Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Miraji Jumanne Mtaturu (28 total)

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja katika Kamati hizi mbili ambazo zimewasilisha taarifa zao, nami nipo kwenye Kamati ya Miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumshukuru sana Mungu ambaye ni mwingi wa rehema kutujalia uzima na kuweza kuendelea kufanya majukumu haya kwa ajili ya Watanzania wenzetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nitumie nafasi hii kwanza kumshukuru sana Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ambaye kwa hakika mwelekeo na dhamira yake imekuwa inarahisisha sana utendaji wa Serikali. Hii yote ni kwa sababu wananchi wa Tanzania wamekuwa na imani naye na ndiyo maana basi naye amekuwa akifanya kazi hii kama ambavyo wananchi wanatarajia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapongeza kwa namna ambavyo tumeendelea kupata bajeti kwenye hii Wizara yetu ya Ujenzi kwa maana ya kutekeleza majukumu yaliyopo ndani ya Wizara hii. Kama alivyoeleza Mwenyekiti wetu pale asubuhi, ni kwamba tumepata fedha za kutosha kutekeleza miradi mbalimbali ambapo haya mashirika mbalimbali na taasisi yalileta taarifa zao kwenye Kamati yetu na kuona namna ambavyo Serikali iliendelea kuleta fedha. Najua bado kuna changamoto lakini ninaamini zitatatuliwa kulingana na muda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushahidi pekee ni pamoja na maeneo mbalimbali ikiwemo ununuzi wa ndege, ujenzi wa barabara za lami katika nchi yetu, mawasiliano mbalimbali, kwa maana minara inajengwa na hata juzi tumesaidi mkataba kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunapeleka minara kwenye vijiji vipatavyo 555 nchi nzima. Yote hiyo ni dhamira ya dhati ya Serikali kuhakikisha kwamba inaboresha mawasiliano na huduma mbalimbali zinazotokana na Wizara yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili nitumie nafasi hii kuendelea kumshukuru sana Mwenyekiti wetu Mheshimiwa Selemani Kakoso pamoja na Makamu wake Mheshimiwa Hawa Mchafu ambao wamekuwa wakiongoza vizuri Kamati hii. Vile vile Wajumbe kwa pamoja tumekuwa tuna ushirikiano mkubwa katika kuhakikisha kwamba tunahoji mambo ya msingi kwa ajili ya maslahi ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati yetu tulipata fursa ya kukutana na taasisi mbalimbali zilizopo chini ya Wizara hii ya Ujenzi, Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Mawaziri wake walituletea wataalam hao na tumeendelea kuhojiana kwenye Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia sekta mbili ambazo nilidhani niweze kuzitolea maelezo ndani ya Bunge lako Tukufu. Nianze na wenzetu wa Wakala wa Huduma za Meli. Kama ambavyo tunajua kwamba sisi kijiografia katika ukanda huu tumekaa vizuri sana katika biashara kwa maana ya bandari na tumekuwa tukifanya hivyo kwa miaka mingi na tumekuwa tukipata faida kubwa ya fedha tunapotoa mizigo hapa kwenda kwenye nchi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi nzuri inayofanywa, changamoto moja kubwa sana ambayo tumeigundua; tumefanikiwa kukutana na wadau wa sekta hiyo ambao ni wasafirishaji mbalimbali wanaoleta mizigo kupitia bandari yetu, wamekuwa na malalamiko mbalimbali ikiwemo ucheleweshaji wa mizigo yao kutolewa kwenye bandari. Hii imesababisha baadhi ya wafanyabiashara kuhamisha mizigo yao na kushushia kwenye bandari nyingine ikiwemo Beira pamoja na pale Mombasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ukilisikiliza kwenye Kamati tumeenda kwa kina sana. Kwa kweli ni jambo ambalo tusipolifanyia kazi, wafanyabiashara wataondoka wengi wataenda kushushia mizigo eneo ambalo siyo hapa kwetu. Hii itakuwa ni athari kubwa kwenye uchumi wetu; na haya ambayo tunampongeza leo Mheshimiwa Rais na Serikali yake hawawezi kufanya bila kuwa na fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la storage limekuwa ni tatizo kubwa lakini pia kumekuwa na urasimu mkubwa sana katika utoaji wa mizigo. Kuna manung‟uniko makubwa kwa wadau. Tunaiomba Serikali ikakae na wadau iwasikilize na watoe ushauri wao namna ya kuenenda. Wao hawana tatizo na ulipaji, wana tatizo na urasimu mkubwa uliopo ndani ya mamlaka hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivi, tutakuwa tunaitendea haki nchi yetu na kwa hakika tutakuwa tuna uwezo wa kuongeza mapato ya kutosha kwa ajili ya kuwa na uhakika wa kutekeleza miradi ya kimaendeleo ambayo tunayo katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wametueleza wenzetu pale kuhusu uchakavu wa bandari nchini. Ni ombi letu kupitia Bunge lako Serikali iende ikaboreshe miundombinu iliyopo kwenye bandari zetu. Najua juhudi zinaendelea, lakini kwa sasa wao wenyewe kama mamlaka walituambia kwamba changamoto kubwa ilikuwa ni uchakavu wa bandari zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile ushindani. Chombo hiki kinachosimamia biashara hii ni vizuri ikajua kwamba wenzetu wanafanyaje? Maana leo hii baadhi ya wengine wanaona wanakuwa na comfort kubwa kuwa kwenye bandari nyingine kuliko kwenye bandari yetu ya hapa Dar es Salaam. Tukifanya hivyo, tutakwenda kuongeza nguvu kubwa ya kuvutia wafanyabiashara kushushia mizigo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwenye sekta moja ya ujenzi ambayo ni wenzetu wa TBA. TBA ni wakala, anafanya kazi nzuri. Lengo la kuanzishwa kwake ilikuwa ni kusaidia eneo la ujenzi katika majengo mbalimbali ya Serikali yaliyopo hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumegundua pamoja na juhudi wanazofanya, wenzetu wa TBA wana upungufu mkubwa wa rasilimali watu, hawana wafanyakazi wa kutosha katika kutekeleza miradi yao. Kwa hiyo, ombi letu wahakikishe kwamba wanaongezewa rasilimali watu ili waweze kufanya kazi yao vizuri na lile lengo la kuanzishwa kwao liwe limetimia kwa sababu wanakwenda kufanya kazi ambayo inaenda kusaidia Sekta ya Ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, ni namna ambavyo menejimenti yao, flow ya fedha na vitu kama hivyo nayo imekuwa ni changamoto katika usimamizi. Ombi letu ni kwamba kupitia Kamati tuliishauri na hapa ninaomba niongezee tena kwamba TBA wakiwezeshwa wanaweza kuwa wanafanya kazi nzuri sana na wakaingia kwenye soko la ushindani katika Sekta ya Ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tena kusema kwamba sisi wote ni Watanzania, tuendelee kwa pamoja kuwa kama Taifa moja, tofauti zetu za kimitazamo zisianze kutuingiza kwenye machafuko ambayo hayana sababu. Ninaamini kabisa wote tuna nia njema ya kuwatumikia Watanzania, lakini kila mmoja ana views zake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ombi langu ni hilo tu kama ambavyo leo asubuhi tumejadili baadhi ya wenzetu wanapotuchonganisha na Jumuiya za Kimataifa, nadhani inatuweka katika hali ambayo siyo salama sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya, naomba kuunga hoja mkono kwa asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti hii. Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2021/2022 ambayo iliwasilishwa hap ana Mheshimiwa Waziri wa Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema kutujalia uzima na kuweza kukutana hapa. Lakini pili nichukue nafasi hii kwa dhati ya moyo wangu kabisa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu, Jemadari wetu, Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuiongoza nchi vizuri kwa muda huu ambao tukonae na kwa namna ambavyo amekuwa akisikiliza maoni ya Wabunge. Miongoni mwa sifa inayompamba kiongozi yeyote ni kusikiliza watu wake; Mama yetu anatusikiliza na anawasikiliza wananchi na anatuongoza vizuri, tunampongeza sana na tunamtakia afya njema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushahidi ni huu ambao tumeuona tumeongea sana hapa wakati tunachangia bajeti za kisekta. Tulizungumza sana habari ya barabara zetu ziliziko vijijini na tukaeleza kiu yetu ya namna ambavyo tunatakiwa kutenga fedha nyingi za kutosha kwa ajili ya kujenga barabara za vijijini. Kama haitoshi ameweza kutoa milioni 500 kwa kila jimbo na hivi tunavyoongea ma-manager wetu wa TARURA wanaendelea kufanya kazi ya kufanya maandalizi ya kujenga barabara hizi. Maana yake barabara za vijijini zikiwa salama maana yake huduma mbalimbali za kijamii ikiwemo kusafirisha mazao zitaenda kufanikiwa katika vijiji vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada yamaneno hayo niseme nimpongeze sana kaka yangu Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Mchemba, kwa kuwasilisha vizuri bajeti hii ambayo tunaijadili. Kwa hakika bajeti hii imejikita katika kutatua kero za wananchi, bajeti hii imeonesha muelekeo wa Serikali kwa mwaka mmoja ujao; kwa kweli, nimpongeze yeye pamoja na watendaji wake akiwemo Naibu Waziri pamoja na katibu mkuu kwa kazi nzuri ya kutuandalia bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizi nimeona maeneo mengi yamefanyiwa kazi, lakini ni vizuri nitoe ushauri wangu ili tuweze kubeba kwa pamoja bajeti hii ambayo inaenda kuboresha maisha ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwenye eneo la kilimo, wote wamezungumza hapa tumepongeza juhudi mbalimbali, lakini tumeangalia katika hili kwamba, bajeti ya Serikali inaeleza wazi kwamba, kilimo kinachangia fedha katika Serikali asilimia zaidi ya 26, lakini tunatenga fedha kidogo sana za maendeleo za kuhakikisha kwamba, tunapanga vizuri mipango ya kilimo cha nchi yetu, lakini wote tunajua kwamba, asilimia zaidi ya 65 ya wananchi wetu ndio wanafanya kilimo vijijini. Maana yake nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwamba, shughuli kubwa inayofanywa na wananchi wetu wa Tanzania ni kilimo, lakini kilimo hiki kikitumika vizuri tukapata mazao ya kutosha tutaweza kupeleka malighafi nyingi kwenye viwanda. Maana yake tutakuwa na uwezo mkubwa wa kukuza viwanda na ambayo itatusaidia sana kuongeza pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ombi langu nilikuwa nataka niseme tu kwamba, pamoja na kuwa nchi yetu imeingia kwenye kipato cha kati na kama tusipoangalia vizuri tutarudi tena nyuma, ombi langu ni kwamba, tuongeze nguvu sana kwenye kilimo cha nchi yetu. Wananchi wetu wasaidiwe walime kilimo cha kisasa. Ninajua juhudi zipo kubwa na kwenye hili nitaongelea zao la alizeti kwa asilimia kubwa kwa sababu, zao hili linalimwa sana katika mikoa 19 ya nchi yetu, pamoja na Mkoa wa Singida tunalima sana alizeti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa Majaliwa. Tarehe 13 mwezi wa sita aliitisha kikao cha wadau wa alizeti katika Mkoa wa Singida na alionesha wazi kwamba, Serikali imedhamiria kuwekeza sana, ili kuondokana na kuagiza mafuta nje ya nchi. Tunatumia fedha zaidi ya bilioni 400 kuagiza mafuta kila mwaka ili kufidia gape lililopo la mafuta katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka nieleze kwamba, tumepata mwanga mzuri juzi tulivyokaa na wadau. Na Mheshimiwa Waziri Mkuu ametumia muda wa saa nane amekaa kwenye kiti anasikiliza maoni ya wadau, ikiwemo sisi Wabunge. Niombe sana eneo ambalo limeelezwa sana ni sehemu ya kupata pembejeo ikiwemo mbegu bora zenye kutoa tija. Niombe sana kupitia bajeti hii tuongeze fedha za mbegu bora, ili wananchi wetu waweze kulima alizeti itakayoleta mafuta mengi, uzalishaji mwingi na kusaidia viwanda vyetu viweze kuzalisha mafuta mwaka mzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi tunavyoongea kwa sababu uzalishaji ni mdogo tumegundua kwamba, wanafanya miezi mitatu tu ya mwanzo, miezi iliyobakia yote hakuna uzalishaji wa mafuta kwa sababu, hakuna mbegu za mafuta za kukamua. Kwa hiyo, niombe sana kwenye eneo hili tumesema kwamba, tutahakikisha kwamba, miundombinu ya umwagiliaji tutaiongeza. Kwenye eneo hili ninaomba sana Serikali iongeze nguvu kwani kilimo hiki kikiwepo kitasaidia sana uzalishaji wa kutosha bila kutegemea mvua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwenye hili niseme kwenye eneo moja tumekuwa tukitengewa fedha, lakini hazitoki kwenye skimu ya umwagiliaji katika kata yangu moja inaitwa Mang’onyi. Skimu ya umwagiliaji hii ikikamilika itasaidia wakulima wengi kupata kilimo cha umwagiliaji na kuongeza tija katika kilimo chao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama haitoshi tumeongelea habari ya upimaji wa udongo. Kuna maeneo mengi wakulima wanalima tu ilimradi wanalima, lakini hawajui ardhi yao ina uwezo gani wa kuzalisha mazao. Tumeomba sana watafiti wetu wafanye kazi hiyo kuhakikisha kwamba, ardhi ambayo tunalima inakuwa ni ardhi inayojulikana wazi; kama inahitaji mbolea ijulikane ni mbolea kiasi gani, ili wakulima wetu waweze kulima kwa uhakika. Na kwenye hili Waziri Mkuu ameelekeza kwamba, wenzetu wataalamu wa kilimo waweze kufanya kazi yao vizuri, washauri kwenye halmashauri zetu ili tuweze kuhakikisha tunalima kilimo cha uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kilimo hiki ni pamoja na kuhakikisha kwamba, tunaongeza kilimo cha chakula kwa maana ya mazao mbalimbali yanayotokea huku, ili tuwe na usalama wa chakula. Niseme tu, nieleze tu kwamba, pamoja na kwamba, tunaongelea kilimo, lakini nishukuru sana Mheshimiwa Rais ameonesha wazi kwamba, bajeti hii ni kweli ni bajeti ya kazi iendelee. Kwa sababu, miradi yote ya kimkakati amesema itaendelea na juzi akiwa Mwanza amezindua tena ujenzi wa reli ya SGR kutoka Mwanza kwenda Isaka maana yake sasa inakutana katikati iweze kukamilika ianze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, imeeleza waziwazi usafiri wa anga pamoja na ununuzi wa meli ambao amesaini juzi meli tano zinaenda kujengwa pamoja na uboreshaji wa bandari. Hili ni jambo jema kabisa, tuendelee kuiomba Wizara, tuendelee kutoa fedha ambazo zimetengwa ili miradi hii isikwame njiani ili tuweze kupata matokeo ambayo tunayatarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye eneo hili nitaongelea kidogo kwenye eneo la wilaya yangu. Wilaya ya Ikungi tulikuwa na maombi ya muda mrefu, tunaomba tuwe na mradi wa kimkakati na sisi tuwe na stendi ya wilaya; hatuna stendi ya mabasi ambayo inaweza kukidhi haja iliyoko pale katika wilaya yetu. Lakini kwenye eneo hili pia nilikuwa naomba tupate soko la kisasa katika eneo lile katika wilaya yetu, ili kuongeza mapato ya halmashauri ili yasaidiane na bajeti ya Serikali katika kuleta maendeleo ya wananchi wetu katika vijiji vyetu pamoja na wilaya zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niongelee jambo la tatu ni jambo la maslahi ya watumishi. Hili eneo niipongeze sana Serikali kwa kuamua sasa kwamba, wafanyakazi wapatoa 94,000 wanaenda kupandishwa madaraja na fedha zipo katika bajeti hii. ni jambo jema sana pamoja na kuwa tunasema waongezewe mshahara, lakini ukipandishwa daraja una uhakika na kulipwa mshahara katika daraja lako. Wengine wanajiendeleza katika elimu, lakini wanakuwa wanabaki hawapandishwi madaraja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Wizara husika ihakikishe inasimamia vizuri wafanyakazi hawa wapate haki yao ya kuhakikisha wanapanda madaraja. Nimeona zimetengwa karibia bilioni 400 zinaenda kufanya kazi hii ni jambo jema sana tunamshukuru sana Rais, tunamshukuru sana Waziri kwa kuwasilisha jambo hili; lakini niendelee kuomba tuendelee kuendelea kuwaza kuongeza mapato, ili tuweze kuongeza mishahara ya watumishi ambayo kwa kweli, wameendelea kuomba kila mara na dhamira ya Mheshimiwa Rais tunaiona atawaongezea kama alivyosema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini eneo hili tumeongelea pale Madiwani, Madiwani wanafanya kazi nzuri sana kule. Nipongeze kwamba, fedha zile ambazo walikuwa wanalipwa posho yao itaenda moja kwa moja kutoka kwenye Serikali kuu ni jambo jema. Lakini niombe sana Mheshimiwa hii ilikuwa ni hiyo fedha wanalipwa huko nyuma kwa hiyo, wamekuwa na maombi ya kuda mrefu tunaomba posho ziongezwe za Madiwani ili wafanye kazi nzuri ambayo wanaendelea kuifanya katika maeneo yetu. Sisi tukiwa huku wao wanafanya kazi vijijini kule kukaa karibu na wananchi katika kusimamia maendeleo, tukiwaongezea wataongeza motisha, wataongeza nguvu kubwa ya kusimamia maendeleo na fedha hizi tunazozipeleka kule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo tumeongelea habari ya suala la Madiwani, lakini kuna namna ambavyo tunadhani kule kwenye vijiji tuone namna ambavyo tutaongeza fedha kwa ajili ya kuwasaidia viongozi wetu wa vijiji ili waweze kufanya kazi kwa tija.

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga. Ahsante sana.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo ninaunga mkono asilimia 100 bajeti hii. Nawatakia kila la heri, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuweza kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu Mpango wa Miaka Mitano na ule wa Mwaka Mmoja. Kwa hakika nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kutujalia uzima na kuweza kukutana leo hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda basi niende moja kwa moja kwenye kuchangia Mpango ulioko mbele yetu. Kwanza nianze kwa kupongeza Mpango ule wa Pili wa Miaka Mitano ambao ulipita, tumeuona tathmini yake na katika muda huu tumeona maendeleo makubwa ya nchi yetu. Nichukue nafasi hii kumpongeza sana Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, pamoja na Serikali na watumishi wote ambao wameshirikiana katika kutekeleza Mpango ule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunapokuja kwenye Mpango huu wa Miaka Mitano na hasa ule wa Mwaka Mmoja tunaona namna ambavyo tumejipanga kwenda mbele na nitachangia sana leo kwenye eneo ambalo limesema kufungamanisha ukuaji wa uchumi na maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri kwamba Watanzania wengi wanafanya kilimo katika nchi yetu, zaidi ya 70% wanafanya kilimo na kilimo ndiyo uti wa mgongo wa Taifa letu. Naomba nikiri wazi kumekuwa na juhudi mbalimbali za kuhakikisha kilimo chetu kinabadilika na kama ambavyo Mheshimiwa Rais amesema katika hotuba yake, kwamba tutaongeza juhudi katika kuwekeza kwenye kilimo na kilimo chenyewe ni kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo tukikifanya vizuri pamoja kuwa kitatusaidia kwenye chakula lakini mapato mengi yanapatikana kwenye kilimo. Leo Halmashauri zetu nyingi zinategemea mapato makubwa kutoka kwenye mazao mbalimbali, kwa hiyo maana yake tukiwekeza kwenye kilimo kutakuwa na mapinduzi makubwa ya kiuchumi na itatusaidia sana kwenda mbele kama Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hoja yangu ni kwamba ni wazi tumefanya research nyingi, ni wazi tumepata maoni mengi, ni wajibu wa Serikali sasa kuyatendea kazi mawazo yale. Hatuwezi kuwa tunatoa ushauri na ushauri ule tunauacha kwenye makabati. Ombi langu nataka niiombe Wizara ije na mpango mahususi katika kukuza kilimo chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongelea kwenye suala dogo sana la ambavyo tunasema Tanzania ya viwanda, lakini viwanda vyetu haviwezi kwenda mbali kama hatujawekeza kwenye kilimo kwa sababu tunahitaji malighafi kwenye viwanda vyetu. Kama leo hatujawekeza vizuri kwenye kilimo chenye pembejeo, mbolea, viatilifu na Maafisa Ugani ambao wanafanya wajibu wao. Naamini huko vijijini wote tunatoka hali ya Maafisa Ugani ni imechoka, hali ni mbaya idara ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii anaweza kwenda kiongozi yeyote ukakutana na Afisa Ugani, wewe unaweza kuwa na uelewa mkubwa kuliko Afisa Ugani maana yake Afisa Ugani huyu hawezi kumsaidia mkulima. Ombi langu nataka niiombe Serikali hasa Wizara ya Kilimo itusaidie kuongeza nguvu kwenye Maafisa Ugani. Naamini kabisa wao pia ni mashahidi kuna baadhi ya mazao ya kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa leo nitaongelea zao moja tu la alizeti, mafuta; leo hii sisi tunaagiza tunatakiwa kwa mwaka kutumia metric tons 570,000 za mafuta, lakini uwezo wetu ni 210,000 tu, maana yake ni karibu nusu tunaagiza nje ya nchi. Kwa hiyo maana yake ni kwamba tunatumia fedha za kigeni nyingi kuagiza mafuta ya kula, hili jambo ni vema tukabadilisha mwenendo wetu tuhakikishe kwamba zao la alizeti pamoja na mazao ya mbegu za mafuta, tuchukue hatua kubwa katika kuhakikisha tunawekeza vya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatumia karibu bilioni 460 kwa mwaka kuagiza mafuta nje ya nchi, ndiyo maana leo tunakuta kuna upungufu wa mafuta ni kwa sababu hatujawekeza vizuri kwenye eneo hili. Niseme tu kwenye eneo hili tukija na mpango kweli unaosema kwamba wa block farming itakuwa ni jibu la tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia mkakati wa Serikali katika kuhakikisha kwamba inakuza kilimo cha umwagiliaji kutoka kwenye heka zile ambazo zimeelezwa 461,000 tutakwenda kuhakikisha kwamba tunaongeza zinakuwa 694,000, bado tuna safari ndefu. Lazima tuwe na mapinduzi ya kweli ya kuhakikisha kwamba tunawekeza kwenye kilimo cha umwagiliaji, tusiendelee kusubiri mvua ambayo hatuna uhakika nazo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunavyoongea habari ya umwagiliaji, tunasemea habari ya kwamba uhakika wa kilimo chetu tusitegemee mvua, lakini wengine walisema hapa, maji yanayomwagika haya kwenye mito kila mwaka, tunayatumiaje ili kuweza kuhakikisha kilimo chetu kinakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hilo la alizeti, nadhani kuwe na mkakati au msukumo maalum, kama tunaweza kuwa na Bodi ya Korosho, kama tunaweza kuwa na Bodi ya Pamba, kwa nini tusiwe na Bodi ya Alizeti ili kuweza kuweka msukumo mkubwa zaidi. Tumeambiwa hapa kuna zaidi ya mikoa nane inayoweza kulima alizeti. Tukiwa na Bodi hii ya Alizeti tutaweka mkakati maalum wa kuhakikisha kwamba tunalima alizeti kwa wingi, tunawezesha viwanda vyetu na mwisho wa siku tunakuwa na mafuta ya kula ya kutosha. Kwa hiyo ombi langu, naomba kama tunazo hizo nyingine, basi na hii Bodi ya Alizeti iwe ni jibu la kuhakikisha kwamba tunapata mafuta ya kula ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya, naomba nichukue nafasi hii kuunga mkono hoja, naomba niwaachie changamoto hiyo Wizara ya Kilimo. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa Mwaka 2022/2023, ikiwa ni maandalizi ya bajeti ijayo. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujalia uzima kukutana jioni ya leo. Pili, nichukue nafasi hii kumpongeza sana na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu, Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoifanya ya kujenga nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama haitoshi ameendelea kuunganisha nchi yetu na dunia kuhakikisha kwamba, anashirikiana na nchi nyingine katika kuiunganisha nchi yetu kidiplomasia. Sisi tumekuwa tukipata faida kubwa sana ya kimaendeleo na fursa lukuki za kusukuma mbele ajenda za maendeleo ya Watanzania na ukiangalia ni juzi tu tumetoka kupata fedha ambazo zinaenda kupunguza matatizo makubwa ambayo tunayo kwenye sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya, maji na huduma nyingine za kijamii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze moja kwa moja kwenye Mpango ambao umewasilishwa na Waziri wa Fedha. Nichukue nafasi hii kumpongeza yeye pamoja na wasaidizi wake kwa Mpango waliotuletea ambao unatupa fursa sisi kuanza kuuchambua na kutoa maoni yetu; nikianza na dhima ya Mpango wenyewe ambao unaeleza kwamba, ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikipita kwenye eneo hilo wengi wetu tumeeleza hapa, asilimia zaidi ya 65 ya Watanzania wanafanya shughuli za kilimo. Wote tusipoongelea kilimo maana yake tutakuwa hatujagusa Watanzania wengi ambao tunafanya nao kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili kama ulivyosema mwenyewe kwenye mpango haijaelezwa kinagaubaga, ni namna gani Serikali imejipanga kuwekeza fedha za kutosha kuhakikisha kwamba, tunabadilisha kilimo ambacho kinaajiri watu wengi. Kwenye eneo hili tusipoongea kwa kina na kujadiliana kama Taifa hatuwezi kuvuka. Eneo ambalo unapata fedha kwa maana ya unaingiza pato zaidi ya asilimia 26 huwezi kuacha bila kuwa na mpango mahususi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mdogo, ukiangalia eneo hili ni kwamba, tunapiga kelele sasa hivi, leo tunaenda kwenye msimu wa kilimo hatuna mbolea na mbolea iko juu sana, lakini juzi tumetoka kuazimia hapa kama Bunge tukaielekeza Serikali itafute fedha za kununua mazao ya wakulima. Kwa hiyo, kuna mambo mawili yanagongana hapo, tunahamasisha wakulima walime, lakini mwisho wa siku hakuna masoko ya kutosha ambayo yalipaswa yafanywe na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, leo tunataka kwenda kwenye kilimo chenyewe pamoja na athari za UVIKO-19 Serikali ina wajibu wa kuwasaidia wakulima hawa ili tusiendelee kulalamika. Kwa hiyo, nadhani kuna mahali ambapo hatutimizi wajibu wetu kama Taifa. Naomba na nilishasema hapa kwenye Bunge lako siku za nyuma, sehemu ambayo ina wasomi wengi ukiangalia Maprofesa, Madokta na baadhi ya watu ambao wamesoma vizuri nenda ukaangalie ni sekta ya kilimo, wako pale Wizarani pamoja na maeneo mengine. Wamefanya researches za kutosha, wametoa ushauri wa kutosha, lakini tatizo lililopo tuna tatizo la kutenga fedha za kukisaidia kilimo cha nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunaongelea habari ya bajeti ya bilioni 80, wakati tunasema sisi tunataka kufikia malengo ya kuongeza kilimo cha umwagiliaji ambacho kinahitaji uwekezaji wa kutosha. Hatuko serious kama Taifa kama hatujaingia kwenye eneo hili.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mtaturu nikuhakikishie wale Maprofesa na Madokta walioko Wizara ya Kilimo hawana hata robo eka wao wenyewe. Kama wewe unayajua mashamba yao nipeleke siku moja nikaone. Ahsante, endelea kuchangia. (Kicheko)

