Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita (3 total)

MHE. DKT. STEPHEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa niweze kumuuliza Mheshimiwa Wazir Mkuu swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kuwa Serikali yetu ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais wetu mpendwa Dkt. John Pombe Magufuli imejinasibu kuhamasisha ujenzi wa viwanda vikiwemo viwanda vya kuchakata nyama na mazao mengine yanayotokana na mifugo.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba wafugaji wanatengewa maeneo ya malisho na malisho hayo yanaendelezwa kwa kujenga na kukarabati mabwawa, kuchimba visima vya maji na kuwekewa miundombinu mingine muhimu ili kuboresha afya ya mifugo ili waweze kukidhi haja ya hivi viwanda kwa ajili ya ng’ombe hawa wanapokuwa wameongezewa thamani, wafugaji watapata bei yenye tija? Ahsante sana.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Kiruswa Mbunge wa Longido kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli, kama ambavyo nimesema awali kwamba Serikali yetu imejikita katika kuhamasisha ujenzi wa viwanda kwa lengo la kukuza uchumi wetu; na nimeeleza vizuri sana mwanzo manufaa ya viwanda ikiwemo na kuendeleza sekta yenyewe. Kwa kiwanda cha nyama kuwepo kwake Wilayani Longido tuna uhakika wafugaji wetu watapata faida kubwa kwa kufuga kisasa, kwa kupata masoko ya uhakika lakini pia na sisi tutanufaika kwa kupata nyama iliyopitia kiwandani yenye ubora ambao na sisi tumeuona kwamba ni ubora uliohakikiwa na taasisi yetu.

Kwahiyo, uwepo wa kiwanda kile na mwekezaji huyo, Wizara yetu ya Mifugo na Uvuvi imeweka utaratibu mzuri sana sasa; kwamba wale wote waliowekeza viwanda tumewaunganisha na taasisi yetu ya NARCO kwa kuwapa maeneo yaliyotengwa kama ni maeneo ya malisho, kwa kuwapa eneo la kuhifadhia ng’ombe wao, kuwakuza ng’ombe wao na zile taratibu zote zile za mifugo ili ziweze kukamilika kabla hajaingia ndani ya kiwanda kwa lengo la kutoa nyama iliyo bora kwa ajili ya chakula kama ambavyo tumetaka iwe.

Kwa hiyo tumebaini kwamba ranchi zetu zote nchini au maeneo yote ya malisho nchini. Hawa tumewapa maeneo hayo kwanza wale wenye viwanda lakini pili wafugaji wakubwa na tatu tumewatambua pia na wafugaji wadogo ambao wana ng’ombe kuanzia 100 na kuendelea, ambao tumesema tusiruhusu kuwa na ng’ombe 100 vijijini kwa sababu kunakuwa na migogoro mingi ya mifugo kula mazao, mifugo kuharibu miundombinu mingine. Kwa hiyo tumewatengea maeneo kwenye hizo Rachi zetu au kwenye maeneo hayo ya malisho.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa utaratibu huu tumetambua jitihada za wafugaji na kuboresha namna ya ufagaji wao na mahali pa kuuzia, kwa maana ya soko kwenye kiwanda. Mwekezaji naye sasa naona lengo la nchi la kumlinda mwekezaji wetu kwa kumpa maeneo ya kuhifadhia ng’ombe wake halafu awapeleke viwandani. Tunatarajia kuendelea kutenga maeneo mengi zaidi ya malisho na kutoa fursa nyingi zaidi kwa wafugaji wetu wa ngazi zote; wakubwa, wa kati na wadogo ili waendeshe shughuli zao za mifugo vizuri.

Mheshimiwa Spika, Waziri wetu pamoja na Naibu Waziri wake na Makatibu Wakuu wa Wizara hii wanafanya kazi hiyo kila siku, unawaona hata kwenye vyombo vya habari wakiendelea kuratibu maeneo haya ya malisho kwa lengo la kuboresha ufugaji nchini na pia kwa lengo la kukuza sekta ya nyama, kwa maana ya kuwa na viwanda vinavyotengeneza nyama hizi, zinazo-process nyama hizi kwa ajili ya chakula cha ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge aendelee kuhamasisha na kuhakikishia wapiga kura wake kwamba Serikali yetu imejikita katika kuhifadhi na kulinda wafugaji wetu wote na kuhakikisha kwamba tunawatengenezea fursa za kupata pia na masoko yake. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kumwuliza Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo unafahamu mwaka huu nchi yetu ilivamiwa na nzige wa jangwani na ikanipelekea kupenda kufahamu mkakati wa Serikali katika kupambana au kudhibiti majanga yanayoweza kuathiri usalama wa chakula na mazao mengine ya kiuchumi katika nchi yetu ikiwemo mifugo. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Kiruswa, Mbunge wa Longido, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anataka kujua mkakati wa Serikali wa namna ya kukabiliana na majanga. Amezungumzia chakula, lakini majanga yapo mengi. Mkakati huo upo ndani ya Serikali, pale ambapo Ofisi ya Waziri Mkuu kimeanzishwa Kitengo cha Maafa. Kitengo hiki ambacho kipo Ofisi ya Waziri Mkuu, tumekishusha pia kipo ngazi ya Mkoa, kiko Kamati ya Maafa; ngazi ya Wilaya tuna Kamati ya Maafa na pia ngazi ya Tarafa ina Kamati ya Maafa.

