Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Shamsia Aziz Mtamba (12 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kujenga hospitali ya kisasa ya Benjamin Mkapa iliyopo Dodoma, lakini napenda kuishauri Serikali kwamba hospitali ile ina upungufu mkubwa wa madaktari pamoja na wauguzi. Hivyo basi Serikali iangalie hospitali ile kwa ukaribu mkubwa kwani inahudumia wananchi wa maeneo mengi sana kama vile UDOM ambapo wanafunzi takribani wote wanatibiwa pale, Wabunge na wananchi wa Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na ongezeko kubwa la udhalilishaji wa wanawake na watoto. Naishauri Serikali iweze kutoa mafunzo pale akina mama wanapokuja kliniki ni namna gani inapotokea kubakwa kwa mtoto wake. Katika hatua ya awali kitu gani afanye ili ushahidi wa awali uweze kupatikana. Mara nyingi ushahidi huu hukosekana kwa vile huwasafisha kwa kuwakosha wakiona wanaweka vizuri kumbe wanapoteza ushahidi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Viwanda na Biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya nzuri na leo hii kuweza kusimama katika Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa pongezi za dhati kabisa kwa Mwenyekiti wangu wa Chama-Taifa, full bright, Profesa Ibrahim Lipumba kwa kazi kubwa ambayo anaifanya ya ujenzi wa Chama changu. Pia napenda kutoa pongezi za dhati kabisa kwa Naibu Katibu Mkuu, Mheshimiwa Magdalena Sakaya kwa kazi kubwa ambayo anaifanya ya ujenzi wa Chama changu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niingie katika mada. Wakati Tanzania tunaelekea katika uchumi wa viwanda, ni lazima tuwe na umeme wa uhakika na hakuna mwekezaji atakayekubali kujenga kiwanda ili apate hasara kwa sababu umeme unapokosekana kwa saa nne tu ni hasara kubwa kwa mwekezaji. Kwa mfano, itabidi apunguze wafanyakazi lakini pia wafanyakazi wataliobaki wanahitaji mishahara. Pia uzalishaji utakuwa chini ya kiwango, kwa mfano, kiwanda kilichopo kule kwetu Mtwara, Kiwanda cha Saruji cha Dangote kama kilikuwa kinazalisha kwa siku tani 100, umeme unapokatika uzalishaji utapungua, kiwanda kitazalisha tani 60 badala ya tani 100. Hii ni hasara kubwa kwa Taifa na mwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije katika masuala ya ajira. Umeme unapokuwa wa mgao au unapokatika mwekezaji itabidi apunguze wafanyakazi. Akifanya hivyo atakuwa amepunguza ajira na familia nyingi zitaishi maisha ya dhiki kwa kuwa kipato cha familia kitakuwa kimepungua.

Mheshimiwa Spika, vijana wengi sasa wameamua kujiajiri kwenye viwanda vidogo vidogo kama viwanda vya kuchomelea (welding), viwanda vya kuwekea samaki, viwanda vya kutengeneza barafu, viwanda vya salon za kike na za kiume, vyote vitakuwa hazifanyikazi kwa kukosa umeme wa uhakika. Hii ni hasara kubwa kwa Taifa.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije upande wa kodi za Serikali. Uzalishaji wa viwandani ukipungua hata kodi za Serikali nazo zitapungua. Serikali itashindwa kutimiza majukumu yake ya kupeleka miradi ya maendeleo kwa wananchi wake. Ushauri wangu kwa Serikali iwekeze nguvu kubwa katika uzalishaji wa gesi iliyoko kule Msimbati, gesi ya Mnazi Bay ili iweze kutimiza majukumu yake ya kusambaza umeme wa majumbani na viwandani.

Mheshimiwa Spika, niongelee masuala ya kibiashara. Akina mama wengi tumepata mwamko wa kufanya biashara lakini kikwazo kikubwa tunachokumbana nacho ni kodi kubwa tunazotozwa na Maafisa wa TRA, tunafanyiwa makadirio makubwa mno. Naiomba Serikali yetu Tukufu ya Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli itupunguzie kodi hizi kwa sisi wajasiriamali, kama maduka ya nguo, vifaa vya ujenzi, mahoteli, biashara ya magari ya abiria yaendayo mikoani na daladala. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuwarudisha kazini wale wote ambao waliachishwa kazi kwa sababu ya kuwa na elimu ya darasa la saba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali iangalie kwa jicho la huruma hospitali ya Rufaa ya Mtwara. Katika hospitali hii kuna upungufu mkubwa wa Madaktari pamoja na Wauguzi. Hospitali hii inahudumia wagonjwa wengi sana kutoka maeneo mengi sana ya Mkoa wa Mtwara. Katika hospitali pia kuna upungufu mkubwa wa dawa.

Naomba hospitali hii iongezewe bajeti ili wananchi wa Mkoa huu wa Mtwara waweze kupata dawa na huduma za kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha za vijana/ akinamama. Kwa mujibu wa sheria, kila halmashauri ina majukumu ya kutenga asilimia 10 kwa ajili ya vijana asilimia tano na akina mama asilimia tano. Hata hivyo, kwa kuwa vyanzo vya mapato ya kodi za majengo (property tax) na ushuru wa mabango vimechukuliwa na TRA, Halmashauri haziwezi kutoa fedha za mikopo kwa akinamama na vijana. Hii inasababisha vijana na akinamama kuchukua mikopo BRAC, FINCA na kadhalika. Taasisi hizi zina riba kubwa na akinamama wanachukuliwa vyombo vyao vitanda, makochi, TV, radio na kadhalika pale wanaposhindwa kulipa riba hizo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Spika, naanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uhai na uzima. Naomba Askari wetu waongezewe mishahara katika bajeti hii kwani wanafanya kazi katika mazingira magumu sana, usiku na mchana, jua lao mvua yao. Kwa hiyo, naishauri Serikali iwaangalie Askari wetu hawa waongezewe posho kwani hali ya maisha ni ngumu sana. Posho ya shilingi 300,000/= kwa mwezi ni ndogo sana, haitoshi. Ina maana Askari huyu pamoja na familia yake inabidi atumie shilingi 10,000/= kwa siku kuanzia asubuhi mpaka jioni. Je, itamtosha Askari huyu? Hali hii inasababisha Askari wetu wajihusishe na masuala ya rushwa ili wakidhi mahitaji yao.

