Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro (17 total)

MHE. OTHMAN OMAR HAJI aliuliza:-

Moja kati ya malego makuu ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ya Mwaka 2017/2018 ilikuwa ni kukamilisha kuandaa Sera mpya ya Mambo ya Nje:-

(a) Je, mpango huo umefikia wapi?

(b) Je, ni maeneo gani mapya kisera?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako na kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Othman Omar Haji, Mbunge wa Gando lenye vipengele (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara imekamilisha kuandaa Rasimu ya Sera ya Mambo ya Nje kama ilivyopendekezwa na wadau wakati wa zoezi la kufanya tathmini ya utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje ya 2001. Rasimu hiyo ya Sera hivi sasa ipo katika hatua ya kusambazwa kwa wadau mbalimbali kama vile Wizara, Idara na Taasisi za Serikali, sekta binafsi na taasisi zisizo za Kiserikali ili kupata maoni yao yenye lengo la kuiboresha zaidi.

Mheshimiwa Spika, maeneo mapya ambayo yamejumuishwa katika Sera inayopendekezwa ni pamoja na: Kuwatambua na kuwajumuisha Diaspora kwenye juhudi za kuleta maendeleo ya Taifa; kutambua mihimili mingine kama wadau wa sera yaani Bunge na Mahakama; kuzingatia mikakati na mipango ya muda mrefu ya nchi na Jumuiya za Kikanda na Kimataifa; utekelezaji wa Sera kufikia hadi ngazi ya Wilaya na Mikoa (Decentralization of Foreign Policy conduct); na vijana na tasnia ya michezo na burudani kutumia kama njia ya kuitangaza Tanzania nje. Aidha, Rasimu ya Sera inaelekeza nchi kuimarisha mahusiano na nchi nyingine yanayolenga kukuza uchumi wa nchi kwa kuzingatia mipango ya Serikali ya muda mfupi na mrefu.
MHE. ALLY SALEH ALLY aliuliza:-

Chuo cha Diplomasia kimekuwa na umuhimu mkubwa katika masuala ya kidiplomasia na uwakilishi wa Tanzania nje ya nchi.

(a) Je, Chuo cha Diplomasia kimetoa wahitimu wangapi na mgawanyiko wake ukoje hadi sasa?

(b) Je, wahitimu wangapi hadi sasa wamepanda na kuwa Career Diplomats?

(c) Diplomasia inaenda sambamba na mawasiliano, je, Serikali haijafikiria kuongeza lugha zinazofundishwa chuoni hapo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali namba 118 kutoka kwa Mheshimiwa Ally Saleh Ally, Mbunge wa Malindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tangu kuanzishwa kwa Chuo cha Diplomasia mwaka 1978 hadi hivi sasa, chuo kimetoa jumla ya wahitimu 3,421, kati ya hao, wahitimu katika ngazi za Shahada ni 72, Stashahada ya Udhamili katika Menejementi ya Uhusiano wa Kimataifa ni 503, Stashahada ya Udhamili katika Diplomasi ya Uchumi ni 341, Shahada ya kawaida ni 2,084, ngazi ya Cheti ni 347 na wahitimu 74 ni wa Mafunzo Maalumu ya Maafisa Waandamizi wa Mambo ya Nje.

Mheshimiwa Spika, katika idadi hiyo ya wahitimu wa Chuo cha Diplomasia, wanawake ni 1,060 na wanaume ni 2,361. Wanafunzi hao walitoka nchi za Afrika Kusini, Algeria, Angola, Botswana, Burundi, Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Guinea, Kenya, Komoro, Libya, Malawi, Msumbiji, Namibia, Palestina, Rwanda, Sudan, Zambia, Zimbabwe pamoja na hapa kwetu Tanzania.

