambaye ni mashuhuri duniani amejulikana pamoja na mambo mengine ujenzi wa miundombinu ya usafiri na usafirishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais alipoapishwa mojawapo ya kauli mbiu zake kubwa sana ni kuifungua nchi na kukuza uchumi. Uchumi na miundombinu ni sawasawa na chakula na vyombo vya kulia chakula. Miundombinu ndiyo inayofikisha uchumi kwa wananchi. Kwa hiyo, mtu unaweza ukakuza uchumi wa nchi yako. Sasa, kama miundombinu hakuna faida zile zitashindwa kufika kwa wananchi wako. Kwa hiyo, tumpongeze sana Mheshimiwa Rais kwasababu amedhamiria kwamba uchumi huu unaokuzwa uwafikie wananchi hasa wale wa maeneo ya vijiji; na ndiyo maana tunapata fedha nyingi kwa ajili ya barabara za vijijini na maeneo mengine. Nchi hii ni pana sana, ina eneo kubwa, inahitaji mtu mashuhuri kuweza kutengeneza miundombinu ya kufikia nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli pamoja na yote ambayo yamesema juu ya miradi tunayoiona kwa macho yetu, miradi ya reli, ndege, meli na kadhalika lakini hayo sisi Watanzania tunayaona kabisa na wala hatuna haja ya kuambiwa na mtu. Kinachonifurahisha ni kwamba hata dunia imeona haya yanayofanyika na kuweza kumfikisha Mama hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la pili, ningependa, kwa vile makao makuu ni hapa Dodoma na Bunge hili tunazungumzia kutoka Dodoma; nilisoma taarifa ya tathimini ya ile Tume iliyotoa zawadi hii, mojawapo ya vitu ambavyo walivizungumzia ni barabara hii ya ring-road ya Dodoma. Kwa hiyo, ni matumaini yangu kwamba watendaji wetu watahakikisha kwamba inamalizika kwa wakati ili mwaka ujao tupate zawadi nyingine kubwa zaidi kuliko hii ambayo tumepata kwa sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie tu hotuba ya Mheshimiwa Rais wakati anapokea tuzo hii jinsi ambavyo imetuma ujumbe kwa dunia. Jambo la kwanza ambalo nimeli-note kwa umuhimu sana, ni kwamba Mheshimiwa Rais wakati anapokea tuzo hii alitambua mchango wa watangulizi wake katika kufikia hapo alipofikia. Kipekee kabisa alitambua mchango wa Serikali ya Awamu ya nne chini ya Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, akatambua Awamu ya Tano chini ya Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huu ni ujumbe kwa Afrika, kwamba nchi inapokuwa na utaratibu wa kubadilishana madaraka kwa amani na kwa katiba na sheria wananchi wanapata faida kubwa ya muendelezo wa mambo mema ambayo yalikuwa yakifanyika tofauti na pale ambapo tunabadilishana kwa kupambana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili liko jambo ambalo limejibiwa kwa vitendo na tuzo hii. Pamekuwa na dhana kubwa kwamba tunahitaji maono ya Kitaifa. Fine, lakini sasa hapa kuna majibu ya vitendo, kwamba kuna uendelezaji wa mambo ya awamu zilizopita, na siyo kwamba kila awamu inapokuja ina jambo lake. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kipekee kabisa, nalipongeze Bunge lako Tukufu kwa kuja na azimio hili, nampongeza kipekee dada yangu Mheshimiwa Zainab Katimba, kwa kutuongoza kwenye hili na ninaunga mkono hoja hii na ninaomba Waheshimiwa Wabunge tuunge mkono hoja hii kwa nguvu zetu zote, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa Mwaka 2021 (Toleo la Kiingereza)
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata nafasi hii ya kuchangia hoja hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niipongeze Serikali kwa kutuletea Muswada huu katika wakati huu ambao ni muafaka. Naomba nieleze kabisa hapo kwamba mimi nimekuwa Wakili wa Kujitegemea kwa takribani miaka 25 sasa, kwa hiyo, nimeshuhudia hizi changamoto zinazozungumziwa juu ya ugumu wa kupata haki au wa kufikia haki kwa kutumia lugha ambayo si ya mhusika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mahakimu wetu na Majaji na Waendesha Mashtaka wamepata taabu kidogo katika kuendesha mashauri wakati ambapo sheria inataka yawe kwa kiingereza. Kwa hiyo, wanasikiliza kwa Kiswahili, wanaandika kwa Kiingereza baadaye wanaandika hukumu kwa kiingereza, lakini wanapata taabu tena kuanza kuwatafsiria watu na mtu anasomewa shitaka inabidi litafsiriwe kwanza. Kwa hiyo, kwa kweli imekuwa ikileta changamoto kubwa. Niwapongeze Mahakimu wetu, Majaji na wadau wengine wamejitahidi sana katika kwenda katika ugumu huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka mwaka 2007 Mahakama za Kazi zilishatutangulia, ziliundwa zile Labour Court Rules (Kanuni za Sheria za Mahakama za Kazi za mwaka 2007) ambazo ziliruhusu matumizi ya Kiswahili. Kwa hiyo, Mahakama zetu zimefanya juhudi kubwa, na zipo hukumu nyingi za kuanzia wakati wa Mheshimiwa Marehemu Jaji Mwaipopo, Jaji Rweyemamu na hata Jaji Samatta katika hukumu ile ya Kesi ya Dibagula, ile kesi maarufu iliyotokea Morogoro, walijitahidi kufanya hivyo. (Makofi)