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunikumbusha hilo. Kwa hiyo, maana yake ni kwamba, tupo kwenye theory zaidi, hatupo kwenye practical. Kwa hiyo, ombi langu kwa Serikali, kama kweli tunasema tunataka kuwekeza, wengi wetu toka jana na juzi wamesema, tuhakikishe tunapata angalau trilioni moja iwekezwe ndani ya sekta ya kilimo ili tuweze kupata Maafisa Ugani wa kutosha, tuweze kuwa na mbolea ya uhakika, lakini zaidi tuwe na uhakika wa Maafisa Ugani ambao ni wataalam wa kilimo kwenye vijiji vyetu. Tusipofanya hivyo, hatuwezi kuvuka na hatuwezi kukibadilisha kilimo chetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaongelea habari ya kilimo cha kutegemea mvua, leo hii wenzetu wa hali ya hewa wametuambia kwamba, tutakuwa na mvua chini ya wastani msimu unaokuja. Je, mkakati uko vipi katika eneo hili kupitia Mpango huu ambao tunaenda kuuweka? Tunayo taarifa nzuri tunaletewa na Serikali, hali ya hewa wametuambia hatutakuwa na mvua ya kutosha, sisi kama Taifa tumejiandaaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni kwamba, tunasubiri baadaye tuje tuseme kulikuwa na changamoto ya mvua chache wakati tulijua kabla. Kwa hiyo, nadhani kwenye eneo la uwekezaji tumesema hapa kuhusu mabwawa, tumesema hapa namna ya kilimo cha umwagiliaji, lakini tumejiandaaje kweli kuwasaidia wakulima wetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukienda kila halmashauri hapa inaongelea habari ya upungufu wa Maafisa Ugani, ambao ni wataalam. Leo wakulima wengi wanalima kilimo cha kurithi, kilimo kilekile cha mazoea ambacho mtu anapata debe mbili, tatu kwenye eka moja, kitu ambacho anapoteza muda tu. Kwa hiyo, ombi langu kwenye eneo hili, Mpango uweze kubainisha bayana namba gani tutaweza kutoka kumsaidia mkulima ambaye yuko pale kijijini ambaye kwa hakika anaweza kuendelea kusaidia hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu namna ambavyo amejitahidi kupita kila mahali anahamasisha kilimo hiki. Anahamasisha kilimo mbalimbali…

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge makofi kwa Waziri Mkuu jamani. (Makofi)

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, tumpigie makofi mengi Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

MWENYEKITI: Kweli kabisa. katika eneo la kilimo amehangaika sana, kushoto, kulia na kasi. Endelea Mheshimiwa Mtaturu. (Makofi)

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio maana nimembatiza Mheshimiwa Waziri Mkuu, yeye ndio Afisa Ugani Mkuu katika nchi yetu. Anafanya kazi nzuri ya kuhamasisha kilimo, pasipowezekana panawezekana kwa namna ambavyo anakaa na sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushahidi ninao alikuja Singida amekaa na sisi siku nzima bila kutoka kwenye kiti. Tukaweka mkakati wa namna ambavyo zao la alizeti litaenda kusaidia nchi hii katika mafuta ya kula. Kwa hiyo, kwenye hili Mheshimiwa Waziri Mkuu tunampongeza na sisi kama Wabunge tuiombe Serikali iongeze fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba, maeneo hayo tunakwenda vizuri. (Makofi)

MWENYEKITI: Nikupe Taarifa uende nayo Mheshimiwa Mtaturu, Singida safari hii kwenye alizeti mtakuwa wa pili baada ya Dodoma. (Makofi)

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwa sababu, wewe mwenyewe umesema ndani ya Hansard imeandikwa, tunaendelea tutakukumbusha. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nataka niongelee eneo la miundombinu. Ili uweze kuleta uchumi, uchumi uimarike lazima uwe na miundombinu mizuri ya kutoa mazao kwenye maeneo ya wakulima. Eneo hili nitakumbusha barabara ambazo zimetajwa miaka yote; mfano, Barabara ya Mkiwa – Itigi kwenda Makongolosi. Barabara ile ilitengewa fedha, ikasemwa tutaanza kwenye Mpango uliopita tutajenga kilometa 50, lakini juzi wamesema kilometa 20 na mpaka sasa tunavyoongea bado haijatangazwa hata kutangazwa. Hili nalo ni tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Barabara ya Singida – Kwamtoro kwenda Kiberashi mpaka Tanga; nayo barabara ile ilitengewa kilometa 20, mpaka leo haijaanza. Tunategemea nini kama Mpango huu hauwezi kwenda kutekelezwa na kuwa na mpango.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele ya pili, Mheshimiwa Mtaturu.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya, naomba nirudie tena kusema Serikali ijipange vizuri kuleta mpango mzuri ambao utakuja kutusogeza mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja ambayo ipo mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimshukuru Mungu wa Rehema kutujaalia uzima na afya na wale wanaotekeleza Mwezi Mtukufu wa Ramadhani tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa neema hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza kwa kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, mama yetu, Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya kwa ajili ya kuwaletea Watanzania maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha mwaka mmoja wa uongozi wake tumeona maono yake, tumeona dhamira yake na kwa hakika tumeona huruma yake kwa ajili ya Watanzania na sisi tunao wajibu wa kuendelea kumuombea na kumuunga mkono sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri kwa kutuwasilishia hotuba nzuri leo asubuhi. Hotuba ambayo imetuonesha dhamira ya dhati ya ofisi hii katika kuwaletea maendeleo wananchi. TAMISEMI ndiko ambapo wananchi walipo wengi. TAMISEMI ndiyo inatoa huduma nyingi kule vijijini. Ukiongelea Halmashauri au Mamlaka za Serikali za Mitaa unaongelea wananchi wa kwenye vitongoji. Maana yake ni kwamba kule tuliko sisi wananchi. Kwa hiyo, leo tumeona dhamira ya Serikali kupitia Wizara hii na kwa hakika nimpongeze sana kaka yangu Mheshimiwa Innocent Bashungwa kwa namna ambavyo amekuwa akitupa ushirikiano kwa muda wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kila mara tumekuwa tukimpa ushirikiano na kero ambazo zipo kwenye maeneo yetu amekuwa akizitatua kwa wakati, kwa hakika tunasema wewe ni hazina ya Taifa na tunaendelea kukuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo hivyo kwa wenzetu Naibu Mawaziri wake Davis Silinde ndugu yangu pamoja na Ndugu Dkt. Ndugange mnafanya kazi nzuri sana. Kipekee kabisa Profesa Shemdoe pamoja na wenzake wote katika Wizara watendaji mnafanya kazi nzuri ya vijijini na niendelee kukumbusha tu kwamba kule Kipompo ambapo Profesa Shemdoe uliahidi shule ya msingi itapauliwa wananchi washajenga madarasa manne pamoja na nyumba ya mwalimu, tunasubiri mkapaue ili shule ile iweze kusaidia wananchi ambao watoto wanatembea kilometa tisa kutoka pale wanakoishi kitongoji cha Kipompo katika Kata ile ya Mang’onyi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwa maana ya mwaka mmoja huu ambao tunauona, Halmashauri ya Ikungi tumepokea zaidi ya shilingi bilioni saba ambazo kwa hakika ni fedha nyingi sana za maendeleo ambazo leo tunaona ziko kwenye maeneo mbalimbali ya vijiji vyetu na zaidi tumeona jambo kubwa lililofanyika la kujenga madarasa 67. Tulipata jumla ya shilingi bilioni 2.6; ni fedha nyingi kwa wakati mmoja. Sisi tunashukuru sana na tunaipongeza Serikali kwa hatua kubwa ya mapinduzi makubwa ya kielimu katika Halmashauri yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikisema hayo pia tumepata eneo la vituo vya afya. Lakini nishukuru sana tumepata Hospitali yetu ya Wilaya imepata shilingi milioni 800 inakwenda kukamilika sasa ambayo tulikuwa hatuna huko nyuma. Lakini kwenye eneo hili niseme tu kwamba katika Kata zangu 13 za Jimbo la Singida Mashariki, Mheshimiwa Waziri mimi nilipata kituo kimoja tu. Kata 13 za Jimbo la Singida Mashariki tumepata Kituo cha Ntuntu. Nashukuru kwamba tumepata shilingi milioni 500 na tunaenda kumaliza kabisa tatizo la afya katika eneo lile la Kata ya Ntuntu ambayo iko mbali na Wilaya. Lakini kwa maana ya Kata 12 zilizobaki, niombe sana kwenye bajeti hii angalau tukipata vituo vingine vitatu tutakuwa tumegusa maisha ya wananchi. Tukiweza kupata Misuwakha, tukiweza kupata katika Kata ile ya Mang’onyi, tukapata na Kata ya Isuna, tutakuwa tumesambaza vizuri huduma na tutawasaidia wananchi wetu kutembea kwenda kupata huduma mbali. Nikisema hivyo, kwa sababu naenda sambamba pamoja na watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi katika Halmashauri yetu ya Ikungi tuna upungufu wa walimu wengi sana. Walimu ukiangalia hesabu yetu tunahitaji walimu 2,685 lakini tunao walimu 1,305 tu maana yake tuna upungufu wa walimu 1,380. Walimu hawa ni wengi sana katika kuhakikisha kwamba tunaboresha elimu yetu. Leo tunataka ufaulu upande, lakini hatuwezi kupandisha ufaulu bila kuwa na walimu wa kutosha, hatuwezi kusema leo tunaenda kuongeza uwezo wa kufundisha watoto wetu kwenye shule za msingi, unakuta walimu wako watano kwenye shule ya msingi yenye watoto zaidi ya 700 usitegemee mapinduzi ya elimu katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunashukuru sana tumeweza kupata fedha katika shule shikizi, shule za Simbikwa, shule za kule Talu Mlimani, shule ya kule Mau, shule ya Mboghantigha tumepata kule ambapo sasa tumepata madarasa na shule zile zinakwenda kusajiliwa. Lakini leo hii tumepanga tusajili zile shule zianze, lakini ina mwalimu mmoja, wawili katika shule, usitegemee mabadiliko makubwa ya kitaaluma katika eneo lile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana tuisaidie Idara ya Elimu ipate walimu wa kutosha ili hata Afisa Elimu anaposimamia awe na uwezo mzuri wa kuelekeza namna ambavyo Serikali inataka kuboresha elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiongelea eneo hilo nikikazia zaidi kwenye eneo la afya pia tunao upungufu mkubwa sana. Kuna zanahati unakuta ina mganga au nurse mmoja ni kilometa zaidi ya 60 kutoka Makao Makuu ya Wilaya na kila mwezi anatakiwa apeleke report. Siku anapeleka report au anakwenda benki kutafuta mshahara, ile zahanati inafungwa, huduma haitolewi, ugonjwa hauna taarifa, hauwezi kujua leo umepeleka report. Kwa hiyo, wananchi hawawezi kupata huduma kwa sababu hatuna waganga au wahudumu wa afya wa kutosha. Niombe sana Serikali mnapokuja mje mtuambie mkakati ambao mmeupanga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo hili la elimu, lakini pia na kuwasaidia vijana wetu ajira. Mimi niseme tu kwamba naishukuru Serikali tulipata fedha au tulitengewa shilingi bilioni mbili kujenga Chuo cha VETA pale Ikungi. Leo tunavyoongea mimi na wewe kile chuo sasa hivi kimesimama ujenzi. Watu wa VETA walipewa kandarasi ya kujenga kile chuo, namshukuru sana Naibu Waziri Mheshimiwa Kipanga ulikuja, ulivyokuja ukasema sasa tutabadilisha iende Halmashauri. Hivi ninavyongea wamerudisha tena imekwenda VETA, hivi ninavyoongea sasa hivi wale wakandarasi hawajalipwa, mradi umesimama, vifaa hakuna, zaidi ya mifuko ya cement 1,800 ilikuwa inaletwa Ikungi imepotea njiani. haijafika. Leo hii imesimama ujenzi, hakuna kinachoendelea na kuna watu wanadai. Usitegemee hawa vijana ambao tunategemea wakasaidiwe elimu pale hawana mahali pa kufundishiwa. Kwa hiyo, usitegemee kwamba tutapata mabadiliko ya kielimu au kusababisha ajira za wananchi wetu. Kwa hiyo, nilitaka nilieleze hili eneo katika kuhakikisha kwamba tunaboresha elimu katika eneo letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie na suala la barabara; barabara kweli tumepata fedha shilingi bilioni 1.5 kwenye maeneo yetu imeleta mabadiliko makubwa tunaipongeza Serikali. Lakini kwa barabara za vijijini ambazo tunahitaji vivuko na madaraja, fedha ambazo tunasubiri hizi za pamoja na bajeti hatutengi tutakuwa tunategemea kitu ambacho hatujakipanga.

Kwa hiyo nimeona hapa kuna fedha mmeongeza kweli lakini fedha zile hazitoshi, mngekuwa kwenye fedha za maendeleo zinatoka moja kwa moja TARURA tunatenga kwa ajili ya vivuko na madaraja ili Mameneja wa Wilaya wabaki kwenye eneo la kutengeneza barabara tu na matuta. Lakini ukisema leo wafanye kazi ile ile shilingi milioni 800 haifiki hata shilingi bilioni moja kwa mwaka usitegemee mabadiliko ya barabara katika Halmashauri zetu. (Makofi)

Kwa hiyo niombe sana tuwe na mpango maalum wa fedha maalum ambazo zinakwenda kwa ajili ya kujenga madaraja na vivuko ili isaidie barabara zetu za vijijini. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE: MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo maneno naomba nirudie tena kushukuru, lakini naomba niseme naunga mkono hoja, kuna mambo ya kimkakati ambayo nitamuandikia Mheshimiwa Waziri kwa ajili ya maboresho. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ambayo iko Mezani kwa ajili ya Bajeti ya mwaka wa fedha 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa taarifa aliyotusomea hapa Bungeni, taarifa ambayo imesheheni mipango mizuri ya Serikali kwa mwaka wa fedha unaokuja. Ninaamini kabisa mipango hii ambayo imeelezwa hapa ikitekelezwa vizuri tutakwenda kubadilisha kabisa maisha ya Watanzania na kuweza kusogeza mbele gurudumu la maendeleo, ikiwemo utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ambayo tuliahidi tutakwenda kuleta maendeleo kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla sijakwenda kuchangia hoja ambayo iko Mezani, nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoifanya kwa ajili ya Watanzania. Kazi kubwa anayoifanya katika muda wa mwaka wa fedha huu tunaomaliza sisi watu wa Singida Mashariki kwa maana ya Wilaya ya Ikungi, tumeona fedha nyingi zimeshuka katika halmashauri yetu. Na hii haijawaki kutokea, tumeweza kupata fedha nje ya bajeti iliyopangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi tulipokea zaidi ya bilioni 12 katika muda wa mwaka huu wa fedha. Imetekeleza miradi mingi sana. Miradi ambayo hatutaisahau ni miradi ya barabara. Barabara zetu ndiyo uhai wa wananchi wetu katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, barabara zaidi ya kilometa 157 ambazo zilikuwa hazipitiki kabisa zimetengenezwa na kuimarishwa ikiwemo kuwekwa madaraja. Kwetu sisi tuliona tusiposema haya tutakuwa hatumtendei haki na tutakuwa hatuitendei haki Serikali yetu. Tunashukuru sana kwa namna ambavyo Rais ametuletea fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la barabara kwa mara ya kwanza tunakwenda kupata barabara za lami katika Mji wetu wa Ikungi. Tumepata kilometa mbili ambazo zinaendelea kujengwa na wakandarasi na kuna mpango wa kuweka taa za barabarani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaamini kabisa Mji wa Ikungi sasa utakwenda kuwa na mwanga katika saa za usiku na itasaidia hata wafanyabiashara wadogowadogo kufanya shughuli zao hata kipindi cha usiku kuweza kuhudumia watu wanaopita katika eneo hili. Kwenye hili tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais na tunaendelea kumuombea kila la heri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kama haitoshi, kwenye eneo la elimu tumeeleza sana, lakini tumepata zaidi ya madarasa 109 ambayo yameweza kutumika, na ni zaidi ya bilioni nne na milioni 900 imetumika. Kwetu sisi ni mabadiliko makubwa sana ya kimaendeleo na tunaamini kwamba tutakwenda kuboresha elimu ya watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutaeleza mengi, lakini tutaeleza upande wa REA; REA imeendelea kusambaza umeme katika maeneo yetu. Tarafa ya Mungaa ambayo nilikuwa nailalamikia leo kila kijiji kimepelekewa nguzo. Tunategemea ndani ya muda mfupi vijiji vyote vitakuwa vimepata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye hili niendelee kuomba, kama ambavyo tumeambiwa REA hii Awamu ya Tatu itakwenda kupeleka kwenye vitongoji, basi kuna vitongoji ambavyo havijapata umeme. Tuweze kuangalia katika bajeti hii inayokuja. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa maeneo yote hayo, sina haja ya kurudia yote, lakini tunasema tunashukuru, na waungwana wanasema kushukuru ni kuomba tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo nianze sasa kuchangia bajeti ambayo iko mbele yetu ya Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, na ameeleza zaidi katika eneo la barabara kuu ambazo zinaunganisha mikoa yetu.

Mheshimiwa Spika, sisi watu wa Singida bado tuna changamoto ya kuunganisha barabara katika mkoa. Tunayo changamoto ya kutoka Tanga kuja Singida, lakini bado tuna changamoto ya kutoka pale Mkiwa (Itigi) mpaka kwenda kule Mbeya. Tunayo maeneo hayo mawili bado hatujaunganishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tunayo furaha kwamba tuliwekwa kwenye bajeti inayoisha mwaka huu tuliambiwa tutajengewa kilometa 2,100. Barabara zilizotajwa ni pamoja na Mkiwa – Itigi – Makongorosi – Mbeya. Barabara hii bado hatujapata mkandarasi. Lakini bado kuna barabara ya Singida – Kwamtoro kwenda mpaka kule Kibrashi, Tanga, bado hatujaanza ujenzi wa barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, barabara hizi zitakapokamilika zitakwenda kuongeza uchumi wa wananchi wetu, zitakwenda kuongeza thamani ya miradi ambayo tunaitengeneza. Mfano barabara hii ya Tanga kutoka Handeni kuja mpaka Singida itakwenda kuihuisha Bandari ya Tanga ambayo tumewekeza fedha nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaomba sana tuhakikishe kwamba barabara hii mkandarasi anaingia. Tuliambiwa tutatumia mfumo wa EPC+F, mpaka leo tunavyoongea wako kwenye negotiation, hawajamaliza hatua za manunuzi. Wamalize mchakato wananchi wanasubiri barabara hizi kwa hamu kwa sababu Serikali ilishawaahidi katika mwaka wa fedha tunaokwenda kuumaliza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye eneo hili la watumishi, na nieleze la watumishi kwa maana nilikuwa nalenga kwenye fedha zinazoletwa. Tunaomba sana wananchi kwa maana ya wale waliopata nafasi ya kuwa watumishi wa Umma waitendee haki nchi. Fedha zinaletwa nyingi katika maeneo yetu; wawe wazalendo ili fedha hizi ziwe na thamani. Kwa sababu kabla hujaamua kufanya ufisadi kwenye miradi hakikisha wewe kijiji unachotoka kimemaliza matatizo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tungekuwa tunaangalia umaskini uliopo kwenye vijiji vyetu tunapotoka ninaamini hakuna mtumishi wa Umma ambaye angefuja fedha za Serikali. Niwaombe sana tuwe wazalendo, tuitendee haki nchi yetu kuhakikisha kwamba tunakwenda vizuri katika kujenga Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la ajira pamoja na wastaafu; naishukuru sana Serikali, tumefanya kazi nzuri ya kuendelea kuajiri, na tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. Na juzi hapa tumetangaziwa tena ajira nyingine 21,000. Ni jambo zuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo hili ninataka niombe; tumekuwa na wahitimu wa mwaka 2015, 2016 mpaka 2020, tumekuwa tukitangaza nafasi hawapati. Watu hawa wameshakaa mtaani vya kutosha. Zimetangazwa hizi ajira za sasa hivi, tunaomba sana wapewe kipaumbele, waweze kuajiriwa ili wasiondoke kwenye muda ule wa utumishi.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu wakicheleweshwa leo katika miaka mitano ijayo watakuwa hawaajiriki na itakuwa haina sababu ya kuwasomesha kwa fedha nyingi. Na wengine wamekopa kwenye mfuko wa elimu ya juu, maana yake watashindwa kulipa fedha hizi. Eneo hili tukifanya vizuri tutakuwa tumewatendea haki vijana wetu ambao wanatafuta ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hili la wastaafu ninataka niunganishe; tumekuwa na malalamiko ya baadhi ya wastaafu. Wanalalamika wanapomaliza utumishi wao wamefanya kazi nzuri lakini wengine wamekuwa wakilalamika hawalipwi fedha zao kwa wakati. Hili eneo limekuwa likilalamikiwa na sisi Wabunge tumekuwa tukipata malalamiko hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mzee wangu mmoja ambaye barua yake ninayo hapa, ameniletea kama Mbunge wake. Anaitwa Simon Alberto Makia, ni mzee wangu kutoka pale Siuyu, Singida. Niombe sana nitaikabidhi hii barua yake, amekuwa akilalamika anasubiri kupewa fedha zake ambazo amestaafu.

Mheshimiwa Spika, leo hii tunavyoongea amekuwa akija mpaka Bungeni hapa nje akifanya juhudi za kumuona Mheshimiwa Waziri aweze kumwambia kilio chake. Nitaomba sana kama Mbunge wake nikabidhi na ninaomba sana wa aina hii waweze kutendewa haki kwani wamefanya kazi nzuri katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nimalizie kwenye eneo la utawala, lakini kabla ya eneo hilo, niishukuru sana Serikali kwa kutupatia chakula cha kupunguza makali cha bei nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, chakula mwaka huu kimetusaidia sana watu wa Ikungi, tumeweza kupunguziwa makali ya njaa ambayo ilikuwepo. Hatukuvuna vizuri msimu uliopita lakini toka mwezi Novemba tumekuwa tukiletewa chakula cha bei nafuu. Wananchi wetu wamefarijika, wanaishukuru Serikali na wanamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa upendo wake na huruma yake. Ninaamini kabisa mwaka huu hali ni nzuri, tumeona mazao na huenda Mungu akajalia tukavuna vizuri. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais pamoja na Serikali.

Mheshimiwa Spika, nimalizie eneo la utawala; sisi Wilaya ya Ikungi tunayo majimbo mawili ya kiutawala lakini majimbo haya yamepewa majina ambayo ukiangalia haraka haraka ukimtajia mtu hajui kwanza jimbo liko wapi. Ninaamini kabisa sisi hatuombi eneo jipya tunachoomba ni jina tu libadilike. Tunayo Singida Mashariki na Singida Magharibi; ombi letu, na kwenye RCC tulishaleta, tunaomba tupate majina halisi ya maeneo husika. Kwa mfano tukipewa jina laJimbo la Ikungi angalau linaweza kuleta maana nzuri.

Mheshimiwa Spika, lakini ukiletewa Jimbo la Puma au Jimbo la Sepuka maana yake unakuwa umeshaweka identity ya eneo husika. Ninaamini kabisa hili jambo si kubwa, na pacha wangu ananipigia makofi maana yake anakubaliana, ili tuhakikishe kwamba tunapata identity halisi ya majimbo haya na wananchi wajue Wabunge wao tunapotaja Jimbo la Ikungi, Jimbo la Sepuka maana yake ni Wabunge wanaotokana na Wilaya ya Ikungi.