Mheshimiwa Spika, wajibu wetu ni kuhakikisha kwamba tunaepusha utokeaji wa majanga haya. Wakati mwingine huwezi kuyaepusha, ila ni kushughulikia majanga haya yanapojitokeza. Kwa hiyo, eneo la chakula nako pia linapotokea janga ambalo linapoteza vyakula ambavyo wananchi walikuwa wanavitegemea, nayo pia tunashughulikia.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dkt. Kiruswa atakumbuka siku za hivi karibuni kule Longido na maeneo mengine tulivamiwa na nzige, nami niliwenda pale, nikaenda mpaka Monduli kwenda kuona hali ya nzige. Ndiyo majanga hayo, wadudu wamekuja kutoka huko, wameruka wanakuja kushambulia chakula, lakini tulikabiliana nao kabla hawajaanza kushughulikia chakula chetu. Kwa hiyo, hiyo ndiyo njia mojawapo ambayo tunaitumia kukabiliana na majanga. Tulienda kuwakabili kabla hawajaanza kula chakula chetu na tukamudu kuwapoteza wote.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumeimarisha kitengo hiki kwa kuweka vifaa, watalaam na pia pamoja na utaalam huo tumeendelea kushusha elimu hii kwa wananchi wenyewe waanze kushughulikia majanga pindi tu inapotokea majanga haya. Vile vitengo husika na vyenyewe vikikaa na kuratibu, vinashughulikia, lakini pale wanaposhindwa ngazi ya Kata, wanajulisha Wilaya, janga linapokuwa kubwa zaidi ya ngazi ya Wilaya wanajulisha Mkoa na Mkoa unaposhughulikia janga hilo likionekana limeshindikana, wanajulishwa Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Waziri Mkuu imekuwa ikifanya kazi hiyo vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwahakikishie Watanzania kuwa na uhakika na Serikali yao na kuiamini kwamba pia tumejipanga kwenye eneo hilo la kupambana na majanga mbalimbali ili kuhakikisha kwamba shughuli zote za Watanzania zinaenda vizuri na tuweze kuwa na akiba ya kutosha kwenye chakula na pia usalama wa maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kumwuliza Waziri Mkuu swali. Kwa kuwa lengo la Sera ya Manejimenti na Ajira katika Utumishi wa Umma, ilitengenezwa toleo la pili mwaka 2008 ili kuboresha utumishi wa Umma na huduma zinazotolewa na Serikali kupitia watendaji wake kwa kuzingatia sifa na usimamizi unaotoa mwelekeo: Je, Mheshimiwa Waziri Mkuu…

SPIKA: Mheshimiwa naona kuna karatasi hapo mbele, kama vile unasoma. Hebu mwangalie Waziri Mkuu, halafu uliza swali.

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Waziri Mkuu, nilikuwa nataka kunukuu lengo la Sera ya Menejimenti na Ajira katika Utumishi wa Umma ambao unasisitiza kwamba watumishi wanaoajiriwa ni wale wenye sifa na ndio watakaosimamia matokeo tunayohitaji katika utendaji wa Serikali.

Na kwa kuwa tuna watumishi wengi wenye sifa katika ngazi ya kada za Watendaji wa Vijiji ambao wamefanya kazi hiyo kwa kujitolea kwa miaka mingi na kumekuwa na tatizo la kutoa vibali vya kuajiri:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwaajiri ili kuondoa hiyo kero ya hawa watumishi ambao hawana ufanisi kwa sababu ni…

SPIKA: Ahsante sana. Umeeleweka Mheshimiwa.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Kiruswa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tulianzisha mfumo ambao unaweza kuwafikia Watanzania wote katika kuajiri badala ya kuziachia sekta ambazo zilikuwa zinaajiri au kwa upendeleo au kwa namna ambayo wengi walikuwa wanalalamikia. Kwa kuunda Tume ya Ajira, tunakusanya nafasi kwenye taasisi zote zinazoombwa, tunaziombea kibali kwenye mamlaka. Tukishatoa kibali, Tume yetu inatoa tangazo Watanzania wanapata nafasi ya kuomba na kuitwa kwa ajili ya usaili halafu wanaweza sasa kuajiriwa.

Mheshimiwa Spika, hawa ambao wanafanya kazi kwa kujitolea kwenye maeneo yetu ya vijiji, kata na pia kwenye Halmashauri zetu wapo kwenye sekta kama afya na elimu, tunao. Wale wote ambao wanafanya kazi kwa weledi na wana sifa ya kuajiriwa, pindi tunapopata vibali kutoka Utumishi, tunawaajiri. Sasa hivi tumeshatoa maelekezo kwenye Halmashauri, wako vijana ambao wanafanya kazi kwenye Halmashauri zetu kwenye nafasi mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kwenye sekta ya elimu wako walimu wanajitolea na wana nafasi nzuri; kwenye kata, pale kwenye mapengo tunao vijana kwenye vijiji vile, wanafanya kazi yao vizuri. Hawa wote tunaendelea kuwaangalia na kukusanya taarifa zao na sifa zao. Inapotokea kuwa na vibali ambapo sasa vinaendelea kuzalishwa kuajiri kada mbalimbali, itakapofikia kwenye kada hiyo, nao pia tunawapa nafasi ya kuwaajiri.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali inaendelea kuwaangalia hawa wote ambao wamejitoa, wameamua kufanya kazi bila mshahara, lakini pia wanataka kuonesha uwezo wao na kuutumia muda wao vizuri kulisaidia na kulihudumia Taifa hili, wote wanapata kipaumbele kwenye ajira.

Mheshimiwa Spika, niwahakikishie wale wote ambao wanajitolea, tulikuwa tunazungumza na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Ummy Mwalimu, juu ya vijana wetu ambao wanafanya kazi kwa kujitolea kule kwamba, hawa sasa waorodheshwe tuwatambue ili baadaye ajira inapotokea, waweze pia kuingia kwenye orodha ya waajiriwa. Kwa hiyo, huo ndiyo utaratibu ambao tunautumia kwa sasa. Ahsante sana. (Makofi)