Sasa tunapofikia mahali pa kuwatungia sheria nadhani tunairahisisha hii kazi, itafanyika vizuri na ninaamini sasa Serikali itawekeza, kwa hiyo, hata ile shida, changamoto walizokuwa wanapata zitapungua na haki itatendeka kwa vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeandikwa kwa Kiswahili na Kiingereza, lakini kwa kutambua umuhimu wa Kiswahili kama lugha ya wengi, imeelekezwa kwamba panapokuwa na mgongano basi ile tafsiri ya Kiswahili ndiyo ambayo itazingatiwa. Sasa umefika wakati kwa sheria zetu ambazo zinatungwa chini ya mamlaka ya Katiba hiyo hiyo nazo pia zitungwe kwa Kiswahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo huo tukumbuke kwamba katika mihimili mitatu ambayo inaundwa chini ya Katiba yetu; Serikali, Bunge na Mahakama, mihimili miwili tayari inatumia lugha ya Kiswahili, umebakia Mhimili mmoja tu wa Mahakama. Nadhani sababu ya kutumia Kiswahili katika mihimili hii miwili ni kuwezesha huduma yake kufika kirahisi na wale wahudumiwa/wananchi, waweze kuifikia hii mihimili. Mahakama imebaki peke yake, wakati umefika sasa mahakama nayo itumie Kiswahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Taarifa ya Kamati ilivyoeleza ni kwamba kile kifungu cha 84(1) kinaelekeza kwamba lugha ya Mahakama zetu na vyombo vingine vya kutoa haki iwe Kiswahili na hiyo ni kwa sababu ya kuwahudumia walio wengi. Lakini kifungu hiki cha 84(2) kinazungumzia sasa haki za wale walio wachache kwamba endapo watu watakuja Mahakamani na wanapenda kesi yao iende kwa Kiingereza basi wanaruhusiwa pia kufanya hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tusipofanya hivyo tukakamilisha huu Muswada kama ulivyoletwa nadhani tutaingia kwenye tatizo, wanaharakati wanaweza siku moja wakajitokeza hata wakatushtaki kwamba tunaingia kwenye lile kosa, sasa unisamehe kwamba lazima nitumie Kiingereza kuna kitu wanaita class legislation, kwamba tunatunga sheria ambazo zinahangaika na tabaka moja tu.

Lakini katika kutibu hilo kuna kitu wanaita reasonable classification ambacho ndicho kilichofanyika hapa; kwamba tunawahudumia wale walio wengi lakini pia wale walio wachache nao pia wanapata nafasi ndani ya sheria hiyo hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Muswada huu ni wa kihistoria, kwa hiyo ni vizuri tukaupitisha kwa umakini wote. Lakini pia naamini Serikali itawekeza ipasavyo katika ku- manage hiki kipindi cha mpito ili sheria hizi zitafsiriwe vizuri na tufikie mahali ambapo tutaendesha mashauri yetu kwa lugha ya Kiswahili bila kuathiri haki za watu na bila kuwapa ugumu utakaokwamisha utoaji haki wale ambao wanahusika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata ukienda kwenye mpango ambao tumemaliza kuujadili siku ya leo, unasisitiza juu ya suala la utawala bora. Utawala bora utafikiwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na 2) wa Mwaka 2021 (Toleo la Kiingereza)
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kupata nafasi ya mwisho kuchangia. Hoja ya Wakili Msomi au sio msomi siku nyingine ukinipa nafasi nitaizungumzia vizuri kwa sababu Mheshimiwa Jaji Barnabas Samatta aliyekuwa Jaji Mkuu wa Tanzania aliwahi kutoa definition nzuri sana ya who is a learned person ambayo sijaona mahali pengine popote, siku nikipata nafasi hiyo tutayasema. Hatujiiti wasomi ila watu wanatuita wasomi, inaonekana wanatuona tumesoma. Ahsante sana.

SPIKA: Kesho tutakuwa na muda wa kutosha, mjiandae mawakili wasomi kuna sheria tutakuwa tunajadili na hiyo nayo tutapenda mlisomeshe, siyo Wabunge tu lakini mlisomeshe Taifa pia. (Makofi)

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, ataanza Mwanasheria Mkuu kwa sababu yeye ndiye Advocate Number One.

SPIKA: Ahsante endelea Mheshimiwa na dakika zako tunakulindia. (Kicheko)

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, kwanza mimi nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kuleta Muswada huu katika wakati huu muafaka na hasa Muswada wa Marekebisho unaohusu Sheria ya Makampuni Sura 212 ambayo ndiyo sana nitakayozungumzia pamoja na kwamba nitazungumza kidogo kama muda utaruhusu juu ya Sheria ya Mahakama za Mahakimu.

Mheshimiwa Spika, Muswada huu umeletwa kwa wakati muafaka kwa sababu Serikali ya Awamu ya Sita imejipambanua wazi kabisa kwamba inaweka sekta binafsi mbele kama engine ya maendeleo na Sheria hii ya Makampuni inahusu zaidi Sekta Binafsi. Kwa hiyo, ni muhimu kabisa sheria hii ipitiwe vizuri na ifanyiwe marekebisho kila wakati na ije tu tutaendelea kuifanya.

Mheshimiwa Spika, ninamshukuru sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na timu yake walikuwa na ushirikiano mkubwa sana kwenye Kamati. Tumejadiliana na kama ambavyo imesemekana hapa ni kwamba maeneo mengi tulikubaliana na yamekuja vizuri tu kama ambavyo tuliweza kufikia muafaka, hiyo ni kazi yetu na wala hatuhitaji kupongezwa au kuona kwamba mtu mwingine hakufanya kazi yake wakati tumewekwa kwa ajili hiyo ya kushirikiana ili tupate document ambayo inafaa kwa manufaa ya nchi yetu. Kwa hiyo, nitakazia tu marekebisho ya ile Ibara ya 30 ambayo imeitwa hapa kwamba ni hatari, ukasema tu-sanitize kwanza lakini mimi sijaona hatari mpaka sasa hivi kama ambavyo nitaeleza. Nitazungumzia pia Ibara ya 36 pamoja na ile Ibara inayohusiana na Sheria ya Mahakama za Mahakimu.

Mheshimiwa Spika, nikianza na Ibara ile ya 30 iliyoitwa kwamba ni ya hatari, labda nianzie mwisho ndiyo nirudi mwanzo. Mimi sioni tatizo linakopatikana kwa sababu Kamati yako kwa umakini wake ililiona hili, tukalizungumza na Serikali, tukawashauri na wakakubali kuondoa kile kifungu. Hata ukienda kwenye schedule of amendment (f) pale, kama utaniruhusu kusoma inasema ‘in clause 30 by deleting the proposed subsection 5’ sasa kama Serikali ilishakubali ikafuta, hiyo hatari sasa sijui inatoka tena wapi.

SPIKA: Unajua Mbunge mwingine anapokuja, anakuja ana ile Bill, zile amendment labda za Serikali au nini hajaziona. Kwa hiyo, mengine tunasameheana tu. Endelea Mheshimiwa.

