Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Constantine John Kanyasu (58 total)

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu ambayo ameyatoa lakini sasa naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru wafadhili ambao walijitokeza katika kuja kuendeleza Mji wa Kilwa kwa shughuli mbalimbali ambazo zimetolewa. Hata hivyo urithi wa sasa upo mbioni kutoweka kwa sababu yale yaliyofanyika kama Wizara imeshindwa kuyasimamia katika kuendeleza utalii Kilwa. Kuna shida ya miundombinu ya kutoka Kilwa Mjini kwenda Kilwa Kisiwani,kwa maana ya usafiri wa boti; kumekuwa na boti ile ya kizamani ambayo haina usalama zaidi. Ningependa Serikali sasa kuweka miundombinu sawa ili kuufanya Mji wa Kilwa uweze kuendelea katika upande huo wa utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Kilwa bado kuna maeneo ya Kilwa Kivinje kuna magofu pale ambayo waliishi wakoloni lakini bado hayajaendelezwa kwa ajili ya utalii katika Mji wa Kilwa. Sasa ningeomba kuiuliza Serikali wanatumia njia gani kutangaza kwanza utalii Kilwa lakini ni kwa namna gani wizara hii sasa itakuja Kilwa kuona magofu ambayo wameshindwa kuyaendeleza kwa muda mrefu ili kufanya utalii wa Kilwa kuendelea. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza kwa nafasi hii nimpongeze sana Mheshimiwa Hamida Mohamed Abdallah kwa juhudi kubwa ambayo amekuwa akiifanya kuulizia namna gani wizara inaendeleza utalii katika Mikoa ya Lindi na Mtwara kwa ujumla na amekuwa akitusumbua sana ofisini ili kuweza kufahamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba eneo hili miundombinu imekuwa ni mibaya kutokana na eneo hili kushindwa kujiendesha kutokana na mapato madogo ambayo yamekuwa yakipatikana kutokana na watalii wachache wanaokwenda maeneo hayo. Kwa hiyo, wizara katika kulitafutia ufumbuzi suala hili, imeyagawa maeneo yote ya malikale ambayo yametambuliwa ambayo ni maeneo 18 kwa taasisi zake nne. Eneo hili la Kilwa tumewapa TAWA; TAWA watachukua eneo hili wataliingiza katika packageyao ya utalii na kwa sababu hiyo watalazimika kulikarabati na kutengeneza miundombinu ili liweze kutumika vizuri na watu waweze kupata huduma zote ambazo Mheshimiwa Mbunge amesema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ni kweli kwamba pamekuwa na tatizo la watalii wachache katika maeneo haya na sababu kubwa ni kwamba maeneo haya yamekuwa hayatangazwi. Sasa ili kukabiliana na suala hili, tumeyaingiza mambo haya yote kwenye taasisi na TAWA watakapokuwa wamechukua rasmi watayaingiza katika package zao za utalii ambazo zitakuwa pia zinajumuisha mbuga za wanyama na kwa hali hiyo suala hili la kuongeza mapato na kuongeza usimamizi wa vituo hivi utakuwa umelipa. Naomba nikushukuru.
MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi. Katika majibu yake Mheshimiwa Waziri amezungumzia faida tunazozipata kwa kutunza haya maeneo ya urithi wa dunia. Selous ni moja ya world heritage; nilitaka kumuuliza Waziri kwamba serikali imeamua kujenga bwawa la umeme katika eneo hilo na nina amini Serikali ilifanya upembuzi yakinifu na kuangalia hasara na faida. Anaweza akaliambia Bunge hili ni kwa kiasi gani tutaathirika na UNESCO baada ya sisi kuamua kujenga bwawa hilo na kwamba tunapunguza ile dhana nzima ya urithi wa dunia katika Selous.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Serikali ina mradi wa umeme katika Mbuga ya Selous na kwamba mradi mzima wa umeme katika Mbuga ya Selous unachukua 1.8 ya eneo zima ambalo ni la Selous, na kwa hali hiyo utafiti ulifanyika kwanza hauna madhara yoyote ya uwepo wa Selous na pili hakuna pingamizi lolote ambalo Serikali mpaka leo imepata kutoka UNESCO. Kinachofanyika tu ni kuwaelimisha na kuwafanya waelewe zaidi kwamba uwepo wa bwawa hilo na mradi huo utaiongezea nguvu Serikali namna ya kuifanya Selous iwe mbuga bora zaidi.
MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Kondoa kuna michoro ya mapangoni Kolo – Kondoa Irangi,na michoro hii ni urithi wa dunia kama alivyosema yeye mwenyewe Naibu Waziri, na mpaka sasa wananchi wa Kondoa na hata watanzania hatujafaidika vizuri na michoro ile kwa sababu haijatangazwa ipasavyo.

Je, Serikali ina mikakati gani ya kutangaza michoro ya mapangoni pale Kolo-Kondoa Irangi ili wananchi wa Kondoa wafaidike na Watanzania wote kwa ujumla?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye swali la msingi kuhusu Kilwa, maeneo mengi sana haya ya malikale yalikuwa hayatangazwi na sasa wizara yetu imechukua hatua ya kuyagawa kwenye taasisi zake 4 ambazo ni TANAPA, TFS, Ngorongoro pamoja TAWA. Eneo hili la Kolo-Kondoa tumewapa watu waTFS ambao watafanya kazi zote za uendelezaji ikiwa ni pamoja kuandaa mazingira lakini na kutangaza ili kufanya eneo hilo liweze kufikika na kuvutia watalii.
MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Vipo vijiji vingine. Ukiacha Mtepera na Zinga, kuna Vijiji vya Miguruo na Ngarambi, navyo vinapakana na Pori la Akiba la Selous. Ni lini zoezi hili litafanyika katika vijiji hivyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, uhamishaji umefanyika, wananchi wana uelewa wa mipaka yao kwa kutumia alama zile za asili kama milima na mabonde. Kwa mfano, katika Kijiji cha Zinga pale pana mlima mkubwa unaitwa Nandanga, sasa Mheshimiwa Waziri yuko tayari kufuatana nami ili kwenda kurekebisha mipaka ile kwa kuzingatia alama zile za asili kama milima na mabonde?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Vijiji vya Miguruo na Ngarambi, zoezi hili tutalifanya wakati tukipitia upya. Zoezi la kwanza lilikuwa ni kuweka alama kulingana na GN inavyosoma, lakini kuna maeneo mengi ambayo tuligundua yana migogoro. Kinachofuata sasa ni kupitia upya kuangalia ni maeneo gani ambayo migogoro ina faida kwetu au kwa wanakijiji na tutaangalia namna ambavyo tunaweza tukaisuluhisha. Kwa hiyo, tutakapoanza zoezi hili ambalo tunakwenda kulifanya, tutapita katika vijiji hivi viwili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili; ni kweli kwamba alama nyingi ambazo zimetumika kama mipaka ya vijiji zilikuwa ni alama za asili; miti mikubwa, labda mto fulani, alama ambazo zimekuwa zikitoweka. Kwa hiyo, tumepata taabu katika kuelewa mipaka ya vijiji na pia mipaka ya mapori haya ya akiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namhakikishia Mheshimiwa Ngombale kwamba nitakuwa tayari kuambatana naye ili kwenda kuona hizi sehemu zenye mgogoro.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, kwa kuwa msingi wa swali ni kuhamishwa kwa mipaka ambayo imesababisha mpaka na wanyama wamechanganyikiwa, matokeo yake wanyama sasa wanavamia makazi ya wananchi na hasa wanyama waharibifu kama tembo na viboko: Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba maeneo kama ya Vijereshi, Longalombogo na maeneo mengine ambayo yanaathiriwa na tembo kuongezeka kuja katika makazi ya wananchi yatadhibitiwa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, kimsingi sisi tunapokwenda kuweka mipaka tunafuata GN. Kwa sababu wananchi katika maeneo mengi walikuwa wanatambua mipaka yao kwa alama za asili, ndiyo wamekuwa wakifikiri kwamba tunaingia kwenye maeneo ya vijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetambua maeneo mengi yenye migogoro na Wizara yetu sasa baada ya kumaliza zoezi la kuweka vigingi, inapitia upya kuangalia ni kwa namna gani migogoro hii itaisha? Kwa hiyo, tutafika Kijereshi na Longalombogo ili kwenda kuangalia ni kwa kiwango gani tunaweza tukatengeneza mipaka ili kuhakikisha kwamba wanyama hawa hawaleti tena madhara kwa wananchi.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Serikali yenye kutia matumaini, nina maswali mawili madogo ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa eneo hili la Mkomazi lina barabara ambayo inaunganisha utalii wa ukanda wa juu na ukanda wa chini kwa maana ya barabara ya Hekicho – Kwekanda - Lugulua, je, Wizara hii iko tayari kukaa na wenzetu wa TAMISEMI kupitia TARURA ili waweze kuboresha miundombinu wageni waweze kufika kwa urahisi katika geti hili ambalo tunakusudia kulifungua?