Mheshimiwa Spika, tangu kuanzishwa kwa chuo hiki mwaka 1978, zaidi ya wahitimu 500 kutoka Tanzania wameweza kuwa Career Diplomats na kufanya kazi katika maeneo mbalimbali ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, chuo kinatambua umuhimu wa lugha katika nyanja za masuala ya mahusiano ya kimataifa na diplomasia. Chuo kimeongeza idadi ya lugha za kigeni zinazofundishwa, mpaka hivi sasa chuo kinafundisha lugha saba (7) ambazo ni Kiarabu, Kichina, Kifaransa, Kihispania, Kingereza, Kikorea na Kireno. Halikadhalika, chuo kimetayarisha mtaala wa kufundishia lugha ya Kiswahili kwa wananfunzi wa kigeni ili kueneza lugha hiyo kimataifa. Mafunzo hayo yataanza kutolewa kuanzia mwaka wa masomo 2019/2020.
MHE. USSI SALUM PONDEZA aliuliza:-

Viongozi wa Kitaifa wanaofanya ziara Tanzania walikuwa wakifika Zanzibar na kuonana na Rais wa Zanzibar:-

(a) Je, kwa nini katika siku za karibuni viongozi hao wamekuwa wakiishia Tanzania Bara?

(b) Je, ni viongozi wangapi wa Kimataifa ikiwemo Marais ambao wamefanya ziara Tanzania katika kipindi cha 2016/2017 na nchi wanazotoka?

(c) Je, kati ya viongozi hao wangapi wamefika Zanzibar na wangapi hawakufika na kwa sababu gani?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ussi Salum Pondeza Mbunge wa Chumbuni len ye kipengele (a), (b) na (c) kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Spika, kwa kawaida viongozi wa Kitaifa wanapokuja nchini wanakuwa na ratiba ya maeneo ambayo wameyaainisha kuyatembelea kulingana na muda waliopanga kuwepo nchini. Pamoja na hilo Wizara imekuwa ikiwashauri viongozi hao kuzuru maeneo m balimbali ya nchi hususan Zanzibar ili pamoja na mambo mengine kukutana na kufanya mazungumzo rasmi na viongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2015 hadi Aprili, 2019 jumla ya viongozi 21 wa Kimataifa walitembelea Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Viongozi hawa walitoka katika nchi za Afrika Kusini, Burundi, Chad, Cuba, Ethopia, India, Jamhuri ya Democrasia Congo, Jamhuri ya Korea, Msumbuji, Morocco, Mauritius, Misri, Malawi, Rwanda, Uturuki, Uganda, Vietnam, Sudan Kusini, Sri Lanka, Switzerland, Zambia na Zimbabwe.

Mheshimiwa Spika, kati ya viongozi hao wa Kimataifa waliotembelea Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tisa walifika Zanzibar na 12 kati yao hawakufika Zanzibar. Sababu zinazopelekea kutofika kwao ni kutokana na aina ya ziara, ratiba ya ziara husika na ufinyu wa muda katika ziara. Sababu nyingine ni vipaumbele na malengo ya ziara za viongozi hao pamoja na utashi wa kiongozi husika. Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeendelea kushauri viongozi wa Kitaifa kutoka nchi za kigeni wanaozuru nchini kutembelea Zanzibar katika ratiba zao. Aidha, Wizara kupitia Idara ya Mambo ya Nje Zanzibar imekuwa ikifanya maandalizi stahiki ya kiitifaki ili kurahisisha viongozi hao kutembelea Zanzibar.
MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza:-

Watanzania wengi wanaoishi nje ya nchi wamejikuta ni raia wa nchi wanazoishi kwa sababu mbalimbali ikiwemo kazi lakini si kwamba hawaipendi Tanzania:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwatambua Watanzania waliochukua uraia wa nchi nyingine ili waweze kukuza uchumi wa nchi na kusaidia ndugu zao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kusimamia masuala yanayohusu Watanzania wanaoishi nje ya nchi (diaspora) pasipo kubagua wale waliochukua uraia wa nchi nyingine kwa lengo la kuhakikisha kuwa mahitaji yao ya kikonseli yanashughulikiwa na pia kuongeza ushiriki wao katika kuchangia maendeleo ya nchi na ndugu zao.