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, hata kama basi zile amendment hazikuonekana, hoja iliyotolewa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali hapa ukurasa ule wa Tisa kama utaniruhusu pia kurejea ‘aidha, kufuatia maoni ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, Serikai kupitia jedwali la marekebisho imefanya marekebisho kwa kufuta mapendekezo ya Kifungu (5) kilichokuwa kinazuia watu waliowahi kutiwa hatiani katika makosa fulani kuanzisha makampuni ili kuondoa uwezekano wa watu hao kuadhibiwa mara mbili kwa kosa moja’ (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme tu kwamba hii hatari ambayo imesemekana hapa tukajichanganya changanya haipo na tusipate hiyo impression kwamba kuna hatari yoyote. Tulizungumza kwenye Kamati vizuri na Serikali, wakatuelewa. Schedule of amendment imekuja, wameondoa kile na hoja ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imesema wazi. Kwa hiyo, sioni hapa kama kuna tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo tu kwamba Serikali iliamua kukiondoa tu kwa sababu imekiondoa lakini ziko sababu kama ambavyo tumezungumza kwamba suala la kuanzisha kampuni linahusiana na haki ya mtu kumiliki mali ambayo ni haki ya Kikatiba. Sasa ile haki tunailinda kwa sababu tunataka Watanzania wa-enjoy hiyo haki na hata wawekezaji wa nje wanaokuja waweze kufurahia hiyo haki. Mtu akishahukumiwa akatumikia adhabu yake, akaimaliza anabakia kuwa mtu msafi tu na ndiyo maana kuna utetezi kwamba ukinifungulia kesi ambayo nilishahukumiwa nayo ule ni utetezi tayari. Sasa naogopa tena hili neno la wasomi lakini kuna lugha ya kilatini hiyo defense inaitwa autrefois acquit kwamba nilishafunguliwa hii na nikaachiliwa huru kwa hiyo, huwezi tena ukanifungulia kesi hiyo hiyo ukanitia hatiani. Sorry, hiyo ni autrefois convict kwamba ulishanifungulia hiyo, ukanitia hatiani, nika-serve sentence yangu nikamaliza sasa huwezi tena kunishtaki mara ya pili au nipate madhara yoyote yanayotokana na ile hukumu hilo halipo na Serikali ililizingatia vizuri ndiyo maana wakafuta hiki kifungu. Kwa hiyo, nadhani tupate amani katika hilo.

Mheshimiwa Spika, pia lazima tukumbuke pia kwamba mtu anapokwenda gerezani kwa mfano kwenye ile adhabu anaenda kule kurekebishwa. Magereza yetu yanafanya vizuri, anarekebishwa akitoka kule ni mtu salama anaweza akafanya kitu. Kama kuna muda wa uangalizi kwa mfano katika mambo ya kugombea wanayosema kwamba labda baada ya miaka fulani hiyo ni sawa, unaweza ukawekewa muda wa probation wa kutazamwa lakini siyo kukatazwa milele na milele haikuwa hivyo na ndivyo ambavyo sheria hii inakuja.

Mheshimiwa Spika, pia kabla sijazungumzia Kifungu kingine cha Sheria ya Makampuni niongelee pale kwenye Sheria ya Mahakama za Mahakimu kwa sababu pia kama nilisikia vizuri nilizungumza hapa kwamba wale Wazee wa Baraza (Assessors) wameondolewa hata hilo naona siyo sahihi kwa sababu ukienda kwenye jedwali la marekebisho ile schedule of amendment Ibara ya 54 labda nisisome yote kwa sababu ni ndefu lakini wale Wazee wa Baraza wameondolewa bado wapo katika kesi zote ambazo zinahusiana na Sheria za Kimila na sheria za Kiislam na haya ndiyo mambo yanayohitaji Wazee wa Baraza kwa sababu mimi naweza nikaenda Tadayo Mpare hapa na digrii yangu nakwenda kule Mwanza, natakiwa kuhukumu hata kama nina digrii lakini natakiwa kuhukumu kesi katika sheria za kimila za Wasukuma, nahitaji Mzee wa Kisukuma pale aje aweze kunisaidia juu ya zile mila na mimi niangalie sasa kama kwenye sheria za kimila zinazokubalika haikinzani na Katiba niweze kuamua nimeshauri, hivyo hata hilo pia sioni kama kuna tatizo hapo labda tu watu walikuwa hawajajielekeza vizuri kwenye jedwali hili la marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho nirudi tena kwenye Sheria ya Makampuni ile Ibara ya 36 ambayo imepunguza umri wa watu kuruhusiwa kuwa Directors na imeondoa ule ukomo wa juu. Hili niipongeze Serikali kwa sababu kwa kweli tulikuwa tumechelewa. Maeneo mengi sana ambayo nimepitia Sheria hizi za Makampuni, age of majority mtu anaruhusiwa ni miaka 18 na umri wa juu hakuna haja, mtu ana kampuni yake, anataka Mkurugenzi anaona mtu ana miaka 75 lakini ana busara, akili kiwembe kinakata, muacheni aendelee kufanya kazi, aendelee kupata haki yake ya kipato na pia tuendelee kufaidika na ile akili yake ambayo anayo.

Mheshimiwa Spika, labda hapa wito tu ni kwamba marekebisho kama haya yanapofanyika basi ni vizuri sasa wataalam wetu wa elimu nao katika mifumo na mitaala basi wajielekeze hivyo sasa. Wasomi wetu wanaandaliwa kuhakikisha kwamba vijana wetu wanaandaliwa…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa!

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, ni kengele ya pili.

