Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro (26 total)

MHE. OTHMAN OMAR HAJI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini pamoja na hayo, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Sera ya Tanzania kuhusu Ukombozi wa nchi za Bara la Afrika na nje ya Afrika iliipatia heshima kubwa nchi yetu ya Tanzania. Nataka kujua Sera hii ya Ukombozi mpaka sasa inaendelea hasa kwa zile nchi ambazo bado hazijapata uhuru kama vile Sahara na Palestina?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, hivi karibu tulisikia kuzorota kwa mahusiano ya kidiplomasia kati ya Jumuiya ya Nchi za Ulaya na Tanzania mpaka ikapelekea mwakilishi wao kurudi nyumbani. Nini mustakabali wa kisera kwa pande hizi mbili ambazo zina mzozo huo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Othman Omar Haji, Mbunge wa Gando kwa maswali yake mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, ni wazi kwamba Tanzania imejijengea heshima kubwa sana katika Sera yake ya Ukombozi wa nchi mbalimbali Barani Afrika. Heshima hiyo bado ipo kwa Tanzania kwa sababu bado Sera ya Tanzania ya kupinga unyanyasaji, ukoloni na kutweza utu wa nchi yoyote ile inaendelea. Hivyo, msimamo wa Tanzania katika suala la Sahara pamoja na Palestina bado upo kama ambavyo ulikuwepo mara tu baada ya uhuru.

Mheshimiwa Spika, ikumbukwe kwamba Tanzania ni nchi ya kwanza duniani kuwa na Ubalozi Palestina. Bado tuna heshima hiyo na bado tuna mahusiano hayo mazuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili ni kuhusu mahusiano kati ya Tanzania na Jumuiya ya Ulaya. Mahusiano ya kidemokrasia na diplomasia kati ya Tanzania na nchi zote duniani yanaratibiwa na Mkataba wa Vienna wa mwaka 1961 na 1963.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa mkataba huo kila nchi inawajibu wa kuheshimu vipengele vya mkataba huo na endapo pande mmoja haitaheshimu vipengele vya mkataba huo, nchi nyingine ambayo imekosewa inawezaikachukua hatua stahiki. Na pale nchi inapochukua hatua stahiki haimaanishi kuwa mahusiano ya kidiplomasia yamevunjika hapana ni sehemu ya utekelezaji wa mkataba wa Vienna.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwakilisha.
MHE. ALLY SALEH ALLY: Mheshimiwa Spika, ahsante. Katika siku chache ambazo nimeridhika la jibu la Serikali, this is a very good answer from the Government. Kuna takwimu za kutosha, kuna maelezo ya kutosha. Hivi ndivyo ambavyo ningetarajia majibu ya Mawaziri wengine yawe kama haya. Nina maswali mawili ya ziada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, chuo chetu ni cha miaka mingi hivi sasa na kama uzoefu, basi upo wa kutosha: Je, Mheshimiwa Waziri katika muongo ujao, miaka kumi ijayo, anakionaje chuo chetu? Kitakuwa kimefikia hadhi na kiwango gani?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kada ya wana- diplomasia ni muhimu sana, kuna ambao tunaamini kwamba chuo hiki kinapaswa kuwa ndiyo alama ya Tanzania maana Career Diplomacy na hata Political Diplomacy wote wanapita hapa ili kwenda ku-shape sera na mitizamo na namna ya kuilinda na kuitetea Tanzania.

Je, kwa kiasi gani chuo hiki kinaweza kutumika kuwa ni think tank ya kujenga sera na mikakati ya kidiplomasia ili kwenda kuitetea nje kwenye ushindani na ukinzani wa Kidiplomasia?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Awali ya yote, nichukue fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Ally Saleh kwa pongezi alizozitoa kwa jibu ambalo tumelitoa. Pili, nichukue fursa hii kujibu maswali yake mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza aliuliza: Je, tunakionaje chuo kwa miaka kumi ijayo? Naomba tumweleze Mheshimiwa Ally Saleh, Mbunge wa Malindi pamoja na Watanzania wote kwamba Chuo chetu cha Diplomasia ni chuo ambacho kinaheshimika sana Barani Afrika. Umeona idadi ya nchi ambazo zimeleta wanafunzi hapa na zinaendelea kuleta wanafunzi hapa, hiyo ni ishara tosha kwamba heshima ya chuo hiki ni kubwa.

Mheshimiwa Spika, Mpango wa Wizara ni kukifanya Chuo hiki sasa kivuke mipaka kwenda nje ya mipaka. Tuna makubaliano ya awali na ndugu zetu wa Argentina waweze kukitumia chuo hiki kupata elimu ya Diplomasia. Hiyo ni ishara kwamba tunavyokwenda miaka kumi ijayo, yajayo yanafurahisha zaidi.

Mheshimiwa Spika, swali la pili aliuliza; je, Chuo kinaweza kuwa kama think tank? Hivi sasa kada ya Diplomasia inakuwa vizuri, tumepata wataalam wengi na sisi kama Serikali tunaendelea kuimarisha hiki chuo kwa kuweza kusomesha waatalam wengi zaidi na kuleta wengine kutoja nje kwa kupitia nyanja za ushirikiano ili kukifanya chuo hiki kiendelee kuheshimika na kitoe waatalam wengi watakaosaidia Tanzania katika Diplomasia.
MHE. USSI SALUM PONDEZA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nashukuru sana kwa majibu hayo mazuri ya
Mheshimiwa Waziri lakini je, Serikali ya Muungano au Wizara hii ya Mambo ya Nje inazishauri zile nchi wakati zina mpango wa kuja kutembelea Tanzania kuziarifu kuwa nchi yetu ya Tanzania ina sehemu mbili za Muungano na kila sehemu ina mahitaji yake ya kiuchumi. Hivyo basi, Wizara ingekuwa inazishauri kwa sababu ukiangalia nchi tisa tu ambazo zimekuja Zanzibar naamini zingekuja na hizi nchi nyingine 12 kuna fursa nyingi ambazo ziko Zanzibar ambazo bara hakuna na kuna fursa ambazo ziko bara ambazo Zanzibar hakuna.