Mheshimiwa Spika, nyumba wanazoishi Askari wa Magereza ni aibu, nyumba za Polisi Mtwara ni za tangu enzi za mkoloni na hazijaboreshwa. Jengo la Kituo cha Polisi cha Mtwara ni chakavu, kuta zina nyufa, hali inayosababisha kuwa na hatari kwa Askari wetu na wanaweza kuangukiwa na jengo hilo.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa, tunaomba Jeshi la Polisi lisitumike vibaya kwenye masuala ya kisiasa. Jeshi hili lifanye kazi yao kwa weledi bila kuegemea upande wowote.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya Wiwanda na Biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya mzuri na leo hii nikaweza kusimama katika Bunge hili. Pia nitoe pongezi zangu za dhati kabisa kwa Fulbright Prof. Ibrahimu Haruna Lipumba kwa kuchaguliwa na Wajumbe wa Mkutano Mkuu Taifa kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi CUF. Nitoe pongezi zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Muftaha Abdalla Nachuma kwa kuchaguliwa na Wajumbe wa Mkutano Mkuu Taifa kuwa Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi CUF. Vilevile nitoe pongezi za dhati kabisa kwa Baraza Kuu la Uongozi wa Taifa kwa kumchagua Mheshimiwa Magdalena Hamis Sakaya kuwa Naibu Mkuu wa Chama cha Wananchi CUF. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, azma ya Serikali ni kuelekea Tanzania ya viwanda. Katika kuelekea Tanzania ya viwanda hatua ya kwanza ni kuondoa urasimu pale wanapokuja wawekezaji kwa kuwapatia maeneo ya ujenzi haraka na mapema iwezekanavyo. Hata hivyo, Wizara ya Viwanda kumekuwa na urasimu na kodi kubwa hali inayopelekea baadhi ya wawekezaji kuhamia nchi jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano ni Kiwanda cha Kubangulia Korosho cha Olam ambacho kilikuwa katika Mkoa wa Mtwara. Kiwanda kile kilifanya kazi vizuri sana na kuliweza kutoa ajira kwa wanachi wa Mkoa ule vijana na akina mama waliweza kuendesha maisha yao kupitia kiwanda hicho lakini mpaka sasa napozungumza kiwanda hicho hakipo kimehamia nchini Msumbiji. Je, Serikali haioni kuwa inakosa mapato na ajira kwa Watanzania? Nataka commitment ya Serikali hali hii ya kuhamahama wawekezaji katika nchi yetu itaisha lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoimarisha viwanda nchini tunahitaji malighafi (materials) zinazozalishwa na wakulima wetu. Wakulima wakiwa na masoko ya uhakika wataweza kuongeza juhudi za uzalishaji wa mazao ambayo ndiyo malighafi viwandani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee Shirika la Viwanda Vidogovidogo (SIDO). Tanzania tunalo Shirika la Viwanda Vidogovidogo (SIDO) lakini hatulitumii ipasavyo kwa sababu SIDO wanabuni na kutengeza mashine na mitambo mbalimbali inayoweza kutumika katika kilimo, ujenzi, nishati, uchimbaji wa visima, lakini havitangazwi. Tumekuwa tukiona karakana nyingi za SIDO mitambo yake ni chakavu na haifanyi kazi kabisa matokeo yake wananchi na Serikali wanatumia fedha nyingi kununua mashine na mitambo mbalimbali kutoka China. Natoa wito kwa Serikali itumie teknolojia yetu mzuri ya SIDO. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la wafanyabiashara wadogo wadogo. Ni ukweli kuwa akina mama wengi ndiyo wafanyabiashara ndogondogo na za kati, lakini nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kuliona suala la vitambulisho kwa wajasiliamali wadogo wadogo. Pia niishauri Serikali akina mama lishe, wauza matunda, maandazi, samaki, wasamehewe au walipe kidogo kidogo kutokana na kipato chao kuwa kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuchangia katika Mpango huu wa Maendeleo wa Taifa. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya nzuri na leo hii nikaweza kusimama katika Bunge hili, lakini pia nitoe shukrani zangu za dhati kabisa kwa wapiga kura wangu wa Jimbo la Mtwara Vijijini kwa heshima kubwa ambayo wamenipa na leo hii nikaweza kurudi tena katika Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, gesi inayotumika kuzalisha umeme Kinyerezi inatoka Mtwara katika Kijiji cha Msimbati, inapitia Madimba ndipo inaposafirishwa kuelekea Kinyerezi. Kwa mshangao mkubwa sana sehemu ambako inatoka gesi asilia, Msimbati, miundombinu ya barabara ni mibovu mno. Barabara ni mbovu haipitiki kabisa hasa kipindi hiki cha masika. Hivyo, niiombe Serikali katika Mpango huu wa Maendeleo irekebishe barabara hii muhimu ambayo inaleta uchumi wa Taifa, ijengwe kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanaoishi katika eneo ambalo inatoka gesi wana mazingira duni sana. Hivyo, niiombe Serikali iwaangalie wananchi hawa kwa kuwawekea mazingira ya kuwaboreshea afya bora, elimu pamoja na uchumi kiujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wetu wa Mtwara na Kusini kwa ujumla Mwenyezi Mungu ametujalia tuna korosho nzuri na bora kabisa, lakini pia tuna gesi asilia, lakini pia tuna bandari kubwa ambayo ina kina krefu. Kwa masikitiko makubwa sana Bandari hii ya Mtwara haifanyi kazi ipasavyo ukilinganisha na Serikali ilivyotumia pesa nyingi kuwekeza katika Bandari hii ya Mtwara; haifanyi kazi, hii inanyima maendeleo kwa Taifa na maendeleo kwa watu wa Kusini kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mwenyewe ni shahidi. Nikiwa natoka Mtwara naelekea Dar-es-Salaam natumia barabara, lakini napishana na malori njiani ambayo yamebeba simenti pamoja na korosho. Mizigo hii ingeweza kupitia katika bandari yetu ya Mtwara, lakini inatumia barabara. Hii inaleta uharibifu mkubwa wa barabara na inaipa Serikali jukumu kubwa la kuikarabati barabara hii mara kwa mara. Sasa niishauri Serikali katika Mpango huu ione umuhimu mkubwa sana wa kuitumia Bandari ya Mtwara ambayo italeta maendeleo kwa watu wa Kusini, lakini pia kwa Taifa kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka ya nyuma tulikuwa tunaziona meli nyingi zikifika katika bandari yetu ya Mtwara na vijana wengi wa Mtwara waliweza kupata ajira…

