Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Joseph Kasheku Musukuma (65 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niwe mchangiaji katika mjadala unaoendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa Hotuba yake nzuri iliyosheheni matatizo ya Watanzania ambayo tumekuwa tukilia kwa siku nyingi. Tunakutia moyo tunasema endelea na moyo huo, Watanzania wanaona. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze pia Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoendelea kuifanya ya kutumbua majipu na Watanzania wanaona. Napenda kumshauri kama atapata taarifa hizi aangalie hata kwenye Vyama vya Upinzani na kwenyewe kuna majipu ambayo yanatakiwa yatumbuliwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka Bunge la Kumi na Moja Mheshimiwa Lusinde alichangia hapa akasema Chama cha Upinzani kikishindwa zaidi ya mara tatu kinageuka kuwa chama cha kigaidi. Nakubaliana na Mheshimiwa Lusinde kwamba hawa ndugu zetu wanakoelekea sasa ni kutengeneza ugaidi kwenye nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu sina hakika kama mawazo aliyoyasoma Mheshimiwa Kiongozi wa Kambi ya Upinzani ni ya Wabunge wote. Kama ni ya Wabunge wote, Wabunge wote wa Kambi ya Upinzani mtakubaliana na mimi ile hoja yangu ya bhangi tuitafutie muda tuijadili. Niliwaambia humu kuna wateja, sababu ya kuwabanabana wanavuta bila kipimo, wanakuja humu wana stata zimezidi kipimo. Sina hakika kama haya mawazo ni ya watu wote ama ni ya mtu mmoja aliyevuta bila kipimo. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini unaona hata hali halisi ya Kambi ya Upinzani ilivyokaa, ndugu zangu watu wa Upinzani, hebu tumieni akili zenu mlizotumia kuwaomba watu kura kule mkaletwa humu ndani. Mnadanganywa mnatoka kwenye mada, mtu anasimama hapa anasema eti kwa sababu Kiongozi wa Kambi ya Upinzani amesema bado anafikiria naomba kuchangia hiyo ndiyo hoja yangu, hayo ndiyo yamekutoa kwenye Jimbo kukuleta humu Bungeni? Watu wako wana njaa, wana shida ya maji, umeme, madawati, Mawaziri hawa hapa wewe unazungumza suala la Kiongozi wa Upinzani, ana nini humu ndani? (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana tukubaliane na hii hali kwamba yale maneno ya Mheshimiwa Lusinde yanaenda yanatimia. Ukiangalia hata Wapinzani waliobaki humu ndani sasa hivi ni wale waliokosa tu nafasi, ni wana CCM walioingilia dirisha la pili, wanajiandaa kurudi humu ndani. Tukubaliane na hii hali, hawa wenzetu hawana hoja, walikuja na hoja ya CUF ya Zanzibar wamepigwa bao.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Wewe kaa chini. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, walikuja na hoja ya Zanzibar, hoja ya Zanzibar tumewashinda…
MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma keti. Haya taarifa....
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na namshukuru mkomavu wa kisiasa ambaye pia anajua kuzisoma Kanuni vizuri. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kuwasifu baadhi ya viongozi wa upinzani, Waheshimiwa Wabunge kama Mheshimiwa Profesa J, unaonesha uvumilivu wa hali ya juu. Wewe kwa sababu ni kioo cha jamii ningeomba uachane na mawazo ya kufundishwa ukipata nafasi changia, wasanii wanakutegemea humu ndani, usitegemee mawazo ya kuambiwa na wenzio hawa wazoefu hutarudi. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niende kwenye hoja yangu ya msingi. Nataka kuchangia baadhi ya mambo ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu ameandika humu ndani kuhusiana na matatizo yaliyoko kwenye Majimbo yetu. Kwanza ni kuhusiana na suala la TV. Naipongeza Serikali na uongozi wa Bunge, Jimbo langu halina umeme, tulikuwa tunatumia generator kuangalia Bunge na toka mmezuia Bunge vijana sasa wanashinda mashambani. Endeleeni na mpango huu na ikiwezekana vipindi vya Bunge vioneshwe hata saa sita wakati wa kupumzika ili hata usiku kuwe na kazi zingine za kufanya wakati ambao watu wana nafasi. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niishauri Serikali, kumekuwa na kasi ya kutumbua majipu watendaji wa Serikali, tunaipongeza sana Serikali, lakini hatutumbui vyanzo vinavyosababisha wafanyakazi wetu wa Serikali wanakuwa wezi. Nataka kutoa mfano, kuna mkandarasi anaitwa JASCO ambaye amesababisha Mkuu wa Mkoa wa Bariadi akasimamishwa na Mkurugenzi na Mhandisi wakafukuzwa lakini yeye akaachwa palepale kwa kuiba shilingi bilioni 19. Sasa amehamia Geita ana mkataba wa shilingi bilioni tano kwa kilometa tatu, ana mkataba wa shilingi bilioni sita kwa kilometa mbili, ana mkataba wa shilingi bilioni kumi na nne kwa kilometa thelathini na nane na bado anafanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri watu kama hawa kwenye kasi ya wakati wa Waziri Magufuli alikuwa anazifuta hizi kampuni. Tutamaliza watumishi wetu kuwaacha wafanyabiashara wenye uwezo wanawashawishi watendaji wetu kwa pesa, wanawapa mikataba ambayo ni mibovu. Tunawajua kabisa wamefanya hayo Bariadi leo amehamia Geita na tunawaacha wanaendelea kufanya kazi. Je, tunasubiri tena kwenda kufukuza Mkuu wa Mkoa na Wakurugenzi? Kwa hiyo, nashauri kwamba tuchukue hatua kabla mambo hayajawa mabaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilizungumza kipindi kilichopita kuhusiana na suala la ulinzi kwenye Jimbo langu. Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba utuonee huruma. Ukiangalia kwenye taarifa Jimbo langu nadhani sasa hivi Tanzania ndiyo tunaongoza kwa kukatwa mapanga. Nilisema kila mwezi wastani wa watu wanne wanakatwa mapanga. Leo tunavyozungumza nurse kavamiwa hospitali kakatwa mapanga. Kwa mwezi wanakatwa mapanga siyo chini ya watu wane.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lililopo kwa wananchi wa Jimbo langu, kutoka kilipo kituo kikuu cha Polisi Geita ambako kuna usafiri ni zaidi ya kilometa hamsini. Unapopiga simu Geita gari kufika kwenye eneo la tukio inachukua zaidi ya saa moja kulingana na hali ya miundombinu. Pengine kuna njia gani mtufundishe na sisi ambao ni Wabunge wageni tuweze kuwaona Mawaziri mtupe Kanda Maalum. Wakati Rorya watu walikuwa wanaibiwa ng’ombe mkatoa Kanda Maalum na gari, sasa kwetu binadamu wanauawa wanne kwa mwezi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilizungumza humu Mheshimiwa Masauni akasema mwezi mmoja tuangalie tunapata magari sijaona mpaka leo. Mheshimiwa Waziri Mkuu labda mnataka mpaka msikie na Mbunge amekatwa mikono ndiyo mlete helikopta? Naomba mlipe kipaumbele Jimbo langu kwani kwa hali ilivyo sasa tunahitaji kupata gari kwa dharura ambalo litafanya doria kukamata wakata mapanga, pengine wahame basi hata warudi Mikoa ya Kusini huko na ninyi muweze kupambana nao huko. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapiga kelele sana kuhusu suala la maeneo ya kuchimba Geita. Nimeona humu amesema ameongeza ruzuku, Mheshimiwa Waziri Mkuu imekuwa ni porojo. Ndugu yangu Mheshimiwa Kalemani nataka nikwambie uliahidi mara ya tatu juzi akiwepo Waziri Mkuu kwamba tarehe 16 utaachia magwangala hujaachia. Sasa nakusubiri ukivuka feri labda upae na helikopta hutapita pale Geita, tutakusubiri, tutahakikisha tunakupeleka kwenye magwangala wewe ukawe ni mmoja wa waathirika kama wale vijana wanaopigwa mabomu bila sababu kwa kusikiliza kauli yako.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Kitu kizuri huwa hakina mjadala na ndiyo maana umeona wenzetu wale wamekimbia. Hotuba ya Waziri Mkuu inajitosheleza tunachotakiwa sisi ni kuisimamia na tuko tayari kuisimamia na ndiyo maana hata Wapinzani wanakwambia wanakwenda kujipanga. Hakuna cha kujipanga, hiyo ni dalili ya kukwambia Mzee uko safi, endelea na spidi hiyo hiyo na ikiwezekana geukia na upinzani utumbue majipu maana hata kwao kuna ufisadi mkubwa tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka, Mheshimiwa Sabodo walionesha kwenye TV, aliwasaidia shilingi milioni mia mbili na kiwanja Mwenge, mkasema mnajenga Chuo cha Viongozi wa Vyama vya Upinzani, kiko wapi hata tofali hazipo na hela ziko wapi? Kwa hiyo, tuangalie hata kwenye Vyama vya Upinzani. Kama mnataka kuiga siasa ya kweli ya kuwasaidia Watanzania, hii ndiyo mlikuwa mnaililia miaka yote kasi ya jet, nendeni mkajifunze kwa Magufuli na kwa Waziri Mkuu na timu nzima ya Mawaziri, sasa hivi tuko vizuri, mjiandae 2020 kurudi CCM.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba niwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Geita kwa kuniamini, kunipa kura nyingi nami ninaahidi sitawaangusha. Naomba kuchangia kwa haraka sana hotuba ya Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunatoka kwenye maeneo ya madini. Katika kura ambazo tumezipata katika Mkoa wa Geita na nina hakika kwamba Mkoa wangu wa Geita mimi ni Mwenyekiti pale, tukifeli sana ni namba tatu kwenye nchi hii kwenye ushindi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia kubwa ya wananchi waliotuamini ni wachimbaji wadogo wadogo na ndiyo sera ambayo tulizunguka nayo kuomba kura za Mheshimiwa Rais na pia kuomba kura za Wabunge, ukizingatia Geita pia ilikuwa sehemu kubwa sana ya Kambi ya Upinzani kwenye Kanda yetu ya Ziwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili la madini, toka mwaka 2005 Mheshimiwa Jakaya Kikwete anaingia madarakani mpaka ameondoka wananchi wa Geita wanadanganywa. Na kwa mara ya pili Mheshimiwa Kikwete amekuja na Mheshimiwa Muhongo kwenye ziara. Tumezunguka naye, tukafika Nyarugusu Mheshimiwa Rais aliahidi kurudisha eneo la STAMICO kwa wachimbaji wadogo wadogo, ndani ya miezi miwili, mbele ya Profesa lakini baada ya hapo hatukuona utekelezaji wowote. Tulifuatilia ofisi ya Mheshimiwa Muhongo, bahati mbaya aliondolewa kwenye eneo lile, wanasema suala hili haliwezekani kwa sababu wawekezaji (shareholders) wa eneo lile wako Ulaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuomba sana imefika wakati sasa tusidanganywe tena na Mheshimiwa Profesa Muhongo tunakuombea, kwa vile na wewe umepita kwenye changamoto ya kuchaguliwa umeona maswali yanavyokuwa kule kwa wananchi, tunaomba suala hili ulitie kwenye akili zako, hatutaki tena kudanganywa! Amekuja Rais ameahidi miezi miwili, amekuja Mheshimiwa Kinana akaahidi wiki mbili, Mheshimiwa Simbachawene akapiga simu tupeleke watu kwa nguvu. Hatukutaka hivyo kwa sababu sisi ni viongozi.
Kwa hiyo, ninachoomba suala hili watu wameshaahidiwa, hatutaki tena kudanganywa. Kwanza limeshikiliwa na vigogo wa CCM, kwa nini tunaendelea kumkumbatia mtu mmoja tunatesa watu milioni tano. Kwa hiyo, nilikuwa naomba suala hili Mheshimiwa Profesa kama hulijui tukusaidie documents, tunazo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala la pili, hapo hapo kwenye madini. Unafahamu changamoto kubwa ya Mji wa Geita. Tunashukuru juzi kidogo umefunguka ukatuachia magwangala, lakini hatujaridhika! Magwangala ni sehemu ndogo sana. Tunahitaji kuwa na maeneo ya wachimbaji wa kati kwa sababu Magwangala ni ya watu wa hali ya chini wanaookota wanapata shilingi 700,000/= hadi milioni.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, magwangala ni miambataka, waste mine bado hujaelewa Mheshimiwa? Maarufu kama magwangala. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sasa maeneo ambayo tumeshakaa tukakutumia tunayaomba maeneo ya Nyamatagata na Samina uyarudishe kwa wananchi, kwa sababu sheria inasema baada ya miaka mitano wachimbaji wadogo tupewe eneo, lakini wataalam wako wanatupeleka tofauti, wanakwenda kutupatia maeneo tunachimba visima hatupati dhahabu wakati dhahabu ya kwenye magoti iko kwenye maeneo hayo. Sasa kwa sababu tuko wote humu ndani, usipotusaidia mimi kila siku nitawaka na wewe mpaka kitaeleweka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sehemu ya pili ninaomba sana katika suala la maliasili. Maliasili ni tatizo kwenye Wilaya ya Geita na Mkoa mzima wa Geita, kwa bahati mbaya au nzuri nimepangwa kwenye Kamati ile. Mimi sijasomea misitu lakini naielewa kwa sababu nimetokea misituni. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sintofahamu. Mimi mwenyewe kijiji nilichozaliwa miaka ya 1960 tukapangwa kijiji mwaka 1974, juzi ilipoanza bomoa bomoa ya Dar es Salaam kimehamishwa kigingi kutoka porini kimekuja kuwekwa nyumbani tulipozaliwa na wakati kijiji kina watu na kimetoa watu wakubwa sasa. Sielewi hii sintofahamu kwenye Baraza la Mawaziri kwa sababu wanakaa wanapanga sehemu za kufanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii sintofahamu ya bomoa bomoa wengine wanabomoa Dar es Salaam, wengine wanafukuza watu maporini, wengine wanabomoa Mwanza huko, naomba kuuliza, hawa wataalam hili suala la bomoa bomoa, mimi mwenyewe naomba niseme wazi siungi mkono suala la kubomoa, na ninaamini kwamba linaumiza tu watu maskini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano kwa Mkoa wa Mwanza, ukienda Mwanza nyumba za eneo la Ghana pale nyumba zote zimewekwa alama ya “X” ziko kwenye mto unaopita Kirumba kuingia Ziwani pale, lakini wakati huo huo Serikali imetoa kibali kujenga BOT ghorofa 12 hatua tatu tu kutoka kwenye mto, ukienda kituo cha polisi na custom ya Mwanza iko Ziwani. Sasa tunaipeleka wapi nchi hii na hawa wataalam wetu wanaotoa amri huku na huku wanatekeleza vitu vingine?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana kwamba eneo hili la maliasili sisi tunatoka misituni tumeshaleta maombi Wizarani kwamba kama tulikuwa na hekta 15,000 za pori kwa nini tusipewe hekta 7,000? Kwa sababu wakati mnatupa tunatunza hekta 15,000 tulikuwa na wakazi 57,000 leo tuko 300,000 mnatulazimisha tukae kwenye heka 5 haiwezekani! Tunakaa kila siku tunapigana na polisi mpaka lini? Nimuombe Waziri mwenye dhamana aliziangatie hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ni suala la kilimo. Kwenye upande wa Idara ya Kilimo ninamuomba Mheshimiwa Waziri Mwigulu ukae na wataalam wako. Nataka nikuhakikishie ni wezi wa hatari. Kwa nini nasema hivyo? Mfano Wilaya ya Geita tumeletewa tani 5,300, watu wetu wamepewa vibali wakaenda kulipa Shinyanga, ukishalipa Shinyanga unapewa siku saba. Ukitoka Geita kwenda Shinyanga siku moja, kwenda Sumbawanga siku nne lori linatumia siku nne, kupanga foleni kupakia ni siku tatu. Mtu amepakia lori moja anaambiwa kibali kimeisha, halafu kwenu huku mnaonesha mmeshatoa mahindi, wanayauza tena kwa mtu mwingine, tunaomba ulifuatilie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia suala la afya, Mheshimiwa Waziri Ummy Mwalimu ulikuja na Makamu wa Rais, ukadanganywa hospitali nzuri, ukapambwa, sisi hatutaki majengo tunataka dawa. Ile ilikuwa ni bosheni (fake) ya kusafisha mgodi wa dhahabu unaotuibia pale Geita. Tunaomba sasa ufanye follow up ya kuja kuangalia, hakuna chochote, watu wanakuja kufaidi majengo na vitanda hakuna dawa, tunaomba uje uangalie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kitwanga kama yuko humu, ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri hebu buni mbinu nyingine ya kuwakamata hawa boda boda. Kauli yako ulivyotoa ukienda vituo vyote nchi hii vimejaa bodaboda hatuna ujanja mwingine wa kuweza kuwakusanya hao bodaboda na kuwatambua au kuzitambua, kwa sababu hata wale ambao hawana makosa nao wanaombwa hela, tunaomba uliangalie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kiwanda, Mheshimiwa Mwijage, umejipapambanua vizuri sana lakini naomba nikwambie wataalam wako wanakudanganya wana-copy na ku- paste. Unasema tunafungua Kiwanda cha Juice Morogoro. Tanzania hatuna matunda ya kutengeneza juice hapa. Mimi ni mwathirika nimedanganywa na wataalam wako, tumenunua kiwanda, tumeleta wataalam wenye mashine wanatuambia matunda yetu mananasi na maembe ni matunda ya kutengeneza dawa za kienyeji! (Kicheko)
Wataalam wako wame-copy maembe ya Uarabuni wanatuambia yanafaa kwenye viwanda vya Tanzania. Hebu jaribu siku moja ukachukue mti mmoja kila chungwa moja linaladha tofauti, unatengenezaje hiyo juice! Unaongeza pilipili au unatengeneza kitu gani waambie wataalam wako wafanye utafiti na uchunguzi wa kina wasikufanye ukajipambanua hapa watu tunakushangaa. Hatuna matunda, matunda yetu haya yameenda Italy kufanyiwa test yanaonekana ni matunda ya kutengeza dawa za kienyeji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana akina Ndodi mnapambana nao nao huko, na akina nani huyu aliyekamatwa na Mheshimiwa Kigwangalla, hatuna matunda ya juice. Hebu leo tengeneza juice ya mananasi, ukiiacha siku ya kwanza, siku ya pili unapata pombe ya kienyeji. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana kuwashauri wataalam wetu watumie muda mwingi sana kufanya utafiti wa kina kumshauri Rais vinginevyo mtahamasisha watu wafungue viwanda halafu mnakutana na vitu vya ajabu, tunaingia mikopo ya mabenki hatutalipa tutatangazwa kwenye magazeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, nilizungumza juzi watu wakanicheka sana. Suala la mirungi, mimi siyo mlaji lakini nasema tujifunze Kenya mirungi inasindikizwa na bunduki na jeshi, sisi huku tunaiita mihadalati. Na nikuambie pamoja na kuzuia haihitaji kuwa na Usalama wa Taifa wala Polisi. Sasa hivi tuzunguke Dodoma hapa, hapa wanakula na usalama tunao, Tanga wanakula, Dar es Salaam wanakula.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru ahsante sana. (Makofi/Kicheko)
Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naomba niwashukuru sana wananchi wa Jimbo langu la Geita Vijijini kwa kuniamini kwa kura nyingi, hawanioni lakini mmo mtapeleka taarifa, kwa kuniamini na kunipa Jimbo la Geita Vijijini pamoja na mikwara mingi iliyOkuwepo kule maana helicopter ziliteremka zaidi ya mara nne. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nianze kwa kuzungumzia kidogo tu suala la Zanzibar. Ninyi ndugu zetu wa Upinzani acheni kuwachanganya watu, ngoma imetangazwa subirini mkashinde. Watu wanaojiamini hawaji hapa kutafuta sifa za kupiga kelele. Hata leo hii mkitengua uteuzi wangu tukarudia uchaguzi nawapiga bao kwa sababu ninapendwa. Kama mmeshinda kwa halali acheni kuja kuchukua sifa humu ndani za kuwadanganya watu mlishinda, mlishinda vipi, kama mlishinda mbona mko nje? Ujumbe umefika. (Makofi)
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye Mpango wa Maendeleo kama tunavyoendelea kujadili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yamezungumzwa mambo mengi, hapa tunajadili Mpango na sisi Wabunge wapya tunasema Mpango huu ni mzuri isipokuwa tuusimamie. Hatutaki kuzungumzia Mipango iliyopita tunazungumzia Mpango tulionao. Huu Mpango ni mzuri na sisi wenyewe tutakabana kuukamilisha na kuusimamia. Wala tusianze kupotosha kwa kusema mambo ya miaka iliyopita sisi ni wapya tuzungumze haya tunayoanza nayo na kasi ya Mheshimiwa Rais aliyepo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la reli. Upande wa reli naomba tuondoe hii sintofahamu. Sisi watu tunaotumia reli tunaomba kwanza kabla hatujajenga reli ya kwenda kuungana na Rwanda tuimarishe reli zetu ambazo zipo. Tusianze kuongeza mambo ya kutengeneza uhusiano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wakati kwetu huku kumeoza, tuimarishe kwanza ya kwetu, ya kwenda Mwanza, Mpanda, Kigoma baada ya hapo sasa ndiyo tufikirie kutafuta mahusiano na nchi zingine za jirani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine naona humu halizungumzwi kabisa, sisi tunaotoka Kanda ya Ziwa, ukienda Mwanza leo barabara zinazokatisha airpot kwenda Igombe zilishafungwa kwa ajili ya kupisha ujenzi wa kiwanja cha ndege. Kwa kweli ujenzi wa kiwanja cha ndege cha Mwanza umekuwa unasuasua kwa miaka mingi. Humu ndani sijaona kabisa wapi pamesema tutaujenga uwanja wa Mwanza uwe uwanja wa kimataifa na mkizingatia Mwanza ni mji mkubwa nadhani ukiondoa Dar es Salaam sasa Mwanza ndiyo inafuata. Pia Mwanza tuko kilomita 92 tu kwenda Serengeti lakini hatuna uwanja watalii wanatua Arusha wanatembezwa kilometa 300 mpaka 400 na zaidi, kwa nini tusiimarishe uwanja wetu wa Mwanza ili na Mwanza nayo ikawa na utalii, tukajaribu ku-balance na wenzetu wa Kanda ya Kaskazini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana kwenye Mpango huu tuzungumze kuhusu uwanja wa ndege wa Mwanza, ni tegemeo kubwa. Leo hii ukienda Mwanza watu wana hoteli hakuna wateja wa kulala. Sisi Wasukuma ni washamba tukiona ghorofa tunakimbia hatulali humo. Tulijenga ghorofa kwa ajili ya wageni, wageni wanaishia Arusha tu. Niombe sana Mpango huu tuachane na porojo tumalizie Uwanja wa Kimataifa wa Mwanza. Eneo tunalo na nguvu kazi na kila kitu kiko Mwanza, naomba sana hilo tulizingatie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze pia suala la wachimbaji wadogo. Sikuona mahali kabisa linatajwa humu, sikuona! Kwa vile nilishazungumza na Profesa Muhongo nikamwambia Bunge lililopita ulipata figisu figisu ukaondoka, ukaingia kama mwanaume kwenda kugombea Jimbo, umerudi sasa na kasi ya Jimbo, porojo porojo tena hakuna. Kwa hiyo, sisi watu tunaotoka kwenye maeneo ya wachimbaji wadogowadogo tunahitaji kuwa na maeneo yetu ya kudumu, tena uwanyang‟anye Wazungu wala usihangaike kututafutia mapya. Kwa sababu sheria inasema kila baada ya miaka mitano unawanyang‟anya kiasi fulani unaturudishia, upeleke wataalam wako watafute maeneo yenye dhahabu za kina kifupi utukabidhi sisi wachimbaji wadogowadogo tuweze kuchimba na kupata dhahabu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze suala la kilimo na viwanda. Ukianzia Musoma mpaka Bukoba sisi tunazungukwa na Ziwa, ni neema pekee ambayo tumepewa na Mungu. Watu wa Kanda ya Ziwa wala hatuhitaji elimu kubwa ya kutusaidia katika suala la ajira. Tulikuwa na viwanda vingi lakini vimekufa vyote. Sasa ni jinsi gani Serikali inakaa upya na watu wenye viwanda kule Kanda ya Ziwa waweze kuweka mpango mzuri ili viwanda vyote vile vinavyozunguka kwenye kanda ile viweze kufunguliwa na kufanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wengi wana nia sana ya kuwekeza katika viwanda vya samaki na viwanda vingine. Kwa mfano, kwenye Jimbo langu vijiji vya Kagu, Nyewilimilwa, Bugurula tunaweza kuweka viwanda hata vya unga wa muhogo lakini hakuna barabara, umeme na maji hatuwezi kuweka viwanda kama hivi viambatanishi havijafuatana pamoja. Kwa hiyo, niwaombe wahusika waweze kuzingatia hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la viwanda kwa Kanda ya Ziwa tunalihitaji, hatuhitaji maelezo marefu. Nataka niwaambie watu wote wa Kanda ya Ziwa tutaungana kwa sababu tunataka kuwa na viwanda vyetu. Humu hakuna itikadi, watu wanahama vyama lakini tunachotaka ni viwanda, sitaki kusema ni nani mnaelewa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nizungumzie suala la kilimo, sisi tunatoka sehemu za wakulima. Ukizunguka kule kwetu kote wimbo mkubwa ni kilimo cha pamba ambacho hakieleweki na hakuna mtu ataweza kukisimamia hata rafiki yangu Mwigulu hutaweza. Hii ni kwa sababu biashara ile imezungukwa na matapeli na Serikali inaona na tumeshindwa kabisa kuwadhibiti watu hawa.
Sasa mimi nilikuwa napendekeza na nikizungumza humu watu wananicheka, yako mazao ambayo hayahitaji kupigiwa debe. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niliuliza swali, niulize tena kwa sababu tuko kwenye Bunge la pamoja kwamba ni utafiti gani uliwahi kufanyika na waliofanya ni madaktari gani mpaka tukafika mahali tukapitisha mirungi kuwa dawa za kulevya? Nasema kila siku, ukienda Nairobi mirungi inasindikizwa na SMG za Jeshi la Kenya. Kuna ndege mbili Boeing zinateremka kwa wiki mara mbili kupeleka mirungi nchi za Ulaya. Sisi ukienda Tarime, Morogoro, Bunda kuna mirungi mingi, kwa nini tusirudie kufanya utafiti upya ili hii mirungi ikarudi kuwa zao la biashara ambalo halina utapeli, ni biashara inayoenda moja kwa moja? (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia twende sambamba na bangi msinicheke, hata bangi mimi sina hakika kama inafaa kuzuiwa. Watafiti wetu waliofanya utafiti kuhusu madhara ya bangi hebu wafanye na utafiti wa madhara ya viroba. Tufanye utafiti kiroba na bangi ni kipi kinachowaumiza vijana wetu huko mitaani? Mimi naamini huko Usukamani mtu akila bangi analima heka mbili kwa siku. Sasa kwa nini tusiiboreshe tukaangalia madhara yake tukaiweka kuwa zao la biashara? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, humu ndani wako wengi tu wanaotumia bangi tunaweza kutoa mifano na wala hawana shida na ndiyo vigogo kwenye hili Bunge. Sasa kama ninyi wenyewe watunga sheria mnatumia, message imeenda. (Kicheko/Makofi)
WABUNGE FULANI: Aaaaah!
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nizungumzie suala la maji, tunatoka kwenye Ziwa lakini hatuna maji. Tunaamini hii kauli mbiu ya Mama Samia kwamba baada ya miaka mitano akinamama hawatahangaika na suala la maji itatekelezwa. Tuusimamie vizuri Mpango huu ili uweze kwenda sambamba na kauli ya Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwaambie ndugu zangu wa Upinzani, tunapofika humu sisi wageni tunawashangaa. Tulipokuwa kule nje nilikuwa nikiwaona watu fulani sitaki kuwataja nahemkwa kusikiliza, lakini ukikaa humu ndani naona kama watu mnacheza maigizo. Mtu anasimama hapa anasema watu kondoo, wanaoitwa kondoo wenyewe wanashangilia, tunawafundisha nini watu wanaoangalia Bunge?
TAARIFA
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.
MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma, samahani Taarifa, Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Kuhusu bangi au?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mchango mzuri unaoburudisha anaotoa mchangiaji Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, napenda kuumpa taarifa kwa sababu ameuliza kuhusu utafiti kwamba bangi ama mihadarati ya aina ya mirungi ina madhara gani kwa binadamu. Kitaalam napenda kumwambia bangi pamoja na mirungi inasababisha kitu kinaitwa alosto maana yake ni kwamba ukitumia kwa muda mrefu ile addiction ikazidi kwa muda mrefu unaweza ukaugua ugonjwa wa akili unaojulikana kama cannabis-Induced psychosis. Kwa maana hiyo, bangi ina madhara kwa afya ya binadamu na siyo vyema sisi kama viongozi tukatafuta namna yoyote ile ya kuchangia ili kuhalalisha kwa sababu za kiuchumi.
MBUNGE FULANI: Mwambie aache kuvuta bangi.
MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma Taarifa hiyo unaipokea?
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea lakini nataka pia nimwambie afanye uchunguzi na viroba navyo pengine vina madhara zaidi ya mirungi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la bangi, sigara na bia...
MWENYEKITI: Una dakika mbili zimebaki malizia.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo hizo nazitumia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana unaona hata upande wa pili kuhusu huu mwongozo wa Mheshimiwa Kigwangalla hawauungi mkono. Naomba tuendelee kufanya uchunguzi wa kina. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia pia suala la elimu bure. Ndugu zangu wa Upinzani tumwogope Mungu, pengine ninyi hamtoki huko na wala hamjapokea taarifa kutoka kwenye shule zenu, hebu fanyeni ziara kwa kukashifu hili neno la elimu bure. Kaka yangu mmoja alikuwa anaomba Mwongozo hukumpa, hebu nenda kule Usukumani ukazungumze hayo mambo watakushangaa.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu bure ndiyo sera yetu na hata Wabunge wengine wa CHADEMA na Madiwani wanaunga mkono, kwa nini tusibadilike, huu ni mwanzo. Kama ameahidi Mheshimiwa Rais elimu bure miezi mitatu au siku mia moja utamaliza matatizo yote? (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani ndugu zangu wa Upinzani wajazie nyama, zungumzia upungufu unaouona katika suala hili ili Serikali iyachukue ikafanye marekebisho tukirudi Bunge lijalo tunamsifu Rais kwa mpango wa elimu bure.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hotuba ya mambo ya nje.
Kwanza nianze kwa kumpa taarifa tu kidogo mzungumzaji aliyemaliza kwa kutambua umuhimu wa Wabunge makini wa CCM wageni…
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hotuba ya mambo ya nje.
Kwanza nianze kwa kumpa taarifa tu kidogo mzungumzaji aliyemaliza kwa kutambua umuhimu wa Wabunge makini wa CCM wageni…
tunategemea kwenda kuomba Marekani, ameingia kigogo hataki kwenda Marekani mnamlazimisha kusafiri, hela zipo hapa hapa. Na nataka niwaambie ninyi ndio makuwadi wa wezi wa hela za Tanzania na mtabanwa mpaka mtaeleweka tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia umezungumza ukasema kwamba kuna watu wanapewa Ubalozi kama shukrani, huko kwenu huko watu wamepewa Ubunge kama shukrani hawajawahi kusimama hata kwenye jukwaa mbona husemi? Mbona husemi kwamba kwenu kuna watu wameokotwa hawajui hata CHADEMA ikoje wamepewa Ubunge; wewe umetoa mapovu miaka mitano umekuja kupambana Jimboni kuna watu wamepewa bure kule, hebu bisheni tuwataje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa tumewazoea hawana jipya, watu hawa wanatuchonganisha na Mabalozi; wanasema Mabalozi wetu ni sawa na Mabalozi wa Nyumba Kumi…
Ngojeni mje muugue mkienda India ndio mtajua…
Tuna Mabalozi waliosoma wala hawakupewa shukrani, achana na taarifa Mzee acha nimalize…
Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu ni mwenzetu pengine anataka kuniongezea nondo…
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kusema Mheshimiwa Msigwa ili utambue…
Kama ni muongo anasema Wabunge wa East Africa hawapewi mikopo ya magari sijui…
MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma naomba ukae.
Taarifa...
MHE. JOSEPH K MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipokea, Mheshimiwa lakini message imeenda. Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Msigwa amesema Wabunge wetu wa East Africa hawapewi magari, pengine hana kumbukumbu sahihi na aliwataja nilitaka wangekuwepo pale wakamdhihirishia Wabunge hawa wa East Africa wanapewa mikopo ya magari kama tunavyopewa sisi na wana exemption ya magari mawili na ndio maana gari zao zinaandikwa namba za Ubalozi, wewe msomi gani huelewi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninarudia kusema kwamba kwa hali ilivyo Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Magufuli ilivyojipanga hawa hawana cha kusema zaidi ya kutoka nje. Na mnasema kila anaposimama Mheshimiwa Dkt. Tulia, Mheshimiwa Naibu Spika mtatoka nje, tokeni; kama mlizoea Spika ambaye hafuati kanuni mlizitunga wenyewe wenyeji sisi wengine ni wageni. Tunakuomba Mheshimiwa Naibu Spika simamia Kanuni hawa watoke nje; tunawataka watoke nje kila siku tena ukae asubuhi tu kile kipindi cha live wafyatuke wakae wenyewe humu ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sina mengi naomba kuishia hapo.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwa ufupi dakika tano. Nianze kwa kumshukuru mdogo wangu Mlinga kwa kunitaja pengine na mimi kesho naweza kuwa mahabusu kwa amri ya Makonda. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie tu na mimi kwenye sehemu ya dawa za kulevya. Niliwahi kuchangia wakati nazungumzia kuhusu bangi na mirungi, nilieleza Taifa hili lina vyombo vya ulinzi na usalama, tuna Polisi, Usalama wa Taifa, Majeshi, vyombo vinavyoweza kutujua tabia zetu na vina utaalamu wa kuweza kumfuatilia mtu na kugundua kama kweli hiki kilichosemwa anahusika nacho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napata mshtuko sana kwa hiki kinachoendelea, ni haki yangu kuzungumza kama Mbunge, kama Waziri Chikawe akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani alisema ana orodha ya wauza unga, ameingia Mheshimiwa Kitwanga akatuaminisha mwezi mzima anataja, amewapa siku 21, hawakutaja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Taifa linafanyia kazi orodha ya Makonda, napata wasiwasi. Hii ndiyo tulikuwa tunaisubiri awamu zote kuanzia kwa akina Marehemu Amina Chifupa kwamba hawa ndiyo waliofanyiwa uchunguzi wakakutwa kweli wanauza dawa za kulevya? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kweli ndivyo, basi hili Taifa tunakokwenda hatuendi sawasawa. Hivi kweli Watanzania tunaambiwa kuna msururu wa wauza dawa za kulevya wamekamatwa anatajwa Chid Benz na Ray C, watu ambao Taifa hili limeingia gharama ya mabilioni kumsaidia Ray C na watu walichanga kwenye M-pesa, mgonjwa unamchukua unamtia mahabusu, hatuko serious kumaliza suala la dawa za kulevya. (Makofi)
Mhehimiwa Mwenyekiti, hili tuongee lugha moja wote kwa pamoja kuondoa hata uvyama, wauza dawa za kulevya wanajulikana na hata wengine walio vigogo wa kukamata wenzao wanashinda nao na wanawasafirisha kwenda Marekani. Kwa nini vyombo vya ulinzi na usalama visimhoji Makonda, mtu ambaye siyo mfanyabiashara ameenda Marekani, Paris, Dubai kwa mshahara wa u-RC huu? (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani ndugu zangu hiki kitu lazima tupate muda tuzungumze. Mheshimiwa Rais mimi nakuunga mkono, inawezekana Mheshimiwa Rais ana uchunguzi sahihi kuliko wa Makonda. Kama amesema kila mtu akamatwe hata mke wa Rais akamatwe na Makonda aanzie wa kwake aliowapangishia majengo. Kwa nini wa kwake wako nje na wametajwa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Dar es Salaam mitaa ya wauza unga inajulikana…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Musukuma, muda wako umemalizika.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Makao Makuu ya CHADEMA ndiyo wauza unga wamejaa pale mateja.
Tunaenda kuchukua mateja tunajaza magereza.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kuwapa pole wananchi wangu wa Jimbo la Geita Vijijini ambao watoto wao wamefariki kwa ajali ya kuzama kwenye Ziwa Victoria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anazozifanya, lakini pia nimpongeze sana kwa kumteua Profesa Maghembe kwenda kushika Wizara ya Maliasili na Utalii. Lakini sitakaa nimpongeze Maghembe hata siku moja kama hajabadilika, aliyemteua nampongeza, lakini Profesa Maghembe sitakaa nimpongeze hata siku moja.

Waheshimiwa Wabunge, sisi tunaotoka kwenye majimbo ya vijijini kuna matatizo makubwa hata ya Ikwiriri nikwa sababu yanaandikwa kila siku kwenye magazeti. Lakini kwa sisi ambao tunaishi pembeni mwa mapori tuna matatizo makubwa na ndio maana nasema siwezi kumpongeza Profesa Maghembe kwa yafuatayo; kwanza kwenye Halmashauri zetu tumepitisha sheria, mwananchi akiwa na nusu debe, gunia moja tu la mkaa haruhusiwi kukamatwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hebu nenda Ofisi za Maliasili, kumejaa baskeli tunasubiri sijui hata hiyo minada mtamuuzia nani hizo scrapers za baiskeli, watu wameshikwa na gunia moja au madebe mawili anakamatwa na ananyang’anywa baskeli, ananyang’anywa pikipiki yake. Sasa hivi sisi kwetu Kijijini ukiona gari ya Maliasili bora ukajitundike hata kwenye mti kuliko kusubiri kile kipigo utakachokipata.

Mheshimwia Mwenyekiti, lakini mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Maghembe ya Maliasili, napata shida sana kujiuliza labda sisi Kanda ya Ziwa tulikuja kwa bahati mbaya kwenye hii Tanzania. Mbona yanayofanyika Kanda ya Ziwa, kule Kanda ya Kaskazini mbona hayafanyiki wakati na wao wana mapori. Waziri ametoa siku tatu tukamatiwe ng’ombe kwa kisingizio ng’ombe ni za Wanyarwanda. Wakati huo huo watumishi wake wanaowaingiza Wanyarwanda wanawaambia toeni ng’ombe wale Wanyarwanda, mnaenda kukamata ng’ombe za Wasukuma, halafu mnazipiga mnada, na Wabunge mnada wenyewe unavyopigwa ni wa deal.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ng’ombe 600 unaambiwa lete shilingi milioni tatu wanatoa watu wao Ubungo, halafu nakupongeza kwa sababu gani. Na mimi nataka nikwambie Profesa Maghembe kama Mwenyekiti King, tunajua mipango inayofanyika kwenye Wizara yako na nimewapigia kabisa watumishi wako, mtumishi mmoja anaitwa Masaro mwingine anaitwa Kidika, ananiambia mliipenda wenyewe, kwa kauli yake kama Mwenyekiti wa Chama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kesho yake akapiga ng’ombe za watu mnada, ng’ombe 500 zinauzwa shilingi milioni tatu, kwa nini msituite sisi ambao wenye ng’ombe tunashindwa kutoa milioni tano. Halafu mnasimama humu mnaipongeza Wizara kwa sababu gani, nataka nikuambie Profesa inawezekana ninyi mmesoma na Mungu amewasaidia hamjui uchungu wa kufuga ng’ombe kuanzia moja mpaka kumi. Hamjui watu tumeshindwa kwenda shule kwa sababu ya kuchunga ng’ombe tukawasomesha ninyi mkawa Maprofesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na sisi Wasukuma sasa tumeamua, na nimezungumza uelewe, tutaziroga hizo ng’ombe mtavimba matumbo mnaozila huko Dar es Salaam. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani kwa nini wanunuzi watoke Dar es Salaam peke yake, yaani leo siku ya mnada watu wametoka na malori Pugu, wanajuaje kama wanakuja kushinda kwenye mnada! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnatukamatia ng’ombe hivi hii Serikali imekosa sehemu ya kukusanya hela mpaka mkanyang’anye ng’ombe za wafugaji, haiwezekani Mheshimiwa Maghembe hata kama utanielewa vibaya lakini huo ndio ukweli. Kuna manyanyaso makubwa, mwananchi wangu wa Bukombe amepigwa risasi ya jicho hakuna fidia, aliyempiga yupo, halafu mimi nakusifu kwa sababu gani! Haiwezekani na ninaomba sana haya maneno yaingie hivo hivo nilivyoyaongea.

T A A R I F A...

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa mikono miwili, nasubiri na nyingine kama hiyo. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumwambia tu Profesa kwamba ingekuwa ni mimi nateua yaani katika Mawaziri walio-fail wewe ni namba moja. Sijui ni wewe ama ni watu wanaokuzunguka ni mfumo wa hiyo Wizara sielewi. Inawezekana vipi Mheshimiwa Waziri mtumishi wako kabisa anayelipwa mshahara na Serikali unampigia simu mimi kama Mwenyekiti wa Chama namwambia kuna tatizo gani kwa nini msikae na hawa watu mkawapa ng’ombe hata wiki moja wauze watoke. Anasema hili ni agizo la Rais, hivi Rais kabisa huyu tunayemjua mwenye upendo na maskini anaewajengea watoto wa Dar es Salaam maghorofa, anayewapa watu hela, anaetoa misaada, anatuuzia ng’ombe sisi kwa sababu gani, kwa nini wasiseme watumishi wako kuwa wewe ndo umewaagiza. Na kwa nini yafanyike Kanda ya Ziwa tu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeenda Loliondo na Kamati, unataka kuwatoa wafugaji kwenye Pori la Loliondo kwa kisingizio wanaharibu ili umpe Mwarabu tukakutalia mbona hujaenda kuwanyang’anya kule, haiwezekani na hiki kitu haitawezekana. Kwa mara ya kwanza nitatoa shilingi hata kama ziko nne zote nitaondoka nazo. Nitatoka shilingi lazima uje na majibu ya msingi ni kwa nini mnatudhulumu mali zetu. Hivi kwa nini msingetupa hata kipaumbele kwama mnataka kukusanya hela za kuuza ng’ombe za watu, kwa nini msitupe kipaumbele mkatuambie njoo tarehe fulani saa fulani wote tukapambana kwenye mnada, kwa nini wanunuzi watoke Dar es Salaam?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vitu vingine vinauzi potelea mbali hata kama tutatoka humu tumenuniana lakini message imeenda inauma sana. Kwa wale waliozaliwa kwenye ufugaji mmesomea ng’ombe, ng’ombe inalelewa kama binadamu, kwa nini ng’ombe wa Tanzania anageuka kuwa adui. Akiingia Serengeti mnakamata, hivi mlishawahi kuona ng’ombe amekula Simba, kwanza ng’ombe ni chakula cha wanyama hata digidigi ng’ombe hali. Ana madhara gani ananyanyasika ng’ombe wa Kisukuma?

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua sheria pengine zinamlinda Mzee Maghembe lakini hivi vitu vinauma sana, wewe leo ukienda ku-draw hela kwenye akaunti yako ukakuta hakuna hela kuna zero, utachanganyikiwa utawekaje hata mafuta kwenye gari. Ukituuzia ng’ombe ndo benki yetu sisi ambao hatukusoma tuliishia darasa la saba, ukilima pombe una nunua ng’ombe halafu tena ng’ombe unakuja mna- deal na watu wa Dar es Salaam. Sisi tumefuga ng’ombe ili wakale watu wa Dar es Salaam, sitaunga mkono hoja yako kabisa Mheshimiwa Maghembe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, mimi nina Hifadhi kwenye Jimbo langu la Geita inaitwa Rubondo, ina Sokwe Mtu wameletwa miaka ya 1962 wanafundishwa kukutana na binadamu. Na kuna watu wanakula posho kila siku na Wizara inatoa hela. Umri wa sokwe kuzeeka yaani maisha yake niliwahi kuuliza wataalamu wakasema miaka 45 mpaka 50. Leo sokwe hawa bado wanafundishwa yaani umri wao umezidi na bado wanaishi kwa huruma ya Mungu lakini sokwe bado hawajaanza kutizamwa. Lakini kingine Maghembe, hifadhi yetu na yenyewe ni ya miaka mingi, tunahamasisha watalii wanaenda kule, kuna gari moja tu juzi umepeleka mbili haitoshi, watalii wakienda 30 mpaka wasubiriane na wakati wamekuja timu moja. Kwa nini msiongeze gari kama zilivyo kule kwenye mbuga zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Ngorongoro huko Kilimanjaro zimejaa, kwa nini usipunguze ukaleta kwenye mbuga zetu hizo ambazo hazina usafiri na watalii wanataka kwenda huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine uwekaji wa mipaka wamezungumza na wenzangu, Mheshimiwa Waziri toka Dar es Salaam zunguka huko vijijini uje uone beacon za watu wako walivyoziweka. Sijui mna huruma ya design gani au mnataka kuipanga Tanzania kwa style nyingine. Haiwezekani vijiji vipo toka mwaka 1974 watu wamezeekea hapo wametoka maprofesa hapo na wengine ma-king kama mimi halafu unakuja kuniwekea kigingi katikati ya kijiji changu. Halafu na simama hapa nakuunga mkono, sitaunga mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine Profesa kuna Tume ya Wizara sita, mbona majibu yake hayatoki? Sisi tunasubiri hiyo Tume ambayo imezunguka kisanii sanii wala haijatuhoji mmeulizana wenyewe na Wakuu wa Wilaya hatujapata majibu, umeleta kutuuzia ng’ombe. Tuelekeze wapi tuzipeleke ng’ombe zetu kama unataka tuziue tununueli kwa bei tuliyofuga nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, nikiendelea hapa naweza kutoa machozi halafu huyu Mzee akapata laana. Ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia. Kwanza kabisa niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi nzuri inazoendelea kuzifanya kwa kuweza kunipandishia barabara ya halmashauri ambayo iko kwenye jimbo langu yenye urefu wa kilometa 80 na kuipeleka Serikali Kuu (TANROADS). Pia, kuweza kunipandishia Kituo cha Afya Nzela na sasa kuwa Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kutoa mfano kabla sijachangia. Jamaa wawili walikuwa wanabishana mchana kweupe, saa sita. Mmoja anamwambia mwenzie hili joto lililopo linaletwa na lile jua pale juu, mwingine anasema lile sio jua ni mwezi. Sasa wakati wanabishana jua na mwezi, wamevaa vizuri na suti na tai, akapita mama mmoja wakamuuliza mama tunaomba utuamue, hili ni jua au ni mwezi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, yule mama akawaangalia wamevaa vizuri kabisa wastaarabu, akaona dawa yao ni kuwaambia jamani mimi sijui akaondoka. Wakaendelea kubishana akapita baba mwingine, walivyomwona wakasema awaamue wakamuuliza baba tusaidie, hili ni jua au ni mwezi? Saa sita mchana, akawaangalia juu mpaka chini, ni wastaarabu kabisa, akawapa jibu tu kwamba, jamani mimi hapa ni mgeni, akaondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunachosumbuka nacho humu ndani ni huo mfano kwamba, wanaona kabisa hili ni jua, lakini wanang’ang’ana kusema huu ni mwezi. Hata mngejitetea vipi Mheshimiwa Mpango hawawezi kukuelewa hawa, watakwambia ni mwezi na wakati ni saa sita mchana. Kwa hiyo, dawa yao wewe waambie hapa ni mgeni, ili uende vizuri na safari ya kutuletea maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme nchi hii ina misingi mizuri sana na sisi wenzenu tumekuwa wavumilivu toka miaka ya sabini na kitu wakati nchi hii inatengenezwa. Leo ukienda Kanda ya Kaskazini utakuta lami zinaenda kuishia kwenye migomba ambako hakuna uhitaji, sisi watu wa Kanda ya Ziwa hatukupiga kelele kwa sababu, tulijua Serikali inatengeneza maendeleo kwa awamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukienda Kilimanjaro unakuta kuna KIA, ukienda Moshi Mjini kuna uwanja mdogo, ukienda Arusha kuna uwanja mdogo. Sasa hapa kumetokea mambo watu wanapiga kelele katika Uwanja wa Ndege wa Chato. Nataka niwaambie, Mheshimiwa Waziri hizi kelele ziache waambie wewe hapa ni mgeni. Napendekeza mkimaliza kujenga ule uwanja wa mkakati wa Chato, jengeni mdogo Geita, kama ulivyo wa Moshi, ili tuwe na viwili hesabu ya kulilia uwanja ujengwe Geita iishe, kinachowauma mimi sikioni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri na Serikali inisikilize katika viwanja ambavyo ni vya mikakati, ukiwemo na Uwanja wa Chato, Songwe na Mtwara, imarisheni. Huwezi kwenda kujenga uwanja wa ndege Iringa, kuna ndege inabeba magogo hapa? Tunatengeneza viwanja vyenye kupandisha uchumi wa nchi. Geita tuna dhahabu, tuna samaki ambao hata ndege ikitua itabeba, hakuna Boeing inabeba magogo kupeleka China, kwa nini tunaanza kuchambana humu ndani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Uwanja wa Ndege wa Chato, nawashangaa sana Wabunge wa Kanda ya Ziwa, Mbunge wa Biharamulo, Mbunge wa Karagwe, Mbunge wa Kasulu, Mbunge wa Muleba, mnaacha watu wanashambulia uwanja wa Chato. Sisi tungekuwa na tamaa tungeujenga uwanja ule Geita Mjini, lakini impact ya uwanja ni biashara, hawa wote hamuwezi kwenda tena Bukoba mnakaa humu watu wasiojua hata ramani wanashambulia kwa ku-google kwenye mtandao, kwa nini msisimame mkatetea? Leo mtu wa Biharamulo utaenda Bukoba uwanja uko Chato? Mtu wa Ngara? Mtu wa Muleba? Mtu wa Kasulu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kwa tabia zetu Wasukuma hatuna upendeleo tunagawanaga keki na ndio maana tumeweka katikati kama mlivyoweka ninyi pale KIA. Kwa hiyo, nawaomba sana suala la ku-discuss Uwanja wa Chato acheni Mpango wa Serikali ufanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Chato kilometa 30 tu kuna hifadhi pale inaitwa Rubondo, lakini tuna dhahabu pia, palepale Chato. Hata ukiangalia historia, msiofahamu, Chato, Mkoa wa Geita kila mahali kuna uhitaji muhimu; ukienda Geita sisi eneo lote la Geita mnalolipigia kelele kuna wazungu wanachimba under ground sasa hivi, ukienda kwangu sisi tunavua na kulima. Sasa kama tumechagua eneo ambalo lina usalama angalao wa miaka 200 mbele mnapiga kelele bila kujua, mnataka uwanja ukawekwe kwenye mahandaki yanayochimbwa under ground? Acheni Mpango wa Serikali ufanye kazi, jadilini matatizo ya mikoa yenu. Hamjatumwa humu kuja kutetea uwanja wa ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri ameliweka vizuri kwamba, mtajenga na Moshi, mtajenga na Tanga; yote haya uwanja huu ungekuwa unajengwa Moshi wala kulikuwa hamna kelele humu, lakini niwaambie tumekuwa wavumilivu vya kutosha. Chuo Cha Madini ambacho kimejengwa na GGM, GGM iko Geita, kwa kuwa tu ninyi mlikuwa kwenye madaraka mka-divert mkapeleka chuo kikajengwa Moshi; dhahabu itengenezwe Geita mkajenge chuo chetu moshi, tumekaa kimya. Tusianze kufukua makaburi humu tunaelewa mengi sana. Tusianze kufukuliana makaburi na nawaona watu wa Kanda ya Ziwa mnasimama kubwabwaja kuhusu mambo ya Kanda ya Ziwa, mnatumika kama matela. Tutakutana 2020 labda ule mtindo wenu wa kunini na kunini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kuhusiana na suala la mahindi. Naiomba sana Serikali ishikilie msimamo wake wa kutokuruhusu mahindi yasiende nje, mimi nakuwa tofauti na Wabunge wenzangu. Nataka niwaambie na Serikali ina system, hebu tumeni system huko kunakolalamikiwa kuna mahindi kama utakuta mahindi ya mnyonge yako pale. Tunakuwa na Bunge la kujadili mabwanyenye walanguzi, wakulima wa mahindi..

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila mpangilio)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mnisikilize nyie mmechangia mie nimekaa kimya; wakulima wa mahindi kuna mabwanyenye wanaowekesha gunia 15,000/= wakati wanaanza kupanda, wakishamaliza kuvuna yanachukuliwa yale mahindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hata huko Sumbawanga kuna watu tunanunua nao mahindi 35,000/=. Yaani tunakuja na katimu ka kutetea mabwanyenye, tumeni watu mkaone mkulima mwenye magunia 150 au 30, 10 kama ana mahindi. Halafu mimi ni Mbunge wa Kanda ya Ziwa ambapo mahindi yalikuwa yanauzwa Sh.110,000/= leo tunauziwa mahindi Sh.60,000/=, nikubali mahindi yaende nje ili turudi kwenye Sh.110,000/=? Shikilia msimamo, mtu anayetaka kufanya biashara koboa unga, peleka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri Mheshimiwa Keissy ametoka, wakati tunatetea ng’ombe alisema mang’ombe yauzwe, sasa yeye kwenye mahindi hatutoi mahindi, Serikali isilegeze kaza uzi. Mnaona kama mzaha, ruhusuni, fanyeni hesabu kuyaruhusu haya mahindi yaende nje, yakienda nje haya mahindi mwezi wa kwanza hili Bunge tunaanza kujadili njaa.

T A A R I FA . . .

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namheshimi sana. Mimi ni Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na bahati nzuri kwenye jimbo lake mimi nanunua mahindi. Hawa watu muwe mnatafuta reference twende ukatuoneshe, mkulima tunayemtetea humu ndani ni mkulima anayelima kwa jembe la mkono, hatuwezi kutetea walanguzi...

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila mpangilio)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie kidogo suala la mazao na maliasili. Nimpongeze sana Mheshimiwa Kigwangalla ameanza vizuri, hakuna Waziri atakayepambana na wanyonge akabaki kuwa Waziri. Wanyonge wana machozi na machozi yanasikilizwa na Mungu na mifano mmeiona. Simamia uzi huohuo wa kutetea wanyonge. Kumeibuka mambo tunaomba atusaidie; watu wana miaka 10 wanaishi maeneo ya porini, halafu leo wanaibuka tu wataalam wanaenda wanachoma nyumba, tunakubali chomeni nyumba, chakula ambacho kimebakiza mwezi mmoja kivunwe wanafyeka na kuchoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namhakikishia Mheshimiwa Waziri asipodhibiti hili, hii ndio laana yake ya kwanza kabisa. Awaambie wawaache wananchi wetu wavune kwanza chakula ndani ya miezi miwili, halafu wawadhibiti kuingia mle ndani. Sisi kama Wabunge wawakilishi hatuwezi kuwa na wananchi ambao wana njaa. Bahati mbaya sana tumetoka kwenye njaa, Mungu ametupa neema watu wamelima, chakula kimebaki miezi miwili, mitatu DC anaonekana kwenye TV anafyeka chakula na kuchoma tena kama shujaa, halafu sisi Wabunge tumekaa kimya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Mheshimiwa Waziri Kigwangalla tumeona aliyoyafanya Loliondo.
Achunguze, hata hizi operations…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishauri kwenye dhahabu. Niliwahi kumshauri Mheshimiwa Waziri kwamba, mzee huwezi kupambana na wafanyabiashara wadogowadogo ambao wanatorosha dhahabu yetu ambayo ni nyingi kuliko hata inayosafirishwa na migodi. Ushauri wangu, hebu aondoe ile asilimia tano ya kodi ya wachimbaji wadogowadogo, a-deal na watu wa migodi mikubwa ambao wao hawawezi kukwepa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa watu wa mifukoni kuwadhibiti ni ngumu sana na yeye kwenye bajeti yake aliwahi kukusanya milioni 88 tu, hebu aruhusu dhahabu iwe free market kama ilivyo Dubai, kama ilivyo Uganda, watu wa Kongo, wa Zaire, wa Burundi walete dhahabu Tanzania, sisi tupate asilimia moja peke yake ya kusafirisha dhahabu, hatapambana na hao watu anaowakamata bandarini na watu watamwonesha kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namshauri sana watalaam wake wakubali kuachia free kwenye dhahabu humu ndani liwe soko la uhuru, Waganda walete. Leo hii Uganda ni asilimia 0.5 nani atakubali kuja kulipa asilimia 6.0, si afadhali niifiche kwenye soksi, sasa atakamata wangapi kwa mwaka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ajaribu kuangalia kama anaweza kutoa hiyo asilimia tano abakize asilimia moja tu ya kusafirisha. Hatakamatana na watu tutamletea dhahabu kama anavyotaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa
nafasi niweze kutoa mchango wangu.
Kwanza nianze kumpongeza sana Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu kwa kazi nzuri
waliyofanya katika kuandaa taarifa yao. Pia nimpongeze Waziri na Wizara yake, wamekuwa
wakifanya vizuri sana kwenye barabara zetu za Geita kwa ujumla, tunaona kazi za TANROADS
zinavyofanyika vizuri, hatuna mashaka. Lakini zipo changamoto ndogo ndogo ambazo
tunaiomba Wizara iweze kuzipa kipaumbele barabara ambazo tayari Mheshimiwa Rais wa
Awamu ya Tano akiwa Waziri alianzisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya kutoka Geita kwenda Kahama, lakini na
barabara ya kutoka Bwanga kwenda Biharamulo na kwenda Runzewe, yakikamilishwa haya
ataongeza tija sana kwenye Mkoa wetu wa Geita. Pia nimuombe Waziri aendelee kuona
huruma zile kilometa 57 tulizoahidiwa kwenye Jimbo la Geita Vijijini, sisi wenzenu huko
tulikozaliwa vijijini hatujawahi kuona lami kabisa, tunaiona mjini tu kwa wale ambao wanapata
bahati ya kusafiri. Sasa angalau kwa mwaka huu ukianza hata kilometa moja/mbili na sisi
tukapata kuzungumza kwamba tunaanza kuingia kwenye dunia ya Awamu ya Tano.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini kwa
kazi nzuri ya kuandaa taarifa pamoja na changamoto mbalimbali mlizokumbana nazo. Niiombe
Wizara pamoja na kwamba wametuwekea umeme kwenye Jimbo la Geita Vijijini, tumepata
umeme mijini tu, kwenye vijiji vingi ambavyo vinazalisha hasa vya wakulima, umeme haukuingia,
lakini tumeahidiwa kwenye REA Awamu ya Tatu mtatukumbuka. Nimuombe Waziri kwa huruma
yako uwaangalie wananchi wa Jimbo la Geita Vijijini katika vijiji ambavyo tumeviomba
viingizwe kwenye REA Awamu ya Tatu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kushauri, nimekuwa nikizungumza hapa mara nyingi
kuhusiana na suala la wachimbaji wadogo kwenye Mkoa wangu wa Geita na kwenye Jimbo
langu la Geita. Wananchi wa Geita wamekuwa na kilio cha muda mrefu sana na awamu zote
tumekuwa tukiahidiwa, Awamu ya Tano ilipofika tulipomuomba Mheshimiwa Rais aliona huruma
na akaturuhusu tupewe magwangala. Sasa nimuombe ndugu yangu Mheshimiwa Profesa, ni
kweli ulivyotuahidi kwamba mnang‟ang‟ania kuomba magwangala mtakiona cha moto, sio
mchezo tuliona cha moto kweli kweli maana badala ya kupewa magwangala tulipewa mawe
ya kujengea nyumba. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikawaambia ndicho ulichokiahidi kwenye mkutano kwamba
tutakiona cha moto, tulivumilia tu, tumekula hasara na wananchi wangu sasa hawana tena
shida na magwangala kama ulivyosema. Wamenituma nikuombe kwa kuwa eneo la GGM ni
kubwa na wewe ni mtaalam wa miamba ninaamini hutarudia tena kuwapa kwa sababu sisi na
wananchi wangu wote ni darasa la saba kule, hawana utaalam wa miamba kule sisi tuna
utaalam moko tu kuchimba. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe kwa kuwa wewe ni Profesa, term hii basi usirudie
kuwapa na wewe ule mwamba wa mbali kama uliowapa mwaka 2012, uwaangalizie
Nyamatagata na Samina walipokuomba. Ni sheria, sasa imeshapita miaka mitano, wamege lile
eneo ambalo wachimbaji wangu wakienda na la saba lao wakichimba tu wakifika kwenye
magoti angalau wawezi kupata hata dhahabu kidogo kidogo kufidia yale machungu ya
SACCOS zile ulizoziunda wewe. Kwa kweli cha moto tumekiona, na tumeamini Profesa wewe ni
bingwa kwa sababu wa darasa la saba tumefeli kwenye hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe tu Mheshimiwa Waziri, kumekuwa na kilio cha
muda mrefu sana kwa wananchi wa Wilaya ya Geita kwenye eneo la STAMICO, na eneo
linalopiganiwa ni dogo sana na wewe ulivyokuja kule term hii ulituahidi leseni zile zinaisha mwezi
wa tisa, tunazisubiria, ama uwape wazungu au uturudishie, hapo hatutajali cha Profesa
tunaanguka la saba kwa nguvu mule.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nikuombe sana usi-renew hiyo leseni bila kumega
eneo ukatupa la saba na sisi tukapate riziki pale, tumelia mara nyingi Rais ametuahidi,
umetuambia kuna kesi ya Sinclair lakini Sinclair, wewe unazo message kwenye mtandao wake
anamtukana mpaka Mkuu wa nchi, kwamba anaendesha nchi kibabe na unaijua hiyo email,
lakini bado unasema tukimnyang‟anya ile atatupeleka mahakamani.
Sasa kama muda wake unaisha mwezi wa tisa wallah nakwambia la saba tutakaa pale,
yaani ikifika tarehe 27,28 tunaanguka porini. Na ulituahidi ukajisahau ukatamka na tarehe,
bahati nzuri la saba huwa hatusahau tarehe, tunasahau kila kitu tarehe 28 tuko kwenye lile
eneo, tutalichukua kwa nguvu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niliona mchakato wa EWURA wakati anatumbuliwa
Mkurugenzi wa EWURA nikawa najaribu kujiuliza, hivi kweli kwa nini Mkurugenzi wa TANESCO
anatumbuliwa peke yake na Wakurugenzi wale wengine, ni kwa sababu kweli walifanya vikao
mpaka wakakubaliana na EWURA bila Profesa kupita kuona documents zile? Nikawa
nashindwa kuelewa, nikasema ipo siku ntapata nafasi, ninayo document ya Mheshimiwa
Profesa Muhongo ambayo yeye mwenyewe anamwandikia Mheshimiwa Dkt. Mpango tarehe
30, Septemba akimpelekea mpango kazi wa TANESCO, na wameweka mapendekezo yao
humu ndani ukihitaji nitakupa kama unahitaji wanamuomba EWURA kufikia mwezi wa 12 awe
amepandisha umeme, na yeye ameisaini hii document, iko saini yako hapa usitikise kichwa
ntakukabidhi Mheshimiwa.
Baada ya mwezi wa 12 amevua koti tena akawasakizia wenzie, na saini yake iko humu.
Naomba sana hebu tuangalie tusiwe tunatumbua tu watu.
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, lile la wachimbaji wadogo…
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, lile la wachimbaji wadogo kupelekwa kupewa ruzuku ya Katavi…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Musukuma muda wako umekwisha. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia.