Mheshimiwa Spika, tunaiomba Wizara iweze kuzishawishi wakati nchi za nje zinapoweza ku-engage kuja Zanzibar kuja kutembelea Tanzania. Basi iziambie kuwa Tanzania ina nchi mbili na nchi hizo mbili kila upande una vipaumbele vyake vya kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, swali la pili ambalo nataka niliseme, Wizara inafanya jitihada gani kuwashawishi wale viongozi ambao hawakuja Zanzibar kutembelea wakati wa ziara zao lakini kufanya ushawishi wakutane na viongozi wa Zanzibar huku Tanzania Barai ili wale viongozi wa Zanzibar waweze kutoa haja zao na kuweza kutoa ushahwishi wao wa kuiona Zanzibar nayo inanufaika na ugeni ule. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, nchi yetu ni nchi moja kwa mujibu wa Ibara ya 1 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977. Na masuala ya nje ni sual ala Muungano kwa m ujibu wa Ibara ya 4 nyongeza ya kwanza ya Katiba. Kwa hiyo, uhusiano wetu na mambo ya nchi za nje unachukulia maanani suala la kwamba ni nchi moja.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mahusiano yetu mara nyingi tukiwasiliana wanafahamu kwamba kuna nchi moja inaitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pamoja na hayo, Serikali na Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje imekuwa ikifanya jitihada kubwa sana kuhakikisha kwamba kwa sababu ya historia ya Muungano wetu na hali halisi kwamba ni Muungano ambao umetokana na nchi mbili tunahakikisha ya kwamba wakati viongozi hao wanapokuja nchini, tunajenga ushawishi mkubwa ili watembelee Zanzibar na ndiyo maana kuanzia 2015 mpaka sasa viongozi 21 waliotembelea nchini kwetu. Tisa kati yao wametembelea Zanzibar, vile vile ifahamike kwamba kuna wengine vile vile ambao wametembelea Zanzibar tu wala hawajatembelea upande mwingine wa Jamhuri.

Mheshimiwa Spika, naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kati ya masuala ambayo yanapewa kipaumbele sana katika uhusiano wa Kimataifa ni Muungano wetu ndiyo maana hata kwenye Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje kuna Idara maalum inahusika na mambo ya Zanzibar. Mualiko wowote au kiongozi yeyote akija ushawishi mkubwa unafanyika ili aweze kutembelea pande zote mbili za Muungano.

Mheshimiwa Spika, sasa mara nyingi kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi mara nyingine linakuwa ni suala la utashi wa kiongozi mwenyewe na hauwezi kumlazimisha. Kwa hiyo, nimueleze tu kwanmba kwa kweli Serikali inajitahidi sana kuhakikisha kwamba viongozi hawa wanapata fursa ya kutembelea maeneo yote na hasa kujaribu vile vile kuelezea kuhusu fursa za kiuchumi na za kitalii zilizopo Zanzibar.
MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Waziri, ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Mheshimiwa Waziri ametuambia kwamba wapo Watanzania zaidi ya milioni moja wanaishi nje ya Tanzania kama diaspora. Sheria ya Citizenship ya Tanzania inakataza uraia pacha. Je, ni lini Serikali ya Tanzania itabadilisha sheria hiyo na kuruhusu uraia pacha? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, mwaka 2014 Serikali ya Tanzania ilitoa uraia kwa wageni waliokuwa wanaishi kama wakimbizi 150,000 nchini Tanzania. Je, Serikali haioni kwamba kutoruhusu uraia pacha tunawanyima haki Watanzania wanaoishi nje ya nchi kuja kushiriki na kujenga nchi yao na kukaa na ndugu zao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nimshukuru Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo kwa swali lake zuri la msingi lakini na maswali yake mazuri mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza linahusu kubadilisha sheria ili kuruhusu uraia pacha. Suala la uraia pacha ni la Kikatiba, kwa hiyo kabla hatujaongelea sheria tunapaswa kwanza tukaongelee Katiba. Mchakato wa kubadilisha Katiba bado unaendelea, pale Katiba itakapobadilika na kuruhusu uraia pacha ndipo tutakwenda kurekebisha Sheria ya Uraia Na.6 ya mwaka 1995 ili kuongeza kipengele cha kuruhusu uraia pacha.

Mheshimiwa Spika, swali la pili anasema kwamba hatuoni kwamba kuzuia uraia pacha tunanyima haki. Watanzania hawa ambao wako nje tunaowaita diaspora, bado wanaendelea kufurahia haki nyingine ambazo zimetolewa hapa Tanzania ikiwemo haki ya kuwekeza kwa mujibu wa Sheria ya Uwekezaji ya mwaka 1997 na haki nyingine ambazo wangeweza kuzipata.

Kwa hiyo, tunashauri kwamba Watanzania hawa kwa hivi sasa na ambao wamefanya kazi nzuri sana kama ambavyo nimeeleza, ikiwemo kuleta misaada mingi sana katika huduma za afya na baadhi ya Majimbo kama Chakechake, Kondoa, Makunduchi, Kivungwe pamoja na Namanyere yamefaidika, bado tunaendelea kushirikiana nao na wanaendelea kufurahia haki zao kama diaspora.
MHE. MBAROUK SALIM ALI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Pamoja na majibu hayo nina maswali mawili madogo tu ya nyongeza. Katika majibu yake ya msingi Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba wananchi wa Pemba pamoja na wananchi wetu wa Tanzania tayari wameshaunganishwa na soko hili la Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Spika, bado niko kwa Pemba tu, nataka nijue kwamba hii Pemba imeunganishwa kinadharia au kivitendo kwa sababu karibu mwaka wa saba huu Viongozi Wakuu wa Afrika Mashariki walikubaliana kuijenga bandari ya Wete. Hizo ni jitihada na fedha kwa mujibu wa Naibu wa Wizara hii hii aliyepita ambaye kwa sasa hivi ni Naibu katibu Mkuu wa CCM Zanzibar alisema kwamba fedha tayari zilishakuwepo. Lakini mpaka leo hakuna lolote ambalo limefanyika nilitaka kujua ni nadhalia au ni vitendo.