Mheshimiwa Spika,baada ya maneno hayo kwa heshima kabisa ninaomba kuunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri Mkuu lakini naomba tupitishe bajeti hii ili Waziri Mkuu afanye kazi nzuri anayoendelea nayo. Naunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja Iambayo iko mezani. Kwanza nianze kwa kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayofanya ya kuwaongoza Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, kaka yangu na swahiba wangu Abdallah Bin Ulega pamoja na Naibu wake ndugu yangu David Silinde pamoja na Wizara nzima kwa ujumla kwa hotuba nzuri yenye maono, yenye uelekeo mzuri ambayo inaonekana wazi kwamba tunapata mapinduzi makubwa kwenye Sekta ya Uvuvi pamoja na Mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu nimeipitia hii hotuba na nimemsikiliza Mheshimiwa Waziri, nimesikiliza pia maoni ya Kamati ambayo mengi yameipongeza Wizara. Nasema kama haya waliyoyaandika ndani ya hii hotuba wataenda kuyatengenezea mpango kazi, Mheshimiwa Waziri tutatoka kidedea na tutaona namna ambavyo sekta hii itafanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Waziri kama ambavyo wamepongeza wengine kwa uteuzi alioupata pamoja na wenzake lakini niamini kwamba kwa nguvu aliyonayo, maono aliyonayo, hamu aliyonayo, Wizara hii itaenda kubadilika na italeta matokeo chanya yaliyotarajiwa na Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimejaribu kupitia taarifa ya Mheshimiwa Waziri na bahati nzuri sana imejieleza kwenye Kamati, kuna malengo waliyojipangia hawakuzidi asilimia 40, kwa maana kwenye mapato, kwenye maduhuli ambayo walitegemea. Pia kuna mipango mingi ilikwama katika mwaka wa fedha uliopita. Hiyo ni kwa sababu ya rasilimali fedha, lakini mipango yao inawezekana haikufika vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini mwaka huu wamejifunza na wamefanya tathmini, tunaamini mwaka mmoja ujao tutakuwa na mabadiliko mengine ambayo tumeeleza. Hata hivyo, nikiangalia katika hili tunayo mifugo mingi sana, tunao ng’ombe milioni 36 kwa mujibu wa taarifa ambayo tumeiona hapa. Tunaona tuna mbuzi wa kutosha, tuna kondoo wa kutosha, lakini kama haitoshi tuna rasilimali kwenye Bahari pamoja na Maziwa yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini tukitumia vizuri hii mipango tuliyoipanga, tutakuwa na matokeo makubwa na Wizara hii itachangia fedha nyingi kwenye pato la taifa. Tumeona wamesema ni asilimia saba tu inachangia kwenye pato la Taifa, bado ni ndogo. Kama walivyosema wengine ni kwamba mifugo tuliyonayo inawezekana kuna changamoto ambayo tunapaswa twende nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ambalo nimeliangalia kidogo, ni upande wa ukusanyaji maziwa. Ukiangalia Nchi za Afrika Mashariki wenzetu wa Kenya wameweza kukusanya lita 1,241,000, watu wa Uganda wamekusanya maziwa Lita 707,560, lakini sisi Tanzania tumekusanya lita 64,837. Sisi tunasema tuna ng’ombe wengi, tunasema tunayo rasilimali nyingi, tuna eneo kubwa la kufugia, lakini bado tunaweza kukusanya maziwa kiasi hiki kidogo, maana yake bado kuna kazi hatujafanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu gani? Sisi tunafanya ufugaji wa kienyeji. Ng’ombe wetu si kwamba tunawaona kwa mazingira, ng’ombe wetu ni wadogo, hawana kilo nyingi, nyama zao hazivutii kuliwa. Tukienda kuchoma mnadani tukala tunaamini nyama nzuri, lakini ikienda kwenye vipimo na vipimo vinavyotakiwa nyama ile ni kama haitakiwi. Nini tunatakiwa tufanye? Lazima tupige hatua moja mbele na ndio maana nakuja na ushauri. Mheshimiwa Waziri, amefanya kazi nzuri, mipango ni mizuri, lakini nimeona nami niweke mchango wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni eneo la Ranch za Taifa. Mheshimiwa Waziri Ranch zetu hazifanyi kazi, ni kama hazipo, yamebaki kuwa mapori tu. Ranch hizi ziliwekwa makusudi ili zisaidie mapinduzi ya ufugaji nchini. Kulikuwa na uwezo wa wafugaji wetu kwenda kujifunza, maeneo mengi leo Ranch zimebaki kuwa na walinzi tu. Mameneja wale wapo tu wanaangalia kulinda angalau wasije wakaibiwa majengo yale ambayo yako pale. Hii sio sawa. Hata ukiangalia leo Waziri ametuambia hapa Ranch ya NARCO amenunua vitu lakini vitu venyewe vilivyonunuliwa ni vichache, yaani bado hawezi kujivunia kwamba kuna hatua watapiga. Kwa hiyo, naamini kabisa kwamba Ranch zetu zingine ziko grounded kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ninayotaka kusema ni hii, huu mpango mnaokuja nao wa kuwasogeza wawekezaji ambao watakuja kufanya na sisi ili waweze kutumia miundombinu tuliyoiweka kama Serikali kuweza kunenepesha ng’ombe, kuweza kuongeza utaalam, uhamilishaji na vile vituo kwa sababu viko karibu na wananchi, wananchi waje wajifunze pale. Mheshimiwa Waziri hapo ndiyo atakuja kuleta mapinduzi makubwa ya ufugaji hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri hili walilokuwa wanataka kulianza la kuhakikisha kwamba wanakwenda kuwakaribisha wawekezaji ambao watakwenda kusimamiwa na wataalam wetu wengi ambao wako Wizara ya Mifugo, Wizara ya Mifugo ni kama Wizara ya Kilimo ina wataalam wengi sana. Mheshimiwa Waziri awatumie hawa waweze kuleta mapinduzi ya ufugaji katika nchi yetu. Nilitaka nieleze hilo kwa upande huu wa Ranch zetu, najua mipango wameshai-set, lakini naongezea eneo hilo. Wafanye vizuri, wakaribishe wawekezaji, wawasimamie, naamini tutapata matokeo ambayo tunayatarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni miundombinu. Tumekuwa tukijenga majosho, tumekuwa tukijenga mabwawa, tumekuwa tukijenga miundombinu mbalimbali inayosaidia ufugaji wetu. Hata hivyo, hizi fedha tumekuwa tukizitupa kwenye halmashauri, kule hakuna mechanism ya kuzisimamia, leo majosho mengi yamekufa, mabwawa mengi yamekufa hatuna uwezo hata wa kuyakarabati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumshauri Mheshimiwa Waziri kwamba tuunde kama ikiwezekana Tume maalum kama ilivyokuwa Tume ya Umwagiliaji, tuwe na Tume ambayo itaenda kuratibu rasilimali ya mifugo kule kwenye Halmashauri zetu. Kule kwenye Halmashauri unakuta Afisa Mifugo yupo mmoja tu wakiingia pale Mkurugenzi vipaumbele vinakuwa ni sekta nyingine lakini sekta ya mifugo haiangaliwi ambayo ndiyo inabeba watu wengi kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana Mheshimiwa Waziri eneo hili muone namna ambavyo mtaweza kufanya, kuundwe Tume fulani mfano kwenye maji tuliona tatizo tukaunda RUWASA tuliona kuna matatizo tukaunda TANROADS leo hii kuna barabara zinajengwa, leo hii unaona kuna ufuatiliaji na mambo kama hayo, kwa nini tusifanye kwenye mifugo inawezekana tukiamua ili fedha nyingi zinazoenda kule zikasimamiwe na tume maalumu ambayo italeta matokeo ambayo tunayatarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili pia nina maombi yangu katika Wilaya yangu ya Ikungi, eneo hili kama wafugaji tunao tunahitaji majosho, tunahitaji mabwawa lakini tuna maeneo ya Kata za kimkakati ambazo tukiwekewa majosho haya yatasaidia kuleta mapinduzi. Mojawapo ni Kata ya Siuyu, Kata ya Mang’onyi, Kata ya Isuna, Kata ya Mkiwa na Kata ya Misughaa maeneo haya Mheshimiwa Waziri yanao wafugaji wengi wakiwekewa miundombinu ya mabwawa, wakiwekewa majosho utaona mabadiliko ya ng’ombe wetu na utaalam ambao unataka kutuletea wa yale madume ya mbegu ambayo yataenda kubadilisha kizazi cha mifugo ninaamini kabisa tutabadilidha ufugaji wa watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho nimalizie kuhusu uvuvi pamoja na kuwa sisi hatuko Pwani, pamoja na sisi tuko Kati huku Mheshimiwa Waziri lakini na sisi tuna mabwawa na tuna maziwa, ninaomba sana Mheshimiwa Waziri ninalo bwawa langu linaitwa Muyanji liko pale Singida, bwawa hili limejengwa toka enzi za ukoloni, bwawa hili tumekuwa tukipata kitoweo cha samaki lakini hapa katikati tumekuwa tukipata ups and downs kwa sababu hatupati samaki wazuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2018 tulipeleka vifaranga 3,500 kupitia Halmashauri yetu tukapandikiza mle ndani, wananchi wameendelea kupata kitoweo pale, vijana wetu wanapata shughuli za uvuvi pale, ninakuomba sana ikikupendeza bwawa lile limepungua kina nikuombe sana tupate fedha tukatoe zile tope zilizoingia mle ndani, tuliboreshe vizuri kwa kujenga miundombinu sehemu ya kunyweshea mifugo iwekwe ili isiendelee kutifuatifua udongo utakaoingia ndani ya bwawa lile, ili bwawa lile la Muyanji liendelee kutoa Samaki, kwa sababu Wizara yako inatusaidia kwenye protini na samaki kule pia tuwapate kwenye Wilaya yetu ya Ikungi na hasa kwenye eneo langu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kwenye eneo hili ukilifanyia kazi utakuwa umetufanyia vizuri, baada ya maeneo haya nakushukuru, naunga mkono hoja, nakushukuru nakutakia kila la kheri. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja ya bajeti ya mwaka 2022/2023 Wizara yetu ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa dhamira yake ya kukibadilisha Kilimo cha Tanzania akiamini kabisa kwamba tukiboresha kilimo cha Watanzania maana yake ndiyo unaboresha uchumi wao na ni majority ya Watanzania ambao wanafanya kazi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili nichukue nafasi hii kumshukuru tena Mheshimiwa Rais, nimshukuru zaidi Mheshimiwa Waziri Bashe kwa namna ambavyo watu wa Ikungi tulipokuwa tuna changamoto ya njaa ya upungufu wa chakula wakatuletea chakula cha bei nafuu. Tulipata chakula kile kilitusaidia sana na kwa hakika leo tunaenda kufanya mavuno chakula kile kimetusaidia tunashukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa kutupa kibali kupata NFRA wasogeze chakula pale kwenye Wilaya yetu na wananchi wale nilikuwa kwenye ziara siku mbili hizi wanatoa shukrani nyingi na wanamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizo nichukue nafasi hii kushukuru kwa bajeti, kwa maana ya wasilisho la Mheshimiwa Waziri ambalo aliwasilisha pale jana, ni bajeti nzuri imeonekana kila mwaka inapanda, maana yake ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba kilimo kinakua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaenda mbali ninahitaji nionyeshe tu kwamba kuna document kubwa yenye heshima ambayo nchi hii tumeipitisha, Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020/2025 inaeleza wazi na inakazia sana suala la kilimo. Ukienda kwenye ile Ibara ya 35 inaeleza wazi kuhusiana na kilimo, imeweka tamko. Imeweka tamko kwamba kilimo cha kisasa ndiyo msingi katika kujenga uchumi na kina nafasi ya kimkakati katika kukuza ustawi wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haitoshi kwenye ilani imeeleza wazi kwamba makadirio mpaka 2025 tunapaswa tufikie Pato la Taifa tufikie asilimia 28 ya Pato la Taifa. Ukiangalia katika wasilisho la Mheshimiwa Waziri tumewasilisha vizuri kwamba sasa tumefikia asilimia 26.1 maana yake tunaenda vizuri miaka miwili na nusu ijayo huenda tukafikia asilimia 28 ambayo iko kwenye lengo la Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri mnaenda vizuri niwapongeze sana wewe na wataalam kwa kazi nzuri ambayo mnaifanya kwa sababu ni jambo ambalo litaenda kufanya vizuri, wananchi wengi zaidi ya asilimia 65 wanafanya kilimo. Maana yake ukiwagusa asilimia 65 ni kama watu milioni 40 wanafanya kazi ya kilimo katika nchi yetu. Kwa hiyo, nilitaka nianze na hilo ili kwanza kuonesha kwamba tunaona matokeo ya kweli yanaenda vizuri na ambayo kwa kweli tukiyasimamia vizuri na ushauri ambao tunatoa Wabunge huenda tukabadilisha kilimo chetu na kikawa kilimo chenye tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye eneo ambalo ni mkazo uliowekwa kwenye Ilani ya Uchaguzi. Ilani ya Uchaguzi imesema ni kusimamia kikamilifu hifadhi ya matumizi endelevu ya maji, ardhi ya kilimo na kuongeza miundombinu ya umwagiliaji. Nataka nianze kwenye eneo la umwagiliaji. Ninaamini kabisa tabianchi imeathiri sana kilimo cha Tanzania, siyo kilimo cha Tanzania, cha maeneo mengi Afrika, kama tutaendelea na hali ya kusubiria huruma ya Mungu kuleta mvua peke yake hatutakisogeza kilimo hiki. Kila mwaka tutakuja na sababu kwamba mwaka jana hatukufikia lengo kwa sababu mvua hazikunyesha za kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu, ninaona kwamba kuna package nzuri kwenye eneo la skimu za umwagiliaji. Niombe huenda tunaweza kuweka fedha nyingi, kwanza tunaiona dhamira ya Wizara tunaiona dhamira ya Waziri, tunaiona dhamira ya watendaji lakini tunapelea kwamba fedha hata Wabunge wote wanaomba hapa skimu za umwagiliaji, lakini nani anaenda kuzitunza zile skimu kule chini? Skimu nyingi zimekufa, skimu nyingi hazisimamiwi vizuri. Skimu nyingi hazitoi matokeo lakini kama haitoshi kuna baadhi ya maeneo hata hawajui maana ya skimu zenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo maana yake tunaenda ku-dump fedha, tunaziacha pale, hakuna usimamizi. Nikuombe Mheshimiwa Waziri tutafute mechanism nzuri ya kusimamia skimu ya fedha nyingi tunazopeleka kwa wananchi kule chini. Ninaamini tukifanya hivyo tutaleta matokeo tunayoyatarajia kwa sababu tusipofanya hivyo tutakuwa hatuna maana yoyote, tunawekeza fedha hakuna uendelevu wowote, maana yake hatuna matokeo ambayo tunayalenga. Tuna maeneo ya mito mingi, tuna maji yanapita kila mahali lakini tusipoyazuia maji na kuyatumia vizuri maana yake kilimo chetu hakiwezi kubadilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili Mheshimiwa Waziri nikuombe sana tunajua kwenye Wizara yako umeniangalia katika skimu ya Mang’onyi pale, lakini Mheshimiwa Naibu Waziri mliniambia kwamba mtafanya. Niombe wakati wa ku-wind up nataka kusikia watu wa pale Mang’onyi wanataka kusikia Wizara inasemaje. Mwaka huu wa Fedha tujengewe ile skimu tuboreshe kwa sababu sasa hivi tuna soko la mboga mboga katika Mgodi mkubwa wa Shanta ambao uko pale Mang’onyi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri baada ya kuwa nimeeleza eneo la skimu ambalo litaleta matokeo nieleze kidogo kwenye eneo la transformation ya kilimo katika nchi yetu. Tukitaka ku-transform kilimo cha nchi yetu tunahitaji mambo matatu. Tunahitaji utaalamu kwa maana ya technology au elimu, tunahitaji uwekezaji au fedha lakini tunahitaji pembejeo ambazo zinafaa katika maeneo yetu. Mambo haya matatu tukifanya vizuri tutakibadilisha kilimo chetu. Leo ukienda kwenye utaalam ni Maafisa Ugani wangapi ambao wana uwezo wa kumsaidia mkulima pale kijijini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Maafisa Ugani wengi Mheshimiwa Waziri, wakulima wana uwezo mkubwa kuliko Maafisa Ugani uliowapeleka kule vijijini. Maafisa Ugani
wamefanana na wananchi lakini wengine wamezidiwa uwezo na wananchi, kuna haja ya kuwasaidia, kuwabadilisha mtazamo wa kazi wanazozifanya. Uwekezaji kama nilivyosema tunaiomba Serikali iongeze fedha za kutosha kwenye sekta ya kilimo ambayo watu milioni 40 wanafanya kazi hii, tukifanya vizuri eneo hili tutaweza kubadilisha kabisa kilimo na uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu ni eneo la mbolea, viuatilifu, na mbegu. Eneo hili tukiongeza utafiti, tukaongeza mbegu za kutosha zinazofaa, zitamfanya mkulima awe na matokeo makubwa kwenye eneo lake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, nchi hii imekuwa sasa, kutoka Mtwara mpaka Kigoma watu wanataka wote walime zao moja linaitwa korosho, haiwezekani. Hatuwezi kuwa na kilimo cha korosho nchi nzima. Hata mazingira au hali ya hewa hairuhusu. Maana yake hata concentration ya namna ya kusaidia kilimo haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani leo kila mtu anataka kulima alizeti nchi nzima. Haiwezekani mtu atoke kule Tandaimba, anataka kwenda mpaka kule Mwanza alime alizeti, haiwezekani Mheshimiwa Waziri! Tufike mahali tuwe na kanda maalum kwamba hii kanda ni ya alizeti. Kama ni Singida, tu-concentrate pale Singida na mikoa ambayo inaweza kutoa alizeti. Leo hii mahindi hayawezi kulimwa nchi nzima. Mfano, kama Singida leo, hatuwezi wote kulima mahindi. Tutalima mtama, tutalima uwele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Parseko Kone, aliwahi kuwa Mkuu wa Mkoa wa Singida, alizuia kabisa kilimo cha mahindi kwenye maeneo ambayo hatuwezi kulima mahindi, akasema lazima watu walime mtama. Mtama ukizalishwa kwa wingi, nao ni nafaka, itauzwa, tutanunua chakula kingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuwe wakali, tuwasimamie wananchi, tuwasaidie ili Ilani ya CCM iweze kutekelezwa vizuri, tuwe na usalama wa chakula na mwisho wa siku pato la Taifa liongezeke kupitia sekta hii ya kilimo. Tusipofanya hivyo Mheshimiwa Waziri, tutakuwa tunayumba kila siku, kila mmoja anakuja na proposal yake. Lazima sisi kama nchi, tukubaliane kwamba kanda hii ni chakula hiki, kanda hii ni zao hili, mwisho wa siku nchi ikikusanya, tutasonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo ndio nilitaka niyaseme…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie nafasi hii kuunga mkono hoja, nawatakia kila la heri.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja iliyoko mbele yetu ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kutujalia uzima na kuweza kukutana asubuhi ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nichukue nafasi hii kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya ikiwemo kuridhia fedha nyingi ambazo zinakuja kwenye Wizara hii ambayo ni Wizara inayoendesha na kusukuma uchumi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yetu ya Ujenzi na Uchukuzi ndiyo imebeba daraja la uchumi wa nchi yetu. Kwa hiyo, Wizara hii ndiyo imebeba mabadiliko ya uchumi ambao tunautarajia. Nachukua nafasi hii kwa kweli kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya katika kujenga barabara, kujenga miundombinu, tunajenga reli, tunanunua meli, tunanunua ndege na kadhalika. Kazi hii inafanyika vizuri na kwa hakika ataendelea kuandikwa kwenye kitabu cha dhahabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nachukua nafasi hii kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Profesa Makame Mnyaa Mbarawa pamoja na wasaidizi wake, Manaibu Waziri, ndugu yangu Kasekenya pamoja na Atupele ambao wanafanya kazi nzuri sana ya kumsaidia Mheshimiwa Waziri; Katibu Mkuu pamoja na Manaibu Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi kubwa; na bahati sisi wengine ni Wajumbe wa Kamati ya Miundombuni, tunaona kazi nzuri inayofanyika katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi na shukurani hizo, nichukue nafasi hii kwa hakika nianze kuchangia maeneo kama matatu kama nitapata muda. Nianze na kuchangia upande wa TANROADS ambayo ndiyo imepewa dhamana ya kusimamia ujengaji wa barabara kuu na barabara zinazounganisha wilaya na wilaya katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, TANROADS wanafanya kazi nzuri sana Wizara hii chini ya Eng. Mativila na wenzake wote. Wanawasimamia wakandarasi katika maeneo mbalimbali kujenga barabara, kujenga madaraja makubwa na madogo na kusimamia miundombinu mbalimbali katika eneo letu. Kazi hii ni nzuri na tumesikia kwenye taarifa yetu ya Kamati pamoja na Waziri mwenyewe ameeleza vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili nipongeze, kwa mujibu wa utaratibu wao tuliojiwekea ni kuhakikisha kwamba tunaunganisha barabara za mikoa na mikoa. Hii ni pamoja na kazi kubwa ambayo imefanyika na imeelezwa. Napongeza sana utaratibu mpya ambao umeanzishwa wa kujenga barabara kwa mfumo mpya wa EPC + F. Mfumo huu utaenda kuwa ni jibu ya barabara ambazo zilikuwa hazijakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Waziri ametueleza hapa, tunaenda kusaini barabara zenye urefu wa kilomita 2,035. Barabara hizi ambazo zimejengwa pamoja na Barabara ya Handeni – Kiberashi – Kwa Mtoro – Kiteto mpaka Singida, barabara ya kilomita 460. Barabara hii ikikamilika itaenda kubadilisha kabisa uchumi wa eneo hili. Leo hii Bandari ya Tanga ambayo tunaiboresha, itaenda kuwa na majibu kupitia barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana mkandarasi apatikane mapema, tumeambiwa mwezi wa Sita mkataba utasainiwa. Namwomba Mheshimiwa Waziri kwa heshima kabisa, tuhakikishe barabara inasainiwa mapema ili Wabunge wa maeneo ya kutoka pale Handeni, ndugu yangu Mheshimiwa Omari Kigua; ndugu yangu wa Kiteto, Mheshimiwa Olelekaita; ndugu yangu Mohamed Monni pamoja na mimi tuweze kufarijika na wananchi wetu waendelee kupata raha kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikimaliza hapo, Mheshimiwa Waziri nilikuomba barabara. Mlinipa barabara ya kilomita moja ndani ya wilaya yangu. Naomba sana mniongezee kilomita 10 kwa barabara ya kutoka Ikungi – Londoni kwenda Kilimatinde (Solya) kwa ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Chaya ili barabara ile ijengwe kwa kiwango cha lami kwa sababu tuna mwekezaji mkubwa wa madini pale ambaye yuko maeneo ya Mang’onyi. Ikiwepo barabara hii itaongeza thamani ya mradi ule ambao tumeuweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni wenzetu wa ATCL kwa maana ya Shirika letu la Ndege. Kwa muda mrefu tumeendelea kudogolesha Shirika letu na kwenye Kamati imeelezwa vizuri. Katika eneo hili nitaongea maneno mawili. Ili uweze kukuza uchumi wa nchi hii, ukiboresha Shirika la Ndege utaenda kuongeza thamani ya utalii. Watalii wengi watakuja. Biashara zinazofanyika kwenye maeneo mbalimbali duniani, ukiwa na ndege yako mwenyewe utakuwa na uhakika wa biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunategemea kupata ndege hivi karibuni ile ya Cargo ambayo itakuja kubeba mazao ya mboga mboga na maua kwenda nchi za Ulaya na Asia ambapo huko wanahitaji sana bidhaa hizo. Naomba sana shirika hili liangaliwe na Serikali, liendelee kuwezeshwa ili kuhakikisha kwamba linapata faida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili, pamoja na changamoto nyingine, kumekuwa na changamoto za madeni la shirika hili. Kwenye taarifa yetu tumepata sisi kwenye Kamati, wao walikuwa wanadaiwa karibia Shilingi bilioni 236 ambazo ni fedha walizokuwa wanadaiwa wakati hili shirika halifanyi kazi, lakini wamejitahidi kulipa karibia Shilingi bilioni 136, wamebakiwa na Shilingi bilioni 100. Serikali iangalie namna ya kumaliza deni hili ili tuweze kuweka mizania sawa ya hesabu za shirika hili, kuondokana na hasara ambayo inaweza kujitokeza na kulifanya shirika letu lifanye kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ni kuondoa matatizo ya kukamatwa ndege katika nchi nyingine ambazo zinaidai Tanzania. Ndege hizi zimekuwa zinashikwa, siyo ATCL inadaiwa, inadaiwa Serikali, lakini kwa sababu Shirika la Ndege halimiliki zile ndege, hizi ndege zinamilikiwa na Wakala wa Ndege za Serikali, ETGF, maana yake ni kwamba hao ni kama Serikali. Kwa hiyo, deni lolote linaloihusu Serikali, likipatikana eneo lolote, ndege yetu inakamatwa. Maana yake mtiririko wa usafiri unaondoka. Leo hii ATCL ikiondoka ndege moja tu, kama inaenda Mumbai ama nchi nyingine, maana yeke unapunguza mtiririko wa abaria. Maana yake usitegemee kupata faida. Leo hii CAG ataenda kuona kila siku shirika linapata hasara kwa sababu ni mpango ambao tumeuweka wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Serikali iangalie uwezekano wa kurudisha ndege hizi ATCL ili ziweze kumilikiwa na Shirika la Ndege lenyewe ili kuleta faida na kulifanya shirika letu liweze kufanya kazi vizuri. Ambacho ni mzigo mkubwa, leo hii Shirika la Ndege linalipa karibia Shilingi milioni 700 kwa ajili ya kukodisha ndege za Serikali. Hivi Serikali na Serikali zinakodishiana, kuna haja gani? Ndiyo maana shirika letu haliwezi kuendelea kwa sababu linakwazwa na mambo mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana kwenye hili Mheshimiwa Waziri atakaporudi, atuambie ni mpango gani wa Serikali umefikiwa kwa ajili ya kurudisha ndege hizi ATCL kuondoka kwenye Wakala wa Ndege wa Serikali na changamoto ambazo shirika linapata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu ambalo ni la mwisho ni suala la Bandari. Bandari ni lango kuu la biashara. Bandari yetu kwa maana ya mkao wa kijiografia Bandari yetu ya Dar es Salaam imekaa vizuri sana kistratejia. Bandari hii tukiitumia vizuri, inaweza ikaleta mapato mengi kuliko eneo lolote. Leo hii pamoja na mchango inayotoa lakini bado, haitoi mchango wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeboresha sana gati Na. 8 mpaka 11, tumeweza kujitahidi kuongeza masuala ya usalama katika bandari, ni sawa, lakini tumeongeza cranes ambazo bado ni kidogo sana. Cranes mbili zile zinazofanya kazi pale, tukiangalia bandari nyingine ambazo ziko kama Mundra kule India, kule Dubai na nchi nyingi, bandari nyingine zinafanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, tumeongeza mapato ya Shilingi bilioni 700 mpaka Shilingi trilioni moja tu, ambayo kimsingi ukiangalia hizi fedha bado ni ndogo kwa bandari yetu ilivyokaa. Nchi nane zinategemea Bandari ya Dar es Salaam, maana yake ni kwamba tukiboresha vizuri, Bandari ya Dar es Salaam itakuwa ni jibu la fedha ambazo hatuzipati katika maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana, pamoja na mambo haya, kuna changamoto chache zinakwaza bandari yetu. La kwanza, bado hatujakuwa na mifumo ya kusomana ambayo inaweza kumsaidia mteja kuvutika kuja kufanya biashara na sisi. Naomba sana tuhakikishe kwamba tunaangalia namna ya kumleta mwekezaji ambaye atashirikiana na Serikali. Siyo jambo la dhambi, PPP imetajwa kwenye sheria za nchi yetu, tusiwe waoga Watanzania tunapotaka kubadilisha maisha ya Watanzania wetu.
Tukiweza kuwekeza vizuri, itasaidia sana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mtaturu, ahsante sana.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Naam!

Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika moja nimalizie, ni-conclude hii hoja.

MWENYEKITI: Mheshimiwa, malizia sekunde thelathini muda wako umeisha.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa sekunde thelathini.

