Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Godfrey William Mgimwa (12 total)

MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la umeme hasa kwenye uunganishaji limekuwa ni tatizo kubwa hasa kwenye maeneo ya mita. Wananchi wengi na wateja wengi wamekuwa wakilalamika kwamba mita ambazo wanafungiwa zinaharibika baada ya muda mfupi. Ningependa kujua kutoka kwa Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba je, analifahamu hili na kama analifahamu, hatua gani zitachukuliwa, ili kuhakikisha kwamba, utaratibu huu mbovu unasitishwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Jimbo la Kalenga limekuwa lina changamoto kubwa katika masuala haya ya umeme na nina vijiji kadhaa ambavyo mpaka dakika hii viko gizani na vinahitaji umeme. Kijiji cha Lupalama katika Kata ya Nzii, Kijiji cha Kipera, Kijiji cha Itagutwa, Kijiji cha Magunga na Lyamgungwe; ningependa kusikia commitment ya Mheshimiwa Waziri, je, ana utaratibu gani na mpango gani kuhakikisha kwamba, vijiji hivi vinapata umeme? Na kama je, yuko tayari kuungana na mimi kwenda moja kwa moja Kalenga ili kuweza kuwapa hamasa wananchi wangu? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge, wakati REA wanapofunga umeme ni mara nyingi sana imekuwa ikitokea kwamba zile mita inaonekana kama hazina nguvu, tatizo siyo kwamba mita ni mbovu, tatizo tu ni kwamba umeme unaokuja ni wa low voltage.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge ni vizuri tukawaeleza baada ya REA kuunganisha umeme sasa, umeme tunaotumia ni wa low voltage ambao ni kilovolt 30 na mwingine 11 zaidi ni 132. Kuanzia Julai mwaka huu kuna mradi sasa wa kuongeza nguvu za umeme ambao ni kilovolt 400 utapita kwenye maeneo ambayo tuliyataja. Kilovolt 400 zitakapoingia na kuanza matatizo ya kukatika kwa umeme kwenye tatizo la mita yatakoma mara moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na vijiji alivyotaja Mheshimiwa Mgimwa, vijiji vitano vya Lupalama, Lupelo, Magunga na vingine ni kweli kabisa havijapata umeme na tulishavitembelea, kwa sasa tumezungumza na Mheshimiwa Mgimwa, kati ya vijiji vitakavyoanza kupatiwa umeme kwenye Jimbo lake tutaanza na hivi vijiji vitano ambavyo Mheshimiwa Mgimwa amevitaja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ameomba sana tupate fursa ya kutembelea kule mimi pamoja na Mheshimiwa Waziri tumekuwa tukitembelea sana maeneo ya Morogoro, hata hivyo, bado tumhakikishie baada ya Bunge lako Tukufu kuisha mimi na Mheshimiwa Mbunge bado tutakwenda kutembelea zaidi, hata akisema mara tano bado tutakwenda kuhakikisha wananchi wanapata umeme.
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kuweka minara kwanza niipongeze sana Serikali kwamba imeendelea kupeleka minara katika Jimbo la Kalenga kwa kasi zaidi. Tatizo ninalolipata ni kwamba baada ya kusimikwa ile minara upatikanaji sasa au uanzaji wa kuanza kupata mawasiliano unatumia muda mrefu sana. Ningependa kujua Serikali ina mkakati gani ili mara baada ya kuwekwa ile minara mawasiliano yaanze kupatikana kwa muda unaostahili. (Makofi)
Swali langu la pili, narudi tu kwenye majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba amesema vijiji vilivyotamkwa hapa mwishoni vya Kaning‟ombe na Ikuvilo vitapita katika utaratibu wa kupitia UCSAF lakini katika tovuti ambayo nimekuwa nikiipitia ya UCSAF nitoe tu statistics kidogo inaonyesha kwamba kwa mwaka 2015 zilitangazwa zabuni175, Kata zilizopata wazabuni 116 hii kwa ni Tanzania nzima, idadi ya vijiji 156, miradi kuanza ilikuwa ni Mei, 2015. Lakini katika orodha hii yote hakuna vijiji ambavyo tayari vilishaanza kupatiwa mawasiliano ni zero, kupitia mradi ya UCSAF.
