Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Shabani Omari Shekilindi (91 total)

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa kuniona. Kwa kuwa tatizo la Arumeru Mashariki linafanana kabisa na tatizo la maji la Lushoto.
Je, ni lini Serikali itaondoa adha hii kwa wananchi wa Lushoto?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Wilaya ya Lushoto mlalo wake wa ardhi ni mzuri kuruhusu ujenzi wa mabwawa. Tumeweka mpango wa kujenga mabwawa katika awamu hii ya programu ya pili ambayo yatasaidia kwenye irrigation pamoja na kuhakikisha kwamba tunapata maji ya kunywa kwa wananchi wa Jimbo lake.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa, Wilaya ya Lushoto inafahamika kwamba ni ya kilimo cha matunda na mbogamboga. Je, ni lini Serikali itajenga kiwanda cha matunda na mbogamboga katika Wilaya ya Lushoto, ili mazao yale yasiendelee kuharibika?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wananilazimisha kufungua bajeti yangu kabla ya muda, lakini anayelipa mahari anayo ruhusa ya kumwangalia mwari hata kabla ya siku ya harusi!
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kiwanda kinaitwa Sayona kitawekwa Mkoa wa Pwani, kitakuwa na uwezo wa kusindika tani 25,000 kwa mwaka. Kitachukua matunda yote ya ukanda wa Pwani mpaka ukanda wa Ziwa. Kuna kiwanda kinaitwa Osasuna kitajengwa Handeni kwa Msisi, kitaanza kuchakata Nanasi, kitakuwa na uwezo wa kulima nanasi kwa shamba la mwekezaji hekta 3,000 lakini out growers watapewa hekta 17,000 kumzunguka na yule mwekezaji atawajibika kuwasaidia wananchi wazawa namna ya kulima kisasa. Mwaka 2018 Novemba, tunaanza kutoa juice ya kwanza.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante, kwanza kabisa nimpongeze Waziri Lukuvi na timu yake kwa kunifungulia Baraza hili la Ardhi na hata watu wa Wilaya ya Lushoto sasa walimuombea dua maalum Lukuvi na timu yake kwamba kama kuna gagaziko basi liondolewe Mungu awaletee wepesi liweze kuondoka. Sasa naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza;
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba Waziri amekuja kutufungulia Baraza la Ardhi lakini bado tuna migogoro mikubwa ya ardhi kati ya kijiji cha Nywelo na msitu wa Shume; kati ya Shamba la Mkonge Mnazi na vijiji vya Kwemng‟ongo na kijiji cha Kwemkwazu; kijiji cha Kwetango na kijiji cha Kweulasi; kijiji cha Kwemashai na kijiji cha Kilangwi.
Je, ni lini Serikali itakuja kutatua migogoro hiyo?
Swali la pili; Kwa kuwa, Wilaya ya Lushoto yenye Tarafa za Lushoto, Mlola, Mlalo, Mtae, Umba, Bumbuli, Soni na Mgwashi. Je, ni lini sasa Serikali itapima maeneo yao kwa kuwapatia hati za kimila ili wapate fursa za kukopa kwenye mabenki kuinua uchumi wao?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na hilo la mgogoro wa ardhi kati ya Mkonge Mnazi Estate na vijiji vya Kwemkwazu na Kwemhong‟o, Kwemlazi na Kwetango, Kwemashai na Kilangwi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, unajua haya majina ya watani wangu kidogo ni magumu kutamka usipoangalia unaweza ukakosea, lakini nadhani nimeyataja vizuri. Kwa sababu tulikwishatoa maelekezo na kwenye kitabu cha migogoro, mgogoro huu umetajwa na hatua za kuanza kwenda kutatua au kutwaa tena lile eneo kuna hatua za kupitia ikiwemo na kutoa notes kwa mhusika, tayari Halmashauri wamekwishatoa notes kwa huyu Mmiliki wa Mnazi Estate, kwa hiyo mara muda wa notes zile siku 90 zitakapokuwa zimekwisha, basi hatua zingine zitachukuliwa ili kuweza kumaliza kabisa mgogoro huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe sana ndugu zangu, watani zangu wa Kwemashai, Kilangwi, Kwaulasi, Kwetango na Kwemkwizu na Kwemng‟ongo kwamba notes zikikamilika hatua kamili zitachukuliwa kama atakuwa ameshindwa kujitetea kama tunavyotarajia.
Swali lake la pili ameulizia habari ya upimaji katika Tarafa za Lushoto, Mlalo, Mlola, Mtae, Umba, Bumbuli, Soni na Mgwashi. Naomba tu nimhakikishie kwamba iwapo tutapitisha pia bajeti ambayo ndiyo inakwenda kupitishwa leo, tayari kule tumetenga pesa kwa ajili ya upimaji, takribani bilioni 8.8 ambazo zinakwenda kununua vifaa na vifaa hivi vitagawiwa katika ofisi zetu za Kanda ili watu waweze kupima katika maeneo kwenye Kanda zao ikiwemo haya maeneo ya Lushoto, Mlalo, Mtae, Umba, Bumbuli na maeneo mengine kama nilivyotaja hizi Tarafa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye suala la umilikishaji ardhi ambapo tunataka watu wote wawe na umiliki halali kwa maana ya kuwa na hati, tayari katika bajeti yetu tumetenga bilioni 13.8 ambazo zinakwenda kufanya kazi ya umilikishaji wa ardhi. Kwa hiyo haya yote yatakwenda kufanyika mara bajeti yetu itakapokuwa imepita, pia ni jukumu la Halmashauri zetu kuwa tayari katika suala hilo kwa sababu suala la upimaji pamoja na kwamba Wizara inafanya kazi hii, pia Halmashauri zinapaswa kujipanga vizuri kuweza kuona ni namna gani wanafanya matumizi bora ya ardhi katika baadhi ya vijiji vyao. Kwa sababu kiasi hiki bado kinaweza kisikidhi upimaji katika maeneo yote. Hivyo, kila Halmashauri inakumbushwa pia waone nao ni jukumu lao pamoja na kwamba Wizara itafanya kazi hiyo kupitia hizi pesa zilizotengwa, lakini bado Halmashauri wanao wajibu wa kupima maeneo yao.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa redio ya Taifa (TBC)haipatikani kabisa katika maeneo ya Lushoto hasa maeneo ya Makanya, Mlolo, Mlalo, Lushoto na Bumbuli.
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga mitambo hiyo ili wananchi wa Wilaya ya Lushoto waweze kupata taarifa za nchi kama wananchi wengine?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoeleza kwenye swali la nyongeza la Mheshimiwa Hamida, bahati nzuri kwenye hotuba yangu ya bajeti hapa tuliorodhesha Wilaya ambazo tutaboresha usikivu wake na Wilaya anayotoka Mheshimiwa Mbunge ni katika Wilaya tulizozitaja kabisa kwenye hotuba ya bajeti tuliyoiwasilisha hapa Bungeni.
Kwa hiyo nataka nikuhakikishie kwamba tathimini imekamilika, sasa kwa kuwa mmepitisha jana Finance Bill hapa fedha zitaanza kutoka na tutaweka kipaumbele kwenye eneo lako. Nikupongeze kwa kazi nzuri unayofanya kuwatetea wananchi wa Jimbo lako.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Kwa kuwa, Wilaya ya Lushoto ni ya wakulima wa mbogamboga na matunda hasa maeneo ya Mkuzi, Kishangai, Boeloi, Ubili, Lukozi, Baga na Mazumbai na wakulima hawa hawapati ruzuku za pembejeo. Je, Serikali ina mpango gani sasa kuwapatia wakulima hawa pembejeo ili na wao waweze kunufaika kama wakulima wengine wa nafaka?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa kama tulivyosema kwamba siyo mazao yote hupata ruzuku, nilifahamishe Bunge lako Tukufu kwamba mpango wa kutoa ruzuku ambao umeanza kwa muda sasa kuanzia mwaka 2003 umekuja kwa sababu ya kufanya mambo makuu matatu:-
(i) Kuongeza uzalishaji wa chakula, lakini vilevile kujaribu kuwafanya na kuwahamasisha wakulima waweze kutumia mbolea na mbegu bora.
(ii) Kuwasaidia wakulima ambao wana kipato cha chini kuweza kuongeza tija. Tumeanza na baadhi ya mazao kama nilivyosema kwa sasa Serikali inatoa ruzuku na pembejeo kwenye mazao makuu mawili katika maana ya Mpunga na mahindi lakini vilevile kwenye yale ya biashara kupitia bodi zao lakini pale tutakapoona kwamba inafaa tutaendelea kuongeza utaratibu wa kupatikana kwa ruzuku kwa mazao yote.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba nilieze Bunge lako Tukufu kwamba lengo la kutoa ruzuku siyo kufanya wakulima wawe wategemezi lengo ni kuwafanya wao waone umuhimu wa kutumia pembejeo. Kwa hiyo, kama wakulima wenyewe wanauwezo wa kujinunulia pembejeo bila kupata ruzuku.
MHE. SHABANI O. SHELIKINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa suala la umeme wa REA ni suala la Kitaifa, je, ni lini Serikali itawapatia umeme wananchi wa Makanya, Ngwelo, Kwemashai, Gare na maeneo yote yaliyoba katika Jimbo la Lushoto?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya Makanya pamoja na Ngwelo ambayo yalizungumzwa na Mheshimiwa Mbunge ambayo kwa sasa hayajapata umeme, taratibu zinazofanyika sasa ni kukamilisha upatikanaji wa umeme kwenye maeneo ya REA Awamu ya Pili na maeneo aliyoyasema Mheshimiwa Mbunge, maeneo matatu kwa sasa yameshawekwa kwenye orodha ya maeneo ambayo yatapatiwa umeme kwenye REA Awamu ya Tatu inayoanza mwezi Julai mwaka huu.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kituo cha Polisi Lushoto ndiyo cha kwanza na ndiyo kituo kikongwe Tanzania na sasa hivi kinajengwa upya na kinaishia kwenye mtambaa wa panya na kwenye Bajeti sijaona fungu lolote lililotengwa kwa ajili hiyo.
Je, Serikali ina mpango gani wa kumalizia kituo kile?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tuna matatizo ya uchakavu na upungufu wa Vituo vya Polisi katika maeneo mbalimbali nchini. Kwa hiyo, Kituo cha Lushoto ni kimojawapo katika maeneo ambayo yana changamoto hizo. Niseme tu kwamba kama ambayo nimekuwa nikijibu mara kadhaa hapa, tunafahamu changamoto hizo na tutajitahidi kuzipunguza kwa kadri ambavyo tunaweza kupata fedha za kutosha.
Mheshimiwa Naibu Spika, naamini kabisa, kwa kasi hii ambayo Serikali yetu ya Awamu ya Tano imeanza nayo ya ukusanyaji na udhibiti wa matumizi, basi katika muda wa miaka michache ijayo tunaweza tukapata bajeti ya kutosha kuweza kurekebisha matatizo haya ya Vituo vya Polisi pamoja na makazi ya Polisi.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Kiwanda cha Chai cha Mponde kimefungwa takribani miaka mitatu sasa na Msajili wa Hazina alivyokuja alitamka kuwa zimetengwa shilingi bilioni 4 na kwenye bajeti ya mwaka huu hazipo. Je, Serikali ina mpango gani wa kufungua Kiwanda cha Chai Mponde ili wakulima wale wasiendelee kupata adha ile?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha Mponde, shilingi bilioni 4, usitegemee pesa ya kuingia kwenye viwanda uione kwenye bajeti yangu, tunawasiliana na watu wenye pesa watawekeza pale. Nimekwenda mbele zaidi, nafanya mazungumzo na Serikali ya Misri kusudi chai ya Kagera - Maruku na chai ya Mponde - Tanga iuzwe moja kwa moja Misri. Mimi nina maslahi na kiwanda cha Mponde.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa Wilaya ya Lushoto ina Mjimbo matatu na Ofisi ya TRA ni moja tu kwa Majimbo yote matatu; je, ni lini Serikali itaipandisha hadhi Ofisi ya TRA, Lushoto na kutoa TIN Number, Motor Vehicle na License za udereva ili wananchi wasipate taabu ya kwenda mpaka Tanga Mjini?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tunajua Wilaya ya Lushoto ina Majimbo matatu na tuna Ofisi moja ya TRA.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama Mheshimiwa Mbunge atakumbuka ndani ya wiki mbili zilizopita, nilijibu kuhusu ufunguzi wa Ofisi za TRA, lakini kwa kuwa tuna Ofisi ya TRA Lushoto, kinachohitajika ni kupandishwa hadhi; namuomba Mheshimiwa Mbunge tuonane ili tuweze kukaa pamoja na tuone ni jinsi gani sasa tutaweza kuipandisha hadhi ofisi hii ili huduma hizi muhimu ziweze kupatikana kwa ajili ya wafanyabiashara wetu.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa kuwa Wilaya ya Lushoto ni ya wakulima wa mboga mboga na matunda. Je, ni lini Serikali itawajengea mabwawa, hasa wakulima wa Mavumbai, Mavongo, Kwaiboheloi, Ubili, Mbwei, Mlola, Kichangai na ngwelo ili na wao waweze kulima kilimo cha umwagiliaji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, katika Bunge hili tumeelekeza na tumeagiza, kwamba Wakurugenzi wote wa Halmashauri kila mwaka wahakikishe wanasanifu bwawa moja kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji na maji ya matumizi ya binadamu na mifugo.
Mheshimiwa Naibu Spika, niagize tena kila Halmashauri wahakikishe wanafanya hivyo, na wanaomba pesa Wizara ya Maji na Umwagiliaji tuweze kuwapa, ili tuhakikishe tunapata mabwawa ya kutosha kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge ninaomba sana, pengine sasa hivi Mkurugenzi hanisikii, lakini tukimaliza Bunge leo mpigie simu ahakikishe kwamba anafanya utafiti au tunawasiliana naye kuhakikisha kwamba, katika hili eneo basi tuhakikishe kwamba tunapata bwawa ambalo litahakikisha linapata maji, kwa ajili ya kuendeleza kilimo cha mboga mboga.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa Wilaya ya Lushoto ina majimbo matatu na Hospitali ya Wilaya ni moja. Je, ni lini sasa Serikali itapanua hospitali ile hasa wodi ya akinamama wajawazito?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikiri kwamba si chini ya wiki tatu au nne Mheshimiwa Shekilindi na Mheshimiwa Shangazi walikuja ofisini kwangu. Lengo la kuja ofisini kwangu ilikuwa ni ajenda ya barabara halikadhalika huduma ya afya katika maeneo yao. Licha ya ajenda ya kuhakikisha tunapanua hospitali ile lakini miongoni mwa ajenda walizokujanazo ni kuimarisha vile vituo vyao vya afya viweze kufanya kazi vizuri. Kwa hiyo, kama nilivyomuahidi Mheshimiwa Shekilindi alivyokuja ofisini, jukumu letu kubwa ni kubainisha na aliniambia nipite route tofauti nione jiografia ya eneo lake, nikija naomba anipitishe niione vizuri lakini tupange mikakati ya pamoja kuwasaidia wananchi wetu.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI, napenda kuongeza majibu kwenye swali la Mheshimiwa Shekilindi, Mbunge wa Lushoto kwamba katika sera ya afya sasa hivi tunataka kuondoka kwenye Hospitali ya Wilaya twende kwenye Hospitali za Halmashauri.
Kwa hiyo, nataka kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge wote ambao Wilaya zao zina Halmashauri zaidi ya mbili, tatu, sasa hivi kisera tunapendekeza kila Halmashauri iwe na hospitali yake badala ya kuwa na Hospitali ya Wilaya. Kwa kufanya hivi tunaamini tutaweza kutatua mlundikano wa wagonjwa katika hospitali mbalimbali za Wilaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tutatoa maelekezo rasmi ya kisera katika Halmashauri mbalimbali.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa Wilaya ya Lushoto ni Wilaya yenye vivutio vingi vya kitalii na vijana wa Lushoto wanafanya kazi ile kwa mazoea. Je, ni lini Serikali itafungua Chuo cha Kitalii ili kuwajengea uwezo vijana wa Lushoto ili wasifanye kazi ile kwa mazoea?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nawapongeza vijana wa Lushoto kwa moyo wao wa kujitokeza kupenda kufanya kazi katika eneo hili, kwa sababu kupitia kwao, tutaweza kufanya ajira kwa vijana ikawa imepata mchango mkubwa sana kupitia Sekta ya Utalii na kupitia kwao tunaweza kuchangia vizuri zaidi uchumi wa Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kufanya kazi kwa mazoea na mahitaji ya kupata mafunzo, kwanza nipate takwimu kwa sababu kwa sasa hivi Mheshimiwa Mbunge ametoa maombi ambayo ni ya jumla, nimtake sasa tuweze kushirikiana, nione kwamba kwenye eneo la Lushoto lile kuna vijana wangapi ambao wamejitokeza kupendelea kuingia katika fani hii. Kwa sababu ninachoamini ni kwamba vyuo tulivyonavyo bado havijaelemewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa taarifa zilizopo mpaka sasa hivi, vyuo tulivyonavyo bado vina uhitaji wa wanafunzi; lakini kama itajitokeza kwamba vyuo vinalemewa na kuna uhitaji wa kuongeza vyuo vingine, au kuboresha mazingira ya vyuo vilivyopo ili viweze kupokea wanafunzi zaidi, basi Serikali itaweza kuchukua hatua muafaka ili kila mmoja mwenye nia na kiu ya kujiunga kwenye mafunzo yatakayompelekea kuwa na taaluma muhimu ya kushiriki vizuri zaidi kwenye Sekta hii ya Utalii aweze kufanya hivyo bila mashaka yoyote.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, asante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne alipofika Lushoto alituahidi kilometa nne za barabara ya lami.
Je, Serikali ina mpango gani wa kutekeleza ahadi hiyo iliyotolewa na Rais Mstaafu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Spika, hicho kiwango cha kilometa nne ni ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne, na kama ambavyo nimekuwa nikisema kila wakati, dhamana tuliyopewa ni kuhakikisha tunatekeleza ahadi zote za viongozi wetu.
Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba kazi hii itafanyika katika kipindi hiki cha miaka mitano, kama ambavyo tumeongea huko nyuma na ninamsifu sana Mheshimiwa Shekilindi kwa kufuatilia, tutalitekeleza kama ambavyo nimekwambia huko nyuma.
Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kumjibu Mheshimiwa Shekilindi. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi, ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa Mradi wa REA Awamu ya Pili umeshapita baadhi ya maeneo tena ya barabarani katika Jimbo la Lushoto. Je, Serikali inaniahidi lini itapeleka umeme wa REA Awamu ya Tatu hasa katika Kata za Kilole, Kwekanga, Makanya, Ngwelo pamoja na maeneo mengine yaliyobaki?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kusema tu Mradi wa REA Awamu ya Tatu unapeleka umeme katika vijiji vyote, katika vitongoji vyote na katika taasisi zote za umma, lakini hata miji ambayo pia, iko isolated. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kijiji chake cha Kilole kitapelekewa umeme hata kijiji cha Makanya kitapelekewa umeme kwa sababu, ni mpango wa Serikali kupeleka umeme katika vijiji vyote kupitia REA Awamu ya Tatu.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa, upandaji wa miti ndiyo hasa unaoleta uoto wa asili; Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha wananchi wa Lushoto katika upandaji wa miti hasa maeneo ya msitu wa Magamba, Mazumbai ili kurudisha uoto wa asili uliotoweka?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepokea wazo lake na kwa kweli ni msisitizo kwa kile ambacho Serikali inakifanya, lakini na yeye sasa nimwombe arudi kule kwa wananchi aanze kuwashawishi kwa kuwaelewesha kwanza umuhimu wa misitu, lakini pia kuwafanya wajipange kwa ajili ya kupanda miti ili kuungana na jitihada za Serikali ambazo tayari zipo kwenye mipango.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, tulishatoa maelekezo kwa Wilaya na Mikoa yote kwamba kila Wilaya inalazimika kupanda miti 1,500,000. Kabla ya msimu wa kuanza kupanda kila Wilaya, sasa inawajibika kuhakikisha kwamba inaandaa mbegu, vitalu na kuhakikisha kwamba miche ya kupanda kila eneo inapatikana. Kwa sasa hivi sisi Wizara tunahakikisha tunawapelekea maelekezo ya kila eneo miti gani inayoota na inayoweza ku-survive bila matatizo. Kwa hiyo, kila Wilaya wanalo jukumu hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi ndani ya Wizara ya Maliasili pamoja na hii Ofisi ya Mazingira kwa maana ya Ofisi ya Makamu wa Rais, tutaendelea kusaidia pale inapobidi lakini ni mkakati wa kila Wilaya na Mkoa kuhakikisha kwamba kila Wilaya inapanda miti hiyo kwa mwaka inapofikia kipindi husika.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Jimbo la Lushoto limezungukwa na vyanzo vingi vya maji: Je, Serikali ina mpango gani ya kuwatua ndoo kichwani akinamama hasa wa Kilole, Kwekanga, Mbwei, Makanya, Ngulwi, Ubiri, Kwemakame na maeneo mengine yaliyobaki katika Jimbo la Lushoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, katika mpango wa maji kwa sasa hivi ambao Waziri wa Maji wakati wote huwa anaelezea hapa, lengo letu kubwa ni kumtua mama ndoo kichwani.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Shekilindi, kwamba, katika ratiba yangu kama tulivyoongea, tarehe 24 mwezi huu wa Novemba, nitakuwa katika Jimbo lake la Lushoto. Naomba tukiwa kule kule site tuweze kubadilishana mawazo. Hivyo vyanzo vilivyoko, lakini vile vile na wenzetu Wizara ya Maji ambao Mheshimiwa Waziri wa Maji yuko makini muda wote kuhakikisha kwamba wananchi wa Tanzania wanapata maji, tutaangalia na kushauri vizuri jinsi gani tutafanya kwa maeneo ya Wilaya ya Lushoto ili wananchi waweze kupata maji. Kwa hiyo, naomba tutumie vizuri ziara yetu ya tarehe 24 kuangalia vyanzo vilivyoko na mambo mengine kuwasaidia wananchi wa Lushoto.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri.
Kwa kuwa Jimbo la Lushoto lina kituo kimoja tu cha afya, ambacho kinahudumia takribani Kata saba; je, Serikali haioni sasa kuwa umefikia wakati wa kujenga vituo vya afya hasa katika Kata ya Makanya, Ngwelo, Kilole, Gare, Ubiri, Magamba, Malibwi pamoja na Kwai?
Swali la pili, kwa kuwa wananchi wa Lushoto wamejitolea kujenga zahanati katika vijiji vya Mzalagembei, Bombo, Mavului, Mbwei, Mazumbai, Ilente, Mbelei, Makanka na Kwemachai, lakini zahanati hizi zimebakia kukamilika tu.
Je, Serikali inatoa tamko gani sasa la kumalizia zahanati hizi pamoja na kupeleka watumishi ili wananchi wa Jimbo la Lushoto waondokane na usumbufu wa kutembea umbali mrefu hasa kwa mama zetu na dada zetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, kwanza katika kumbukumbu yangu Mheshimiwa Shekilindi amekuwa akiuliza maswali mengi sana ya sekta ya afya, ofisi yetu inakiri mchango mkubwa wa Mheshimiwa Shekilindi katika Jimbo lake na wananchi wake.
Mheshimiwa Spika, katika kulifanikisha suala hili, Serikali tumeelekeza mpango wetu wa sasa tunaondoka nao, jinsi gani tutafanya katika mwaka huu wa fedha, kuhakikisha kwamba tunajenga vituo vya afya. Mheshimiwa Shekilindi kwa sababu jana nilikujibu hapa kwamba nina mpango wa kuanzia katika Mkoa wako wa Tanga, tena ratiba nimeibadilisha nitaanza siku ya tarehe 21, na Mheshimiwa Shangazi, nitakuwa naye hiyo tarehe 21, tutaangalia jinsi gani tutafanya baada ya kuwa kule site, kutembelea hivyo vituo. Katika mpango wa bajeti inaokuja lengo kubwa ni kuimarisha vituo vya afya, katika ujenzi kwenye maeneo yetu, tumelenga kwamba angalau kila Halmashauri katika mwaka wa fedha tunaoondoka nao tujenge kituo kimoja cha afya.