Mheshimiwa Mwenhyekiti, naomba sana Watanzania tusiwe waoga kwenye mambo ya msingi ili kuhakikisha kwamba tunaweza kubadilisha na kuongeza uchumi wa nchi yetu, kusaidia Taifa hili tuweze kujenga madarasa, tujenge miundombinu mbalimbali kwa ajili ya maisha ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya, naunga mkono hoja. Nashukuru sana kwa nafasi. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika hoja ambayo iko mezani. Kwa sababu leo itakuwa ni siku ya kwanza kuchangia naomba nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi na uhai wa kuweza kuchangia hoja hii ambapo naishauri Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake ya Wizara nzima, Naibu Waziri pamoja na Katibu Mkuu na watendaji wote kwa kuandaa na kutuletea Mpango huu ambao kwa kweli ni Mpango ambao umeendelea kutuonesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kuwaletea Watanzania maendeleo. Naomba nichukue nafasi hii kuwapongeza na naomba niseme tu kwamba tutaendelea kutoa ushauri ambao utakuwa na tija kwa ajili ya kuleta maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba Mpango wenyewe huu unakwenda kumalizia katika Mpango wa Miaka Mitano ninajua mambo mengi yako dhahiri ambayo yameonekana yameshafanyika. Zaidi niseme tu kwamba kuwa na Mpango ni jambo moja lakini kuusimamia na kuutekeleza ni jambo la pili. Kwa hiyo, sisi kwenye hili tunawapongeza kwa sababu tumekuwa na Mpango na sasa tunaona namna ambavyo kwa muda huu unaenda kumalizika mwaka wa tano mafanikio makubwa katika maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kwa kweli kwa dhati kabisa kumpongeza sana Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa namna ambavyo ameonesha dhamira ya dhati katika kuhakikisha kwamba anawaletea wananchi maendeleo. Najua kwamba utashi wake ndiyo ambao unatupa hata jeuri au inaipa jeuri Serikali kuhakikisha inafanya kazi vizuri kwa sababu tumekuwa tukipata fedha ya kuweza kutekeleza miradi hiyo. Tunaweza tukawa na mipango mizuri sana isipowezeshwa itakuwa ni kazi bure na itakuwa inabaki kwenye vitabu kama ambavyo tumekuwa tukiona baadhi ya maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba maeneo mengi ambayo naweza kuyasema ni yale ambayo nasema kwamba tumeanza kuona dhamira ya Serikali katika kukusanya mapato. Unaweza ukawa na mpango mzuri lakini ukawa hauna fedha lakini ukiwa na mpango mzuri ikiwa ni pamoja na kukusanya mapato inakusaidia wewe kuhakikisha kwamba unatimiza malengo ambayo yako mbele yetu. Jambo kubwa ambalo ni vizuri tukalisema ni dhamira ile ya kusimamia na kuzuia mianya yote ya kukwepa kodi katika nchi yetu. Siyo hivyo tu ni pamoja na kusimamia na kutokomeza kabisa rushwa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika baadhi ya maeneo ambayo tulikuwa tunateseka sana ni pale ambapo baadhi ya watumishi ambao hawana dhamira njema wamekuwa hawafanyi vizuri sana katika kusimamia mapato yetu. Kwenye hili, naomba niipongeze Serikali kwa namna ambavyo imesimamia na imeendelea kuongeza mapato katika nchi yetu yanayonifanya tuweze kutekeleza mipango ambao tunajipangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo yote nieleze sasa yale ambayo yanaonekana waziwazi. Tumeona namna ambavyo tunaboresha sana miundombinu ya barabara ambayo kwa kweli imekuwa ndiyo nguzo kuu ya uchumi wa nchi yetu. Niseme hapa katika mpango nimeona namna ambavyo mwaka huu ambapo tunaelekea kwenye bajeti tutaenda kujikita katika kuongeza fedha ambazo zinakwenda kuongeza uwezo wa kujenga barabara zetu ikiwa ni barabara za lami na madaraja makubwa na kadhalika. Niombe tu kwamba haya ambayo yamepangwa basi yawekwe vizuri kwa ajili ya kutoa fedha ili tuweze kuona miradi hiyo inaweza kufanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hivyo tumeona reli ya SGR inajengwa. Ni dhamira ya dhati tuliamua kama Taifa na leo tunavyoona speed ni kubwa sana tuko zaidi ya asilimia 60 ya utekelezaji wa mradi. Kwa hiyo, niseme tu kwamba hii nayo itakuwa ni kichocheo muhimu katika uchumi na usafirishaji wa mizigo ikiwa ni pamoja na kupunguza bei ya bidhaa sokoni. Bei ya bidhaa ikipungua maana yake itamsaidia mwananchi wa kawaida kuweza kupunguza mfumuko wa bei kwa sababu bei itakuwa chini katika usafirishaji wa mizigo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo yote hatutaacha kusema maneno machache kwenye sehemu ya uboreshaji wa ununuzi wa ndege. Hili jambo tusipolisema na dhamira ya dhati ikaonekana maana wengine wamekuwa wakipotosha eti wanathaminisha ndege wanasema vingejengwa vituo vya afya kadhaa. Niseme tu kama Taifa lazima tuamue nini cha kufanya, huwezi kusema unaogopa kununua shati jipya kwa sababu huna utoshelevu wa kubadilisha kula mboga, huwezi kuogopa hilo, lazima uamue kwamba ndege zinazonunuliwa zinaenda kuongeza uwezo wetu wa kuweza kuhudumia sekta ya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tumekuwa tukiona na tukilalamika na mimi nimekuwa nikiwaona Waheshimiwa Wabunge wanasema ndani ya Bunge kwamba haiwezekani watalii washukie Kenya waletwe kwa magari kuja kwenye mbuga zetu na baadaye warudi wakapandie Kenya kwa shirika lingine la ndege. Leo tunapata ndege maana yake tuna uwezo sasa wa watalii wale wote kushuka kwenye viwanja vyetu ndani ya nchi yetu na wanakwenda moja kwa moja kwenye utalii. Utalii ndiyo sekta ambayo inaongoza katika mapato katika nchi yetu. Kwa hiyo, tunapoboresha Shirika la Ndege maana yake moja kwa moja tunaiboresha hii sekta ya utalii ambayo ndiyo inaleta fedha nyingi ambapo mwisho wa siku itajenga vituo vya afya, shule, itaboresha elimu bure pamoja na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Taifa lazima tujivunie kwa sababu lazima nchi isonge mbele kwa kuwekeza kwenye mambo makubwa. Kwa hiyo, hatuwezi kuwa sisi wenyewe tunafanya mambo makubwa lakini hatujui kama tunafanya mambo makubwa. Hii haitatujenga kama Taifa, Watanzania tuipende nchi yetu kwa yale makubwa mazuri tunayoyafanya. Tofauti ya vyama vya siasa isitufanye tuondoke kwenye reli, lazima tujivunie na sasa hivi tunaona ATCL wanafanya vizuri, Mheshimiwa Waziri anayehusika na sekta hii yupo pale kwa kweli kazi inafanyika vizuri na sisi kama Waheshimiwa Wabunge ni lazima tuunge mkono juhudi kubwa hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kueleza maelezo haya, kabla muda wangu haujaisha, nitoe maneno machache ya ushauri kwenye suala la kilimo. Waheshimiwa Wabunge wengi wamesema, lakini naomba na mimi nieleze kidogo, asilimia 80 ya wananchi wetu wanafanya kilimo. Kama kweli tutaweza kuwekeza kwa dhamira ya dhati katika kilimo itasaidia sana kutuongezea pato la Taifa lakini itasaidia uchumi wa mwananchi mdogo kule chini chini, wakati wa kutegemea msimu wa mvua umepitwa na wakati, tuongeze nguvu katika kilimo cha umwagiliaji na zaidi tuongeze uwezo wetu wa kusimamia miradi hiyo na itoe matokeo, katika baadhi ya maeneo tuweze kuvuna zaidi ya mara mbili ili tukipata mapato ya kutosha kwenye eneo hili itasaidia hata mapato ya ndani katika halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halmashauri zetu nyingi zinategemea mazao katika mapato, tukiwekeza kwenye kilimo naamini kabisa tutaenda kuongeza uwezo wa wananchi wetu na kipato chao katika kaya. Kipato cha kaya kikifanikiwa ndiyo tutasaidia kwenda kwenye huo uchumi wa kati ambao tunausema kwa sababu tunaangalia na tunatathimini namna ambavyo mwananchi anajipatia kipato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiondoka kwenye eneo hilo, niende sasa kwenye eneo la pili la miundombinu. Tunaamini zile barabara kubwa zile trunk roads zinajengwa kwa kiwango cha lami, lakini nieleze kidogo kwenye barabara ambazo ziko chini ya TARURA. TARURA wamekuwa wakitengewa fedha kidogo sana naamini wanataka kujenga madaraja, wanataka kuongeza uwezo wa ujengaji wa barabara zao, lakini fedha wanazopata ni ndogo sana hazina uwezo wa kututoa pale na ile dhamira ya kuanzisha hii agency haitakuwepo kama hatutawapa fedha za kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana kwenye mpango huu naona imeguswa na imewekwa, lakini naona kabisa namna ambavyo mfano kama Wilaya ya Ikungi pale, zipo barabara ndevu lakini nyingi hazijawahi kutengenezwa, ni barabara za asili kama mapalio, naamini kabisa Mheshimiwa Waziri ananielewa ninavyoeeleza hayo, kwa sababu TARURA huwa wanaleta maombi yao na yamekuwa wakipata fedha kidogo sana, wakati ambapo barabara hizi zikijengwa zitasaidia kusogeza mbele suala la kuleta maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikimalizia kwenye eneo la umeme juhudi naziona ni nzuri sana, nipongeze sana Serikali kwa namna ambavyo wizara imeendelea kusimamia upatikanaji wa umeme kwa kupitia miradi ya REA, tatizo kubwa ambalo naliona lipo kwa wakandarasi, wakandarasi wamekuwa hawatekelezi miradi kulingana na mikataba yao, wakandarasi wengine wanalalamikiwa hata na wafanyakazi wao, hivyo inasababisha kufifisha juhudi za kuwapelekea wananchi umeme, kwenye eneo hili ni vizuri Serikali kupitia Wizara husika waweze kusaidia kuhakikisha kwamba wananchi wanapatiwa umeme mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ndogo ambayo ipo pia ni maeneo yale ambayo wanasema kwamba wanapelekewa umeme kwenye vijiji lakini wanapelekewa vijiji ambavyo viko pale pale centre, umeme hauendi mpaka kwenye vitongoji. Inawezekana dhamira ya Serikali ni hiyo, lakini imekuwa tunavuka baadhi ya vitongoji, jambo hili linatuweka kwenye wakati mgumu ambapo tunakosa majibu, wakati hamu ya wananchi ya kupata umeme ni ya hali ya juu. Baada ya maneno haya, naomba tu niendelee kusema CCM hatujakataa kuingia uwanjani, tuko tayari, lakini naomba pia na wao wafuate mwongozo uliowekwa ili waingie uwanjani wakiwa salama. Huwezi kuingia uwanjani huna viatu wakati wenzako wanaingia na viatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kuniona na kuweza kuniweka kwenye orodha hii. Kwa hakika ni bahati ya pekee kwa sababu ya muda, lakini nichukue nafasi hii kwa sababu ni mara ya kwanza, kumshukuru Mwenyezi Mungu kuweza kunijalia afya na uzima na kuweza kusimama mbele ya Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kuwashukuru sana wananchi wa Singida Mashariki pamoja na chama changu, Chama Cha Mapinduzi chini ya Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuniteuwa na kugombea ubunge na hatimaye wananchi wa Singida Mashariki walinichagua kwa kura nyingi za kishindo. Niwahakikishie uongozi uliotukuka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze tu na maneno machache kwa maana ya kwamba, kiongozi wetu, Rais wetu ametoa hotuba nzuri ambayo imetoa muelekeo wa miaka mitano ijayo Tanzania tunayoitaka na hii imeanza toka mwaka 2016 alivyoingia hapa alionesha dira na kwa miaka mitano tumeona mambo makubwa yaliyofanywa katika nchi hii na kwa hakika ni historia ambayo haitafutika. Lazima sisi kama Watanzania tujivunie viongozi wa aina hii na tuendelee kuwapa moyo na kuwaunga mkono kwa sababu Tanzania yetu imepiga hatua kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, lakini kama ambavyo unajua miundombinu ipo ili iweze kuwezesha Watanzania au wananchi kuweza kuleta maendeleo. Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa, ni vizuri kama Watanzania tuendelee kuunga mkono juhudi hizi na kwa hakika kwa miaka mitano ijayo tumeona dira yake kwa hiyo, ombi langu tu nilikuwa nataka nieleze maneno machache kwenye eneo la elimu.

Mheshimiwa Spika, bado tuna changamoto kwenye maeneo ya miundombinu ya elimu. Niiombe sana Serikali kupitia Rais alivyoeleza tuendelee kuongeza nguvu ya kuleta fedha kwa ajili ya kuimarisha vyumba vya madarasa, kuimarisha mambo ya maabara, kuimarisha suala la mabweni kwa ajili ya watoto, hasa watoto wa kike. Watoto wa kike wengi wanapoteza ndoto zao za kusoma kwa sababu mazingira ni magumu katika shule zetu za kata ambazo wanatembea karibu kilometa zaidi ya tisa kufuata shule hizo. Kwa hiyo, niombe sana Wizara ya Elimu kuhakikisha kwamba tunaboresha miundombinu hiyo.

Mheshimiwa Spika, lakini nieleze hili suala ambalo wenzangu wote wamesema, suala la miundombinu ya barabara. Ninaamini kabisa TANROADS inafanya kazi nzuri kwa sababu imewezeshwa, lakini tulivyoamua kuanzisha Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA), lengo lilikuwa ni kuondoa urasimu uliokuwepo wa kuleta fedha kupitia Mfuko wa Barabara. Leo hii tunavyoleta mgawanyo wa asilimia 70 kwa TANROADS na asilimia 30 kwa barabara za TARURA ni kama vile tunaifanya taasisi isifanye kazi yake, inakuwa haina maana ya kuianzisha TARURA kama hatuipi fedha.

Mheshimiwa Spika, leo hii tuna barabara nyingi sana kwenye vijiji vyetu ambazo zinaenda kuboresha kilimo. Niombe sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja basi aeleze mipango ya kuiongezea TARURA fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba barabara za vijijini ambazo zinaleta huduma mbalimbali ikiwemo elimu, afya, zahanati nyingi ziko vijijini. Tusipokuwa na barabara nzuri maana yake hatuwezi kuwahudumia wananchi ambao wako maeneo mbalimbali ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nieleze maneno machache sana. Mheshimiwa Rais alikiri mbele ya Bunge kwamba ataboresha demokrasia, lakini utawala bora. Kwa miaka mitano tumeona kazi nzuri iliyofanyika ikiwemo kusimamia watumishi wa umma ambao walikuwa hawafanyi vizuri sana katika maeneo yetu. Watumishi wa umma wengi walikuwa wengine hawawatendei haki Watanzania na tumekuwa wengi tunalalamika hapa.

Mheshimiwa Spika, leo hii Mheshimiwa Rais amesimama amesema, lakini sisi wote ni mashahidi, leo hii kuna baadhi wanasimama hapa wanasema hakuna demokrasia, lakini utawala bora hakuna. Niwaulize wao wenyewe hivi leo wanataka turudi tulikotoka ambapo Watanzania wengi walikuwa wanalalamika baadhi ya watumishi ambao hawafanyi vizuri katika maeneo fulani?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe sana kama chama cha siasa wajibu wako wewe ni kuhakikisha unahudumia wananchi, lazima utatue kero zao. Wenzetu hawa wanaongea…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Miraji Mtaturu.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwa sababu ya muda naunga mkono hoja iliyoko mbele yetu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja iliyoko mbele yetu ya Wizara yetu ya nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kutujalia uzima kukutana jioni ya leo, pili, kama ambavyo wamepongeza wengine, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa dhamira yake kuifanya sekta hii sasa angalao tunaona tunaenda, hii inaonesha wazi kwenye miradi mbalimbali ambayo tunaisimamia, ukiwemo mradi mkubwa wa Mwalimu Nyerere ambao utaweza kutotolea megawati 2,115 ambazo zitaweza kusambaza umeme katika nchi nzima. Kwa hiyo, jambo hili ni kubwa, linastahili pongezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Ndugu yangu Mheshimiwa Januari Makamba pamoja na Naibu wake Ndugu yangu Mheshimiwa Byabato, Katibu Mkuu pamoja na Wakuu wa Taasisi wote walioko kwenye Wizara hii ya nishati. Wanafanya kazi nzuri, tunaona kazi zao, tuna-enjoy kazi zao na kwa hakika wanatupa heshima kama Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kama ambavyo tumesema tunaona tunaelekea vizuri kwenye miradi ya REA - umeme vijijini. Tumeambiwa na Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake asilimia karibia 82 sasa tuna-cover nchi nzima. Ni jambo zuri tunaona tunabakia kama na asilimia 18. Asilimia 18 inaonekana kuna miradi iko kazini, iko on progress kitu ambacho ni kizuri sana. Nataka nishauri tu mfano kwenye Jimbo langu la Singida Mashariki nilikuwa na ugomvi mkubwa na Wizara yako Mheshimiwa Waziri, nilikuwa na tatizo la Tarafa nzima ya Mungaa. Tarafa nzima ya Mungaa ilikuwa haina umeme hata Kijiji kimoja katika vijiji vile 26 leo ninavyoongea vijiji vyote vimewekewa nguzo na asilimia 40 viemshawashwa umeme. Maana yake ni kwamba, tunaona dalili njema na sisi ya kuonja keki ya Taifa kwenye upande wa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nikuhakikishie kwamba, tutakapofika mpaka Disemba kama Wakandarsi wataenda hivi, tunaamini tutamaliza vijiji vyote vilivyobaki. Hilo nalisema kwa sababu, kuna Tarafa ya Ikungi ambayo ilianza kupata umeme ilikuwa ina tatizo la baadhi ya vijiji kama Ng’ongosoro, Matongo, pamoja na pale Mwanjiki, hivi ninavyoongea saa hizi hatuna ugomvi na wewe umeme unaenda kuwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hoja yangu ni ambayo tunaisema wote hapa, tunaenda kumaliza vijiji Mheshimiwa Waziri, tuna tatizo la vitongoji. Nikuombe sana vitongojini ndiko waliko wananchi. Nikuombe sana huo mpango ambao umesema angalao vitongoji 15, Mheshimiwa Waziri havitoshi, tutakuwa na kelele kubwa sana. Nikuombe sana kama utaweza unapokuja ku-wind up hapo kesho utueleze namna ambavyo utakuwa na mipango ya muda mfupi ya kuongeza angalao ili tuweze kuvifikia vitongoji vingi kwani vitongoji hivyo ndiko waliko watu, ndiko ziliko kaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilometa mbili ambazo tulikuwa tunapata hazitoshi kwenda popote, ninaamini zinagusa maeneo machache sana. Kwa hiyo, kwa sababu umeme kila mmoja anapouona anatamani na kwake upatikane. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, ninajua wewe ni msikivu, ni kijana mwenye nguvu, Mheshimiwa Rais amekuamini, hebu simamia hii sekta. Wananchi wa kule kijijini nao waweze kupata umeme kama ambavyo wengine wanapata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumaliza eneo hili nihamie kwenye eneo la mambo kama matatu ambayo ni mahsusi nataka niyaeleze. Mheshimiwa Waziri kwenye eneo hili la umeme wa maji tumekuwa tukisema tunaongeza uwezo, lakini tumeona umesaini mkataba juzi wa umeme wa jua pale Kishapu ni jambo zuri sana, lakini tumekuwa na kilio cha muda mrefu cha umeme wa upepo. Umeme wa upepo tumezungumzia Makambako, tumezungumzia Singida, hivi ninavyoongea kuna watu wameonesha nia ya kuweza kuwekeza, lakini mpaka sasa bado hatujaona dalili yoyote ya kuanza kwa umeme huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umeme wenye uhakika ambao hautakuwa unaangalia tabianchi, ninaamini kabisa tukiongeza kwenye gridi ya Taifa umeme wa upepo naamini kabisa uta-cover nchi yetu vizuri. Nikuombe sana unapokuja utuambie mipango mahsusi ya Wizara yako na wewe tunakuamini unaweza kuongeza hili jambo na kuongeza speed pale tulipokwama. Kumekuwa na siasa nyingi, naomba hizo siasa tuziondoe, tuhakikishe kama mradi ule wa Singida uanze mapema ili tuweze kuingiza kwenye Gridi ya Taifa wakati tunasubiri vyanzo vingine. Ninaamini hili utalifanya na litatuongezea uwezo mkubwa wa kusambaza umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili kwenye eneo la kiwanda. Kiwanda ili kiweze kufanya kazi, kwa maana naongelea Shirika la TANESCO, lazima uwe na vitu kama mitambo na mashine na technology, jambo la pili lazima uwe na fedha za kuwekeza ambazo tunazitafuta wote, tatu ni rasilimali watu. Ukishakuwa na rasilimali watu yenye furaha, yenye motisha, yenye kupewa support muda wote, utafanya kiwanda kifanye kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimemsikia Mheshimiwa Mkundi amesema asubuhi, kumekuwa na manung’uniko kidogo, kwa upande wa wafanyakazi wa TANESCO, kumekuwa na dalili ya kwamba, mnaweza mkapunguza wafanyakazi. Leo hii Shirika unao wateja milioni nne nchi nzima katika nchi yetu, lakini unao wafanyakazi 9,900 tu wastani wa mfanyakazi mmoja anahudumia wateja 424. Maana yake ni kwamba, kuna mfanyakazi mmoja anahudumia wateja wengi sana, maana yake huwezi kutegemea tija pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, leo unapotaka kwenda kupunguza wafanyakazi maana yake unaenda kupunguza uwezo wa kuwahudumia wateja ambao leo tunasema tuende vijijini tukaongeze idadi ya wateja wetu. Usitegemee kupata ufanisi kama hili jambo lipo kweli na tumeendelea kupata taarifa kwamba mnaendelea kupita kwenye Mikoa kuwaambia kuna mpango wa kupunguza, mfano kama Mkoa wa Ilala wa ki-TANESCO, kuna wafanyakazi 288 unasema utabakiza wafanyakazi 86, unategemea uta-cover vipi huduma pale katika Mkoa wa Ilala? Mkoa wa Dodoma kadhalika una wafanyakazi 162, unategemea wabaki 86, watahudumiaje wateja wa Mkoa huu? Maana yake ni kwamba, unaenda kuanguka, unaenda kufeli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Mheshimiwa Waziri najua hili huna taarifa, kumekuwa na fukuto ndani kwa ndani linaendelea kwenye Menejimenti, lifanyie kazi, waite kama Vyama vya Wafanyakazi mzungumze ili muwafanye wafanyakazi hawa waendelee kufanya kazi ambayo tunaitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sana niongelee jambo moja la mwisho ambalo ni kuhusiana na wenzetu hawa ambao wanafanya vinasaba, ambao ni TBS. Mheshimiwa Waziri umesikiliza Wabunge wengi wanaongea, kumekuwa na kampuni ya SISPA ilifanya kazi hiyo ya kuweka vinasaba na ilikuwa ina uwezo mkubwa lakini cha kushangaza tulivyowapa TBS wanatoka hawana uwezo wa kutengeneza vinasaba wanaenda tena kwa SISPA kuchukua tena vinasaba wanavileta huku. Mheshimiwa Waziri wakati tunaamua maamuzi mengine tuwe tunafikiria kwa kina, tunaweza kuwa tunataka Serikali ifanye, lakini mwisho wa siku uwezo tunao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaweza kujikuta wenyewe, kama hivi mmeambiwa Mheshimiwa Mwambe anakwambia tunaongeza gharama ya mafuta, tunamtesa nani, tunamtesa mlaji ambaye ni mwananchi. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri eneo hili ukalifanyie kazi, ninaamini kabisa tunayo nia njema wote kama Taifa, kuna baadhi ya mambo kama tumefeli tuangalie nyuma tulikotoka turekebishe ili nchi yetu iweze kwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijamaliza, niendelee tena kurudia kuomba sana kwenye kuhakikisha kwamba, umeme unakuwa wa uhakika. Mnajua mna miradi ya gridi imara, mnafanya kazi vizuri, niombe sana tuangalie maeneo yote. Tunayo maeneo ambayo umeme unakatika mara kwa mara, mfano leo Wilaya ya Manyoni na Ikungi umeme unakatika bila utaratibu, kumekuwa na malalamiko mengi sana. Ninaamini kabisa tuki-stabilize umeme tutafanya uchumi uende mbele na tutafanya watu wafanye kazi zao vizuri kwa uhakika na waendelee ku-enjoy kazi nzuri inayofanywa na Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya Mheshimiwa Waziri ninaomba sana suala la vitongoji tutazame tuweze kumalizia vitongoji vilivyobaki ili tuende pamoja kama Taifa. Mungu akubariki sana na ninaomba Waheshimiwa Wabunge wote tumpitishie ndugu yangu aweze kupita aende kufanya kazi zake vizuri. Ahsante sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)
Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, washindwe kabisa kwa jina la Yesu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana, haya ni majaribu katika dunia, tunamwomba Mwenyezi Mungu atupitishe salama.

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kupata nafasi hii, lakini pili kabla sijapongeza kiongozi wetu wa nchi, nianze kwa kueleza kwamba uchumi duniani unaendeshwa kwa misingi mliyokubaliana kama Taifa na uchumi unazingatia maandiko na sera mlizokubaliana wenyewe, na nchi yetu imekubali sekta binafsi kufanya kazi na Serikali, kwa hiyo sekta binafsi kama tulivyosikia wengine inabeba shughuli za uchumi kwa asilimia 90 na ndio Serikali inawaalika sekta binafsi, lakini Ilani ya Chama cha Mapinduzi na hili lieleweke Ilani ya CCM sio kadi ya CCM, ieleweke ni Ilani ya Chama cha Mapinduzi, sera na ndio ahadi tulizoahidi mwaka 2020, kwa hiyo tunaponukuu kitabu hiki tunaenda kwenye reli tuliyokubaliana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Ilani hii kwenye Ibara ya 9(b) pamoja na Ibara ya 14 zinaeleza wazi na kwa sababu ya msingi wa maelezo yangu, nisome maneno machache tu, inasema; “kukuza uchumi wa kisasa, fungamanishi, jumuishi na shindani, kwa kuweka mazingira wezeshi kwa sekta binafsi kukuwa na kustawi pamoja na kuvutia wawekezaji ili kuleta mchango stahiki katika maendeleo ya nchi yetu; lakini pili yake inasema CCM inatambua na kuthamini nafasi ya sekta binafsi hivyo itaendelea kusimamia Serikali katika kuhakikisha kuwa inalinda sekta binafsi pamoja na kuweka mazingira ya kiuchumi na kibiashara yanayo vutia wawekezaji nje na ndani ya nchi yetu.”

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 63(3)(e) inaeleza wazi mikataba yote itakayokuwa inakutana kati ya nchi na nchi italetwa Bungeni. Ninapoenda kumpongeza Mheshimiwa Rais ni kwa mara ya kwanza ninaweza kusema tunapata mkataba wa nchi na nchi unaletwa ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Jambo hili ni jambo tunatakiwa tumpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa dhamira yake ya dhati ya kuweka mambo hadharani katika mambo makubwa yenye maslahi ya Tanzania. (Makofi)

Kwa hiyo, nataka niwahakikishie Watanzania kwamba, maslahi mapana ya Tanzania yanalindwa kwa sababu sisi tunawawakilisha Watanzania wote ambao ni zaidi ya milioni 61. Kwa hiyo nikisema hivyo nielekee sasa kwenye mchango wangu.

Mheshimiwa Spika, nimeusoma huu mkataba, nimeusoma mkataba kwa maana ya makubaliano hayo, lakini sina haja ya kwenda details za huko nyuma, naomba nieleze tu kwamba pale nyuma..., naomba hiyo, kwa sababu nimehama kiti.

Mheshimiwa Spika, mimi sio mwanasheria nimesoma engineering, kwa hiyo nintaka tu niseme kwamba ile appendix I imejibu hofu ya watanzania. Imeeleza kwamba areas of cooperation, imeeleza kwa maana ya phase one na imeeleza phase two tutakazoenda kushirikiana katika jambo hili. Kwa hiyo, nataka niwaombe Watanzania kwamba wanasheria wetu wamesimamiwa na Serikali na kwa sababu na namna ambavyo tumejiandaa vizuri kwenye uwekezaji na kwa historia mbalimbali za huko nyuma ninaamini kabisa makubaliano haya yatakuwa na maslahi ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninachotaka kusema hapa katika msingi ule ule wa kufungamanisha biashara za wananchi na katika biashara na wananchi wetu ni kwamba sisi tunayo Bandari ya Dar es Salaam, Bandari ya Dar es Salaam wanakwmbia inaendeshwa chini ya kiwango kwa maana ya jiografia tuliyonayo, lakini tumekuwa tukishauri hapa Bungeni kwamba tumekuwa tunaendesha chini ya kiwango, tumekuwa na malalamiko mengi ya bandari yetu, tumekuwa hatuwapati wateja wote ambao tunatakiwa kuwapata, lakini meli nyingi zimekuwa zikichelewa hata kushushwa maana yake ni kwamba kuna mambo hatufanyi vizuri ndio maana Serikali ilipofanya tathmini ikajiridhisha kwamba inapaswa iingie sasa utaratibu wa uwekezaji wa ubia ili kuhakikisha kwamba bandari yetu inafanya kazi kama inavyotakiwa.

