Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Justin Joseph Monko (8 total)

MHE. JUSTIN J. MONKO aliuliza:-
Barabara ya Singida - Ilongero - Mintiko hadi Haydom inayounganisha Mikoa ya Singida na Manyara ni kiungo muhimu katika kusafirisha mazao ya wakulima na bidhaa za wafanyabiashara na inapita katika Hospitali ya Rufaa ya Haydom ambayo wananchi hufuata huduma kwa kukosa Hospitali ya Serikali katika Halmashauri.
Je, ni lini barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami ili kunusuru maisha ya wananchi wa Singida Kaskazini?
NAIBU WAZIRI UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Justin Joseph Monko, Mbunge wa Singida Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Singida – Ilongero – Mtinko - Nkugi na Kidarafa hadi Haydom ni barabara ya mkoa yenye urefu wa kilometa 93.4 ambapo kilometa 84.36 zipo mkoani Singida na kilometa 9.04 zipo katika mkoa wa Manyara. Barabara hii inahudumiwa na Wakala wa Barabara nchini (TANROADS).
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa barabara hii kwa wananchi wa Mikoa ya Singida na Manyara kwa ajili ya usafirishaji wa abiria, mazao, bidhaa za biashara na pia wananchi wanaokwenda kupata huduma ya matibabu katika hospitali ya Haydom. Hivyo kwa umuhimu huo Serikali imekuwa ikiifanyia matengenezo ya aina mbalimbali barabara hii kila mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2017/2018 barabara hii ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni 2.246 kwa ajili ya matengenezo mbalimbali. Aidha, Serikali imejenga jumla ya kilometa 8 kwa awamu kwa kiwango cha lami kuanzia Singida Mjini kuelekea Ilongero na jumla ya kilometa tano za barabara hii zimepangwa kujengwa kwa kiwango cha lami katika mwaka wa fedha 2018/2019.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa kipaumbele cha Serikali ni kuunganisha kwa barabara za kiwango cha lami makao makuu ya mikoa na nchi jirani na baadae barabara za mikoa zitafuata.
MHE. JUSTIN J. MONKO aliuliza:-
Mradi wa REA Awamu ya Pili katika Jimbo la Singida Kaskazini ulisimama tangu mwaka 2016 na kukosesha huduma hiyo kwa vijiji vilivyokusudiwa mwaka 2017, utekelezaji wa REA Awamu ya Pili katika vijiji 30 kati ya 64 vilivyokusudiwa umeanza.
(a) Je, ni nini kauli ya Serikali juu ya ukamilishaji wa mradi wa REA II?
(b) Je, ni lini mkandarasi wa REA II awamu ya pili atapatikana na kuanza kazi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Justin Joseph Monko, Mbunge wa Singida Kaskazini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Mradi wa REA Awamu ya Pili katika Mkoa wa Singida ulisimama kutekelezwa mwaka 2016 kutokana na mkandarasi Spencon Ltd. kushindwa kukamilisha kazi zake baada ya kufilisika. Hata hivyo, tayari vifaa vyote vya mradi vilikuwa vimenunuliwa na kuhifadhiwa. Wakala wa Nishati Vijijini wamesaini mkataba mpya na Kampuni ya JV Emec Engineering Ltd. & Dynamic Engineering and System Co. Ltd. wenye thamani ya shilingi milioni 991.6 kwa ajili ya kukamilisha kazi za REA Awamu ya Pili katika Wilaya ya Iramba, Mkalama na Singida Vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, Wakala wa Nishati Vijijini umesaini mkataba na Kampuni ya JV East African Fossils Co. Ltd & CMG Construction Co. Ltd. wenye thamani ya shilingi 459.23 kwa ajili ya kukamilisha kazi katika Wilaya ya Manyoni. Mikataba yote miwili imesainiwa mwezi Machi, 2018 kwa muda wa miezi sita. Kazi ya kusambaza umeme katika meneo yaliyotajwa zitakamilika mwezi Septemba, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza, kazi za mradi zinatekelezwa na Mkandarasi M/S CC- Etern Consortium Ltd. ya China, kazi za Mradi wa REA III mzunguko wa kwanza katika Mkoa wa Singida zinajumuisha kuvipatia umeme vijiji 150 ambapo Jimbo la Singida Kaskazini litaunganishiwa umeme jumla ya vijiji 30 na kuunganishia wateja wa awali 870. Mradi utakamilika mwezi Juni, 2019.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kusambaza umeme katika Mkoa wa Singida kwa miradi ya REA awamu ya tatu mzunguko wa kwanza na wa pili zinajumuisha ujenzi wa kilometa 286.1 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33, kilometa 568 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4, ufungaji wa transfoma 284 na kuunganishia wateja wa awali 8,659. Kati ya wateja hao, wateja 7,795 wa njia moja na wateja 864 wa njia tatu. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 29.56 na dola za Kimarekani milioni 5.34.
MHE. JUSTIN J. MONKO aliuliza:-