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, basi naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii. Awali ya yote niungane na wenzangu wote kumpongeza Mheshimiwa Rais, Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwanza kwa kuweza kuendeleza kwa kasi mambo yote yaliyokuwa yakifanywa na Serikali ya Awamu ya Tano, lakini pili kama alivyoahidi mwenyewe, kuleta mambo mengine mapya mazuri kwa ajili ya nchi yetu na mojawapo ya mambo mapya ambayo ameyaleta ni bajeti hii ambayo leo hii tunaendelea kuijadili hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nampongeza sana Ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba pamoja na Naibu wake na timu yote kwa kuaminiwa kuleta na baadaye kusimamia bajeti hii ambayo imeamsha matumaini makubwa sana kwa Watanzania katika Nyanja mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo kazi kubwa sasa ambayo inahitaji uzalendo mkubwa sana ya kusimamia haya ambayo tumeyakusudia na kuyapitisha kwenye bajeti hii. Yako mambo ambayo yanahitaji umakini na ushirikiano mkubwa siyo wa TRA au Wizara ya Fedha peke yake, lakini Wizara nyingine pia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, yale marekebisho yaliyopendekezwa Kifungu cha 35 cha Sheria ya Usimamizi wa Kodi, Sura ya 438, juu ya kuwataka wale ambao wanaweka kumbukumbu zao ki-electronic kuwa na servers hapa Tanzania. Kubaini jambo kama hili kwamba ni yupi anayo server hapa ndani na yupi hana, linahitaji ushirikiano mkubwa na pia ni uzalendo, kwa sababu watu hawa wanakuja na teknolojia, kama wanakuja kwenye vita ya kiuchumi. Kwa hiyo, tunahitaji umakini wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala zima la kodi, kunakuwa na pande mbili; kuna upande wa Serikali ambayo ndiyo inasimamia kutoza kodi halafu kuna upande wa yule mlipa kodi. Sasa kwa upande wa Serikali, majukumu yake nafikiri yanaeleweka, ambayo tumeyaona sana kwenye bajeti hii yakizingatiwa ya kuweka mazingira wezeshi ya kumwezesha yule mlipa kodi kuzalisha ili aweze kupata kodi ya kulipa, na pia kutoza kodi au kuweka viwango vya kodi ambavyo vinashabihiana na kipato cha yule mlipa kodi; tatu, kuwa na mifumo rafiki ya ukusanyaji kodi; na la nne, kuweka sheria zisizo na utata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria za Kodi zinapaswa kuwa sheria ambazo hazina utata, kwa sababu kodi mwisho wa siku inagusa haki ya kikatiba ya mtu ya haki ya kumiliki mali. Kwa hiyo, sheria zake zinapaswa ziwe precise na ziwe pia rahisi kueleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe tu mfano wa sheria moja ambayo utata wake unaleta matatizo kwa watu. Kifungu cha 90 cha Sheria ya Kodi ya Mapato (Income Tax Act) kinachozungumzia juu ya masuala ya Capital Gain Tax; kifungu kile hakikuwa wazi juu ya suala la mtu anapotoa ardhi yake au mali yake kwa ule mfumo ambao tunasema wa natural love and affection kama baba anapompa mtoto au babu anapompa mjukuu. Sheria pale haikuweka wazi kwamba hawa hawatalipa Capital Gain Tax kwa sababu Capital Gain Tax ni pale ambapo mtu anapata faida inayotokana na kile alicholipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake ziko property nyingi ambazo zimekaa bila umiliki wake kurasimishwa kwa sababu wale wazee wanaowapa watoto wao au wababa wanaowapa wake zao au akinamama wanaowapa waume zao wanakuwa pengine wakati huo hawawezi kulipa capital gain tax na in fact hawapaswi kulipa. Kwa hiyo hii ndio inanifanya niseme kwamba sheria ya kodi inapaswa kuwa precise na pia iwe rahisi katika kuitafsiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jukumu lingine la Serikali ambalo hasa linakwenda sana kwa walipa kodi wadogo ni kutoa elimu ya mlipakodi. Wakati mwingine watu wanakuwa waoga wa kodi kwa sababu tu ya kukosa elimu ya mlipa kodi. Utakuta mtu mdogo ana-raise invoice yake analipwa lakini anakatwa withholding tax, lakini kufuatilia apate ile withholding tax certificate ili aweze kupata ile benefit ya ile kodi, anakuwa hajui hilo. Kwa hiyo mwisho wa siku mtu ana mzigo mkubwa wa kodi, lakini kumbe anazo nafuu nyingine ambazo angeweza akazipata ndani ya mfumo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona marekebisho ya ile Sheria ya Mikopo na Dhamana za Serikali, Sura ya 134 juu ya masuala yale ya guarantee ya Serikali. Kwa kweli nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake kwa hili kwa sababu lilikuwa ni moja ya mambo ambayo yalikuwa yanashangaza kidogo pale ambapo tunakataa au tunachelewa bila sababu kwa muda mrefu kutoa hizi dhamana wakati ambapo mtu anataka kufanya biashara. Ilikuwa inaonekana kama vile pengine hatuwaamini wafanyabiashara wetu. Hili ni jambo zuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kile kifungu cha 10 cha Sheria ya Kodi ambacho kinampa mamlaka Waziri kutoa msamaha kwa ile miradi ambayo ina wafadhili. Matumaini yangu ni kwamba katika utekelezaji wake Mheshimiwa Waziri atalisimamia kwa karibu kwa sababu kifungu hiki kimekuwa na changamoto, utakuta labda kuna mradi wa wafadhili wa package nzima labda ni dola milioni 20, halafu ikagawanyika katika miradi labda 20. Sasa yapo maeneo mengine na nilishuhudia hili kwangu kwamba, unapofika wakati yule mzabuni anatekeleza ule mradi, anakuwa hapati ule msamaha wa kodi mpaka apate barua rasmi kwa ajili ya mradi ule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, utakuta iko GN kwa ajili ya kusamehe miradi yote iliyofadhiliwa na yule mfadhili, lakini bado inatakiwa tena ipatikane barua kwa kila mradi. Sasa usumbufu ule wakati mwingine miradi inatekelezwa mahali ambapo ni mbali kidogo, ni remote, imekuwa ikileta shida kubwa kidogo. Naamini Mheshimiwa Waziri kwa umakini wake ambao tunaufahamu, atalisimamia kwa karibu hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia suala la Tax Ombudsman, limekuwepo lakini naona utekelezaji wake umekuwa sio wa makini sana. Hata hivyo, kwa jinsi ambavyo limekuja sasa hivi naamini kabisa litatekelezwa. Tax Ombudsman itatusaidia sana kwanza kumpa nafuu mlipakodi, kwamba halazimiki kwenda kupitia ile mifumo ambayo ni migumu, lakini pia itaondoa adha ya kodi zetu nyingi kushikiliwa kwenye hii mifumo ya kikesi kesi ambayo imekuwa mahakamani au kwenye mabaraza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachokiomba na kukishauri ni kwamba uteuzi wa hii Tax Ombudsman uzingatie sana weledi na uwezo. Pia zile kanuni zitakazotengenezwa, zisiwe tena ngumu zikafanya tena watu wakabaki kuchelewa kama ambavyo ilikuwa kwenye mahakama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na namshukuru sana Mheshimiwa Waziri na kumpongeza na timu yake. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Na.3 wa Mwaka 2021 (Toleo la Kiingereza)