Mheshimiwa Spika, lakini leo tunavyoongea tumeweza kujenga reli yetu ya SGR. Reli hii ni reli ambayo tumewekeza fedha zaidi ya trilioni 17; ni fedha nyingi sana. Tusipoangalia reli hii au treni hii itakuwa kama toroli kama matoroli mengine, haitakuwa na faida yoyote katika nchi yetu kwa sababu reli inataka mzigo, reli inataka mzigo, kama hatuna mzigo mzuri kutoka Congo na maeneo mengine, reli hii haitarudisha fedha tuliyowekeza pale. Kwa hiyo, ndio maana tukasema kwamba lazima bandari yetu ambayo ni hab iweze kuwa na mzigo wa kutosha na mzigo wa kutosha hauwezi kuja bila kuboresha huduma za kibandari.

Mheshimiwa Spika, tukiboresha huduma za kibandari itasaidia kuchachua uchumi wa nchi yetu wamesema wengine hapa. Kwa hiyo, hoja ni kwamba tunachoangalia hapa ni matokeo yatakayotokea pale mbele yetu, lakini SGR hii itakwenda kuwa na tija kama tutakuwa na mzigo kama nilivyoeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niendelee zaidi niseme mapato yetu ya nchi yetu yanategemea sana pale kwenye bandari yetu. Leo hii soko lile la pale Kariakoo linategemea kwa asilimia kubwa namna mzigo unavyoingia katika bandari yetu. Maana yake ni kwamba leo bandari isipofanya vizuri automatic Kariakoo haitafanya vizuri. Kwa hiyo, nilitaka niseme huu uwekezaji unapokwenda kuwekwa utaenda kuwa na tija kwenye maslahi ya Taifa letu, lakini kama haitoshi tumeambiwa mapato yataongezeka kutoka trilioni saba mpaka trilioni 26 maana yake nini? Sisi bajeti yetu ya mwaka ni trilioni 42 tukiweza kukusanya kwenye bandari peke yake trilioni 26 maana yake tutakuwa na asilimia 62 ya mapato yetu yote yataenda ku-cover kwenye Bajeti Kuu ya Serikali, maana yake tutaondoka kwenye utegemezi wa misaada kutoka nje kwa wale washirika wa maendeleo, maana yake sasa hivi tunategemea asilimia 20 kutoka nje. Maana yake tukiweza kupata trilioni 26 hizi zitaenda kuondoa lile gap tulilokuwa nalo kama Taifa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hoja yangu nilitaka niseme azimio hili tunapoenda kulipitisha, linaenda kuanzisha safari nzuri ya maendeleo ya uchumi wa Tanzania. Wale ambao wanapotosha wanaweza wakawa wana nia mbaya kwa sababu wengine hawapendi tuendelee kupiga hatua, lakini kama haitoshi Mheshimiwa Rais anataka aone nchi yake inakwenda. Tumekuwa hapa na kelele kwenye Mradi wa Mwalimu Nyerere, tumekuwa tunataka kuwa na umeme wetu wa uhakika, tunaenda kuzalisha zaidi ya megawatts 2115, tutaenda kujibu kiu ya Watanzania ya kupata umeme vijijini lakini mradi ule tungekuwa tumesikiliza kelele leo tumefikia asilimia 87. Mheshimiwa Rais ameusimamia vizuri, tungesikiliza watu hawa leo tungerudi tunaendelea kuwa na matatizo ya umeme nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe sana mradi huu twende mbele matokeo watayaona Tanzania tunayo itamani inakuja kupitia uboreshaji wa bandari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini maneno mawili ya kuzingatia maombi yangu makubwa ni kuomba sana tutakapomaliza hii IGA kupitisha leo niwaombe kwenye HGAs wataalam wetu na Serikali wasimamie mikataba ya miradi itakayoenda iweze kuwa na maslahi kwa ajili ya Watanzania, ile hofu ya watanzania ambayo ipo iondolewe kupitia mikataba midogo midogo itakayoenda kuwekezwa, lakini kama haitoshi tumeambiwa TPA ndio watakaoendelea kuwa msimamizi wa bandari yetu kwa mujibu wa Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Naamini kabisa tutasimamia vizuri mambo ya kiusalama, tutasimamia vizuri sana mambo yote yanayoelekea huko.

Mheshimiwa Spika, nimalizie…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: La mwisho ni kulinda ajira za Watanzania ili waweze kuwa na faida na mradi huu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema maneno hayo ninaunga mkono na ninaomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu tuunge mkono azimio hili ili Serikali iweze kufanya kazi. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2023/2024 ambao imewasilishwa na Mheshimiwa Waziri kaka yangu Dkt Mwigulu Lameck Nchemba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kutujalia uzima na kukutana asubuhi ya leo. Pili, kwa dhati ya moyo wangu na kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Singida Mashariki nasema hivi wananchi wa Jimbo la Singida Mashariki walionipigia kura nyingi sana natamka hadharani kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa aliyoifanya katika muda wa miaka miwili. Kazi kubwa aliyoifanya katika uongozi wake kudumisha demokrasia nchini, kuweka uwazi wa Serikali, diplomasia na kutekeleza miradi ya maendeleo ambayo leo tunajivua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakika Mheshimiwa Rais kwa kazi anayoifanya na vijana siku hizi wanasema Mheshimiwa Rais anastahili kupewa maua yake ya kutosha kwa kazi nzuri anayoifanya. Kwa hakika wale wenye nia njema hawatakuwa na kusita kumpa maua yake, tumpe maua mengi Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumetokea tabia ambayo nataka ienee katika nchi yetu, eti kwamba tusipongezane kwa mambo mazuri yanayofanyika, wengi wamefika mahali wanasema ukimpongeza unakuwa wewe ni chawa. Hata kwenye Biblia imeandikwa kwamba: “moyo usiyo na shukurani hukausha mema yote” Kwa hiyo Watanzania tusijengewe, kwa sababu tu humpendi Fulani, kafanya jambo zuri, mpongeze afanye kazi zaidi. Kwa hiyo Mheshimiwa Rais anapofanya kazi nzuri, uungwana wa kawaida unatakiwa umpongeze kwa sababu anafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Jimbo letu la Singida Mashariki, Wilaya ya Ikungi katika muda huu tunaoenda kumaliza bajeti ambayo tumeletewa, fedha tulizoletewa za kutekeleza miradi ni zaidi ya bilioni saba zimeshuka katika wilaya yetu. Kwa hiyo maana yake ni kwamba fedha nyingi zimeshuka kutekeleza miradi, si kwamba tunatarajia fedha zimekuja na hivi tunavyoongea miradi lukuki imetekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajivunia sana uongozi wa Mheshimiwa Rais, tunajivunia kiongozi wetu anavyofanya vizuri. Sisi wananchi kuna maeneo yalikuwa hamna madarasa, leo madarasa yapo, kulikuwa hamna vituo vya afya, kuna vituo vya afya, kulikuwa barabara zimejifunga, barabara zimefunguka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo katika Wilaya yetu ya Ikungi tulikuwa hatujawahi kuwa na lami, sasa lami inawekwa, tulikuwa hatuna taa za barabarani, tulikuwa gizani usiku, tunalala mapema, leo taa za barabarani zinawekwa. Tutakuwa watu wa ajabu kabisa bila kumpongeza Mheshimiwa Rais na kuishukuru Serikali kwa kazi nzuri. Mzee Mkapa alisema kushukuru ni kuomba tena, tunaamini tunaposhukuru tunamwomba tena Mheshimiwa Rais atuletee fedha tuweze kuleta maendeleo ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, nampongeza sana Mkuu wa Mkoa ndugu yangu Peter Serukamba kwa kazi nzuri ya kusimamia shughuli za maendeleo, nampongeza sana DC wa Ikungi ndugu yangu Thomas Apson kwa kazi nzuri ya kusimamia maendeleo na nampongeza Mkurugenzi wetu Justice Kijazi kwa kazi nzuri ya kusimamia maendeleo. Hivi tunavyoongea tumepata hati safi kwa sababu ya usimamizi mzuri unaoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno hayo, naomba nichangie maeneo mawili makubwa ambayo yatasaidia katika kutoa ushauri kwenye bajeti yetu tunayoenda kuipitisha. La kwanza ni sekta ya uzalishaji, lakini pia nitaongelea ushirikishwaji wa sekta binafsi kwenye ukuaji wa uchumi wa nchi yetu. Katika maeneo haya mawili nitaomba niende haraka kwa sababu yamejaa mambo muhimu kwa ajili ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni sekta ya uchumi, ambayo ni sekta ya uzalishaji upande wa kilimo. Kilimo kimeongezewa fedha katika mwaka huu wa fedha. Tumpongeze sana Mheshimiwa Rais, tumpongeze Waziri wa Fedha, tuwapongeze kwa kuleta fedha nyingi katika kutupitisha zikatekeleze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili nitakuwa specific kwenye eneo la kilimo cha alizeti, kwa maana ya mafuta ya kula. Tulikuwa tukilalamika hapa nchi yetu ina upungufu wa mafuta ya kula mpaka tukalazimika kwenda kuagiza nje ya nchi. Tumekuwa tukitumia fedha nyingi za kigeni kwa ajili ya kununua mafuta nje ya nchi. Ukaja mkakati kupitia Wizara ya Kilimo, tuzalishe alizeti ya kutosha, wakaleta mbegu, wananchi wakawezeshwa, leo tunavyoongea wananchi wamevuna vya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavyoongea bei ya debe la alizeti limeshuka, wananchi wangu wanalalamika. Wanaomba Serikali itusaidie kuhakikisha kwamba ili ile alizeti yao inawapa faida. Kwa hiyo nataka nimwombe sana Waziri ahakikishe kwamba tunasaidia zao hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia hapa kwenye eneo na namna ambavyo tunapunguza kodi katika refined mafuta kwa asilimia 25 badala ya 35 ambayo tunadhani ingekuwepo. Niombe sana kwenye semi refined tunayo asilimia 10, lakini kwenye crude oil tunayo asilimia sifuri ili kusaidia viwanda vya ndani. Niombe sana kama tunataka kuendana na mpango mzuri wa Wizara ya Kilimo, nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha turudishe asilimia 35 kwenye refined hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufanya hivi kutasaidia kupunguza mazao yanayotoka nje kwa maana ya bidhaa ya nje isiingie humu ndani ili tuweze kuwa na uwezo mkubwa wa kuzalisha na tumsaidie mkulima aliyoko pale kijijini. Hiyo ndiyo itakuwa na maana kubwa kwa uwekezaji wa kilimo cha alizeti ambacho tunasema, pia itaongeza mafuta mazuri ya alizeti katika nchi yetu ambayo nje ya nchi wanayahitaji, maana yake tutauza mpaka nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe ili kumkomboa mkulima na kwenda na kauli moja, kwa maana ya lugha ya pamoja, tunaomba sana tupandishe kuwa asilimia 35 badala ya 25 ambayo tunaipendekeza ambayo kiukweli itaenda kuua soko, itaenda kuua kilimo cha mwananchi wetu wa kawaida kitu ambacho siyo lengo la Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana hilo na Wabunge wengi wameshauri, naomba sana hili lichukuliwe na namwomba Waziri anapokuja kuhitimisha aje atuhakikishie hilo, wananchi wanasubiri huko nje, wanatuambia tusaidieni, tuokoeni tuweze kupata faida ya kilimo chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, ni suala la ununuzi wa ndege ya cargo ambayo tumeipokea juzi na Mheshimiwa Rais ametuongeza, tunapongeza sana. Maana yake ni kwamba leo tunakuwa na uwezo wa ku–export moja kwa moja mazao ya mbogamboga mpaka na mazao ya matunda ikiwepo parachichi ambayo inatakiwa sana duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili tumekuwa na mpango mzuri wa mazao ya mbogamboga horticulture katika maeneo yetu. Wizara ya Kilimo ina mpango mzuri kwa upande wa horticulture. Tunaomba sana sana kumekuwa na changamoto ya vifaa vya kuhifadhia mbogamboga pamoja na matunda. Tumekuwa na hizi cold rooms kwa maana ya tracks hizi ambazo zinasafirisha mazao yetu ili yasiharibike, lakini tumekuwa pia na cold rooms equipment’s ambazo zinatakiwa katika maeneo ya mashamba ya wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Serikali na Mheshimiwa Waziri aje na mpango wa kuondoa angalau ushuru au kodi ili kuingiza vile vifaa ambavyo vinaenda ku–support kilimo cha mbogamboga katika maeneo yetu kwa sababu vile vifaa ni vya gharama kubwa. Wananchi wengi hawawezi wenye mashamba ambao wamejitahidi kuingia kwenye jambo hili na ili wawekezaji ambao wameamua ku–support na ile ndege ili ipate mzigo mkubwa wa kupeleka nje ya nchi, tuweze kuuza na kupata fedha za kigeni ili fedha za kigeni zije zisaidie hapa nchini, niombe sana Mheshimiwa Waziri afanye hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri akiweza kufanya hivyo atasaidia kilimo cha wananchi wetu ambao wameamua kujiwekeza kwenye eneo hili, lakini hii ndege ambayo tumeinunua itakuwa na maana kubwa ya kuhakikisha tunasafirisha mzigo kwa maana ya mzigo mkubwa kwenda nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, ni suala la ushirikishwaji wa sekta binafsi katika ukuaji wa uchumi. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Miundombinu na naomba niseme wazi, nimekuwa nikiongea mara tatu hapa katika suala la bandari kwa muda mwingi sana. Niombe sana, eneo hili la bandari, bandari ndiyo kioo chetu. Kumekuwa na kauli mbalimbali na nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu jana ametoa kauli nzuri sana kuhusiana na bandari, mawazo tutaendelea kuyachukua, hatutarudi nyuma tunataka tuwekeze ili tuongeze pato la Taifa, kusiwe na upotoshaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili kuna makundi manne ambayo yanatukwamisha. Kundi la kwanza ni suala la wapinzani wetu kutaka kutuzuia tusiendelee. La pili, ni wafanyabiashara wasio waaminifu wameingilia mchakato huu ili wao waendelee kufaidika na udhaifu wa bandari yetu. Watu wa tatu ni baadhi ya wafanyakazi wa TPA na wa TRA wanaofaidika na mfumo huu mbaya wa kuendesha bandari yetu na watu wa nne ni bandari shindani zilizoko katika ukanda huu ambazo hazipendi sisi tufanikiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hao DP World ni wana uwezo mkubwa sana. Niombe sana tuendelee kuwaza kwamba nchi hii haitauza bandari, bandari ni ya Watanzania, Mheshimiwa Rais ameshasema tuondelee hofu kwa sababu hatuna sababu ya kuogopa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, hofu hii ipo niongee hili neno dogo tu. Tulikuwa na stendi yetu pale Mnazi mmoja Kisutu, stendi ya Wananchi wa Dar es salaam waliandamana kwa sababu inapelekwa Ubungo wakasema ni mbali sana, wakaenda, tukaenda kujenga stendi Ubungo, leo Ubungo imeonekana ni mjini katikati, lakini leo tunavyoongea stendi iko wapi? Iko Mbezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi waondoe hofu nia yetu ni njema twende kuiunga mkono Serikali ili iongeze mapato kwa ajili ya maendeleo ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja ili iweze kupitisha bajeti hii ikalete maendeleo ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunifanya niwe wa kwanza kuchangia hoja iliyoko mbele yetu na kwa hakika inawezekana ni baraka za Mheshimiwa Shekilindi kwa namna ambavyo amekuwa ni mtu mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kutujalia uzima na afya kukutana na leo, lakini pili nichukue nafasi hii sauti yangu sio nzuri sana, lakini nitajitahidi hivyo hivyo.

Namshukuru sana Mheshimiwa Rais na kumpongeza kwa kazi nzuri anayofanya kuliongoza Taifa letu hasa kwenye sekta hii ya utalii tunamshukuru sana kwa namna alivyojitoa kimasomaso, kuhakikisha kwamba anatangaza vivutio vyetu kupitia The Royal Tour ambayo kwa kweli sisi tunaona ina maana kubwa sana kama nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, The Royal Tour imeenda kuzinduliwa katika sehemu ambayo watu hawavijui vivutio vyetu, imeenda kuzinduliwa katika nchi za Ulaya. Nina amini kabisa wale ambao walishiriki na kuona vivutio vile leo tunaanza kuona matokeo yake. (Makofi)

Kwa hiyo, yule ambaye anaenda kupinga au ku-criticize suala la Royal Tour huyo ajui mambo ya utalii tumuache. Kuna nchi zimefanya kazi kubwa ya kufanya promotion ya vivutio vyao, sisi tumefanya kwa kiasi, lakini mkuu wa nchi alivyoingia na kufanya jambo hili limetupa heshima kubwa sana duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii ile filamu kila mtu akiangalia anajua kabisa anatoka Ulaya anakwenda kuona Serengeti, anakwenda kuona Mlima Kilimanjaro, anaenda kuona vivutio mbalimbali ambavyo ni vya kipekee katika nchi yetu. Kwa hiyo, sisi Watanzania tuendelee kumuunga mkono Mheshimiwa Rais, Wizara kazi aliyoifanya Mheshimiwa Rais muendelee kui-brand vizuri, tusiibeze na tusiiache kazi hii ni kubwa ina heshima kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kiongozi wa nchi kuacha kazi zake na kuingia kufanya kazi ya sekta ni jambo kubwa na la kupigiwa mfano. Kwa hiyo mimi nilitaka nianze na hili kumpongeza sana na kuhakikisha kwamba tunafanya hivyo, matokeo tumeanza kuyaona, tumeanza kuona watu wengi wanaanza kuingia nchini kwetu kwa ajili ya kuja kuanza kuangalia vivutio vyetu, hilo nataka nisema kama la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili nimpongeze sana dada yangu Mheshimiwa Waziri Pindi Chana...

MHE. RAMADHAN SULEIMAN RAMADHAN Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

TAARIFA

MHE. RAMADHAN SULEIMAN RAMADHAN: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe taarifa mzungumzaji kwamba huu muda tunaongea mchezaji aliyekuwa wa Manchester United ambaye sasa hivi anacheza PSG ya Ufaransa Ander Herrera yuko Serengeti na matokeo ni Royal Tour. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Haya, Mheshimiwa Mtaturu.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, napokea kwa heshima kabisa hayo ndio matokeo ya Royal Tour ambayo tumeifanya, sasa katika hili nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri dada yangu Pindi Chana kwa kupewa heshima kubwa ya kuongoza sekta hii. Tunakujua wewe ni mtu ambaye unajua namna ya kufanya kazi hii nzuri ya kuweza kwenye eneo la diplomasia ulifanya vizuri, lakini eneo hili ninaamini utafanya vizuri zaidi ukisaidiana na mwenzako Naibu Waziri dada yangu Mary Masanja pamoja na Katibu Mkuu na wote katika wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaamini kabisa tutaendelea kuwapa support kuhakikisha kwamba lengo la nchi yetu kufikisha watalii milioni tano kufika mwaka huu wa fedha tunapoenda kwa sababu ilani yetu ya uchaguzi imeeleza wazi kwamba lengo letu tufikishe watalii milioni tano, hatuwezi kufikisha milioni tano bila kutangaza vivutio ambavyo tunavyo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo nilitaka nishauri mambo machache ya kuweza kuongeza chachu katika eneo hili. La kwanza kumekuwa kweli kuna tozo mbalimbali zinatozwa, kumekuwa na kelele huko nyuma kwamba watoa huduma ambao ni wenzetu ambao walikuwa wanafanya kazi hii wamekuwa wakilalamikia baadhi ya tozo, niipongeze sana Serikali kuna baadhi ya tozo zimeondolewa, leo hii kuna baadhi ya watoa huduma wameanza kufaidika na kazi hiyo nzuri ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini bado tunawaomba mkae na watoa huduma hawa ambao wanafanya kazi nzuri sana ya kuhakikisha inaleta na kusimamia na kuwaleta watalii. Lakini eneo hili wanaomba sana mtawanyiko wa maofisi ya kwenda kulipa tozo walipe TARA, waende halmashauri waende wapi imekuwa ikiwapotezea muda wanaomba wawe na dirisha moja la kuweza kulipa tozo zote wasipoteze muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tozo zinaweza karibia 50 ukasema siku tatu/nne unashughulikia tu kulipa mgeni mmoja inapoteza muda na itatuchelewesha sana kufikia lengo la kupata watalii wengi. (Makofi)

Lakini la pili ni suala la VAT; VAT kweli hamna anayekataa kulipa lakini kumekuwa na tatizo la kulipa VAT on deposit, anapolipa mgeni kule nje analipa moja kwa moja kwa yule mtoa huduma, mtoa huduma yule anakuwa anakatwa palepale VAT, ikitokea huyu mtalii ame-cancel safari yake ile VAT analipa huyu mwenzetu wa Tanzania, maana yake ni kwamba anaingia hasara na inatia hasara kampuni yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe sana hizi fedha zilipwe pale kwenye deposit, lakini waje kwenye maeneo ya tozo mbalimbali hiyo itakuwa umemtendea haki huyu mtoa huduma, lakini pia itakuwa ni halisia, unaweza kujikuuta unalipisha VAT mara mbili, mara tatu kitu wanachofanya destination ya Tanzania inakuwa ghali kuliko eneo lolote. Hii nayo itakuwa kikwazo kwa ajili ya kuhakikisha kwamba hatupati watalii wa kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la tatu ni suala la viza wamekuwa wakilalamika kwamba viza yetu wanapolipia online kumekuwa na ucheleweshaji iko slow sana yuko kule anataka alipie viza ili apate ruhusa ya kukata tiketi anashindwa. Kwa hiyo matokeo yake ana-cancel safari anashindwa na ameamua kutafuta eneo lingine, hili nalo ni kikwazo kingine naomba mkalifanyie kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho ni suala la wanyama hawa wavamizi kama tembo, mimi naomba nitoe pole sana kwa wananchi wangu wa Ikungi, Singida Mashariki kwenye Kijjiji cha Ntewa pale Ntuntu, juzi mtoto wa miaka miwili na nusu alikanyagwa na tembo. Eneo la Ikungi ni mbali sana na hifadhi leo hii tunaongea habari ya Ikungi sasa tunaanza kuwa na uvamizi wa tembo, lakini mnatuambia tembo wako karibu 60,000 mnasema ni tembo wachache, je, wakifika laki moja, mbili hawa tembo itakuwaje nchi hii? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima wenzetu wataalam wa Wizara hii wakae wasiwe wanatuletea story iliyozoeleka ya corridor/mapito ya tembo ya miaka, leo hii watu wengi wanaumia wanakufa mali zao zinaharibiwa kwa sababu tu tembo wanazunguka kila mahali. Inawezekana kuna mazao wanahitaji kula majani fulani, inawezekana maji hakuna maeneo ya hifadhi, basi wataalam wetu watumike kupanda hata miti au mazao yanayohitajika ndani ya hifadhi ili tembo wasitoke kuja mtaani.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama haitoshi kama maji ni machache kule kwenye hifadhi, wachimbe mabwawa ya kutosha hiyo ndio maana ya kusema kuwepo kwa professional tuna wataalam wengi katika Wizara hii, tunawaamini, hebu nendeni mkakae mnapofanya utafiti fanyeni na eneo hili tusibaki kupeana story kwamba ohh haya ni mapito ya tembo miaka yote inapita, najiuliza kule Ntuntu mapito ni lini walikuwa wanaenda wapi hawa tembo, tembo wamekaa wiki nzima/wiki mbili wanafanya wananchi washindwe kufanya shughuli zao za kawaida. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tutajikuta kwamba tunawahamasisha wananchi wafanye kazi, lakini hawezi kufanya kazi kwa sababu kuna tatizo la tembo wanazunguka nani hatari kwa maisha ya wananchi. (Makofi)

Kwa hiyo, nilitaka niombe sana anapokuja waziri hapa atueleze mkakati ni upi wa kitaalam, sio hoja hii ya kila siku imekuwa kama msamiati ambao haueleweki haya ni mapito, sijui ni corridor, sijui lugha zingine zinawasumbua wananchi hawajui.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana kazi nzuri mnayoifanya lakini eneo hili linatutia doa kama Taifa twendeni tukafanye kazi kwa pamoja. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja iliyopo mezani kwetu ambayo ni hoja ya Bajeti Kuu ya Serikali mwaka 2022/2023. Nianze kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutujalia uzima na kukutana asubuhi ya leo. Pili, nichukue nafasi hii kwa dhati kabisa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya katika kuiletea nchi yetu maendeleo. Tumeona kwa vitendo mambo mbalimbali ambayo yanajitokeza baada ya kuwa yeye ametoa kauli na kuonyesha utashi wake wa kweli katika kuiletea Tanzania maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata leo hii bajeti ambayo imesomwa na kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, Waziri wa Fedha imeonyesha wazi maono yake, imeonyesha wazi dhamira yake na imeonyesha wazi namna ambavyo anaitekeleza vizuri Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuwa nimetoa shukrani kwa Mheshimiwa Rais, sasa nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri mtoa hoja, kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba kwa kazi nzuri aliyoifanya kutuletea hoja hii ambayo imeonyesha wazi bajeti hii itakwenda kuondoa maumivu yaliyokuwepo kwa wananchi. Bajeti hii imegusa nyanja mbalimbali za kimaendeleo, bajeti hii imegusa sekta zote kwa umakini mkubwa, lakini zaidi imeonyesha waziwazi kwamba imeenda kumgusa mnyonge chini kabisa pale. Kwa hiyo, naamini kabisa kama bajeti hii itaenda kufanyiwa kazi itaenda kuleta mabadiliko na kufanya mapinduzi makubwa ya uchumi wa nchi yetu. Hongera sana kwa Mheshimiwa Waziri pamoja na wasaidizi wake ndugu yangu Mheshimiwa Chande na Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kushukuru sana, nimeona kwenye bajeti hii pamoja na bajeti za kisekta ambazo tumekuwa tumepitisha, tumeona katika Jimbo langu, Wilaya yangu ya Ikungi tumeona namna ambavyo tumepata mgao wa fedha, tumepata mgao kwenye maeneo ya afya, maji, elimu huduma mbalimbali za kijamii zinaenda kuguswa, lakini kama haitoshi tumeona namna ambavyo miundombinu ya barabara itaenda kuletewa fedha kwa ajili ya kutengeneza lami katika maeneo ya Mji wa Ikungi ambapo tunapata kilometa mbili, zitaenda kujengwa pamoja na taa zitawaka katika mji wetu. Hii italeta mabadiliko makubwa sana, hivyo, tunaishukuru Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru kwa namna ambavyo imeamua sasa kujenga barabara ile ya Singida - Kwa Mtoro – Ugashi - Tanga ambayo imekuwa tukisemea kwa muda mrefu. Kilometa 462 zikienda kujengwa itaenda kuchachua uchumi wa wananchi wetu na tutaona maendeleo ya haraka yatapatikana. Tumekuwa tukisema Bungeni na leo nashukuru Mheshimiwa Waziri ameitaja barabara hii, tunaamini wananchi wanaisubiri na tunaomba sana mchakato ufanywe mapema, tupate mkandarasi ili barabara iende kufanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kueleza hayo, naomba niende kwenye eneo ambalo nimesoma katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri, eneo la ukuzaji wa uchumi. Eneo hili tumeelezwa vizuri mpango wa Serikali namna ambavyo tutakuza uchumi, lakini tumeelezwa kwamba ukuaji wa uchumi wanategemea mpaka mwakani 2023 tutafikia wastani wa ukuaji wa pato la Taifa kwa asilimia 5.3, wakati huo wastani wa Ilani wa CCM inasema asilimia 6.9. Kama Serikali ikiangalia vizuri tumekuwa tunapanda kwa taratibu sana kwa sababu kuna baadhi ya vyanzo vya mapato hatujaviangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nitazungumzia sana sekta ya uchumi wa makaa ya mawe pamoja na chuma kilichopo kule Ludewa. Tumekuwa na changamoto kubwa ya kuwa tunatamka lakini hatuchukui hatua. Eneo hili tumekuwa tukilizungumza kwa miaka mingi, lakini leo tutaangalia kwamba kwenye Ilani ya CCM imeeleza wazi kwamba mapinduzi ya uchumi kwa maendeleo ya watu, Ibara ile ya 17, imeelekeza waziwazi kwamba kutumia rasilimali za Taifa kwa ajili ya maendeleo na manufaa ya Watanzania. Leo hii tunavyoongea makaa yale yalioko pale Ludewa hatujayachimba, leo tunavyozungumza tunazo leseni tulizowapa NDC ambao wamepewa leseni zipatazo nane, lakini wamezishikilia tu, hawajawahi kufanya utafiti, hawajawahi kuchimba, mali iko pale ardhini haijawahi kuguswa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo ukienda utasikitika, Kamati yetu ilifika kule, imeona namna ambavyo yale makaa ya mawe huhitaji kuchimba wala kutumia nguvu kubwa. Unachukua chepe tu, unachimba, unachukua yale makaa ya mawe unaenda kuuza. Hayahitaji kutumia fedha nyingi. Leo hatujaweza kuyachimba, hivi ninavyoongea, NDC wamepewa leseni nane kama nilivyosema, PL 6986 ya mwaka 2012, PL 6710 ya mwaka 2010, PL 10263 ya mwaka 2014 pamoja na ya 2015, zote hizi hazijawahi kuchimbwa mpaka leo.