(Hapa kengele ililia)

MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuni… eeh, si nimesikia kengele?

MWENYEKITI: Ni kengele ya kwanza Mheshimiwa, bado ya pili.

MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali na niishauri kwa ajili ya Taifa kwa ujumla, ione umuhimu wa kuwekeza katika Bandari hii ya Mtwara ili iweze kufanya kazi ipasavyo. Bandari hii ingeweza kupata mizigo mingi kutoka Songea, Makambako, lakini pia na sehemu nyinginezo, wangeweza kuitumia bandari hii, leo hii hali ya maisha ya watu wa Mtwara yamekuwa magumu kwelikweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wengi walikuwa wanajipatia ajira katika bandari hii, lakini cha kushangaza bandari hii imetupwa kabisa, imesahaulika kabisa wakati bandari hii ina kina kirefu cha kupokea meli zaidi hata ya 15 au 20. Kwa hiyo, niiombe Serikali ione umuhimu wa kuitumia bandari hii. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuchangia hotuba hii ya Waziri Mkuu. Awali ya yote, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya nzuri na leo hii nimeweza kusimama katika Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miongoni mwa matatizo makubwa yanayowakabili wananchi wa Jimbo langu la Mtwara Vijijini ni maji. Ifike wakati Serikali itoe fedha kwa ajili ya kusambaza maji kutoka Mto Ruvuma hadi kwa wananchi wangu. Sijui kwa nini suala hili limekuwa gumu wakati Serikali ilitenga fedha na wananchi walifanyiwa uthamini mwaka 2015 ili mradi huu uanze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo langu la Mtwara Vijijini lina kata 21, lakini ndani ya kata hizi 21, zote zimekuwa na changamoto kubwa sana ya maji ikiwemo Kata ya Mango pacha nne. Kata hii tokea tumepata uhuru haijawai kabisa kufurahia huduma hii ya majisafi na salama. Nikija Kata ya Libwidi, nayo imekuwa na changamoto kubwa sana ya maji; halikadhalika na Kata za Naguruwe, Kata ya Mkutimango, Kata ya Mbalawa na Makome, Kata ya Naumbu na Pemba Pwani nazo zimekuwa na changamoto kubwa sana ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Mkoa wa Mtwara kiujumla tuna changamoto kubwa sana ya maji, ndiyo maana tunataka mradi huu wa Mto Ruvuma ufanye kazi. Mradi huu wa Mto Ruvuma utaleta manufaa kwa maeneo mengi. Sitafaidika mimi katika jimbo langu tu, wanaweza kunufaika kwa kaka yangu Mheshimiwa Chikota; kwa kaka yangu Mheshimiwa Katani; utakwenda Nanyumbu; watakwenda Songea na Namtumbo. Kwa hiyo, mradi huu wa Mto Ruvuma una faida sana na utanufaisha maeneo mengi wataweza kupungukiwa na kero hii ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Mtwara uchumi wetu mkubwa ni Korosho. Naomba katika Bajeti hii, zao hili la Korosho lisiyumbishwe yumbishwe, mwachie bodi ifanye kazi yake. Naiomba Serikali irudishe Mfuko wa Pembejeo. Mfuko huu ulikuwa ni mkombozi kwa mkulima wa Korosho. Kwa hiyo, wananchi na wakulima wa Korosho wa Mtwara wamenituma, ni lini Mfuko huu wa pembejeo utarudishwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingi nikisimama ndani ya Bunge nimekuwa nikizungumzia sana masuala ya matibabu kwa wananchi hasa kwa wananchi wangu wa Mtwara Vijijini. Kusema kweli wamekuwa wakipata taabu sana wanapokwenda katika hospitali zetu hasa wale wenye magonjwa makubwa kama moyo pamoja na figo. Wapokwenda katika hospitali zetu wanakuta Madaktari Bingwa hakuna, wanaambiwa waende Muhimbili. Kutokana na uchumi wa watu wetu wanashindwa kwenda Muhimbili. Hivyo, naishauri Serikali iweke utaratibu angalau kwa miezi miwili au mmoja wawe wanatuletea Madaktari Bingwa katika mikoa yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta ya Uvuvi iboreshwe hasa katika Jimbo langu la Mtwara Vijijini. Sekta hii napenda iboreshwe katika maeneo yafuatayo: wavuvi wapewe elimu ya kisasa, wapatiwe mikopo na vyombo vya kisasa vya uvuvi kama mashine za boti, nyavu, ndoana, pamoja na vifaa vingine. Pia wavuvi wapewe semina mbalimbali za kuwajengea uwezo ili kuhifadhi hifadhi ya bahari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na doria mbalimbali katika bahari zetu. Jeshi la Polisi wamekuwa wakifanya doria mbalimbali, lakini wavuvi wamekuwa wakilalamika kupigwa pamoja na kuchomewa nyavu zao. Kwa hiyo, naomba wasitumie nguvu kubwa, watoe elimu ya kutosha kwa wavuvi. Wakikamilisha haya, Serikali na Halmashauri wataweza kupata mapato ya kutosha kutokana na uvuvi. Pia zitengwe bandari maalum kwa ajili ya uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuchangia katika hotuba hii ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya nzuri na leo hii nikaweza kusimama katika Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilizungumza bajeti ya mwaka jana kuwa changamoto kubwa ambayo inatukabili hasa katika Jimbo langu kwenye masuala ya barabara ni barabara ya ulinzi ambayo imepita Kilambo – border kuelekea Kitaya mpaka Tandahimba. Barabara hii ni barabara muhimu mno hasa kwa usalama wa watu wetu pamoja na vyombo vyetu vya ulinzi. Hivyo, nilikuwa naiomba sana Serikali iingalie barabara hii kwa umuhimu wake na tunatambua hali ambayo inaendelea katika mipaka yetu kule, niiombe sana Serikali iweze kujenga barabara hii muhimu kwa kiwango cha lami ili vyombo vyetu vya ulinzi vinapofanya doria katika maeneo yale basi viweze kufika kiurahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna barabara ya uchumi ambayo inatoka Mtwara Mjini kuelekea Msimbati ambapo kuna mitambo na visima vya gesi, barabara hii nayo imesahaulika. Barabara hii ni mbovu sehemu ambapo tuna mitambo ya gesi kule barabara ni mbovu na haipitiki kabisa hasa kipindi cha masika. Hivyo, ninaiomba sana Serikali iangalie barabara hii ya uchumi ijengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa changamoto kubwa ambazo zinatukabili wananchi wa Mkoa wa Mtwara ni suala la maji, suala hili la maji bado limekuwa sugu sana katika Mkoa wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna chanzo kikubwa cha maji chanzo cha Mto Ruvuma, niiombe sana Serikali itumie chanzo hiki cha maji cha Mto Ruvuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2015 uthamini ulishafanyika kwa wananchi, wananchi wangu wa Mtwara Vijij,ini hawaelewi wamenituma niwaulize chanzo hiki cha maji mtatumia lini na lini mradi huu utaanza? Maana wananchi wanashindwa kuendeleza maeneo yao kutokana na kutokulipa fidia mpaka leo.