Mheshimiwa Spika, hali kadhalika katika suala zima la maboma nimesema, tulifanya assessment katika Halmashauri zote, na hili ni agizo la Kamati ya Bajeti, maboma yote ambayo hayajakamilika, tumepata idadi ya maboma. Ndiyo maana nimesema katika bajeti ya mwaka huu unaokuja sasa, ninaomba Waheshimiwa Wabunge, tuungane pamoja kwamba jinsi gani tutafanya mpango mkakati wa kibajeti tuweze kumaliza maboma yale ambayo Mheshimiwa Shekilindi umeyazungumza katika maeneo yako, tukimaliza yale tutakuwa tumesogeza kwa ukaribu zaidi huduma za afya kwa wananchi wetu. Kwa hiyo, nakuunga mkono katika hilo na Serikali imesikiliza kilio chako.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa maji ni kilio cha muda mrefu sana hasa katika Jimbo la Lushoto na ukizingatia Jimbo la Lushoto lina mto mkubwa sana unaitwa Kibohelo, lakini unakuta Lushoto mto ule hautumiki unamwaga tu maji kuelekea bondeni Mombo bila kutumika maeneo yote.
Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuhakikisha maji yale yanaenda hasa katika vijiji vya Dochi, Ngulwi, Miegelo, Kwekanga pamoja na Gare?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Shekilindi anafahamu si muda mrefu sana nilitokea katika Jimbo lake na Jimbo la ndugu yangu Shangazi na kwa bahati nzuri hapa kuna mwalimu wangu hapa kutoka huko huko Lushoto amekuja hapa leo na hili naomba niwahakikishie ni kwamba ni commitment ya Serikali kuangalia jinsi gani tutatumia fursa zote zilizokuwepo kutatua tatizo la maji. Na katika Mpango wa Maji wa Awamu ya Pili, Waziri wa Maji amezungumza hapa mara kadhaa, lengo letu ni kwamba kutumia hizi fursa zilizokuwepo nikwambie ndugu yangu Shekilindi kwa sauti eneo lile nilivyofika kule Lushoto niwaagize wataalam wetu wa maji katika Halmashauri ile waanze michakato ya awali suala zima tufanyeje sasa matumizi halisi ya mto ule uweze kutumika vizuri kwa ajili ya wakazi wa Lushoto.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza na nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, nini commitment ya Serikali juu ya kuwapandisha madaraja watumishi hawa kwa wakati?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, katika bajeti ya mwaka huu, Serikali imetenga kiasi gani cha fedha ili kuondoa adha hii wanayoipata walimu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Spika, kimsingi ni kwamba kama ambavyo tumekuwa tukizungumza kila wakati ni kwamba madaraja ya watumishi husika ikiwemo walimu yatakuwa yanapandishwa mara baada ya zoezi la uhakiki ambalo pengine wengine hawapendi kulisikia lakini ni zoezi muhimu sana litakapokamilika. Kwa hiyo, nikuhakikishie tu kwamba mara zoezi hilo likishakamilika tutafanya hivyo.
Mheshimiwa Spika, lakini la pili kuhusiana na kiasi gani cha bajeti kimetengwa, naomba tusiiwahishe
shughuli, siku yetu ya bajeti mtapata majibu mazuri zaidi. Ahsante sana.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona. Kuna changamoto kubwa sana ya vijana wa Lushoto hasa wa bodaboda kupata leseni; Je, ni lini Serikali itaipandisha hadhi Wilaya ya Kipolisi Lushoto ili vijana wa Lushoto waweze kupata leseni bila kutumia gharama kubwa za kwenda hadi mkoani?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Naibu Spika, ili Wilaya iweze kupandishwa hadhi, iwe Kanda Maalum ama Mkoa wa Kipolisi kuna utaratibu ambao unatakiwa ufuatwe kabla ya kutoa maamuzi. Naomba nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Lushoto siyo katika maeneo ambayo mpaka sasa tumeweza kupata maombi rasmi ya mchakato wa kuongeza hadhi ya Kipolisi, ikiwa kuna vigezo vinakidhi basi Mheshimiwa Mbunge kwa kushirikiana na Viongozi wa Jeshi la Polisi katika eneo lake waanze mchakato huo ili tuweze kuchukua hatua stahiki kwa mujibu wa taratibu zilizopo.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona ili niweze kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Mamlaka ya Mji
wa Lushoto sasa hivi ina zaidi ya miaka nane. Je, Serikali haioni sasa imefikia wakati wa kuipandisha hadhi kuwa Halmashauri ya Mji wa Lushoto ukizingatia Mheshimiwa Jafo alitembelea kule na kuona Mji wetu wa Lushoto jinsi unavyopendeza na ulivyokuwa mkubwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani concern hii Mheshimiwa Mbunge aliileta ofisini kwetu na ndiyo maana Waziri wangu aliniagiza niweze kufika Lushoto kule na nimeweza kufika. Kimsingi wana mambo mengi, kuanzisha hii Mamlaka ya Mji wa Lushoto, suala zima la Halmashauri ya Mlalo, kuna mambo mengi sana yamejitokeza kule. Kwa hiyo, kama Serikali Waziri wangu alituma timu kule ikaenda kufanya assessment na taarifa zile ziko Ofisi ya TAMISEMI katika uchambuzi pale itakapoonekana kwamba vigezo vyote vimekidhi basi hakutakuwa na tatizo. Mheshimiwa Shekilindi naomba vuta subira tu wakati maamuzi yanaenda kufanyika kwa kuangalia kama imekidhi vigezo mbalimbali basi mtapata jibu halisi. Na mimi nimefika pale nimeona ile hali halisi basi tuache michakato iweze kuendelea baadaye tufanye maamuzi sahihi.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni muda mrefu sasa wananchi wa Wilaya ya Lushoto hawapati mawasiliano hasa ya redio ya Taifa na hili swali nimekuwa nikiliuliza mara kwa mara.
Je, ni lini Serikali itajenga mitambo hiyo ili wananchi wa Wilaya ya Lushoto waweze kupata taarifa kama ilivyokuwa kwa wananchi wengine waishio mjini?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu kumuomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira swali linalokuja linaongelea masuala ya usikivu wa redio katika nchi ya Tanzania.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa Waziri kunijibu majibu mazuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijauliza maswali mawili ya nyongeza, nitoe pole kwa wananchi wa Jimbo la Lushoto na Wilaya ya Lushoto kwa ujumla kwa mvua zinazoendelea kunyesha maana mpaka sasa hakuna mawasiliano kati ya Dar es Salaam - Lushoto, Arusha – Lushoto na Tanga - Lushoto. Nimeongea na Meneja wa TANROADS Mkoa akaniambia kwamba atashughulikia suala hilo. Hata hivyo, nikiangalia tatizo lile ni kubwa sana, madaraja yamekatika zaidi ya kilometa 32. Kwa hiyo, nipaze sauti Serikali ipeleke msaada maeneo yale haraka iwezekanavyo ili kunusuru maisha ya wananchi wa Lushoto na uchumi unaotegemea barabara ile. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kutoa pole hiyo kwa wananchi wangu wa Wilaya ya Lushoto na mkoa mzima kwa ujumla basi niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri amenijibu kwamba kwa kuwa Serikali itaanza ujenzi katika Wilaya ya Lushoto mara baada ya kukamilisha miradi ya Vyuo vya VETA vilivyoanza. Je, Serikali haioni kwamba itaendelea kulimbikiza vijana wengi wa Wilaya ya Lushoto bila kupata elimu ya VETA?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tayari kuna majengo ya kuanzisha Vyuo vya VETA je, Waziri yupo tayari kuongozana nami ili kwenda kuona majengo yale kama yanafaa na kutoa tamko la kuanzisha Chuo cha VETA? Hata kama VETA hiyo itaanzishwa chini ya mti, lakini naomba wananchi wangu hususani vijana wangu waweze kupata elimu hiyo ya VETA, hiyo ndio shida kubwa. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, si lengo la Serikali kudidimiza Jimbo la Lushoto na kimsingi Serikali imekuwa ikijitahidi kuhakikisha kuwa vyuo vilivyopo vinaweza kudahili wanafunzi wengi zaidi na ndiyo maana kwa sasa badala ya kusubiri tu kujenga chuo kipya, tunaona kuna haja pia ya kuongeza idadi ya mabweni katika vyuo vilivyopo ili kuchukua hata wanafunzi wa mbali. Kwa hiyo, lengo ni kuweza kujenga Chuo cha Lushoto muda muafaka utakapofika na fedha zitakavyopatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la kuongozana naye kwenda kuona majengo yaliyopo, kwa moyo mkunjufu kabisa niko tayari na endapo majengo haya yataweza kufaa aidha kwa kutumiwa kama VETA au Chuo cha Maendeleo ya Jamii tutafanya hivyo.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona ili niweze kuuliza swali moja la nyongeza. Kwa kuwa bomba hili la mafuta ghafi linaishia Bandari ya Tanga, je, Serikali imejipangaje kuona kuwa vijana wa Kitanzania hasa vijana wa Mkoa wa Tanga wanapata ajira hii katika soko la Kitanzania kupitia fursa hii ya uwekezaji?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimhakikishie Mheshimiwa Shekilindi, hili bomba la mafuta kutoka Hoima (Uganda) kuja Tanga (Tanzania) lina urefu mpana sana, lina jumla ya kilometa 1,443, lakini sehemu kubwa ya bomba hilo ambayo ni urefu wa kilometa 1,047 ni za hapa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, bomba hilo litapita karibu mikoa sita ya Kagera, Geita, Shinyanga, Dodoma hadi Tanga, kwa hiyo ni manufaa makubwa sana. Hivyo basi, ipo fursa kubwa sana kwa bomba hili kutoa ajira kubwa kwa Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Shekilindi na wananchi wa Tanga kwamba ajira na fursa nyingi sana za kazi zitapatikana. Sambamba na hayo, tunawasiliana kwa karibu sana na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji ili kutoa fursa nzuri sasa kwa Watanzania kuwekeza kwa kutumia fursa hiyo ya bomba la Hoima hadi Bandari ya Tanga.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, wakati Waziri anaendelea kufanya utafiti juu ya Grafo Gemu, je, Serikali ina mpango mkakati gani wa haraka wa kuweza kuwapatia baadhi ya vifaa ili wataalam wetu hao waendelee kuwasaidia watoto wetu pamoja na kwamba suala hili litakuwa ni suala la Kitaifa?
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tano ni ya hapa kazi tu; je, Mheshimiwa Waziri yupo tayari kuongozana na mimi wakati Bunge likiahirishwa ili akaone juhudi za wataalam hawa watokao SEKOMU wanaofanya kazi kubwa kuwasaidia watoto wetu hasa mama yangu mtaalam anaitwa mama Gorosho? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimezungumza kwamba Wizara ingependa kujiridhisha namna gani teknolojia hiyo inavyofanya kazi na namna gani inavyoweza kuwanufaisha wanafunzi wengi zaidi na wananchi kwa ujumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyo kawaida yetu sisi Waheshimiwa Mawaziri wengi tumekuwa tukiambiwa kutembelea maeneo na tunafanya hivyo. Kwa hiyo, nimwambie tu kwamba nitakuwa tayari kutembelea katika eneo la Mheshimiwa Mbunge ili kujiridhisha lakini vile vile kuona uwezekano wa kutoa vifaa ambavyo vitahitajika kama ambavyo ameomba. Namshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wake. (Makofi)
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Elimu ya ufundi ni muhimu ili kuwawezesha vijana wetu kuajiriwa au kujiajiri. Je, ni lini Serikali itajenga Chuo cha VETA Wilayani Lushoto?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye swali la msingi, Serikali kwa sasa ina mpango wa kujenga vyuo 43 katika Wilaya mbalimbali hapa nchini, tayari tumeanza taratibu katika wilaya saba.
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo letu ni kwamba Wilaya zote nchini katika wakati mmoja au mwingine zinakuwa na Vyuo vya VETA. Kwa hiyo, hata kwake Mheshimiwa Mbunge, Lushoto, kwa vyovyote vile ni sehemu ya Tanzania na ipo katika mipango hii. Naomba tu avute subira kama Waheshimiwa Wabunge wengine vilevile nitakapowaeleza, kwa sababu Serikali imedhamiria kwamba itaendelea kujenga vyuo hivi kadri ya fedha zitakavyopatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nimwombe Mheshimiwa Mbunge pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengine kwamba inakuwa ni rahisi zaidi Serikali kuingiza mikono yake au jitihada kama wananchi wenyewe wamehamasika. Kwa hiyo, pale tunapoona wananchi wenyewe wameanza kujichangisha na kuhamasika inakuwa ni rahisi hata Wizara kutumia fedha ambazo zinapatikana kusaidia.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Lushoto lina Kituo cha Afya kimoja tu, lakini kwa juhudi za wananchi wamejitahidi kujenga Vituo vya Afya viwili, ambapo kituo cha kwanza kipo Ngwelo, Kituo cha pili kipo Gare. Je, nini kauli ya Serikali juu ya kumalizia vituo vile vya afya ili wananchi waweze kupata huduma wasiende mbali kufuata huduma za afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake Mheshimiwa Shekilindi anasema tayari wameshajenga Vituo vya Afya viwili, lakini kwa bahati mbaya hajafafanua vimejengwa to what extent? Kama vimekamilika au la! Maana kama vimekamilika, kinachotakiwa ni kuhakikisha kwamba huduma inapatikana kwa kupeleka Waganga pamoja na Wauguzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba Vituo vya Afya vyote vinakamilika na viweze kutoa huduma ambayo tunakusudia na hasa upasuaji wa dharura kwa akina mama na watoto. Kwa hiyo, naamini baada ya kujua status ya hivyo Vituo vya Afya ambavyo vimejengwa kwake, Serikali iko tayari kuhakikisha kwamba inachangia ili huduma hiyo ambayo tumeikusudia, iweze kutolewa.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa barabara ya kuanzia Mombo - Soni – Lushoto ni nyembamba hata mvua zikinyesha magari hayapiti, kuna maporomoko ya mawe na magari ambayo yana mizigo mikubwa na upana mkubwa hayawezi kupita. Je, ni lini sasa Serikali itafanya upanuzi wa barabara ile?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa barabara ndiyo kichocheo cha uchumi wa nchi yetu, je, ni lini sasa barabara ya kuanzia Nyasa - Gale Magamba - Mlola itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu upanuzi wa barabara ya Mombo pamoja na ujenzi kwa kiwango cha lami kwa barabara ya Nyasa - Mlola, naomba Mheshimiwa Mbunge suala hili tukalitafakari ndani ya Wizara, tuwahusishe wataalam ili tuweze kuleta majibu ya kitaalam. Kwa sababu hiyo, namwomba Mheshimiwa Mbunge alilete swali lake rasmi kama swali la msingi ili liweze kushughulikiwa kikamilifu.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa Wilaya ya Lushoto ina misitu ya Shume Magamba na mingine midogo midogo na vijana walio wengi Lushoto hawana ajira, je, Serikali haioni sasaimefikia wakati wa kuwapatia vijana hao vibali ili na wao waweze kuwa na ajira?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi na kama nilivyojibu kwenye maswali ya nyongeza yaliyotangulia, ni kweli kwamba, kama Taifa sasa tunakwenda kuhakikisha kwamba tunapunguza kwa kiwango kikubwa na kwa kadri itakavyowezekana jinsi jitihada zinavyozidi kuendelea ni nia ya Serikali ikiwezekana kumaliza kabisa changamoto hii ya ajira nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, na nimesema kwamba Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia sekta zilizoko chini ya Wizara hii na sekta ya misitu ikiwa ni mojawapo tunaweza kutoa mchango mkubwa na ndio mwelekeo kwamba tunaenda kutoa mchango mkubwa wa kuweza kutoa ajira kwa ajili ya makundi mbalimbali nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kusubiri vibali kwa ajili ya kuvuna misitu ya Taifa haliwezi peke yake likawa ni suluhisho la ajira katika Taifa, isipokuwa kupitia vibali hivyo vidogo au vichache vikundi vinaweza vikapata mitaji. Lakini kutokana na vyanzo vingine vikundi hivyo baada ya kujiunga viweze kujenga uwezo wa kuwezesha kuweza kupata mikopo kutoka kwenye benki mbalimbali ili waweze kujiunga na kuweza kuanzisha mashamba yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na mashamba yao wenyewe wataweza kuwa na misitu ambayo itakuwa ni mikubwa, lakini pia wataweza kutokana na biashara ya misitu hata wakaanzisha viwanda vidogo vidogo vya mbao (saw mills). Kama nilivyosema kwenye majibu ya msingi na baada ya pale ajira itakuwa ni ya uhakika kwa ajili ya wao wenyewe kwenye vikundi lakini pia wanaweza kuajiri hata wengine ambao watakuwa wako jirani nao.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa
Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa niweze kuuliza swali dogo la nyongeza Wilaya ya Lushoto ina vyanzo vingi sana vya maji lakini wananchi wa Lushoto hawana maji safi na salama.
Je, Serikali ina mpango gani wa kumtua mama ndoo kichwani hasa akina mama wa Makanya, Kilole, Kwekanga, Kwemakame, Ngulwi, Ubiri, Handeni na Miegeo? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitembelea Lushoto nikakuta hilo tatizo na nikamuelekeza Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Tanga aweze kutekeleza miradi ya maji katika Halmashauri yake, hadi jana nimepiga simu tayari wamekamilisha taratibu za manunuzi, Baada ya siku 14 mikataba itasainiwa, utekelezaji uanze.
Mheshimiwa Mbunge nikuhakikishie kwamba maeneo yote ya Halmashauri yako yatapata maji.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi iliniweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza kabisa nimshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri na pia nishukuru kwa kutupatia bilioni 1.66.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mamlaka ya Maji katika Mji Mdogo wa Lushoto ilipatiwa fedha kwa ajili ya kujenga tenki la lita za ujazo 650,000 na banio katika eneo la Kindoi, lakini mpaka sasa mradi ule bado haujaanza. Nilifuatilia kwa Mkurugenzi wa Tanga UWASA alisema taratibu tushazikamilisha hivyo tunasubiri kibali kutoka Wizarani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wananchi wamesubiri mradi ule haujaanza kwa muda mrefu sasa, naamini wananchi wananisikia na kuniona. Je, ni lini Mheshimiwa Waziri kibali hicho kitapatikana ili Mkandarasi aanze kazi mara moja, kwani mradi ule ukikamilika utaendelea kuhudumia Kata za jirani ambayo ni Ngulu na Ubiri?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Wilaya ya Lushoto ina vyanzo vingi vya maji pamoja na mito inayotitririka maji kutoka milimani. Je, Serikali ipo tayari kwa sasa kuhakikisha inatumia vyanzo hivyo pamoja na maji yanayotiririka kutoka milimani kujenga mabwawa na kutumia vyanzo hivyo ili kuwapatia wananchi wa Lushoto maji safi na salama na hasa kutimiza dhana nzima ya kumtua mama ndoo kichwani; hasa kina mama wa Kwekanga, Kwemakame, Mkuzi, Mazashai, Mazumbai, Ngwelo, Miegeo, Handei, Masange, Kwemashai, Gare pamoja na Magamba Coast? (Makofi/Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Shekilindi kwa jinsi anavyofuatilia huduma ya maji katika Jimbo lake; na kwamba nishakwenda Lushoto, mazingira ya Lushoto ni mazuri, ni milima milima upo uwezekano mkubwa kabisa kuwapatia wananchi wa Lushoto maji safi na salama kwa zaidi ya asilimia mia moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza la Mbunge linahusu kibali, nitahakikisha kabla ya Bunge hili kukamilika kibali kitatolewa; kwa hiyo naomba sana tuwasiliane ili kibali kitolewe na utekelezaji wa mradi uendelee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili, ni kweli kuna vyanzo vingi vya maji Lushoto na tutahakikisha kwamba tunaweka mabanio ya kutosha kule milimani na kuweka mabomba kwa sababu maji ni ya mserereko hayana gharama kubwa na pale itakapobidi tutajenga hadi mabwawa ili maji yawe ya kutosheleza.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto ilihamisha walimu 210 kwa wakati mmoja, lakini mpaka sasa hivi walimu wale hawajalipwa stahili zao.
Je, ni lini walimu wale wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto watalipwa pesa zao za uhamisho?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza tulichukue hilo tujue kwa nini kwa sababu kuna fedha maalum tulizitoa kwa EPforR kwa ajili ya kuhakikisha walimu wanahamishwa katika maeneo mbalimbali na stahili zao zinapatikana. Kesi kama hiyo tumeshaanza kuishughulikia katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa ambako nadhani kuna maeneo mbalimbali imejitokeza kesi kama hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaangalia nature ya uamisho huo ulikuwaje na kwa nini watu walikuwa hawajalipwa, na kama walikuwa hawajalipwa ikiwa tayari Serikali ilishatoa pesa kwa EPforR tutaangalia nini tufanye.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Shekilindi naomba tulichukue hilo kama Serikali kwa concern ya eneo la Lushoto pamoja na maeneo mbalimbali ambayo yatakuwa na kesi kama hiyo. Tutaweza kuratibu vizuri jinsi gani ya kuondoa tatizo hili ambalo hatimaye kama nilivyosema awali tunataka walimu waweze kuhama kwenye maeneo ya kazi wakiwa wamefanya kazi kwa amani kama inavyokusudiwa. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa barabara kuu ya kuingia Wilayani Lushoto ni moja tu, na hizi mvua zinazoendelea kunyesha mawe na vifusi vinaziba barabara.
Je, Serikali haioni sasa imefikia wakati wa kutujengea barabara mbadala ya kutoka Dochi-Ngulwi hadi Mombo ambayo ni kilomita 16 tu ili kunusuru maisha na mali za wananchi wa Wilaya ya Lushoto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, swali ambalo nikiri kwamba ni mara ya pili kuniuliza, ingawa ni mara ya kwanza kuniuliza ndani ya Bunge. Naomba nikiri kwamba analifuatilia sana suala hili na niwapongeze sana wananchi wa Lushoto kwa kumpa dhamana hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nafasi hii niliyopewa ninamuelekeza Meneja wa TANROADS Mkoa wa Tanga, naye alete maoni yake kuhusu ombi hili, kama ambavyo nilimuelekeza awali ili hatimaye tulifanyie maamuzi na tuone namna ya kulitekeleza.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni muda mrefu sasa wananchi wa Wilaya ya Lushoto hawapati mawasiliano hasa ya redio ya Taifa na hili swali nimekuwa nikiliuliza mara kwa mara.