Tarafa ya Mtinko Jimbo la Singida Kaskazini yenye Kata sita haina kituo cha afya cha Serikali:-

(a) Je, Serikali ipo tayari kukamilisha jengo la kituo cha afya katika Kata ya Makuro lililojengwa na wananchi ili wananchi waweze kupata huduma za rufaa kutoka katika Zahanati zilizopo?

(b) Je, Serikali ipo tayari kutenga fedha za majengo ya ziada katika kituo cha afya Kata ya Makuro ili kutoa huduma bora kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Mnweyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Justin Joseph Monko Mbunge wa Singida Kaskazini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tarafa ya Mtinko yenye Kata sita ina zahanati tisa na haina kituo cha afya. Hata hivyo, wananchi wa Tarafa hiyo hupata huduma za afya za rufaa kwenye hospitali teule ya Wilaya ya St. Carols Council Designated Hospital.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2018/2019, Halmashauri ya Singida imepokea jumla ya shilingi bilioni 2.6 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya Wilaya na kukarabati vituo vya afya viwili yaani kituo cha afya cha Msange na kito cha afya cha Mgori ili kuweza kutoa huduma za upasuaji kwa mama na mtoto. Serikali itaendelea kujenga na kukamilisha maboma ya vituo vya kutolea huduma za afya kwa awamu kadri ya upatikanaji wa fedha utakavyowezeshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo cha afya cha Makuro kimejengwa kwa nguvu za wananchi na mpaka sasa jengo la wagonjwa wa nje lipo katika hatua za ujenzi kwenye ukuta. Nazielekeza halmashauri kutenga fedha kwa ajili ya kukamilisha maboma na vituo vya kutolea huduma kwenye maeneo yao ya kiutawala. Serikali itaendelea kukamilisha maboma na kujenga kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Ahsante.
MHE. JUSTIN J. MONKO aliuliza:-

Katika mitihani ya Taifa ya Vitendo kwa Kidato cha Nne utaratibu mpya ulioanzishwa mwaka 2017 ambao ni bora zaidi ulibadilika na kupelekewa checklist ambayo sasa inahitaji vifaa vingi zaidi na practical nyingi ikilinganishwa na hapo awali ambapo ‘instructions’ ya mwezi mmoja ilitolewa kabla:-

(a) Je, Serikali iko tayari kuongeza fedha za vifaa vya Maabara kufidia ongezeko la gharama za vifaa hivyo ambavyo vinazidi fedha iliyoingizwa kwa mwaka?