Mheshimiwa Waziri wa Maji ninakuomba utakapokuja mbele kwenye majumuisho utueleze mradi huu ni lini utaanza na lini wananchi hawa watalipwa fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la bandari. Bandari ya Mtwara ipo Tanzania wala haipo nchi jirani, lakini kwa masikitiko makubwa sana bandari hii imesahaulika bandari hii imesahaulika. Serikali imewekeza fedha nyingi sana katika bandari hii ya Mtwara lakini imesahaulika na haifanyi kazi ipasavyo. Hivyo, ninaiomba sana Serikali katika msimu wa mwaka huu tunataka kuona bandari ya Mtwara inafanya kazi ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka kuona korosho yote ya msimu ya mwaka huu inatumia bandari yetu ya Mtwara. Pia tunayo kila sababu ya kuitumia bandari hii kwa sababu tuna mizigo, mizigo ambayo itatoka Malawi inaweza kupitia bandari hii ya Mtwara, pia tuna cement ya Dangote inaweza kutumia bandari hii ya Mtwara. Leo hii barabara ya Lindi – Dar es Salaam ni mbovu kila siku inafanyiwa matengenezo kutokana na uharibifu wa malori ambayo inaharibu barabara hii. Serikali kama mngekuwa mnatumia bandari ya Mtwara leo hii barabara yetu isingekuwa inatengenezwa mara kwa mara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kupepesa maneno nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea viuatilifu kwa wakati kwa wakulima wetu wa korosho. Nimpongeze pia Mheshimiwa Waziri naye sitamtendea haki kwa kulisimamia suala hili mpaka leo hii kutuletea viuatilifu vya korosho kwa wakati kwa wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kitu kimoja tupange utaratibu wa kugawa viuatilifu hivi ili kuondoa mkanganyiko ambao ulijitokeza kwenye msimu uliopota. Ninaiomba Serikali ni lazima kuwe na takwimu katika ugawaji wa viuatilifu hivi na takwimu maalum za kila mkulima ili wakulima wote waweze kupata viuatilifu hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya nikushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuchangia katika bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya nzuri na leo hii nikaweza kusimama katika Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwapongeze Waheshimiwa Mawaziri kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya, pia nijielekeze katika mchango wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza kwenye suala la afya. Jimbo langu la Mtwara Vijijini nina Kata 21, Vijiji 110. Jambo cha kusikitisha ni kwamba nina zahanati 28 tu, nina vituo vya afya vitatu. Hivyo, niiombe sana Serikali ituongezee vituo vya afya pamoja na zahanati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna hospitali yetu pale ya Wilaya Nanguruwe. Hospitali hii imekuwa na uhaba mkubwa sana wa watumishi. Kwa mfano ukiangalia upande wa maabara katika hospitali hii ya Wilaya tuna mtu mmoja tu pale ambaye anatoa huduma, lakini ukija kwenye suala la Mfamasia, ngazi ya degree hatuna Mfamasia kabisa, lakini ngazi ya diploma tuna Mfamasia mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali hii ya wilaya ambayo ipo Nanguruwe inahudumia watu wengi sana lakini kuna Manesi Wanane tu katika hospitali hii. Hivyo, niiombe sana Serikali ituongezee watumishi wa kutosha katika hospitali yetu hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali hii bado inaendelea kujengwa, kuna wodi ambazo zinajengwa, idadi ya watumishi ni chache. Kwa hiyo ninaomba tuongezewe watumishi wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu zahanati, katika Kata ya Mpapura Kijiji cha Nanyani, kuna ujenzi wa zahanati pale tokea Julai, 2017, lakini mpaka leo takribani miaka minne mitano, zahanati ile imekwisha na imejengwa vizuri lakini haijafunguliwa mpaka leo. Nimuombe sana Mheshimiwa Waziri alichukue hili, ile zahanati sasa hivi inaharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nimetembelea, mchwa wameanza kula katika milango na madirisha. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri lichukue hili, zahanati hii ianze kufanya kazi ili wananchi waweze kupata huduma pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuja kwenye suala la TARURA. TARURA ni muhimu sana katika barabara zetu, lakini changamoto kubwa ambayo inatokea katika TARURA ni ukosefu wa fedha, wana shida ya fedha ya kutengeneza barabara zetu za vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara zetu za vijijini ni mbovu mno, hasa katika Jimbo langu. Barabara ni mbovu na hazipitiki kabisa. Barabara nyingine zimejifunga kutokana na mvua kubwa ambazo zilikuwa zinanyesha. Kwa mfano, barabara ya Mkunwa – Namayakata. Barabara hii ni mbovu nayo, haipitiki. Pia kuna barabara inayohudumia Wilaya ya Tandahimba – Newala, barabara hii pia ni mbovu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ya Msanga Mkuu, ni kilometa 17. Barabara hii inahudumia vijiji takribani vinne; Ziwani, Nalingu, Msakara pamoja na Mkubiru. Barabara hii nayo imekuwa ni changamoto kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunayo barabara nyingine ambayo nayo imejifunga kabisa, yaani haipitiki, wa huku wa huku, wa huko wa huko. Kwa hiyo, naomba barabara hii iangaliwe. Barabara ambayo inaanzia Naumbu – Kabisela. Barabara hii nayo ni mbovu, ni kilometa 21.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara nyingine ni barabara ya Dihimba (kilomita 17) nayo ni mbovu sana. Hivyo, niombe sana Serikali na Wizara mlichukue hili muweze kututengenezea barabara zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la elimu kwa haraka haraka. katika Jimbo langu la Mtwara Vijijini tuna changamoto kubwa sana katika Sekta hii ya Elimu. Tuna uhaba mkubwa sana wa watumishi kwa shule za msingi na sekondari, pia tuna changamoto kubwa za nyumba za walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jimbo langu hali ni mbaya mno. Nyumba za walimu hakuna. Kwa mfano, Shule ya Msingi Mnete, hakuna nyumba za walimu. Mdui, Nanyati, Nanyani, Milumba hakuna nyumba za walimu. Nina vijiji 110…

