Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Miraji Jumanne Mtaturu (33 total)

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nianze kumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kunijalia kuingia kwenye Bunge lako Tukufu na kuweza kuwawakilisha ipasavyo Wananchi wa Jimbo la Singida Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Ikungi pamoja na Jimbo la Singida Mashariki ni kama ambavyo swali la msingi lilivyouliza lina matatizo yanayofanana na jimbo lililoulizwa katika swali la msingi. Pamoja na matatizo hayo zimefanyika jitihada, Serikali ya Awamu ya Tano chini ya kipenzi chetu Dkt. John Pombe Magufuli, wameshatuletea takribani bilioni 1 na milioni 500 kuchimba visima virefu 28.

Mheshimiwa Spika, sasa nimekuja hapa kuomba kwa kupitia Waziri, wako tayari, tumeshafanya tathmini ya kutosha tuweze kupata, maana kuchimba maji na kuyapata ni jambo moja na kutoka maji ni jambo la pili. Kwa hiyo, ninaomba Mheshimiwa Waziri anihakikishie kwamba, kupitia tathmini iliyofanyika na iko Wizarani tunahitaji jumla ya bilioni 2 ili tuweze kutengeneza miundombinu ya maji Wananchi wa Singida wapate maji. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, kwanza namfahamu vizuri alikuwa Mkuu wa Wilaya, lakini nataka niwahakikishie wana-Singida Mashariki hili ni jembe wembe walitumie vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, katika kuhakikisha kwamba, tunatatua tatizo hili la maji tumeshafanya jitihada za uchimbaji. Nimuombe baada ya Bunge Saa saba tukutane tupange mikakati ya kwenda kutatua tatizo la maji kwa haraka kabisa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wilaya ya Ikungi ni Wilaya iliyoanzishwa mwaka 2013; na hivi tunavyoongea, ofisi au OCD anakaa kwenye majengo ambayo yalikuwa ni maghala ya mkoloni. Kwa sababu ulishaanzwa ujenzi wa kujenga jengo la OCD kwa maana ya wilaya, ni lini sasa Serikali itamaliza, kwa sababu limesimama muda mrefu, miaka mitatu iliyopita?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mimi na Mheshimiwa Mtaturu tulishazungumza pembeni kwamba niende Jimboni kwake, nimhakikishie kwamba moja katika mambo ambayo tutafanya ni kwenda kukitembelea kituo hiki kwa pamoja halafu tushauriane juu ya utaratibu muafaka wa kukimaliza kituo hiki kwa haraka.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona.

Matatizo ambayo ameyaeleza Mheshimiwa Kiula yamefanana na Wilaya ya Ikungi ambayo ndiyo Jimbo la Singida Mashariki lilipo. Wakati nauliza swali hili naomba niwahakikishie wananchi wa Jimbo la Singida Mashariki, niko imara kuwawakilisha katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilitaka niseme tu, kwa kuwa barabara au miundombinu ya barabra ndiyo inayosaidia kukuza uchumi wa wananchi; na kwa kuwa barabara ya Njiapanda – Makiungu – Kwamtoro mpaka kule Handeni ni barabara ambayo imekuwa ikifanyiwa upembuzi muda mrefu: Ni lini sasa Serikali itaanza kuijenga na kuweza kusaidia kukuza uchumi wa wananchi wa Wilaya ya Ikungi na Mkoa wa Singida? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa
Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mtaturu na nimhakikishie tu kwamba tutampa ushirikiano wa hali ya juu katika kutekeleza majukumu yake ya kibunge katika eneo lake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba, barabara anayoitaja Mheshimiwa Mbunge kutoka Njiapanda kupitia Makiungu kwenda kwa Mtoro, itatoka Chemba kwenda mpaka Handeni, kilometa 461; ni kweli kwamba usanifu umeshakamilika na kwa kadri tutakavyopata fedha tutaanza kujenga barabara hii. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi kwamba mradi huu mkubwa wa Kilometa 461 utawanufaisha sana wananchi wa eneo lake na kwa kweli tumejipanga kama Serikali kuona kwamba tunawahudumia vizuri wananchi katika eneo lake.nnAhsante. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa majibu ambayo yanaeleza zaidi barabara za kawaida kwa sababu milioni 900 haina uwezo wa kujenga kilometa ya lami hata moja. Kwa hiyo naomba sasa kujua kwa sababu Mji wa Ikungi ni mpya kwa maana ya wilaya ni mpya na kwa sababu Makao Makuu ya Wilaya tunategemea yawe na lami. Sasa naomba nijue kwa sababu Mheshimiwa Waziri Mkuu alituhakikishia tangu 2019 na leo ni 2021; je, ni lini hasa Serikali itatenga fedha kwa ajili ya kujenga hizo kilometa tano ya lami ili wananchi wa Ikungi nao waweze kupata lami na kufaidi matunda ya uhuru? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika,
ahsante sana. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge ametaka kufahamu ni lini sasa Serikali itatenga fedha kwa ajili ya kujenga kilometa tano za lami katika Makao Makuu ya Wilaya yake katika eneo la Ikungi. Ni kwamba, kama katika jibu letu la msingi tumeainisha hapa kwamba katika mwaka huu wa fedha 2021/2022, tumepanga kupitia Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini kwa maana ya TARURA kutenga fedha kwa ajili ya kufanya usanifu na tathmini za gharama ya ujenzi kwa kiwango cha lami katika eneo hilo. Kwa hiyo mara baada ya usanifu na tathmini ya kina ambayo itakwenda kufanyika katika mwaka huu wa fedha maana yake katika mwaka wa fedha unaofuatia tutaanza kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa lami katika eneo la Ikungi. Nimhakikishie, Serikali ya Rais wa Sita, mama Samia Suluhu Hassan iko tayari kukamilisha ahadi hiyo kwa vitendo. Ahsante sana.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana barabara hii tuna maslahi nayo kama alivyojibu swali Mheshimiwa Naibu Waziri na kwa sababu barabara hii inaunganisha mikoa minne na barabara hii inahistoria katika nchi yetu imefika wakati sasa Serikali iamuwe kuijenga barabara hii kilometa 461 iishe kuliko kuanza kuwa na vipande vidogo vidogo.
WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ina Wabunge wengi ambao wanaifuatilia sana na ninawashukuru sana kwa kuweza kuwa wanatukumbusha kila mara umuhimu wa barabara hii. Lakini kama alivyosema Mbunge barabara hii inaurefu wa kilometa 460 na tunaendelea kujenga kwa vipande kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka huu unaoendelea kama nilivyosema katika swali lilipita tutajenga kipande kimoja na katika bajeti hii ambayo tuna ijadili mwaka huu barabara hiyo vilevile imezingatiwa kwa hiyo napenda kuwaahidi wananchi tangu mikoa ya Singida hadi Tanga ambayo barabara hiyo inapita kwamba vipande vinaendelea kujengwa na barabara hiyo tutaizingatia kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kunipa majibu ambayo pia nahitaji nipate uhakika.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa umeme ni chachu ya maendeleo na kwa kuwa ni asilimia 44 tu ya vijiji vya Singida Mashariki vina umeme, ninalotaka kujua na wananchi wa Singida Mashariki, hususan Tarafa ya Mungaa ambayo ina kata saba na ambayo haina umeme kabisa.