Je, ni lini Serikali itajenga mitambo hiyo ili wananchi wa Wilaya ya Lushoto waweze kupata taarifa kama ilivyokuwa kwa wananchi wengine waishio mjini?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu kumuomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira swali linalokuja linaongelea masuala ya usikivu wa redio katika nchi ya Tanzania.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa nia ya Serikali ni kupanda miti nchi nzima ili kurudisha uoto wa asili uliopotea na vikundi vya Wilaya ya Lushoto vimeanza kutosha miche ya miti, hasa Kikundi cha Friends of Usambara. Je, Serikali itasaidiaje vikundi hivi, hasa hiki cha Friends of Usambara, maana mpaka sasa kimeshaotesha miche zaidi ya milioni tatu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza Serikali inaunga mkono jitihada zote ambazo zinafanywa na mtu mmoja mmoja, lakini pia hata na vikundi. Hii ni taarifa njema ambayo Serikali inapokea kwa mikono miwili, uwepo wa vikundi katika eneo ambalo amelizungumzia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namshauri Mheshimiwa Mbunge kwamba awaelekeze wale wanakikundi waweze kuwasiliana na Wizara ili tuweze kuona namna gani Wizara inaweza kuwa-support.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwanza kabisa nimshukuru Naibu Waziri, Mheshimiwa Nditiye kwa kutuma wataalam wake kwenda kubaini maeneo ambayo hayana minara katika Jimbo la Lushoto. Je, ni lini sasa utekelezaji utaanza ili wananchi wa Lushoto waweze kupata mawasiliano?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyoeleza kwenye swali la msingi na kama nilivyoeleza kwenye maswali mengine ya nyongeza, Mheshimiwa Shekilindi kuanzia mwezi wa Saba baada ya Bunge la Bajeti nitafanya ziara ndefu sana ya kutembelea maeneo yote yenye changamoto za mawasiliano nikiambatana na timu ya Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina hakika nitafika jimboni kwake na pia nitafika kwa Mheshimiwa Nape naye ambaye najua kabisa anasumbuka sana kuhakikisha tu kwamba mawasiliano kwa nchi yetu yote yanapatikana bila tatizo.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri. Naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa Chuo cha VETA kiko mbali sana na Wilaya ya Lushoto na hii imesababisha vijana wengi wa Lushoto kukosa fursa ya kujiajiri na kuajiriwa, je, Serikali haioni kwamba imefikia wakati sasa kuchukua hatua za haraka ili kuwajengea chuo hicho vijana wa Lushoto waweze kupata elimu hiyo ya ufundi? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali pili, kwa kuwa kuna majengo ya TBA na majengo yale yana karakana ya Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto. Je, Serikali haioni sasa kuwa kuna haja ya kurudisha majengo hayo katika Wizara ya Elimu kwa nia ya kufungua Chuo cha VETA katika majengo hayo ili vijana wa Lushoto waliokosa elimu hiyo ya ufundi kwa muda mrefu waweze kuipata sasa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shaabani Omari Shekilindi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kuhusu ni lini Serikali itajenga Chuo cha Ufundi Stadi Lushoto, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kama nilivyoeleza kwenye jibu la msingi, Serikali itaendelea kujenga Vyuo vya Ufundi Stadi katika wilaya na mikoa yote kadri fedha zitakavyopatikana. Kwa hiyo, kwa sasa nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba fedha zikipatikana Serikali itajenga Chuo cha Ufundi Lushoto kama itakavyofanya katika maeneo mengine.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusu majengo ya TBA kama ni wakati sasa wa kurudishwa Wizara ya Elimu ili yaweze kutumiwa kama Chuo cha VETA, naomba nimshauri Mheshimiwa Mbunge kwamba hili linawezekana lakini wao waanzishe mchakato katika ngazi yao ya halmashauri, wawasiliane na TBA. Wakishapata yale majengo kwa maana ya wakiruhusiwa, sisi Wizara ya Elimu tuko tayari kuja kuyakagua na kuangalia kama yanafaa kuwa VETA na hatimaye tukiona yanafaa hatuna kipingamizi, tutahakikisha kwamba majengo yale yanageuzwa kuwa VETA.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wakulima wa mbogamboga wa Wilaya ya Lushoto wanachimba vidimbwi vidogovidogo kwa ajili tu ya kunyeshea mazao yao. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha kwa kuwajengea mifereji hasa wakulima wa mabondeni hasa Mabonde ya Boheloi, Mshizii, Kwai, Milungui, Ubiri, Kwekanga, Mazumbai, Mlola, Mboi hadi Makanya?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, kaka yangu, Mheshimiwa Shekilindi (Bosnia), kwa kazi nzuri anazozifanya katika Jimbo lake la Lushoto. Kubwa ambacho nataka nimwambie ni kwamba nchi yetu sasa hivi tunakwenda katika uchumi wa kati, tumeona haja sasa ya kulima kilimo cha umwagiliaji. Nimhakikishie kwamba sisi Wizara yetu ya Maji tumetenga shilingi bilioni 29.767 katika kuhakikisha tunawekeza katika kilimo cha umwagiliaji. Niwaombe tu wataalam wetu wa Lushoto wasilale, wamsaidie Mheshimiwa Mbunge katika kuhakikisha jambo lake linatimilika kwa wakati.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu pia niendelee kumpongeza Waziri Kalemani na Naibu pamoja na timu yake kwa kutuma wataalam kuja ku-survey katika Kata za Kwekanga, Mbwei, Migambo, Nguli, Lushoto, Magamba na Mlola.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, je, pamoja na ku-survey kata zote hizo pamoja na alilozitaja, ni lini sasa wananchi wangu watakuja kupimiwa hawa ili waweze kupata umeme kwani umeme ni huduma ambayo walikuwa wanaisubiri kwa muda mrefu sasa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, mkandarasi aliyepewa kazi ya kujenga umeme katika Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto tokea mwaka jana mpaka leo hii amejenga kitongoji kimoja tu ambacho ni cha Magamba Mabughai. Hii inaonyesha uchelewaji mkubwa sana, je, Serikali haioni sasa kuwa kuna haja ya kubadilisha mkandarasi huyu kuweka mkandarasi mwingine ambaye anaendana na kasi ya hapa kazi tu?
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Shekilindi anavyofuatilia masuala ya umeme katika Jimbo lake la Lushoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tunakubali kupokea pongezi kwa kazi nzuri zinazofanywa na sehemu nyingine ya mkandarasi lakini zipo changamoto kweli kwa mkandarasi na nimeongea na Mheshimiwa Mbunge. Kwanza nilikuwa nimempa vijiji vinne tu kati ya vijiji kumi na mbili, nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge kwa niaba ya wananchi wa Lushoto tumemuongezea vijiji vingine vinane vipya ambavyo vimeshafanyiwa survey na mkandarasi anaanza kuvifanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu lini vitapelekewa umeme, tunapoongea hapa mkandarasi ameshaweka magenge mawili, anaendelea na usambazaji wa nguzo pamoja na kufunga nyaya katika Kijiji cha Magamba pamoja na Mabughai. Kwa hiyo, ni matarajio yetu kwamba ndani ya mwezi huu wataviwasha vijiji hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la pilli la uwezo wa mkandarasi, ni kweli mkandarasi huyu alianza kwa kususasua lakini tumeshakaa naye na ameshaweka magenge kumi na mawili kwenye Jimbo la Mheshimiwa Mbunge ni matarajio yetu mbali ya kumbadilisha tutamsimamia, tutamshinikiza, tutahakikisha kwamba anafanya kazi na anakamilisha ndani ya wakati.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri. Pia nashukuru kwa kuona hilo kwamba kweli Hospitali ya Wilaya ya Lushoto ina msongamano mkubwa sana.
Je, Serikali haioni sasa kuwa ipo haja ya kumalizia vituo vya afya vilivyoanza kujengwa kwa nguvu za wananchi ambavyo ni Ngwelo, Makanya ambayo ni zahanati inayotakiwa ipandishwe hadhi iwe kituo cha afya, pamoja na Gare ili kupunguza msongamano uliopo katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa x-ray machine iliyopo katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto haina uwezo mkubwa wa kuhudumia watu wengi na hivyo kuzidiwa na kuharibika mara kwa mara na wagonjwa kukosa huduma hiyo muhimu; je, ni lini Serikali itapeleka x-ray machine ya kidijitali katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto na kupunguza usumbufu uliosababishwa na ubovu wa mashine hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Shekilindi katika swali lake la kwanza kuhusu kumalizia maboma kwenye vituo vya afya vitatu kikiwemo kimoja ambacho wanataka kukipandisha hadhi; nimwambie tu kwamba Serikali inaunga mkono. Mimi naomba sana katika fedha za ruzuku ambazo tutazipeleka hivi karibuni, Halmashauri iweke kipaumbele kikubwa kwenye hivyo vituo ambavyo Mheshimiwa Mbunge amevitaja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu x-ray, naomba tuendelee na mawasiliano, mwaka wa fedha mpya unaoanza ili angalau ifikapo mwezi wa kumi tuwe tumeshafanya maendeleo mazuri kwenye upande wa x-ray.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nimsahihishe Naibu Waziri, amesema Msitu wa Mkussu; siyo Mkusu ni Mkuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa misitu ya Wilaya ya Lushoto iliyoungua tokea mwaka 2004 ni takribani miaka 14 sasa, lakini mpaka sasa hivi miti ile ya asili haijaota, imebaki vichaka tu. Je, nini commitiment ya Serikali juu ya kurudisha haraka uoto wa asili uliopotea kwa kupanda miti katika maeneo ya misitu iliyoungua pamoja na sehemu za maporoko? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Wilaya ya Lushoto ina vijana wengi wamejiunga kwenye vikundi, je, Serikali ipo tayari kuwapa miche ya miti ya asili bure ili kurudisha haraka uoto wa asili uliopotea kwa muda mrefu sasa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shabaani Shekilindi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nachukue nafasi hii kumpongeza sana kwa jinsi ambavyo amekuwa akifuatilia sekta ya misitu na kwa jinsi ambavyo amekuwa akitoa ushauri kwa namna mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, eneo lolote lile ambalo ni misitu ya asili, ukienda kuanza kupanda miti mingine utaharibu ule uoto wa asili. Tunachofanya sisi ni kuliacha lile eneo kama lilivyo. Tukishaliacha kama lilivyo, ikifika kipindi ile miti itaota yenyewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kabisa kwamba katika lile eneo ambalo Mheshimiwa Mbunge anasema imechukua muda mrefu haijaota, lakini hivi sasa Wakala wa Taifa wa Misitu Tanzania wanafanya utafiti ili wapate mbegu na miche bora ile ya asili iliyokuwepo katika lile eneo ili tuone kama tunaweza tukaipanda katika eneo lile kusudi kurudisha ule uoto wa asili.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusu miche hii ya asili ambayo inaweza ikapandwa katika eneo hili na wale vijana waweze kupata ajira, kama nilivyosema Wakala wa Taifa wa Misitu anafanya utafiti. Tukishakamilisha, tukabaini mbegu au miche mizuri ya asili katika eneo lile, basi tutaenda kuhakikisha kwamba inapandwa katika lile eneo na wale vijana watapata ajira.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa, Wilaya ya Lushoto ina milima inayotiririsha maji hasa kipindi cha mvua. Je, Serikali haioni sasa ipo haja ya kujenga mabwawa hasa katika maeneo ya Kwekanga, Mbwei, Kwai, Makanya, Bweloi, pamoja na Bonde la Ubiri kwa ajili ya wakulima wa Wilaya ya Lushoto kulima kilimo cha umwagiliaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge Shekilindi kwa kazi nzuri anayoifanya, lakini nikubaliane na yeye ipo haja ya Serikali kuwekeza katika kilimo cha umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha tunafikia azma ya viwanda lazima tuwekeze katika kilimo cha umwagiliaji. Wizara yetu Mheshimiwa Waziri ameona haja sasa ya kupitia mpango kabambe wa mwaka 2002 wa Tume ya Umwagiliaji katika kuhakikisha tunauboresha umwagiliaji ili uweze kuwa na tija na manufaa kwa nchi yetu. Nimhakikishie katika uboreshaji huo watu wa Lushoto hatutawaacha katika kuhakikisha wanawakeza katika kilimo cha umwagiliaji.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Vitongoji vingi katika Jimbo la Lushoto havijafikiwa na Mpango wa TASAF wa kunusuru kaya maskini nchini. Je, ni lini TASAF itavifikia vitongoji hivyo katika Mpango wake wa Kunusuru Kaya Maskini nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS (MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kujibu swali moja dogo la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi, Mbunge wa Jimbo la Lushoto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwamba Awamu ya Pili ya Mpango na Mradi huu wa TASAF tunaanza kuutekeleza Juni, 2019. Nimezungumza hapa kwamba tulikuwa tumebakiza asilimia 30 ya kuhudumia zile kaya maskini sana. Pia nimesema tumeboresha madodoso na tutayafanya kielektroniki na tutahakiki ili kupunguza zile kaya hewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimwambie Mheshimiwa Shekilindi kwamba zile asilimia 30 ambazo nimezisema hapa kwamba zimebaki basi na Jimbo la Lushoto litakuwa mojawapo pamoja na majimbo yote na Watanzania wote ambao wanaishi katika kaya maskini wote tutawafikia. Halmashauri zile 185, vijiji, shehia na mitaa zaidi ya 15,000 vyote tutavifikia. Ahsante.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nimshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Sasa naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, ni ukweli usiopingika kuwa bodaboda zimetoa ajira nyingi sana hapa nchini. Je, Serikali haioni sasa kuwa kuna haja kubwa ya kuwawezesha vijana hawa mikopo kwa wakati kuliko ilivyokuwa sasa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa vijana wengi wamejiunga na vikundi na hawajawahi kupata mikopo, je, Mheshimiwa Naibu Waziri, yupo tayari kuongozana na mimi kwenda kuona vikundi vile vya vijana na kuwapatia mikopo ambayo hawajawahi kuiona wala kuisikia, hasa kwa vijana wa Wilaya ya Lushoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shaabani Omari Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na swali la kwanza la uwezeshaji kwa wakati kwa vikundi hivi vya bodaboda. Kama nilivyojibu katika jibu la msingi ni kwamba Serikali inachokifanya hivi sasa ni kushirikiana na Mamlaka za Halmashauri, Manispaa, Wilaya na Majiji ili kuona namna bora ya kusaidia uundwaji wa vikundi hivi kwa sababu ni ngumu sana kumwezesha bodaboda mmoja mmoja pasipo kukaa katika vikundi. Ndiyo maana sasa hivi kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Ndani tumeendelea kufanya maandalizi kuhakikisha kwamba vyama hivi vya bodaboda katika mikoa na katika ngazi ya Taifa vinasajiliwa ili tupate namna bora ya kuweza kuwahudumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mikopo linategemea utayari wa wahusika kwa maana ya kuunda vikundi na kuunda katiba ili wawe tayari kwa ajili ya kukopeshwa. Nitoe rai kwa vikundi vyote vya bodaboda nchini ambavyo viko rasmi watumie fursa ya mikopo inayotolewa na Serikali na taasisi mbalimbali za fedha, hasa ukiwemo Mfuko wa Uwezeshaji Vijana Kiuchumi ambao umelenga katika kuwapatia maendeleo vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, ni kuhusu vijana wa Kilindi. Nitoe tu rai kwanza kwa Waheshimiwa Wabunge wote, wale ambao wana vikundi vya vijana na wangependa kunufaika na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana, sharti moja kubwa ambalo lipo ni uanzishwaji wa SACCOS ya vijana katika halmashauri husika. Hivyo, nipo tayari kwenda Kilindi pamoja na Mheshimiwa Omari Shekilindi kwenda kuangalia vikundi vya vijana. Vilevile kama watakuwa wamekidhi mahitaji ya uwezeshaji wa Mfuko wa Vijana basi tupo tayari kuwawezesha vijana wa Kilindi ili nao waweze kunufaika na fursa zilizopo katika nchi yao.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niipongeze Serikali, nimpongeze Rais wangu Mungu azidi kumjaza hekima na maisha marefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, pamoja kwamba tumepata fedha zote hizo kama nilivyosema nashukuru lakini bado sekondari nyingi katika Jimbo la Lushoto hazina hosteli na hii imepelekea watoto wengi kufeli na watoto wengi wa kike kupata ujauzito. Je, Serikali ina mkakati gani sasa tena wa haraka kuhakikisha kwamba wanajenga hosteli katika sekondari ambazo hazina hosteli?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wananchi wa Jimbo la Lushoto kwa nguvu zao wamejenga majengo ya maabara tena yote matatu lakini mpaka sasa majengo yale hayajamalizika. Je, Serikali haioni kuwa kuna umuhimu sasa wa kumalizia maboma yale ili watoto wetu waweze kusoma elimu kwa vitendo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimjibu Mheshimiwa Shekilindi maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nampongeza Mheshimiwa Mbunge nimefika kwenye Jimbo lake la Lushoto, wananchi wa eneo lile na yeye mwenyewe wamefanya kazi kubwa kuongeza miundombinu ya elimu lakini pia afya na maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza anaomba kujua mpango wa Serikali kuongeza hosteli. Katika bajeti ambayo inaendelea kujadiliwa sasa kila mtu akipitia kwenye kitabu cha bajeti cha Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, utaona kuna maeneo mbalimbali fedha zimetengwa kwa kazi hiyo lakini iko miradi mingine ya elimu itakayoimarisha hosteli mbalimbali. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge avumilie mwaka huu wa fedha tumetenga fedha na kadri zitakavyopatikana tutaweza kumaliza hiyo shida kwa watoto wa kike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ni kuhusu maboma ya maabara, tumeanza kupeleka vifaa na kukamilisha maboma katika shule nyingi kadri itakavyowezekana. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge tuwasiliane huenda shule au maeneo yake anayotaja tutapeleka vifaa vya maabara lakini pia tutamalizia maboma ya maabara hizo. Lengo ni ili tupate wataalamu wa sayansi ili tutakapoanza issue ya viwanda tuwe na wataalam wa kutosha.
MHE. SHAABAN O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Wilaya ya Lushoto ni wilaya kongwe na bahati nzuri Waziri Mheshimiwa Ndalichako alitembelea Wilayani ya Lushoto na akaona hali halisi ilivyo. Je, ni lini Mheshimiwa Waziri utatuma wataalam wake kwenda kuona majengo yale ya Halmashauri, ili ikimpendeza tuweze kuanza sasa kukarabati majengo yale na watoto wetu waanze kusoma masomo ya VETA?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba, leo hii tukitoka mimi na yeye tutapanga ni lini tutawapeleka hao watendaji kule.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Waziri yenye kutia moyo lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa Serikali ina mpango wa kukarabati Vituo vya Afya na Hospitali za Wilaya na kutoa vifaatiba. Je, ni lini sasa itatoa X-ray mashine katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto ili kupunguza msongamano au usumbufu wa wananchi wangu kutoka Lushoto kwenda mpaka Tanga hadi Muhimbili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Jimbo la Lushoto lina Kata 15 na Kituo cha Afya kimoja tu. Wananchi wa Kata za Gare na Ngwelo kwa nguvu zao wenyewe wameanza kujenga maboma hayo ya Vituo vya Afya. Je Serikali ina mpango gani wa kuongeza fedha au wa kuwapatia fedha zile ambazo zinatolewa shilingi milioni 400 kwa ajili ya kujenga vituo hivyo? Nia na madhumuni ni kupunguza msongamano mkubwa uliopo katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shekilindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la kwanza juu ya uwepo wa X-ray, naomba nimtoa wasiwasi Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Lushoto kwamba mchakato uko kwenye hatua za mwisho kupitia MSD. Muda si mrefu X-ray ile itapatikana ili wananchi wa Lushoto na maeneo ya jirani waweze kupata huduma ya vipimo hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika swali lake la pili, naomba nimpongeze yeye mwenyewe na Mheshimiwa Shangazi wamekuwa wakifuatilia sana kuhusiana na Hospitali ya Lushoto. Naomba pia niwapongeze wananchi ambao wameanza ujenzi wa Kituo cha Afya. Hakika pale ambapo wananchi wanaanza Serikali inawaunga mkono mara moja. Naomba nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwa kadri bajeti itakavyoruhusu na fedha ikipatikana tunahakikisha tunapeleka maeneo ambayo tayari nguvu ya wananchi ilishakuwepo. Mchakato utakavyokamilika hakika hatutawasahau wananchi wa eneo alilolitaja.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Hata hivyo, kabla ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza, naomba nitumie nafasi hii kuwapa pole wananchi wa Wilaya ya Lushoto kwa mvua zinazoendelea kunyesha takriban sasa ni miezi minne bila kujua zitaisha lini. Niwatoe hofu kwamba taarifa za mvua zimefika sehemu husika, ni imani yangu kubwa sasa kwamba baada ya mvua kupungua miundombinu ile itarejeshwa na wananchi watapata huduma kama ilivyokuwa awali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naomba niulize maswali mwili ya nyongeza. Kwanza nimpongeze kwa majibu mazuri Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kusema kuwa ametupatia fedha za maabara, ni kweli. Hata hivyo, kuna shule nyingi sana katika Wilaya ya Lushoto zaidi ya 50 lakini zenye maabara hazifiki sita. Kwa nini sasa Serikali isitumie mfumo kama ule wa mwaka jana wa kutoa fedha za kukarabati maboma ya madarasa ili kukarabati maabara kuepusha usumbufu kwa wanafunzi wetu hasa wasichana ambapo tutaepusha mimba za utotoni?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Jimbo la Lushoto lina sekondari nyingi sana zaidi ya 28 lakini zenye hosteli naamini hata tatu hazifiki. Je, kwa nini sasa Serikali isitupe hata fedha kwa mwaka huu ili kukarabati maboma ya hosteli ambayo yameshajengwa kwa nguvu za wananchi mfano Mlongwema…

