Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Rashid Abdallah Shangazi (68 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwanza, napenda kuwapongeza wananchi wa Jimbo la Mlalo kwa imani yao kubwa ambayo imenifanya leo nasimama mbele ya Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda niungane na Wabunge wenzangu kuchangia Hotuba ya Mheshimiwa Rais kama alivyoitoa tarehe 20 Novemba, 2015.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitaanzia na zoezi zima la utunzaji wa mazingira. Duniani kote sasa hivi tunazungumzia mabadiliko ya tabia nchi. Nadhani tutakubaliana sote kwamba hata haya matatizo ya maji tunayoyazungumza kutoka kwenye Majimbo tofauti yamesababishwa
na namna ambavyo tumeharibu mazingira yetu. Tunapozungumzia utunzaji wa mazingira, tunamaanisha pamoja na utunzaji wa vyanzo vya maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitatoa mfano katika Jimbo langu la Mlalo, tunao Msitu wa Asili wa Shagayu mwaka 2012 uliungua moto takribani hekari arobaini na tisa lakini ni hekta kumi na moja tu ndizo ambazo zimepandwa. Cha kusikitisha mvua za Desemba zimesababisha maafa makubwa kwa sababu ardhi imekuwa loose, imesababisha maporomoko na mafuriko katika kata za Mtae, Shagayu, Mbalamo na Mnazi. Hii yote ni kwa sababu ya uoto wa asili ambao umeondoka.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na tatizo la uharibifu wa mazingira katika maeneo ambayo yanazunguka msitu wa Shagayu vilevile kuna tatizo la nguvu kazi. Msitu wa Shagayu unazungukwa na takribani vijiji kumi na tano lakini wako Watendaji wawili pekee na wanatumia
pikipiki moja. Nimuombe Waziri wa Maliasili kupitia Serikali yetu sikivu ahakikishe kwamba anawasaidia Watendaji ili waweze kufanya kazi hii ya utunzaji wa mazingira na misitu kwa ufanisi unaotakiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili nitajikita kwenye kilimo. Kama sote tunavyotambua kilimo ndiyo mhimili wa uchumi wa nchi yetu ya Tanzania. Kwa wakazi wa Jimbo la Mlalo na Halmashauri ya Lushoto kwa ujumla wake, ni takribani asilimia tisini na nane wanategemea
kilimo. Tunaomba kupitia hotuba hii ya Mheshimiwa Rais, Wizara inayohusika itufanyie yafuatayo katika Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto. Tunayo maeneo ya aina mbili, ya milimani ambapo tunaendesha kilimo cha mbogamboga na matunda katika kata za Lukozi, Malindi, Rangwi, Sunga na Shume. Kuna tatizo kubwa la wakulima kunyonywa pindi wanapovuna mazao yao kwa kutumia mtindo wa lumbesa. Lumbesa imekuwa ni sehemu ya unyonywaji wa wakulima, hivyo mwisho wa siku hawaoni faida ya yale mazao ambayo wanayavuna. Hivyo, naomba Bunge lako Tukufu, tuisimamie Serikali kuhakikisha kwamba kunakuwa na udhibiti wa ufungaji wa mazao kwa njia ya lumbesa. Tunatambua Wizara ya Viwanda na Biashara ina Wakala wa Mizani na Vipimo, tunaomba ilisimamie suala hili ili liweze kupatiwa ufumbuzi wa mwisho.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni ukanda wa tambarare. Ukanda huu tunapata changamoto kwamba mvua zinazoshuka katika mabonde yetu na makorongo zinaelekea baharini na maji yanapotea bure. Tunaomba Wizara ya Kilimo ije na mpango wa kutujengea
mabwawa ili tuweze kuhifadhi maji yanayotiririka wakati wa msimu wa mvua. Maji haya yatasaidia wananchi kuendesha kilimo chenye tija kwa msimu mzima wa mwaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika maeneo hayo tunayo mapori mazuri ambayo yakitumika vizuri kwa kuzingatia rasilimali ardhi, tunaweza tukaanzisha benki ya ardhi ambayo itakuwa ni kivutio kimojawapo kwa wawekezaji ambao wanatafuta maeneo ya kuwekeza. Pia
kwa kutumia mipango ya ardhi, tunaweza pia tukawatengea wafugaji ambao nao pia wanapatikana katika eneo hili, wakapata maeneo ili waachane na kasumba ya kuswaga ng‟ombe kila mahali. Tutakuwa tumewajengea uwezo wa kukaa mahali pamoja ambapo hata
Serikali inaweza ikapata kodi yake stahiki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia hotuba hii nzuri ya Rais lazima pia tufungue fursa mpya za kuwawezesha wananchi wetu. Jimbo la Mlalo, Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto inapakana na nchi jirani ya Kenya. Tunao mpaka kule ambao unatumiwa kwa ajili ya shughuli za kupitisha magendo pamoja na kupitisha Wasomali ambao wanapita kwa njia za panya.
Niiombe Serikali ione kwamba hii ni fursa ya kufungua kituo cha mpaka katika eneo la Kata ya Lunguza ili tuweze kufanya biashara na nchi jirani ya Kenya. Ni jambo jema kabisa kwamba ulinzi wa mipaka yetu ni jukumu ambalo halikwepeki lakini tukiweza kuweka kituo cha biashara na mpaka itasaidia wafayabiashara kuweza kwenda nchi jirani na pia itatusaidia na sisi kuuza mazao yetu katika nchi jirani ya Kenya.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua suala zima la umeme vijijini. Tunashukuru umeme vijijini umesambazwa kwa kiwango cha kutosha lakini pia niombe Waziri anayehusika na nishati katika Jimbo langu bado kuna kata zaidi ya nne hazijaguswa na nguzo hata moja. Naiomba
mamlaka inayohusika kupeleka umeme vijijini atambue Kata za Shagayu, Mbaramo, Mbaru na Sunga ili nazo ziweze kupewa kipaumbele katika usambazaji wa umeme vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo napenda kulizungumzia ni rushwa.
Mheshimiwa Rais ameanza vizuri, anapambana na majipu makubwa katika ngazi ya kitaifa. Kupitia Bunge lako Tukufu, naomba pia Waziri wa TAMISEMI, ashuke huku chini katika Halmashauri zetu, miradi mingi inafanywa chini ya utekelezaji uliokusudiwa. Huku nako kuna
mchwa wanatafuna pesa, miradi haina tija, miradi haikamiliki kwa wakati, wanawazungusha Madiwani kwa sababu wanatumia uelewa hafifu wa Madiwani wetu walioko huko vijijini pamoja na Watendaji wa Vijiji. Naiomba Wizara husika ilisimamie hili kwa jicho la karibu zaidi.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo naomba kuwasilisha, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nitoe pole kwa Taifa kwa kupoteza wapiganaji hawa wawili, Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma wa zamani Mheshimiwa Said Mwambungu pamoja na Mzee Paul Sozigwa. Mwenyezi Mungu aziweke roho za marehemu mahali pema peponi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe mchango wangu katika Wizara hii na kwa kipekee kabisa naomba nianze na suala la Chuo cha Ufundi Lushoto. Juzi hapa Mheshimiwa Shekilindi alikuwa na swali linalohusu VETA, Mheshimiwa Naibu Waziri wakati analijibu nadhani hakuwa anaifahamu Lushoto vizuri, sasa naomba kidogo nimpitishe kwenye jiografia aitambue vizuri Lushoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Lushoto ni Wilaya ambayo hali ya hewa ni kama hivi tulivyo humu Bungeni, siku zote tupo hivi hakuna joto, kwa hiyo, tunazaana sana. Population ya Wilaya ya Lushoto ni karibia watu 700,000, tunazo shule za sekondari 85, ikiwemo Kifungiro, St. Mary’s Mazinde Juu, Kongei, hizi ni zile ambazo zinafanya vizuri zaidi. Kwa mazingira hayo tunahitaji kuwa na vyuo vya ufundi. Bahati nzuri huko nyuma tulikuwa na Chuo cha Ufundi cha Kanisa KKKT cha Magamba Trade, baada ya wenye chuo kubadilisha matumizi sasa hivi kimekuwa ni Chuo Kikuu cha SEKOMU hivyo, hakuna chuo cha ufundi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika kata ya Lushoto Mjini pale tulikuwa na karakana ya RRM - Rural Roads Maintanance zile za zamani zile, hapa palikuwa na mitambo mpaka sasa hivi ipo na yale majengo yanamilikiwa na Halmashauri na pana mitambo mbalimbali ya kufanya ufundi selemala, kufua vyuma na kadhalika.

Kwa hiyo, tunapozungumza suala la VETA Lushoto hatuna maana kwamba tukatafute mapori. Zipo karakana ambazo tayari zipo kimsingi ni namna tu ya kuziboresha. Pia KKKT hawa wana shule ya ufundi ambayo ni kwa watu wenye mahitaji maalum, hata Mheshimiwa Marehemu Dkt. Elly Marco Macha amesoma katika shule hii inaitwa Irente, pale pana chuo cha ufundi cha watu wenye mahitaji maalum.

Kwa hiyo, ninakuomba Mheshimiwa Waziri ama Naibu Waziri, ujipe nafasi ya kuja Lushoto uweze kuona haya mambo, tunapolizunguza VETA tuna maana kwamba population iliyopo ni kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tukisema tuende mpaka Tanga bado sisi wenyewe katika ndiyo Mkoa wa Tanga tunaongoza kuwa na sekondari nyingi, eneo lile peke yake linatosha kuwa na Chuo cha VETA na maeneo yapo, tupo tayari kukupa majengo ambayo yapo tayari. siyo ya kuanza kujenga.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni uchapishaji wa vitabu. Serikali ilipoamua kuifuta Bodi ya EMAC tulikosea. Kama kulikuwa na makosa ilipaswa turekebishe, lakini kuifuta na hili jukumu kuipa Taasisi ya Elimu pekee ni suala ambalo kwa kweli linakinzana hata na kauli mbiu hii ya Serikali ya viwanda. Tunavyozungumza sasa yapo makampuni ya sekta binafsi yalikuwa yanafanya kazi hii ya uchapishaji, kampuni za kizalendo wapo kampuni ya Ujuzi, wapo Mkuki na Nyota, Mture, Education Book Publisher, E&D pamoja na AIDAN ambapo mwanzoni walikuwa wameungana na Macmillan. Haya makampuni sasa hivi hayawezi yakafanya biashara kwa sababu Serikali imechukua ili ifanye yenyewe biashara, Serikali imeingia kwenye uchapishaji na matokeo ndiyo tunayoyaona hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, makosa haya kwenye kitabu cha jiografia pekee cha form four yapo zaidi ya makosa 15, kwenye kitabu cha form three yapo zaidi ya makosa 18, humu kwenye I Learn English Language ndiyo usiseme yako mengi, hata neno below linaandiwa double L, ni jambo la kusikitisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaitaka Serikali kwamba bado hatujakosea sana kwa sababu mambo haya yamefanyika humu Bungeni tuone namna gani tunaweza tukairejesha tena ile bodi ya EMAC ambayo inaweza ikaja kufanya hii kazi ya uhakiki wa vitabu. Pia lazima tuangalie kwamba hii sekta binafsi itafanya wapi biashara. Tunazungumza sasa hivi kiswahili kinakua katika Afrika ni lugha ya pili kwa ukubwa, kama kiswahili kinakua tunatarajia kwamba Serikali peke yake ndiyo itachapisha hivi vitabu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni wakati maufaka kabisa kuwajengea uwezo ili waweze kushindana na hawa akina Oxford University Press, washindane na kina Pearsons, washindane na kina Longhorn, kwa sababu haya ni makampuni makubwa duniani na yapo hapa Tanzania wanachapa vitabu, tena wao mara nyingi wanachapa nje ndiyo maana hata vitabu vinakuwa bei nafuu. Sisi gharama za uchapishaji kwa hapa ndani peke yake zitakuwa ni kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba Mheshimiwa Waziri hili jambo kama lilifanyika kwa mihemuko ya kisiasa hebu sasa kaa na hawa wadau, hawa ni Watanzania wenzetu, tujaribu kupata mbinu muafaka ambazo zitakuja kutatua tatizo la elimu ya hawa watoto wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la ukarabati wa shule kongwe. Nimeangalia katika kitabu sijua labda nimeangalia kwa haraka lakini sikuona sekondari kongwe za Tabora Boys na Tabora Girls. Mheshimiwa Waziri umesoma Tabora Girls, na mimi nimesoma Tabora Boys ni lazima tukumbuke tulikotoka. Naomba uangalie namna ya kuboresha mazingira ya sekondari hizi. Tulikuja ofisini kwako na timu ya Elites ya watu wa Tabora Boys, tukionesha kwamba tunaweza kuunga mkono jitihada za Serikali katika hili na ukatuambia kuna nia njema, sasa tunataka nia njema hiyo iende hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, isiishie hapo iende na shule ya Malangali, Mimi nilipotoka Tabora Boys nilikwenda Malangali nayo sijaiona humu. Mheshimiwa Waziri mimi nimesoma shule za zamani ndiyo maana siyo mtu wa mchezo mchezo, naomba shule hizi tuzifufue. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika elimu, Chuo Maalum cha Ualimu cha Patandi pia humu sijakiona. Tanga Galanos sijaiona lakini Korogwe Girls pia sijaiona, Korogwe TTC sijaiona. naomba sana Mheshimiwa Waziri, hivi pia ziingie katika mfumo huu na ninadhani ulishaniambia kwamba zipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nizungumzie vifaa vya maabara. Hapa tumeona kwamba mmesambaza vifaa vya maabara katika maeneo mbalimbali, tunashukuru kwa hivyo ambavyo tumevipata. Katika Halmashauri ya Lushoto tumepata katika shule tisa pekee. Kama nilivyokuambia tukizungumza Lushoto kama Halmashauri tuna sekondari 65, tukichanganya na Bumbuli ambayo ina Halmashauri yake ndiyo zinafika 85. Kwa hiyo, utaona kabisa kwamba kati ya shule 65 zikipata tisa ina maana bado shule nyingi zimekosa hivi vifaa.

Kwa hiyo, nikusihi sana utuangalie kwa jicho hilo kwamba tumejitahidi katika ujenzi wa hizi shule za sekondari, zipo kata Mheshimiwa Waziri kuna kata moja ina vijiji vinne kila kijiji kina sekondari. Utaona kabisa kwamba huu muitikio ni mkubwa na maabara hizi tumezijenga kwa nguvu za wananchi kwa kiasi kikubwa, tupo tu katika hatua za usafi tunaomba sasa mtuunge mkono katika usafi pamoja na vifaa. Naomba sana utuangalie katika mukhtadha huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala zima la mitaala kwamba mitaala iangaliwe ili iweze kwenda na mahitaji ya Tanzania ya sasa. Tunagundua kwamba sisi angalau tuliobahatika kwenye mitaala ile ya Mwalimu Nyerere ndiyo maana unakuta hata mtu akimaliza darasa la saba anaweza akajiongeza mwenyewe. Lakini tumegundua kwamba sasa hivi, wanafunzi wa sasa anamaliza Chuo Kikuu bado hata kuandika barua au hata yeye mwenyewe kutafuta namna ya kujiwezesha inashindikana. Kwa hiyo, hapa tatizo moja kwa moja inaonekana kwamba ni mitaala yetu haimuandai mwanafunzi ili aje kuwa nani.