Ni lini mkandarasi atakwenda kuanza kazi kama alivyosema mwezi Machi mpaka sasa hajapatikana na tunataka tujue jina la mkandarasi huyo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa kuwa, vijiji ambavyo amevitaja anasema vina umeme na kwa sababu kuna mradi wa ujazilishaji na mpaka tunavyoongea sasa ni unaenda taratibu mno. Hawaoni sababu ya kuongeza kasi ya kuweza kuweka umeme katika vitongoji vilivyobaki? (Makofi)

SPIKA: Yaani Mheshimiwa Mtaturu kuna tarafa ambayo haina umeme, tarafa nzima?

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, Tarafa nzima ya Mungai yenye Kata za Mungaa, Lighwa, Makiungu, Kata ya Ituntu, Mungaa na Kikiyo pamoja na Kata ya Msughaa zote hazina umeme ambazo ni mpakani mwa Chemba.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mtaturu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tunakiri ni kweli kwamba mpaka sasa kuna baadhi ya vijiji Tanzania havijafikiwa na umeme. Kama tulivyosema tulianza tukiwa na vijiji 12,268 lakini tumepunguza mpaka sasa tuna vijiji 1,974 ndio havina umeme na mpango uliopo kwa sasa ni kuhakikisha kabla ya mwezi Disemba, 2022 vijiji vyote hivyo 1,974 vyote vinakuwa vimepata umeme na tuko tayari tumeshawapata wakandarasi wa kupeleka umeme kwa kila eneo katika REA III, Round II.

Mheshimiwa Spika, Jumanne ya wiki hii tulikuwa tuna kikao na wakandarasi hao ambao tuymewapa kazi hizo na tumewaagiza kabla ya Jumatatu inayokuja wawe wote wamewapigia simu Waheshimiwa Wabunge pamoja na viongozi wengine kwenye maeneo kuwaambia kwamba tumekuja na tumeripoti kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Waziri juzi kuna maeneo wakandarasi wetu wameenda, lakini hawakuwa wametoa taarifa ya kutosha kwa Waheshimiwa Wabunge ambao ni wawakilishi wa wananchi, ili kuweza kujua kwamba wapo. Sasa mimi nimechukua jitihada ya kuwapatia wakandarasi namba za Waheshimiwa Wabunge na kuwaelekeza kabla ya Jumatatu nitakuwa nime-verify kwa Mbunge mmoja-mmoja kujua kama amepigiwa simu au kutumiwa message kuambiwa kwamba mimi ninaenda kuripoti katika eneo hilo. Kwa hiyo, niseme katika maeneo hayo ambayo Mheshimiwa Mtaturu ameyataja kazi inaendelea na tutafikisha umeme katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, lakini katika swali la pili, kwenye densification (ujazilizi); mkandarasi anayeendelea kufanya kazi katika Mkoa wetu wa Singida anaitwa Sengerema, ni mkandarasi mzuri, anafanya kazi yake vizuri na anakwenda hatua kwa hatua na tunatarajia kufikia mwezi Disemba mwaka huu atakuwa amemaliza vitongoji vyote. Kwenye kupeleka umeme kwenye vitongoji tunapaleka kupitia miradi yetu ya REA ambao wanapeleka kwenye vijiji wanashuka kwenye vitongoji, lakini tuna mradi maalum huu wa densification ambao wenyewe unalenga vitongoji, lakini pia na wenzetu wa TANESCO bado wanalenga vitongoji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kufikia mwaka 2022 tunatarajia kuwa tume-cover vijiji vyote, lakini tunakuwa tume-cover vitongoji vingi sana. Mpango wetu kuendelea kupeleka umeme katika vitongoji kwa sababu kupeleka umeme ni zoezi endelevu.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nipongeze majibu ya nyongeza ya Mheshimiwa Naibu Waziri katika Jimbo la Mheshimiwa Mtaturu.

Mheshimiwa Spika, ni kweli jimbo la Mheshimiwa Mtaturu kimsingi ile tarafa ambayo haijapata umeme pamoja na tarafa nyingine zote wakandarasi wameondoka jana kwenda Singida kwenda kufanya kazi, pamoja na tarafa hiyo. Mheshimiwa Mtaturu alikuwa na vijiji 12 ambavyo havijaguswa kabisa pamoja na hiyo tarafa.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mtaturu pamoja na Waheshimiwa Madiwani na Waheshimiwa wananchi wa Singida katika jimbo lake wote watapata umeme ndani ya miezi 18 kuanzia jana walipoondoka wakandarasi. (Makofi)
MHE. MIRAJI J MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake lakini katika swali langu la msingi mpango wa Serikali ni kujenga Kituo cha Afya kila Kata na katika Jimbo la Singida Mashariki tuna Kata 13 na tunacho Kituo cha Afya kimoja tu ambacho pia hakina huduma nzuri. Kwa sababu Kata hizi hazina Kituo cha Afya, naomba kujua Serikali ina mpango gani wa kujenga Vituo vya Afya katika Kata zingine ikiwemo Kata za Makiungu na Ntuntu ambayo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan wakati wa kampeni? Swali la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, namshukuru sana Mheshimiwa, ni kweli ametuletea fedha kwa ajili ya kujenga hospitali ya wilaya. Fedha hizo zilirudishwa kama ambavyo tulisema baada ya kuwa mwaka wa fedha umepita. Hivi tunavyoongea zaidi ya miezi sita, fedha hizo hazipo na ujenzi umesimama. Je, ni lini sasa Serikali italeta fedha hizo ikiwemo kuleta vifaa tiba katika hospitali hiyo ili iweze kuanza kutoa huduma? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mbunge wa Singida Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimetangulia kutoa ufafanuzi katika majibu yangu ya msingi kwamba Sera ya Maendeleo ya Afya ya Msingi inakwenda kuboreshwa ili iwe na tija na uhalisia na ufanisi mkubwa zaidi kwa sababu tuna vijiji karibu 12,000 na mitaa karibu 16,000 na tuna kata 3,956. Kwa hivyo, tunataka kwenda kimkakati zaidi kujenga vituo vya afya katika maeneo ya kimkakati ambavyo vitakuwa fully equipped na vitatoa tija zaidi badala ya kujenga kila kata na kila Kijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika jimbo lake, vituo hivi vya afya ikiwemo kituo hiki ambacho ni ahadi ya Mheshimiwa Rais lakini na vituo vile vingine vyote tutafanya tathmini na kama tutaona tija ya kuvijenga vitakwenda kujengwa. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie kwamba mpango huo utaendelea kutekelezwa kwa utaratibu huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, fedha za hospitali ya halmashauri zilizorejeshwa, kwa kipindi hicho zilirejeshwa kwa mujibu wa Sheria ya Bajeti ya Mwaka 2015 lakini Serikali imeshafanya maboresho. Waheshimiwa Wabunge wote tumesikia hapa wakati wa bajeti ya Wizara ya Fedha kwamba kuanzia Mwaka ujao wa Fedha, fedha zinazopelekwa kwenye miradi ya maendeleo hazitarejeshwa baada ya tarehe 30 Juni. Kufuatia hilo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba fedha hizo tutafanya utaratibu kuzipeleka ili kuendelea na ujenzi wa hospitali kama ulivyopangwa. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, kwa sababu Mheshimiwa Waziri katika jibu lake amesema kwamba wanaruhusu kuwahakiki wazee na kwa sababu mfumo wa kuhakiki wazee haujawa rasmi, mmewaachia Halmashauri na ndiyo unakwamisha wazee wengi kutokupata huduma hii kwa kigezo cha kutokusajiliwa.