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kupata nafasi hii ya kuwa mchangiaji wa kwanza wa Muswada huu. La kwanza niishukuru Serikali kwa hatua hii ambayo wamefikia katika mkataba huu muhimu kwa ajili ya uchumi wa nchi yetu, nadhani hii ni hatua muhimu ya kuifungua nchi yetu kama jinsi ambavyo Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassani amekuwa akisisitiza kwamba lazima tufungue nchi yetu ili tuweze kukuza uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hatua hii inatuma ujumbe mwafaka kabisa kwa Dunia kwamba Tanzania sasa haiko kwa ajili ya mikataba tu ya kuhifadhi ya wakimbizi na kusuluhisha migogoro ya kimataifa, tuko pia kwa ajili ya mikataba hii muhimu ya uchumi ambayo haigusi Tanzania peke yake lakini inagusa dunia pia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu utakuwa mfupi tu kama ambavyo Mwanasheria Mkuu wa Serikali amewasilisha kwa umarihiri kabisa kwamba hii ni intergovernmental agreement ambayo sisi siyo wa kwanza kuanza mkataba kama huu, mikataba kama hii iko sehemu nyingi duniani na hasa maeneo ya Asia. Nimejaribu kupitia intergovernmental agreement ya dry ports ambayo katika nchi za Asia na Pacific imehusisha nchi zaidi ya 16, halafu iko intergovernmental agreement ya Asia na high way network ambayo imehusisha nchi zaidi ya 11.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangali hii mikataba yote katika ibara ya ile ya tatu huwa liko sharti moja ambalo linaweka vitu inaita options mbili, ya kwanza ni kwamba nchi inayotia saini mkataba haina sheria au aijaingia kwenye mikataba mingine ambayo itazuia au kukwamisha utekelezaji wa mkataba husika option ya kwanza, na ya pili ni kwamba hatutatunga sheria au kuingia katika mikataba inayozuia utekelezaji wa mkataba huu. Sasa nadhani hili sasa kwa kuitikia hilo ndiyo maana Muswada huu ukawa umeletwa hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na tusingefanya hivyo hata wawekezaji tusingepata kwa sababu mkataba ambao haujazingatia hii Act 3 (3) unachukuliwa kwamba ni low security agreement yaani ni mkataba ambao una-risk kubwa kwa hiyo hauwi bankable hamuwezi kupata mwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hatua hii nzuri ambayo imefikiwa mimi labda nishauri kwa sababu mkataba unaweza mzuri sana na mara nyingi matatizo ya mkataba huwa hayaanzi mwanzoni, matatizo yanakuja baadaye wakati wa utekelezaji changamoto mbalimbali zinapoanza kutokeza au pengine hata faida zinapoanza kupatikana ndipo matatizo huwa yanaanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Serikali inahitaji kuwa na timu ya wataalamu kwa ajili ya usimamizi wa mkataba huu, katika hizi hii mikataba mingine miwili niliyoitaja ya kimataifa wana kitu kinaitwa working group ambayo siku zote iko pale kazi yake ni kutazama mkataba unavyo tekelezwa kila siku na kama kuna matatizo kutoa ushauri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na timu hizi, sina mashaka juu ya wataalamu wetu kwa sababu hata waliokuja mbele ya kamati kwa kweli wamejieleza vizuri sana mpaka tukawaelewa. Lakini sasa utakuta watu hao hao ndiyo tunategemea kwenye mambo mengi kwa hiyo wako busy. Sasa kwa wenzetu huko Asia wanachofanya ni kwamba wanakuwa na timu ya wataalamu wabobevu kwenye lile eneo ambalo ni wastaafu, ambao wanakaa pembeni kazi yao ni kuishauri hii working group ambayo iko kazini sasa hivi na kwa wenzetu kule mara nyingi huwa wanafanya bure au kwa lugha zile wanaita pro bono, wao kazi yao ni kutazama ule mkataba unavyoendelea kama kuna matatizo wanawashauri ile working group halafu inaleta mapendekezo ya marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kila mkataba wa namna hii unayo sehemu ya marekebisho na ambayo inataratibu zake na timelines, kwa hiyo ni vizuri kabisa kwamba pamoja na kusaini mkataba mzuri lakini tuwe macho sana katika usimamizi na ninasema hivyo. Kwa sababu, mkataba huu siyo mkataba mdogo tunaweza tukadhani labda tunasaini mkataba na total hii ya Ufaransa lakini katika cooperate world unaweza ukakuta hii total ya Ufaransa wanahisa wake wanatoka dunia nzima na ni makampuni makubwa na nyeti sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kila tunachokifanya dunia nzima inapata taarifa kwamba tumefanya nini? Na kama kuna ambao hawatutakii mema pia wanakuwa wanapata habari kwamba nini kinaendelea. Kwa hiyo, tunahitaji kuwa makini na pia ni jambo la kujivunia kwa sababu ukiangalia kwenye shareholding ya Total yako makampuni yanafanya mambo makubwa sana ya mazingira ya kidunia na hata ku-sponsor vitu vikubwa vikubwa kama mashindano ya Ragbi na kadhalika. Kwa hiyo, nadhani na sisi tunaenda kuwa sehumu ya mchakato huu mzuri yaani sehemu ya taasisi hizi ambazo zinafaida kubwa sana kwa dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kama nilivyosema mkataba huu ulishasainiwa na pia niipongeze Bunge lako kwa sababu lilisha- ratify ule mkataba na sisi kazi yetu ni kusaidia tu ili malengo yake yaweze kukamilika na jambo ambalo linafanyika dunia nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na ninashukuru sana kupewa nafasi hii ahsante sana. (Makofi)
THE WRITTEN LAWS (MISCELLANEOUS AMENDMENTS) (NO. 5) ACT, 2021
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata nafasi hii. Awali ya yote nimshukuru sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa niaba ya Serikali kwa ajili ya kutuletea Muswada huu wa Marekebisho ya Sheria Mbalimbali katika wakati huu muafaka, hasa nikitilia mkazo kwenye hii Sheria ya Kuzuia Usafirishaji wa Binadamu pamoja na hii Sheria ya Uhamiaji.