Ningependa kujua Serikali ina mikakati gani kuhakikisha kwamba inaipa pesa UCSAF ili kwamba miradi ambayo imeorodheshwa iweze kukamilika kwa wakati? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mgimwa naomba nikiri kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuwahangaikia watu wake, anafanya hivyo katika maeneo mengi ambayo Wizara yetu inaisimamia ikiwa ni pamoja na barabara, mawasiliano hayo ambayo leo ameyauliza na masuala mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie kwamba yale tunayomweleza anapofuatilia ofisini tunamthibitishia kwamba tutayatekeleza. Nimhakikishie kwamba Awamu hii ya Tano ya Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli inatenda inachoahidi. Mkakati wa kuhakikisha minara ambayo inajengwa inaanza kufanya kazi tutaifuatilia, kwa hili aliloliuliza nadhani ameuliza tu kuongezea utamu, tumemwambia kwamba mnara huo utaanza kufanya kazi mwishoni mwa mwezi Juni kama tulivyoongea, ni kweli na tutafuatilia. (Makofi)
Kuhusu mirafi ya UCSAF, naomba nimhakikishie kama nilivyosema hii Serikali inatenda inachoahidi, katika mwaka huu wa fedha hizo zilizotengwa miradi iliyotangazwa tutahakikisha inakamilika. Lakini usisahau kwamba miradi mingine tuliyoongelea hapa haitekelezwi na UCSAF peke yake mingine inatekelezwa na TTCL na Viettel ambayo katika tangazo hili miradi hiyo hutaiona.
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Tatizo ambalo lipo katika Jimbo la Mheshimiwa Mendrad Lutengano, ni sawasawa na tatizo ambalo liko katika Jimbo langu la Kalenga. Ningeomba kujua Miradi ya Maji ya Weru, Itengulinyi, Supilo, itakamilika lini kwa sababu wakandarasi wamekuwa wakipiga makelele na kudai pesa zao za malipo?
Ningependa kujua kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, ni lini sasa Wakandarasi hawa watalipwa, ili kwamba, miradi iweze kuendelea na wananchi wangu waweze kupata maji? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuna miradi ya maji mingi sana ilisimama. Wakandarasi wali-demobilize mitambo kutoka maeneo ya miradi na sababu kubwa ilifanya kwamba, flow ya fedha, wakandarasi walifanya kazi walikuwa hawajalipwa, certificates zilienda Wizarani, lakini watu walikuwa hawajalipwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, jukumu letu kubwa tulilofanya ni kuhakikisha pesa zinakusanywa kama nilivyosema awali. Hivi sasa nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge wakandarasi wote karibuni sasa hivi kila Halmashauri pesa sasa zimeshapelekwa, ilimradi wakandarasi waweze kurudi site.
Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nilikuwa na Naibu Waziri wa Maji hapa tukifanya mjadala katika hayo, imeonekana sasa hivi hali imeenda vizuri zaidi. Kama tutafanya analysis kama huko Makete kama watu hawajaanza kurudi site, lakini ni kwamba kweli wakandarasi walitoa mitambo mwanzo, lakini fedha sasa hivi baada ya makusanyo mazuri tumeshapeleka site huko ilimradi wakandarasi walipwe, kazi iweze kuendelea. Tutaangalia kama huku katika Jimbo lako kama kuna matatizo kidogo bado yapo, tutaangalia jinsi gani tutafanya kuyatatua kwa pamoja.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hili niweze kuzungumzia hata pale kwa ndugu yangu wa Mufindi pale, ndugu yangu Mheshimiwa Chumi, kulikuwa na suala la pampu pale, tumefanya harakati, hivi sasa ile pampu inafungwa baada ya kupata uhakiki wa kutosha. Lengo letu ni kwamba, miradi yote ikamilike na wananchi waweze kupata maji.