Ni nini hatua ya ziada ya Serikali kuhakikisha wazee wote wanasajiliwa katika muda ambao umepangwa ili wapate haki yao ya matibabu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL):
Mheshimiwa Spika, labda nijibu swali zuri la Mheshimiwa Mbunge, moja; nachukua concern yake kwa sababu ameonesha kuna tatizo kwenye eneo zima la utambuzi wa wazee. Kwa hiyo tutaenda kukaa kuona ni namna gani tunaweza kuboresha hilo eneo hasa la utambuzi wa kujua ni nani mzee na nani siyo mzee.

Lakini kwa sababu tunakwenda, suala hapa ni tiba ni ku-access tiba tunapokwenda kwenye Muswaada wa Bima ya Afya kwa Wote kimsingi hilo litakuwa lipo contained kwenye utaratibu mzima, kwa hiyo, halitakuwa tatizo.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, nakushkuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ni miundombuni ya reli ni muhimu sana katika usafirishaji wa mizigo pamoja na abiria, na kwa sababu reli hii ilianzishwa na Baba wa Taifa; Serikali haioni kwamba kuna umuhimu wa kumuenzi Baba wa Taifa kwa kuifanyia haraka kuijenga reli hii na iweze kutumika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtaturu, Mbunge kutoka Mkoa wa Singida kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi kwamba Serikali inatambua umuhimu wa reli hii, kama alivyosema imeasisiwa na Baba wa Taifa, na tukifanya tathmini ya kujua gharama tutaiboresha reli hii. Hii reli iliopo ni ya zamani itabadilishwa tuweke iwe kubwa zaidi iweze kubeba mzigo mkubwa zaidi.

Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge tupe muda mwaka huu mpaka mwakani utapata majibu ya ujenzi wa reli Singida
– Manyoni na maeneo mengine.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwanza, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tarafa ya Mungaa ina shule zaidi ya nane za O-level na kwa sababu shule hii ya Mungaa ni kongwe ndiyo maana niliomba shule hii iweze kujengwa ili kuwapatia fursa wanafunzi wanaokosa nafasi ya kwenda kidato cha tano na sita kama ambavyo imekuwa ni tatizo kwenye maeneo mengine.