Mheshimiwa Spika, hizo ni jitihada na fedha. Kwa mujibu wa Waziri wa Wiizara hii aliyepita ambaye sasa hivi ni Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, alisema kwamba fedha tayari zilishakuwepo, lakini mpaka leo hakuna lolote ambalo limefanyika. Nilitaka kujua, ni nadharia; ni vitendo?

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri katika jibu lake pia amewataka wananchi kwa ujumla watumie fursa zilizopo ili kulitumia soko la Jumuiya ya Afrika Mashariki. Niseme tu kwamba kuna vikwazo vikubwa vya tozo nyingi pamoja na ushuru hasa katika uzalishaji na usafirishaji wa bidhaa hizo:-

Je, ni lini Serikali nitaondoa tatizo hili hasa kwa wajasiliamali?

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Awali ya yote, namshukuru Mheshimiwa Mbarouk Salim Ali, Mbunge wa Wete kwa kuuliza maswali yake mawili ya nyongeza. Swali la kwanza amesema: Je, Pemba imeunganishwa kwa nadharia au kwa vitendo? Akitolea mfano ujenzi wa bandari kule Pemba.

Mheshimiwa Spika naomba kumjulisha Mheshimiwa Mbunge kwamba Pemba imeunganishwa kwa vitendo kwa sababu Pemba ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Jamhuri yote ya Muungano wa Tanzania imeunganishwa kwa vitendo kwa maana ya soko la pamoja, ambapo ndilo swali lake la msingi. Kwa maana ya mradi ya kimaendeleo ambayo ameisema, miradi hiyo inafanyika sehemu mbalimbali, sehemu zote za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kuhusiana na Bandari ya Pemba tulishajibu ndani ya Bunge hili kwamba Serikali kwa kushirikiana na Afrika Mashariki inashughulikia mradi huo.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, anasema kuna vikwazo vikubwa vya tozo na ushuru. Maana ya soko la pamoja ni kwamba endapo bidhaa inakidhi vigezo vya uasili wa bidhaa (rules of origin), haipaswi kutolewa ushuru au tozo yoyote endapo inasafirishwa au kuuzwa ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Bidhaa ambazo hazikidhi vigezo kama niliongea kwenye jibu la msingi, ni kwamba zimetolewa nje ya Jumuiya Afrika Mashariki, lazima zilipe ushuru au common external tariff ambayo imewekwa na Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. ALLY SALEH ALLY: Mheshimiwa Mwenyekiti, base ya swali langu ni kwamba na-target Jumuiya, Nchi Wanachama na wananchi wanafaidikaje na hali hiyo. Sasa uchaguzi wa Serikali za Mitaa ndio chanzo cha awali kabisa cha kupima utawala bora kwa upande wa haki ya kuchagua na kuchaguliwa, haki ya maoni na kujieleza kwa hapa njia ya kufanya kampeni, lakini pia ni kigezo cha kupata Serikali Shirikishi kadri inavyowezekana.

Je, kwa hali hii ya wagombeaji kutoka upande wa upinzani kukatwa kwa zaidi ya asilimia 90. Je, Tanzania haioni kwamba inakiuka matakwa hayo ya Afrika Mashariki?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kwa matukio tunayoyaona hapa nchini madai ya haki za binadamu ambayo hata Human Right International Watch juzi imetutaja lakini pia kwamba ku-shrink kwa public space pia kuwanyima wananchi fursa ya kuona Bunge live, kuwaweka mashehe wa kiislamu kwa miaka saba ndani bila kuwafungulia shauri na pia kutokuwa na Tume Huru…

MWENYEKITI: Sasa Mheshimiwa Ally Saleh, swali unaongeza, unaongeza uliza mawili tu moja tayari, la pili malizia.

MHE. ALLY SALEH ALLY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Je, Serikali ya Tanzania haioni kwamba haikidhi vigezo vya kuwa na utawala bora na haki za binadamu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza anasema je, Tanzania haikiuki viwango kwa mujibu wa Afrika Mashariki. Tanzania ni nchi ambayo inafuata misingi ya utawala bora, misingi ya haki ya binadamu kama ambavyo imeainishwa kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na nyaraka nyingine za Kimataifa. Endapo kunatokea malalamiko yoyote tumesema bayana kupitia Afrika Mashariki, yeyote ambaye amekwazwa na lolote anaweza akaenda kulalamika kupitia Bunge la Afrika Mashariki pia kupitia Mahakama ya Afrika Mashariki na Serikali ya Tanzania ndio imeamua kuwa mwanachama ili kuwapa fursa wananchi wake kutoa malalamiko kwenye vyombo hivyo. Hicho ni kitendo cha wazi kabisa kwamba Serikali hii inaweza na inajali haki za binadamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, amesema pia kuna malalamiko kuna Human Right International Watch; malalamiko yanatoka mengi sana, ni vizuri yachunguzwe, yanatoka wapi, yanaletwa na nani na kwa nia ipi na yakifika yashughulikiwe kwa mujibu wa muundo ambao unao. Hata hivyo, nimhakikishie Mheshimiwa Ally Saleh (Alberto), Mbunge wa Malindi kwamba Tanzania ni nchi ambayo inaheshimu sana haki za binadamu, demokrasia na utawala bora. (Makofi)
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS NYIMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza kabisa pia nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuunga mkono jitihada za Mheshimiwa Rais wetu kuweza kuirudisha ndege yetu Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la nyongeza litakuwa moja; je, Waziri anaweza kutuambia ni njia gani zinazotumika kwa viongozi wa Wilaya na Mikoa kufuatilia ahadi zinazotolewa na viongozi hawa wanapokuja nchini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Tauhida kwa kazi nzuri ambayo anaifanya kule Zanzibar akiwakilisha wananchi. Amefanya mambo mengi, ametoa kompyuta na kujenga madarasa ya kompyuta na amekuwa akijulikana kama ni rafiki wa wanawake na watoto. Swali lake ni ushahidi tosha kwamba anafanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kupitia Idara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Zanzibar inashirikiana kwa karibu kabisa na viongozi wa Wilaya na Mkoa pamoja na Ofisi ya Rais kule Zanzibar, katika kufanya vikao vya mashauriano ili kuona kwamba ahadi ambazo zimetolewa na hazijatekelezwa zinatekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, niwashauri Mheshimiwa Tauhida tuendelee kushirikiana kupitia viongozi wa Wilaya, Mkoa, Wizara za Kisekta, Ofisi ya Rais Zanzibar pamoja na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki katika kuhakikisha kwamba ahadi zote zinatekelezwa. Kama kuna ahadi sugu ambayo haijatekelezwa nitamuomba tuonane ili tuweze kuitekeleza haraka iwezekanavyo.
MHE. OTHMAN OMAR HAJI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa mujibu wa maelezo ya Serikali ni kwamba APRM Tanzania inafanya shughuli zake chini ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa. Kwa sababu hiyo basi, itawezaje kuisimamia Serikali na kutoa majibu yaliyo sahihi kwa wananchi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, moja kati ya masharti ya APRM kwa wanachama wake ni kwamba mwanachama anatakiwa akubali kufanyiwa tathmini na wanachama wenza. Je, ni mara ngapi Serikali ya Tanzania imewahi kufanyiwa tathmini hii na wanachama wenzake?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, napenda kumpongeza Mheshimiwa Othman Omar Haji, Mbunge wa Gando kwa maswali yake mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, ukisoma mkataba ambao umeanzisha APRM, inaongozwa na Baraza la Usimamizi la Taifa ambalo ni huru, linachaguliwa kutoka kwa watu mbalimbali, asasi za Kiserikali, vyama vya kisiasa na watumishi wa upande wa Serikali. Baraza hilo ni huru katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa kifungu cha 16 cha mkataba huo na kwamba iko chini ya Wizara lakini muundo na utendaji wake unawahakikishia kwamba baraza hilo liko huru na wala haliwezi kuingiliwa na mtu yeyote.