(b) Shule nyingi sasa zimelundika madeni ya Maabara na hushindwa kulipa: Je, Serikali iko tayari kulipa madeni haya yaliyosababishwa na utaratibu huu mpya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Justin Joseph Monko, Mbunge wa Singida Kaskazini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ilitekeleza Sera ya Elimu Msngi bila malipo tangu mwaka 2016 ambapo kila mwezi takribani shilingi bilioni 23.8 zimekuwa zikitumwa moja kwa moja shuleni. Kati ya fedha hizi, takribani shilingi bilioni 1.645 zinatolewa kwa ajili ya ruzuku ya uendeshaji wa shule (Capitation Grand). Matumizi ya fedha za ruzuku ya uendeshaji ni pamoja na kununua vifaa vya kufundishia na kujifunzia, ikiwa ni pamoja na vifaa vya maabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia programu ya EP4R, Serikali imekuwa ikinunua vifaa vya maabara kwa shule mbalimbali za sekondari nchini. Mwaka wa fedha 2017/2018, jumla ya shule 1,800 za sekondari zilizokuwa zimekamilisha ujenzi wa maabara zao, hazikuwa na vifaa, vilipelekewa vifaa hivyo. Aidha, mwaka 2018/2019, jumla ya shule 1,258 zilizokamilisha maabara, zimeainishwa na ununuzi wa vifaa hivyo upo kwenye hatua za mwisho. Pindi taratibu zitakapokamilika, shule hizo zitasambaziwa vifaa hivyo vya maabara, ambapo katika Mkoa wa Singida kuna shule 59 zitakazopatiwa vifaa vya maabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilianza kutekeleza utaratibu wa kupelekea fedha moja kwa moja shuleni mwaka 2016 na hivyo madeni mengi yanayozungumziwa ni ya kabla ya mwaka 2016, ambapo shule zilikuwa zikikusanya ada na kuruhusiwa kutumia kwa ajili ya uendeshaji wa shule ikiwemo ununuzi wa vifaa vya maabara. Hivyo Serikali imeelekeza Mamlaka za Serikali za Mitaa kulipa madeni hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. JUSTIN J. MONKO aliuliza:-

Inapotokea Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa/Kijiji amefariki au kupoteza sifa ya kuwa Mwenyekiti wa Mtaa au Kijiji husika huongozwa na Kaimu Mwenyekiti:-

Je, kwa nini Serikali haioni umuhimu wa kuwepo uchaguzi mdogo kama ilivyo kwa Madiwani na Wabunge?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MIAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Justin Joseph Monko, Mbunge wa Singida Kaskazini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanuni za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa za Mwaka 2019 yaani Kanuni ya 43(1) – (4) na Kanuni ya 45 zinatoa fursa ya kufanya Uchaguzi Mdogo kujaza nafasi iliyoachwa wazi endapo Mwenyekiti wa Kitongoji, Kijiji, Mtaa atafariki au kupoteza sifa za kuendelea kuwa katika nafasi hiyo kutokana na sababu zilizoainishwa kwenye Kanuni ya 44(1) na (2). Uchaguzi Mdogo hautafanyika endapo muda uliosalia kabla ya muda wa Mwenyekiti kuwa kwenye madaraka kukoma ili kupisha uchaguzi ni miezi sita au pungufu yake. Ahsante.
MHE. JUSTIN J. MONKO aliuliza:-

Jimbo la Singida Kaskazini limepata Mradi wa Umeme Vijiji (REA na BTIP) ambapo utapeleka umeme katika vijiji 54 kati ya 84; katika baadhi ya maeneo ambayo mradi umepita umeacha nyumba za wananchi, taasisi za dini, taasisi za Serikali na pampu za maji pasipo kuziunganishia umeme.

(a) Je, Serikali ina kauli gani kwa maeneo hayo yaliyorukwa na wananchi waliokwishafanya wiring kwa matarajio ya kuunanishiwa umeme?

(b) Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika vijiji 30 vilivyosalia?

(c) Je, Serikali ipo tayari kusaidia njia mbadala ya umeme wa jua (solar power) katika maeneo ya huduma muhimu kama zahanati, sekondari na huduma za maji wakati tukisubiri usambazaji katika vijiji vilivyosalia?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Justin Joseph Monko, Mbunge wa Singida Kaskazini lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishaji Vijijini (REA) inaendelea kupeleka umeme vijijini kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Lengo la mradi huu ni kuhakikisha umeme katika vijiji, taasisi, viwanda na miradi ya maji na maeneo yaliorukwa katika Jimbo la Singida Kaskazini zikiwemo nyumba za wananchi, taasisi za dini, taasisi za Serikali na pampu za maji zitapelekewa umeme kupitia mradi wa REA III mzunguko wa kwanza unaoendelea na kupitia Mradi wa Densification II utakaoanza kutekelezwa mwezi Juni, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2020.