Ninaomba sana tuachane na hii dhana ya wanafunzi kumaliza degree halafu kutembea na bahasha mitaani. Tutengeneze mitaala ambayo itakuwa ni shirikishi na inaeleweka kwamba atakapomaliza chuo basi anaweza mwenyewe akajiongeza kwa namna yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa tumeona mlundikano mkubwa huu wa wanafunzi wa masomo ya sanaa, sasa watakuwa hawana ajira, ndiyo anachouliza Mheshimiwa Mlinga waende wapi, kosa lao ni nini, kwa sababu Serikali yenyewe ndiyo iliyofanya udahili leo haiwezi kuwaajiri, ni lazima tutafute vitu mbadala. Pia ni lazima pia tutumie fursa yakuwepo katika hili Shirikisho la Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nichukue nafasi hii kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ya mimi kutoa mapendekezo yangu katika mpango wa maendeleo ya Taifa 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika karne ya 17 hadi 18, Nchi ya Uingereza ilifanya mapinduzi makubwa katika kilimo. Mapinduzi haya baadaye katika karne ya 18 kwenda ya 19 ndiyo yaliyosababisha mapinduzi ya viwanda yaani Industrial revolution. Sasa maana yake ni nini? Maana yake ni kwamba, kama tunataka kwenda kwenye uchumi wa kati, uchumi wa viwanda, nashawishika kusema kwamba ni lazima tujitahidi tuwe na viwanda ambavyo vinatokana na malighafi za kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakapojikita kuzungumzia viwanda hivi vya uwekezaji wa kutoka nje ambavyo havitakuwa na malighafi kutoka ndani ya nchi, bado tutakuwa hatujasaidia nchi hasa katika suala zima la ajira. Kama tutawekeza kiasi cha kutosha katika kilimo, tija itaongezeka katika uzalishaji, malighafi itapatikana na mwisho wa siku tutapata hivyo viwanda ambavyo tunavikusudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuwa na kilimo kinachotupeleka huko kama tutakuwa tunaendelea kusubiri kudra ya Mwenyezi Mungu ya mvua. Ni lazima tuwe na mipango madhubuti ya kuhakikisha kwamba tunakuwa na mabwawa ya umwagiliaji. Hatuwezi tukaendesha kilimo chochote ambacho ni sustainable kinachoeleweka ambacho viwanda vitakuwa vinasubiri malighafi kama mvua zenyewe ni hizi ambazo lazima kwanza tusubiri miezi kadhaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nishauri kwamba katika mpango nimesoma, sikuona mahali popote panapoonesha kuhusu kuyatumia Mabonde haya nane ambayo tunayo katika nchi yetu. Kwa hiyo niombe sana kwamba kuwe na mpango madhubuti wa kuhakikisha kwamba mabonde yale makubwa; Bonde la Mto Rufiji, Malagarasi, Mabonde ya Mto Ruvuma, Mabonde ya Mto Pangani na Mabonde mengine yote yanatumika vizuri kwa ajili ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili likifanyiwa vizuri ndilo litakalosaidia pia na vijana wengi kupata ajira kwa kujiajiri katika kilimo. Tutakapowezesha vijana kujiajiri katika kilimo maana yake tutapata malighafi ya mazao mbalimbali, hilo nalo litakuja kuchochea kwenye lile suala la viwanda kwa sababu mazao mengine yatahitaji kuchakatwa ili yaweze kudumu kwa muda mrefu, mazao mengine yatahitaji kufungashwa katika vifungashio vilivyo bora ili kuweza kupata masoko yenye tija na hapo moja kwa moja tunaongeza mnyororo wa thamani na kuongeza tija katika mazao yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nizungumze suala ambalo limeandikwa katika mapendekezo ya mpango ambalo ni suala la uvuvi. Katika ukurasa wa 29, uvuvi wanakusudia kuzalisha na kusambaza kwa wakulima vifanga 421,368 na katika maeneo ambayo wameyataja kujenga mabwawa hayo ya samaki 159; Mikoa ya Geita, mabwawa 23; Mkoa wa Ruvuma, mabwawa 51; Mkoa wa Mara, mabwawa 14; Mkoa wa Pwani, mabwawa 52; Mkoa wa Tanga, mabwawa mawili; Mkoa wa Dodoma, mabwawa matatu; Mkoa wa Morogoro, mabwawa matatu; Mkoa wa Tabora, mabwawa saba; Mkoa wa Dar es Salaam, mabwawa mawili na Mkoa wa Kigoma, bwawa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina wasiwasi kwamba wametumia vigezo gani lakini nataka nitoe concern yangu hapa. Mimi natoka Mkoa wa Tanga katika Wilaya ya Lushoto, sisi katika Wilaya ya Lushoto, Wilaya ya Korogwe, Wilaya ya Muheza, Handeni na Kilindi, Wilaya zote hizi hakuna mto ambao unaweza ukawafanya watu wakapata samaki. Kwa hiyo, kwa kiasi kikubwa tulitaraji kwamba na sisi angalau haya mabwawa yangekuja kwa wingi angalau kufika hata 10 na lakini mabwawa mawili kwa mkoa mzima sijui hata utalipeleka upande gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda hapa niliseme wazi; Mheshimiwa Naibu Waziri mwenye dhamana ya Mifugo na Uvuvi amesema hii ni blue economy sasa tunataka tuone unapokwenda kulitekeleza hili. Kule Lushoto kuna upungufu mkubwa wa madini chuma ambayo madini haya yanapatikana kwenye bidhaa za samaki na ndiyo maana sisi kule ukivunjika mguu, ili mguu huo uungwe unaweza ukachukua hata miezi miwili tofauti na watu walioko katika Mikoa ya Pwani ambako wanapata samaki kwa wingi, miguu inaunga haraka kwa sababu madini ya chuma yanapatikana katika samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili tunaona kwamba, upande mmoja Serikali ikilifanya vizuri inakuja kutibu tatizo ambalo linaweza likatokea siku za mbeleni. Kwa hiyo niombe sana kwenye mpango hili la mabwawa kwa Mkoa wa Tanga yaongezwe ili tupate mabwawa ya kutosha zaidi. Kama nilivyosema ni Wilaya tatu pekee, Kilindi, Tanga Mjini na Pangani ndiyo ambazo ziko pembezoni mwa bahari hizi Wilaya nyingine zote zilizobaki ziko mbali na bahari kwa hiyo tunahitaji na sisi mabwawa kwa ajili ya ufugaji wa samaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la miundombinu. Miundombinu ya barabara ni suala muhimu sana ili kuwezesha mazao kuweza ku-flow kutoka vijijini na kwenda kwenye masoko au kwenda kwenye viwanda. Hata hivyo, nataka nitoe sikitiko langu kwamba, katika mvua za masika za mwaka huu tulipata tatizo kubwa la maporomoko katika Wilaya ya Lushoto. Barabara ilijifunga kiasi cha wiki moja kwamba hakukuwa na mawasiliano katika ya Lushoto na maeneo mengine ya nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma katika mpango sikuona hili suala mahali popote ambapo limegusiwa kwa sababu tulishazungumza kwamba tunahitaji ile barabara iboreshwe, iongezwe upana pia tupate barabara mbadala ya kuweza kuunganisha Lushoto na maeneo mengine. Hii inawezekana tu kama ile barabara ambayo tunaiomba kutoka Korogwe kwenda Mashewa kwenda mpaka Bumbuli itafanikiwa na barabara hii iko katika Ilani ya Chama lakini mpaka sasa bado hatujaiona katika mpango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika Wilaya ya Lushoto inaweza ikaunganishwa na Wilaya ya Mkinga kwenda mpaka Tanga. Kwa hiyo hili nalo ni muhimu kwamba liingizwe katika mipango ya baadaye ya Serikali, tuunganishe Wilaya ya Tanga Mjini, kuungana na Mkinga, Mkinga iunganishwe na Lushoto lakini wakati huo huo Wilaya ya Lushoto iunganishwe na Same kwa maana ya Mkoa wa Kilimanjaro ili kuweza kuunganisha mikoa hii kwa pamoja na kuweza kufikia yale malengo ambayo tutayakusudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nitoe rai sana kwamba kwa upande wa barabara kwa Wilaya ya Lushoto bado tunauhitaji wa barabara ya kutoka Lushoto kwenda Mlalo kwa kiwango cha lami. Kwa sasa hivi barabara hii inajengwa kilometa mbili mbili kila mkoa kiasi kwamba itachukua miaka mingi, kilometa 42 ina maana itachukua zaidi ya miaka 21.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sasa kwamba barabara hii ni muhimu sana kwa uchumi wa nchi hii kwa sababu sisi ni wazalishaji wa mboga mboga na matunda na ni mazao haya ambayo ni rahisi sana kuoza, tunahitaji tupate barabara madhubuti sisi viazi hatulimi vya vuli. Tunalima viazi kwenye vitivo, tunalima viazi ambavyo vinapatikana mwaka mzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo viazi, carrot, spices zote ambazo unaziona zimejaa katika super market na masoko makubwa nyingi sna zinatoka katika Wilaya ya Lushoto, lakini tatizo kubwa ni barabara. Barabara inatia watu umaskini kwa sababu kama barabara itakuwa siyo madhubuti ndani ya siku moja tayari mtu anaweza akapata hasara kubwa kulingana na aina ya mazao ambayo tunalima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la usambazaji umeme vijijini. Nimezungumza na watu wa REA wametuhakikishia kwamba wao wako vizuri, wamejipanga na Makandarasi wa kutosha wapo, tatizo kubwa ni Serikali haiachii pesa. Disbursement ya pesa bado siyo nzuri na hapa tunazungumza kwamba ikifika mwaka 2020/2021 mradi wa REA utakuwa umefika mwisho, tujione sasa kutoka sasa ni miaka mingapi imebaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe rai kwamba Serikali iachie Mafungu, Mheshimiwa Mpango tafadhali sana aachie mafungu ili tuweze kukamilisha hii program ya umeme vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni program muhimu sana kwa hili suala zima la kuleta mapinduzi ya viwanda kwa sababu tutakapokuwa na viwanda vidogo vidogo hata haya mazao ambayo tunasema kwamba ni rahisi kuoza, yataweza kuchakatwa na kuongezewa ubora yaweze kudumu kwa muda mrefu zaidi. Kwa hiyo suala la watu wa REA kuwezeshwa ili waweze kwenda na kasi ni muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ningependa nizungumzie katika mpango ni suala zima la usafiri wa anga. Hapa inazungumzwa kwamba katika ile mikoa kumi na moja na sisi Mkoa wa Tanga upo. Niombe sana kwa Wizara husika ya Uchukuzi kwamba tunaomba sasa na sisi tuanze kuingizwa katika ratiba ya kupata ndege hizi za ATCL.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika letu hili tumeona mapinduzi makubwa yamefanyika, sasa ni rahisi kwenda Mikoa ta Ruvuma, kwenda Mkoa wa Dodoma, Tabora, Kigoma, Bukoba na kule Songwe, lakini bado tunataka tupate connection kati ya Dar es Salaam, Zanzibar, Tanga mpaka Mombasa. Hii ni muhimu sana na itasaidia sana kwamba kwa kuwa sisi tuko mpakani na nchi jirani ya Kenya, uwepo wa kiwanja cha ndege ambacho kinafanya kazi na ndege kutua itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, tuna mradi mkubwa wa bomba la mafuta, sasa tunataraji kwamba kwa namna yoyote ile Makampuni mbalimbali ambayo yamewekeza katika ujenzi wa hili bomba watahitaji kusafiri. Sasa tusingetaraji kwamba waanze kupoteza muda mrefu wa kusafiri na mabasi kutoka Dar es Salaam kuja Tanga. Kwa hiyo, hili nawaomba sana mliingize katika taratibu zenu na sisi tuweze kufaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la ufugaji hasa huu wa ng’ombe kwamba bado kama Taifa hatujasimama mahali sahihi kuwahudumia wafugaji. Wafugaji kama bado wanaonekana kama ni wageni katika hili Taifa. Sera zetu ziko wazi lakini bado naona Wizara inapata kigugumizi pamoja na Serikali kutoa miongozo mahususi hasa kuanzia katika ngazi za Halmashauri kuainisha maeneo mahususi kwa ajili ya kulisha mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kila mtu ambapo anaenda kutafuta eneo anaonyeshwa eneo lililo wazi lakini unakuta hakuna eneo ambalo liko wazi. Maeneo haya ambayo yako wazi ndiyo maeneo ambayo wafugaji wanayatumia lakini kama leo mtu anakwenda TIC kuomba eneo la uwekezaji anaelekezwa kwenye Halmashauri fulani, matokeo yake ni kwamba anapewa maeneo ambayo kimsingi ni maeneo ambayo yalikuwa yanatumiwa na wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunaomba sasa kuwe na utaratibu mzuri wa kuweza kuwa-accommodate hawa wafugaji wetu ili tuweze kuona na wao wanatoa mchango gani kwa Taifa hili. Mimi katika Halmashauri yangu nina Kata tatu ambazo zina wafugaji. Naweza nikatoa ushahidi namna gani ambavyo wafugaji hawa wamsaidia katika pato la Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mweyekiti, kwanza ni wepesi sana kushiriki katika shughuli za maendeleo, lakini namna bora ya kuwawezesha ni kuwajengea malambo, kuwajengea sehemu za majosho na kuwatengea maeneo mapana ambayo hasa wakati wa kiangazi wanaweza wakapata eneo zuri la kulisha mifugo yao. Sasa pale Serikali inaweza tu ikawa na wajibu mdogo wa kwenda kukusanya mapato na ushuru katika watu hawa. Lakini ni suala muhimu sana tunapozungumza uboreshaji wa Kiwanda cha Gereza la Kalanga kule Moshi sasa kama hakuna ngozi sijui kama watafanya kazi ya namna gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini bado pia tunahitaji kuwa na Taifa ambalo watu wanakunywa maziwa, bado Watanzania wanaokunywa maziwa ni wachache sana tena wengi wanakunywa baada ya kushauriwa na daktari. Isifike hatua kwamba hili ni Taifa ambalo watu wanakunywa maziwa baada ya kushauriwa na daktari, liwe ni Taifa ambalo lina tamaduni hizo za kuongeza vitu vyenye vitamini katika miili yao na kuweza pia kuondoa maradhi mbalimbali ambayo yatatupunguzia hata gharama za matibabu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana naomba hili alichukue kwa umakini mkubwa ili tuweze kuwasaidia wafugaji wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika hoja ambayo iko mbele ya Bunge lako Tukufu. Nami nianze kuwapongeza kwa kazi nzuri sana ambayo Mawaziri wote wawili pamoja na Naibu Mawaziri wamekuwa wakifanya katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nitoe salamu za pole kwa mtani wangu Mheshimiwa Kakunda kwa shida aliyoipata ya ajali, lakini Mwenyezi Mungu ameendelea kumsimamia na kumuimarisha; naamini ni kwa sababu ya mambo mema anayowatendea Watanzania, basi hata Mwenyezi Mungu ataendelea kumlinda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Rais Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa namna ambavyo anatenda kazi na hasa katika Wizara hii ya TAMISEMI. Hivi karibuni alitoa tangazo la kuzuia pesa za Halmashauri ya Bumbuli kutokana na tatizo kidogo la wapi yajengwe Makao Makuu ya Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natumia fursa hii kutoa shukrani kwa sababu jana yeye mwenyewe amempigia Mbunge wa Bumbuli Mheshimiwa Januari Makamba na kwamba pesa zile zimerudishwa na zitaendeleza ujenzi wa jengo la Makao Makuu ya Halmashauri ya Bumbuli. Tunamshukuru sana kama Wanatanga, hili ni jambo jema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ninazo changamoto kadhaa; ya kwanza ni eneo la kiutawala. Lengo la Serikali za Mitaa, madaraka mikoani pamoja na ugatuzi ni kurahisisha shughuli za maendeleo katika maeneo ya Serikali za Mitaa, lakini bado Mkoa wa Tanga unaonekana ndiyo mkoa wenye Halmashauri nyingi nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyozungumza, Mkoa wa Tanga una Halmashauri 11, una Majimbo ya Uchaguzi 12. Kwa hiyo, hata kuitendaji, baadhi ya shughuli zinasuasua. Mkoa wa Tanga una Shule za Msingi zaidi ya 1,032. Utaona ni mzigo mkubwa sana kuwa na Afisa Elimu ambaye anasimamia shule hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurudi katika Halmashauri ya Lushoto ina shule 162. Sasa utaona kwamba hii ni idadi kubwa ya shule na tunashindwa kuzisimamia na wakati mwingine hata matokeo yanapotoka mara nyingi unakuta hatufanyi vizuri. Kwa hiyo, inawezekana hatufanyi vizuri siyo kwa sababu watu hawana uwezo ama hatujaandaa mazingira wezeshi ya wanafunzi kupata elimu, lakini tatizo ni kwamba, ni eneo kubwa la kiutawala kiasi kwamba wanashindwa kusimamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua liko zuio kwamba sasa hivi hakuna kugawanya mikoa ama Majimbo na kadhalika, lakini ni lazima ukweli tuseme, ieleweke hivyo kwamba Mkoa wa Tanga ndiyo mkoa pekee katika Jamhuri ya Muungano wenye Halmashauri 11 inafuata Morogoro, ina Halmashauri tisa; Mtwara ina Halmashauri tisa; Kagera, Halmashauri nane; na Mara Halmashauri tisa. Kote huko ukiangalia kwenye mikoa ambayo ina Halmashauri nyingi kuna matatizo ya kiutawala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni lazima tukae na Serikali iweze kuona. Mathalan kuna mikoa ambayo ina chache. Mkoa wa Rukwa una Halmashauri nne, Mkoa wa Songwe una Halmashauri tano, Mkoa wa Iringa una Halmashauri tano, Mkoa wa Shinyanga, Halmashauri sita; Geita, Halmashauri sita. Kwa hiyo, mkoa wenye Halmashauri 11kulinganisha na mkoa wenye Halmashauri tano au nne, maana yake kwa kweli katika ulinganishi hatuwezi tukatenda sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija katika Shule za Msingi, nimesema Mkoa wa Tanga una shule 1,032; Mkoa wa Kagera 955; Mkoa wa Kilimanjaro 973. Kwa hiyo, Tanga bado inaongoza katika Shule za Msingi. Ukija Iringa kuna Shule za Msingi 499; Katavi kuna shule 177 ambazo ni chache kushinda hata zilizopo Wilaya ya Lushoto. Geita kuna shule 603. Sasa hawa Maafisa Elimu watasimamiaje kwa ulinganifu ambao hauko sawa? Kwa hiyo, tunaomba Wizara hii iweze kuliona hili jambo na kututafutia solution. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukija kwenye suala la miundombinu ya elimu, tunao uhaba mkubwa wa Walimu katika Halmashauri ya Lushoto. Mahitaji ya Halmashauri ni Walimu 2,408, waliopo ni 1,547. Kuna upungufu wa Walimu 861. Utaona ni gap kubwa sana. Kwa hiyo, tunaomba sana tutoe kipaumbele kwa maeneo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa upande wa Walimu wa Sayansi tunazo sekondari 60 ambazo zina upungufu wa Walimu 123.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ningependa nilizungumzie ni suala la mipango pamoja na TARURA. Sasa hivi mpango wa Serikali ni kufikisha umeme vijijini 2020/2021 ndiyo utakuwa mwisho, lakini yapo maeneo ambayo mpaka sasa hivi hayana barabara. Sasa sioni connection kati ya mipango hii ya mwaka mmoja na miaka mitano ya Kitaifa katika Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yangu ni kwamba tunatarajia kwamba TARURA wameanza kuchukua barabara zile ambazo Halmashauri ilikuwa tayari iko nazo, lakini tukumbuke kwamba kuna vijiji vingine viko katika maeneo ya milima kutokana na jiografia, bado havijafikiwa na huduma ya barabara. Ukiwaambia TARURA wanakwambia bado hii hatujaipokea, tumepokea zile ambazo zilikuwa zinahudumiwa na Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe rai kwamba ili mipango ya Serikali isiwe double standard kwamba umeme vijijini mwisho ni 2020/2021, basi iwe sambasamba na utengenezaji wa barabara ili watu wa umeme waweze kufikisha zile nguzo kule. Bila kuwa na barabara, nguzo zitafikaje? Kwa hiyo, nawaomba sana TAMISEMI hili jambo waliangalie kwa kina. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kilimo, nataka nizungumze wazi na kwa sababu tunashauri na kuisimamia Serikali, mimi kwenye Halmashauri yangu, sioni umuhimu wa kuwa na Maafisa Ugani kwa sababu hawaongezi chochote katika kilimo. Hapa juzi nimezungumza suala la kilimo cha kahawa, kila Mbunge ananiuliza kwamba Lushoto kuna kahawa? Maana yake ni kwamba hata Serikali inawezekana hawajui kwamba milima ya usambara kuna kilimo cha kahawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hapa una Maafisa Ugani ambao hawawezi hata kutoa taarifa kwenye Serikali. Kwa hiyo, hata katika huu uhaba wa Walimu hata mimi nimuunge mkono Mheshimiwa Dkt. Kikwembe kwamba ukiniambia uondoe Maafisa Ugani uniletee Walimu, nitashukuru, kwa sababu sioni kazi wanayofanya kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, tumekuwa na idara inayotabiri hali ya hewa, inaeleza kuhusu hali ya hewa kwamba safari hii tutakuwa na mvua chini ya wastani, safari hii tutakuwa na mvua nyingi; unatarajia kwamba Maafisa Kilimo wachukue hizi taarifa za hali ya mvua wazitafsiri kwa wananchi, lakini bado wananchi wanalima kwa mazoea. Hawajui kwamba tukilima mahindi mvua zitakata mapema, hawajui kwamba tukilima labda mahindi sehemu za mabondeni, tumetabiriwa kutakuwa na mvua juu ya wastani, kwa hiyo, kuna mafuriko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, katika eneo hilo napenda kusema wazi kabisa kwamba Idara ya Kilimo katika Halmashauri yangu ya Lushoto, lakini naamini hili ni katika nchi nzima kwa sababu tumeona hata katika mpango kwamba kilimo kinakua kwa asilimia 3.3, kwa hiyo, hili ni eneo ambalo linatakiwa litizamwe kwa mapana sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la utawala bora ambalo tunalizungumza mara kwa mara na kwa bahati Mheshimiwa Mkuchika alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Tanga, anafahamu. Tunao Wenyeviti wa Vijiji na kwa mujibu wa kanuni hapa tunaambiwa kwamba sheria asilimia 20 ya mapato ya Halmashauri inatakiwa iende kulipa hawa Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji. Mpaka sasa wana zaidi ya miaka saba wanadai hawajalipwa chochote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukizungumza hapa asilimia tano na asilimia kumi, tunazungumza tu kwa ajili ya vijana na akinamama, lakini mbona hatuzungumzii hao Wenyeviti wa Serikali za Vijiji ambao mpaka sasa hivi hawapati hizi posho zao, kiasi kwamba hata kwenda kusimamia shughuli za maendeleo wakati mwingine wanafanya kama hisani, kwa sababu hawapi motivation yoyote. Kwa hiyo, nitoe rai kwamba tunapozungumza suala la utawala bora, ni lazima pia tuzingatie maslahi mapana ya hawa watenda kazi katika ngazi za vijiji na ngazi za vitongoji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni miradi ya maji. Tunashukuru kwamba miradi ya maji inaendelea kufanyiwa kazi, lakini kwa changamoto hata Kamati ya LAAC ilivyokwenda katika Mkoa wa Tanga kuna matatizo makubwa ya usimamizi wa miradi ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani kwa utafiti wangu, tatizo liko kwa Mhandisi wa Maji wa Mkoa. Anaonekena aidha kama nilivyozungumza awali kwamba ana Halmashauri nyingi za kuhudumia, kwa hiyo, anashindwa kuwa na ufanisi kiasi kwamba hasimamii vizuri maeneo haya ya miradi, inachukua muda mrefu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninao mradi wa kutoka Gorogoro, Manoro hadi Kijiji cha mwisho ambacho ni Madala, eneo la mradi ni kilometa 54, lakini sasa nazungumza hapa ni mwaka wa tatu, bado kasi ile hairidhishi. Nitoe rai sasa kwamba wasimamie kwa kina kwamba tunapo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzunguzaji)

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kutoa mchango wangu katika hoja iliyoko mbele ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mpango pamoja na Naibu wake Dkt. Ashatu Kijaji kwa kazi nzuri ambayo wanaendelea kuifanya. Hali kadhalika shukurani hizi pia zifike Mamlaka ya Mapato (TRA) kwa kazi nzuri ya ukusanyaji ambayo inaendelea na watendaji wote walioko katika Wizara hii. Mwisho, lakini si kwa umuhimu bali kwa kipekee kabisa nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri sana ambayo anaifanya.