SPIKA: Mheshimiwa Shekilindi nafikiri umeeleweka, majibu ya maswali hayo Mheshimiwa Naibu Waziri.
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFlSI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza umeona Mheshimiwa Mbunge amehemewa, mimi nimeenda Lushoto pamoja na kwa Mheshimiwa Shangazi ni kweli wana shule nyingi na wanajenga kwa nguvu za wananchi. Nawapongeza sana Mheshimiwa Shekilindi na Mheshimiwa Shangazi kwa kazi nzuri ambayo wanafanya katika kupeleka elimu katika maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nimetembelea baadhi ya maboma ya maabara ambayo kwa kweli hayajakamilika. Maombi ya Mheshimiwa Mbunge tumeyapokea, Serikali ina mkakati wa kuhakikisha kwamba tunapata maabara katika kila shule ya sekondari kwa sababu ni lazima tuwe na masomo ya sayansi ambayo yanafundishwa kwa vitendo na siyo nadharia.

Mheshimiwa Spika, kwa bajeti ya mwaka huu na bajeti ambayo tunaendelea nayo, nimhakikishie kwamba katika maombi ambayo ameshayaleta pale ofisini tutayafanyia kazi, hawezi kukosa baadhi ya maabara ambazo zitakamilika. Hatujengi maabara tu, tunajenga maabara lakini pia kupeleka vifaa ili wanafunzi waweze kufanya mazoezi kwa vitendo.