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri – TAMISEMI, kuhusu Jimbo la Kalenga tayari nimeshaongea na Mheshimiwa Mbunge na tumeangalia vitabu, tumeshapeleka shilingi milioni 365. Nikawa nimemuomba Mheshimiwa amfahamishe Mkurugenzi kwamba, kama kuna certificate zozote walizonazo mezani watuletee, ili tuweze kukamilisha malipo Wakandarasi waendelee na kazi.
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa, tatizo ambalo linaonekana la kuwanyanyasa wananchi ambalo linafanywa na Polisi linafanana sana na malalamiko mbalimbali ambayo yanatoka katika Idara ya Uhamiaji kwamba Idara ya Uhamiaji nao wanafanya unyanyasaji mkubwa kwa wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ningeomba kujua kwa sababu katika Idara hii kuna watumishi ambao hawajalipwa mishahara yao kwa kipindi kirefu sana. Serikali inasema nini au ina tamko gani kuhusu watumishi hawa wa ajira mpya ambao hawajalipwa mishahara yao ili Serikali iweze kutoa majibu yanayoeleweka, kwamba watalipwa lini mishahara yao watumishi hao wa ajira mpya?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza suala la watu kunyanyaswa lina pande mbili. Sisi tumesema yale ambayo tunajiridhisha nayo tunachukua hatua, lakini suala la kutimiza wajibu ni suala la Watanzania wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Askari wapya ambao hawakuwa wamelipwa mishahara yao, nimhakikishie Mbunge kwamba tatizo hilo kweli lilikuwa kubwa na niwaombe radhi wale askari wetu ambao wamefanya kazi kwa muda bila kupata haki yao, kwa sababu mshahara na posho siyo hisani ni haki yao. Serikali imeshafanya kazi kubwa. Mwanzoni kulikuwa na idadi kubwa waliokuwa wanadai zaidi ya 297, lakini Askari 181 tayari walishapewa mishahara yao na watapewa na yale ambayo yalikuwa malimbikizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na tatizo ndani ya Wizara na nilishatoa maelekezo. Kuna watu bado wanafanya kazi kwa mazoea wakidhani labda Askari anatakiwa aishi kimsoto msoto hivi. Hakukuwa na sababu ya kutokupeleka majina yale Utumishi na kuyaingiza kwenye mfumo ili waweze kulipwa. Kuna watu kwa sababu zao wenyewe na nilielekeza wachukuliwe hatua, wamekaa na majina hayo kwa muda mrefu bila kupeleka Utumishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naelekeza kwa wale wachache ambao walikuwa bado wanafanyiwa uhakiki waharakishe haraka, wale wanaostahili waweze kulipwa na walipwe na malimbikizo yao ili waweze kufanya kazi bila manung’uniko.
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya kupeleka mawasiliano katika Jimbo langu.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, swali hili nimeuliza mwaka 2014 nikajibiwa kwamba 2015 nitapata majibu ya uhakika, sikupata majibu. 2015 nikapata nafasi ya kuuliza nikaambiwa 2016, leo hii ni 2017 naambiwa ni 2018. Naomba niweze kupata majibu ya uhakika leo kwamba ni lini sasa vijiji hivi vilivyoorodheshwa vitapata minara ya simu na wananchi wangu waweze kupata mawasiliano hayo ya simu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; katika minara ya simu ambayo inajengwa katika maeneo mbalimbali katika Jimbo langu la Kalenga service levy hailipwi moja kwa moja kwenye Halmashauri, inaenda kulipwa kwenye makampuni yenyewe ambayo mengi yapo Dar es Salaam. Wananchi katika Jimbo langu wanakosa mapato ya ndani kutokana na minara hiyo ya simu. Ningependa kujua kutoka Wizarani, je, ni namna gani sasa wanaweza kuwapelekea fedha hizi wananchi ambao nao wanatakiwa kwa namna moja au nyingine waweze kupata faida kutokana na minara hii ya simu, kwa sababu inayotumika pale ni ardhi?
Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba fedha ambazo yanapata makampuni haya au faida ambazo zinapata kampuni hizi zinakwenda pia kuwasaidia wananchi katika maeneo husika? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, tunapojibu maswali hapa huwa tuna dhamira ya dhati ya kutekeleza kile tunachokijibu na kwa kawaida Wizara huwa tunajiandaa kujipanga kutekeleza kile ambacho tunakijibu hapa. Inapofika wakati wa bajeti inaweza ikatokea kama ilivyotokea kwa eneo hili kwamba Mfuko wetu wa Mawasiliano kwa Wote huwa unakosa fedha, unapokosa fedha tunatarajia tuifanye hiyo kazi mwaka unaofuata, hiyo inabakia dhamira yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie kwamba dhamira yetu ni kuhakikisha vijiji hivi kama tulivyosema katika jibu la msingi, tunavitekeleza katika mwaka huu wa 2017/ 2018 na fedha tunatarajia kuziomba na tunaamini mtazipitisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ile minara ya simu pale inapojengwa kwa kawaida yale makampuni yanaingia mikataba na ama vijiji au mwenye ardhi husika, kwa kawaida Wizara hatuingilii sana katika mikataba hii ya kulipa gharama za ardhi inayotumika na wawekezaji katika minara ya simu. Hata hivyo, nalichukua wazo lake au pendekezo lake ili tuangalie namna gani Wizara inaweza kusaidia katika kuhakikisha minara hii ambayo imewekwa katika Jimbo hili la Kalenga inatumika na inawanufaisha wananchi kupitia mikataba yao ambayo wameweka.
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nitakuwa na swali moja tu la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Halmashauri nyingi zimekuwa hazitengi fedha hizi kwa ajili ya vijana na akina mama; lakini vile vile tuna tatizo sasa hivi ambalo tungekuwa makini zaidi kuliangalia suala la ndugu zetu walemavu, kwamba kuweze kuwa na uwezekano sasa wa kuzitenga fedha kutoka katika hizi asilimia 10 kwa ajili ya walemavu, vijana na akina mama.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa sababu majibu ya msingi yameshatolewa ningependa kufahamu kwa hizi Halmashauri ambazo kwa ujumla zimeshindwa kutenga fedha hizi kwa ajili ya vijana kama mimi akina mama; na kama tulivyoongea kuhusu walemavu ningependa kufahamu sasa.
Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba inazibana halmashauri hizi ili ziweze kupata mapato ya ndani kwa uhakika na kuhakikisha kwamba inatenga fedha hizi kwa ajili ya makundi haya? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa swali la nyongeza ambalo linawagusa akina mama na vijana nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kupitia Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI ameshatoa waraka tangu mwaka jana mwezi wa saba kuelekeza Halmashauri zote nchini kuhakikisha kwamba wanatenga asilimia 10 kwa ajili ya mikopo ya vijana na wanawake na hilo ndiyo maana nimesema hapa kupitia Bunge lako Tukufu kwamba ni lazima watenge na wasipotenga sasa Serikali itaanza kuchukua hatua za kiutumishi dhidi ya Wakurugenzi ambao hawatengi.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni kwa sababu kinachotakiwa kufanyika ni kutenga kile ambacho kimekusanywa, kama kimekusanywa bilioni 10 basi asilimia 10 ya bilioni 10 lazima itengwe kwa ajili ya wanawake na vijana. (Makofi)