Mheshimiwa Spika, swali la pili la kuweza kuhakikiwa au kufanyiwa tathmini na wanachama wenza. Naomba tu nimkumbushe Mheshimiwa Othman Omar Haji kwamba APRM ilianzishwa na nchi za Kiafrika ili kuweka viwango vya kujitathmini ambavyo vinakubalika na Afrka na nchi za Kiafrika. Kwa hiyo, Tanzania imeruhusu nchi nyingi za Afrika, SADC na Afrika Mashariki kuweza kushiriki kwenye tathmini na kuweza kuzitathmini kwa mara nyingi zaidi. Ahsante.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kujibu maswali vizuri kwa mara ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini napenda Serikali itambue kwamba wananchi wa Urambo wanashukuru kupata hifadhi lakini kwa kuwa kulikuwa na mgogoro wa muda mrefu tangu 2013/2014 kuhusu mipaka, je, Serikali haikuona kwamba kuna haja ya kumaliza ile migogoro kabla ya kuwa na hifadhi ili wananchi waendelee na maisha yao ya kufuga nyuki ambao sasa hivi hawaruhusiwi kufuga mifugo na kulima?

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, lini Mheshimiwa Waziri atakuja ajionee mwenyewe kwa sababu mpaka sasa hivi wameshakuja Naibu Mawaziri wawili, alishakuja Mheshimiwa Ramo wakati ule, Mheshimiwa Naibu Waziri Angelina Mabula alikuja na pia alikuja Mheshimiwa Kiwangalla aliyekuwa Waziri lakini bahati mbaya mvua ilinyesha hakuweza kufika maeneo yale. Je, ni lini Serikali inakuja ione jinsi ambavyo wananchi wanataka maeneo waendelee kuendesha maisha yao kwa kilimo, kufuga nyuki na mifugo pia?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kuhusiana na suala la mgogoro, Serikali inayoongozwa na Chama cha Mapinduzi siku zote imekuwa ikishirikiana na wananchi wake katika kutatua changamoto mbalimbali. Migogoro ya ardhi imeshapatiwa suluhisho kupitia Tume ya Mheshimiwa Rais ya Mawaziri Nane iliyoongozwa na Mheshimiwa Lukuvi. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Margaret Sitta kwamba suala hilo nalo limeshapatiwa ufumbuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili kuhusiana na lini tutakwenda? Nimhakikishie Mheshimiwa Margaret Sitta mara baada ya Bunge hili nitaambatana naye kwenda jimboni Urambo kuhakikisha tunatatua suala hili. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, naomba niweke wazi tu kwanza kwamba sijaridhika na majibu ya Mheshimiwa Waziri na Wizara kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla wake sekta ya utalii kwa Mkoa wa Arusha na nchi nzima imeathirika sana. Wananchi wengi sana wamekosa ajira, madereva wamekosa ajira kwa sababu magari hayatembei kutokana na uchache wa watalii, guides wamekosa ajira, wafanyakazi wa mahoteli wamepunguzwa kwenye maeneo yao, magari ambayo yangetembea, yangeweka mafuta shell zingeweza kufanya biashara zao.

Mheshimiwa Spika, tukiangalia kwenye ukanda wa Afrika Mashariki, karibu nchi nyingi zimeweza kupunguza tozo kipindi hiki. Mfano, Kenya, Nairobi National Park wamepunguza tozo kutoka Dola 43,000 mpaka 35,000. Ukienda Rwanda kwenye masuala ya gorilla wamepunguza kutoka Dola 1,500 mpaka Dola 500. Ukienda Uganda kwenye masuala pia ya gorilla wamepunguza kutoka Dola 700 mpaka 500. Naomba Wizara ya Maliasili na Utalii iangalie athari za ugonjwa wa Corona kwenye masuala ya ajira na masuala mengine.