Mheshimiwa Spika, Wizara imeweka mikakati mbalimbali ya kuwatambua diaspora katika kukuza uchumi. Mikakati yao ni pamoja na kuhimiza diaspora kujisajili kwenye Balozi zetu na maeneo ya uwakilishi; kuratibu makongamano ya diaspora ndani na nje ya nchi; kuratibu mikutano ya diaspora na viongozi wa Serikali wanapofanya ziara za kikazi nje ya nchi; kuhamasisha diaspora kuunda na kusajili jumuiya zao na kuwahimiza kuwa washawishi wazuri wa uwekezaji kutoka mataifa mengine kuja kuwekeza nchini.

Mheshimiwa Spika, idadi ya diaspora wa Kitanzania nje ya nchi inakadiriwa kuwa ni zaidi ya milioni moja, ambapo idadi ya diaspora waliojisajili kwa hiari kwenye Balozi zetu na maeneo ya uwakilishi ni takribani laki moja. Aidha, diaspora hao wamekuwa wakimiliki akaunti kwenye taasisi mbalimbali za kifedha kama vile Benki za Azania, CRDB, NMB, Stanbic na pia kuwa wanachama wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ya NSSF na PSSSF, ikiwa ni pamoja na kumiliki nyumba 166 zilizouzwa na Shirika la Nyumba la Taifa zenye thamani ya shilingi bilioni 5.5 hadi kufikia Februari, 2019. Pia diaspora wameleta mafanikio makubwa kwa ndugu zao na taifa kwa ujumla kwa kuchangia sekta mbalimbali kama vile afya ambapo tumekuwa tukipokea wataalam wa afya na magonjwa yenye kuambukiza na yale yasiyoambukiza kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, tunao mfano mzuri katika sekta ya afya ambapo Novemba, 2019 tulipokea msaada wa sanamu ya vitendo (simulative manikin) kutoka kwa Jumuiya ya Watanzania Wanaoishi Uingereza yenye thamani ya shilingi milioni 100; vitabu vya afya vyenye thamani ya shilingi milioni 30 vilivyogawiwa katika Maktaba Kuu ya Shirika la Elimu Kibaha, Taasisi ya Jakaya Kikwete, Hospitali ya Namanyere iliyopo Sumbawanga, Mkoa wa Rukwa, Mbeya pamoja na Pemba.
MHE. MBAROUK SALIM ALI aliuliza:-

Pemba ni Kisiwa kinachozalisha viungo (spices) kwa wingi na wajasiriamali huzalisha bidhaa zinazotokana na viungo hivyo:-

Je, ni lini wakulima na wajasiriliamali wa Pemba wataunganishwa na soko la Afrika Mashariki ili waweze kufaidika na soko hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mhe. Mbarouk Salim Ali, Mbunge wa Wete kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, napenda kumtaarifu Mhe. Mbunge kuwa, wananchi wa Pemba na wa maeneo yote ya Tanzania wamekwisha unganishwa na soko la Afrika Mashariki kupitia Itifaki za Umoja wa Forodha na ya Soko la Pamoja la Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Spika, kwa mkulima au mjasiriamali yoyote kuweza kuuza bidhaa zake ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki anapaswa kukidhi vigezo vya Afrika Mashariki vya kutambua uasili wa bidhaa (Rules of Origin). Nchi Wanachama zilikubaliana na kuweka vigezo vinavyoshabihiana kama bidhaa husika imezalishwa ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Vigezo hivyo vimejengwa katika misingi ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, bidhaa kuzalishwa ndani ya Jumuiya kwa kiwango cha asilimia mia moja mfano, bidhaa za kilimo, uvuvi, madini na kaadhalika; bidhaa kuzalishwa ndani ya Jumuiya kwa kutumia malighafi ya kutoka nje yenye thamani (ex-works price) ya kiwango kisichozidi asilimia 70 ya bei ya bidhaa hiyo bila kodi ikiwa kiwandani, mfano label za plastik, kuongeza ugumu wa kioo, utengenezaji wa nyaya za umeme na vifaa vingine vya umeme, utengenezaji wa pikipiki na baskeli n.k; bidhaa zinazozalishwa ndani kwa kutambua mchakato katika uzalishaji (process rule) kama vile uunganishaji wa magari na kusafisha mafuta ya petroli (refining); na bidhaa kubadilika utambuzi wa uasili kwa kubadilika umbo na matumizi kutokana na mchakato wa viwandani mfano malighafi ya plastiki kuchakatwa kuwa meza, viti, sahani n.k.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia misingi ambayo nimekwisha ielezea hapo juu, nichukue fursa hii kupitia Bunge lako Tukufu kuwashauri wananchi wa Pemba na Tanzania kwa ujumla kuzichangamkia fursa za kibiashara, ajira, uwekezaji n.k. zitokanazo na Jumuiya ya Afrika Mashariki katika kujihakikishia maendeleo.