Kwa hiyo, naiomba Serikali katika tathmini hiyo iweze kuchukua umuhimu wa pekee kuhakikisha shule hiyo inajengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, katika vikwazo ambavyo Mheshimiwa Naibu Waziri ameeleza ni pamoja na vikwazo vya watoto wa kike katika shule zetu za sekondari zikiwemo shule za kata. Ni nini mkakati wa Serikali kujenga hosteli za kuweza ku-accommodate wanafunzi wote wa kike katika shule zetu ambazo ziko katika Jimbo la Singida Mashariki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali madogo ya nyongeza ya Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mbunge wa Singida Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza alikuwa ameelezea tu kwamba Tarafa ya Mungaa ina shule nane za O-level na hivyo alikuwa anasisitiza tu kwamba tuiweke kwenye tathmini. Katika jibu la msingi tumekubali kwamba kwenye tathmini ya zile shule 100 ambazo tunakwenda kuzifanyia upanuzi nchi nzima kwa ajili ya kupokea watoto wa kidato cha tano miongoni mwa shule tutakayoifanyia tathmini ni Shule ya Mungaa. Kwa hiyo, hilo tumelikubali litafanyika katika mwaka huu wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili kuhusu vikwazo kwa watoto wa shule ambao wanatembea umbali mrefu kuelekea shuleni, moja ya mkakati wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Rais mama yetu Samia Suluhu Hassan ni pamoja na kujenga hosteli. Ndiyo maana katika mwaka huu wa fedha tumetenga fedha nyingi tu kuhakikisha kwamba tunajenga hosteli katika maeneo mbalimbali na ninyi mmepitisha bajeti hiyo. Kwa hiyo, tunachosubiri tu ni fedha zitakapotoka tutaainisha maeneo mbalimbali na tutazingatia Jimbo la Singida Mashariki. Ahsante. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nachukua nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mafupi ambayo bado hayajaondoa kabisa hamu ya wananchi wa Singida Mashariki kutumia banio hili. Kwa kuwa kilimo cha umwagiliaji kimeonekana ni kilimo chenye tija na hapa Bungeni tumekuwa tukizungumza mara kwa mara; na kwa kuwa soko la mbogamboga lipo kubwa sana kwenye mgodi wa Shanta Gold Mine pale Mang’onyi ambapo tunategemea utaanza hivi karibuni, ambalo litakuwa ni soko kubwa la mbogamboga na matunda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali haioni umuhimu wa sasa kutenga fedha ambazo zilikadiriwa shilingi milioni 580 ili kuweza kukamilisha upande uliobakia kumalizia banio hilo lililokuwa limeandaliwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Kwa kuwa chanzo cha maji na Bwawa la Mwiyanji alilolieleza limejaa tope na kusababisha maji kuwa siyo ya kutosha; na kwa kuwa tumekuwa tukipiga kelele kuhusiana na mabwawa hapa nchini yajengwe mengi ili kuongeza uwezo: Ni lini sasa Serikali itaweza kutenga fedha kwa ajili ya kuondoa tope za bwawa hilo la Mwiyanji ili liwe na kina cha kutosha na maji mengi na kuweza kujenga bwawa lingine ambalo litajengwa katika Kijiji husika cha Mang’onyi? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaruru, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza na la msingi ni kwamba Serikali inatambua umuhimu wa kilimo cha umwagiliaji. Kwa kuwa kilimo hiki kinagusa pia sekta ndogo ya mbogamboga, Serikali itaendelea kuweka mkazo mkubwa kuhakikisha kwamba mradi huu unakamilika kwa hekta zilizobaki ili wananchi wa eneo la Mang’onyi waweze kupata huduma hii ya kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakika ni kwamba, katika bajeti inayokuja tutatenga fedha kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa mradi huu ili wananchi waweze kulima kupitia kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ili mradi huu uweze kutekelezeka vizuri, na Mheshimiwa Mbunge bahati nzuri amelieleza jambo hili vizuri na amekuwa mtetezi wa kweli kwa wananchi katika jambo hili, lazima katika fedha ambazo zitatengwa zijumuishe pia namna ya kuweza kuondoa tope katika Bwawa la Mwiyanji ili maji yaweze kutiririka kwa urahisi ili wananchi waweze kupata huduma hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nikuondoe hofu; pia mimi na wewe tumepanga kwamba baada ya hapa tutakwenda kutembelea na kuzungumza na wakulima ili kuona skimu nzima na kuona namna Serikali inaweza ikawasaidia kwenye skimu hiyi.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali moja la nyongeza. Chuo hiki cha Bandari ni chuo ambacho kiko kwenye ukanda huu wa Afrika Mashariki, na ni chuo muhimu sana kwa ajili ya mafunzo haya; na kwa sababu vijana wanaokwenda kufundishwa pale wanahitaji kufundishwa kwa vitendo; na kwa sababu chuo hiki kina tatizo la kuwa na meli ya mazoezi. Je, ni lini Serikali sasa itatenga fedha kwa ajili ya kununua meli ya mazoezi kwa ajili ya kuwasaidia vijana kwa ajili ya mafunzo ya vitendo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtaturu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ameuliza ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya mafunzo. Nimhakikishie tu Mheshimiwa kwamba, katika suala hili, pamoja na mambo mengine ya uboreshaji wa chuo hicho, ikiwa ni sambamba na ujenzi unaoendelea, zipo pia fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya vifaa vya kufundishia na kwenye hili suala la meli ni sehemu ya mpango huo. Kwa hiyo kulingana na upatikanaji wa fedha tutalikamilisha hilo na Serikali hii imekuwa ikifanya kazi kwa speed, tutalikamilisha. Ahsante.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, namshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu mazuri ambayo yanaleta matumaini kwa wananchi wa Singida kwa kufufua reli hii ya Singida – Manyoni. Pamoja na majibu hayo, ninayo maswali ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kupata commitment ya Serikali, nataka kujua ni fedha kiasi gani zimetengwa kwa ajili ya kutekeleza mradi huu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa lengo la reli hii lilikuwa ni kukuza uchumi, kubeba mizigo ambayo ipo katika ukanda huu na hasa ililenga sana wakati huo Mwalimu Nyerere akianzisha reli hii ni kubeba ngano ambayo iko kule Basutu katika Mkoa wa Manyara. Sasa kwa sababu tunakuza eneo la kilimo na tuna madini yako pale kwenye Mkoa wa Singida, ni mpango gani wa Serikali sasa kuujenga kwa kiwango cha SGR ili iwe na uwezo mkubwa wa kubeba mizigo katika eneo hilo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mbunge wa Singida Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya mwaka 2022/2023, tumetenga fedha kiasi cha shilingi bilioni 3.45 kwa ajili ya ukarabati wa tuta pamoja na makalavati na uwekaji wa tabaka la kokoto na tutajenga kama ambavyo tuliboresha reli ya kutoka Tanga kwenda Arusha kupitia Moshi kwa maana ya kutumia force account.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, anapenda kujua ni lini sasa hii reli itakuwa katika kiwango cha standard gauge? Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa kwa jitihada zake pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengine wa Mkoa wa Singida, Serikali mara baada ya kufanya ukarabati huu wa awali, tukifungua malango/tukifungua njia, ndipo tutakapoanza sasa kufanya tathmini, feasibility study kwa ajili ya SGR. Ahsante.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba tulipitisha bajeti ya Bilioni Moja na Milioni Mia moja kwa ajili ya kujenga Kituo cha Polisi pale Ikungi na leo ni mwezi wa Novemba. Je, ni lini sasa Serikali italeta fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho kama bajeti ilivyopitishwa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtaturu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba bajeti hiyo ilipitishwa kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho kinachofanyika ni Jeshi la Polisi limewasilisha mpango wa ujenzi ambao utakapopitishwa na Wizara utawasilishwa Hazina kwa ajili ya kutoa fedha. Ni matarajio yetu fedha za maendeleo kwa ajili ya ujenzi wa kituo hiki kwa vile zinatoka kwenye Mfuko ambao tunauzungumzia kwa ukamilifu wiki iliyopita zitatoka kwa ajili ya kuwezesha ujenzi wa kituo hicho kuanza. Ninaashukuru. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake kama anavyosema mwenyewe Milioni 100 kwa upungufu ambao upo ambao ni zaidi ya asilimia 62 itatuchukua muda mrefu sana kukamilisha ujenzi wa nyumba hizi, kwa sababu walimu wetu wanafanya kazi nzuri na tuliwajengea madarasa mazuri huko vijijini mbapo tunatakiwa wakae karibu.

Je, ni mkakati upi wa haraka wa kutafuta fedha za kutosha kuweza kumaliza tatizo hili ambalo limekuwa kubwa na linapunguza ari ya walimu kufanya kazi? (Makofi)

Swali la pili ni pamoja na kwamba juhudi zinaendelea za kupata Walimu lakini walimu nao ni wachache sana ambao hawa-fit idadi ya wanafunzi ambao tunao, kwa sababu Serikali imetangaza ajira za Walimu na kwa sababu Halmashauri ya Ikungi ina upungufu mkubwa.

