Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Zainab Mndolwa Amir (5 total)

MHE. ZAINAB M. AMIR aliuliza:-
Mboga za majani ni lishe bora kwa afya ya binadamu na wakulima wengi wa mbogamboga katika Jiji la Dar es Salaam wanatumia maji yasiyo salama kwa ajili ya kumwagilia na huenda maji hayo yana kemikali zinazoweza kusababisha mbogamboga hizo kudhuru afya za wananchi badala ya kuziimarisha:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia maji safi na salama wakulima hao wa mbogamboga?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Mndolwa Amir, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu kwa kuzingatia umuhimu wa afya za wananchi inaendelea kutoa miongozo na ushauri kuhusu maji yanayofaa kwa matumizi ya binadamu na kwa shughuli za uchumi. Katika kuhakikisha wananchi wanalima mbogamboga katika maeneo sahihi, Serikali iliunda Kikosikazi kwa kushirikisha Maafisa wa Baraza la Mazingira la Taifa (NEMC).
Mheshimiwa Spika, kikosi hicho kilitembelea baadhi ya mito iliyopo Dar es Salaam na kugunda uchafuzi mkubwa wa mazingira unaosababishwa na utiririshaji wa maji taka kutoka majumbani na kwenye viwanda na hivyo maji hayo kuwa na kemikali zisizofaa kwa matumizi ya kilimo cha mbogamboga, kwa mfano maji ya Mto Msimbazi.
Mheshimiwa Spika, Serikali inawakataza wananchi kulima mbogamboga katika maeneo hayo yenye uchafuzi kwa kuwa maji hayo yana athari kwenye afya. Aidha, kwa kuwa suala hili ni mtambuka na linahusu uchafuzi wa mazingira, Wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira, inaendelea kupima maji ya mito hiyo na kutoa taarifa za hali ya maji. Pia halmashauri za manispaa katika Jiji la Dar es Salaam zinashauriwa kutunga na kusimamia sheria ndogo kwa ajii ya kudhibiti uchafuzi wa maji ya mito hiyo.
Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutoa elimu kwa wananchi ili waweze kufanya shughuli zao za kilimo cha umwagiliaji, ikiwemo umwagiliaji wa mbogamboga katika maeneo sahihi.
MHE. ZAINABU M. AMIRI aliuliza:-
Je ni lini Serikali itapunguza bei ya gesi kwa matumizi ya majumbani ili kuwawezesha wananchi wengi zaidi kutumia gesi kwa matumizi yao ya nyumbani na kuondokana na matumizi ya kuni na mkaa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainabu Mndolwa Amiri, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, gesi iliyogunduliwa nchini ni gesi asilia (natural gas) ambayo husafirishwa kutoka kwenye visima vya gesi hadi kwa watumiaji kupitia mabomba. Mpaka sasa watumiaji wakubwa wa gesi hapa nchini ni viwanda na mitambo ya kufua umeme. Mradi wa majaribio wa gesi asilia kwa ajili ya matumizi ya nyumbani ulianza kupitia mradi wa mfano (pilot project) ambapo nyumba 70 zilizopo Mikocheni Jijini Dar es Salaam zimeunganishwa na gesi kwa matumizi ya nyumbani.
Mheshimiwa Spika, hivi sasa gesi inayotumiwa na wananchi kupikia majumbani ni Liquefied Petroleum Gas (LPG) ambayo huagizwa na wafanyabiashara kutoka nje kama ilivyo katika mafuta ya petrol, diesel na mafuta ya taa au ndege. Gesi hii hujazwa katika mitungi kwa ujazo tofauti tofauti na gharama ya gesi hii inategemeana na soko la dunia.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuhamasisha wawekezaji katika sekta ya gesi kwa ajili ya matumizi ya majumbani ili kuleta ushindani katika sekta hii. Mpaka sasa makampuni mengi yameanza kujenga miundombinu ya gesi katika sehemu mbalimbali za nchi na kuonesha nia ya kushirikiana na Serikali katika kusambaza gesi asilia nchini.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TPDC imeanza matayarisho ya kutekeleza mradi wa kuunganisha gesi majumbani ambapo awamu ya kwanza ya mradi huo utapita katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam na Mtwara na baadaye katika mikoa mingine ya nchi yetu. Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. ZAINAB M. AMIRI aliuliza:-
Daraja la Kigamboni ni kichocheo cha maendeleo ya kiuchumi na mawasiliano.
(a) Je, tangu daraja lianze kutumika Serikali imekusanya kiasi gani cha fedha kinachotokana na malipo kwa wanaovuka na vyombo vya moto?
(b) Je, ni lini Serikali itaweka utaratibu wa kutumia kadi maalum (smart card) kulipia kwa mwezi malipo kwa wanaovuka darajani hapo kwa vyombo vya moto?
wanaovuka darajani hapo kwa vyombo vya moto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Mndolwa Amiri, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) ambao ndiyo wanasimamia uendeshaji wa daraja hilo hadi kufikia mwezi Machi, 2018 limeshakusanya kiasi cha Sh.19,734,655,482.70 tangu daraja hilo lilipoanza kutumika rasmi mwezi Mei, 2016. Aidha, katika mapato hayo, shilingi bilioni 15.2 ni makusanyo ya waliovuka na vyombo vya moto na shilingi bilioni 4.7 ni faida na pato la ziada la mtaji lililotokana na upatikanaji wa fedha hizo katika dhamana ya Serikali.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii lipo katika hatua za mwisho za kumpata Mkandarasi wa kuweka mfumo utakaotumia kadi maalum (smart card) kwa malipo ya wanaovuka darajani hapo. Mvukaji atakuwa na hiari yake ya kulipia kwa siku, wiki au mwezi kulingana na uwezo wake.
MHE. ZAINAB M. AMIR aliuliza:-