Mheshimiwa Spika, vilevile, kuwasihi wananchi kuzitambua taratibu za kufuata katika kuzitumia fursa za kibiashara zilizopo katika Jumuiya ya Afrika Mashariki ikiwa ni pamoja na kuwa na cheti cha Uasili wa Bidhaa (East African Communicate Certificate of Origin) na vibali/ nyaraka zinazobainisha kuwa bidhaa imezalishwa ndani ya Jumuiya kutoka mamlaka husika kutegemea na aina ya bidhaa mfanyabiashara anazotaka kuuza/kununua katika soko la Afrika Mashariki.
MHE. ALLY SALEH ALLY aliuliza:-

Moja ya misingi mikuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ni utawala bora, haki za binadamu na demokrasia sambamba na kukuza uchumi za Nchi sita Wanachama:-

(a) Je, hilo linatimizwa kwa kiasi gani ndani ya Jumuiya na Wanachama?

(b) Je, kuna mfumo gani wa kukosoana ndani ya Jumuiya katika eneo hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Saleh Ally, Mbunge wa Malindi, lenye vipengele (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 6 ya Mkataba wa Uanzishaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki imeainisha misingi mikuu ya kuzingatia ili kuiwezesha Jumuiya ya Afrika Mashariki na Nchi Wanachama kufikia malengo yake. Katika kutekeleza matakwa ya Ibara hiyo, nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zimegawanya madaraka katika mihimili mitatu yaani Bunge, Mahakama na Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki. Mihimili hii inajiendesha kwa kanuni na taratibu zake ambapo Wakuu wa Nchi kupitia Baraza la Mawaziri husimamia utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Jumuiya ya Afrika Mashariki ikiwemo maelekezo na maamuzi ya Wakuu wa Nchi; Bunge limepewa mamlaka ya kuwakilisha wananchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, kutunga sheria, kusimamia utekelezaji wa miradi na programu za Jumuiya pamoja na kupitisha bajeti ya Jumuiya; na Mahakama ina mamlaka ya kutafsiri Sheria za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dhamira hiyo ya kusimamia misingi mikuu ya Utawala Bora na Demokrasia ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Nchi Wanachama hupokezana Uenyekiti wa Jumuiya. Aidha, uendeshaji wa shughuli za Jumuiya hufuata vikao rasmi ambavyo ni shirikishi kuanzia ngazi ya Wataalam, Makatibu Wakuu, Baraza la Mawaziri na Wakuu wa Nchi, hivyo maamuzi yanayofikiwa ni yaliyokubalika na nchi zote sita (consensus). Mathalani, nchi hizo zimekubaliana kutuma waangalizi wa uchaguzi kwenye chaguzi kuu za nchi wanachama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Jumuiya ya Afrika Mashariki hutoa fursa kwa Sekta Binafsi na Asasi za Kiraia kuwasilisha hoja na masuala mbalimbali ambayo hufanyiwa maamuzi kupitia vikao rasmi. Pia, wananchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kupitia Mabunge ya nchi zao hufanya uchaguzi wa Wabunge wanaowawakilisha nchi hizo katika Bunge la Afrika Mashariki. Halikadhalika, Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ina mamlaka ya kusikiliza mashauri mbalimbali kuhusu ukiukwaji wa haki za binadamu ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo wa ukosoaji katika Jumuiya ya Afrika Mashariki unafanyika kupitia Bunge na Mahakama ya Afrika Mashariki. Bunge hilo limepewa mamlaka ya kusimamia utekelezaji wa shughuli za Jumuiya ya Afrika Mashariki ikiwa ni pamoja na kuandaa ripoti mbalimbali zinazowasilishwa na kujadiliwa ndani ya Bunge.

