Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Wanu Hafidh Ameir (1 total)

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. WANU HAFIDH AMEIR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi hii ili nichangie katika Hotuba hii ya Waziri wa Afya. Kwa kuanzia kwanza niipongeze Serikali yangu ya Awamu wa Tano kwa kazi nzuri ambayo imekuwa inafanya na hili halitaki tochi kabisa mwenye macho anaona kabisa kwamba kazi inafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Afya pamoja na Naibu wake kwa kazi yao nzuri ambayo wamekuwa wakiifanya. Hongera za pekee nimpelekee Mheshimiwa Waziri, amekuwa akishirikiana kwa karibu sana na Wizara ya Afya ya Zanzibar, pamoja na kwamba si Wizara ya Muungano lakini amekuwa akionesha ushirikiano kiasi kwamba kumekuwa na hamasa kidogo ya kazi katika Wizara ya Afya, Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba Mheshimiwa Waziri amekuwa akionesha mashirikiano, bado kuna changamoto kidogo katika mashirikiano haya. Tunashukuru sana kwamba anaonesha imani kwa upande wa Zanzibar, lakini bado kuna changamoto panapotokea mikutano ya Kimataifa kwa kweli upande mmoja unakuwa hauangaliwi vizuri. Kwa hiyo, tunaomba kuwe na mpango mahsusi ambao utashirikisha upande mmoja wa Muungano kunapotokea mambo kama haya ili na wao wawe wanafaidika katika fursa ambazo zinapatikana kutokana na washirika wa maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine katika Hotuba ya Mheshimiwa Waziri katika ukurasa wa 69 amezungumzia kuhusu tafiti ambazo wamekuwa wakifanya. Naomba niishauri Serikali wanapofanya hizi tafiti basi na upande ule mwingine wa Zanzibar wawe wanawashirikisha. Kwa sababu huwezi ukawa unatibu upande mmoja au unafanya tafiti upande mmoja lakini upande ule mwingine unakuwa tatizo liko pale pale. Nitachukua mfano, kwa mfano Zanzibar tuko vizuri katika kutibu malaria, tuko chini asilimia moja lakini kwa upande wa bara kuna mikoa ambayo iko even above 20 percent, kama kungekuwa na ushirikiano naamini Zanzibar ingeisaidia Tanzania Bara katika kupunguza Malaria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika maradhi mengine ya mlipuko kama kifua kikuu na UKIMWI huwezi ukaacha upande mmoja na kushughulikia upande mmoja kwa sababu kwa mfano kama kifua kikuu ni maradhi ambayo yanaambukizwa na hewa na sisi katika hii nchi yetu tuna pande mbili na kuna free movement za hizi pande mbili. Kwa hiyo, kama unatibu upande mmoja lakini upande mmoja hakuna matibabu yoyote na wana-cross kupita upande wa pili bado matatizo yanakuweko palepale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru kwa nafasi na naunga mkono hoja.