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi. Mchango mwingine nitaleta kwa maandishi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuchangia hotuba hii ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya nzuri na leo hii nikaweza kusimama katika Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nitaanza kwa kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuhakikisha Watanzania wa mijini na vijijini wanapata maendeleo. Kwa hakika wanawake tunaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze kwa dhati Waziri Mkuu kwa kuguswa katika Jimbo la Mtwara Vijijini, tulipopata maafa makubwa kweli ya mafuriko. Tunamshukuru sana kwa kuchukua hatua ya haraka kuwafikia wahanga wa mafuriko na kutupatia misaada ya kibinadamu. Kwa kweli Mheshimiwa Waziri Mkuu wananchi wa Jimbo langu hasa wa Kata ya Kivava, Kata Mahurunga, Kijiji cha Kivava wanakushukuru sana. Misaada imewafikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Mkuu wangu wa Mkoa wa Mtwara, Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, na vyombo vya ulinzi na usalama vyote, kwa kweli wamefanya kazi kubwa ya kuhakikisha wahanga wa mafuriko wapo katika sehemu nzuri na wanapata huduma nzuri. Ninawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu nitazungumzia sehemu tatu. Kwanza, nitaanza kuzungumzia kuhusu Wizara ya Uchukuzi. Tokea nimekuwa Mbunge katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nimekuwa nikizungumzia sana suala la barabara; barabara ya ulinzi na pia barabara ya uchumi inayotoka Mtwara Mjini kuelekea Msimbati ambako kuna mitambo na visima vya gesi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna barabara yetu ya ulinzi, ina umuhimu mkubwa sana. Barabara hii ni muhimu Serikali iiangalie kwa macho mawili kwa sababu itaweza kulinda usalama wa watu wetu na kutoa urahisi kwa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kufika katika maeneo kwa uharaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tumekwenda kule kwa wahanga wa mafuriko, barabara hii ni mbovu na haipitiki kabisa. Sehemu ambayo tulitakiwa tutumie muda wa saa moja, tumetumia karibu masaa manne kutokana na ubovu wa barabara. Ninyi mnafahamu hali halisi iliyopo katika maeneo yetu kule mipakani, kwa hiyo, barabara hii ina umuhimu mkubwa sana wa kututengenezea kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija kwenye barabara ya uchumi ambayo inatoka Mtwara Mjini kuelekea Msimbati, ambako kuna mitambo na visima vya gesi kule. Ninaongea kwa masikitiko makubwa sana, ni aibu, sehemu ambayo tumewekeza uwekezaji mkubwa, barabara ni mbovu; sehemu ambayo kuna mitambo kule ya gesi, kuna visima vya gesi, barabara ni mbovu. Ninaiomba sana Serikali mwiangalie barabara hii kwa macho mawili na kwa umuhimu wake, mtujengee kwa kiwango cha lami kwa uharaka kutokana na umuhimu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kuzungumzia kwenye suala la maji. Katika majimbo sugu yenye changamoto ya maji, ni Jimbo la Mtwara Vijijini. Bajeti iliyopita nilizungumza hapa katika maeneo ambayo bado hayajafikiwa vizuri kwenye huduma hii muhimu ya maji safi na salama, ni Jimbo langu la Mtwara Vijiji. Kuna maeneo mengi yana changamoto ya maji. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali, na Mheshimiwa Aweso nimekufuata mara nyingi, nakuomba kaka yangu utuone kwa macho mawili katika Jimbo langu Mtwara Vijijini, bado tuna changamoto kubwa ya maji katika maeneo mengi. Maeneo mengine toka tumepata uhuru wa nchi hii, hawajawahi kabisa kufuruhia huduma hii muhimu ya maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna mradi wa maji wa Mto Ruvuma. Kuna bomba limepita katika maeneo yale, na kuna wananchi walishafanyiwa uthamini tokea mwaka 2015, takribani miaka nane, mpaka leo hii wananchi wale hawajapewa fidia karibu vijiji 25; Kijiji cha