Hatua hii imewezesha Bunge hilo kutoa mapendekezo ya hatua za kuchukuliwa na Baraza la Mawaziri. Vilevile, kupitia Mahakama ya Afrika Mashariki wananchi hupeleka mashauri mbalimbali na Mahakama hiyo imeweza kufanya maamuzi ya kesi mbalimbali dhidi ya Serikali za nchi wanachama.
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS NYIMBO Aliuliza:-

Je, Serikali ina maelezo gani juu ya viongozi kutoka nje ya nchi wanaokuja Tanzania na kutembelea baadhi ya maeneo na kisha wanapokuta miradi ya wananchi huahidi kusaidia na baadae kushindwa kutimiza ahadi zao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tauhida Cassian Gallos, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania imekuwa ikipokea viongozi wageni kutoka nje ya nchi na makundi aina mbili yaani wa Kiserikali na wasio wa Kiserikali. Viongozi hao hutembelea Tanzania kwa ziara za kikazi na binafsi ambapo hupata fursa ya kuona miradi ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ina jukumu la kuratibu na kusimamia ziara za kikazi za viongozi wa Serikali kutoka mataifa ya kigeni ikiwa ni pamoja na kufuatilia utekelezaji wa ahadi mbalimbali zinazotolewa na viongozi hao kwa kushirikiana na Wizara za kisekta na taasisi za Kiserikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahadi ambazo hutolewa na baadaye kushindwa kutimizwa, Wizara huratibu vikao vya majadiliano vinavyoshirikisha wahusika pamoja na Wizara za kisekta na taasisi za Kiserikali ili kupata mwafaka juu ya suala husika.
MHE. OTHMAN OMAR HAJI aliuliza:-

Lengo kuu la Mpango wa Kujithathmini Kiutawala Bora Barani Afrika (APRM) ni kuziwezesha nchi za Afrika kuimarisha utawala bora kwa kuwawezesha wananchi wake kubainisha changamoto:-

Je, ni hatua gani ambazo zinachukuliwa na Tanzania katika kutekeleza mpango huo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Othman Omar Haji, Mbunge wa Gando, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Tanzania ni miongoni mwa nchi 38 kati ya nchi 54 Barani Afrika zinazoshiriki katika Mpango wa Kujitathmini Kiutawala Bora Barani Afrika (APRM) ambapo ilijiunga mwaka 2004 na Bunge la Tanzania liliridhia makubaliano hayo mwaka 2005. Hii ni kutokana na imani kubwa iliyonayo katika lengo kuu la Mpango wa APRM ambalo ni kuziwezesha nchi za Kiafrika kujitathmini kwa vigezo vinavyokubalika vya utawala bora.

Mheshimiwa Spika, matokeo ya tathmini hizo ni kubaini changamoto zilizopo ili ziwekewe mikakati ya kugeuzwa kuwa fursa za maendeleo na pia kubaini maeneo ambayo nchi inafanya vizuri ili kuyaimarisha pamoja na kuigwa mataifa mengine. Tathmini hiyo hufanywa katika maeneo ya siasa na demokrasia, usimamizi wa uchumi, uendeshaji wa mashirika ya biashara na maendeleo ya jamii.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ilikabidhiwa jukumu la kuwezesha utekelezaji wa APRM hapa Tanzania. Katika kutekeleza jukumu hilo, Wizara iliandaa semina na uhamasishaji juu ya Mpango wa APRM ili kuwaandaa wananchi kushiriki kikamilifu katika mpango huo na pia kuwawezesha kuchagua Wajumbe watakaowakilisha makundi yao katika Baraza la Usimamizi la Taifa. Hivyo, mwaka 2006 Wizara iliwezesha kuundwa kwa Baraza la Usimamizi la Taifa lenye Wajumbe 20 kutoka kwenye taasisi za Serikali na taasisi zisizo za Kiserikali.