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Wilaya Lushoto ina vivutio vingi vya utalii na vingi bado havijatambulika ikiwemo utalii wa maliasili lakini pia na utamaduni ikiwemo makazi yale ya Chifu Kimweri, Waziri uko tayari kuongozana nami kwenda Lushoto ili angalau waweze kuvibaini vivutio hivi viweze kugeuka kuwa fursa ya kiuchumi kwa wananchi wa Lushoto?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, baada ya kuwahakikishia ufunguzi wa lango hili, TANAPA watashirikiana na TAMISEMI kuona
namna kurekebisha barabara hii ambayo Mheshimiwa Mbunge anaomba kutoka Hekicho kwenda Kwekanda ili kuweza kufungua pia lango la utalii kwenye maeneo haya ya misitu.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusu kuvitambua vivutio vya utalii ambavyo bado havijatambuliwa, niko tayari kuongozana na Mheshimiwa Mbunge kwenda kuangalia vivutio hivi na kuviweka kwenye package ya pamoja kuhamisha watu wa TANAPA waweze kuvitangaza.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya niweze kuuliza swali la nyongeza kwa Waziri wa Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wananchi wa Wilaya ya Longido wanaoishi katika vijiji 32 vilivyopo Ukanda wa Magharibi unaokwenda mpaka Ziwa Natron waliungana wakatenga eneo la Hifadhi la Wanyamapori ambalo wameliita Lake Natron Wildlife Management Area, wakapita mchakato mzima na hatua zote za usajili ikabaki kipengele kimoja tu ambacho kipo katika dhamana ya Waziri ya kuwapatia user right yaani haki ya matumizi ya rasilimali ya wanyama pori katika eneo hili. Jumuiya hii imetumia rasilimali nyingi kupitia mchakato ambao wote mnaujua siyo wa bei nafuu na umetumia fedha za wafadhili na za Serikali, ni lini sasa Jumuiya hii itapewa user right wawe kuanza kulisimamia na kutumia rasilimali ya eneo hilo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali Dkt. Kiruswa, Mbunge wa Longido, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuna mchakato mrefu sana wa kusajili WMA na kama Mheshimiwa Mbunge ananihakikishia kwamba taratibu zote za awali zimekwishatimia, nitakwenda kufuatilia na kuona kama kipengele kilichobaki kinamhusu Waziri peke yake basi nitamshauri Mheshimiwa Waziri kutoa hiyo user right.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri kutokana na swali hili. Kwa sababu sasa Harvesting Plan imekamilika ina maana sasa Serikali inaenda kuanza kupata mapato kutokana na msitu huo. Hata hivyo, kama ilivyo watu wa baharini au ziwani, uchumi wao mwingi unategemea mali ya bahari na mali ya ziwa. Vilevile sisi tulio kwenye misitu uchumi wetu mkubwa unategemea mazao ya misitu. Sasa kwa nini Serikali mpaka leo hii ile cess haijapata kuongezwa kutoka asilimia tano tunayoipata kutokana na uvunaji huu wa misitu, angalau ifike asilimia 10 ili kuweza kuinua kipato cha Halmashauri tunazozunguka?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, TFS wamekuwa na tabia ya kutotoa ile responsibility kwa vijiji vyetu yaani ile incentive. Sio hivyo tu kuna mazao ambayo yamevunwa na wavunaji haramu ambayo yapo kwenye Halmashauri zetu kwa muda mrefu yanaendelea kuharibika. Je, Serikali haioni sasa inaweza kutoa kwenye Halmashauri husika yale mazao ambayo yamevunwa kwa haramu ili yaweze kunufaisha kwenye vijiji vyetu, kwa mfano mazao ya mbao, yanaweza kutusaidia kutengeneza furniture au viti, meza na madawati kwa ajili ya shule zetu na hospitali zetu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia tano ya cess ambayo TFS wamekuwa wakitoa kwenye Halmashauri, iko kwa mujibu wa Sheria ya Serikali za Mitaa ya mwaka 1982 na sisi kama Wizara hatuwezi kuibadilisha na hatuwezi kuikiuka. Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge kama anataka ibadilike anaweza kuanzisha mchakato huo, lakini kwa sasa maelekezo yetu ni kutoa asilimia tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, ni kweli kwamba maeneo ya Liwale kuna mbao nyingi ambazo zilikamatwa wakati wa Operation Tokomeza, na mbao hizo bado kesi zake ziko Mahakamani. Hata hivyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, mara uvunaji huu niliosema utakapoanza, tutawaelekeza TFS kuhakikisha kwamba wanatoa misaada kwenye shule zote ambazo ziko jirani na maeneo ya uvunaji.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwanza nianze kuishukuru sana Serikali kwa hatua iliyochukua kuhakikisha kwamba wanapeleka wanyama hawa pundamilia na swala ili kuongeza utalii katika eneo lile la Kitulo. Hata hivyo, nina swali dogo la nyongeza tu kwamba pamoja na hao ambao wanapeleka kwa kuwa wanyama kama twiga huwa wanaweza wakachangamana na wanyama hawa ambao wametajwa pundamilia na swala. Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza wanyama wengine nje ya hawa swala ama twiga ili waweze kuvutia watalii kwa kuwa watalii wengi wanapenda kuona twiga katika eneo lile?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ambalo pia niulize Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba barabara angalau inayoenda kwenye ile mbuga za wanyama ile barabara ya Chimala – Matamba inakuwa katika hali nzuri muda wote ili kuweza kuvutia utalii katika eneo lile? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Profesa Norman Sigalla, amefanya juhudi kubwa kuhamasisha Wizara kupeleka wanyama kwenye hii Hifadhi na lengo kubwa ni kujaribu kufungua Hifadhi hii ili iweze kuvutia Watalii. Pia nimpongeze kwa kweli kwa kusimama imara kuhakikisha kwamba hili zoezi linakamilika mapema.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba twiga, swala na pala wanaweza kuishi katika mazingira ambayo yanafanana, lakini kabla ya kupeleka wanyama kwenye Hifadhi ya Kitulo, Taasisi yetu ya TAWIRI ilifanya utafiti na kujiridhisha kwamba wanyama hawa wanaweza kuishi katika maeneo hayo na kwamba ikolojia zinafanana. Kwa hiyo ili tuweze kupeleka Twiga nitawaagiza watu wa TAWIRI waweze kufanya utafiti na kuona kwamba wanyama hawa wakipelekwa katika Hifadhi ya Kitulo wanaweza kuishi na hawatakuwa na madhara.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali lake la pili, ni kweli kwamba ili watalii waweze kufika maeneo ya utalii na kwenye maeneo ya Hifadhi, taasisi zetu zimekuwa siku zote zikitengeneza miundombinu kuruhusu watalii kuweza kufika maeneo hayo kirahisi. Maeneo ambayo tunayatengeneza ni yale ambayo kimsingi yako chini ya usimamizi wa Wizara yetu. Kwa hiyo nimhakikishie tu kwamba barabara zote ambazo ziko chini ya usimamizi wetu tutazitengeneza kuhakikisha kwamba tunahamasisha utalii katika Hifadhi ya Kitulo.
MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mimi ndiye mwakilishi wa wananchi wa Kijiji cha Igwata na Jimbo la Maswa Magharibi. Msitu huu ulipanuliwa na wakati wanapanua hawakushirikisha wananchi, ukamega mashamba ya watu. Sasa nataka niulize maswali ya nyongeza. Moja; kwa nini Serikali isirejeshe mashamba haya yaliyomegwa kwa wananchi ili waendelee kuyatumia kwa shughuli zao za kilimo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, sehemu ya mashamba au eneo lililomegwa kuna makazi ya watu, Serikali inasemaje juu ya watu hawa ambao wameweka makazi kwenye eneo ambalo limeongezwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mashimba Ndaki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimpongeze sana Mheshimiwa kwa namna ambavyo amekuwa akifuatilia sana malalamiko ya wananchi wake ambayo yalitokana na uwekaji wa alama. Sisi kwenye Wizara yetu kimsingi hatukuchukua mashamba mapya ila tuliweka alama, lakini naomba nimpongeze sana kwa namna alivyofuatilia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zoezi ambalo tunaendelea nalo sasa katika Wizara yetu ni kupitia upya malalamiko yote yanayoletwa na Waheshimiwa Wabunge pamoja na viongozi wa Serikali katika maeneo husika. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Mbunge kama uchukuaji wa eneo hili una malalamiko, Wizara yetu inapokea malalamiko hayo na tunatekeleza agizo la Mheshimiwa Rais la kuhakikisha kwamba, tunarejesha maeneo ambayo yana malalamiko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali lake la pili, iwapo kuna wakazi ambao wakati wa uwekaji wa mipaka hii walikumbwa na zoezi hili nitamtuma Afisa wetu wa TFS kwenda kuangalia. Iwapo itathibika kwamba, maeneo hayo wananchi bado wanayahitaji tuta-review mipaka ili kuweza kuwaachia waweze kukaa.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niulize swali la nyongeza. Wananchi walioko Urambo katika Kata za Senda, Ukondamoyo na hasa Kijiji cha Yueta wana matatizo makubwa sana ya migogoro ya ardhi kutokana na kupakana na Pori la Akiba la Ugawa na kuwasababishia kukosa nafasi ya kulima na kufanya shughuli zao za mifugo. Je, Serikali itakuja lini Urambo kutatua tatizo hili ili wananchi hawa wanaopakana na Pori la Ugawa wafanye shughuli zao za kilimo na mifugo kwa raha? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Margaret Sitta, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Mashimba Ndaki, tumeelekezwa kupitia upya mipaka na malalamiko ya wananchi kwenye maeneo ambayo Mheshimiwa Mbunge anasema. Kwa hiyo, katika zoezi hili linaloendelea namwomba Mheshimiwa Margareth Sitta kwa sababu, wanaoleta malalamiko haya ni Halmashauri na Mkoa, atuletee malalmiko haya na tutayafanyia kazi.
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona. Mheshimiwa Rais alipokuja Mkoani Morogoro kwa ziara aliagiza wananchi wa Mtaa wa CCT Mkundi ndani na Manispaa ya Morogoro wasibughudhiwe, lakini hivi sasa Maafisa wa Maliasili wameendelea kuwabughudhi wananchi wale. Je, ni kwa nini maafisa hawa wanapuuza agizo la Mheshimiwa Rais?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Minja, Mbunge wa Viti Maalum Morogoro, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Maafisa wetu wa Maliasili, kwa maana ya TFS, wamekuwa wakisimamia sheria hasa kuangalia mipaka ya kihalali ambayo ipo katika maeneo husika, lakini kama kuna maagizo ambayo yalitolewa na Mheshimiwa Rais kwamba, wananchi wasibughudhiwe, nitakwenda kufuatilia kuona ni kwa namna gani maafisa hao wanakiuka na tutatoa maelekezo.
MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili ya kumuuliza Mheshimiwa Waziri. Kwa kuwa, bado wananchi wa jimbo langu hasa wanaoishi kandokando mwa Mto Ruvuma wameendelea kupoteza maisha na kupoteza viungo vyao kwa kasi kubwa sana. Je, Mheshimiwa Waziri yupo tayari sasa kuendelea kutimiza makubaliano yetu ya kuchimba visima katika vijiji sita vilivyobaki ili wananchi wa maeneo hayo waweze kupata unafuu wa kuathirika na suala la mamba?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali langu la pili, Mheshimiwa Waziri anakiri kwamba, lipo tatizo kubwa, lakini tatizo lililopo ni kwamba, wenzetu wa TAWIRI ambao wanatoa vibali vya kuvuna mamba wanatoa idadi ndogo sana ya vibali, kama alivyoeleza ni mamba tisa, lakini takwimu zinaonesha katika eneo hilo pekee lina mamba zaidi ya 300. Je, yupo tayari kutoa vibali zaidi ili wananchi hao waweze kuondokana na tatizo hili kwa kuvuna mamba?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya Mheshimiwa Bwanausi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nitumie nafasi hii kumpongeza kwa namna anavyofuatilia haki za wananchi wake walioshambuliwa na mamba. Kuhusu swali lake la kwanza amesema tatizo la wananchi kushambuliwa na mamba bado linaendelea na palikuwa na makubaliano na Wizara yangu kupitia TAWA ya kuchimba visima. Kama makubaliano hayo yalifanyika na Serikali haina kipingamizi, nitawaelekeza TAWA kuhakikisha kwamba, makubaliano hayo yanatimizwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali lake la pili, ni kweli kwamba, kabla ya kuvuna mamba Shirika letu ya Utafiti la TAWIRI huwa linafanya utafiti kujiridhisha na idadi sahihi na kama idadi hiyo ni tishio katika eneo husika. Nitawaelekeza pia, TAWIRI wafanye upya utafiti na iwapo itathibitika kwamba, idadi ya mamba waliopo sasa ni tishio tutatoa tena kibali cha kuvuna mamba hao kupunguza athari kwa wananchi.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuunipa nafasi ili niulize swali moja la nyongeza. Sisi Babati tuna ziwa ambalo lina viboko na wavuvi wanapokwenda kufanya kazi zao wamekuwa wakiuawa na viboko hao, lakini hakuna fidia. Tulipohoji pia, hata kwa Wataalam wa Halmashauri wanadai kwamba, wavuvi wanakuwa wamefuata viboko hivyo, hawastahili fidia. Naomba nifahamu Wizara inatusaidiaje ili kujua kwamba, wavuvi wa Babati na wananchi wale wanastahili fidia au la?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gekul, Mbunge wa Babati, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli yapo matukio ya wananchi wa Babati kushambuliwa wao wenyewe na viboko, lakini pia mashamba yao kuharibiwa na mamba. Kimsingi wananchi wale wanastahili kupata fidia iwapo shambulio hilo litatokea nje ya eneo la makazi ya viboko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu ya sheria viboko hawa wanapokuwa katika eneo lao makazi
wanapomshambulia mtu inakuwa ni mtu ndiye aliyekwenda kuwavamia katika eneo lao. Nimhakikishie Mheshimiwa Gekul, iwapo kuna wananchi ambao malalamiko yao yapo na walishambuliwa nje ya eneo ambalo ni makazi ya viboko, Wizara yetu itachukuwa hatua ikiwa ni pamoja na kuagiza pia watu wa TAWIRI kufanya utafiti na kuona idadi ya mamba hao kama wanaleta tishio ili waweze kuvunwa.
MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ambayo sijaridhika nayo ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Serikali la kuzuia wanyama hai kusafirishwa nje ya nchi nina hakika lilikuwa ni zuri lakini lilikuwa linalenga wanyama hai wakubwa, sidhani kama Serikali ilikuwa inalenga vipepeo ambao ni kama wadudu. Wananchi hawa wa Fanusi wamekuwa wakifanya biashara hii ya kupeleka vipepeo nje ya nchi kwa muda na walikuwa wanapata pato zuri tu, karibu shilingi laki tatu mpaka nne kwa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi hiki ambacho Serikali imezuia biashara hii wananchi wamepata matatizo sana. Naibu Waziri mmepiga marufuku biashara hii kwa muda wa miaka mitatu ambayo inakwisha Mei mwaka huu. Je, baada ya muda huo Wizara itakuwa tayari kuwapelekea rasmi barua wanakijiji wa Fanusi ili biashara hiyo iweze kuanza?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Waziri mwenyewe alifika kwenye maeneo haya na alitembea pale kwenye Kijiji cha Fanusi na kuona wananchi namna walivyobuni na kuanza huu mradi wa kufuga hawa vipepeo. Aliahidi na kumwelekeza Mkurungezi Mkuu wa TFS apeleke wataalam ili aweze kuwasaidia wale wananchi kukuza ubunifu wao na pia kuboresha mazingira yale. Ni lini wataalam hao na uboreshaji huo utaanza? Nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Balozi Adadi Mohamed Rajab, Mbunge wa Muheza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba wakati tunazuia uuzwaji wa wanyama hawa hai nje ya nchi wapo wananchi wa vikundi mbalimbali walikuwa na vikundi vyao na walikuwa wanapata mapato na kulipa kodi kutoka na mauzo hayo. Hata hivyo, kama nilivyojibu kwenye swali langu la msingi ni kwamba ulitokea ukiukwaji mkubwa wa sheria na taratibu na Serikali ikaona itafute utaratibu mwingine wa kusimamia zoezi hili. Kama alivyosema itakapofika Mei, Serikali itatoa tamko sasa ni kwa namna gani tutaendelea na zoezi hili ili kutoaathiri kabisa shughuli hii hapo baadaye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili kuhusu Mheshimiwa Waziri kuagiza kupelekwa wataalam, ni imani yangu kwamba baada ya agizo la Mheshimiwa Waziri wataalam hao walielekezwa kwenda lakini kama bado hawajafika nitahakikisha kwamba wanakwenda kutoa elimu kwenye vikundi hivi ambavyo vinashughulika na biashara hii.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, napenda kuongezea ziada ifuatayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilifika katika Kijiji cha Fanusi, niliona jitihada za akina mama wale katika kikundi kile na niliona adha wanayoipata kwa Serikali kuzuia kusafirisha vipepeo nje ya nchi kutokana na ile blanket ban ambayo kama Serikali tuliitoa miaka mitatu iliyopita. Naomba kuweka sawa tu rekodi kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sasa hatutaruhusu tena usafirishaji wa wanyama hai kutoka nchini mwetu kwenda nchi yoyote ile na tutafanya mabadiliko ya sheria ili kuzuia jambo hilo lisitokee tena katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, utaratibu ambao tunaushauri kwa wananchi wote ambao wamekuwa wakifuga wanyamapori hawa watafute namna nyingine ya kupata faida kutokana na maliasili hiyo na siyo kutegemea kusafirisha kwenda nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa akina mama wa pale Fanusi niliwashauri Halmashauri na nikaagiza washirikiane na
TFS kutafuta namna ya kufanya shughuli ya utalii wa vipepeo katika eneo lile kwa sababu kwa kweli vipepeo walioko pale ni wazuri mno na watu wangeweza kwenda kuwaona pale na kingekuwa ni kivutio cha utalii na wangepata kipato ambacho walikuwa wanakitarajia. Kwa hiyo, huo ndiyo uelekeo, waondokane na mentality kwamba kuna siku tutafungulia vibali vya kusafirisha nje ya nchi kwa sababu tumezuia na hatutafungua tena.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninalo swali, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na faida ya watalii kuja kuona vipepeo, nimegundua watalii wengi wakishaona wanafanya identification na wanachukua sample za vipepeo na kuondoka nazo. Je, Serikali yetu imeshafanya utafiti wanaenda kufanyia nini hivyo vipepeo wanavyochukua ili kuhakikisha hatupotezi rasilimali ya Taifa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yussuf, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba watalii wengi baada ya kuona vipepeo hutamani kuondoka nao na baada ya kuondoka nao kitu ambacho tumegundua ni kwamba nao wanakwenda kufanya biashara ileile ambayo sisi tunafanya ili watalii waje Tanzania. Kwa hiyo, ni kwa sababu hiyo Wizara ikaona hamna sababu tena ya kuendelea kuuza wanyama hai nje ya nchi.
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Spika, ahsante, nina maswali mawili ya nyongeza. Vijiji vyenye mgogoro wa mipaka na Hifadhi ya Serengeti ni vijiji vinane, Kijiji cha Merenga, Machochwe, Nyamakendo, Mbalibali, Tamkeri, Bisalala na Bonchugu. Ukiona wananchi wa vijijini wameungana, wameenda mahakamani, wameishinda Serikali, halafu Serikali imekata rufaa ni kama kuwaonea na wananchi hawana shida na mambo ya rufaa.

Mheshimiwa Spika, Hifadhi ya Serengeti imeanzishwa kwa GN namba 235 ya mwaka 1968 na ikatengenezewa ramani iliyosajiliwa kwa registration namba 14154. Ramani hii imefichwa, imeanza kutengenezwa ramani nyingine na ndio kisa cha wananchi kushinda mahakamani. Sasa tunataka kujua kwa nini Serikali haitaki kwenda kukaa na wananchi wa vijiji hivi ili kukubaliana mpaka, sio kupoteza muda kukaa huko mahakamani na wananchi wanaumia. Kwa hiyo ni lini Wizara na Wizara ya Ardhi wataenda kukaa na wananchi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti ni kweli imekiri kwenye barua kwamba ilifanya makosa kwenye kutekeleza mipaka kwenye GN iliyoanzisha Pori la Ikorongo, wamekiri na wanahitaji utaratibu tu wa kwenda kurekebisha ile mipaka. Kwa nini Wizara pamoja na Wizara ya Ardhi wasiende kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti kwa ajili ya kurekebisha ile mipaka?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Marwa Ryoba Chacha Mbunge wa Serengeti kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali haiwezi kuwa na lengo la kuonea wananchi kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge anasema, lakini taasisi hizi zilipokuwa zinapitia mipaka na baada ya migogoro hii kuwepo na baada ya wananchi kushinda kwenye kesi yao ambayo walikuwa wamefungua, Taasisi kwa sababu ilikuwa inafahamu mipaka yake ya awali iliamini kwamba ikikata rufaa inaweza ikabadilisha matokeo. Kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi sisi Serikali baada ya kesi hii kwenye Mahakama ya Rufaa kuamuliwa tutatumia hukumu hiyo kuweka mipaka ambayo itamaliza mgogoro huu na kama mipaka hiyo itakuwa ni hii ya sasa ambayo vijiji vinatambua, hatuna pingamizi.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, kama nilivyojibu kwenye swali langu la msingi tutakwenda kupitia upya hii mipaka ya Ikorongo na kuweka alama kwa kutumia Wizara ya Ardhi pamoja na ushirikiano na Wizara yetu ili kumaliza mgogoro huu kwenye suala lake la pili.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Kabla ya maswali haya mawili ya nyongeza naomba kuitahadharisha Serikali katika jibu la msingi Serikali inasema kwamba watatoa vibali.

Katika suala la vibali bila shaka litaleta mazingira ya rushwa ili watu waweze kupata hivyo vibali na bila shaka litaongeza shida na watu wetu wataendelea kupata tabu sana.

Mheshimiwa Spika, swali langu la nyongeza la kwanza, ikiwa katika majibu ya msingi ya Serikali inakiri kwamba hali imeimarika ya watumishi na mambo ya udhibiti na mambo ya ukaguzi. Je, sasa Serikali haioni ikiwa hali imeimarika ni wakati muafaka wa kuondoa zuio hili ili kusudi mazao ya misitu yapate kusafirishwa muda wowote kadri mtu anavyotaka ku- speed up uchumi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa sababu wakati mwingine Serikali ina shaka sana na mbao pori na bahati nzuri Mheshimiwa Spika wewe ni mhifadhi. Je, Serikali iko tayari kuturuhusu sisi ambao mbao hizi, nguzo, mirunda zinatokana na miti ambayo tumepanda sisi wenyewe na siyo mbao pori. Je, Serikali iko specifically tayari kuruhusu kwa mbao ambazo zinatokana na miti ya kupandwa ziruhusiwe kusafirishwa muda wowote ambao mwananchi au mfanyabiashara anaona kwake ni muafaka ili ku-speed up uchumi kwa sababu Serikali iko kazini 24/7 masaa 24 siku saba, hakuna mahali Serikali imelala na inafanya ikaguzi kuna vituo, magari ya patrol. Je, Serikali iko tayari hasa kwa miti ambayo sisi watu wa Mafinga, Mufindi, Iringa, Njombe, Ruvuma tunapanda kwa nguvu zetu kuruhusu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza nakubaliana kabisa na Mheshimiwa Cosato Chumi kwamba tukiweka mazingira magumu ya upatikanaji wa vibali tutasababisha vibali hivi kutolewa kwa upendeleo na pengine kutasababisha kuchochea rushwa nakubaliana naye. Kutokana na sababu hiyo ndio maana tumesema kwa sasa tumefikia mahali huduma zimeimarika na tutaondoa zuio la usafirishaji wa mazao ya misitu kutokana na misitu ya kupandwa ambayo ilikuwa inasafirishwa mchana peke yake sasa kuanza kusafirishwa kwa masaa 24. Nafikiri hilo tayari katika majibu yangu ya msingi nilisema na tuko kwenye hatua za mwisho za kuondoa zuio hilo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tutaendelea kuwa na zuio kwenye mbao za misitu ya pori na hii ni kwa sababu ya kulinda kwanza misitu yenyewe ambayo inaelekea kutoweka, lakini pili kuendelea kuisimamia vizuri ili kupunguza udanganyifu. Hata hivyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ruhusa ya usafirishaji wa misitu ya kupanda ambayo nimeizungumzia ikiwa ni pamoja na mirunda na mazao yake tutaitoa hivi karibuni na hapatakuwa na masharti kwa mtu ambaye amekamilisha vibali.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri na yenye kujitosheleza ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba nikupe comfort kwamba suala hili tumeshaanza kulifanyia kazi hata kabla ya kupokea swali la kutoka kwa Mheshimiwa Chumi na tupo katika hatua za mwisho mwisho za kuweka utaratibu kwa ajili ya kufungua usafirishaji usiku wa mbao ambazo ni za kupanda.

Mimi binafsi sio muumini sana wa kuzuia watu wasifanye kazi usiku mara mabasi hayasafiri usiku, mara malori hayasafiri usiku, mbao hazisafiri usiku, tunachelewesha ukuaji wa uchumi.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo mtazamo wangu ni kwamba ili kutia chachu ya ukuaji wa uchumi watu ni lazima wafanye kazi mchana na usiku na ndio maana nimetoa agizo ndani ya Wizara kwamba walete ushauri wa kitaalam wa namna ambavyo tutaweka control ili kudhibiti uhalifu na vitu vingine lakini watu waruhusiwe kusafirisha mazao yao usiku.
MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza na kumshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya, lakini pia kwa kutuliza joto la wananchi katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa na mambo mawili makubwa ambayo nilikuwa nataka niishauri Serikali. Kwanza, nimwambie Mheshimiwa Waziri, sikusudii kumzungumza au kuwatetea wavamizi wa hifadhi hizo. Ila swali langu linalenga katika hifadhi zilizovamia vijiji vyetu, maana kesi ya watu wa Chalinze ni hifadhi imevamia vijiji.