Mheshimiwa Mwen yekiti, mimi ningetaka kuanza na hili hili la korosho ambalo naona kama linataka kuligawa Taifa. Sisi ni watunga sheria, sisi tunasimamia maslahi ya wananchi, hivyo ni lazima wakati tunafanya wajibu huo tuhakikishe kwamba ndimi zetu tunazielekeza katika kujenga Taifa na si katika kulipasua. Tutajadiliana kwa hoja, tutabishana kwa hoja mbalimbali lakini msingi wetu mkubwa uwe katika namna bora ya kujenga, siyo namna ya kuanza kugawana mbao za Taifa hili la Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tukianza kuzungumza kanda, kanda, kanda naamini hatutabaki kuwa na Taifa linaloitwa Tanzania. Kwa hiyo nitoe rai sana kwa Waheshimiwa Wabunge tujadili ma mbo haya kwa hoja, kwa fact, kwa data lakini tusiingize haya mambo ya kuanza kuvutana kwa misngi ya Kanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili suala la korosho ambalo kwa Sheria hii ya Mwaka 2010, nataka nianzie hapo hapo kwamba, lazima kwanza pia tutafakari kwamba kwa hiyo miaka mitano, hizi pesa zilivyokuwa zinakwenda zimefanya kazi ya kuongeza uzalishaji kwa kiasi gani? Sasa hapa ni lazima Wizara ikiwezekana ifanye uhakiki wa namna bodi ilivyoweza kusimamia hizi hela tangu hiyo mwaka 2010 hadi sasa; je, ni kwa kiasi gani imeongeza tija si tu katika uzalishaji lakini kwa yale makusudio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu mojawapo ya kuanzisha hii export levy ilikuwa ni ku-discourage kusafirisha korosho ghafi kwenda nje ili ikiwezekana sasa tuwe na viwanda vya kubangua korosho. Hata hivyo tunachoshangaa ni kwamba viwanda vingi vya kubangua vimezidi kufungwa. Wameanza Feeder Hussein na kiwanda chao cha Premier cash wamefunga, Olam wamefunga kiwanda wamepelela Msumbiji, Mohamed Enterprises nae amefunga kiwanda; kwa hiyo lazima tuone huu mchakato mzima…

T A A R I F A . . .

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza anachofanya yeye ni kuwahisha shughuli. Nilikuwa nataka nije kwenye sababu, sababu mojawapo ambayo viwanda hivi vimeshindwa ni kwamba wenzetu India kule wao korosho ghafi wanaipa incentive. Kwa hiyo maana yake ni kwamba huku wakati tunaweka export levy ku- ban export wenzetu kule wanatoa incentive ku- encourage watu wasafishe korosho ghafi. Kwa hiyo kama viwanda binafsi vimeshindwa hata vya Serikali pia haviwezi vika-compete kwenye hilo soko. Kwa hiyo lengo hapa ni kwamba, tutafute mjadala wa pamoja siyo huu wa kutishana. Tukianza kutishana na wengine tunazalisha carrot, tunazalisha viazi tutaanza kusema na vyenyewe…

T A A R I F A . . .

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ni hoja yake yeye, sasa hiyo atabaki nayo yeye, mimi ya kwangu ni hayo ambayo nimeyaeleza kwa maana kwamba tujadili mambo haya kwa mapana zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nataka nilizungumzie ni suala la transit goods; TRA hapa lazima tuangalie, tuongeze wigo wa hizi siku, siku 30 ku-clear mizigo ni siku chache sana. Kwa nini nasema chache? Katika siku 30 utoe weekend, wiki nne ukitoa siku mbili mbili ni siku nane, kama itaangukia nayo kuna sikukuu nayo uitoe. Pia tunajua utendaji katika nchi yetu, kuna siku utaambiwa leo system haiko vizuri siku zinazidi kushuka. Kwa hiyo unaweza ukakuta kwamba utendaji kamili wa hizi siku 30 za ku-clear mizigo ni kama siku 20.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri aliangalie hili jambo kwa mapana. Ili bandari yetu iweze kushindana na bandari nyinginezo kama Beira, South Africa na kule Angola, ni lazima tuhakikishe kwamba tunaongeza wigo wa siku angalau zifike 60 hadi hata 90 kwa sababu hili ni eneo ambalo tunaweza tukalitumia vizuri sana kuongeza mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi mzigo unaotoka labda Burundi au Rwanda ukifika pale unatakiwa ndani ya siku 30 uwe umeondoka. Kwanza utakapobaki tunapata storage, tunapata wharfage, kwa hiyo ni lazima suala hili tuliangalie kwa kina; lakini sambamba na mafuta ambayo yanasafirishwa kwenda katika nchi ambazo zinatuzunguka, yakifika siku 30 wanatakiwa waya-localise kama bado yamebaki. Kwa hiyo namshauri sana Mheshimiwa Waziri jambo hili aliangalie kwa kina, linaweza likatusaidia sana kuongeza mapato na pia likaweza kuifanya bandari yetu iweze kushindana. Hii itatusaidia pia kuboresha Bandari hizi za Mtwara na Tanga na hata Bandari mpya hii ya Bagamoyo kwamba zitakuwa za kibiashara zaidi kuliko hivi zilivyo sasa, inakuwa kama ukiritimba umekuwa ni mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ningelizungumza ni suala la kilimo hasa tunapoanza na Benki hii ya Kilimo. Benki ya Kilimo walitakiwa waanze katika mikoa mitano Tanga ikiwemo lakini mpaka sasa bado hawajaanza shughuli zote katika Mkoa wa Tanga. Nadhani kuja kwa Benki ya Kilimo ilikuwa ni mahususi kwa ajili ya kuja kufufua zao la mkonge ambalo zao hili sasa limeanza tena kupanda soko huko ulimwenguni. Kwa hiyo nimsihi sana asimamie katika eneo hili ili Benki hii ya Kilimo iweze kwenda kwenye ile mikoa mitano ambayo inatakiwa ikafungue matawi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kuna suala la kuangalia ushuru katika bidhaa za ambazo zinaingia kama vifungashio; hivi vinaingia kwa zero tax kiasi kwamba sasa vinaathiri uzalishaji wa magunia. Viwanda ambavyo vinazalisha magunia kwa kutumia bidhaa ya mkonge kwanza vinashindwa kupata soko kwa sababu mkonge kidogo upo ghali na hata hii korosho tunayoizungumza ingekuwa ina maana sana kama tungeisafirisha katika magunia yaliyotengenezwa kwa mkonge, maana yake tungeongeza uzalishaji zaidi. Kinachotokea sasa hivi kwamba, tunaingiza vifungashio vinaingia bila ya kodi, vinasafirisha korosho na mazao mengine; kwa hiyo matokeo yake ni kwamba viwanda vinavyozalisha bidhaa za mkonge vinakosa kuzalisha, vinakosa kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo nizungumzie suala la chikichi kule Kigoma. Mheshimiwa Dkt. Mpango anaona wenzetu wanaanza kugawana mbao za Taifa naye anatoka Kigoma. Nadhani uwe ni wakati muafaka wa kuhakikisha kwamba zao la chikichi kule Kigoma nalo linapewa umuhimu wa kipekee. Tukishakuwa na uzalishaji mkubwa wa michikichi; na nadhani kuna maandiko kadhaa kwenye RCC yao kule Kigoma wameshayapitisha, itaweza kusaidia uzalishaji wa mafuta tukichanganya na mafuta haya ya alizeti. Matokeo yake ni kwamba tutaweza kuondokana na hii adha ya kuagiza mafuta kutoka nje na ambayo wakati mwingine yanatuletea shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimsihi sana, michikichi iliyopo kule imeshazeeka sana, haiwezi tena kuzalisha mafuta haya. Kwa hiyo lazima tuanzishe utafiti mpya kwa ajili ya kuweza kuangalia hali ya hewa lakini pia tupate mbegu bora zaidi ambazo zitakuja kuwa na tija katika uzalishaji wa hili ambalo tunalikusudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, ambalo ningependa kuzungumzia suala hili la electronic stamp naye jana alilizungumzia vizuri. Nakubaliana naye kabisa kwamba hili suala ni vizuri tukaenda kwa hatua; tukaanza katika haya maeneo ambayo tayari wameshaanza stamps hizi kawaida, kwenye maeneo ya mvinyo, vinywaji, sigara na vinywaji vikali, kwamba tungeanza huku kabla hatujaingia kwenye hizi daily
consumable goods hizi soda, maji na juisi, kwanza tuziache tuanze na hizi hizi ambazo wameanza nazo ili tuone performance iko namna gani…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi hii na mimi niishie hapo hapo alipoishia mzungumzaji wa mwisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili tuweze kuwa na timu ya Taifa madhubuti tukiziweka akili zetu kwa kutegemea kwamba Simba na Yanga ndio zitakazofanya timu ya Taifa iwe bora tutakuwa tumechelewa sana. Taifa lolote duniani linawekeza katika sera na katika michezo Taifa lenyewe na Taifa kama Senegal, Mali na mengine yote yaliyoko katika ukanda wa Magharibi yamewekeza katika tasnia ya ufundi, lakini pia yakawekeza katika academy. Hili ndilo jukumu la msingi la Serikali, lakini hatuwezi tukaviachia vilabu jukumu la kuendesha timu ya Taifa hiyo haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninachotaka kusema wakati Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita anahutubia Bunge lako Tukufu alieleza wazi hapa kwamba sasa ataanza kutenga fedha kwa ajili ya kuziwezesha timu zetu za Taifa. Huku ndio tunakopaswa kuelekea, hatupaswi kuelekea kuzisubiri Simba na Yanga kwamba ndio zitakuja kututengenezea timu ya Taifa, ni lazima uwekezaji ufanyike kwa maana kwamba tuandae wakufunzi waende wakapate mafunzo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tuandae uwezeshaji wa kisera wa kuwezesha academy ziweze kufanya kazi, lakini pia na uwekezaji katika tasnia nzima ya michezo uweze kuwa wenye kueleweka kama ambavyo kwenye Klabu ya Simba sasa hivi tunaanza kuona matunda ya uwekezaji wetu baada ya miaka minne ya mwekezaji wetu Mohamed Dewji - Mo, ambaye sasa anatupeleka katika hatua ya champions league katika kipindi cha misimu mitatu, mara mbili tumefika hatua ya robo fainali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningetaka kuchangia eneo lingine ambalo limezua mjadala kidogo katika Bunge lako Tukufu. Nataka niseme katika historia ya mpira wetu tangu mwaka 1961 ambapo Taifa hili limepata uhuru, huko nyuma hatukuwahi kuwa na wachezaji wa kigeni hebu tujiulize ukiondoa mwaka 1980 ambao tumekwenda AFCON, ni wakati gani mwingine tumewahi kufika hatua hizo wakati huo hatukuwa na wachezaji hawa wa Kimataifa. Isije ikawa watu wanapaliwa na hili biriani ambalo Simba inacheza ndio wanaanza kuleta hoja nyepesi nyepesi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kusema kwamba mpira ni uwekezaji kuna mtu pale ataweka bilioni 20 kuwekeza ni lazima aoneshe mchezo wake katika uwanda mzima wa kibiashara. Kwa hiyo, hili jambo tuliweke katika mawanda hayo.

MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Rashid Shangazi kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Hassan.

T A A R I F A

MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante napenda kumpa taarifa mzungumzaji anayeongelea kuhusiana na wachezaji wa kigeni. Wachezaji wa kigeni sio tu wanaleta ubora wa ligi yetu ya Tanzania bali wanaongeza kipato cha nchi. Mfano, mchezaji mmoja ambaye ni wa nchi za SADC ili uweze kumsajili maana yake unahitaji kutumia dola 4,700 ambapo ni sawa na shilingi 11,128,880 huyo ni wa nchi za SADC. Mchezaji wa Afrika Mashariki ili uweze kumsajili mchezaji mmoja unatakiwa utumie dola 3,260 sawa na shilingi 7,621,880. Kwa hiyo, kwa timu moja ikiweza kusajili wachezaji wa nchi za SADC kumi maana yake Taifa linakwenda kupata kipato cha shilingi 111,880,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ikiweza kusajili wachezaji 10 wa Afrika Mashariki maana yake Taifa linakwenda kupata kipato cha shilingi 76,218,800. Kwa hiyo, wachezaji waruhusiwe kuja kwa wingi kutoka nje ya nchi ili Taifa liweze kupata kipato. Ahsante kwa taarifa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Rashid Shangazi unaipokea taarifa hiyo?

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Zidadu ambaye ndiye Mwenyekiti wa timu ya Namungo, anaelewa hiki ninachokizungumza. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa taarifa hii pia nimuombe Mheshimiwa Zidadu, juzi wakati lile goli la Bernard Morrison linafungwa wanafunzi wa shule ya Nyangao walishangilia sana, tumepata taarifa kwamba wale wanafunzi wana kesi kidogo kule kwa hiyo, wanafunzi wale wasamehewe. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka kuzungumza ni kuhusu TFF. TFF hii tutende haki imefanya kazi kubwa sana, nadiriki kusema ukiondoa TFF ya Leonard Chila Tenga hii ndio inayofuata kwa kusimamia mpira. Sasa hivi timu zote under 17, under 20, timu za wanawake pamoja na ligi ya wanawake inachezwa hapa nchini ni kwa sababu ya TFF hii chini ya Karia pamoja na Wilfred Kidau wanafanya kazi nzuri sana. Huwezi ukafananisha na FAT ambayo ilikuwa na Mheshimiwa Mhata pale na hii TFF ya leo, wanafanya kazi kubwa sana. (Makofi)

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Rashid Shangazi kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kakunda.

T A A R I F A

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Shangazi kwamba kwa mara ya kwanza tangu dunia iumbwe Tanzania imetoa mchezaji wa mpira wa miguu mwanamke kwenda kucheza mpira wa kulipwa nje ya nje. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Rashid Shangazi unaipokea taarifa hiyo?

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa hiyo kwa mikono miwili na hiyo ndio kazi ambayo anaisimamia Wallace Karia pamoja na Wilfred Kidau.

Waheshimiwa Wabunge lazima tujikumbushe tunapokimbilia kwenye kanuni, haswa tukizingatia mchezo namba 208 ambao kuna watu wanajificha kwenye kanuni; kanuni hizi hizi katika msimu wa mwaka 2016 kuna timu moja ililipa nauli kwa timu ya Ndanda FC itoke Mtwara ije icheze mechi ya mwisho uwanja wa Taifa Dar es Salaam. Wakati kanuni inataka kwamba mechi ikachezwe uwanja wa ugenini kule Ndanda wakati ule kanuni hazikuwepo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna timu moja imemsajili mchezaji wa timu ya Taifa Kelvin Yondani akiwa kwenye jezi ya timu ya Taifa kwenye hoteli ya TANSOMA pale gerezani kanuni zikiwepo. Kuna mchezaji anaitwa Mbuyu Twite amesajiliwa kwa kanuni hizo hizo kwa milango ya uani na Mheshimiwa Tarimba, yote hayo unayajua leo mbona tunamhukumu Karia kwa kuvunja kanuni? (Makofi)

T A A R I F A

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Rashid Shangazi kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Tarimba Abbas.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba afute kauli yake kwa sababu mimi habari hizo sizitambui, ili zisiwepo katika Hansard tafadhali sana. (Makofi/ Kicheko)

NAIBU SPIKA: Haya, Mheshimiwa Rashid Shangazi uzifute taarifa zinazomhusu Mheshimiwa, ama ufute jina la Mheshimiwa Abbas Tarimba kwa sababu yeye hizo taarifa unazosema hana taarifa nazo.

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, hizi taarifa anazo na anafahamu kwamba wakati Mbuyu Twite anasajiliwa yeye alikuwa wapi na ni mdau mkubwa sana wa michezo. (Makofi)

Sasa nilitaka tu niseme kwamba TFF kama kuna mapungufu ni mapungufu ya kibinadamu, lakini kazi inayofanyika pale ni kazi nzuri tunapaswa tuwapongeze. Hata hii hatua ya Simba na Namungo kufika hatua ya robo fainali hatuwezi tukazipongeza hizi vilabu bila kuitaja TFF, wala bila kugusa tasnia nzima ya michezo kwa namna ambavyo imeshiriki. (Makofi)

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge taarifa zimeshakuwa nyingi sana na muda wangu unakimbia taarifa hii itakuwa ya mwisho. Mheshimiwa Katani Katani.

T A A R I F A

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, najua wewe ni mtaalam wa sheria na kwenye sheria wanasema kutenda kosa ni kosa kurudia kosa ni uzoefu wa makosa. Sasa kilichofanywa na Klabu kubwa ni kuwanyoosha watu wasimamie sheria, nampa taarifa mzungumzaji. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Rashid Shangazi unaipokea taarifa hiyo?