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza niishukuru Serikali kwa kupeleka fedha kwa ajili ya miradi hii ambayo imeorodheshwa, lakini kwa uhalisia ni kwamba miradi hii haijakamilika kwa asilimia mia, miradi miwili mradi wa Mfyome na Mradi wa Magunga – Isupilo kuelekea Lumuli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii kwa sababu imekaa kwa muda wa miaka miwili haijakamilika na Halmashauri imeshapelekwa Mahakamani kwa ajili ya kufanyiwa arbitration, napenda sasa kupata commitment ya Serikali ikiwa kama arbitration itaenda kinyume na matakwa ya Serikali, yaani Serikali ilipe fedha hizi kwa mkandarasi, itatumia mida gani kukamilisha malipo haya kwa wakandarasi ili wananchi wangu waweze kupata maji katika miradi yao? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika utaratibu wa kutafuta wakandarasi, Serikali inawaagiza wakandarasi kununua vifaa na hivyo katika ununuzi wa vifaa wakandarasi hawa wanatozwa kodi ya VAT, lakini wakati wa malipo baada ya kupeleka zile certificates Wizarani, Serikali hailipi zile fedha ambazo wakandarasi wameingia kwa maana ya VAT na hivyo basi miradi inaendelea kusimama…

MHE. GODFREY W. MGIMWA: ...miradi inaendelea kusimama kwa sababu ya kutofanyika kwa malipo haya. Napenda kujua, je, Serikali ina mtazamo gani sasa kuhakikisha kwamba VAT inalipwa kama fidia kwa hawa Wakandarasi ambao wako katika miradi hii? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza linahusu shauri lililopo katika taasisi inayoitwa Arbitration, kwamba je, ruling ikishatokea Serikali italipa Mkandarasi kwa muda gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge, swali hili nilijibu tu kwamba shauri linaendelea na linazungumzwa kwa mujibu wa sheria na taratibu za mikataba, kwa hiyo ruling itakapofikia pia tutalipa kutokana na taratibu zinazoendelea za kimkataba bila wasiwasi wowote. Labda niseme, nikuhakikishie kwamba Hazina, Serikali yako ya Awamu ya Tano kwa sasa hatuna mgogoro mkubwa; wakandarasi wakishaleta certificate wakati wowote tunalipa, hatuchukui muda mrefu. Kwa sasa nina shilingi bilioni saba, angeleta hata leo basi tusingechukua wiki moja tungekuwa tumeshamlipa tayari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili linahusu kodi, VAT; Mheshimiwa Mbunge, sisi tushughulikie utekelezaji wa miradi. Serikali imejigawa katika taasisi mbalimbali, suala hili lina wahusika na wahusika hao wameainishwa katika mikataba na Mkandarasi anajua inapofikia suala la VAT aende wapi. Kwa hiyo, tuliache suala hili litekelezwe na wahusika ambao ni watu wa TRA.
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza na nitakuwa na maswali mawili.
Mheshimiwa naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imefanya kazi kubwa kuhakikisha kwamba inapeleka miundombinu kwenye vijiji na miji midogo. Hata hivyo, bado hakujakuwa na mbinu mbadala ambayo inaweza ikasababisha mabenki haya yakaenda kuanzisha benki katika vijiji. Napenda kufahamu, ingawa hakuna sera, sasa Serikali kwa sababu imeshafanya haya yote, ina utaratibu gani sasa kuhakikisha kwamba Benki zinapeleka huduma zao kule vijijini? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni kwamba mabenki mengi hasa Benki za Kilimo na Benki ya Wanawake bado hazijapata fursa ya kupeleka huduma vijijini. Mwezi huu na miezi inayofuata benki hizi zitakwenda kufungua matawi Dodoma na Mwanza, lakini bado hazijagusa katika vijiji husika ambako kuna asilimia kubwa ya wakulima na wananchi wetu wapo kule ambao wanategemea sana shughuli za kibenki.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kufahamu; je, kwa nini sasa Serikali inaendelea kuruhusu mabenki haya kuanzishwa au kufunguliwa katika miji mikubwa na siyo vijijini ambako ndiko kwenye tija?
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kukushukuru, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza ameuliza kuhusu mpango mbadala.
