Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Abdallah Majurah Bulembo (1 total)

MHE. ABDALLAH M. BULEMBO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba nimuulize swali Mheshimiwa Waziri na kwa kuwa umeshasema hakuna nyongeza sasa itabidi niunganishe hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza linasema hivi; Serikali imeandaa Sera na kutunga sheria ili kuruhusu wageni kufanya kazi na kurithisha ujuzi kwa Watanzania. Je, wageni hawa wanatakiwa waruhusiwe kufanya kazi kwa muda gani?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bulembo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli maswali yanayohusu takwimu ni ngumu kupata takwimu halisi kwa sasa kwa sababu maandalizi yetu ni ya kisera zaidi. Nchi inao utaratibu wake, iko Sheria ya Ajira na iko Sheria inayohusu waajiriwa wa ndani ya nchi na nje ya nchi na kwa bahati nzuri jambo hili liko kwenye ofisi yangu, Ofisi ya Waziri Mkuu. Sheria namba moja ya mwaka 2015 ndiyo ambayo hasa inagusa kwenye mambo ya ajira na inapotokea ajira zinahusisha sekta za kitaalam na zinahitaji wageni kutoka nje ya nchi tumeweka ukomo. Tunayo ile ratio ya 1:10 kwamba kwenye Watanzania kumi kunakuwa na mgeni mmoja.

Mheshimiwa Spika, tunachokifanya; tunatoa kibali cha kufanya kazi nchini. Ukomo wetu ni miaka miwili na katika hiyo miaka miwili, moja kati ya jukumu kubwa analolifanya huyu mgeni mwajiriwa ni kurithisha, kufundisha utaalam kwa Mtanzania ili anapomaliza miaka miwili basi Mtanzania awe ameshajua kazi ile ili Mtanzania aweze kuendelea na ile kazi.

Mheshimiwa Spika, pale ambapo tunaridhika kwamba ule utaalam bado Watanzania hatujapata vizuri, sheria pia inaruhusu kumpa fursa ya kuwaomba tena kuongezewa muda wa miaka miwili mingine. Tunaamini katika vipindi hivyo viwili vya miaka miwili miwili Mtanzania anaweza kuwa sasa ameshazoea kazi ile ambayo alikuwa anaifanya mgeni ili kuwapa uwezo Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hili makampuni yote yanayokuja nchini na wataalam hao tumeyapa sheria ya kwamba, kampuni inapoendesha sekta za kitaalam lazima waweke kipengele ambacho kinatoa mafunzo kwa Watanzania. Lengo ni kwamba, wanapomaliza muda wao, basi Watanzania kupitia mafunzo yale, wawe wameshazoea kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, masharti hayo yanatofautiana kwa hao ambao na wao wanaajiriwa kama wafanyakazi, lakini pia wakati mwingine sheria inabadilika kama kunakuwa na mwekezaji anakuja kuanzisha kampuni yake na pia inahitaji utaalam. Kwa hiyo tunaangalia mazingira hayo na huwa tunatoa fursa ya mwekezaji huyo kufanya kazi nchini na kiwanda chake au aina ya uwekezaji ambayo pia Watanzania nao watapata ajira zaidi.

Mheshimiwa Spika, hayo ndiyo ambayo tunapenda zaidi kuwakaribisha wawekezaji kujenga, kuwekeza, ili tuweze kufungua fursa zaidi za ajira kwa Watanzania. Kwa hiyo msisitizo hapa ni Watanzania kuendelea kupata nafasi za ajira nyingi za kutosha pamoja na kupata utaalam ambao hatukuwa nao kupitia hao wawekezaji. Huo ndiyo utaratibu wa nchi.