Kwanza kabisa naipongeza sana hotuba ya Waziri Mkuu kwa kazi nzuri iliyofanyika. Pia nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoendelea kuwafanyia Watanzania. Hata ukiangalia michango ya Wapinzani, imebaki mambo machache ambayo naamini baada ya bajeti hii, watakaa sawa tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilishasema humu ndani kwamba mimi ni darasa la saba; na humu ndani tuna matabaka tofauti, inawezekana ni vizuri zaidi kila mtu akatetea wenzie. Nampongeza Mheshimiwa Rais alipoenda pale bandarini akiwa anazungumza na watumishi wa Bandari kuhusiana na suala la vyeti fake na wale walio-forge kutoka darasa la Saba kuwa na vyeti vya form four, alitamka waziwazi mchana kwamba wale wote walio-forge vyeti kutoka darasa la saba kwenda form fourwafukuzwe kazi, lakini wale walio na vyeti vyao vya darasa la saba na kazi wanazozifanya wanafanya vizuri, waendelee na kazi, kila mtu alisikia na suala hili lilisemekana lilizungumzwa mchana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa humu ndani kuna wasomi wengi, lakini pia kuna wa darasa la saba wengi na huko nje hata ninyi wenye degree humu ndani, kuna ndugu zenu wa darasa la saba ambao walikuwa wameajiriwa hizo ajira ndogo ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaishauri sana Serikali yangu, ninashangaa ni kwa nini wamewafukuza Watendaji wa Vijiji wa darasa la saba. Wanataka hizi nafasi za darasa la saba, hizi za utendaji wapewe watu waliotoka Vyuo Vikuu. Ni wapi? Ni Wilaya gani? Ni Kijiji gani ambako mmepeleka Mtendaji graduate akaweza kufanya kazi akawazidi darasa la saba? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefukuza madereva, hivi niwaulize ndugu zangu Waheshimiwa Mawaziri, wewe unasomesha mtoto wako English Medium kwa hela nyingi anaenda sekondari, form six, Chuo Kikuu, akitoka Chuo Kikuu tena akawe dereva? Hivi tunafanya mambo gani ya ajabu? Ninaomba sana Serikali yangu tena na Wabunge wenzangu wa CCM tuitake Serikali itoe tamko la kuwarudisha watendaji hawa kwenye kazi, siyo kuwalipa. Haiwezekani mtu amefanya kazi toka mwaka 2004, unakuja kumfukuza leo. Hatuzungumzi suala la kulipwa mafao, warudishwe kazini watoke kwa muda wao wa kustaafu na hili limefanyika hata kwenye Majeshi. Kwenye majeshi enzi hizo, watu walikuwa wanachukuliwa darasa la saba, leo wengine ni Mameja, wengine ni ma-OCD, wameachwa mpaka wastaafu. Iweje Watendaji tunawafukuza? Mtu amebakiza miaka miwili, unamfukuza! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuiombe Serikali iwarudishe. Kama Serikali itakaidi, mimi nataka niwape ushauri, kwa sababu humu ndani kuna Wabunge kama sikosei 100 na zaidi wa darasa la saba, siyo la saba tu, hata form four failure wamo, vyuo vikuu wenye vyeti havieleweki wamo humu ndani. Ninaomba sana Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi mnisikilize vizuri, ni kwamba kama hamwezi kuwarudisha hawa Watendaji na sisi Wabunge wa darasa la saba humu ndani mtufukuze. Halafu siyo kwamba mtufukuze, kwa sababu ukiangalia…

T A A R I F A . . .

MHE. JOSEPH K MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sioni kama ni taarifa, lakini record yako inajulikana Chuo Kikuu ulikuwa na kazi gani. Sasa unaweza ukawa ni wewe mmoja wao. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sioni hata sababu ya Wabunge wa darasa la saba kuwa humu ndani na wale wenye vyeti ambavyo nimevitaja, ni bora katiba ikatuondoa humu ndani. Mkituondoa, mturudishe kwa Viti Maalum kama makundi mengine yaliyoko humu ndani, kwa sababu na sisi tuko wengi wa darasa la saba. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitaka kuangalia, hebu naomba uangalie tu ukurasa wa 49, kipengele cha elimu ukisoma namba 80 pale waliodahiliwa kuingia darasa la kwanza walikuwa milioni mbili, waliodahiliwa kutoka darasa la saba kwenda form one mpaka form four ni 500,000. Kwa hiyo, darasa la saba tena wamekuwa wengi kuliko walioenda sekondari. Ukiisoma hii taarifa, haikufafanua kutoka kwenye 500,000 kwenda chuo kikuu utakuta kuna 100,000. Kwa hiyo, ukipiga hesabu ya kawaida, sisi tuko asilimia 85. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ukiangalia walipakodi wakubwa Tanzania na Mheshimiwa Mipango na Waziri wa Viwanda yuko hapa, wajasiliamali wanaolipa kodi kubwa na wenye viwanda vingi ni darasa la saba. Hebu asimame hapa anitajie mtu mwenye kiwanda anayelipa kodi Serikali mwenye chuo kikuu hapa. Wote tumewaajiri, halafu sisi tunakuja tunatozwa kodi, tunaonekana hatufai hata kwenye kazi zinazolingana na elimu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuomba sana, kama tunaondolewa kwenye Katiba, nasi tuwekwe kwenye kundi la Viti Maalum kama wanawake na walemavu, nasi tuwakilishe, twende hivyo hivyo na kwenye Baraza la Mawaziri. Kwa sababu tunakosa wawakilishi kwenye Baraza lenu ndiyo maana mnataka kuwatoa hawa watu.

Naiomba sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi, kwa hili Waheshimiwa Wabunge tuungane kwa pamoja, ondoeni hata uvyama kwa sababu hawa darasa la saba mna shangazi na wajomba zenu waliofukuzwa, mkijipigia makofi wenye Chuo Kikuu wachache tutakutana 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka nizungumze suala la uvuvi. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, suala hili hiyo operation nilizungumza kipindi kilichopita, operation ina maana nzuri na hakuna mtu anayekaa kwenye Kanda ya Ziwa aneyeshabikia uvuvi haramu. Ila uendeshwaji wa zoezi haukufuata haki. Tunazo mpaka risiti za watu wa Wizara, mtu ametozwa shilingi milioni 20 halafu risiti ikaandika 2,015, tunazo. Kwa nini mnakuwa wagumu kuunda Tume ya kuwachunguza hawa watu. Kuna Bray sijui kuna Sokomba huko Wakurugenzi, ni miradi wametoa watu wao Dar es Salaam kuwapeleka kule, wanachukua hela za watu wetu. (Makof)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri iundwe Tume ikachunguze zoezi hili. Nataka nikwambie kwamba ujasiriamali anaohamasisha Mheshimiwa Rais, sisi darasa la saba tunaupokea kwa hali na mali. Kuna watu leo wako Sirari pale, wamepewa vibali vya Serikali na Wizara ya kuleta mitego; mtu amepewa kibali mwezi wa Tano, mwezi wa nane, akaanza process za mkopo, akapata hela mwezi wa kumi na moja, akapeleka order. Amerudi hapa mwezi wa kwanza. Serikali imekagua ikasema iko sawa, Wizara ya Uvuvi, TBS sawa; kodi ikalipwa, kesho yake Mheshimiwa Waziri Mpina amesema mitego isitoke. Nimefuta vibali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu mtu mpaka leo anaendelea kutozwa storage ya pale Sirari. Hakuna huruma, halafu mnahamasisha watu wafanye kazi. Ndugu zangu naomba sana, Mheshimiwa Waziri hebu unda Tume ichunguze suala hili la uvuvi. Kiukweli sisi watu tunaotoka maeneo ya uvuvi, mnatupa wakati mgumu sana kuzungumza na watu wetu. Hamfanyi haki. Naombeni sana iundwe Tume. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, nilikuwa naomba kuishauri Serikali, katika uchumi wa Mheshimiwa Dkt. Magufuli anataka tujitegemee sisi wenyewe kwa kulipa kodi, tuachane na wahisani, lakini hizi sheria ambazo tunazitumia, ni za Kiingereza ambazo zinataka sisi tuendelee kuwa Watumwa wa Wazungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe mfano, kuna sababu gani kijiji ambacho kama Mjumbe mmoja aliyechangia kwamba watoto wa shule wanatembea kilometa 11, wananchi wamehamasishana, wamejenga madarasa mawili, matatu wakajenga Ofisi ya Mwalimu, wakajenga choo kizuri na mazingira mazuri. Wizara inakataa kufungua, inasema mpaka tufikishe madarasa saba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule inaanzaga na darasa la kwanza, siyo darasa la saba. Ziliwekwa zile sheria ili tuendelee kukopa, tukamilishe kila kitu, tutaanza vipi? Umejenga madarasa mawili, unaanza na darasa la kwanza, mengine yatajikuta shule imefunguliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo hivyo, kuna sheria ambayo imewekwa inasema Kituo cha Afya hakiwezi kuwa Hospitali ya Wilaya. Ni hizo hizo sheria za kuendelea kufanya sisi watumwa tukakope hela kwa Wazungu. Kama tunatumia hizi hizi hela zetu za kupeana shilingi 200/shilingi 300/=, mimi Kituo changu cha Afya kinapungukiwa majengo mawili, kwanini ile shilingi 200 isiki-top kile Kituo halafu kikawa Hospitali ya Wilaya? Tunadanganyana hiki kitakuwa Kituo cha Afya halafu hapo hapo tutajenga Hospitali ya Wilaya, ambapo unaniletea shilingi milioni 500. Miaka 20 mimi nimeshakufa, Ubunge simo, nani anapata hiyo faida?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali na Wawaziri mfikirie upya kuangalia hizi sheria za kuendelea kutufanya sisi tuwe tegemezi. Kama tunajitegemea wenyewe, turudi kwenye kile ambacho tunaweza kukifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la Wizara ya Viwanda, Mheshimiwa Waziri Mwijage naomba sana kwa ushauri wangu hata nchi za China tunaenda kule, hawakuzingatia sana mambo ya viwango ndiyo maana wamefika hapa, ndiyo maana ukienda leo utapata shati la Tanzania, utapata shati la Marekani bei inakuwa tofauti. Sasa kuna kitu mnasema gauge 32, gauge 34, ushauri wangu kwa Mheshimiwa Waziri tuachie hata gauge 38 hata 40 kulingana na umaskini wa Watanzania watu wetu Wasukuma wanataka wauze mahindi anunue bati aezeke nyumba, wewe uking’ang’ana na hiyo size yako ya gauge 30 mbona kwenye Matembe na majani huendi kuzuia?(Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. Nampongeza sana rafiki yangu Mheshimwa Khatib kwa maneno mazuri sana leo aliyozungumza lakini hata vitabu vya dini vinasema umpende jirani yako kama unavyojipenda wewe mwenyewe. Kwa hiyo, maneno matamu aliyoongea na mazuri yenye usia mzuri kama Mtanzania halisi angeanza kwanza kushauriana na majirani wakimsikiliza kwamba ushauri wake ni mzuri sisi wa mbali tutapokea bila wasiwasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nichangie upande wa biashara ya madini. Sisi tunatoka kwenye maeneo ya madini, nilitaka nimpe ushauri kaka yangu Mheshimiwa Mpango, biashara ya madini ni ngumu sana na kodi iliyowekwa kwa mchimbaji wa kawaida ni asilimia saba, maana yake loyalty asilimia sita na export levy ni asilimia moja na wachimbaji wameitikia wito wa kulipa hiyo kodi, hawana tatizo. Wanapomaliza kulipa hizi kodi unawarudishia tena dhahabu wakauze wao wenyewe, haijalishi ina ukubwa wa kiasi gani. Sasa hawana uwezo wa kupeleka Kenya, pengine hawana passport, hawana nini wanaenda kuuza kwa watu wa kawaida, lakini baada ya mwaka unakuja tena kuwakamata unataka wakupe document ya ku-export ile dhahabu, biashara ya dhahabu ya dola moja faida yake ni shilingi 15,000 au 20,000 mtu hawezi ku-afford kwenda kuuza dhahabu Kenya au wapi, anauza humu ndani kwa watu wa kawaida anaendelea na biashara yake. Baada ya mwaka unakuja kumwambia tunaomba document za export levy na kama hauna utulipe 18% ya VAT.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu hiki sio sahihi na ninyi Serikali mimi nawashangaa kwa sababu unawezaje kuchukua dhahabu ukaitoza kodi halafu ukamrudishia mwenyewe akauze huku mnahangaika na kangomba, mnahangaika na kahawa, kwa nini msinunue hii dhahabu mkaiweka stock kuliko kuhangaika na mbaazi na kangomba hawa wanaotusumbua. Mnachukua hii kodi mnaenda kuhangaika na kangomba Mtwara. Nakuomba sana kama kuna uwezekano sisi tumeitikia kulipa kodi vizuri muichukue hii dhahabu, muiweke stock kwa sababu dhahabu haishuki bei kama hizi kangomba tunazohangaika nazo humu ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nilikuwa nazungumzia suala la upanuzi wa viwanja vya ndege. Mheshimiwa Waziri ninakuomba sana katika viwanja hivi ambavyo kiukweli vinaisaidia shirika letu kama Mwanza na Mbeya, tengeni pesa ya kutengeneza hivi viwanja tuache maneno ya kusema kila siku kitu ambacho hakitekelezeki.

Mimi nataka niwape mfano Waheshimiwa Wabunge wanaotumia uwanja wa Mwanza, ukienda ndege ya jioni inapoenda Dreamliner inaenda na watu zaidi ya 200, Wasukuma wameitikia kuchangia nchi yao. Inaenda FastJet na watu 100, inaenda Precision Air ina watu 70, mnapoteremka kwa wakati mmoja ni aibu, Mheshimiwa Waziri usipite VIP hebu pita huku wanapopita watu wa kawaida, ni msongamano ambao kile kichumba kinaweza kupokea wageni 30, kinapokea watu zaidi ya 400 na kama hatuna hela basi mruhusu tuweke hata maturubai maana kuna mvua na kuna vitu vingine, lakini nikuombe ujaribu kuangalia uwezekano wa kuwahisha ujenzi wa nyumba ya kupokelea wageni pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine Mheshimiwa Waziri, tunakubali kabisa kwamba tunahitaji nchi yetu tulipe kodi na tuchangie kwa kutumia EFD machine. Mimi najiuliza hizi hesabu wanazopiga pengine Wakuu wa Mikoa na Serikali inaruhusu, ukikaa hapa Dodoma ikifika saa 5.00 usiku karandinga inazunguka, kalaleni. Wageni wakija hapa, sasahivi nchi imehamia Dodoma unaweza ukaja kumuona Waziri, huna kazi nyingine hamjui mtu, ukaambiwa utamuona Waziri kesho kutwa, inabidi ukae kusubiri, kwa hiyo, mchana wote unaambiwa ukakale baa hazifanyi kazi, vitu vingi vimefungwa, kuna tatizo gani? Kwani mnaambiwa na nani kwamba, mkiwalaza watu saa 5.00 usiku wanaenda kulala?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pengine watu wanaingia vyumbani wanajifungia, lakini mngeruhusu watu wakanywa bia watachangia pesa. Watu wakiingia kwenye ma-guest watapewa risiti. Tuache huu ukiritimba wa kuwalaza watu saa 5.00 usiku tujifunze kwenye nchi zinazoendelea. Sio kwamba, mkiwalaza watu saa 5.00 usiku ndio itakuja hela, tunapoteza pesa kwa vitu ambavyo tunataka kujiuliza tuna wasiwasi gani kwamba, ma-group ya majambazi yana nguvu kuliko polisi wetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye usafiri mnataka magari yasisafiri mwisho saa 5.00 usiku. Mtu anataka afanye kazi Mwanza aende akanunue vitu Dar es Salaam, polisi ni wengi wafanye doria na magari yaruhusiwe pia kutembea usiku na mchana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la viwanda. Suala la kufungua viwanda Tanzania kiukweli mnahamasisha vizuri na Rais wetu anafanya kazi nzuri, lakini sijui kama mnajua hizo adha zilizoko kwenye ufunguzi wa viwanda; unafuata procedure zote TIC, ukienda TIC pale OSHA yupo, migration yupo, taasisi zote zipo, lakini hazina mandate ya kuruhusu. Ukimaliza kujadili pale tena wanabeba makaratasi kumtafuta Waziri aweke muhuri, hiyo ni miezi sita.

Ukiruhusiwa kufungua kiwanda tena anakuja mtu wa mazingira anafunga, mtatuua na madeni tutauzwa na benki, jaribuni kutengeneza utaratibu mwingine. Jaribuni kuangalia hivi vitu vyote viishie TIC pale kuna kila kitu kiko pale, kwa nini tunawasumbua wawekezaji wetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri mimi juzi wakati imetangazwa kwamba kutakuwa na mdahalo wa wanachuo kikuu pale wanaojadili uchumi, sikutoka nje na niliweka mpaka tv huko jimboni kwangu watu waone Serikali ilivyofanya kazi, lakini haya mambo huwa ninazungumza kila siku wasomi wetu ndio tatizo mnapotufikisha. Mimi nilidhani mtachambua na kuwaeleza watu kwamba, uchumi wetu kutoka miaka mitatu alipoingia Rais Magufuli tumefanya hiki kwenye kitengo fulani, tumefanya hivi kwenye dhahabu, tumefanya hivi kwenye nini, badala yake tena wasomi wetu mmeenda kuchambua tu hotuba za Rais ndio mmetuwekea kwenye tv. Maana yake Rais wetu anafanya kazi nzuri, wasomi wakubwa mmeshindwa kuwaelimisha watu wakajua tulikotoka na tulipo kelele hizi zikaisha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnaenda kuchambua maprofesa wazima mnachambua hotuba za Rais zilezile ambazo Mheshimiwa Rais Magufuli anatueleza na tunampenda kwa sababu hiyo hiyo. Nilikuwa naomba sana maprofesa mliomo humu, ikitokea tena mnafanya huo mjadala mtukumbuke na darasa la saba tuna akili za kushauri kuliko za kwenu za makaratasi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nataka kuchangia kuhusiana na biashara ya sukari. Nimesikia kuna wafanyabiashara kule Kahama na wapi wamekamatwa. Mimi najiuliza hebu mfanye utafiti, issue hapa sio kukamata wafanyabiashara, watu wanarudishwa maisha yale ya kawaida na ninasikia Wabunge wengi kila mtu anasimama anasema hali ni mbaya hali ni mbaya, ningekuwa nategemea kila Mbunge aseme Rais alegeze wapi, pesa zilizopotea ni zile za wizi na kanjanja, haya maisha sisi tumeyazoea vijijini siku zote wala hatuna tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pesa zilizopotea sio kwamba labda ziko kwenye biashara ya sukari, mimi nikiuliza leo ukisema sukari sijui inaletwa kutoka nje, kama biashara ya sukari inaletwa kutoka nje wanafanya re-bag wanaweka kwenye mifuko ya Tanzania tumuite na mtu wa biashara ya majani ya chai tumuulize naye kama anauza na yeye biashara ni mbovu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi niombe tu haya mambo bya mabadiliko ya tabia ambayo sasa hivi Watanzania tunaishinayo tutapata taabu sana kuyaelewa kama tutakuwa hatufanyi research za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala lingine nilikuwa nataka kuzungumza kuhusiana na suala, niliwahi kuzungumza humu watu wengi wakanicheka na sioni ajabu kuzungumza, suala la bangi. Mnaona na bahati nzuri mimi natumia simu ya tochi, ninyi wote humu wengi mna simu za whatsapp, za mitandao hizi na nini, ukiangalia Canada juzi wameruhusu, foleni iliyokuwepo haijawahi kutokea utafikiri wanachagua Rais wa nchi, kwenda kununua bangi iliruhusiwa hadharani, ukienda Lesotho, ukienda Zambia, ukienda South Africa hivi vitu vimeruhusiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka niwambie wataalam mnaofanya research mnasema bangi ina matatizo, mimi sio mvutaji, ina matatizo, mnaokula diclopa, mnakunywa coca cola, red bull, hizi zote ni bangi ni ganzi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kupata muda wa kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza sana Serikali, lakini pia kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa aliyoifanya pale bandarini. Kwa kipindi cha miezi ya nyuma pale, Waheshimiwa Wabunge wengi walilalamika humu ndani kwamba bandari yetu sasa watu wameikimbia wameenda Beira na Mombasa, lakini kwa jitihada za Serikali tumeweza kufanya vizuri, sasa hivi bandari yetu ipo vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo, nataka kutoa ushauri kwa Mheshimiwa Waziri. Bandari yetu ya Dar es Salaam wateja wetu wakubwa ni watu wa Congo, Zambia, Malawi na nchi nyingine. Tayari watu wengi wameshaingia mikataba na wasafirishaji wa Tanzania, nasi Watanzania wengi tumechukua mikopo tukanunua magari na miundombinu mingine kwa ajili ya kupata hiyo mikataba ya kusafirisha hayo makontena kutoka bandarini na kwenda huko Congo na Zambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa utaratibu aliouweka Mheshimiwa Waziri, ni kwamba sasa tunaenda kuiua kabisa Bandari ya Dar es Salaam, totally inaenda kufa. Watu wengi wa Congo na Zambia watakimbia bandari yetu ya Dar es Salaam watahamia Beira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfanyabiashara anapoenda kununua bidhaa kule nje, kontena linabeba uzito wa tani 33 na tayari nao wameshafunga mikataba na viwanda kule nje. Sasa ukija ukibadilisha ghafla, maana yake ni lazima akukimbie kwa sababu hawezi. Pia walio na mikataba, tayari wameshasaini mikataba ya kubeba tani 33. Sasa naona Serikali imeenda kusaini mkataba na nchi za East Africa kama Kenya, Burundi na Uganda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania hatuna biashara ya transport ya moja kwa moja na Kenya. Kenya ndiyo mshindani wetu mkubwa kwenye bandari. Kwa hiyo, kilichoingiwa hapa ni kutaka kututoa kwenye mood halafu watu watarudi Mombasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu Wakenya wao wana sheria hiyo ya magari yenye tairi mbili toka zamani, lakini sisi tunakopeleka kama Zambia na Malawi, wao wanatumia super single. Sasa Serikali inapokuja leo kusema tu ghafla tubadilishe kutoka kwenye super single twende kwenye tairi mbili, haiwezekani, utaua watu na pressure. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana, jitihada ambazo zimefanywa na Mheshimiwa Rais kuifufua bandari yetu ya Dar es Salaam, ni vizuri wataalam, tunaamini mmesoma vizuri, lakini hebu jaribuni kufikiri nje ya box, maana pengine hizi degree za makaratasi zinatusumbua, mtaua watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana wajaribu kukaa na wadau ambao wameweza kumiliki hivi vyombo watusikilize. Naamini wasafirishaji wengi, ukitafuta Tanzania nzima wenye degree nyingi, wengi ni Darasa la Saba. Sasa kwa style mnayoenda hii, hamjatusikiliza, wala hamjapata experience. Kwa hiyo, ni vizuri mkapata muda wa kuwasikiliza. Hizi sheria hamtungii magari, mnamaliza kutunga sheria, inaanza kutula sisi wenyewe na wengine wamo humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, ni vizuri tukaacha kubeza jitihada za Rais, hizi sheria ngumu ambazo zinaenda kuua bandari yetu, ni vizuri tukaziangalia upya na ikiwezekana tuziache, hazitusaidii katika Serikali inayotaka kukua kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ni-declare interest, mimi nafanya biashara ya mabasi, nazungumza kwa ajili ya watu wenye mabasi. Biashara ya mabasi ni kubwa sana na unaweza ukaona mtu anamiliki mabasi 30, lakini hakuna mtu anayenunua basi kwa cash, wote wanakopa. Hata hizo installments tu za shilingi milioni tano kuzipata kwa mwezi ni shughuli kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria zilizowekwa, mtu anafanya kosa moja, anapigwa faini ya shilingi milioni tano. Tafsiri yake sasa ninyi mnataka kumchonganisha Mheshimiwa Rais na wasafirishaji. Haiwezekani mtu kama alikuwa anapigwa faini ya shilingi 30,000/= na shilingi 250,000/=, ika- shoot kutoka hapo kwenda kwenye shilingi milioni tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri apate muda, aache kupuuza mawazo ya wadau, aanze upya kuzungumza na wadau wamweleze kero zao na awasikilize. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo tatizo la mabasi. Nampongeza Mheshimiwa Kangi alivyoanza alisema sasa mabasi yasafiri usiku wote. Unajua ni kitu cha kushangaza! Ukienda kwenye nchi tunazopakana nazo, watu wanasafiri usiku; na dunia hii imebadilika; na nchi hii inaenda kubadilika kuwa nchi ya viwanda. Sasa unataka watu walale. Najiuliza, ni kitu gani ambacho kinashinda Serikali kutengeneza utaratibu wa kuruhusu magari yasafiri usiku?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kweli hiyo ndiyo sheria kwamba mabasi yataleta matatizo? Mbona treni inasafiri usiku? Ina maana hata tukianza kutumia treni ya Stiegler’s Gorge hiyo, itasafiri mwisho saa saba? Si lazima ifanye kazi usiku na mchana? Watu wanataka kufanya kazi Dar es Salaam walale Morogoro au Dodoma halafu saa kumi waondoke kurudi Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba, kama tatizo ni usalama, afadhali kama Jeshi letu limepungukiwa Askari, tuchukue hata JKT wapewe semina wakae barabarani, gari zisafiri usiku na watu wawe na uhuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda nchi nyingine tunaona. Sisi tunasafirisha kwenye nchi za East Africa, wenzetu wamefanyaje? Mabasi hayaingii mizani. Mabasi kuyaingiza mzani ni ku-create tu rushwa, hakuna basi inayozidi zaidi ya shilingi 30,000/=, shilingi 15,000/=. Kwa nini, Serikali isione umuhimu wa kuondoa hii sheria ya mabasi kupita kwenye mizani? Kwanza mnaleta usumbufu kwa abiria, mnasababisha watu wanachelewa kwenye kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri Serikali ikaangalia vitu ambavyo vimetukwamisha tuviondoe, twende kwenye Serikali ya kuvutia na watu wengine waje kufanya kazi hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine naona huko kwenye usafirishaji, pia Idara yake katika Wizara ya Miundombinu, sasa hivi ukienda Dar es Salaam wameondoa Hiace kule mjini, hata ukija Dodoma leseni ya Hiace ikiisha hawataki, ukienda Mwanza hawataki. Mimi najiuliza; na nilifanya research ndogo tu. Ukienda kule Dar es Salaam, pamoja na kuziondoa zile gari (Hiace) kule ndani, lakini watu wanasimama kwenye daladala, wanatoka safari wanasimama, gari zinabeba watu mpaka 110, lakini watu wanapanda bodaboda na bajaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti iliyofanyika ya kuziondoa Hiace mimi sioni kama ni halali. Sana sana ni kwamba tumewaonea wale wafanyabiashara. Ukiondoa Hiace ina matairi manne, mbona sisi gari zetu za Mawaziri zinaruhusiwa kupita kule? Kama ni hivyo na hizo gari ziondoke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye nchi nyingine zilioendelea, magari yana umbali wake ya kuwekwa; yape magari ya binafsi, wote tuning’inie kwenye daladala moja ndio mwone huo uchungu wa kuziondoa hizo gari huko ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa naishauri Serikali, pale ambapo tunakuwa hatuna umuhimu wa kushikiria sheria ambazo zimepitwa na wakati, leteni amendment humu tuziondoe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumze kidogo kwenye ndege. Kwa bahati nzuri mimi ni captain. Unajua nikisema mimi ni Darasa la Saba watu hawaelewi! Mimi ni mtaalam wa kurusha helicopter. Kwa hiyo, lazima niwaambie kidogo hapa. Pamoja na huo ungo pia naweza kurusha. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilimsikiliza dada yangu, Mheshimiwa Ester Bulaya hapa, alilalamika kwamba marubani wetu wa Tanzania wanabadilishwa tu kutoka bombadier kwenda airbus kwenda dreamliner, jamani hili sio basi, ndege ni kitu kikubwa sana. Captain wa ndege hawezi kuruhusiwa kutoka kwenye ndege moja kwenda kwenye ndege nyingine bila kupewa training na kupewa leseni ya kuendesha ile ndege. Hata kwanza wale airbus wasingewaruhusu kuwapa ndege rubani wa bombadier akaendeshe ndege ya airbus au dreamliner. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ndiyo mabadiliko ambayo pia na wenzetu wanatakiwa wayakubali, kwamba zamani tulizoea kuona marubani wazuri ni Wazungu, sasa hivi vijana wetu wamesoma vizuri, tunawapongeza. Kwa hiyo muwe na imani kwamba hawa watu wamepita kwenye training na wana leseni za kuweza kuendesha hiyo ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia limezungumzwa suala la faida; ndege huwezi ukaona faida leo. Sisi tunafanya usafirishaji, ukitaka kujua faida ya ndege, asimame Mchumi hapa aniambie, kama hutaona kuingiza kwenye hela uniambie wale ile ndege iliyowabeba, wale waliowahi Dar es Salaam wamepata faida gani na kule walikoenda kununua. Kwa hiyo ina components nyingi, lazima tuvumiliane tu, mtakuja kupata utaalam zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia mapendekezo ya mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango kwa kazi nzuri unayoifanya, wenye macho tunaona. Na usitegemee kusifiwa na kila mtu Mzee Dkt. Mpango, nikuombe usikate tamaa, tufanyie kazi. Sisi wenye uhitaji na msaada wako na akili yako bado tunayo imani na tunaendelea kukushauri uendelee kupiga kazi, Watanzania tunakuamini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikiliza wasomi wetu hawa, amesema Waziri aliulizwa faida ya ndege akasema dola milioni 14, nilikuwepo kwenye kupokea ile ndege, ni sawa milioni 14 lakini kama msomi alitakiwa kuelimisha umma faida ya ndege haiji kwenye ndege peke yake, vipo vitu vingi ambavyo kwa kupitia ndege tulizozileta tumeshapata faida. Ingetokea muda wakataja faida zote ambazo baada ya kuleta ndege. Sasa tatizo ndio hili Mheshimiwa Heche unazungumza halafu unakimbia, ungekaa humu ukasikiliza.

Angeweza kupata fursa ya kuambiwa faida ambazo tumeshapata kwenye hizi ndege, haya maneno hayatakiwi kuzungumzwa na mtu msomi kama hawa. Ndio maana tukisema vilaza watu mnaanza kutuzomea humu ndani. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Taarifa.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma naomba muendelee tu.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba tumshauri ndugu yetu Mheshimiwa Dkt. Mpango. Tunaona kazi ambazo mnazozifanya za kuweza kubuni vitu ambavyo kiukweli kila mtu anafurahia Serikali ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwana ushauri mchache; Serikali imeamua kurudi Dodoma, ni lazima tubuni vitu ambavyo baada ya miaka mitano tunaona sasa hivi Dodoma inaenda vizuri kwenye makusanyo labda kwenye kuuza viwanja na kodi za majengo lakini tungebuni vitu ambavyo baada sasa ya hivi vitu kuisha tuwe na kitu cha kudumu hapa Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, Mheshimiwa Waziri tungeweza kutengeneza bandari kavu Dodoma, kukawa na ICD Dodoma ambapo makontena yanayoenda Rwanda na Burundi yawe yanachukuliwa Dodoma hapa hapa. Tutakuwa tumetengeneza chanzo kikubwa kwanza kwenye treni yetu itakuwa inatoa makontena kuleta hapa lakini tutapata ajira ya malori kusafirisha makontena kuleta hapa na malori ya Burundi na Rwanda hayataenda tena Dar es Salaam, yataishia Dodoma na kurudi. Tutakuwa tumefungua chanzo kikubwa sana kwa wananchi wa Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, naishukuru pia Serikali, katika watu waliofaidi kwenye Awamu ya Tano na mimi naweza nikajisifu nimefaidi. Ile kauli ya Mheshimiwa Rais ya juzi kwamba halmashauri zote zirudi kwenye maeneo ya wananchi, Halmashauri mojawapo ni ya Geita DC ambayo imerudi Nzela naipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba kukueleza tu Mheshimiwa Mpango kwamba kwenye mpango sasa uweke, tumekubali tumerudi kwenye nyumba hizohizo tunabanana. Kuna halmashauri ambazo tayari walikuwa wana pesa wameshaanza kujenga lakini kuna Halmashauri ambazo hatukukuwa na bajeti kabisa kwenye kipindi hiki, tumerudi sasa tumeamua kuanza lakini kwenye mpango ujao tunaiomba Serikali ifikirie namna yoyote ya kuweza kutuma pesa kwenye hizi halmashauri ambazo hazikuwa kwenye huu mpango wa kujenga majengo ya halmashauri na nyumba za watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nilikuwa napenda kushauri pia kwenye suala la viwanda. Tunaipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuhamasisha viwanda na kuja na Sera ya Viwanda, lakini nilikuwa na ushauri mdogo. Mawazo ya Mheshimiwa Rais ya kusema tuwanyang’anye viwanda watu ambao wameshindwa. Ni mawazo mazuri, lakini ninyi Wasaidizi wake, mngeenda mbali zaidi mkafikiria. Kabla ya kuwanyang’anya viwanda, mngewanyang’anya mawazo yao kwanza; mkawaita mkawasikiliza, mkawauliza ni kwa nini walikwama kuendeleza viwanda? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna mtu anayeweza kuingia pressure ya kukopa fedha kwenye Taasisi za Benki ukafungua kiwanda halafu ukakitelekeza. Haiwezekani! Lazima kuna sababu zilizopelekea watu wakashindwa kuendesha viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakupa mfano. Twende wazi tu, awamu iliyoisha haikuwa na mfumo wa kuendeleza viwanda vya Tanzania. Huwezi ukafungua kiwanda ukazalisha kitu ukakiuza shilingi 1,000/= halafu kinaletwa kutoka China kinauzwa shilingi 200/=, kwa vyovyote vile lazima utakimbia tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, hawa watu ambao walikuwa na viwanda ambavyo Serikali mmevichukua, ni vizuri mkawaita mkawapa nafasi. Mfano ni mzuri tu, tulimshauri vizuri kipindi kile kuhusu dhahabu; na walipowaita watu wa dhahabu wakawaeleza matatizo yao, leo unaona pesa wanazokusanya kwenye dhahabu. Vivyo hivyo Mheshimiwa Rais aliwaita watu kule Ikulu akawasikiliza, wakamweleza matatizo yaliyoko TRA. Leo unaona kila mtu hapa anasimama anasema bandari imejaa makontena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri, hebu awaite hao watu walionyang’anywa viwanda; hata Serikali tunachukua tu viwanda, lakini hatuna alternative. Mmechukua viwanda, leo ni miaka miwili tumevifunga tu; hamwashi mashine, hamna ulinzi, watu wanajiibia tu vitu vya watu. Namwomba Mheshimiwa Waziri awaite, awasikilize, wakwambie wamekwama wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nataka nikuhakikishie, Wafanyabiashara mliowanyang’anya viwanda wako tayari kuandika commitment ya kuvifungua viwanda hivyo kwa sababu Serikali yetu inalinda viwanda vya ndani. Kwa hiyo, nina uhakika hata nikiingia madeni nitazalisha kitu nitauza. Haiwezekani ukasema mimi ninazalisha chini ya target. Utazalishaje kitu hakinunuliwi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri hebu wachukue hawa watu tuliowanyang’anya viwanda, awaite azungumze nao, waandike commitment, wafungue viwanda na ndiyo msimamo wa Serikali ya Awamu ya Tano, Serikali ya Viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nilikuwa najaribu kumshauri Mheshimiwa Waziri, kwenye Mpango ujao, nilikuwa namsikiliza mtu mmoja jana aliulizwa swali, Naibu Waziri wa TAMISEMI akajibu. Mimi natoka kwenye Halmashauri, kumekuwa na purukushani huko, kila Halmashauri inaandika andiko la kujenga masoko, stendi na minada. Mheshimiwa Waziri kama ni chenga mnayotaka kupigwa sasa ni hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania wa hali ya chini hakuna aliye na uhitaji wa soko la kisasa la ghorofa. Tuna shida za maji na barabara. Hakuna aliye na shida ya stendi ya ghorofa. Nikuulize Mheshimiwa Waziri, nanyi wasomi hebu fanyeni research tu ndogo, ni lini mliwahi kuboresha soko halafu mkafaulu? Nakupa mfano, Soko la Machinga Complex mliboresha, leo limekuwa kichaka tu cha kulala wezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkaboresha Soko la Makumbusho, likachakaa na lenyewe mpaka mkalazimisha kuingiza daladala. Haya, tukaenda Mwanza Rock City Mall, tulifukuza watu, leo limechakaa liko vilevile. Namwomba Mheshimiwa Waziri, tubadilike. Hili suala la kutengeneza stendi za kisasa lifanyike na wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa mfano mwingine kwa Mheshimiwa Waziri. Mimi nakaa Mwanza, kuna zaidi ya shilingi bilioni 70 tunajenga Stendi ya Nyegezi iliyokuwa inazalisha, gari zilikuwa hazijabanana tunajenga soko la mjini katikati…

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti taarifa!.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, soko la mjini katikati wanaoteseka ni wananchi.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi hawahitaji soko, wanahitaji kukusanya hela, wamekopa mabenki, unakuja kuwahamisha unawapeleka mjini.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, acha kunipiga taarifa bwana, ngoja nizungumze.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, aarifa!

MWENYEKITI: Mheshimiwa mwache aendelee. (Kicheko)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri uko Mwanza. Kataa haya maandiko ya kuboresha masoko. Masoko ni mapambo ya miji, watu tunataka kutengeneza miradi mikakati. Tunamwomba Mheshimiwa Waziri kama kuna kitu ambacho Serikali hii inafanya na watu wataikumbuka…

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tujengeeni reli, tujengeeni majengo mazuri, hata ukinipa taarifa…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma, subiri akupe taarifa tumsikilize. Haya, Mheshimiwa Stanslaus.

T A A R I F A

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kidogo tu napenda kumpa taarifa mzungumzaji, Mwenyekiti Mstaafu, Mheshimiwa Musukuma, Stendi ya Nyegezi gharama yake na design ni shilingi bilioni 14 peke yake na siyo shilingi bilioni 70. Nashukuru.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema kuna miradi mitatu. Shilingi bilioni 14 Stendi ya Nyegezi, shilingi bilioni 21 soko, shilingi bilioni 20 na kitu Ilemela. Sasa hiyo ni shilingi ngapi? Nauliza hii stendi ya shilingi bilioni ya 14 ina miaka saba tu toka imefunguliwa. Wakati inafunguliwa tuliambiwa stendi mpya. Sasa hivi imekuwa kuukuu, tunajenga mpya pale pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, naomba sana tujikite kwenye matatizo ya wananchi. Hatuwezi kuwa na maandiko ya kuboresha stendi. Nami nataka niwaambie tu wale Wabunge wanaotoka kwenye maeneo ya kawaida, twende Nzega pale kwenye Stendi ya Bashe pale alipojenga, wale mnaopita pale, hizo ndizo stendi za kukusanyia hela. Hakuna mtu aliye na urafiki na stendi. Stendi ni sehemu ya kufika mtu unasafiri. Huwezi kuzunguka ghorofani, utaachwa na basi. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri tu, haya maandiko na yanakuja haraka haraka, wakati sisi tunataka kwenda kwenye uchaguzi. Kama kweli ndiyo, basi mlete pesa tujenge kwa force account, lakini haya mambo ya kuruhusu maandiko, yanatosha hayo; waliobahatisha basi, walioliwa waliwe, hakuna kuongeza tena hela. Tuchimbie maji, tutengenezee miundombinu ambayo kiukweli Watanzania wengi tunahitaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, Mheshimiwa Waziri hataachwa kusemwa, acha usemwe lakini watu tunajua kazi unayoifanya. Suala la uchaguzi, mimi natoka Kijijini na kwangu sikupitishi Jimbo zima. Nawapa mfano hawa Wapinzani, kosa kubwa mlilolifanya ni kushindwa kwenda kuelewesha watu wenu jinsi ya kujaza fomu.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mnakula bata kwenye mitandao huku, watu hawajui kujaza kule! Wanaandika CHADEMA, wala hawajui kujaza Chama chao full. Mimi nina watu kwenye Jimbo langu, ameulizwa kirefu cha ACT, hajui kuandika. Ungekuwa ni wewe na Kanuni unazo, ungefanyaje? Mmekalia ku-tweet, mitandao, nendeni kwenye Majimbo yenu mkafundishe watu wenu. Mkiendelea hivyo, hata kwenye Ubunge tunagonga mageni kama hayo. Nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwa mara ya kwanza. Niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu katika kutoa pole kwa wananchi wa Arusha.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwaangalia rafiki yangu Mheshimiwa Kangi Lugola, ameondoka; naanza kwa kuunga mkono hoja, nami ndiye nitakayeongoza ile sauti ya ndiyo ambayo atazunguka nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Rais, pia nampongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kazi nzuri wanayoifanya kwenye Idara ya Maji. Sisi wengine ni waathirika wa miaka mingi na tunaona mabadiliko yanavyokwenda kwa speed. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niko tofauti kidogo na Waheshimiwa Wabunge wenzangu wanaosema tusipitishe, hela ni ndogo. Binafsi yangu naona hii hela ni nyingi sana, tatizo itoke yote. Kwenye bajeti ya mwaka 2016 ukisoma ukurasa wa 13 utaona tulipitisha shilingi bilioni 915 lakini mpaka leo ni shilingi bilioni 181 tu. Kwa hiyo, Wizara ya Fedha wakitoa pesa yote, hii pesa ni nyingi wala hata hizi kelele hatutazisikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu cha pili, kwenye Ilani ya CCM tumeahidi kumaliza matatizo ya maji, lakini hatukuahidi kumaliza mwaka huu peke yake, bado tuna miaka mitano. Kwa hiyo, kazi zilizoahidiwa kwenye Ilani ni nyingi, wala siyo moja na kila mahali tunataka pesa. Sisi tunataka barabara, tumepiga kelele tunataka afya, tunataka watoto wasome bure; kwa hiyo, hizi hela ni nyingi, tuziunge mkono, wala tusiwasumbue, tuwape nafasi waende wakafanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine, mimi nashangaa wana-CCM wenzangu, jana nimesikiliza mchango wa Mheshimiwa Kitwanga analalamika anasema yeye ataenda ku-mobilize wananchi 10,000 wakazime mashine. Nilisikitika sana! Nataka niwaulize ninyi Mawaziri wa Mheshimiwa Dkt. Magufuli, hivi vile viapo mnavyovila mnavifahamu maana yake? Kama hamvijui sina hakika kama mko sawasawa na kama hamko sawasawa Mheshimiwa Ndalichako hebu apitishe operation ya vyeti, pengine na kwenyewe kuna feki za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, inawezekana vipi mtu aliyekuwa Waziri anasimama anasema kwa kuwa nilikuwa Waziri, nilikuwa nimebanwa kuzungumza. Kwa hiyo, sisi ambao hatuzungumzi kwa kuwasaidia ninyi, tumebanwa na nani? Anasimama anasema nilikuwa nimebanwa, sasa nazungumza, naenda kuunganisha wananchi 10,000 wakazime mashine ya Ihelele. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwakumbushe kidogo, mwaka 2014 Mheshimiwa Kitwanga nilitegemea atakuwa pale. Akiwa Waziri wa Nishati na Madini, aliyekuwa anashughulika na mambo ya madini, alikuja Geita, mimi kama Mwenyekiti wa Mkoa niliwalazimisha wananchi wasitoke mpaka walipwe na Mzungu. Yeye akaja, akamwambia Mkuu wa Mkoa, hata kama kuna Mwenyekiti wa Mkoa, piga mabomu. Kweli kesho yake tulipigwa mabomu!

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimwambie Waziri wa Mambo ya Ndani, siku anaenda kuunganisha wale wananchi, apeleke mabomu Misungwi pale, aonje joto la jiwe. Haiwezekani Waziri aliyeapa kiapo, akitimuliwa anakuja humu anatuchanganya sisi wengine ambao hatujui mambo mnayoongea kwenye Cabinet.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ndugu yangu Mheshimiwa Nape yuko hapa, jana alichangia…

Hakuna kuogopana humu, anayeguna nani? Mimi ndio nachangia. Ndugu yangu Mheshimiwa Nape aliyekuwa Mwenezi wangu wa Taifa, jana alizungumza mambo mazuri, lakini kuna moja alisema tusipowatekelezea suala la maji wananchi, hawataturudisha, haiwezekani! Wananchi wa Tanzania wanatutegemea kwa mambo mengi wala siyo maji peke yake na tumewafanyia vizuri. Hata hizi Ilani hazijaanza kuzaliwa kwenye Awamu ya Tano, tumepitisha awamu nne, zote zilikuwa zinaandaa hayakamiliki. Kwa hiyo, suala hapa siyo kulazimisha Ilani yote ikamilike. Rais gani aliyewahi kutekeleza asilimia mia moja ya Ilani? Tusibebeshane mzigo! Wewe ulikuwa unaongea nilisikiliza, sikiliza! Kwa hiyo, tupeane nafasi, Rais wetu anafanya kazi nzuri, tusianze kumchambachamba humu ndani. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri aliyoifanya pale Geita. Tulikuwa na malalamiko ya awamu mbili. Leo ukifika Geita, hatujawa na asilimia mia moja lakini tuna nafuu. Tuna mradi wa shilingi bilioni sita; uko asilimia karibia 85, halafu tusimame hapa kuiponda Serikali ya Awamu ya Tano, kwa miaka miwili! Haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Wabunge wamo humu akina Mheshimiwa Mnyika, unataka tumalize tatizo la maji leo, kwa nini haisemi population ya Dar es Salaam? Wakati anaomba maji Awamu ya Kwanza alivyokuwa Bungeni, Jimbo lake lilikuwa na watu wangapi? Kila siku binadamu wanaongezeka, hatuwezi kumaliza tatizo hili kwa awamu moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tuipitishe bajeti hii kwa speed, tushauri tu kwamba Wizara ya Fedha iachie fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongee kidogo kwamba tumeona mfano kwa CEO wa DAWASCO; hivi Mheshimiwa Waziri watu kama hawa, wamesifiwa mpaka na Kamati, tunawezaje kutafuta watu kama akina Ruhemeja kwenye Tanzania hii? Mtu amekuta kuna deni la shilingi bilioni 40 na kitu, leo hakuna deni! Kwa nini watu kama hao msiwachukue na kuwapa vyeo vingine vikubwa ili wakawafundishe na Wakurugenzi wa kwenye Halmashauri nyingine na Majiji mengine? Tusikae hapa kuponda bajeti, issue kubwa hapa hela zitoke. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba Waheshimiwa Wabunge wenzengu wa CCM, Kanuni ya 105 imeelekeza jinsi ya kufanya, hatuhitaji kuponda bajeti hapa, tunahitaji kuwapa zile siku sita wakajadili, waje watuambie, lakini bajeti ipite tena kwa ndiyo. Kama Mheshimiwa Kangi Lugola anataka kuzunguka na ndiyo za Waheshimiwa Wabunge, term hii sasa aandae record, ataenda na za bass ambayo hajawahi kuiona.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia mpango huu. Kwanza naipongeza Wizara na Mheshimiwa Profesa Mpango kwa kazi kubwa kweli ambayo yeye na wataalam wake wameionyesha kwenye kipindi cha miaka mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nianze kwa kuipongeza sana Serikali hasa sekta ya madini ambayo mimi ni Mjumbe wake, kwa kazi nzuri sana iliyofanya na imetuonesha hata kwenye taarifa kwamba kutokana na kupokea mawazo ya wadau, Serikali imeongeza kipato kikubwa sana kutokana na wadau wa madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Waziri na pia nampongeza sana Mheshimiwa Rais pale alipotupa nafasi sisi wa darasa la saba tukaishauri Serikali na akatusikiliza. Baada ya kutusikiliza leo Serikali inavuna mabilioni kutokana na mawazo tuliyoyatoa sisi wa darasa la saba ambao ni watendaji wakubwa kwenye Taifa la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe tu ushauri kwa upande wa Serikali. Nianze na suala la miradi. Tumeona Serikali katika kipindi kilichopita imekuwa na miradi mikubwa ya mabilioni ya pesa ambayo haina impact yoyote kwenye Taifa na Watanzania wale chapakazi hasa wale wa chini, hatuoni faida ya miradi mikubwa ambayo Serikali imewekeza mabilioni ya pesa. Nimejaribu kuwasikilisha wiki iliyopita, Waheshimiwa Wabunge wengi wanalia kwamba kwenye TARURA hakuna hela; na nikijaribu kuangalia mawazo ya wenzangu huko chini, naona tunafikiria labda kwenda kuongeza kwenye mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe mifano miwili mitatu. Mimi nilipoanza Ubunge nilikuwa Kamati ya Ardhi na tulienda kukagua mradi mmoja Morocco kwenye nyumba za watu wenye hali ya chini; nyumba za maskini; yale majengo mazuri yaliyoko Morocco. Tuligombana sana, sijui ndiyo kilisababisha Mheshimiwa Spika, ukanihamisha kunipeleka Kamati ya Madini! Niliwaambia, ikitokea uchumi ukiyumba, humu tutalaza popo. Wapo Wajumbe tuliokuwa nao hawakunisikia. Leo sasa unaona jengo lile limeisha na hakuna chochote kinachoendelea pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya, nataka kutoa mfano tu kwamba siyo mradi mmoja wa Morocco, tunayo miradi kwa mfano Soko la Morogoro, Machinga Complex na sasa tuna Soko la Ndugai. Wote ni mashahidi, yamefeli, ni mabilioni mangapi yametumika? Ni kwa sababu pengine wasomi wanashindwa kutafakari kwamba wanapojenga masoko, stendi kubwa za mabilioni, ile ni huduma. Sasa wanaviweka kama vitega uchumi; na watu wanaowawekea vitega uchumi ni masikini, hawa Mama Ntilie, hawawezi kwenda mle. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata sisi kuingia humu ukumbini kwa sababu hili jengo nalo lilitumia hela nyingi za Watanzania, pengine na sisi tungekuwa tunachajiwa getini, tungeona uchungu kwa yale tunayoyapanga kwa wale wananchi kule chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ushauri wangu ni kwamba fedha hizi za mabilioni ambazo tunawekeza kwenye vitu ambavyo havizalishi, tungewekeza zaidi kwa watu wa chini. Kwa mfano, tungechukua haya mabilioni, kila Halmashauri ikaandika miradi kama pesa mnazo, tukaenda kuboresha barabara zetu kule vijijini, wakulima watalima vizuri na mazao yao yatasafirishwa kwa bei nafuu. Itakuwa na impact kwenu walaji, mtapata kwa bei ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nataka kushauri kuhusiana na suala la biashara mitaani. Tusioneane aibu wala tusifichane, kweli hali ni mbaya. Watu wanafunga maduka, watu wamekata mitaji, lakini sioni namna ambayo Serikali yetu na viongozi wetu na Mawaziri labla wanakuja na mawazo mbadala ya kuweza kuona namna gani ya kuwabeba hawa wafanyabiashara wanaofilisika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimetokea kwenye tasnia ya biashara huko mtaani, nina uzoefu mkubwa. Ni kweli maduka yanafungwa, wala tusifichane. Kwa nini yanafungwa? Tuone namna ya kuzibadilisha sheria. Wafanyabiashara wale waliomo humu enzi za nyuma kabla ya Serikali ya Awamu ya Tano, ilikuwa inawezekana kukamatwa ukapigwa faini ukalipa. Ilikuwa inawezekana kujadili. Serikali ya Awamu ya Tano hakuna mahali mtu anaweza aka-temper kulipa kodi. Ila sheria zinazotumika kulipisha kodi sasa hivi ni zile zile wakati bado unaruhusiwa kulipa viwili, vinane vinapita bure. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vizuri tuone namna Serikali kama tunaweza; na namshauri sana Mheshimiwa Rais, kwenye hiki kipengele naona kama Mawaziri wanamwogopa Mheshimiwa Rais. Sasa kwa sababu sisi Wabunge ni Wawakilishi wa wananchi wote kwenye maeneo yetu tunayotoka, namwomba Mheshimiwa Rais awaite wafanyabiashara, awaite waagizaji, awaite wenye viwanda na wauzaji. Tukiendelea kufumbiana macho, watu wanafilisika. Ni lazima tuwaite, tuwasikilize, tuone namna na tujifunze kutoka hata kwenye Wizara ya Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipomfuata Mheshimiwa Rais ilikuwa ni kukamata, nyang’anya, kamata, nyang’anya, tukamwambia Mheshimiwa Rais, utatumalizia hela. Tuite utusikilize. Akatuita, tukamweleza, akapangua kutoka kodi ya asilimia 50 kurudi asilimia saba peke yake. Kwa hiyo, nadhani hata kwa hawa wafanyabiashara wa viwanda, maduka na watu wengine, tukiwaita, tukawasikiliza tutaondoa lawama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi ukipita huko mtaani, watu wengi tu wanasema, Magufuli amebana. Serikali imebana hela. Imebana wapi? Ni kwa sababu hatujarekebisha kodi rafiki ambazo mtu atalipa bila kuumia na Serikali itakusanya fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka mwaka 2016, Mheshimiwa Dkt. Mpango alivyokuja hapa alikisia kukusanya milioni 81 peke yake kwa wachimbaji wadogo, tulibishana sana hapa kama Hansard inaweza ikakumbusha. Nikamwambia hiyo ni kodi ya mtu mmoja, baada ya kutusikiliza hebu leo ona kutoka 4.6 pato la madini mpaka kwenda kwenye five point. Kwa hiyo naomba Mheshimiwa Rais awaite wafanyabiashara awasikilize, haya maneno ya kusema hali ni nzuri, tusione aibu watu wanafilisika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nilikuwa namuangalia Mheshimiwa Rais kwenye siku ya sheria alitaja orodha ya benki ambazo zinawadai wafanyabiashara kwamba zimechukua hela na hawajarudisha na benki wameenda mahakamani. Ni kweli, watu wameenda Mahakamani kwa sababu? Sababu ni nyepesi. Kwa mfano, mimi nina mtaji wangu wa shilingi milioni 50, nimeaminiwa na benki shilingi milioni 500, nafanya biashara vizuri nalipa rejesho langu vizuri inafika mahali anaingia TRA anasema tunakudai shilingi milioni 500, zinaenda zile hela za benki. Kesho yake mimi nakuja kuuziwa nyumba, nitakubalije? Ni bora nikimbilie benki na mimi nikapaki tu huko tuelewane. Kwa hiyo, ni vizuri haya mambo Serikali yetu iweze tukayapitia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikiliza juzi wajumbe wanazungumza sana kuhusu Bodi ya Mikopo, mimi nadhani Bodi ya Mikopo inafanya vizuri sana na Serikali inatoa hela nyingi ila nina ushauri mdogo tu. Serikali inaamini ubongo bila mkataba, mtu anakuwa tu na elimu yake amefaulu anaenda kuaminiwa mkopo mpaka anapata degree, karatasi. Kwa nini Serikali isije na wazo mbadala kwamba baada ya kumpa ile degree, kwa sababu sisi tunaohudumia watoto mpaka kupata degree kwa kweli kule vijijini tunakuwa tumeshamaliza na ng’ombe tumezeeka, Serikali ije na dirisha lingine kwamba mtu anapopata degree karatasi kuwe na dirisha la mikopo ya hela wakaanze biashara aweke dhamana ile degree kwenye lile dirisha. Akiweka kile cheti chake cha degree at least hata milioni 10 au 20 tupunguze hizi kelele za watu kukaa wanatembea na ma-degree. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukifungua simu za Wabunge wako kila mtu ana CV za watu kutoka Jimboni kwake 10, 20 au 30. Sasa kama mkifungua hili dirisha mkopeshe na mitaji kwa kutumia vyeti tutaweza kuondoa ule usumbufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni la kumuongeza Mheshimiwa Rais muda, mimi naliona tofauti kidogo. Nimejifunza kwenye awamu ya kwanza, ya pili, ya tatu, ya nne na ya tano ukijenga hoja hapa, nazidi tu kumuomba Rais afikirie hili kwamba kwa nini watu wanasema Rais aendelee? Nikiangalia kutoka huko tulikuwa tumeshapaki anzia treni, ndege tumekata skrepa, treni tulikuwa tumeshaanza kununua skrepa leo hivi vitu vyote vinaendelea. Tunaanzisha miradi mikubwa kwa ujasiri wa mtu mmoja na hakuna ubishi kwamba bila Magufuli mawazo yake yale tusingefika hapa tulipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tujifunze kwa wenzetu wa Zimbabwe. Mimi siyo msomi lakini kwa sababu ya biashara nimezunguka kidogo. Wazimbabwe walipoamua kuwafukuza Wazungu na kujitegemea Wazungu waliwapimia tu wakasema itafika mahali hawa watakuja kutupigia magoti, wakawawekea vikwazo. Wakafanya miradi yao ilivyokamilika kuwafukuza Wazungu wakajenga mpaka na kiwanda cha fedha. Ilipofika muda zilipoisha karatasi za ku-print pesa wazungu wakawaambia hatuwezi kuwapa hizi material za karatasi kwa sababu mko kwenye vikwazo. Ndiyo Serikali ya Zimbabwe ikaanza kuwa inabadilisha tu Rais anatangaza noti ya milioni moja inakuwa ya milioni 10. Baadaye watu wakaanza kulipwa mshahara kwenye kiroba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nikuombe haya mambo ambayo Rais ameyafanya na tumeona mengine yanaangukia 2024, 2025, kwa ujasiri ule ule tunaweza kuona namna kama alivyosema Mzee Butiku juzi tukamuongeza muda kwani kitu gani? Mbona wenzetu wamefanya? Ina maana sisi Watanzania tunaijua demokrasia zaidi ya Wachina ambao ni matrilionea na kila mtu ana teknolojia yake? Wamefika mahali wakasema tumuone kwa mawazo haya, tumuongeze muda hata miaka 20 mbele ili aweze kukamilisha yale ambayo alikuwa ameyapanga. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Musukuma.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho tu…

MWENYEKITI: Muda hauko upande wako. Nakushukuru sana kwa mchango wako.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja asilimia 100. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia. Kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu kwa kuteuliwa kuwa Rais wetu wa Awamu ya Sita, lakini pili nikushukuru wewe kama mlezi wetu sisi Wabunge, najua na sisi tulipoanza humu tuliitwa vijana, lakini naona sasa tunaenda tunazeeka-zeeka kwa sababu umesajili vijana wengine, Mungu akubariki sana.

Mheshimiwa Spika, lakini nimpongeze sana Katibu Mkuu Mstaafu, Mheshimiwa Bashiru, tunakushukuru sana. Kwa sisi tuliosota CCM tunatambua mchango wako Mheshimiwa Katibu Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi nzuri uliyoifanya. Umeweza kutuunganisha Wabunge wote pamoja na Serikali yako unayoiongoza, lakini pamoja na Mawaziri unaowasimamia.

Mheshimiwa Spika, nitaanza kushauri upande wa kodi, nimezungumza humu zaidi ya mara mbili mara tatu nikiomba Serikali ione namna ya kuweza kukaa na wafanyabiashara, ili kuweza kuona jinsi nzuri ya watu walipe kodi bila kuichukia Serikali na bila kuwa maadui na wataalamu wetu wa TRA. Lakini mara nyingi mawazo mazuri tunapoyatoa sisi kwa kuwa ni darasa la saba, yaani tukitoa wazo, yaani kabla hamjalielewa ninyi wasomi mnalibeba linakuwa la kwenu wakati utafiti umefanywa na watu wengine.