Mheshimiwa Spika, leo hii kwa sababu ni kampuni ya Serikali, ni vizuri waruhusu sekta binafsi waingie kwenye uchimbaji wa madini haya ambayo kimsingi wataenda kwa kasi kwa sababu wao wanaangalia faida. Inawezekana hawa NDC kwa kuwa wao ni Serikali hawaoni manufaa sana na hawaoni haja hiyo kwa sababu haiko kwenye mipango yake, lakini kama tunataka kuangalia chanzo cha uhakika, lazima tuangalie namna ya kuchimba ile chuma, namna ambavyo tutachimba yale makaa ya mawe ambayo kimsingi yataenda kuleta kwa sababu yana soko nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama haitoshi, tutaunganisha na namna ambavyo tutakuza bandari hii ya Mtwara. Bandari ya Mtwara itapata mzigo wa kutosha kupeleka nje. Tumeanza kuona saivi kuna meli zinaondoka zinakwenda India kutokea Bandari ya Mtwara. Kwa hiyo, uwekezaji wa Bandari ya Mtwara kama tutaweza kupeleka mzigo wa kutosha, utakuwa na maana na utarudisha fedha ambazo Serikali imewekeza. Kwa hiyo, niombe sana, eneo hili waliangalie kwa makini ili waweze kuona namna ambayo tutaongeza pato la Taifa ambalo kimsingi kwetu ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo hili niwaombe, kuna barabara ya kutoka pale Njombe kwenda mpaka Manda Ludewa. Barabara ina kilomita 210, Serikali imeanza kujenga kilomita 50 kwa kutumia concreate, leo hii wameshajenga kilomita kama 30 na kitu hivi. Kwa hiyo, niombe sana, kilomita zilizobaki ziweze kujengwa kwa sababu kutakuwa na movement kubwa ya magari ambayo yatakuwa yanatoka kule kwa ajili ya kupeleka kwenye Bandari zetu za Tanga na eneo lingine. Kwa hiyo, eneo hili tukilifanyia kazi vizuri, tutafikia lengo ambalo liko mbele yetu la kukuza uchumi na kuongeza pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili niongelee sekta ya utalii. Utalii ndiyo unatuingizia fedha nyingi kuliko sekta yoyote katika nchi yetu. Utalii huu ambao tumepewa kama tunu na Mwenyezi Mungu, lazima tulinde rasilimali tulizonazo na vivutio ambavyo tunavyo. Mheshimiwa Rais amefanya kazi nzuri ya kutangaza vivutio vyetu kupitia royal tour. Tunaona matokeo yake, watu wanakuja kuona. Hivi leo hii tukitangaza vivutio ambavyo kesho havipo, inakuwa haina maana hata juhudi zote za kutangaza vivutio hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii tunasema wote kwa pamoja, utalii unatuingizia fedha. Tunawavutia watalii waje waone, hivi wakialikwa, wakaja kukuta vivutio vimekwisha itakuwa na maana gani? Niombe sana Serikali ijikite katika kulinda rasilimali zetu. Isiache watu wachache ambao hawana nia njema wakaharibu vivutio vyetu, kwa sababu tu ya lengo, wengine wanakuja na sababu ndogo tu, kwamba Serikali inajali wanyama kuliko wananchi, si kweli. Wote wanaishi nchi hii, lazima tuwe na vipaumbele, tulinde vivutio na huku tunalinda na binadamu, ndiyo maana wanapewa huduma. Hatuwezi kuruhusu hali hii kwa sababu eti kuna watu fulani wataona wanaonewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Pori la Loliondo lilianzishwa mwaka 1951. Mpaka leo kama ingekuwa hatujatunza vizuri, maana yake leo hii tungekuwa hatuna vivutio hivyo. Hatuwezi kuacha watu wachache wakatuharibia, tena bahati mbaya wanatumika na nchi zingine kuharibu kwa sababu ya ushindani wa utalii. Niombe sana Serikali iwe makini kuhakikisha inalinda ili tuendelee kuwa na hali hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tusipoangalia hili jambo, tutaanza kuingia kwenye huruma ambazo nyingine hazina sababu, wengine wana ajenda zao na kwa hakika leo hii pori lile lilikuwa na ukubwa wa kilomita za mraba 4,000. Serikali imepunguza 2,500 imewaachia kule wananchi waweze kufanya shughuli. 1,500 ambayo ni chanzo cha ikolojia ya kulinda kule Serengeti ambayo tunasifiwa leo, ni mbuga ambayo inasifika duniani. Watu wengi wanataka kuja kuona pale Serengeti, leo hii tukiua ile, ikolojia ile ya kutunza wale wanyama, nyumbu wanapita kila mwaka kwenda pale wanazaliana. Nyumbu zaidi ya 600,000 wa ndama wanapatikana pale, kupitia ikolojia hii ya njia hiyo. Leo hii tukiacha pale, vyanzo vya maji ambavyo vinapatikana kwenda kutunza kule Serengeti vinapitia pale Loliondo. Leo hii tukianza kuja na sababu ndogo ndogo tu, nyingine hazina mashiko, hatutafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi ni kubwa, kama kunaonekana watu eneo lile hawana sehemu nzuri ni ukame na nini, wapatiwe eneo lingine la kwenda kuishi, Tanzania bado ni kubwa. Ardhi hii iko chini ya Mheshimiwa Rais. Aruhusu waende popote, waweze kuacha eneo lile liweze kulindwa na liweze kuhifadhiwa na tuweze kuendelea kupata utalii kama ambavyo tumeendelea kulinda katika miaka yote, toka mwaka 1951.

Mheshimiwa Spika, sekta ya utalii bado sisi tunaendelea kuona kama ndiyo mboni ya jicho letu. Serikali isisite, ichukue hatua, isimamie na wale waliopewa kazi hii ya kuhifadhi, wafanye kazi yao kwa mujibu wa sheria. Eneo hili naomba sana kama kuna watu ambao wanafanya tofauti na haki za binadamu, wachukuliwe kama wao siyo ionekane kama Serikali nzima haijatenda haki kwa wananchi wale. Kwa hiyo, nilitaka nieleze eneo hili ili tukuze uchumi wetu. Zaidi naomba nirudie tena kushukuru sana na kuipongeza Serikali kwa kuleta bajeti ambayo leo inaenda kutuheshimisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kunipa nafasi ya kuweza kuchangia hotuba ya bajeti ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ambayo ipo mbele yetu.

Kwanza, nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kutujalia uzima na kuweza kuwepo hapa leo asubuhi kwa ajili ya kutoa mchango katika maendeleo ya Taifa letu. Pili, nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kuanza vizuri na kutoa mwelekeo wa Taifa letu ambalo, hivi karibuni tumeondokewa na Rais wetu mpendwa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, mwanamapinduzi wa kweli, mzalendo na anayeipenda nchi yake. Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahala pema peponi.

WABUNGE FULANI: Amina.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa wasilisho lake aliotoa jana, lakini nimpongeze yeye pamoja na wasaidizi wake wote kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kuratibu shughuli za Serikali. Kama ambavyo tunajua wao ndio waratibu wa shughuli za Serikali, kwa ujumla wake Wizara zote wanazisimamia wao. Nimpongeze sana mama yangu Jenista Mhagama pamoja na Manaibu Waziri ambao wako katika ofisi hiyo kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizo nichukue nafasi hii kupongeza kwa kazi kubwa iliyofanyika katika kipindi kilichopita. Taarifa tuliyosomewa hapa na Mheshimiwa Waziri Mkuu inaonyesha wazi kwamba Serikali ina dhamira ya dhati katika kuleta maendeleo ya nchi yetu. Tumeona huduma za kijamii ambazo zimetajwa hapa zimefanyika katika kipindi kilichopita. Tumeona pia barabara kwa maana ya miundombinu lakini pia tumeona katika maeneo ya elimu, umeme, pamoja na usafirishaji ikiwemo na utalii kazi imefanyika kubwa katika kuhakikisha kwamba Tanzania inasonga mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo haya ni pamoja na miradi ya kielelezo, miradi mikubwa ambayo imeanzishwa katika kipindi kilichopita ikiwemo SGR, ununuzi wa ndege, uboreshaji wa shirika letu pamoja na umeme wa Mto Rufiji. Kwa hakika hii ni misingi mikubwa ya kuleta maendeleo katika nchi yetu. Uchumi wetu lazima uimarishwe kupitia mambo kama hayo makubwa.

Kwa hiyo, leo hii ukisikia mtu anabeza juhudi zilizofanya na Serikali katika muda huu, mtu huyo hajui maana ya maendeleo. Watu hao sometimes utakuta wanalalamika kwamba Serikali haijaweka mipango mizuri, tukija kutekeleza wao wanarudi wanageuka kuanza kuilaumu Serikali. Naomba nimwombe Waziri Mkuu tusonge mbele na kama alivyotuambia jana miradi yote itekelezwe iliyoanzishwa na Serikali ambayo inaweza kuleta matumaini makubwa katika maendeleo ya nchi yetu, tusirudi nyumba kwa sababu tumejipanga vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunajivunia tumefikia uchumi wa kati au kufika uchumi wa kati bila kuweka mipango kama hii. Leo hii tunapunguza gharama za usafirishaji kwa kujenga barabara nzuri. Leo tunahakikisha tuna shirika letu wenyewe la ndege, tunaambiwa sasa zitafika kumi na mbili ni shirika au nchi itakuwa na uwezo wa kuwa na usafirishaji na kuvutia watalii katika nchi yetu, mwisho wa siku tutaweza kuongeza fedha za kigeni na kuweza kuongeza uwezo wa Serikali kuhudumia wananchi wake. Kwenye hili nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na naomba niseme sisi Wabunge tuunge mkono Serikali yetu katika kazi nzuri inayofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikieleza hivi hayo ni maono ya viongozi wetu, lakini maoni ya viongozi wetu pia yanasimamiwa na Ilani bora kabisa ya Chama Cha Mapinduzi ambayo imepanga mipango na imetafsiriwa vizuri sana katika Dira ya Maendeleo pamoja na Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano. Kwa hiyo, niseme tu kwamba maendeleo haya yanayofanyika yanaenda kulenga kumkomboa Mtanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika maendeleo haya yaliyofanyika huwezi kuondoa viongozi walioshiriki kwa muda wao katika kuhakikisha kwamba wanaisaidia nchi hii. Legacy ambayo imewekwa katika nchi hii, Mwenyezi Mungu amemtanguliza mbele ya haki Rais wetu Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, hatutamsahau kwa kazi kubwa aliyofanya katika nchi yetu. Ndio maana kama Bunge tuliazimia kwa pamoja kumpongeza na kutambua juhudi zake. Kutambua juhudi za Hayati Dkt. John Pombe Magufuli ni kuwafanya akina Dkt. John Pombe Maguguli wengine waendelee kufanya kazi kama aliyofanya yeye. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo sisi tuwe na wivu wa kuona mtu aliyefanya kazi vizuri; mapungufu madogo madogo kila mmoja hapa ana yake, inawezekana, lakini kwa yale mengi aliyofanya mazuri lazima tumuenzi na kumpongeza sana na kumuunga mkono katika mambo haya. Mfano mdogo, alikuwa ni jasiri katika kupambana na vita ya majangili wa tembo, wote tuajua, miaka ya nyuma tulikuwa na tatizo kubwa la majangili wa tembo. Tulifikia tulikuwa na tembo karibu 100,009 miaka ya nyuma ya 2014, lakini leo tembo walipungua mpaka kufika 43,000, lakini leo kwa sababu ya kazi nzuri iliyofanywa na wenzetu wa maliasili, tunafikisha tembo 60,000 katika nchi yetu. Maana yake nini? Maana yake ni kwamba tumeweza kusimamia vizuri kazi ambayo tumeachiwa rasilimali au maliasili tuliyoachiwa katika nchi yetu. Kwa hiyo, niwaombe sana twende kifua mbele, kazi inayofanyika ni nzuri, tusibabaishwe na kelele za pembeni, sisi tumejipanga vizuri kuhakikisha Tanzania inakwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hili la utalii mafanikio yake yameonekana, leo hii tunavyoongea hapa tumeongeza kuvutia watalii. Mwaka 2015 watalii 1,137,000 mpaka kufikia 2019 tumeongeza watalii, wamefika 1,527,000; maana yake ni kwamba kupitia hivi vituo vyetu tumeongeza watalii kiasi hicho, kuja katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya hapo tumeongeza fedha kama ambavyo ametuambia Mheshimiwa Waziri Mkuu, kufikia mwaka 2015 tuliongeza fedha dola bilioni 1.9 ziliongezwa katika utalii, lakini kufikia mwaka 2019 tuliongeza fedha za kigeni bilioni 2.6 ambazo zinakwenda kuongeza uwezo wa Serikali wa kutoa huduma za kijamii katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hii ni kubwa ni nzuri, niwaombe sana wenzetu wa maliasili, Tanzania lazima tuongeze nguvu katika maliasili kwa sababu ndipo tunapopata fedha nyingi za kigeni. Leo hii Simba wamesema visit Tanzania, naomba niongeze tena, niseme visit Tanzania, the land of Kilimanjaro, Serengeti and Zanzibar ili iweze kuvutia zaidi tunapokwenda kwenye ile robo fainali ili dunia nzima ione kwamba tuna vivutio vikubwa vya Serengeti na Zanzibar ni sehemu nzuri ya kupumzika pamoja na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kupongeza kazi nzuri iliyofanyika, lakini naomba nikuhakikishie kwamba Watanzania wanajua kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya CCM pamoja na viongozi wake. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti iliyoko mbele yetu ya Wizara yetu ya Maji. Nianze kwa kumpongeza sana Waziri pamoja na wasaidizi wake wote kwa kazi nzuri wanayofanya lakini kwa bajeti nzuri waliyotuwasilishia hapa mezani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme wazi kabisa Mheshimiwa Aweso toka akiwa Naibu Waziri wa Wizara hii ali-perform vizuri sana na ndiyo maana Mheshimiwa Rais akaamua kumpa Uwaziri kamili. Tuendelee kupongeza na niwatie moyo vijana wengine waendelee kuiga mfano wa aina ya Mawaziri kama akina Aweso, unafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kusema kwamba Ilani yetu ya Uchaguzi, ukurasa ule wa 7, Ibara ya 9(d)(i) inaeleza wazi kwamba katika miaka mitano tutaongeza nguvu katika upatikanaji wa maji vijijini na mijini. Katika taarifa yake aliyotusomea hapa kwa sasa kwa vijijini tumefikia asilimia 85 na kwa mijini tumefikia asilimia 95.

Mheshimwa Spika, kasi inatakiwa iendelee kuongezeka katika kuwekeza Zaidi, najua kazi kubwa imefanyika. Mimi nina ushahidi katika jimbo langu au Wilaya yetu ya Ikungi tuliweza kupata jumla ya shilingi bilioni 3.7 katika mwaka uliopita na hata sasa tumeangalia pale wametutengea fedha naona safari hii kidogo wametuminya sana kwa wilaya nzima kwa majimbo yote mawili tumepata shilingi bilioni 1.7. Kwa shida ya maji tuliyonayo katika wilaya yetu, bado tuko chini sana, naamini kunahitajika juhudi kubwa kuongeza fedha kwa ajili ya kuwekeza zaidi.

Mheshimiwa Spika, nipongeze kwamba katika shilingi bilioni mbili 2 ambazo tulipata tumeweza kupata maji katika Vijiji vya Kipumbuiko, Kinku pamoja na Lihwa, hivi


ninavyoongea wananchi wanapata maji. Hata hivyo, ndiyo kama wanavyosema wenyewe kwamba tuendelee kula mtori nyama iko chini basi tunaendelea kuamini kwamba katika muda ujao tutaendelea kupata zaidi kwa sababu Vijiji vile vya Mkunguwakiendo, Sakamwau navyo vitapata fedha kwa ajili ya kuongeza uwezekano wa upatikanaji wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu ni usimamizi wa miradi hii. Mradi hii tunawekeza fedha nyingi lakini tunaenda kuacha kwenye Kamati za Maji ambazo hazina uwezo kabisa wa kusimamia miradi. Unaenda kuwekeza zaidi ya shilingi milioni 700 kwenye mradi wa maji unakuta hawana uwezo kwa sababu hawana ujuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kumekuwa na upungufu mkubwa wa hawa mainjinia au ma-technician wanaosimamia miradi hii. Pia kumekuwa na urasimu, unakuta huyohuyo injinia au technician anaagizwa aje asaidie wananchi mradi, unaende pale wanaomba hela ya mafuta na kadhalika, ucheleweshaji ni mkubwa sana katika maeneo hayo. Kwa hiyo, unakuta mpaka wamefika mradi umeharibika kabisa. Kwa hiyo, niombe sana kufanyike marekebisho katika eneo hili. Kama tumewekeza fedha tujiandae kutunza miradi ambayo inapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naamini sheria iliyoanzisha Kamati za Maji ni jambo zuri la ushirikishaji lakini hawana uwezo, miradi mingi inakufa. Tunaweza kusema kwamba wanajipange kutengeneza koki tu lakini hata mhasibu tu hawana kwa sababu pale hakuna mtu mwenye professional ya accounts. Kuna mtu wa kawaida tu mama mmoja amewekwa pale ana mradi anausimamia wa shilingi bilioni 1 hana uwezo wa kuendesha mradi ule. Kwa hiyo, ombi langu kama Taifa tuangalie upya suala la usimamizi wa miradi ya maji ambayo tunawekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo hili la Ikungi sisi tulikuwa tumeomba tuwe na Mamlaka ya Maji Mjini. Tunaamini tukiwa na Mamlaka hiyo itatusaidia sisi kuwa na uwezo wa upatikanaji wa fedha zingine. Mchakato ulianza miaka miwili iliyopita, Waziri utakapokuja hapa uniambie ni lini sasa tutapata Mamlaka ya Maji Mjini Ikungi ili isaidie kuongeza uwezo wa kupata fedha kwa ajili kuongeza miradi hii. Hii itasaidia sana kuongeza kasi ya usimamizi wa maji.

Mheshimiwa Spika, mfano kama Wilaya ya Ikungi leo tunapata maji asilimia 52 tu maana yake tuko chini hata lengo la Ilani, hii ilikuwa kiwango cha mwaka 2000 leo ndiyo sisi tunakitaja kile kieneo pale, asilimia 52 kwa wilaya nzima kwa majimbo yote mawili. Maana yake ni kwamba tuko nyumba sana hata miaka mitano ikiisha kama hatutafanya juhudi za makusudi hatuwezi kuvuka. Maji ni muhimu na hayana mbadala, huwezi kunywa kitu kingine badala ya maji.

Mheshimiwa Spika, nimuombe sana Waziri anapokuja kuhitimisha atuambie kuhusu suala hili. Tuna tatizo la maji katika Vijiji vya Ntuntu, Tunataru, Mboho, Mwaru, Mahambe, Choda, Manjaru, Tumaini na Matongo, Inang’ana. Haya maeneo yote watu wanashiriki kunywa maji pamoja na mifugo, hii ni hatari sana hata kwenye afya zao. Kwa sababu Mheshimiwa Rais ana mpango wa kutua akina mama ndoo kichwani niombe sana juhudi ziongezeke katika eneo hili ili tusaidiane kuwasaidia wananachi hawa waweze kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili yake ni kujenga mabwawa kwa ajili ya unyweshaji wa mifugo. Sisi kule ni wafugaji naomba tuongeze uwezo wa kuchimba mabwawa ili angalau yapunguze tatizo la maji katika maeneo yetu. Mabwawa haya yakichimbwa yatasaidia sana kupunguza tatizo la maji kwa ajili ya kufulia au kunywesha mifugo ili maji machache yanayopatika yawe kwa ajili ya kunywa tu. Hii itasaidia sana kuondoa tatizo la maji katika maeneo yetu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Mtaturu.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, vinginevyo nirudie tena kukushushukuru sana, Wizara inafanya kazi nzuri lakini tunaomba tuongeze bidii katika maeneo haya.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunirejesha tena kwenye orodha yako. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutujalia uzima na kukutana leo katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuishukuru na kuipongeza sana hotuba nzuri ya Waziri wetu wa Ujenzi ambayo ameitoa hapa asubuhi, ambayo imeonyesha dira ya kuweza kuboresha miundombinu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze yeye pamoja na Manaibu Waziri, Makatibu Wakuu na watendaji wote wa Wizara hii ambao wanafanya kazi nzuri sana kusimamia shughuli za ujenzi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi wote tunakiri wazi kwamba miundombinu ya barabara reli na usafirishaji ni kiungo muhimu katika uchumi wa nchi yetu. Kwa hiyo, maana yake ni kwamba maendeleo ya nchi yetu yanategemea sana ujenzi katika miundombinu pamoja na usafirishaji. Tukifanikiwa kuimarisha ujenzi wa miundombinu katika nchi yetu tutaharakisha sana uchumi wa nchi yetu, ndio maana leo tunapopata nafasi ya kuchangia hapa tunatoa ushauri kwa Serikali yetu ili kuboresha namna bora ya kuweza kuongeza miundombinu katika maeneo yote ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali, imekuwa ikiongeza fedha mwaka hadi mwaka katika kuhakikisha kwamba tunaimarisha sana miundombinu. Ushahidi uko wazi, katika trend ya utoaji wa fedha imeonekana katika bajeti hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa pamoja na juhudi hizi, ninataka nieleze tu kwenye maeneo haya ya barabara kwa maana ya barabara zetu zinazojengwa. Tumekuwa na kikwazo, kumekuwa na utaratibu wa kwamba lazima GN itoke ndiyo ifanikishe ujenzi uanze.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo haya niwaombe sana Wizara, niwaombe Serikali waondoe urasimu wa ucheleweshaji wa GN kutoka. Hizi fedha ambazo tunasema leo zimetoka haziwezi kuanza kazi mpaka GN itoke. Imekuwa ni kikwazo maeneo mengi, wakandarasi wanakuwa wako tayari lakini wanazuiliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini muda mwingine mradi unakuwa labda una miaka miwili au mitatu. Katika muda wa mwaka mmoja ukiisha ule muda wa lot ya kwanza unakuta haiwezi kuendelea mpaka GN itoke tena, tunatangaza upya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana Serikali kwenye eneo hili, niendelee kushauri kwamba waongeze bidi katika eneo hili, inawezekana sisi wenyewe mawasiliano ndani ya Serikali tuweze kuongeza nguvu katika kutoa GN kwa wakati ili kuisaidia miradi hii iweze kutekelezwa kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto hii ya GN inakwenda sambamba pia na utoaji wa fedha za miradi. Tumekuwa tukipitisha hapa kwenye bajeti hizi za kila mwaka, lakini tumekuwa tunachelewa kutoa fedha. Lakini pia kuna wakandarasi ambao hawalipwi kwa wakati, wameshamaliza wamewasilisha zile certificates zao lakini bado hawalipwi kwa wakati. niiombe sana Wizara, niiombe Serikali wawalipe wakandarasi kwa wakati ili wawe na nguvu ya kuitekeleza miradi hii ambayo tunawapatia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili nitaongelea kwenye upande wa viwanja vya ndege. Viwanja vyetu vya ndege huko nyuma walikuwa wanajenga wenyewe Mamlaka ya Viwanja vya Ndege, kwa mujibu wa sheria walikuwa wao wanasimamia lakini pia wanafanya ujenzi. Lakini baadaye TANROADS walipewa jukumu hili la kujenga viwanja vya ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, sina tatizo kabisa na TANROADS, TANROADS ni wazuri sana kwenye maeneo ya runways, wanajenga vizuri kabisa. Lakini tuna changamoto


ya facilities nyingine katika viwanja vya ndege. Kwa hiyo, eneo hili limekuwa na utata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana Serikali ifikirie upya; wawarudishie Mamlaka ya Viwanja vya Ndege wajenge wenyewe viwanja vyao kwa sababu sheria inawafanya wao wasimamie viwanja. Ili wasimamie vizuri lazima wajenge wenyewe ikiwemo kuangalia facilities zinazotakiwa katika viwanja hivyo zikiwemo zile airport towers, lounges zile za kuweza kusimamia kwa ajili ya kuchukulia abiria. Kwa hiyo, nilitaka niseme hili Serikali iangalie upya maelekezo haya waliyokuwa wameyatoa huko awali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu upatikanaji wa fedha nimeeleza vizuri. Nieleze kukumbusha barabara muhimu sana za uchumi; barabara ya Singida – Kwa Mtoro – Kiberashi – Tanga ni barabara yenye kilometa 461. Barabara hii pamoja na kuwa sasa tutaitumia na ni barabara ya kihistoria, na ni barabara inayogusa mikoa minne, tunachoangalia kwenye randama hapa, tumetengewa sasa kilometa 20 badala ya 50 hata zilizotajwa mwanzoni. Barabara hii itachukua muda mrefu kuimaliza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu, ninaomba iongezewe fedha ili iweze kumalizika kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii imeongoza thamani sasa, inapita sambamba na bomba la mafuta linalotoka Tanga kwenda Hoima. Kwa hiyo kiulinzi na kiusalama barabara hii ni muhimu sana. Niombe barabara hii ijengwe kwa sababu imesubiri kwa muda mrefu kuunganisha mikoa hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama haitoshi, barabara ile ya Mkiwa – Itigi mpaka kwenda kule Rungwa kwenda mpaka Makongorosi. Barabara hii nayo imeshatajwa muda mrefu. Niiombe sana Serikali tutenge fedha barabara hii ikamilike ifungue fursa za uchumi katika mikoa yetu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo lile la Wilaya yangu pale Ikungi kuna barabara inaitwa Ikungi – Mang’onyi mpaka kule Kilimatinde. Barabara hii ni ya kiuchumi, kuna kampuni kubwa za madini zitalipa kodi. Niombe barabara hii iangaliwe namna ya kuwekewa lami ili iongeze fursa za uchumi katika eneo letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilidhani nikieleza suala la barabara kwa nguvu sana pia nikumbushe barabara ile ya wenzetu kule Kahama, barabara ya Bulyankulu – Kahama, kilometa 51. Nayo ni barabara muhimu sana ya uchumi ili nayo ikiwekwa lami kwa sababu kodi tunapata nyingi kupitia madini itasaidia kuongeza uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, niendelee kusema tena barabara ni muhimu, miundombinu ni muhimu, naomba Serikali iweze kujenga barabara za lami ili kukuza uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo, ninaunga mkono hoja iliyoko mbele yetu kwa asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti hii muhimu iliyopo mbele yetu ya Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Spika, wote tunakubaliana hapa kwamba kilimo ndiyo kimebeba uchumi wa nchi yetu. Asilimia 80 ya Watanzania wanafanya kilimo na kumekuwa na juhudi mbalimbali zinafanyika, naipongeza Serikali na katika hili juhudi inatakiwa kuongezeka na tumeendelea kushauri mara nyingi, nataka nishauri kwenye eneo moja kubwa sana la mbegu.