Mheshimiwa Spika, la pili, nikushukuru na kukupongeza, naona leo umemwalika Bwana Pierre Liquid, ni jambo jema, lakini ushauri wangu naomba kwa Wizara, inapofanya kazi katika kuweka hivyo vigingi na beacons itushirikishe sana sisi wawakilishi wa wananchi ili tuweze kuwapa ushirikiano na kuwakumbusha vizuri ili wasije kuvuruga kabisa zoezi zima.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza, naomba nipokee pongezi hizo ambazo amempa Mheshimiwa Rais. Ni kweli kwamba hata kabla ya tamko la Mheshimiwa Rais maeneo haya yamekuwa ndani ya migogoro mingine kwa zaidi ya miaka 20; na yapo maeneo ambayo yalikuwa yana GN mbili; eneo lina GN ya uhifadhi lakini pia kuna GN ya kijiji au kata katika eneo la hifadhi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Rais alichokifanya ni kulifanya tatizo hili liweze kushughulikiwa.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la kwanza, amesema kwamba hifadhi ndiyo zimevamia maeneo ya vijiji. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama nilivyojibu katika jibu langu la msingi, baada ya kazi ya Kamati tutakwenda katika maeneo husika yote yenye migogoro na tutashirikisha wawakilishi wa wananchi, wakiwemo Wabunge na Madiwani, kuhakikisha kwamba eneo tutakaloliwekea mipaka halitakuwa na migogoro tena.
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza kabisa napenda niishukuru na niipongeze Serikali yangu kwa namna ambavyo imekuwa ikiwajali wananchi hasa wanaoishi vijijini na pia kuangalia namna gani ya kutatua matatizo ya wananchi. Pamoja na pongezi hizo za kupongeza Serikali yangu, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la kwanza; ni kwa kiwango gani Taarifa ya Wizara hizi ambazo zilikaa kama Kamati ambazo zimeweza kuja na ushauri namna gani ya kutatua matatizo ambayo hasa katika vijiji mfano katika Jimbo langu la Kavuu, vijiji vyangu ambavyo ni vijiji vya Ikopa, Itura, Luchima, Sentaunyenye, Iziwasungu, Kabunde na kwingineko?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; kwa kuwa tuna migogoro mikubwa katika kijiji cha Luchima na mpaka wa TANAPA kwa ajili ya mto wa Kavuu na nilikwishaleta maombi mwaka jana na TANAPA walikwishaanza kujenga kisima kwa ajili ya kupunguza mgogoro uliopo kati ya wananchi wa Kijiji cha Luchima pamoja na mpaka wao. Je, ni lini sasa hawa ndugu zangu wa TANAPA wataweza kumalizia kile kisima ili wananchi wangu wa kijiji cha Luchima waweze kuwa huru katika kufanya shughuli zao za kilimo na uvu vi bila kuingiliwa na askari wa TANAPA.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa sababu amekuwa akifuatilia kwa karibu sana suala la migogoro baina ya maeneo ya uhifadhi na vijiji ambavyo amevitaja. Naomba nichukue nafasi hii kuwajulisha Wabunge wote ni kwamba taarifa hii ambayo Wizara yetu pamoja na Wizara zingine imeshiriki, itakapokuwa tayari kutumika sasa baada ya maelekezo ya Mheshimiwa Rais tutashirikisha Wabunge na viongozi katika Serikali za vijiji vyote na Halmashauri kuangalaia mipaka mipya ambayo tutaiweka ambayo itaondoa migogoro hii ambayo imekuwepo kwa muda mrefu. Kwa hiyo, nimuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili kuhusu TANAPA kukamilisha mradi wa kisima cha maji, nawaelekeza TANAPA kwa sababu mradi huo walikwishaanza kukamilisha kisima hicho haraka katika mwaka huu wa fedha.
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, namshukuru pia Naibu Waziri kwa majibu mazuri na kwa kuwa Serikali sasa imekiri taarifa hizi, na tunafahamu kwamba siyo kila jambo linalojadiliwa na Jumuiya ya Afrika Mashariki zinakubaliana na tumeshaona kwamba ni tatizo. Je, Serikali inachukua tahadhari gani ili basi jambo hili lisije kutokea kwa sababu litakuwa na madhara makubwa?

Pili, iwapo Serikali ya Kenya itasimama kutekeleza mradi huo; Je, ni madhara gani makubwa ambayo yanatarajiwa hasa kiikolojia na athari zake katika mzunguko wa wanyama, yaani Wild West Movement? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimpongeze sana kwa swali lake zuri sana, kimsingi uhai wa Mto Mara ndiyo uhai wa Hifadhi ya Serengeti, na ikolojia ya Serengeti inaanzia katika hifadhi zilizoko nchini Kenya. Kwa hiyo, uwepo wa Mto Mara na uhai wa uhifadhi wa Serengeti ni kitu ambacho sisi kama Wizara tunakitilia kipaumbele sana, kwa hiyo, nampongeza sana kwa maswali yake mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la kwanza; Je, Serikali inachukua tahadhari gani tumewaelekeza TANAPA kuanza kufuatilia kwa karibu mienendo yoyote ile ambayo inaweza ikapelekea utekelezaji wa mpango huu, na kwa kuwa tunaamini kwamba sisi Serengeti ni Mbuga yetu ambayo tunaitegemea, pia tumewaelekeza kuangalia kama inawezekana kujenga mabwawa ya kuhifadhi maji ili pale utekelezaji wa miradi hii itakapofanyika wanyama wasije wakaathirika kwa ukame.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, ni madhara gani makubwa yanayotegemewa ni kwamba kimsingi wanyama tunaowaona Serengeti wengi katika msimu wao wa mwaka mzima huwa wanatembea katika nchi hizi mbili. Kwa hiyo, Wild West Movement ambayo huwa inatokea Tanzania, huwa inapita mpaka Maasai Mara. Kwa hiyo, iwapo ikolojia hii itaharibiwa, maana yake ni kwamba wanyama hawa wataacha sasa kuwa wana-cross border kuja Tanzania au ku-cross kwenda Kenya na matokeo yake utalii huu ambao ni urithi wa dunia unaweza ukaathirika.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa majibu haya yaliyotolewa na Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Mnamo mwezi wa pili mwaka huu wahifadhi wa Rwafi Game Reserve, walifyeka mazao ya wananchi wa kijiji cha King’ombe zaidi ya hekari 359 za mazao mbalimbali. Wakati wanafyeka agizo la Mheshimiwa Rais lilikuwa limekwishatolewa na sasa wananchi hawa hawana chakula. Je, Wizara ipo tayari kufidia chakula hicho walichofyeka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili chakula ni uhai na moja kati ya hitaji la msingi la maisha kwanini Wizara inafikiria kwamba kufyeka ni kusuluhisha migogoro inayojitokeza badala ya kutafuta suluhisho lingine?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimpongeze kwa sababu amekuwa akitoa ushirikiano mkubwa sana katika kutetea wananchi wanaoishi kando kando na maeneo ya hifadhi. Lakini taarifa kwamba mwezi wa pili mwaka 2019 askari wa Rwafi Game Reserve walifyeka mazao kwenye hekari 359, ndiyo nazisikia leo na iwapo ni kweli kwamba taarifa hizi zipo na zimefika katika Wizara yangu, basi Wizara itachukuwa hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili Mheshimiwa Mbunge anataka kufahamu kwamba kufyeka mazao ndiyo suluhu ya migogoro hii lakini pia athari zake kubwa kwa wananchi ambao watakosa chakula. Mheshimiwa Rais alikwisha toa maelekezo na askari wetu wote wanajua katika hifadhi zetu zote za Taifa ni marufuku kufyeka mazao ya wakulima kwa sababu mazao mengi ni ya muda mfupi na iwapo hili linaendelea kutokea naomba Mheshimiwa Mbunge tuwasiliane ili tuweze kuchukuwa hatua.
MHE. RUTH H. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Migogoro kati ya wananchi na hifadhi zetu ni ya muda mrefu kwanza ni-declare interest kwamba nilikuwa kwenye Bodi ya TANAPA, na wakati ule walitayarisha ramani ambayo wameainisha maeneo ambayo wanaweza kuwaachia wananchi na maeneo ambayo watawatoa wananchi kwa kuwapa fidia kwa sababu ya ikolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni kwanini Serikali haitumi hiyo ramani ya TANAPA ambayo walishaitayarisha kuweza kutoa suluhu ya hii migogoro kati ya wananchi na hifadhi ambayo imekuwa inaendelea kwa muda mrefu.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba migogoro hii ya maeneo ya hifadhi na vijiji imekuwepo kwa muda mrefu, na nadhani kama Mheshimiwa Mbunge anafahamu, wakati Mheshimiwa Rais anatoa maelekezo ya kutokuviondoa vijiji 366 ambavyo vinapakana na hifadhi. Vijiji hivi havikuwa vimeanza migogoro miaka ya hivi karibuni vingine vipo vimesajiliwa tangu miaka ya 70.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Tume Maalumm iliyoundwa na Serikali kupitia jambo, hili imegundua kuna vitongoji zaidi ya 800 ambayo vina migogoro pamoja na hifadhi zetu za taifa. Kwa hiyo, nimuombe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba ushauri wake huu wa kutumia ramani ambayo ilipendekezwa na watu wa TANAPA tumeupokea, lakini pia tuendelee kusubiri maelekezo ya Tume Maalum iliyoundwa kumaliza kabisa migogoro hii ya hifadhi.
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Pamoja na Serikali kuendelea kutatua mgogoro wa hifadhi, uko mgogoro mkubwa kando kando ya mapori yetu wanyama wakali tembo kusababisha vifo kwenye maeneo ya Mwalali, Kuyu na Matongo. Serikali ina mkakati gani sasa kutatua mgogoro mkubwa huu kwa sababu tembo wanaendelea kuzaliana, na wanaleta madhara makubwa katika maeneo yetu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nikiri kwamba baada ya Serikali kuongeza juhudi za ulinzi wa hifadhi na kudhibiti majangili, limekuwepo tatizo la wanyama wengi sasa kuanza kuvamia maeneo ya vijiji na maeneo mengi ambayo taarifa tumezipokea ni kwamba, wanyama kama tembo na wanyama wengine wamevamia mashamba na kuna maeneo ambayo wamesababisha vifo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ambayo Wizara imechukua, kwanza tumeimarisha kikosi chetu cha ulinzi lakini tunaelekea sasa kuanzisha vituo maalum kwa ajili ya ulinzi kwenye kanda. Katika maelekezo ambayo tumeyatoa, maeneo mbalimbali tuliyokwenda tumezielekeza halmashauri zote ambazo zinapakana na maeneo ya hifadhi kuhakikisha kwamba katika maombi yao ya watumishi wanaajiri Maafisa Wanyamapori ambao wataweza kufika kwenye maeneo yenye migogoro kabla sisi askari wetu hawajafika.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali ambayo yanaridhisha na yanakidhi swali langu, naomba niulize maswali mawili, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa mpaka sasa Bodi ya TAWA haijakabidhiwa rasmi uendeshaji wa shughuli hiyo ili waweze kutekeleza mipango waliyotarajia. Ni lini sasa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa itawakabidhi TAWA ili waweze kufanya kazi zao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari tuongozane siku ya Jumamosi akaone hali halisi ambayo naizungumzia? Ahsante?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mwanne Mchemba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba kumpongeza kwa sababu amekuwa akifuatilia kwa karibu sana kuimarishwa kwa bustani hii kama chanzo cha mapato cha Mkoa wa Tabora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa swali lake la kwanza, naomba kumhakikishia kwamba taratibu za kukabidhiwa kwa TAWA zimekamilika na ndiyo maana mshauri mwelekezi amepatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili, niko tayari kuongozana na Mheshimiwa Mbunge kwenda Tabora kwenda kuangalia bustani hiyo.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mpaka wa hifadhi wa Guruneti na Mto Rubana katika Vijiji vya Hunyali, Mariwanda, Kihumbu, Sarakwa na Mgeta lakini limekuwa tatizo la buffer zone inayotoka kwenye mto kuelekea vijijini na kuzuia watu kwenda kunywesha ng’ombe na malisho kwenye maeneo haya. Mheshimiwa Waziri alishatoa maelekezo ya mdomo lakini ni lini Serikali itapeleka sasa vigezo vya kisheria vya kuondoa eneo hilo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kweli kwamba kutokana na matatizo ya mwingiliano wa shughuli za kibinadamu na wananchi na hifadhi pamekuwepo na migogoro mingi ambayo sasa hivi kama ambavyo nimekuwa nikijibu maswali yangu mengi Serikali inayafanyia kazi. Nimkumbushe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba suala lake tumekwishalizungumza, tunasubiri maelekezo ya Kamati ambayo iliundwa na Mheshimiwa Rais itakapotoa maelekezo tutatengeneza buffer zone ambayo itaruhusu wafugaji kwenda kwenye mto kunywesha mifugo.
MHE. HAMIDU H. BOBALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mheshimiwa Naibu Waziri anajua kwamba kijiji cha Ruhoma, Jimbo la Mchinga kimevamiwa na tembo na wanakula mashamba ya wakulima. Nataka kujua hawa watu mnafanyaje kuwa-compensate gharama zile za mashamba yao kuliwa na tembo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nikiri kwamba, tatizo la wanyama kuvamia mashamba na makazi ya watu limeongezeka. Limeongezeka baada ya usimamizi wa maeneo haya yenye wanyamapori pia, kuimarika na watu waliokuwa wanafanya mauwaji ya wanyama kwenye hifadhi zetu kupungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili limesababisha pia, uharibifu mkubwa wa mazao kwenye maeneo mbalimbali. Lakini utaratibu upo kwamba, pale ambapo wanyama hawa wanapovamia eneo na kuharibu mashamba ya wananchi utaratibu umewekwa kwamba, afisa wetu wa wanyamapori apewe taarifa. Tunamuelekeza anakwenda pale anafanya tathmini na tathmnini ile inapofika katika Wizara yetu tunaelekeza kulipa mara moja.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Awali ya yote, niishukuru Serikali kwa kuliona hili na kupandisha hadhi Hifadhi ya Selous, lakini baada ya kupandisha hadhi au baada ya Serikali kuimarisha uhifadhi katika hifadhi zetu suala la wanyamapori limekuwa ni shida sasa hivi, hasa wanyama kama tembo. Wanyama hawa sasa hivi wanasumbua kwenye maeneo yetu na niliuliza swali hapa kuhusiana na Serikali kuleta Muswada pengine kupata fidia wakasema haiwezekani, lakini bado suala la kifuta machozi hakipatikani. Je, Serikali ipo tayari kutupatia fedha hizi mapema iwezekanavyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maliasili inapozungumzia utalii Kanda ya Kusini, bado napata changamoto. Mwaka jana tumepata fedha kuendeleza utalii Kanda ya Kusini, lakini Wizara hii inapozungumzia Kanda Kusini wanazungumzia Morogoro, Mbeya na Iringa, lakini Mkoa wa Lindi, Mtwara na Songea hautajwi. Je, Serikali kwa upande wake inapozungumzia kukuza utalii ukanda wa kusini unaamanisha mikoa ipi? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Kuchauka, Mbunge wa Liwale, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa namna ambavyo amekuwa akifuatia haki za wananchi wake hasa wanaoathirika na matatizo ya kuharibiwa kwa mali zao na kuhatarisha usalama wao na wanyama waharibifu kama tembo. Nilifanya naye ziara kwenye jimbo lake na tulifanya mikutano takriban mitatu na tulizungumza na wananchi hasa kwenye mgogoro wao wa mpaka na Selous.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, ni kweli kwamba tuliahidi hapa tutaleta marekebisho ya kanuni, kanuni zipo lakini Wizara yetu inazipitia upya ili kanuni hizo zinapokwenda kulipa fidia hiyo fidia iwe angalau na thamani kulingana na uharibifu uliofanywa kwa sababu zimekuwa za muda mrefu. Kanuni hizo zimekuwa ziko tayari na Mheshimiwa Waziri hivi karibuni alikuwa amealika wadau kuzipitia na mara baada ya wadau kupitia, tutazitangaza na zitaanza kutumia. Kwa hiyo nimwondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge ni kweli awali zilikuwa malipo yake ni kidogo, lakini tumezipita.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kuchelewa kwa kifuta jasho suala hili linahusisha taratibu na taratibu zinaanzia kwenye halmashauri yenyewe kwenye vijiji. Wataalam wetu wa vijiji wa kilimo wanapaswa kulifanya suala hili kwa haraka kwa kulipeleka kwa Afisa Wanyamapori wa Wilaya na baadaye linafika kwenye level yetu ya Wizara na kwa sababu ni la nchi zima, mara nyingi tumekuwa tukiangalia first in, first out. Kwa hiyo nimwondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, ni suala la utalii kusini, ni kweli imekuwepo tafsiri kwamba unaposema utalii kusini unamaanisha Lindi, Ruvuma na Mtwara, lakini tunapozungumzia kwenye Mradi wa REGROW ni utalii wa Nyanda za Juu Kusini. Sasa hivi Wizara yetu ipo katika hatua za mwisho za kuandaa utaratibu ambao tutafanya mkutano tena kama tulivyofanya na watu wa Nyanda za Juu Kusini ili kufungua utalii wa kusini kwa maana ya Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma. Kwa hiyo nimwondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge hatujasahau eneo hili, tunalifanyia kazi na Wizara inashirikisha wataalam kutoka vyuo vikuu mbalimbali katika kuangalia maeneo ambayo yanaweza kutuletea mafanikio ya haraka ikiwa ni pamoja na kufungua milango ya mikoa hii yote ambayo inapakana na bahari na hasa katika maeneo ambayo tuna mali kale nyingi kama maeneo ya Mikindani na Kilwa. Nakushukuru sana.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri na Mheshimiwa Naibu Waziri, napenda kuongezea majibu kwenye sehemu ya swali la Mheshimiwa Zuberi Kuchauka kwamba tunapozungumzia utalii Kanda ya Kusini, hatuzungumzii utalii wa Kanda ya Kusini ambayo ipo kwenye nyanda ya juu peke yake, tunazungumzia kusini kwa ujumla wake. Mradi wa REGROW pamoja na ku-include na pori la Akiba la Selous la zamani na sasa Nyerere National Park ambayo ipo kusini proper huku lakini pia imejikita kutengeneza Mji wa Iringa kama kama hub ya utalii, lakini mradi huu upo kwenye awamu hii ya kwanza awamu ya pili utatanua maeneo zaidi kwenye upande wa Kanda ya Kusini upande huo wa akina Mheshimiwa Zuberi Kuchauka.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo kuna miradi mingine mikubwa inayoendelea kule ikiwepo Mradi wa SECAD lakini pia ikiwemo mradi wa kukifanya Kisiwa cha Kilwa Kisiwani ile malikale iliyopo pale kama kivutio cha kipekee. Pale tumewaelekeza TAWA ambao kwa sasa tumewapa dhamana ya kuwaendeleza utalii kwenye eneo hili Kilwa Kisiwani, wanunue boti ya kitalii ambayo itakuwa ya first class na business class, lakini pia wawekeze kwenye lodge ya kitalii ambayo itakuwepo katika eneo hilo la kisiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna mradi mkubwa utakuja pale kama wananchi watatoa ushirikiano, kuna zaidi ya trilioni moja itawekezwa pale katika eneo la fukwe zilizopo pale kusini kuanzia Kilwa mpaka Msimbati na hivyo tunaamini utalii wa fukwe unaweza ukakua kwa kiasi kikubwa sana katika eneo lile kama wananchi watatoa ushirikiano ili tuweze kuilinganisha Hifadhi ya Taifa ya Nyerere na fukwe zilizopo pale kusini. Ahsante.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba niipongeze Serikali kwa dhati kabisa kwa juhudi zake za dhati za kuboresha utalii katika nchi yetu. Kama Mbunge, nimesikitishwa na kauli za baadhi ya Wabunge wa Upinzani kubeza juhudi za Serikali za kuboresha utalii na kuchochea kwa kutumia wasanii wa ndani. Niwaambie tu wasanii, Serikali ya Awamu ya Tano inatambua mchango wao mkubwa katika kuijenga nchi yetu. Kwa hiyo iwapuuze hao, hii ni tabia yao na ndivyo walivyo.