Mheshimiwa Spika, napenda kumjulisha Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wengine wote mwaka huu ambao tunaendelea nao tumetenga fedha kwa ajili ya kukamilisha maabara na majengo mbalimbali lakini na mwaka huu ambao tunaanza mchakato wa bajeti tutatenga fedha. Nitoe wito kwa Waheshimiwa Wabunge Halmashauri huko wanaendelea kutengeneza bajeti ni muhimu kwenye bajeti hii ambayo tunaenda nayo 2020/2021 tutenge fedha kuanzia vyanzo vya Halmashauri na sisi Serikali Kuu tutatafuta fedha tuwekeze pale ili tuweze kuboresha maabara, majengo ya hosteli, kumbi za mikutano na nyumba za walimu. Ahsante sana.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza, barabara hii ya Mlalo, Ngwelo, Mlola, Makanya, Milingano mpaka Mashewa ambazo ni kilomita 53. 7 inapita kwenye halmashauri tatu na majibo manne. Na barabara ya kutoka dochi Ngulu hadi Mombo ambayo yenye kilometa 16.3 inapita kwenye halmashauri mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na isitoshe tumeandika barua ya kupandisha hadhi barabara hizi kabla ya kuanzishwa kwa TARURA lakini mpaka sasa hakuna kinachoendelea zaidi ya wananchi kuendelea tabu ya usafiri pamoja na mazao yao. Je, Serikali ina mkakati gani wa haraka barabara hizi ziweze kushughulikiwa kwa haraka ili tukiendelea kusubiri upandishwaji wa hadhi wa barabara hizi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kwakuwa mheshimiwa Waziri wewe mwenyewe ni shahidi kwa kuona barabara hii ya dochi Nguli Mombo na kuongea na wananchi wa kijiji cha Nguli na ukawahidi kwamba changamoto hii utaimaliza. Je, upo tayari sasa kutuma wataalam wako kwenda kuona hali halisi ya barabara hiyo ili kuondoa kadhia wanayoendelea kuipata wananchi wa Nguli?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hizi anazotaja Mheshimiwa Mbunge ni kweli kwamba inapita katika maeneo mengi kwa maana jimbo lake la Lushoto, Jimbo la Mlalo, Jimbo la Bumbuli, na Korogwe vijijini na eneo hili ni muhimu sana kwa sababu inapitisha watali wengi kwenda kwenye hifadhi yetu ya Mkomazi lakini pia kuna uzalishaji mkubwa wa mazao na nilitembelea eneo hili nilishuhudia changamoto ambazo ziko kwenye barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa kujibu swali lake niseme tu mkakati wa kwanza mkubwa ni uanzishwaji wa TARURA na TARURA wamefanya kazi kubwa wa kuzitambua barabara zote nchini kwa lengo la kuhakikisha kwamba barabara zinapata bajeti au zinapata fedha kulingana na changamoto na hali ya barabara ilivyo kwa hiyo hii zoezi ilikuwa inafanyika na kazi ya TARURA ilipokamilika imepelekwa taarifa zimepelekwa kamati maalum ambayo inashirikisha wenzetu wa TAMISEMI wenzetu wa Wizara inayoshughulikia mambo ya utalii wenzetu wa Wizara ya ardhi kwa hiyo kamati muhimu hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu Mheshimiwa Mbunge anahitaji wataalam waende nimuelekeze tu Meneja wa TANROAD wa Mkoa wa Tanga na coordinator wa TARURA wa Mkoa wa Tanga watembelee barabara hizi mbili muhimu ili waweze kushauri kamati maalum tuone namna gani ya kuzifanyia matengenezo makubwa barabara hizi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge naomba uvute subira nitafuatilia kuona wataalam wanatembelea eneo lako ili kuweza kuwezi hizi juhudi ambazo unazifanya Mheshimiwa Mbunge kuhakikisha kwamba wananchi wako wanapata huduma nzuri ya barabara katika maeneo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitaifuatilia na niwaombe hao kwa sababu ni wajumbe wa bodi ya barabara kwenye mkoa mapendekezo yatakayokuwa nayo pia wayazungumze katika bodi ya mkoa ili tuweze kuzitendea haki barabara hizi.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Barabara ya kuanzia Mombo – Soni - Lushoto ni nyembamba mno hata kuhatarisha maisha ya watu pamoja na mali zao. Je, ni lini upanuzi wa barabara ya Soni – Mombo - Lushoto utaanza ili kuondoa kadhia wanayoendelea kuipata wananchi wa Lushoto?
WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Mbunge kuhusiana na barabara ya Mombo – Lushoto, kwamba ni nyembamba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli barabara ile ni nyembamba lakini imepita katika milima mirefu na udongo ule uko sensitive sana kwenye erosion. Kwa hiyo, tulijenga katika hali ile lakini baadaye tuta-redesign na kuipanua huku tukiwa waangalifu kwa sababu ni lazima ukate milima. Sasa utakapokata milima maana yake unaifanya tena ielekee kwenye mwelekeo ikinyesha mvua nyingi iweze kubomoka. Mwaka jana Mheshimiwa Mbunge ni shahidi, udongo uli-slide ukaifunika barabara moja kwa moja.

Kwa hiyo, ile barabara lazima ijengwe kwa uangalifu sana kwa sababu udongo wake mvua ikinyesha mara nyingi unaporomoka.
MHE. SHABAN O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Barabara ya kuanzia Dochi- Nguli – Mombo ambayo ni kilometa 16 mara nyingi nishauliza swali hili lakini sipati majibu na sasa hivi hali ya barabara ile sio nzuri. Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kuhakikisha kwamba barabara ile inatoboka ili wananchi wangu waweze kupata huduma ya haraka?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mvua zilizonyesha hivi karibuni ziliathiri karibu maeneo yote ya Mkoa wa Tanga na sisi kama Serikali tumejipanga kurejesha maeneo hayo yaliyoharibiwa ikiwemo maeneo ya Dochi kwenda Mombo na eneo la kule Mchinga na maeneo mengine ya kule Pangani tumejipanga vizuri, wenzetu wa TANROADS wako kazini, Mheshimiwa Kilindi aondoe hofu tunafanya marejesho makubwa na kazi zinaendelea.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kama inavyofahamika, kituo cha Polisi katika Wilaya ya Lushoto ni cha tangia Mkoloni, lakini
nashukuru Serikali imetutengea fedha tumejenga kituo cha Polisi lakini kituo kile mpaka sasa hivi takribani miaka mitano sasa kiko kwenye mtambao wa panya. Je, ni lini Serikali itapeleka fedha kumalizia kituo kile?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi, Mbunge wa Lushoto kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa lugha ambayo ameitumia kidogo imenipa utata kuielewa…

SPIKA: Iko kwenye leta.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Ameseama mtambaa wa panya…

SPIKA: Iko kwenye lenta, pale, wanaita mtambaa wa panya.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, sawa sawa. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge, kama ambavyo amependekeza, tutakweda mimi na yeye kuangalia nini cha kufanya ili sasa tuvuke hapo mtandaa panya kuelekea kwenye kukimaliza kitu hicho.
MHE. SHAABAN O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona, kutofaulu kwa wanafunzi hasa wa masomo ya sayansi kuna changiwa sana na kutomalizika kwa maabara, Je, ni lini Serikali itapeleka fedha za kutosha katika maabara hizi ili ziweze kumalizika hasa katika Jimbo la Lushoto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Mbunge, na anajua nimetembelea kwenye Jimbo lake, na anafanya kazi kubwa sana kuwasemea wananchi wake, na wananchi wa Lushoto wamejenga Shule nyingi ikiwepo shule ya high school, na nilienda akaniambia kuna upungufu wa Walimu, na namuahidi kwamba tulipomaliza kugawa mgao wa Walimu hawa wa Sekondari naye amepata mgao, na hili tumelipokea, vifaa ambavyo tumeelekeza, kama ile Shule ambayo nilitembelea ilikuwa na changamoto kubwa ya watoto wa kike wengi hawajapata vifaa ambavyo vya kuwasaidia ili waweze kusoma masomo ya sayansi. Ahsante.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Barabara ya kuanzia Mlalo – Ngwelo – Mlola – Makanya – Milingano hadi Mashewa iliombewa kupandishwa hadhi toka mwaka 2009 sambamba na barabara ya Dochi hadi Mombo.