Mheshimiwa Spika, jukumu kubwa la Baraza ni kusimamia utekelezaji wa shughuli za mpango na kuhakikisha kuwa zinafanyika kwa uwazi, uadilifu na zisiingiliwe kisiasa. Kwa kushirikiana na Wizara, Baraza liliajiri Sekretarieti inayofanya shughuli za APRM za kila siku na taasisi nne za kufanya utafiti katika kila eneo la tathmini.

Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwaka 2019, APRM imekwishaandaa taarifa mbili za utawala bora, taarifa ya ndani ya nchi na taarifa ya nje ya nchi. Pamoja na taarifa hizo, umeandaliwa mpango kazi wa APRM wenye lengo la kutatua changamoto za utawala bora zilizobainishwa kwenye taarifa zilizotajwa.

Mheshimiwa Spika, ili kuwezesha utekelezaji wa taarifa za APRM kimeundwa kikosi kazi cha APRM chenye jukumu la kuandaa taarifa za utekelezaji wa kila mwaka na taarifa hizo huunganishwa kuwa taarifa moja ya nchi. Serikali imekuwa ikitenga bajeti kwa ajili ya kazi za APRM kila mwaka na kulipa michango yake kwa taasisi hii kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa kushirikiana na Wizara na taasisi za Serikali pamoja na sekta binafsi inaendelea kutatua changamoto za utawala bora kama ilivyoelekezwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015 na kuainishwa kwenye mpango kazi wa APRM.
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakamilisha mpango wa uvunaji wa mikoko kwa wananchi wanaoishi maeneo ya Delta wanaotegemea zao hilo kuendesha shughuli zao za kimaisha?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI K.n.y. WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba ama napenda kujibu swali la Mheshimiwa Twaha Ally Mpembenwe, Mbunge wa Kibiti, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, misitu ya mikoko ina umuhimu mkubwa katika nyanja za kiuchumi na kimazingira, kutokana na kuvamiwa kwa misitu hii kwa kufanya shughuli zisizokubalika kiuhifadhi kama vile kilimo, ufugaji utayarishaji wa chumvi, Serikali ilisimamisha uvunaji wa mikoko yote kote nchini ili kutoa fursa ya kuweka mipango na mikakati ya matumizi endelevu. Hivyo, Wizara inaandaa mpango na mwongozo wa usimamizi wa matumizi endelevu ya misitu ya mikoko utakaotoa utaratibu wa uvunaji. Mipango na miongozo hiyo ipo katika hatua za mwisho za maandalizi na inatarajiwa kukamilika robo ya kwanza ya mwaka 2021/2022 na baada ya kukamilika utaanza kutumika.
MHE. DKT. ASHATU K. KIJAJI aliuliza: -

(a) Je, ni lini Serikali itaelekeza kwa wananchi maamuzi ya Timu ya Mawaziri iliyozunguka kwenye maeneo yenye migogoro kati ya wananchi na mapori ya hifadhi?

(b) Je, ni lini Serikali kwa kushirikiana na wananchi itaweka mipaka kati ya mapori ya hifadhi na vijiji vinavyoyazunguka ili kupunguza migogoro iliyopo na kuwezesha wananchi kufanya shughuli za kiuchumi bila usumbufu?
NAIBU WAZIRI WA MADINI K.n.y. WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kachwamba Kijaji, Mbunge wa Kondoa, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza maamuzi ya Baraza la Mawaziri, Serikali imeandaa mpango kazi kwa ajili ya kuwaeleza wananchi juu ya uamuzi wa Serikali kuhusu migogoro kati ya wananchi na hifadhi. Katika kutekeleza mpango kazi huo, timu ya Mawaziri wa Kisekta itapita katika mikoa husika kwa lengo la kutoa elimu na ufafanuzi kwa viongozi wa mikoa pamoja na wilaya.

Zoezi hilo litaenda sambamba na timu ya watalaam itakayojumuisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Uongozi wa Mikoa, Wilaya na Vijiji.