Mheshimiwa Spika, tusipokuwa na mbegu zenye tija hatuwezi kubadilisha kilimo chetu. Wananchi wataweka juhudi zao, muda wao, rasilimali zao lakini bado tutajikuta tunarudi nyuma, hatuwezi kwenda mbele. Kama hivi tunavyoambiwa wenzetu nchi nyingine wanalima eneo dogo lakini wanapata uzalishaji mkubwa ni kwa sababu ya utafiti mkubwa walioufanya kwenye mbegu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kama hiyo haitoshi kumekuwa na ruzuku inayotolewa kwa ajili ya mbegu. Nitajitika kwenye eneo la zao la alizeti. Leo hii tunalia wote hapa kwamba tuna tatizo kubwa la mafuta ya kula, Serikali inatumia fedha nyingi kwa ajili ya kuagiza mafuta ya kula wakati tuna ardhi ya kutosha na mazao mengi yanayoweza kutoa mbegu za mafuta. Mfano zao la alizeti, tumekuwa na mawazo mengi ya kuhakikisha kwamba tunaongeza uzalishaji, kuna baadhi ya mbegu zile za kienyeji unatoa magunia matatu kwenye heka, unapoteza muda mrefu sana kufanya kazi ambayo haina tija.

Mheshimiwa Spika, tumekuwa na mawazo ya mbegu mbalimbali ambao zimeendelea kufanyiwa utafiti kwenye maeneo yetu. Kwenye eneo hili nimeona kuna fedha zimetengwa kwa ajili ya kuongeza utafiti. Nimuombe Waziri tuongeze nguvu kwenye eneo hili, watafiti wetu wapo, vituo vyetu vipo viongezewe fedha za kutosha kwa ajili ya kuja na mbegu zenye uzalishaji wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano mdogo kumekuwa na mawazo ya kuwa na GMO, tunatakiwa kuwa makini sana kwenye kuingiza mbegu hizi. Kuna baadhi ya nchi ambazo ni ushahidi leo wanapata mbegu hizo za GMO asilimia 100 hawana mbegu zao za asili katika nchi yao. Niombe sana Serikali inapoamua kufanya haya iwe na uhakika na tunachoenda kukifanya.

Mheshimiwa Spika, lakini kama hiyo haitoshi kilimo cha umwagiliaji kipewe nafasi kubwa. Hekta hizi ambazo zinatengwa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji hazitoshi, hatuwezi kujitegemea kwa chakula. Katika eneo hili pia tuongeze wataalam wa kutosha kwenye Halmashauri zetu. Leo hii unaweza kusema unaweka skimu ya umwagiliaji unawakabidhi wakulima ambao wao wenyewe hawana uwezo wa kuendesha mradi ule, tunapoteza fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumesikia Tume ya Umwagiliaji inaboreshwa, niombe sana nguvu ziongezeke tuwaweke wataalam wale mpaka kwenye Halmashauri zetu ili waweze kusimamia kweli kilimo cha umwagiliaji. Kilimo cha umwagiliaji tukikifanya vizuri, maeneo mengine wamefanya vizuri kwenye eneo dogo tunapata uzalishaji mkubwa. Leo nchi yetu inapata mvua nyingi sana kila mwaka, tuna baadhi ya maeneo mpaka zinaharibu miundombinu, tumekuwa tunalalamika hapa barabara zetu zinaharibika ni kwa sababu ya mvua nyingi. Yale maji yanapotea yanakwenda baharini. Naombe sana Serikali iweke nguvu kwenye kuvuna maji ya mvua na tuwe na mabwawa ya kutosha kwenye maeneo yetu ambayo yatatumika kwenda kuwasaidia wakulima wetu wawe na kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni masoko ya mazao yanayopatikana, lazima tuwe na uwezo wa kuhakikisha kwamba mkulima anapolima ana uhakika anakwenda kuuza wapi. Mfano mdogo kwenye eneo la kilimo cha alizeti kuna baadhi ya maeneo kama Singida kule imeshuka kwa sababu kuna baadhi ya maeneo wakulima wanakopwa bado wapo shambani, watu wanakwenda kununua shambani bado mtu hajavuna. Maana yake ni kwamba anauza kwa bei ya kutupa, mkulima huyu mwakani hawezi kurudi kulima. Naomba Maafisa Biashara, Maafisa Mipango na Maafisa Kilimo kwenye Halmashauri zetu wasimamie vizuri suala la masoko ili kumfanya mkulima huyu afaidike na kilimo chake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba Maafisa Biashara, Maafisa Mipango kwenye Halmashauri zetu na Maafisa Kilimo wasimamie vizuri suala la masoko ili kumfanya mkulima huyu afaidike na kilimo chake. Tunaposema tuwe na usalama wa chakula kweli chakula, tutaendelea kuwa na uwezo wa kuhifadhi, lakini kuna mazao ya biashara tumesema hapa tuwe na kilimo biashara. Eneo dogo, tuweze kuwa na uzalishaji wa kutosha na mwisho wa siku mwananchi huyu tuweze kumkomboa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hili nilikuwa nataka niongee kidogo sana kwenye eneo la Benki yetu ya Kilimo. Leo tunaipigia chapuo, ni benki imepewa fedha isimamie, lakini masharti yale siyo rafiki kwa wakulima walioko vijijini. Mfano, mimi ninayo AMCOS moja pale kwangu Misughaa pale Ikungi, leo hii ile AMCOS wamekopeshwa shilingi milioni 85 tu. Leo ninavyoongea mimi na wewe, wale AMCOS kwa sababu tu msimu uliopita haukuwa na mvua ya kutosha, wamepelekwa TAKUKURU, wamepelekwa Mahakamani, ni kama vile ambavyo hapakuwa na mkataba. Usitegemee wakulima hao mwakani wakaenda tena kwenye Benki ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana, nitakukabidhi document hiyo Mheshimiwa Waziri ili uweze kufuatilia. Haiwezekani watu waliokuwa na mkataba wa makubaliano ya mkopo na walikubaliana kwamba watu wa bima wapo, wameshachukua ile nafasi ya bima halafu mwisho wa siku kwenye msimu wasipovuna vizuri wanapelekwa TAKUKURU, wanapelekwa Mahakamani, hakuna sababu. Huyu mkulima unamfanya aogope hata kwenda kukopa kwenye hiyo Benki ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, pamoja na juhudi zinazofanyika za kuongeza fedha, lakini kuna treatment siyo nzuri inafanywa na baadhi ya maeneo kwenye Benki yetu ya Kilimo, kwa sababu haimsaidii mkulima, inaenda kumnyonya zaidi na kumwondoa kwenye mawazo mazuri ya kukopa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndiyo tunaposema kwamba kuna baadhi ya benki hazina urafiki na wananchi wa kawaida. Basi hata hii Benki ya Kilimo ambayo Serikali imeweka fedha, tuwawekee mazingira mazuri wakulima wetu waweze kuwa na uwezo mkubwa wa kulima eneo kubwa, wawe na pembejeo za kutosha, wawe na vifaa ikiwemo matrekta ili kubadilisha kilimo chao kutoka kwenye kilimo kile cha kawaida. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa Miraji.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja, nawatakia kila la heri Wizara hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii muhimu ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Nianze kwa kuwapongeza sana Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa kazi nzuri, lakini pia kwa wasilisho lao ambalo wameliwasilisha mbele yetu. Wasilisho hili limeonesha mipango mizuri ambayo wanaipanga kwa ajili ya mwaka mmoja ujao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze pia Katibu Mkuu pamoja na Watendaji wote kwa kazi nzuri wanayoifanya kuratibu shughuli hizi. Wote tunajua kwamba sekta ya utalii ni miongoni mwa sekta zinazotupatia fedha nyingi sana katika mapato ya nchi. Kwa hiyo ni maana yake ni kwamba, tunapotoa ushauri hapa tunataka tuendelee kuwa na uhakika wa mapato hayo ili kuisaidia nchi katika maendeleo. Wengi wamenukuu taarifa yake asilimia 17 ile ya Pato la Taifa, lakini tunapata asilimia 25 ya fedha ya kigeni, ambazo kwa kweli ni fedha nyingi zinazotuimarisha katika kuleta huduma za wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa maeneo yangu nitasema pamoja na kuwa TANAPA, TTB, pamoja na wenzetu wa TAWA wanavyoratibu shughuli za utalii, lakini kuna wenzetu hawa wa sekta ya binafsi ambao ni tour operators, wanafanya kazi nzuri sana kusaidiana na Wizara. Ombi langu ni dogo tu kwamba, kuna baadhi ya mambo ambayo yanapaswa tuwawezeshe na kuwaimarisha ili waweze kufanya kazi nzuri kwa niaba ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kiukweli watu hao wanafanya kazi nzuri na Wabunge wengi wamesema hapa. Hivyo, changamoto zilizopo ni vizuri tukazitafutia ufumbuzi ili waweze kufanya kazi nzuri na kusaidiana na Serikali, kwa sababu wao wanakutana moja kwa moja na watalii, wao ndiyo mawakala wanaowaleta watalii katika nchi yetu. Baada ya sisi kutangaza kama nchi, wao ndiyo wanaratibu kule katika shughuli zao mbalimbali kwenye vivutio vyetu. Kwa hiyo, niombe Serikali wapate muda, wakae na na hao wenzetu, waweze kuwapa taarifa mbalimbali zinazohusiana na taarifa za watalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watalii hawa lazima tufikirie kwamba wao wanataka nini ili tuweze kuwatafutia kile wanachotaka, tusiwe tunaandaa sisi kwa utashi wetu. Ni sawasawa wewe una duka, stahili ya nguo fulani unauza unazozipenda wewe badala ya kutafuta nguo wanazopenda wateja. Kwa hiyo, hili ndiyo tatizo ambalo tunaliona liko mahali pale. Kwa hiyo niwaombe sana Wizara wakae na hawa tour operators waweze kuwaambia taste ya watalii wanaokuja nchini wanataka nini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kikwazo kimojawapo ni pale mfano Serengeti; wamekuwa wana limitation katika yale makambi, wamezuia kuwa na mahema 10, sheria inasema kuwe na mahema kumi, maana yake mnamlazimisha huyo tour operator aweze kuwa na kambi nyingi ambazo zinamwongezea mzigo. Kwa hiyo niombe sana angalau waongeze badala ya kuwa na hema kumi, ziwe hema 25 zisaidie kuwa na watali wengi katika eneo moja kwa ajili ya kusaidia kupunguza gharama ambazo wanaziingia hawa watalii ambao wanakuja kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niongelee tu kwamba wawe na mikataba, badala ya miaka mitatu basi waende hata minne na kuendelea ili wawasaidie kuwa na muda wa kutosha. Kama wachangiaji mbalimbali walivyosema leo limetokea tatizo la Covid-19 waweze ku-compensate gharama zao ambazo wamewekeza katika eneo hili, vinginevyo tutawafanya washindwe kuendelea kutusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu ambalo ni muhimu sana, Wizara wanajua katika sekta hii kuna tozo na kodi 20 ambazo ni nyingi sana, zinawaletea vikwazo wale wanaoendesha sekta ya utalii. Mfano mdogo, ukiangalia, kuna tozo nyingi ambazo zimekuwa ni kikwazo, ni vizuri wakaziangalia upya mfano kuna TALA, kuna Halmashauri, kuna COSOTA, kuna NEMC, OSHA, Fire, Land Rent, Property Tax na Swimming Pool License yaani zote analipa huyu ambaye anatakiwa kuja pale. Maana yake nini, unamfanya huyu mtu awe na mlolongo na utitiri mkubwa wa zile kodi ambazo zinawaletea matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri waangalie upya namna ambavyo wataweza kusaidia kupunguza gharama na mlolongo huu wa utitiri wa kodi, kwa sababu tunajua kwamba kodi inasaidia kuboresha maisha ya wananchi kweli, lakini ni vizuri watu walipe kodi kwa furaha ili kodi hii iwe endelevu kwa ajili ya kuipata kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, niongelee suala la sisi kujitangaza. Kuna mikutano mbalimbali, niiombe sana Wizara iweze kuhudhuria kwa ajili ya kutangaza vivutio vyetu katika dunia. Mfano, kuna wenzetu wa World Travel Market ambao ni WTM, tuendelee kwenda kule kwa ajili ya kupeleka taarifa zetu za vivutio katika nchi yetu ili kusaidia utalii wetu kuweza kutangazika duniani kote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo, naunga mkono hoja na naomba niwatakie kila kheri Wizara hii. Ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsate sana kwa kunipa nafasi ili nichangie hoja ambazo ziko mezani. Nitachangia zaidi kwenye Kamati ya Miundimbinu. Nianze tu kwa kuipongeza Serikali na Mheshimiwa Rais, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuijenga nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu nitaongelea zaidi kwenye upande wa miundombinu nitajikita sana kwenye ujenzi wa miundombinu ya barabara, nitaanzia eneo hilo. Tumepitia vizuri taarifa zote za Kamati zinazoelezea utendaji kwa mwaka mzima. Tumeona namna ambavyo fedha za kuwezesha miradi mbalimbali zilivyoletwa, miradi ambayo iko kwenye majimbo yetu na nchini mwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo kubwa ambalo nitalieleza zaidi ni eneo la hizi barabara ambazo zinaunganisha mikoa. Hizi ni barabara ambazo zinasaidia uchumi katika nchi yetu. Kulikuwa na fedha ambazo zimetengwa, barabara katika maeneo mbalimbali zilitangazwa kwamba zitajengwa. Nitaeleza barabara chache, barabara ya Singida – Kwa Mtoro kwenda hadi Kibrashi Tanga, Barabara ya Mkiwa kupitia Itigi mpaka Makongoros Mbeya na barabara nyingine ambazo zinatoka Singida – Hydom, ni barabara ambazo ni muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka hivi ninavyoongea bado barabara hizo hazina wakandarasi. Tusitegemee katika muda wa mwaka wa fedha uliobaki, tukianza leo kutangaza kama barabara hizo zitakamilika. Kwa hiyo niiombe Serikali iweze kuhakikisha kwamba barabara hizo zinaanza kujengwa ili kufikia malengo yaliyopangwa na bajeti hii tunayoimaliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili pia naomba niseme kwamba, kumekuwa na kikwazo cha GN ambazo ni Wizara ya Fedha. Wizara ya Fedha imekuwa kikwazo katika kutoa GN kwa ajili ya kuruhusu barabara hizi zijengwe hata kama tumetenga fedha hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Serikali ikae pamoja. Haiwezekani Wizara ya Ujenzi inailalamikia Wizara ya Fedha, haiwezekani Wizara ya Mawasiliano inailalamikia Wizara ya Fedha, haiwezekani kwa sababu Serikali ni moja. Niombe sana, kupitia Kamati hii tumejadili, tunaendelea kuishauri Serikali ihakikishe GN inatoka mapema ili kuruhusu barabara hizi zijengwe kwa wakati ili kuweza kuharakisha maendeleo ya kweli ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hapo niipongeze sana TANROAD, wanafanya kazi nzuri sana ya kurekebisha barabara na kujenga barabara mpya. Pia katika kuwasimamia wakandarasi wamekuwa mfano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikihama eneo hili, niombe sana niende kwenye mawasiliano. Hapa nitaeleza zaidi kwenye bundle tunazoweka kwenye simu zetu. Kumekuwa na malalamiko makubwa sana na zaidi ya hapo tumeeleza sana TCRA kwamba wawasimamie watoa huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo unaweka bundle la wiki moja, kabla hujamaliza wiki, zile fedha zinaondoka ilhali ulilipia mwenyewe. Wananchi wanalalamika, tunaiomba Serikali kuhakikisha kwamba inawasaidia wananchi ili waweze kuwa na haki hayo ya msingi wakiweka bundle kwenye simu. Hili limekuwa ni tatizo, na hakuna majibu; hata customer care wanapopigiwa simu hawana majibu ya moja kwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba sana Serikali ilifanyie kazi eneo hili ili kuwapa haki hawa wanaoitwa wateja, ambao ni wananchi wetu huko vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili tumezungumza kwenye Kamati, lakini na hapa nimeona pia nilieleze ili Bunge lako Tukufu liweze kufahamu na wananchi wajue kwamba Wabunge tunawasemea kuhusiana na eneo hili ambalo limekuwa ni changamoto sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu nitaelezea Kampuni yetu ya Ndege ya ATCL. ATCL wanafanya kazi nzuri, wamehuishwa, tumewanunulia ndege za kutosha zinazozunguka nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili kuna maeneo mawili ambayo ni changamoto kubwa. Kwanza ni kuhusu bei; tumekuwa na changamoto ya bei za tickets za ndege. Leo hii ukiangalia bei kutoka Dar es Salaam kuja Dodoma gharama inaanzia laki nne mpaka laki saba, kwa wale ambao wamekwenda Dubai; ni kama vile unaenda Dubai ilhali uko Tanzania. Kwenye hili kumekuwa na changamoto na hakuna majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi kumekuwa na changamoto pia ya kwamba leo mnafanya booking ya ndege; nimeangalia leo, ukiangalia hata kwenye schedule…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante, unga mkono hoja Mheshimiwa.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga hoja mkono, lakini niiombe sana ATCL waangalie upya bei zao. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. MIRAJI J. MTATURU K.n.y. MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MIUNDOMBINU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuhitimisha hoja yetu ambayo tuliiwasilisha pale asubuhi.

Mheshimiwa Spika, kwanza nitumie nafasi hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja hii. Tulipata Waheshimiwa Wabunge 11 ambao walichangia kwenye hoja ambayo tuliiwasilisha hapa. Nawashukuru sana, sina sababu ya kuyarudia majina yao.

Mheshimiwa Spika, katika hoja ya jumla, ilionekana kuna tatizo la bajeti, kwamba Wabunge walikuwa na mashaka makubwa na sisi Kamati tulieleza, kwamba wakati tunawasilishiwa taarifa ilikuwa ni asilimia 23 tu hivi ya bajeti ambayo ilishafika kwenye Wizara zetu.

Mheshimiwa Spika, maelezo ambayo tumeendelea kuyapata ni kwamba kuna baadhi ya tenda ambazo zilikuwa kwenye utaratibu, ziko kwenye process. Bahati nzuri Mheshimiwa Naibu Waziri wa Habari, Mawasilioano na Teknolojia ya Habari alieleza kuna tenda kama ya minara ambayo tayari kama minara 700 hivi ambayo huenda ikafanyiwa kazi ndani ya miezi hii miwili. Kwa hiyo, maana yake ikikamilika ile ita shoot kwenda mbele zaidi tofauti na hii ya sasa. Kwa hiyo, nina amini kabisa maoni yetu ambayo tulisema yamechukuliwa na Serikali na sisi kama Kamati tunaendelea kusisitiza kwamba fedha zitolewe ili miradi iweze kutekelezwa kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, kumejitokeza hoja mahususi kama tatu na mojawapo ni hii ya SGR kipande cha Tabora- Kgoma ambacho kimeelezwa hapa na kimsingi ni kwamba umepata majibu ya Serikali kwa ufupi kutoka kwa Mheshimiwa Naibu Waziri. Naomba niseme tu kwamba sisi Kamati tumepokea maoni ya Wabunge ambao wameonesha concern hiyo kwamba ni vizuri kama kuna haja basi Mheshimiwa Spika kwa maelekezo yako, unaweza kuielekeza Serikali iweze kupitia kwa sababu haya ni maslahi mapana ya Taifa na ili iweze kuonekana kwamba Serikali inafanya kazi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika,kama itakupendeza Kamati ya Katiba na Sheria ipo lakini pia sisi Miundo Mbinu tupo,ukielekeza upya wanaweza kutuletea kwa niaba ya Bunge tuweze kuitazama upya na kuona utaratibu mzima ulivyofikiwa. Lakini sisi kama Kamati tunaendelea kusema tena tutaendelea kusimamia Wizara hii katika kuhakikisha Miradi yote inatekelezwa kama ilivyopangwa na Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja mahususi nyingine ambayo ilijitokeza ni hoja ambayo aliitoa Mheshimiwa Daktari Faustine Ndungulile ni hoja ya Vivuko. Na hili nieleze kwamba Mheshimiwa Ndungulile amekuwa ni mdau muhimu sana na eneo la Kigamboni kumekuwa na matatizo ya vivuko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunakiri wote kwamba katika maeneo ambayo Serikali au Taifa liweze kuchukua hatua ni kuhakikisha kwamba vivuko vinafanyiwa ukarabati iwezekanavyo ili watu wetu waendelee kuwa salama. Lakini eneo lile la Kigamboni watu wengi sana wanavuka kutoka mjini kuja Kigamboni. Kwa hiyo, nakubaliana na yeye kabisa kwamba TEMESA, hata sisi ndani ya Kamati tumekuwa na wasiwasi mkubwa na namna ya utendaji wa TEMESA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika,Kwa hiyo, niombe tu hili la kupeleka au kutangaza tenda na kupata mwingine baada ya ushindani, ninadhani iwe ni hoja ya sasa kama alivyosema Mheshimiwa Spika. Tuache ifanyiwe ukarabati kitengenezwe Kivuko ili wananchi wa Kigamboni wawe salama ili waweze kuishi salama na wasafiri salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu suala la maji hatuwezi kusubiri baadae kuja kuanza kutoa rambirambi kwa kitu ambacho kinakuja kuonekana wazi tungeweza kutengeneza. Kwa hiyo, niombe tu mchakato ambao ulitumika Mheshimiwa Naibu Waziri ameeleza na ninaamini kabisa umeenda sawa. Tunachotakiwa ni tusimamie Vivuko viwe salama, MV Magogoni itokee na iweze kuleta usalama wa wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, hoja mahususi ambayo ni ya mwisho ilikuwa ni ya Mheshimiwa Josephat Gwajima. Askofu alieleza suala la barabara ya kule Tegeta kwamba tuangalie barabara zenye uchumi mkubwa ziwe ni kipaumbele ziweze kutengenezwa ziweze kuzalisha mapato mengine ya kuweza kutengeneza barabara zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hili ni sahihi kabisa na sisi kwenye Kamati tuliliona tulipokwenda kutembelea barabara ile ya kule Ludewa ambayo ina changamoto ya milima mikubwa sana. Tulienda kule tukashauri barabara ile iweze kutengenezwa ili chuma pamoja na mkaa ulioko kule utoke kwa haraka uende kule kwa ajili ya kwenda kuuzwa katika Bandari zetu na uweze kuleta pato kubwa la Taifa. Kwa hiyo, tunamkaa wa kutosha uko kule, kuna chuma ya kutosha kule lakini haitoki kwa sababu tatizo ni barabara haipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunashukuru Serikali juzi tulivyoenda kukagua tumefanikiwa kupata Bilioni Tano imewekwa pale kwa ajili ya Milima fulani. Mheshimiwa Mbunge wa Ludewa pale alikuwa ananiambia amefurahi kuona Serikali imewawekea fedha ya kutengeneza angalau sehemu ya Mlima kama Kilometa Saba. Kwa hiyo, nilitaka niseme kwamba hoja yako ni nzuri. Niombe Serikali ichukueni hii, barabara yenye uzalishaji na uchumi mkubwa zichukuliwe kipaumbele ili ziweze kuzalisha mapato ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hoja kubwa nyingine ilikuwa ni ile ya kuzima simu tarehe 13 Februari. Ninaomba nirudie tena kusema ili tuweze kuondokana na tatizo la Kimtandao, Serikali isirudi nyuma wale ambao hawajahakiki tarehe 13 tunamuunga Mkono Mheshimiwa Waziri simu zile zifungwe. Ili tujue nani hasa mwenye simu yake vinginevyo tukiendelea kufanya danadana tutaendeleza tatizo la kimtandao na hatutamaliza utapeli kwenye simu ambazo ziko kwenye mtaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, baada ya maneno hayo. Ninaomba nirudie tena kushukuru kwa hoja zote zilizotolewa, naomba nirudie tena sasa kwa heshima kabisa naomba kutoa hoja ili ipitishwe na Bunge ili yawe maazimio ya Bunge yakuweza kupitisha taarifa yetu, ahsante sana. (Makofi)

MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kweli kwa kunipa nafasi hii lakini kwa hakika nitakuwa mchoyo wa fadhila bila kukupongeza sana leo asubuhi umefanya jambo kubwa katika Taifa la kuruhusu mjadala ambao una maslahi makubwa katika Taifa letu. Hongera sana, tumepata salamu nyingi kutoka kwa Watanzania kwamba Bunge sasa linakwenda kuishauri Serikali na kwa muda muafaka na tunategemea maagizo yako yatatekelezwa. Ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kaka yangu Masauni kwa namna ambavyo anasimamia Wizara hii, lakini pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kuhakikisha uwepo wa usalama wa nchi yetu kama walivyokasimiwa madaraka na Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, Wizara hii ni muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu, kama hakuna usalama hakuna maendeleo. Kwa hiyo, nilitaka niseme hayo tunayoshauri lengo letu ni kuhakikisha usalama wa Tanzania na kwa hakika waweze kufanya kazi zao vizuri. Mfano mdogo ni huu wa juzi uliotokea wa panya roads wameweza kuharibu sana amani ya wananchi katika maeneo ya Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, nitakwenda haraka haraka kwenye mchango wangu. Nianze kwanza kwenye eneo hili ambalo nalisema la Kituo cha Polisi pale Ikungi, ni kituo ambacho amekieleza Mheshimiwa Sangu Ndugu yangu, kimeanza ujenzi katika miaka saba iliyopita. Hapa ndani ya Bunge hili nimeuliza maswali siyo chini ya matatu kuulizia kituo kile; na majibu yamekuwa ni yale yale. Kama haitoshi kwenye Kituo cha Polisi kinachotumika sasa hivi, ni kituo ambacho unaweza kusema ni kama stoo, siyo Kituo cha Polisi chenye hadhi ya Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Spika, niombe sana nimeona imetajwa ndani ya bajeti na tuliongea na Mheshimiwa Masauni, alishafika pale mwaka 2018 akiwa Naibu Waziri wa Wizara hii. Nimwombe sana, leo nisipopata majibu ya kutosheleza kwa hakika kwa mara ya kwanza nitashika shilingi ili nipate ufafanuzi wa kutosha kuhusu Kituo cha Ikungi pamoja na vituo vingine nchini, nini mkakati wa Serikali katika kuhakikisha vituo hivyo vinajengwa na kuweka hadhi ya Jeshi la Polisi ambao wanafanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa vyombo vya usafiri tumeambiwa hapa Wilaya ya Ikungi ina kilometa za mraba 5,800, ni wilaya kubwa lakini ina magari mawili ambayo ni chakavu sana. Leo ukihitaji leo waende waka-attend tukio lolote, wanaweza kwenda wakati kabla hawajarudi wanaambiwa tukio lingine limetokea; kwa hiyo, hawawezi kuwahi matukio mbalimbali. Hiyo, kama haitoshi mimi kama Mbunge niliwahi kuwachangia pale nikawasaidia pikipiki mbili ili kupunguza makali hayo. Nilishamwomba Mheshimiwa Waziri atupatie gari katika mgao wa magari hayo, naomba hata angalau atuongezee gari lingine moja ili kumfanya OCD aweze kufanya kazi vizuri na watu wake.