Mheshimiwa Spika, swali langu la nyongeza, Wizara ya Maliasili na Utalii ina mpango gani wa kuipa ahueni sekta ya utalii ili kuweza kunusuru changamoto kubwa ya ajira ambayo imewaathiri wananchi wa Mkoa wa Arusha pamoja na Tanzania kwa ujumla?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kama ambavyo Mheshimiwa Gambo ametoa takwimu, wenzetu wamepunguza kutoka Dola 1,500 mpaka 1,000, kutoka Dola 700 mpaka 500; hizo ndiyo takwimu zake. Viwango vya kuingia katika hifadhi zetu bado viko chini sana ukilinganisha na ubora wa hifadhi tulizonazo. Ukisema Serengeti hulinganishi na hifadhi yoyote iliyoko katika Afrika Mashariki; kule Rwanda unaona gorilla tu. Serengeti is a jewel, bado ni Dola 60. Kwa hiyo, viwango bado viko chini sana. Nilitaka kwanza hilo niliweke sawa.

Mheshimiwa Spika, la pili, Serikali inatoa tahafifu gani hasa kwa kipindi hiki? Wizara imegawa suala la utalii katika misimu miwili; high season na low season. Ongezeko hilo ambalo tunalisema litagusa kwenye high season tu; low season bado rates zitabaki pale pale.

Mheshimiwa Spika, hii ni kwa nini? Katika high season, sehemu kama Ngorongoro kwa siku moja yanaingia magari 400 ambayo yanaathari kubwa kiikolojia wakati kwenye low season yanaingia magari 70. Tunataka tu-balance sasa, hawa wafanyabiashara wetu ambao tutawapa tahafifu, waende sasa kwenye low season ili tutunze pia na ikolojia iliyopo.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, AJIRA, KAZI, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, pamoja na kuunga mkono majibu mazuri yaliyotolewa na Wizara ya Maliasili na Utalii, lakini swali la msingi na maswali ya nyongeza yamegusa pia sekta ya ajira katika sekta hiyo ya maliasili.

Mheshimiwa Spika, naomba kuliambia Bunge lako Tukufu, wakati wa Covid, hata sasa na hata baadaye, kama kunatokea tatizo lolote linalohusiana na suala la wafanyakazi, tunaomba wafanyakazi, waajiri watumie platform yao ambayo ni ya dhana ya utatu ambayo tumekuwa tukiitumia mara nyingi kuamsha mijadala na kutafuta solution katika mazingira ya mawanda hayo ya sekta ya kazi, ajira na Serikali. Kwa hiyo, nawashauri watumie platform hiyo.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Miaka 20 iliyopita ndani ya Jimbo la Momba Ivuna, kuna kimondo kidogo kilidondoka (Ivuna Meteorite) na kikachukuliwa na watu wa NASA. Je, Serikali ina mpango gani wa kufuatilia kimondo hiki kwa ajili ya kukirudisha na kuendelea kuongeza idadi ya watalii nchini? (Makofi)
WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nampongeza kwanza Mheshimiwa Condester kwa kazi nzuri anayowafanyia wananchi wa Momba na ndiyo maana walikuchagua kwa kura nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara kwa kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, imeshaanza kufanya mawasiliano na Balozi wetu aliyeko nchini Marekani kuanza kufuatilia jambo hili. Tutakapopata majibu, tutamjulisha Mheshimiwa Condester na Bunge lako Tukufu. Ahsante.
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Makao Makuu ya TANAPA Kanda ya Magharibi yako Bunda; na kwa kuwa Halmashauri ya Mji wa Bunda ilitoa eneo kwa ajili ya kujenga ofisi zao za Kanda ya Magharibi. Je, ni lini TANAPA wataanza kujenga ofisi hizo? (Makofi)
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, nimshukuru Mheshimiwa Robert Maboto kwa swali lake hilo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, TANAPA ina kanda nyingi nchi nzima na kila kanda inahitaji fedha ili tuweze kujenga miundombinu husika. Katika bajeti ambayo tutaileta mwaka huu tumeomba fedha kutoka Hazina ambazo ni mahsusi kwa ajili ya kujenga na kuboresha miundombinu ikiwemo Ofisi ya Kanda ya TANAPA pale Bunda.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa tatizo la mifugo kuingia katika hifadhi za Sikonge linafanana kabisa na tatizo lililopo katika Wilaya ya Namtumbo kwenye eneo la Hifadhi ya Selous au sasa hivi Mwalimu Nyerere, mifugo mingi iliyofukuzwa kutoka Morogoro imeingia katika hifadhi hiyo na kuharibu ecology ya tembo na sasa tembo wamekuwa wanakuja katika vijiji wanapoishi wananchi na jana wameuwa Imam wa Msikiti katika Kijiji cha Luhangano, Kata ya Mputa, Je, Serikali itafanya nini kuondoa mifugo hiyo na kutuletea askari wakae kule moja kwa moja kuzuia tembo kuleta madhara ya vifo kama yaliyotolea jana?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Kawawa kwa kazi nzuri anayowafanya wananchi wa Jimbo la Namtumbo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli tumekuwa na changamoto ya mifugo kuingia katika hifadhi ambayo inasukuma wanyamapori wakiwemo tembo kuja sasa kwenye maeneo ya wananchi. Tunaendelea na operation ya kuondoa mifugo hiyo na kuwarudisha tembo katika maeneo yao stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, operations zinaendelea jana tu tumefanya operation katika Wilaya ya Tunduru na msiba anaosema katika Kijiji cha Mputa tayari Maafisa Wanyamapori watawa wapo Mputa hivi sasa kushughulikia suala hilo. Naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Spika, katika Bunge la Februari nilitoa ombi kutokana na majibu hayo kwamba Kijiji cha Ngombo ambacho kinatajwa kihame tuliomba tuko radhi kipunguziwe ukubwa wa mipaka na kupunguza mifugo Zaidi ya 90% ili wananchi waweze kubaki sehemu iliyobaki ichukuliwe kwa ajili ya uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, lakini pia eneo kubwa la Jimbo huo mpaka wa 2017 tuliomba tupewe walau mita 700 kama siyo kilomita 1 kwa ajili ya shughuli za kiuchumi kwa maana umbali sehemu ambayo tunafanya shughuli mpaka mto ni mrefu sana tofauti na ambavyo inasemwa kiujumla. Kwa hiyo, je Serikali iko radhi kuridhia maombi haya?