Napenda kuliarifu Bunge lako tukufu kwamba mpango mbadala upo na Serikali inausimamia vizuri na ndiyo maana katika huduma za fedha jumuishi, Taifa letu kwa Afrika nzima linaongoza kuwa na huduma za fedha jumuishi kama mpango mbadala wa kuwafikia wananchi kule walipo. Katika ulimwengu mzima, Taifa letu linachukua nafasi ya tatu kwamba linafanya vizuri katika kuhakikisha huduma za fedha jumuishi zinawafikia wananchi wetu kule walipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi ni mashahidi, kumekuwa na wakala wa mabenki yetu, kumekuwa na huduma hizi kupitia makampuni yetu ya simu, wananchi wetu tunawafikia. Kama nilivyosema katika jibu langu la msingi kwamba tuko katika soko huria katika sekta ya fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, haiwezekani kulazimisha mtu ambaye anakwenda kufanya biashara kwamba lazima afungue sehemu fulani. Serikali inachokifanya ni kutengeneza mazingira mazuri na ndiyo maana tunaongoza katika Afrika katika mfumo wa huduma wa fedha jumuishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kuhusu Benki yetu ya Kilimo na Benki ya Wanawake; napenda kuliambia Bunge lako tukufu kwamba kama yeye alivyokiri, mwezi huu wa tano na mwezi wa sita Benki yetu ya Kilimo inafungua tawi lake hapa Dodoma na kule Mwanza na hii ni katika jitihada za Serikali yetu kuhakikisha huduma za benki hizi ambazo zinafanya kazi moja kwa moja na wananchi wetu zinawafikia wakulima. Tuzipe nafasi benki zetu hizi tutawafikia wananchi kule walipo.
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza naomba niseme kwamba mradi huu una zaidi ya miaka 35 na idadi ya watu ambao wapo katika eneo hili sasa hivi imeongezeka zaidi ya mara tatu na miundombinu yake imechakaa. Halmashauri imeomba fedha jumla ya shilingi milioni 276 lakini fedha zilizopelekwa ni shilingi milioni 59 tu, napenda kufahamu, hizi shilingi milioni 59 ambazo zinagawanywa katika majimbo mawili katika wilaya moja zitawezaje kukamilisha mradi wenye idadi ya watu wengi kama huu ambao unategemewa na wananchi zaidi ya 36,000? Hilo swali la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni kwamba, je, Naibu Waziri au Waziri wanaweza wakawa wako tayari kuungana na mimi ili twende Kalenga tukaone mradi huu ambao kwa kweli ukikamilika utakuwa unaleta tija kwa wananchi wangu?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa faida ya Wabunge wote, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mgimwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa tumeshaweka utaratibu kwamba, hatukuletei fedha mpaka uzalishe. Kwa hiyo, hiyo shilingi milioni 59 imekuja kulingana na certificate uliyoleta. Ungeleta certificate ya shilingi milioni 200 basi tungekupa shilingi milioni 200. Hatuleti fedha ukae nayo, kwanza lazima uzalishe ndio tuweze kuleta fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali la pili, nilishafika huko, lakini pia nitamruhusu Naibu Waziri wangu tukishamaliza Bunge ataambatana naye. Hata hivyo, niwape utulivu wananchi wa Kalenga kwamba ule mradi sasa ni mkubwa tunahitaji fedha nyingi siyo shilingi milioni 200 tena. Ndiyo maana katika jibu la msingi la Mheshimiwa Naibu Waziri amesema tunataka tuufanyie usanifu kwa sababu utagharimu hela nyingi ili tuweze kutafuta fedha kwa wafadhili tuhakikishe kwamba maji yanawatosheleza wananchi wote wa eneo hilo.
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Mwenyekiti,ahsante; nitakuwa nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto kubwa kwenye vituo vyetu vya afya na zahanati na changamoto kubwa ni upatikanaji wa magari ambayo yanawasafirisha wagonjwa (ambulance). Ningependa kufahamu katika vituo hivi ambavyo tunavyo katika Jimbo la Kalenga vituo kama vinne, tuna gari mbili tu lakini moja linatumika kupeleka wagonjwa katika Jimbo zima. Ningependa kufahamu, je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba tunaongezewa gari hasa katika Kituo cha Afya cha Mgama? (Makofi)
Tuna changamoto kubwa ya madawa kwenye vituo vyetu vya afya na zahanati mbalimbali hasa katika Jimbo langu la Kalenga. Ningependa kufahamu kwa sababu vituo hivi vya afya vinatumika kwa wananchi wengi. Ningependa kufahamu katika Kituo cha Ng’enza, Kituo cha Itwaga na Kituo cha Muwimbi ni lini sasa madawa yataanza kupelekwa kwa sababu kuna vituo vimeshafunguliwa kupitia mwenge lakini mpaka sasa hivi havina madawa na havijaanza kufanya kazi, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MIKOA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maswali yake mawili ya nyongeza la kwanza anaulizia juu ya suala zima la upatikanaji wa gari (ambulance). Naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mgimwa, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba gari zinapatikana kwa kadri hali inavyoruhusu na hivi karibuni tunatarajia kupata gari 70 na katika gari hizo 70 ambazo tunatarajia kuzipata ni matarajio ya Serikali kwamba tutalenga katika maeneo ambayo yana upungufu mkubwa sana. Nina amini eneo la kwake kama ni miongoni mwa maeneo ambayo yana upungufu mkubwa litakuwa considered.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili anaulizia juu ya vituo vya afya vitatu ambavyo amevitaja kwamba vituo vya afya hivyo dawa hazipatikani. Naomba nikiri kwa fursa niliyopata ya kuzunguka katika maeneo yote ya Tanzania kwa mara ya kwanza ndiyo nasikia kwamba kuna vituo vya afya ambavyo havipati dawa. Ni vizuri tuwasiliane na Mheshimiwa Mbunge ili tujue tatizo ni nini kwa sababu ni azma ya Serikali kuhakikisha vituo vyote vinapokamilika na dawa ziweze kupatikana ili huduma iliyokusudiwa na Serikali iweze kupatikana kwa wananchi.