Wananchi wengi wamejenga makazi yao bila kuzingatia mipangomiji na matokeo yake kuvunjwa nyumba zao bila kupata fidia pindi Serikali inapoanza ujenzi unaozingatia mipangomiji:-.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwapatia wananchi elimu stahiki ili waepukane na adha hiyo?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Mndolwa Amiri, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikitekeleza mikakati mbalimbali ya kuwaelimisha wananchi kuhusu ujenzi unaozingatia mipangomiji ili kuepuka madhara mbalimbali ikiwemo kubomolewa nyumba zao bila kulipwa fidia. Mikakati hiyo ni pamoja na kutoa elimu kwa njia ya vyombo vya habari kama vile redio, luninga, magazeti, vipeperushi, machapisho mbalimbali, mitandao ya kijamii pamoja na tovuti ya Wizara.

Mheshimiwa Spika, sambamba na utoaji wa elimu kupitia vyombo vya habari, viongozi wa Wizara wamekuwa wakitumia mikutano ya hadhara katika ziara zao nchini kutoa elimu kuhusu umuhimu wa wananchi kujenga kwa kufuata utaratibu hususan katika maeneo ambayo yametangazwa kuwa ni maeneo ya kimipangomiji. Aidha, kupitia kaulimbiu ya ‘funguka kwa Waziri wa Ardhi’ Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi pamoja na mambo mengine amekuwa akipokea changamoto mbalimbali kuhusu ujenzi holela mijini na kutoa elimu stahiki kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kujenga kwa kufuata utaratibu uliowekwa kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Spika, kwa maeneo ambayo yameendelezwa bila kupangwa, Serikali imetoa fursa kwa wananchi kurasimishiwa makazi yao na kupatiwa hatimiliki. Urasimishaji makazi pamoja na mambo mengine unasaidia kuwapatia wananchi fursa ya kutumia ardhi yao kama mtaji, kutoa miundombinu ya msingi, kupunguza migogoro, kuvutia uwekezaji na kuweka huduma za kijamii. Katika maeneo mengine ambayo urasimishaji haufanyiki, utambuzi wa milki na uhakiki hufanyika na wananchi wa maeneo hayo kupewa leseni za makazi ambazo zinasaidia kuimarisha usalama wa milki na kutumika kama dhamana za mikopo kutoka katika taasisi za kifedha.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kusisitiza kuwa wananchi wazingatie sheria na taratibu za uendelezaji miji ili kujiepusha na ujenzi holela. Aidha, wananchi waepuke kujenga mijini bila kuwa na vibali vya ujenzi ili kuepuka maafa na madhara kwa mali zao.
MHE. ZAINABU M. AMIRI aliuliza:-