Mheshimiwa Spika, sasa nataka nishauri, tunajua kwamba, Mheshimiwa Waziri amepewa maagizo na Mheshimiwa Rais kwamba, nendeni mkarekebishe TRA, hawawezi kurekebisha. Na mimi nikuombe kwenye hili hata Waziri tunamvalisha kengele ambayo hawezi kuicheza. Ningeomba Mheshimiwa Rais awaite wafanyabiashara, suala hapa sio harassment, suala hapa ni kodi ambazo ni za miaka 25 ya nyuma. Kwa maisha ya sasa inabidi tubadilishe kulingana na hali halisi, ukisema tu wasitusumbue bado wanakuja na mavitabu yaleyale, kilichobadilika wamekuwa tu na ka-lugha, tunaomba utulipe, wameacha kufunga yale makufuli, lakini kodi ni ileile.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ningeomba ni vizuri Mheshimiwa Rais akawaita wafanyabiashara akakaanao, kama tulivyofanya kwenye madini, wamwambie hiki kinatukwaza, hiki kinatukwaza, aone namna aseme nendeni mkabadilishe hili. Kama hatutabadilisha hakuna namna ambayo mtamsaidia mfanyabiashara wa Tanzania bado mateso ni yaleyale na ninadhani ndio kama rushwa itaongezeka japokuwa haitaombwa kwa ukali, itakuwa ni ya maelewano tutoe kidogokidogo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni vizuri mawazo haya mkayafanya yawe endelevu muwaite wenye matatizo. Ninyi wengi huku mnaoelekezwa mnakaa ofisini, hamjui huko field watu wanavyoteseka. Kwa hiyo, ningeshauri Mheshimiwa Waziri Mkuu ni vizuri Rais akawasikiliza wafanyabiashara ndio hub yetu kwenye nchi yetu. Baada ya kuwasikiliza aone namna ya kitu gani na kitu gani tutakachokiondoa, ili wafanyabiashara wawe na amani na walipe bila kusumbua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, natoa mfano; leo ukienda Kariakoo utakuta watu wamekimbia wale wafanyabiashara, nakupa mfano mdogo tu wa glasi. Glasi ina aina kama sita, kuna glasi inauzwa 200/= tunatumia kule kwetu kijijini, kuna ya 1,500/= wanatumia Wagogo, kuna 15,000/= wanatumia Dar-es-Salaam, ukienda kwenye kodi tariff inayotajwa ni ushuru wa glasi. Inawezekanaje ushuru uni-charge 2,000/= wakati glasi inauzwa 1,000/=? Kwa hiyo, ni vizuri tukawa na uwanja mpana wa kuweza kuwasikiliza hawa wafanyabiashara ili muweze kukusanya kodi bila kusumbuana na bila kuwalaumu watu wa TRA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la pili, napenda nishauri kwenye upande wa tanzanite. Maisha yangu nimekulia kwenye madini ni vizuri wakatusikiliza watu tunaotoka kwenye madini. Huwezi ukasema tanzanite inatoroshwa, na sisi kama kamati tumeenda kwenye tanzanite pale Mererani, kwa kweli Serikali imefanya kazi kubwa sana na askari wetu wako pale wanalinda vizuri na kamera. Tumeingizwa chumba cha kamera unaona mita 50 nje mita 50 ndani ni ulinzi ambao unajiuliza sisi watu wa dhahabu tungepewa huo ulinzi pengine Serikali ingekusanya mara tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nataka nishauri mnaibiwaje Serikali. Unaweza ukalaumu wanajeshi, unaweza ukalaumu wizi uko pale, naomba nitoe mfano; tangu mpate lile jiwe la Laizer lile lililotangazwa kwenye TV la bilioni sita mkatoza kodi, halafu mkapeleka ma-valuer mkaweka na askari na askari na askari, kama aina tatu za maaskari wako pale na watu kweli wanapita kwenye geti. Niwaulize swali, ni lini toka mmepata jiwe la Laizer ni lini mmepata tanzanite ambayo imezidi milioni thelathini, arobaini? Ni kwasababu, nyie mkipewa mawazo kabla hamjayafanyia kazi mnapeleka utaalamu. Sasa watu wanawapigia chenga palepale na tochi yenu mnamulika pale.

Mheshimiwa Spika, ni watu wanazunguka na wale vijana wa tochi pale. Hatuna sababu ya kutumia akili nyingi ya degree tu. Mnaona degree zinatufelisha, naomba nikupe dawa moja ndogo tu; kesho Serikali iwe na hela pale waweke vijana wa darasa la saba tu wanaojua mawe, tunahitaji tochi wala sio binocular hiyo mnayotumia pale, muwaweke pembeni pale hawa ma-valuer wenu wenye degree wapimee wakifika mwisho wakisema hii ni milioni 30 muwape wale vijana wa darasa la saba wachungulie wawaambie kama ni 30 mpe mara moja muone kama hawatayakimbia mawe pale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mnapigwa chenga palepale na askari wenu wako pale. Kwa hiyo, ni vizuri wataalam mtutafute tuwape madini, msione aibu kufundishwa na darasa la saba tumekulia huko, nyie field yenu mmesoma miezi mitatu sasa sisi tumekulia kulekule. Kwa hiyo, ni vizuri msishikane uchawi wowote wizi mnapigwa na makamera yenu yako pale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nishauri pia, nchi kama Tanzania tuna ma-valuer wasiozidi kumi na moja, kumi na tano, ni aibu. Kama tuko serious chukueni wanajeshi hata 100 ni miezi sita tu kujifunza u-valuer kwa nini tuwe na watu kumi na moja, kumi na mbili? Walewale wanazungumza, ukizungumza na huyu akimaliza deal biashara imeisha? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikuombe sana ushauri wangu hawa wataalamu waweze kuufanyia kazi, lakini nataka nizungumze kuna mtu mmoja msomi humu mtaalamu Profesa alizungumza juzi akasema dhahabu hatujafanya vizuri. Nimekulia Geita, wakati wa utawala wa Mhesimiwa Profesa Muhongo wachimbaji wadogo mwaka 2015 tulikusanya gramu 120, 2016 wakati tumeanza kuruhusu wachimbaji wadogo baada ya kupokelewa mawazo yetu tumekusanya 337,000 gramu kwa mwaka, 2017, 800,000, 2018,6 1,600,000, 2019 4,000,000, na 2020 5,000,000. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tunahitaji kuwa na maprofesa wa design hii? Hata kama hatujui kusoma, hatuoni haya maandishi hapa ndani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni vizuri mtu anapofanya kazi nzuri tusitengenezeane ajali lazima apewe sifa. Hongera sana Waziri wa Madini, umefanya kazi nzuri wala hutuhitaji kupata degree hapa, tunajumlisha hesabu tunajua kutoka gramu 120 leo tuko milioni tano halafu mtu anasimama hapa anaanza kubeza. Nakumbuka maneno ya mtu mmoja nikiwa sio Mbunge, alikuwa anakaa pale nikimuangalia kwenye TV anaitwa Mheshimiwa Kigwangala, alimwambia binafsi hajawahi kuona Profesa muongo kama Mheshimiwa Muhongo kwa sababu… (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Musukuma namlinda Mheshimiwa Mbunge Profesa Muhongo. Sijui yupo humu ndani?

MBUNGE FULANI: Hayupo.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, atapata taarifa.

SPIKA: Nadhani ametoka kidogo? (Kicheko)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, univumilie kidogo ninazungumza kwa uchungu. Mwaka 2016 Mheshimiwa Profesa Muhongo akiwa Waziri nimemuita Geita kumwambia Waziri tunaibiwa; hadharani kwenye mic, tunaibiwa haya makinikia wakipakia humu kuna dhahabu.

Mheshimiwa Spika, Profesa alishika mic ananiambia wewe ni darasa la saba, nyie watu wa Geita mlikosea kuchagua mtu wa darasa la saba. Tukamchenga Profesa, dakika moja Mheshimiwa nimalizie hoja yangu, tukampelekea marehemu Mheshimiwa Magufuli kamfuko tu kadogo tukamwambia Mheshimiwa hatuhitaji Profesa, naomba utusimamie tuoshe haka kamfuko tu kadogo tukaoshea na Coca-cola.

Mheshimiwa Spika, dakika 15 tulikuwa na dhahabu ya milioni 16, Mheshimiwa Dkt. Magufuli akawakia na kwenye gia. Sasa maprofesa wa design hii watatuchelewesha ni vizuri mtuiamini na sisi LY tunaumia, tunatumia nguvu kuwapa material halafu wanakuja wanapotosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. Kwanza niipongeze sana wizara lakini, nianze nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri. Mheshimiwa Waziri kwa sisi tunaotoka kwenye maeneo ya madini ninaweza nikasema ni waziri wa kwanza umevunja rekodi hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia niwapongeze wasaidizi wako Katibu Mkuu pamoja na timu yake na hili ni fundisho kwamba ukiangalia hii wizara, ni mjumbe wa kamati. Tunama- professor wa kutosha na kweli wameutendea haki u-professor wao. Ukiangalia tulikotoka na tulipo mwenyewe na-appreciate mchango wa ma-professor wa madini, wa wizara ya madini hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nianze kwa kusema tulipofikia sasa kwenye Wizara ya hii Madini tusirudi nyuma, tusikatishane tamaa, tuangalie wapi ambapo tuna mapungufu tubadilishe twende mbele. Na mfano mzuri unaweza ukaona leo wakati unatangaza wageni pale ni wizara ya kwanza ambayo mabenki yote yamehudhuria hapa kwasababu wanajua hii wizara ni pesa. Tusirudi nyuma turekebishe yale mapungufu ambayo yamejitokeza kwenye kipindi hiki cha miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, nilitaka kushauri kwenye upande wa Tanzanite, ni mjumbe wa kamati, Serikali lazima tuje na utaratibu mpya na ni lazima tuambizane ukweli na Mheshimiwa Rais ametuambia tuseme ukweli. Ni aibu kubwa sana kuwa na Taifa ambalo lina-search watu kwa kuvua nguo hii haiwezekani! Sisi tumeenda kama wajumbe mimi nimejionea mwenyewe mwanajeshi ambaye ni jeshi ambalo tunaloliamini anafanya kazi ya ku-search wamasai hii ni dharau ya hatari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata kama kuna mtu alikamatwa nyie ambao hamjapita kwenye machimbo, mtu anaweza kukaa huko maduarani akakaa wiki nzima hajapata hata mia tano. Kwa hiyo, mtu ukimkamata anakagonga kashilingi 2000 inasababisha watu wa-search-iwe kuvuliwa nguo kweli una benefit nini nakajiwe kashilingi 2000. Na hata ukiangalia pale kesi nyingi anakamatwa mtu na vumbi kwenye koti linathamani ya Shilingi 700 halafu mnatumia difenda kutoa pale melelani kumpeleka kituo cha polisi hii ni kitu ambacho lazima tuone namna ya kubadilisha ule utaratibu wa pale tu-deal na wezi tusi-deal na watu wanaganga njaa. Lakini lingine…

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Kuna taarifa Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma Mheshimiwa Christopher Olonyokie Ole-Sendeka.

T A A R I F A

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kutoa taarifa kwa Mheshimiwa Mbunge, sio tu kwamba wananchi na wachimbaji wa Mererani wanavuliwa nguo, wakati ule kabla ya kamati zote mbili za Mbunge kufika, bali hata baada ya maelekezo ya Waziri wa Madini na maelekezo ya Kamati ya Madini, na baada ya ziara ya Kamati inayoshughulikia masuala ya ulinzi, mpaka leo watu 20 wanawekwa chumba kimoja, wanavuliwa nguo, zote halafu mnaambiwa mchuchumae halafu ukaguliwe na mtoto wa miaka 23, ambaye amevaa kombati za jeshi ni ukiukwaji wa haki za binadamu nchi yetu inaheshimu na kuthamini misingi ya utu, usawa na haki za binadamu. Kitendo hiki ni cha aibu ni fedheha, na mimi baadaye nitataka kujua Waziri mwenye dhamana… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka tusije tukafanya mambo kinyume na kanuni zetu sisi wenyewe, naona hapa na yeye ana fursa yake ya kuchangia baadaye, na hicho alichokuwa anakisema kwasababu kama ninavyosema siku zote sina taarifa hapa maana hizo ni tuhuma mahususi. Kwa hiyo, ndio maana sitamuuliza Mheshimiwa Musukuma kwamba anapokea hiyo taarifa au hapana. Kwa hiyo, Mheshimiwa Musukuma malizia mchango wako.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nina dakika mbili nilizochangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nishukuru sana ile timu ya Spika, Mheshimiwa Ndugai, alipounda timu kwenda kuchunguza Mererani, ilifanya kazi nzuri sana, ikiongozwa nadhani na Mheshimiwa Doto na Wajumbe wengine na Tume ndiyo ilimuondoa hata ndugu yangu, Mheshimiwa Simbachawene. Baada ya hapo Mheshimiwa Rais aliunde Tume iliyoongozwa na akina Profesa Mruma na Mheshimiwa Profesa Kabudi ya kuchunguza mgogoro wa Mererani. Baada ya kutoa taarifa ilionekana yule ni mwizi na akakubali kulipa. Sasa tunatafutiana ajali, kama mtu amehojiwa na timu ya maprofesa na ameshakiri kuachia mgodi, anaitwa Bungeni kuja kuhutubia Kamati yaani criminals tunaanza kuwaleta Bungeni, tunarudi kubaya. Niombe, tulipo ni kuzuri, tusikubali tena kurudi nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine nizungumzie CSR. Mimi natoka Geita, tulipiga makofi mengi sana, Alhamdulillah tunapata CSR shilingi bilioni 10 kwenye halmashauri yetu. Hata hivyo, hii CSR haina mpangilio, ni kama likitu tu limetupwa, halina mwenyewe. Wizara ya Madini na TAMISEMI ni nini kiliwafanya mkatoa uhuru wa kumuachia Mkuu wa Mkoa anakuwa anatuamulia sisi? Mkuu wa Mkoa amepewa mamlaka ya kuamua hela za Halmashauri kajenge darasa, kajenge hoteli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna vitu vingine vinauma, najua nachokiongea na Mheshimiwa Waziri anakijua. Mimi ninazo nyaraka hapa, kwa mwaka mmoja Halmashauri za Geita na Geita Mjini, Mkuu wa Mkoa na timu yake wamejilipa posho zaidi ya shilingi milioni 600; hiki kitu hakiwezekani, ninao ushahidi hapa. Kwa nini hizi pesa za CSR zisitumike kwenye Halmashauri yetu, watu wa GGM wao waje kufanya kama ukaguzi na manunuzi yote yafanywe na procurement yetu ya Halmashauri. Tofauti na ilivyo sasa, mmempa mamlaka Mkuu wa Mkoa kuingia kama Waziri anasema sitaki hiki, nataka hiki, sasa sisi tuna kazi gani kama Halmashauri? Niombe sana Mheshimiwa Waziri akinyanyuka hapa aje na hayo majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wachimbaji wadogo wanafanya kazi kubwa sana na tunapolilia maeneo mkubali kuyaachia. Natoa mfano kule Geita, kuna eneo kule Busolwa linamilikiwa na TLS, miaka nenda rudi. Wachimbaji wanachimba kama mbayuwayu, halafu hapa tunajisifu tunakusanya kutoka kwa wachimbaji wadogo. Mheshimiwa Waziri, ni kwa nini asitamke leo kwamba lile eneo mnawaachia vijana wetu waweze kuhangaika kwa sababu hata muda wa leseni umeshamalizika?

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine naomba Serikali mzungumze lugha moja. Mheshimiwa Spika jana amezungumza kitu kizuri sana kwamba Serikali ni moja, inakuwa na kauli tofauti, Wizara ya Madini inatoa leseni, ukipewa leseni ukiipeleka kule unakutana na DC naye ana maamuzi yake. Mimi sitaki kuwa muongo, Waziri nenda Bariadi leo, leseni zina karibu miezi sita DC amekataa.

Sasa nauliza Wizara na DC nani mkubwa? Zungumzeni lugha moja, kama mnataka leseni atoe Mkuu wa Wilaya tusihangaike kuja kutupa nauli zetu huku, tukae na Wakuu wa Wilaya wamalize. Mtu anakuja anakaa mwezi, anarudi kule tena anakutana na DC naye ana masharti yake anataka kufuta leseni, Tanzania gani hii? Ni vizuri sana tukazungumza lugha moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namuomba shemeji yangu, yeye ni Mjumbe mwenzetu…

MBUNGE FULANI: Nani?

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Anajijua, amezungumza kuhusu TEITI. Mimi nadhani ungeshauri waongozwe hela, sisi wote tunasoma, tunaletewa ripoti Pamoja, tunachoangalia hapa OC ya TEITI wanapewa asilimia 100; tunazo taarifa. Wamefanya utafiti kwa kum-consult Mzumbe, amelipwa shilingi milioni 250 mwaka jana na sasa wanaendelea. Tunaposema hawana hela, mimi nadhani…

T A A R I F A

MHE. JESCA D. KISHOA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Musukuma, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Jesca Kishoa.

MHE. JESCA D. KISHOA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nataka nimpe taarifa mzungumzaji anayeendelea kuzungumza sasa hivi, yeye anazungumzia fedha za OC, mimi nazungumzia fedha za maendeleo ambazo zimeweza kuwawezesha TEITI kuendelea kuboresha majukumu yao.

NAIBU SPIKA: Kwanza kabla sijakuuliza Mheshimiwa Musukuma, nilikuwa najiuliza, hapa nimemtambulisha Mwenyekiti wa Bodi ya TEITI, siyo? Ama mimi ndio nilikuwa nimesoma vibaya, si yupo?

WABUNGE FULANI: Ndiyo.

NAIBU SPIKA: Sasa kama anayosema Mheshimiwa Jesca Kishoa yako sawasawa, hii taasisi hapa ilikuwa inafanya nini? Kwa sababu si maana yake hawafanyi kazi yoyote kwa sababu hawana hela, ndiyo maana yake. Kama hawafanyi kazi sasa hapa wamekuja kufanya nini?

Mheshimiwa Waziri atatupa maelezo baadaye kwa sababu kama hawafanyi shughuli yoyote wanatumia hela zetu kwa ajili ya nini? Maana mchango unaonesha hakuna fedha isipokuwa za kula, si ndiyo Other Charges. Hakuna shughuli yaani, si ndiyo maana yake? Amesema hapa mwishoni ili wafanye kazi, maana yake hawafanyi kazi. Mheshimiwa Waziri, atatufafanulia jambo hilo.

Mheshimiwa Musukuma endelea na mchango wako.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, simuelewi Mheshimiwa Jesca, hii kazi inayofanywa na Mzumbe ni matumizi ama ndiyo kazi ya TEITI? Sasa sielewi, lakini najua kinachomsumbua shemeji yangu, wala msiwe na wasiwasi, ni kukaa mbali na shemeji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mie niweze kuchangia, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kukuteuwa Profesa Mkumbo kuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, mimi binafsi naamini kwamba umefanya vizuri sana kwenye Wizara ya Maji, wakati ukiwa mtendaji. Imani yetu sisi wafanyabiashara kwenye kipindi chako hiki kwenye hii Wizara ya Viwanda na Biashara na kwa kuwa ni bajeti yako ya kwanza hatutakupiga mishale mikubwa sana, utegemee mwakani ndio utakutana nayo kama hutabadilisha haya mambo huko Wizara ya Viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ningependa kumshauri Mheshimiwa Waziri afanyie kazi kwamba Serikali iongee lugha moja, shida ambayo uwa nazungumza mara nyingi kwamba yaani ukiangalia katika mfumo Wizara ya Viwanda na Biashara ni kama hauna kazi yoyote, kwa sababu watu wengi hawaoni umuhimu wa Wizara ya Viwanda na Biashara kwa sababu kila tatizo utakalokumbana nalo kwenye biashara lina Wizara yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukikumbana na mazingira lina Wizara yake, ukikumbana na kodi lina Wizara yake, ukikumbana na Halmashauri lina Wizara yake. Sasa nikuombe, mnapoenda kukutana kwenye cabinet lazima ulilie power ya Wizara yako. Nakupa mfano Mheshimiwa Waziri, sasa hivi kuna mjumbe mmoja hapa amechangia, mnahamasisha watu wawekeze viwanda, lakini hivi viwanda mngekuwa mnazungumza lugha moja mngekuwa mnavipanga kiwilaya hata kimikoa. Ni kweli kwamba ni nani atakayefuata juice Geita akaiuze Dar es Salaam wakati juice hiyo hiyo inatengenezwa tena Dar es Salaam?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba mnatoa vitu ambavyo hamjapanga maeneo sahihi kwamba hiki kikae huku na hiki kikae huku. Lakini nikupe mfano tu sasa hivi kuna shida ya mnafungua refinery; nakupa biashara moja tu, refinery imejengwa Mwanza, imejengwa Geita, imejengwa hapa na ukiangalia kiuhalisia dhahabu nyingi inatoka Geita; kwa nini msingetengeza tu kama zone ya dhahabu mtalii yeyote au mnunuzi akija ukitaka dhahabu nenda Geita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unafungua refinery Geita, unafungua refinery Mwanza, sijui mtu wa Mwanza atatoa wapi hiyo dhahabu ya kutengeneza! Kwa sababu sisi watu Geita hatutakubali itoke dhahabu Geita ipelekwe Mwanza halafu Manispaa ya Mwanza ikakusanye levy yetu ambayo ingetengenezewa huku. Kwa hiyo ni vizuri mzungumze lugha moja na ukalilie madaraka kabisa kwenye cabinet kwamba na wewe ni waziri ambaye unaweza kujitosheleza.

T A A R I F A

MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Taarifa Mwenyekiti.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma taarifa tusikilize ya Mheshimiwa Almas.

MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kumpa taarifa mzungumzaji wa sasa hivi kwamba ilitokea hiyo tumbaku inalimwa Tabora, Viwanda vya Tumbaku vyote viko Morogoro. Tatizo kubwa sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma unaipokea hiyo taarifa?

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea ndio maana nimemwambia Profesa tunakupa mwaka mmoja ukajaribu kurekebisha haya mambo tuwe na zone, kila kitu kipatikane mkoa fulani. Na hili la Mheshimiwa Waziri najua Serikali ilikuwa na nia nzuri sana ya kutaifisha viwanda na ninashukuru sana kwa sababu pia Katibu Mkuu wa sasa alikuwa Katibu Mkuu wa Fedha na Mheshimiwa Rais amekurudisha kwenye Wizara ya Viwanda na Biashara na hili ujisifu, tunahitaji viwanda vifanye kazi, hakuna Wizara inayojisifu kuua viwanda, kuua taaluma unayoisimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakupa mfano Mheshimiwa Waziri mimi nina maslahi na kiwanda fulani kule Tanga kiwanda cha furniture, wakati Serikali inabinafsisha kazi ya mwekezaji ni kutengeneza, kazi ya kulinda masoko ni kazi yenu Serikali msikwepe majukumu. Huwezi ukanipa mimi kiwanda nikiendeshe kinatengeneza furniture, mteja mkubwa niliyemlenga ni Serikali, ninyi wenyewe mmetukimbia mnanunua vya Kichina, sasa lazima uzalishaji uwe wa kubambanya, lakini wewe unataka nizalishe kwa asilimia 100 hii kitu haiwezekani ni kazi yenu ninyi Serikali kulinda viwanda vya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mkumbo ninatamani sana kukuomba ukatembelee Kiwanda cha Play and Panel pale Tanga kimefungwa kikiwa na malighafi eti kinazalisha asilimia 20. Twende Moshi pale Kiliwood imefungwa na Kiliwood iliuzwa na Serikali na ninyi wenyewe kwenye mkataba mkasema material mtamgawia ninyi kutoka kwenye mashamba yenu. Lakini mashamba yale material mnawagawia walanguzi mwenye kiwanda mnampa asilimia moja, sio sawa ni wakati tunaona sasa Serikali inafungua akaunti ilizozifunga hii ni hatua nzuri fungueni na viwanda. Hao mliowanyang’anya viwanda wengine wana uwezo, mliwasababisha kufunga viwanda ni ninyi kutokulinda soko la ndani. Huwezi ukanishindanisha mimi mzawa ambaye ninakopa CRDB mkopo asilimia 14 ukanishindanisha na mtu wa nje ana mkopo asilimia mbili, ni hesabu za design gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina kuamini sana Profesa, ninakuomba utembelee hivi viwanda niko tayari hata kesho tufuatane mimi na wewe ukaone uonevu huo uliotokea huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Kiwanda cha Moproco pale Morogoro lazima tuwaambie ukweli, sijui ni hesabu za design gani na ndio maana mimi nikisema hapa mnanilaumu kwamba nawalaumu maprofesa, sitakulenga sana profesa kwa sababu wewe ni rafiki yangu. Kiwanda cha Moproco ni kiwanda cha mafuta ya alizeti, alizeti inapatikana miezi mitatu tu, mtu anataka kuzalisha mwaka mzima unatoa wapi hiyo alizeti? Ni jukumu la Serikali kuwahamasisha watu walime alizeti ili mtu azalishe miezi 12. Sasa ninyi mkikuta amefunga kipindi ambacho hakuna material mnamnyang’anya kiwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri dhambi hii ya kupora vitu vya watu isikuangukie mikononi mwako, kama Serikali imeanza kufungua akaunti kaa na Katibu wako mfungue hivyo viwanda, wapeni muda kama ni mwaka mmoja, kama ni miezi sita, wakope hela mambo yaendelee tumeshambiwa kazi iendelee halafu bado umeshikilia viwanda vya kazi gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine Mheshimiwa Waziri nikuombe sisi kule kwetu jimboni kwangu tutalima mananasi yanaliwa tu shilingi 200/shilingi 300, ukiingia kwenye internet Dubai kule nanasi linauzwa mpaka dola 15; ni kazi yenu Serikali kututafutia masoko. (Makofi)

Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri uje uone mananasi tunayoyauza kwa mafungu kama mafenesi, njoo uone ili uone namna wataalam wako wakazunguke huko duniani tupate masoko tuweze kuuza bidhaa zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho Profesa nimesema wewe ni rafiki yangu lakini nikuombe sana mimi sio kwamba nadharau maprofesa, lakini vitendo vya maprofesa wakati mwingine ndio vinatufanya tulaumu hata kama mtatusema namna gani. (Makofi)

Naomba nitoe mfano mdogo tu wakati wa Marehemu Hayati Magufuli najua Marais wetu wanatupenda sana Watanzania wote, Mheshimiwa Rais aliunda tume ya kuchunguza corona, ikachunguza ile hatoe jibu kwa Watanzania, ikaja corona ya mapapai, ya mbuzi, ya maembe, na tukaona mpaka Mabunge ya Ulaya yanamsifu Rais Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa sasa watu mkaanza kuchachamaa mitandaoni Mama yetu Samia naye ameunda tume, tume ya Mama Samia miezi mitatu baadaye tuchomwe sindano mnataka kumaliza sisi ambao sio wanasayansi. Sasa niwaombe sana wasomi wetu muwe makini, lazima muwe makini hatuwezi na Profesa miezi mitatu kasema corona ya mapapai huyohuyo miezi mitatu baadaye corona ya kuchoma sindano na ninamuomba mama sana atumie busara maprofesa hawa kama watamchanganya tuko huku kitaa tumsaidie. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi chanjo zinasemwa tunachanjwa tupunguze nguvu za kiume na sisi bado tunataka kuzaa, Serikali inasema tuzae maprofesa mnatuchanganya. Mama achana na hawa ma-professor wametufikisha pabaya. Wazungu wenyewe walisifu Tume ya Marehemu Magufuli akasema mapapai na mbuzi. Mbunge lilijadili Bunge la Ulaya tunaona mitandaoni miezi mitatu baadaye tunang’ang’anizwa kuvaa mabarakoa, maprofesa hao hao. Sasa niwaambie na sisi Chama cha Waganga tutakaa na sisi tutoe taarifa yetu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana ahsanteni sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoendelea kuifanya, pia kwa usikivu ambao sisi wabunge tumekuwa na mambo mengi tumelalamika kwa muda mfupi lakini kwa muda mchache aliokaa madarakani tumeona ameanza kutekeleza kila Mbunge hapa amepata milioni mia tano kwenye jimbo, hongera sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hongera sana Mheshimiwa Waziri umeanza vizuri na mimi kama Mbunge mzoefu kidogo nadhani mishale mikubwa tutakupiga Bunge lijalo, hakuna Mbunge ambaye hajaridhia na hajaridhika na Mpango huu wa Bajeti uliowasilisha kwetu. Tunaimani kama sasa utausimamia na kuyatekeleza yale ambayo umeyazungumza kwa kauli yako utakuwa umetubeba sana sisi Wabunge ambao bado tunahitaji kuendelea kuwa kwenye Bunge hili kipindi cha mwaka 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Mheshimiwa Waziri nikupongeze sana katika suala la kupandisha na kuwachukua Waheshimiwa Madiwani kuwaweka kwenye bajeti ya Serikali. Mheshimiwa Waziri mimi ni zao la Diwani, mimi kuingia humu nimefanya kazi nzuri na ya mateso nikiwa kama Diwani, lakini baadaye nimepanda kuja huku Mheshimiwa Waziri umefanya kazi kubwa sana Diwani awe na mshahara unaotambulika na Serikali siyo hisani za Wakurugenzi, umetuheshimisha hata mizinga kule kwenye Baraza la Madiwani kwa Madiwani wetu na ninakushukuru leo Serikali imewatambua na kuwaweka kwenye mpango sasa mtalipwa mshahara kama mtumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuomba sana Mheshimiwa Waziri ulitekeleze na ikikupendeza sitaki kutamka kiwango bado mshahara wa madiwani ni mdogo sana ukilinganisha na majukumu yao kwa hiyo ukafikirie sitaki utamke ni shilingi ngapi kwenye windup, lakini…

T A A R I F A

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Msukuma kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Cecilia Paresso.

MHE. CECILIA DANIEL PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nataka nimpe taarifa mchangiaji kwamba kilichoridhiwa siyo mshahara ni posho badala ya kulipwa na halmashauri sasa inalipwa na Serikali Kuu, ukiongea habari ya mshahara ni habari nyingine ambayo ina utaratibu wake itakuja kuwa na makato yake, itakuja kuwa na pension na mambo mengi. Kwa hiyo kinacholipwa ni posho siyo mshahara. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Hilo moja, labda lingine ni kwamba, kwa sababu umetawaja wale wa kwangu, wale wakwangu hawahusiki kwenye mpango huo maana sisi ni jiji na tunaweza kujilipa wenyewe. Kwa hiyo, wale wapo vizuri Mheshimiwa Musukuma usiwe na wasiwasi.(Makofi)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, watanisaidia kuwaambia wale ambao wapo jirani na Jiji la Mbeya message yangu itafika. Mheshimiwa nilindie muda wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru iwavyo vyovyote vile kama taarifa ilivyotolewa, lakini naishukuru Serikali iwe posho, iwe mshahara iwavyo vyovyote ni jambo la msingi Mheshimiwa endelea kuchapa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine Mheshimiwa Waziri nakupongeza sana kwenye faini ya bodaboda, nataka nikuambie katika kitu ambacho Mungu atakukumbuka kukuongezea hata siku zako za uhai wako ni suala la faini ya bodaboda. Mimi nilikuwa najiuliza wachumi wetu mpo namna gani inawezekanaje faini ya bodaboda anayebeba watu wawili unamlinganisha faini na basi la watu 65. Mimi nilikuwa nashauri Mheshimiwa Waziri hata hiyo elfu kumi bado ni nyingi, tungeweka hata elfu mbili, lengo letu siyo faini!

WABUNGE FULANI: Aaah!

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mnabisha nini Waheshimiwa Wabunge.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilindie muda wangu, lengo siyo faini lengo letu ni kuwawezesha watu watoke kwenye bodaboda wanunue magari, hakuna mtu anapenda kuendesha bodaboda miaka mitano, miaka kumi anaumia kifua, kwa hiyo mimi nadhani bado mimi kama Mbunge nashauri hata hiyo elfu kumi umeanza vizuri, lakini tufikirie kwenda hata kwenye elfu mbili hata buku kwani kuna shida gani nchi ina pesa nyingi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuchangia kuhusiana na suala la machinga, Mheshimiwa Waziri katika jambo ambalo nakuomba sana Mheshimiwa Waziri hamna tajiri yeyote anaanza kuwa tajiri bila kuhangaika huku chini. Machinga ni mtu muhimu sana Mheshimiwa Waziri na mimi niliona Dar es Salaam ni sehemu ambayo Watanzania wote tunaitegemea nilienda tu hizi siku mbili tatu nikazungukia kule Kariakoo baada ya kuona Mkuu wa Mkoa mmoja anasema tunaondoa machinga, nyinyi Waheshimwa Wabunge kama mnakumbuka Wabunge wenzangu wa CCM katika raha tuliyoipata kwenye uchaguzi wa 2020 ni pamoja na machinga kutuunga mkono, kwa sababu tuliwawezesha walikuwa busy na kazi zao hawakusikiliza mambo ya kudanganywa danganywa na wanasiasa ambao hawana mwelekeo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa leo anasimama mtu mmoja anasema tuondoe machinga tuwarudishe vijijini, nendeni mkafanye research Dar es Salaam machinga wengi sasa hivi waliopo huko mitaani wengi wana degree moja na wengine degree mbili wameamua kujiajiri, pili, unapom- disturb machinga usidhani unamuharibia maisha yeye watu wengi waliopo kule kwanza tuliwaambia wanunue vitambulisho ili wafanye biashara yao kwa uhuru na Serikali imechuma bilioni 43 halafu leo gafla mtu mmoja anasema tuwatoe machinga unapomuharibia mtu biashara mnaharibia taasisi za kifedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna watu wapo pale tayari wana mikopo, wamekopa, wamekopeshwa wanafanya biashara yao wanamarejesho eti tunathamini magari, kwani Mheshimiwa Waziri tuna shida gani tukisema magari yasiingie Kariakoo ili iwe center ya biashara watu wafanye biashara yao kwa uhuru wasibugudhiwe. Hii kitu Mheshimiwa Waziri mimi huwa najiuliza hivi mnaona faida gani magari yaingie elfu moja ambayo hayalipii au kuachia machinga wafanye biashara kwa uhuru kama tulivyowaahidi halafu nyie mkusanye kodi. Machinga ndiyo anafanya research ya biashara Tanzania nzima nyie wote wenye degree hapa hakuna mtu anafanya research ya biashara machinga hauzi kitu ambacho hakinunuliwi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wafanyabiashara ndiyo watu wanaowategemea leo mtu mmoja anasimama ndiyo maana huwa najiuliza tunao Wachumi nchi hii au tuna vicheche tu, maana siwaelewi kabisa. Kwa hiyo niwaombe sana mliangalie wasisumbuliwe hawa watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Musukuma hebu usiwaite watalaam wetu vicheche tafadhali, ondoa hilo neno kwa sababu wamesoma ili watusaidie na haya yote tunayoipongeza Serikali wachumi wamefanya kazi nzuri. (Makofi)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaliondoa, lakini wafanyekazi kwa ufasaha wadhihirishe yale waliyoyasoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine nimeona kwenye kodi za wachimbaji wadogo unapendekeza kuongeza kodi Mheshimiwa Waziri nikushauri kumbuka kabla hatujarekebisha kodi za wachimbaji wadogo Serikali ilikuwa inakusanya bilioni 168 baada ya marekebisho ya sheria tupo bilioni 544. Ukiongeza kodi ukiwanyima faida wafanyabiashara ya elfu mbili, elfu tatu utaongeza utoroshaji hutapata hela hii, nikuombe sana ondoa hayo mawazo ya kuongeza hiyo asilimia tatu sijui asilimia saba tufikirie zaidi kupunguza kwa sababu tunaona tunawekeza mpaka viwanda vikubwa hapa halafu tunaongeza masuala ya kodi siyo sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nazungumza kwa upole sana kwa sababu Mheshimiwa Ndumbaro ni Waziri ambaye ni rafiki yangu kuhusu suala la Ng’ombe. Mimi nipo humu Bungeni nimeshuhudia mawaziri wawili Mzee Magembe alikaa pale na rafiki yangu ndugu yangu Mpina na juzi amelizungumza kwa uchungu kuisumbua Ng’ombe sidhani kama tunafanya sahihi hata kutuchaji tu elfu hamsini Ng’ombe ikikamatwa kwenye maliasili kule mbugani haifai, kwa sababu Ng’ombe haina uharibifu wowote.

Mheshimiwa Naibu Spika, hebu tufanye ulinganisho, tembo akienda kula mahindi hana faini Ng’ombe akienda kula majani anafaini kwa sababu gani? tufikirie kuondoa hii faini Ng’ombe anaenda kula majani na hii ni roho mbaya kwa wataalam Ng’ombe akiingia kula majani aharibu miti na mwisho wa siku majani mnayachoma moto sasa sielewi mnajenga viwanda vya kuchinja wapi kule Dar es Salaam na sehemu zingine machinjio za kimataifa halafu Ng’ombe mnazipiga vita mnataka kuchinja fisi au mnachinja vituo gani.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe sana Mhehimiwa Waziri tuondoe faini haiwezekani twende hata kitaalam tu kwamba kama ni sahihi kumkamata mtu ana Ng’ombe ukaichaji laki moja au elfu hamsini wakati thamani ya Ng’ombe ni laki mbili hebu tujaribu ma-traffic wakikamata VX wakuchaji milioni mia nusu ya bei uliyonunulia mbona tutayakimbia magari. Nifikirie sana Waziri kukushauri kwamba tuondoe hizi kodi ambazo zinaonea watu na tuache Ng’ombe ya Mtanzania itembee na uhuru popote ambapo itataka kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho nimemsikia Mheshimiwa Rais jana ameelekeza kwa uzuri tu, kwamba dhahabu ziingine kutoka Kongo na sehemu zingine, ni kweli, lakini Mheshimiwa Waziri naujua udhaifu tulionao naomba uzungumze na watu wako wa TRA wasisumbue wafanyabiashara. Wafanyabiashara wanapeana taarifa kuliko hata mitandao ya simu akikamatwa mmoja tu, wanaambizana wote hawaji na tunafungua viwanda tunategemea material kutoka Kongo ambapo kuna dhahabu ambazo hazina utaratibu. Kwa hiyo nikuombe sana tuwape uhuru wafanyabiashara na wasisumbuliwe na mambo ya polisi na mambo ya TRA.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru sana. (Makofi)
Itifaki ya Nagoya ya Kusimamia Upatikanaji na Mgawanyo Sahihi wa Faida zitokanazo na Matumizi ya Rasilimali za Kijenetiki.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme maneno machache sana kwa leo, hii safari tuliyonayo ya kuibadilisha Tanzania hawa wenzetu hawako na sisi. Kwa hiyo, ni kama tunampigia mbuzi gitaa. Hakuna mtu aliye tayari kusafiri na hii kasi tuliyonayo. (Makofi)


Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumza rafiki yangu hapa amechangia anasema tunaletewa Hati za Dharura, toka nimekuwa Bungeni taarifa zote za Kamati huwa tunapewa hapa, zinasomwa tunaanza kuchangia, sijaona jipya wakisoma taarifa tunagawiwa na sisi hapa tunasoma baadaye tunaanza kuchangia. Sasa kama ninavyowaona hawa, mtu mwenye akili hata kama ungepewa siku kumi huwezi kuelewa ambaye huna akili. Lakini mwenye akili haya masuala tumeshapewa leo na Kamati ya Uongozi imeshakaa imeshauriana sioni sababu ya kushindwa kuendelea na kujadili.

T A A R I F A . . . . .

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania wamemsikia Mheshimiwa anayejiita shemeji yangu kwa kusema nilisha-declare mimi sijasoma. Ni bora ukasema mimi ni darasa la saba kuliko kuwa na hivyo vyeti ulivyo navyo wakati akili huna. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumza haya maneno yanayozunguzwa humu ndani, yote haya ni propaganda kinacholengwa humu ni makinikia. Hawa watu


wanachokitaka ni safari ya kurefusha mjadala kwamba tusijadili hizi sheria ili tukabanane na wazungu tulipwe pesa, lengo lao ni kurefusha masafara ili wakatafute cross-cross kule Morena walikokuwa wanakaa. Hatukubaliani nayo ngoma imeletwa tupige leo hii hii tumalize.

Nafahamu hawa wenzetu hawana uchungu na hii miswada mara nyingi hawana uchungu, sisi wenzenu tulioumia tunatamani hata ingepigwa siku moja hii sheria ambayo inataka kwenda kumbana mzungu atulipe pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri tuende na ile slogan ya juzi kwamba hela zikitoka hawa tusiwape, zije kwenye majimbo yetu sisi wenye shida. Haiwezekani mtu anasimama hapa anazungumza anasema Wabunge tumekaa miezi mitatu tumechoka kutafuta nini wakati tunalipwa pesa, tuongezwe hata wiki mbili. Watu wenyewe njaa humu zimetuua humu watu mkifukuzwa mnatoa macho, halafu unakuja kuanza kuzungumza vitu vya ajabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nafikiria masuala haya yaende kama yalivyopangwa na hakuna mambo ya kutishana mambo ya Kibiti kuna nini. (Kicheko)

MWENYEKITI: Kuhusu Utaratibu.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana, unajua Waheshimiwa Wabunge Spika anatuelekeza vizuri uwe na tabia ya kuwasiliza na wenzio huwa tunavumilia, wewe umesema hapa tumekuwa Bunge la vibogoyo, kutoa macho unaumia? Na kweli umeyatoa macho! Tunawaona hapa mkifukuzwa mnavyotoa macho kule mtaani. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo suala la kuzungumza kukodoa macho au watu wamehongwa ni maneno yako tu na vitendo vyako vinadhihirisha kwenye Umma. Hivi kweli unategemea hiyo Serikali ya kuitoa CCM ya ninyi mnaowatetea wezi kwa style hii! Serikali ya ninyi mnaokataa kujadili Miswada ya kwenda kudai pesa zetu. Mimi nilikuwa nashauri tu kwamba hawa wenzetu hawapo pamoja na sisi katika safari ya kuibadilisha Tanzania, hapo wamekaa tu kizungumkuti lakini muda wowote walikuwa wanaondoka nje.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
TAARIFA YA KAMATI YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE KUHUSU SHAURI LA KUDHARAU NA KUDHALILISHA BUNGE LINALOMKABILI NDUGU PROF. MUSSA ASSAD, MDHIBITI NA MKAGUZI MKUU WA HESABU ZA SERIKALI
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Naomba nianze kunukuu maneno ya Katiba ambayo Mwenyekiti wetu wa kudumu wa upande wa pili ameyatumia kwenye Ibara ya 18. Katiba hiyo ambayo ameitumia, ukisoma Ibara ya 30 nadhani uhuru una mipaka yake. Mfano mwingine mzuri, sioni cha ajabu. CAG sio mtu wa kwanza kulikosea heshima Bunge. Tumekuwa na Wakuu wa Mikoa, tumekuwa na Waheshimiwa Wabunge akina Mheshimiwa Ester Bulaya. Hata hivyo, walipoitwa kwenye Kamati walijieleza na wakomba radhi. Walipokuja humu ndani, baada ya kuwasikiliza tuliwasamehe na kazi zikaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najuliza hii huruma inayotaka kuoneshwa humu Bungeni, hebu niwakumbushe, kuna watu akina Mheshimiwa Zitto walitumikia chama fulani kwa nguvu kubwa kukijenga, lakini walivyokiuka mipaka yao walifukuzwa juu kwa juu. Leo sisi kama Bunge tumetoa nafasi ya CAG kujitetea na kashindwa kuutumia uhuru wake, halafu tunaonesha huruma ya kazi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ingekuwa CAG ameitukana Serikali ambayo ndiyo iliyomteua ilikuwa siyo jukumu letu kuingilia hayo maamuzi, lakini Bunge, mimi nimeingia humu kwa kura 98,000. Mtu anakuja anasema ni dhaifu plus watu wangu, halafu tunamsamehe! Haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami niwaombe Watanzania, kuna watu dhaifu humu ndani, tunawaelewa. Wawachambue waone kama wanahitaji kuwa dhaifu wawaoneshe huruma yao. Sisi ambao sio dhaifu kwa maelezo ya kamusi, tunaomba yaendelee maamuzi ya Kamati.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Raisi kwa kazi nzuri anayoifanya, na mim ni mmojawapo wa watu ambao kwa kipindi chake tumeshanufaika na mabilioni ya Mheshimiwa Rais Samia. Nimepata madarasa siyo chini ya sabini, lakini kwenye barabara nina zaidi ya Billioni Nne ni kazi kubwa sana, tunampongeza sana na tunamuombea aendelee kufanya kazi na kusaka pesa Watanzania waweze kufaidi Urais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka kumshauri Mheshimiwa Waziri kwamba katika mpango unaoandaa hebu angalia ukamilishaji wa miradi. Tunakuwa na miradi mingi ambayo haifiki mwisho, ukiangalia kuna baadhi ya Halmashauri mpya zilipewa Billioni Moja za kujenga majengo na ramani ikaletwa ya ghorofa, leo tunamaliza mwaka hamna hela wala sioni kama kuna dalili ya kupewa tena hela ya kumalizia kwa kipindi kifupi, watu wameshamaliza majengo utakuta wengine wameweka na kenchi mbao zinaoza mirunda imeoza, ikija tena Bilioni Moja mnakuwa tena kama mnaaza kukarabati majengo upya. Kwa hiyo ninaomba katika mpango wako upange kukamilisha ile miradi ambayo Serikali ilikuwa imeianzisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vivyo hivyo Mheshimiwa Waziri hata kwenye hivi vituo vya afya ulivyotoa pesa milioni 250 tutajenga majengo mengine yatafika renta na ramani mmeleta, mengine yatakamilika tutabakiza ukamilishaji, tena tunasubiri miaka miwili mitatu ndiyo unafikiria kutuletea, kwa hiyo ni vizuri ukatoa kama ni hizi chache mlizotoa zikamilishwe ziishe ili mwakani muanzishe nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavyozungumza hapa kuna watu wengine humu ndani wana Hospitali za Wilaya bado hazijakamilika mpaka leo, kuna wengine pesa zao zilichukuliwa na mfumo wa Serikali ule wa mwezi wa sita mpaka leo Halmashauri yangu inadai milioni 290 mpaka leo, sasa tunaenda kuanzisha zingine. Kwa hiyo, ni vizuri mpango mzuri ni ule unaokamilisha na watu wanaanza kukitumia, tunaanzisha vitu tunasema vizuri majukwaani halafu kitu kinakuwa ni jengo halina huduma, haliwasaidi Watanzania na sidhani kama wanafaidika sana na hiyo mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo linguine tunazungumza kukuza Shirika latu la Ndege, nimeona kwenye mpango unataka tukushauri unajenga viwanja, Mheshimiwa Waziri, ninashauri tu naona hapa Dodoma hatujakaa vizuri, uwanja wa Dodoma unatumika mwisho saa 12. Ninyi wenyewe ni mashahidi ukiwa na kazi Dar es Salaam umeitwa Dodoma tunakimbizana kweli kuvizia ndege kila siku imejaa. Uwanja ule uliwekwa taa za kutua usiku lakini feki, kwanini msiweke taa ndege ikatua mpaka Saa Mbili, Saa Tatu, Saa Nne tukawa na route za usiku, tumefungiwa taa mpya mpaka leo zinamaliza mwaka hazifanyi kazi, bora kama tulipigwa famba na Mheshimiwa Waziri agiza taa tumalize uwanja huu uwanja wa kiuchumi, watu wanataka kuja kufanya kazi Dodoma wamalize mikutano Saa Mbili wakalale Dar es Salaam, haya ndiyo maisha Mheshimiwa Rais anasema nchi imefunguka kwa hiyo tufunguke vitu vyote siyo kufungua vitu nusu nusu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumza kwa upole sana suala la wamachinga maana nikizungumza kwa ukali nitasemwa mimi siyo Mtanzania, lakini nilivyolisema mwanzo nadhani watu hamkunielewa. Nikishukuru sana Chama cha Mapinduzi kupitia Mwenezi wake alinisaidia, niposema niliambiwa mimi ni Mrundi siyo Mtanzania lakini Mheshimiwa Mwenezi wangu kwa sababu yeye ni mweupe nilitegemea alivyosema wangesema yeye ni Mwarabu, sasa kwa vile imekuwa ngoma draw nitalizungumza kwa upole sana.(Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi natoka vijijini nami ni mkulima wa mpunga, tunavyozungumza leo gunia la mpunga ndani ya mwezi mmoja limeshafika Shilingi 90,000, mimi nimeuza jana shilingi 90,000 na wiki mbili tatu tulikuwa tunauza shilingi 40,000 hadi shilingi 50,000 nikawa najiuliza huu mpunga tunauza nchi gani ambako kumefumka njaa, hakuna! yaani mchele umepanda hapa hapa ndani kwetu nikajiuliza swali ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefanya research kulingana na akili yangu kidogo tu, kwamba walaji wa mchele sasa hivi wameongezeka, ukienda huko Njombe, Lushoto na sehemu zingine wauza viazi vya chipsi wanalia vinaoza hamna walaji! Kwangu nauza mananasi tulikuwa tumezoea ukipeleka mananasi Mjini wananunua machinga hawa wanakatakata wanawauzia watu Shilingi Mia Mbili, Mia Mbili, Mia Moja linanunulika, hakuna Watanzania wengi wanaoweza kununua nanasi la Shilingi Elfu Tatu au tikiti maji ambalo lilikuwa linauzwa kwenye kapu shilingi 500 sasa hivi hayanunuliki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge niwaambie ukiondoa kama hatuna maisha ya Kibunge hata mimi naamini humu ndani Wabunge wenzangu kwamba kama Wasukuma wenzangu tunazaa watoto 10 - 15 bado Shangazi na nani wamekuja kukusalimia, unaweza kweli ukakaanga chipsi mkala mlo wa usiku, utaweza hiyo gharama za kuandaa chipsi? kwa hiyo watu wote wamerudi kwenye wali, tunakula tunabakiza na kiporo cha chai! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wanasomesha wana watoto labda 15, wana Watoto watatu hata Dar es Salaam, mtoto anatoka Mbagala anasoma shule ya Uhuru, ulikuwa unampa elfu moja, maisha ni magumu elfu moja anakula chipsi kavu kwenye nailoni, sasa hivi machinga wote wamefurumshwa mnataka watu wakale kwenye restaurant. Kwa hiyo, ni vizuri mimi nilielewa kabisa Mheshimiwa Rais alivyosema tukawaandalie mazingira mazuri, mazingira mazuri ni yapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo yameandikwa public interest labda mimi kwa sababu sijui kizungu yana kazi gani? Kwa mfano Mnazi Mmoja ile ipo wazi, public interest sasa hivi wamebaki kukaa mateja tu wavuta unga kwanini msiwaweke pale wamachinga, unamtoa mtu unampeleka Mbagala kwa hiyo ni vizuri Mheshimiwa Waziri tuchunguze vizuri kwamba tunawatoa watu tunawapeleka kule tunapobaki hapa tunaanzisha vita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mimi nina duka Kariakoo nijitolee mfano nina siku ya Saba sijauza kila siku ninatuma nauli hapa, hebu jifikirie mfanyakazi wangu ambaye nilikuwa nampa elfu tatu posho ya chakula leo anatakiwa akale restaurant chai Shilingi Elfu Mbili, mchana Shilingi Elfu Tano inakuwa Shilingi Elfu Nane nitaitoa wapi? Kama mnabisha Waheshimiwa Wabunge wewe nenda tu pale Kariakoo sasa hivi pale Congo, utaona kila anaefungua duka ana mfuko una hotpot, watu wanakuja na makande, watu wanakuja na wali wa kiporo, haiwezekani kuhudumia kwa sababu hatuuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nakushauri sana Mheshimiwa Mwigulu, jaribu kuliangalia na bahati nzuri umenitaja nakushukuru maana wewe ni Waziri wa Fedha inawezekana una takwimu vizuri kwamba mimi ni tajiri, mimi ni zao la machinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, machinga wapo wa aina tofauti, kuna machinga mwingine anashinda tu mlangoni kupiga debe anakaribisha watu anapata elfu mbili, usifikiri watu wote wana mitaji na hao wenye mitaji ndiyo wanaowawezesha machinga huwezi kuwatenganisha, ukiwatoa machinga mtaa wa Congo biashara imekufa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanaofanya research ni machinga, unataka unitoe Mwenge nikanunue Congo halafu nije nimepanda daladala, machinga akinunua Congo anakuja kwa miguu anauza barabarani, kwa hiyo ni vizuri hili zoezi tulichukue kwa uzuri. Hata ukiangalia nilikuwa napata takwimu za Mkoa wangu wa Geita, vijijini tunataka kwenda kupiga watu Katoro kuwatoa machinga, hatuna mtaro wa maji, hatuna waenda kwa miguu, hatua yaani ‘bagosha’. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tufike mahala kwa kweli kwenye mpango najiuliza vizuri, mlitengeneza maandiko mazuri sana mkajenga stendi mkajenga masoko, chukua mfano soko la Kisutu, soko la kuku bahati nzuri kuku zinatoka kwa Waziri wa Fedha kwa Mwigulu, kuku ya Singida huko Kinampanda unaipeleka kwenye soko ya kioo na kigae, ikidonoa hivi inaumia mdomo, ikiangalia juu kuna taa hee! Zimeshindikana, ndiyo maana Rais anawaambia jamani haya masoko mengine tuyageuza yawe ukumbi wa starehe hamumuelewi! Kwa nini msifanye hizi gharama za kuandaa stendi na masoko ya ajabu ajabu mkawekeza kwa wamachinga kuliko kuwatesa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli najiuliza mpaka kuna masoko mengine ambayo machinga tumeanzisha wenyewe, tunaenda kupigwa. Mfano Mwanza Nyamagana, kuna soko linaitwa Buhongwa kule barabarani watu wameenda wameanzisha miaka na miaka, leo eti unatengeza mazingira bora, unaenda unawatoa barabarani unawapeleka dampo wanapotupa vinyesi….

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma muda wako umekwisha.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru Mheshimiwa Waziri wa Fedha umenipata vizuri kuhusu kuku.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia. Kwanza niwapongeze sana Wenyeviti wa Kamati na Wajumbe kwa taarifa nzuri, pia ninaipongeza Ofisi ya CAG kwa taarifa ambayo ametupa Wabunge kuweza kuona mapungufu.

Mheshimiwa Spika, ningependa nianze kwa upande wa Halmashauri. Jana nilimsikia rafiki yangu Boniphace Getere alizungumza kwa uchungu sana kuhusiana na madudu yaliyofanyika kwenye Halmashauri yake, hili ni somo zuri sana la kujifunza. Sisi Wabunge wote humu ndani tunamheshimu sana Mheshimiwa Boniphace Getere kwa sababu ya information, ni mtu ambaye anajua vitu kabla ya wengine hamjajua. Hebu fikiria mtu tunaemheshimu kama hivi Halmashauri yake kuongoza kuwa na Hati Chafu. Hili ni suala ambalo tunahitaji pia Serikali itusikilize.

Mheshimiwa Spika, siyo kwamba Mheshimiwa Boniphace Getere hajawahi kuona haya matatizo kabla, ameyaona hata kabla ya Mkaguzi lakini sasa ni nani anachukua hatua ambapo Mheshimiwa Boniphace anapoona yale matatizo akiyapeleka kwa wahusika yanachukuliwa kama majungu.

Mheshimiwa Spika, sasa najiuliza mara mbili mbili, hivi ni kweli Wabunge kwenye Halmashauri zetu tunasubiri mpaka Mkaguzi wa Hesabu za Serikali atutangaze kwenye vitabu kwamba Halmashauri yako ina Hati Chafu? Hapana hii ni aibu. Ni lazima tuone namna! Nilikuwa najaribu kujiuliza kaguzi kama tatu nikiwa hapa Bungeni, madudu mengi sana yanaonekana yako Halmashauri, ni kweli tunajadili humu na tunasema, sasa najiuliza tulitengeneza Sheria kwamba Mheshimiwa Rais anakabidhiwa ripoti ya CAG halafu inasema ipelekwe Bungeni sasa kujadiliwa kwenye Bunge la Wananchi, nasi tunakuja tunaongea, lakini mwakani yale yale yamezaa na kuzaa! hii siyo sawa nafikiria nasi tubadilike ni lazima na sisi tuone namna ya kuishauri Serikali au tuone namna kama ni Sheria tulitunga Sheria mbaya basi tubadilishe, hakuna maana ya kuja kujadili wizi kila mwaka, wizi wakati hakuna hatua zinazochukuliwa.

Mheshimiwa Spika, najaribu kuchukua mfano mmoja, utanisamehe maana wewe ni Mwalimu wa Chuo Kikuu cha Law School. Ni kama pale Law School watoto wanavyolalamika kila mwaka, wanalalamika wanafunzi 600 wanafaulu 26 na sisi hatuchukui hatua, sasa najiuliza wakalie wapi? Kwa sababu tatizo ni walimu au tatizo ni wanafunzi? Maana kila mwaka Law School wakimaliza Mia Sita wanafaulu wanafunzi 20 au wanafunzi 30 na hakuna hatua tunachukua kama Bunge. Sasa ndiyo kama huku, kama chuo hakifaulishi tatizo ni Walimu wa Chuo au tatizo ni Wanafunzi? Sasa tunaambiwa kila siku na CAG matatizo yako Halmashauri na Bunge tunawalalamikia Viongozi wetu huku kuna wezi, huku kuna nini lakini matatizo yanajirudia yaleyale na hatuchukui hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili suala ningeomba sana Wabunge tuone aibu na ingependeza zaidi, maana wananchi wetu wanajua na ikitokea Halmashauri yako imepata hati chafu wa kwanza kuwa mchafu ni Mbunge kwa sababu wewe ndiyo wamekuchagua uwe mle, uwasaidie kuwasemea, uwasaidie kusema huyu ni mbovu, sasa unanioneshaje mimi kama Mheshimiwa Musukuma ni mchafu na sina uwezo wa kukagua hesabu, sina uwezo wa kusimamia miradi mpaka inakuja kusemwa na CAG? Nilikuwa nashauri sana kama wenzetu huko nyuma walikosea kutunga sheria, hili Bunge ni la kisasa tubadilishe sheria ili tutengeneze adhabu humu ndani. Nami naunga mkono maneno ya ndugu yangu Mheshimiwa Kunambi, mengine hatuungani lakini hili nakuunga mkono.

Mheshimiwa Spika, labda tufike wakati hizi nafasi za Wakurugenzi zitangazwe. Ukiuliza Wabunge humu kila mtu ana presha na Mkurugenzi! Mbunge pale yupo yupo tu kama mpita njia, yale mambo mabovu anajua sasa hivi mko kwenye Bunge anapitisha fastafasta na anakualika leo kesho ngoma inatembea, ninaomba sana kama tulifanya makosa huko nyuma ni vizuri tukarekebisha maana sote ni Wabunge, tunatoka kwenye Majimbo kwa hiyo, siyo vizuri na siyo sahihi kusemwa humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ninadhani hata kwenye Ofisi ya CAG inatakiwa tuseme vizuri, kuna vitu najaribu kuona hapa sijui kama nitatumia lugha ya kuudhi kwamba muda mwingine hizi hati safi na hati chafu hazipatikani hivi hivi, kuna sehemu ambapo ni pachafu pamepewa hati safi, sitaki kutaja ni wapi. Sasa najiuliza, wenzetu hawa wanapokuja kukagua pengine huwa kuna mazungumzo ili itengenezwe hati safi na hati chafu au ni vitu gani? Kwa hiyo, nishauri na wao watu wa CAG wanyooke kama wanavyotaka sisi tunyooke kwenye ripoti ili ripoti zao ziwe na msimamo mzuri. (Makofi)

Mheshimwa Spika, kwa mfano, kwenye Halmashauri tunapata wageni kwa mfano Mawaziri mnapokuja. Na hili Mawaziri mtusikilize mtuelewe, mnapokuja kwenye Halmashauri zetu punguzeni mwendokasi kwa sababu haya mambo tunayajadili humu mnayasikia na kila siku tunawauliza maswali, lakini Waziri unakuja dakika kumi unapelekwa kwenye majengo huna muda wa kusikiliza, sasa unajiuliza yaani Waziri unakwenda kupima performance ya Halmashauri kwa kukagua tu jengo au darasa lililopakwa rangi vizuri? Hapana kaeni ndani mtusikilize tunazungumza nini, sikilizeni Madiwani, kuna sehemu Madiwani hawana nafasi hata ya kuwashauri Wakurugenzi.