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa vizuri kwa sababu Bernard Morrison alisajiliwa na Yanga tarehe 17 Januari wakati dirisha la usajili limefungwa tarehe 15 Januari, amepita dirisha gani kusajiliwa ndio maana ilikuwa rahisi kutoka Yanga kwenda Simba. Kwa hiyo, mpokee haya machungu wakati tunaendelea kuboresha, lakini ukweli ndio huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana ahsante kwa nafasi hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia katika bajeti ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Mlalo, Tarafa ya Umba ni tambarale hivyo maji yanayotiririka kutoka milimani yanapotea bure kwenda baharini upande wa nchi jirani ya Kenya. Rai yetu ni kupata mabwawa makubwa kwa ajili ya kuanzisha skimu za umwagiliaji katika Kata za Mnazi, Lunguza na Mng‟aro. Hili ndiyo eneo pekee lenye ardhi ya kutosha katika Halmashauri ya Mlalo na Lushoto ambalo bado halijatumika.
Mheshimiwa Naibu Spika, ufugaji pia ni changamoto kwani hakuna hata josho moja. Aidha, hakuna hata mabwawa ya kunywesha mifugo ya wafugaji wa Bonde la Hifadhi ya Mkomazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Mlalo jiografia yake ni Milima ya Usambara na kuwa kikwazo kwa shughuli za uvuvi kwa kuwa hakuna mito na maziwa. Tunaomba Wizara ituweke katika mpango wa kutupatia mabwawa ya samaki ili wananchi wangu waweze kupata bidhaa hii katika ubora na kuondokana na tatizo la kuwa na upungufu wa madini ya chuma.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna tatizo sugu la ufungaji wa mazao kwa mtindo wa lumbesa na kuwanyonya kwa kiasi kikubwa wakulima ambao wengi wao ni wanawake na wanalima kilimo hai ili waweze kupata tija ya mazao yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili tuendeleee tunahitaji mambo manne muhimu nayo ni ardhi, watu, siasa safi (good policy) na uongozi bora. Mheshimiwa Waziri hakikisha kupitia halmashauri nchini tunaweka utaratibu wa kuweka Reserve Land Bank ili wakati tunapopata wawekezaji wa kilimo tuwaelekeze huko.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuwajengee uwezo watu wetu hasa wafugaji ili kupata namna bora ya kuwashawishi kupunguza idadi ya mifugo na kupata tija wawapo na mifugo michache. Vile vile badilisha sera ambazo siyo rafiki kwa Wizara yako ikizingatiwa Wizara hii ndiyo mhimili wa uchumi wa Taifa, pia ndiyo chachu ya kuelekea Tanzania ya viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama mnataka mali mtaipata shambani.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Na mimi naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, ameitendea haki Wizara hii tangu Serikali ya Awamu ya Nne na hii ya Tano. Vilevile nampongeza Dkt. Yamungu Kayandabila, nadhani hii ni hotuba ya kwanza ambayo tumekuja humu ndani tukiwa very comprehensive; ina information za kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nampongeza na Naibu Waziri Mheshimiwa Dkt. Angeline Mabula, naye naamini kwamba ameitendea haki nafasi ya wanawake katika uongozi. Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara yako, kwa kweli lazima tuwatendee haki; na kama ambavyo Mheshimiwa Rais anasema tumuombee dua, naamini Watanzania wote watakubaliana na mimi kwamba dua hizo pia tuzielekeze katika Wizara yako.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, Wizara yake inapambana na mapapa wakubwa wa ardhi, lakini tumeona anavyothubutu na kuchukua maamuzi ambayo yana tija kwa wananchi walio wengi. Mimi binafsi napenda nimpongeze kwa kutupatia Halmashauri ya Lushoto Baraza la Ardhi, hiki kilikuwa ni kilio cha miaka mingi na tunaposema Baraza la Ardhi wote tunafahamu kwamba wanaoathirika zaidi na masuala ya ardhi ni akinamama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani wanawake kule Lushoto hasa wale wajane ilikuwa ni lazima wasafiri kwenda mpaka Korogwe wakati mwingine anaambiwa aje na mashahidi wasiopungua sita, sasa yeye ni mjane anaambiwa leta mashahidi, awasafirishe, wakati mwingine awalaze. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri amesikia kilio chetu kwa haraka sana na amechukua hatua na ofisi ile imefunguliwa rasmi Mei 13, tunamshukuru sana na naamini dua hizi za wajane pia zitaelekea kwake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye hii orodha ya mashamba na migogoro ya matumizi bora ya ardhi, katika Wilaya ya Lushoto ameainisha maeneo mawili. Kuna shamba namba 902/3 lakini pia kuna eneo la Kijiji cha Shumenywelo pamoja na shamba la misitu ya hifadhi la Shume. Mgogoro ule ni wa siku nyingi, namwomba sana afike Lushoto akatatue mgogoro huu, umechukua muda mrefu sana na naamini kwa kasi hii ambayo ameanza nayo na ambayo naamini kwamba sio nguvu ya soda atafika maeneo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunalo tatizo la shamba la Mnazi, Mnazi Sisal Estate, lilikuwa chini ya mamlaka ya mkonge. Kama yalivyo mashamba mengine yote na lenyewe limebinafsishwa. Shamba hili lina ukubwa wa takriban hekari 6,000 na ndani yake yapo mashamba matatu. Amepewa mwekezaji mmoja kutoka nchi jirani ya Kenya. Wakati anakabidhiwa shamba hili, amekabidhiwa hekari 1,500 zenye mkonge. Hivi ninavyozungumza hapa, hekari ambazo zina mkonge ni 45 tu. Kwa hiyo, kadri muda unavyozidi kwenda ndiyo anavyozidi kushusha uzalishaji. Nimwombe Mheshimiwa Waziri, shamba hili tulirudishe kwenye miliki ya Serikali halafu tutalitafutia uwekezaji mwingine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, shamba hili pia lina migogoro na vijiji vinavyolizunguka, kipo Kijiji cha Kwemng’ongo na Kijiji cha Kwemkazu. Hawa kuna wakati fulani mwekezaji huyu aliwapa hekari 750, lakini baadaye amewanyang’anya kwa hiyo, naomba sana suala hili tulifanyie kazi kwa sababu ardhi hii imekaa haina kazi yoyote na Wilaya ya Lushoto kwa ujumla ina matatizo ya ardhi na hii ndiyo ardhi pekee ambayo tunaweza tukaipata kubwa ya kuweza kutusaidia katika masuala mazima ya uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo Wilaya ya Lushoto maeneo mengi sana yanamilikiwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania. Kwa ukweli wanayamiliki kihalali, lakini yapo baadhi ya maeneo ya Taasisi haswa shule pamoja na vituo vya afya yapo katika maeneo haya. Nimwombe Mheshimiwa Waziri kwamba, kwa busara anaweza akatukutanisha nao ili angalau yale maeneo ambayo yanatumiwa na umma waweze kuyatoa kwenye hati zao ambazo wanazimiliki kwa mujibu wa taratibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni suala zima la land bank, kwamba Halmashauri zetu nyingi hazina hifadhi ya ardhi na huko kwenye Halmashauri wanatoa ardhi hovyo hovyo hasa kwa watu ambao wanakuja mara nyingi kwa kigezo cha uwekezaji. Sasa niombe Wizara kupitia sera ije na sera mahsusi ambayo inazitaka Halmashauri zetu zitenge maeneo mahsusi kwa ajili ya uwekezaji, kwamba yawepo tu, yawekwe kama hifadhi ya ardhi kwa ajili ya uwekezaji wa siku za usoni. Kama ambavyo juzi Mheshimiwa Mbowe alikuwa anazungumzia suala la hekta 11,000 – zile kwenye suala la uwekezaji wa ardhi ni chache sana. Kwa hiyo, nataka niseme kwamba ni lazima kuwe na sera madhubuti ambayo inalizungumzia suala hili ili tunapo zungumza kwamba tunataka maendeleo tuwe na ardhi, watu na siasa safi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siasa safi hapa ni good policy. Policy ambazo ni nzuri za kuweza kuwa na matumizi bora ya ardhi ili iweze kuleta tija kwa wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo, naomba nikushukuru sana na niwapongeze pia timu ambayo inamsaidia Mheshimiwa Waziri, tunawatakia kazi njema na ufanisi mwema. Ahsanteni sana.
Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Na mimi napenda kwanza kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa wasilisho lake japo lina upungufu, lakini ndiyo mwanzo wa Serikali yetu ya Awamu ya Tano. Tuko hapa kwa ajili ya kuyaboresha ili angalau bajeti itakayokuja mwaka unaofuata waweze kuyarekebisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza na suala zima la TBC. Kama alivyomaliza kuzungumza mzungumzaji aliyemaliza, mawasiliano ya TBC hasa kwa mikoa ya pembezoni bado hayapatikani na hususan katika Wilaya ya Lushoto ambayo ina population ya watu takribani 500,000 wanapata redio zinazotoka Kenya, hasa Mombasa na Nairobi. Sasa ipo hatari kwamba wananchi hawa watakuwa hawapati huduma za habari la Taifa lao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Nape pamoja na Mkurugenzi wa TBC Dkt. Ayoub Rioba, najua yuko hapa, kule Lushoto hatupati matangazo ya TBC. Mwandishi wa habari, ndugu yangu Suleiman Mkufya, tulikuwa naye kwenye kampeni, kila mahali alipokuwa anakatiza ndiyo swali alilokuwa anaulizwa kwamba mbona TBC Lushoto haipatikani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nizungumzie la soka. Nitatofautiana na wachangiaji waliotangulia kwa maana ya kuipa uhai timu ya Taifa. Naamini katika hii miaka ya karibuni hata tufanye vipi, hakuna miujiza ya kuweza kwenda kwenye mashindano makubwa kwa kupitia crash program. Bila uwekezaji wa maana kufanyika katika soka, soka haina njia ya mkato.
Nawapongeza sana wenzetu wa Alliance Academy wale wa Mwanza, vile ndiyo vitalu ambavyo vinaweza vikatufanya siku za usoni tuweze kuheshimika katika medani za soka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna Chuo cha Michezo cha Malya. Chuo hiki kilikuwa kinatoa elimu za michezo lakini kinatoa ngazi ya preliminary. Tunaomba Mheshimiwa Waziri alifanyie kazi, waanze kuongeza, angalau kitoe mpaka ngazi ya diploma pamoja na ngazi ya Shahada. Tutakapokuwa na walimu wa michezo wa kutosha na tukawatawanya kwenye shule, ndiyo hawa baadaye wanaweza wakaleta tija kwenye ulimwengu wa michezo katika Tanzania yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hivi kama tunataka mafanikio ya njia ya mkato, basi tutayapata kupitia timu ya wanawake ya Twiga Stars. Twiga Stars ilikuwa inafanya vizuri sana na mara zote ilikuwa inafika hatua ambayo kama kungekuwa na uwekezaji wa maana, kama ingekuwa inatafutiwa wafadhili kama ambavyo zinatafutiwa timu za wanaume, naamini timu hii ingekuwa imeshafika katika fainali za Afrika. (Makofi)
Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Waziri na wenzetu wa TFF, Mheshimiwa Kadutu yuko humu ndani, kwamba tujaribu kuweka uwekezaji kwenye timu ya Twiga Stars. Timu hii inaweza ikatutoa kwenye suala la crash program, kwa muda mfupi tunaweza tukaenda mahali fulani na tukafanikiwa. (Makofi)
Suala lingine ni kuhusu Baraza la Sanaa la Taifa. Baraza hili linafanya kazi kama wenzetu wa TFDA kwamba wanasubiri bidhaa ziko sokoni ndiyo wanaenda kukamata wauzaji wa zile bidhaa. Nawaomba wasifanye kazi kwa namna hiyo. Tumeona video ya chura ambayo imekuwa kwa kweli inadhalilisha, nashangaa bado hatujapata matamko kutoka kwa akina mama, lakini video ile haistahili kuangaliwa na Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tuna tamaduni zetu. Ni vizuri Baraza la Sanaa la Taifa likasimamia wasanii wetu kuhakikisha kazi wanazofanya lazima ziwe zinazingatia maadili na tamaduni zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uandishi na utangazaji; ni kweli kabisa kwamba waandishi wetu wanafanya kazi katika mazingira magumu, wakati mwingine habari hizi wanazozitafuta hasa habari za uchunguzi, zikiwemo za mauaji ya vikongwe, albino pamoja na habari za huko mikoani, nyingi wanazifanya katika mazingira hatarishi. Ni vizuri Wizara ikaja na sera maalum ya kuweza kuwalinda waandishi wa habari ili waweze kupata bima ili wanapokuwa katika kazi zao, waweze kuwa na uhakika wa maisha yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine pia tuhakikishe kwamba kuna chombo cha kupima weledi wa waandishi wa habari, kwa sababu wapo wenzetu waandishi wanageuza baadhi ya watu kuwa bidhaa. Unashangaa gazeti kila siku linaandika habari za mtu mmoja ambazo ni habari za kutunga, wakati mwingine hazina uhakika wowote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, weledi katika uandishi uzingatiwe, tuepuke uchochezi. Watangazaji nao siku hizi kunakuwa na mipasho mingi kwenye vyombo vyetu vya habari, hawaongei mambo ya msingi, hasa katika vipindi vya taarabu, wanazungumzia mambo ya mitaani ambayo hayana tija sana kwa Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa mwenyekiti, suala lingine ndugu zangu, nilikuwa naongelea suala zima la deni la Serikali. Serikali imekuwa inakwenda pale TFF na kuingia kwenye akaunti zao na kuchukua pesa. Mwanzo wa mambo yote haya ni katika mechi ile ya Tanzania na Brazil. Mechi ile kwa tunaofahamu ni kwamba iliandaliwa chini ya Serikali ya Awamu ya Nne kupitia Ikulu na zilitolewa takribani shilingi bilioni tatu kwa maandalizi ya mechi ile. Mapato yaliyopatikana kwenye mechi, nadhani ni kama shilingi bilioni 1.8, hizo nyingine hatujui kwamba Mheshimiwa Rais alizitoa wapi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo TRA walikuwa mara kwa mara wanaingia katika akaunti za TFF na kuchukua pesa. Sasa msingi ni kwamba mechi ile iliandaliwa na Kamati maalum, haikuandaliwa na TFF. TFF walikuwa tu ni waendeshaji wa mpira lakini katika mechi ile hawakuhusika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine katika hilo hilo, ni kwamba kulikuwa na mshahara wa kocha ambaye aliletwa na Serikali ya Awamu ya Nne, Marcio Maximo. Kwanza tunamshukuru sana kocha huyu kwa sababu alileta hamasa kubwa sana katika mpira wa Tanzania, aliifanya TFF ya Rais Leonard Chila Tenga kuwa taasisi ambayo iliheshimika sana na mwamko katika nchi uliongezeka sana. Kocha huyu alikuwa analipwa pia kupitia Serikali. Sasa tunashangaa baada ya muda TRA wanadai kodi ya mapato ya mshahara wa kocha wa TFF. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuishauri Serikali kwamba hebu ilifanyie kazi suala hili TFF inajiendesha yenyewe kupitia mapato ya mlangoni, haina ufadhili wa kutosha. Sasa hivi tumeiachia pia jukumu la kuandaa timu ya Taifa ambapo kimsingi wenzetu wa Afrika Magharibi timu hizi zinaandaliwa na Serikali. Bila Serikali kuweka mkono katika timu ya Taifa, tusitarajie miujiza yoyote kama tunaweza tukaenda huko ambako tunatabiri kwenda. Ni lazima Serikali iweke uwekezaji wa kutosha lakini wakati huo huo iwa-support wenzetu wa TFF, wanayo kazi ngumu, zipo timu zaidi ya nne ambazo wanatakiwa kuziandaa, wao peke yao hawatoshi. Hiki kidogo ambacho tunakipata, bado Serikali inaenda inakichukua ilhali suala la mshahara wa kocha lilikuwa limetokana na mshahara ambao Rais aliahidi kwamba atatoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine naomba kwa mara ya kwanza leo nimpongeze Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Mheshimiwa Sugu, amezungumzia suala zima la miziki ya ndani kupigwa kwa asilimia 80. Mimi nasema, isiwe 80, twende hata mpaka 90. Sasa hivi hata hao wasanii wetu wanakuwa wa Marekani zaidi ama wa…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, ahsante sana na naunga mkono hoja
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi ya kutoa mchango wangu katika Wizara hii muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu. Nianze kwa pongezi, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri na kubwa ambayo anaifanya hasa katika eneo la kuboresha miundombinu ya elimu; elimu msingi, elimu secondary, lakini pia na katika ngazi ya vyuo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ameelekeza pesa zile za UVIKO takribani shilingi bilioni 300 kwa mkupuo mmoja kwenda katika Sekta ya Elimu ambazo zimekwenda kujenga madarasa takribani 13,000 nchi nzima na sasa tumeweza kuona tija kubwa ya elimu, hasa katika eneo la miundombinu. Hii ni historia, ni lazima tuiseme bila kificho, kwa sababu, katika uhai wa Taifa letu hakuna uwekezaji mkubwa kwa wakati mmoja katika Sekta ya Elimu ambao umefanyika kuliko kipindi hiki cha miaka miwili ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nimpongeze pia, Waziri mwenye dhamana hii ya Sekta ya Elimu, kaka yangu, mtani wangu, Mheshimiwa Profesa Mkenda pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Kipanga, lakini na watumishi wote wa Wizara hii ya Elimu kwa kazi nzuri ambayo wanaendelea kuifanya. Kipekee niwapongeze kwa rasimu ile ya Sera ya Elimu, ni rasimu ambayo imekuja wakati muafaka na wakati sahihi. Niwaombe sana sasa waendelee kuchukua na kupata maboresho kutoka kwa wadau mbalimbali ili tuboreshe jambo letu hili liweze kuwa na tija ambayo tunaikusudia, lakini ambayo itakuwa ya muda mrefu zaidi katika Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile niwapongeze Kamati, wamefanya kazi nzuri, wasilisho zuri. Kwa hiyo, kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kuchangia katika eneo ambalo Kamati imelitaja kama changamoto. Eneo ambalo kuna mgongano wa wazi kati ya taasisi mbili za Serikali, Wizara mbili; Wizara ya Elimu ambayo kimsingi inasimamia sera, lakini kuna Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ambayo yenyewe inasimamia utekelezaji wa elimu katika Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hawa wawili kuna wakati wanatoa maelekezo ambayo yanawachanganya, hasa sekta binafsi. Kwa bahati mbaya sana sekta binafsi haina chombo ambacho inakisimamia, hakuna Wizara mahususi ambayo inaisimamia sekta binafsi ya utoaji wa elimu. Hawa kama Wizara wanasimamia eneo la sera peke yake, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa wanasimamia shule, lakini wanasimamia shule zinazomilikiwa na umma, maana yake ni kwamba, shule za sekta binafsi hazina msimamizi. Ndio maana kuna nyakati yanatoka matamko ambayo moja kwa moja yanaenda kuathiri utendaji kazi wa shule hizi za binafsi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niombe kwamba, kama ambavyo pia Kamati imeshauri, ni vizuri Serikali ikatengeneza chombo ambacho kitakuwa kinasimamia Sekta ya Elimu msingi na sekondari, kwa maana kama Tanzania Education Sector Authority, ili iweze kuchukua wajibu kama wa TCU katika ngazi ya vyuo vikuu kwa sababu TCU wanasimamia vyuo vikuu vyote vya binafsi na vile vya umma, lakini ukija katika vyuo vya kati kwa maana ya vinavyotoa certificate na diploma ambapo kuna NECTA VETA pale, nayo inasimamia eneo la vyuo binafsi, lakini na vyuo vya umma. Kwa hiyo, hii itasaidia sana katika kuondoa huu mgongamo ambao upo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo ambalo linafanyika, si jema sana kwenye sekta ya binafsi. Kuna tozo karibu 17 ambazo zinatozwa katika sekta binafsi. Kwa kweli, tunawanyanyasa kwa sababu, hawa ni watoa huduma, lakini sisi tunawachukulia zaidi kama wafanyabiashara. Kwa nini nasema ni watoa huduma? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi ukiangalia wanafunzi walioko katika shule za binafsi kuanzia awali mpaka sekondari ni takribani wanafunzi 860,000. Maana yake ni kwamba, shule hizi zisingekuwepo Serikali ilikuwa ina wajibu wa kuhakikisha kwamba, watoto hawa wanakuwa na miundombinu, wanakuwa na Walimu, wanakuwa na capitation, wanakuwa na kila kitu ili waweze kupata elimu, lakini watoto hawa wakimaliza elimu huko wanakosoma, wanakuja kuajiriwa katika Taifa hili ambalo pia, watatoa mchango wao. Sasa ni kwa nini sisi bado tunaichukulia sekta ya binafsi ya elimu kama biashara, badala ya kuichukulia kama wasaidizi na watoa huduma? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo napenda kushauri kwamba tozo hizi 17 kama ambavyo tumeweza kupunguza tozo kwenye kilimo, tumepunguza tozo kwenye mazao mbalimbali na sasa tutazame tozo hizi katika sekta ya elimu, tukianza na service levy ambayo kwanza inakinzana hata na Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa. Hili ni jambo la muhimu sana la kulitazama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ukilitazama hapa utaona kwamba sekta binafsi ina mchango mkubwa katika eneo hili ni idadi ya walimu ambao wameajiriwa na sekta binafsi. Takribani walimu 55,000 hii ni idadi kubwa sana. Na hawa huko walipo wanalipa kodi za Serikali na wanasaidia sasa eneo zima hili la kutoa elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yake ni kwamba zisingekuwepo hizi hawa nao ilikuwa ni tatizo ambalo Serikali ilibidi iwatafutie ajira. Kwa hiyo, hili ni jambo muhimu sana, kuwatazama sekta binafsi kama watoa huduma na tusiwatazame kama wafanyabiashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo ninataka kulisema ni hili la udhibiti ubora ambalo limezungumzwa, ni jambo ambalo kwa kweli inabidi tutafute chombo ambacho ni huru zaidi kama CAG fulani hivi wa upande wa elimu, ili atoke katika ofisi ambayo haina hata mgongano wa kimaslahi na hawa anaokwenda kuwasimamia. Hii itaongeza tija kubwa sana katika elimu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ni kikwazo, naliona sasa limekuwa kama ni fashion, kuna wakati tunazungumza suala la elimu bila malipo ama elimu bure ambapo Serikali inaweka ruzuku pale. Lakini sasa kuna utitiri wa mitihani ambayo inafanyika, kuna mtihani wa Kijiji, mtihani wa Kata, mtihani wa ujirani mwema, wa Jimbo, yote hii inakwenda kwa mzazi. Kwa hiyo, mzazi huyuhuyu aliyeondolewa mzigo wa michango huku anajikuta sasa anachangia mitihani ambayo imekuwa mingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatukatai, mitihani ni kipimo, lakini hawa walimu nao ambao kila siku wako katika hatua mbalimbali za kuandaa mitihani, mitihani yenyewe inatakiwa ichapwe, inatakiwa isimamiwe, inatakiwa isahihishwe, wanapoteza muda mrefu wa kufundisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi wote tumesoma katika hizi shule. Huko zamani hakukuwa na utitiri huu wa kupima mitihani ambayo ni mingi kiasi hiki. Kwa hiyo, ninadhani kwamba ni busara sana tuangalie eneo hili vizuri kuona kama kuna tija ya huu utitiri wa mitihani. Kwa sababu pia unachukua muda mrefu sana kuanzia kuandaa, kusimamia, kusahihisha na mambo mengine. Kwa hiyo kwa maoni yangu, nadhani inapunguza muda wa kufundisha na ndiyo maana sasa watoto wetu wakati mwingine labda wanakuwa ni wa matokeo zaidi kuliko wa hali halisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho ninalotaka kulichangia ni suala la sekta binafsi kama ambavyo nimetangulia kusema na usimamizi mzima wa sekta hiyo, na hasa yale maeneo ambayo bado tunayaona kwamba hayana chombo kinachosimamia.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni ilitokea sintofahamu ya mabasi yanayosafirisha watoto, hasa katika shule binafsi kwa sababu ndiyo zenye utaratibu huo, lakini yakatoka matamko kutoka kwa Kamishna wa Elimu na kwingineko, kitu ambacho kwa kweli siyo sawa, ni lazima hawa wadau wakae kwa pamoja waweze kutafuta suluhisho la pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yangu ni nini, maana yangu ni kwamba sasa hivi tukitazama, kwa mfano watoto wanaokuwa bweni wameambiwa waanzie angalau darasa la tano ni jambo jema, lakini lazima watu wakae kwa pamoja tutazame hizi changamoto vizuri ili tupate suluhisho la pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa mabasi tusitake kuaminishwa kwamba wanaume ndiyo watu ambao hawafai katika jamii, kwamba akifanya kosa mwanaume mmoja basi wanaadhibiwa wanaume wote, kwamba sasa kwenye basi awepo mhudumu wa kike na wa kiume, lakini tunajua kabisa mmomonyoko wa maadili umeigusa jamii yote, wake kwa waume.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Nami naomba kwanza nitoe shukurani za dhati kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa Hotuba yake nzuri ambayo ime-reflect Mpango wa Serikali wa Miaka Mitano; lakini vile vile imejikita katika Hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa Novemba, wakati anazindua Bunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza na kumpongeza sana Waziri wa Nishati Profesa Sospeter Muhongo, kwa kupigana na kuwezesha Serikali yetu kupata mradi ule wa bomba la mafuta kutoka Ziwa Albert kule Uganda hadi katika Bandari ya Tanga. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ile ni fursa nzuri kwa sisi Watanzania kuitumia kama comparative geographical advantage kwamba isiishie tu kwenye kusafirisha mafuta ghafi; lakini iendane sambamba na upanuzi wa Bandari ya Tanga ili iweze kuwa hub ya mizigo ya nchi ya Uganda na pia ushirikiano na wenzetu wa Sudani ya Kusini ambao wamejiunga katika Jumuiya Afrika Mashariki. Tukiitumia fursa hiyo vizuri ya kupanua Bandari ya Tanga kuboresha miundombinu ya reli kutoka Tanga, Moshi, Arusha hadi Musoma; pia sambamba na kuboresha Bandari ya Ziwa Victoria katika bandari ya Musoma, itaweza kuleta tija zaidi kwa Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiwa katika bajeti ya TAMISEMI kama ambavyo iko mbele yetu, naomba na mimi nichangie katika maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza, nitajikita katika eneo la ugatuzi wa madaraka, maana dhana nzima ya ugatuzi ni kuweza kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi, lakini ninavyozungumza hapa mimi ni Mbunge wa tatu wa Jimbo la Mlalo, tunayo maombi yetu Wizara ya TAMISEMI ya kutaka tupate Halmashauri ya Mlalo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Mlalo linaundwa na tarafa tatu, kata 18, vijiji 78, vitongoji 599, sekondari 29, shule za msingi 93. Tunao mwingiliano wa mabasi ya kwenda Arusha, Dar es Salaam na kadhalika. Tunayo magulio makubwa ambayo yanaweza yakaleta watu wengine kutoka Zanzibar, Comoro na Mheshimiwa Ally Salehe pale Mbunge wa Malindi; naye alitoa mchango wake kushuhudia katika hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ombi letu sisi ni kuweza kupata Halmashauri, ili tuweze kuhudumia wananchi kwa ukaribu. Tunavyo vituo vya afya vya kutosha zaidi ya vinne, na viwili tayari vinafanya shughuli ya upasuaji, kwa hiyo, ni imani yangu kwamba Wizara husika italichukua hili na italifanyia kazi kadri inavyowezekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sikupata fursa ya kuchangia kwenye bajeti ya Waziri Mkuu, kulikuwa na suala zima la Baraza la Uwezeshaji la Taifa. Kama ambavyo Hotuba ilivyotoka Baraza hili ndilo litakalohusika na dhana nzima ya hizi shilingi milioni 50 kwa kila kijiji na kwa kila mtaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu ni kwamba, ahadi ya milioni 50 imetokana na zao la kisiasa, kwamba ni utekelezaji wa Ilani ya Chama lakini kwa kuwa tuna uzoefu na mamilioni ya JK; kwamba hayakuwafikia walengwa waliokusudiwa, nitoe rai kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu na Baraza zima hili wa Uwezeshaji kwamba pesa hizi zipitie kwenye mabenki. Mabenki ambayo yana network mpaka kwenye vijiji hata kama ni microfinance pesa hizi zitengenezewe utaratibu tusije tukajidanganya tukazipeleka kwa Makatibu wa Vijiji, ama zikaishia kwenye halmashauri halafu wao ndio wazipeleke huko; tunaweza tukakumbana na kadhia kama ambayo tumekutana nayo katika mamilioni ya JK.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nataka kuchangia ni suala zima la mazao ya kilimo. Serikali ya Awamu ya Tano imejipambanua wazi kwamba tunataka kwenda kwenye uchumi wa kati wa viwanda, ni jambo zuri. Yako mazao ambayo hayapo katika utaratibu huo wa kuwa kwenye viwanda vikubwa; mfano mazao yanayotokana na mbogamboga. Mazao haya kwa halmashauri ya Wilaya ya Lushoto ni kama viazi, kabichi, karoti, nyanya, vitunguu na kadhalika. Mazao haya huwa wanatumia mfumo wa lumbesa kuyapeleka masokoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo huu ulikuwa ni wa unyonyaji sana kwa wakulima. Kwa hiyo, mwisho wa siku mkulima hawezi kupata tija kwenye mazao ambayo anatumia muda mrefu kuyazalisha. Niiombe Serikali kupitia halmashauri waweke utaratibu mzuri wa kuzibana halmashauri zote ziweze kudhibiti huu ufungaji wa mazao kupitia lumbesa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu huu utawasaidia hao wananchi ambao hawawezi kwenda kwenye uchumi wa viwanda; waweze kupata mazao yao katika ubora mzuri wa kupata tija ya faida ya mazao ambayo wanayazalisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la uwezeshaji wa wananchi kupitia miundombinu ya masoko. Huko vijijini masoko bado ni tatizo kama ambavyo nimetangulia kusema kwamba Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto inapokea wageni kutoka maeneo mbalimbali kutoka Zanzibar na Comoro, lakini bado hatuna miundombinu mizuri ya masoko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai kwa Baraza la Uwezeshaji la Taifa kwamba watujengee masoko na kwa kupatikana masoko; inaweza ikawa ni tiba mojawapo ya kupunguza haya matatizo ya lumbesa kwa sababu naamini wakulima watakuwa wanauza mazao yao katika masoko yaliyoko karibu na maeneo yao, hawatakuwa na haja ya kuwauzia wachuuzi ambao huwa ndiyo wanapeleka katika mtindo wa lumbesa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la utawala bora; nimefarijika kuona katika Hotuba ya Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora wamezungumzia suala zima la uanzishaji wa Idara ya Mikataba na Utendaji Kazi Serikalini. Jambo hili ni jema, tunaomba lifanyiwe kazi na utaratibu uanze mara moja ili mwisho wa mwaka waweze kupima tija ya wafanyakazi wa umma pamoja na wafanyakazi katika idara mbalimbali za Serikali. Hii itazidi kuongeza uwazi na uwajibikaji miongoni mwa Taasisi na Idara za Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la chaguzi zetu ambazo tumekuwa tunaendelea kuzifanya. Lazima tukumbuke kwamba chaguzi hizi zinafanywa kwa mujibu wa sheria, lakini pia zipo tume ambazo zinasimamia, ni vizuri sana tusilitumie Bunge kama sehemu ambayo kila siku tunaongelea jambo ambalo limekuwa linatolewa ufafanuzi mara kwa mara. Tunapozungumza dhana zima ya utawala bora pamoja na utumbuaji wa majipu tusijaribu kuegemea upande mmoja hata kwenye vyama vyetu ni lazima tuhakikishe kwamba dhana nzima ya utawala bora pia inapatikana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mfano ambao nisingependa sana kuutumia kwa jinsi ambavyo namuheshimu kaka yangu Mheshimiwa Zitto Kabwe, lakini naomba tu niutumie, kwamba hata yeye alipokuwa na kesi na chama „X‟ siku ambayo hukumu imesomwa basi wamemtangazia pale pale mahakamani kwamba kuanzia wakati ule sio mwanachama wa chama kile, hawajampa hata muda wa kufanya hiyo natural justice. Sasa haiwezi ikawa akijisaidia kuku ndiyo kajisaidia, lakini akijisaidia bata basi inakuwa ni matatizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ezekiel Wenje Mbunge wa Nyamagana kwenye Bunge lililopita, alizungumza sana kuhusu suala la Mheshimiwa Kabwe ambaye alikuwa Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza, sasa leo anatumbuliwa hadharani bado watu tunahoji kwa nini huyu mtu hapewi haki ya kusikilizwa. Niwaombe tunaposema upinzani, tunataka kwamba tuwe na Serikali mbadala na naamini kwamba upinzani wa kweli umeondoka na Mheshimiwa Zitto Kabwe na Mheshimiwa Dkt. Willbroad Slaa, uliobaki Bungeni sasa hivi ni upingaji sio upinzani, tumeona kete moja ya ACT Wazalendo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona na mimi nichangie katika bajeti hii muhimu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nianze na suala la Mkaguzi na Mdhibiti wa Serikali (CAG) kwamba pesa alizotengewa shilingi bilioni 44.7 ni pesa ambazo haziwezi zikamfanya afanye kazi yake kwa ufanisi. Tunapozungumza matatizo yaliyoko kwenye Halmashauri zetu tunayatambua na Serikali ya Awamu ya Tano imejipambanua kwamba ni Serikali ambayo imekuja kudhibiti ufisadi, sasa huyu mtu ambaye ndiye anayetambua ngazi ya mafisadi katika ngazi ya Halmashauri na kwenye taasisi tunapompa fungu dogo maana yake tusitarajie kwamba hata yale majipu yatakuja kupasuliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumeona kwamba ofisi hii tangu imeanza kufanya kazi imekuwa inafanya kazi nzuri sana, kazi ambayo kila mwaka ilikuwa inatoa tija na ilikuwa inaleta mwanga hata kwenye Halmashauri zetu na walikuwa wanatujengea uwezo hata Waheshimiwa Wabunge kupitia Kamati hizi za LAAC namna ambavyo tunaweza kudhibiti mianya ya pesa za Serikali ambazo zinapotea kupitia Halmashauri zetu.
Kwa hiyo, nitoe rai kwa Waziri wa Wizara husika aliangalie suala hili kwa jicho la tahadhari sana kwamba kama tutamnyang’anya CAG uwezo maana yake ufisadi uliotamaliki katika Halmashauri zetu utaendelea zaidi kutafuna miradi mbalimbali inayoelekea katika Halmashauri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili nizungumzie suala la gratuity (mafao haya ya Ubunge). Mimi niseme kwamba Mheshimiwa Waziri amewahisha shughuli, suala la mwaka 2020 analizungumza leo, niungane na wenzangu kusema kwamba anatu-beep Wabunge. Niseme Sheria Namba 4 ya mwaka 1999 inazungumzia wigo mpana wa hawa wanasiasa ambao walikuwa wamesamehewa hii kodi. Kwa nini wawe Wabunge peke yao, hili ni suala la kutufanya tuamini kwamba kweli anatu-beep. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niseme kwa kuwa kodi hii ya mwendo kasi ambayo anajaribu kwenda nayo atukimbize kwa miaka minne ambayo haina tija kwa bajeti ya mwaka huu basi alitafakari kwa kina sana na aangalie hivi vilio vya hawa Waheshimiwa Wabunge sisi huko majimboni kila jambo ni la kwetu.
Vipaimara vinatuhusu, Maulid tunamaliza sisi, kukiwa na watoto kwenye chanjo, kwenye mwenge, kwenye kila kitu sisi ndiyo tunaohusika. Kwenye majimbo huko michezo inabembwa na Wabunge na hata ukitoka kwenye mageti yetu sasa hivi pale unakuta wauza mipira wote wamejaa kwenye mageti wanasubiri zianze Jimbo Cup, utashangaa mara Mhagama Cup, Mwinyi Cup, Cosato Chumi Cup yote haya ni matatizo ambayo yanawasibu Wabunge. Naamini hata kule Mbeya mwaka huu utasikia Tulia Ackson Cup. Sasa Mheshimiwa Waziri tunakuomba sana uliangalie hili kwa jicho la tahadhari. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye tozo ya utalii ya asilimia 18 kwenye VAT kwenye suala la usafirishaji, hili nalo ni eneo ambalo lazima tuliangalie kwa jicho la tahadhari sana. Wenzetu Kenya miundombinu yao ya utalii ni wezeshi sana, Shirika la Ndege linawa-support sana katika utalii sisi bado ndiyo kwanza tumepanga tununue ndege tatu za kuweza ku-boost eneo letu la utalii.
Ningemshauri Waziri kwamba angalau tuende taratibu, hii VAT tunayotaka kuiweka kwenye tozo ya usafirishaji ya utalii hebu kwanza twende kwa tahadhari. Sasa hivi kutokana na nchi jirani ya Kenya kutokuwa na usalama wa kutosha kutokana na mashambulizi ya magaidi wa Al-Shabab sisi tuna advantage nzuri ya kuteka hili soko. Kwa hiyo, ni vizuri tusiongeze gharama za ziada, twende hivi hivi kwanza soko letu liwe madhubuti mbele ya safari huko tunaweza tukaangalia maeneo gani tunaweza tukaboresha.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala zima la reli ya Tanga – Moshi - Arusha - Musoma. Tunapozungumzia msongamano mkubwa wa mizigo na magari katika Bandari ya Dar es Salaam tiba pekee ni kuiwezesha reli ya Tanga kufanya kazi inavyotakiwa. Tunashukuru tumepata neema ya bomba la kusafirisha gesi ghafi kutoka Ziwa Albert kule Uganda mpaka Bandari ya Tanga. Sambamba na hili bomba la mafuta tungeweza kuboresha Bandari ya Tanga ili mizigo ya nchi ya Uganda pamoja na Sudan Kusini iweze kupitia Bandari ya Tanga. Tukipitisha mizigo katika bandari hii tutakuwa tumeimarisha uchumi wa Mikoa ya Kanda ya Kaskazini mpaka kule Musoma na tutakuwa tumewawezesha wananchi wote ambao wanapitiwa na hii reli ya Tanga - Arusha - Musoma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la afya. Afya yetu ya msingi inaanzia katika ngazi ya zahanati, lakini pia tunavyo vituo vya afya vingi sana katika nchi yetu. Pamoja na nia nzuri ya Wizara ya Afya kwamba watakuwa wanaleta sera kwamba kila Halmashauri iwe na hospitali ambayo inaweza ikawa na ngazi ya Hospitali ya Wilaya basi lazima pia waviangalie vituo vyetu vya afya. Kule Mlalo tunacho kituo kikubwa cha afya kinatoa huduma za upasuaji, lakini kinakosa miundombinu ya wodi za wagonjwa lakini pia miundombinu wezeshi kama ambulance kwa ajili ya kuwasafirisha hawa wagonjwa wanaofanyiwa operesheni kama ita-fail katika kituo kile cha afya.