Mboga za majani ni lishe bora kwa afya ya binadamu na wakulima wengi wa mbogamboga hasa Jijini Dar es Salaam wanatumia maji yasiyo salama kwa ajili ya kumwagilia na huenda maji hayo yana kemikali zinazoweza kupelekea mbogamboga hizo kudhuru afya za wananchi badala ya kuziimarisha:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia maji safi na salama wakulima hao wa mbogamboga?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba mboga za majani ni lishe bora kwa afya ya binadamu na wakulima wengi wa mboga hizi waliopo Jiji la Dar es Salaam hutegemea Bonde la Mto Msimbazi kwa ajili ya kuendeleza shughuli zao. Hata hivyo, Mto Msimbazi unaendelea kukabiliana na changamoto za uharibifu wa mazingira unaosababishwa na shughuli za kiuchumi na kijamii ikiwemo kilimo cha mbogamboga kando ya mto huo.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali kwa kushirikiana na wadau imeendelea kutoa elimu kuhusu hifadhi ya vyanzo vya maji na kutekeleza mipango na shughuli mbalimbali kwa ajili ya kulinda mazingira ya mto huo yasiharibiwe.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imeandaa mradi wa kuboresha Bonde la Mto Msimbazi ili kukabiliana na changamoto zitokanazo na uharibifu wa mazingira katika mto huo. Mradi huu unalenga kupunguza athari za mafuriko, kudhibiti mmomonyoko wa udongo unaosababishwa na shughuli za binadamu kando ya mto huo, kujenga uwezo wa jamii inayozunguka Mto Msimbazi kuendelea na shughuli za kiuchumi pasipo kuathiri mto, kupanda miti kwa ajili ya hifadhi ya mazingira ya mto, kuweka mkakati wa udhibiti wa taka ngumu katika mazingira ya Mto Msimbazi na kujenga mazingira wezeshi kwa wajasiriamali wadogo kuendeleza shughuli zao pasipo kuathiri mazingira ya mto huo.

Mheshimiwa Spika, kwa kuboresha mazingira ya Bonde la Mto Msimbazi, tunategemea kwamba uchafuzi wa mazingira katika mto huo utapungua. Hata hivyo, Kifungu cha 57 cha Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya Mwaka 2004 kinazuia shughuli za kudumu na ambazo kwa asili yake inaweza kuhatarisha au kuathiri vibaya utunzaji wa bahari au kingo za mto na mabwawa katika eneo la hifadhi mita 60 kutoka vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Spika, aidha, sheria hii inampa mamlaka Waziri mwenye dhamana ya usimamizi wa Mazingira kuandaa mwongozo wa matumizi endelevu wa eneo hilo. Kwa muktadha huo, Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais imeandaa rasimu ya mwongozo wa mita 60 wa kuhifadhi vyanzo vya maji. Rasimu hii inaainisha matumizi endelevu ya eneo la mita 60 kutoka vyanzo vya maji ikiwemo shughuli za kilimo kando na vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Spika, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Zainabu Mndolwa Amiri kwamba Serikali itaendelea kuboresha Sera, Sheria na Kanuni ili kuhakikisha kwamba kunakuwepo na usimamizi thabiti wa mazingira ya nchi yetu. Aidha, ni matumaini yangu kuwa Waheshimiwa Wabunge watakuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha wananchi kuzingatia sheria zilizopo katika kufanya shughuli za maendeleo ili kufanikisha azma ya Serikali ya kuhifadhi mazingira na kuboresha ustawi wa jamii.