Mheshimiwa Spika, Mimi najiuliza sijui muundo wetu sijui ulikuwaje kwa sababu hebu jiulize, huwa namuona Mheshimiwa Waziri Mkuu akienda mahala anakaa anaanza kutaja Tarehe Fulani, wiki fulani, document fulani huwa anatoa wapi hizo document? Kwa sababu nanyi ni Mawaziri, mbona huwa hampati huo muda wa kuwaambia hivyo wale mnaoweza kuwawajibisha? Lakini tunaona Mheshimiwa Waziri Mkuu anapoenda akifika pale anaeleza yale, anasindikizwa na Kamati ya Ulinzi na Usalama hili nalo ni tatizo lingine tukitaka kukomesha haya mambo. Kwa sababu Kamati zetu za Ulinzi na Usalama, Mkuu wa Wilaya uwezo ni mdogo wa Kwenda kukagua, ili akakague anahitaji mafuta ya Mkurugenzi, hivi vitu hawezi kuvikemea hata kidogo, kwa sababu mtu amekuwekea mafuta, ukute amekuandalia na lunch, haya mambo utafanya kwa design gani? unakuwa kama mtumwa! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unajisikiaje Mheshimiwa Waziri Mkuu ukifika pale unakosoa? Niliona kajengo Milioni 20, mimi naweza kukajenga kwa Milioni Moja na Laki Tano na Kamati ya Ulinzi ipo, unawaambie eeh… na jana walienda ku-reck njia ya Waziri Mkuu anapoenda pale, sasa najiuliza kwa nini tusifukuze wote wale? Kwa sababu kuna vitu vingine kwenye muundo wa Serikali vilitengenezwa kwamba hili litafatiliwa na mtu fulani, lakini wenzetu hawatimizi majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningeomba sana suala la Halmashauri linahitaji muda, Wabunge tupewe heshima tunapoleta matatizo yetu kwa Mawaziri, Mawaziri chukulieni serious, sisi siyo wapiga majungu! Mnachukua maneno yetu mnayapeleka kule ndani yanageuka kwamba huyu ni mwongeaji! Hapana, mwisho wake mtatukatisha tamaa na sisi tuwe watazamaji ili mkija, nakaa nyuma, ukiuliza maswali na mimi nashangaa. Hivyo, ni vizuri zaidi tuone wivu na Ubunge wetu siyo vizuri kuanza kukosoana humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni suala la asilimia Kumi, kama tuna mahala tulikosea muundo wake ni hapa. Hizi ni hela unamchukua mtu wa Maendeleo ya Jamii, unamkabidhi Halmashauri kama ya Geita ambayo kwa mwaka inatoa asilimia Kumi Shilingi Bilioni Moja, halafu anakwambia miaka mitatu sijakusanya. Hivi tuna watu wangapi waliosoma mambo ya uhasibu, mambo ya fedha? Kila siku benki zikitangaza kazi watoto wanaomba mpaka Elfu Tano, Elfu Kumi, kwa nini tusiwe na Kitengo cha Benki kwenye Halmashauri ambapo zinao uwezo? Kama hatuwezi kuna Mbunge mmoja jana alisema, tukubaliane na mabenki, tupunguze tu masharti kwenye kitengo cha vijana walemavu na akina mama, lakini fedha ziwe benki, watu ambao wana uwezo wa kuzikusanya hizo hela. Unakuta Halmashauri inadai karibia Bilioni Kumi na Sheria inakutaka utoe, sasa tunachukua hela tunaenda kuzigawa ambazo hazina return siyo vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilitaka nizungumze kuhusu DART, nimesoma kwenye DART yale mambo ya mwendokasi, huwa najiuliza mara mbilimbili kwamba, DART tunamiliki miundombinu, kuna mwingine anaendesha magari, hata mwaka mmoja kila siku ana-declare matatizo, lakini Serikali inachukua ela inarundika kutengeneza mabarabara, tuliutumia mfumo mzuri kweli kwamba, Serikali inatumia mabilioni ya pesa kutengeneza barabara kwa ajili ya kumtengenezea mtu mmoja apitishe magari ambayo tena hayafanyi vizuri! Sasa najiuliza tuna Mkurugenzi, tuna nani, tuna makoloko kwenye idara ambayo haizalishi! Ni vizuri tukawa tunatengeneza miradi ambayo inazalisha

Mheshimiwa Spika, nilikuwa namsikiliza Ndugu yangu Mheshimiwa Kunambi hapa anasema hotel nyota tano sijui nini, lakini kama kuna vitu wasomi mnatuangusha, Mimi ni Daktari wa heshima ni hapo, kutengeneza vitu ambavyo havina return. Mimi ninakaa Dodoma hapa huwa naumia sana nikipita pale nikiona ile hotel najiuliza kwamba, wasomi walikaa na ku-discuss kutengeneza ile hotel wanaita mmh! (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, wakati hapa Dodoma kuna maeneo ya heka kumi na yeye ndiye aliyekuwa anauza viwanja! Hii hotel ilikuwa nzuri na ya mfano ya kutengeneza Jiji, ingekuwa sehemu yenye heka tano, hivi vitu unatengeneza soko halafu unajisifu, tuambiwe return hizi ni hela za wananchi…

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, taarifa!

SPIKA: Mheshimiwa Musukuma, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kunambi.

T A A R I F A

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa ndugu yangu Musukuma kwamba, tulikuwa tumeangalia kwenye hotel anazosema, kuna ile ya Mjini inaitwa Drop off Hotel na lengo tuliangalia viability of the project, returns on investment, tuliangalia pia muda gani utatumika. Kwa ile kulingana na andiko letu ilikuwa ni miaka sita, sasa hoja tulisema wawa-engage operator ili a-operate, lakini ndani ya miaka sita ile fedha ilikuwa inarudi Bilioni Tisa. Kwa maeneo anayosema, Mji wa Serikali tukaona lile eneo ni kubwa, tukatengeneza hotel nyingine ambayo ni ya nyota nne yenye parking kubwa sana. Kwa hiyo msingi wa hotel ya Mjini ni drop off hotel hata Dubai zipo. Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Msukuma unapokea taarifa hiyo.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, siipokei taarifa hiyo, mwenye macho ameona na mwenye masikio amesikia, kwa sababu tutajibishana na ninamheshimu ni mdogo wangu na nimheshimiwa Mbunge lakini ni lazima tushauri vitu vyenye maendeleo.

Mheshimiwa Spika, ukichukua hiyo hotel anayoisema na vitu viwili vitatu umevisema ukiweka na soko la Ndugai nikikuuliza return yake hata na mimi nitakuwa nimeshakufa bado hata theluthi moja haijawahi kuwa na return, halafu unasema hiki tunatengeneza chanzo baada ya kumaliza ardhi, Hapana! Tutengeneze vyanzo vyenye maslahi, tushauri watu, vitu vyenye maslahi.

Mheshimiwa Spika, kuna Mjumbe jana alisema humu ndani, ukienda kwenye kila Halmashauri wote tunaandika maandiko kwa sababu hela zipo tunataka stendi, lakini stendi siyo mradi endelevu. Kuna watu wengine wameweka stendi baada ya miaka mitano au 10 haina return yoyote. Lazima tuone sehemu kama Dodoma, Dar es Salaam, Mwanza, kwenye Majiji sawa lakini unachukua stendi ya Bilioni 29 unaenda kuweka kwenye Halmashauri inayokusanya Laki Tatu na Hamsini kwa siku, halafu unaita mimi nimesoma, nimefanya upembuzi yakinifu, hiyo haiwezekani! Tunawaingiza chocho kwa sababu wanaolipa ni wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakubaliana na wewe kwamba tunavyo vyanzo vya mapato ambavyo vitalipa yale madeni, kwa nini tusifikirie kuisaidia Serikali kama ulivyojenga kule Mlimba Vituo vya Afya na vitu vingine ambavyo moja kwa moja vitakwenda kuwasaidia wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ningeomba nishauri suala lingine moja la mwisho. Nimepita pale Dar es Salaam ninajua tu hili litakuja kuamka, jana humu ndani nimesikia wamechangia. Ukiangalia mwendo kasi leo wa kutoka Mbagala stendi yake imeenda kuangukia pale kilipojengwa kitovu cha ramani nzuri sana ya mwendokasi mkubwa, watoto wa mjini tunaita Tanzanite pale. Jiulizeni jamani mtu anatoka Mbagala halafu kituo kinakuja kuangukia palepale kwenye ramani ambayo tunachukua ramani hata Kimataifa tunarusha kwamba mwendokasi, tunadondoshea kituo pale cha watu wanatoka Mbagala. Kwa hiyo, mwingiliano ule ni vizuri yaani…(Makofi/Kicheko).

Mheshimiwa Spika, kwanza hata ramani, najiuliza kwa nini tusingeondoa elimu za darasani tukatumia kama yangu ya heshima? Yaani nafikiria unajiuliza kabisa kwamba wamekosa sehemu yoyote ya kuweka kituo? Ramani ya ile Tanzanite, glass yote ile nzuri, halafu inakuja kudondoshewa pale pale giiih!, Mtu ametoka rangi tatu kule, huku inaka…jamani, jamani ndugu zangu na lenyewe tunasubiri CAG mwakani atuletee taarifa? Kwa hiyo, ninaomba sana niwashauri, tuna wivu na Ubunge na Wasomi wetu tunawapenda, ningeomba mtumie shule zenu vizuri. Ninakushukuru ahsante sana.(Makofi/Kicheko)

SPIKA: Kengele ya pili Mheshimiwa.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Ulega kwa kuchaguliwa kuwa Waziri wa hii Wizara. Nina matumaini kwamba Mheshimiwa Ulega atakuwa msikivu kwa sababu kama ni mwanafunzi amesoma kama miaka minane hiyo elimu ya Uwaziri, sasa sitegemei kama atatuangusha. Mwanafunzi mzuri ni yule anayesikiliza walimu wake na baadaye anafaulu, tunamwombea sana Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nianze kwa kusema sisi tunatoa tu ushauri kwa Serikali, wanaweza wakakubali au wakakataa, lakini mkikataa mbeleni tutakuja kuulizana maswali. Mwaka 2017/2018 ndugu yangu Mpina akiwa Waziri yeya akiwa Naibu, tulizungumza hapa kuhusu usumbufu waliokuwa wanaufanya Ziwani kwamba madhara yake tutayaona baadaye hawakutusikiliza. Leo tunalia samaki wameisha, wavuvi wamefilisika haya yote Mheshimiwa Waziri ameyapitia sasa tunataka tumpe ushauri atoke hapo alipoikuta Wizara, aende sehemu ambayo Mungu atamsaidia aendelee kubaki kwenye hii Wizara kama Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita tu kwenye suala la herein. Inahitaji kuwa mjinga sana kwa kizungu mnasema you need to be very ignorant kizungu ndiyo mnasema hivyo? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake unatakiwa kuwa mjinga wa mwisho, kutoutambua huu mtego. Hawa wafugaji ni watu maskini na Serikali lazima wasikilize, hii biashara wanayoiweka wanaolalamika ni wananchi, wanaotutuma ni sisi Wabunge. Mwaka 2025 watasimamisha kukitetea chama chetu na kuomba tena nafasi ya kurudi humu kama hatuwasikilizi hawa na kuyaleta malalamiko humu ndani wakayafanyia kazi, wakaanza porojo za kupandishana, kuwekeana maneno mdomoni, haitatusaidia huko mbele tunakoenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, herein, mimi nafuga ng’ombe, watafiti na wataalam, waliosomea mambo ya mifugo, walianza wakaja hapa na mihuri ya kugonga si wao? Wakashauri tukiweka hivi tunapata thamani ya ng’ombe, wakagonga ngozi, wakaja wakavalisha bangiri, sasa wamekuja na hereni nataka niwaulize swali halafu mbaya zaidi tunatafuta takwimu sahihi za mifugo. Unaenda kuchukua wakala akufanyie takwimu ndiyo akukabidhi, hivi hatuna wasomi waliosoma mambo ya TEHAMA, tunasomesha watoto wetu kwa kazi gani? Nataka waniambie tulihesabu binadamu sensa yetu ya mwaka jana, kwa nini hawakuweka wakala? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iliingia gharama bilioni 400, wakanunua vishikwambi, watu wakafanya kazi. Watoto wetu wamesoma TEHAMA, hawana ajira, wanaenda kuchukua mabilioni ya hela wanamrundikia wakala yumo humu ndani, ana-lobby lobby eti tufunge herein. Nataka niwaulize swali, sipingani na maagizo ya Waziri Mkuu, tunaboresha wasini-quote vibaya, hiyo hereni wanayoenda kuifunga, sidhani kama wamefuga ng’ombe, hivi ng’ombe wakigombana kule porini ikadondoka herein, wataniambia aliyepigana naye ni nani? Haya ng’ombe waangu wakihibiwa, wakaenda Mtwara kutoka Geita watanipigia Musukuma usiende pPlisi fuata wako Mtwara? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni utapeli ambao wanataka kutuingiza kutuchonganisha na wananchi. Mheshimiwa Waziri asikubali huu mtego, Wizara yakw iombe hela Serikalini, aajiri vitengo, katika kila halmashauri na kila kata tuna bwana mifugo ana kazi gani? Kwa nini asimpe takwimu za ng’ombe? Nataka niwaambie tusikubali huu mtego na Bunge likawa wakala wa kupitisha dili za watu humu ndani, haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfugaji ni maskini, ili apate laki tano lazima auze ng’ombe, hivi Serikali nataka niwaulize, huyu mfugaji ambaye Tanzania hii hathaminiki anaishi kama mbayuwayu tu yuko huku, yuko huku, unaenda kuhesabu ng’ombe ambao leo wako Geita kesho wako Mtwara, kesho Bagamoyo, yanakoota majani ndiyo mfugaji anaenda. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri kama kuna sehemu sasa amewekwa target ni hapa. Najua hili jambo alikuwa ulipendi maana tulikuwa tunateta kantini, sasa nataka nimwone term hii. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu wakala anayezungumzwa humu alishatajwa na Mheshimiwa Shabiby, atusamehe sana, sisi wote ni Wabunge na kila mtu ana neema kwenye jimbo lake. Jimbo la Kibaha linafuga kuku, tuzifunge kuku hereni kwanza kabla ya ng’ombe. Haiwezekani, hata kuku ni nyama na zinaingiza pato la Taifa. nikuombe sana Mheshimiwa Waziri akae vizuri asikubali huu mtego na najua watu tukizungumza humu wanasema huyu kafanyiwa lobbying kapewa hela, hakuna cha kutupa hela mimi ni mfugaji na Jimbo langu lina wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu anayepiga upatu jimbo lake linaongoza kwa mabanda ya kuku, tuanze na kuku, tuone mfano, lakini tukimaliza hapo Mheshimiwa Ulega, najua tena nafurahi jana kulikuwa na wageni mashehe leo hawapo. Mashehe kazi yao ni kuomba na najua na wewe kwako kuna ng’ombe, tujaribie Wilaya ya Mheshimiwa Waziri kwanza hizo herein, zikifaulu ndiyo walete hawawezi kuwa wanafanya majaribio kwa watu maskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sana hatuna nia mbaya na mategemeo ya Mheshimiwa Waziri, lakini anatuweka kwenye angle ambayo kiukweli siyo nzuri na Serikali yetu imetulia tunaenda kwenye chaguzi, watu wana amani, tumemaliza purukushani za machinga unaingia tena machinga mfugaji, hii kitu haiwezekani. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri na hata yule anayepiga dili tuangaliane kwa macho hivi, sijui kaenda wapi? Kahamia wapi? Tusikubali hili suala, najitoa muhanga, tusikubali hili suala likazungushwa humu ndani. Waziri aweke teknolojia, aombe Serikali impe kompyuta agawe kwa kila Bwana Mifugo, Afisa Ugani kule katika kila Kata wapo, leo Maafisa Ugani kule wamekuwa wanywa gongo tu, wanakaa maofisini, ukienda wamechoka hawana hata kazi. Ni watu wa operesheni tu midomo, sijui miguu, hawana kazi za kufanya, Mheshimiwa Waziri apeleke watu, alafu aone maisha yanavyoenda… (Makofi)

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma, kuna taarifa.

TAARIFA

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpa taarifa mzungumzaji kwamba hivyo anavyozungumza tayari Wasukuma, wafugaji wote wa Mtwara, Geita, Mwanza na Magu wote ng’ombe zao zina herein, je, watarudishiwa fedha?

MWENYEKITI: Mheshimiwa Msukuma, taarifa unaipokea?

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa mimi ni mfugaji, kwanza ukiacha alizoziona zina hereni, kuna zinazodai yaani hata uwekaji wa hereni unalipa kwanza, unaingiza kwa mtu hela, halafu ndiyo anaenda kutengeneza. Nchi hii jamani inahitaji kusoma kwa mtaa kabisa, tuache shule za darasani. Nakubaliana na yeye kwamba kuna hereni, kuna nini, lakini ni maumivu makubwa ambayo wafugaji wanayo kule kijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao wafugaji wamekuja kusikiliza hii Wizara, tokeni nje hapo muwaulize hii si kitu wala siyo hitaji. Kama hitaji ni la Serikali tengeni bajeti, mbona sisi binadamu wametuhesabu bila kutuomba hela. Hivi binadamu na ng’ombe nani ana thamani unaacha binadamu anayeingiza kipato kumhesabu hata kwa shilingi elfu mbili mbili anatuhesabu bure, halafu ng’ombe wanaomlisha mtu anapata madini mwilini, wanaichaji elfu mbili. Hawana soko, hawana machungio, hawana sehemu ya kunyweshea maji, wagosha wajameni! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana tubadilishe mwelekeo, Mheshimiwa Waziri…

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma kuna taarifa, kutoka kwa Mheshimiwa Emmanuel Shangai.

TAARIFA

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa mzungumzaji, kwenye minada yetu Wizara inapata shilingi 2,500 kwa kila mfugo unaouzwa. Watumie hizo fedha kuwahesabu hao ng’ombe.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana nayo. Nimwombe tu Mheshimiwa Waziri, asikubali kuingia kwenye huu mtego na hili akusanye hela atoke kwenye asilimia moja ya pato la Taifa, Mheshimiwa Waziri ananisikiliza au anachati? Atoke kwenye hii nafasi aliyobananishwa na naamini Wizara yake ina wasomi, tunamwamini sana rafiki yangu, msomi mwenzangu Shemdoe, wakae watengeneze utaratibu mzuri, haya mambo ya dili dili waachane nayo, ili upate kipato kizuri tujifunze kwenye Wizara ya Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Madini ilikuwa inachangia asilimia moja kwa sababu wachimbaji wadogo walikuwa wanawaona kama wezi, kila wanapovumbua madini wanawapeleka polisi, wanapiga watu wanaweka wazungu wenye leseni. Tulishauriana nao humu ndani leo angalia tunavyochangia kwenye pato la Taifa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Sina tatizo na, Mheshimiwa Ulega, lakini wakati wa ku–wind up hapa akija na jibu la mawenge mawenge namdakia shilingi yake, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2017/2018
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa ujasiri aliouonesha kwenye makinikia hayo yaliyoshikwa huko bandarini. Pia nimpongeze kwa ujasiri na kwa bahati mbaya leo Profesa Muhongo hayupo hapa, nilitaka nimkaribishe darasa la saba huwa tunakaa huku ili tuwe tunamfundisha hali halisi ya Watanzania tunayoina kule majimboni, tukaachana na ule u-profesa.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wengi humu wanaopiga kelele wamekaa na wawekezaji na wengine hata dhahabu hawaijui. Wanasema hatujaisoma Sheria ya Madini lakini yeye hajawahi hata kuona madini, anamiliki nyanya, kwa hiyo hivi vitu bora akakaa ili tuzungumze watu tulio na uchungu. Iringa na dhahabu wapi na wapi? Huyu mtu anamiliki nyanya, kuku na mbwa halafu anakuja kuanza kujadili vitu vya msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimwambie rafiki yangu msomi kabisa tuachane suala la mchanga; anifafanulie na aelewe wizi ambao uko kwenye migodi hii mikubwa. Ukienda kwenye uhalisia kwenye hii migodi ya North Mara ukienda Buzwagi, ukienda Kahama Mining kote kuliko na migodi hii kuna kanembo kadogo kameandikwa ACACIA; na ACACIA ana hisa asilimia 21 kila mgodi na ameziuza kule Uingereza amepata Dola bilioni 275 na Serikali yetu TRA wakaenda kudai kodi, akawaambia mimi sina file kwenu, tumeshinda kesi amekata rufaa. Sasa alichokiuza kule Uingereza ameuza nini? si ameuza North Mara ya Mara, ameuza ACACIA, ameuza Buzwagi ya Kahama, ameuza Kakola? Sasa hawa watu wana kesi nyingi na ndiyo maana Mheshimiwa Rais amesema tuwachunguze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halafu kingine, suala hili siyo la Bunge, ni Mbunge gani aliyegundua kama tunaibiwa ule mchanga pale? Ni Mheshimiwa Rais na jitihada zake, acheni akamilishe Tume atuletee humu ndani. Tunaacha kushughulika na mambo ambayo tumelipwa posho kuzunguka kama Kamati tukayaibua sisi wenyewe, mtu kaibua mwenyewe, hajakamilisha uchunguzi wake, ninyi mnaanza kusema anafukuza wawekezaji, anawafukuza wapi? Hii ni mifano tu, hili Bunge siyo lile mlilozoea kwamba mnakaa kule nyie wenye midomo, mnapewa hela kuja kutupigisha makofi, mtazirudisha time hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata wenzangu hawa upinzani wengine humu ndani mnapiga makofi bure wenzenu wamekula hela Morena pale mnataka tuwataje? Acheni watu wafanye uchunguzi tufike mahali Rais atoe mwelekeo. Rais ndiyo ameshika makontena wala hayakushikwa na Tundu Lissu. Nawashangaa Wanasheria mimi siyo Mwanasheria huyu ndiyo Rais. Dira ya Wanasheria wetu inayoongozwa na Rais Tundu Lissu ndiyo hiyo ya kupingana na sisi tunaibiwa? Naomba sana hawa vijana watulie Mheshimiwa Rais afanye kazi, kile ni kichwa acha kishike na mtashikwa na mengine zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama kweli huu mchanga wanavyosema wenzetu kwamba ukipelekwa kule Japan wao wanatoa madini ya aina tatu; wanatoa dhahabu, copper na silver. Sasa uchunguzi tu wala hatuhitaji Maprofesa waliohangaika na wanaoendelea kupiga maneno humu ndani, watupeleke kule Japan wakatuoneshe ule mchanga baada ya kutoa yale madini matatu ule mchanga una madini 32 ule unaobaki una nini? Kama una mali tuuze basi kule Japan hata kama wameyafyatua matofali si tutavunja tu hivi, tunapima, tunapata yale madini yetu? Tunapiga hesabu kubwa ambazo hawa hawaelewi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi natokea kwenye hiyo migodi mikubwa, nataka niwaambie ambao hawaijui hata dhahabu. Tunanunua mfuko mmoja wakati hawajaanza kusafirisha na bunduki, vijana walikuwa wanazunguka na wale madereva ukiuziwa kamfuko kamoja karambo ka- Azam kale Sh.800,000 unapata Sh.16,000,000 na tulikuwa tunaiba kweli na watu wamepata hela. Sasa kama hakuna dhahabu kwa nini wanasindikiza na Mapolisi mbele na nyuma na makontena yale yanalindwa hata yakiwa bandarini?

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwaambie Watanzania wajue na kama ingekuwa Mheshimiwa Rais anaweza kupokea ushauri wangu; hawa wanaobwabwaja huku tukawaruhusu wakafanye mikutano kule Kanda ya Ziwa, hamtarudi ninyi, hamjui shida tulizonazo. Tumeibiwa vya kutosha, tumuache Mheshimiwa Rais afanye kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Ole Milya kwa sababu yeye anajua maana ya Tanzanite, anajua tunavyohaingaika, ameunga mkono, achana na hao watu, mtu wa Dar es Salaam na dhahabu wapi na wapi? Mnyika anamiliki mtambo wa kujengea nyumba, hakuna kitu, hawa wanatusumbua watuache, tumemwamini Mheshimiwa Rais afanye kazi

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Muhongo...

KUHUSU UTARATIBU ....

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Mheshimiwa Waitara asifikiri mimi ni mwoga wa kupokea taarifa, kwa vile umefafanua nilikuwa right tu kuwataja, lakini nitawavumilia. Nimwambie tu kwamba, kwa vile yeye ameona nimesema uongo, anaweza akasimama yeye akatuambia kule African dream aliyelipa posho ni nani kwenye kile kikao kilichofanyika? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tunaotoka kwenye machimbo tunaiomba Wizara ya Nishati na Madini, maeneo mengi yamemilikiwa na watu wanakaa Dar es Salaam wala hawayachimbi. Sisi tunapata shida kila mwaka kuomba Wabunge wa Geita na Mungu katupa neema hii. Mheshimiwa Waziri alikuja akatuambia mwezi wa Saba na wa Tisa kuna maeneo yanarudishwa kwa wananchi tunayasubiria.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo nataka niwaambie wako wawekezaji wazawa wadogo tu wamewekeza zaidi ya bilioni 30 migodi kama ya GGM kwa nini Serikali na Wizara yake isiwakuze watu kama hawa? Uko mgodi wa Busolwa Mining, uko mgodi huko Bunda, kwa nini tusijaribu kuwakuza hawa tukaachana na hawa Wazungu wababaishaji? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Geita siku moja ilikuja ile helicoptor kuchukua dhahabu. Ilipofika pale wakazidishia tofauti na mkataba ulivyo, akakataa kurusha helicoptor, lakini TMAA hawa walikuwa wamegonga dhahabu iende kwa kiwango kile kile. Kwa hiyo, hawa wanaopiga kelele hawaelewi jamani nchi inaibiwa wajaribu kuja kututembelea wenzenu tunaachiwa mahandaki. Naliomba Bunge tumuachie Rais kazi hii aimalize, potelea mbali hata kama tunashtakiwa kwani Sheria ni ruler au ni glass kwamba ikidondoka itavunjika? Tukishtakiwa kwani Tundu Lissu asiposhtakiwa ana kazi gani? Wanasheria wetu watafanya kazi tuiachie Serikali na tumuachie Rais, sisi kama Bunge tumuunge mkono na mimi binafsi sijawahi kuona Rais wa ajabu kama Tundu Lissu, huyu ndiyo wa kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia. Kwanza, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri aliyoitoa Bungeni leo. Nina imani tunampongeza pia kwa kuwa ni Waziri ambaye anafanya kazi kwenye mazingira mazuri sana ya utawala bora.

Mheshimiwa Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri afungue nafsi, tunamtegemea sana kukuza wafanyabiashara, hasa wazawa wa Tanzania, kwa kipindi hiki ambacho nadhani ana uhuru mkubwa sana wa kuwasikiliza watu na kuamua. Tatizo ni kwamba Wizara haimalizi matatizo ya wafanyabiashara, yaani imekuwa kama ni mahakama, nenda, rudi, njoo kesho au keshokutwa. Nimwombe Waziri asiyakimbie matatizo ya wafanyabiashara. Wafanyabiashara wana matatizo mengi sana, wanategemea busara ya Waziri na yeye ni daktari na madaktari huwa hatukimbii matatizo, unakabiliana nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nataka nizungumze kidogo Mheshimiwa Waziri atakapokuja kujibu hapa aniambie. Tuna kampuni inaitwa SICPA, anaifahamu, inafanya kazi ya kuweka stika kwa ajili ya kukusanya kodi ya TRA; wafanyabiashara wamemlalamikia sana Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri afikirie mkataba waliouweka miaka mitatu iliyopita, kila kizibo kimoja cha juisi inayotengenezwa Tanzania anakusanya shilingi nane na Serikali inapata shilingi sita. Mtu wa kuja na briefcase anachukua shilingi nane. Waziri anatambua mkataba wao umeshaisha miaka mitatu. Bado wameongeza muda na wazawa ndio wanafanya hiyo kazi. Swali langu ni kama lilelile la jana, najiuliza hivi kweli wasomi wetu wa Tanzania waliosomea mambo ya IT wameshindwa ku-copy ule mfumo tukauendesha wenyewe? Kwa sababu na mkataba unasema ile mali imeshakuwa mali ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, najua wakati wanasaini mkataba walipunjwa kwa sababu labda kulikuwa na viwanda 19, leo tuna mia na kitu. Kiwanda kimoja tu nimefanya mfano wa Azam, anachukua karibu milioni 300 mpaka 400 kwa siku. Ukienda viwanda vilivyoongezeka mia mbili na kitu mwaka jana peke yake kaondoka na shilingi bilioni 100 na wazawa na makampuni mengine yako Tanzania yanakwambia tuko tayari kuendesha huu mfumo kwa shilingi moja, Waziri ameng’ang’ania nini kwenye shilingi nane? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huyu anayekuchaji wewe Tanzania shilingi nane…

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Musukuma, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Tabasam.

TAARIFA

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, kampuni hiyo inayofanya kazi hiyo ya kuweka stempu inapewa leseni na Kampuni ya Serikali inayofilisika ya Posta. Posta wangeweza kufanya kazi hii na pesa zote zikaenda Serikalini. Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Musukuma, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, naipokea. Darasa la saba huwa tuko active sana; nampongeza Mheshimiwa Hamis. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii kampuni inayochukua kazi hiyohiyo shilingi nane Tanzania, inafanya kazi Kenya kwa shilingi moja, inafanya kazi Uganda kwa chini ya shilingi moja. Sasa mtu huyu bado anaongezewa mkataba. Mkataba umekwisha, ongeza tena mwaka mmoja.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Tuamini kwamba Watanzania hatuna uwezo wa kuuendesha huu mfumo.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mfumo ni mali yetu, halafu tunaweka wakala tu katikati, mtu briefcase, anakusanya hela anapeleka Ulaya, halafu huku tunang’ang’ana kukamata mabegi ya watu huko Kariakoo wamebeba vijora viwili, vitatu. Hili… (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Musukuma, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kingu.

TAARIFA

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nataka nimpe msemaji taarifa kwamba kulingana na utafiti uliofanywa pamoja na kushirikisha Federation ya Wenye Viwanda Tanzania, kampuni hii Tanzania ndiyo nchi peke yake Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati kwa kutoza fedha nyingi zinaoumiza viwanda na Watanzania katika kugonga stempu za kielektroniki kwenye bidhaa. Federation ya Wafanyabiashara wameshapeleka concerns zao Serikalini, lakini ninachoshangaa kampuni hii bado imeendelea kukumbatiwa katika Taifa letu.

SPIKA: Mheshimiwa Musukuma, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, naipokea.

Mheshimiwa Spika, sasa nimwombe Mheshimiwa Waziri; kweli hatupendi aondoke au kuharibu huu mfumo, lakini sasa hivi margin ni kubwa. Viwanda 19 kwa viwanda 200, halafu hela zote zinakwenda nje, Wizara inachukua shilingi sita, mtu kati shilingi nane, inahitaji kwenda shule kweli? Si bora muwe Madokta kama mimi wa wa heshima tu tumalizane huko? Jamani! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wafanyabiashara wamekuja kwa Mheshimiwa Waziri, wameshakaa vikao zaidi ya kumi; ugumu uko wapi kuchukua maamuzi? Watuambie nani yuko nyuma ya mchezo huu, kwa sababu ni suala ambalo kwa mtu wa kawaida ukielezwa unajiuliza tu mara mbili, hata nikikataa kupunguza, wafanyabiashara wanasema tupunguze turudishe hata shilingi tatu wamemwambia, barua tunazo hapa, lakini Kiswahili, come tomorrow, wafanyabiashara mwisho wake labda wanasema kuna mtu nyuma yake. Haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimwombe Waziri, asiyakimbie matatizo, yeye ni daktari wa akili, wa kisomo. Amalize matatizo ya Watanzania wafanyabiashara wafanye kazi kwa uhuru. Mheshimiwa Rais anafungua masoko, wafungue uwanja wa kusikiliza watu na wawe na tabia ya kumaliza matatizo. Hatuna sababu ya kuja kupigizana kelele humu ndani, wala hatuhitaji tutajane, Hapana. Kama kuna mtu yuko nyuma ya mchezo amekula ametosha, watu wameshanawa, matongotongo yameisha, tuanze upya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haiwezekani, maana hata Wabunge tu kwa hili somo la muda mchache la Dkt. Musukuma hapa, wameelewa mchezo unaendaje. Sasa unahitaji kutumia degrees mbili mpaka tatu kwenye hili? Haiwezekani!

Mheshimiwa Spika, nazungumzia suala la wafanyabiashara kulalamika kuhusu TRA. Tunajua Mheshimiwa Rais akitamka watu wa viwanda na biashara wafanye kazi ya kukamilisha ndoto ya Mheshimiwa Rais. Alipokuwa Bukoba alisimama kwenye mic akawaambia TRA msisumbue watu madeni ya miaka mitatu au minne nyuma. Mpaka leo bado wanasumbuliwa, ukiwauliza TRA wanasema hatujapata maelekezo kutoka Serikalini. Sasa wanataka watu wakimwona Rais wetu anazungumza tuamini kwamba wao hamna uwezo wa kutekeleza? Kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Waziri, afanyie kazi matatizo ya wafanyabiashara ili aweze kuendana na kasi ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, nazungumza kwa uelewa wangu na sitaki taarifa kuhusiana na Tanga Cement. Unajua sheria mbovu ndiyo zinatufukuzia wawekezaji. Najua kila mtu ana wasiwasi, lakini lazima Wabunge tuwe na akili za kufikiria mara mbilimbili. Hili suala la Tanga Cement kuna mchezo tunachekechwa, ama humu ndani au huko nje, kuna mtu pia yuko nyuma.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia watu waliofungua kesi ya Tanga Cement kuna kampuni inaitwa Chalinze Cement Limited. Nataka waniambie hii kampuni iko wapi. Nataka waniambie Kiwanda cha Cement cha Chalinze kiko wapi. Tanzania hii mimi ni mwenyeji, hiki kiwanda kiko wapi? Watu wana kiwanda mfukoni halafu wanakwambia kiko Chalinze. Nimetoka Chalinze juzi, nimezunguka Lugoba yote sijaona, na Mheshimiwa Ridhiwani yumo humu, nimemuuliza kiwanda kiko wapi, Mbunge hajui. Aasa huyo Chalinze ni nani anayetufungulia kesi? Maana yake tunachekechwa hapa, tusioneone aibu, tusitembeze dili humu ndani Waheshimiwa Wabunge. Chalinze na Chama cha Kutetea Walaji kiko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yaani tunatengeneza hofu, wanatengeneza utawala bora halafu wanajenga tabia mbaya. Mtu anawaambia mimi nimefilisika, nauza mali yangu, kama sheria ni mbovu, haya, akifunga tutauza skrepa? Wanampeleka wapi? Akiamua kufunga sasa mmezuia nisiuze. Nashauri, inawezekana hawa wenzetu wakati mwingine ni wajanja, wanatukwepa tusipate kodi ile ya zuio. Serikali isimamie mchakato, lakini hawa wacheza dili Waziri akija hapa najua anashughulika na hili suala, naomba atutangazie humu Bungeni hicho kiwanda cha Chalinze kiko wapi.

Mheshimiwa Spika, Wabunge ni wafanyabiashara; mimi ni Chalinze ninayefungua kiwanda cha cement, lazima nijue mkubwa ambaye nitashindana naye ni fulani, halafu anafilisika mimi nasema hapana, usifilisike, wakati mimi ndio nataka kufungua kiwanda. Jamani, hizi dili zitatumaliza Tanzania, lazima tutumie akili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri akija hapa aje na majibu mazuri, tusije tukaharibu image ya nchi yetu kwa wahuni wanaotembea na briefcase kwenye kwapa, hatuwezi kuishi kwa madili. Mshindani wako unamwoneaje wivu kufilisika mpaka ukafungue kesi, ulishaona wapi hii? Kama sheria tulitunga mbovu tuacheni kutembea na madili kwapani jamani, tutetee Tanzania. Rais anataka wawekezaji tumwache aoneshe ndoto zake, tutaulizana baadaye, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Wizara ya Ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Geita Vijijini kwa kazi kubwa aliyotufanyia na nasimama kwa kujiamini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaiona hii siti niliyokaa, hata mwaka 2026 niko hapa hapa, kwa sababu ya hii Wizara. Mimi nakaa kilometa 54 tu kutoka ninakotoka jimboni kwangu kwenda Geita Mjini, lakini kilometa kama 105 kutoka jimboni kwangu kwenda Mwanza ambayo ndiyo Geneva yetu kwa Kanda ya Ziwa. Tulikuwa tunatumia saa saba hadi kumi kwenda Mwanza; saa tatu kwenda Geita. Pamoja na kwamba sina lami, lakini nikupongeze sana kaka yangu Mbarawa, Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa na Wizara yako unayoendelea kunifanyia kwenye jimbo langu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiukweli pamoja na kwamba umenipiga kidogo kanzu kwenye kusaini, sijaona kwangu lakini Meneja wangu yuko hapa tusije tukakabana baadae naamini kabla ya mwezi wa saba na mimi nitafanya sherehe kubwa ya kusaini mkataba wa lami kwa mara kwanza toka miaka 60 ya uhuru na tunapata hizo kilometa 20 na nikuombe Mheshimiwa Mbarawa tutakutana kwenye corridor pale, ongeza tano ziwe hata 25 at least sijaona humu, lakini mimi naamini Serikali inafanya kazi kubwa, imetutambua hata sisi watu wa kijijini, wananchi wangu wananiona hapa, nina kila sababu ya kukupongeza na kuipongeza Wizara yako kwa sababu kwa kweli pamoja na kuwa hatuna lami, kwetu kunapitika Mheshimiwa Waziri kunapitika, unatereza hata mimi mwenyewe naenda vizuri tu nalala kijijini kwangu wala sina shida, Mungu akubariki sana wewe pamoja na Wizara yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri wananchi wangu wananisikiliza. Tumehaidi mwaka jana na mzee wa sarakasi tulikuwa batch moja. Umeishasaini kule kwa mzee wa sarakasi, sasa mimi bahati nzuri sana ni bondia ambaye nilitarajiwa kupambana na January akanimbia, sitaki kupambana mimi na wewe maana mimi nakula ugali Mheshimiwa Waziri kisije kikakutokea kitu cha ajabu.

Naomba ukamilishe mchakato uje usaini mkataba kwa wananchi wangu nakuomba na mkataba huo utasainiwa Nkome watu wanasuburi kuona lami. Unajua kwetu ukiona lami Gwajima yuko hapa, ndiyo itakuwa sehemu ya kwenda kuogea hata mizimu Mheshimiwa Mchungaji hata mizimu unaogea maana tunaogea kwenye mawe sasa tukipata ka-lami utakuwa unaogea hata roundabout. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, wananchi wa jimbo langu wanatamani kuona lami na nikuombe nisikilize na njoo uweke mimi na wewe hatuna tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nilindie dakika zangu mimi ni mmoja wa Wabunge nilioenda Dubai kuona uwekezaji ulioko Dubai wala sijifichi nilienda kwenye ziara ya Kamati ya Mheshimiwa Mbarawa na mimi kidogo sijui unaweza ukanunua akili yangu bei gani, maana na mimi ni la saba mwaminifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tunachelewa kwenda kwenye maendeleo kwa sababu ya degree. Mimi na twende taratibu degree risk assessment, mchakato; haya mambo yatatuchelesha, upembuzi yakinifu jamani..., tulikuwa humu Bungeni Bunge lililopita. Mimi nilikuwa Mbunge wa kwanza kwenye Wabunge tulioenda kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere, risk assessment humu, sijui nini walichelewesha haya mambo na kuna wengine wanapinga humu ndani walikuwa Mawaziri kwenye hizo. Mazingira tutakata miti, kuna vyura.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi unajengaje reli ya kisasa ya matrilioni kwenda Congo, kwenda Mwanza halafu una bandari inayotoa mabehewa 120 kwa siku. Tunachelewa sana ni lazima ninyi wasomi sasa ikifika mahala tutagawana, unajua gita lina kitu cha kukoleza, Nape ni mtaalam, mimi nitaondoka na kale kakukolezea spika hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachelewa kwa sababu ya watu wachache wajinga ambao kila kitu unataka ushirikishwe, sawa. Tunataka tuletewe mkataba humu kila mtu atachangia dakika kumi lipi ambalo unaweza kupinga kwenye dakika kumi? Twende taratibu ni lipi? Niulize humu lipi? hivi tumefika mahala sasa na watalamu wotee ni wajinga? Mpaka CAG naye anayetugombanisha humu nae ni mjinga? Maana sisi tuna jicho lakini hatuamini, haya mtu anakuja anazungumza miaka kumi, miaka 20 ya TICTS ilitufikisha, ikatupeleka; sawa miaka 20 si tulikuwa darasani au wenzangu hamsomi? Tumefika mahala sasa tunang’amua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dubai DP World ukifika pale mimi nilienda na Wabunge wenzangu tukawa kama 30; kule bandarini mimi sikuona watu, niliona mashine tu zinapishana hivi “kakakaka” kadada kadogo hivi nikakaomba na namba ninayo hapa kakibonyeza hivi kontena linaenda. Tutoke huko tulikobaki hatuwezi kwenda kwenye hiyo mifumo...

MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: (Hapa hakutumia kipaza sauti).

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Nasikia sauti Mheshimiwa naongea na kiti.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma, endelea na mchango wako.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Naendelea.

Mheshimiwa Mwambe nakuheshimu sana, usiingie kwenye kumi na nane, mimi hunipigi swagga brother. Tulikupa nafasi na uli-fail, ndiyo maana uko-backbencher, tena nyuma yangu nipige taarifa uone.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusiwasikilize watu wa hovyo, hii nchi ni yetu wote, tunajenga meli Mwanza ya mabehewa kwenda Uganda, tunatengeneza reli kwenda Congo halafu unakuwa na watu kama Mwambe huyu, simama huyu. Wewe mchakato, tulikupa nafasi kutoka EPZ mimi mwenyewe umenifelisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili Taifa ni letu wote, mliosoma na sisi, niwaombe tena tumechelewa, tumechelewa kila mtu ana uwezo wake humu ndani, kuna mtu ana uwezo wa akili na mtu mwingine anauwezo kama wa kwangu mimi najivuna kwa sababu gani? Sina shule, lakini mimi ni msukuma, najisimamia mwenyewe, hatuwezi kutembeza imprest Bungeni humu. Tusitembezee mawazo ya watu wachache kuja kununua Bunge, pinga haya tusimamishe anayepinga hapa atueleze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania wanajua tunatoka sasa reli ya ngongongo au labda mwenzangu hajapanda treni, ngongongo tunaenda mshale, halafu una watu 900/1200 bandarini hayo si mawazo potofu kama ya kina Mwambe hawa. Nikuombe sana huyu ni Mbunge mwenzangu, usijichanganye kunipiga swagga, kwa sababu nimemsikia amesema wewe; na yeye ni mpingaji.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma endelea na mchango wako…

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, nikuombe hii nchi ni ya kwetu wote na nazungumza kwa sababu mimi ninafaida na reli ya mwendokasi, tusisubiri haya mawazo ya kujaribisha, twende mbele, hawa watu wanao tuletea mawazo ya kujaribisha kutegana tegana humu mimi nina miaka 61 leo ya uhai wangu tusije kuchambuliana ma–file humu ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe na niwashawishi Wabunge wenzangu kwamba kiukweli huwezi kuwa na train ya mwendokasi, unatoka kwenye makontena ya kusahihisha, basi inawezekana wenzangu hawajawahi kupita bandarini. Ukipita pale bandarini usumbufu uliopo unaweza ukalipa TPA, ukaambiwa leo sijui portal, sijui Harris hayupo, mnakaa hata wiki mnasubiria makontena na storage inasoma. Jamani hatuwezi, tunasomesha watoto wenye degree zao watu wa IT halafu tunang’an’gana kukaa analogue. Mimi mwenyewe natoka kwenye analogue sasa hivi ni doctor. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niangalieni vizuri natoka kwa sababu naendana na wakati ningepewa hii doctor ya heshima miaka kumi iliyopita nisingeelewa lakini leo tu–complete na mimi na mtu anayepinga hapa tukakae kwenye tv watu watusikilize tumwage material, hatuwezi kuwa na degree ambazo hazija..., kizungu mnasemaje?

MBUNGE FULANI: Hazija-qualify.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Hazi–qualify, yaani kwenye maisha halisi, nashukuru kukaa na yaani lazima tutoke huku, unaweza ukajaza Taifa la degree za watu wa hovyo na mkabaki kuwa wa hovyo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika moja.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Sekunde 30.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika moja. Ukienda Dubai nakupa mfano mzuri. Mimi nimebahatika kumuona Mfalme wa Dubai, huyu hapa nilikuwa na mtafsiri wangu. Ziara yangu kutoka jimboni na wananchi wangu wananisilkiliza. Nikamuuliza umeijengaje Dubai? akaniambia wakati naanza kutoka kwenye maisha ya Dubai kuwatengeneza watu waione Dubai tunayoiona leo, wakaniambia nilivyoanza kuwaruhusu watu wajenge kutoka mataifa mbalimbali wale wazee maarufu wa Dubai wakaandamana. Walivyoandamana akawaambia njooni tuzungumze Ikulu. Wakaenda kuzungumza akawaambia mna shida gani? Unauza Dubai kila mtu unampa hati; kuna Wanaigeria kuna Watanzania, kuna Wahindi kuna Wazungu; mwisho wa siku sisi tunaondoka Dubai, akasema, sasa mna tatizo na nilichokifanya? ndio. Tufanyeje? akawaambia sasa nyie mmekuja wangapi? 150. Nawagawanya mara mbili 75 mtakaa airport, 75 mtakaa bandarini. Ndio njia ya kutoka Dubai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiona mtu amekuja na nyumba anaipakia kwenye meli nakutumia na jeshi mnisaidie kunipigia simu tu. Leo Dubai ukienda pale sijui vizuri kizungu utaona majumba. Nyinyi mnang’ang’ana na vitu vya kijinga. Mtu akitaka kujenga unawaambia huyu ni mzungu, ukimpa ardhi tuta, ndiyo tutabaki na tunalima mazabibu. Haiwezekani. Tuachane na wapingaji tutengeneze Tanzania ya kisasa, tupambane na bandari zinazotuzunguka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Samia kwa ubunifuu alioufanya kwenye Filamu yake ya Royal Tour. Na huo ni mfano mzuri, kwamba unapoandaa kitu kizuri lazima usemwe, lakini ukisemwa usikate tamaa ili mafanikio yaje yatokee badaye.

Mheshimiwa Spika, la pili, nikushukuru sana Mheshimiwa Mchengerwa, na ninakupongeza sana. Nimpongeze pia Rais kuwahamisha kama pair wewe pamoja na Dkt. Abbasi. Mimi kama mdau wa michezo nakumbuka kazi kubwa nzuri mliyoifanya kwenye Wizara ya Michezo. Mpaka leo tunaona Yanga inacheza fainali; hiyo ni kazi yako nzuri sana. naamini system uliyoondoka nayo kule tunakukumbuka mpaka leo. Sasa tunaomba na huku kwenye utalii uache alama ileile, na ninakuamini utafanya vizuri.

Mheshimiwa Spika, nitazungumza mambo machache. Mheshimiwa Waziri, kwanza katika kipindi ambacho Watanzania tunaoishi pembeni mwa hifadhi tulikuwa na bahati na raha ilikuwa ni kipindi cha mama huyu mwenye huruma, mama Samia. Alipounda timu ya Mawaziri Nane hakuwawekea mipaka, aliwaambia nendeni mkalete changamoto halafu mnishauri.

Mheshimiwa Spika, lakini mlichokwenda kukifanya kule kiukweli si sahihi. Na mimi nataka kujiuliza, hivi kweli ninyi mnaamini kwamba mtu mpaka anakwenda kukaa yale mazingira, ujue kumemshinda huku, hakununuliki. amekwenda kukaa pale kwa sababu ya shida zake. Mtu anayevumilia kukaa jirani na simba na tembo maana yake hana namna nyingine ya kufanya, na mwingine amekaa zaidi ya miaka 30. Ukienda leo na plan ya kumwondoa hii ni kutengeneza migogoro isiyoisha na Serikali. Na wewe Mheshimiwa Mchengerwa umekuta sisi Tanzania tuna timu za mwendawazimu lakini umetutengeneza mpaka tumekwenda fainali, achana na hayo mambo ya ku-create migogoro ya ujirani mwema.

Mheshimiwa Spika, siku moja nilimwona Mheshimiwa Waitara analia hapa na nikaona watu wanasema Mkurya ametudhalilisha; na mimi nina asili hiyo. Kwanza, ni kwa sababu humu labda viti vimefungwa na hizi mic, hasira ikikupanda Kikurya unachukua kitu chochote unasukuma mbele ili hasira yako ipumue. Kwa hiyo alipolia alilia kabisa akiwa anapumua ili hasira zake ziishe.

Mheshimiwa Spika, ninaomba Mheshimiwa Waziri, hebu utafute namna. Labda tulikosea, unajua tukikosea si vibaya kujikosoa. Hili Jeshi la Wanyamapori tangu tumelitengeneza hebu jaribu kuangalia kabla ya Jeshi Usu na sasa, migogoro iko wapi? Kwa sababu siamini huo utaalamu mnaoutumia kutengeneza hilo jeshi kweli mnawatuma kwenda kupiga watu? Mimi sielewi; mbona majeshi mengine hayako hivyo, yana taratibu zake? Yaani hawa imekuwa ni tatizo. Mnatengeneza Jeshi la kwenda kuwabaka dada zetu, kweli? Hii haiwezekani. Nikuombe Mheshimiwa Waziri utakapokuja hapa usiponiambia mpango mkakati kama hili jeshi lilitengenezwa kimakosa utakuwa Waziri mzuri sana ukilifumua na kutengeneza jeshi jipya na la kisasa. Haiwezekani tukawa na watu wanapiga watu tu, kila siku kupiga watu; haiwezekani.

Mheshimiwa Spika, mimi nakaa kwenye maeneo hayo yanayopakana na mapori ya hifadhi; ni tatizo. Ukitaka kujua njoo ukae, usije na magari, ukae siku moja tukuweke kwenye familia kama wiki halafu ufanye kosa kidogo uone utakavyopata mpite mpite. Kwa hiyo tukilalamika humu mtusikilize; nadhnai kuna makosa tumefanya kwenye uundaji wa Jeshi Usu. Lazima uje na mpango wa kulirekebisha, wale wabovu ondoa, baki na watu walio na nia ya kulinda maliasili, siyo kutengeneza migogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka kujiuliza; Maliasili mnatukamatia ng’ombe, sawa, tuna makosa, mnawapiga mnada, rundo la ng’ombe mnauza kwa bei mnazotaka wenyewe. Na nimejifunza, kwa sababu niliwahi kuongea – kuna Mawaziri sijui kama wako humu au wametoka – kwamba minada inakuwa kama dili, lakini mkifukuzwa tunaanza kusikia mnafuga ng’ombe. Kwa hiyo mnawafuata kiujanja ujanja, mnanunua ndani kwa ndani mnawafuga. Hizo ni laana! Na mtakufa vibaya, lazima niwaambie.

Mheshimiwa Spika, hebu jifikirie umenikamatia ng’ombe wangu 100, yaani naona wanakwenda sina uwezo wa kwenda polisi kwa sababu kuna bunduki. Haya, nina kosa, unawachukua ng’ombe wangu unawauza, mimi narudi maskini. Halafu baada ya miezi sita unaanza kunihudumia na hela ya TASAF. Hiyo ni akili ya design gani jamani? Kwani ni chanzo cha mapato?

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, na makosa mengine tengenezeni utaratibu wa kutuonya. Unamkuta mtu ameingia mita 100, mita 200 ng’ombe wanachungwa au wanakunywa maji, unazoa ng’ombe wangu wote nirudi tu nyumbani nainze kusema maliasili; mtakufa vibaya. Lazima niwaloge; hiyo lazima tuambizane ukweli.

Mheshimiwa Spika, maana nikienda polisi utanishinda, mahakamani sina hela ya kwenda, mtalogwa mtakufa vibaya, lazima Mheshimiwa Waziri. Hebu rudisha moyo, tengeneza ujirani mwema ule wa maana. Kama huna maafisa mahusiano kwenye Jeshi Usu lako tafuta maafisa mahusiano watengeneze mahusiano. Mtatuchonganisha bure na Mawaziri, mara mkienda kule mnashika hasira mnasema na matusi, lazima. Kwa sababu sisi tunalia.

Mheshimiwa Spika, mimi ukinichukulia ng’ombe wangu ambao nategemea mtoto wangu wangu yuko chuo kikuu, mwingine anasoma sekondari. Haya, wamekwenda, ukienda kule kuna bunduki; nakaa tu kimya kweli? Na hii Serikali kweli tumekosa chanzo cha mapato mpaka chanzo cha mapato kiwe kuuza ng’ombe?

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mchengerwa, hiki kitu jamani kwa kweli hakiwezekani. Fikirieni namna, makosa mengine muonye, mbona ninyi mnakosea na tembo akija huku hatuwashitaki, tunawaambia tu mambo yanaisha? Ninyi kosa lenu ni kuchukua tu na kupiga faini. Mheshimiwa Mchengerwa, mimi sitaki kuamini kama na wewe utaendelea kuwa Waziri wa mafaini; haiwezekani. Nikuombe uwe Waziri utakayetengeneza hifadhi tuzione kama mali zetu, siyo za Wizara.

Mheshimiwa Spika, sisi wote ni Watanzania, na mimi nilipongeze sana aliposimama ndugu yetu hapa wa Kiteto, tulimwambia, na ndugu yangu wa Monduli. Tulikuwa tunamshauri mpaka canteen, huyu hapa, kwamba kwa staili Serikali ilivyoamua kuwahamisha, yaani kutoa mpaka na gari ng’ombe wa Kimasai mara ya ya kwanza amepanda fuso, halafu unapiga kelele, nyumba, maji, shule. Tumemshauri sana Mheshimiwa humu, na akina Mheshimiwa Ole-Sendeka mpaka yakaisha.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi nataka kuuliza; kule Nyatwali ni Tanzania, wale ni wananchi. Halafu mimi nataka kujiuliza Mheshimiwa Waziri ukipanda hapo uniambie ni hifadhi gani ambayo labda umekwenda kuangalia huko duniani, maana sisi tunatembea, nikishindwa kutembea na-google; kwamba unatoka mbugani unakatiza lami unakwenda moja kwa moja ziwani, pembeni kuna kijiji kinaitwa Lamadi, huku kuna Bunda. Kule ziwani sisi tunatega samaki, kule ziwani tunanywesha ng’ombe wetu, halafu na simba tukutane nao kulekule. Mna mpango gani ndugu zangu? Yaani mmefikiria kitu gani, au mtaweka fensi kuzia sasa simba wasiende?

Mheshimiwa Spika, mimi najuiliza mara mbilimbili, hizi ni research za design gani? Ndiyo maana wakati mwingine mimi najiuliza, siyo kwamba napingana sana na degrees za darasani, yaani matendo yenu huwa yananichanganya mpaka nafika mahli najiuliza mara mbili.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana jana nilikuwa nasikiliza kwenye nishati, watu wanasema tumnyang’anye TBS turudishe tena aliyekuwepo, wakati Bunge hilihili tulijadili, na ninyi ni wasomi, tukapitisha, TBS hatujampa uwezo, anategemea kukopakopa kama Musukuma hapa.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi najiuliza hiyo research kweli mnadhani itatufikisha? Kwani kimepungua nini; mmeambiwa kwamba wanyama wamebanana Serengeti mpaka mfukuze kile kijiji wale wanyama wawe wanakwenda? Je, kule kwenye ziwa ukikutana na wavuvi nani anawalinda? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kule kwenye ziwa tukikutana sisi tunaonywesha ng’ombe wetu maji nani anawalinda? Wale wanyama miaka yote toka mbuga imeanza wanajua huku wanaishi binadamu, sasa mkiwaambia wapite mpaka kule huku pembeni Lamadi na huku Bunda, nani anaweka ulinzi? Mnataka kutuletea matatizo, na ninajua hamtafaulu.

Mheshimiwa Spika, hivi kweli mnataka ku-achieve kitu gani kufukuza wale wananchi halafu unamlipa mtu milioni mbili? Halafu walewale wanawaangalia Wamasai wamebebewa ng’ombe kwenye fuso; hapana bwana, hii keki ni yetu sote Mheshimiwa Mchengerwa. Maeneo mnayo mengi, kama mmepungukiwa, kama wanyama wamejaa beba leta hata Geita kule tuna mbuga haina wanyama. Haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho; mimi nina Hifadhi inaitwa Rubondo, ni kisiwa. Ile kata inahesabika kata ya Musukuma, kata ya Geita Vijijini, lakini langu kuu limewekwa Chato, sina tatizo. Sasa, historia ya ile hifadhi ni kwamba ina matambiko yetu ya Kizinza, mlango mkuu ulikuwa Nkome, na upo, na ofisi zipo, lakini yaliyopita si ndwele, turudishe lile geti la Nkome. Kama kule meli sisi bado tunahitaji tu kuwa na boti kwa sababu hata ukiingilia kule Mganza inabidi uje mpaka hifadhi, halafu halafu vile vivutio vyote viko karibu kabisa na jimbo langu. Kwa hiyo nikuombe, ile ni kata yangu. Mimi sitaki kufunga geti la Chato, lakini ninachotaka tuwe na geti la pili, ule utalii wa magari uanzie kwenye jimbo langu ili na sisi tuone Wazungu, siyo tuwe tuna-google tu ndiyo tunaona Wazungu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nina imani kwamba Mheshimiwa Mchengerwa utakapokuja hapa kikubwa kwangu, Nyatwali iwe sawa na…

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa, Ahsante sana.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: … Loliondo; pili, utaratibu wa kulitengeneza Jeshi Usu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. JOSEPH MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nitazungumzia kidogo suala la uvuvi. Wabunge wengi tuliomo humu kila mmoja ana neema ambayo Mwenyezi Mungu amempa na kila mtu ana kitu ambacho wananchi wake wanakitegemea. Jimbo la Geita Vijijini sisi dhahabu yetu kubwa ni uvuvi lakini toka nimezaliwa sijawahi kuona hizi sheria zinazotumiwa na Mheshimiwa Mpina. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umri wangu huu nimeshuhudia Mawaziri awamu zote, nafikiria sasa ndiyo tunaanza kutunga sheria au hii sheria ilikuwa imefichwa sasa ndiyo imeibuka. Nataka kutoa rai kwa Mawaziri kwamba Mawaziri wa dizaini kama hizi nawashauri sana mpunguze mihemuko kwa sababu hata sisi tunatamani kuendelea kuwa Wabunge humu ndani, lakini kwa dizaini mnazoenda mtuambie mmewapanga kina nani mnaotaka wakae Wabunge kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumza kwa Wabunge wanaotoka Kanda ya Ziwa; Mheshimiwa Lwakatale, Mheshimiwa Mwijage, Mheshimiwa Tibaijuka, Mheshimiwa Kalemani, Mheshimiwa Lolesia, Mheshimiwa Musukuma, Mheshimiwa Kanyasu, Mheshimiwa Mabula wa Mjini, Mheshimiwa Mabula wa Ilemela, wa Magu, tunaenda kwa Mheshimiwa Bulaya, unaenda kwa Mheshimiwa Airo Musoma, sidhani kama sisi tutarudi humu Bungeni. Sijawahi kuona Waziri anasimama anasema mimi kwetu hakuna samaki natamani wote tusile samaki, Mungu ametupa neema tofauti. Sijawahi kuona unaenda unakamata mitego dakika 10 unaomba faini mtu hana unachoma, hujahakikisha ni ile feki unayoitafuta au original. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukienda Jimboni kwetu na huko kwenye Majimbo ya Kanda ya Ziwa debe la dagaa linauzwa Sh.50,000 yaani maana yake hata dagaa haturuhusiwi kula. Ukisikiliza madaktari wanatuambia tukila dagaa tunaongeza madini joto, akija Mpina anasema ni haramu, tufuate la nani? Namwomba Waziri Mpina atakapokuja hapa atuambie ni sheria zipi anazozitumia kama siyo mihemuko. Kwa sababu hata Mheshimiwa Rais aliyepo sasa hivi Magufuli alikuwa Waziri aliunda BMU watu wakawa wanafundishwa na uvuvi haramu ukaisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukienda kwenye maeneo yetu hakuna samaki inayotakiwa kuliwa. Nina mfano halali, mimi nafanya biashara ya mabasi, basi yangu imesimamishwa na watu wa Maliasili wakaingia ndani kukagua wakakuta mtu ana samaki za kukaanga tatu naombwa kutoa Sh.10,000,000 na nimempigia simu Mpina anasema watu wangu wanasema sijui wamefanya nini, nikawaambia chukueni gari mkauze. Hivi inawezekana vipi watu wa mabasi anakaa ruler yake kupima samaki kwamba hii samaki inatafutwa na Mpina, kwa nini usiweke polisi stendi? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mpina pamoja na apizo alilolifanya kwamba asipomaliza uvuvi haramu atajiuzuru, mimi nakwambia…

T A A R I F A . . .