Je, ni lini barabara hizi zote mbili zitapandishwa hadhi ili wananchi wangu waweze kuondokana na adha wanayoendelea kuipata sasa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ninapenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi al-maarufu kama Bosnia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara alizotaja Mheshimwa Mbunge yaani kwa maana ya ile barabara ya kutoka Mlalo kwenda Makanya na hii barabara ya Dochi, kama nilivyozungumza kwamba kamati maalum inaendelea na kikao kufanya mapitio ya kuweza kurekebisha na kuweka hadhi za barabara zetu zote nchini. Kwa hiyo, Mheshimiwa Shekilindi naomba avute subira, baada ya zoezi hili tutamfahamisha kwamba barabara zake hizi zime-meet vigezo ili tuone kama zinaweza kupandishwa hadhi, lakini lazima shughuli za kitaalum zifanyike kabla ya hatua ya kupandisha hadhi barabara hii, kwa hiyo, vuta subira muda siyo mrefu utapata majibu yake.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimshukuru Waziri kwa majibu yake mazuri. Kwa kuwa mradi wa REA utaanza Februari hii ambapo leo ni tarehe 3 na katika Jimbo la Lushoto kuna vijiji vimerukwa kwa muda mrefu sana hasa katika Vijiji vya Kilole, Ngulu, Gale, Miegeyo, Handei, Magashai, Tambwe, Mazumbai, Ngwelo, Milungui na kata nzima ya Makanya. Je, Serikali haioni kwamba sasa vijiji hivi lazima vipewe kipaumbele kwa ajili ya kupata umeme kwa sababu wamesubiri kwa muda mrefu sana?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Jimbo la Lushoto lina vitongoji zaidi ya 32 na Mheshimiwa Waziri Kalemani yeye ni shahidi ametembelea Lushoto na akaona Wilaya nzima ya Lushoto hakuna nyumba ya nyasi hata moja na wananchi wote wameshafanya wiring wanasubiri umeme. Je, ni lini sasa vitongoji vile vya Wilaya ya Lushoto vitapata umeme kwa wakati ili wananchi wapate huduma stahiki kama wenzao wanavyopata huduma?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, commitment ya Serikali ni kwamba, ifikapo tarehe 15 Februari, 2021 vijiji vyote vilivyobakia 2,150 ambavyo havikuwa vimepata umeme katika REA Awamu I, II na III mzunguko wa kwanza vitapelekewa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu uliofanyika sasa hivi ni kuhakikisha kwamba mkandarasi mmoja hapewi kazi kubwa sana. Kwa hiyo, tutaona maajabu makubwa katika kipindi hiki ambapo tutaanza kupeleka umeme katika maeneo mengi kwa wakati mmoja kwa sababu mkandarasi mmoja pengine inaweza ikawa anapeleka umeme au jimbo moja. Kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Shekilindi, kwamba huduma anayotupatia ya dawa na sisi tutapeleka huduma ya umeme kwenye kwa kadri tulivyoelekeza katika kipindi hiki hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali la pili la kupeleka umeme kwenye vitongoji, Wizara ya Nishati kwa maelekezo ya Serikali inatekeleza mradi unaoitwa densification na sasa tuko katika densification 2B ambao ni mradi jazilizi kwa ajili ya kupeleka umeme katika vitongoji na kufikia mwezi Mei tutakuwa tayari tumesaini mikataba kwa ajili ya kupeleka umeme kwenye vitongoji zaidi ya 2,800 katika nchi yetu ya Tanzania. Kwa hiyo, tunaamini katika upanuzi huo wa miradi jazilizi, basi Jimbo la Lushoto pia litapata maeneo kadhaa ya kuwekewa umeme katika maeneo ya vitongoji vyake. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza, nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri, kwa kweli nimehakikisha mwenyewe kwamba kazi inaendelea.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kama unavyojua jiografia ya Wilaya ya Lushoto ni ya milima na mabonde ambayo husababisha kutopata huduma katika maeneo mbalimbali hasa Makanya, Mavului, Mbwei na maeneo mengine ya Mazumbai. Je, ni lini sasa Serikali itaenda kujenga minara ile ili kuondoa kadhia wanayoipata wananchi wa Wilaya ya Lushoto?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Wilaya ya Lushoto ina changamoto ya usikivu wa Radio ya Taifa yaani TBC na hili suala nilikuwa naliongelea mara kwa mara lakini mpaka leo hii hakuna majibu yoyote wala hakuna mnara wowote uliojengwa. Je, ni lini Serikali itaenda kujenga minara ya habari ndani ya Wilaya ya Lushoto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shabani Omari Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hatua ambazo Serikali inazichukua kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote kwanza kabisa ni kujiridhisha na ukubwa wa tatizo wa eneo husika. Ukubwa huo unaweza ukategemea na tatizo lenyewe, inawezekana katika maeneo fulani mawasiliano hakuna kabisa; maeneo mengine mawasiliano ni hafifu; lakini kuna maeneo mengine ambapo unakuta kwamba mawasiliano yako hapa hayako hapa; kunakuwa na dark sport za kutosha. Sasa Serikali inapofanya tathmini ni kujiridhisha pia na ukubwa wa tatizo ili kujua teknolojia gani ambayo tunaweza kwenda kuitumia pale ili kutatua tatizo la eneo husika kulingana na tathmini iliyofanyika.

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri tumekuwa na mawasiliano mazuri na amekuwa akiwapambania kweli wananchi wa Jimbo lake na sisi kama Serikali kwa sababu ndio jukumu letu na kupitia Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi, ibara ya 61(f) na (g) inaeleza kabisa kwamba ni jukumu la Serikali kwenda kufikisha mawasiliano kwa wananchi wote, kwa hiyo, suala lake litaangaliwa baada ya tathmini kufanyika.

Mheshimiwa Spika, vilevile suala la usikivu ni jambo lilelile ambalo pia kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) wanaendelea na kufanya tathmini katika maeneo yote pamoja na maeneo ya mipakani kuhakikisha kwamba palipo na changamoto ya usikivu basi Serikali inafikisha mawasiliano katika maeneo husika.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Kituo cha Afya cha Mlola ndiyo kituo pekee kinachohudumia zaidi ya kata nane lakini kiuo kwa muda mrefu hakina gari la wagonjwa.

Je, Serikali ina mpango gani wa haraka kuwapatia Kituo cha Afya Mlola gari la wagonjwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, vituo hivi vya Gare na Ngwelo ni vituo vilivyojengwa na nguvu za wananchi kwa muda mrefu sana. Vituo hivi nilianza kuviongelea tangu 2017, 2018, 2019, 2020 mpaka sasa hivi 2021 lakini hakuna majibu ya kuridhisha, majibu ni haya ya nadharia bila vitendo. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yupo tayari sasa kuongozana nami ili akaone kazi iliyofanywa na wananchi wale? Nadhani hapo ndipo atatupa fedha za kujenga vituo vile.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shabani O. Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Mlola kinahudumia wananchi wengi, kata nane katika Jimbo lile la Lushoto na ni kituo muhimu sana kuhakikisha kwamba kinapata gari la wagonjwa ili kiweze kufanikisha rufaa lakini pia na huduma dharura kwa ajili ya wananchi wa Jimbo la Lushoto. Naomba nimhakikishe Mheshimiwa Shekilindi kwamba Serikali inatambua kwamba kituo hicho kinahitaji kuwa na gari la wagonjwa na taratibu za kupata magari ya wagonjwa katika kituo hicho lakini pia katika Vituo vingine vya Afya zinaendelea kufanyika na tutaendelea kupelekea magari hayo kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hilo tumelichukua na tunalifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusiana na Vituo vya Afya vya Gare na Ngwelo kuanza kujengwa kwa nguvu za wananchi kwa muda mrefu, kwanza, Serikali inawapongeza sana wananchi wa Lushoto kwa kujitolea kuchangia kuanza ujenzi wa Vituo hivi vya Afya. Serikali inatambua sana mchango wa wananchi na itaendelea kutenga bajeti kwa ajili ya kuunga mkono nguvu za wananchi katika kukamilisha vituo hivi vya afya. Naomba nimhakikishie, pamoja na kwamba vituo hivi kwa muda mrefu vimekuwa vikiahidiwa kupatiwa fedha, jitihada zinaendelea kuendelea kutafuta fedha na mara zitakapopatikana Vituo hivi vya Afya vitapewa kipaumbele.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara ya kuanzia Mombo - Soni - Lushoto ni nyembamba mno na husababisha usumbufu mkubwa sana kwa watumiaji wa barabara hiyo hasa katika kipindi hiki cha mvua.

Je, Serikali ina mpango gani wa kupanua barabara hiyo ya Mombo - Soni - Lushoto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara ya Mombo - Lushoto ni nyembamba. Nimhakikishie Mheshimiwa Shekilindi barabara hii itakapoingia kwenye mpango wa kuikarabati upya na ujenzi mpya tutaiangalia; ndio maana kunakuwa na usanifu mpya. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii itakapoingizwa kwenye mpango wa kuijenga upya itafanyiwa Design upya na itapanuliwa ili kuweza kuingia kwenye viwango vya sasa vya barabara za mita saba na nusu kama zilivyo barabara nyingine. Ahsante. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Kwa kuwa Wilaya ya Lushoto ina mvua inayonyesha kwa mwaka mzima na kuharibu miundombinu ya barabara zetu, je, Serikali ina mpango gani wa kujenga mabwawa hasa maeneo ya Makanya, Mbwei, Garibo Eloi, Kwayi, maeneo ya Kata ya Ubiri ili wananchi wale waweze kulima kilimo cha umwagiliaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shekilindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Tanga na tukizungumzia kuanzia Wilaya ya Lushoto, Wilaya ya Handeni kuelekea mpaka Muheza ni wilaya ambazo kwetu ni priority kama Wizara ya Kilimo. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kuanzia mwaka ujao priority yetu ni kutumia resources zetu wenyewe kwa maana ya kujenga mabwawa. Sasa hivi tunafanya comprehensive study ya kuangalia maeneo ambayo tunaweza kujenga mabwawa kwa gharama nafuu. Kwa hiyo, maeneo yake ni miongoni mwa maeneo ambayo tunayapa kipaumbele, avute subira tutayafanyia kazi.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Lushoto ina wakulima wadogo wadogo wa njegere na zao hili linapendwa sana nchi za nje; je, Serikali ina mpango gani wa kuwaongezea mitaji wakulima hawa hasa wakulima wa Kijiji cha Bombo, Ubiri, Jogoi, Ngare na maeneo mengine ya Wilaya ya Lushoto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shekilindi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitumie Bunge lako Tukufu, pamoja na kujenga mazingira mazuri ya mabenki kuendelea kuwapatia mikopo wakulima niziombe Halmashauri za nchi yetu mnatenga asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya kukopesha wajasiriamali, kilimo ni biashara, wajasiriamali siyo mama ntilie tu wala siyo madereva wa bodaboda. Niziombe Halmashauri pelekeni asilimia 10 mnazotenga katika Halmashauri zenu kwenye sekta ya Kilimo return on investment is 100% na wala hakuna defaulters kwenye kilimo unless kuna risk. Tuache kukopesha wachuuzi twendeni kwenye uzalishaji. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Serikali imejiridhisha kuwa barabara ya kuanzia Dochi kupitia Ngulwi hadi Mombo ambayo ni kilometa 16 kuwa itajengwa na TANROADS: -

Je, ni lini barabara hiyo itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama alivyosema Mheshimiwa Shekilindi barabara ya Dochi - Mombo yenye urefu wa kilomita 16 itajengwa na TANROAD, lakini katika mpango huu kwa mwaka huu wa bajeti, barabara hii haimo. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba TANROADS kupitia Serikali, barabara hii katika mipango ijayo itajengwa kama ilivyoahidiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza namshukuru Waziri kwa majibu yake mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto ina Shule za Msingi 163 na Shule za Sekondari 53. Jumla ni shule 216 na watumishi ambao wapo pale kwenye shule ya msingi na sekondari mwaka 2006 ambao ni asilimia kama 40. Kuna upungufu watumishi 1,958: -

Je, Serikali ina mpango gani wa haraka kupeleka walimu 1,958 kada ya uwalimu katika Wilaya ya Lushoto ili kuendeleza taaluma ya Wana-Lushoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Halmashauri ya Lushoto ina Hospitali ya Wilaya moja na vituo vya afya na zahanati 68, lakini watumishi walioko pale ni 335. Kwa hiyo, kuna upungufu wa watumishi 763. Hiyo ni idadi kubwa sana. Kwa hiyo, ni asilimia kama 35: -