Ni nini Serikali itafanya kuhakikisha kwamba inapunguza kabisa tatizo la idadi ya walimu ambao wapo katika Halmashauri yetu ya Ikungi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mbunge wa Singida Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tunatambua kwamba kuna changamoto na fedha ambazo zimetolewa katika Halmashauri ya Ikungi ni ndogo. Mkakati wa Serikali kwa mfano, kama sasa hivi moja ya mikakati ya Serikali ni kuhakiksha kila sekondari mpya tunayoijenga ama shule mpya tunajenga na nyumba za walimu na ninyi mmekuwa mfano three in one. Yote hii ni katika kukabiliana na changamoto ya nyumba za walimu.

Mheshimiwa Spika, tuna mikakati mingi ikiwemo kutafuta fedha na jukumu letu kubwa la sasa ni kuhakikisha tunamaliza kwanza ujenzi wa madarasa na shule latika maeneo yote yenye uhitaji, mara baada ya kumaliza hiyo hatua yetu ya pili ni kuhakikisha tunajenga nyumba kwa Walimu hususan katika yale mazingira magumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu upungufu wa Walimu katika Halmashauri ya Ikungi nimhakikishie tu Mhehsimiwa Mbunge katika hatua ambazo tumeshatangaza ajira, Ofisi ya Rais, TAMISEMI sasa hivi tutaajiri Walimu 9,800 na katika hizo ajira 9,800 tutakazoajiri sehemu ya Walimu tutapeleka katika Halmashauri yako. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nikuondoe shaka na hilo.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Singida uko karibu sana na Makao Makuu ya nchi Dodoma na kwa sababu ya kiusalama uwanja wa ndege wa Singida ni muhimu sana na kwa sababu Marais wote wawili wametaja kwenye hotuba zao hapa Bungeni Rais John Pombe Magufuli pamoja na Rais Samia Suluhu Hassan walisema katika viwanja 11 na kiwanja cha Singida kitajengwa.

Sasa naomba nijue ni lini sasa Serikali itatenga fedha ili kujenga uwanja ule ambao upo karibu na Makao Makuu ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtaturu, Mbunge wa Singida kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, maelezo ya Mheshimiwa Mbunge ni sahihi na ni kweli kwamba viongozi wameahidi uwanja huu uweze kujengwa na mimi naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara tayari ina mpango wa kuanza kufanya tathmini ya uwanja huu ili iweze kuujenga lakini pia kama ulivyosema ni uwanja ambao upo karibu na Dodoma kwa ajili ya usalama. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hilo Wizara inalo na muda si mrefu itaanza kulifanyia kazi, ahsante.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali kwa sababu imekuwa ni kilio cha muda mrefu kupata stendi ya kisasa katika Mji wetu Ikungi. Sasa. ili kujiridhisha, ni hatua gani sasa zimeanza kuchukuliwa katika kuanza ujenzi huu mapema?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa fedha zilizotengwa, kwa maana milioni 110, ni fedha kidogo. Nini mkakati wa kuongeza fedha za kujenga stendi yenye hadhi ili tuweze kuwa na stendi kubwa kwa sababu ni main road na inapokea magari mengi yanayoelekea Dar es Salaam na Mwanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna uhitaji wa stendi katika eneo hilo la Ikungi, na tayari shughuli za awali za ujenzi ikiwemo kusafisha eneo lakini pia kufanya upembuzi imeshaanza kwa ajili ya kuanza ujenzi huo; na tunaamini shilingi milioni 110 itaanza kazi katika mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Spika, lakini tathmini iliyofanyika inahitaji shilingi milioni 700 ili kukamilisha stendi hii ya Ikungi. Tumeshakubaliana kama Serikali kupitia mapato ya ndani ya halmashauri kila mwaka watatenga shilingi milioni 150 na katika mwaka ujao wa fedha 2023/2024 halmashauri imakwishatenga fedha hiyo kwa ajili ya kuendelea na ujenzi ahsante.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Jimbo la Singida Mashariki ni miongoni mwa majimbo yenye wafugaji wengi sana, na Mheshimiwa Waziri alishawahi kuniahidi majosho takribani matatu kwenye Kata za Siuyu, Ulyapiti, pamoja na Isuna.

Sasa ni nini kauli yake kwa mwaka huu wa fedha?
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, namtafutia majibu.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, zoezi la TASAF, kwa maana ya kukwamua familia maskini ni zoezi zuri. Huko nyuma lilikuwa liko kwenye package ya kuwalipa tu kwa ajili ya kuwasaidia kwenye mambo mbalimbali; sasa kumeongezwa package ya kuwapa hadhi halafu wanalipwa. Lakini maeneo mengi tumeanza kuona wazee wetu…

SPIKA: Swali lako Mheshimiwa Mtaturu.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, tumekuwa wazee wetu wakitumikishwa wanafanya zaidi ya miaka 60 kitu ambacho sio kizuri katika maeneo yetu; je, Serikali inasemaje kuhusu jambo hili?

SPIKA: Ngoja kabla sijaiambia Serikali nataka nikuelewe wewe kwa hiyo ni jambo bayo kufanya kazi na kulipwa? Yaani uliza swali lako vizuri ili Serikali ijue inakujibuje, ni jambo bayo wale maskini kuambiwa wafanye kazi halafu walipwe?

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, si maskini watu wazee zaidi ya miaka 70 wanafanya kazi ya kuchimba mitaro, kutengeneza barabara, ambayo package hiyo ilikuwa inalenga kwa ajili ya vijana ambao wanatoka kwenye familia maskini swali langu ndio hilo.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI
WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge Mtaturu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba katika baadhi ya maeneo malalamiko haya yamekuwepo. Sisi kama Serikali tumekwishatoa mwongozo na huo ndio mwongozo unaoongoza shughuli za TASAF; kwamba wazee wote walio juu ya miaka 60 na akina mama wajawazito pamoja na watoto wadogo hawaruhusiwi kufanya kazi katika mazingira hayo ambayo yeye anayasema. Isipokuwa Serikali, na sheria vinaelekeza kwamba vijana wenye nguvu watafanya kazi kwa niaba ya wazee hao. Na kama itatokea kwamba mzee amelazimishwa basi sheria itafuata mkondo wake katika kuchukua hatua za msingi. (Makofi)

SPIKA: Sasa hayo maelezo ni ya jumla najaribu kuwaza mzee kama anao uwezo wa kufanya hiyo kazi halafu anyimwe; nadhani pengine huo mwongozo wa Serikali utazame. Kuna wazee kweli hawawezi kufanya kazi lakini wapo wazee wanaweza kufanya kazi na kama ameenda yeye kuomba hiyo kazi hoja ya kulazimisha ndiyo shida. Kama yeye ndio alienda kuomba kazi ni kwamba hiyo kazi angeweza kuifanya sehemu nyingine. Na hata humo ndani kuna wazee ambao wanaweza ubunge, wako wazee wanapewa mikataba hata Serikalini, sasa tukiweka kwa jumla namna hiyo Mheshimiwa Naibu Waziri hii inakaaje?

NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA): Mheshimiwa Spika,
kwa niaba ya Serikali naomba nitoe maelezo mafupi juu ya jambo hili.

Mheshimiwa Spika, Mwongozo wa Serikali unataka wazee walio juu ya umri wa miaka 60 wasipewe kazi hizo kwa sababu ya ugumu wake; lakini inapotokea kwamba mazingira hayo yapo mwongozo unawaongoza kwamba wachukuliwe vijana ambao ndani ya kaya ile anayetoka huyo mzee ili wafanye kazi kwa niaba ya yule mzee. Sasa kumekuwa na incidence ambazo vijana wanakataa kwenda kufanya kazi au wakati mwingine wanawakatalia wazee wao kufanya kazi, kwa hiyo mzee kwa kutambua kwamba kuna hela ataikosa anaamua mwenyewe aende kufanya kazi hiyo. Sasa haya ni mazingira yaliyopo, lakini sisi kama Serikali tumeweka sheria na miongozo ambayo iko very strict, kwamba mzee aliyezidi miaka 60, mama mjamzito, mtoto chini ya miaka 18 hawaruhusiwi kufanya kazi.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naishukuru sana Serikali kwa kutusaidia kuweka miradi ya maji kwenye vijiji takribani Vinne kikiwemo Kijiji cha Matare pale katika Jimbo la Singida Mashariki. Hoja yangu na swali langu Mheshimiwa Waziri, mradi umekamilika na Mkandarasi amemaliza kazi changamoto iko kwenye umeme na tumeshalipia watu wa TANESCO mpaka leo umeme haujawekwa.

Je, ni lini Serikali itahakikisha umeme unawekwa ili wananchi wa Matare waanze kutumia maji. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Wizara ya Maji inafanya kazi kwa ukaribu sana na Wizara ya Nishati na wamekuwa msaada mkubwa kwetu, hili jambo tutalifuatilia kwa haraka kuhakikisha ujenzi wa eneo hilo linakamilika kwa haraka. Ahsante sana.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Barabara ya Singida kupitia kwamtoro mpaka Kedashi - Tanga, ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu na kwa sababu mlituambia tayari imekwishawekwa kwenye mpango wa kujengwa, na imetangazwa katika kilomita 2100. Ni lini sasa mkandarasi atakuja kwa ajili ya kuanza kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba barabara hiyo tuna mpango thabiti wa kuijenga kwa kiwango cha lami. Kama tulivyokuwa tunaelezea kwamba nitajengwa kwa mpango wa EPC+F na ninaomba Mheshimiwa Mbunge, avute subira ataisikia tutakapokuwa tunawasilisha bajeti yetu. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba tu kumwuliza swali Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwa sababu ni muda mrefu hapo nyuma ajira zilikuwa hazijatoka na kuna vijana wengi waliomaliza elimu zao toka mwaka 2014, 2015 mpaka sasa: Ni nini kauli ya Serikali kwamba baada ya kuwa mmetangaza ajira hizi 13,000 na kuwapa kipaumbele waliokuwa wame-graduate mapema zaidi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika tangazo la ajira ambalo Serikali imetoa kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa walimu 13,390 imewekwa pale kwamba wale wa 2015 ndiyo wataanza kuingia, watakuja wa 2016 wa 2017 ili wasikae muda mrefu baada ya kuwa wamemaliza masomo yao ya ualimu. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.

Swali la kwanza; kwa kuwa ukuaji wa shughuli za kiuchumi unaongeza changamoto za kiusalama katika maeneo yetu na kwa kuwa tulikubaliana kuwa na Polisi Kata, Polisi Kata ambao hawana vituo itakuwa ni sawa na bure. Ni nini mkakati wa Serikali sasa kujenga Vituo hivi vya Polisi katika maeneo ya pembezoni, ikiwemo Mkiwa na Misughaa pamoja na Mungaa ili kuweza kusaidia ulinzi na kwa sababu wananchi wameshafyatua matofali 1000 katika Kata ya Mkiwa na mimi kwenye Mfuko wa Jimbo nimeanza kuwaunga mkono. Ni nini Serikali itafanya kwa ajili ya kutusaidia kumalizia ujenzi huo? (Makofi)

Swali la pili; Askari wetu wanafanya kazi nzuri sana na maeneo mengi hawana nyumba za kuishi, wanakaa mtaani. Ni nini mkakati wa Serikali hususan kwenye Wilaya ya Ikungi, ambayo hatuna nyumba hata moja ya Askari, hata Mkuu wa Polisi Wilaya anaishi mtaani.

Ni nini mkakati wa Serikali kuwajengea makazi Polisi wetu. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, Nakushukuru. Naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema awali, tunapongeza sana juhudi za Mheshimiwa Mbunge lakini na wananchi wa Jimbo kwa kuanzisha ujenzi wa Vituo hivi vya Polisi katika Kata hizo ambazo amezitaja. Mkakati wa Serikali ni kuhakikisha tunaunga mkono juhudi za wananchi ili kuhakikisha tunakamilisha ujenzi huo. Katika hili tuwasiliane na Wizara ili kuhakikisha tunakamilisha majengo hayo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameyataja na wameanza kufanya kazi kwa ajili ya kujenga na kukamilisha vituo hivyo vya Polisi Kata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, moja ya mikakati ya Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuimarisha ulinzi na usalama ni kuona Askari wanaishi katika maeneo stahiki na yenye tija au hali nzuri katika maeneo ya kazi. Kwa hiyo, moja ya maeneo ambayo inaangalia ni kujenga nyumba za Askari katika maeneo yote ikiwemo katika Kata hii. Kwa hiyo, katika mipango ya Serikali ni kuona tunaendelea kujenga makazi ya Askari Polisi na Watumishi wengine ambao wanastahili kupata nyumba hizo ili waweze kufanya kazi zao kwa ubora zaidi. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, Jimbo la Singida Mashariki, Kata ya Misupaa pamoja na Isuna hazina vituo vya afya;

Je, ni lini Serikali itajenga vituo hivyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutajenga vituo vya afya hivi katika Kata ya Isuna na nyinginezo kule Singida kadiri ya upatikanaji wa fedha, na tutaangalia kwenye bajeti inayofuata kuona ni kiasi gani kimetengwa ili Serikali ianze ujenzi huo.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Tunaishukuru sana Serikali kwa kuanza kutekeleza miradi ya Vijiji vya Mkongokieyendo, Minyinga pamoja na Sakaa, lakini kwa masikitiko makubwa, mpaka sasa miradi ile imesimama na inasemekana mkandarasi hajalipwa fedha: Ni lini sasa Serikali italipa fedha ili mkandarasi amalizie miradi ile ambayo ina faida kubwa kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtaturu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji hivi vyote alivyovitaja Mheshimiwa ni kweli miradi inaendelea na sisi kama Wizara tumeshaanza kulipa wakandarasi. Hapo katikati kidogo fedha hatukuwanayo, lakini tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, ametupatia fedha tayari na tunaanza kulipa wakandarasi. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Ninamshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri aliyotoa kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Kondoa, lakini ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu majosho haya yanalenga katika kuboresha afya za mifugo ambayo mwisho wa siku tunapata kitoweo kizuri. Ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba ujenzi huo unasimamiwa vizuri na majosho yale yakamilike kwa muda uliopangwa?