Mheshimiwa Spika, swali langu namba moja, maeneo au halmashauri nyingi ambazo zimezungukwa na National Park hawanufaiki na shughuli za utalii kwa kuwa hoteli zile zimejengwa ndani ya zile mbuga. Sasa je, Seriakli haioni sasa umefika wakati wa kuweka utaratibu wa kujenga hoteli zile za kitalii nje ya zile hifadhi ili wananchi wa maeneo yale waweze kunufaika kama kodi na vitu vinginevyo.

Mheshimiwa Spika, swali namba mbili, tunafahamu nyamapori ni tamu sana. Mtalii anapoona akatamani na akala, itavutia watalii wengi sana kuja hasa wa ndani. Je, Serikali haioni sasa umefika wakati iweke utaratibu wa kuweka vigenge vya nyama choma ndani ya mbuga zile ili mtalii anapoona nyama ile anaitamani halafu anaila sio aone, atamani, aondoke. Ahsante.
NAIBU WAZIRI, MALIAISILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza kipekee kabisa naomba nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mlinga, watu wengi wanapomuona hapa Bungeni huwa wanafikiri ni mtu wa vituko lakini nikuhakikishie Mheshimiwa Mlinga ni mfuatiliaji mkubwa sana wa masuala ya uhifadhi lakini na masuala ya kiuchumi yanayohusu wananchi wake na halmashauri yake. kwa hiyo nampongeza sana Mheshimiwa Mlinga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba hivi karibuni tumefanya mabadiliko ya Kanuni na tunaandaa Kanuni ili kuruhusu matumizi ya nyama ya wanyamapori kwa watu wengi na katika kufanya hivyo tunapitia upya kanuni ili tuweze kuruhusu uwindaji wa ndani lakini pia kufunguliwa kwa mabucha ambayo yatakuwepo katika maeneo mbalimbali na kuyasajili. Kwa hiyo, taratibu hizo zitasaidia pia kuhakikisha kwamba nyama hii ya wanyamapori inapatikana katika maeneo yote yaliyoko katika hifadhi na maeneo ya mapori ya akiba ambapo wafanyabiashara watataka kupeleka nyama hiyo.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili Mheshimiwa Mlinga anataka kujua maoni ya Serikali ni kwanini hoteli zisijengwe nje ya hifadhi. Nakubaliana na Mheshimiwa Mlinga kwamba hivi sasa kwa mfano katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, nafasi ya kujenga hoteli ndani zimejaa na uzoefu tulionao ni kwamba kadri hoteli nyingi zinavyozidi kujengwa ndani ndivyo uharibifu wa mazingira unazidi kuondoa uhalisia wa hifadhi yenyewe ya Serengeti.

Mheshimiwa Spika, tumekubaliana kwa sasa kwamba wawekezaji wote wapya tutawapeleka nje ya Hifadhi ya Serengeti na hifadhi zingine za Taifa ili kuvutia pia wananchi wanaozunguka maeneo hayo kuweza kujishughulisha na biashara ndogondogo moja kwa moja na hoteli hizo. Kwa hiyo, tunauchukua huo kama ushauri ingawa hauwezi kutumika hivyo katika hifadhi zote kwa sababu zipo hifadhi ambazo bado zina nafasi ambazo zimetengwa kwa ajili ya uwekezaji. (Makofi)
MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, nina swali moja dogo. Kwa mujibu wa United Nation World Tourism Organization mwaka 2018 dunia nzima imekuwa na watalii bilioni 1.4 ni kwanini Tanzania imeendelea kusuasua imeshindwa ku- capitalize kuwavutia watalii hawa kuja nchini ikizingatiwa kuwa watalii kutoka Israel na kutoka Ulaya hususan Ujerumani wamekuwa ni wale wale wanaokuja kutoka enzi za utawala uliopita?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza Mchungaji Msigwa ni Mjumbe wa Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa hiyo ninaamini kwamba kama ana mchango wowote utakaosababisha watalii waje nchini anaweza kuutoa kwenye Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la pili kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi tumetoka kwenye watalii 1,100,000 mpaka 1,500,000 watalii ni tofauti kabisa na mzigo wa mahindi kwamba unaweza ukaamka asubuhi ukawa na tani 10 kesho ukaleta tani 100. Wanahitaji maandalizi makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ikitokea leo Tanzania ikapata watalii 3,000,000 kwanza nafikiri takwimu wanazo, Tanzania kwa ujumla wake na hoteli zake zote hatujazidi vitanda 30,000. Sasa ikatokea leo tukapata watalii 2,000,000 kwa mpigo, Tanzania nzima itajaa watalii na inawezekana hata sehemu ya kuwapeleka hakuna. Lakini tunahitaji miundombinu. Katika nchi nyingi ambazo unaona zinapata watalii wengi, hakuna seasonal za utalii. Watalii wanafanya utalii mwaka mzima. Sisi katika kipindi kifupi cha mwaka tuna high season ambacho ndicho tunachopokea watalii 1,500,000 tunachofanya sasa hivi ni kuimarisha miundombinu, tunafungua barabara zipitike mwaka mzima, tunaimarisha usafiri tuwe na shirika ambalo linaweza likasafirisha watalii ndani na tunaendelea kuyafikia masoko na kuhamasiaha uwekezaji ili tuweze ku-accommodate idadi kubwa ya watalii ambao wanakuja nchini.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Msigwa kwamba idadi ya watalii wanaokuja sasa anaweza akawa ni yule yule kutokana na experience aliyoipata Tanzania nafikiri unafahamu kauli yetu ya Tanzania unforgettable kwa hiyo mtu anaweza kutamani kurudi mara kumi lakini tunaendelea kuyafikia masoko mengine nje na hivi sasa tunaendelea kufika Urusi, China, India masoko ambayo hatukuweza kuyazoea awali. Kwa hiyo naamini kwa muda mfupi ujao tutafikia watalii ambao anawataka Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naamini kwa muda mfupi ujao tutafikia watalii wengi ambao anawataka Mheshimiwa Mbunge.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Tunatambua na tunajua kuwa maliasili ni kitu muhimu sana katika ustawi wa Taifa letu la Tanzania na huchangia pato la asilimia 17 kutokana na utalii huo. Mkoa wetu wa Lindi ni miongoni mwa sehemu ambazo zinapitiwa na Selous ambayo sasa hivi ni Mwalimu Nyerere National Park.

Mheshimiwa Spika, sasa katika Mkoa huu wa Lindi, kuna tatizo ambalo lipo katika Tarafa ya Melola, Kata ya Milola na Tarafa ya Mkinga, Kata ya Mchinga ambalo hili ni Jimbo la Mchinga. Wanyama kama tembo wanaingia katika maeneo hayo hata Mbunge wa Jimbo hilo Mheshimiwa Bobali ana ushahidi juu ya jambo hili. Pia wanyama hawa wanapoingia wanaleta uharibifu wa mazao na vilevile wanasababisha baadhi ya watu kupoteza maisha yao.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatuambia nini au inawaambia nini wananchi hawa juu ya uharibufu huo ambao umetokea katika maeneo hayo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba majibu ya Serikali. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwa kweli naomba nikiri kwamba kutokana na mafanikio makubwa ya uhifadhi ambayo yametokea katika kipindi hiki cha Awamu ya Tano, migogoro mingi ya wanyama na binadamu imeripotiwa katika almost nchi nzima. Nakubaliana na Mheshimiwa Mama Salma kwamba katika maeneo ya Melola imeripotiwa sana kwamba tembo wanavamia makazi ya watu na kula mazao; lakini siyo huko tu, ni maeneo mengi, almost nchi nzima.

Mheshimiwa Spika, tumeafanya nini kama Wizara? Moja, tumeelekeza taasisi zetu zote ikiwemo TAWA, TANAPA, TFS na Ngorongoro kuimarisha vitengo vinavyo-respond na matukio haya. Wote tumewaambia wawe na kikosi ambacho kipo tayari. Hata hivyo, imetokea mara nyingi kwamba wakati wanyama wanakuwepo kijiji kingine, wakati mwingine tumeshindwa kuwahi. Naomba nitumie fursa hii kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba tumetoa maelekezo na suala hili tunalifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu fidia ya mazao, Wizara imerekebisha kanuni ili kuweza kutoa kifuta jasho na kifuta machozi kinachoridhisha. Kanuni hizo zimekamilika, tutahakikisha kwamba malipo haya yanawahi kwa waathirika ili kuweza angalau kuwafuta machozi na jasho kwa muda mu Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. ALMAS A. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya kitaalam kuhusu uUwanja wa Ndege wa Ipole nilitaka kujua sasa, je, lini uwanja unaopendekezwa katika mapori ya Ugala utamalizika?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nina swali la pili, Serikali ina mpango gani wa kuyatangaza maeneo ya Kwihara pamoja na yaliyokuwa makazi ya Marehemu Mirambo kwa ajili ya utalii? Ahsate sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Almas, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba kumpongeza Mheshimwia Almasi pamoja na kwamba ameuliza kwa niaba ya Mheshimiwa Joseph Kakunda, pia amekuwa ni mshauri mzuri na mdau mzuri sana wa mambo ya utalii. Kama nilivyojibu kwenye jibu letu la msingi ni kwamba tulisitisha ujenzi wa Uwanja wa Ndege ya Ipole kutokana na ushauri wa kitaalam tuliopata kutoka Wizara ya Mawasiliano. Tulielekeza Wilaya kuangalia eneo lingine ambalo linafaa kwa ajili ya ujenzi. Kwa bahari mbaya eneo lote linalozunguka maeneo hayo ni ardhi oevu na ni eneo ambalo ni chepechepe yaani wetland na imekuwa vigumu kupata eneo ambalo tunaweza tukajenga uwanja kwa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika Hifadhi mpya ya Ugala tunavyo viwanja viwili vidogo vya ndege, kiwanja cha Siri na kiwanja cha Muhuba ambavyo vipo kama takribani kilometa 100 kutoka uwanja wa Ipole ulipokuwa. Kwa sasa Wizara yetu imebadilisha hadhi ya Pori la Akiba la Ugala na kuwa Hifadhi ya Taifa, tumeelekeza TANAPA kuboresha viwanja hivyo ili viweze kutumika wakati wote kwa huduma ambazo zilikuwa zimekusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili ni mpango wa kuyatangaza makazi au maeneo ya kale ya Mtemi Mirambo. Kama tulivyofanya nchi nzima tumeelekeza maeneo mengi ya mali kale kuchukuliwa na Taasisi zetu zote zinazofanya utalii nchini. Eneo hili la Mirambo kama tulivyofanya kule Iringa tutawaelekeza TANAPA kuwekeza pale utaalam na nguvu ili kuhakikisha kwamba tunayahusisha katika product ya utalii kuwawezesha watalii wanaotua Tabora na maeneo mengine ya Mkoa wa Tabora kuyafahamu maeneo haya ya historia.
MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa wananchi wa Vijiji vya Myesi, Utimbe, Naliongolo na maeneo ya Mchoti wamekuwa wakipoteza maisha, pia kujeruhiwa kutokana na wingi wa mamba waliopo katika Mto Ruvuma. Serikali kupitia Bunge Tukufu ilishawagiza TAWA ili waende kuchimba visima kuwaokoa wananchi hawa kutokana na kutegemea Mto Ruvuma kwa matumizi ya maji yao. Je, Serikali inatoa tamko gani kuwaelekeza TAWA waende wachimbe visima hivyo haraka iwezekanavyo?
NAIBU WAZIRI WA WALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwanausi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nikiri kwamba itakuwa swali la tatu la aina hiyo nalijibu lenye uhusiano na wingi wa mamba kwenye maeneo mbalimbali ya Mto Ruvuma. Ni kweli kwamba kuna ongezeko la wanyama wa aina mbalimbali wakiwemo mamba na wamekuwa wakiathiri matumizi ya asili ya wananchi ya maji ya Mto Ruvuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliekeleza hapa kwamba katika ushauri tuliopata kutoka kwa wanasayansi wa Wizara yetu ni kwamba maeneo ambayo wananchi wanatumia yanaweza kuwekewa kingo maalum ili kuzuia mamba kufika na ushauri wa pili ilikuwa ni kuchimba visima kandokando ya eneo hilo. Kwa kushirikiana na Wizara husika, Wizara yangu ilizungumza na watu wa Wizara ya Maji na waliahidi kupeleka visima maeneo hayo. Naomba nichukue ushauri wa Spika kuwaekeleza tena TAWA kufanya tathmini na kupitia na kuona kama TAWA tunaweza tukafanya kazi ingawa kazi ya msingi kabisa ya kupeleka maji maeneo hayo itafanywa na Wizara ya Maji.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo :-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; kwa kuwa uharibifu wa mazingira umekuwa ni mkubwa sana katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa pamoja na Mkoa wa Geita kwa maana ya kwamba hifadhi za misitu zinatoweka kwa haraka sana kwa mfano Hifadhi ya Msitu ya Geita, Rwamgasa, Rwande na Miyenze inatoweka kwa haraka. Sasa je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kuweza kudhibiti hali ya uharibifu wa mazingira na utowekaji wa misitu unaofanyika kwa sasa katika mkoa huo wa Geita.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe haina maafisa wanyamapori, je, Serikali ipo tayari sasa kutupatia maafisa wanyamapori ili huduma yao iweze kuonekana kwa wananchi wa Wilaya ya Mbogwe, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kutumia nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa namna ambavyo amekuwa akiwasiliana na mimi kuhusu uharibifu wa misitu aliyoitaja; Misitu ya Rwamgasa na Rwande ambayo kwa ujumla imevamiwa sana na wachimbaji wadogowadogo na wakataji wa kuni na mkaa lakini tumeshirikiana nae kutoa maelekezo ili kuilinda. Kwa hiyo, naomba nimpongeze sana kwa juhudi hizo ambazo ameendelea kuzionesha.