Mheshimiwa Spika, la pili, majibu ya Naibu Waziri kuhusu wanashughulikia hii Tume ya Mawaziri nane ni tangu mwaka jana wanasema tunashughulikia tutajibu tutajibu watu tuko pending hatufanyi shughuli za kilimo, hatujui hatma yetu. Lini hasa Serikali itatoa msimamo wa mwisho juu ya jambo hili ili tuendelee kuwaza mambo mengine tulimalize?

Mheshimiwa Spika, la tatu, kwa wale ambao tayari wameshalima Wizara inaridhia kipindi hiki tuweze kuvuna? Ahsante
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ningependa kutoa ufafanuzi kwa Mheshimiwa Antipas kwamba mipaka ya Bonde Tengefu la Kilombero iliwekwa mwaka 1952 kwa GN Namba 107 na ikarejewa mwaka 1997. Mipaka hiyo haijawahi kurekebishwa mpaka sasa kilichofanyika ni wananchi wa maeneo mbalimbali kuvamia maeneo hayo na kutokana na uvamizi huo Serikali ikachukua hatua ya kuunda kamati maalum ya Mawaziri ikiongozwa na Waziri Mwandamizi Mheshimiwa William Vangimembe Lukuvi ambapo taarifa yake imefikia hatua ya mwisho tunaenda kutoa tathimini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo maombi hayo yote tayari Mawaziri walishakwenda kule wamefanya tathmini ripoti iko tayari na watajulishwa wananchi. Kuhusiana na kulima hatuwezi kuendelea mtu kulima ndani ya hifadhi. Kwasababu mpaka unajulikana unaposema unaomba tulime maana yake unataka tulime ndani ya hifadhi madhara ya kulima ndani ya hifadhi hii ni kuhujumu mradi wa umeme wa Mwalimu Nyerere. Kwa hiyo, tusubiri maelekezo ya kamati maalum ya Baraza la Mawaziri tutajua hatma ya suala hili.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Serikali ina mpango gani wa kuutangaza utalii wa ndani kwa kutumia Wabunge pamoja na Halmashauri zetu? Naomba kuwasilisha. (Makofi)
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana nimpongeze Mheshimia Asia kwa swali lake hilo zuri pia nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango mkakati kabisa wa kushirikiana na Halmashauri zote na Serikali za Mikoa na Wilaya katika kutangaza Utalii ikiwemo kuwatumia Wabunge pia katika kutangaza utalii. Ni wazi umeona tayari Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri na baadhi ya Wabunge tumeshaanza kushirikiana nao kuhakikisha kwamba tunatangaza utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiongezea kwenye majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri ni kwamba maelekezo ya Mheshimiwa Hayati Dkt. Magufuli yalikuwa ni kwamba tupunguze gharama za utalii ili kuwezesha Watanzania wengi zaidi na watalii wengi zaidi kwenda kwenye sehemu za vivutio vya Utalii, zoezi hili tumeshalianza tunaamini gharama hizo zitashuka na Watanzania waweze kufaidi maliasili zao. (Makofi)
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi kwa kuwa utalii unakwenda kwa package na mbuga ya Katavi pamoja na hifadhi nyingine ni sehemu ya utalii kusini na kituo cha utangazaji na taarifa zote kinatakiwa kujengwa Iringa katika sehemu inayoitwa Kisekiroro ni lini Serikali itaanza ujenzi huo?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa kituo hicho unafadhiliwa na Benki ya Dunia katika Mradi wa RIGRO. Mradi huo ulichelewa kidogo kutokana na tatizo la COVID ambalo liliwakuta nchi mbalimbali ikiwemo wafadhili wa Mradi huo. Sasa hivi tayari mradi huo umeshaanza, jana Katibu Mkuu amekabidhi magari 12 kutokana na mradi huo kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Jesca na Wabunge wote wa Iringa na Nyanda za Juu Kusini kwamba kituo hicho kitajengwa haraka iwezekanavyo.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa kuuliza swali la nyongeza. Ni dhahiri kwamba kwa Afrika nchi yetu inahifadhi nzuri inawanyama wengi ukienda Ruaha ukienda Serengeti, Ukienda Tarangire na maeneo mengine…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Bulaya ukipewa swali la nyongeza usianza na utaalam mwingi nenda straight to the question.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mikakati ya Serikali ni ile ile ya kushiriki matamasha ya Kimataifa, kutangaza kwenye TV lakini bado hayajatuletea manufaa chanya ya ongezeko la watalii kulingana na vivutio vyetu na hifadhi zetu.

Je, hamuoni kwamba ni wakati muafaka wa kuwa na mikakati Madhubuti ya kiushindani ili idadi ya watalii iendane na hifadhi zetu na vivutio vyetu? (Makofi)
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nimshukuru Mheshimiwa Ester Bulaya kwa swali lake hilo, takwimu zetu zimeonesha kwamba idadi ya watalii imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka. Ongezeko hilo limetokana na juhudi ya Serikali ambayo imeifanya katika kutangaza utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma Ilani ya Chama Cha Mapinduzi imeelekeza wazi kwamba tuje na mazao mapya na mikakati mipya katika kutangaza utalii, mikakati yote ipo mezani iko tayari kinachotukwamisha ni gonjwa hili la Covid, nimhakikishie Mheshimiwa Ester Bulaya pindi ugonjwa huu utakapokwisha ataona ongezeko kubwa la watalii hapa Tanzania, ahsante. (Makofi)
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, napenda kumshukuru Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Naibu wake, walipokuja jimboni kwetu walichukua hatua kuhusu askari wa TAWA, baadhi ambao walikuwa wakiwaonea wananchi wetu. Na kuwa Mheshimiwa Waziri aliahidi pale katika mkutano ule kwamba atatujengea soko la samaki, Ifakara, Kilombero. Naomba kuiuliza Serikali ni lini ahadi ile nzuri ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii itaanza?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Asenga kwa kuuliza swali hilo na kujali wananchi wake:-

Mheshimiwa Spika, mpango wa kujenga soko katika Daraja la Mto Kilombero upo katika bajeti ya Wizara katika mwaka huu 2021/2022. Kwa hiyo, mara baada ya bajeto hiyo kupitishwa mkakatin huo utaanza.
MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kuniona.