Swali la pili, kwenye Jimbo la Singida Mashariki katika Kata ya Siuyu tulikuwa na josho ambalo sasa hivi limeingiliwa na eneo la Kanisa la RC pale Siuyu na tuliomba lihamishwe liende eneo lingine kwa sababu linakosa sifa ya kutumika pale. Tumeshatenga eneo katika Kijiji cha Siuyu na tuliomba muda mrefu zaidi ya miaka mitatu sasa. Ni lini Serikali itajenga josho kwa ajili ya kutoa huduma ya mifugo katika Kata ya Siuyu. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Swali la kwanza la Mheshimiwa Mbunge ni kwamba amepongeza hii jitihada ambayo tumeifanya lakini vilevile ametaka kuona kwamba kunakuwa na usimamizi mzuri na kuhakikisha haya majosho yanakamilika ili kuimarisha afya ya mifugo. Kwa hiyo, nimuondoe hofu kwamba Wizara ya Mifugo na Uvuvi chini ya Waziri Ulega pamoja na mimi Msaidizi wake tunaahidi kabisa kwamba haya yote yaliyopangwa katika mwaka wa fedha unaokuja na yale ambayo hayajakamilika tutahakikisha katika mwaka wa fedha unaokuja yanakamilika kwa wakati kwa sababu hili ndiyo lengo letu na ndiyo lengo la Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ujenzi wa josho katika Kijiji cha Siuyu ambacho Mheshimiwa Mbunge amekitaja hapa basi naomba jambo hilo nilipokee kwa sababu nitaangalia katika orodha ambayo tunayo hapa kama tumelitenga katika mwaka huu fedha na kama halipo tuone namna gani tunatafuta fedha ili kuliweka katika moja ya vipaumbele vyetu. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa afya za wananchi ni muhimu na ni uwekezaji wa Serikali kwa ajili ya nguvu kazi, kumekuwa na jitihada za wananchi kujenga zahanati katika maeneo mbalimbali kwa nguvu zao na kumekuwa na bajeti ndogo kwenye halmashauri baadhi ambazo hazina uwezo. Je, ni nini mkakati wa Serikali kuweza kutenga fedha kwa ajili ya kumalizia zahanati zilizojengwa na wananchi katika maeneo yetu?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kama nilivyojibu kwenye swali la pili la nyongeza la Mheshimiwa Deus Clement Sangu, kwamba moja ya mkakati wa Serikali hususan katika maeneo ambayo kuna nguvu za wananchi ni kupeleka fedha na kazi kubwa inayofanywa na Ofisi ya Rais, TAMISEMI ni kutafuta fedha kwa ajili ya kumalizia maeneo ambayo wananchi wameweka nguvu zao. Kwa hiyo katika maeneo ambayo Mheshimiwa Mbunge, ameyaainisha yapo katika mpango ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ahsante. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali, lakini naomba niulize swali moja la nyongeza. Kwa sababu suala la ujenzi wa barabara tunatumia fedha nyingi na maeneo mengine mvua zimekuwa zikiharibu miundombinu hii, hii ni kwa sababu labda hatukufanya design au hatukufanya utafiti wa kutosha kwenye athari ya kimazingira. Je, ni nini mkakati wa Serikali katika kuhakikisha kwamba kabla ya ujenzi wa miundombinu hii ambayo inatumia gharama kubwa kuangalia athari za kimazingira zisilete matatizo katika miundombinu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge Mtaturu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara na hasa hizi za udongo na za changalawe mara nyingi zinaharibika hasa kipindi cha mvua na Serikali imekuwa ikitenga fedha nyingi kwa ajili ya kufanya ukarabati na hasa kutengeneza mitaro na mifereji ili kutoa hayo maji, kwa sababu moja ya chanzo kikubwa cha kuharibu barabara ni maji. Pia Serikali inaendelea kutoa elimu kwa wananchi kutotumia barabara kwenye hifadhi za barabara na kupitisha mifugo kwenye barabara. Kwa sababu hicho pia ndiyo chanzo kikubwa cha kufanya uharibifu wa barabara, kwa sababu ukishalima karibu na barabara unatuamisha maji na hivyo barabara zinaharibika. Ahsante. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Tarafa nzima ya Mungaa katika Jimbo la Singida Mashariki nilishasema hapa haina umeme hata kijiji kimoja. Lakini juhudi zilifanyika, kata nne zimeshawekewa nguzo leo ni mwezi wa nne unakwenda wa tano.

Ni lini sasa mkandarasi atarudi kuja kuweka nyaya na transfoma ili wananchi wale waanze kupata umeme wakati wengine wanasubiria kumalizia nguzo zilizobaki?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtaturu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kulitokea changamoto ya ongezeko la bei, hasa kwenye bidhaa za vyuma, copper na aluminium ambazo zinatumika kutengeneza transfoma, nyaya na accessories nyingine katika uunganishaji wa umeme.