Kwa hiyo, niiombe Wizara pamoja na kwamba safari hii wametenga takribani shilingi trilioni 1.9 ambayo ni sawa na asilimia 92 basi tujitahidi bajeti inayokuja mwakani angalau tufike asilimia 15 ili kufikia yale Maazimio ya Abuja ili tuweze kuhudumia wananchi wetu vile ambavyo inapaswa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza pia Wizara kwa kukufuta kodi kwenye vifaa vya walemavu. Mwalimu Nyerere aliwahi kusema ukitaka usawa wa binadamu ndugu zetu walemavu tuwaajiri. Kwa hiyo, niipongeze Wizara kwa kuliona hili, lakini tunaomba kwamba misaada hii waisimamie ili iende kwa wale ambao wanakusudiwa. Miundombinu hii isiishie tu kwenye wheelchair na vitu vingine vya kawaida, lakini ifike pia kwenye zile facilities kwa mfano wale ambao wanauoni hafifu vifaa vyao vyote viweze kupatikana kwa urahisi. Aidha, isingekuwa tu kuwaondolea kodi lakini pia Serikali ingeenda mbali zaidi hata kuweza kuwajengea uwezo wa kupata hivi vifaa bure kabisa kwa watu wale ambao wana ulemavu mahsusi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo nataka kulizungumzia ni suala zima la maji. Tumeona kwenye bajeti iliyopita maji yameelekezwa zaidi mjini. Tunaiomba Serikali ihakikishe kwamba pesa zilizotengwa kwa ajili ya miradi ya maji vijijini safari hii zote zinaenda.
Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Makamu wa Rais wakati wanapita kuomba kura walikuwa na kauli mbiu ya kumtua mama ndoo kichwani. Ninachoamini kwamba akina mama ambao wanabeba ndoo kichwani ni wale ambao wako vijijini, mijini maji mengi yanachotwa kwa mabomba tu nje hatua chache. Ili kumtua mama wa kijijini ndoo kichwani ni lazima tuhakikishe kwamba pesa zilizotengwa katika bajeti hii zinakwenda katika maeneo mahsusi na Wizara inasimamia miradi yote ili wananchi hao waweze kufaidika na huduma za jamii katika nchi yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho nimalizie kodi kwenye muamala wa simu. Hili suala nalo ni muhimu, naomba Waziri atakaposimama ku-wind up alitolee ufafanuzi maana wapo baadhi ya wanasiasa wanalipotosha huko nje kwa wananchi. Kwa hiyo, hapa inatakiwa lielezwe kwa ufasaha. Vilevile pia Wizara itumie nafasi hii kuwabana hawa wenye makampuni za simu kwa sababu wengi wanaofanya miamala ni wananchi wa kawaida na hata wale wanaofanya biashara hii ya uwakala pia ni wananchi wa kawaida ambao wanatumia mitaji yao wenyewe lakini gharama ambazo mashirika haya yanachukua ni kubwa zaidi kuliko wale mawakala wanachokipata. Unakuta wakala anapata pesa ndogo sana wakati mtaji ni wake, wafanyakazi ni wake, yeye ndiyo analipa kodi lakini makampuni haya yanachukua gawio kubwa zaidi kuliko hao mawakala ambao ndiyo wanaofanya kazi kubwa zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia katika Wizara hii muhimu kwa kukuza uchumi wa nchi yetu. Msitu wa Shagayu uliopo Wilaya ya Lushoto uliungua mwaka 2012 ambapo hekta 49 ziliungua hata hivyo mpaka sasa ni hekta 11 tu ambazo zimepandwa katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuungua kwa eneo la msitu huo lilisababishwa ardhi kutokuwa na vizuizi vya maji, hivyo mvua za mwaka 2015 zilisababisha maafa makubwa ya maporomoko na mafuriko katika maeneo yanayozunguka msitu huu. Mheshimiwa Waziri pamoja na eneo kubwa la msitu ambao unazungukwa na vijiji 15, lakini msitu una wafanyakazi wawili tu ilhali unazo nyumba za kutosha familia sita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo tunaomba Idara ya Misitu kupitia Wizara watuongezee watumishi wanne kufikia sita ili waweze kuhudumia vizuri eneo la msitu ikiwa ni pamoja na kuwapatia usafiri wa pikipiki kwani kwa sasa ipo pikipiki moja tu. Tunaomba ziongezwe pikipiki mbili zaidi ili ziweze kuleta tija katika kuhudumia msitu huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miundombinu inayozunguka maeneo ya msitu wa Shagayu sio rafiki, tunaomba Wizara kupitia Wakala wa Misitu ya Asili ili kuboresha miundmbinu hasa ya barabara ili isaidie kukabiliana na majanga hasa ya moto pale unapojitokeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mbuga ya Mkomazi iliyopo katika Mikoa ya Tanga na Kilimanjaro, lakini Mlanga (lango) la kuingilia hifadhini lipo katika Wilaya ya Same, hivyo kuwasumbua watalii wanaotembelea Wilaya ya Lushoto na vivutio vyake kulazimika kwenda mpaka Same.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Wizara kwa kushirikiana na Mamlaka ya Hifadhi za Taifa na hususani Hifadhi ya Mkomazi kutuwekea mlango wa kuingia hifadhini kupitia Wilaya ya Lushoto katika Kata ya Lunguza, Kijiji cha Kiringo ili kukuza na kuchochea shughuli za utalii katika eneo hili la Tarafa ya Umba ili kusaidia kupunguza umaskini na kuchochea maendeleo ya watu wa Lushoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uhifadhi na ujirani bado unasuasua katika Hifadhi ya Mkomazi, hivyo kuweka mazingira hafifu ya ushirikiano baina ya hifadhi yetu na wananchi wa maeneo husika. Tunaiomba Wizara ihakikishe ile asilimia saba ya mapato yatokanayo na makusanyo ya hifadhi husika basi yaelekezwe kwenye vijiji na jamii inayozunguka hifadhi ili kuchochea shughuli za maendeleo na kupunguza uhasama baina ya hifadhi na wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya ardhi baina ya hifadhi zetu bado ni jambo linalosumbua sana hasa katika Kijiji cha Kiringo ambapo mpaka upo jirani sana na makazi ya watu hivyo kuleta misigano isiyokuwa ya lazima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Operesheni Tokomeza katika Wilaya ya Lushoto umeacha ardhi ya watu wakiwa na athari za kimwili, kiafya na kiuchumi. Silaha ambazo zimechukuliwa toka kwa wananchi waliopo jirani na hifadhi lakini hazikuhusika katika shughuli haramu za ujangili zirejeshwe kwa wamiliki halali ili waweze kujilinda kwa usalama wao kama walivyoziomba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni matarajio yetu kuwa uhifadhi wa misitu na mbuga zetu utaenda sambamba na ustawi wa jamii yetu ya Kitanzania kwa ajili ya vizazi vya sasa na vijavyo.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, single customer territory imeanza utekelezaji wake mwaka 2014 Januari, kwa nchi za Kenya na Uganda na kwa Tanzania imeanza rasmi Julai, 2014. Changamoto mpaka sasa kwenye himaya hii ya forodha ya pamoja ni kwamba kati ya nchi zote tano za Afrika Mashariki ni Tanzania na Rwanda pekee ambazo zinatekeleza makubaliano haya kwa asilimia mia moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, Uganda na Kenya bado wanakusanya kwenye baadhi ya bidhaa tu, huku Burundi ikiwa haijawahi kutekeleza.
Mheshimiwa Naibu Spika, dhana hii ya SCT ni njema sana kama itakuwa inatekelezwa na nchi zote wanachama. Ndio maana nchi ya Congo DRC imeomba iingizwe katika utaratibu huo. Ni jukumu la Serikali kuhakikisha kuwa nchi zote zilizoridhia SCT zinatekeleza ili kudhibiti unyonyaji wa mapato kutoka kwa baadhi ya nchi ambazo hazitekelezi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Serikali yetu iwasiliane na Serikali ya Jamhuri ya Mozambique ili kupitia bandari ya Beira pia utaratibu huu uweze kutumika. Hii itasaidia kuwadhibiti wale wafanyabiashara wasiokuwa waaminifu.
Mheshimiwa Naibu Spika, faida za SCT; kudhibiti ukwepaji kodi kupitia mizigo ya transit, hapo awali kabla ya utaratibu huu mizigo mingine ilikuwa inashushwa ndani ya nchi yetu, hivyo kuwepo na ukwepaji kodi na kuikosesha Serikali mapato.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushindani hafifu wa kibiashara, kwa sababu wafanyabiashara hasa wakubwa walikuwa favored na utaratibu huo, kuliko wajasiriamali wadogo. Wasafirishaji wa mizigo kwenda Congo wamekuwa wakifanya trip nyingi zaidi baada ya utaratibu huu wa SCT kwa kuwa hakuna usumbufu, tofauti na ilivyokuwa huko nyuma; ilikuwa inawagharimu wasafirishaji zaidi ya miezi miwili hadi minne kusafirisha na ku-clear mizigo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo; ufufuaji wa zao la Mkonge katika Mikoa ya Tanga, Morogoro na baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Pwani, zao la mkonge limepanda thamani sana duniani na kati ya mashamba 56 yaliyopo nchini mashamba 37 yapo Mkoa wa Tanga na mengi yamekuwa mapori.
Mheshimiwa Naibu Spika, Bandari, Bandari ya Tanga ifufuliwe na kupanuliwa ili iende sambamba na ujenzi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Uganda–Ziwa Albert hadi katika Bandari ya Tanga. Hii itasaidia pia usafirishaji wa mizigo kutoka Tanga Tanzania hadi Uganda na nchi jirani ya Sudani Kusini.
Mheshimiwa Naibu Spika, Viwanda, Kiwanda cha Afritex kilichokuwa kina uwezo wa kuajiri wafanyakazi 2000, kimefungwa na kipo Mkoani Tanga kikitengeneza aina mbalimbali za bidhaa za nguo. Serikali inakosa mapato, lakini pia ajira inapungua kwa kiasi kikubwa. Ahsante.
Muswada wa Sheria ya Upatikanaji wa Habari wa Mwaka 2016
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Na mimi nashukuru kwa kupata nafasi hii ya kuchangia katika muswada huu. Niseme tu kwamba muswada huu nimeushiriki kwa maana umepita katika Kamati ya Katiba na Sheria ambayo nami nimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Muswada huu wa Sheria ya haki ya kupata taarifa, kuainisha wigo wa taarifa ambazo umma unayo haki ya kupewa, kukuza uwazi na uwajibikaji na wamiliki wa taarifa na kuweka masharti mengine yanayohusika nayo; niseme kwamba ni muswada ambao umekuja wakati muafaka kwa sababu sasa hivi tuna ugatuzi ambapo majukumu mengi yanafanyika katika Mabaraza yetu ya Halmashauri, kwa maana huko Waheshimiwa Madiwani, Wenyeviti wa Vijiji, Vitongoji na kadhalika ndio ambao wako karibu zaidi na wananchi na kuna taarifa ambazo wanapaswa wazipate.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda kwa Kiswahili sahihi tu ni kwamba hapa tunazungumzia haki ya kupata taarifa. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, tusichanganye; tusijipige chenga wenyewe; kuna suala la taarifa na suala la habari. Ninavyofahamu mimi ni kwamba hata habari inatengenezwa kupitia taarifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hapa tunazungumzia haki ya kupata taarifa na hasa hizi taarifa ambazo kimsingi zinatokana na maamuzi katika Idara za Serikali, Wizara za Serikali, Mashirika ya Umma lakini pia katika Ofizi za binafsi zile ambazo zina maslahi mapana ya umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme kwamba kuna maeneo ambayo nimeyaona yanahitaji yafanyiwe maboresho. Suala la kwanza ni suala zima la siku 30 za kupata taarifa. Tumezungumza na Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana, ameonyesha nia kwamba nia yao ni njema, lakini pamoja na nia yake njema hii tusichukulie zaidi kwa maana inazungumzwa na mtu na hizi Wizara unaweza ukakuta kesho akawekwa mtu mwingine ambaye hana dhamira hiyo kama yeye ambayo ametuaminisha, ni vizuri hizi siku zikatazamwa upya, kwa sababu jambo lenyewe hili siyo suala ambalo kwamba linaoneka ni geni. Ni jambo ambalo sasa hivi ukitazama kwenye website nyingi za Wizara na Idara za Serikali unaona tayari kuna taarifa ambazo zinapatikana. Kwa hiyo, inapotokea kwamba kuna taarifa mahsusi ambayo labda haiko kwenye website ya Wizara ama ya Idara, basi mwananchi angalau apunguziwe siku za kupata hizi taarifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kama tunakusudia kwamba taarifa hii aipate mwananchi yule wa kijijini, sasa inawezekana wakati huo ndiyo greda linapita, linatengeneza barabara na mwananchi huyu anataka ajiridhishe kwamba barabara hii inayotengenezwa inatengenezwa kwa kiwango gani? Atakapohitaji taarifa akaambiwa ni baada ya mwezi mmoja wakati greda limeshapita, ina maana dhana nzima ya kupata taarifa kwa wakati itakuwa haikuzingatiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme pamoja na kwamba sheria hii inakwenda kutengeneza kanuni, lakini basi hizi kanuni ziainishe ni taarifa zipi ambazo siyo lazima mwananchi aziombe? Ziwe tu tayari kwamba Halmashauri zetu zinapofanya maamuzi, zinapoazimia maamuzi fulani, basi ziwekwe kwenye mbao za matangazo, ziwekwe kwenye website, watu wawe tu wanaweza ku-access wakati wowote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, pia ni suala zima la gharama hizi ambapo tunapohitaji taarifa hizi lazima kutakuwa na gharama. Tumejaribu kuainisha kwamba zipo baadhi ya documents ambazo labda ni ya page mbili haina gharama kubwa, lakini inawezekana kuna wengine wanatafuta taarifa hizi kwa ajili ya kufanya tafiti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na wenzetu wa Shirika la SIKIKA ambao walitoa mfano kwamba pale TAMISEMI wakiwa wanahitaji taarifa yoyote ndani ya TAMISEMI wanaipata kwa muda usiozidi siku saba. Kuna taarifa ambazo wamezipata ndani ya siku moja; kuna taarifa ambazo wamezipata ndani ya siku mbili, lakini pia ziko taarifa ambazo zinapatikana kwa maximum ndani ya siku saba. Kwa hiyo, tumeona kwamba hili ni jambo zuri, lakini kwa kuwa wao taarifa hizi nyingi wanazichukua kwa ajili ya kwenda kufanya tafiti, basi ni vyema sana tukaangalia hizi siku 30 angalau Mheshimiwa Waziri pamoja na kanuni za kwenda kutengeneza lakini liangaliwe kwa jicho la upana zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala zima la uwazi na uwajibikaji. Kama tunavyoainisha kwenye suala zima la ugatuzi, maana yake ni kwamba tunaenda kuongeza uwazi na uwajibikaji kwenye Halmashauri zetu lakini kwenye taasisi zetu za umma. Kwa hiyo, hili ni jambo ambalo linapaswa tuliunge mkono na sina tatizo nalo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la muda wa kutoa taarifa kwa yule ambaye taarifa hizo hazipatikani. Kuna eneo ambalo linazungumzia kwamba mwomba taarifa akishamwandikia mtoa taarifa atamjibu ndani ya siku hizo kwamba taarifa hiyo inapatikana au ataipata mahali pengine. Siku hizi nazo bado zinaonekana ni nyingi, tungependa sana kwamba kama taarifa haziko kwa mmiliki wa taarifa aliyoombwa, basi afanye hima kwa haraka amtaarifu mhusika kwamba taarifa hizo anaweza akazipata katika eneo gani lingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo limekuwa na wasiwasi kwa wenzangu nami pia nina wasiwasi nalo ni suala zima la sheria hii kwamba inatokana na Ibara ya 18(d) ya Katiba ambayo inasema kila mtu anayo haki ya kupata taarifa. Sasa kuna maeneo ambayo ametumika kama raia, lakini tukasema kwamba pamoja na kwamba ni mapendekezo ya Kamati pia kwamba ionekane kila mtu anayo haki ya kupata taarifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kwa wenzetu wa nchi ambazo zimeendelea, hata hapa nilipo sasa hivi naweza nika-access information za Marekani na nikapata baadhi ya taarifa. Niseme tu kwamba napingana na wenzangu wanaozungumzia suala la kuweka wazi hizi sheria ambazo zimekatazwa hasa za Usalama wa Taifa, ni vyema tusiziweke taarifa hizi zikawa wazi; ziwe vilevile kwa mujibu wa sheria ile ziendelee kulindwa kwa sababu hatuwezi tukaliweka Taifa letu hadharani kwa kiasi hicho. Mambo ya usalama haya ni lazima tuyazingatie japo tunaamini kwamba yapo maeneo mengine kuna baadhi ya watumishi wanaweza wakatumia kama kichaka cha kuweza kuficha taarifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hili ni lazima wakati tunapambana na uanzishwaji wa sheria hii, lakini vilevie kubadilisha mitazamo na mind set za Watanzania, kwa sababu kuna watu ni wakiritimba tu wa kutoa taarifa hata kama taarifa hizo ni kutaka tu kujua kwamba idadi ya waathirika labda wa ugonjwa fulani katika eneo fulani ni wangapi, lakini bado mtu atakuzungusha pasipo sababu za msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa nataka tusichanganye haya mambo kwamba zipo baadhi ya Idara za Serikali wana ukiritimba tu wa kutoa taarifa, lakini pia ni lazima sana tulinde haki yetu hii ya Sheria za Usalama wa Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni eneo hili la taarifa za Jeshi letu la Polisi. Hapa ndipo ambapo napaona kidogo kuna tatizo japokuwa zipo sheria za uanzishwaji wa Jeshi la Polisi lakini tuangalie hii sheria itafanya kazi vipi kwenye zile taarifa ambazo zinatolewa na polisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo ambayo labda kumetokea ajali, kumetokea mapigano kati ya wahalifu na polisi, lakini unakuta kila polisi anayeulizwa, Afisa husika anasema mimi siyo mtoa taarifa wa Jeshi la Polisi. Kwa hiyo, kunakuwa na ukiritimba kwamba lazima habari zitoke Makao Makuu labda ya Jeshi la Polisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana ndiyo ilivyo kwenye kanuni zao, lakini nataka sasa hili tuliangalie kwa upana zaidi, kwa sababu sasa hivi kutokana na uwepo wa mitandao hii ya kijamii, tayari ni kwamba Jeshi linaposhindwa kutoa taarifa hizi kwa wakati, watu mmoja mmoja wanaanza kuzisambaza na baadaye zinaonekana sasa kama ni sababu za uchochezi ama ni sababu ambazo hazina msaada kama ambavyo zingetolewa kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, taarifa hizi pia katika baadhi ya Idara za Serikali, Idara ya Serikali unaikuta iko Wilayani ama Mkoani, lakini bado wanakwambia kwamba taarifa hizi zinapatikana Wizarani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunapozungumza dhana nzima ya ugatuzi ni lazima sasa tusigatue tu mambo ya utawala na fedha lakini pia na hizi taarifa, hao watu walioko huko chini, wamiliki wa taarifa kama ambavyo tumependekeza kwenye Kamati wawe wahakikishe kabisa kwamba kunakuwa na Maafisa wanaotoa taarifa wakati wote na pia kama ambavyo nimependekeza kwamba taarifa zile ambazo ni edible, ambazo zinahitajika tu kwa Umma, zitolewe kupitia hata kwenye website bila kuleta haja ya kuziomba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sitakuwa na mengi, yangu ni hayo machache. Ahsante sana, nakushukuru sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata fursa hii ya kuchangia katika hoja ambayo ipo katika Bunge lako Tukufu. Moja kwa moja ningependa kuanza na suala la himaya ya pamoja ya ushuru wa forodha (single customs territory). Hii single customs territoryilianza mwaka 2013 lakini utekelezaji wake katika nchi za Afrika Mashariki ulianza mwaka 2014, Kenya na Uganda walianza Januari lakini ilivyofika Julai Tanzania na Rwanda nazo zikaanza utekelezaji wake hadi hivi ninavyozungumza wenzetu wa Burundi bado hawajaanza kutekeleza hii dhana nzima ya single customs territory.