Mheshimiwa Spika, nasema kwamba, sheria hizi zimekuja kwa wakati muafaka kwa sababu ni sehemu kubwa kabisa ya utekelezaji wa dhana ya Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Mama yetu Samia Suluhu Hassan ya kuifungua ncbi yetu na kukuza uchumi. Unapofungua nchi na kukuza uchumi lazima kuzingatia kuweka sheria ambazo kwanza zinarahisisha uhusiano wa kimataifa; lakini pili zinawalinda hata Watanzania wenyewe dhidi ya mambo ambayo yanaweza yakajitokeza katika mchakato huo wa kufungua nchi, yakawaathiri Watanzania.

Mheshimiwa Spika, nikianza na Sheria hii ya Kuzuia Usafirishaji wa Binadamu, ambapo ile Ibara ya 4 inayorekebisha kile Kifungu cha 3 na kutoa yale makosa ambayo yanakatazwa chini ya sheria hii, ikiwa ni pamoja na haya ambayo mzungumzaji mmojawapo aliyetangulia aliyazungumza, juu ya mambo ya forced marriage na kadhalika. Katika hasa hili la forced marriage naomba tu nilipongeze Bunge lako Tukufu kwamba, pengine ndio tunaingia katika historia kwa sababu, mwezi wa Tatu mwaka huu Mahakama ya Uhalifu wa Kivita (ICC) katika ile kesi ya Dominick Ogweni wa Uganda ilitoa mojawapo ya sehemu ya hukumu yake ilitamka wazi kwamba, forced marriage, yaani hizi ndoa za kulazimisha ni crime against humanity, ni uhalifu dhidi ya binadamu.

Mheshimiwa Spika, suala hili halikuanzia pale. Kulikuwa na mtanange mkubwa sana wa kisheria na kikesi Siera Leone, halikwisha kwa sababu Mahakama zilikuwa zikitofautiana tofautiana, likaenda Cambodia, baadaye ICC ndiyo wakatoa hukumu hiyo mwezi Machi mwaka huu. Natarajia kwamba baada ya hukumu hiyo, nchi sasa zitarekebisha sheria zake kuendana na tamko hili la Mahakama hii kubwa la dunia. Kwa hiyo, angalau Tanzania tumekuwa moja kati ya nchi za kwanza kufanya hivyo kurekebisha sheria yetu hii na ninaamini idara na sekta nyingine pia zitaangalia sheria zao ili ikiwezekana ziendane na maamuzi haya ya Kimataifa.

Mheshimiwa Spika, labda kabla sijaendelea, nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge ambaye alikuwa na wasiwasi juu ya hii definition ya mambo ya slave kwamba pengine inaweza ikatuathiri kwenye mazingira yetu. A slave, yaani mtumwa sifa ya kwanza ni kwamba anakuwa ni property (mali) ya yule ambaye anammiliki. Ili awe mali yake, ni lazima yule awe amelipiwa, amepatikana kwa thamani, kwa consideration.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni vigumu sana hizi extended family zetu kwamba mtoto wa shangazi amekuja kukaa kwangu, hata kama kwangu kuna kazi nyingi kuliko zile za kule kwao, kuangukia kwenye tafsiri ya mtumwa, siyo jambo ambalo ni rahisi kabisa. Kwa sababu ili uwe mtumwa lazima uwe mali ya yule ambaye anakumiliki; na kuwa mali ni lazima uwe ulilipiwa fedha au bei na uwe unatumika kwa faida ya yule anayekutumia tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juu ya suala la Sheria ya Uhamiaji, la kwanza ni vizuri tukakubaliana kwamba Idara ya Uhamiaji ina majukumu ya kidiplomasia na ina majukumu ya kiusalama na mengine ya kiulinzi; na sheria nyingine zote zinatambua majukumu haya ya Idara ya Uhamiaji na zinaipa majukumu hayo. Sheria inawapa mamlaka ya kukamata powers of arrest mamlaka ya kuchunguza, ambayo hayo yote ni mamlaka ambayo yanafanywa na chombo ambacho ni cha kiusalama na cha kiulinzi.

Mheshimiwa Spika, hata ile Tume ya Utumishi ambayo inaangalia maslahi yao, inaangalia maslahi ya Polisi, inaangalia maslahi ya Magereza lakini wao wanaingia ndani ya Tume ile, lakini hawana hadhi kama wenzao. Hili linaleta mkanganyiko. Kwa hiyo, marekebisho hayo ni muhimu yanapofanywa ili sasa kuwawezesha kufanya kazi zao kwa mamlaka zaidi.

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Sita imeingia kwenye miradi mikubwa ambayo inatufanya tuingie zaidi kwenye mahusiano ya Kimataifa. Hata mradi wa bomba la mafuta for that matter ni mradi ambao unatufanya masuala ya Kimataifa yawe ni ya kila siku na hata Royal Tour ambayo ipo kwenye mchakato wa kutengenezwa, sasa hivi litaifungua nchi hii suala la kuingia na kutoka wageni litakuwa ni kubwa sana. Kwa hiyo, nilazima tuwe na Idara ambayo ina mamlaka ya kisheria ya kuwapa hata imani wale wanaoingia na kutoka kwamba wapo kwenye mikono salama.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu ni mfupi, nimalizie tu kwanza kwa kukubaliana na tafsiri ambazo wamezizungumza wenzangu juu ya suala hili la Katiba linalozungumziwa. Alivyozungumza Mheshimiwa Mwinyi na Mheshimiwa Olelekaita nakubaliana nao, labda tu niwekee tu msumari wa mwisho kwenye huu mjadala kwamba hii Ibara ya 147 ambayo tumeizungumza sana iko wazi kabisa kwamba kwa madhumuni ya ibara hii; siyo kwa madhumuni ya Katiba hii, ila kwa madhumuni ya ibara hii, ndiyo ikatoa definition ya mwanajeshi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa madhumuni ya Katiba hii, ni ibara ya 151 ambayo inatoa definition ya jeshi ambayo nadhani wote tunakubaliana kwamba ni hata jeshi lililoundwa na sheria nyingine yoyote. Jeshi lingine lolote lililoundwa kwa sheria nyingine yoyote. Kwa hiyo, kwa vile hatuzungumzii suala la Ibara ya 147 peke yake, tunazungumzia Katiba hii, tafsiri sahihi ni ile iliyopo kwenye Ibara ya 151. Kwa hiyo, hatukatai kwamba Ibara 147 Ibara ndogo ya (4) ni ibara halali ya Katiba hii na inayotoa tafsiri, lakini kwa madhumuni ya kazi tunayoifanya leo, kwa vile inahusu Katiba yetu nzima na sheria nyingine, tafsiri inayo- prevail ni ile Ibara ya 151 ambayo inatoa tafsiri inayohusika na Katiba nzima, siyo ile ya 147 ambayo inahusika na ibara moja tu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 7) wa Mwaka 2021
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kupata nafasi hii. Niungane na wote kwa kukupongeza kwa ajili ya kuaminiwa, nasi tunaimani kubwa na wewe iliyothibitishwa na kura zetu asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Muswada huu kwa kweli naona umekuja wakati muafaka kwa sababu ni wiki iliyopita tu tulikuwa na maadhimisho ya wiki ya sheria ambapo niliposikiliza hotuba ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hotuba ya Mheshimiwa Jaji Mkuu na hotuba ya Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu, niliona kabisa azma ya Serikali yetu ya kuibadili kabisa na kuboresha sekta yote ya utoaji haki hasa suala zima la hakijinai.