Katika kujadili tatizo hili na kulitatua imetuchukua kidogo muda, lakini tunakaribia kumaliza jambo hili na tunaamini mwishoni mwa mwezi huu basi habari ya kuvuta waya, kufunga transfoma na mengine yataendelea kwenye maeneo ambayo tayari nguzo zilishasimamishwa. Na ninaelekeza kwa wakandarasi yale maeneo ambayo bado nguzo hazijasimama basi kazi zisizohusika na ongezeko la bei ziendelee kufanyika wakati mambo mengine haya yakiendelea kukamilika, kuhakikisha kwamba umeme unafika kwa wakati.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Serikali kuhusiana na wastaafu kulipwa mafao kwa wakati, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na malalamiko ya kuchelewa kulipwa mafao yao mapema na malalamiko makubwa yamekuwa kwamba kuna baadhi ya wastaafu makato yao yanakuwa hayajapelekwa kwenye mifuko hiyo. Nini kauli ya Serikali kwenye eneo hili kwa sababu limekuwa na usumbufu mkubwa ambao hauna sababu kwa sababu wamekuwepo kwenye utumishi kwa miaka yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, wastaafu wamekuwa wakiombwa taarifa zao upya baada ya kuwa wameshastaafu. Serikali inakuwa ina taarifa zao zaidi ya miaka 30 haioni kwamba ni usumbufu wa kuwaomba wastaafu ambao wamekuwa nao kwa miaka yote ya umri wao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mbunge wa Singida Mashariki kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kuhusiana na malalamiko ya ucheleweshaji wa malipo tayari tumekwishakufanyia kazi, unakumbuka katika Bunge lako hili yalitolewa maelezo mahsusi na Waziri mwenye dhamana, wakati huo Mheshimiwa Mhagama, na sasa Mheshimiwa Prof. Joyce Ndalichako, tumekwishakuanza kufanya tathmini na mapitio upya kuweza kuhakikisha kwamba wanalipwa kwa wakati na tayari kuna mifumo mbalimbali ya kitehama ambayo imeanzishwa, ikiwemo mfumo wa MAS pamoja na CFM, hii yote ni kwa ajili ya kutengeneza ile membership administration system ambayo ni mfumo wa ki-TEHAMA.

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya hapo hivi karibuni tutaanza ziara ya mkoa kwa mkoa kuweza kuanza kusikiliza changamoto za wastaafu ikiwa ni pamoja na kuhakiki taarifa mbalimbali ili kuweza kuhakikisha kwamba wanalipwa kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali lake la pili, ameulizia kuhusiana na hawa wastaafu wanapoombwa taarifa mpya. Utakumbuka kwenye Bunge lako hili tulitoa taarifa kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu kwamba hili suala la uombaji wa barua za wastaafu limefikia mwisho, kwa sababu taarifa hizi sasa ni wajibu wa mifuko yenyewe kuweza kuhakikisha zinatunza kumbukumbu sahihi za wanachama wake ikiwa ni pamoja na ndani ya huo mfumo wa membership administration service system, pamoja na mfumo wa NSSF weyewe ambao ni core fund management system zote hizi taarifa zitakuwa mle.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaendelea kutumia fursa hii kuwasihi waajiri kote nchini kuwasilisha michango kwa wakati ya wanachama ili wasihangaike. Pili kuhakikisha mfuko wenyewe unahakiki taarifa za wale wastaafu hata mwaka mmoja kabla ya kustaafu ili kupunguza usumbufu kwa watumishi hawa waliotumikia Taifa vizuri. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba niulize swali la nyongeza kwamba kwa sababu ili Serikali iweze kuweka uvutiaji wa wawekezaji katika sekta ya maziwa ni wajibu wake pia kujenga vituo vya kukusanyia maziwa. Ni nini mpango wa Serikali kujenga vituo vya kukusanyia maziwa katika Mkoa wa Singida ili iwe rahisi wawekezaji kuja kuwekeza kwenye sekta hiyo?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, ni kweli kama nilivyosema kwenye majibu ya nyongeza, kwamba; moja ya maeneo ambayo Serikali ya Awamu ya Sita inaweka msisitizo sana ni maeneo ya vituo vya kukusanya maziwa na hasa na kuweka storage facilities ambazo zitasaidia kutunza maziwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mtaturu kwamba, eneo hilo pia nako tutakuja kuweka vituo hivi vya kukusanyia maziwa na hasa vifaa hivi vya kutunzia maziwa ili yasiharibike wakati yanasubiri kwenda kwenye viwanda.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu ya Serikali. Sasa nina maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa coverage ya maji katika Wilaya ya Ikungi ni asilimia 53 ambayo iko chini sana, kuna maeneo ambayo yana changamoto kubwa. Sasa nataka tu nijue, ni nini mpango wa Serikali wa muda mfupi kuwapatia maji wananchi wa Wilaya ya Ikungi kwa maana ya Kata za Kikio katika Kijiji cha Nkundi, Lighwa katika Kijiji cha Mwisi na Issuna katika Kijiji cha Issuna A, Kitongoji cha Manjaru?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kuna visima vilivyochimbwa ambavyo bado havijawekewa miundombinu. Nilitaka nijue kwamba, visima hivyo katika vijiji vya Msule, Mkinya, Mang’onyi na Mbwanchiki pamoja na Ujaire.

Ni lini sasa Serikali itatenga fedha ya kujenga miundombinu ili kuondoa adha ya maji katika maeneo haya niliyoyataja? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mpango wa muda mfupi kwenye kata na vijiji alivyovitaja Mheshimiwa Mtaturu, ni kwamba tutaendelea kufanya jitihada za kuhakikisha tunakuja kuchimba visima.

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie Bunge lako Tukufu nimwagize RM Singida, ahahakikishe anakwenda kwenye hizi kata, wafanye usanifu ili kuona wapi tunaweza tukapata maji chini ya ardhi ili sasa waweze kupelekewa gari wakachimbe visima na wananchi waweze kupata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, lini tutatenga fedha kwa ajili ya miundombinu kwenye visima tulivyochimba; kwa utaratibu wa Wizara, tukishachimba visima kazi inayofuata ni usambazaji. Kwa hiyo, nina uhakika kama mwaka huu wa fedha kwa maana ya kuanzia leo mpaka Juni, Wizara tukawa tumepata fedha ambazo hazitoshelezi kuwafikia, mwaka ujao wa fedha lazima maeneo haya yote tuje tusambaze maji katika visima ambavyo tumevichimba.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba niulize swali la nyongeza kwamba kwa sababu ili Serikali iweze kuweka uvutiaji wa wawekezaji katika sekta ya maziwa ni wajibu wake pia kujenga vituo vya kukusanyia maziwa. Ni nini mpango wa Serikali kujenga vituo vya kukusanyia maziwa katika Mkoa wa Singida ili iwe rahisi wawekezaji kuja kuwekeza kwenye sekta hiyo?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, ni kweli kama nilivyosema kwenye majibu ya nyongeza, kwamba; moja ya maeneo ambayo Serikali ya Awamu ya Sita inaweka msisitizo sana ni maeneo ya vituo vya kukusanya maziwa na hasa na kuweka storage facilities ambazo zitasaidia kutunza maziwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mtaturu kwamba, eneo hilo pia nako tutakuja kuweka vituo hivi vya kukusanyia maziwa na hasa vifaa hivi vya kutunzia maziwa ili yasiharibike wakati yanasubiri kwenda kwenye viwanda.