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanini nasema haya? Nayasema haya kwa sababu hili ni eneo mojawapo ambalo sisi kama Tanzania inawezekana ikawa tumepigwa goli kwa sababu hii mizigo ambayo inakwenda Kongo sisi tunapo-charge hapa katika Tanzania halafu wengine hawafanyi hivyo ndio hii sasa ambayo wenzetu wanatumia mwanya kupitisha bandari nyingine hizo ili kukwepa hii single customs territory.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninaomba nitoe ushauri kwa Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana na Serikali kwa ujumla kwamba kwa kuwa hii single customs territory imeanza kwa nchi za Afrika Mashariki na nchi ya Kongo walivyoona kwamba ina manufaa wakaomba wao wenyewe kwamba bidhaa zinazokwenda katika nchi yao zitozwe kodi katika maeneo yetu. Basi naiomba Serikali sasa iweze kuwaandikia Kongo ikiwezekana pia wawaombe na Mozambique nao waingie katika huu utaratibu ili kwamba bandari zote ziwe fair. Lakini kama sisi tutaendelea kutekeleza wakati Mombasa hawatekelezi kwa asilimia 100 na kule Beira hawamo kabisa katika mpango huu na kule Walvis Bay kule Namibia pia hawamo katika mpango huu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili ni jambo la Serikali kwa kuwa limeamuliwa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki basi warudi kule wakahakikishe kwamba mambo haya yanatekelezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo lina faida ambayo faida yenyewe imejificha sana sio rahisi kuonekana kwa jicho la karibu. Faida namba moja ni kwamba kabla ya utaratibu huu haujaanzishwa mizigo mingi ya kwenda Kongo ilikuwa inakuwa dumped katika nchi yetu, mizigo ambayo inatakiwa kwenda transit haiendi inabaki katika soko la ndani, matokeo yake ni kwamba nchi inakosa uwezo wa kukusanya kodi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hiyo, pia wakati huo hata wasafirishaji waliokuwa wanapeleka mizigo Kongo unaweza ukakuta lori limefika Kongo, akaa zaidi ya mwezi mwenye mzigo hajalipa mwezi mwenye mzigo hajalipa kodi kwa hiyo anashindwa kushusha, unakuta unatumia muda mrefu nina ushahidi wa wazi kabisa mimi ni-declare interest nilikuwa ni mdau katika eneo hili, yapo malori ambayo yanaweza yakafanya trip mbili kwa mwaka huko nyuma, lakini baada ya hii single customs territory kuanza kila mtu anaondoka hapa na mzigo ambao umelipiwa kodi anashusha kwa wakati na anarudi na tumekuwa tunatengeneza mpaka trip nane kwa mwaka. Kwa hiyo, ni jambo zuri lakini lazima lifanyiwe utafiti vizuri tuhakikishe kwamba utekelezaji wake usiwe wa nchi moja bali uwe wa Jumuiya nzima ya Afrika Mashariki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo pia nizungumzie suala zima la mpango pamoja na dhana nzima ya kilimo, kwamba ni kweli kwamba huoni connection ya moja kwa moja kati ya kilimo na hii dhana nzima ya uanzishwaji wa viwanda. Kwa hiyo, ningependa kuwashauri Serikali kwamba sasa hebu ije na comprehensive information ya kuweza kufanya integration kati ya kilimo kitaungana vipi kwenda kwenye viwanda. Hivi viwanda ambavyo mjomba wangu Mheshimiwa Mwijage anavinadi lazima tupate tafsiri ni viwanda vya namna gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ninavyofahamu mimi kwa Tanzania yetu kwa sababu sisi ni wakulima basi viwanda hivi vinatakiwa viwe vingi vya maeneo yanayoendana na mazao ya kilimo ili tutengeneze wigo mpana wa kuwasaidia wananchi wetu. Hatutarajii kuwa na kiwanda pekee kitakacho ajiri watu 500 lakini tunataka tuwe na kiwanda ambacho kitaajiri watu 500 kwenye kiwanda wafanye kazi za kiwanda, lakini hawa outgrowers huku nje nao waweze kuwa supported, watu wawe busy kwenye mashamba na wawe na masoko ya uhakika kupitia hivi viwanda ambavyo tunakusudia kuvianzisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika hili ni lazima hata tafiti za kilimo zifanyike upya. Sasa hivi wakulima wetu wengi wanafanya kazi hizi za kilimo kwa mazoea, tunazungumzia tatizo kubwa la mabadiliko ya tabia nchi duniani. Hali ya hewa imebadilika, tunaona hata mvua zinachelewa sio kwa wakati kama ilivyokuwa zamani. Kwa hiyo, hii yote inategemea pia na watu wa tafiti nao waende mbali zaidi watafiti kwa hali ya hewa iliyopo sasa ni mazao gani tuyapande yanayoendana na hali ya hewa husika? Kwa hiyo, niishauri Serikali kwamba eneo hilo ni lazima walifanyie mkazo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo mazao ya biashara, mkonge, kule kwetu Mkoa wa Tanga tunalima sana mkonge na takribani mashamba 56 yaliyopo nchini, mashamba 36 yapo Mkoa wa Tanga. Kwa hiyo, naomba eneo hili pia lipewe kipaumbele ili kuweza kukuza uchumi wa Mkoa wa Tanga na nchi kwa ujumla. Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia jambo ambalo liko mbele ya Bunge letu Tukufu. Nitaanza na suala zima la kuchangia katika Kamati ya Katiba na Sheria ambayo na mimi ni Mjumbe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati yetu haikufanya kazi vizuri kwa sababu bajeti ilikuwa ni finyu. Kuna maeneo ambayo tulipaswa kwenda kufanya ili tuweze kuona uzoefu na pesa ambazo zimekwenda kwenye miradi lakini tumeshindwa kufanya hivyo. Jambo la kusikitisha zaidi ni kwamba, kama utakumbuka Bunge letu Tukufu liliridhia kwamba na sisi tutoe mchango kwa wenzetu wale waliopatwa na tetemeko kule Kagera lakini pia Kamati yetu ambayo inaitazama Ofisi ya Waziri Mkuu tulishindwa kwenda hata kuwaona wenzetu wale waliokumbwa na ile kadhia. Kwa hiyo, nitarajie kwamba jambo hili tuliangalie kwa kina katika bajeti zijazo, Kamati hizi ziweze kupewa uwezeshaji wa kutosha ili zifanye kazi yake kamili ya kuisimamia Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika katika Wizara ya Sheria na Katiba, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora; Tume hii haikutengewa fedha kabisa ya kufanya kazi, zaidi ya mishahara na OC hakuna kingine ambacho kimewekwa katika Tume hii. Sasa tutakubaliana kwamba sasa hivi kwa kadri utandawazi unavyoongezeka na kadri ambavyo hata shughuli za kiuchumi zinazidi kupanuka, uwekezaji unaongezeka katika nchi yetu, basi pia matukio ya uvunjaji wa haki za binadamu nao unaongezeka. Kwa hiyo, tulitarajia kwamba, Tume hii iongezewe nguvu ya kifedha ili iweze kufanya kazi. Matukio yale yalilyokuwa yanatokea mwanzo siyo yanayotokea sasa. Sasa hivi teknolojia jinsi inavyokua na matukio nayo ya unyanyasaji na uvunjifu wa haki za binadamu nayo ndivyo yanavyozidi kuongezeka. Kwa hiyo, natarajia kwamba ofisi hii itaongezewe uwezo ili iweze ikafanya kazi yake vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tulipotembelea Ofisi ya Waziri wa Sheria, tulikutana na changamoto kwamba hata jengo la ofisi liko katika mazingira ambayo siyo mazuri sana. Mheshimiwa Mshua ambaye niko naye hapa karibu aliweza hata kupoteza fahamu tukiwa ndani ya ofisi ya Waziri wa Sheria na Katiba, kwa maana kwamba ofisi haikuwa hata na mazingira mazuri kiasi kwamba hata watumishi pale sijui hata afya zao zitakuwa katika hali gani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo niendelee katika Ofisi ya Rais, Utumishi pamoja na Serikali za Mitaa, kwamba tuna tatizo katika Halmashauri ya Lushoto. Pesa ambazo tunazipata kutokana na own source tunazipeleka kulipa Watumishi wa Serikali ambao bado hawajapata vibali vya ajira kutoka Serikali Kuu. Takribani shilingi milioni 28 zinatumika kulipa Watumishi wa Halmashauri. Kwa hiyo hii inachangia kwamba pesa hizi ambazo zilipaswa kwenda kwenye asilimia tano ya akinamama na asilimia tano ya vijana na pia asilimia 20 kwa ajili ya kuwawezesha Wenyeviti wa Serikali za Vijiji kupata posho zao zinashindwa kwenda katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo limekuwa ni tatizo, Wenyeviti wa Vijiji katika Halmashauri yangu wana miaka zaidi ya 10 hawajawahi kupata fedha, hili ni tatizo kubwa linawafanya sasa wanashindwa hata kutekeleza wajibu wao. Kwa hiyo, niiombe Wizara hii ya Utumishi ihakikishe kwamba inatupokea mzigo wa watumishi hawa ili angalau pesa hii iende kwenye maeneo ambayo yanahusika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala zima la watumishi pia linaenda katika Idara ya Afya. Tumejenga zahanati 10 ambazo ziko tayari lakini hazina watumishi. Tumeiunga kauli mbiu ya Serikali ya Awamu hii ya Tano ya kujenga zahanati kwa kila kijiji, lakini sasa zahanati zile zinaanza kuchakaa bila kutumika. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali ihakikishe kwamba hawa watumishi wa afya wanaajiriwa kwa haraka ili waende kuwatumikia wananchi hawa wa Halmashauri ya Lushoto. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la ufungaji wa mazao kwa mtindo wa Lumbesa. Namwomba ndugu yangu Mheshimiwa Simbachawene kwamba hili tangazo bado halijaenea vizuri huku katika Halmashauri. Huku kwenye Halmashauri bado wanasubiri hawa wanaofunga Lumbesa kwenye yale mageti ya kukusanya ushuru, nadhani kwamba ingependeza zaidi kwa sababu hawa wanaofunga haya mazao wanafunga kutoka kwenye magulio na kwenye vijiji basi hii kazi wapewe Watendaji wa Vijiji wakishirikiana na Wenyeviti, kule kule wanakofungasha haya mazao ndiko ambako waanze kuwabana ili angalau hili tatizo liweze kuondoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumza tatizo hili tunamaanisha kwamba akinamama ndiyo wanaoathirika sana kwa sababu ndiyo wazalishaji wakubwa katika halmashauri zetu. Utakuta wameshavuna viazi, wameshavuna nyanya na karoti halafu anakuja mwanaume anafunga kwa kadri anavyoweza, gunia moja linafungwa mpaka debe 10. Kwa hiyo, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri kwamba, ule waraka ambao ameutoa basi aendelee kuukazia ashuke mpaka katika ngazi za vijiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la TASAF; TASAF nayo ina changamoto kwa sababu vile vigezo ambavyo vimeainishwa vya kaya maskini inawezekana katika zile hatua za awali, wananchi hawakujitokeza vizuri kwenye mikutano, kwa hiyo wakajiangalia walioko kwenye mikutano maskini ni nani wakaandika wale walioko kwenye mikutano, lakini baada ya uhakiki, inaonekana kabisa kwamba maskini halisi waliachwa majumbani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naiomba Serikali pamoja na nia njema hii ya kuhakiki, naomba niendelee kwa sababu hata mimi katika pitapita zangu kuna mmoja ambaye alikuwa ni mnufaika wa TASAF yeye alikuwa siku za TASAF ndiyo ambazo ananunua bia na tulivyombaini tukatoa taarifa na akaondolewa kwenye ule mpango. Kwa hiyo, tuendelee kufanya utafiti ili watu hawa ambao hawastahiki wasiwepo katika hilo eneo la kupata hizi fedha za uwezeshaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo niongelee kuhusu asilimia tano kwa vijana na akinamama kwamba Halmashauri nyingi zinashindwa kutenga hii pesa katika Halmashauri zao na sababu ziko wazi. Huko nyuma, Serikali ya Awamu ya Nne ilikuwa imetoa matamko mengi ya kujenga haya majengo ya sekondari ambayo hakukuwa na mafungu, kwa hiyo Wakurugenzi nao kwa kuwa wanabanwa wakawa wanatafuta mahali gani wataweza kupata hizi pesa. Kwa hiyo, niombe kwamba sasa hivi hizi pesa hebu tuzitengenezee utaratibu mzuri Halmashauri wakati zinakaguliwa hasa na Kamati ile ya Serikali za Mitaa, tuangalie ni asilimia ngapi wametoa kwa ajili ya hawa vijana, ni asilimia ngapi zimetoka kwa ajili ya akinamama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama itapendeza kutokana na hili lindi la watu wenye ulemavu kuongezeka kwenda mijini, nashauri Bunge hili kwamba tufike mahali kwa nini tusipunguze japo asilimia moja katika hizi, tukatoa asilimia moja kwa vijana na asilimia moja kwa akinamama ili tukatengeneze asilimia mbili zikaenda kwa wenzetu walemavu kwa sababu huko kwenye Halmashauri ikiwa tunaweza kuwatambua itakuwa ni eneo zuri pia la kupunguza wao wasiende mijini. Kwa hiyo, kama tutaona linafaa tunaweza tukaliingiza, hizo asilimia angalau na wenzetu hawa wenye ulemavu waweze kupata asilimia hii kutoka katika mapato ya halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho nikazie kwenye asilimia 20 ambayo inapaswa kwenda kwa Wenyeviti wa Vijiji na Serikali za Mitaa. Hizi pesa Mheshimiwa Waziri Simbachawene haziendi. Halmashauri hazitengi hizi pesa, Wenyeviti hawapati posho na wakati mwingine inakwamisha hata tunapohamasisha shughuli za maendeleo, wanakosa nguvu ya ushawishi. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri akazie hili kwamba Halmashauri ziwatengee pesa hizi za posho Wenyeviti wa Serikali za Mitaa na Wenyeviti wa Vijiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nami naomba nichangie kwenye Kamati hii ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama. Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza na suala zima la tozo ile ya fire. Tunapolipia road licence kuna shilingi karibia Sh.30,000 mpaka Sh.40,000 zinakwenda kwenye huduma za zimamoto kwa maana ya fire. Sasa nataka kujua kupitia Kamati na Wizara kwamba pesa hizi zinatumika katika eneo gani? Kwa sababu huduma za zimamoto katika miji mikubwa kama Dar es Salaam, Mwanza, Arusha, Tanga na Mbeya bado tunaona wanatumia magari ambayo hayana uwezo wa kutoa huduma hii katika maghorofa marefu zaidi. Mheshimiwa Mwenyekiti, ni matarajio yangu kwamba kwa sababu pesa hizi zinakusanywa kupitia TRA na zina uhakika wa kupatikana sasa zingekwenda kuboresha huduma ya hivi vyombo vya kuzimia moto katika manispaa zote ili angalau tuwe na vyombo vya zimamoto vya kisasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo kwa Jiji la Dar es Salaam ambalo sasa hivi tuna huduma ya mabasi yaendayo kasi, ni kweli tumeingia katika dunia ya ushindani wa teknolojia lakini gari hizi zinazobeba magari yaliyoharibika kwa maana ya breakdown bado wanaendelea kutumia land rover ambazo mara nyingi zinasababisha kuharibu zaidi hata hayo magari. Kwa sababu siyo magari yote yanayovutwa na breakdown ni mabovu, mengine labda wame-pack katika maeneo ambayo sio sahihi, kwa hiyo wakati wanayavuta haya magari wanasababisha uharibifu kwa magari yanayovutwa. Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Mambo ya Ndani kwamba yeye ni kijana wa kisasa hebu alete huu usasa katika hizi breakdown tupate ambazo zinaendana na wakati tuliokuwa nao. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nizungumzie suala zima la ulinzi na usalama hasa katika Mkoa wetu wa Tanga ambapo tulikumbwa na tukio moja ambalo lina harufu ya ugaidi. Mwezi wa Nane na wa Tisa yalitokea mapigano, watu wenye silaha walivamia baadhi ya vijiji katika Jimbo la Mlalo na Lushoto wakafikia hatua wakachoma bweni la Chuo cha SEKOMU. Kwa hiyo, ni rai yangu kwamba kwa kuwa Mkoa wa Tanga uko pembezoni mwa nchi jirani ya Kenya na tunajua kabisa kwa kule upande wa Kenya kuna tishio la Al-shabaab, basi nataraji kwamba zile harufu lazima zitakuwa zinapenya katika maeneo yetu. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia wapo askari hodari ambao wameweza kupambana katika tukio hili, kuna Inspector Joram ambaye mara ya mwisho alifanikiwa kukamata magaidi wawili wa Kisomali katika hilo kundi na hawa ndiyo waliokwenda kuonesha silaha zaidi ya tisa zilizokuwa zimefichwa kwenye kaburi na wakasaidia angalau kuufuatilia ule mtandao. Nitoe rai kwa Waziri mwenye dhamana awaone hawa vijana ambao wanafanya kazi nzuri waweze kupongezwa kwa sababu kazi waliyofanya ni kazi ya kishujaa na kizalendo. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kwa upande wa magereza tunalo gereza kongwe sana linaitwa Gereza la Kilimo la Mngalo, ni miongoni mwa magereza ya mwanzo kabisa yanayojishughulisha na kilimo. Hata hivyo, gereza hili linatumika chini ya kiwango kwa sababu lina uwezo wa kubeba wafungwa 100 lakini wapo 38. Niombe kule kwenye msongamano ikiwemo Rorya, Tarime na kwingineko basi unaweza ukawasogeza huku Mlalo waweze kutusaidia katika shughuli za kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia katika Wizara hii hasa eneo la ubora wa zana za ufundishaji hasa vitabu vya kiada. Tangu Serikali ilipovunja Bodi ya EMAC uhakika wa vitabu umekuwa dhaifu sana na kusababisha upotoshaji mkubwa kwenye taaluma, hivyo kuchochea Taifa kudondokea katika umbumbumbu, ujinga na kukosa maarifa kwa watoto wetu. Vitabu vilivyopo sasa ni ushahidi wa dhahiri kuwa uwepo wa EMAC usingeweza kupitisha makosa haya. Pia dhamira ya kuirejesha EMAC iendane na suala zima la kuihusisha sekta binafsi ifanye kazi hiyo na Serikali ibaki kuwa mthibitishaji ili hata makosa kama haya yakijitokeza yasiiathiri moja kwa moja Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Serikali ya Awamu ya Tano ni kukuza uwekezaji katika viwanda. Serikali inapoamua kuchapa vitabu yenyewe sio lengo baya, lakini inakinzana na sera ya viwanda. Aidha, uwepo wa sekta binafsi katika tasnia ya uchapishaji itasaidia Serikali kuyaona mambo kwa jicho la mbali na jicho pana zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niweke ushahidi wa vitabu vifuatavyo kuonyesha makosa ya dhahiri na ya wazi katika uchapishaji kuonyesha udhaifu mkubwa wa Taasisi ya Elimu kusimamia tasnia hii ya ukuzaji maarifa na utoaji elimu kwa vijana wetu.