Mheshimiwa Spika, uharibifu wa misitu ambao unaendelea karibu nchi nzima ni tatizo ambalo ningependa kulitolea maelekezo. Imekuwepo tabia ya Halmashauri nyingi kufikiri jukumu la kulinda misitu ni la TFS au Wizara lakini misitu hii mingi ipo kwenye maeneo ya Halmashauri na mingi ni misitu ya vijiji na Halmashauri na misitu michache inayosimamiwa na TFS inalinda vizuri. Kwa hiyo, nizielekeze tu Halmashauri zote nchini kuhakikisha kwamba zinashirikiana vizuri na maafisa wetu wa TFS kulinda na kudhibiti wanaoharibu misitu hii kwa kasi katika maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili la nyongeza amesema Halmashauri ya Mbogwe haina afisa wa wanyamapori. Na naomba tu nitumie nafasi hii pia kuwaambia Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe kwamba katika maombi yao ya watumishi tunawaelekeza Halmashauri zote ambazo zinapakana na hifadhi ambazo zimekuwa na historia ya migogoro ya wanyama na binadamu kuhakikisha kwamba wanaomba kuwa na maafisa wa wanyamapori katika halmashauri hizo kwa sababu hawa ni watu wa kwanza ku-respond na matukio ya wanyama waharibifu wanaoenda kwenye maeneo ya makazi ya watu.

Kwa hiyo, naelekeza halmashauri hiyo katika maombi yao ya watumishi ya mwaka huu waweze kuomba afisa wa wanyamapori.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa spika, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri na kwa kuonesha wazi kwamba kama Wizara wanatambua namna ambavyo Mji wa Mwanza una vivutio vingi na unaweza kuwa sehemu ya utalii kwenye nchi hii. Sasa nilikuwa na maswali mawili madogo ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa spika, moja ni kwamba pamoja na mazingira na vivutio vingi vilivyopo ni nini sasa mkakati wa Wizara kuhakikisha kwamba ili watalii waje ni lazima wapatikane watu wanaosababisha watalii kuja. Tunatambua ili watalii hawa waje wanatakiwa wawe na watu wenye weledi ambao vijana wamefundishwa kwa kuona maeneo ambayo tunaweza kuwa na ma-tour guide wazuri ni nini mkakati wa Wizara kuhakikisha vijana wengi waliopo Mwanza wanapatiwa mafunzo haya na kufanya kazi hii vizuri.

Mheshimiwa spika, la pili; tunatambua kwamba TTB tayari kushirikiana na Halmashauri ya Jiji la Mwanza pamoja na St. Augustine University wameanzisha Mwanza Tourism na kupitia mkakati huo tayari Wizara kwa maana ya halmashauri pamoja na Ubalozi wa Ujerumani wameanza ukarabati wa ile Gunzeki House ambayo iko pale Makoroboi itakayokuwa ni moja ya majumba ya maonesho ya historia pamoja na ile Gallostream Nini mkakati wa Wizara kuhakikisha maeneo haya yanapewa kipaumbele na kuwa moja ya vivutio katika Mji wa Mwanza, nakushukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Mabula kwa namna ambavyo tumekuwa tukishiriki kwa pamoja katika juhudi hizi za kuifanya Mwanza kuwa hub ya utalii wa Mikoa ya Kaskazini Magharibi. Tulikuwa nae kwenye kongamano hilo ambalo nimelisema na alishiriki kwenye kuchangia mambo mazuri sana ambayo Wizara inayafanyia kazi, kwa hiyo nampongeza sana.

Mheshimiwa Spika, ameuliza ni mkakati upi wa Wizara katika kuhakikisha kwamba tunapata washiriki wengi katika shughuli za utalii katika mikoa hiyo. Kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, Wizara katika nyakati mbalimbali imefanya mikutano na wadau katika Mkoa wa Mwanza na tumeendelea kufanya semina mbalimbali kupitia ofisi yetu ya idara ya utalii lakini pia kupitia TTB na hivi karibuni tutafanya mkutano mwingine kutathmini kikao tulichokifanya pale awali.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wito wangu tu ni kwamba naomba kuwakaribisha wadau wote wa utalii wa Mkoa wa Mwanza na watu walio na interest ya kufanya biashara ya utalii kama alivyosema mwenyewe, watalii wanaletwa na watu na watalii wanatafutwa lazima wawepo wapo Mkoani Mwanza wanaotafuta watalii. Sisi tutakuwa tayari kufadhili mafunzo hayo ili kuhakikisha kwamba tunapata watu wengi wanaoshirikiana na jambo hili.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili amezungumzia kuhusu ukarabati wa jengo lililopo Makoroboi na kwamba ni upi mkakati wa Wizara. Wizara yetu imeendelea kutoa utaalam katika maeneo haya na katika maeneo mengine kwa mfano pale Mkoani Iringa lilikuwepo pia jengo la mkoloni ambalo zamani ilikuwa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya lilikarabatiwa na kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha RUCO sasa hivi jengo hilo ndilo ambalo linaonesha makumbusho na historia mbalimbali ya Mkoa ywa Iringa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nawapongeza sana Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino kwa kuandaa kila mwaka Mwanza Tourism ambapo wamekuwa wakipeleka watu mbalimbali katika Kisiwa cha Saa Nane na kuwazungusha katika Jiji la Mwanza. Juhudi hizi tunaziunga mkono tutaendelea kushirikiana na Mkoa wa Mwanza.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri aliyoyatoa, lakini kwa kuwa circuit ya Kaskazini Magharibi ni circuit ya Kimkakati kwenye Serikali ya Awamu ya Tano hususan kwenye Sekta ya Kiutalii, napenda niongeze mambo yafuatayo ambayo tunayafanya na tunakusudia kuyafanya katika circuit hii ya Kaskazini Magharibi.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza, Serikali inawekeza kwa kiasi kikubwa sana kwenye miundombinu (hard infrastructure) kama vile Reli ya SGR ambayo itafika mpaka Mwanza, viwanja vya ndege; Kiwanja cha Ndege cha Mwanza kitakuwa cha Kimataifa na sasa hivi ujenzi unaendelea pale. Vile vile ukiunganisha na mtandao wa Viwanja vya Ndege vilivyopo katika circuit hii, Kiwanja cha Ndege cha Chato, Kiwanja cha Ndege cha Bukoba, Kigoma, Tabora pamoja na cha Musoma vyote vinafanyiwa first lifting ili kuhakikisha kuna ndege zinatua regularly katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, hiyo ni sambamba na mtandao wa lami. Pia tunawekeza katika softly infrastructures ambapo sasa hivi tumewaelekeza Chuo cha Taifa cha Utalii wafungue Tawi kwa ajili ya kuongeza idadi ya vijana ambao wanasomea mambo ya utalii, tour guiding, upishi na vitu vingine katika Jiji la Mwanza.

Mheshimiwa Spika, mbali na hayo yote, circuit hii ya Magharibi ina bahati ya kuwa na maziwa na mito na tumeona kwamba hii ni unique feature ambayo kama tukiitumia vizuri itaifungua kwa kasi sana circuit ya Kaskazini Magharibi ambapo kwa kuanzia, tumewaelekeza TANAPA na tayari wameshafanya manunuzi ya boti ambayo itakuwa ni luxury kwa ajili ya utalii, itakuwa inachukua watu 50 na itakuwa inazunguka kutoka spix gulf kwenye eneo la Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, inakwenda, ina-dock Mwanza, itakuwa ina-dock pale Kisiwa cha Saa Nane, Kisiwa cha Rubondo lakini pia kwenye eneo la Katete ambapo Hifadhi ya Taifa ya Burigi Chato inaanzia. Hii boti itakuwa ni luxury na itakuwa inatumia masaa takribani matatu na nusu mpaka manne kutoka Serengeti kufanya huo mzunguko wote.

Mheshimiwa Spika, tunakusudia boti hiyo itakuwa ni ya business class lakini tumewaelekeza pia TANAPA wawekeze kwenye manunuzi ya boti nyingine ambayo itakuwa economy class ambayo itachukua watu 300 kwa ajili ya kuwazungusha kwenye Ziwa Victoria ili kuvinjari katika Ziwa, lakini pia Visiwa vilivyoko pale na maeneo ya Hifadhi ambayo yanaungana moja kwa moja na Ziwa Victoria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilipenda kuongezea hayo. (Makofi)
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru nashukuru pia majibu ya Waziri kwamba amekiri kwamba Serikali haina Chuo inachotoa haya mafunzo, mafunzo yanayotoa ni ya swimming na snockling mafunzo haya ni muhimu sana kwa maisha ya watu wetu nchi yetu imezungukwa na bahari na maziwa na watanzania wengi wanatumia bahari na maziwa na mito kwa ajili ya kutafuta riziki zao.

Je, Serikali sasa haioni ni muda muafaka wa kuanzisha chuo na kama hawana walimu kutafuta walimu kuja kufundisha ili kuepusha maafa kama haya yaliyotokea Kilindini Kenya mtu amezama kwa siku saba hajatolewa katika bahari?

Swali la pili nchi yetu kama nilivyosema imezungukwa na bahari na mito na watu wetu asilimia kubwa ndiyo wanatumia bahari na mito kwa ajili ya kutafuta riziki zao.

Je, Serikali haioni sasa kwamba ni muda muafaka kutafuta vijana wakawafundisha risk who divers kwa ajili ya uokoaji zinapotokea ajali za baharini? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi ni kweli kwamba kama nchi hatuna chuo maalum kinachofundisha diving peke yake lakini vyuo vyetu vyote vya uvuvi ukianzia Nyegezi, Mbegani, Kunduchi na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa wanafunzi wote wanaosoma masomo ya uvuvi au masomo ya sayansi ya majini lazima wasome somo hilo kama sehemu ya masomo ya lazima ya kufaulu na katika jibu langu la msingi nimesema kutokana na uhaba wa wataalamu Serikali ilikwisha chukua hatua ya kupeleka wataalamu watatu nje ya nchi ili wataalam hao watakaporejea waweze sasa kulichukulia somo hilo kama somo muhimu kwa ajili ya kwanza shughuli ya utalii lakini pili kwa ajili ya uokoaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba umefika wakati ambapo suala hili tunalichukulia kwa uzito mkubwa na mara wataalam hawa watakaporejea watatoa mafunzo kwa vijana wetu na kwa watu wote wanaoshughulika na kuongoza watalii.
MHE. MBARAKA K. DAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nilikuwa na swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri anakiri kwamba Kisiwa cha Mafia ni maarufu na ni eneo zuri sana kwa ajili ya snorkelling, scuba diving na aina nyingine za uzamiaji:-

Je, Serikali itakuwa tayari sasa kuleta hicho chuo ikakiweka Mafia ili wananchi wa Mafia wanufaike nacho? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dau, Mbunge wa Mafia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye majibu ya nyongeza ya Mheshimiwa Yusuph; baada ya wataalam hao kurejea; na kwa sababu wataalam hao wametumwa na Serikali kwenda kuchukua masomo hayo maalum kupitia vyuo ambavyo vipo; ninachoweza kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge ni kwamba katika maeneo ambayo tutayapa kipaumbele ni pamoja na Kisiwa cha Mafia.
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, napenda nimshukuru Naibu Waziri kwa majibu yake nina maswali mawili ya nyongeza;

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye swali la msingi Kata za Isakamaliwa Mbutu, Igunga, Nguvumoja, Lugubu, Itumba na Igoweko kwenye Wilaya ya Igunga zimo ndani ya Mbuga ya Wembere na mimi nilizaliwa na kukulia humo na kuna migogoro mikubwa sana ya wafungaji wakulima pamoja na mbuga hiyo.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ni kwa nini ile Kamati ya Mawaziri iliyokuwa imeagizwa na Mheshimiwa Rais kupitia maeneo ya namna hii ili kutafuta suluhisho haikufika Igunga?

Mheshimiwa Spika, swali la pili ni lini Serikali itapima eneo hili kupunguza maeneo ambayo yamekosa sifa kuwapa wananchi, lakini maeneo ambayo yanahitaji kuhifadhi kama alivyoeleza umuhimu wake yaendelee kutumika?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa sababu amekuwa akifuatilia kwa umakini sana utekelezaji wa agizo la Mheshimiwa Rais kuhusu maeneo yote yenye migogoro na ambayo wananchi tayari wamekwishaanza kuyatumia lakini yamepoteza hadhi ya kuifadhi. Kwa ujumla wake pamoja na Wabunge wengine taarifa hii kama nilivyojibu kwenye Swali la Mheshimiwa Mipata iko mezani kwa Mheshimiwa Rais na tunasubiri maelekezo.

Mheshimiwa Spika, kwa kujibu swali lake la kwanza Kamati ilipewa mwezi mmoja kuwa imekamilisha taarifa ya nchi nzima na kwa kweli haikuweza kuzunguka nchi nzima kufikia maeneo yote, lakini kwa kutumia mfumo wa Serikali ambayo ipo kila sehemu kupitia Wakurugenzi, Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa, Kamati ilipokea maeneo yote yenye malalamiko ya nchi nzima. Kwa hiyo, ninachoweza kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge ni kwamba eneo hili pamoja na Kamati kutokufika katika eneo hilo, limo ndani ya mjadala ambao tuliuendesha katika Kamati ya Mawaziri Nane na majibu yatakapotoka itakuwa pamoja na eneo hili.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ni lini Serikali itaondoa maeneo ambayo yamepoteza hadhi ya uhifadhi. Yapo maeneo mengi nchi nzima yenye hali kama hii na ndiyo ambayo sasa hivi yamevamiwa na wananchi na tumeelekezwa na Serikali kuangalia kama yamepoteza hadhi tupendekeze kuyaachia ili wananchi waweze kuyatumia, pamoja na swali lake la kwanza tunasubii maelekezo ya Kamati ambayo Mheshimiwa Rais aliiunda.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge Kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Kafumu ambaye katika nyakati tofauti tofauti amewaleta wazee kutoka katika Kata zilizoathirika nami binafsi nimeonana nao na kuwapa ahadi kwamba maombi yao yamefika mahala muafaka na tutayashughulikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ili kuongezea kwenye majibu mazuri aliyoyatoa Mheshimiwa Naibu Waziri ni kwamba katika mchakato wa kuchora ramani upya ya Pori Tengefu la Wembere ili kulipandisha hadhi sehemu yake kuwa Pori la Akiba tutazingatia maombi ya wananchi wa Kata ambazo zimetajwa, eneo la pori la akiba litakalobaki litakuwa dogo zaidi kuliko hili la square kilometa zaidi 8,000 lililopo sasa. Lengo hasa ni kubakisha walau eneo dogo ambalo litakuwa intact na ambalo tutalilinda ipasavyo kwa ajili ya faida za kiuhifadhi na hiyo connectivity kati ya hifadhi zilizopo kusini na hifadhi ambazo ziko upande wa Kaskazini, maombi ya wananchi yatazingatiwa na kwa hivyo eneo ambalo wanaweza kulitumia kwa kufuga kwa kilimo na kwa makazi litabaki kwa wananchi na wataishi kwa uhalali kuliko ilivyo sasa wananyanyasika.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza. Kwa kuwa matukio haya yamekuwa yanajitokeza mara kwa mara hususan katika Kijiji hicho cha Kabukome; na kwa kuwa Serikali imetoa maelekezo kwa Halmashauri kwamba wananchi hawa waweze kuwasilisha madai yao ili waweze kulipwa kifuta jasho: Je, Naibu Waziri pengine baada ya Bunge hili kufika katika eneo hilo ili kuweza kushauriana pia na wananchi wa eneo hilo kuona ni namna gani ya kuweza kuzuia tukio hili lisiweze kuwa endelevu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa kuwa Kijiji hiki cha Kabukome kinavyoathirika inafanana sana na baadhi ya vijiji katika Jimbo la Ngara vinayopakana na Hifadhi ya Taifa ya Burigi - Chato, Kijiji cha Gwakalemela Kata ya Kasulu na Kijiji cha Rusumo Kata ya Rusumo kwa sababu matukio haya yamekuwa yakijitokeza mara kwa mara, anaweza akafika pia katika maeneo hayo kwa ajili ya kushauriana na wananchi wanaoishi katika maeneo hayo namna gani ya kuweza kuendelea kudhibiti uvamizi wa wanyama hawa hasa tembo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kumpongeza Mheshimiwa Alex Gashaza kwa kuwa mshiriki mzuri katika uhifadhi, amekuwa pia akitusaidia sana kurejesha mahusiano kati yetu na wananchi katika maeneo yanayozunguka pori la Burigi - Chato. Pia namshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Oscar Mukasa kwa sababu amekuwa akifuatilia sana haki za wananchi wake katika eneo hili ambalo wamepata mgogoro wa wanyama.

Mheshimiwa Spika, taratibu za kulipa fidia ndiyo zinazosumbua kwenye maeneo mengi. Inatakiwa mwananchi anapopata tatizo la kuliwa kwa mazao yake au kushambuliwa na wanyama, ndani ya siku tatu, kama ni shamba awe ametoa taarifa kwenye Serikali ya Kijiji; na Afisa wa Kilimo amekagua na kuwasilisha kwa Afisa Wanyamapori wa Wilaya. Afisa Wanyamapori au Afisa wa Kilimo wa Wilaya ndiye anayeleta taarifa hizi kwenye Wizara yetu nasi tunashughulikia.

