Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Additional Questions to the Prime Minister from Hon. Cosato David Chumi (1 total)

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii, nami niweze kumwuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali ambalo nimeona kuna umuhimu wa kuliuliza kwa sababu jana nilisikia ufafanuzi kutoka kwa Mheshimiwa Rais, lakini bado nimeendelea kupokea message kutoka kwa watu mbalimbali wakiuliza kuhusu swali hilo. Suala hilo ni kwamba, kumekuwepo na taarifa katika mitandao ya kijamii na mitaani kwamba Serikali imefuta ajira hali ambayo imesababisha tahamaki na taharuki miongozi mwa wahitimu mbalimbali waliokuwa wanatarajia kuajiriwa na Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia, taarifa hizo za mitandaoni na mitaani zinasema pia kwamba Serikali haitafanya tena promotion wala kupandisha madaraja, hali ambayo pia inawafanya Watumishi wa Umma kwa namna fulani morali yao kushuka.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa napenda kusikia ukweli halisi ni upi katika suala hili. Je, ni kweli kwamba Serikali haitaajiri tena? Ni kweli haitapandisha madaraja tena? Nakushukuru.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimejibu swali la Mheshimiwa Mbogo, ni kwamba sasa hivi kuna watu wengi hupenda kusema maneno ambayo siyo sahihi na hili pia napenda nikanushe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa bahati nzuri sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, jana kwenye hotuba yake ya Maadhimisho ya Miaka 50 ya Benki Kuu, ametoa ufafanuzi mzuri sana. Nami nataka nitumie nafasi hii kurudia tu yale ambayo Mheshimiwa Rais ameyasema kwa kuwahakikishia Watumishi wa Umma na wale ambao wanatarajia kuajiriwa kwamba Serikali haijasitisha ajira. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imesimamisha kwa muda kuajiri kwa sababu tunaendelea na zoezi la uhakiki wa watumishi hewa. Kazi hii ilishaanza, sasa hivi tunaikamilisha. Katika ukamilishaji huu, tunataka tujue sasa watumishi hewa ni akina nani kwa kila idara na kila sekta na watumishi walioko sasa kazini ni akina nani; ili tuweze kujua idadi ya watumishi waliobaki na pengo yaliyopo ndipo sasa tuweze kuajiri kwa ajili ya kusheheneza mahitaji ya watumishi kwenye maeneo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia Serikali inafanya mapitio ya Miundo ya Utumishi kwa lengo la kuboresha. Tunaposema kuboresha, maana yake sasa tunataka tupate tija zaidi kwa watumishi. Kwa hiyo, naomba niwasihi Watumishi wote wa Umma kwamba zoezi hili halilengi kuwakandamiza watumishi; kazi hii hailengi kuathiri utumishi wao na madaraja yao, bali kuboresha watumishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwahakikishie Watumishi wa Umma kwamba Serikali hii inawapenda sana na inajali mchango mkubwa ambao watumishi mnautoa kwa Serikali hii. Ili tuweze kufanya kazi kwa motisha, Serikali hii imeona ni muhimu sasa kuboresha zaidi miundo mbalimbali na maslahi mbalimbali, lakini pia kuona idadi ya watumshi tuweze kutumia fedha inayotakiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka muwe na amani kwamba kazi hii inayoendelea ni ya muda mfupi sana. Itakapokamilika, ajira zote ikiwemo na elimu, afya, majeshi, ambazo pia zilikuwa tayari zianze karibuni, zote zitarudishwa na watu watapelekwa kwenye vituo vya kazi kwenda kuanza kazi zao na madaraja mapya yatakuwa yameshatolewa.