Je, Serikali ina mpango gani wa dharura kupeleka watumishi wa kada ya afya 763 katika Halmashauri ya Lushoto ili kunusuru kuokoa maisha ya wananchi wa Lushoto hasa akina mama wajawazito, watoto na wazee? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shabani Omari Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya watumishi wa Sekta ya Afya na Sekta ya Elimu iko nchini kote na Serikali imechukua hatua. Kwanza hatua ya kufanya tathmini ya upungufu wa watumishi katika sekta zote, lakini pili katika mwaka wa fedha uliopita zaidi ya watumishi 9,000 waliajiriwa, lakini pia kupelekwa katika halmashauri hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi kubwa ambayo imefanyika, tumefanya tathmini kwa kuweka mpangilio na kutambua mikoa na halmashauri zenye upungufu mkubwa zaidi ikilinganishwa na mikoa na halmashauri nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna halmashauri ambazo ndani ya mkoa husika zina upungufu mkubwa ikilinganishwa na halmashauri ndani ya mkoa huo huo. Tumetoa maelekezo Makatibu Tawala wa Mikoa kufanya internal redistribution ya watumishi ndani ya mkoa ili halmashauri yenye upungufu mkubwa ndani ya mkoa ipate watumishi kwanza ndani ya mkoa. Pili, tunakwenda kwenye ngazi ya mkoa kwa maana katika nchi nzima kuhakikisha ile mikoa yenye upungufu mkubwa zaidi inapata kipaumbele kwenye ajira zinazofuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Shekilindi kwamba kwenye ajira zinazofuata halmashauri yake itatoa kipaumbele cha hali ya juu kwa sababu ya upungufu huo ili kuhakikisha Walimu na watumishi wa sekta ya afya wanapata huduma bora. Ahsante sana.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kumekuwa na ahadi ya muda mrefu sana kupeleka gari ya wagonjwa katika Kituo cha Afya Mlola. Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hiyo kupeleka gari Kituo cha Afya Mlola?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shabani Shekilindi, Mbunge wa Jimbo la Lushoto kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, halmashauri ya Lushoto itapewa gari la wagonjwa jipya kati ya Oktoba na Novemba mwaka huu, kwa hivyo nimuombe Mheshimiwa Mbunge kwa kushirikiana na Mkurugenzi waone uwezekano wa kupeleka gari hili katika kituo cha afya cha kipaumbele kikubwa zaidi ikiwemo hicho ambacho amekitaja. Ahsante.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Lushoto kuna uwanja wa muda mrefu sana lakini uwanja ule unatakiwa ukarabati. Je, nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba inapeleka fedha kwa ajili ya ukarabati uwanja ule?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa michezo ni ajira. Je, Serikali ina mpango mkakati gani wa kuibua, kubaini na kuwahakiki vijana ambao wanataaluma ya michezo hususan Wilaya ya Lushoto hasa Lushoto Vijijini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kunipa nafasi na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Shekilindi swali lake la kwanza amependa kufahamu ni lini Serikali inatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa uwanja huo wa Lushoto lakini viwanja vingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika majibu yangu ya msingi nimeeleza kwamba Sera yetu ya michezo imezitaka Serikali kwa ngazi zote Serikali Kuu lakini Serikali za Mitaa kutenga fedha. Ni rahisi sana kama halmashauri zetu, Wakurugenzi pamoja na Waheshimiwa Wabunge na Madiwani tukasimamia kupitia Idara ya Michezo fedha zikatengwa na viwanja hivi vitajengwa na ninyi ni mashahidi tumeanza sisi kwenye wizara bajeti iliyopita tumetenga zaidi ya bilioni 10 kwa ajili ya kujenga viwanja vya kitaifa. Kwa hiyo, naomba nitoe rai tuendelee kutenga fedha kwa Serikali kwa ngazi zote ili tujenge viwanja hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili Mheshimiwa Shekilindi amependa kufahamu ni jinsi gani tunashirikiana na TAMISEMI pia kuhakikisha vipaji vinaibuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wizara tumeshatoa maelekezo kwa ngazi zote na kwa vyama vyetu na mashirikisho, kwamba vipaji vinapoibuliwa vyama na mashirikisho yaweze kushiriki. Naomba nipongeze kwa niaba ya Waziri, Wabunge na Madiwani ambao wamekuwa wakichezesha ligi mbalimbali katika maeneo yao, maana yake wanaibua vipaji. Sisi kama Wizara tunakuja na mtaa kwa mtaa kuhakikisha kwamba tunapofika kwenye lengo la Taifa la Taifa cup tunahakikisha kwamba huko chini vipaji vimeibuliwa. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; kwanza nimpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Pauline Gekul kwa kujibu maswali vizuri. Ofisi ya Rais, TAMISEMI tunashirikiana vema na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo katika kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi ambayo imetuelekeza kupitia Sanaa, Michezo na Utamaduni tunatengeneza ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitoa maelekezo kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa, Shule za Msingi na Sekondari kote nchini kuhakikisha maeneo yanapimwa na tunapata haTi kufika Disemba, 30; na nimeelekeza kopi ya hati ije Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili niweze kujiridhisha kila shule ya msingi na sekondari imepimwa na kupata hati. Tunafanya hivi ili kuhakikisha maeneo ya shule tunapunguza uvamizi ikiwemo maeneo ya michezo kwa maana ya viwanja vya michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nitumie nafasi hii kuwaagiza Wakurugenzi kufanya kipaumbele kwenye bajeti za Mamlaka za Serikali za Mitaa, kutenga fedha kwa ajili ya kujenga viwanja vya michezo ni moja ya vipaumbele katika kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. SHABAN O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Takribani miaka sita sasa imepita katika Kata ya Kwai iliahidiwa na Serikali mradi wa maji lakini mpaka sasa mradi ule hakuna chochote kilichofanyika. Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka maji katika Kata ya Kwai ili wananchi waondokane na adha hii wanayoendelea kuipata sasa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kata zake nyingi katika jimbo tumeshazishughulikia, hivyo hata kata hii ipo katika mkakati wa kuona kwamba na wao wanaenda kupata maji safi na salama ya kutosha. Tukishindwa kukamilisha ndani ya mwaka huu wa fedha basi mwaka ujao wa fedha tutahakikisha hii kata nayo inakwenda kunufaika na kumtua mama ndoo kichwani.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pia nishukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa, mfumo huu wa kutumia dirisha la wazee unaonyesha una mapungufu makubwa. Je, Serikali haioni kuwa ipo haja sasa kubadilisha mfumo huu na ikiwezekana wazee wapewe kadi kabisa za bima ya afya, kuliko kupewa vitambulisho kama ilivyokuwa sasa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa wazee wengi wanaoishi vijijini hawajui kabisa kwamba kuna dirisha lile la afya, kutumia huduma za afya; je, Serikali ina mpango gani wa kuwafikia wazee hawa ili nao waweze kupata huduma hii muhimu kwao kama wazee wenzao wanaoishi mijini? (Makofi)
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Shabani Omari Shekilindi kwa maswali yake mawili ya nyongeza hususani katika kuhakikisha kwamba wazee wetu wanapata huduma bora za matibabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba tubadilishe mfumo wa kutumia dirisha la wazee lakini tutumie mfumo wa bima ya afya kwa wote. Nitumie Bunge lako Tukufu kuwashawishi Waheshimiwa Wabunge wote, Ijumaa kupitisha Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa wote, kwa sababu moja ya jambo ambalo linakwenda kutatua ni kuhakikisha kwamba wazee pia wanapata huduma za matibabu bila ya kikwazo cha fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Wizara ya Afya tunaamini kwamba, kutungwa kwa Sheria ya Bima ya Afya kwa wote kutaboresha upatikanaji wa huduma za afya kwa wazee ikiwa ni pamoja na dawa. Kwa sababu wazee wengi sasa hivi wanakwenda kwenye dirisha la wazee, dawa hakuna, wakiwa na bima tunaamini watapata dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Wazee wa Vijijini hawapati hii huduma, tumekinyanyua kile kitengo kilichokuwa kina shughulikia huduma za wazee, kimekuwa sasa ni section, kwa hiyo, kina Mkurugenzi Msaidizi, kazi yake kila siku ni kuangalia huduma za matibabu kwa wazee, huduma za rehabilitation pamoja na huduma za palliative za shupaa. Kwa hiyo, tunaamini kabisa pia hii itaongeza muamko katika kutatua changamoto za wazee. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona. Hali ya upatikanaji wa maji katika Kata ya Makanya, Kwekanga na Kwayi ni mbaya sana na ukizingatia sisi hatuna matatizo ya vyanzo vya maji. Je, ni lini Serikali itapeleka maji kwa haraka iwezekanavyo katika kata hizo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kata hizi alizozitaja pamoja na Makanya zipo kwenye utendaji wa kiwizara. Naomba nitumie Bunge lako Tukufu kumwarifu Mheshimiwa Mbunge kwamba nitasimamia kuhakikisha ndani ya mwaka huu wa fedha haya maeneo yanapata maji.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Jimbo la Lushoto wananchi pamoja na Serikali yao wamejenga vituo vya afya pamoja na zahanati, lakini kumekuwa na changamoto kubwa sana za nyumba za watumishi. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga nyumba za watumishi katika Wilaya ya Lushoto?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo swali la msingi lilieleza kwamba kwa mwaka huu wa fedha zinaenda kujengwa nyumba 300. Naomba tukae na Mheshimiwa Mbunge tuangalie katika hizi 300 kama Lushoto eneo analolizungumzia limeguswa kama halijaguswa, tuone mapema tunaweza tukafanya nini ili hilo litekelezeke.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kupeleka maji katika Kata ya Kwai, Kwekanga pamoja na Makanya?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge Shekilindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kata hizi alizozitaja Mheshimiwa Mbunge Shekilindi, nimeongea naye juzijuzi na nimemhakikishia kwamba kazi hii tutaenda kuifanya. Tumeshakubaliana kwamba tunakwenda kuangalia mradi na tutahakikisha unatimizwa kufanyiwa kazi yake kwa wakati.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa mwenyekiti, nakushukuru, pia namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa majibu mazuri. Nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Lushoto lina Mahakama za mwanzo mbili, kwa maana Mahakama ya Mlola na Mahakama ya Gare. Lakini hii ya Gare takribani miaka 20 sasa haifanyi kazi yani jengo lake limekeuwa ni gofu.

Je, Serikali in ampango gani wa kujenga upya Mahakama ya Gare pamoja na kata jirani ili waweze kupata huduma?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshmimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi kama ifuatavyo: -

Mheshmimiwa Mwenyekiti, kimsingi Mahakama ya Tanzania katika mpango wake inajenga Mahakama za Mwanzo katika Makau Makuu ya Tarafa zote hapa nchini.

Kata ya Gare haipo kama sehemu ya Makao Makuu ya kata kwa sababu iko ndani ya Tarafa ya Lushoto yenyewe. Hivyo tunaangalia uwezekano wa kuzipa umuhimu kata ambazo zina uhitaji maalum. Baada ya Bunge hili tutawasiliana na Mheshimiwa Mbunge kujua uhalisia wa tatizo la Gare lakini kwa sasa tunaelekeza nguvu zetu Makao Makuu ya Tarafa hapa nchini.
MHE. SHABAN O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona. Kwanza nishukuru Serikali kwa kututengea fedha za nusu kilomita kwa Barabara ya Magamba kwenda Mlalo na Barabara ya kutoka Magamba kwenda Mlola. Hata hivyo, mara nyingi tumekuwa tukiomba kwamba tuongezewe kilometa tano, je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza kilometa tano ambazo tumeziomba? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii tumeamua kuijenga kwa awamu na naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kupitia Ofisi ya Meneja wa TANROAD wa Mkoa wa Tanga, barabara hii tutaenda kuijenga kwa awamu kadiri fedha zitakapopatikana. Kwa hiyo tutaendelea kuijenga kwa vipande vipande mpaka tukamilishe hizo kilomita tano. Ahsante.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, namshukuru Waziri kwa majibu mazuri, lakini pia nimshukuru kwa kutupa milioni 2008. Kama unavyojua Wilaya ya Lushoto ni kubwa sana. Kwa hiyo, milioni 208 ni fedha chache sana. Swali la kwanza, je, Serikali haiona sasa kwamba kuna haja ya kuongeza fedha zile angalau zifike hata bilioni moja ili kumaliza upimaji katika Wilaya ya Lushoto?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; takwimu za nchi nzima zinaonesha kwamba ni asilimia 25 tu ya sehemu ya ardhi ndiyo iliyopimwa katika nchi hii ya Tanzania. Je, haioni Serikali kwamba inasuasua sana kwa suala hili la kupima na kuleta migogoro ndani ya nchi hii. Sasa Serikali ina mpango gani au ina mkakati gani wa haraka kuhakikisha kwamba inatenga bajeti ya kutosha na kupima ardhi hii nchi nzima ili kuondoa migogoro ndani ya nchi hii ya Tanzania? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu maswali ya nyongeza Mheshimiwa Shekilindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza Serikali imeendelea ku-support hatua mbalimbali zanazofanywa na halmashauri zetu kuhakikisha kwamba miradi au maeneo yetu yanapimwa. Katika kufanya hivyo Serikali imepata mkopo wa dola milioni 150 kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa umilikishaji wa ardhi ambapo katika moja ya mambo makubwa yanayoenda kufanyika ni kuendelea kupima na kupanga ardhi ya Tanzania. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba pamoja na kwamba anaona fedha hizi hazitoshi lakini mipango kwa ajili ya kupima Tanzania nayo pia inaendelea.

Mheshimiwa Spika, pili, katika ardhi ya Tanzania, takribani asilimia 20 ya maeneo ya Tanzania yamepimwa ambapo viwanja zaidi ya 2,800 na mashamba zaidi ya 28,000 yamekwisha tambulika. Hivyo nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba zoezi linaendelea kufanyika na ni mipango na maelekezo ya Serikali kuhakikisha kwamba ardhi yote ya Tanzania inapimwa. Ahsante.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Je, ni lini Chuo cha VETA kilichojengwa Wilayani Lushoto Eneo la Mlola kitaanza udahili?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa Chuo cha VETA Lushoto ni miongoni mwa vile vyuo 25 vya awamu ya kwanza, ambapo ujenzi wake umeshakamilika kwa asilimia 100. Nimuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kama nilivyokwishajibu kwenye majibu ya swali la msingi vyuo hivi vyote 25 vya awamu ya kwanza, tunapeleka samani, vifaa vya kufundishia pamoja na kuandaa rasilimali watu. Ni matumaini yetu katika mwaka wa fedha 2023/2024 vyuo hivi vyote 25 vya wilaya na vile vinne vya mikoa vinaenda kuanza kutoa mafunzo rasmi.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kuna changamoto ya mawasiliano kwenye Kata za Makanya, Malibwi, Kwai na maeneo mengine katika Jimbo la Lushoto: -

Je, ni lini mawasiliano yatapelekwa katika kata hizo?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shabani Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba inafikisha huduma ya mawasiliano nchini kote na tunakwenda kwa awamu. Hivyo, nalipokea ili wataalam wetu waende wakafanye tathmini katika maeneo hayo na tujiridhishe changamoto yenyewe iko katika upande upi ili tuweze kuchukua hatua stahiki.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; Masoko ya Wilaya ya Lushoto hupoteza zaidi ya tani 400 za mbogamboga na matunda kwa kila mwezi. Je, Serikali haioni sasa kuna haja ya kujenga soko kubwa lenye cold room kwa ajili ya kuhifadhi mazao yale au mbogamboga zile ili wananchi wasiendelee kupata hasara?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha kwa kuwapelekea wawezeshaji wakulima wa mbogamboga ili kuongeza mnyororo wa thamani katika mazao yetu haya ya mbogamboga na matunda?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shekilindi, kwa pamoja, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wilaya ya Lushoto na Wilaya za Mkoa wa Tanga, Serikali sasa hivi inafanya tathmini ya kuangalia maeneo ya kujenga masoko, kwa sababu hatutaki kufanya makosa ambayo yamewahi kutokea huko nyuma katika baadhi ya miradi ambapo hata katika wilaya ya Lushoto, kuna jengo lililojengwa la Ubaridi (cold room facility) ambayo mpaka leo haitumiki. Kwa hiyo, nataka nitumie nafasi hii kumwambia Mheshimiwa Mbunge, hivi sasa tunavyoongea wataalam wa Wizara wako Mkoa wa Tanga wakiangalia wapi tuweke masoko ili tuweze kutatua tatizo la mazao ya mbogamboga na matunda hasa machungwa.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Bweni la Sekondari ya Mlongwema ni dogo sana na halikidhi mahitaji kwa wanafunzi wale; je, Serikali ina mpango gani wa kujenga bweni kubwa ambalo linaweza kukidhi mahitaji ya wanafunzi wa Mlongwema? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ni kipaumbele cha Serikali kujenga mabweni katika shule zote za A-Level. Tutakaa na Mheshimiwa Mbunge kuweza kuona shule hii ambayo ameitaja mahitaji hasa ni yapi ili tuweze kutafuta fedha ya kwenda kumalizia au kujenga mabweni mapya katika shule hiyo.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, huu ni mwaka wa nane Serikali iliahidi kupeleka maji katika Kata za Makanya, Mlola, Kwai, Kwekanga hadi Kilole.