Mayembe, Mitambo, Madimba, Kitaya, Kihamba, Kivava, Mahurunga, Kitunguli, Kihimika, Litembe mpaka Mtwara Vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo haya wananchi wanashindwa kuendeleza maeneo yao kutokana na kutolipwa fidia. Kwa hiyo, naiomba Serikali iangalie maeneo haya, wananchi wanashindwa kufanya maendeleo kutokana na kulipwa fidia yao. Kama wameshindwa kuendeleza, Serikali naomba mtueleze ili maeneo haya wananchi waweze kufanya shughuli zao za maendeleo, waweze kufanya shughuli zao za kilimo, waweze kufanya shughuli zao za ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia suala la afya. Tunaishukuru sana Serikali kwa kutujengea majengo mengi katika vijiji vyetu; zahanati na vituo vya afya, lakini kuna uhaba mkubwa wa watumishi katika maeneo yetu, hasa katika maeneo ya vijijini. Tunaiomba Serikali watuletee watumishi wa kutosha. Utakuta zahanati nyingi muuguzi yupo mmoja; mgawa dawa ni huyo huyo, mchoma sindano ni huyo huyo, mzalishaji ni huyo huyo. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali iangalie maeneo mengi ya vijijini, kuna uhaba mkubwa sana wa watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nitazungumzia kuhusu suala la kilimo. Sisi wananchi wa Mkoa wa Mtwara, kilimo chetu kikubwa ni zao la korosho, uchumi wetu mkubwa ni zao la korosho. Tunaomba msimu wa mwaka huu usiyumbishwe yumbishwe. Tunaiomba sana Serikali watuletee viuatilifu kwa wakati. Pia nilizungumza kwenye bajeti ya mwaka jana 2022, tunaiomba Serikali ifanye takwimu kwa kila mkulima wa korosho kwa ajili ya ugawaji wa viuatilifu ili kuondoa mikanganyiko inayojitokeza mara kwa mara katika ugawaji wa viuatilifu hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza hayo, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya TAMISEMI. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya nzuri na leo hii nikaweza kusimama katika Bunge hili lakini pia nikupongeze kwa namna unavyoliongoza vizuri Bunge letu, Mwenyezi Mungu akujalie Spika wetu ili uweze kutuendelea kutoongoza vizuri katika Bunge letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitaanza kuzungumzia kwa upande wa wakulima wa korosho. Upande wa wakulima wa korosho, dawa, viwatilifu vipelekwe kwa wakati. Kumekuwa na mabadiliko kila mwaka aina nyingine ya dawa kila mwaka aina nyingine ya dawa hali hii inapelekea wakulima wetu kutofanya vizuri katika uzalishaji wa korosho.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niiombe Serikali iangalie kama kutakuwa na mwaka mwingine kunakuwa na mabadiliko ya dawa basi naomba watu wetu wa kilimo wawe wanatoa elimu kwa wakulima wetu juu ya matumzi ya dawa hiyo. Maana mara nyingi wakulima wamekuwa wakitumia dawa bila kuwa na uhakika. Hali hii inapunguza tija kwa uzalishaji wa korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije kuzungumzia kwenye suala la afya. Mara nyingi nimekuwa nikisema hapa ndani ya Bunge kuhusu juu ya matibabu kwa wananchi wangu wa Jimbo la Mtwara Vijijini. Wananchi wangu wa Jimbo la Mtwara Vijijini wanapata tabu sana wanapokwenda kwenye matibabu hasa wale wenye magonjwa ya moyo, figo na magonjwa mengine. Wanapokwenda katika hospitali zetu kupata matibabu kwa kweli wamekuwa wanakosa madaktari Bingwa. Tumekuwa na uhaba mkubwa sana wa madaktari bingwa katika Mkoa wetu wa Mtwara. Hivyo niiombe sana Serikali itupatie madaktari bingwa wa magonjwa haya ya moyo, figo na magonjwa mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunaomba Serikali iweke utaratibu hata kwa mwezi mara moja wawe wanatuletea madaktari bingwa katika mkoa wetu wa magonjwa haya; kwa sababu watu wetu wanapata shida sana wanapokwenda kwenye hospitali tumekuwa na changamoto kubwa ya madaktari bingwa. Wanaambiwa waende Muhimbili wanapewa rufaa ya kwenda Muhimbili sasa kutokana na kipato cha watu wetu wanashindwa kwenye Muhimbili kwa ajili ya kupata matibabu.