(b) Mheshimiwa Spika, zoezi la uwekaji wa mipaka kwenye maeneo yote yenye migogoro litafanywa na timu ya wataalam kutoka katika sekta za Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Wizara ya Maliasili na Utalii. Timu hii, itapita katika maeneo yote ili kufanya tathmini, uhakiki na kuweka mipaka kulingana na uamuzi wa Serikali. Aidha, katika zoezi hilo wananchi watashirikishwa ili kuondoa uwezekano wa kujitokeza migogoro mingine. Ahsante.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa haraka na wa kudumu wa kudhibiti wanyamapori katika Hifadhi ya Taifa Serengeti hasa Tembo na Simba ambao wamekuwa wakivamia vijiji na kuharibu mashamba pamoja na kuua watu?
NAIBU WAZIRI WA MADINI K. n. y. WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jeremiah Mrimi Amsabi, Mbunge wa Serengeti, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mwingiliano kati ya binadamu na wanyamapori umekuwepo kwa muda mrefu. Hata hivyo, miaka ya hivi karibuni mwingiliano huo umeongezeka na kusababisha madhara kwa wananchi, ikiwa ni pamoja na kuua mifugo na kuharibu mali nyingine za wananchi ikiwemo mazao. Changamoto hii ipo katika maeneo mengi nchini hususan yanayopakana na maeneo yaliyohifadhiwa kama ilivyo kwa Hifadhi ya Taifa Serengeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, kufuatia kuwepo kwa changamoto ya wanyamapori wakali na waharibifu katika maeneo mbalimbali nchini, Serikali imeanza kutekeleza Mpango Mkakati wa Kitaifa wa Kukabiliana na Wanyamapori Wakali na Waharibifu. Mpango huo unahusisha yafuatayo: -

i. Kutoa mafunzo yatakayowawezesha wanajamii kukabiliana na kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu;

ii. Kutoa vifaa mbalimbali kwa ajili ya kujikinga na wanyamapori hao, na wananchi kuhamasishwa kufuga nyuki kwa kutumia mizinga ya kisasa; na

iii. Kutoa namba maalum za simu (toll free number) endapo matukio hayo yanajitokeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. EDWIN E. SWALLE aliuliza: -

Je, ni kwa nini Serikali isiteue Majaji wa muda mfupi (Acting Judges) ili kusikiliza kesi za mauaji zinazochukua muda mrefu Mahakamani?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria napenda kujibu swali la Mheshimiwa Edwin Enosy Swalle, Mbunge wa Lupembe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, uteuzi wa Majaji upo Kikatiba. Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haina ibara inayotambua au kuruhusu uteuzi wa Majaji wa muda mfupi (Acting Judges). Aidha, Ibara ya 117(3) ya Katiba inatambua uwepo wa Mahakimu wenye mamlaka ya nyongeza ya kusikiliza baadhi ya mashauri ya Mahakama Kuu yakiwemo kesi za mauaji.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA aliuliza: -

Je, Serikali haioni umuhimu wa kupitia upya mfumo wa haki jinai ili kupunguza changamoto ya idadi kubwa ya mahabusu kuliko wafungwa magerezani?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria naomba kumjibu Mheshimiwa Neema Kichiki Lugangira, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuhakikisha maboresho ya mfumo wa haki jinai nchini yanafanyika ili kuimarisha upatikanaji wa haki jinai nchini ikiwemo kuondokana na mlundikano wa mahabusu katika magereza yetu. Kutokana na umuhimu huo, Wizara imeandaa andiko la mapendekezo ya maboresho ya mfumo wa haki jinai ikishirikiana na Taasisi Zisizo za Kiserikali, Taasisi za Dini na Vyuo vinavyotoa elimu ya sheria ili kuhakikisha kwamba Mfumo wa Haki Jinai unafanyiwa marekebisho na kuwekwa sawa. Ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali nakuona umesimama.