Kwa kuwa mgogoro unaoendelea kati ya askari wetu wa uhifadhi na wananchi wanaozunguka katika msitu wa Marang unafanana kabisa na mgogoro unaoendelea hivi sasa kati ya wananchi wa vijiji vya Kimotorok kwa upande wa Simanjiro na Kijiji cha Kiushiuborko kwa upande wa Kiteto dhidi ya pori la Mkungunero Game Reserve askari wanaoishi Mkungunero Game Reserve na kwa kuwa mgogoro huu ni wa muda mrefu na ulifikia Serikali kukubali kurudisha eneo ambalo walipima kwa makosa kinyume na GN iliyotakiwa Mkungunero Game Reserve imebaki Kondoa sasa imevuka mipaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itaamua sasa kuja kukaa na wananchi wa vijiji vinavyozunguka Mkungunero Game Reserve kumaliza mgogoro huu ili kuepusha maisha wa watu na vitendo vinavyofanana na hivi ambavyo Waziri akihitaji, hata hapa ndani nitoe ushahidi wa vitendo vya kinyama walivyofanyiwa wananchi wa Kimotorok na wahifadhi, nitakupa kwenye simu yangu hii? Nitakupa nashukuru sana naomba swali langu lijibiwe. (Makofi)
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa ufafanuzi ambao aliutoa awali, lakini pia niweze kumjibu Mheshimiwa Ole-Sendeka kwamba tunapotaka kutatua tatizo lazima twende kwenye kiini cha tatizo. Wote tunajadili hapa na hakuna siri ni kweli yanatokea mapigano kati ya askari wa Maliasili pamoja na wananchi, lakini mapigano haya yanatokea ndani ya maeneo ya hifadhi.

Kwa hiyo kwanza Mheshimiwa Ole-Sendeka na Waheshimiwa Wabunge wote tusaidiane kuelimisha wananchi wetu kwanza tusiingie, na endapo wananchi wanaingia kwa bahati mbaya na akatendewa visivyo tutoe taarifa, tupate huo ushahidi, tuwawajibishe askari hawa ambao hawafanyi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeshawawajibisha askari kadhaa, nilitoa takwimu hapa, askari 61 tumewafukuza kazi kwa sababu ushahidi umeletwa. Kwa hiyo, niwaombe Waheshimiwa Wabunge pale wananchi wetu ambapo wanafanyiwa ndivyo sivyo tuletewe ushahidi ili tuwashughulikie askari hawa, lakini na sisi tuna wajibu wa kuwashauri na kuwaelekeza wananchi wetu tusiingie kwenye maeneo haya yaliyohifadhiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pili ameongelea suala la Mkungunero, tulifanya kikao mimi Mheshimiwa Lukuvi pamoja na Mheshimiwa Olelekaita kuhusiana na Mkungunero kuhusiana na dispute ya mpaka wa Mkungunero na tukakubaliana tunapeleka wataalam kwenda kuhakiki mpaka huo kwa mujibu wa coordinates ambazo zimewekwa kwenye GN. Niseme hapa kuna tatizo moja, katika maandishi katika maneno imesema ni Wilaya ya Kondoa lakini coordinates zimefika Wilaya ya Kiteto, sasa kitaalam zile coordinates zina prevail, kwa hiyo, wataalam waende wakatuoneshe coordinates hizi zinatakiwa kuvuka au zisivuke ili tutatue mgogoro huo.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. DKT. THEA M. NTARA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Suala hili limekuwa lina muda mrefu sana, na watoto wanazidi kunyanyasika kwa kuolewa na umri mdogo; je, Serikali imejiwekea muda gani wa kufanya marekebisho hayo ya sheria?

Mheshimiwa Spika, swali labgu la pili; hivi hamwoni kwamba ipo haja ya kusitisha suala la maoni ya wadau, kwa sababu suala hilo ni wazi halafu hao wadau wengi ni hao hao wanaopenda kuoa watoto wadogo?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa majibu kwa swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Thea Ntara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, baada ya Mahakama ya Rufani kutoa maamuzi kwamba Serikali ibadilishe umri wa chini wa mtoto kuweza kuoa au kuolewa, Serikali ilileta mapendekezo hapa Bungeni. Bunge lako tukufu ndilo liliagiza Serikali ikachukue maoni zaidi kutoka kwa wadau mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, maelekezo hayo tumeyatekeleza, tumekamilisha na tuko tayari sasa kuja mbele ya Bunge ku-share maoni hayo pamoja na mapendekezo yaliyowekwa Mezani. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa, hapa Bungeni nyie mnapaswa kuleta Muswada. Ndiyo unamaanisha mko tayari kuleta Muswada? Kwa sababu maoni na mapendekezo, maana yake unayaleta kule ofisini, siyo hapa ndani. Sasa nataka nielewe vizuri, mnaleta Muswada au mnaleta hayo maoni na mapendekezo? Kwa maana maoni na mapendekezo hayawezi kuja hapa Bunge, hapa Bungeni tunasubiri Muswada.

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, tuko tayari kuleta Muswada. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri pamoja na kutaka kuwasaidia watoto hawa wa kike lakini mahakama ilisema sheria ya ndoa ibadilishwe;

Je, ni lini Serikali mtaanza kutekeleza sheria hiyo na kubadilisha ili tusiwe na watoto wengi ambao wanaozeshwa wakiwa na umri mdogo?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, ninaomba kujibu swali la kwanza la Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari Serikali ilitoa maelekezo katika Bunge lako Tukufu, kwamba mchakato wa kukusanya maoni kwa ajili ya kurekebisha sheria ya ndoa umekamilika, na kwamba tarehe 26 Aprili, yaani kesho, kutakuwa na kongamano la mwisho kupitia maoni hayo na baada ya hapo Serikali italeta muswada huo Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali dogo la nyongeza. Kiutaratibu Mahakama inapokuwa imetoa maelekezo kwenye jambo hili la watoto wa kike kuolewa chini ya umri, Mahakama ilishatoa maamuzi kwamba Serikali ilete mabadiliko ya sheria Bungeni.