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri, ingawa katika maeneo aliyozungumza kuhudu REGROW hajaeleza kiuwazi kwamba itakuwa ni lini makumbusho yatakuwa yameanza. Nina maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza ni kwamba, wananchi wa Jimbo la Kalenga hasa katika Kata husika ya Kalenga hawanufaiki na chochote kupitia Makumbusho haya ya Mkwawa Mkwavinyika, zaidi wanapata zile fedha ndogo ndogo kupitia watalii ambao wanakuja kununua bagia, maandazi na mbogamboga. Sasa sijui Serikali ina utaratibu gani kuhakikisha kwamba wananchi wa Kalenga hasa katika Kata husika ya Kalenga wananufaika na Makumbusho haya ya Mkwawa Mkwavinyika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni kwamba, kutokana na utaratibu ambao umeanzishwa na Serikali kuhakikisha kwamba tunajenga au kuboresha barabara ya Iringa Mjini kuelekea Ruaha ambayo iko katika utaratibu wa REGROW ningependa kufahamu kupitia Mheshimiwa Waziri kwa sababu Ruaha National Park ni mbuga kubwa katika Bara la Afrika na Tanzania kwa ujumla. Ningependa sasa kufahamu, je, utaratibu wa ujenzi wa barabara hii ambayo inaenda Ruaha National Park ukoje ukizingatia kwamba Wizara ya Ujenzi imeshaeleza kwamba itaijenga barabara hii, lakini vile vile kwa sababu inakidhi mahitaji ya Wizara ya Maliasili, je, kuna mawasiliano yoyote kati ya Wizara hizi mbili kujua barabara hii itaanza kujengwa lini?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajibu maswali mawili ya Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa kwanza niwape salamu Wanayanga wote, kamwene, mnogage.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya salamu hizo kwa Wanayanga, naomba kujibu maswali ya Mheshimiwa Mgimwa kama ifuatavyo:

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza ni kwamba, Mtwa Mkwavinyika Mnyigumba Mwamuyenga ni shujaa wa Taifa, ni alama ya Utanzania wetu na ni miongoni mwa watu mashuhuri ambao sisi watoto wa Tanzania tunajinasibu nao. Pia hawezi kuwa mtu ambaye anaweza kutupa historia inayoleta faida kwa watu wa Kalenga peke yake, kwa hivyo mafanikio yatakayopatikana kutokana na Mtwa Mkwavinyika Mnyigumba kuwa ni Mtwa wa Wahehe na ngome yake kuwa pale Kalenga ni kuvutia watalii kuja katika eneo lile na hiyo multiplier effect anayoizungumza kwamba watalii watalala, watatembelea maeneo mbalimbali, watajifunza historia ya Wahehe, wataacha pesa pale, lakini sio lazima moja kwa moja kwa kuwa Mtwa Mkwavinyika alikuwa wa eneo lile, basi iwe tu ni kwa faida ya watu wa pale, huyu ameshakuwa alama ya Taifa. Kwa hivyo, kinachopatikana kutokana na utalii kinaingia kwenye taasisi za Serikali na wananchi wanafaidika na kodi inayotokana na Sekta ya Utalii kwa ujumla wake na pia wananchi wanafaidika kwa kufanya shughuli mbalimbali ambazo zinaendana na mnyororo mzima wa kazi au shughuli za utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuhusu barabara ya kutoka Iringa kwenda Msembe, ni barabara muhimu sana kiutalii na ni barabara ambayo tunaipa kipaumbele cha hali ya juu katika kuifungua