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu yaliyotolewa na Mheshimiwa Naibu wa Waziri wa Ardhi kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria ningependa kurejesha kumbukumbu sahihi za kazi ya Bunge hili kwamba Sheria Namba 1 ya mwaka 2022 iliyotungwa na Bunge hili mwezi wa pili ilizuia kufikishwa mahakamani kwa kesi ambazo upelelezi bado isipokuwa kwa makosa yale makubwa. Hiyo ni hatua moja kubwa sana na iliyolenga kupunguza msongamano wa mahabusu. (Makofi)
MHE. JUDITH S. KAPINGA aliuliza: -

Je, kuna mkakati gani wa kurekebisha sheria ili ubakaji na ulawiti kwa watoto uwe na kifungu tofauti cha sheria?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI) K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria naomba kujibu swali la Mheshimiwa Judith Salvio Kapinga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Kanuni za Adhabu, Sura ya 16 inaainisha ubakaji na ulawiti kuwa ni makosa ya jinai. Kwa mujibu wa sheria hii, kosa la ubakaji limeainishwa chini ya kifungu cha 130 na adhabu yake imeainishwa kwenye kifungu cha 131. Aidha, kosa la ulawiti na adhabu yake zimeainishwa chini ya kifungu cha 154 cha sheria hii. Makosa yote mawili yametolewa adhabu tofauti kulingana na mazingira na namna kosa lilivyotendeka. Adhabu ya chini kwa makosa hayo ni kifungo cha miaka 30 na adhabu ya juu ni kifungo cha maisha jela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vifungu hivyo makosa yote mawili yanapotendeka kwa mtoto chini ya miaka 10 adhabu yake ni kifungo cha maisha jela, pia adhabu hizo zinaweza kuambatana na kulipa fidia kwa kiwango kinachoamuliwa na Mahakama, ahsante. (Makofi)
MHE. JUDITH S. KAPINGA K.n.y. MHE. DAVID M. KIHENZILE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakamilisha usajili wa Shirikisho la International Federation of Cross and Crescent nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI) K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria naomba kujibu swali la Mheshimiwa David Mwakiposa Kihenzile Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Shirikisho la Kimataifa la Msalaba Mwekundu (International Federation of Red Cross and Crescent - IFRC) ni Shirika la Kimataifa linalounganisha vyama vya nchi mbalimbali vya Msalaba Mwekundu. Nchini Tanzania Chama cha Msalaba Mwekundu kilianzishwa chini ya Sheria Na. 71 mwaka 1962 kufuatia nchi yetu kuridhia mikataba ya Geneva yam waka 1949. Kazi kubwa ya Shirikisho hili ni kufanya shughuli za kusaidia wahanga wa maafa na kuimarisha uwezo wa wanachama wake katika kukabiliana na maafa. Kutokana na umuhimu wa Shirikisho hilo kwa nchi yetu, tayari Serikali imekamilisha majadiliano na uongozi wa IFRC na zoezi la kuwashirikisha wadau wote wanaohusika hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa, Serikali iko katika hatua za mwisho kukamilisha mkataba na shirikisho hilo, hatua hizo zitakapokamilika mkataba utasainiwa na Ofisi za IFRC kufunguliwa nchini na kuanza kufanya kazi. Ahsante.
MHE. ELIBARIKI I. KINGU aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawasilisha Muswada wa Sheria unaozuia Polisi kukamata na kuwashikilia watuhumiwa kabla ya kukamilisha upelelezi?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Elibariki Immanuel Kingu, Mbunge wa Singida Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilifanya mabadiliko ya Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai Sura Na. 20 kupitia Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Na. 1 ya mwaka 2022 mwezi Machi, 2022, ambapo kwa sasa Sheria imeweka masharti ya kutofungua mashtaka mpaka upelelezi utakapokamilika, isipokuwa kwa makosa makubwa tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupitia sheria zinazokinzana na Sheria Namba 4 na 5 juu ya umiliki wa ardhi kwa wanawake?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Neema Kichiki Lugangira, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Ibara ya 24 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inampatia kila mtu bila kujali jinsia yake, haki ya kumiliki mali ikiwemo ardhi na haki ya kuhifadhi kwa mali yake aliyonayo kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, kama kuna Sheria inayokinzana na Katiba na Sheria za Ardhi Na. 4 na Na. 5 ya mwaka 1999 kuhusu umiliki wa ardhi kati ya mwanaume na mwanamke, Serikali itaanzisha mchakato wa kuzifanyia mabadiliko Sheria hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu umiliki wa ardhi kwa watoto chini ya miaka 18 wanaweza kumiliki ardhi kwa kupitia waangalizi wao kwa mujibu wa sheria.