Mheshimiwa Spika, kama ni shamblio la mauaji, Afisa wa Kijiji anatoa taarifa Polisi na Polisi na Daktari wanafanya postmortem na baadaye taarifa hizi zinafika kwenye Wizara yetu nasi tunaweza kulipa. Hata hivyo, sehemu nyingi taarifa hizi zinachelewa kufika, zinafanyika baada ya tukio kupita muda mrefu, kwa hiyo, wanapokwenda watu wa kufanya tathmini, wanakuta shamba lilishapata uoto mwingine wa asili.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba sisi Wizara yetu iko tayari kutoa kifuta jasho na kifuta machozi mara tu tukio hili linaporipotiwa ndani ya muda.

Mheshimiwa Spika, swali la pili la Mheshimiwa Mbunge, anaomba mimi Waziri nipate nafasi kwenda Jimboni kuweza kushirikiana kutoa elimu katika vijiji vya Benako, Kalemela na Kasulo, naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba niko tayari na nitafanya hivyo baada ya Bunge hili. (Makofi)
MHE. EDWIN M. SANNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Wananchi wa vijiji vya Chemchemi, Tampori, Iyoli kule Kata ya Kingale pamoja na Muluwa Kata ya Serya wamekuwa wakipata athari kubwa sana kutokana na wanyama waharibifu hawa tembo, almaarufu kule Zanzibar, Unguja ya Kusini kama ndovu.

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru sana Serikali, wameanza kufanya malipo ya vifuta jasho na vifuta machozi kuanzia mwaka 2016 kwa baadhi ya vijiji, lakini athari hizi zimeanza 2012, taratibu zote zilifuatwa na pia madai yakawasilishwa Wizarani.

Sasa Je, kuna mpango gani wa kufanya malipo ya maeneo yaliyoachwa tangu mwaka 2012 kwa watu wote na kwa maeneo yote ambayo yalipata athari?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sannda, Mbunge wa Kondoa Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba athari za wanyama zimeendelea kuwepo na kwa sasa hivi zimeendelea kusumbua nchi nzima. Labda tu nitumie nafasi hii kuwafahamisha Waheshimiwa Wabunge kwamba kabla ya miezi michache iliyopita, ilikuwa ni jukumu la TAWA peke yake kupitia kikosi cha KDU kwenda ku-respond na matukio ya wanyama waharibifu yanapotokea, lakini Wizara imefanya marekebisho kama ilivyo kwenye maelekezo na hivi sasa popote ambapo tuna Hifadhi ya Taifa au tuna pori la akiba iwe ni TANAPA au TAWA au ni TFS katika eneo hilo, wanawajibika ku-respond na wanyama waharibifu wanapotokea kwenye maeneo ya vijiji. Kwa hiyo, maelekezo haya tumeshayatoa kwenye Taasisi zetu zote hizi.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tulianza kulipa mwaka 2016 na hii ilisababishwa na kutokuwepo kwa kumbukumbu za kutosha huko nyuma. Mwaka 2018 peke yake Wizara yangu imelipa shilingi bilioni 1.6 kama kifuta jasho na fidia. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tatizo la kutokulipa huko nyuma pamoja na kumbukumbu lilikuwa pia ni tatizo la fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, mwaka huu peke yake mpaka leo tuna madai ya wananchi yanayofikia takriban shilingi bilioni 3.2 lakini mfuko wetu hauwezi kuzidi shilingi bilioni 1.6. Kwa hiyo, pale ambapo kumbukumbu zitaonyesha kwamba kuna wananchi bado wanadai, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara yangu itafanya mpango wa kulipa.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi ya kuuliza maswali ya nyoneza. Kwanza nipongeze Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri, lakini nitakuwa na maswali mawili, la kwanza kwa mujibu wa maelezo ya waziri, Wizara inafungua Ofisi za Kanda Mwanza pale zikijumuisha Idara ya Utalii pamoja na kodi ya utalii, lakini kuna taarifa kwamba TANAPA imegawa shughuli zake Kikanda, na moja ya Kanda hizo ni Kanda ya Kaskazini Magharibi na kwa mujibu wa taarifa tulizonazo ni kwamba uongozi wa bodi umeelekeza Ofisi za Kanda ziwe Bunda eneo ambalo ni jarani sana na Serengeti. Lakini ili kusaidia ukuzaji wa utalii kwenye maeneo ya Ukerewe, Saanane, Lubondo nakadhalika. Ni kwa nini Ofisi za TANAPA za Kanda hizi, Kanda ya Kaskazini Magharibi isiwe Mwanza ziliko Ofisi za Utalii pamoja na Bodi ya Utalii badala yake zipelekwe Bunda? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kama Mheshimiwa Waziri alivyosema Wizara tayari imetambua uwepo wa vivutio vya utalii na sasa inahitaji kuviendeleza na kuvitangaza. Sasa ili kufanikisha hili ni kwa nini wizara sasa isiwekeze pesa pale Ukerewe kwa ajili ya maandalizi ya miundombinu lakini pamoja na ku-train wadau mbalimbali wakiwemo hizi local groups ambazo zimekuwa zikibainisha vivutio hivi ili kama maandalizi sasa ya kukuza na kutangaza utalii ulioko kwenye Visiwa vya Ukerewe? Nashukuru sana.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninamshukuru kwa pongezi zake, kwa wizara ambazo amezitoa na kulidhika na majibu yake ya maswali ya msingi. Lakini Mheshimiwa Mkundi ameomba kufahamu kwamba TANAPA katika juhudi za kuboresha shughuli za kukuza na kusimamia uhifadhi na utalii wamefungua Ofisi Kaskazini Magharibi, lakini Ofisi hiyo wameipeleka Bunda badala ya Mwanza na ameshauri kwa nini Ofisi hiyo isikae Mwanza ambapo kuna Ofisi za TTB na Ofisi za utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakubaliana na ushauri wa Mheshimiwa Mbunge nitawasiliana na TANAPA na kuona sababu za msingi zilizowapeleka Bunda, lakini ninaamini kwamba ushauri wake ni wa msingi kwa sababu Mwanza bado ni kitovu cha Kanda ya Ziwa ambapo ingelikuwa rahisi zaidi kuwahudumia wateja kuliko Bunda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wake wa pili swali langu la msingi limejibu kwamba baada ya kuziimarisha vituo hivi vyote vya mali kale tunajielekeza sasa kwenye kushirikiana na taasisi zetu mbalimbali ambazo tutazikabidhi kwenye maeneo mengi ili ziweze kuviambatanisha vituo hivi pamoja vivutio mbalimbali vya utalii kama nilivyosema Saanane na Lubondo. Kwa hiyo, nimuhakikkishie Mheshimiwa Mbunge kwamba moja ya vituo ambavyo tutahakikisha kwamba vinapata pesa kwa ajili ya uendelezaji na kwa ajili ya kuviimarisha itakuwa ni Ukerewe ili kuhakikisha kwamba Kisiwa cha Kirewe kinatumika kama Kisiwa cha utalii katika Ziwa Victoria.
MHE. JAMES F MBATIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, mwaka 2014 Tanzania ilikuwa inashika nafasi ya pili kwa vivutio vya utalii kati ya nchi 133 vyenye kushindana kwenye ubora wa vivutio vya utalii duniani ambapo GDP yetu wakati huo ilikuwa ni asilimia 17 na miundombinu ya utalii ya vivutio ya kutoa ubora wa utalii ilikuwa tunashika nafasi ya 110 kati ya nchi 133.

Je, kwa mwaka huu Tanzania inashika nafasi ya ngapi kwenye ubora vivutio vya utalii duniani na tunashika nafasi ya ngapi kwenye miundombinu bora ya kuchochea vivutio bora vya utalii duniani? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASII NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba miaka hiyo 1984 anayosema Tanzania ilikuwa ni nchi ya pili kwa vivutio na bado ni nchi inayoongoza kwa vivutio vya utalii duniani na hivi karibuni nafikiri uliona mchakato wa kuingiza moja ya vivutio muhimu kabisa ambavyo vilikuwa vinatangazwa kwenye vivutio vya dunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake kimsingi ili niweze kulijibu vizuri na kufahamu takwimu zote ambazo amezisema ni kwamba lilipaswa kuwa swali la msingi lakini nimuhakikishie Tanzania bado ni nchi yenye vivutio bora na ni nchi ambayo katika Afrika ni nchi ambayo ina vivutio bora zaidi na katika dunia ni nchi ambayo ni huwa nadhani ni nchi ya pili baada ya Brazil.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, utafiti uliofanyika kati ya mwaka 2012 mpaka 2014 ulitoa taarifa kwamba Tanzania inashika nafasi ya pili kwa vivutio vya nature duniani. Kutokea kipindi hicho mpaka sasa haujafanyika utafiti mwingine wa kuweza kutupa position yoyote ile tofauti na ile ya awali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini matokeo ya katikati ya utafiti huu ambao unafanyika kila baada ya miaka mitano yalitoka Tanzania ilionekana imeshuka kutoka nafasi ya pili mpaka nafasi ya nane kwa vivutio vya nature duniani. Na sababu kubwa iliyosababisha Tanzania kushuka ilikuwa ni uharibifu wa mazingira pia ikiwemo uvamizi wa mifugo na makazi katika maeneo ya vivutio vya utalii vya nature. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kazi kubwa imefanyika katika Awamu ya Tano ya kuwaondoa wananchi ambao wamevamia maeneo hayo, pia kupandisha hadhi baadhi ya maeneo, ninauhakika watakapofikia conclusion ya utafiti huo baada ya miaka mitano ambao ni mwaka huu pengine matokeo ya nafasi ambayo Tanzania inashika katika vivutio vya nature inaweza ikawa imeongezeka zaidi. (Makofi)
MHE. ZAINAB N. MWAMWINDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Leo nasimama mara ya tatu katika Bunge lako Tukufu nikiikumbusha Serikali kuhusu barabara hii itokayo Iringa kwenda Ruaha National Park.

Mheshimiwa Spika, barabara hii urefu wake ni kilometa 104 na kama majibu ya Naibu Waziri alivyosema kwamba imetengenezwa kwa kiwango cha lami kilomita 14. Kwa masikitiko makubwa ninasikitika kwamba barabara hii kwa hizo kilomita 14 imejengwa na Marais wote wanne. Upembuzi yakinifu ulishafanyika na kila mwaka Serikali inapanga fedha za ujenzi wa barabara hii. Je, ni kwanini Serikali inapata kigugumizi kuikamilisha barabara hii?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Ruaha, barabara zote za ndani ni mbovu na wakati wa masika ni mahandaki, kiasi kwamba upitaji wake na watalii wanapata shida inapunguza pato la Taifa. Swali ni lini Serikali itapanga pesa kwa ajili ya kutengeneza barabara hii? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza nakiri kwamba katika jibu langu la msingi nimesema tumekwisha jenga kilometa 14 kati ya kilometa 130 ambazo zipo katika barabara hiyo, na barabara hiyo tayari imekwisha fanyiwa upembuzi yakinifu. Mheshimiwa Mbunge anafahamu juhudi za kilometa 14 ambazo zimekwisha fanyika sio haba. Lakini anafahamu yeye ni mjumbe wa Kamati ya Maliasili, tumekuwa naye katika ziara juhudi za Wizara yetu katika kuhakikisha kwamba barabara hizo zinajengwa ni kubwa, nimuombe awe na imani na Serikali kama yalivyo maeneo mengine barabara hii itajengwa.

Mheshimiwa Spika, swali lake kuhusu ubovu wa barabara zilizopo ndani ya Ruaha ni kweli, pamekuwa na tatizo la ubovu wa miundo mbinu mbalimbali katika hifadhi ya Ruaha. Lakini nimesema katika jibu la msingi tunao mradi mkubwa REGROW, ambao tayari tulikwisha saini mkataba na umeanza kutekelezwa, Barabara zote pamoja na miundo mbinu mingine katika hifadhi ya Ruaha imo katika mkataba huo.

Mheshimiwa Spika, na nimhakikishie kwamba wakati kutengeneza mkataba huo maeneo yote haya ambayo yamekuwa yakisababisha hifadhi hii kushindwa kutumika wakati wa masika yatakuwa yamefanyiwa matengenezo makubwa na moja ya eneo ambalo Wizara yetu imehakikisha kwamba inaipa kipaumbele kufungua utalii maeneo hayo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ninafahamu juhudi zake kubwa za kupingania utalii maeneo ya Mkoa wa Iringa na kusini kwa ujumla lakini nimhakishie kwamba Serikali inalitilia maanani suala hilo.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, nashukuru katika hifadhi ya Ruaha tatizo sio barabara tu, hata Mto Ruaha mkuu ambao ndio kitovu cha hifadhi ya Ruaha, unatanuka na unakauka kwa baadhi ya vipindi hali ambayo inahatarisha maisha ya wanyama na inahatarisha hifadhi nzima yenyewe kutoweka kabisa. Sasa Serikali inachukua hatua gani kuona kwamba ule mto hautanuki na maji yanaendelea kutitirika katika kipindi cha mwaka mzima ili wanyama wetu waendelee kuhuika katika hifadhi ile?
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza ni kweli historia inaonyesha Mto Ruaha ulikuwa una flow maji yake kwa mwaka mzima na kwa miaka ya hivi karibuni umeendelea kuwa na tabia tofauti kwa maana unapoteza maji katika kipindi cha miezi miwili mpaka mitatu kwa mwaka. Lakini sababu zinafahamika ikiwemo pamoja na matatizo ya taabu ya nchi lakini pia matumizi makubwa yanayofanywa na wakulima walioko kwenye mabonde yaliyoko juu Mto Ruaha.

Mheshimiwa Spika, katika mradi wetu wa REGROW moja ya maeneo ambayo yanaenda kushughuliwa ni pamoja na elimu kubwa itakayotolewa kwa wakulima hao. Lakini miundombinu ambayo itatengezwa ili kuwafanya wanaotumia maji kwa ajili ya kilimo katika maeneo hayo iwe ni miundombinu ya kisasa ambayo itaruhusu flow ya maji kuendelea kuwepo, kuliko hivi sasa hivi wakulima wanazuia maji na kuyaweka kwenye mabwawa ya akiba kwa mwaka mzima hata kama maji hayo hawayatumii. Kwa hiyo, mpango huu kwa ajili mto huo tunao katika mradi wetu mkubwa.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante pamoja na kadhia hiyo, Serikali imekuwa ikichukua muda mrefu sana kulipa fidia na kifuta machozi lakini gharama hiyo pia haiakisi gharama ya uharibifu unaofanywa.

Je, Serikali ipo tayari kubadili kanuni zake kwa kuongeza gharama za kifuta machozi?

Mheshimiwa Spika, binafsi nimekuwa nikichukua hatua ya kumpigia simu Meneja wa TAWA Maswa Game Reserve lakini amekuwa haonyeshi ushirikiano wowote.

Je, Serikali ipo tayari kuwapatia mizinga wananchi katika vikundi katika Kata ya Lukungu, Mwakiloba, Kilejeshi na Wilaya zote za Mkoa wa Simiyu ili kuweza kukabiliana na tatizo la tembo hao?
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ni kweli yamekuwepo malalamiko ya muda mrefu ya kiwango kidogo cha kifuta machozi na kifuta jasho ambayo yamekuwa yakitolewa na Wizara yangu. Lakini nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara yangu inapitia upya viwango hivyo, na mara itakapokamilisha tutatangaza na kuwajulisha waathirika tumefanya marekebisho na nina imani ingawa haiwezi kulipa thamani halisi ya maisha ya mtu na mazao yaliyoharibika lakini itakuwa imeongeza kiwango ambacho tumekuwa tukitoa kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili nimefahamu kuwa Mheshimiwa Leah Komanya amekuwa akipiga simu mara kwa mara kutetea wananchi hasa wakati mazao yanapokuwa yamefamiwa na wanyama. Nimhakikishie tu kwamba huyu afisa ambaye hatoi ushirikiano tutampa maelekezo, lakini nitoe maelekezo kwa maafisa wetu nchi nzima kuhakikisha wana-respond haraka sana wanapopata taarifa za uwepo wa wanyama.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu sasa hivi wanyama hawa wameongezeka baada ya kudhibiti ujangili kwa kweli limekuwa ni tatizo lipo nchi zima. Kwa hiyo, niwaelekeze maafisa wanyamapori popote pale walipo kuhakikisha kwamba wana wajibika haraka wanapopata taarifa hizi ili kuweza kutoa ushirikiano kwa wananchi. Na nimhakikishi tutawasiliana ili tuweze kuona namna watakavyoweza kutoa mizinga hii ya nyuki katika maeneo ya vijiji hivi.
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Wilaya Bariadi kama ilivyo wilaya ya Busega, Bunda na Serengeti ni miongoni mwa Wilaya au maeneo yanayopakana na Hifadhi ya Serengeti. Lakini kikosi dhidi ya ujangili ofisi zake zipo Bunda na ofisi hiyo ndio inahusika na malipo ya kifuta jasho na kifuta machozi. Imekuwa ni shida sana kwa wananchi wanaotoka nje ya eneo la Bunda kama Baridi na baya zaidi wanapokuja kufanya malipo haya wanakuja kulipia malipo haya kwenye guest house.