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake hii ya kupeleka maji katika maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shabani Shekilindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwenye kata hizi zote alizozitaja Mheshimiwa Mbunge tuna miradi ambayo tunaielekeza katika mwaka wa fedha ujao. Lakini vilevile maeneo yote ambako miradi tulishaanza kuitekeleza tutakwenda kuikamilisha. Mheshimiwa Mbunge hili tumeshajadiliana muda mrefu na ameshafika ofisini mara nyingi. Naomba nimpe ahadi kwamba baada ya hapa kama tulivyokubaliana tutakwenda na tutahakikisha miradi ile tunaifanya vizuri.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, pia nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri. Ni kweli kitalu kiko tayari na wakulima wanaendelea kupata miche ya kahawa. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa zao la kahawa ni zao ambalo linaingiza fedha nyingi za kigeni: -

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha zaidi zao hili la kahawa hapa nchini?

(b) Je, ni lini Serikali itaruhusu bei ya zao la kahawa kuamuriwa na nguvu ya soko?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na swali la kwanza la kuboresha na kuhakikisha kwamba tunatafuta masoko ya uhakika. Ni dhamira ya serikali ya awamu ya sita kuhakikisha kwamba zao la kahawa linaendelea kuwa na mchango mkubwa katika kuingiza fedha za kigeni na kubadilisha maisha ya wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa tunaendelea na kuitangaza kahawa yetu nje ya mipaka ya Tanzania kwa sababu wanunuzi wakubwa wanatoka nje ya mipaka ya Tanzania. Tunashirikiana na Balozi zetu mbalimbali na kupitia matamasha na maonesho mbalimbali tumekuwa tukiitangaza kahawa yetu na jambo hili limetuletea tija kubwa sana. Nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kuhakikisha kwamba tunaweka miundombinu wezeshi ili zao hili liweze kupata soko la uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili la kuhusu bei ya kahawa kuamuliwa na nguvu na soko. Mwenendo wa masoko rejea ya kahawa duniani ndiyo ambayo huwa yanaamua bei ya kahawa. Masoko haya ni masoko ya New York kwa kahawa ya arabika na Euronex Uingereza kwa ajili ya robusta. Sisi kama Serikali tumehakikisha kwamba mara zote tunahakikisha wakulima wetu kupitia taarifa hizi wanapata taarifa sahihi na mwisho wa siku waweze kupata bei ambayo itamnufaisha. Kwa hiyo kama Serikali tumeacha nguvu hiyo ya soko iamue, lakini tunawasaidia wakulima wetu kuzalisha kahawa bora ambayo itasaidia pia kuongeza tija katika Soko hilo la Kimataifa. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kumekuwa na changamoto kubwa sana ya mawasiliano katika Kata ya Makanya, Mbwei na Maibwi; je, ni lini Serikali itapeleka mawasiliano katika Kata hizo?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Shabani Omari Shekilindi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tayari tulishawasiliana na Mheshimiwa Shabani Omari Shekilindi na amekuwa akinijulisha kuhusu changamoto hiyo. Maeneo na kata ambazo zina changamoto hizo tayari Serikali imeshazipokea na imeziingiza kwenye mpango wa utekelezaji wa miradi ambayo inakuja kadri ya upatikanaji wa fedha utakavyoruhusu, ahsante sana.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na namshukuru Waziri kwa majibu mazuri. Changamoto ya kukosa maji katika Kata ya Kwekanga, Kwai, Malibwi, Mbwei, Makanya na Mlola ni changamoto muda mrefu sana. Suala hili nimeliongelea zaidi ya takribani Mikutano Kumi bila mafanikio yoyote na wananchi wangu wakiendelea kupata tabu ya maji.

Je, nini mkakati wa dharura wa Serikali kupeleka gari la kuchimba visima katika kata nilizozitaja?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kuna Mradi wa Magamba eneo la Gelwa Ali unaitwa Mtaa Na. 9 na survey imeshafanyika. Mradi ule ukikamilika unakwenda kuhudumia kata zaidi 13. Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya kutekeleza mradi huo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kumpongeza Mheshimiwa Shekilindi, amekuwa mfuatiliaji nilikuahidi nitafika jimboni Mheshimiwa Mbunge, kipindi kilichopita sikuweza, baada ya Bunge hili nitahakikisha tunakwenda kuona maeneo haya na kuweka msisitizo ili kuhakikisha miradi hii inatekelezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati wa dharura tayari Mheshimiwa Mbunge tumekutengea shilingi milioni 300. Tunataka baada ya ukamilishaji wa hii survey visima hivi vichimbwe na hatutaishia tu kuchimba visima. Tutahakikisha tunasambaza na kujenga vichotea maji kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, fedha za Miradi ya Mbao tayari usanifu umekamilika. Mheshimiwa Mbunge, tayari tutaendelea kukuletea fedha. Sasa hivi tumekutengea milioni 300 na mgao ujao tutahakikisha tunakutengea fedha. Mimi mwenyewe nitakuja jimboni kuleta msukumo hii miradi iweze kutekelezeka.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muda mrefu sasa Kituo cha Afya Mlola hakina gari la wagonjwa na hii imepelekea hasa kwa wagonjwa mahtuti kupelekwa na bodaboda katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto. Je, Serikali lini itapeleka gari la wagonjwa katika Kituo cha Afya Mlola ili kuokoa maisha ya wananchi wetu?

Swali la pili, nimeongea kwa muda mrefu sana kuhusu kupeleka fedha katika Kituo cha Afya Gare lakini mpaka sasa hivi hakuna mafanikio yoyote, kama waswahili wanavyosema kuona ni kuamini. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri upo tayari kuongozana na mimi kwenda kuona nguvu za wananchi wale wa Gare kwa ajili ya ku-support Kituo kile cha Afya Gare?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Shekilindi kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa sababu amekua akifuatilia sana suala hili la magari katika Kituo cha Afya Mlola.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye kumjibu maswali yake mawili ya nyongeza hili la magari Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Daktari Samia Suluhu Hassan imetenga fedha shilingi bilioni 93 kwa ajili ya ununuzi wa magari 316 ambayo kila Halmashauri ya Wilaya itapata walau magari mawili ya kubebea wagonjwa. Vilevile kuna bilioni 61 ambayo Serikali hii ya Daktari Samia Suluhu Hassan imetenga kwa ajili ya ununuzi wa magari mengine ambayo kila Halmashauri itapata gari moja walau la supervision katika Halmashauri za Wilaya ili wataalam wetu wa afya waweze kutembelea zahanati zetu na vituo vyetu vya afya. Hivyo nimhakikishie Mheshimiwa Shekilindi kwamba tutahakikisha vilevile katika magari haya mgao huo basi Mlola nayo inapewa kipaumbele kupata gari hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la Kituo cha Afya cha Gare kule Wilayani Lushoto nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge niko tayari kuongozana naye Mheshimiwa Shekilindi, kuelekea Wilayani Lushoto kwa ajili ya kuweza kukagua jitihada hizi za wananchi na kuona ni namna gani Serikali kuu inaweza ika-support juhudi hizi za wananchi wa eneo la Gare.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, Shule ya Msingi Mshizii, Mategho na Mavului zina hali mbaya sana. Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kupeleka pesa kwa ajili ya ukarabati wa shule hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kumuelekeza Afisa Elimu wa Mkoa wa Tanga kufika katika Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto na kufanya tathmini katika shule ambayo ameitaja Mheshimiwa Shekilindi na tathmini hiyo ikikamilika basi wawasilishe Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kuona namna gani tunatafuta fedha katika mwaka wa fedha unaofuata kwa ajili ya ujenzi wa maboma hayo katika shule hiyo.

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; je, ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba katika zahanati za Wilaya ya Lushoto zilizokamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itapeleka vifaa tiba kwenye zahanati za Wilaya ya Lushoto pale ambapo tutaanza utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha wa 2023/2024 ambapo Serikali imetenga shilingi bilioni 112 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba kote nchini.

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pia nishukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, Serikali ni lini itapeleka fedha kujenga Vituo vya Afya katika Kata ya Kwayi pamoja na Kata ya Makanya? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa Kituo cha Afya Gare kimezungukwa na kata mbili ambazo hazina vituo vya afya. Je, Serikali haioni sasa ipo haja ya kupeleka gari la wagonjwa ili kurahisha huduma kwa wananchi wetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shekilindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza hili kuhusu ujenzi wa Vituo vya Afya vya Kwayi na Makanya, tutakaa na Mheshimiwa Shekilindi kuona katika mwaka wa fedha wa 2023/2024 ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya Ujenzi wa Vituo vya Afya katika Halmashauri yao na tuhakikishe fedha hizi zinakwenda katika walau kituo cha afya kimojawapo, kwa sababu ni mpango wa Serikali wa kujenga vituo vya afya kwenye maeneo ya kimkakati nchini kote ikiwemo Kwayi na Makanya.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la gari ya wagonjwa katika Kituo cha Afya cha Gare. Mheshimiwa Mbunge ni shahidi kwamba muda siyo mrefu kituo hiki cha afya kimetoka kukamilika kwa maana kilipelekewa fedha na tayari kimeshakamilika. Sasa kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi kwamba Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imenunua magari 316 kwa ajili ya kila Halmashauri kupata walau magari mawili ya wagonjwa. Sasa magari haya mawili yatayoelekea kule Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto waelekeze moja katika Kituo hiki cha Afya cha Gare. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kumuuliza swali la nyongeza Mheshimiwa Naibu Waziri, wananchi wa Kata ya Gale, na Kata ya Makanya, wamejenga viuo vya afya kwa nguvu zao wenyewe.

Je, ni lini Serikali itatoa milioni 250 kama ilivyokuwa inatoa fedha hizo kwenye vituo vingine? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeweka mkakati ambao umeendelea kutekelezwa na Waheshimiwa Wabunge wote ni mashahidi kwamba Serikali imeendelea kupeleka fedha Milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya, tumeendelea kupeleka Milioni 50 kwa ajili ya ukamilishaji wa zahanati na hospitali za Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi vituo ambavyo wananchi wameanza ujenzi, Serikali itapeleka fedha ili tuweze kukamilisha ujenzi huo, ahsante. (Makofi)
MHE. SHABAN O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mahakama ya Wilaya ya Lushoto ni ya zamani tangia mkoloni. Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati au kujenga Mahakama mpya Wilayani Lushoto?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi Mbunge wa Lushoto kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Lushoto nilifanya ziara hivi karibuni na tayari wataalam walishafanya assessment juu ya ukarabati ule. Kwa hiyo, muda wowote jengo lile la Wilaya linaweza likaanza ukarabati. Ahsante.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri na ni kweli kituo kile kinamalizika niishukuru Serikali kwa kutupa fedha milioni 417, lakini pia nimshukuru IGP Sirro alikuja kule na akamuomba Mkuu wa Wilaya aitishe harambee ya kuchangia majengo ya watumishi, lakini Mkuu wangu wa Wilaya alifanya hivyo na mpaka sasa hivi tunavyosema kuna zaidi ya shilingi milioni 210 kwa ajili ya kujenga nyumba za polisi namshukuru sana Mkuu wangu wa Wilaya na timu yake ya Kamati ya Ulinzi na Usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza; Gereza la Lushoto lipo katikati ya Mji wa Lushoto na hivyo kusababisha wafungwa wetu kukosa hata sehemu ya kuota jua, lakini wakati huo huo kuna eneo lipo nje ya mji kidogo wanaita Yogoi.

Je, Serikali haioni kuwa kuna umuhimu wa kwenda kujenga gereza hilo maeneo ya Yogoi na ambako ndiyo kwenye nafasi kubwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Wilaya ya Lushoto ina wakazi wengi sana kama unavyofahamu, lakini ina taasisi nyingi za binafsi na za Serikali, lakini ikitokea changamoto ya majanga ya moto huwa wanapiga simu Korogwe ambayo kutoka Lushoto kwenda Korongwe ni kilometa zaidi ya 70. Kwa hiyo, mara nyingi wananchi wetu wanapata hasara.

Sasa basi niiombe Serikali, je, Serikali haioni kuwa kuna umuhimu au ulazima haraka kujenga kituo cha zimamoto katika Wilaya ya Lushoto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Shekilindi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru kwa kutambua juhudi za Wizara lakini na hususani Jeshi la Polisi kufuatilia maendeleo ya ujenzi wa kituo cha polisi pale Lushoto. Lakini nimshukuru pia DC kwa harambee aliyoifanya kupata shilingi milioni 210 kwa ajili ya nyumba za wafanyakazi, nadhani ni jambo jema la kuigwa na maeneo mengine.

Sasa kuhusu gereza la Lushoto ambalo tunatambua liko katikati ya mji na eneo lile ni finyu ni kweli baada ya Wizara kuona changamoto hizo inayo mpango wa kuhamishia gereza hilo eneo ya Kambi ya Yogoi ambayo iko nje kidogo ya Mji wa Lushoto. Kwa hiyo, pale itakapopata fedha za ujenzi wa gereza hilo, gereza hilo tutalihamisha ili jengo lililopo lifanye kazi nyingine za kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na lingine kuhusu ombi lake la zimamoto tunalipokea ni suala tu la kibajeti tutakapo kuwa tumepata fedha tutajenga Ofisi ya Zimamoto ndani ya Wilaya ya Lushoto. Nashukuru.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, Wilaya ya Lushoto hasa Lushoto Mjini stendi yake ni yazamani sana. Je, Serikali inampango gani wa kujenga stendi mpya sasa Wilayani Lushoto?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi, Mbunge wa Jimbo la Lushoto kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe halmashauri ya Lushoto na Mheshimiwa Mbunge kushirikiana nao kama sehemu ya Baraza la Madiwani kutuletea mapendekezo yao, lakini na tathimini ya gharama ili sasa Serikali iweze kuona utaratibu ambao utatumika kujenga stendi hiyo kwa sababu ni mahitaji ya wananchi. Ahsante.

MHE. SHABAN O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mahakama ya Wilaya ya Lushoto ni ya zamani tangia mkoloni. Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati au kujenga Mahakama mpya Wilayani Lushoto?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi Mbunge wa Lushoto kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Lushoto nilifanya ziara hivi karibuni na tayari wataalam walishafanya assessment juu ya ukarabati ule. Kwa hiyo, muda wowote jengo lile la Wilaya linaweza likaanza ukarabati. Ahsante.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba kumuuliza swali la nyongeza Mheshimiwa Waziri;

Je, ni lini Zahanati za Jimbo la Lushoto zitapata vifaa tiba vya kutosha?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, naomba nimjibu Mheshimiwa Mbunge, swali lake zuri. Kama ambavyo alishuhudia wiki mbili zilizopita, Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan amezindua vifaa mbalimbali. Nimuombe Mheshimiwa Mbunge nikienda kukaa kwenye kiti changu, aje hapa tuwasiliane na DM wake aorodheshe vinavyohitajjika, ili tuweze kupeleka mahitaji MSD mara moja, vifaa vianze kupelekwa kwenye Zahanati zake za Lushoto.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Shule za msingi Kwai, Kweboma zimechoka mno; je, ni lini Serikali itapeleka fedha za ukarabati katika shule hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali hii ya Awamu ya Sita ilitenga zaidi ya bilioni 230 kote nchini kwa ajili ya ukarabati wa shule za msingi zilizochoka na ujenzi wa shule mpya za msingi, zikiwemo nyingine kule Jimboni kwa Mheshimiwa Shekilindi. Hizi shule alizozitaja za Kwai na kwingineko Serikali itaendelea kutafuta fedha na kadri ya upatikanaji wa fedha itapeleka fedha kwa ajili ya ukarabati wa shule hizi.