MHE. JOSEPH MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru. Anataka kukaa kwenye Youtube kwamba alimpa taarifa Musukuma. Tunajua Jimboni kwako unazomewa, kwa hiyo, unatafuta kick unatetea wanyonge. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, ninachoomba Waziri Mpina pamoja na timu yake wajipange kuwafundisha wavuvi wetu kule siyo kuwafilisi. Nataka nitoe ushahidi mdogo tu kwamba Waziri Mpina wameenda kisiwa kimoja kule Izuma Cheli Jimboni kwangu wakakuta watu wameunda SACCOs wamekopa wanadaiwa shilingi bilioni 1.4, mitego ndiyo wameishusha usiku huohuo asubuhi imekamatwa hata kuombwa risiti wamenunua wapi ili wakapambane nao na siyo haramu imechomwa moto kwa kukosa rushwa ya shilingi milioni 30. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sana Waziri na wengine wanaosikiliza kwamba nashauri sana zoezi analoliendesha Waziri Mpina lazima liundiwe Tume iende ikachunguze na tuone hizo hela watu wetu walizotoa kama zimetolewa risiti za Serikali. Tuna ushahidi wa watu waliofanyiwa uhuni kwenye Majimbo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mengine yanauma sana, unajua wengine humu ndani hawana hiyo bahati ya kuwa na ziwa, naamini hata Jimbo la Mheshimiwa Waziri wao wanakulaga panki zikikatwa kule kwetu wao wanapelekewa mapanki. Sasa asitake kutufananisha yaani sisi tufe njaa na ziwa liko pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, waje na shule maalum itakayotufundisha, hata sisi hatupendi uvuvi haramu lakini siyo kuzuia kila kitu. Kwa sababu kwanza kule ziwani hata ukizuia tusivue sisi Watanzania hakuna barrier samaki wataenda Kisumu, samaki wataenda Uganda na ndiyo kinachofanyika. Rais Magufuli anasema tufanye kazi, tukuze uchumi wetu, mwingine anaenda kusema choma kila kitu, wavuvi wote wa Kanda ya Ziwa wamehamia Uganda na Kenya sasa nani anapata faida? Nyie ziwa lenu mmekuwa mnatunisha samaki wakikua wanatembea wanaenda Kisumu tunavua tunauza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshauri sana Mheshimiwa Mpina utakapokuja kujibu hapa na hata ukichomoa hapa kwenye bajeti tutakutana lazima utueleze ili hii operesheni ya uonevu inayoendelea ikome.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. Naipongeza Wizara kwa kazi nzuri inazofanya pamoja na mambo madogo madogo yanayoendelea kutokea lakini hizo ndizo changamoto lazima ukabiliane nazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia kuhusiana na suala la umeme, jana kuna mchangiaji nilimsikia anazungumza kuhusu sub-station ya Geita. Ni kweli tulimuona hata Mtendaji Mkuu wa TANESCO Ndugu Maharage kwenye vyombo vya habari anatangaza kufunga mkataba na GGM ambayo tunategemea kupata karibu Bilioni Tano kwa mwezi na utekelezaji wake ulitakiwa uwe umekamilika mwezi wa 12.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshauri Waziri kuwanyang’anya biashara ya mafuta ya exemption GGM siyo kazi ndogo, ubovu mwingine Serikali ukishajitangaza kwenye tv hamna ufuatiliaji, nilijaribu kufuatilia kule GGM hakuna kitu kinaendelea ndiyo kwanza wako kwenye manunuzi na wakati ujenzi wa sub-station ulitakiwa uwe umekamilika mwezi wa 12, kama leo ni mwezi wa Sita ndiyo kwanza wanaanza manunuzi, maana yake kuna miaka miwili ijayo.

Mheshmiwa Mwenyekiti, tunajua sisi tunaoishi pale kwamba wanatumia zaidi mafuta karibia zaidi ya lita Milioni Tatu kwa mwezi, siyo kazi ndogo na kuna deal za watu pale, siyo kazi ndogo ni lazima TANESCO muwe na mkakati mzuri maana ya kujenga ile sub-station ya Geita ilikuwa ni pamoja kulilenga lile soko la mgodi mkubwa wa GGM sasa naona kama tuna mizaha mizaha ambayo ninaimani wenzetu ndiyo wanatumia kama nafasi. Kwa hiyo, ni vizuri Mheshimiwa Waziri fanya ufuatiliaji uone wamefikia wapi usikae kuletewa tu taarifa za makaratasi, naamini hazitakusaidia na sisi wengine tulioko kule tunaona hali siyo nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili mimi kwenye Jimbo langu nimepata Ofisi ya TANESCO ambayo Meneja wetu pale anaenda mpaka kilometa 100 mpaka kilometa 90 kwenda kutoa huduma, tulikuwa hatuna gari anatumia pikipiki tena bodaboda, hapa amebeba viatu vya kukwea kwenye nguzo amebeba na vifaa vya kwenda kutengenezea. Nilipozungumza humu mmetuletea gari ambayo kiukweli ni kama dharau bora angebaki tu kwenye bodaboda. Gari inasukumwa kilomita moja ndiyo inawaka! Sasa nikuombe Mheshimiwa Waziri mimi ni Mjumbe wako wa Kamati najua mipango uliyonayo, toka akiwa Waziri Kalemani mnasema mna magari 100 yamefikia wapi? Au yamekuja yameenda wapi? Huko Mjini watu wana vitendea kazi sehemu ambazo mmepeleka huduma vijijini pelekeni magari ili watu waweze kufurahia huduma ya Tanesco vizuri pale wanapokuwa wamepata matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la tatu nazungumza kwenye suala la mafuta. Nilizungumza hapa tunaishukuru Serikali imechukua hatua kupunguza kuweka bei, kuweka ile Bilioni 100 imepunguza lakini imepunguza wapi? Mimi naiona tu kwenye karatasi mpaka leo, yaani imepunguza kwa mletaji imepunguza kwa watu wa Dar es Salaam mimi ninayetoka Nzela Vijijini na Wabunge wenzangu mafuta ya vituo vyetu almaarufu madumu bado bei ni ile ile na imeongezeka sehemu zingine. Sasa Mheshimiwa Waziri mtusaidie maana tukitoa ushauri saa nyingine huwa hamtusikii tunawaeleza kila siku legezeni masharti ya vituo vya vijijini ili watu wakafungue vituo. Unawekage sharti kituo cha kijijini kinachouza lita 200 unaweka masharti sawa na kituo cha Kariakoo kinauza lita 15,000? Kwa hiyo, utakapokuwa umelegeza masharti nikuhakikishie kwamba madumu kule yatapungua na bei zitakuwa zinafuata utaratibu kwa sababu watu watakuwa na reserve ya kutosha. Kwa hiyo nikushauri narudia kushauri na kwenye Kamati nimezungumza ni vizuri tukabadilika mwaka wa pili hii tunazungumza karibia wa tatu tulegeze masharti ya kituo cha mafuta cha kijijini kisifanane na vituo vya mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Nne Mheshimiwa Waziri ni kuhusiana na suala la biashara kwenye hili naungana na Prof. Muhongo. Unajua biashara inataka vitu vingi sana, siyo tu degree kuipeleka TPDC kwenda kufanya biashara ya mafuta nakuambia ukweli mimi naungana na Mheshimiwa Profesa Muhongo hatutafika popote ni suala la muda tu. Tulikuwa na kampuni inaitwa COPEC iliingia kwenye hizi biashara ilienda wapi? Ilikufa sasa hivi tumeibuka tena na TAN OIL tunasema ni shirika, kampuni tanzu lakini bosi ni huyo huyo Mataragio na hii nawapa labda mwaka mmoja tu na yenyewe mnapotea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara ya mafuta ina akili nyingi, kwa mfano watu kama MOIL na wengine wenye vituo vya mafuta wanawakopesha wateja wakauze kwenye madumu walete haya huko kwenye TANOIL unamkopeshaje mteja? inaweza ikaharibika tu pump ya kutengeneza kwa 15,000, 20,000 unaanza procurement siku tatu mpaka mafuta yanakupandia bei. kwa hiyo niombe sana mimi nakubaliana na Muhongo TPDC ibaki kwenye kazi yake ya taaluma ya kutafuta mafuta na kutafuta gesi kwenye biashara tuwaachie private sector mimi nakuhakikishia Mheshimiwa Waziri hii pesa kwa mfano ungempa private sector akafanya na huu mtaji baada ya miezi zita tungekuwa na faida kubwa sana lakini leo pamoja na kwamba ni Kampuni ya Serikali nakuhakikishia Mheshimiwa Waziri huko tuendako bado tuko Bungeni kuna mzinga ambao najua tu utakuja wala siyo muda mrefu tutakuja kuujadili tena humu. Tuziache private sector zifanye kazi za biashara sisi tufanye kazi ya taaluma kuwaonyesha watu wafanye kama walivyosomea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kuhusu mafuta ninataka kumuuliza Waziri na wataalam wake mimi ni mfanyabiashara kama sifanyi biashara ya mafuta lakini nina biashara zingine zina-attach na mafuta. Katika hii biashara ya kushusha bei jana Tarehe Mosi nataka mnipe majibu kwenye ku-wind up aliyepata faida ni mwagizaji au muuzaji? Kwa sababu kuna watu wana vituo huko vijijini wamefumaniwa na lita 20,000 jana na wao wameshazinunua cash na hizi pesa tunakopa benki kwa asilimia 22, amekutwa na labda lita 100,000, 200,000 bei imeshuka hakuna utaratibu wa ku-return hela zao, sasa hiyo hasara inabebwa na nani? Kwa sababu mlikuwa mnafanya tathmini ya kushusha mafuta Tarehe Mosi mlifanya utafiti kwa Watanzania ambao wana vituo huko mijini na vijijini kwamba tutakaposhusha watakula hasara gani, kama ni hapana lazima tukae chini tuangalie tumewatia umaskini watu wetu hawa wanaouza vituo vya vijijini na Mikoani kwa sababu pengine hatukufanya utafiti mzuri na haya ndiyo mambo ambayo bado ninasema Mheshimiwa Waziri tuiache TPDC ifanye kazi ya taaluma, hii kazi ya biashara tuwaachie private sector hii zimamoto Mheshimiwa Waziri wewe bado ni wa kwetu tutakuja kukaa tena na wewe bajeti ijayo bahati nzuri watu wengine computer inawezekana hawatunzi vizuri vile vipaumbele vyako ulivyovigawa jana usubiri mwakani vinakuja kukusulubu tena humu ndani. Nakueleza ukweli kwa sababu watu wametunza zile wanakusubiria mwakani, tunajua ni bajeti yako ya kwanza hii ya mkakati wako lakini mwakani tunakung’ang’ania tuko na wewe tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine Mheshimiwa Waziri Mkoa wa Geita tumepata bahati mbaya sana, tumepata Mkandarasi ambaye wenzetu tayari miradi inaendelea akaonekana hana uwezo, tumepata mwingine nikuombe Mheshimiwa Waziri hakuna siasa nzuri Tanzania kwa wanasiasa kama umeme tukuombe hawa Wakandarasi uwasimamie vizuri na Mheshimiwa Waziri imetosha muda wa kukaa ofisini wa mipango, umemaliza karibia miezi sita zunguka! Watanzania tunataka kukuona huko kwenye nguzo huko tunakueleza nguzo zinaanguka unaona, tukizungumza nguzo zinatengenezwa ni fupi unaona zunguka usiletewe makaratasi, mimi nakukaribisha sana kwenye Mkoa wangu wa Geita lakini na Jimbo langu uje uone na hayo matatizo ninayo kuambia, tunayo ofisi lakini bado watu wakitaka kwenda kulipa labda bili au nini wanatakiwa watembee kilometa 57 na ofisi ya TANESCO iko pale, tunashindwa nini gharama ya kufunga mfumo na kufanya zile correction na kuwahudumia watu tatizo liko wapi Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana Mheshimiwa Waziri haya matatizo yako kila mahala kwa Wabunge ambako vimepelekwa vituo vidogo bado mtu anaona bango la ofisi ya TANESCO lakini unaambiwa tembea kilometa 100 kwenda kulipia bili au kutatuliwa tatizo la kimsingi. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri uwe makini na uzunguke kwa ajili ya kuona matatizo ambayo tuko nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine Mheshimiwa Waziri la bwawa la umeme, nazungumza tena ninakuomba Mheshimiwa Waziri.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma muda wako umekwisha.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru na ninaunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitoe pongezi kubwa sana kwa Serikali kwa Mheshimiwa Rais kwa kusikiliza maoni ya Wabunge na kutoa maamuzi magumu kwenye KADCO ambayo imetesa miaka yote ya Ubunge wangu miaka Nane tunajadili KADCO, hongera sana Serikali na tunajipongeza kama Wabunge.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kumteua Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo kuwa Waziri wa Mipango, mimi nakuamini sana Mheshimiwa Kitila Mkumbo kwa research wewe ni bingwa kabisa. Mheshimiwa Rais amefanya vizuri amewakabidhi fedha na akawakabidhi na mipango, ninyi wote mnatoka Iramba, ndoho mayo mkiharibu tutauana, nina imani mtafanya vizuri na wapiga kura wenu tunawategemea na kule kwa shemeji zangu wanajua sasa mambo yanaenda vizuri kwa sababu mmekabidhiwa wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Kitila Mkumbo kwa mpango mzuri lakini lazima tukushauri, kupanga siyo makaratasi, mara nyingi tumekuwa na mipango lakini mipango inakuwa haitekelezeki. Najaribu kuona vitu ambavyo baadae tutakuja kukusulubu humu kukuuliza, nakupa tu mfano mdogo. Kwa mfano, unasema tunajenga vituo vya gesi kwa ajili ya ku-refuel magari, lakini najiuliza wenzangu labda mnaweza mkanisaidia tunayo magari haya yanayotumia gesi Tanzania, kwenye takwimu tuna magari sijui 3000 na kitu, ni sawa. Lakini kweli mnaona jinsi ambavyo yale magari yanavyobadilishwa kutoka mfumo wa mafuta kwenda kwenye mfumo wa gesi, yaani inakushawishi nini mpaka ukaanze kujenga vituo kwa design ile ya magari yaliyoko Tanzania?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mungu ametupa bahati ya kuwa na maliasili, maliasili kama tumegundua tuna gesi ambayo inaweza kutumika kwenye magari, kwa nini Waziri wa Mipango, usingeleta mpango hapa tukachukua wataalam tukawapeleka kusoma huko Japan, halafu wakaja na teknolojia ndiyo tukaanza kuliko kukurupuka. Nakupa mfano, ukipanda kwenye gari ambalo limebadilishwa mfumo wa mafuta kwenda kwenye gesi limewekewa drum huko kwenye buti na Wajapani walivyotengeneza gari lile buti ni kwa ajili ya kuweka mabegi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi najiuliza nyinyi wenzetu Mawaziri kidogo hadhi yenu ni kubwa mnavyoanza hii teknolojia ya gesi, mimi nilikuwa nashauri muanze na gari za Serikali za Mawaziri tuwawekee yale ma-drum ya gesi kule nyuma, halafu usafiri na hilo gari hupati hata usingizi! Naona kabisa tunaenda kupoteza hela kwenye vitu ambavyo haviwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu nchi zilizoendelea wanaotumia gesi wanatoa oda ya magari yao kwamba yanakuja special kwa ajili ya gesi, lakini angalia hata hayo malori ya Dangote mkikutana nayo watu wanachomelea ma-drum yanawekwa nyuma ya cabin, yaani kwanza gari lenyewe linakuja limeshapoteza na uzito ile capacity yake, kwa hiyo, mimi naona kabisa tunaenda kufeli tutaanza lakini hawa watumiaji wenyewe kwa sababu sisi wengine tunajifunza kutoka kwa Serikali, kwamba Serikali inapoona gari fulani ni zuri, kwa mafano V8, tukiona mmekuwa nazo nyingi Serikalini na sisi tunakimbilia kwa sababu Serikali imeshaona ni gari zuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeshauri gari la Waziri wa Fedha, kwa sababu wewe ni Mchumi na Waziri wa Mipango, kwa sababu wewe unatupangia tukufungie gesi kwenye buti lile drum liwe mfano kwa sababu wewe utabana matumizi, kuliko kwenda kuweka rehani maisha ya Watanzania kwa kuweka teknolojia za kijiweni halafu Serikali inaingia gharama kwenda kupitisha bajeti ya kujenga vituo, naona kama hatuendi sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemsikiliza hapa Mbunge wa Ngorongoro, amezungumza suala la ng’ombe, ndugu zangu mimi huwa nazungumza kila siku ng’ombe huwa hawaongei lakini wana machozi, sisi tuliokuzwa na ng’ombe tunafahamu, Waziri rafiki yangu sana Mheshimiwa Kairuki, hili suala ukisimama hivi unavyosimama, mimi niliwahi kulia humu nikamlilia Mheshimiwa Magembe aliekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, hakumaliza siku tatu akala kichwa, akaja na mwingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba busara kwenye suala la watu maskini, hivi tunahitaji shule gani kuona kwamba watu wetu wanaonewa? Nimemsikiliza kaka yangu AG, anasema ukomo, Mahakama ina ukomo, Mahakama ya Mkoa, hivi mtu wa Darasa la Saba anayefuga ng’ombe unamuambia hicho kiingereza alichozungumza hapo cha ukomo wa Mahakama, nani anaelewa hayo mambo? Huku akienda anaambiwa tunafanya uchunguzi, kumbe ninyi mnashughulika na kuuza ng’ombe! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu jiulize yaani hukumu imetoka Tarehe 31, halafu mnauza ng’ombe Tarehe 01. Maana yake dalali alikuwepo siku hiyohiyo wala ile hukumu haikuwa na alternative lipa faini, yaani ni vitu ambavyo, kwa kweli unafika mahali unajiuliza pengine hii nchi ni ya matajiri tu maskini hatutakiwi kuwa Tanzania! Haiwezekani...

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Waitara achana na taarifa kwanza …

TAARIFA

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma, kuna taarifa kwa Mheshimiwa Waitara, kwa ufupi kabisa.

TAARIFA

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mchango mzuri wa Mheshimiwa Musukuma, namuongezea kwamba TANAPA hao ndiyo walikamata ng’ombe, TANAPA walipeleka Mahakamani, TANAPA ndiyo walipewa hukumu kwamba wameshinda, TANAPA wamepiga ng’ombe mnada na ng’ombe mmoja amenunuliwa chini ya shilingi laki moja kila ng’ombe mmoja. (Makofi)

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, hakuna taarifa juu ya taarifa. Mheshimiwa Musukuma taarifa ya Mheshimiwa Waitara, unaipokea.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea na ninaomba Waheshimiwa Wabunge, kwa sababu ndiyo kasi inaingia namba tatu hebu pumzikeni kwanza, wekeni pause hizo taarifa kuna wanaokuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninahitaji kuwa na elimu ya namna gani kugundua kwamba hii ni dili kuanzia huko TANAPA, na watu wetu wanakuwa maskini. Halafu unapanga mpango huo mpango ukawafaidishe wakina nani? Mnataka watu wote sasa muwalishe na TASAF, hii kitu hakiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri achana na mambo ya kusema nisome sheria, tunajua wewe ni Mwanasheria mzuri lakini ukisimamisha Wabunge humu ndani wanaokaa jirani na mapori siyo mtu wa kwanza leo, wakikosa hela wanaenda kuswaga ng’ombe wanaziingiza kwa bunduki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jiulize hukumu imetoka tarehe 31 haina hata notice kwamba mlipe faini au ziuzwe, zimeuzwa kesho siku hiyo hiyo zimepakiwa zimeenda Dar es Salaam, unahitaji kuwa na degree kujua hiyo mipango? haiwezekani! Ni lazima Mheshimiwa Waziri, toka kwenye boksi hapo ukienda hivi, wafugaji sisi huwa tuna kitu chetu tukitoa machozi Mungu atatusikia huko aliko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshauri Kaka yangu Waziri wa Mipango, niambie unahitaji kuwa na shule gani kwamba watu tunafeli, angalia Dar es Salaam, mna mwendo kasi, kuna DART na kuna UDART. DART anamiliki lami, ile barabara ambayo haifi miaka 100, halafu anamiliki mifumo ambayo inaweza kusimamiwa na TAMISEMI na mtu mmoja tu, unaweka Mkurugenzi, unaweka Chief, unaweka ma-V8 na makorokoro mengi kwenye kitu ambacho hakizalishi. Mwisho wa siku kila mtu anasubiri mshahara tu! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mifumo mmeua kwa ajili ya kupiga, magari yenyewe yameisha, sasa kama kuna mtu mmemkodisha barabara kwa nini huyu msimamizi DART, fukuza wote pale, weka hapo mtu mmoja tu, kwa nini tunasimamia POS nchi nzima unashindwaje kusimamia Mfumo wa U-DART? Hicho ni kitu ambacho mnatengeneza mipango mizuri halafu mashirika yetu hayaendelei. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushauri pamoja na Waziri wa Mipango, fukuza wote pale, unaenda unachukua wazee wastaafu umedumbukiza ma-V8 mpya kwenye kitu ambacho hakizalishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumza suala la bangi. Leo nazungumza mara yangu ya tatu, mnaona kama naongea vitu vya ajabu, nami sishabikii bangi ya kuvuta. Huwa nawaangalia Polisi wanafyeka kule na ma-TV, lakini hiki ni chanzo. Angalieni Canada, Colombia, Pakistan, dunia nzima inapiga kelele na madawa ya kulevya wao ndiyo chanzo cha mapato. Sasa tunafyeka kwa ajili gani, tungedhibiti watumiaji, nchi jirani wanatumia, sasa kwa nini tunazuia, unaenda unafyeka unaonyesha na kwenye TV, unafaidika kitu gani wakati hilohilo zao ndilo linaweza kukuingizia kipato kutoka nchi ya Jirani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumza kidogo suala la CAG. Uliona mchakato wa CAG ulivyokuwa, nashauri ili tuende vizuri tunapofika kipindi cha kuhoji wale Wakuu wa Taasisi, kwa sababu huu ni Muhimili unajitegemea siyo wa kihuni, tuna Serikali, tunayo Mahakama na tunalo Bunge. Ninashauri ukiondoa wale Viongozi Wakuu wa Serikali wanne wa juu, hawa wengine bila kuangalia nyota au ngao za mabegani, hakuna kuja humu na ma-bodyguard, watu wanaogopa kuwahoji, kwani nani ataingia na bunduki huku ndani? Tunakuja tumekaguliwa mpaka mlangoni pa kuingia, sasa mtu anaitwa kuja kuhojiwa, mfano ana ngao mbili hapa mabegani, anakuja na walinzi nane mnanyanyuliwa mpaka na kwenye viti utamhoji vipi huyo mtu? Mimi nashauri wakifika pale protocol zao ziishie kule, maana hata sisi tukiwa watuhumiwa kwenye taasisi zao hatuendagi na mbwembwe tunaenda mmoja, waje humu watu wawahoji bila kuwa na wasiwasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi natokea Kanda ya Ziwa na nimeshangaa sana Waziri wa Mipango, umenisahau. Hivi ninyi watu wa Kanda ya Ziwa labda huwa mnatuona kama sisi ni Waganda au namna gani? Uwanja unaoingiza pesa Tanzania ukitoa Uwanja wa Dar es Salaam, Uwanja wa pili ni Uwanja wa Mwanza, kigugumizi ni cha nini kutuwekea International Airport Mwanza, mnieleze. Halafu mnakuja na mpango, nawaangali na Wabunge wenzangu wa Kanda ya Ziwa mnapiga makofi, sisi tunakuja kusindikiza kila siku humu ndani? Uwanja wa Ndege wa Mwanza unajiuza, una wateja tuna nchi jirani zinategemea pale. (Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mnajenga reli …

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Brother, tuliza basi.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Musukuma, muda wako umeisha naomba umalizie.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuomba namalizia huyu ameingilia muda wangu, kama unataka tuelewane ukinichenga hapa Mheshimiwa Waziri wa Mipango, mwaka huu ni mwisho kutudanganya mlisingizia uwanja umekataliwa na Ilemela, mmerudishiwa na hela bilioni 4.5, tunaomba kwenye bajeti inayokuja tuone hapa unakuja na hela, ukija na swaga tutazinguana. Nakushukuru. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania wa Mwaka 2018
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuwapongeza sana SUMATRA, wamejitahidi kiasi chake kuweza kusimamia upunguzwaji wa ajali barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mimi nilikuwa napenda kushauri yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kama mdau wa usafirishaji; huko barabarani hususan kwenye mabasi kuna kitu kinaitwa king’amuzi. King’amuzi kimefungwa na spidi 85, lakini shida iliyopo kule kuna utata kati ya polisi na king’amuzi. Kule kwenye gari unaweza ukakuta king’amuzi hakijafika 85 lakini ukikamatwa na traffic wakikupiga tochi unakuta inasoma 90. Sasa nilikuwa nashauri hivi vyombo viwili pia viweze kukaa na kushauriana kuona ni jinsi gani wanaweza kuweka kitu cha pamoja kitakachozuia mgongano kule njiani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili nizungumzie kuhusu hilo hilo suala la king’amuzi. Hiki king’amuzi kimewekwa sana kwa ajili kama ya kukusanyia pesa. Nilikuwa nashauri, kama lengo lilikuwa ni kupunguza ajali za barabarani kwanini tusiweke vitu ambavyo vinaweza kufunga speed kama gavana ambapo ilikuwa ina uwezo gari ikifika speed 80 inakuwa haiwezi kuendelea; kwa hiyo kunakuwa hakuna ule upigwaji wa faini kwa madereva kwa sababu faini hizi zinapopigwa anayetakiwa kulipa ni dereva anayeendesha gari. Sasa unakuta dereva mwingine pengine amepitiliza moja tu, amepigwa amefika mpaka milioni 5 kwenye leseni na anatakiwa kulipwa, mshahara wa dereva ni laki 3. Kwa hiyo tunakuta madereva wengi wanazikimbia gari kutokana na hizi adhabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ushauri wangu mimi nilikuwa naomba kama Mheshimiwa Waziri anatusikia ni vizuri zaidi tukatoka kwenye king’amuzi cha kukusanya hela kwa madereva tukawa na king’amuzi kinachoitwa gavana kinafunga speed inayotakiwa na Serikali, tuachane na haya mambo ya kuwaonea watu kuwatoza hela ambayo hawana uwezo wa kuzilipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulishauri sana kwenye muswada, nimeona humu ndani hayakuingia. Ukisoma kwenye kipengele cha 6(1)(f) tulishauri kwamba ukaguzi wa magari uendelee kufanyika na traffic.Sisahihi kwamba hawa LATRA wakifika waanze kutukagulia magari. Tanguzamani professional ya ukaguzi wa magari tunaomba sana libaki kuwa kazi ya polisi. Waangalie ni jinsi gani SUMATRA walivyokuwa wanafanya kazi na polisi kwa ushirikiano wakawaacha hawa waendelee na utaalam wao, tusiwapore madaraka hawa ma-vehicle waliosoma kazi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kipengele cha 6(1)(e)tulishauri pia, sikuliona humu kwamba vizuri anapotoka kwenye Chuo cha VETA tuendele na utaratibu ule ule. Kwamba ma-vehicle lakini pia na watu wa TRA ndio wawajibike kutoa leseni ya dereva. Hili la kusema kwamba wao kama LATRA ndio wasimame kumuhoji dereva na kutoa leseni na kufanya kazi zilizokuwa zinafanywa na vehicle na TRA si sahihi kwa sababu mtu anayepambana na dereva kule porini ni vehicle kwa hiyo libaki kama liliyokuwa zamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia LATRA amejipa mamlaka makubwa sana kwenye kifungu cha 18(2). Wanataka incase ikitokea gari imepata tatizo wao wanajipa mamlaka ya kufunga kampuni. Hatukatai, lakini wao hao hao wanajipa mamlaka ya kuifilisi kampuni; si mahakamakama ilivyokuwa zamani, huu si utaratibu hata kwenye Sheria ya Makampuni inayo sheria zake. kwamba kama kuna mgongano wa maamuzi yoyote au Serikali imefunga kampuni yako unaweza kuamua kuuza ama kufanya kitu chochote, si kwamba wao waamue hapo hapo na kwenda kuuza magari. Si sahihi, tunaomba ibaki kama ilivyokuwa zamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia suala la faini. Kwenye kipengele cha faini inaonekana gari likionekana na kosa kama ni kampuni itozwe milioni tano lakini kama ni mtu binafsi atozwe shilingi milioni tatu. Waziri pengine mnataka hizi kazi zisifanyike huko barabarani, hakuna mtu anaweza ku-afford kulipa hizo gharama ukilinganisha uendeshaji wa mabasi na vyombo vya usafirishaji ni mkubwa. Kwa hiyo, tungeomba tu ikabaki at least kwenye ile faini ya zamani ya shilingi laki tano;kwa sababu vyombo hivi inaweza ikatokea imepata hitilafu katikati ya barabara lakini ukikutana na vyombo hivi vinavyohusika kama LATRA huko mbele wao watapiga faini ya shilingi milioni tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusu suala la malori. Mheshimiwa Waziri mmeweka sheria ya kupunguza uzito kwenye malori huko barabarani, unataka gari ya super single ibebe tani 29 kutoka tani 34, na gari ya tairi mbili ibebe tani 32. Sasa Waziri mimi nikuombe tu, pengine haujafanya upembuzi, hakuna tatizo pamoja na kwamba utawaingiza watu wanasema na wengine watashindwa kuendelea na hii kazi na watafilisiwa; unapopunguza ule uzito kwa muda mfupi kama hivi ulivyoamua tarehe moja sijui mwezi wa pili au wa tatu; tatizo litakuja kwa mlaji ndio atakayeumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, sisi tunabeba cement kutoka Dar es salaam, tulikuwa tunapakia tani 34 mpaka 33 kwenye tairi ya super single, ukiondoa tani tano ikabaki 29 ujue tafsiri yake gharama za mafuta na posho za wafanyakazi zipo pale pale, kwa hiyo zile tani tano zitafidiwa na bei ambayo itaongezeka kwenye cement kwa sisi tunaotoka kwenye maeneo ya mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa namuomba Mheshimiwa Waziri; haya mambo yalikuwepo tangu mwanzo, sasa kama kumetokea mabadiliko tupeane muda ili tuweze kujiandaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine, mmeweka sheria ya kusema hamtaki tena tairi za super single Tanzania. Mheshimiwa Waziri nakupa mfano kuna watu wana magari 100, leo ukimwambia hatutaki kuona gari ya tairi ya super single barabarani maana yake unataka twende kwenye tairi mbili kwa tera(trailer).Tera moja linauzwa dola 50,000 na tera la super single linaunzwa dola 25,000. Mtu mwenye mkopo na ana magari 100 ukimwambia abadilishe matera sana sana unachotaka ni presha na kumuua. Kwa hiyo nilikuwa naomba Waziri hivi vitu mnavyoviandaa ni kuwapa muda, hizi sheria tunazozitunga zinarudi kwa watu na tayari watu walishaingia mikataba na mabenki na vitu vingine. Kwa hiyo, ni vizuri zaidi Mheshimiwa Waziri ukaangalia uwezekano wa kuweza kuacha haya mambo tukaenda nayo taratibu hata kipindi kingine tupo tayari kuyabadilisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mmeweka sheria ya watu wanaposafirisha ng’ombe kutoka kwa mfano Mwanza kuleta Dar es Salaam lazima awe na kibali cha abnormal kwamba ng’ombe zinatikisika zinaweza kuhiribu barabara, hii si sawa. Kama unaamua hivyo tunakubaliana kwamba tukate abnormal kwa ajili ya ng’ombe kwa sababu ng’ombe hata pembe haliwezi kutoka ndani ya tera, linakuwa katikati ya tera. Sasa ukisema linatikisika ni vizuri hata kwenye mabasi mseme na kwenyewe tukate abnormal kwa sababu hata binadamu anavyokaa kwenye basi lazima atikisike. Sasa ukitubagua hivi inaonekana kama unatuonea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sana twende utaratibu ule wa zamani kwa sababu ukiweka hivi tunataka tuone pia hata mtu mwenye tanker iliyobeba mafuta na yenyewe inatikisika. Hivi vitu haviwezekani tusitunge sheria za kupoteza mapato ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye upande wapolisi (tochi) sijui tuangalie uwezekano gani kwa sababu tukiendelea kuacha hizi fujo zilizopo, ndiyo maana unaona polisi wanapigwa ngumi na watu kule barabarani. Watu wengine unakuta umewekwa picha na gari lakini rangi ya gari si ya kwako. Sasa hivi vitu ni vizuri tukaangalia, kama tunaangalia utaratibu mwingine mzuri ili hawa polisi wasitumike vibaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pengine zamani ilikuwa inawasaidia ile kukaa kuzungumza na madereva wana- negotiate kua vitu walikuwa wanapata vidogo vidogo inaleta shida sana ile mtu anakuja kukusimamisha anakwambia ulipita tarehe 15 unasomewa license si ya kwako, plate namba ya kwako; lazima ngumi zitapigwa kila siku. Kwa hiyo, kwa kuwalinda vijana wetu ni vizuri tukatengeneza utaratibu mwingine mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pindi kunapotokea ajali kwenye mabasi, wamejipa mamlaka ya kusema popote pale itakaposababishwa ajali kama kuna binadamu amejeruhiwa ni lazima mmiliki alipe gharama kufidia yule mtu aliyeumia, si sahihi. Kwenye magari tuna bima, lakini pia kuna mahakama navehicle lazima procedure zifuatwe mpaka kuja kupigwa faini. Ukiweka hii nafasi ya kwamba ajali tu inapotokea mtu lazima umlipe, sasa tunakata bima ya kazi gani au LATRA inajigeuza kuwa bima?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kuna vitu vingine mkubali kuviondoa japokuwa humu hamkuviweka, tubaki kama ilivyokuwa zamani. Tunatambua kwamba LATRA itafanya kazi nzuri kama ilivyokuwa inafanya SUMATRA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la VITS, king’amuzi, wewe unafahamu; suala la king’amuzi hebu tunataka uliangalie vizuri, mmiliki wasever ni SUMATRA mmiliki wa teknolojia ni mtu mwingine baki, anayeendesha king’amuzi ni mtu mwenye basi. Sasa kila mwezi tunalipishwa elfu sitini. Waziri nikuombe, hivi Serikali haiwezi ku-control yenyewe kuliko kuwa na dalali hapo katikati ambaye kitu kinauzwa dola 50 watu wanalipishwa shilingi 60,000 kila mwezi wakati hiki kitu kinaweza kupatikana kwa shilingi 15,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini kama ninyi mnataka kukusanya pesa kutumia king’amuzi na ku-control system ya magari; na server mko nayo kwa nini hivi ving’amuzi msiviuze wenyewe kama Serikali kuliko kuwa na watu wana teknolojia, wanajitegemea ofisi mtaani, Serikali nayo inakaa na server na mimi namiliki king’amuzi? Hii sio sawa. Mheshimiwa Waziri nikuombe sana tunapoenda kuanzisha hiki chombo hivi vitu vyote viwe mali ya Serikali; na ikiwezekana turuhusiwe wenyewe tununue kwa sababu vinapatikana, ninyi kazi yenu muingize programu na kuweka server lakini haya mambo ya kumpa mtu mmoja ni kutaka kutuonea sisi wamiliki wa mabasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na Waziri nakutakia kila la kheri.
Muswada wa Sheria ya Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Ardhini wa Mwaka 2018
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuwapongeza sana SUMATRA, wamejitahidi kiasi chake kuweza kusimamia upunguzwaji wa ajali barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mimi nilikuwa napenda kushauri yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kama mdau wa usafirishaji; huko barabarani hususan kwenye mabasi kuna kitu kinaitwa king’amuzi. King’amuzi kimefungwa na spidi 85, lakini shida iliyopo kule kuna utata kati ya polisi na king’amuzi. Kule kwenye gari unaweza ukakuta king’amuzi hakijafika 85 lakini ukikamatwa na traffic wakikupiga tochi unakuta inasoma 90. Sasa nilikuwa nashauri hivi vyombo viwili pia viweze kukaa na kushauriana kuona ni jinsi gani wanaweza kuweka kitu cha pamoja kitakachozuia mgongano kule njiani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili nizungumzie kuhusu hilo hilo suala la king’amuzi. Hiki king’amuzi kimewekwa sana kwa ajili kama ya kukusanyia pesa. Nilikuwa nashauri, kama lengo lilikuwa ni kupunguza ajali za barabarani kwanini tusiweke vitu ambavyo vinaweza kufunga speed kama gavana ambapo ilikuwa ina uwezo gari ikifika speed 80 inakuwa haiwezi kuendelea; kwa hiyo kunakuwa hakuna ule upigwaji wa faini kwa madereva kwa sababu faini hizi zinapopigwa anayetakiwa kulipa ni dereva anayeendesha gari. Sasa unakuta dereva mwingine pengine amepitiliza moja tu, amepigwa amefika mpaka milioni 5 kwenye leseni na anatakiwa kulipwa, mshahara wa dereva ni laki 3. Kwa hiyo tunakuta madereva wengi wanazikimbia gari kutokana na hizi adhabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ushauri wangu mimi nilikuwa naomba kama Mheshimiwa Waziri anatusikia ni vizuri zaidi tukatoka kwenye king’amuzi cha kukusanya hela kwa madereva tukawa na king’amuzi kinachoitwa gavana kinafunga speed inayotakiwa na Serikali, tuachane na haya mambo ya kuwaonea watu kuwatoza hela ambayo hawana uwezo wa kuzilipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulishauri sana kwenye muswada, nimeona humu ndani hayakuingia. Ukisoma kwenye kipengele cha 6(1)(f) tulishauri kwamba ukaguzi wa magari uendelee kufanyika na traffic.Sisahihi kwamba hawa LATRA wakifika waanze kutukagulia magari. Tanguzamani professional ya ukaguzi wa magari tunaomba sana libaki kuwa kazi ya polisi. Waangalie ni jinsi gani SUMATRA walivyokuwa wanafanya kazi na polisi kwa ushirikiano wakawaacha hawa waendelee na utaalam wao, tusiwapore madaraka hawa ma-vehicle waliosoma kazi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kipengele cha 6(1)(e)tulishauri pia, sikuliona humu kwamba vizuri anapotoka kwenye Chuo cha VETA tuendele na utaratibu ule ule. Kwamba ma-vehicle lakini pia na watu wa TRA ndio wawajibike kutoa leseni ya dereva. Hili la kusema kwamba wao kama LATRA ndio wasimame kumuhoji dereva na kutoa leseni na kufanya kazi zilizokuwa zinafanywa na vehicle na TRA si sahihi kwa sababu mtu anayepambana na dereva kule porini ni vehicle kwa hiyo libaki kama liliyokuwa zamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia LATRA amejipa mamlaka makubwa sana kwenye kifungu cha 18(2). Wanataka incase ikitokea gari imepata tatizo wao wanajipa mamlaka ya kufunga kampuni. Hatukatai, lakini wao hao hao wanajipa mamlaka ya kuifilisi kampuni; si mahakamakama ilivyokuwa zamani, huu si utaratibu hata kwenye Sheria ya Makampuni inayo sheria zake. kwamba kama kuna mgongano wa maamuzi yoyote au Serikali imefunga kampuni yako unaweza kuamua kuuza ama kufanya kitu chochote, si kwamba wao waamue hapo hapo na kwenda kuuza magari. Si sahihi, tunaomba ibaki kama ilivyokuwa zamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia suala la faini. Kwenye kipengele cha faini inaonekana gari likionekana na kosa kama ni kampuni itozwe milioni tano lakini kama ni mtu binafsi atozwe shilingi milioni tatu. Waziri pengine mnataka hizi kazi zisifanyike huko barabarani, hakuna mtu anaweza ku-afford kulipa hizo gharama ukilinganisha uendeshaji wa mabasi na vyombo vya usafirishaji ni mkubwa. Kwa hiyo, tungeomba tu ikabaki at least kwenye ile faini ya zamani ya shilingi laki tano;kwa sababu vyombo hivi inaweza ikatokea imepata hitilafu katikati ya barabara lakini ukikutana na vyombo hivi vinavyohusika kama LATRA huko mbele wao watapiga faini ya shilingi milioni tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusu suala la malori. Mheshimiwa Waziri mmeweka sheria ya kupunguza uzito kwenye malori huko barabarani, unataka gari ya super single ibebe tani 29 kutoka tani 34, na gari ya tairi mbili ibebe tani 32. Sasa Waziri mimi nikuombe tu, pengine haujafanya upembuzi, hakuna tatizo pamoja na kwamba utawaingiza watu wanasema na wengine watashindwa kuendelea na hii kazi na watafilisiwa; unapopunguza ule uzito kwa muda mfupi kama hivi ulivyoamua tarehe moja sijui mwezi wa pili au wa tatu; tatizo litakuja kwa mlaji ndio atakayeumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, sisi tunabeba cement kutoka Dar es salaam, tulikuwa tunapakia tani 34 mpaka 33 kwenye tairi ya super single, ukiondoa tani tano ikabaki 29 ujue tafsiri yake gharama za mafuta na posho za wafanyakazi zipo pale pale, kwa hiyo zile tani tano zitafidiwa na bei ambayo itaongezeka kwenye cement kwa sisi tunaotoka kwenye maeneo ya mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa namuomba Mheshimiwa Waziri; haya mambo yalikuwepo tangu mwanzo, sasa kama kumetokea mabadiliko tupeane muda ili tuweze kujiandaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine, mmeweka sheria ya kusema hamtaki tena tairi za super single Tanzania. Mheshimiwa Waziri nakupa mfano kuna watu wana magari 100, leo ukimwambia hatutaki kuona gari ya tairi ya super single barabarani maana yake unataka twende kwenye tairi mbili kwa tera(trailer).Tera moja linauzwa dola 50,000 na tera la super single linaunzwa dola 25,000. Mtu mwenye mkopo na ana magari 100 ukimwambia abadilishe matera sana sana unachotaka ni presha na kumuua. Kwa hiyo nilikuwa naomba Waziri hivi vitu mnavyoviandaa ni kuwapa muda, hizi sheria tunazozitunga zinarudi kwa watu na tayari watu walishaingia mikataba na mabenki na vitu vingine. Kwa hiyo, ni vizuri zaidi Mheshimiwa Waziri ukaangalia uwezekano wa kuweza kuacha haya mambo tukaenda nayo taratibu hata kipindi kingine tupo tayari kuyabadilisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mmeweka sheria ya watu wanaposafirisha ng’ombe kutoka kwa mfano Mwanza kuleta Dar es Salaam lazima awe na kibali cha abnormal kwamba ng’ombe zinatikisika zinaweza kuhiribu barabara, hii si sawa. Kama unaamua hivyo tunakubaliana kwamba tukate abnormal kwa ajili ya ng’ombe kwa sababu ng’ombe hata pembe haliwezi kutoka ndani ya tera, linakuwa katikati ya tera. Sasa ukisema linatikisika ni vizuri hata kwenye mabasi mseme na kwenyewe tukate abnormal kwa sababu hata binadamu anavyokaa kwenye basi lazima atikisike. Sasa ukitubagua hivi inaonekana kama unatuonea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sana twende utaratibu ule wa zamani kwa sababu ukiweka hivi tunataka tuone pia hata mtu mwenye tanker iliyobeba mafuta na yenyewe inatikisika. Hivi vitu haviwezekani tusitunge sheria za kupoteza mapato ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye upande wapolisi (tochi) sijui tuangalie uwezekano gani kwa sababu tukiendelea kuacha hizi fujo zilizopo, ndiyo maana unaona polisi wanapigwa ngumi na watu kule barabarani. Watu wengine unakuta umewekwa picha na gari lakini rangi ya gari si ya kwako. Sasa hivi vitu ni vizuri tukaangalia, kama tunaangalia utaratibu mwingine mzuri ili hawa polisi wasitumike vibaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pengine zamani ilikuwa inawasaidia ile kukaa kuzungumza na madereva wana- negotiate kua vitu walikuwa wanapata vidogo vidogo inaleta shida sana ile mtu anakuja kukusimamisha anakwambia ulipita tarehe 15 unasomewa license si ya kwako, plate namba ya kwako; lazima ngumi zitapigwa kila siku. Kwa hiyo, kwa kuwalinda vijana wetu ni vizuri tukatengeneza utaratibu mwingine mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pindi kunapotokea ajali kwenye mabasi, wamejipa mamlaka ya kusema popote pale itakaposababishwa ajali kama kuna binadamu amejeruhiwa ni lazima mmiliki alipe gharama kufidia yule mtu aliyeumia, si sahihi. Kwenye magari tuna bima, lakini pia kuna mahakama navehicle lazima procedure zifuatwe mpaka kuja kupigwa faini. Ukiweka hii nafasi ya kwamba ajali tu inapotokea mtu lazima umlipe, sasa tunakata bima ya kazi gani au LATRA inajigeuza kuwa bima?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kuna vitu vingine mkubali kuviondoa japokuwa humu hamkuviweka, tubaki kama ilivyokuwa zamani. Tunatambua kwamba LATRA itafanya kazi nzuri kama ilivyokuwa inafanya SUMATRA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la VITS, king’amuzi, wewe unafahamu; suala la king’amuzi hebu tunataka uliangalie vizuri, mmiliki wasever ni SUMATRA mmiliki wa teknolojia ni mtu mwingine baki, anayeendesha king’amuzi ni mtu mwenye basi. Sasa kila mwezi tunalipishwa elfu sitini. Waziri nikuombe, hivi Serikali haiwezi ku-control yenyewe kuliko kuwa na dalali hapo katikati ambaye kitu kinauzwa dola 50 watu wanalipishwa shilingi 60,000 kila mwezi wakati hiki kitu kinaweza kupatikana kwa shilingi 15,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini kama ninyi mnataka kukusanya pesa kutumia king’amuzi na ku-control system ya magari; na server mko nayo kwa nini hivi ving’amuzi msiviuze wenyewe kama Serikali kuliko kuwa na watu wana teknolojia, wanajitegemea ofisi mtaani, Serikali nayo inakaa na server na mimi namiliki king’amuzi? Hii sio sawa. Mheshimiwa Waziri nikuombe sana tunapoenda kuanzisha hiki chombo hivi vitu vyote viwe mali ya Serikali; na ikiwezekana turuhusiwe wenyewe tununue kwa sababu vinapatikana, ninyi kazi yenu muingize programu na kuweka server lakini haya mambo ya kumpa mtu mmoja ni kutaka kutuonea sisi wamiliki wa mabasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na Waziri nakutakia kila la kheri.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. Kwanza kabisa nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri aliyoifanya. Sisi wananchi tulioteseka na machimbo na wawekezaji wakubwa wa migodi tunamwomba aendelee kukaza buti, sisi tuko nyuma yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwatake Watanzania kuuona Upinzani wetu ulioko Tanzania kuwa ni kama maigizo. Watu wanaingia humu ni kwa sababu tu pengine ya kutafuta maisha, lakini hawana nia thabiti ya kulikomboa Taifa hili. Lingine wajiulize hawa ndio Wabunge wanaowatuma kuja kuwawakilisha, badala ya kushughulika na matatizo yaliyoko kwenye Majimbo yao wanahangaika na kutetea wezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niliwahi kusema kwenye mchango wangu kwamba tunafahamu na wengine tumeshuhudia sikupata nafasi na kuwataja na wakiguna naweza kutaja, kwamba watu walivuna mpunga sasa mpunga ule jinsi ya kuurudisha inakuwa ni vigumu, kwa hiyo wanataka kufa na tai shingoni. (Makofi_

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niseme tu kwamba Mheshimiwa Rais kazi aliyoifanya ni fundisho hata kwa Upinzani. Namshukuru Mama mmoja kule nyuma amesema suala hili liwe la wote. Hata mimi nakubaliana na tumekuwa tukiomba sana sisi Wabunge wa CCM kwamba, tumuunge mkono Rais kwa jitihada aliyoifanya wakawa wanatupinga. Toka mwanzo nilimsifu sana Mheshimiwa Ole-Millya yeye aliunga mkono. Wengine wote humu mlitolewa na Mheshimiwa Ester Bulaya kama watoto wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kwa sababu imeonekana na Wazungu wamekubali kutulipa wanakuja humu kupiga makofi na kung’ang’ana na miongozo. Mimi niwaombe tu Wapinzani wa Tanzania mjifunze kwa kuona mfano kutoka kwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri pia kwamba pamoja na kuhusiana na kodi za makinikia na sisi watu wa Geita GGM imetunyonya vitu vingi sana, tumepiga kelele muda mrefu, tunakosa support na bahati nzuri Mheshimiwa Rais anatoka kwenye Mkoa wetu. Ukiambiwa fedha tulizokwisha kulipwa kwa Geita dola milioni tatu kwa miaka miwili ukiangalia makorongo yaliyoko pale tunahitaji Serikali iunde timu ya uchunguzi kwenye mgodi pia wa GGM ambao upo Geita na watu wa Geita tunasema hatujafaidika kabisa na mgodi ule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu gani tulikuwa hatuna uwezo kama Halmashauri wa kuweza kupiga hesabu na Wawekezaji hawa. Tumekuwa tukilalamika sana, tunapewa pesa kama hisani na mtu anayetupa hesabu ndiyo TMAA ambao ni wezi wameshikwa na Mheshimiwa Rais kwamba hawafai. Kwa hiyo, tunamwomba pia Mheshimiwa

Rais aunde Tume ambayo itaenda kwenye migodi ile kuangalia kwa sababu wale tuliokuwa tunategemewa wanatupa hesabu sahihi ndiyo hao wameonekana kwenye ripoti ya Osoro kwamba hawafai, kwa hiyo, turudie hata mgodi wa GGM.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie tu ninyi ambao hamuelewi migodini baada ya kauli za Rais na yule mkubwa wa Barrick kuja, jana watu wa GGM Geita walituita tukutane wanataka kutupa bomba la maji kwa mpango wa haraka. Tumekataa kwa nini mtupe bomba la maji, tunataka tupigiwe hesabu, haiwezekani Rais anachachamaa kushika wezi sisi tunapewa maji. Tutajitwisha ndoo kichwani tutabanana na Waziri humu, lakini Serikali iunde Tume kwenda kuchunguza mgodi mkubwa wa GGM ambao una mapato makubwa na una dhahabu nyingi kuliko hata Kahama. Kwa hiyo, naomba sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, nampongeza sana Mheshimiwa Rais na Profesa Osoro amekuwa jasiri, amewataja wezi, amewataja watu waliosababisha matatizo mengine tunao CCM. Tufike mahali tuambizane ukweli tuache mizaha. Ripoti imesomwa tumeangalia watu wote wenye Degree ma- Professor na wengine ambao hatukusoma na wananchi wetu kule vijijini. Halafu watu waliotajwa Bunge kutoka CCM wanaanza kuweka kwenye twitter wanasema mimi sihojiwi mpaka nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi kweli wezi wana kinga gani? Kama wametajwa ni wezi haiwezekani hata kama yuko CCM. Hili siyo suala ya mzaha kuna maisha ya watu na watu tumeumia. Watu mmetajwa Wabunge wenzangu wa CCM humu halafu mtu anaanza na heshima zake, tunamheshimu kabisa Mzee wetu humu ndani ana-twitt kwenye twitter anasema mimi siwezi kuhojiwa mpaka nipelekwe Mahakamani, yeye ni nani? Kama tunataka kumaliza matatizo haya sisi wengine tuliburuzwa sana, tuliburuzwa sana miaka iliyopita watu wakafunga mikataba wakafungia Ulaya wakagawana hela na bado wanakuja kutuletea upinzani kule kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kama kuna uwezekano wa hawa watu kama ni Mbunge kama ni nani wakamatwe. Wanaotusumbua humu ni hawa ni hao hao wametajwa kwa professa Osoro, katajwa Mheshimiwa Kafumu, katajwa Mheshimiwa Ngeleja, Mheshimiwa Chenge, wana kinga gani kama wezi? Kwani Magereza yamewekwa ya akina Babu Seya peke yake.Tufike mahali tulipiganie Taifa hili, CCM siyo kichaka cha kuja kujificha wezi. Kila mwaka mtu anatajwa, kila tuhuma, yeye ni nani. Tufike mahali tuweserious na suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nimesoma kwenye kitabu cha Waziri, ukurasa wa 55, ukisoma pale kipengele kinasema atatoza kodi ya asimilia tano kwenye dhahabu kwa wachimbaji wadogo. Halafu Mheshimiwa Waziri akasema mwishoni, anategemea kukusanya milioni
88. Hivi anaendaje kufanya pressure ya kuhangaika na wachimbaji wadogo ambao kimsingi huwezi kuishika ile dhahabu. Akiweka haya masharti kuna asilimia nne ya TMAA kuna asilimia tano ya kwake na kuna asilimia moja ya kusafirisha dhahabu, karibia asilimia 10 wakati ukienda Kampala ni one percent. Sasa kwa nini Waziri, Wizara ya Fedha wasiondoe kodi zote za kuingiza dhahabu ili tukapata na watu wanaotoka Malawi, Congo, Zambia, Uganda na Burundi wakaleta dhahabu Tanzania kwa sababu hakuna ushuru, tuka-deal na asilimia moja tu ya kusafirisha tukapata hela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata Mheshimiwa Waziri aking’ang’ana na hizo kodi zake nilishasema humu ndani, hawezi kumshika msafirisha dhahabu tunajua tunavyobeba, kwa nini asilegeze masharti tukaweka zero halafu hii one percent atapata hela nyingi kuliko hizi milioni 88. Kwa hiyo, nashauri sana Mheshimiwa Waziri ajaribu kufikiria na alione hili suala kwa macho mawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais na nimekuwa nikifuatilia taarifa zote hata alivyomtumbua Mheshimiwa Profesa Muhongo, sijui kama yumo humu ndani nina hamu naye kweli, alisema niliamini

vyeti, vyeti vimeniangusha! Juzi tena kasema mara tatu PhD 17. BOT hii ndiyo return yake Ma-PhD?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali tuangalie uwezo wa mtu na ikiwezekana hata Mawaziri hawa wawe wanafanyiwa hata interview, haiwezekani unakuwa na watu wana PhD za kutisha, wanapogundua wezi hao wenye PhD wanaanza kututishia sisi ambao hatuna PhD. Hata hivyo, suala hili ni halali, ziko wapi degree tunazozitegemea hapa? Watu wamebeba Dokta, PhD sijui nini, halafu mwisho wa siku tunapopata matatizo wanatutisha wanatupeleka Mahakamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Taifa hili, watu wengi hawana vyeti na watu wengi hawana elimu kwa kuwa Katiba ilisema watu kupata vyeo fulani inataka elimu kubwa wamefoji hizo digrii ambazo input yake tunaiona leo hapa. Kwa nini tusijifunze kwenye nchi zilizoendelea? Kuna nchi ambazo zimeweka watu ambao hawana hizo digrii na zinafanya vizuri. Tuking’ang’ana na hizo degree ndugu zangu tutakuja kupata matatizo, uwezo ni mdogo makaratasi ni makubwa. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nataka kushauri kuhusiana na mwelekeo wa Serikali ya Awamu ya Tano, hata kwenye ushauri wangu nilipochangia mwanzo nilisema…..

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia.

Nilikuwa namwomba Mheshimiwa Waziri wa Sheria afikirie upya na kuendelea kufanya ziara hasa kwenye Majimbo yetu yaliyoko kule vijijini. Tuna shida kubwa sana ya Mahakama, namaanisha majengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama ni sehemu ambayo kila mtu anategemea akatendewe haki, lakini kweli Mahakama nyingine hata huyo hakimu kwenye kutenda haki inamuwia vigumu kutokana na mazingira yenyewe ya kufanyia kazi. Huwezi ukafanya kazi ya kuhukumu watu halafu umekaa kwenye jengo limejaa popo, unakwepana na mavi ya popo, halafu ukatenda haki sawa sawa. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri ajaribu kufanya ziara, aangalie hasa kule vijijini, tuna hali mbaya sana kuhusiana na majengo ya Mahakama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha pili, Mheshimiwa Waziri, Mahakama nyingi zimejaa mahabusu ambao kimsingi wengine wako mle tu kwa makosa ambayo yanastahili hata ungeleta amendment tukabadilisha sheria wakapigwa hata makofi tu wakarudi nyumbani. Kwa mfano, Gereza letu la Geita, capacity yake ni watu 141, lakini mpaka jana watu 750 wako ndani. Hii ni hali mbaya sana. Ukiangalia watu wengi walioko humo, wana kesi ndogo ndogo kuingia kwa jinai. Mtu ameingia tu labda eneo la mgodi, amekutwa karibu na ziwa kwenye maeneo ya hifadhi huko Rubondo; wamerundikwa wako mle.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa nakuomba sana Mheshimiwa Waziri, hebu jaribu kuangalia uwezekano, ikiwezekana hata kupanua Magereza, lakini ikiwezekana kujaribu kuleta tubadilishe hizo sheria makosa ambayo hayastahili mtu kuingia ndani, basi aachwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda nchi za wenzetu zilizoendelea, nakumbuka siku moja nilikuwa China, nilifanya kosa Hong Kong, nilivyokamatwa, nilikuwa na kosa tu, tumebishana tukataka kupigana ngumi na mwenzangu, lakini nilivyoitiwa oolisi, walikuja wakaniomba kitambulisho changu peke yake. Nilivyowapa kitambulisho, wakaniachia na mwenzangu wakamwachia. Siku ambayo tunataka kutoka, tulitozwa faini ya dola 5,000 pale pale immigration wakati wa kugongewa passport. Lakini Tanzania unakuta mtu anamwambia tu huyu amenitukana, huyu amenidhulumu, hata hawajahakikisha, mtu amerundikwa Magereza. Kwa hiyo, nilikuwa naomba sana Mheshimiwa ukaze buti, lakini nikuhakikishie Mheshimiwa Kabudi unaenda sawa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nilikuwa najaribu kuangalia michango, hata rafiki yangu Mheshimiwa Lema mwenye uzoefu kule Magerezani, anakushauri tu, ni mambo madogo madogo, ujaribu kuyarekebisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba sisi kama Waheshimiwa Wabunge ambao tunatunga hizi sheria, tuviache vyombo vifanye kazi. Haya mambo ya kuwa watu wanakuja humu wanasema nani kapotea, Beni Saanane, hata watu wa CCM wamechinjwa wengi tu. Kibiti wamechinjwa, hatujapiga kelele, tumevikabidhi vyombo vifanye kazi. Kwa hiyo, hata wale ambao mnasema wamepotea, polisi wanafanya kazi. Ukitaka kujua vizuri, acha kupiga kelele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiona watu wanapiga kelele, tunaelekea kuzuri, kwa sababu kila siku tunaambiwa tufuate sheria bila shuruti, lakini watu wanajitokeza na viburi vyao.

Mhshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa kwenye kampeni ile ya Kinondoni. Tumepiga kampeni na hawa wenzangu, nani hajui kama mlikuwa mnasema watu waandamane mbebe majeneza 200? Ungekuwa wewe ni Serikali ungewaacha watu wanahamasisha watu wafe? Mimi nilikuwa nadhani tuviache vyombo vifanye kazi, nina hakika polisi na watu wengine wasitishwe na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata mimi niliwekwa ndani, si nilikuwa na kosa, kuna shida gani? Ni vizuri hata Waheshimiwa Wabunge hawa wakorofi korofi wanapowekwa Magereza kule wanapewa fundisho.

Unamwona hata rafiki yangu Mheshimiwa Lema sasa hivi kidogo amekuwa binadamu! Tena nashukuru hata leo amenisalimia vizuri. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nimekuwa nikisikia mara nyingi sana wanapiga kelele kuhusiana na matamko ya Rais kwamba anavunja Katiba, lakini humu ndani kuna wasomi Wabunge, wanasahau kwamba Waheshimiwa Wabunge mnatunga sheria, lakini na tamko la Rais nalo ni sheria. Kwenye Katiba Ibara ya 37 inampa mamlaka Rais kusikia au kutokusikia ushauri. Sasa kama mnaona ni tatizo, leteni hoja humu ndani tubadilishe sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia. Niseme tu kiukweli Mheshimiwa Waziri na Serikali ni vizuri wakaangalia uwezekano wa kurekebisha sheria, hasa kwenye makosa madogo madogo ambayo ndiyo yamepelekea magereza yetu mengi yamejaa mahabusu kwa kesi ambazo kiukweli zingine zinastahili tu hata makofi mtu anaenda nyumbani. Kwa hiyo, nashauri sana, hizi sheria zilitungwa Watanzania tukiwa milioni 20, leo tupo milioni 55 bado mtu anawekwa mahabusu wiki mbili kwa kesi ya kuiba kuku. Ni vitu ambavyo kiukweli lazima tufikirie adhabu ambazo zitaweza kupunguza mrundikano wa mahabusu kule ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili; nimeona kwenye taarifa ya Waziri katika mahakama zilizojengwa zimo na ya Geita, Chato na Bukombe na mimi natokea Geita ambako kumejengwa mahakama hiyo. Nimwombe tu Mheshimiwa Waziri, aongeze msukumo mahakama ile iweze kukamilika. Sio kweli kwamba imekamilika kama alivyoandika kwenye kitabu chake na tunaona kesi kubwa zinakwenda kufanyika kwenye vyumba vya Wakuu wa Wilaya, sio haki. Ni vizuri tukayakamilisha yale majengo ili yaweze kutoa haki kwa wahusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nilikuwa nasoma kwenye Kitabu cha Kambi Rasmi ya Upinzani kuhusiana na uteuzi wa Majaji pamoja na kwamba yameondolewa lakini ukiangalia kwenye Katiba, Ibara ya 109(7) na (8) pale inampa mamlaka Mheshimiwa Rais kuteua na anakuwa na jopo ambalo linamshauri. Ningewashauri tu wenzangu, ni vizuri tukamuachia Rais madaraka yake, akafanya kazi kwa mujibu wa Katiba yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho; nimeongea hapa nasikia rafiki yangu Mheshimiwa Sugu ananiita mboyoyo, nakubali, sawa, lakini Watanzania wanajua kati yangu mimi na wewe mboyoyo ni nani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili; dada yangu, Mheshimiwa Upendo nilikuwa namuuliza tu kwa nia nzuri, amesema Humphrey Polepole amesema uteuzi wa wanawake wa CHADEMA unapatikana mpaka wapitiwe na Mwenyekiti. Mimi sikuelewa Kiswahili ndiyo maana nikauliza kwa sababu ninavyofahamu Humphrey yupo sawa; yule ni Mwenyekiti wa chama lazima apitie majina ya watu wake, kuna tatizo gani analolalamika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nilikuwa najaribu kuangalia kumbukumbu yangu kichwani, Serikali imewekeza pesa nyingi sana kwenye michezo hasa mchezo wa mpira. Nikirudisha memory zangu naona kama mpira wa miguu na michezo hiyo mingine haitusaidii sisi kama Serikali kutangazwa kwenye nchi nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijabu kuangalia, sisi inawezekana tuna bahati sana ya kutangazwa na wasanii hasa wa muziki na filamu. Wamefanya vizuri, tumeona leo hata ukienda huko nje kwenye clubs za Wazungu inapigwa miziki ya Kiswahili unapata morali hata wewe wa kuingia club na kucheza. Ila kwa style zinazoendelea kwa Mheshimiwa Waziri na yenyewe hii tasnia tunaenda kuipoteza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia sana hapa kipindi cha katikati fungia fungia. Msanii anafanya kazi yake nzuri; na wewe ni mpenzi wa muziki, nakufahamu. Kinachomfanya mtu ahamasike kulipa kiingilio kwenda kwenye muziki ni pamoja na matangazo mazuri atayokuwa ametangaza msanii. Kwa sasa kinachoendelea, msanii anafanya kazi nzuri, kwenye kushuti akikosea tu kidogo mpasuo, Mheshimiwa Waziri huyo, amefunga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka kumwuliza, anafungia miziki ya Tanzania au anawafungia wasanii wa Tanzania kupasua sketi kuonesha mpasuo, hebu aangalie miziki ya akina Rihana na ndiyo wanakaa wanaangalia humu kwenye youtube kila saa. Hii ya Tanzania ambayo mnataka wasanii wetu wavae sijui dela, sijui wavae pekozi, hakuna mtu aliye na hobby na miziki ya pekozi kwa sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia msanii anafanya kazi nzuri, ana-invest hela kwa mkopo na nini, akikosea tu mpasuo anafunga. Tukienda Samora, mbona akinamama tunaona kama zile nguo wanazovaa kule Samora Samora zinafafana tu na Wanamuziki, kwa nini kule hawapeleki kifungo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namshauri Waziri Mheshimiwa Mwakyembe, hebu tujifunze wasanii wetu wanaiga miziki ya Ulaya, halafu wanaiga na style za Ulaya na miziki Ulaya huwezi ukapeleka muziki mtu amevaa kanzu au dela haiwezekani!