Mheshimiwa Spika, tuna hospitali yetu ya kanda ya kusini; Kwanza ninaishauri Serikali kwa kutujengea hospitali ya kanda ya kusini. Tunaishukuru sana Serikali kwa kuliona hili katika mkoa wetu lakini pia kumekuwa na changamoto kubwa katika hospitali hii ya kanda ya kusuini. Tumekuwa na changamoto ya nyumba za kulala watumishi, watumishi wanaishi mbali na hospitali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niiombe sana Serikali itujengee nyumba kwa ajili ya watumishi wetu katika hospitali yetu ya kanda ya kusini lakini pia ituletee madaktari bingwa pamoja na vifaa tiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna upungufu mkubwa sana wa watumishi kwenye zahanati na vituo vya afya kwenye Jimbo langu la Mtwara Vijijini. Tumekuwa na upungufu mkubwa sana wa watumishi katika sekta hii ya afya kwenye zahanati zetu watumishi hawapo wa kutosha kwenye vituo vya afya watumishi hawapo wa kutosha. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali ituletee watumishi wa kutosha katika vituo vyetu vya afya pamoja na zahanati zetu.

Mheshimiwa Spika, niwapongeze wananchi wangu wa Jimbo la Mtwara Vijijini kwa kweli wamekuwa wakijitolea sana kujenga maboma kwa ajili ya zahanati. Wamekuwa wakifanya kazi kubwa sana wananchi wangu ya kuhakikisha wanapata zahanati katika ngazi zetu za vijiji lakini sasa wanashindwa wanakwama na wakikwama maboma yanakaa muda mrefu bila muendelezo. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali iwaangalie wananchi hawa wa Jimbo la Mtwara Vijijini ambao wanajitoa kuhakikisha wanajenga wenyewe na maboma ya zahanati. Kwa hiyo, Serikali lazima itie mkono na lazima iwape nguvu.

Mheshimiwa Spika, sasa nije nizungumzie suala la maji. Kila nikisimama kwenye Bunge hili siachi kuzungumzia suala la maji. Katika Jimbo langu la Mtwara Vijijini bado tumekuwa na changamoto kubwa ya maji katika Jimbo la Mtwara Vijijini bado hatujafikiwa kwenye huduma hii muhimu ya maji safi na salama. Sielewi tatizo liko wapi, tuna vyanzo vya maji, tuna Chanzo cha Maji cha Mto Ruvuma, tuna Chanzo cha Maji cha Bwala la Kitere tuna Chanzo cha Maji cha Makonde.

Mheshimiwa Spika, vyanzo vya maji tunavyo, tatizo liko wapi, kwa nini Serikali haitumii vyanzo vya maji hivi ili kumaliza tatizo la maji katika Jimbo langu la Mtwara Vijijini ili kumaliza tatizo la maji katika Mkoa wetu wa Mtwara. Vyanzo vya maji vipo lakini tatizo ni nini msitumie vyanzo hivi vya maji ili kuwatua ndoo kichwani wamama wa Mtwara Vijijini. Wamama wa Mtwara Vijijini wanapata tabu sana, ndoa zinakufa, wamama wanaliwa na wanyama wakali kwa sababu ya kutafuta maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika jimbo ambalo limekuwa na changamoto ya maji ni Jimbo langu la Mtwara Vijijini. Niiombe sana Serikali iliangalie hili vyanzo vya maji tunavyo. Naomba mtumie vyanzo vya maji hivi ili kumaliza tatizo la maji katika Jimbo langu la Mtwara Vijijini.

Mheshimiwa Spika, nikija kwenye suala la elimu; tuna upungufu mkubwa sana wa walimu kwenye shule za msingi na sekondari katika jimbo langu. Kuna mapungufu makubwa ya walimu, kwa hiyo, niiombe sana Serikali iangalie katika jimbo langu mtuletee walimu wa kutosha wanafunzi ni wengi, walimu ni wachache. Kwa hiyo niiombe sana Serikali iangalie katika upande huu ya kutuletea watumishi katika Jimbo langu la Mtwara Vijijini.