Mheshimiwa Spika, Muswada huu ni uthibitisho wa azma hiyo kwa sababu marekebisho yote ambayo yameletwa ni yale ambayo yanawanufaisha wananchi, wale watu wa chini ambao mara nyingi wanakuwa ni victims, yaani wahanga wa mambo haya ya kushitakiwa.

Mheshimiwa Spika, tukienda tu kwa haraka haraka kuangalia mifano, tukianza na ile Ibara ya 23 ambayo inarekebisha kifungu cha 4 cha sheria ya mwenendo wa Makosa ya Jinai, ambayo inaelekeza kwamba sasa ni lazima pale ambapo kuna mgogoro wenye sura ya jinai na madai, ni lazima kwanza wahusika wamalize kwenye madai; hiyo ni hatua kubwa sana ya kuwakomboa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi sote ni mashahidi kwamba kuna watu walikuwa wanapelekwa Polisi wanalala kabisa kwa sababu ya kudaiana madeni tu jambo ambalo watu walipeana kwa hiyari wakaandikishana, wakati mwingine ugomvi wa ardhi, hata mirathi watu walikuwa wanapelekwa ndani. Kwa mujibu wa marekebisho haya ni kwamba, masuala ya namna hiyo ni lazima kwanza uende kwenye madai ili haki kule iamuliwe kwamba mwenye haki ni nani, sasa kama yule ambaye imeamuliwa dhidi yake akikataa ndiyo masuala ya Polisi yanaanza kuja. Kwa hiyo, marekebisho haya ambayo yako kwenye Ibara ya 23 ni ya muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu Ibara ya 25 ambayo inarekebisha kifungu cha 91 kinachohusiana na nolle prosequi, ni vizuri tukazungumza kidogo kwamba suala la nolle prosequi limekuwa na changamoto duniani kote. India walihangaika na changamoto za nolle prosequi mpaka mwisho wakaishia kufanya kwamba lazima itolewe kwa concept ya Mahakama; lakini wameendelea kupata changamoto. Sasa ile sheria lengo lake hasa ni kumpa DPP power kwa sababu ndiye mwenye mamlaka ya kuendesha kesi zote.

Sasa unapoichanganya na Mahakama, madhumuni yake yana-fail. Canada walipambana na changamoto, mwisho wakakubaliana kwamba nolle prosequi ikitolewa baada ya mwaka mmoja ukipita bila shitaka kufunguliwa, basi mtu anaachiliwa moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, hata sisi Tanzania tumekuwa na changamoto nyingi. Nafikiri wako watakaokumbuka mwaka 1991 kesi ya Mahbob Akbar ambapo alifanikiwa kwenda ku- challenge kitu kilichofanywa na DPP baada ya nolle, kwa sababu baada ya nolle, DPP alihama akaenda kufungua kesi mahali pengine. Alipokwenda Mahakamani, Mahakama ikakubali kwamba DPP alikosea kutumia nolle kama kutafutia Mahakama ambayo inamfaa.

Mheshimiwa Spika, ambacho kimetokea sasa hivi, nadhani sisi ndiyo tumekwenda vizuri kuliko maeneo mengi ambayo changamoto hizi zimekuwa zikitokea. Nasema hivyo kwa sababu kwa utaratibu ambao umeletwa na marekebisho haya kwamba mtu akishaachiwa kwa nolle prosequi, kukamatwa tena ni pale ambapo upelelezi umekamilika na atakapoletwa Mahakamani ni moja kwa moja PH inaanza. Maana yake hapo ni kwamba ume- balance DPP kubaki na powers zake, lakini amezuiliwa kuzi- abuse, lakini pia Mahakama imekaa pembeni, haijihusishi tena na suala hili ambalo liko chini ya power za DPP na pia inalinda haki za wale washitakiwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi nasema kwa kweli marekebisho haya ni ya kipekee kabisa. Kila kifungu kilichorekebishwa kinalenga kuwapa nafuu wanyonge walio wengi jambo ambalo ndiyo lililoakisiwa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais, ya Jaji Mkuu na ya Mwanasheria Mkuu kwenye Siku ya Sheria Duniani.

Mheshimiwa Spika, hata ukienda ile Ibara ya 26 ambayo inaongeza kifungu cha 131A inayoelekeza kwamba mtu asipelekwe Mahakamani mpaka upelelezi ukamilike. Hapa niseme tu kwa kweli, kwa marekebisho haya, Serikali imejitoa muhanga, kwa sababu itabidi kuwe na uwekezaji mkubwa kuhakikisha kwamba masuala ya upelelezi, Idara ya Upelelezi inapewa vifaa vya kutosha na mafunzo ya kutosha ili kuendesha kasi ya upelelezi kuhakikisha kwamba mtu anapopelekwa Mahakamani, upelelezi umekamilika.