circuit ya Kusini hususan kuitumia Hifadhi ya Taifa ya Ruaha kwa faida zaidi kiutalii. Pia ni barabara ambayo Serikali katika bajeti hii tutakapokuwa tukitoka hapa tuna uhakika itakuwa imepitishwa na katika mikakati yetu ni kwamba tutaanza sisi wenyewe kuijenga barabara hii japokuwa tayari tuna fedha kutoka Benki ya Dunia kwa ajili ya barabara hii kuunganisha pia na Mradi wa Kuboresha Uwanja wa Ndege wa Nduli. Kwenye uwanja wa ndege wa Nduli uliopo pale Iringa tayari Mkandarasi atatangazwa muda si mrefu, tunabaki na hii barabara ya kuunganisha Iringa Mjini na Hifadhi ya Taifa Ruaha kwenye eneo la Msembe. Kwa hivyo, hii barabara naijua vizuri japokuwa mimi sio Waziri wa uchukuzi wala wa Ujenzi kwa sababu ni barabara muhimu sana kiutalii kama anavyosema Mheshimiwa Godfrey Mgimwa.
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Spika, ahsante, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi lakini pia niishukuru Serikali kwa majibu mazuri kwa sababu barabara hii imekuwa ni ya muhimu sana lakini sasa tumeenda kupata hizi bilioni 4 kwa hiyo tunaishukuru sana Serikali kwa jitihada hizi.

Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza, swali la kwanza ningependa kujua je, katika utaratibu ambao unaendelea sasa hivi wa upembuzi yakinifu, Serikali imejipaga vipi kuhakikisha kumba fidia kwa wananchi wale katika barabara ile inapatikana kwa wakati na yenye tija?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, nilitaka nifahamu, kuna barabara ambayo inatoka Wasa kuelekea Kiponzelo mpaka Kalenga ambapo unaenda kuunganisha katika na hiyo barabara ya Ruaha Msembe. Ningependa kufahamu, kwa kuwa barabara hii nayo ni ya muhimu sana kiuchumi. Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba inaitengeneza au kuiboresha barabara hii katika kiwango cha lami ili wananchi wa maeneo haya waweze kuungana na wale wanaoenda Ruaha National Park? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa
Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mgimwa kwa sababu amekuwa akifuatilia sana barabara hii na barabara nyingine hii ya Wasa – Kiponzelo – Kalenga aliyoitaja. Serikali imekamilisha uthamini, wa wananchi watakuwa na stahili ya kupata fidia katika maeneo haya na takribani shilingi bilioni 2 imekadiriwa kwamba itatumika kuwalipa fidia wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nikuhakikishie tu kabla ujenzi haujaanza kama ilivyo taratibu wananchi hawa wa maeneo haya watalipwa fidia kama wanavyostahili kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara yako ile uliyoitaja Wasa – Kipanzelo – Kalenga takribani kilomita 70 hivi, ni barabara ambayo inasimamiwa na wenzetu upande wa TARURA na sisi mkazo mkubwa kupitia Mfuko wa Barabara ni kuhakikisha kwamba wanapata fedha za kutosha barabara iweze kupitika.

Kwa hiyo, utaratibu wa sasa wa Serikali ni kuunganisha maeneo ya mikoa na mikoa, na maeneo muhimu ya uzalishaji. Kwa hiyo, siku za mbeleni pia barabara hii tutaitazama baada ya kuwa muunganiko umekuwa mzuri kwa barabara za lami.