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie faida tunazozipata kwa hawa wasanii wetu. Ni bora wakatafuta muda wakawapa semina kuliko kuwaacha, mtu anafanya kazi nzuri, anagharamika, halafu anakosea kosa moja tu, unamfungia miezi sita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niulize swali lingine, mwanamuziki ameimba muziki mwaka mzima na nusu, halafu Mheshimiwa Waziri anaibuka anasema huu muziki umekiuka maadili, anafungia. Sasa huko vijijini watu wameshaweka kwenye simu, kwenye computer, unapambana nao vipi? Anatupa shida sana sisi wenzake wa vijijini kwa sababu wana- create ujinga kwa watu walioko vijijini huko, Watendaji, akina nani, akikosa kazi tu anaanza kukamata computer zina miziki imefungiwa na Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri pia yeye ni mtu wa zamani kidogo ninavyomwona umri wake, hebu nataka anisaidie, vazi halisi la utamaduni wetu sisi la Kitanzania ni lipi? Kwa sababu nakumbuka wale wenye umri kama wangu wanafahamu, hata ngoma za utamaduni za Kitanzania akinamama hasa Wasukuma na Wagogo, wanafunga tu kwenye maziwa hapa, wanafunga na hapa chini, huku chini inakuwa kivutio. Sasa mbona hii miziki ya sasa hivi wanaleta figisu ambayo hatuwaelewi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli namwomba sana Mheshimiwa Waziri ajitahidi kukaa na wasanii, asitumie muda mwingi sana kufunga, ni bora kutumia muda mwingi kuwafundisha na kukemea yale mambo madogo madogo ili hii tasnia iendelee. Wanaona wanamsumbua Diamond hapa masikini wa Mungu, wanaona yaliyofanyika Kenya? Wenzenu wamempokea, wanamwambia imba kila kitu ulichozuiliwa. Wamempa kiwanja, wamempangia nyumba. Tutapoteza hizi bahati tubaki kung’ang’ana na mipira ambayo imeshakuwa kichwa cha mwendawazimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwulize Mheshimiwa Waziri kidogo atakapokuja kuhitimisha anisaidie. Waganga wa Kienyeji kule vijijini, ukiwa Wilayani Halmashauri wako chini ya Afisa Utamaduni. Naamini Waganga wa Kienyeji ni watu wazuri sana, tumeshindwa tu jinsi gani ya kuwatumia. Kwa kuwa Mhehimiwa Rais ameanza utaratibu wa kutoa tuzo kwa wale waliovumbua vitu, nadhani hata huku kwa Waganga wa Kienyeji aingie kidogo ili aone mambo yalivyo. Shida iliyoko, kwa nini wanawazuia kufanya matangazo wakati Wazungu wakileta chanjo za Polio wanawaruhusu watangaze kwenye…. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Hoja Kuhusu Bei ya Kuuza na Kununulia Mahindi
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Naomba sisi Wabunge tumwogope Mungu. Nakumbuka mwezi wa Februari na Machi tulipokuwa tunapiga kelele humu kulalamikia mfumuko wa bei, tulipotuma lawama ni Serikalini. Sasa, kama Serikali imeamua kuweka utaratibu ili tukipiga kelele iwe na majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilinde, mimi ni mfanyabiashara na mimi na–export mahindi. Humu kuna wengine hawafanyi biashara hiyo. Mimi najitoa kusema, nafanya hiyo biashara. Hakuna mahali Serikali imezuia kutoa mahindi nje, mpaka leo mimi natoa, lakini nataka niwaulize Wabunge wenzangu, ni nchi gani ambayo inafanya biashara kiholela? Juzi Watanzania zaidi ya 50 waliandamana Zambia. Walikwenda kununua mahindi Zambia, yakakamatwa kwa sababu hawakufuata utaratibu.

Mheshimiwa Spika, masharti yaliyowekwa ni kukata leseni na kufungua Kampuni. Waheshimiwa Wabunge tumwogope Mungu. Mimi nafanya hiyo biashara na Jimbo langu linaongoza Kanda ya Ziwa kwa kulima, Wabunge wanafahamu. Watu wanatoka Uganda na mitumbwi wanakuja kukaa Ziwani wananunua, wanapakia na hela za Uganda na mataka taka bila kufuata utaratibu. Ninyi ni wasomi wa design gani? Tutawezaje ku–control hata hizo dola tunazohangaika? Serikali iweke utaratibu, watu wafuate utaratibu na hela ziwe kwenye system ya Serikali, ndio tutapata hata dola kutoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutakaribisha magaidi, wafanyabiashara watakatishaji. Nikuombe masharti ya kufungua kampuni ukianza leo sasa hivi saa ni nne, saa kumi una leseni, wanaogopa nini? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye bajeti ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunaingia Bungeni hapa nilijifunza kupitia Wizara tatu ambazo zilikuwa pressure kubwa sana kwa Wabunge wote ambazo ni Wizara ya Maji, Wizara ya Afya na Wizara ya Ujenzi. Sasa najiuliza mara mbili mbili sielewi ndiyo maana sasa hivi wanawake wana kamsemo wanasema wanawake wanaweza. Hivi kwa nini pressure ya Wizara ya Afya imeisha kabisa yaani hata nilikuwa nasikiliza Wapinzani wanashauri lakini Wizara hii kila mwaka humu ndani lazima tulumbane, kuna tatizo gani Wizara ya Maji?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona hata Rais akienda kwenye ziara huko mikoani kwetu anapata pressure na maswali mengi na mabango ya maji. Ndugu yangu, rafiki yangu Kamwelwe kwani wewe huwezi kumaliza matatizo yako ukawa mbunifu kama Mheshimiwa Ummy alivyofanya kwenye Wizara sumbufu kabisa ya Afya? Gari mpya umepewa, mafuta yapo, ukija mikoani tatizo dakika mbili huyo kwenye ziara kwa Mkuu wa Mkoa, hukai na walengwa/ wawakilishi wakakuambia matatizo? Huwezi kuyamaliza haya matatizo kwa kuja unajifungia kwenye air condition kwa Mkuu wa Mkoa unaenda kuonyeshwa miradi tu iliyofanya vizuri, miradi mibovu hauonyeshwi. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niongee kidogo na Mheshimiwa Waziri. Tunaona kuna zoezi linaendelea kwamba wakandarasi wengi wamelipwa asilimia 80 lakini kazi hazifanyiki. Nataka nikwambie Waziri mtawafunga wakandarasi wote. Hii miradi ya maji ya Benki ya Dunia asilimia 90 ya wakandarasi waliofanya hizo kazi wengi wameuziwa nyumba na wengine wame-paralyze kwa sababu mnawasainisha mikataba ya mabilioni ya hela halafu hela haziendi. Mtu anafanya kazi, amekopa benki bilioni aki- rise certificate ya 500 inakuja baada ya miezi tisa nyingine miaka mitatu, nyumba imeuzwa na pressure anayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini Waziri asiunde Tume ikachunguza hizi hela zinarudi Wizarani kwako. Nataka nikwambie usiposikia ushauri wetu utapambana na maswali bajeti ijayo. Kule Wizarani kwako kuna watu wanacheza na watu wa huko Halmashauri hela zikija zinarudi kwako huko huko. Mimi nimekuwa Meya nafahamu, nimekuwa Mwenyekiti wa Halmashauri nafahamu, makampuni ya ushauri ambayo yanatutia hasara kwenye Halmashauri zetu yako ndani, ni ya watumishi wa Wizara yako na unao. Sasa ni bora ukasikiliza mawazo ya Wabunge ukaunda Tume ikaenda kuchunguza, kama hauwezi umuombe Spika aunde Tume ya Wabunge ikachunguze hili suala tukija bajeti ijayo mzee tusikuulize haya maswali mengi mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namuuliza rafiki yangu Mheshimiwa Waziri na ulipita jimboni kwangu, hivi kweli kitabu kizima cha kurasa 200 na kitu hata shilingi milioni tano hamna kwenye jimbo langu au ni style gani tuitumie kuomba? Jimbo langu mimi asilimia 85 ni ziwa, lakini hatuna maji, kweli Waziri hata kisima kimoja? Labda wengine humu tumekuja kwa bahati mbaya au mtufundishe style ya kuomba ili tuweze kupata angalau hata visima viwili. Mbunge unajadili bajeti nzima ya mabilioni unatoka humu unasifia tu wenzio hata kisima kimoja hamna, kweli Mheshimiwa Waziri? Nisikitike sana lakini nina imani wewe mzee ni msikivu na ni mtani wangu utatekeleza, nadhani utaangalia hata kwenye ukokoukoko huo utupie hata visima vitatu kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusiana na suala la kuongeza shilingi 50 kwenye mafuta. Nashauri kabisa kama walivyoshauri Wabunge wengine, Wabunge wote tuazimie na wewe ufanye kazi ya kubanana na sisi ile shilingi 50 iongezwe. Sisi wengine huku vijijini bado tuna uhitaji mkubwa sana wa maji. Mheshimiwa Waziri nilishawahi kukwambia kwamba kwangu kuna mradi umeshapitwa na Wabunge watatu walionitangulia wa shilingi bilioni 1.2 skimu ya umwagiliaji, mashamba ya watu mmechukua, kutengeneza hamtengenezi, mmeleta shilingi milioni 200 zimeisha kugawana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine Mheshimiwa Waziri Wizara yako hii Wahandisi wa Maji wengi walioko kule Wilayani kwetu siyo Wahandisi wa Maji ni Environmental Engineer ndiyo wanaokuangusha. Jaribu kufanya paranja, ma-engineer wa maji wapo wengi vyuo vikuu vinatoa acheni kufanya upendeleo kuweka watu wasiohusika. Mtu wa mazingira na visima wapi na wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri kwa sababu namheshimu sana nilitaka nichangie tu hapo lakini nikwambie Mheshimiwa Waziri kama alivyosema Mbunge mwenzangu wa Geita unavyosema asilimia za maji zilizoko Geita watu wanatushangaa sisi humu Wabunge ndani. Hebu jaribu uje hata ziara ya kushtukiza uone hizo asilimia unazozitaja kwenye kitabu haziko Geita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko miradi mingi imekwama, Chankorongo na Mharamba kwenye jimbo langu haitekelezeki. Mtu anamaliza mradi wa shilingi bilioni tano anakabidhi wiki moja hautoi maji, lakini ukija wanakuchukua unakaa kwa Mkuu wa Mkoa unateleza na air condition.

Mimi nikuombe sana Mheshimiwa Waziri sihitaji kubishana na wewe mzee wangu, baada ya Bunge hebu njoo mkoani kwangu ufanye ziara, hasa Jimbo la Geita Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, niipongeze Wizara ya Fedha na Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kazi nzuri iliyofanyika leo ambayo Mheshimiwa Rais ameitolea maamuzi pale bandarini. Nawaomba na Waheshimiwa Wabunge wenzangu tuweze kupongeza hatua hiyo ambayo Mheshimiwa Rais ameionesha pale bandarini leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wakati Mheshimiwa Rais anafanya kazi leo bandarini ilikuwa live amesema iletwe amendments tuweze kuweka sheria ya kuwabana watu wasilete raw material ya vyakula kutoka nje ili kuwasaidia wakulima wetu wa ndani. Kwa slogan hii, ndugu yangu Mheshimiwa Tizeba, jirani yangu, umesikiliza michango ya Wabunge na mimi tangu nimekuwa Mbunge, lazima niseme wazi kwa kweli leo kimenuka, si cha kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie kuhusiana na ununuzi wa pamba, mimi natoka maeneo ya pamba na bahati nzuri Mheshimiwa Tizeba tuko jirani. Ukienda Jimbo la Geita hakuna go-down hata moja la chama cha ushirika, jimbo zima na sisi tumewahamasisha wananchi walime na pamba iko nyingi. Hebu nikuulize Waziri mnapoweka haya masharti ya vyama vya ushirika wanunue wanaiweka wapi hii pamba? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati zao hili limeachwa kulimwa tumefanya kazi kubwa sana ya kuwahamasisha wananchi. Naamini hata Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu pengine labda hawakupata taarifa sahihi. Hakuna mtu kwa sasa aliyeupokea huu ushirika, hayupo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushirika ni mzuri tunautaka lakini haujaboreshwa kutoka kule tulikoharibikiwa mpaka tulipo sasa. Ukimwambia leo mwananchi apeleke pamba kwenye ushirika yaani ushirika uwe broker wa wenye pesa? Maana yake mkulima ataenda kuuza siku ya kwanza na kwa hesabu nyepesi tu ni kwamba labda kijiji kimoja kinaweza kuwa na vituo nane mpaka kumi; sasa kituo kimoja kinaweza kununua kilo 200, 500 kwa siku, pamba hiyo haiwezi kuchukuliwa na gari gharama ni kubwa, ili ipatikane tani 10 pengine itachukua siku saba, aliyeuza siku ya kwanza atakuwa na siku saba anasubiri pesa, ni kitu ambacho hakiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata wewe mwenyewe ni shahidi, unazunguka kule unaona hali halisi. Ushirika uliopo sasa hivi ni uleule umejibadilisha kwa maneno, kwamba walewale waliotuibia ikafa Nyanza na SHIRECU mmewarudisha tena, yaani mtu akasimamie ushirika amejaa viraka matakoni halafu tukampe kazi ya kusimamia hela za wananchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unisamehe, lugha yetu Wasukuma Kiswahili kidogo kilitupiga chenga, nafuta maneno hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali na michango ya Waheshimiwa Wabunge mmeiona mliangalie suala hili. Mheshimiwa Waziri kabla hujafika mwisho wa kuhitimisha hoja yako naomba kesho asubuhi uje na kauli ya kuondoa ushirika kwa sasa ili tufanye maandalizi ya kuweka ushirika mwaka ujao. Naamini kila mtu analalamika kwa upande wake, kuna watu wanalalamikia mahindi, mahindi tulishakosea tusiende kukosea na kwenye pamba ambayo sasa iko sokoni. Tusilimbikize tena matatizo ya mahindi tukaweka na pamba tutaua soko hili la wakulima na wakulima hawatakuwa na moyo tena wa kulima kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia suala la bei, tulikubaliana kabisa kwenye kikao kwamba tupunguze hizi kodi na bahati nzuri kwenye ukurasa wa 46, umesema umefuta mfuko wa CDTF, kwa nini tena unaweka Sh.100? Maana yake unatugeuza huku tukiangalia huku unasema tena tulipe Sh.100 ni kwa sababu wakulima wengi hawajui kusoma au hii ni design gani? Kwa hiyo, tunakuomba usimamie suala la bei mkulima afaidike ili mwakani tuwe na pamba nyingi hamtakuwa na shida ya kuagiza mafuta machafu kutoka nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala lingine, Mheshimiwa Waziri wewe mwenyewe ni shahidi sisi tunatoka maeneo ya wananchi waliotuleta hapa, kuna tatizo gani la kuwalipa mawakala? Tatizo ni nini? Uhakiki gani usioisha? Kila mtu analalamikia mawakala na kila mwaka tunazungumza tunaambiwa mnafanya uhakiki. Mheshimiwa Waziri kwenye kuhitimisha tueleze kwamba pesa haipo ili kama Bunge linaweza kuamua kukuombea pesa likuombee pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wamekufa. Usione watu wamefanya biashara ya kuwakopesha wananchi siyo pesa zao wamekopa kwenye taasisi za benki. Watu wameuziwa nyumba, watu wana matatizo huko, vitu vyao vinapigwa minada Serikali ipo tu inaangalia. Mheshimiwa Waziri, bahati nzuri wewe unatoka sehemu ya wakulima wa pamba, rudisha moyo, kama hii kazi ni ngumu, pia kazi ya kukaa huku kuwasaidia Mawaziri kujibu ni nzuri tu unakuja tunakukaribisha huku nyuma. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekti, suala lingine, nawashangaa sana Waheshimiwa Wabunge, yaani mtu anasimama anasema tumekosea sana kununua ndege. Mimi nikiwaangalia ninyi wote si wa kupanda basi, mbona mnazipanda? Kwa hesabu nyepesi tu ya kibiashara lazima uwe na vitu vya kuingiza. Sasa kuhusu suala la ndege, ndege inasaidia kuleta pesa kwenye utalii. Hii kauli kila siku ya kuponda kununua ndege tunataka tuwaone msiwe mnapanda Bombardier muendeshe magari yenu kwenda Dar es Salaam. Haiwezekani mnaponda humu halafu jioni tunadandia wote Bombardier kwenda Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ndiyo teknolojia na nchi inayoendelea lazima iwe na vitu vya kuwawahisha watu wafanye kazi Dar es Salaam, asubuhi tuwe Dodoma kwenye Bunge. Kwa hiyo, mimi nawashangaa sana wote mnaobwabwaja kuzungumzia suala la ndege. Pengine ni suala la wivu ambalo kimsingi Watanzania tunahitaji kulipuuza na tusilisikilize kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nakuomba Mheshimiwa Waziri, Maafsisa Ugani wawe wanaleta mrejesho kama tulivyomuona Rais anawataka Mabalozi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitaunga mkono hoja mpaka atoe majibu ya kueleweka.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwa kuwa leo nimevaa vazi adhimu la Kiislam na pengine nitasema maneno makali kidogo naomba nianze kwa Sala “Audhubillah mina-Shaitwani Rajeem, Bismillah Rahmani Raheem”

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Mpango na Naibu wake na watu wote wanaomsaidia kwenye Ofisi yake. Naomba niseme kwa hisia zangu kwamba yeye ni Waziri wa kwanza toka Serikali zote zianze, Waziri ambaye anapambana na Watanzania kuwabadilisha kuwatoa kwenye kukwepa kodi, kuwapeleka kwenye kulipa kodi. Kwa hiyo, nimwombe na nimshauri asikate tamaa, hii mishale anayopigwa ni moja ya maboresho lakini kazi yake hata Wapinzani wanajua anafanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nimshauri Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mpango, nianze na biashara ya dhahabu. Biashara ya dhahabu ameweka kodi ya asilimia 14 ukichukua makorokoro kuanzia kuchimba mpaka kuuza. Kodi hiyo hiyo anatozwa anayechimba gramu moja, anatozwa na mtu mkubwa kama GGM kodi moja. Ukija kuchunguza wale ambao wanachimba kwa kiasi kidogo, wachimbaji wadogo ni kama wanamtumikia tu yule mkubwa apate faida, sisi tuendele kupata hasara.

Mheshimiwa Spika, tulishawahi kushauri mara nyingi Mheshimiwa Waziri kwamba ukienda nchi kama Uganda wao wana-charge 0.5 kwa wachimbaji wadogo, ukienda Rwanda 0.6, ukija Tanzania 14. Kwa nini Mheshimiwa Waziri asiondoe kodi kwa wachimbaji wadogo ikawa hata zero ili tukapate dhahabu nyingi kwa sababu kui-control dhahabu ni kazi ngumu, dhahabu wengine tunaiokota mashambani, ataidhibiti vipi?

Mheshimiwa Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri kwa nini asiondoe kodi huku kwa wachimbaji wadogo ikawa zero tuwavutie na wengine wauze Tanzania ili sisi tupate tu asilimia moja kwenye export. Mtu anayesafirisha ndiyo amlipe lakini kwa kodi asilimia 14 dhahabu ya milioni 100 unaweza ukapata faida ya milioni 2,500,000, unataka mimi nikalipe bei gani? Lazima nikwepe. Kwa hiyo, nimshauri sana Mheshimiwa Dkt. Mpango aliangalie hilo.

Mheshimiwa Spika, lingine ni kuhusiana na mikopo ya halmashauri, nilikuwa napiga hesabu kwenye halmashauri yangu ni kama Mbunge wa nane. Ukipiga hesabu ya ambazo tumekopesha tuna karibu bilioni mbili toka tuanze Ubunge pale, lakini hizi hela hazina ufuatiliaji. Kwa nini Mheshimiwa Dkt. Mpango Waziri asizigeuze hizi halmashauri zikawa na Taasisi, tunapokopesha zile hela tuwe na taasisi kabisa, tuna karibu bilioni mbili Geita, ingekuwa ni benki tayari iliyokuwa na sifa ya kukopesha ikawa na commitment ya kuwadai wakulima, lakini sasa kila mwaka tunakopesha, hakuna mtu anayedai, tukikopesha hela hakuna mtu anayedai, pesa zinakwenda na hazina mfuatiliaji. Ukimweka Afisa Ushirika kufuatilia akienda kule na yeye anaomba kuku tu na mkaa. Kwa hiyo, nashauri tujaribu kubadilisha taswira hii tuangalie kama hizi halmashauri tunaweza tukazigeuza zikawa ule mkopo wake tunaotoa kwa wakulima kuwe na Taasisi ya kuweza kudai kabisa zile pesa na yenye commitment na kazi hiyo peke yake.

Mheshimiwa Spika, suala lingine Mheshimiwa Dkt. Mpango; naona kuna Benki ya Wakulima, ndugu zangu Wabunge hii Benki ya Wakulima tunawapelekea matapeli tu, hakuna mkulima ana-qualify kukopa kwenye zile Benki hayupo, wala mkulima wa kijijini hahitaji kukopa bilioni moja sana sana wanakopa laki mbili, hakuna sifa za kuwakopesha wakulima na ndiyo maana nikaona tujaribu kubadilisha haya mazingira tuwe na benki zinazoendeshwa na halmashauri zenyewe kutokana na hizi pesa tulizokwishazikopesha.

Mheshimiwa Spika, lingine, ni suala la makinikia, wazo la Serikali ni zuri sana, kwanza sisi tunaotoka kwenye dhahabu tunaona kama ni neema Mungu ametuletea, lakini naomba nishauri mfanyabiashara wa Tanzania siyo adui na sisi tumo humu kwa ajili ya kutetea watu wetu.

Mheshimiwa Spika, niliona Mheshimiwa Waziri wa Madini alitoa kauli akasema “kuanzia kesho hakuna kusafirisha carbon”, Mheshimiwa Waziri anaongoza Taasisi za fedha; hawa walio na illusion plant kule kijijini, kule Mwanza na sehemu zingine, nataka niseme hapa kama yuko mtu atanibishia wote ni darasa la saba, lakini wamekopa benki na benki zinataka marejesho ukiawaambia leo wote mrudi Geita wengine Singida kuna changamoto. Mwingine unakuta siku hiyo ndiyo mwezi wake wa kulipa marejesho, carbon imezuiwa kusafiri.

Mheshimiwa Spika, mwingine amekopeshwa na yule aliye na illusion kule Mwanza, jinsi ya kukusanya ile hela ni kazi, hata unapomwambia kesho arudi kule anapokwenda tena mfano mmoja tu ni Geita; maeneo wanayopewa wale wenye plant kuhamisha kujenga hakuna umeme, hakuna barabara, inachukua miezi miwili. Mtu anapigwa interest za benki, kwanini tunawaona wafanyabiashara kama maadui?

Mheshimiwa Spika, nimshauri Mheshimiwa Dkt. Mpango, maamuzi mengine haya tuwe tunayapa muda, mimi sikatai wazo na watu tumelipokea vizuri, lakini tungesema basi kwamba tunawapa siku 60 au 40 ili muweze kujiandaa kuhamisha mashine zenu hakuna mtu ambaye angelalamika kwa sababu hata wakati wanakwenda kujenga huko walikokuwa ni Taasisi za Serikali zilitoa vibali na kukubali watu wawekeze, kwa nini tunakuwa tuna vigeugeu?

Mheshimiwa Spika, suala lingine, mara nyingi najiita Chief watu wanadharau, haya maneno yaliyotokea jana nilizungumza mwanzo kwamba mimi na abiria wangu tulikamatwa na samaki piece tatu, kwenye basi tukaombwa ruler, hamkujua? Sasa jana ruler Bungeni, lakini niseme tu ukweli kutoka moyoni mimi kama Chief kwa mara ya kwanza leo nimeamini Wagogo, watani zangu kumbe wana akili kubwa sana. Ulichokifanya Mheshimiwa Spika kusamehe na kusema ukichukizwa unasamehe Waziri ajitafakari! Hilo ni neno kubwa bora hata ungechukua hatua nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hilo neno la kwamba mtu amekuudhi kwa hatua ile halafu unakaa kimya, Wizara hii tumekuwa na Mawaziri nakumbuka watano tena wote Madokta, Mheshimiwa Rais wangu, Dkt. Magufuli, Dkt. Mathayo, Dkt. Kamani, Dkt. Tizeba wote hawa walifanya kazi yao nzuri na uvuvi haramu walikuwa wanapambana nao kwa style yao kama viongozi, leo tumeleta Mgambo sijui shule za design gani hizikila siku huwa nashangaa, lazima tufike mahali tuchukie. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, huwa nasema kila siku ni vizuri tukakaguliwa vyeti, watu wana elimu za kuunga unga unamkabidhi Taifa kama hili tutakufa. Sasa hebu jiulize, yeye mwenyewe anakiri anasema mimi niliamua kuwaita ili tutekeleze zoezi la operation, yeye ndiyo mtunga sheria? Hajui Sheria za Bunge jinsi ya ku-arrest Bunge? Anazijua kabisa anaamua kukiuka kwa kutafuta kick na huu Urais utakuja kuwatokea puani. Hata sisi Wasukuma tumelia na tumelalamika tulipokosa msaada, tumefanya ulichokifanya wewe. Tumeamua kunyamaza na kumuachia Mungu apambane naye. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kumteua Waziri wa Madini, dada yangu Mheshimiwa Angellah na kuwateua mapacha, vijana wazuri na namwomba sana dada yangu Mheshimiwa Angellah awalee hawa vijana, najua yeye ni senior kwao na tunaona kazi wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niliwahi kusema humu Bungeni ni vizuri sana Waheshimiwa Wabunge, kila mtu ana neema tofauti, ni vizuri sana ukajikita kwenye neema ambayo iko kwenye Jimbo lako kulikoni kuja kuropoka vitu ambavyo huna takwimu na huvielewi na haviwasaidii Watanzania wanaoumia na sekta ya madini. Nimesikia mchangiaji mmoja hapa anaropoka vitu ambavyo ni tofauti kabisa. Ukiangalia Wizara hii kwa sasa na zamani tulivyokuwa tunalalamika, acha Wabunge wananchi tunaowawakilisha, ni tofauti kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna watu humu ndani wana vitu ambavyo wanaweza kuzungumza wakati Wizara ya Miundombinu ilikuwa hapa, Mbunge mmoja tu nataka nimwambie, angeweza kuchangia kwa nguvu kubwa kwa sababu yeye ana fly over ya ghorofa. Kuna Wizara ya Maliasili ni vizuri sana mtu anayemiliki mbuga za wanyama Serengeti akajikita kuchangia kwenye Serengeti kusaidia watu wake kulikoni kuja kupotosha watu. Mtu anamiliki flyover anakuja kuchangia mambo ya dhahabu, anapotosha wananchi na hatusaidii watu ambao tumeumia na sekta hii ya madini. Nadhani wamejielewa watu ninaowazungumza, hiyo ni preamble, sasa naenda kuchangia. (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo siyo taarifa wala siipokei. Hawa ndiyo wasomi tunaowategemea, huyo ni Mwalimu, ndiyo maana huwa nalalamika kila siku tuchunguze vyeti. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchangia sasa kwenye agenda halisi za Wizara ya Madini. Watu wa Geita tumekuwa tukilalamika muda mrefu kuhusiana na Mgodi wa GGM na kumekuwa na kutokuelewana. Kwa vile Wizara na dada yangu Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake ni wasikivu, mje mkae na Madiwani wa Halmashauri za Geita kwa kina, siyo kwa harakaharaka siku moja, mtusikilize mtoe maamuzi ili hili suala la kudaiana kati ya wananchi wa Geita na Mgodi liweze kuisha. Mnavyokuja tu mna-rush, mnatuma barua, hawa watu hawatusikilizi, ndiyo maana tunafika mpaka mahali tunasema tijichukulie sheria mkononi, siyo vizuri, namshauri sana Mheshimiwa Waziri hebu atafute muda aje atusikilize na aweze kufikia mwisho wa kulimaliza suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, sijui huu mgodi au sisi watu wa Geita tuna tatizo gani? Tulilalamika kuhusu tanzanite, Mheshimiwa Spika akaunda Tume. Kumekuwa na Tume ya Makinikia, watu wa Geita tumeomba mara nyingi kwa nini isiundwe Tume kwa ajili ya kuuchunguza Mgodi wa Geita GGM? Kwa bahati nzuri Mheshimiwa Rais ameshawapa tu mwongozo kwamba muangalie, mgodi ule ulikuwa unatoa dhahabu bila kuchunguzwa, sasa hivi tunaingia mpaka Halmashauri kuna tofauti kubwa, muanzie hapa ili muweze kuunda Tume.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine wako watu ambao wamekutwa na leseni ya mgodi, Mheshimiwa Kanyasu jana alizungumza vizuri. Wameenda Mahakamani, wamehukumiwa tarehe 19 Desemba, 2016, tarehe 20 baada ya hukumu ya Majaji sita, mgodi ukaandika tena warning ya kuwatoa wachimbaji wale. Jana Mheshimiwa Kanyasu alivyochangia tu, leo ninayo barua hapa jana mgodi unaandika kuwafukuza watu ndani ya eneo lao ambalo Majaji sita wamewapa haki ya kukaa pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wabunge tuna haki ya kutetea watu wetu, Mheshimiwa Kanyasu amechangia jana leo kuna barua ya kuwafukuza, siku saba. Najua GGM wako hapa, Mheshimiwa Waziri akija hapa nataka atuambie kama GGM ni zaidi ya Serikali na ni zaidi ya mhimili wa Majaji sita tuelewe, lakini kama si sahihi basi naomba Mheshimiwa Waziri achukue hatua ya kuweza kuwasaidia watu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mhimili ambao tunautegemea baada ya Serikali na Bunge kushindana ni Mahakama. Kama Mahakama ya Majaji sita, tena Majaji wanaoaminika Tanzania wametoa hukumu ya kuwapa haki wananchi hawa, inatokeaje mtu mmoja tu GGM anatoa siku saba kuwafukuza watu baada ya Mbunge kuchangia, hii ni dharau. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri alifanyie kazi na ana vijana shapu wanaweza kwenda hata kwa basi kusikiliza kesi hizi. Namwomba sana aende akatoe maamuzi kwenye hili suala hapa.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni Mgodi wa Buhemba, niombe sana Mheshimiwa Waziri katika vitu ambavyo tutakosea ni kuangusha wawekezaji wawili ambao mimi kama mfanyabiasha wa hiyo dhahabu, Mgodi wa Baraka na Mgodi wa Mauza, watu hawa tukifika mahali tukawafanya wakafilisika hatutakaa tupate mwekezaji Mtanzania atakayeweza kufanya kazi ya dhahabu. Sisi kama Kamati tumeenda tumeona, sawa kulikuwa na mwingiliano wa Jeshi lakini nataka niwaambie tu kwamba mazungumzo kama yanaendelea vizuri, ni vizuri tukawasaidia hawa watu wamewekeza zaidi ya dola milioni 25. Mtanzania wa kawaida amekopa, anaumiza kichwa tena darasa la saba, kitu ambacho hata watu wenye ma-degree wanaoropokaropoka humu hawawezi kufanya hivyo vitu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri tusije tukafanya hiyo dhambi ya kuwaangusha hawa wawekezaji wazawa. Hata kama kulikuwa na makosa kwenye Wizara ya Madini na Wizara ya Ulinzi kaeni mmalize migogoro yenu watu hawa wapewe leseni waweze kuendelea na shughuli zao. Hata kama leseni inachukua process ndefu kuna njia nyingine mnayoweza kuitumia ili aweze ku-cover hayo mambo aliyonayo. Hawa watu wanadaiwa na mabenki, tukiwa-ignore hawa hamtamkuza Mtanzania yeyote kwenye biashara hii ya dhahabu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka kutoa ushauri…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja lakini dada yangu kwenye shilingi ujaribu kuja na majibu mazuri naweza nikaondoka nayo. (Kicheko)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia.
Napenda nianze kwa kuzipongeza sana Kamati zote mbili, lakini nitachangia pande zote mbili nataka nianze na uvuvi. Tuliwahi kulalamika sana wakati wa operesheni lakini tukafika mahali tukakubaliana na Mheshimiwa Waziri na tukaamua kumuunga mkono na zoezi la wavuvi haramu kwa kiasi fulani limepungua.

Mheshimiwa Spika, sasa baada ya kutoka kwenye ule uvuvi ambao Mheshimiwa Waziri alikuwa anaukataa, hata huu uvuvi tulionao tena kuna tatizo kubwa. Sasa hivi kwenye ziwa Wizara imeweka masharti kwamba unavua mwisho sentimita 50 mpaka 85, lakini mitego ile ambayo Wizara ilipendekeza ukiitupa kwenye maji inavua mpaka sentimita 100 na kuendelea, sasa inaonekana tena mtu akivua sentimita 86 na lenyewe ni tatizo anatakiwa kuadhibiwa na kutozwa faini ya mamilioni. Sasa tunashindwa kuelewa, labda leo Mheshimiwa Waziri atakaposimama aniambie kwamba hiyo mitego uliyotaka tuitumie tutumie njia gani tukiitupa kule ndani isichukue zile sentimita 86 iwe inabagua zile unazozitaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama hiyo haitoshi siyo kwamba haya masharti uliyoweka watu hawavui, nataka nikwambie Waziri Mpina umeongeza magendo makubwa kwenye ziwa letu. Hii mitego unapoitupa kule kwenye maji wanapopata wale samaki wakubwa ambao wewe huwataki na wanashikwa na mitego yako, soko lake kubwa liko Uganda na Kenya. Hata viwanda vyetu vya sasa vilivyoko huku Kanda ya Ziwa hawakubali kupokea samaki anayezidi sentimita 85, kwa hiyo, watu wanawapata wale samaki wanapeleka kwenda kuuza Uganda.

Mheshimiwa Spika, tatizo lingine hata kwenye soko la kimataifa samaki wetu wamekosa soko. Wewe ni shahidi kwenye viwanda imejaa minofu haisafirishwi kwa sababu minofu yetu ni ya samaki wachanga, wale samaki wenye afya njema wako Uganda na Kenya ndiyo wamechukua soko hilo.

Mheshimiwa Spika, nimwombe Waziri, pengine una utaalam wa kuweza kuwaelewesha wavuvi wetu kwamba mitego uliyotupa wewe mwenyewe inashika sentimita kubwa hukutaka tushike sentimita ndogo, tatizo tena limekuja kwenye sentimita kubwa. Nikushauri sana Mheshimiwa Waziri utakapokuja hapa utueleze.

Mheshimiwa Spika, lakini pia Waziri umeharibu biashara ya bondo. Wewe mwenyewe unafahamu unaposhika samaki mwenye bondo kubwa na soko lake ni kubwa. Wachina ambao walikuwa wananunua mabondo ya Tanzania sasa wamehamia Uganda na Kenya, nadhani ukija hapa utatoa ufafanuzi ili tuweze kukuelewa.

Mheshimiwa Spika, lakini suala la pili niliwahi kusema hapa mpaka nikatoa machozi kuhusiana na suala la ufugaji Mheshimiwa Maghembe akiwa Waziri. Nashangaa sana mtu ambaye hatampongeza Mheshimiwa Rais, labda wale wanaokaa mijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama mnakumbuka vizuri nilisema kuna watu humu wanafuga mbwa na nyanya, hawawezi kuona thamani ya mashamba kwa sababu vitu vinakaa kwenye mazingira ya binadamu. Kwa hiyo, nataka niseme hivi kwa mtu yeyote anayetoka jamii ya wafugaji, anayetoka vijijini asipompongeza Mheshimiwa Rais kwenye hili suala la kuruhusu watu wamegewe maeneo ni mtu wa ajabu na Watanzania mnaotutizama kwenye TV hawa ndiyo Wabunge wenu wanakaa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwenye kazi nzuri aliyoifanya, lakini sisi tunaotoka vijijini tunasema Mheshimiwa Rais tunakupongeza sana na ndiyo kilikuwa kilio cha wanyonge unaowatetea na ikiwezekana endelea na maeneo na mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, linguine ni suala la wakulima. Sisi tunaotoka kwenye jamii ya wakulima yako matatizo mengi sana ya mbolea. Unaweza ukakuta sasa hivi wakati wa kupanda mbolea inakuja mwezi Juni au Novemba wakati mnavuna. Mimi najiuliza Mheshimiwa Rais mimi namhurumia wakati mwingine atapasuka hata kichwa. Wakati akipokea Taarifa ya CAG mwaka jana alizungumza akaielekeza Wizara msiagize mbolea ya nje chukueni Minjigu, Minjingu godown zimejaa mbolea hamnunui. Mbolea ya kupandia inakuja wakati wa kuvuna mbolea ya kuvuna inakuja wakati tumeshamaliza hata kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa napenda Waziri akija hapa atuambie na bahati nzuri Mheshimiwa Rais alikuwa live wakati akielekeza Wizara kwamba lazima mkanunue mbolea ya Minjingu kwa sababu mbolea ya Minjingu ni ninyi wenyewe mmeipima mkaiona inafaa na mkatoa TBS. Utaalam wenu wenyewe tena mnaona kama haifai mnaenda kuagiza mbolea ya nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ukiangalia kwenye hii mbolea, mimi ni mkulima ndiyo maana nalalamika, ukienda Kenya, Uganda na Burundi wao hawaagizi mbolea ya nje wanaagiza mbolea ya Minjingu ambayo sisi tunaiona haifai. Sisi tunang’ang’ana kuagiza nje huku tunasema Serikali ya Viwanda. Jamani naomba Waheshimiwa Mawaziri husika mkija hapa mnipe majibu na sisi tunataka kumuunga mkono Mheshimiwa Rais kweli anachokitaka kifanyike kutengeneza viwanda vyetu vya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesikia watu wakilalamika hapa kuhusiana na suala la mashamba. Bado nazungumza tu yaleyale, unajua watu tunapishana kuna watu wanatoka mijini, kuna ghorofa, wengine wanakaa juu, wengine ghorofa ya tatu, sisi ambao tunakaa plot kwa plot hakuna mtu atawasikiliza na mnajipaka nuksi, watu wakiwasikia mnang’ang’ana mashamba yarudi kwa mabepari hiki kitu Watanzania hawakikubali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niseme mimi ni mwana CCM mzuri nilikuwa Mwenyekiti. Ukisoma ukurasa wa 41 kwenye Ilani ya CCM, kifungu cha 6 kuna baadhi ya watu humu, wana CCM wenzangu wanapiga midomo kwamba tutetee mashamba, wao ndiyo walikuwa viongozi na ndiyo walioanza kuisemea Ilani hii ikiielekeza kwamba tutakapochukua Serikali tuangalie mashamba makubwa tuyafute tuyapeleke kwa wananchi, leo tena wamegeuka ya kwao yaleyale wameyageuza tena.

T A A R I F A

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, naikubali hiyo taarifa. Tunataka Wabunge wazalendo kama hawa wanaoijua vizuri Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilichokuwa nasema ni Ilani ambayo imeelekeza haya yafanyike Serikalini. Nami nataka niwape moyo wanaosimamia hizi sheria, Waziri Lukuvi na wenzio futeni mashamba, futa, yaani hata yale mengine futa. Haiwezekani watu wanachukua hati wanaenda kukopea nje ya nchi wanapata hela wanaenda kuwekeza Dubai sisi tunaachiwa mapori huku. Naomba wale wanaosimamia Wizara hii futeni wala msiogope. Najua yatakuja maneno ya kusema mmehongwa, mmepewa rushwa, ukiwa unatekeleza sheria kuhongwa ni maneno ya kukukatisha tamaa, futa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia. Kwanza kabisa naunga mkono taarifa za Kamati zote mbili. Pili, nimpongeze sana Mheshimiwa Profesa Kabudi kwa uchapaji kazi na usimamizi wake wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya wanaotambua na kuthamini kazi anazofanya na Geita nadhani ni namba moja. Ukiangalia Geita ya leo na Geita ya mwaka mmoja tu uliopita kabla ya yeye kuamua kutekeleza sheria na kuisimamia ni vitu viwili tofauti. Wengine hata tukiona wanavyomshambulia, tunaumia sana, lakini tunaomba aendelee kukaza buti kwa sababu msimamo wake ndiyo unaofanya hawa watu wapige kelele humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, sisi tunaotoka vijijini tunaishukuru sana Serikali pamoja na Wizara. Mheshimiwa Kabudi, Mahakama inayotembea ni suluhisho kubwa sana kwa watu wa vijijini. Ukienda Jimbo la Geita Vijijini lenye watu takribani 600,000 lina Mahakama moja tu ya Mwanzo na yenyewe inapatikana pengine kilometa 150 ndiyo unaiona Mahakama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaishukuru sana Serikali. Ombi letu ni kwamba sasa Mheshimiwa Kabudi tumeona mmezindua juzi, tunatarajia baada ya muda mfupi, tutayaona haya magari yanakuja huko vijijini kuanza kuchapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, nilishauri Bunge lililopita kwamba makosa mengi, ukienda kwenye Magereza kuna mlundikano wa wafungwa na mahabusu lakini watu wengine wana makosa tu ya kuiba kuku. Watu wengine wana makosa ya kukamatwa uzururaji, hata faini yake pengine inakuwa shilingi 100,000/= lakini ameshakula ugali zaidi miaka miwili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Kabudi kwa uchapaji wake kazi hebu aangalie namna anavyoweza kufanya, makosa mengine tuwe tunamalizana nayo hata kwa viboko watu waendelee kuchapa kazi huko mitaani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, sisi Wabunge ndio tunaotunga sheria. Pamoja na minyukano inayokuwa humu ndani, lakini sisi ndio tunaotunga sheria. Kwa hiyo, sheria inapotekelezwa, tusidhani tunapopitisha sheria, tunapitishia mbwa; tunapitishia binadamu tukiwemo na Wabunge. Kwa hiyo sometimes sheria inapotulenga sisi, lazima tukubali kutii sheria bila shuruti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikia watu wengi wanasema; na bahati mbaya rafiki zetu wakizungumza, wanawahi Canteen hawamo humu ndani. Amezungumza Mheshimiwa Lema hapa, anasema alitekwa Makuyuni. Hivi mtu anatekwa halafu anapelekwa Kituo cha Polisi? Hicho ni kitu cha uhuni. Mimi mwenyewe nilikamatwa, siwezi kusema nilitekwa. Unakamatwa, unapelekwa Kituoni, unamaliza shida zako, unaachiwa. Ndiyo maana leo Mheshimiwa Lema yumo humu Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitoa mwongozo wangu jana kwa Mheshimiwa Spika kuhusiana na suala la Mheshimiwa Tundu Lissu. Nimeona mitandaoni wananitukana, wananichamba, lakini sishangai. Bahati nzuri wengine tunaongea nao huko. Hili suala nililolizungumza jana kuna watu wanalifurahia kwa sababu michango inawaua na hawana kitu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili naomba nizungumze, katika Bunge hili hakuna mtu ambaye hatarajii kuugua; hata sisi, hata yeyote. Tunatambua kabisa kwamba Mheshimiwa Tundu Lissu alipata matatizo. Wengine tunaomba kimya kimya, siyo lazima wote tupayuke kama nyie. Tumekuja kushtuka, mtu tunayemwombea ni mcheza sinema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi toka nimekuwa Bungeni hapa, hatujawahi kukaa Bungeni zaidi ya masaa matano tuna-break, tunarudi masaa matano, tunaahirisha Bunge. Naomba niwaambie kwa sababu tunazunguka zunguka na sisi ni wazima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukichukua kutoka alikokuwa anatibiwa Mheshimiwa Tundu Lissu, ziara yake ya kwanza ameenda Uingereza. Kutoka Ubelgiji kwenda Uingereza ni masaa manne kwenye Ndege. Huyo ni mgonjwa. Kutoka Uingereza kwenda Marekani ni masaa 10 mpaka 11, huyo ni mgonjwa. Haya, kutoka Marekani kwenda Ujerumani, ni zaidi ya masaa 14, huyu mtu anaitwa mgonjwa, haiwezekani. Hili lazima tuungane mkono. Nanyi mnaomtetea, nataka niwaambie ukweli, pamoja na ….

T A A R I F A

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nilichokuwa nakisema; na wenzangu Waheshimiwa Wabunge na wananchi wa Singida Mashariki walichagua Mbunge na wao ni wamoja wa watu ambao wanamwombea Mbunge wao apone, hawakuchagua mtu wa kula bata, wanayemwona kwenye TV na magazeti kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachokisema hapa, sheria tulizitunga wenyewe. Nashangaa sana na Bunge lako, kwa nini hatutekelezi matakwa ya kanuni? Kama mtu amepona anaweza kusafiri masaa yote na kukaa kwenye hotuba kutukana Taifa...

T A A R I F A

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ndugu yangu Mheshimiwa Mwakajoka, najua wewe Timu Tundu Lissu, unadhani anakuona ili akupitishe jina. Ninakuomba utulie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nasema, wananchi wa Singida Mashariki hawana mwakilishi; na sheria inatutaka mtu akiwa mzima, asipohudhuria vikao vitatu, kuna hatua ya kuchukua na mliitunga wenyewe, inasubiri kutekelezwa wakati gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wasichukue point hapa. Humu humu ndani tunao Wabunge wenzetu wanaumwa, wala hamna mtu anawajadili. Tunaye Mheshimiwa Mkono…

T A A R I F A

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ninachokisema hapa, ni vizuri Mheshimiwa Spika akachukua hatua ya kuweza kutengua uteuzi wake ili wananchi wa Singida Mashariki waweze kupata mwakilishi wasiwe na mwakilishi anayewawakilisha kwenye TV.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri, tunao watu wanaumwa hapa, lakini kwa sababu wananchi wao wamewatuma kufanya kazi, tunaye Mbunge wa Singida Magharibi hapa Manyoni, ni mgonjwa, anakuja na gongo lake humu ndani; tunaye Mheshimiwa Ridhiwani, tunao watu kibao. Hhaiwezekani mtu anayeweza kukaa kwenye ndege masaa 14 halafu akaachwa tukaendelea kumwona anakula mshanara. Watanzania wanatupima na wanatuona.

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumpongeza sana Waziri Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe kwa hotuba yake nzuri na pia taarifa ya Kamati. Nimwambie Mheshimiwa Waziri na Wizara yake wamefanya vizuri sana kwenye tasnia ya muziki. Watanzania wengi tunawaelewa na tunaamini mnawasimamia vizuri vijana na tunapata burudani za kutosha ikiwemo na hii aliyomaliza kuitoa msanii mkubwa nguli Sugu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitazungumzia sana kipande cha wasanii kwa sababu nimejaribu kumsikiliza Mheshimiwa Sugu kama msanii mkubwa nilitegemea atazungumza matatizo makubwa ya wasanii badala yake Mheshimiwa Sugu leo kageuka kuwa mwanasheria kuzungumzia mambo ya magazeti na vitu vingine.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, wasanii wa muziki kwa nini wanafanikiwa? Wanafanikiwa kwa sababu hawategemei kuuza filamu, wanapotoa nyimbo zao wanachokitegemea wao ni kufanya matamasha na kukodiwa na kuchukua viingilio. Ni lazima Wizara ione huruma kwenye tasnia ya filamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa najaribu kuangalia kwenye kitabu hiki mipango ya Bodi ya Filamu siamini kama watu waliotengeneza hiki kitabu ni hawa wanaosimamia tasnia ya filamu. Tasnia ya filamu iko hoi bin taaban na ndiyo maana unakuta wasanii wetu wa Bongo Movie hawana kitu, sasa hivi wanategemea misiba wapate michango na kufungua madanguro na kuwa makuadi kwa wanaume. Wako hoi bin taaban, kwa nini? Tumeruhusu vitu vya kijinga ambavyo vimekuja kuuwa kabisa tasnia ya filamu na filamu ndiyo sehemu kubwa ambayo sisi Watanzania ilikuwa inatupa mafunzo ya utamaduni wetu wa kitanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii kuna filamu inaitwa Sultan hakuna Mtanzania ambaye haiangalii na mbaya zaidi imetafsiriwa Kiswahili. Hivi ni nani anaweza kwenda kumuangalia Marehemu Majuto akaacha kwenda kuangalia Sultan? Tunapata faida gani kwenda kuzungumza mambo ya Waturuki tunaacha kukuza utamaduni wetu wa ndani? Hakuna Mtanzania anayeangalia Bongo Movie leo hayupo na hawa hawa watu wanaotafsiri Kiswahili ni wasanii wanatulipa nini kama Serikali? Kwa hiyo, nimwombe Waziri anusuru wasanii wa Tanzania wanamfia mikononi mwake.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine ukitengeneza filamu ya Kibongo ina ukaguzi zaidi ya 1,000 lakini zikija filamu za Kikorea hakuna ukaguzi, nani atakayeenda kuangalia sinema ambayo mmewaambia Watanzania wavae madera na kanzu wakati filamu za Kikorea watu wamepiga miniskirt lazima watu wataenda kwenye miniskirt. Kwa hiyo, niombe sana kama tunaweka ukaguzi wa filamu lazima na filamu zinazotoka nje zikaguliwe ziendane na maadili yetu ya Kitanzania otherwise wasanii wetu wa Kitanzania wote tunaenda kuwapoteza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitengeneza filamu ya Tanzania unapoitoa inabidi ulipe kodi, mfano iwe shilingi milioni moja na mwakani lazima uilipie shilingi milioni 1, hii kitu siyo sawa. Filamu inaangaliwa mara moja inachuja lakini wewe unamweka kwenye library yako kumtoza shilingi milioni moja kila mwaka. Wasanii wetu wamekata tamaa na Mheshimiwa Waziri naomba sana uitumie kauli ya Mheshimiwa Rais kwamba chukua maamuzi ya kusafisha hiyo Bodi ya Filamu, wametuulia filamu yetu ya Kibongo na ukitaka nikutajie hata majina ya wanaouwa nitakueleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wako vinara Tanzania Bodi ya Filamu inawafahamu wako Kariakoo, hawa watu wanaleta makontena na makontena ya dublicate kazi za Watanzania. Hata Waziri unawafahamu ukitaka nikutajie kwa ruhusa yako nakutajia. Hawakamatiki, wanatengeneza dublicate ya kazi za Kitanzania wanazileta kama export wanazipeleka Kongo na Kenya. Ukifika Kongo leo filamu ya Tanzania inauzwashilingi 500, hivi ni nani atakayeweza kufanya kazi ya kutengeneza filamu hapa Tanzania? Makontena yanaingia kutoka Korea, China na wanaoyaleta wanafahamika. Hata wakikamatwa na hizo dublicate faini yake ni shilingi milioni tano, mtu ana mzigo wa bilioni kumi na makontena yake anarudishiwa. Ni nani atakayeangalia kazi za wasanii wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wewe unatokana na CCM hawa wasanii ni watu wakubwa sana kuanzia mwaka huu mwezi Novemba kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa tutawatumia, mwakani tutawatumia, tusipowasaidia hawa wakipotea tutakuja kuchaguana watu wenye sauti nzuri humu tutageuka wasanii na kufurahisha kwenye majukwaa wakati wa uchaguzi. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, mimi nalalamika na wewe na nakueleza vizuri kwamba shughulika na wasanii wa Bongo Movie wamepotea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii ukiingia Sinza madanguro makubwa yote ni ya wasanii. Ukitokea msiba, watu wanaokwenda kusimamia michango ni wasanii angalau wapige ganji wapate kitu. Nakuomba sana Mheshimiwa Waziri, usiopochukua hatua kwenye hili, nami natarajia kuja kushika shilingi, uhakikishe kwamba unanifuata hapa tuongee unieleweshe vizuri vinginevyo nitalia na wewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya yanayozungumzwa humu tunakoelekea yatatokea tu, kwa sababu hakuna cha kuzungumza. Sera ya Chama cha Upinzani ilikuwa ni kukosoa; na kweli walikuwa na sababu za msingi, mimi nilikuwa shabiki wao kuwaangalia. Walikuwa wanasema Tanzania hatuna ndege; haya mambo yametengenezwa yote. Sasa hawana cha kuzungumza. Mbunge anasimama anakwambia unaenda na ving’ora. Hiyo ndiyo kazi wamemtuma watu wa Mbeya, wala tusishangae, hakuna kitu cha kuzungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu anasimama hapa kwa mujibu wa kitabu chetu tumegaiwa hapa, unamwambia badilisha, anasusa kusoma taarifa nzima ya Kambi ya Upinzani, halafu na wenyewe wanampigia makofi. Naamini ukitamka neno baya kwa mwenzio, utegemee linakurudi wewe. Humu ndani tuliitwa mboyoyo, lakini tumeona leo mboyoyo ni nani; mtu anaacha kusoma taarifa ya Kambi ya Upinzani, watu wanampigia makofi. Kwa hiyo, mboyoyo wanaeleweka kwenye hili Bunge. (Makofi)

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia. Naomba nianze kwa kuipongeza sana Wizara. Nampongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wengine kwa kazi nzuri kwa kweli ambayo tunaona mnaifanya. Hata ukiangalia michango ya Waheshimiwa Wabunge toka nimekuwa Mbunge kwenye Wizara ya Maji kipindi cha bajeti, kidogo hii bajeti ya 2019/ 2020 imejikita kushauri Wizara iweze kuboresha yale ambayo hayakukaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naipongeza Wizara kwa kutusaidia mradi mkubwa wa maji pale Geita Mjini. Nilichokuwa naiomba tu Wizara, ijaribu kuangalia, kwa sababu huu mradi sehemu unapowekwa, lile tanki kubwa likiwekwa vizuri linaweza kumaliza kabisa matatizo ya maji Geita Vijijini na Geita Mjini. Kwa hiyo, ni vizuri upembuzi yakinifu ukafanyika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine, huwa napata taabu sana, najiuliza sijui watu wengine huwa wanafanyaje; nimejaribu kuona Wizara ya TAMISEMI kwa Mheshimiwa Jafo, imeanzisha TARURA; pamoja na changamoto ilizonazo, lakini kiukweli tunaanza kuona mabadiliko yanayofanyika kule vijijini. Najaribu kuangalia hata Wizara ya Afya, Mheshimiwa Ummy amefanya vizuri sana. Tumejenga hospitali, zahanati, vituo vya afya, magari, kila mtu kiukweli tunaona kazi zinafanyika. Tatizo, najiuliza huku kwenye Wizara ya Maji kuna mchawi gani?

Mheshimiwa Waziri, lazima tukueleze ukweli. Mheshimiwa Rais anapozunguka kila siku anakueleza kuna wezi, hushughuliki nao; anakueleza, Wizara imeoza, hushughuliki nao; Waheshimiwa Wabunge humu, nimemsikia ndugu yangu Mheshimiwa Keissy jana amesema kuna mwizi kaiba, haushughuliki nao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mawazo yangu naomba nitoe ushauri wangu, hata kama tungeongeza shilingi 200/=, hii Wizara ina wezi, zitaenda kuliwa. Ukimsimamisha kila Mbunge humu ndani, kila atakayesimama ana mradi wa maji lakini umepigwa; kila anayesimama humu, atasema mimi nina mradi, lakini umepigwa.

Mheshimiwa Spika, tulikuwa na mradi wa Chankolongo kwa dada yangu Mheshimiwa Lolesia toka mwaka 1978, umekamilika mwaka huu. Tuna mradi kwa Mheshimiwa Hussein Nassor Nyang’hwale, umepigwa mabilioni, umekamilika term hii. Kila Mbunge atakayesimama hapa ana mradi lakini umeibiwa. Sasa ninachouliza Waheshimiwa Wabunge tunataka kubebesha mzigo wananchi wetu mara kwenye simu, mara kwenye mafuta, tukaongeze hela kwa watu wanaotuibia hela, haiwezekani. Hayo ni mawazo yangu, haiwezekani. Tutafute kwanza mchawi wa hii Wizara. Profesa fukuza wezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli tuseme tu wazi, alifumua Mainjinia nchi nzima. Leo TANROADS imesimama, ilikuwa na wapigaji. Sasa wewe kila siku Mheshimiwa Rais akienda huko, kisima; jana nilikuwa naangalia kwenye TV, Mheshimiwa Rais kasimamishwa huko aliko Mbeya watu wanalalamika kisima kimechimbwa kwa shilingi milioni 475. Kuna Mkurugenzi, kuna engineer na ziara mnaenda.

Mheshimiwa Spika, nashauri Waheshimiwa Wabunge, tusijaribu kuongeza hela, hizi hela ni nyingi sana. Tusijaribu kabisa. Kama tumetumia leo shilingi bilioni 300 na kitu, hii kitu haiwezekani kuwaongezea wezi hela, tutafute kwanza mchawi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kule vijijini mimi huwa najiuliza, Maprofesa wetu na Mainjinia, ukitoka hapa kwenda Mwanza utaona madaraja zaidi ya 1,000. Madaraja kazi yake ni kupitisha maji; maji yanaachwa tu yanasambaa yanaenda kupotea maporini. Ikija hela ya utafiti, watafiti wanaenda ku- drill kwenye milima ambako hakuna maji. Tunakosa maji na hela zimelipwa, haiwezekani. Naomba kabisa, suala la kuongeza hela shilingi 50/=, kama Waheshimiwa Wabunge tutajaa kingi hii ya kukubaliana naye, anayebeba mzigo ni wanyonge walioko kwetu. Kuna watu wanaishi kwa kipato cha shilingi 5,000/=, analima mchicha, ukamwambie akatwe shilingi 50/= anampigia mtu njoo ununue mchicha wangu shambani, hiki kitu hakiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba, Profesa anafanya kazi vizuri sana, Profesa Mkumbo anafanya kazi vizuri, Naibu Katibu Mkuu Engineer jamani, mkishindwa term hii labda tufute tu hii Wizara. Kwa sababu mimi najiuliza, hili suala kuanzia Profesa Mwandosya alishindwa maji, akaja Prof. Lwenge akashindwa, akaja Profesa Maghembe akashindwa, hebu jaribuni basi na darasa la saba. Mimi nitaziba mitaro tu, yatajaa maji kwa watu wote humu ndani. Hiki kitu hakiwezekani. Serikali mjiulize mara mbili. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana jana nilikuwa nasikia ndugu yangu Mheshimiwa Mboni hapa analia, ooh, Mheshimiwa Mbarawa tupe maji, Mheshimiwa Aweso tupe maji, Mkumbo tupe maji. Huyu atatoa maji wapi? Angekuwa Mheshimiwa Mwijage na Mbunge wa Bukoba wangetoa maji. Hawa watu wa hapa Singida utatoa maji, hayo maji yana chumvi, haiwezekani. Nilichokuwa naomba, tuangalie kwanza tatizo tulilonalo ndani ya Wizara.

Mheshimiwa Spika, hakuna sehemu ambayo Mheshimiwa Rais anapata shida kubwa ya maswali na Waheshimiwa Wabunge tunadhalilika kwa sababu ya maji.