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu kabisa. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya nzuri na leo hii nikaweza kusimama katika Bunge hili. Lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa January Makamba na Naibu wake, wajomba zangu wale wote wawili, kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuhakikisha Watanzania wa mijini na vijijini wanapata huduma hii muhimu ya nishati ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo langu la Mtwara Vijijini, nina vijiji 24 ambavyo vinahitajika kuwashwa umeme. Vijiji tisa kati ya 24 ndivyo vimewashwa umeme, vijiji 11 bado vinaendelea, mkandarasi yupo site anaendelea na kazi; vijiji vinne bado kabisa havijafikiwa kuwashwa umeme. Kwa maelezo ya mkandarasi amezungumza mpaka kufikia Desemba vijiji vyote 24 vya Mtwara Vijijini vitakuwa vimewashwa umeme. Kwa hiyo nimuombe mkandarasi ambaye anashughulika na suala hili katika Jimbo langu la Mtwara Vijijini aongeze speed ili mpaka kufikia Desemba basi vijiji vyote viwe vimekamilika kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, gesi hii inatoka katika Jimbo langu la Mtwara Vijijini katika Kijiji cha Msimbati, lakini kwa masikitiko makubwa sehemu ambayo inatoka gesi asilia umeme unawaka maeneo ya barabarani, ukiingia ndani hakuna umeme. Vijiji na vitongoji vingi umeme hakuna katika Kijiji hiki cha Msimbati ambapo gesi hii asilia inatoka. Kwa hiyo hii ni aibu, ni aibu kubwa sana. Niombe sana Mheshimiwa Waziri, wewe ni msikivu sana, nikuombe Kaka yangu tuhakikishe vijiji hivi vinapatiwa umeme haraka sana kutokana na umuhimu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vijiji ambavyo vina shida ya umeme ni Kijiji cha Mnuyo katika Vitongoji vya Mnamba, Bumbwini, Lianje pamoja na Vitongonji wa Najibu na vitongoji vingine vingi sijavitaja. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri tunakuomba sana, sehemu hii ni sehemu muhimu, sehemu hii ndio sehemu ambako gesi inatoka. Kwa hiyo niombe Mheshimiwa Waziri wananchi hawa waweze kufurahia huduma hii ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sehemu ambayo gesi inachakatwa, Madimba, maeneo mengi na vijiji vingi navyo hakuna umeme. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri, nayo sehemu hii kwa umuhimu wake naomba umeme ufike kwa haraka kwenye vijiji pamoja na vitongoji. Kwa mfano Vitongoji vyote vya Mahiva, Uvikwani, Litembe, Miembeni, Namnaida B, Namindondi pamoja na Mitambo Shuleni hakuna umeme. Hii ni aibu kubwa kweli kweli kwa sababu maeneo haya sehemu ambayo gesi ipo, sehemu ambayo inachakatwa gesi umeme hakuna. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, na nikushukuru Mheshimiwa Waziri, kwa moyo wangu wa dhati kabisa, nilizungumza na wewe nikakueleza juu ya changamoto hizi, nashukuru Mheshimiwa Waziri jitihada ambazo umezichukua zinaendelea kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa hivi ninavyozungumza…

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa inatokea wapi? Aah! Mheshimiwa Shamsia Mtamba kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Soud.

TAARIFA

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba tu kumpa taarifa Mheshimiwa Shamsia kwamba ni utaratibu ambao Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania umeuwekwa kwamba wale ambao either kama ni source ya maji au ni ya umeme basi kwanza waanze kupata umeme wao kabla ya kusambaza katika maeneo mengine. Kwa hivyo kama kweli kuna maeneo ambayo gesi inapita lakini hao hawanufaiki nayo basi nafikiria Mheshimiwa Waziri lazima ajitahidi awa support hao.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Shamsia Mtamba unaipokea taarifa hiyo.

MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Spika, ninaipokea tena kwa mikono miwili.

Mheshimiwa Spika, sehemu hii ya Msimbati na Madimba ni sehemu muhimu sana, na nimekuwa nikisema katika Bunge hili; barabara mbovu hakuna, huduma ya nishati ya umeme ndio kama hivyo hakuna, miundombinu ya watu wale maskini ya Mungu ni duni. Kwa hiyo, sehemu kama hii ni sehemu ya kuiangalia sana, sehemu kama hii inahitaji miundombinu ya shule nzuri ziwepo, maeneo haya shule nzuri hakuna, miundombinu ya afya, huduma za afya nzuri katika maeneo haya inahitaji ziwepo lakini miundombinu hiyo hakuna. Kwa hiyo ninaipokea taarifa ya Mheshimiwa kwamba maeneo haya ni lazima wayaangalie kwa macho mawili kutokana na umuhimu wake. Watu wale wanaweza wakahujumu kule. Kwa hiyo lazima Serikali muone umuhimu wa Vijiji vya Msimbati na Madimba, muwawekee mambo mazuri ili wananchi wale basi wafurahie na neema hii waliopewa na Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mwisho kabisa ni kusisitiza. Mheshimiwa Waziri, kwanza tunakushukuru kwa unyenyekevu wako na usikivu wako. Tumekaa kikao na wewe sisi Wabunge wa Mtwara, na Wabunge wa Mtwara kwa kweli tuna changamoto kubwa sana ya umeme. Tuna changamoto kubwa wananchi wetu wanalalamika, wananchi wetu vitu vyao vinaungua, wanapoteza vitu vyao kila siku kutokana na changamoto ya umeme ya kukatika katika. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri tunakuomba sana tuliyoyakubaliana kwenye kikao yafanyike kwa wakati na uamuzi mzuri uliouchukua wa kuhakikisha unakuja kutatua changamoto ya umeme katika Mkoa wetu wa Mtwara ndani ya siku 90 basi Mheshimiwa Waziri tunakuombea kwa Mwenyezi Mungu uweze kutimiza hili ili wananchi wa Mtwara waweze kufurahia huduma hii bora, huduma hii muhimu ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mambo mengi kwa kweli yamesimama, mambo mengi hayaendi, viwanda vingi sasa hivi wawekezaji wanashindwa kuja Mtwara kutokana na umeme kutokuwa wa uhakika. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nikuombe, wewe ni mtu msikivu wewe ni mtu ambaye unafikika, wewe ni mnyenyekevu njoo umalize tatizo la umeme katika mkoa wetu haraka. Njoo umalize tatizo la umeme katika Mkoa wa Mtwara kwa uharaka kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuzungumza hayo, ninakushukuru sana. (Makofi)