Je, ni lini Serikali itafungua ofisi ya KDU mjini Bariadi ili kuondokana na adha hii hasa kwa akina mama ambao hawapendi kwenda guest house kwenda kupokea malipo yao?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba ofisi yetu ya KDU kwa sasa kikosi cha ujangili ipo Bunda na ni kwa sababu tuliamini kwamba Bunda ni katikati na eneo la Serengeti. Lakini nimhakikishie kwamba eneo hili analo lizungumzia yeye la Bariadi linapakana na Maswa, tunao maafisa wetu wa wanyamapori na tunaye afisa wa wanyamapori katika Maswa Game Reserve na wengine.

Mheshimiwa Spika, tutakachofanya ni kuwaelekeza hawa watu wa KDU wahakikishe kwamba wanakuwa na mawasiliano ya haraka na watu wetu wa halmashauri ambao kwa utaratibu ni watu wa kwanza wanafika maeneo ambayo mazao yameharibiwa kabla ya maafisa wa KDU kufika ili kutupa taarifa na kuweza kurahisisha mfumo wa malipo. Kwa hiyo, tumechukua ushauri wake wa kuwa na ofisi Bariadi, na tutakapo liangalia suala hili kulingana na uwezo wetu tutalizingatia.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa muda wa miradi hiyo kutokukamilika umekuwa mrefu sana, je, Serikali iko tayari kupeleka pesa ya kutosha ili miradi hiyo iweze kukamilika?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kwa kuwa Makao Makuu ya Wilaya za Kibondo na Kakonko upatikanaji wa maji umekuwa ni wa kusuasua, na wilaya hizo zina watu wengi kutokana na ongezeko la watu wengi wakiwemo wakimbizi, na zipo taasisi nyingi ambazo ziko pale zikiwemo hospitali, shule pamoja na ofisi za mashirika ya wakimbizi. Ni lini sasa Serikali itapeleka pesa katika Wilaya za Kakonko na Kibondo kumaliza tatizo la maji katika miji hiyo mikuu ya wilaya hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kutumia nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa juhudi zake kubwa za kuhakikisha kwamba anapigania akinamama wa Wilaya za Kakonko na Kibondo waweze kupata maji safi na salama na yenye kutosheleza.

Mheshimiwa Spika, katika jibu langu la msingi nimesema kwamba Serikali itatoa pesa ili iweze kukamilisha mradi ambao ulikuwa umekwama na tayari kazi hiyo imekwishafanyika, na sasa hivi Wizara inakamilisha taratibu ili kazi ambayo ilikuwa inasababisaha miradi hiyo isikamilike iweze kukamilika.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili, naomba kumfahamisha kwamba katika Wilaya ya Kibondo, tayari Serikali ilipeleka pesa shilingi milioni 500 kwa ajili ya mradi wa maji, na katika Wilaya ya Kakonko taratibu zinaendelea ili waweze kupatiwa pesa kwa ajili ya kukamilisha, tunafahamu kwamba eneo hili lina watu wengi, na hasa wakimbizi kama alivyosema.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kweli jibu limekuwa la ujumla sana nipende tu kusema kwamba Kata za Bendera, Ndungu, Kihurio zina ukame mkubwa sana na hata hivi tunavyoongea hakuna hata msitu mmoja ni Kata ya Maore tu ambayo ina kamsitu kadogo kaasili.

Swali langu la pili ni je, Serikali iko tayari kusaidiana na wanavijiji kutenga maeneo kisheria ambayo yatakuwa ni misitu ya vijiji badala ya kusema halmashauri inafanya wakati hatuoni kwamba sehemu hizi zinatendewa haki kwa kuotesha miti ambayo itapunguza ueneo wa jangwa katika eneo hili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi kwamba zoezi hili limekuwepo la uhamasishaji wa upandaji miti na Wizara yangu ina mkakati wa katika mwaka 2016 – 2021 kupanda miti milioni mia mbili na themanini katika maeneo mbalimbali ya nchi. Tumechukua mapendekezo ya Mheshimiwa Mbunge kwenda katika eneo husika kwa kushirikiana na Serikali za vijiji ili vijiji vyenyewe vitoe ridhaa ya maeneo ambayo vinataka tuyatenge na kuyachukua na kuyaboresha kwa ajili ya misitu hiyo lakini uzoefu unaonesha sehemu nyingi ambazo tumekwenda baada ya kuyachukua maeneo haya na kuyaboresha wanavijiji tena wamerudi na kuyadai maeneo haya waweze kurejeshewa. Kwa hiyo, kama Mheshimiwa Mbunge yuko tayari kutoa ushirikiano Wizara yangu itakuwa tayari kutoa ushirikiano huo wa kwenda kuhamasisha upandaji miti katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, lakini katika swali lake la pili tutatuma wataalam wetu katika Wizara yetu kwenda kuangalia uwezekano wa kuanzisha vitalu vya miti katika Kata hizo alizozitaja Mheshimiwa Mbunge.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN Mheshimiwa Spika, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawli ya nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, ametaja vituo vya Mafia, Dar es Salaam na Tanga ambavyo vinatoa mafunzo ya elimu hii; nilikuwa nataka kujua vinatoa mafunzo kwa kiwango gani? Wanatoka Ma-diving instructor, diver masters au wanafunzi wa kiwango gani wanaotoka katika vituo hivyo vya kufundishia?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; siyo tu kwamba ile mitetemo wanapolipua wale wavuvi inawatisha na inawasumbua wale Ma-divers wanapokuwa chini ya maji lakini pia eneo ambalo limepigwa lile bomu huwa linaathirika sana na kupoteza ule uhalisia wake kiasi kwamba mpaka rangi ya eneo lile huwa inabadilika. Je, Serikali ina mpango wowote wa kufanya utafiti kuona ule uoto wa asili unarudi pale yale Matumbawe yaliyoharibiwa kwa muda wa miaka mingapi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kimsingi kwa mujibu wa swali lake la kwanza, mpaka sasa hatuna vyuo ambavyo vinatoa vyeti maalum lakini tuna vituo ambavyo vinatoa mafunzo kwa ajili ya kusindikiza watalii wanaokuja kwa ajili ya uzamiaji. Katika vyuo vyetu vyote vya Mbegani na wapi hatuna certificate maalum kwa ajili ya divers au snorkel au nini ambayo inatolewa katika maeneo hayo. Wanapata uzoefu kutokana na wale ambao wamekuwa waki-practice kwa muda mrefu kwahiyo vituo hivyo ndiyo nimevitaja katika jibu langu la msingi.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili amesema kuna utafiti gani unafanyika kujua athari zinzaotokana na ulipuzi; ni kweli kwamba milipuko inapolipuka ndani ya maji uharibu kabisa maumbile ya Dunia ndani maji na hasa Matumbawe ambayo ndiyo kivutio kikubwa cha wazamiaji na maeneo yote baharini na kimsingi maeneo haya ambayo yamekuwa ukifanyika uzamiaji yamekuwa ni maeneo yanayolindwa na kwa mfano, ukienda kule Mafia kuna kikosi maalum ambacho kinalinda maeneo hayo na kina patrol maalum. Kwa hiyo, uzoefu wa maeneo hayo kushambuliwa na wazamiaji haupo, kwa hiyo nimuhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba katika maeneo ambapo tunapeleka watalii kwa ajili ya shughuli hii ni maeneo ambayo yanalindwa na kusimamiwa vizuri na hakuna uwezekano wa matumizi ya mabomu.

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba tena ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kuongezea kujibu swali la Mheshimiwa la Mheshimiwa Yussuf kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza vilevile Mvuvi mwenzangu Mheshimiwa Kanyasu kwa majibu yake yale ya awali. Lakini pia nieleze tu kuwa katika chuo Kikuu cha Dar es Saalam katika kozi ya Aquatic Science moja ya jambo la msingi kabisa kwenye kozi ile watu wanafundishwa kitu kinachoitwa swimming and snorkeling.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, swimming and snorkeling mtu anayekwenda kupata shahada ya swimming mathalani mimi mwenyewe hapa ni lazima unafundishwa namna ya kuweza kuogelea na kuweza kuingia kwenye maji kwa muda mrefu na ndipo upate degree yako. Lakini kama haitoshi alivyosema Mheshimiwa Kanyasu kuwa Ndegani wanao utaratibu ambao wanashirikiana hasa na Mamlaka ya Bahari Kuu ambapo wanafundishwa pale kwa muda mfupi nakupewa udhoefu. Wataalam wetu ambao wanakwenda kuwa observer’s watazamaji katika meli hawa pia wanafundishwa namna hata ya ku-dive.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili la Matumbawe ni conservation, Matumbawe yanachukua si pungufu ya miaka 50 hadi 100 yale ambayo yamevunjwa na mabomu, kwa hivyo kitu pekee ambacho sisi wataalam wa Sayansi ya Majini tunachokifanya ni kuhakikisha kuwa maeneo yaliyoharibiwa namna hiyo yanakwenda kuhifadhiwa tumefanya jitihada kubwa kwa kupitia mradi wetu mkubwa unaitwa sea offish ukanda wa Pwani ambapo kuanzia Tanga kule MOA mpaka Mtwara maeneo ya Mtwara mwishoni kule tumekuwa na huo mradi ambao tunadhibiti na kuyalinda maeneo yetu ya miamba na tumeonesha mafanikio makubwa sana katika Wilaya ya Kilwa, hivi sasa hata mazao yanayopatikana katika miamba ile kwa maana ya Matumbawe yameongezeka kwa kiasi kikubwa sana.
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nakushukuru Tanzania imebarikiwa kuwa na vivutio vingi na pamoja na vivutio hivyo bado iko nyuma sana kwenye Utalii kwa mfano Utalii wa fukwe kuliko nchi za wenzetu waliotangulia Kenya, Msumbiji na Zanzibar.

Sasa nataka kufahamu ni lini Serikali yetu itayazingatia na kuyapa umuhimu kipaumbele maeneo ya Coco Beach na kuona kwamba yanaendelezwa ili yaweze kufikia malengo hayo na kuleta watalii wengi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili ningependa kufahamu kwamba kwa mfano nchi zinazoongoza kwa kupokea watalii wengi kwa mfano Swaziland, USA Brazil na nchi nyingine za jirani zimewekeza katika aina mbalimbali za Utalii kwa mfano vitu vingine Mheshimiwa Waziri amevitaja kwa mfano, Cable car ikiwemo nchi jirani ya Rwanda balloons.

Je, ni lini sasa Tanzania itaona kipaumbele na kuwekeza katika maeneo hayo ili kuwepo basi kwa mfano kule Kilimanjaro Cable cars watalii waweze kuja wengi na kuliingizia pato nchi yetu ya Tanzania? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Amina Mollel kwa sababu katika maswali ambayo nimekuwa nikijibu hapa nimeshajibu maswali yake matatu yote yakihamasisha uhifadhi na Utalii nakupongeza sana Mheshimiwa Amina Mollel. Kama nilivyojibu ni kweli kwamba Tanzania tumekuwa na Utalii wetu wa asili ambao umezingatia sana safari kwa maana ya kutembelea mbuga za wanyama na maeneo mengi ambayo yamepatia nchi nyingine pesa nyingi za kigeni kama Utalii wa fukwe na aina nyingine za Utalii kwa kweli zimekuwa hazikuzingatiwa.

Mheshimiwa Spika, sasa ili kufikia katika malengo hayo Wizara imeliona hilo tuliunda kikosi kazi maalum cha kutafiti kwa nini Tanzania imekuwa nyuma katika Utalii wa fukwe na tukagundua kwamba palikuwa na udhaifu katika usimamizi wa hizi fukwe, fukwe nyingi zimevamiwa, lakini fukwe nyingi zimepewa watu ambao wameshindwa kuziendeleza. Katika kulibaini hilo tumependekeza kuanzishwa Mamlaka maalum ambayo itakwenda kusimamia Utalii wa fukwe na kuhakikisha kwamba fukwe hizi zinaundiwa sheria maalum ili zisiweze kuvamiwa.

Mheshimiwa Spika, na katika eneo la Coco beach juhudu mbalimbali zimefanyika lakini kuna mgogoro unaoendelea kati ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam katika Manispaa ambayo iko katika eneo hilo na mwekezaji katika eneo hilo na Ofisi ya TAMISEMI imeingia na kuelekeza. Aidha, Manispaa wamlipe yule muwekezaji aondoke au amruhusu aendelee na kazi yake lakini kuna ucheleweshaji wa kufanya maamuzi ndio maana Wizara imeona tuanzishe Mamlaka maalum.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ni kweli kwamba watalii ambao tumekuwa tukiwapata katika Mlima Kilimanjaro karibu kufikia asilimia 100 ni miaka 18 na mpaka miaka 50, chini ya miaka 18 na juu ya miaka 50 hawawezi kuja kwa sababu hawawezi kupanda Mlima Kilimanjaro ili kuweza kuwapata hawa tumefikiria kushauri TANAPA kuangalia uwezekano wa kufikiria kufanya utafiti kuona kama tunaweza kuweka cable car na kama hili litafanikiwa litaweza kutuletea watalii wengi zaidi kama tulivyoona takwimu katika nchi alizozitaja.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; kwa kuwa fedha zote ambazo zinakusanywa kutokana na utalii wa Kimondo Mbozi huwa zinachukuliwa na Serikali kuu na hakuna hata shilingi moja ambayo imewahi kurejeshwa kwa wananchi wa Kijiji husika cha Ndolezi na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi: Je, Serikali haioni kwamba huu ni ubaguzi kwa wananchi wa Wilaya ya Mbozi kwa sababu maeneo mengine yenye utalii, wananchi hurejeshewa sehemu kidogo ya fedha zilizotokana na utalii? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Vivutio vya Utalii vya Majimoto pamoja na Mapango ya Popo vimekuwepo kwa muda mrefu sana tangu uhuru. Je, Serikali kwa nini inaendelea kusuasua kutenga bajeti ya kuviendeleza vivutio hivi vya utalii ambavyo vipo katika Kijiji cha Nanyala, Kata ya Nanyala, Wilaya ya Mbozi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza katika swali lake la kwanza Mheshimiwa Mbunge ametaka kufahamu ni kwa nini Serikali imekuwa ikikusanya pesa hizi na kutokuzirudisha Halmashauri? Jambo hili siyo kweli.

Mheshimiwa Spika, unafahamu kwamba maduhuli yote yanayokusanywa na Taasisi mbalimbali za Setikali yanachangia katika mfuko Mkuu wa Serikali na pesa hizo ndizo zinazorudi kwa ajili ya uendeshaji wa huduma mbalimbali za jamii zikiwemo hospitali, kulipa walimu pamoja na mambo mengine na ujenzi wa miundombinu. Kwa hiyo, makusanyo haya yanayofanyika katika Serikali siyo lazima yarudi kama token kwenye Halmashauri, bali yanarudi kwa style ambayo wananchi wote katika Mkoa wa Songwe wanapata.

Mheshimiwa Spika, nimkumbushe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kimsingi jukumu la kuleta watalii na kuongeza mapato kwenye Halmashauri yake linaweza pia kufanywa na yeye. Kama mnavyofahamu, pamoja na kwamba tunapata watalii milioni 1.5 Tanzania, sehemu kubwa ya watalii hawa wanaokuja Tanzania wanatafutwa na wadau wa utalii.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhamasishe Mheshimiwa Mbunge kuihamasisha Halmashauri yake na yeye mwenyewe kukitangaza kivutio hiki cha utalii, lakini pia kuweka miundombinu kwa kushirikiana na Halmashauri ili kuweza kuingiza mapato mengi zaidi kwenye Wilaya yake.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili amesema kwamba tumekuwa tukisuasua katika kutangaza Majimoto. Hatujasuasua, nimemweleza katika jibu langu la msingi Mheshimiwa Mbunge kwamba Majimoto haya na Pango la Popo tumeviingiza katika kumbukumbu za Serikali. Jukumu la kuvitangaza na kuvifanya vilete watalii linaweza kufanywa na mtu mmoja mmoja. Kama mnavyofahamu, ni kwamba sisi kama Serikali tunasimamia sera lakini jukumu la mtu mmoja mmoja linaweza kutangaza kituo kile na kuleta watalii na kuongezea Serikali mapato.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Kwa kuwa suala la utalii limezingatia zaidi utalii wa mbuga za wanyama na fukwe, kuna utalii ambao umesahauliwa ambao nao pia ni mzuri na unawagusa wananchi moja kwa moja; utalii wa kitamaduni.

Mheshimiwa Spika, Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini hususan Songwe na hata Wilaya yangu ya Ileje, tuna vivutio vingi ambavyo vingeendelezwa vingesaidia sana suala hili na wananchi wangenufaika. Tuna ngoma za jadi, tuna mila zetu na desturi, tuna aina zetu za nyumba na mavazi ambapo watalii wengi wangependa kuona, lakini tuna tatizo kubwa hatuna Maafisa Utalii katika Wilaya zetu. Tumekuwa tukiuliza mara nyingi tutafanyaje tupate Maafisa hao ili wawezeshe sasa kuboresha hii miundombinu ambayo tunaihitaji kwa ajili ya utalii wa utamaduni.

Mheshimiwa Spika, tunaomba sasa Serikali ituambie lini watatupa Maafisa Utalii ambao wamebobea katika masuala ya utalii ili watusaidie katika suala hilo?