Swali langu, Serikali imepata wapi nguvu ya kukiuka maamuzi ya Mahakama ya kuleta Muswada wa Sheria Bungeni na badala yake inakwenda kukusanya maoni ya wadau kuhusiana na sheria hii? (Makofi)
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salome Wycliffe Makamba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Mahakama ya Rufani kutoa maamuzi ya mwisho kuhusiana na jambo hili, Serikali ilileta Muswada hapa Bungeni. Muswada huo ulipokelewa na kwa maelekezo ya Bunge lako tukufu tulielekezwa na Bunge tukakusanye maoni zaidi. Kwa hiyo ilichokifanya Serikali ni maelekezo ya Bunge, otherwise Serikali ilishaleta Muswada hapa. Tumetekeleza hayo maelekezo ya Bunge na tuko tayari kurudi tena kupokea maoni mengine ya Bunge itakavyoona inafaa. (Makofi)
MHE. DKT. THEA M. NTARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ubakaji na ulawiti kwa watoto ni zaidi ya uuaji. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuondoa dhamana kwa wale wanaume wanaolawiti na kubaka watoto? (Makofi)
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Thea Ntara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania dhamana ni haki ya mtuhumiwa na inaweza ikaondolewa tu pale ambapo inaonekana ni muhimu na mazingira yanalazimisha lazima iondelewe. Katika kesi nyingine zote hizi discretion ya kuondoa dhamana inabakia kwa Mahakama, endapo Mahakama itaridhika kwenye mazingira haya, huyu mtu asipate dhamana, basi hatapata dhamana hata kesi hizo za ulawiti na ubakaji kama ambavyo Mheshimiwa ameuliza. (Makofi)
MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru nina swali moja dogo la nyongeza.

Kwa kuwa, idadi kubwa ya mahabusu walioko kwenye magereza zetu wanaipa mzigo mkubwa sana Serikali yetu kuwahudumia. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuleta sheria ambayo itawezesha watuhumiwa wakapewa nafasi ya kujidhamini wenyewe ili kuipunguzia Serikali mzigo na kuwapunguzia adha wananchi wanaotekesaka kwenye magereza, kwa makosa mbalimbali ambayo kimsingi yanaweza kudhaminika?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Elibariki Immanuel Kingu, Mbunge wa Singida Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la mtuhumiwa kujidhamini au kudhaminiwa ni kuhakikisha kwamba anarudi mahakamani kwa tarehe itakayotakiwa. Kwa hivi sasa Serikali imejikita katika mpango wa kuweka anwani za makazi pindi zoezi hili litakapokamilika tutakuwa na uwezo wa kujua kila mtu anaishi wapi, hivyo kutakuwa na uwezekano wa kujidhamini wenyewe. Kwa hiyo, kazi ambayo Mheshimiwa Nape anaifanya ikikamilika, pamoja na vitambulisho vya Taifa NIDA, itawawezesha Watanzania kujidhamini wenyewe, hivyo kupunguza msongamano wa mahabusu ambao watakuwa wako nje. (Makofi)
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa kero kubwa ya msongamano wa mahabusu na wafungwa magerezani imekithiri. Je, Serikali inaonaje ikaleta utaratibu wa vifungo vya nje kwa makosa madogo madogo ili kupunguza msongamano huo? Ahsante.
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Njau, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunapitisha bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria mwaka huu, tulisema moja kati ya vipaumbele ni kwenda kuangalia upya, kuufumua na kuupanga upya mfumo wa jinai hapa nchini. Katika mpango huo moja kati ya jambo ni hili kuangalia adhabu mbadala ambazo zitasaidia kupunguza msongamano wa mahabusu magerezani. (Makofi)
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, kwa mujibu wa takwimu za Serikali ya mwaka 2016 zinaonesha kwamba ni asilimia 19 tu ya wanawake ambao wanamiliki ardhi wakati wanachangia takribani asilimia 54 ya uzalishaji katika kilimo ambao ndiyo uti wa mgongo wa uchumi. Nina maswali mawili ya nyongeza: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; Je, Serikali imeweka kipaumbele gani kuhakikisha kwamba umiliki wa ardhi kwa wanawake unaongezeka kwa kuipa uhai na meno Sheria Na. 4 na Sheria Na. 5.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; mila, tamaduni na desturi ni kati ya sababu kubwa ambazo zinachangia kutokumiliki ardhi kwa wanawake. Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba sheria za kimila za umiliki ardhi, pamoja na sheria zingine ambazo zinakinzana na Sheria Na. 4 na 5 haziwi juu ya hii Sheria Mama ya Umiliki wa Ardhi wa Sheria Na. 4 na Sheria Na. 5? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Neema Kichiki Lugangira, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la kwanza, ni kweli idadi ya wanawake ambao wanamiliki ardhi hapa Tanzania bado ni ya chini na hiyo haisababishwi na sheria, inasababishwa na mtazamo wa jamii, inasababishwa na mila na desturi zetu ambazo ni lazima sasa tushirikiane kati ya Serikali na Asasi za Kiraia, kati ya Serikali na Wadau wote kutoa elimu kuhusu haki ya mwanamke kumiliki ardhi kwa mujibu wa Katiba kama ambavyo imeelezwa kwenye Ibara ya 24, lakini pia kama ambavyo imeelezwa katika Sheria ya Ardhi, Kifungu cha 3(2).

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na swali la pili, Sheria hizi za kimila zimekuwepo toka zamani lakini ni wazi kama ambavyo Mheshimiwa Neema amesema zinakinzana na haki za wanawake ambazo zimeelezwa kwenye Katiba na Mikataba mingine ya Kimataifa ambayo tumesaini. Hivyo basi, sisi kama Serikali tumejipanga kuzipitia upya sheria hizi ili kuweza kupendekeza mabadiliko na endapo Bunge lako litaridhia, basi kadhia hii itaweza kuondoka kabisa.