(b) Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutekeleza miradi ya kusambaza umeme vijijini ambapo vijiji 30 vilivyosalia katika Jimbo hilo vitapatiwa umeme katika mzunguko wa pili wa mradi wa REA III utakaoanza kutekelezwa kuanzia mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021.

(c) Mheshimiwa Spika, mwaka 2018/2019 Serikali kupitia Mradi wa Results Based Finance unaotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) iliendelea kufanya utafiti ya kujua kiasi cha nguvu ya jua kinachopatikana nchini ikiwa ni pamoja na eneo la Singida Kaskazini.

Mheshimiwa Spika, baada ya kukamilika kwa utafiti huo Serikali itaanza kazi ya kupeleka miundombinu ya umeme wa nguvu za jua katika Jimbo la Singida Kaskazini. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. JUSTIN J. MONKO aliuliza:-

Kumekuwa na changamoto za kiusalama katika Jimbo la Singida Kaskazini kutokana na jiografia yake na rasilimali zilizopo:-

Je, ni lini Serikali itaongeza Vituo vya Polisi katika Kata ya Mughunga, Mgori na Merya ili kuimarisha usalama wa wananchi na mali zao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Justin Joseph Monko, Mbunge wa Singida Kaskazini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua uhaba wa vituo vya Polisi nchini ikiwemo Kata za Mughunga, Mgori na Merya. Hata hivyo huduma za kiusalama kwa wananchi wa Kata hizo zinatolewa na vituo vya Polisi vya Misange na Ngimwa kwa uratibu wa kituo cha Polisi cha Wilaya ya Singida Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ujenzi wa vituo vya Polisi kwa nchi nchi nzima unahitaji rasilimali fedha nyingi, Jeshi la Polisi limeweka vipaumbele vya kiusalama katika kutekeleza ujenzi wa vituo hivyo ikiwemo katika Kata ya Mughunga, Mgori na Merya na kadhalika kwa kushirikisha wadau mbalimbali wa maendeleo ikiwemo wananchi.
MHE. JUSTIN J. MONKO aliuliza:-

Mifugo ya Wafugaji wakubwa hapa nchini imekosa ubora wa mazao yake kutokana na maradhi ya nayo changi wa na kuko sekana kwa wataalam waliobobea katika fani na kukosa Maabara za Mifugo:-

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza wataalam ama vitendea kazi kama njia mbadala ya kuwasaidia wataalam wachache waliopo kutoa huduma bora kwa wafugaji?

(b) Je, ni lini Serikali itajenga maabara za mifugo katika maeneo ya wafugaji ili wananchi waache kutibu mifugo yao kwa kubahatisha?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Justin J. Monko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inafanya juhudi za kuongeza idadi ya Maafisa Ugani wa mifugo kwa kuwezesha Wakala wa Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo (LITA) kuongeza udahil i wa wanafunzi wa ngazi ya Astashahada na Stashahada katika fani za uzalishaji, afya ya mifugo, nyanda za malisho na maabara kutoka wanafunzi 2,536 mwaka 2018/ 2019 hadi wanafunzi 3,634 mwaka 2019/2020; sawa na ongezeko la wanafunzi 1,098 ambalo ni asilimia 43.3.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na mpango wa ujenzi wa maabara za mifugo kwenye kila mkoa. Mpaka sasa kuna maabara za mifugo za Serikali kumi na moja kwenye kila Kanda. Katika mwaka wa fedha 2019/2020 Wizara inategemea kujenga Kliniki za mifugo zenye maabara katika Halmashauri mbili za Chato na Meatu. Aidha, katika mwaka wa fedha 2020/2021, Wizara imepanga kujenga Kliniki nyingine kumi kwenye Halmashauri mbalimbali nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Sindiga Vijijini.

Mheshimiwa Spika, Wizara pia imeshavielekeza vituo binafsi 1,709 vya kutolea huduma ya afya ya mifugo (Private Veterinary Centers) vilivyopo kwenye Halmashauri zote 185 kuhakikisha vinakuwa na maabara ndogo kwa ajili ya kutoa huduma ya uchunguzi wa awali wa magonjwa ya mifugo.