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kama nchi, tumekuwa tukitangaza zaidi utalii wa asili kwa maana ya utalii wa safari (Mbuga za wanyama) lakini pia na utalii wa fukwe. Uko utalii wa aina nyingi sana na aina mbalimbali na labda nitumie fursa hii kuwaambia Waheshimiwa Wabunge kwamba, bado katika maeneo yote Tanzania tuna vivutio vya utalii ikiwemo ngoma za asili kama alivyosema lakini maisha yetu peke yake ni vivutio vya asili ambavyo wageni wangetamani kuona.

Mheshimiwa Spika, ushauri wa kuwa na Maafisa Utalii katika kila Halmashauri, nimekuwa nikijibu swali hili hapa mara kwa mara kwamba Wakurugenzi wetu wanapowaomba Watumishi kwenye maombi yao kila mwaka, waingize maombi ya Maafisa Wanyamapori na Maafisa Utalii kwa sababu hawa ni watu ambao watakuja ku-promote utalii katika maeneo ya Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba tu nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumechukua ushauri wake, lakini niwakumbushe Wakurugenzi wote kwamba wanapoomba watumishi, waingize watumishi wenye taaluma ya utalii na wanyamapori ili kuweza kuzisaidia Halmashauri.
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni kumekuwa na mkanganyiko wa matamko kutoka kwa Wakala wa Misitu nchini kwamba mtu akipatikana na kilo 50 za mkaa ni lazima awe na kibali maalum; ni marufuku kwa mtu kupatikana na kilo 200 za mkaa na adhabu yake ni kifungo cha miezi kumi au kulipa faini ya shilingi 50,000 na shilingi milioni 12. Hivi ni sahihi kabisa watu kama akina mama lishe, mama ntilie, akina mama wa nyumbani, adhabu hii inawahusu?

Mheshimiwa Spika, katika swali langu la pili kwa kuwa gesi siyo ajenda tena kwa Serikali hii ya wanyonge na mtungi wa gesi hivi sasa kilo 15 ni kati ya shilingi 45,000 mpaka shilingi 50,000; hivi ni kwa nini Serikali isione kuna umuhimu wa kuondoa kodi katika gesi ili kuwawezesha wananchi waweze kutumia gesi badala ya kutumia mkaa na kuni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Devotha Minja, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza ninakiri kwamba limekuwepo tamko kutoka ofisini kwetu linalohusiana na namna tunavyojipanga kudhibiti ukataji na uchomaji hovyo wa mkaa na tumeelekeza kwamba wahusika wa biashara ya mkaa ambao wanafanya biashara, siyo watumiaji, wahusika wa biashara ya mkaa ambao wanasafirisha mkaa kwa ajili ya kuuza wanapaswa kuwa wamepitia taratibu mbalimbali kabla ya kuchoma mkaa na taratibu hizo zinaanza katika level ya vijiji, tunaowazungumzia hapa siyo watumiaji wa mwisho kwa maana ya mama lishe na watumiaji wa ndani hawa watakwenda kununua katika maeneo maalum ambayo tumeelekeza maeneo yote yanayofanya biashara ya mkaa yatasajiliwa na wale wanaofanya biashara ya mkaa pale ndiyo watakaowauzia watumiaji wa mwisho.

Kwa hiyo, ni makosa kuwakamata watumiaji wa mkaa wa ndani ambao wamenunua kwa muuzaji ambaye ametambuliwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ni kweli kwamba gharama ya gesi iko juu na hii imesababisha watu wengi ku- opt kutumia mkaa na kuni hasa maeneo ya vijijini, lakini watafiti wanaonesha kwamba bado kwa gharama ya sasa matumizi ya gesi ni gharama nafuu kuliko matumizi ya mkaa. Kwa mfano sasa hivi gunia la kilo 50 la mkaa katika Jiji la Dar es Salaam linauzwa mpaka shilingi 60,000 wakati mtungi wa gesi unauzwa shilingi 50,000 na muda wa matumizi ya gesi ni muda mrefu kuliko matumizi ya mkaa.

Mheshimiwa Spika, lakini nimechukua mapendekezo ya Mheshimiwa Mbunge na tutajadiliana na Wizara husika kuona kama tunaweza tukaomba kuondolewa kwa baadhi ya kodi kwenye gesi ili kuhamasisha matumizi ya gesi na kupunguza matumizi kuni. (Makofi)
MHE. MBARAKA K. DAU: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru na ninamshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri isipokuwa nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, pamoja na uzuri na vivutio vyote hivi vya utalii alivyovisema Mheshimiwa Naibu Waziri, Kisiwa cha Mafia hakijawahi kuonekana kwenye channel ya utalii inayoonyeshwa katika Azam. Sasa je, ni lini Mheshimiwa Naibu Waziri atawaelekeza wahusika wa vipindi hivyo waje kufanya shooting pale Mafia na vivutio vile viweze kuonekana?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika majibu yake Mheshimiwa Naibu Waziri anasema Serikali inajitahidi kuimarisha miundombinu ya kuingilika Mafia ili kuweza kupata watalii wengi zaidi. Tunaishukuru Serikali imetupatia boti ile ya DMI ambayo kwa sasa inamaliziwa matengenezo pale, lakini imekwama kupata kibali cha TASAC kutokana na matatizo ya hitilafu za kiufundi na kuna matatizo ya kibajeti ya Chuo cha DMI.

SPIKA: Swali Mheshimiwa?

MHE. MBARAKA K. DAU: Je, sasa Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kushirikiana na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano mtaweza kuwasiadia Chuo cha DMI matatizo yao ya kibajeti ili waweze ili waweze kulipia boti ile na iweze kuja Mafia?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba lengo la kuanzishwa kwa channel ya utalii ni kuhakikisha kwamba inatangaza vivutio mbalimbali vilivyopo katika nchi yetu katika maeneo yote na maeneo hayo ni pamoja na Kisiwa cha Mafia. Lakini naomba nikiri kwamba channel hii imeanzishwa tu, haina muda mrefu na uandaaji wa vipindi hivi ni unahitaji gharama na pesa nyingi na nchi yetu ni kubwa, bado hatujamaliza kuandaa vipindi, lakini naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kisiwa hiki ni maeneo yetu ya kimkakati ambayo tumeyaweka kwa ajili ya kuhamasisha utalii na nimechukua pamoja na maombi yake lakini ni mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba watu wetu wanaoandaa vipindi kupitia TBC wanakwenda katika eneo hili kuvitambua na kuvirekodi vivutio vyote vya utalii na kuvitangaza.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba pamoja na kwamba haijaonekana tutahakikisha kwamba tunatoa maelekezo kisiwa hiki kiweze kupewa kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili, kwanza naomba nimshukuru kwa kuipongeza Serikali kuboresha miundombinu mbalimbali hasa uwanja wa ndege ambao Mheshimiwa Mbunge amesahau kusema kuna uwanja wa ndege bora kabisa pale Mafia na nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba boti hii ambayo imekwama kwa masharti machache pale DMI nitashirikiana na wenzangu wa Wizara ya Uchukuzi kuhakikisha kwamba taratibu zinakamilishwa ili boti hii iweze kuanza kutoa huduma na kupeleka watalii katika Kisiwa cha Mafia, ahsante sana.
MHE.DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Kisiwa hichi cha Mafia ni eneo nyeti sana sio tu kwa ajili ya shughuli za utalii bali pia ni eneo ambalo linatulishia samaki, mazalia ya samaki katika bahari yetu. Sasa kwa kuwa ni kisiwa kiko strategic Wizara hii ya Maliasili na Utalii kwa nini sasa isikae na Wizara ya Mifugo na Uvuvi pamoja na TAMISEMI kuleta mkakati mahususi wa kuwezesha shughuli za wananchi katika maeneo haya ya Mafia ambao wako duni sana na majority ni wavuvi, wainuliwe kiuchumi na kuweza kuinua utalii pamoja na shughuli za uvuvi ili kuinua zaidi uchumi wetu kwa ujumla nchini?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba maeneo ya Kisiwa hiki cha Mafia ni maeneo ambapo kwanza kuna visiwa vingi, lakini maeneo yenye wavuvi wengi, lakini ni maeneo ya mazalia ya samaki na baadhi ya maeneo haya ambayo nimeyataja kwamba yako chini ya marine park ni maeneo yanayohifadhiwa kwa ajili ya mazalia ya samaki pia ndipo ambapo utalii wa kuzamia majini unafanyika na ndipo ambapo kuna akiba ya under water cultural heritage nyingi ambazo ziko maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa sababu suala hili ni cross cutting linahitaji pengine kujadiliwa na wizara nyingi mbalimbali. Tumechukua wazo lake lakini nimhakikishie kwamba mpaka wavuvi na wananchi katika maeneo hayo wanaandaliwa vizuri ili kuhakikisha kwamba wanafaidika na uwepo wa shuguli za uvuvi pia na uwepo wa shughuli za utalii katika maeneo hayo.
MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa uwepo wa mamba pia ni sehemu ya kivutio kwa watalii lakini kutokana na ongezeko kubwa sana mazalio ya mamba katika Mto Ruvuma na kuleta athari kubwa sana kwa wananchi.

Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuja kwenye Jimbo langu kuona athari kubwa zinazojitokeza na kutafuta changamoto za kutatua tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba limekuwepo ongezeko kubwa sana la mamba katika maeneo yetu mengi mamba, boko na wanyama wengine ambao hawatumiki moja kwa moja sana na kuhamasisha utalii na katika eneo hili la Mto Ruvuma ambalo Mheshimiwa Mbunge amekuwa akisema wamesababisha shughuli za uvuvi na shughuli za matumizi ya maji ya kawaida ya Mto Ruvuma kushindikana.

Mheshimiwa Spika, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kama nilivyomjibu hivi karibuni kwenye swali lake la msingi kwanza tulielekezwa watu wetu wa TAWA kuhakikisha kwamba wanapeleka visima vya maji karibu katika vijiji ambavyo viko karibu na maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, pili, tuliwaagiza watu wetu wa TAWIRI kufanya utafiti na kutueleza mamba waliopo wamezidi kwa kiasi gani ili tuweze kuweka mkakati wa kuwavuna, lakini nimhakikishie pia Mheshimiwa Mbunge kwamba niko tayari kwenda katika eneo hilo kwenda kuangalia hali halisi na kuzungumza na wananchi.
MHE. GIMBI D. MASABA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu ya Serikali, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, ifahamike kuwa gharama za kukodisha mashamba zinapanda kila siku, unakuta kukodisha hekari moja ni Sh.200,000, uandaaji wa shamba ni kama Sh.300,000 bado ushuru wa Serikali. Je, Serikali haioni kwamba sasa inatakiwa kuweka mkakati wa lazima kuhakikisha wananchi hawa wanapata kifuta machozi ambacho kinastahili?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa tatizo hili ni kubwa sana na utafiti umeonyesha kuwa miti ya pareto, pilipili, mizinga ya nyuki inasaidia kuwafukuza wanyama hawa. Je, Serikali ina mpango gani kuanzisha kampeni mahsusi kuhakikisha kwamba wanapanda hiyo miti kwenye maeneo yanayozunguka hifadhi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, naomba nikiri kwamba swali hili limeulizwa mara nyingi sana hapa Bungeni na matukio ya wanyama kama tembo kuendelea kuharibu mashamba yanaendelea katika maeneo mengi na hivi karibuni Kalambo, Same yameendelea kusumbua. Kwa hiyo, tunakiri kwamba tunahitaji kuwa na mkakati kama nchi wa kuangalia namna tunavyoweza kuendelea kulinda mali za wananchi pia na maisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nakubaliana na swali lake la pili kwamba kama Serikali tunahitaji mkakati na tumewaelekeza watu wa TFS kuhakikisha kwamba wanatoa elimu na kusaidia kusambaza mizinga ya nyuki katika maeneo yote ambayo yamekuwa yakipata athari za wanyama hawa mara kwa mara. Pia katika mikutano yote ya hadhara tumekuwa tukihamasisha upandaji wa pilipili. Katika maeneo mengi zao za pareto siyo maarufu lakini limeaminika kwamba linapokuwa limepandwa kwenye mipaka ya mashamba linasaidia kuzuia tembo wasisambae. Kwa hiyo, tunachukua ushauri wa Mheshimiwa Mbunge tutaufanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kuhusu kifuta machozi, ni kweli kwamba hata lugha inayotumika kwenye majibu yetu ni kifuta jasho na kifuta machozi sio fidia na gharama za kuandaa shamba heka moja zinakadiriwa kuwa takribani Sh.300,000 mpaka Sh.350,000 ambapo sisi kwenye taratibu zetu tumekuwa tukilipa pesa isiyozodi Sh.100,000. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge moja ya maeneo ambayo tunayarejea sasa kuyaangalia vizuri ni kuangalia gharama kutokana na hali halisi ya sasa zikiwemo gharama za uandaaji wa mashamba pamoja na mbegu na mambo mengine. Kwa hiyo, tumemaliza hatua ya wadau wa ndani na tunajielekeza sasa kupata maoni ya wadau wa nje na mara taratibu hizo zitakapokamilika tutakuwa tumefikia kwenye kiwango ambacho kinaweza kikawa angalau ni cha kuridhisha.
MHE. MBAROUK SALIM ALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pamoja na majibu ya Naibu Waziri, lakini mimi swali langu lilikuwa linajumuisha maliasili zote kwa ujumla ingawaje yeye amekwenda very specifically kwenye misitu, lakini hayo tuache.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, zoezi hili la ushirikishwaji wa jamii ni la muda mrefu kwa kweli, inasikitisha kwamba bado kuna malalamiko mengi ya migogoro na mambo mengine mengi. Nilitaka kujua ni kwa nini mpaka leo hii WMA’s nyingi hawapati gawio lao kwa wakati na kwa ukamilifu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, pamoja na miradi mingi ambayo inafanywa na Serikali katika jamii hizi ambazo zimezungukwa na maliasili hizi ni sawa lakini jamii hizi ni maskini wa kutupwa na miradi mingi imeelekea zaidi kwenye miradi ya kijamii. Je, Serikali haioni kwamba sasa kuna haja au ulazima wa kubadilisha mwelekeo na kuelekeza nguvu zao zaidi kwenye miradi ya kiuchumi na kuwapatia taaluma wananchi ili waweze kujikimu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbarouk Salim Ali, Mbunge wa Wete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge anasema swali lake lilikuwa linauliza maliasili kwa ujumla na ili kumjibu swali hilo labda pengine ningehitaji nusu saa nzima kwa sababu kama unavyofahamu maliasili kwa ujumla almost asilimia 50 ya nchi hii iko kwenye maliasili. Nimwombe Mheshimiwa Mbunge kama ana swali la nyongeza tunaweza tukawasiliana ili kuweka vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge anataka kufahamu kwa nini WMA nyingi hazipati migao yake ya fedha kwa wakati na kwa kiwango cha thamani halisi. Naomba kwanza nitoe maelezo mazuri kwamba WMA ni jumuiya ambazo zinaanzishwa na vijiji kwa kutenga maeneo yao wanaanzisha jumuiya ambayo wanatafuta mwekezaji ambaye wanaingia naye mkataba kwa kutumia vikao mbalimbali wanakuwa na uongozi wao ambao unawajibika moja kwa moja kwenye kusimamia maslahi ya WMA. Hapa katikati tulirekebisha kanuni baada ya kuona tulikuwa na viongozi wengi ambao walikuwa wanapokwenda kwenye vikao hivi vya WMA wanazidiwa maarifa na wawekezaji tukarekebisha kanuni ili kuruhusu aina fulani ya elimu ili iweze kutumika lakini jumuiya ya WMA yenyewe imerudi na malalamiko kwamba inataka watu wote ili mradi anajua kusoma na kuandika waingie kwenye uongozi wa WMA. Kwa hiyo, hii ilikuwa ni changamoto lakini tumetoa maelekezo maalum kupitia Mkurugenzi wa Wanyamapori kuhakikisha kwamba inatoa msaada wa kitaalamu na kitaaluma katika usimamizi wa WMA ili iweze kupata maslahi yake kwa mujibu wa mkataba walioingia na mwekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, jamii nyingi ambazo zinazunguka maeneo haya yenye maliasili ni maskini na kwa sababu Serikali labda imejielekeza zaidi katika miradi ya kijamii kama shule na kadhalika. Miradi yote inayofanywa na Mapori yetu ya Akiba na Hifadhi za Taifa na WMA ni miradi inayochaguliwa na vijiji vyenyewe. Vijiji vinakaa na kutenga miradi ya kipaumbele na vinapeleka muhtasari wa makubaliano haya kwenye mamlaka husika ya hifadhi, ndiyo inakwenda kujenga au kutoa msaada huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumeanza hivi karibuni sasa kuweka package ya kutoa elimu ya fursa mbalimbali ambazo zipo katika maeneo yanayopakana na hifadhi ili kuwaruhusu wananchi hawa kushiriki moja kwa moja kwenye mapato na biashara ya hifadhi na utalii yanayopakana na maeneo yao ya vijiji. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge naomba tu nikushukuru kwamba maoni yako na ushauri wako tayari tumeanza kuufanyia kazi na tunashukuru kwa mtazamo huo na ndiyo mtazamo wa Wizara kuanzia sasa kuwashirikisha wananchi wote katika farsa ambazo zinapatikana katika maeneo yao.