Mheshimiwa Spika, natoa mfano, kwenye Wilaya yangu nilikuwa na mradi huo niliosema wa Chankorongo, tumejenga miaka 20 na kitu hauishi; mara tanki linapasuka, mara linafanya hivi. Akaja Mheshimiwa Jafo, nikamwambia mimi ni mkandarasi wa darasa la saba, lakini nina wasiwasi na huyu engineer, hebu tukague cheti chake. Huyu engineer gani anatengeneza bwawa linafumuka? Tulipokagua tukakuta ana cheti cha environmental. Tukafukuza, maji yameanza kutoka. Hivi Profesa unataka ufundishwe design gani?

Mheshimiwa Spika, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge tusijaribu kuingia kingi ya kutoa shilingi 50/=, hakuna 50 inayotoka, wananchi wetu ndio tutakaowapa mzigo. Kama tunataka kuongeza shilingi 50/=, lazima tuangalie anayeongezewa mzigo ni nani? Sisi Waheshimiwa Wabunge tunavaa suti, tuna mshahara mzuri. Kuna watu kule wanauza mchicha, wanauza dagaa, haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wako watu wazuri sana, sipigi debe, mimi natoka Kanda ya Ziwa. Kuna engineer anaitwa Sanga kule, miradi yote inayoshindikana kutoka Halmashauri anapewa, anakesha vijijini kule, kamaliza mradi wa Lolesia, kamaliza Chato, kamaliza mpaka Musoma. Engineer Sanga, kwa nini watu wazuri kama hawa wasipandishwe vyeo ili uzuri wake ukaonekana nchi nzima? Kuna watu wabovu kabisa wamekalia madaraka, hela zinatumwa Halmashauri halafu tena zinakuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ameenda Lindi amekuta Mhindi ameshalipwa hela mradi hautoi maji. Alivyosema nyang’anya Passport, watu wameanza kushughulika na hela zililipwa. Chalinze hivyo hivyo hela zimeliwa; Morogoro, kila mahali, halafu tukaongeze tena hela ndugu zangu. Ukienda kwa Mheshimiwa Keissy hela zimeliwa.

Mheshimiwa Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, hili suala la kuongeza hela, tuondoeni hayo mawazo Waheshimiwa Wabunge, tushughulike na hela tulizonazo. Hizi shilingi bilioni 600 zikienda zote; na ushauri wangu kwenye Serikali, ili kuondoa hii kesi, toeni hela kwa muda muafaka. Hizi shilingi bilioni 600 zikitolewa kwa muda muafaka, watu wote watajaa maji.

Mheshimiwa Spika, huo ndiyo ushauri wangu. Nakushukuru sana. (Makofi)

SPIKA: Haya, ushauri huo.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia. Naomba niipongeze sana Wizara ya Afya. Kipekee kabisa nampongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Katibu Mkuu wake. Wao wanajua ni kwa nini nawapongeza. Bila jitihada zako Mheshimiwa Ummy ukishirikiana na mama wakati akiwa TAMISEMI, sisi watu wa vijijini huko Nzera tusingekuwe na Hospitali. Nataka nikuhakikishie kazi mliyoifanya ni kubwa sana na tutawakumbuka milele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, huwa nazungumza mara nyingi, hii Wizara wakati tunaanza Ubunge ilikuwa ni Wizara ambayo kila mtu anailalamikia, lakini leo Wizara hii ukisikiliza michango ya Wabunge, nadhani mwaka ujao tutakuwa tunaijadili siku moja tu mambo yanaisha tunapitisha bajeti. Hata kama kungekuwa na tuzo ya kutunzwa Mheshimiwa Waziri anayefanya vizuri, kiukweli bila upendeleo Mheshimiwa Ummy unastahili kuwa Waziri bora kabisa katika Bunge la 2018. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, alipopita kule kwetu aliahidi hospitali, umetupa. Jimbo zima watu laki 500,000 hatuna kituo cha afya. Kwa huruma yake alipandisha vituo viwili. Tusaidiwe pesa ili tuweze kupata kituo cha afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tunajenga Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Geita. Hii hospitali imesimama toka mwezi wa Kwanza, certificate hawataki kulipa. Lipeni certificate tuweze kujenga hospitali yetu. Kuna tatizo gani? Tunategemea hiyo hospitali ndiyo iwe hospitali ya kutukomboa sisi watu wa Geita. Tuko zaidi milioni tano na kitu. Tusaidieni kulipa hiyo certificate ili waweze kuendelea kujenga hospitali yetu ya mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri sana kiukweli, alipofanya ziara kwenye Hospitali ya Rufaa ya Bugando alitualika Wabunge wa Kanda ya Ziwa, nami nilikuwepo. Bahati nzuri Gwajima alikuwa bado Wizarani, naye alikuwepo. Niwapongeze sana. Katika miaka yote inaoneka kweli Serikali mmekuwa serious kutukomboa sisi watu wa Kanda ya Ziwa. Ninaona kabisa jitihada za Serikali kujiona ni sehemu ya ile Hospitali ya Kanda ya Ziwa ya Rufaa ya Bungando. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pale tukiwa na Mheshimiwa Waziri tulizungukia majengo, aliyaona majengo mazuri, lakini kule ndani hakuna MRI na wagonjwa wengi wanatoka Kanda ya Ziwa. Tunamwomba Mheshimiwa Waziri aweke mpango mkakati tununuliwe MRI, watu wetu wanakufa kwa kukosa gharama za kufuata MRI Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile tunaishukuru Serikali. Tunatibu wagonjwa wa saratani. Wagonjwa wa saratani Tanzania wanaongoza toka Kanda ya Ziwa. Tunaomba mlete wataalam wakae Mwanza. Mtu wa kuanzia Singida hana nauli ya kuja Dar es Salaam, atakuja Mwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia watujengee wodi, pamoja na kwamba vifaa vipo, lakini mtu anapotaka kufanyiwa operation, hakuna wodi ya kuwalaza wale watu. Kwa hiyo, tunamwomba sana Mheshimiwa Waziri kwa ukaribu alionao, namkushukuru sana Mheshimiwa Waziri na ninamwomba sasa awe karibu na hiyo hospitali aweze kutusadia watu wa Kanda ya Ziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tunashukuru, juzi nilitembelea nikaona; mlituahidi kutujengea jengo la TB kama la Kibong’oto na lenyewe limejengwa kwa shilingi milioni 120. Ni suala ambalo kweli tunaona Serikali mpo karibu na watu wa Kanda ya Ziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia waliahidi kutoa matibabu ya bure kwa wagonjwa wenye saratani. Tunaona, tunatuma watu wetu wanasaidiwa masikini bure. Tunaiomba Serikali ingalie kwa jicho la huruma, ikamilishe vitendea kazi kwenye hospitali yetu ya Bugando. Hiyo ndiyo hospitali kombozi kwenye kanda ya ziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Ummy anakumbuka, wakati tulikuwa tunaenda, hospitali ilikuwa inakusanya shilingi bilioni mbili. Leo inakusanya shilingi bilioni tisa. Na mimi napenda huyu mtu mngempongeza Wabunge wa Kanda ya Ziwa. Kutoka shilingi bilioni mbili hadi shilingi bilioni tisa na siyo matibabu ya kugombana, ni matibabu rafiki; leo watu hawaendi hospitali za mtaani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zamani ilikuwa ukiambiwa unaenda Bugando unajihesabu unaenda kufa, lakini leo ukifika pale unatibiwa vizuri, unakaribishwa vizuri na watu wanatoa pesa zao bila wasiwasi. Watu kama hawa, Wakurugenzi akina Makubi wangekuwa wanaalikwa kwenye Mabunge kama haya tunawapa pongezi na wao wanajisikia ili waweze kwenda kuongeza morali.

MBUNGE FULANI: Yuko hapo.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Yuko hapa, nashukuru sana Mheshimiwa Waziri. Leo ukienda Bugando, ni kweli kabisa, hata operation za mitaani zimepungua. Watu wanapewa motisha kule ndani, Bugando imekuwa nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, yangu ni hayo. Nakupongeza sana Mheshimiwa Ummy; ya Jimboni kwangu unikumbuke lakini na hospitali yetu ya Bugando hatuhitaji sana kuwafuata Madaktari Dar es Salaam, tunataka tutibiwe Mwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuruku sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuuomba mhimili wa Bunge kwamba sisi Wabunge tunapoapishwa kuwa Wabunge ni vizuri sana kama mhimili uone umuhimu wa kuchukua ile miezi mitatu ya mwanzo kutupeleka kwenye Chuo cha Jeshi cha Kunduchi cha NDC ili tuweze kujifunza kuzungumza maneno yanayoilinda taifa letu. Chuo hiki ni kizuri na mimi nina imana kama Bunge litakubaliana na mimi kwamba Wabunge tukapate miezi mitatu ya kufundishwa pale, hii migongano ya maneno ya hovyo hovyo yanayotokea humu ndani haitakaa itokee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri ni wa leo tu, asubuhi Mheshimiwa Spika ametueleza kuhusiana na Mbunge kijana Mheshimiwa Masele anayetuwakilisha kwenye Bunge la PAP, kijana huyu pengine angekuwa amefundwa pale Kunduchi haya yote yaliyotokea kule PAP yasingetokea. Kwa hiyo, ni muhimu sana sisi kama Bunge tukubaliane twende tukafundishwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitazungumzia kidogo tu kuhusu SUMA JKT. Sisi Wabunge tunaotoka kwenye maeneo ya migodi, nilikuwa naishauri Serikali maeneo haya ya migodi na hasa hii migodi mikubwa ni vizuri Serikali malindo yale ambayo yanalindwa na vyombo ulinzi vya nje wangepewa watu wa SUMA JKT. Kwa mfano, kwenye migodi mikubwa kama Geita wanalindwa na Kampuni inaitwa G4S, mlinzi mmoja analipwa karibu dola 800 yule mzungu mwenye kampuni na retired officer kutoka huko South Africa. Lakini vijana wetu wanalipwa shilingi 200,000/300,000 na mimi nimeona SUMA JKT wamefanya vizuri mpaka wametoa na gawio kwenye Serikali. Hizi fedha wangelipwa SUMA JKT wangefanya vizuri zaidi hapa wangetupa gawio kubwa zaidi kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona kule migodini kwa kuwa hawa watu waliopewa hizo kampuni za ulinzi ni wazungu wa South Africa, wanawa-train vijana wetu vibaya na nilishazungumza hata humu ndani, ukienda kule Geita kwenye migodi ile kama GGM na migodi mingine ya Kahama, wale walinzi wa kule wakimkamata kijana aliyeenda kule tu hata kuokota mawe wanawapiga, wanawanyanyasa na hata wanawakamata wanawake wanaenda kuwalalisha na mbwa. Sasa ni vizuri walinzi wale wangepewa walinzi wetu ambao wamefundishwa na wana maadili mazuri ya Kitanzania, nadhani ingekuwa ni vizuri zaidi na Jeshi letu lingeweza kupata fedha nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niombe tu, kiukweli amezungumza kaka yangu pale kuhusuana na kauli zinazotolewa na wenzetu. Mimi niombe tu kwamba kiukweli maadui huwezi kujua wako ndani ama wako nje. Tukianza kulisema Jeshi kwa ubaya kwamba wakae kimya, mambo yakiharibika mimi natoa mfano tu siku moja humu ndani uliwaka moto, kila mtu alikimbia humu. Hebu lijaribu liripuke bomu humu ndani tuone mtu jasiri wa kuweza kukaa humu ndani. Kwa hiyo, mimi niombe tu sisi kama Wabunge kwa Jeshi letu hili la mfano linasifika kimataifa, Wizara kama hii siku inayoletwa humu ndani, tusilifananishe Jeshi na vyombo vingine vya ulinzi na usalama. Ni watu ambao kiukweli muda wao mwingi wanafikiria kutulinda sisi tukae salama na nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa binafsi yangu nikuombe na Wabunge wenzangu, Jeshi linafanya kazi nzuri, ni watu wanaotakiwa kupewa moyo na mimi ningeomba kama tungeweza kupata muda kidogo tukapelekwa Jeshini kama wiki mbili, ukaona ule msoto ulioko kule halafu bajeti inaletwa humu watu wanaanza kuongea mambo ya hovyo hovyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze sana ndugu zangu wanajeshi mnafanya kazi nzuri na sisi kama Wabunge tunawaombea endeleeni kuilinda nchi yetu, haya maneno madogo madogo... (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante, unga mkono hoja.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati Kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia. Mimi ni mjumbe wa Kamati ya hii, na nilikuwa namsikiliza mjumbe mwenzangu na najaribu kukuangalia hata wewe ulivyokuwa unahangaika kutupa maelekezo sisi wajumbe wa Kamati.

Mheshimiwa Spika, wala usishangae. Labda tu nikukumbushe ni vizuri wajumbe unapotuteua kutupeleka kwenye kamati ukafuatilia na michango yetu kwenye kamati na mahudhurio.

Mheshimiwa Spika, kuna baadhi ya wajumbe umewateua wakishasaini wanaondoka haya ndio matatizo tunayopata. Haya tunayosema, tuna mahudhurio lakini pia tuna maoni kwenye maoni kwenye Kamati hakuna mahala ambapo Heche ameshawahi kuchangia, akisaini anasepa. Kwa hiyo ni vizuri pia ukatufuatilia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimemsikiliza vizuri mchangiaji mimi nilidhani mawazo alikuwa anayachangia kuhusiana na uchimbaji…

MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Spika, kuhusu utaratibu, amenitaja jina.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA:… Mheshimiwa Spika, Heche sikutegemea kama atatoa haya mawazo…

KUHUSU UTARATIBU

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, nadhani umeona, haya ndiyo yanayotokea kwenye Kamati. Nimemsikia rafiki yangu, mdogo wangu amesema yeye ni chuma, chuma kinaanzia kwenye kuokosea kanuni kama hivyo. Lakini la pili nimekusikia vizuri ukimtafuta Waitara usingehangaika hata Ester yupo hapa kiboko yake; na chuma chepesi huwa kinaanziwa kuyeyushwa na moto mdogo ule wa wahunzi, sasa moto mkubwa unakuja mzee nadhani ungejipanga. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia. Maneno aliyoyazungumza mchangiaji kama mjumbe wa Kamati ambaye kwa asilimia 90 naye ni kama Musukuma anategemea maisha ya wachimbaji nilitegemea angekuwa mtu wa kwanza kumpongeza waziri kwa kazi nzuri aliyofanya. Haya maeneo yangezumzwa na Msigwa rafiki yangu anayefuga mbwa kule wala tusingepiga kelele. Lakini kusema ukweli Heche hujatenda haki. Leo haya maneno kama wachimbaji wanakusikia unailaumu Wizara ya Madini ninakushangaa; na nina imani una muda mrefu hujaenda kutembelea wachimbaji.

Mheshimiwa Spika, mimi natoka Geita aje Heche tumuonyeshe refinery inaojegwa na hatua zilizofikiwa. Haya mambo hatubabaishi, yamefanyika na yako yanaendelea…

MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Spika, kuhusu utararibu.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA:… Mheshimiwa Spika, nilikuwa nashauri tu mambo mazuri yanapokuja kiukweli lazima kuwe na taratibu. Tunakuona vizuri sana Mheshimiwa Waziri unatusikia kwenye madini changamoto ndogo ndogo. Kwa mfano anayejenga (smelter) refinery kule Geita jaribu kuongea na Wizara ya Viwanda wampe vibali, amekwama kupata vibali vya EPZ, ili aweze kuendelea na uwekezaji wake kwa kuwa kuna vitu anakwamba kwenye kodi. Kwa hiyo ni vizuri ukazungumza na watu wa viwanda wajaribu kuwahisha michakato ili aweze kuendelea.

Mheshimimiwa Spika, kwa sisi watu tunaokaa vijiji, leo ukizungumza umeme, wapiga kura wakakusikia unamlaumu Kalemani Waziri wa umeme, yaani sijui. Mimi nadhani wakati mwingine ni wivu tu na lile neno ulilolisema, upinzani. Mimi jimbo langu tulikuwa hatujawahi kuona umeme awamu zote; hata huko kwao Heche; leo kwenye awamu ya tano mzee kijiji changu kila mahali ni mjini, kuna umeme. Leo unasisimama humu kweli Mheshimiwa Heche hata kwa hicho ulichonacho? Mimi nadhani Waitara hakukosea kuchukua maamuzi ya kwenda hilo jimbo, nimeanza kuamini. Kwa design hii watu wako watachelewa kufika, kwa hiyo ni vizuri wakakupiga chini akaja mtu mwingine.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumezunguka hii nchi sisi wajumbe, kila mahala tumeenda kukagua utekelezaji miradi ya meme na nishati na madini Heche tulikuwa wote, leo unakuja huku unaanza kupiga kelele kupinga mafanikio makubwa yaliyofanyika? Mimi naomba nikukushukuru sana kunipeleka kwenye Nishati na Madini. Kwa kuwa mimi natoka kwenye madini nikisimama hapa nakwambia mzee ingekuwa Spika unatutembelea Wabunge wako njoo utembelee mkoa wa Geita sidhani kama kuna mbunge hata rudi humu ndani. Kwa sababu watu wetu wana maisha safi, kila mahala ambapo tulikuwa tunafukuzwa leo tunachimba; kila mahali tulipokuwa tunavumbua dhahabu tunaletewa mabomu leo mambo ni safi, halafu anasimama mtu anakuja anaongea anaponda Wizara! Kwa kweli mmefanya kazi nzuri na hii serikali iendelee kuwa na moyo huo.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri yapo ambayo ningependa kushauri. Kwamba ni lazima tujaribu kuangalia hata kwenye uongozi wa huko kwenye mikoa. Tunafanya vizuri, mimi naamini wawekezaji wengi wazuri wa kati tunawatafuta sisi wachimbaji wadogo wadogo kwa kutumia akili zetu bila kusaidiwa na serikali. Lakini tunapowaleta wawekezaji wetu masharti ni mengi mno Mheshimiwa Waziri. Mimi nina mfano nina mwwekezaji yupo Geita, yupo Nyamauna wewe unamfahamu. Kila siku anapigwa faini mpaka amefunga mgodi. Mara OSHA mara idara ya kazi mara huyu migration faini milioni mia nane na kitu mchimbaji wa kati ataendeala kusaivaive namna gani?

Mheshimiwa Spika, nikiuombe Mheshimiwa Waziri, pamoja na kwamba utakuja kueleza vizuri una vyombo vyako, hao wawekezaji wachimbaji tunavyowatafuta mtu wa kuwalinda ni, wewe usikwepe mzigo. Kama wataondoka wanaopata kazi ya kwenda kuwatafuta ni sisi wachimbaji wadogo, hakuna mahala ambapo tunafurahia; tunaona, unamleta mtu mwenye mtaji wa bilioni tano anazopigwa faini, mara idara ya kazi, mara sijui hana kibali, mara sijui nini; milioni mia tisa na kitu. Nakuomba Mheshimiwa Waziri; na kitabu ninacho hapa naweza nikakukabidhi; ukajionea adhabu mwekezaji huyu wa Nyamauna alivyopigwa; idara ya kazi, sijui osha, sijui nini hadi amefunga mgodi na ni mwekezaji ameajiri watu zaidi 500, hii haiwezekani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nikuombe wewe Waziri na Waziri wa Kazi na wanao husika muwa-guide wale watu mikoani wasione wale wawekezaji kama chanzo kukamilisha ujenzi wa madarasa; hii haiwezeikani nikuomba sana Mheshimiwa waziri uyazingatie haya.

Mheshimiwa Spika, nakushuru sana kwa kazi nzuri kamati hii ilivyozifanya nakupongeza Mwenyekiti kwa umetu-guide vizuri na wajumbe wengine wa CHADEMA wenye akili timamu nadhani wanaelewa. Ninakushuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Madini
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia. kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, kwa sisi jamii tunaotoka kwenye maeneo ya wachimbaji wadogo ni dhahiri kabisa tumepata Waziri ambaye Ofisi yako inaingilika kirahisi. Tuliyaona, kabla ya wewe kulikuwa na Mawaziri Maprofesa hapa siku unataka kukutana naye yaani inabidi uende kwa dobi ukafue hata suluari kwanza, lakini tunakuombea Mungu na uendelee na moyo huo kwa sababu unamsikiliza kila mtu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kwa kweli Wizara hii inafanya vizuri na sisi wapiga kura wetu ambao ni wachimbaji sidhani kama ukimsema vibaya Waziri Doto atakuelewa; tunahitaji tu kukushauri kwa machache ambayo pengine tunaona ukiyafanya utakuwa rafiki mzuri zaidi ya wachimbaji wadogo.

Mheshimiwa Spika, kama alivyoeleza Mheshimiwa Kasu, tunaona kwenye maeneo yetu ya wachimbaji kuna shida kubwa sana ya watendaji, shida kubwa sana. Wachimbaji wadogo wengi wameitikia wito wa kulipa kodi lakini pale ambapo mtu anapotaka sasa afuate zile procedure za kulipa kodi kuwapata watendaji wa Wizara yako ni shughuli; inabidi mtu akae na carbon saa nyingine mpaka siku tatu risk wezi wako kule wanajua carbon imeshaiva. Sasa nikuombe Mheshimiwa Waziri, kama Serikali haijakupa kibali cha kuajiri tunaweza kutumia njia ya dharura tu kama tuliweza kuchukua Wanajeshi wakaenda kuchukua kangomba kule Mtwara tunashida gani? Tumuombe Mheshimiwa Rais akupe Wanajeshi waende wakasimamie ni shida kubwa sana unakuta kwa mfano Geita kuna erosion plant labda 30 mpaka 50 watumishi wanane inawezekana vipi? Ni mateso makubwa. Mimi nikuombe Mheshimiwa Waziri nimeona hata makusanyo ya Wilaya yangu ya Geita tuna kilo karibu 600 sasa hivi kwa miezi mitatu. Mheshimiwa Waziri mimi naangalia kabisa kwa macho yangu na uzoefu wangu hata theluthi bado hujakusanya dhahabu bado inaibiwa.

Mheshimiwa Spika, hebu nikushauri kwa sababu mimi ukikusanya sana wewe na mimi kwenye halmashauri napata pesa nyingi hebu jaribu hata miezi miwili chukua Wanajeshi tusambazie kule uone dhahabu itakayokuja, kuna dhahabu nyingi. Lakini nikuambie kingine ni kwamba watu wako pia si waaminifu ubovu unaanzia kwenye Ofisi yako humo humo kwa wasimamizi na nikuombe Mheshimiwa Waziri ushauri wangu tu pengine unapotaka kuajiri hawa wasimamizi wako Mikoani na Wilayani kuna chuo kile cha Jeshi kiko Kunduchi, nilizungumza hapa, kile cha NDC, hebu wachukue kwanza wakafundishwe uzalendo wa kuyalinda haya madini yetu pengine nakuona kila siku mara unafukuza mara unahamisha utaumiza kichwa unazofukuza ni hela dhahabu ni pesa watafutie utaratibu waende wakafundishwe pale miezi mitatu wakirudi hapo hawataiba, hawatashiriki huo wizi unaoendelea.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine kuna kitu inaitwa inspection fee inachukuliwa kule kwetu kwenye migodi yetu kule asilimia moja. Sasa nilikuwa tu nakushauri hii asilimia moja hebu jaribuni kuangalia hata theluthi ibaki kule mikoani. Leo Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya na Kamati ya Ulinzi na Usalama ndiyo tumemkabidhi majukumu yote; tukishafungua maduka tu tunawaachia walinzi wao kufukuzana na wezi wao halafu hawana kitu unampigia Mkuu wa Mkoa njoo kuna watu wanaiba madini anaanza kuomba mafuta kwa Mkurugenzi, hiki kitu si sawa, turudishieni hata kidogo ili Wakuu wetu wa Wilaya na Wakurugenzi na Wakuu wa Mikoa wale na fungu la kuwapa hata motisha wale watu wanaoenda kufukuzana na wezi kule kwenye machimbo usiku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, linguine, Geita hatujalipwa hela zetu, na wewe mwenyewe unafahamu. Mheshimiwa Nyongo amekuja Geita Mjini Nyamarembo, Magema na Katoma, kuna watu wamefanyiwa compensation miaka minane; na ninapata taarifa kwamba wanaanza kulipwa lakini hizo fidia wanazolipwa ni wamepunjwa nataka nijue kama mdhamini mkuu wa Serikali alishirikishwa kwenda kuhakikisha kwamba watu wetu wanapata pesa inayostahili na maeneo yao au na nyumba zao? Si vibaya Mheshimiwa Waziri mimi nikuambie na yeye wenyewe ulikuwa mjumbe wangu wa Kamati ya Siasa, nilivalia njuga kipindi kile 2013, mama Tibaijuka Mungu amsaidie sana alitusaidia watu walilipwa mabilioni ya pesa si vibaya mkachukua uzoefu wake alitumia njia gani watu wetu wakalipwa, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kukupongeza sana wewe. Nakumbuka wakati tumekuchagua, ulipokuwa unaeleza vipaumbele vyako, moja ya kipaumbele ulichotueleza ni kwamba baadaye sisi Wabunge hatutahangaika tena na makaratasi, utaleta Bunge mtandao. Tunakushukuru sana. Hata mimi mwenyewe sasa hivi sibebi karatasi, nami pia nimekuwa wa kisasa. Mungu akubariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nakaangalia ka Msigwa sijui kameenda wapi, kwa sababu unajua mimi huwa najiuliza, yaani haya maneno yanazungumzwa na mtu anaitwa Mchungaji,…

MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: …anatuaminisha tuache kufuata maelekezo ya Madaktari, watu walioumiza vichwa, wakasoma wanajua kinga ya Corona, anatuaminisha kama Mganga wa Kienyeji, halafu kenyewe kanatoka kanaenda kunawa pale. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hawa watu ni watu wa hatari sana na tusikae kimya Waheshimiwa Wabunge. Sisi tunaelekeza kusikiliza maelekezo ya Madaktari, watu wanaojua; na tutanawa. Tunaiomba Serikali ongezeni hata ndoo barabarani tuendelee kunawa. Hawa watu kama akina Msigwa hawa, anapiga porojo humu anakaa kwenye you tube, kenyewe kamepita mlangoni pale kamenawa maji kameondoka.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba sana watu kama hawa tusiwafumbie macho, lazima tupate muda wa kuwaambia, hili siyo suala la mizaha. Kuna watu wetu kule vijijini walishaamini kabisa na tunanawa mara tatu au nne, anakuja kutueleza Wazungu wananawa maji. Wazungu wa wapi aliowaona wananawa kila dakika? Hata ukiingia kwenye washroom zao kuna makaratasi, halafu mtu anakuja kutuambia mambo ya kihunihuni. Naomba sana watu kama hawa tuweze kuwakemea. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, niwapongeze sana watu wa Mkoa wa Dar es Salaam. Tunaona na kweli Watanzania wameelewa. Jana nilikuwa naangalia kwenye TV, ule mlundikano wa kwenye daladala umeisha automatically. Kwa hiyo, tunaomba na Wakuu wa Mikoa wengine waige mfano kama ule wa Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nikupe mfano mmoja; mimi na mwenzangu Mheshimiwa Tizeba na Mheshimiwa Ngeleja hapa; ili wapiga kura wetu Mwanza, pale kuna pantoni. Ukiondoa ile pantoni ya Serikali kuna ferry za mizigo kule Kamanga Ferry. Hizi ferry zinabeba watu zaidi ya 1,500 wakati uwezo wake wa kubeba labda ni watu 300 au 400. Malori humo humo, mafuta humo humo. Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie namna kwa watu wetu ambao wanatumia hicho kivuko. Ikiwezekana Mheshimiwa Engineer Kamwelwe kama yuko hapa aweke watu wasimamie, zile ferry zinatakiwa zibebe watu 300, haiwezekani ukalundika watu 1,000. Tusije tukasababisha mambo mengine kwa wapiga kura wetu.

Mheshimiwa Spika, lingine, kwanza tunaishukuru sana Serikali. Tumepata taarifa kwamba mmepata mkono ule ambao watu walisafiri kwenda kuupinga. Kitu ambacho nitawashangaa, kama watu walitumia mamilioni kwenda kuharibu tusipewe hela, halafu sasa hivi zimekuja hela, umpelekee mgao wa hizi hela, nitawashangaa Mawaziri. Ninaomba kabisa sisi ambao tulikaa kimya na kuomba kila siku kwa Mungu tupate huo mkopo, mtuangalie, sisi tuna shida na shule zetu. Hao watu ambao walienda kuponda, achaneni nao msiwape.

Mheshimiwa Spika, lingine, tunaishukuru sana Serikali ya Awamu ya Tano, tumepata Halmashauri kwenye vijiji vyetu. Ni kweli Serikali ina wazo zuri kabisa, imepeleka huduma kwa wananchi, lakini naomba kama kuna uwezekano, Serikali ione dharura yoyote, kule tulikohamia hakukuwa na maandalizi na hatukuwa na bajeti. Kwa hiyo, ni vizuri Serikali ikaona dharura sasa, zile Halmashauri ambazo zimegawanywa ziweze kupelekewa hela ili waweze kuandaa makazi na ofisi za kufanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, lingine nilijaribu kuingia siku moja kwenye Kamati ya TAMISEMI, nikawa nasikiliza, kwa mfano Mkoa wa Dar es Salaam; tunapiga kelele kila siku hapa tupeleke hela kwa vijana, watu wenye mahitaji maalum na akina mama, lakini ukisikiliza mpango mzima, tunatengeneza Taifa la watu wajinga tu. Hakuna mtu anapewaga hela ya bure. Zile hela za Halmashauri ni kama tunazitupa tu bila kuwa na mkakati wowote wa kuhakikisha fedha inarejeshwa.

Mheshimiwa Spika, hata kule Bungeni nilikuwa nawasikiliza Wajumbe mle hakuna aliyesema zimelipwa ngapi? Tunang’ang’ana kulundika tu. Mkoa mmoja wa Dar es Salaam peke yake umetoa kama shilingi bilioni nne, hamna mtu anayezifuatilia hizo hela. Mnawaza tu tena na mwakani kulundika. Tutakuwa tunatengeneza watu wajinga tu baadaye hawana akili ya kutafuta.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba kama kuna utaratibu, basi tuangalie baadhi ya mikoa yenye uwezo tuweze kuzilinda hizi hela, tufungue hata taasisi ambaoo tutaweka watu wenye kazi hiyo hiyo kwa ajili ya kushughulika na masuala ya kukopesha na kudai kuliko kuwa tunachukua hela, tunalundika, watu wanaenda kuolea. Hii naona kama haijakaa vizuri.

Mheshimiwa Spika, suala la afya. Serikali imefanya vizuri sana kwenye afya. Tumepata Vituo vya Afya na Hospitali za Wilaya. Naomba sana, mimi kwangu kule ninakotokea, hospitali nzima ya Wilaya nina Madaktari watatu kwenye population ya watu 600,000. Hicho kitu hakiwezekani. Kwa hiyo, naiomba Serikali, yale mazingira ambayo tumepewa hospitali mpya, basi waangalie kwenye huo mgao hao madaktari walioajiriwa watupatie Madaktari kwa sababu unakuta ikama inataka labda watu 20, una Madaktari watatu utafanyaje?

Mheshimiwa Spika, tumepewa x-ray na vitu vyote kama echo machine na kadhalika halafu hakuna mtumishi. Mpaka leo unakuta labda zina miaka miwili yamelundikwa tu ndani lakini hakuna mtaalam wa kuzitumia. Kwa hiyo, naiomba Serikali tunapokuwa tunanunua vitu, tuandae na mpango mzima wa kuweza kusimamia zile hela.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, limezungumzwa suala la Ofisi za Wabunge, kwa kweli ni shida. Waheshimiwa Wabunge wengi hapa ukiwaangalia hapa, Ofisi zao ni magari na wananyanyasika kweli kwa Wakurugenzi. Mkurugenzi mwenyewe hana Ofisi, iwe wewe Mbunge! Kwa hiyo, naomba kama alivyoeleza Mwenyekiti wa Bajeti, ni vizuri suala hili likasimamiwa na Bunge, tuache kupeleka TAMISEMI, hatutapata Ofisi. Unakuta mtu ameniga tai halafu Ofisi iko kwenye gari. Kwa hiyo, ni vizuri walivyopendekeza Kamati, basi mrudishe kwenye Bunge, halafu Bunge lenyewe ndiyo lisimamie kutengeneza Ofisi za Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nimpongeze sana Mheshimiwa Mama Samia kwa kuendelea kumwamini Waziri Awesu na kwa kweli naomba nimpongeze sana Waziri Awesu, kama kijana ameitendea haki Wizara, pamoja na Katibu Mkuu na wasaidizi wake. Niseme wazi kwamba mimi binafsi kama Mbunge wa Geita ninakufurahia sana kazi zako na tungependa na Mawaziri wengine wawe kama yeye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaona Waziri Awesu anavyohangaika na anavyopangua na sisi wengine tumepita huko kwenye ukandarasi kandarasi, tunaona jinsi ambavyo anajaribu kurekebisha hata huko kwenye Wizara yake, kwa sababu wizi mkubwa naamini kabisa unaanzia kutoka Wizarani, unateremka kule chini. Nitoe mfano mmoja, kulikuwa na huu mradi nasoma hapa wa miji 16, lakini sijui wametumia formula gani kwa kweli nawapongeza sana mpaka wametoa miji 29, hizo ndiyo akili tunazitaka, wasomi wawe hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nimshauri Mheshimiwa Waziri, tunaona hata sisi tunachimba, lakini kwenye visima bado, Waziri atafute akili nyingine kwa sababu ukiangalia, leo mimi kama Musukuma nikitaka kuchimba maji kisima changu hapa Dodoma kwa kutumia mitambo ile ile na utaalam ule ule, haiwezi kuzidi milioni tisa au milioni 10, lakini ukienda kwenye kisima kinachochimbwa na Serikali milioni 37, inakuwaje huo utaalam? Kwa nini tusiende kwenye utaratibu mwingine, tukaweza hiyo milioni 33 mpaka 35


ikachimba visima vinne mpaka vitano. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri ajaribu kuona namna ya kuwabana wataalam wake waweze kurekebisha ili tuweze kupata maji kwa wingi na kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Spika, nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kuniwekea mradi kwenye Jimbo langu nimeona ameweka Vijiji vya Nkome, Senga, Nzera, Rwezera, Idosero, Sungusira na Kakubiro, namshukuru sana, lakini kauli yake ni nzuri sana, hivyo Waziri asinizingue term hii kwa sababu bahati nzuri mradi huu ulikuja kubuniwa na Profesa Mkumbo akiwa Katibu Mkuu na Katibu Mkuu wa sasa Sanga ndiye alikuja kufanya upembuzi yakinifu. Sasa Mheshimiwa Waziri hii ni mara ya pili ananiahidi akinizingua bajeti ijayo nitamzingua mara mbili.

Mheshimiwa Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri tutakapomaliza suala hili la bajeti hata katikati hapa tukimbie akaone jinsi sisi Wanajimbo la Geita tulivyo wavumilivu, asilimia 92 ya Jimbo langu ni ziwa, lakini sisi tunaugua kichocho tunachota maji machafu, halafu maji yamevutwa yanaletwa mpaka Dodoma. Sasa hivi vitu nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, term hii asinizingue, tumekuwa wavumilivu vya kutosha, aone namna yoyote ile, baada tu ya bajeti hii, naomba tufungue mradi wa maji kwenye vijiji ambavyo ameniahidi. Nami namwahidi nitampa ushirikiano wa kutosha na hata akitaka utaalam wakati wa kuandaa BOQ aniite ili maji yatoke kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri aendelee na moyo huu. Nimekuwa Mbunge kwa awamu ya pili, hii bajeti Mawaziri huwa wanaugua tumbo, bajeti ya Wizara ya Maji, lakini naona leo mishale ni michache sana. Hii ni ishara nzuri, anapoitwa anaitika na anapoitika anaenda anatoa action ndiyo maana watu wanamshauri na kumwambia aboreshe pale alipovuruga.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, ningeomba Mheshimiwa Waziri, kama hatakuwa na nafasi kwa muda wa karibu kutembelea Jimbo langu, basi namwomba


Mheshimiwa Waziri kwa sababu ametembea na Wabunge wengi huko, aje na Jimboni kwangu angalau nitembee naye aone hivyo vijiji ambavyo…

SPIKA: Unamwomba Naibu au unamwomba Waziri?

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, namwomba Naibu Waziri anaweza ….

SPIKA: Marufuku. (Kicheko)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, Nakushukuru sana. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri, lakini pili naipongeza Kamati kwa ushauri na mapendekezo yake mazuri; naunga mkona hoja zote mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwanza kwa kumteua Mkuu mpya wa SUMA JKT, sisi tuliokuwa kwenye Kamati ya Nishani na Madini mwaka jana tumeona kazi nyingi sana alizozisimamia na nina imani kwamba baada sasa ya kupewa rungu mambo yatakuwa mazuri zaidi, Mungu ambariki sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa napenda kushauri kuhusiana na suala la mfumo, mimi nitazungumzia sana kwenye JKT. Mfumo wa JKT kwa mzamo wangu mimi nikitizama JKT natazama kama uchumi mkubwa sana kwenye Taifa letu, lakini ukiangalia jinsi SUMA JKT inavyochagua vijana wa kwenda kujiunga na JKT inaweka vigezo vya elimu tena ina division na point na wanapoenda kule wanasoma wengine mpaka miaka mitatu wakiwa na malengo haya haya kwamba nitaenda jeshini na kule jeshini wanajua wanavyochagua baadhi ya watu wachache wanaenda, hao wengine wote wanarudi nyumbani.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa shida inakuwa moja, sisi Wabunge humu wengi ikifika kipindi cha vijana wanahitajiwa JKT karibu kila Mbunge ana message za wazazi wanaomba watoto wao waingie kule, lakini wakimaliza tena wakirudi nyumbani, shida inakuwa tena kwa Mbunge yule yule tusaidie kupata ajira.

Sasa mimi ushauri wangu, nilikuwa napenda kushauri kwamba kwa kweli wanafanya kazi nzuri sana JKT, lakini wangeondoa masharti ya elimu, wakachua vijana wote wenye uwezo kwa sababu ninavyoitazama JKT ni kama sehemu ya kwenda kufundishwa maisha halisi ambayo tunaweza kuyafanya hata sisi ambao hatukupata elimu kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama mtu anaenda kufundishwa uselemala, anaenda kufundishwa kulima, anaenda kufundishwa kazi za kila siku, mimi najiuliza kama wanapanda watu cheo kwa kusimamia kazi za ujenzi, inakuwaje mtu unafundishwa JKT, unakaa miaka mitatu, unarudi tena na kusubiri kuajiriwa kwa shilingi 120,000, tunawafundisha vitu gani kule yani kama mgechukua watu wa darasa la saba ambaye anajuwa mimi nikitoka huku na taaluma yangu ya ujenzi, nikitoka shuleni ni kwenda kuomba kibarua nilipwe shilingi 20,000 kwa siku ambayo nitapata shilingi 360,000. Kwa hiyo mimi nilikuwa nadhani, tunatengeneza bomu kubwa sana na ndio maana tunaanza kuona vijana wanaandamana, wanakiukwa masharti ya kijeshi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niombe tu kwamba muone namna wenzetu wa JKT muondoe lile sharti la elimu, mchague vijana kwa uwezo na watu ambao watawaelewa na ninyi muonekane mnafundisha watu, wanaporudi huku wawe na kazi zao za kujitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Waziri, lakini pia nipongeze na Jeshi. Niliwahi kuchangia hapa nikazungumza suala la Mererani kwamba kulikuwa na upekuaji ambao haukuwa mzuri, lakini nikupongeze sana Waziri na Jeshi kwa sababu ule upekuaji tena hakuna. Umerudi upekuaji wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hii ndiyo maana kila siku mimi nasema nidhamu ya Jeshi ni kubwa sana na ninadhani kuna watu walituelewa vibaya, lakini nadhani ninyi mlivyokwenda kuchunguza mliona hiki kitu kinafaa na sasa mmeondoa na mnakagua vizuri na watu hawana kelele tena na kudhalilisha Jeshi letu ambalo sisi tunaliheshimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, nilitoa mapendekezo; mimi nashughulika na mambo ya madini, kwenye taaluma ya assessment ile wanayofanya pale niliomba, mimi naamini sana Jeshi, hebu chukueni vijana 100 muwapeleke wakasome, hawamalizi miezi sita, warudi wapewe hizo nafasi. Hawa waliopo bado tunapigwa na wanajeshi wako pale pale. Kwa hiyo, nilitoa ushauri, kama utaufanyia kazi nadhani baadaye utakuja kuona mafanikio kwa sababu mimi binafsi nina imani kubwa sana na Jeshi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninatoa ushauri na ninatoa ushauri kwa upole sana. Mimi kama ninavyosema, naliheshimu sana Jeshi la Wananchi, lakini sijui ni kwa nini wanajeshi wetu tumewaweka kama tumewasahau kidogo kwenye suala la makazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, najua Serikali inajitahidi kujenga, lakini mkarabati na za zamani. Hebu jaribuni kupita tu, mimi nachukua mfano mmoja, pengine wenzetu hawa wanajeshi hawana watu wa kuwasemea humu ndani, ukipita Mwenge pale unamuona mwanajeshi ametoka amevaa smart, anang’aa, angalia nyumba anayotoka. Nenda Mwanza, nenda kila sehemu, jamani hata kukarabati tu kupiga rangi kweli Mheshimiwa Waziri? Hata wewe mwenyewe ungeishi hiyo nyumba halafu unatoka nje unaendesha V8! Hii siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Jeshi letu linasifika Kimataifa, hata Wachina, Wazungu, wakija waone mwanajeshi anatoka kwenye nyumba nzuri. Tuna maghorofa, tuna majengo mazuri, kupaka tu rangi? Mheshimiwa Waziri, mimi kwenye shilingi kuhusiana na uchafu kwa kweli kwanza mimi niko jirani nao pale Mwenge, sitakubaliana nalo kabisa kama hutokuja na maelezo mazuri. Ninapenda uje na maelezo mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niliona nichangie tu hayo kwa ufupi kwa sababu Jeshi letu linafanya kazi nzuri na mimi nalipenda. Nilitaka nimshauri Waziri kwa hayo machache, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika Bajeti ya Wizara ya Niashati.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kukushukuru sana kwa message uliyotoa kwa vijana wetu ni nzuri sana wakaifanyie kazi. Cheti siyo issue, issue ni Maisha, kwa hiyo, mnasoma mpate vyeti ili muingie kitaa mpige kazi siyo kung’ang’ana kutuma CV kwa Wabunge kutafutiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri aliyoifanya. Wabunge wote tuliomo humu hakuna Mbunge amepata kura bila kutaja Wizara ya Nishati, hasa upande wa umeme. Ni kazi nzuri, tunaendelea kumwombea Waziri pamoja na wataalam wote wafanye kazi bila kuogopa, najua mtapigwa mishale, lakini sisi Wabunge tunawategemea maana 2025 tutategemea tena kuisema vizuri kulingana na ile ahadi waliyosema watamaliza vijiji vyote.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili niseme kuhusu suala la Bwawa la Mwalimu Nyerere. Niwapongeze sana Serikali na Waziri, sisi kama Kamati tulienda kutembelea mradi ule. Ni heshima kubwa sana, asilimia 85 ya mradi wasimamizi wake ni wazawa. Hii ina tafsiri nzuri, baadaye tutakapoanza kujenga mabwawa yetu mengine tutakuwa na wataalam waliobobea ambao tumewajengea uwezo kwa kuwapa zile nafasi za kusimamia mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la tatu naomba nizungumzie suala la depot za mafuta. Ndiyo maana mimi huwa nikisema humu kuna watu wananipiga mishale, sisi Watanzania ni wazuri sana kupanga mipango; Serikali iliamua kupanga mipango na kuwahamasisha wawekezaji wa ndani kwamba mnataka kuwa na depot Mtwara na depot Tanga ili kupunguza msongamano wa malori Dar es Salaam, lakini pia kulinda hata barabara zetu kule Dar es Salaam, mkahamasisha watu wakawekeza Mtwara na Tanga na Serikali Mheshimiwa Rais na viongozi wote wakubwa wameenda kukagua depot zile. Cha kushangaza baada ya wazawa hawa ku-invest kwenye hizo depot, wamekopa benki, Serikali imewatelekeza. Katika mpango mliokuwa mmepanga na tulipitisha sheria hapa kwamba mafuta sasa yatanunuliwa kikanda; Kanda ya Kaskazini watanunua depot ya Tanga, Kanda ya Kusini watanunua depot ya Mtwara, lakini hata yale mafuta yanayoenda nje ya nchi kwenye nchi zinazopakana na Tanzania baada ya ku-invest mpango huu umekufa, watu wamekopa hela kwenye mabenki sasa wako taabani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikuombe Mheshimiwa Waziri ile sheria tuliyoipitisha hapa ya kwamba mafuta yauzwe Kikanda, depot zipo na Serikali ninyi ndiyo wajibu wenu mlileta mpango huo mkawaingiza chocho wafanyabiashara, ni lini mnaanza kuusimamia mpango huu? Sheria na fine tulishapitisha hapa Bungeni watu waende huko, hata nchi kama Rwanda na Uganda mnaweza mkawapeleka Tanga wale wanaotoka Msumbiji wakaenda Mtwara. Hii mnakuza na miji mingine, unapopeleka malori zaidi ya 1,000 unafungua fursa za ma-guest na vitu vingine na hii inasaidia hata hiyo mikoa iliyoko pembezoni kuwa na uchangamfu. Mungu hakufanya makosa kutupa ziwa na tukaligawa katika bandari hizi tatu, nashauri sana Mheshimiwa Waziri akija hapa aje na majibu sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini suala lingine, tulienda kukagua sehemu ya uagizaji wa mafuta kwa pamoja (PBPA), ukiangalia kwa mwaka mzima kampuni za nje tu ndiyo zinachukua kazi hiyo, sisi kampuni za Tanzania tumekuwa kama wasindikizaji. Sababu ni nyepesi, mwanzoni walikuwa wanaagiza kwa pamoja na kampuni zote zilikuwa zinatakiwa ziwe ni za Watanzania, lakini baadaye sheria ikabadilika kwamba tuingize na kampuni za kimataifa, kampuni nyingi zinazo-bid na kushinda ni kampuni za nje lakini zina kampuni za kitanzania, hazitumii kuomba kwenye kampuni za kitanzania zinatumia kampuni za nje. Sasa wanaposhindana na Watanzania, Mtanzania ana mkopo wa asilimia 14 wa CRDB, hawa wenzetu wana mkopo wa asilimia 1 benki za nje. Cha kushangaza zaidi ikitokea Mtanzania umeshinda baada ya kulipa kodi zote za mafuta unatakiwa ulipe income tax na service levy, mtu akishinda na kampuni ya nje halipi income tax wala service levy. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikuombe sana, mimi niko kwenye Kamati hii, hiki kitu hakiwezekani Mheshimiwa Waziri lazima abadilishe sheria, atenganishe sehemu waagize wazawa na sehemu nyingine waagize hao wa nje. Ama zile kampuni za nje watumie zile kampuni zake za ndani ili Serikali iweze kukusanya kodi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, naomba sana wapangaji muwe mnanipanga siku ya kwanza. Hizi dakika tano mashine inachemka, naambiwa ahsante. Nakushukuru Mheshimiwa. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Musukuma. Mheshimiwa Joseph Zacharius Kamonga atafuatiwa na Mheshimiwa Benaya Kapinga.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niwe mchangiaji wa kwanza kwenye Bunge lako kwanza nianze kwa kuipongeza Kamati ya Nishati na Madini kwa kazi kubwa ambayo tumeifanya katika kipindi cha utekelezaji na ufuatiliaji wa miradi iliyotekelezwa kwa kipindi cha mwaka uliopita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia masuala yanayohusu TANESCO peke yake. Mimi ninatokea kijijini, ukifika vijijini sasa hivi tuna taharuki kubwa sana ya masuala ya bei yaliyotolewa na TANESCO.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Kamati mwaka jana tulikaa tukakubaliana kwamba tuchukue hata vile vijiji vya mjini tuviweke kwenye bei moja sawa na vijiji vya vijijini ili wananchi wengi waweze kuingia kwenye mfumo wa 27,000, lakini ghafla mabadiliko yametokea na kuwatenga watu wa mjini na watu wa vijiji. Sasa najiuliza, muda mwingi niko Dodoma na kijijini kwangu; nawaona hata Wagogo maskini wako humu humu ndani kwenye kata za mjini, lakini nikitoka nje ya mji nakuta kuna watu wako vijijini wana hadi ghorofa tatu wanaishi na familia zao. Sasa hiyo hesabu iliyopigwa kwa kweli ukiangalia kiundani naona kama kuna upendeleo. Niishauri Serikali, kwamba ni vizuri wakafuata ushauri wa Kamati, kwamba ile bei ya 27,000 iendelee mpaka kwenye zile kata za mjini ambazo nazo zina watu maskini kama walioko kule vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, suala la kukatika kwa umeme. Hili suala linaleta taharuki kubwa sana. Tuseme ukweli, Kamati imeona kwamba hakuna sababu za msingi, ukisikiliza ni kama ubabaishaji fulani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke, wakati umeme umeanza kukatika tulimwona Mheshimiwa Waziri wetu, Mheshimiwa Makamba aliruka hadi na helikopta akiionesha Tanzania kimataifa, kwamba tuna upungufu wa maji, mito imekauka. Chief Hangaya akaomba tukapata mvua, tumerudi tena kwenye mashine. Sasa, hii mitambo inaendeshwa kwa masaa, ndiyo maana Kamati tumeomba TANESCO walete schedule ya miaka mitano iliyopita service ilikuwa inafanyikaje na si kutuambia mitambo haikufanyiwa service. Kwa mtambo ambao haukufanyiwa service, kwa mitambo ya kisasa hii itapiga honi hakuna mtu atakayekaa humu ndani. Sasa ni kama ubabaishaji tu, hakuna sababu za msingi za kutukatia umeme mara kwa mara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imeshauri kwamba ifanyike service kimkoa, angalau kiupande upande na si kufanya kwa nchi nzima, inakaa gizani na Serikali imehamasisha watu waingie kwenye soko la viwanda vidogo vidogo na viwanda vikubwa. Hii inaleta taharuki kubwa sana. Tuombe TANESCO ije na sababu maalum inayotusababisha sisi tukose umeme katika sehemu nyingi za biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la bwawa la umeme. Niko kwenye Kamati sasa hivi ni mwaka wa sita, ninamshukuru Mungu. Kamati tumeanza kwenda kwenye bwawa hili tangu likiwa pori tukakuta kimondo. Tumerudi mara ya pili na mara ya tatu, ukifika kweli unaona kazi zinafanyika. Sioni sababu ya hizi swaga zinazoendelea, kwa sababu wakati Mama Samia anaingia tulilipa trilioni mbili, certificates zote zilikuwa zimelipwa, hakukuwa na madeni na Mheshimiwa Mama Samia amelipa trilioni moja, hatuna certificate inayodai, tatizo liko wapi? Ni swaga zinaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mnakumbuka hapa Mheshimiwa Waziri alitueleza kwenye Bunge hili kwamba mitambo imefika, tunasubiri crane iko barabarani. Sasa hivi crane imefika bado tunaambiwa yale mashimo ya kuweka ile mitambo iliyokuwa inashushwa kule chini yamejengwa substandard. Unajiuliza, wasomi wenzangu mnaniaungusha sana. Mnaniangusha sana. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na wakandarasi wako pale, tuna watu wanasimamia, mainjinia wamesoma, Watanzania na Wazungu, tunamaliza kujenga foundation ile tunaambiwa imejengwa substandard.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niwe mchangiaji wa kwanza katika hoja ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza sana Mehshimiwa Rais, Mama Samia kwa kazi kubwa na nzuri aliyoifanya kwenye majimbo na katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni dhahiri Wabunge tutakubaliana kwamba kazi imefanyika, tumetoka kukagua miradi mikubwa na midogo hakuna mahali ambapo tumekuta mradi haujapelekewa fedha; hii ni hongera kubwa sana kwa mama na imedhihirisha kweli kwamba kinamama mkiwezeshwa mnaweza wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema hivyo kwa sababu, mimi ninatoka Kanda ya Ziwa, tulikuwa na miradi mikubwa sana kule mradi wa Daraja la Busisi, Hospitali ya Kanda ya Chato, Hospitali ya Musoma…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Musukuma kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Matiko.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Musukuma, kwamba tunashukuru anapo-appreciate kuhusu uongozi wa kinamama lakini najua wanawake tunaweza bila kuwezeshwa. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Musukuma nadhani alikuwa ananyoosha pale mwanzo, naamini ulikusudia kusema hiki ambacho amekisema Mheshimiwa Esther Matiko.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, akina mama ni mama zangu walionilea, siwezi kubishana nao. Ni kama alivyosema, na iwe hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, miradi yote hii mikubwa niliyoitaja, imepelekewa fedha na inafanyika na inaendelea kukamilishwa. Hongera sana kwa Mama Samia na aendelea kuchapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa ushauri. Njua Mheshimiwa Rais, ana majukumu mengi sana na ndiyo maana tukawa na mawaziri na Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, mnapopeleka fedha nyingi kwenye majimbo yetu, inahitaji ufuatiliaji wa karibu wa watu wenye maamuzi; namaanisha mawaziri. Sasa kumekuwa tabia ambazo nilizungumza hata juzi, ile kwamba Waziri anataka kutembelea halmashauri tano mpaka sita kwa siku, hii haina ufanisi mzuri katika kutusaidia kwenye fedha mnazozipeleka kwenye majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni vizuri mkaenda specifically kwenye halmashauri moja mkasikiliza siku nzima, mkaona miradi na kusikiliza matatizo ambayo yako kwenye ile halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba kumshauri Waziri Mkuu, ule utaratibu wake wa kupelekewa kero na kwenda kutatua moja kwa moja kwenye halmashauri, ningeomba aendelee nao. Ukisikiliza Wabunge wengi humu hawawezi tu kutamka moja kwa moja, kila Mbunge ana matatizo kwenye halmashauri yake, na ukileta Mawaziri unaambiwa mchakato unaendelea, tunaunda Tume, tume hazitoi majibu. Inakuwa kama tunapeleka fedha halafu kama hatuwezi kuzisimamia; bado Watanzania hawatatuelewa.

Mheshimiwa Spika, nimeona mtandaoni tangu jana au juzi, kuna clip inazunguka ya Mheshimiwa Mpina; na ninayezungumza ni mimi usiingie kwenye kumi na nane. Na ile clip imechukua sehemu ambayo imeashiria mimi nimezungumza kwenye mchango wangu, halafu imeunganishwa ikawepo kwenye hotuba ya Mheshimiwa Mpina.

Mheshimiwa Spika, mimi kweli nililalamika sana kuhusiana na Bwawa la Mwalimu Nyerere kulingana na taarifa iliyoletwa na Waziri wa Nishati, na ni mjumbe wa Kamati. Baada ya yale majibu sikukata tamaa nilifuata utaratibu kwenda kwa Mwenyekiti, na Mwenyekiti na Wajumbe tukakubaliana tukakuomba kibali cha kwenda kuukagua mradi.

Mheshimiwa Spika, mimi ni balozi, naweza kusema ule mradi umeenda mara mbili ya ulivyokuwa umeachwa na Hayati Dkt. Magufuli, nimeenda kukagua mara nne. Kwa hiyo, tusitengenezeane ajali. Na sisi kama Kamati kwenye taarifa yetu mtaisikiliza mtaiona. Matatizo tuliyoyagundua si mradi, ni wataalam walimdanganya Waziri.

Mheshimiwa Spika, sasa nikisema mimi naomba ninukuliwe mimi, na mtu akitaka kutumia hansard yangu nina haki yangu kama Mbunge nisichukuliwe kwenda kutengeneza uzuri mtu.

Mheshimiwa Spika, mimi ni muathirika mkubwa sana wa Mheshimiwa Mpina. Nikimuangalia Mheshimiwa Mpina na hotuba aliyoitoa; mimi basi yangu mimi Mheshimiwa Mpina amei-cease mpaka leo inaozea kituoni, ilikutwa na Samaki watatu, hebu angalia samaki tatu... (Makofi)

T A A R I F A

MHE. DKT. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nilikuwa najaribu kuieleza Serikali, kwamba mambo haya ni vizuri tukayaangalia vizuri, kwa sababu sisi Wabunge tunapokuwa tunalalamika, huwa wanaona wenzetu kule chini kama tunawaonea. Lakini unavyowatendea wenzio ukitendewa na wewe uvumilie msumari uingie.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba kushauri. Kama alivyozungumza Mbunge wa Arusha, Mheshimiwa Gambo, kwamba kuna mfumuko mkubwa wa bei. Hili ningeomba kutoa ushauri wangu kwenye Serikali kwamba ukiangalia leo bei ya mafuta tunanunua mpaka 3,000 huko Kijijini.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba Serikali ichukue suala hili kama suala la dharura, tuone namna, hata kama ni kupitisha bajeti ya dharura. Serikali yetu kwa sasa inakopesheka, tumefanya hivyo mara nyingi, ilishuka bei ya korosho Serikali tukakaa hapa tukaipitishia tukaenda ku- rescue suala la korosho, sasa kuna mfumuko wa bei ya mafuta (Makofi)

Mheshimiwa Spika, najua kuna fedha ambazo tuliweka kwa ajili ya miradi ya maji, tuliweka kwa ajili ya miradi ya barabara, tunaweza tukaona namna kama ni kiasi gani kimebaki tukaziondoa hata tukaenda kukopa ili tufidie.

Mheshimiwa Spika, kwa hali ya kawaida, mafuta shilingi 3000, na tunakoelekea yatapanda mpaka 3200 Serikali isikae kimya, kazi ya Serikali ni kuwalinda watu wake. Sasa hili lionwe kama suala la dharura ili kama kuna uwezekano, walete agenda yoyote ya dharura hapa tuweze kutafuta fedha yoyote tuweze kushuka mfumuko wa bei hasa kwenye mafuta.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la TARURA, kila Mbunge anaitegemea TARURA hapa. Ukienda ofisi ya TARURA hapa Makao Makuu utapishana na Wabunge 10, 20 kwa siku. Lakini kumekuwa na shida sana kwenye TARURA, ukisikiliza Waziri alienda pale wakasema wanaunda Tume hakuna mwelekeo.

Mheshimiwa Spila, leo sisi tunakuwa Wabunge wengine wawili kwenye halmashauri moja. wameondoa meneja wa kila halmashauri wameweka meneja wa Wilaya. Lakini unamuondoa yule uliyemshusha unambakisha pale pale na cheo ni kimoja, na wote walikuwa ni mameneja; kazi hazienda wilayani huko.

Mheshimiwa Spika, na ukiangalia, TARURA ndilo tegemeo letu kila mtu hapa ndani; tunatoa fedha nyingi; na leo Rais kawaongeza zaidi ya bilioni 900 lakini fedha walikuwa nazo, hata kipindi mwaka wa kwanza wamebaki na bilioni 72, mwaka wa pili bilioni 100, mwaka wa tatu bilioni 130, hizi ni ripoti CAG. Kwanini sasa tusione namna ya kuiboresha TARURA ikakaa vizuri ili hizi fedha zisibaki kama bakaa zitumike kwa sababu ukihoji humu kila mtu ana barabara mbovu. Lakini fedha zinabaki na bado tunaendelea kuwaongeza.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu wa mwisho, naomba sana; Mhesimiwa Shabiby alizungumza juzi hapa, suala la mafuta kuagiza kwa bulk procurement, hili suala hata kama tungeongeza hela bado mafuta hayawezi kushuka. Biashara huria ndio muoarobaini wa hili suala, aruhusiwe kila mtu alete mafuta, kazi yetu Serikali tukusanye kodi, kazi yetu Serikali ipime TBS mafuta ni mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mafuta yako mengi sana huko ya njia za panya yanini tungeshusha bei za mafuta. Sisi hatuna sababu ya kuanza kusimamia mafuta ya warabu, sisi tunachotaka ni mafuta yashuke bei. Tukiruhusu kila mtu alete mafuta watu wataunga na mitaji, wataleta mafuta ya wanavyojua wenyewe, sisi tutakusanya kodi na tutasimamia suala viwango, mafuta yatashuka bei. Nashukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia Wizara hii ya Madini mimi ni Mjumbe wa Kamati.Kwanza nianze kwa kumuunga mkono mjumbe aliyemaliza kuzungumza dadaangu tulivyopitisha hii Sheria ya kurudisha masoko kwenye maeneo husika sisi watu wa Geita ndiyo tulileta hiyo hoja humu mwaka 2017/2018 na Bunge lako Tukufu likatupitishia Sheria.

Mheshimiwa Spika, sisi watu wa Geita ni wanufaika namba moja, na watu wa Simanjiro ningewashauri waje wajifunze kwetu, kwasababu tunakusanya pale sokoni takriban bilioni tatu. Kwa hiyo ningeomba tu kila mtu amepewa neema tofauti, na Mheshimiwa aliyezungumza hii hoja aridhike maana ana utalii mwingi. Arusha ni sehemu ambayo ina utalii mwingi, tusioneane wivu tuache na hii miji midogo nayo ikue kwa kukusanya Service Levy.

Mheshimiwa Spika, suala la pili nilikuwa naomba kushauri kuhusiana na suala la refinery. Mheshimiwa Waziri anafahamu tumetengeneza refinery kubwa sana Geita pamoja na Mwanza na sisi Kamati tulienda kutembelea. Hata hivyo, ninaona kama tumewaingiza chaka wale waliowekeza ile biashara pale. Kwa mwenendo tunaoenda nao sisi wazoefu wa ile biashara; ningependa Mheshimiwa Waziri unisikilize vizuri; hii dhahabu mpaka inaenda kwenye refinery unakuwa umeshatozwa mirabaha ya kutosha, wewe unafahamu; lakini ukifika pale ukishafanya tena usafi ule unatakiwa ulipe tena asilimia sita.