Mheshimiwa Spika, kwenye hili ni OC ya mafuta. Tunategemea nini tunapokuwa tunaamini, tunawawekea ration ndogo sana ya mafuta kwa mwezi, unategemea huyu OCD atafanyaje kazi kilomita 300 kwenda na kurudi kila siku kwa matukio, itakuwa ni ajabu sana, kusema unaruhusu aka-attend matukio wakati hujamwezesha. Niombe sana Mheshimiwa Waziri tuwaongezee bajeti ili hawa polisi wenzetu waweze kufanya kazi yao vizuri na kuweza kuokoa Watanzania pamoja na mali zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la tatu ni mafao. Polisi wetu wanafanya kazi nzuri, wanafanya kazi kwa uzalendo mkubwa na kama ulivyosikia mishahara yao ni midogo, lakini inapofika wamestaafu sasa mafao yao hawayapati kwa wakati. Hivi inashangaza sana mtu amefanya kazi sana zaidi ya miaka 30, siku anastaafu unaanza tena kumwomba vielelezo vya kudai mafao yake; hili siyo sawa. Niombe sana Serikali iweze kuona namna ya kuwasaidia wazee wetu hawa waweze kuendelea kuishi vizuri na wengine wanapostaafu wanakufa haraka kwa sababu wanachelewa kulipwa mafao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno hayo, naunga mkono hoja, ahsante sana, lakini baadaye nitakuja; nitashika shilingi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja iliyoko mezani ya Bajeti ya Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kutoa pongezi nyingi sana kwa Mheshimiwa Rais, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya kwa ajili ya Taifa letu na katika kila hatua anayoendanayo katika muda wa uongozi wake amekuwa akiwaletea matumaini makubwa Watanzania. Ushahidi mkubwa ni huu wa juzi tu pale alipoamua kusikiliza cha wafanyakazi na kuweza kupandisha mishahara kwa asilimia 23. 3, ambayo ni kubwa sana nchi, zote za Afrika hazijafanya hivyo, ni Tanzania peke yake. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri. Tumepokea hotuba yake, tumepokea mipango ya Wizara yake. Kwa hakika Mheshimiwa Bashe unatuheshimisha sana kama Taifa, unafanya kazi nzuri sana. Kama kijana wa Kitanzania unaonekana wazi wazi wewe ni mzalendo wa kweli, na kwa hakika Mheshimiwa Rais hakukukosea na kukuweka kwenye Wizara hii. Hongera sana, tunaomba tukuhakishie kwamba Wabunge tutaendelea kukuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa ndugu yangu Mheshimiwa Antony Mavunde, Naibu Waziri, nawe unafanya vizuri, unamsaidia sana Mheshimiwa Waziri na timu yenu ni timu ambayo inaonekana wazi kwamba inaenda kufunga magoli ambayo ni magoli ya kukiboresha kilimo cha Tanzania. Nimpongeze sana Katibu Mkuu kaka yangu Massawe Pamoja na Naibu Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara hii kwa namna mlivyojipanga vizuri katika kukileta kilimo kiwe ni kilimo cha manufaa kwa ajili ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo nimefurahi kuona kwamba hata bajeti, kama ambavyo nimepongeza Mheshimiwa Rais, ni utashi wa hali ya juu sana kwamba kutoka bajeti ya bilioni 234 kwenda mpaka bilioni 751 si jambo dogo. Naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, lakini hii ni mipango ambayo Wizara ikiongozwa na Waziri wameweza kumpelekea maoni na mapendekezo yao. Nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri, huu mwendo mzuri. Wabunge tumekuwa tukilalamika hapa kwamba bajeti ni ndogo, lakini kwa bajeti hii, ingawa ni ndogo lakini inaweza kuwa nafasi nzuri ya kuanzia katika kuboresha kilimo chetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nitakuwa na maeneo machache kuchangia leo. Nitachangia leo, nitachangia kuhusiana na kilimo cha umwagiliaji, suala la mbegu na nitamalizia ushirika kama muda utanitosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa eneo la umwagiliaji. Nimefurahi sana kwamba katika bajeti hii tunayoenda kuiangalia hapa tumeona ambavyo tumevuka vizuri. Bilioni 51 zitaenda kuleta mapinduzi makubwa kwenye kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu nilikuwa naomba, kama ambavyo ulishasema huko nyuma, kwamba tutajitahidi kuhakikisha kwamba Tume ya Umwagiliaji inakwenda kwenye halmashauri zetu. Kule ndiko kwenye mahitaji, na nivizuri wakiwa Jirani kwa sababu wataweza kusimamia kwa karibu sana. Ni kweli kwamba tumekuwa na maafisa kilimo lakini yeye ana-deal na mambo ya ugani na mambo mengine, lakini suala la umwagiliaji ni component inayoonekana kama Wizara ya maji hivi. Lakini kwa sababu Tume ya Umwagiliaji iko mezani kwako ukiweza kuweka wawakilishi ambao watakuwepo muda wote, wanaamka na kulala pale pale, watasaidia sana kuhuisha kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi niseme tu, kwa bajeti ambayo tumeiona hapa tukijipanga vizuri tunaweza tukaibadilisha sana kilimo chetu kwa sababu kilimo cha kutegemea mvua kwa kweli tumeona kimekuwa hakina tija tena. Ninyi wenyewe ni mashahidi, mwaka huu tulijitahidi kupeleka mbegu, na nipongeze sana kwenye eneo hili; mmepeleka mbegu za kutosha mfano za alizeti kule Singida Mkoa wa Dodoma pamoja na Mkoa wa Simiyu, lakini mvua zimekuwa chache; maana yake jitihada zetu zimekwenda kugonga mwamba. Lakini tungekuwa na maji ya kutosha, tungekuwa na skimu za umwagiliaji wa kutosha leo hii ile mbegu ambayo tumeipanda kule isingepotea, maana kuna baadhi ya maeneo hakuna tena matumaini ya kuvuna alizeti ambayo tumeipanda kwa bei nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kipekee kabisa kwangu mimi kwenye eneo la kwangu pale Jimbo la Singida Mashariki niliongelea Habari ya skimu ya umwagiliaji wa Mang’onyi. Nikushukuru sana Mheshimiwa Waziri, kwamba mmekubali kunipelekea milioni 700 ambayo itaenda kuisaidia sana skimu ile ili ianze kufanya kazi. Wananchi wa Mang’onyi wanatusubiri kwa hamu. Lakini kama haitoshi kwenye ule mgodi wa madini ambao unaenda kufunguliwa hivi karibuni wako tayari kununua mboga mboga kutoka kwenye mashamba ya wakulima wale. Maana yake ni kwamba, soko litakuwepo na hiyo skimu italipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama haitoshi niombe sana tuongeze suala mabwawa katika maeneo mbalimbali katika jimbo langu, tukiweza kuweka mabwawa yatawasaidia wakulima kuendelea kufanya kilimo cha umwagiliaji. Naomba, kama Kata za Mkiwa, Kikio, Isuna, Mang’onyi, Misuwaha paoja na Ndung’unyi tukipata mabwawa yatatusaidia sana kuboresha kilimo chetu ambacho ni kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mbegu ni roho ya kilimo. Tukiwa na mbegu nzuri zitasaidia kuleta mazao mengi, uzalishaji wa mazao ukiwa mwingi maana yake hata mnyororo wa thamani utakuwa umepatikana. Kwa kwa hiyo niombe sana; kuna suala ambalo tumelizungumza hapo nyuma, tuwe na mbegu zetu za asili na tuzilinde.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anajua namna ambavyo GMO tumekuwa tukitumia sasa hivi; lakini kuna mahali ambapo tukitegemea tutakuwa ni watumwa wa mbegu za nje siku moja tutajikuta hatuna mbegu zetu, na hivyo hatutakuwa salama. Hata hivyo tunao wenzetu wa ASA ambao ndiyo wakala wa mbegu nchini...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa; hitimisha hoja yako basi, naona muda wako umekwisha.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: …Mheshimiwa Mwenyekiti, basi ninaomba sana mbegu zipewe kipaumbele ili ziwasaidie wakulima kupata tija na ninaamini kabisa uzalishaji utaongezeka na lengo la wizara itatimia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia bajeti ya Wizara hii ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari. Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Waziri, kaka yangu Mheshimiwa Nape Moses Nnauye, kwa kazi nzuri anayoifanya na tunaona Wizara hii kupitia yeye imeendelea kufanya kazi nzuri sana. Kama ambavyo tumekuwa tukisema kwamba lazima Watanzania wapate taarifa mbalimbali, lakini kupitia Wizara hii Waziri ameweka utaratibu mzuri na tumpongeze sana kwamba tuliwahi kumwona siku moja kwenye Aridhio akiendesha kipindi cha karibu nusu saa. Hongera sana kwa Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri ndugu yangu Engineer Andrea Mathew Kundo kwa namna ambavyo anamsaidia Mheshimiwa Waziri; lakini na timu nzima Katibu Mkuu, pamoja na wasaidizi wao wote katika Wizara na Taasisi zilizopo chini ya Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sababu ya muda nitakwenda kwenye mambo mawili tu. Nitaanza na jambo la kuhusiana na kuboresha mawasiliano nchini. Tunajua kabisa kwamba kuna baadhi ya maeneo ambayo yamekuwa na changamoto kubwa, Serikali imefanya kazi kubwa sana ya kupeleka minara. Ukiangalia mwaka wa fedha uliopita minara mingi imewashwa na mingine inaendelea kufanya kazi. Nikiwa Mjumbe wa Kamati tumekuwa tukiona kazi kubwa inayofanywa na Wizara yetu. Naomba tupongeze sana kwa sababu ni jambo kubwa, kupitia UCSAF hawa Mfuko wa Mawasiliano kwa wote umefanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo hayana mvuto wa kibiashara, makampuni mbalimbali yalikuwa hayaendi, lakini kupitia mfumo huu wa Serikali yetu na tunampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kutoa fedha za kwenda kusaidia ruzuku ya kuhakikisha inajenga minara katika maeneo mbalimbali ya nchini kwetu. Kwa sababu, mawasiliano ni haki ya kila mtu, leo hii kila mtu kule kijijini bibi, babu naye unakuta ana simu yake anataka awasiliane na mjukuu wake popote alipo. Hili jambo kubwa limefanyika, lazima tuipongeze Serikali kwa kazi kubwa, hata mwaka huu wa fedha tumeona kuna fedha imetengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishukuru sana sisi watu wa Singida Mashariki tulikuwa na changamoto kubwa katika Bonde la Misughaa, tumepata mnara ambao ulishakuwa tayari. Sasa hivi tunamsubiri Mheshimiwa Waziri aje azindue rasmi ili wananchi waanze kupata mawasiliano. Kwenye hili wananchi wanaomba, Waziri aruhusu na kampuni nyingine za simu ziweze kuweka mawasiliano yao kwenye ule mnara ili waweze kupata na mawasiliano mengine; kwa sababu pale ni mnara wa TTCL na wanaomba na mawasiliano ya simu zingine ili waweze kuwa na mawasiliano mbalimbali, wengine wanataka Airtel, Vodacom na Tigo. Naamini kabisa Waziri akifanya hivyo itakuwa na maana kubwa ya uwekezaji wa Serikali pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili, pia niombe sana tuongezewe tena mnara, katika Kata ya Libwa mawasiliano ni mabaya sana, lakini pale Mang’onyi tunataka tupate mawasiliano kwa ajili ya Mgodi wa Shanta ambao unakwenda kuzinduliwa hivi karibuni, kutakuwa na mwingiliano wa watu wengi sana. Kwa hiyo, niombe sana watuangalie, tuweze kupata minara angalau mingine miwili katika Jimbo la Singida Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili naomba suala la data, tuongeze uwezo wa data kwa wananchi, inawezekana kukawa na mawasiliano ya simu, lakini data zipo chini, kwa hiyo wamezoea 2G lakini tukiende 3G, 4G, kama Mheshimiwa Waziri alivyokuwa anasema hapa, wananchi watakuwa na mawasiliano, kwa sababu leo, mawasiliano ni biashara, kila mtu anaweza kuwa anafanya biashara kupitia simu yake hata akiwa kijijini kule. Pia na hilo Mheshimiwa Waziri akilifanya itatusaidia sana kuongeza uwezo katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ambalo ni jambo la mwisho, nataka niongelee kuhusu TBC. TBC ndiyo Shirika la Umma; Habari ya TBC kokote ikitoka ni ya uhakika kwa sababu imekuwa edited na Serikali. Baadhi ya vyombo vinafanya biashara, vinaangalia walaji wanataka nini, lakini TBC inajenga umoja wa Kitaifa, ulinzi wa usalama wa nchi, historia ya nchi yetu na mambo mbalimbali. Kwa hiyo, TBC ikiwa na uwezo mkubwa itakuwa inajenga umoja wa kitaifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba TBC imefanya kazi kubwa toka uhuru, lakini leo hii tunaona namna ambavyo tunauhisha; vipindi mbalimbali vinawekwa, bidhaa mbalimbali zinawekwa kupitia TBC, lakini Mkurugenzi Ayubu anafanya kazi nzuri sana. Kwa hiyo niombe sana wapewe fedha ya kutosha, uwekezaji wa kutosha, huko kwenye maeneo ya huko nje kwa maana ya kwenye mipaka ya nchi yetu, kuna baadhi ya watu ambao toka wamezaliwa hawajawahi kusikia TBC kwa maana ya Kiswahili, wanaongea lugha za nje, wengine wanasema hao ni Wanyarwanda mpaka kwenye uraia tunapata shida, kwa sababu toka wamezaliwa wanasikia Kinyarwanda tu. Leo hii ukiwawekea TBC kwa uhakika, maana yake watu wetu utawasaidia kujua Radio yao ya Taif ana Televisheni ya Taifa. Kwa hiyo, niombe TBC wapate fedha ya kutosha ili iweze kufanya kazi nzuri ambayo inaendelea kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania wa Mwaka 2022
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja iliyoko mbele yetu. Nianze kuchangia kwenye Muswada wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi ambao uko mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, kwanza naipongeza sana Serikali kwa kuja na sheria hii ambapo kimsingi tumeisubiri kwa muda mrefu na ilikuwa ni hamu ya Watanzania kupata Sheria hii ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi kwa ajili ya kulinda mambo mbalimbali ambayo yapo kwenye taarifa zao ambazo wamezitoa.

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri sana tulivyoweza kukutana na wadau, walionesha wazi wanaishukuru Serikali kwa kazi nzuri ambayo wameifanya kuileta sheria hii. Kwa hiyo, sisi kama Wabunge tunapaswa kuleta shukurani hizo kwa Serikali na Mheshimiwa Rais mwenyewe kwa dhamira yake, lakini tumpongeze sana Mheshimiwa Waziri pamoja na wataalamu wake kwa kutuletea sheria hii na ufafanuzi wa Muswada huu. Tunaipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Spika, suala la pili ni kwamba namna ambavyo tumekuwa sisi kama nchi, tumeridhia maazimio mbalimbali ya Kimataifa. Miongoni mwa maazimio hayo yalikuwa ni pamoja na kulinda taarifa binafsi za watu. Sisi kama nchi ilikuwa bado hatuna sheria ambayo inaweza kuendana na maazimio hayo. Kwa hiyo, kuja sheria hii ni wakati muafaka kwamba wenzetu duniani sasa wataona namna ambavyo tunaungana nao katika suala hili la kulinda taarifa binafsi za watu.

Mheshimiwa Spika, hiyo kama haitoshi, ni kwamba leo hii tunafanya shughuli nyingi kupitia ICT. Mambo mengi yanafanyika kutoka kwenye kiganja kwa maana tunatumia kwenye utaratibu wa TEHAMA. Hatuna namna ambapo tutakwepa baadhi ya mambo ambayo yako duniani. Kwa hiyo kwenye eneo hili kama nchi tunaamini kabisa itaongeza imani kubwa kwa wawekezaji kuendelea kuwekeza kwenye sekta hii ya TEHAMA. Sekta ya TEHAMA inakuwa, leo hii vijana wengi wamewekeza kwenye TEHAMA, maana yake ni kwamba kuleta sheria hii inaongeza confidence ya wale wanaoshughulika kwenye eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe Waheshimiwa Wabunge wenzangu, kwamba tuipitishe sheria hii ili ikaisaidie Serikali katika kuongeza wigo wa ajira kwa ajili ya wananchi wetu. Naamini kabisa kupitia sheria hii, itakuwa ni jibu ambalo limekuwa likitafutwa kwa muda mrefu katika kutatua changamoto zilizopo kwenye eneo hili la TEHAMA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile wawekezaji wengi katika eneo hili walikuwa wanasita kuwekeza kama ambavyo nimesema. Leo hii wamekuwa wana mahitaji ya kuona namna ambavyo dhamira ya Serikali yetu katika eneo hili. Leo hii tukiweza kufanya hivyo na biashara kubwa duniani leo ni iko kwenye mtandao. Leo hii ukiangalia Shirika letu la Posta wamefanya kazi nzuri sana, wanasema duka lako mkononi mwako, maana yake ni kwamba leo hii kupitia haya tutawafanya watu wawe na imani zaidi na hata na taasisi zetu za Serikali kuacha zile za watu binafsi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme tu mimi binafsi naona sheria imekuja wakati muafaka, tuipitishe kama ambavyo imeelezwa vizuri kwa urefu madhumuni yake, nani ambaye anatakiwa kutoa taarifa, kwa wakati gani na sababu gani, itasaidia sana kuondoa changamoto ambazo tulikuwa nazo huko nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na sheria nzuri hii ambayo Wabunge tunapitisha na bahati nzuri sana wewe mwenyewe umekuwa unatamani sheria hii ambayo tutaipitisha ikafanye kazi vilevile. Kumekuwa na changamoto ya kanuni na tunamwamini sana Mheshimiwa Waziri, niombe sana sheria ikitungwa nzuri iende hivyo hivyo na kanuni zake ziwe nzuri. Tumekuwa tukipitisha hapa baadhi ya sheria tukiruhusu ile room ya kwenda kutengeneza kanuni, kanuni inaenda inaharibu kabisa ile sheria. Mwisho wa siku sasa Wabunge tunaulizwa hivi mlipitishaje hii sheria? Kumbe kanuni imeenda kuharibu kabisa maudhui mazima ya sheria ambayo tumeipitisha hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo msisitizo wangu ni hapo, tunapitisha sheria hii, lakini niombe kama alivyosema asubuhi Mheshimiwa Waziri nitaenda kutunga kanuni kwa mujibu wa kanuni ambayo nimeruhusiwa, lakini ni vizuri kanuni hiyo iendane na sheria hii ambayo tunaenda kupitisha leo kwa sababu kuna baadhi ya kifungu kimeeleza Waziri ataona vinginevyo katika utungaji wa kanuni. Hili eneo linaweza likawa ni mwiba mwingine kwa ajili ya kuharibu sheria ambayo tunaenda kuipitisha leo. Kwa hiyo, niombe sana tutakapokuwa tunakaa ni vizuri hata wewe Mheshimiwa Spika, ukajiridhisha na zile kanuni tu uzione ili angalau zile kanuni ziendane na sheria tuliyopitisha.

Mheshimiwa Spika, wewe bahati nzuri ni Mwanasheria umebobea, lakini leo unaletewa sheria ambayo kesho inaonekana useless haina maana yoyote. Nadhani kupitia Kamati yako ya Sheria Ndogo, kupitia Kamati yako ya Katiba na Sheria wazione hizo kanuni wazipitishe. Ambacho tulibaini, juzi wadau walivyokuja wameonyesha wana imani kubwa na Bunge lako, wana imani na Bunge hili, kwa hiyo kupitia kanuni isiondoe imani ambayo wadau na wananchi wa Tanzania wanayo.

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno haya, naunga mkono hoja na naomba tuipitishe sheria hii ni nzuri sana. Ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi wa Mwaka 2022
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja iliyoko mbele yetu. Nianze kuchangia kwenye Muswada wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi ambao uko mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, kwanza naipongeza sana Serikali kwa kuja na sheria hii ambapo kimsingi tumeisubiri kwa muda mrefu na ilikuwa ni hamu ya Watanzania kupata Sheria hii ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi kwa ajili ya kulinda mambo mbalimbali ambayo yapo kwenye taarifa zao ambazo wamezitoa.

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri sana tulivyoweza kukutana na wadau, walionesha wazi wanaishukuru Serikali kwa kazi nzuri ambayo wameifanya kuileta sheria hii. Kwa hiyo, sisi kama Wabunge tunapaswa kuleta shukurani hizo kwa Serikali na Mheshimiwa Rais mwenyewe kwa dhamira yake, lakini tumpongeze sana Mheshimiwa Waziri pamoja na wataalamu wake kwa kutuletea sheria hii na ufafanuzi wa Muswada huu. Tunaipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Spika, suala la pili ni kwamba namna ambavyo tumekuwa sisi kama nchi, tumeridhia maazimio mbalimbali ya Kimataifa. Miongoni mwa maazimio hayo yalikuwa ni pamoja na kulinda taarifa binafsi za watu. Sisi kama nchi ilikuwa bado hatuna sheria ambayo inaweza kuendana na maazimio hayo. Kwa hiyo, kuja sheria hii ni wakati muafaka kwamba wenzetu duniani sasa wataona namna ambavyo tunaungana nao katika suala hili la kulinda taarifa binafsi za watu.

Mheshimiwa Spika, hiyo kama haitoshi, ni kwamba leo hii tunafanya shughuli nyingi kupitia ICT. Mambo mengi yanafanyika kutoka kwenye kiganja kwa maana tunatumia kwenye utaratibu wa TEHAMA. Hatuna namna ambapo tutakwepa baadhi ya mambo ambayo yako duniani. Kwa hiyo kwenye eneo hili kama nchi tunaamini kabisa itaongeza imani kubwa kwa wawekezaji kuendelea kuwekeza kwenye sekta hii ya TEHAMA. Sekta ya TEHAMA inakuwa, leo hii vijana wengi wamewekeza kwenye TEHAMA, maana yake ni kwamba kuleta sheria hii inaongeza confidence ya wale wanaoshughulika kwenye eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe Waheshimiwa Wabunge wenzangu, kwamba tuipitishe sheria hii ili ikaisaidie Serikali katika kuongeza wigo wa ajira kwa ajili ya wananchi wetu. Naamini kabisa kupitia sheria hii, itakuwa ni jibu ambalo limekuwa likitafutwa kwa muda mrefu katika kutatua changamoto zilizopo kwenye eneo hili la TEHAMA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile wawekezaji wengi katika eneo hili walikuwa wanasita kuwekeza kama ambavyo nimesema. Leo hii wamekuwa wana mahitaji ya kuona namna ambavyo dhamira ya Serikali yetu katika eneo hili. Leo hii tukiweza kufanya hivyo na biashara kubwa duniani leo ni iko kwenye mtandao. Leo hii ukiangalia Shirika letu la Posta wamefanya kazi nzuri sana, wanasema duka lako mkononi mwako, maana yake ni kwamba leo hii kupitia haya tutawafanya watu wawe na imani zaidi na hata na taasisi zetu za Serikali kuacha zile za watu binafsi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme tu mimi binafsi naona sheria imekuja wakati muafaka, tuipitishe kama ambavyo imeelezwa vizuri kwa urefu madhumuni yake, nani ambaye anatakiwa kutoa taarifa, kwa wakati gani na sababu gani, itasaidia sana kuondoa changamoto ambazo tulikuwa nazo huko nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na sheria nzuri hii ambayo Wabunge tunapitisha na bahati nzuri sana wewe mwenyewe umekuwa unatamani sheria hii ambayo tutaipitisha ikafanye kazi vilevile. Kumekuwa na changamoto ya kanuni na tunamwamini sana Mheshimiwa Waziri, niombe sana sheria ikitungwa nzuri iende hivyo hivyo na kanuni zake ziwe nzuri. Tumekuwa tukipitisha hapa baadhi ya sheria tukiruhusu ile room ya kwenda kutengeneza kanuni, kanuni inaenda inaharibu kabisa ile sheria. Mwisho wa siku sasa Wabunge tunaulizwa hivi mlipitishaje hii sheria? Kumbe kanuni imeenda kuharibu kabisa maudhui mazima ya sheria ambayo tumeipitisha hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo msisitizo wangu ni hapo, tunapitisha sheria hii, lakini niombe kama alivyosema asubuhi Mheshimiwa Waziri nitaenda kutunga kanuni kwa mujibu wa kanuni ambayo nimeruhusiwa, lakini ni vizuri kanuni hiyo iendane na sheria hii ambayo tunaenda kupitisha leo kwa sababu kuna baadhi ya kifungu kimeeleza Waziri ataona vinginevyo katika utungaji wa kanuni. Hili eneo linaweza likawa ni mwiba mwingine kwa ajili ya kuharibu sheria ambayo tunaenda kuipitisha leo. Kwa hiyo, niombe sana tutakapokuwa tunakaa ni vizuri hata wewe Mheshimiwa Spika, ukajiridhisha na zile kanuni tu uzione ili angalau zile kanuni ziendane na sheria tuliyopitisha.

Mheshimiwa Spika, wewe bahati nzuri ni Mwanasheria umebobea, lakini leo unaletewa sheria ambayo kesho inaonekana useless haina maana yoyote. Nadhani kupitia Kamati yako ya Sheria Ndogo, kupitia Kamati yako ya Katiba na Sheria wazione hizo kanuni wazipitishe. Ambacho tulibaini, juzi wadau walivyokuja wameonyesha wana imani kubwa na Bunge lako, wana imani na Bunge hili, kwa hiyo kupitia kanuni isiondoe imani ambayo wadau na wananchi wa Tanzania wanayo.

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno haya, naunga mkono hoja na naomba tuipitishe sheria hii ni nzuri sana. Ahsante sana. (Makofi)