Mheshimiwa Spika, kwa kifupi, kwa kweli marekebisho haya yanaendana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo ndani yake ina mkataba wa haki za binadamu au Bill of Rights. Changamoto tu itakuwa ni kwenye kuwekeza ambalo hilo sina mashaka kwamba Serikali yetu inavyoendelea kufanya vizuri katika uchumi na vipaumbele, utoaji haki ikiwa ni mojawapo ya kipaumbele cha Serikali yetu, hatutashindwa kuwekeza kuhakikisha kwamba zinapatikana fedha za kutosha, wapelelezi wanafundishwa vizuri na wanapewa vifaa na uwezeshaji ili haya mambo yote yaweze kwenda sawa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upelelezi ndiyo uti wa mgongo katika haki jinai, kwa hiyo, Serikali inahitaji kuongeza nguvu katika eneo hilo, ili hata marekebisho haya mazuri yasije yakabakia kwenye makaratasi tu, lakini wananchi wafaidike na matunda yake.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja na ninaliomba Bunge lako Tukufu liunge mkono Muswada huu kwa mikono yote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Usimamizi wa Maafa, 2022
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi hii ya kuchangia kama mchangiaji wa kwanza, awali ya yote niishukuru sana Serikali kwa kuleta Muswada huu katika kipindi hiki. Kutokana na changamoto za kimazingira na kadhalika masuala haya ya maafa yamekuwa ni issue kubwa sana sasa hivi, hasa katika baadhi ya nchi zetu hizi ambazo huduma za bima hazijawafikia watu wote, watu wamekuwa wakiachwa maskini kwa sababu ya matatizo hayo.

Mheshimiwa Spika, sheria hii imekuja kwa ajili ya kutekeleza, kama alivyosema Mheshimiwa Waziri, sera ile ya mwaka 2004 ambayo imejikita zaidi katika mambo manne, ya kuzuia, kujiandaa, kukabili na kurejesha hali baada ya maafa kutokea.

Mheshimiwa Spika, sheria ya sasa imezingatia sana kuingiza suala la maafa katika mfumo rasmi wa uongozi, ndio maana kuna kuwa na Kamati za Maafa kuanzia ngazi ya Vijiji, Kata na kupanda juu tofauti na hapo awali ambapo maafa yakitokea tunaanza kutazama Waziri Mkuu yuko wapi au Red Cross wako wapi, lakini sasa imeingia katika mfumo, kwa hiyo yakitokea maafa tunaanza kutazamana wenyewe kwa wenyewe pale kijijini kwamba tumefanya nini ili kudhibiti hali hiyo ambayo imetokea.

Mheshimiwa Spika, sasa ili basi tuweze kufanikiwa, sheria hii nayo ifanye kazi isije ikawa kama ile Sura ya 242 tunayoifuta leo, yako mambo makubwa mawili nafikiri ya kuzingatia. La kwanza, ni suala zima la elimu juu ya kusimamia haya maafa yanapotokea. Hii iko kwenye ngazi mbili; ngazi ya kwanza ni mashuleni na mashuleni isifanyike tu kwa kutumia chaki na ubao, lakini iwe ni halisia katika maana kwamba watumie hasa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kuja mashuleni na kufanya zile drills kuwaonyesha kabisa watoto nini cha kufanya janga linapotokea.

Mheshimiwa Spika, kwenye Jimbo langu la Mwanga yaliwahi kutokea majanga ya moto shuleni mara tatu mfululizo ndani ya kipindi cha wiki moja. Hii ilidhihirisha kabisa kwamba vijana wale hawakuwa na elimu yoyote ya kukabiliana na maafa haya, kwa sababu kama wangekuwa na elimu hiyo basi, lilipotokea shule ya Jirani, actual moja lilitokea kwenye shule moja kwanza katika bweni la wasichana na baadaye likatokea katika bweni la wavulana. Wangekuwa na elimu kidogo basi ingewasaidia hata katika kukabiliana na lile lisingejirudia kiasi hicho.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo la kwanza ni elimu huko kwenye shule watoto wanapokwenda, lakini la pili ni kwenye hizi kamati ambazo tunaziunda, haitasaidia chochote kama tukiunda Kamati ya Maafa pale Kijijini au kwenye Kata lakini tusipowapa mafunzo ya kutosha, maafa yatakuwa yanatokea lakini wanakuwa hawana uwezo wa kufanya chochote, kwa hiyo lazima tuzingatie sana mafunzo kwa hawa.

Mheshimiwa Spika, la tatu ni uwekezaji katika maana ya vifaa vya kushughulika na mambo kama hayo. Utakuta wilaya nzima au hata wilaya mbili, tatu zinazopakana hazina hata gari moja la zimamoto. Napendekeza kabisa kwamba, Serikali ihakikishe kwamba kwa kuanza tu angalau kila wilaya iwe na gari la zimamoto lililoko kwenye hali nzuri na linalofanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ni kwamba suala hili la maafa ni suala mtambuka, linahitaji ushirikiano na linahitaji uwekezaji kwenye kila sekta. Kwa mfano sasa hivi, Serikali imepeleka fedha nyingi sana kwenye maeneo mbalimbali ya ujenzi, lakini fedha hizi hazitazuia mafuriko mvua nyingi kunyesha. Sasa wataalam wetu wanapotumia fedha hizi kujenga kama ni barabara au majengo ni lazima wazingatie kwamba haya maafa yanaweza yakatokea wakati wowote ule.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni vizuri tuhakikishe kwa mfano katika halmashauri zetu tusitegemee kuwa na engineers peke yao wanaweza wakafanya kitu ambacho kinaweza kuwa kikamilifu, lazima tuhakikishe tuna wale wasanifu majengo (architect), tuhakikishe tuna quantity surveyors, halafu ndio na mainjia wawepo ili ile kazi inapofanyika asitokee mtu wa kuja kumlaumu mwenzake kwamba ramani ilisema hivi lakini quantity hazikuwa zimezingatiwa.

Mheshimiwa Spika, lingine ni kuwawajibisha pia hawa ambao wanajenga miundombinu ambayo haiwezi kukabiliana na majanga. Inabidi uwajibikaji uwepo, fedha zile za retention kwenye miradi ya barabara zitumike ipasavyo, zibakie kukarabati ile miundombinu baada ya kujengwa.

Mheshimiwa Spika, lingine ni suala la utafiti. Ni vema utafiti ukafanyika kwa mfano, kuna maeneo mengi tunapata maafa yanayotokana na majanga ya ukame na utakuta kwamba eneo lile lingeweza kustawi mazao yanayostahimili ukame, lakini hakuna utafiti uliofanyika, wale wakulima wakashauriwa, wakalima kitu ambacho kinaweza kikakabiliana na hali ambazo tunazo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa kumalizia tu, niseme kwamba Muswada huu umekuja wakati muafaka, tunahitaji sana haya yaliyoko ndani ya sheria hii, lakini la muhimu ni kuzingatia masharti ya utekelezaji wa yale yaliyosemwa humu, vinginevyo tunaweza tukajikuta baada ya muda tunaifuta tena kama tunavyofuta hii Sura ya 242.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)