Mheshimiwa Spika, haiwezekani kulipa asilimia sita ilhali hii dhahabu naweza kuibeba nikaenda nayo nje kule Dubai nikaisafisha kwa 0.25. Kwa hiyo ninaona kabisa kwamba kama mnaweza kuja na Sheria kidogo ya kibabe kwamba usisafirishe mpaka ufanyie hapa lakini hebu jiulize ungekuwa wewe ndiye mfanyabiashara. Kwa hiyo ningeomba Serikali ione namna ya kushusha hata kama ni asilimia mbili ikawa kivutio; na hizi ndizo attachment za Royal Tour ya Mheshimiwa Rais kwamba watu wanapokuja hapa waje wajifunze vitu vingi tusiweke bei kubwa watu wakawa tena watoroshaji tukaanza kukamatana na kunyang’anyana ni vizuri tukatembea tukaiga kwenye hizo nchi ambazo tayari zina refinery na watu wanapeleka kwenda kusafisha.

Mheshimiwa Spika, suala lingine, ninashauri Mheshimiwa Waziri turudishe suala la minada ya madini. Tunapofanya minada ya madini tutaingiza watalii wengi sana kuja kununua kwenye masoko, na tutangaze tuna madini ya aina gani. Watu watakuja, asiponunua dhahabu asiponunua madini atanunua hata kinyago naona tutakuwa tunaendelea kum-support Mheshimiwa Rais katika ile filamu yake ya Royal Tour. Twende mbali zaidi kwamba Mheshimiwa Rais hakuweza kumaliza kuvitembelea vivutio ambavyo viko kwenye nchi yetu. Tutakapofanya hii minada wazungu watakuja na watu wengine wageni tutapata kipato kikubwa zaidi. Kwa hiyo, nilikuwa naomba suala la minada pia liweze kurudishwa.

Mheshimiwa Spika, lakini lingine, nimesikia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, kwamba ana mpango wa kufungua duka sijui la vilipuzi. Nilikuwa naomba sana kuishauri Wizara; unajua kwanza Shirika letu la STAMICO ndiyo kwanza linaanza kupanda lina madeni na uwezo wake ni mdogo; biashara inatakiwa iachiwe watu wa Private Sector kwa sababu kwenye Private Sector sisi tunapeana kukopeshana ninaweza nikachukua kilipuzi au nikachukua carbon nakudai inabidi nikasubirie mpaka uchome.

Mheshimiwa Spika, sasa ninyi watu wa procurement sijui ugavi sijui vitu gani tunaenda kuziteketeza hizi hela wakati shirika lenyewe halijasimama tuiachie private sector ifanye hizi biashara kuliko kuingia kwenye vitu ambavyo naona hatutafanya vizuri.

Mheshimiwa Spika, lakini lingine nataka nichangie, nalo ni kuhusu dhahabu inayopelekwa sokoni. Mheshimiwa Waziri upatikanaji wa dhahabu wewe umetoka kwenye mkoa wa dhahabu ninaweza kuwa hata natembea nikakaokota barabarani pakuuza ni sokoni. Sasa, nikifika sokoni kumeanzishwa mtindo, kwamb watu wako tena wanataka mpaka niwe na risiti nilikoitoa dhahabu. Sisi lengo letu ni dhahabu na nchi yetu kimataifa ina dhahabu ambayo haina matatizo kwa nini tuanze kuhojiana? Kwa nini tusiachie uhuru watu ambao pengine wanapata dhahabu kwa njia kama za kuokota iweze kuuzwa pale sokoni?

Mheshimiwa Spika, la mwisho, mimi natoka mkoa wa Geita sisi ndiyo wanufaika namba moja wa CSR. Nimemuona mkuu wa Mkoa wa Mara anafukuzana na Afisa Mahusiano kwa sababu ya kutokutekelezeka kwa miradi. Sisi watu wa Geita ni waathirika wakubwa sana kwenye miradi ya CSR, na kumekuwa na mabishano kati ya mgodi na halmashauri nakuomba Waziri utakapohitimisha ili nisichukue shilingi yako uniambie ni lini uko tayari tuwaite GGM kwako na sisi Baraza tuje kwako ili uje utuwekee msimamo mzuri ili kazi zikaweze kwenda kutekelezeka. Nashukuru sana.
Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niwe mchangiaji wa kwanza katika hoja iliyotolewa na Mheshimiwa Kigua kwa ajili ya maslahi mapana ya Taifa letu lakini pia ya wananchi wetu ambao tunawawakilisha humu Bungeni. Nikupongeze pia wewe kwa kukubali kutusikiliza.

Mheshimiwa Spika, sisi tunaotoka kijijini leo bei ya dizeli ambao kwenye Majimbo yetu wengi tunatumia mafuta ya vidumu leo tunauziwa mafuta shilingi 5,000; hii ni hali mbaya sana na ndiyo maana busara yako imeona namna nzuri ya kuweza kutusikiliza.

Mheshimiwa Spika, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Nishati; nilikuwa nataka kuomba Serikali itueleze tu ukweli, kwamba mafuta haya ambayo yamepanda bei juzi ni mafuta yamenunuliwa mwezi wa pili, sasa yamepanda yakiwa kwenye meli. Pamoja na kwamba bei zina-reflect Ulaya, lakini yakiwa tayari yameshanunuliwa kwenye meli bei imeongezeka. Sasa lazima Serikali ione namna.

Mheshimiwa Spika, ni mimi ni mmoja wa wafanyabiashara. Sisi tunacheza na namba tu, ukilegea kwenye namba sisi tunapita hapo hapo. Kwa hiyo, ni vizuri na ni lazima Serikali ione namna.

Mheshimiwa Spika, wewe ulikuwa humu Bunge lililopita, iliwahi kushuka bei ya korosho hapa Serikali ilipeleka Jeshi kwenda ku-rescue ile situation ya korosho; na baada ya hapo mpaka leo hakuna mtu anachezea bei ya korosho kwa sababu wanajua kabisa kwamba kuna tahadhari tukileta mchezo Serikali itaingia kwenda kuchukua hii biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe, Serikali kwenye hili hakuna namna, yaani kazi ya Serikali ni lazima kutuangalia sisi wananchi wake. Kama hali inatokea ya dharura kwa nini Serikali isiwe na dharura? Tuna dola kwenye benki, BoT tuna dola, hili jukumu kama linakuwa ni la kibiashara kwa nini Serikali isichukue dharura ya yenyewe kuagiza mafuta angalau ikakubali kula hasara hata kwa kitu kidogo? Lakini kama hamna, tuone namna kabisa kama Bunge, hii hali siyo nzuri na bado mafuta mwezi ujao yatapanda tena kwa takriban shilingi 3,800. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili suala halikubaliki, sisi Wabunge, kama kuna kodi tuliziweka kwenye mafuta, kuna vitu tuliweka tuone namna ya kuondoa hizo kwa dharura hii ya miezi mitatu ili mafuta yarudi kuwa chini na wananchi waweze kufaidi Serikali yao.

Mheshimiwa Spika, na nipongeze pia Serikali, nimeona hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mawaziri mliokaa jana; hii ndiyo Serikali ambayo tunaitaka, siyo mkae kimya. Sisi tulalamike na Serikali ilalamike hapa, tokeni na jibu. Nimeona mmesema tuwape muda, sisi kama wawakilishi wa wananchi tunasema tumekubaliana na hilo; lakini sasa mtoke na kitu ambacho hata kama ni dharura Bunge tukae tena kutengua hata kitu chochote kwenye bajeti ili tuone namna ya kupunguza bei. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi yetu inakubalika kukopa Kimataifa na tunakopa, tukopeni tufidie hizi gharama ili mafuta yaweze kushuka kwasababu kwa sasa hakuna Mtanzania atakayeweza ku-afford mafuta. Halafu hili Waheshimiwa Wabunge hata sisi wenyewe linatupiga; kwa sababu tunalipwa mileage za kwenda vijijini, leo mimi mileage yangu ya kwenda Geita inaishia Shinyanga, sasa kutoka Shinyanga kwenda kule na kurudi ninarudije, na mimi ni Mbunge bado kuna watu wa chini.

Mheshimiwa Spika, mimi ni msafirishaji yaani kwa sababu tu watanzania tuna nidhamu ya kuiheshimu Serikali na kuwapa muda. Hebu jiulize msafirishaji aliyekuwa anapeleka abiria kwa shilingi 30,000 leo Mwanza. Leo mafuta yamefika shilingi 3,400 bado nauli shilingi 30,000, hili haliwezekani lazima sisi kama Bunge tukubaliane tuishauri Serikali na Serikali ije na kauli nzuri. Hatua mliyoianza ni nzuri, hatutaki tena kusikia tunalalamika, mkae mtoke na kauli moja ili wananchi waweze kufaidi na Serikali yao ya Awamu ya Sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye Wizara ya Elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo ameifanya jana na leo imesomwa hapa Bungeni. Ni kazi kubwa ambayo Watanzania wengi tulikuwa tunaisubiri na sasa amewaachia kazi Mawaziri mfanyie kazi. Watanzania hatutaki kusikia namba, kwamba tutawapa Bilioni 100 halafu Watanzania wasiosoma wenye elimu ya kawaida wanauliza hiyo ni bei gani imepungua kwa lita? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mpaka tarehe moja hiyo mliyotangaza mnatakiwa muwe mmeshatamka kwamba lita itauzwa bei gani ya mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ninakushukuru Mheshimiwa Waziri kwa taarifa nzuri, umeongea vizuri, umeeleza vizuri, pamoja na Kamati pia. Mheshimiwa Waziri mimi nina machache sana kuhusiana na suala la elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri kila biashara unayoifanya lazima iwe na tathmini. Naongea kitu ambacho pengine naweza kuwa tofauti kidogo na wenzangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la elimu bure, Mheshimiwa Waziri kuna kipindi sisi Wabunge unashindwa hata kwenda kutembelea Shule za Msingi huko Vijijini na shule zingine kwa sababu ukifika pale yaani ni kitu cha aibu sababu ni elimu bure. Unakuta darasa moja watoto wanasoma 500, Mwalimu mmoja anafundisha, sasa kwa hatua kama hii unakuta watoto wako Darasa la Tatu hajui hata kuandika jina na wewe bahati nzuri ni Profesa nataka uniambie kwenye majibu yako, hivi ungekuwa wewe una vipindi vitatu vya watoto 400 - 400 ungewezaje ku-concentrate kusahihisha halafu na kupanga masomo hata ya baadae. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, ni vizuri tukafanya tathmini kama tulikosea ni vizuri tukarekebisha. Huu mfumo tunaoenda nao elimu bure tunalundika tu pesa, watoto wanaenda mashuleni lakini hawapati elimu na Serikali inazidi kutumbukiza hela ambazo hazirudi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakupa mfano mimi nina shule ina watoto 3,500 ina Walimu Tisa. Hebu jiulize ungekuwa ni wewe ungewezaje kufundisha?

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuomba Mheshimiwa Waziri ukipata nafasi ya kuwa unazunguka huko Mikoani jaribu kufanya ziara za kushtukiza kwenye shule unaweza ukawa unaongea na Wabunge nataka kutembelea shule fulani ukafanya ziara ya kushtukiza usiende na ving’ora vya magari watajiandaa, ukakuta kile kipindi cha Saa Nne mtu anasahihisha hata haangalii daftari anatia tu hivi watoto wamepanga mstari watu Zaidi ya mia nne. Sasa tunatumbukiza hela kwenye sehemu ambayo kiukweli baadae mtakuja kutulaumu. Mnatengeneza bomu ambalo hatuna uwezo wa kuja kulikabili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumza kuhusu elimu ya juu. Serikali inatoa mikopo tumeambiwa hapa kwenye taarifa kwamba wameshapewa bilioni 400 sasa wameongezewa mpaka bilioni 500, lakini ningekuwa mimi ninayefanya biashara, hili suala nafikia mahali najiuliza, kama Serikali inatoa hizo hela na hatuna uwezo wa kuzikusanya, nimesikia mjumbe mmoja anasema tufungue benki yaani tuajiri wataalam wazidai kama benki, halafu mwisho wake itakuwaje.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina wazo, kwa kuwa Serikali ina watu wasomi na wabunifu na tuone namna ya kwamba watu wanapopewa mikopo na wanafanya research, mtu anaanza mwaka wa kwanza anafanya research mpaka mwisho wa elimu yake, ana-submit research yake, ana-graduate, kwa nini ile research isigeuke kuwa biashara? Kwa sababu research ile kwa kila mtu aliyefanya research yake hiyo tayari ni hela na wewe unaikubali unamfaulisha, unampa cheti. Sasa kuliko kumpa mtu hela halafu anamaliza degree yake umekopesha asilimia 50, hawajaajiriwa wote, wameajiriwa asilimia 15, halafu hizi hela zimepotea wengine wanakufa bila kurudisha deni, wengine wamekaa wamekuwa machinga hwajulikani waliko.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ningeomba tukubaliane na wenzetu wanaosimamia hii mikopo ya elimu ya juu kwamba tuwe na madirisha mawili tuwe na dirisha moja kwa ajili ya kukopesha ili mtu asome, lakini akifanya vizuri wewe ukitoa GPA, kile cheti chake kiwe bond kiwe dhamana kuwe na dirisha la kukopesha kulingana na research yako hata kama ni milioni tatu. Huwa najiuliza kweli ndugu zangu tunaweza tukawa tunaonekana kama tunaongea vitu vya ajabu, lakini naomba niulize swali la moja kwamba leo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaandaa utaratibu kwa machinga mtu ambaye hajulikani leo atakuwa hapa kesho atakuwa hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaandaa utaratibu tunatengeneza utaratibu waanze kukopeshwa na mabenki na tumesikia taarifa tayari wameanza kukopesha sijui Dar es Salaam na wapi, inakuweje machinga anakopeshwa kwa kitambulisho, wameshindwa kutengeneza utaratibu kwa mtu cheti cha degree akapata mkopo akaenda kuwa machinga ambaye amesoma na watu wangekuwa na nia hata ya kusoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, pendekezo langu naomba Serikali ifikirie kuwa na madirisha hayo mawili; tukopeshe kwa ajili ya kusoma; halafu tukopeshe kwa ajili ya mitaji kwa ajili ya watu kwenda kujitegemea. Mimi binafsi ungeniuliza ningesema hata leo tuondoe hiyo elimu bure ya msingi, unamtengenezea msingi usiojitambua, akifika huko juu anakuwa machinga mzigo ambaye hajui kila kitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nadhani tuwe tuna madirisha mawili kwenye Vyuo Vikuu, mtu anapomaliza Chuo Kikuu apate elimu ya mkopo na atumikie mkopo alipe na deni pamoja na ile aliyeikopea mwanzo. Faida ya pili, nimesikia Serikali baadhi ya mabenki yameanza kutoa mikopo kwenye elimu ya kati certificate na diploma, nikajaribu kujiuliza hiki ni kitu kizuri sana, lakini nikawa najaribu kuwauliza watu wa NMB hii inakuwaje, dhamana ni kitu gani kwa sababu certificate, hiki cheti hakikopesheki.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanakopesha kwa dhamana gani wanasema tumeanza na watoto wa wafanyakazi. Hii ni aibu kubwa sana yaani watoto wa maskini ambao wana akili nyingi wanashindwa kwenda kusoma kwa kukosa hela, tunaenda tena kuchukua mtoto wa mfanyakazi, tunamtengenezea utaratibu wa kukopa, kwa nini wasianze na watoto wa maskini na vyeti vyao viwakopeshe wao wenyewe. Kwa nini tukimbilie kukopesha watoto wa watu ambao wana uwezo wa kusomesha watoto wao, kwa hiyo nilikuwa naomba...

MHE. STANLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. STANLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naomba nimtaarifu mzungumzaji kwamba wanaokopeshwa sio watoto ni wazazi kwa sababu moja tu kwamba, mtoto aliye chini ya umri wa miaka kumi na nane wa mujibu wa sheria za nchi yetu hawezi kukopeshwa na benki na watoto wanaokwenda kusoma hivi vyuo vya kati ni wale waliomaliza kidato cha nne hawajaenda kidato cha tano wala cha sita. Kwa hiyo bado ni under 18 na ndio maana anaanza kukopeshwa mzazi kwanza.

NAIBU SPIKA: Mhesimiwa umeipokea taarifa?

MHE. DKT. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea. Nilichokuwa naongea mimi hana tatizo na mawazo yangu lakini ombi langu ni kwamba kwa nini tukaanze na watoto wa dizaini hiyo wa wafanyakazi hawa watoto wa maskini wenye akili wanaotaka kuendelea tuweke masharti nafuu kwenye benki zetu hizi, tuwakopesha hata wazazi maskini wenye watoto wao wako tayari kuweka bond hata mashamba, sio lazima tukaweke pesa ikubali isikubali benki kwamba tunaweza kuweka hata mashamba, au mbuzi au kondoo ili mtoto wangu asome na hiyo ndio kazi ya Serikali kusaidia watu wasiokuwa na uwezo, tunasaidiaje mtu ambaye ana uwezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchangia hayo tu kwa leo nakushukuru. (Makofi)
Azimio la Bunge la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuimarisha demokrasia nchini na kukuza diplomasia ya uchumi
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kutoa shukrani na pongezi kwa Mheshimiwa Rais.

Kwanza naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Chiwelesa, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais pia tunamshukuru Mungu kwa kutupa Rais msikivu, kutokana na kipindi ambacho kwa kweli Mheshimiwa Rais amepokea madaraka haya hakupokea kwa njia ya kawaida, kwa hiyo hakukuwa na maandalizi. Nimshukuru pia kwa kuwa msikivu, tumepita
kwenye majungu mengi kuna watu wameitwa Sukuma Gang humu, kuna watu wameitwa majina tofauti, kuna watu wamepewa makundi tofauti, lakini tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa usikivu wake, ameendelea kuchapa kazi na kuwaacha wapuuzi wanaounda makundi na kuchafua wenzao waendelee nao, pia kazi zetu za Serikali ziweze kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana mimi ni mmoja wa watu ambao nilimwangalia sana Mheshimiwa Rais siku anaenda kwenye mkutano wa CHADEMA kule Kilimanjaro, yaani nilikuwa najiuliza hii CCM yetu tunakwenda kuitumbukiza wapi? Lakini baadae nikaja kuona mtu mpaka kufika kwenye cheo cha Rais ujue amepitia mambo mengi sana.

Mheshimiwa Spika, Watanzania wengi Wana-CCM kule vijijini hawakumwelewa Rais, lakini baadae mimi nilivyokuja kutafakari, leo nataka niwaambie hivyo ndiyo maisha ya wanasiasa tunaishi, kwamba Mheshimiwa Rais alivyoenda kuwasikiliza na kuzungumza nao na kula nao chakula, haya ndiyo maisha yetu wanasiasa. Hata Watanzania mkituona tunazodoana humu na upinzani, tunatoka pale nje tunanunuliana chai.

Kwa hiyo, niwaombe Watanzania sikilizeni hoja za maendeleo kuliko kusikiliza mipasho ya kwenye majukwaa na Mheshimiwa Rais ameonesha mfano, ameenda kuwasikiliza wamepiga cheers lakini sisi huku tunapiga kazi. Kwa hiyo, haya ndiyo Maisha yetu wanasiasa huwa tunaishi hivi. Msije mkasikiliza maneno yetu huku juu wanasiasa halafu mkaenda kuandamana na kuumizwa miguu. Sikilizeni hoja zinazojibu matatizo ya wananchi wetu huko vijijini.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, nazungumza suala la Mkaguzi (CAG); kwa kweli mimi ni Mbunge huu mwaka tunaenda wa nane, nimemuona Mheshimiwa Rais juzi alivyozungumza kwa ukali mpaka akatumia na kaneno ka kizungu wale wenzangu kule hawakukaelewa akasema stupid! Ni kaneno kagumu sana sidhani kama anavyosikiliza Wabunge mnavyosema wale waone milango hakuna mtu anaweza kutoka kwenye mafuta kwa njia ya hiari nchi hii hayupo.

Mheshimiwa Spika, natoa mfano, Mheshimiwa Mbunge Ng’wasi Kamani kwenye Bunge lililopita yeye ni Mjumbe wa Kamati ya LAAC, alitoa mfano mzuri hapa akasema, kuna Mkurugenzi ametoka Ilemela ana tuhuma ya wizi wa shilingi bilioni 11 ameletwa kwa Mheshimiwa Musukuma, kwa miaka 22 sijawahi kupata hati chafu, nimo kwenye milioni sita, kwamba mtu anaiba huku halafu ninyi wenyewe mnamhamisha mnampeleka Halmashauri nyingine, huku anaendelea na uchunguzi anachukua pesa zetu kugharamia kesi ya Ilemela. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikuombe sana ngoma hii ikija humu kama alivyosema mwenzangu Mheshimiwa Tabasam Hamis Mwagao hapa, katika vitu ambavyo Spika Mheshimiwa Dkt. Tulia tutakavyokukumbuka, hatutaki tena kupiga swaga, maana hizi swaga tumepiga mno kila taarifa ya CAG tunaongea, Serikali mnatutengenezea uadui bora mmalize wenyewe, tunataja watu watu hawachukuliwi hatua.

Mheshimiwa Spika, mtu anachukua kesi anaenda anapaki TAKUKURU, hivi TAKUKURU unachunguza mtu CAG ya mwaka jana halafu tena unakutwa na CAG ya mwaka huu? Jamani kama huko TAKUKURU na kwenyewe kuna TAKUKURU si na kwenyewe kuundiwe timu ya kuwachunguza? Tunaelekea wapi? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, haiwezekani tumejadili mambo haya mwaka jana tukataja watu, Kamati ya LAAC imeletwa taarifa na ikataja Halmashauri zaidi ya tisa, halafu hawahawa
wamepata Hati Chafu! Mheshimiwa Rais amefika hatua ya kusema pumbavu, sasa labda aje asomewe taarifa ya mwakani akiwa na kiboko mkononi, kama Bunge hatutachukua hatua ya kumsaidia! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama sheria zetu tulizitengeneza ni mbovu, hili Bunge ndiyo Bunge la wananchi wote, hatuwezi kuwa tunamuona Rais, ina maana kama Rais mwaka jana alisema atakayechezea pesa zangu za miradi ataitambua sura yangu halisi, maana yake hawa waliochezea hizi pesa wamemvizia Mama wakachungulia dirishani wakaiona sura? Sasa wamerudi kwa utaratibu mwingine haiwezekani! (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kauli ya Mheshimiwa Rais mwaka jana mnisikilize vizuri, alisema jamani kama mnakula kuleni kwa urefu wa Kamba, hawa watu hawanunui kamba za katani, wananunua manati likijaa linatanuka! Lazima hili Bunge kwa mara ya kwanza tuoneshe mfano, haiwezekani. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana, naunga mkono hoja tunasubiri ngoma ije hapa tulale nao mbele. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa Mwita hayupo nadhani nitakula na zake nipate 10, hiyo ni zali la mentali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwanza nianze kwa kukupongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kazi kubwa sana kwa kweli uliyoifanya kwenye kipindi cha Bajeti iliyoisha. Mheshimiwa Waziri ni Mbunge nina miaka saba humu ndani. Unaona mishale siyo mingi, kiukweli umefanya kazi kubwa sana katika kila Jimbo tuna kila sababu ya kukupongeza yaliyoko ni madogo madogo ambayo tunahitaji kukushauri uyafanyie kazi ili baadaye mwakani mambo yaendelee kuwa mazuri zaidi tunapoenda kujiandaa na Bajeti nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukushauri sana Mheshimiwa Waziri, Mchango wangu wa leo mwingi nitakushauri. La kwanza; unakumbuka tulikuwa wote pale kwenye vurugu za Kariakoo, watu waligoma tukashinda siku nzima pale na sisi tulishawaambia mapema humu, mkatanguliza mizaha sasa naomba nikushauri. Mbunge mwenzangu Kanyasu hapa alilalamika kuhusiana na utendaji kazi wa mtumishi wa TRA pale Geita anaitwa Bwana Njau kwamba ameshika mtu akiwa kwenye drip ya diagnosis ya kusafisha figo chini ya kiti yaani yuko kwenye stuli na akajibu majibu. Kesho yake mkafuta kesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nikwambie sijui mnataka labda na Geita nako kuandamane kwa sababu mtendaji huyu ana miaka karibia nane pale na kila siku watu wanalalamika. Anaenda anafunga biashara ya watu yaani wewe akikuona una duka la piki piki linafanya vizuri anakuletea kodi, anakuchimba mkwara, anafunga account baada ya wiki mbili yeye anafungua duka la kwake. Ukienda ukiangalia watu wote wenye biashara ya bar pale Geita wanaombwa risiti toa hivi, kesho unafungiwa account yeye bar yake inafanya twenty-four, seven na haina hayo mambo ya risiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimuombe Waziri nimekutajia anaitwa Njau tunalalamika hapa kwa mara ya mwisho. Vinginevyo kitaumana kule. Kama ni mzuri mchukue mpeleke wilaya nyingine, kwetu Geita ametosha tuletewe watu wengine. Hatuhitaji kuendelea kulalamika. Tutachukua maamuzi maana na sisi wananchi wametuamini kule wametuamini tuwasemee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili; nataka kujiuliza na bahati nzuri Ndugu yangu Mwigulu yeye ni mchumi. Tunahitaji kuwa na viwanja vya ndege vilivyo na biashara kubwa. Kiwanja cha Ndege cha Mwanza hivi mmetuonaje yaani kila mwaka sisi mnatusomea tu takwimu, mnatupiga tu kanzu, tunasikia tu mabilioni, kiwanja kiko vilevile. Jengo limejengewa speed limewekewa vioo mpaka vimeanza kuanguka. Tumelogwa na nani Mheshimiwa labda utuambie tuna tatizo gani tulichowakosea? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara ya ndege kwa Tanzania hapa ukiondoa Dar es Salaam kiwanja cha pili kilicho busy ni Mwanza, tatizo ni nini? Haiwezekani, tulikuwa na Mkuu wa Mkoa Gabriel aliyefukuzwa anasema kiwanja kiwe cha halmashauri. Amekuja mwingine aliyepelekwa Morogoro na yeye yule yule. Nimuombe Ndugu yangu Makala na nikuombe na wewe Waziri. Tunahitaji kuwa na kiwanja cha kimataifa cha Mwanza. Kwanza mmenunua ndege kubwa hii ya mizigo. Mnaitoa wapi mizigo kama Kanda ya Ziwa uwanja hauendeki? Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri tunahitaji kuwa na kiukweli Mheshimiwa Waziri usipokuja na jibu zuri kuhusiana na Kiwanja cha Ndege cha Mwanza, hii imeshakuwa ni too much, ni dharau. Tutasimama Wabunge wote wa Kanda ya Ziwa hatutakubaliana na kukupitishia bajeti yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Mheshimiwa jengo lipo, ugomvi uliopo ni kati ya halmashauri. Halmashauri ilitoa shilingi bilioni mbili sijui Serikali rudisheni, unatoaje hela kulia unaweka kushoto? Chukua maamuzi tutengenezee uwanja. Tumechoka kupigwa swaga, mwaka wa saba kila mwaka tunaletewa Bajeti ya Uwanja halafu hivyo hivyo, eeh? Haiwezekani leo ndege zote za Tanzania hapa biashara kubwa iko Mwanza. Tunaingiza fedha mnatuona sisi mbahau tunaona tu watu wanaenda hatuwezi kukubali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, usipokuja na majibu mazuri Mheshimiwa, kutoka Mwanza kwenda Serengeti ni kilometa 90 tunataka kuona wazungu. Tunataka kuona wazungu wanatua Mwanza, hivi hamjiulizi hata matajiri wakubwa wanaotoka Ulaya na jet wala hawaendi Kilimanjaro kwa sababu ni mbali. Kilometa zaidi ya 500. Ukitoka Mwanza wanatua Mwanza wanaacha jet wanaenda na ndege ndogo pale dakika 15 wanaona wanyama tatizo liko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumejenga mahoteli, tumejenga kila kitu na Serikali imewekeza hoteli kubwa sana pale Kapripoint, mmeliacha tu limekuwa jumba la kulala popo kwa sababu hamna mikakati mizuri. Nikuombe Mheshimiwa Waziri ili tusiumane huko mbele nikuombe sana Mheshimiwa Waziri unapokuja hapa ututambie Uwanja wa Ndege jengo lile hebu hata wewe Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ukipita pale Mheshimiwa Waziri unaona mashine kubwa kabisa zimeletwa pale wanalala bundi tu mle halafu tunakaa hapa kupiga makofi, hatutapiga makofi mwishoni hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho; suala la mafuta, kwanza Ndugu yangu Mwigulu una wakati mgumu sana na nikuombe uchukue maamuzi. Nilijua utakuja hapa na taarifa ya kutuambia umepandisha bei, umepandisha ushuru wa mafuta yanayotoka nje ili shemeji zangu wa Singida wale wanaoshinda barabarani maelfu na maelfu wamening’iniza madumu mafuta yao yaende bei kubwa. Hivi kweli watu walivyolima vile kweli ndugu zangu, shemeji zangu wa Singida wale tushushe tena mafuta leo yanarudi shilingi 40,000, shilingi 8,000 kwa lita tano?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Mheshimiwa Waziri kuku kaangukia kwa sheikh kwa hiyo, inabidi uangalie unachinja kuanzia mguuni au unachinjia shingoni. Watu wanakuangalia tunahitaji kuona zao hili na wakulima hawa hawakatishwi tamaa na kushuka kwa bei. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho dakika moja...

MWENYEKITI: Ahsante sana, la mwisho lile kwa hiyo tayari umemaliza, ahsante sana.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sekunde moja. Mheshimiwa Mwigulu, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana sisi tunatoka kijijini. Nyumba zetu kule kijijini ziko hoi usije tena na swaga hapa brother ya kutuletea kutuambia unaongeza buku kwenye cement acha. Njoo na mawazo ya kushusha, tumechoka kulala kwenye matembe na sisi tunataka kuwa na mabati kama mlivyo watu wa Dar es Salaam na mikoa mingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa Duniani na kupewa Tuzo ya mafanikio ya ujenzi wa miundombinu
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Rais. Kweli Watanzania tuna kila sababu ya kujivunia uongozi wa Mama Samia ukizingatia kwenye wakati tuliopita ni wakati mgumu sana, lakini hata baada ya kuondokewa na mpendwa wetu Mheshimiwa Magufuli, tumempata Rais ambaye ameenda kuonesha Afrika kwamba Tanzania ni nchi ambayo inadumisha amani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimemsikiliza mchangiaji mmoja dada yangu Mheshimiwa Tendegu na mimi nimekuwemo Bungeni huu unaenda mwaka wa saba, ni azimio la kwanza kwenye Bunge linaungwa mkono na vyama vyote hata na upinzani ikiwemo CHADEMA, lakini amezungumza vizuri sana dada Mheshimiwa Tendegu kwamba wanawake wanaweza hasa wakiamua jambo lao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikwambie, kwa uongozi wa Mama Samia, sio wanawake tu wanaoufurahia hata sisi wanaume tunamfurahia sana, hata Vvyama vya Upinzani, hebu angalia leo Mbowe ndio anaongoza kwenda Ikulu, najua alipa-miss sana, lakini amepata nafasi ya kuingia na kutoka zaidi ya mara tano. Hongera sana kwa Mama Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulikuwa na ushindani wa nchi zaidi ya 54, lakini Mama Samia ameongoza, nafananisha na ligi ya Tanzania, kama alivyosema mama wa afya ya akili kwamba tumemnyang’anya Nigeria ambaye ndio alikuwa na tuzo hiyo. Ni sawa na Tanzania tu, tunatarajia kumnyanganya mnyama very soon labda Jumapili na ningemwomba Mama Samia huko aliko anisikilize, najua atakuja, nimkaribishe sana Mwanza tumpe zawadi ya Kitanzania. Najua aliyopewa kule ni tuzo aje tumpe mnyama kesho kutwa hapa tunavyomchinja, apate zawadi. Najua tulimpa uwanja wa Taifa alipokuwa mgeni rasmi, aje na Mwanza kule Jumapili tutampa zawadi kama alivyozoea kupewa hata akiwa kule Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo ukizunguka kila jimbo hapa utakuta mtambo unatengeneza barabara. Nimekuwa Mbunge miaka saba, nimelia lami humu miaka saba, leo hata Jimbo la Geita Vijijini tuna kilomita 25. Kwa niaba ya wananchi wa Geita Vijijini, tunamwombea mema sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo ukienda vijijini pamoja na kwamba hatuwezi kujenga lami kila mtaa, kila kijiji, lakini leo tuna pesa za kutosha kujenga barabara zinazopitika mchana na usiku.

Mheshimiwa Spika, sasa utanisamehe sana sisi Wasukuma huwa tukifurahi hatuna maneno mengi, ningekuomba mimi sitaruka sarakasi, wala sipigi magoti, tukifurahi sisi Wasukuma wamo humu wenzangu watanisaidia tunafanyaje?

WABUNGE FULANI: Tunaimba.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Tunafanyaje.

WABUNGE FULANI: Tunaimba.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, sasa naomba niimbe wimbo, utaniruhusu? Tuna imani na Samia…

WABUNGE FULANI: Oyaa, oyaa, oyaa.

SPIKA: Mheshimiwa Musukuma! Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Musukuma magoti na sarakasi haviruhusiwi humu ndani ni pamoja na kuimba, hairuhusiwi. (Makofi/Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Wizara ya Mambo ya Nje. Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri tunaona bidii ya kazi yake anayoifanya, aendelee kurudisha mahusiano ambayo yalivurugika.

Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia 90 ya Watanzania wa hali ya chini tunategemea sana bidhaa kutoka China na Watanzania wale wa kawaida kabisa na hata humu sisi wenyewe Wabunge asilimia kubwa tunatumia bidhaa ya China. Kwa hiyo, rafiki mkubwa wa Tanzania kiuchumi ni Mchina, sasa na mimi ninazunguka huko China mara nyingi na nimemuona Balozi Kairuki hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeenda hadi ofisini kwake Beijing na labda tuone wapi tumekosea. Kweli kwa Watanzania wa hali ya kawaida ambao ni wafanyabiashara wenye elimu ya kawaida ya darasa la saba kuwapeleka kwenye biashara ya mtandao wewe unakaa Kariakoo wengi sana wamekula hasara, niombe sana Waziri na Balozi mkae na wenzetu kama kuna mahali tuliwakwaza au kuna vigezo hatujafikia waone namna ya kuiachia Tanzania kwa sababu kwanza ni soko lao kubwa kwenye bidhaa zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi watanzania wengi pale kariakoo wamekula hasara kubwa sana na wenzetu wa China ni wajanja kweli, watu wengi wanaoagiza bidhaa mtandaoni mara nyingi inapokuja Tanzania inakuwa tofauti na kitu ulichokiagiza, ulichoonesha ni kingine na kilichokuja kwenye kontena ni kingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hata ukirudi kwenye address ya kule china unakuta ameshabadilisha na address kwa hiyo watu wengi wanakula hasara biashara nyingine kama za Kariakoo za nguo za urembo zinahitaji choice ya macho sio ya mtandao, leo ukienda Kariakoo inakufa wewe mwenyewe ni shahidi ukienda Uganda na Kenya wenzetu sasa hivi tunatoka Tanzania kwenda kununua bidhaa Uganda na Kenya tuone namna wapi tulikosea turudishe mahusiano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lazima na wao wawe fair, leo Wachina wapo kila kata wanachezesha kamari yaani kuja kwetu Tanzania hakuna corona, ila sisi tukienda kwao kule kuna tatizo, mahusiano tuyatafute kotekote kwa sababu na wao wenyewe wanafaidika na Tanzania waone namna ya kulegeza. Mimi nadhani kwenye Afrika ni nchi Tanzania pake yake ambayo leo ukienda kila kata asubuhi saa tatu utamkuta Mchina anakusanya fedha kwenye kamari. Sasa sisi kwenda kule ni kwasababu ya yale mahusiano ambayo tumeyajenga pamoja na wao lakini ukienda kwenye biashara za madini wamejaa Wachina, ukienda kwenye contract za miradi wamejaa Wachina, ukienda kila kazi ambayo ina maslahi makubwa wapo Wachina.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Kwenda huko inakuwa ngumu na mimi mwenyewe ni mfano mzuri na Mheshimiwa Amar hapa tumeagiza mitambo unaoneshwa katapira lakini imekuja mitambo ya Kichina mpaka leo Mheshimiwa Hussein amesimamisha mtambo kwa sababu wataalam hawawezi kuja eti kuna corona ila kuja kuchezesha kamari wapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Balozi mtuelewe, mtusaidie Watanzania wengi waliotajirika wametajirika na China, kulikuwa na maonesha tunakwenda kujifunza maonesho ya teknolojia za kisasa ni vizuri waangalie namna ya kuachia yale mahusiano vizuri kabisa ili tuweze kwenda kama tulivyokuwa tunaenda zamani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine ni suala ambalo kila mwaka humu Bungeni huwa linazungumzwa la uraia pacha. Hofu yangu mimi najiuliza ni nini, yaani tunaweka kikwazo kwamba mtu aliyekuwa nje, Mtanzania ambaye nikimsomesha mwanangu akimaliza akasema baba nimepata kazi akafanya maarifa yake akapata uraia, kurudi Tanzania anakuwa ni mgeni, hii ni uonevu mkubwa sana, tunapoteza watoto wetu, tunawanyima fursa kwa sababu ya vitu ambavyo mimi nadhani ni hofu ya kisiasa pia, kwa sababu wanasema eti aruhusiwi kugombea kazi za kisiasa kwanini yaani kwa tatizo gani yaani mtu amesoma, amepata knowledge kubwa akirudi akiwa Waziri hapa ndio watu ambao tunawataka tubadilishe mawazo tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe sana hili halikwepeki, hata mkilikwepa jaribu kufanya analysis ya wahindi matajiri hapa Tanzania wote wana uraia mbili, utamkuta ni Mtanzania ana passport, lakini ana passport ya Canada na ana ya Uingereza kwa kwetu sisi tuna hofu.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo ukienda Uingereza juzi nilikuwa naangalia television tumepata Diwani Msukuma wa Nzela kule Jimboni kwangu kapata Uingereza, tuna Mawaziri wapo sijui Canada, tunaona wivu gani tunasomesha nje ili tupate mawazo mapya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nilikuwa naiomba Wizara hizi hofu tuziondoe turudishe tu hali halisi kwamba watu wapate uraia wa nchi mbili kama anafanya vizuri akirudi hata Jimbo langu agombee, akinishinda basi, ndio vitu tunavyovitaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama Mbunge unajiamini unafanya kazi vizuri hata ukija na degree zako hata ukitoka Marekani unamkuta King kazuia hapo, utapigwa unarudi unajipanga tena. (Makofi)

Kwa hiyo, tuondoe hofu tunapeleka watoto wetu nje ili wapate knowledge ya kuja kulisaidia Taifa na tujifunze hata Asia walipeleka kwanza watoto wao Ulaya wakaiga Ulaya wanafanyaje, waliporudi kwao wakafanya mambo mazuri, tuondoe hofu kazi nzuri Mheshimiwa Waziri, lakini nakusisitiza na kukuomba tena Watanzania wengi wanaitegemea China, hata humu ndani ukiangalia suti nyingi humu ndani ni za Kichina, mnaguna nini wengi tu mmekula (mmevaa) Mchina sasa ukiweka masharti mwisho tutavaa fake ambayo sio choice ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana hata nywele humu nyingi ni za Kichina. (Makofi/Kicheko)
Muswada wa Sheria ya Mamlaka ya Nchi kuhusiana na Umiliki wa Maliasili wa Mwaka 2017.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Kwanza naunga mkono mambo yote yaliyozungumzwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwakumbushe wenzangu, nimewasikiliza wachangiaji walionitangulia wamezungumza sana kuhusiana na suala la Hati ya Dharura. Hata hivyo, nataka niwakumbushe tu kwa upendo mkubwa, uchaguzi wa mwaka 2015 Mgombea Urais wa upande wao alipatikana kwa Hati ya Dharura.

Mheshimiwa Naibu Spika, alipatikana kwa Hati ya Dharura kwa kuwa wao wenyewe walimuona anafaa kwa dharura waliokuwa nayo na Watanzania hawakuwahoji. Kwa hiyo, tunapozungumza suala la dharura mimi nadhani tungeungana mkono kwa sababu hata wao waliiona dharura na kumchukua mtu ambaye hawakufanya vetting, hajui mambo ya CHADEMA, hajui chochote wakampa dharura ya Urais. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashangaa Wabunge wenzangu mnalalamika tunawaburuza katika kutunga hizi sheria, wewe ulituletea mtu ambaye unataka tumkabidhi nchi, tumkabidhi nchi halafu hajui chochote kuhusu CHADEMA, hajui chochote kuhusu Serikali. Kwa vile wao walifanya hivyo mimi nadhani tungeendelea.

KHUSU UTARATIBU...

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Bungara watu wote wanamjua humu, inawezekana hajui kama Magufuli alipatikana kwa procedure ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sisi tunaunga mkono Hati ya Dharura ya Serikali tuweze kupitisha sheria hii ambayo imeletwa mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili, nimesikia wanalalamika sana wanasema tulichelewa kufanya mabadiliko. Nakubali tulichelewa kwa sababu dunia inabadilika na CCM inabadilika, watu waliokuwa wanatuchelewesha wote mmewakumbatia nyie huko. (Makofi)

Serikali hii ilikuwa inaongozwa na Lowassa na Sumaye ndiyo mmewakumbatia kwetu, sisi tulipoona hawafai nyie mmechukua kwa Hati ya Dharura. Kwa hiyo, sasa mtulie tumeamua kufanya mabadiliko kwa Mheshimiwa Majaliwa na kwa Mheshimiwa Magufuli. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesikia wenzetu wanalalamika kuhusu kufanya mabadiliko ya sheria haraka haraka, hebu niwakumbushe 1992 na ninyi wazee mlioko upande wa pili mliokuwepo 1992 kwenye siasa. Bila mabadiliko yaliyofanywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi ninyi msingekuwa humu, ingekuwa CCM yote humu. (Makofi)

Kwa hiyo, mabadiliko yanakuja na faida mtulie baadaye tutaona faida ya mabadiliko haya yanayokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie sasa kwenye Muswada wenyewe. Marekebisho ya Sheria ya Serikali wanasema wanataka kuwa na share asilimia 16. Naomba tu Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha atueleze hii asilimia 16 imetuchukua na sisi wachimbaji wadogo ama ni kwa ajili ya makampuni ya kigeni. Mimi sijawahi kuona hata ukienda Dubai, ukienda China Serikali haiingii hisa kwa wazawa inaingia kwa wageni.

Kwa hiyo, muangalie mtakapokuwa mnataka kuingia kwetu wachimbaji wadogo kwa asilimia 16 ni sawa na mnataka kutufuta wachimbe wachimbaji wakubwa peke yake. Kwa hiyo, ushauri wangu nadhani hii sheria tutunge lakini kwa wawekezaji wageni, lakini sio wazawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni kuhusiana na ile kodi ya asilimia sita. Naomba sana na Wabunge wenzetu mtusaidie sisi wenzenu tunaotoka kwenye machimbo, utakapochukua asilimia sita ya kodi, tunaomba sana asilimia moja angalau ibaki maeneo yanakochimbwa yale madini, kwa sababu ukisema tupate 0.3% peke yake haisaidii. Sisi wengine tunaokaa kwenye machimbo tumekuwa tukilalamika kwamba tuna migodi mikubwa lakini mji ni mchafu, sasa mkituachia ile 1% angalau na sisi tutakuwa na mipango mikubwa ambayo tutaipanga kuiendesha Halmashauri yetu sisi wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya yalifanyika Mtwara na Ngorongoro wala siyo kitu cha ajabu. Mjifunze mlifanyaje Ngorongoro wao wanapewa chakula, wanalipwa, wanasomeshewa watoto na sisi tunaotoka kwenye machimbo tunaomba hiyo offer Serikali iweze kutufanyia hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine suala la sheria hii kifungu cha 10 wanasema kuanzia tarehe 20 madini yote hayatasafirishwa bila kuchakatwa Tanzania. Tanzania hatuna refinery na leo ni tarehe 3 Julai, 2017 maana yake bado tuna siku 17. Ukisema kuanzia tarehe 20 tusisafirishe, kwa wenzetu wale wachimbaji wakubwa kama GGM, Acacia na wengine wao wana mitaji sio shida kwenda kununua refinery, refinery moja ya hali ya chini ni dola milioni mbili kwa sisi wachimbaji wadogo, pengine mpaka muanze kuzungumza na mabenki na mikopo mingine itatuchukua zaidi ya miezi mitatu mpaka hata miezi sita, mnafahamu taratibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani kwa wachimbaji wadogo hii sheria isitubane. Hatukatai kulipa kodi lakini Serikali iangalie kama ninyi mnajenga hiyo refinery mtuambie. Ukisema tarehe 20 tusisafirishe maana yake kuanzia kesho tusichimbe na tusiwashe hiyo mitambo midogo midogo inayozalisha. Kwa sababu mitaji tuliyonayo tunapochimba siku mbili tunauza tunapata hela za kulipa madeni na wafanyakazi. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri aliangalie hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri…

KUHUSU UTARATIBU...

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, namheshimu mwalimu wangu wa darasa la kwanza, kule kwao anafundisha darasa la kwanza kwa taarifa niliyonayo, kwa hiyo, msimshangae hii ni mifano. Ninapozungumza hapa silalamiki naboresha.

Ninachozungumza hapa mimi silalamiki naipongeza Serikali kwa kuboresha, wewe unasema nalalamika, nalalamika kitu gani na Serikali ni ya CCM na mimi ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi, ebo! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa kuboresha pale ambapo tulipokuwa tunafanya kazi za kibajeti kwenye Halmashauri migodi yote ilikuwa haishiriki kwenye bajeti. Sasa tulivyopitisha hii sheria tunashukuru kwamba tutashiriki nao kwenye bajeti hata yale tutakayokuwa tunayapanga tukiwapa wafanye 1,2,3 litakuwa ni la kimkataba na Waziri anasaini na sisi tutawadai kama wadau. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nilikuwa nasema hawa wenzetu hawaelewiki na ninaangalia huko naona wengi sana wasomi rafiki zangu, nakushukuru Mchungaji umesogea chini ili unisikie vizuri kule husikii. Wengine wote wakiongea dakika mbili wanakimbia tusiwajibu, hapa tunazungumzia Muswada wa Madini, mtu msomi, mwalimu ameshaaenda kantini. Mtu msomi kabisa ana masters yake ya sheria badala ya kukaa humu kutushauri, tunazungumza Muswada wa Madini ananyanyuka anazungumzia tv. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshauri Waziri sisi wanyonge na watu tunaotaka mabadiliko ya nchi hii hakuna mtu anayelalamika. Ha hata hawa, jaribuni kufanya mikutano kwenye majimbo yenu watu hawako na ninyi.

Yaani ni kakundi kenu tu mnapiga kelele. Unasimama hapa unaomba zile Taarifa za Tume tuletewe humu kwani Tume imeshakamilisha kazi yake, si bado kuna majadiliano. Amepokea Taarifa ya Tume, anafanya majadiliano tutalipwa, halafu tunaweza kuja kujadili ameshakamilisha kazi yake. Humu hakuna mtu aliyegundua suala la makinikia nilishasema ni suala la Rais tukae kimya amalize kazi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Muswada wa Sheria ya Mapitio na Majadiliano kuhusu Masharti Hasi katika Mikataba ya Maliasili za Nchi wa Mwaka 2017.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Kwanza naunga mkono mambo yote yaliyozungumzwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwakumbushe wenzangu, nimewasikiliza wachangiaji walionitangulia wamezungumza sana kuhusiana na suala la Hati ya Dharura. Hata hivyo, nataka niwakumbushe tu kwa upendo mkubwa, uchaguzi wa mwaka 2015 Mgombea Urais wa upande wao alipatikana kwa Hati ya Dharura.

Mheshimiwa Naibu Spika, alipatikana kwa Hati ya Dharura kwa kuwa wao wenyewe walimuona anafaa kwa dharura waliokuwa nayo na Watanzania hawakuwahoji. Kwa hiyo, tunapozungumza suala la dharura mimi nadhani tungeungana mkono kwa sababu hata wao waliiona dharura na kumchukua mtu ambaye hawakufanya vetting, hajui mambo ya CHADEMA, hajui chochote wakampa dharura ya Urais. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashangaa Wabunge wenzangu mnalalamika tunawaburuza katika kutunga hizi sheria, wewe ulituletea mtu ambaye unataka tumkabidhi nchi, tumkabidhi nchi halafu hajui chochote kuhusu CHADEMA, hajui chochote kuhusu Serikali. Kwa vile wao walifanya hivyo mimi nadhani tungeendelea.

KHUSU UTARATIBU...

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Bungara watu wote wanamjua humu, inawezekana hajui kama Magufuli alipatikana kwa procedure ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sisi tunaunga mkono Hati ya Dharura ya Serikali tuweze kupitisha sheria hii ambayo imeletwa mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili, nimesikia wanalalamika sana wanasema tulichelewa kufanya mabadiliko. Nakubali tulichelewa kwa sababu dunia inabadilika na CCM inabadilika, watu waliokuwa wanatuchelewesha wote mmewakumbatia nyie huko. (Makofi)

Serikali hii ilikuwa inaongozwa na Lowassa na Sumaye ndiyo mmewakumbatia kwetu, sisi tulipoona hawafai nyie mmechukua kwa Hati ya Dharura. Kwa hiyo, sasa mtulie tumeamua kufanya mabadiliko kwa Mheshimiwa Majaliwa na kwa Mheshimiwa Magufuli. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesikia wenzetu wanalalamika kuhusu kufanya mabadiliko ya sheria haraka haraka, hebu niwakumbushe 1992 na ninyi wazee mlioko upande wa pili mliokuwepo 1992 kwenye siasa. Bila mabadiliko yaliyofanywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi ninyi msingekuwa humu, ingekuwa CCM yote humu. (Makofi)

Kwa hiyo, mabadiliko yanakuja na faida mtulie baadaye tutaona faida ya mabadiliko haya yanayokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie sasa kwenye Muswada wenyewe. Marekebisho ya Sheria ya Serikali wanasema wanataka kuwa na share asilimia 16. Naomba tu Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha atueleze hii asilimia 16 imetuchukua na sisi wachimbaji wadogo ama ni kwa ajili ya makampuni ya kigeni. Mimi sijawahi kuona hata ukienda Dubai, ukienda China Serikali haiingii hisa kwa wazawa inaingia kwa wageni.

Kwa hiyo, muangalie mtakapokuwa mnataka kuingia kwetu wachimbaji wadogo kwa asilimia 16 ni sawa na mnataka kutufuta wachimbe wachimbaji wakubwa peke yake. Kwa hiyo, ushauri wangu nadhani hii sheria tutunge lakini kwa wawekezaji wageni, lakini sio wazawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni kuhusiana na ile kodi ya asilimia sita. Naomba sana na Wabunge wenzetu mtusaidie sisi wenzenu tunaotoka kwenye machimbo, utakapochukua asilimia sita ya kodi, tunaomba sana asilimia moja angalau ibaki maeneo yanakochimbwa yale madini, kwa sababu ukisema tupate 0.3% peke yake haisaidii. Sisi wengine tunaokaa kwenye machimbo tumekuwa tukilalamika kwamba tuna migodi mikubwa lakini mji ni mchafu, sasa mkituachia ile 1% angalau na sisi tutakuwa na mipango mikubwa ambayo tutaipanga kuiendesha Halmashauri yetu sisi wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya yalifanyika Mtwara na Ngorongoro wala siyo kitu cha ajabu. Mjifunze mlifanyaje Ngorongoro wao wanapewa chakula, wanalipwa, wanasomeshewa watoto na sisi tunaotoka kwenye machimbo tunaomba hiyo offer Serikali iweze kutufanyia hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine suala la sheria hii kifungu cha 10 wanasema kuanzia tarehe 20 madini yote hayatasafirishwa bila kuchakatwa Tanzania. Tanzania hatuna refinery na leo ni tarehe 3 Julai, 2017 maana yake bado tuna siku 17. Ukisema kuanzia tarehe 20 tusisafirishe, kwa wenzetu wale wachimbaji wakubwa kama GGM, Acacia na wengine wao wana mitaji sio shida kwenda kununua refinery, refinery moja ya hali ya chini ni dola milioni mbili kwa sisi wachimbaji wadogo, pengine mpaka muanze kuzungumza na mabenki na mikopo mingine itatuchukua zaidi ya miezi mitatu mpaka hata miezi sita, mnafahamu taratibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani kwa wachimbaji wadogo hii sheria isitubane. Hatukatai kulipa kodi lakini Serikali iangalie kama ninyi mnajenga hiyo refinery mtuambie. Ukisema tarehe 20 tusisafirishe maana yake kuanzia kesho tusichimbe na tusiwashe hiyo mitambo midogo midogo inayozalisha. Kwa sababu mitaji tuliyonayo tunapochimba siku mbili tunauza tunapata hela za kulipa madeni na wafanyakazi. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri aliangalie hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri…

KUHUSU UTARATIBU...

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, namheshimu mwalimu wangu wa darasa la kwanza, kule kwao anafundisha darasa la kwanza kwa taarifa niliyonayo, kwa hiyo, msimshangae hii ni mifano. Ninapozungumza hapa silalamiki naboresha.

Ninachozungumza hapa mimi silalamiki naipongeza Serikali kwa kuboresha, wewe unasema nalalamika, nalalamika kitu gani na Serikali ni ya CCM na mimi ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi, ebo! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa kuboresha pale ambapo tulipokuwa tunafanya kazi za kibajeti kwenye Halmashauri migodi yote ilikuwa haishiriki kwenye bajeti. Sasa tulivyopitisha hii sheria tunashukuru kwamba tutashiriki nao kwenye bajeti hata yale tutakayokuwa tunayapanga tukiwapa wafanye 1,2,3 litakuwa ni la kimkataba na Waziri anasaini na sisi tutawadai kama wadau. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nilikuwa nasema hawa wenzetu hawaelewiki na ninaangalia huko naona wengi sana wasomi rafiki zangu, nakushukuru Mchungaji umesogea chini ili unisikie vizuri kule husikii. Wengine wote wakiongea dakika mbili wanakimbia tusiwajibu, hapa tunazungumzia Muswada wa Madini, mtu msomi, mwalimu ameshaaenda kantini. Mtu msomi kabisa ana masters yake ya sheria badala ya kukaa humu kutushauri, tunazungumza Muswada wa Madini ananyanyuka anazungumzia tv. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshauri Waziri sisi wanyonge na watu tunaotaka mabadiliko ya nchi hii hakuna mtu anayelalamika. Ha hata hawa, jaribuni kufanya mikutano kwenye majimbo yenu watu hawako na ninyi.

Yaani ni kakundi kenu tu mnapiga kelele. Unasimama hapa unaomba zile Taarifa za Tume tuletewe humu kwani Tume imeshakamilisha kazi yake, si bado kuna majadiliano. Amepokea Taarifa ya Tume, anafanya majadiliano tutalipwa, halafu tunaweza kuja kujadili ameshakamilisha kazi yake. Humu hakuna mtu aliyegundua suala la makinikia nilishasema ni suala la Rais tukae kimya amalize kazi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria mbalimbali (Na. 2) wa Mwaka 2019 (Toleo la Kiingereza).
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi nichangie.

Mheshimiwa Spika, naomba niipongeze sana Serikali kwa hatua kubwa ambayo imechukua ya kuweza kutusaidia hasa sisi tunaotoka kwenye dhahabu. Namsikiliza rafiki yangu anaongea anadhani hizi ni korosho, dhahabu ina wenyewe, hii sio Kangomba. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kweli sheria ni nzuri lakini tunabishana hapa kana kwamba tumeshaweka ushawishi wa nchi jirani kuja kuingiza dhahabu hapa kwetu. Bado tunayo kazi kubwa ya kuendelea kubadilisha mambo mengine ili na wenzetu wale tunao-compete nao kama Uganda na Rwanda na Burundi waweze kuja kuuza Tanzania. Ukienda Uganda wao wanatoza asilimia moja tu. Sasa kwa masharti haya kwamba dhahabu inavyofika border lazima iwekwe warehouse, naomba nikwambie hakuna mtu atakwenda ku-declare dhahabu yake, kwanza huo ushawishi hatuna.

Mheshimiwa Spika, kuna watu wanatembea na kilo kama zilizoshikwa Mwanza tu, akifika pale border a-declare halafu arudi aje aziuze Geita, atembee nazo, nani atakubali hata kupanda hilo gari alimo humo ndani? Kwa hiyo, niombe tu masharti haya yaliyowekwa yaondolewe, dhahabu iwe free kama pesa. Ni kama vile wewe unavyoweza kuweka Sh.100,000 kwenye wallet na mtu awe na uhuru wa kuweka pesa yake mfukoni, tusiweke masharti kabisa kwenye dhahabu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri ananisikia, pamoja na kupunguza hizi kodi lakini kuna shida kule machimboni. Kule machimboni tunapotoa mifuko yetu 100 kwa mfano kwenye duara, lazima jioni watu wa Madini waje wachukue mifuko sita kama share, sasa hilo ni tatizo kubwa. Toka nimekuwa kiongozi sijawahi kuona ile mifuko inayochukuliwa kama kodi na madini inapigwa mnada kwa Sh.1,000,000, huwa inapigwa mnada kwa Sh.10,000 watu wanakula mgao. Kwa hiyo niombe, kama tumeamua kufuta kodi hakuna sababu ya watu wa Madini kwenda kusumbua watu wetu kule kwenye machimbo, waondoke tubaki kwenda kulipa kodi inayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, liko suala la uhaba wa watumishi…

SPIKA: Mheshimiwa Musukuma, nitakuongeza dakika moja, unaweza ukalirudia hilo maana sijalipata kabisa. Hao watu wa Madini ni watu wa Serikali kabisa?

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Spika, kule machimboni kuna utaratibu kwamba mchimbaji anapotoa jioni mifuko yake 100 anaweka juu. Kabla ya zile kodi ambazo tumezijadili humu, watu wa Madini lazima wawe pale wachukue mgao wa mifuko sita kwenye mia. Ile mifuko wanakwenda kuiuza kama mnada kesho yake, inauzwa tu labda Sh.5,000, Sh.10,000 wakati uliyotoka nayo inauzwa Sh.1,000,000.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri ni shahidi, anaweza akathibitisha toka tunawapa ile mifuko sita, sita ni lini ofisi yake imewahi kula pesa ya mifuko hiyo ya madini kutoka Tanzania nzima? Kwa hiyo, tunatengeneza wizi tu wa watumishi wetu walioko kule. Iondoke hiyo kodi ya kuchukulia kule wabaki wanachimba free halafu tukapambane kwenye kodi ambayo mnaipunguza kule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna uhaba sana wa watumishi. Naomba nichukue mfano wa Geita. Geita peke yake tuna elusion kama 300 au 400, watumishi walioko pale ni watano tu na Geita pale kwa uchache kwenye mkoa wetu unaweza ukakuta kuna rush labda 30 mpaka 40 na magari yako mawili, hao watu watano wanaamka kila siku kwenda kufungua kwenye elusion kuchukua kodi ya Serikali. Watu watano hawa wanagawana sasa kwenda kupambana na zile rush zilizopo Geita labda kwa siku zipo 200 au 300, hawana hata usafiri wa kwenda nao, inabidi kama mtu wa elusion umfuate kwa gari lako, mnakwenda mnajadili kwenye gari. Kwa hiyo, mpaka mnafika kule Mheshimiwa Waziri yataendelea tu yale uliyoyakamata juzi Dodoma, utakuta mtu ame-declare kilo moja kumbe ana kilo 30. Kwa hiyo, pia hilo suala la watumishi ni vizuri mkaliangalia na vitendeakazi vikawepo.

Mheshimiwa Spika, liko suala la msamaha wa vitu vinavyo-process dhahabu halikuzungumzwa hapa. Tumesikia wenzetu watani zetu Wagogo wakati wanaomba hapa wamesema wanaomba zile mashine za kuchakata mvinyo na zenyewe ziondolewe ushuru. Hata kwenye dhahabu process ya kuipata ni vitu vingi vinashirikishwa. Kwa hiyo, vile vi-attachment vya ku-process dhahabu nashauri pia Serikali ikaondoa kodi.

Mheshimiwa Spika, dhahabu ni pesa, tusiiwekee masharti. Sisi wachimbaji, naweza kuwa nachimba kwenye rush napata gram kumi au mbili, nakula kidogo tu Sh.30,000 nyingine natunza ili siku nikirudi kwa mke wangu nikamuoneshe dhahabu. Si lazima niiuze leo, naweza nikaitunza siku nina shida nikaja kuiuza hata Dodoma. Sasa haya mambo ya kuweka masharti lazima dhahabu ukitaka kutoka hapa uwe na leseni ya import, haiwezekani hivi vitu. Tutakuwa bado tunamuongezea Rais mzigo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, naungana na mwenzangu Mheshimiwa Bashe, pamoja na kwamba itasainiwa lakini naomba kwenye kutunga kanuni ni lazima washirikishe wadau kwa nia nzuri tu. Wadau washirikishwe watoe maoni yao…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Musukuma.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.