(i) English For Secondary Schools, Form Four – ISBN 978- 9976-61-460-2

(ii) Geography for Secondary Schools, Form Three - TIE of 2016 –ISBN 978-9976-61-479-4

(iii) I learn English Language, Standard Three – ISBN 978- 996-61-545-6. (Vipo ikiwa ni ushahidi wa dhahiri).

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yote yenye makosa yameainishwa na kuwekewe alama maalum kwa (highlighter).

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia mwelekeo wa bajeti kwa Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianzie alipoishia Mheshimiwa Mhagama kwenye suala zima la kilimo. Naanzia hapo kwa sababu huyu ni pacha mwenzangu naye anaendesha kilimo cha tangawizi kama ambavyo mama yetu Mheshimiwa Anne Kilango amesema sasa ni zamu ya
tangawizi. Napenda kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba kule Mlalo, Kata ya Mbaramo, Lunguza, Mnazi na lakini kule katika Jimbo la Madaba na Jimbo la Same Mashariki na Same Magharibi kule ndiko tangawizi inalimwa kwa kiasi kikubwa. Tena sisi tunalima ile tangawizi ambayo ni kilimo hai, tunatumia mbolea ya samadi ambayo inakubalika hata kimataifa. Kwa hiyo, kwa kuungana pamoja na mama yetu Mheshimiwa Anne Kilango naamini jambo hili litapiga hatua kubwa zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa hatuwezi tukawa na kilimo endelevu kama hatutawekeza kwenye kilimo cha umwagiliaji. Kwa mujibu wa takwimu zilizopo ni kwamba ni asilimia moja tu ya ardhi yote ya Tanzania ambayo ni kilimo cha umwagiliaji. Ina maana Serikali inapaswa kuja na mikakati madhubuti kuhakikisha kwamba sasa kilimo chetu kisitegemee mvua. Kutokana na mabadiliko ya tabia nchi mvua zetu zimekuwa sio za uhakika tena. Kwa hiyo, ni wajibu wa Serikali kuhakikisha kwamba tunawekeza miundombinu ya mabwawa katika maeneo mbalimbali ya Halmashauri zetu ili kilimo hiki kiende kutoa ajira iwasaidie Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo wakati mwingine namshangaa Waziri wa Viwanda na Biashara kwa sababu viwanda anavyozungumza bado haviendi kutatua tatizo kubwa la ajira. Tunahitaji tupate viwanda ambavyo ni shirikishi, viwanda ambavyo vitasaidia kunyanyua soko la bidhaa za mazao. Tukiwa na viwanda vya vigae na malighafi hizi za ujenzi pekee bado wananchi hawa hawatakuwa na uwezo wa kununua hivyo vitu lakini bado hatutatatua tatizo la ajira. Kilimo pekee… (Makofi)
TAARIFA...
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hiyo ni nzuri lakini mimi sikuwa nazungumzia kiwanda kimoja specific, nilikuwa nazungumzia kwa maana ya nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ninavyozungumza pale Tanga pana kiwanda kinaitwa AFRITEX kilikuwa kinatengeneza nguo, ni mwaka wa pili sasa kimefungwa.
Mheshimiwa Waziri kila anaposimama anazungumzia viwanda vipya, hivi vya zamani vinavyokufa anavisimamia kwa namna gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia Kiwanda cha Nguo tunamaanisha kwamba wakulima wa pamba ndiyo watakaoweza kulisha pamoja na kupata soko kupitia viwanda hivi. Kiwanda cha AFRITEX pale Tanga kilikuwa kimeajiri watu zaidi ya 2,000 sasa hivi watu wale hawana ajira. Kwa hiyo, lengo langu ni kusema kwamba, pamoja na ajira za viwandani lakini pia ajira hizi zitokane na mazao yanayozalishwa na wananchi katika maeneo mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia Kiwanda cha Rhino Cement palepale Tanga kina tatizo la kupata malighafi. Tatizo lile ambalo alikuwa anakumbana nalo Dangote, Tanga Rhino Cement pia wana shida hiyohiyo. Malighafi wanayopata kutoka kwenye makaa ya mawe kule haitoshi. Uwezo wa kiwanda ni mahitaji ya malighafi tani 20,000 kwa mwezi lakini hawana uwezo wa kupata tani hizo wanaendesha kiwanda mara moja kwa wiki na kiwanda kile wakisimamisha uzalishaji kwa siku moja ina maana ajira zaidi ya watu 700 zitatetereka. Kwa hiyo, pamoja na hiyo nia nzuri lakini tunaomba kwamba viwanda vilivyopo pia viweze kuimarishwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kiwanda cha Chai Mponde, ni mwaka wa tano sasa hakifanyi kazi kiko kule Bumbuli. Kwa taarifa yako Jimbo la Bumbuli lina kata 18, kata 15 zote wanalima chai lakini ni mwaka wa tano sasa kiwanda kimefungwa, wananchi hawana shughuli zozote za uzalishaji kule. Maana yake ni kwamba hata Halmashauri sasa haiwezi kupata mapato kwa sababu ndani ya Halmashauri yenye kata 15 zinazolima chai, leo chai ile haina soko kwa sababu kiwanda kimefungwa. Mheshimiwa Mwijage anafahamu, Ofisi ya Waziri Mkuu hili wanalifahamu, kwa sababu PPF na NSSF wamekwenda kule lakini mpaka sasa hivi hakuna matumaini. Mheshimiwa Mwijage, sisi ni wajomba zako kule, tunakuomba utunusuru katika hili, Kiwanda cha Chai Mponde kifunguliwe ili wananchi wapate ajira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni Kiwanda cha Sabuni cha Foma pale Tanga. Kiwanda hiki kimenunuliwa na mwekezaji Haruna Zakaria lakini amekifunga, kimepoteza ajira zisizopungua watu 1,000. Tunaomba Serikali ikae na mwekezaji huyu kujua kwa nini amekinunua kiwanda na amekifunga, kwa sababu mitambo ipo pamoja na nyenzo nyingine zote zipo pale lakini amefunga. Sasa inawezekana wakati mwingine ni mambo haya ya kodi lakini ni vizuri sasa Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana akaenda kukutana na watu hawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niongelee suala la miundombinu ya barabara katika Mkoa wetu wa Tanga. Mkoa wa Tanga, Wilaya za Pangani na Handeni ni sehemu ambayo Mbuga ya Saadani pia inapatikana, siyo kwamba Saadani inapatikana kwa Wilaya ya Bagamoyo pekee. Ili tuweze kuimarisha utalii katika Mkoa wa Tanga, ambapo pia kuna Mbuga ya Hifadhi ya Mkomazi iliyopo katika Wilaya za Kilindi na Lushoto kwa upande wa Tanga, ni lazima sasa ile barabara ya kutoka Pwani - Pangani - Tanga iunganishwe na barabara ya kwenda Maramba – Bombomtoni – Mlalo - Same Mashariki iweze kunyanyuliwa. Hii barabara iko chini ya Wakala wa Barabara wa Mkoa, tunaomba sasa ianze kufikiriwa kuingizwa katika mpango wa kuwekewa lami. Sambamba na hilo, barabara ya kutoka Lushoto - Mlalo – Mnazi - Same kule Ndungu kwa mama yangu Mheshimiwa Anne Kilango pia lazima na yenyewe ifikiriwe kwanza kuwekwa lami. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nayazungumza haya kwa sababu uzalishaji mkubwa wa mazao ya mbogamboga na matunda katika Wilaya ya Lushoto unategemea sana barabara. Inawezekana kabisa kwamba kama kutanyesha mvua barabara ikasumbua ndani ya siku moja unaweza
ukamtia mtu hasara kubwa sana kwa sababu mazao haya yanaharibika kwa haraka. Kwa hiyo, mpango pekee ni kuhakikisha kwamba barabara hii inawekewa lami ili iweze kuwa na uhakika wa kufikisha mazao ya wananchi masokoni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niongelee suala la MIVAF. Tumetembelea miradi mbalimbali iliyoko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu kule Pemba na Unguja. Nishukuru kwamba MIVAF ni mradi ambao umesaidia sana lakini unakwisha mwaka huu mwezi Desemba. Niiombe Serikali, kuna tetesi kwamba andiko la miradi hii lipo kwenye Ofisi ya Wizara ya Fedha, tunaomba sasa wasisite waweze kuhakikisha kwamba wanasaini hii mikataba ili angalau tuweze kupata na MIVAF II. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kule Jimboni Mlalo, tulipata mradi mmoja wa soko kupitia MIVAF lakini nasikitika kusema kwamba soko lile ni dogo sana. Sisi uzalishaji wetu wa viazi, Mheshimiwa Mhagama ni mkubwa sana, tunazungumzia takribani fuso 40 kwa kila wiki zinaingia Dar es Salaam. Bila Lushoto Dar es Salaam chipsi zitakuwa ni adimu sana. Kwa hiyo, tunaomba pamoja na mambo mengine lakini soko lile pale kwenye Kata ya Malindi ambalo limejengwa kwa fedha za MIVAF liongezewe uwezo liwe kubwa zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyoko mbele ya Bunge lako Tukufu. Nami nianze kushukuru na kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Harrison Mwakyembe pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri ambayo ameleta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme kwamba Wizara hii pamoja na ufinyu wa bajeti, lakini ni Wizara ambayo inaweza ikajitengenezea fedha katika maeneo mbalimbali. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mwakyembe anao wajibu wa kuhakikisha kwamba anakuwa celebrity katika hii Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na Shirika la Utangazaji la Taifa TBC. Bajeti iliyopita TBC kupitia Wizara walituahidi kwamba Halmashauri 81 ambazo TBC ilikuwa haisikiki kwamba wanatafuta fedha na watahakisha kwamba katika bajeti ya mwaka huu maeneo hayo yatakuwa yamefikiwa; nasikitika kwamba mpaka sasa TBC haisikiki katika maeneo ya mbali hasa ya pembezoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimejipa kazi ya kufanya utafiti, ukiondoa kule Mlalo ambako tunapakana na nchi jirani ya Kenya, lakini kule Rombo kwa Mheshimiwa Selasini pia haipatikani. Juzi nilikuwa Peramiho kwa Mheshimiwa Mhagama, nako huko wanapata redio za Msumbiji. Huko Nkasi kwa Mheshimiwa Keissy anapata redio za Kongo; ukienda Kakonko Kigoma, wanapata redio za Burundi. Sasa hii ni hatari sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposema dhima na dira ya Wizara hii ni pamoja na kuwa na Taifa linalohabarishwa vizuri linaloshamirika na kiutamaduni lenye kazi bora za sanaa na lenye umahiri mkubwa katika michezo ifikapo 2025. Bila kuwa na chombo cha habari cha Taifa ambacho kinafikia hayo maeneo, hii itakuwa ni ndoto. Kwa hiyo, naomba sana Wizara ihakikishe kwamba TBC inafanya kazi kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mlata hapa alikuwa anaelezea namna ambavyo Clouds FM wameanza ambayo sasa hivi ni Clouds Media. Walianza kwenye chumba kimoja, lakini sasa hivi Clouds ipo nchi nzima, inasikika kwa mawimbi haya ya FM. Tatizo la TBC ni nini? Kama tatizo ni hii teknolojia mpya kwa nini tusirudi kwenye teknolojia ya zamani? Maana wakati ule wakati wa short wave, medium wave na AM ilikuwa inapatikana nchi nzima. Hawa wasanii akina Mzee Jangala, Majuto na wengineo wote tulikuwa tunawasikiliza kwenye vipindi, hatuwaoni lakini tuna-enjoy. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tunaona kabisa huu ndiyo utamaduni wa Kitanzania; walikuwa na vipindi vizuri vya kuelimisha wakati wa Kampeni za Malaria, Kampeni za Chaguzi na kampeni mbalimbali za nchi hii. TBC sasa hivi nao wanaigiza kwenye redio hizi za kizazi kipya. Nataka nitoe tahadhari kwamba tusipokuwa makini, hata Millad Ayo ambaye ameanza juzi juzi hapa, anaweza akaja akaizidi TBC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala zima la michezo. Mheshimiwa Waziri ameeleza michezo kwa mapana, lakini nasikitika kwamba bado michezo inaonekana kwamba ni mpaka wadau washiriki. Hakuna jitihada Mahususi za Wizara yenyewe kutenga fedha kwa ajili ya kwenda kuhuisha michezo kwenye mashule, vyuo na hata huko mitaani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika sana kuona kwamba wakati wa Mwalimu Nyerere vyanzo vyetu vya bajeti vilikuwa ni vichache sana, tena tulikuwa tunategemea zaidi mazao ya kilimo, yeye aliwezaje? Wale Marijendali wote uliowataja ni wa wakati wa Mwalimu. Inashindikana vipi sasa hivi wakati michezo hii imekuwa ni kama biashara? Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, aanze kuwatambua wadau lakini pia lazima Serikali na yenyewe iweke bajeti mahususi kwa ajili ya kuhuisha michezo mashuleni, vyuoni na katika maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili, naomba nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Naibu Spika Tulia Ackson, yeye ameanzisha mashindano kule Mkoani Mbeya pamoja, Wilayani Kyela. Kwanza alianza na utamaduni na hili ndiyo eneo ambalo lipo katika Wizara ya Mheshimiwa Waziri. Pia kuna mashindano, anashindanisha ngoma za asili za makabila mbalimbali yaliyopo ukanda ule wa Mbeya. Mwaka huu kuna mpango wa kufanya mashindano haya yawe ya Kitaifa, tuone ngoma kutoka Pemba, kutoka Tanga na pengine popote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wadau kama hawa ni vizuri sana tukawaunga mkono ili angalau Watanzania hawa wa kizazi kipya ambao wanaanza kusahau mila na desturi zao waweze kujua kwamba nchi hii ina utamaduni na ina desturi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, mwaka huu pia kulikuwepo na mashindano ya Tulia Marathon,

yamefanyika katika Jiji la Mbeya. Haya ni mashindano ambayo nayo yanapaswa kuungwa mkono. Kwa sababu sasa hivi Marathon pekee tunayoitumia hapa Tanzania inayotambulika duniani ni hii ya Kilimanjaro Marathon. Kilimanjaro Marathon tayari imeshaanza kuzidiwa, sasa hivi washiriki wamekuwa ni wengi sana kiasi kwamba sasa wakati mwingine wanakosa nafasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuitumie fursa hii. Pamoja na jitihada nzuri pia za kutangaza Utalii wa Kusini, tunayo Mbuga yetu ile ya Kitulo, tunayo Ruaha, lakini hizi Mbuga hazijatangazwa vizuri. Kwa kutumia michezo hasa kutumia hii Tulia Trust tunaweza tukazitangaza vizuri kupitia Marathon, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, Wizara yake iweze kukaa na Mdau huyu kuona hii Marathon inaweza ikatambulika Kimataifa ili tupate washiriki mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala zima la michezo hasa mpira wa miguu. Mpira wa miguu sisi bado tumekuwa ni washindani wa kubahatisha. Hawa vijana wa Serengeti Boys ambao tunawapongeza sasa, huwezi ukaona successful plan ambayo inaandaa wengine. Inatokea tu kwamba ni bahati, vipaji vimekusanywa kwa wakati mmoja hasa kupitia wenzetu hawa wa Airtel Rising Star. Kwa hiyo, naomba kwamba lazima tuweke mkakati ambao utasaidia tuanze kuandaa vijana wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na kuandaa vijana wengine, tuandae sasa hii ndio iwe dira yetu ya Timu ya Taifa inayokuja. Hawa vijana tutakapomaliza mashindano haya na tukawaacha wakaingia kwenye vilabu hivi vya Kitanzania ambavyo tunajua namna ambavyo wanawalea wachezaji, tutawaharibu. Kwa hiyo, nitoe rai kwa Mheshimiwa Waziri kwa kushirikiana na TFF tuhakikishe kwamba vijana hawa tunawatunza vizuri, tutafute Mawakala wazuri wa Kimataifa, vijana hawa waweze kupata exposure ya kwenda kucheza soka nje ya nchi ili baadaye waweze kuja kusaidia Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, uendeshaji wa mpira wa miguu bado una wasiwasi mwingi. Baada ya kuondoka Rais aliyepita, Leonard Chila Tenga sasa hivi TFF pameyumba sana. Maamuzi mengi yanafanyika kwa upendeleo, kwa hila; ni hivi juzi tu hapa timu ya Simba imenyang’anywa points zake tatu nzuri kabisa. Sasa sheria ziko wazi kwamba mchezaji akiwa na kadi za njano zaidi ya tatu, haruhusiwi kucheza mchezo unaofuata. Matokeo yake yametoka maamuzi mengine bila kugusia kwamba: Je, kadi ilikuwepo ama haikuwepo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri, tuwaangalie TFF kwa jicho la karibu hasa ukizingatiwa kwamba FIFA ya wakati huu inaruhusu Serikali kuanza kuingilia kuangalia maendeleo katika nyanja hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, Mheshimiwa Waziri amezungumza hapa kwamba timu ya Everton inakuja kucheza na miongoni mwa timu moja ya Tanzania. Nataka niseme wazi kwamba Simba Sport Club ndiyo timu pekee inayoweza ikatoa uwakilishi mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kuishindanisha Simba na Timu ambayo imefungwa na Mbao FC.

Kwa hiyo, naombe sana Mheshimiwa Waziri kwamba hakuna haja ya kushindanisha, Simba Sport Club ndiyo wanatutoa kimasomaso kwenye mashindano ya Kimataifa, hii ni nafasi pekee.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Baada ya sauti hiyo kutoka Bunda sasa ni sauti ya mahaba kutoka Tanga, mubashara kabisa kule ambako mahaba yamezaliwa. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi napongeza kwanza Mawaziri wa Wizara hii, ni Mawaziri wasikivu sana. Kwa kweli nafarijika hata Mheshimiwa Ester Bulaya amemuita ni mzee wa site, kweli huyu ni mzee wa site. Mheshimiwa Naibu Waziri hata anapojibu maswali yetu hapa ndani anajibu kwa data na kwa uhakika. Kwa hiyo, tunawapongeza sana pamoja na changamoto hii ya upungufu wa bajeti katika Wizara yao, niwaombe Waheshimiwa Wabunge tulijadili jambo hili kwa umakini mkubwa, tutafute namna ya kupata vyanzo vya kuwawezesha hawa majembe wakahakikishe kwamba ile dhana ya kumtua mama ndoo kichwani inakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri amefika katika Jimbo la Mlalo lakini pia Jimbo la Lushoto katika Halmashauri ya Lushoto. Ninaomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Mheshimiwa Naibu Waziri amepata wokovu na jiko lake linatoka Mkoa wa Tanga. Kwa hiyo, huyu ni shemeji yetu na ndiyo maana hii kazi unaona anaifanya ni kwa sababu ana mtunzaji mzuri kule nyumbani. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, pale katika Kata ya Manolo ule mradi wa vijiji 10 ulitoa ahadi kwamba ukamilike kabla ya Juni 30, nataka nikuhakikishie kwamba matenki yameshajengwa lakini bado hatua ya usambazaji wa mabomba inasuasua. Hii ni sambamba na kule Lushoto katika mradi ule wa Ngulu, kata ya Kwemashai, nao unasuasua, mkandarasi bado hajaanza hatua ya usambazaji wa mabomba. Kwa hiyo, nikuombe shemeji yangu ujitahidi kabisa kwamba ahadi uliyoiweka ya Juni 30 kwamba miradi hii iwe imekamilika, ahadi hiyo uitekeleze.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunayo miradi mingi, ile miradi ya maji ya mwaka 1972. Tunao mradi wa kata ya Mng’aro, kata ya Mbaramo, kata ya Rangwi, kata ya Lukozi na kata ya Malindi. Hii miradi ni ya mwaka 1972 imeshakuwa ni miradi chakavu na watu wameongezeka sana katika maeneo haya. Vyanzo vya maji vimezidi kupungua hasa kutokana na mabadiliko haya ya tabianchi, kwa hiyo nikuombe Mheshimiwa Waziri na Serikali kwa ujumla kwamba miradi hii twende tukaiboreshe. Tutakapoiboresha katika hatua hizi za awali itatusaidia kwamba hatutakuwa na gharama kubwa ya kuandaa tena miradi mikubwa ya vijiji kumi kumi. Kwa hiyo, niombe sana kwa kuwa miradi hii haigharimu pesa nyingi sana ni vizuri tukaitekeleza wakati huu ambapo bado haijawa na mahitaji makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo ni pamoja na mradi ule wa kata ya Mlola katika Jimbo la Lushoto, nao ule ni mradi wa siku nyingi, mkandarasi alikuwepo site muda mrefu, lakini haupigi hatua. Niwaombe tuchukue jitihada za makusudi ili dhana hii ya kumtua mama ndoo kichwani iweze kutimia kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala zima la umwagiliaji. Katika Hosea 4, aya ya sita, anazungumzia watu wangu wanateketea kwa kukosa maarifa na anasema wazi kwamba kwa kuwa wewe umeyakataa maarifa nami nitakukataa.

Katika Halmashauri ya Lushoto na Wilaya ya Lushoto kwa ujumla na Milima ya Usambara tunatiririsha maji mengi sana ambayo yanapotea tu na kuelekea baharini. Hata sasa tunavyozungumza tuna wimbi kubwa la mafuriko katika Mji wa Korogwe eneo la Mkumbara, lakini maji haya yote yanatoka katika Milima ya Usambara. Yapo makorongo mengi yanayoshusha maji na maji haya yanapotea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niiombe Wizara, hatuwezi tukawa na kilimo endelevu bila kuwa na skimu za kilimo. Nimeona hapa katika ukurasa wa 87 mmetaja baadhi ya skimu za kilimo kwa ajili ya kilimo cha mpunga, lakini kule kwangu kuna skimu ile ya Mnazi ambayo tumeizungumza sana Mheshimiwa Waziri, ambayo pia inakwenda kusaidia na kata jirani za majimbo ya Same Mashariki na Same Magharibi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nikuombe sana kwa pale Mnazi ambapo tulikusudia tujenge mabwawa kwa ajili ya shughuli za umwagiliaji. Vilevile ukumbuke katika Wilaya ya Lushoto hili ndilo eneo pekee ambalo lina wafugaji, wenzetu hawa Wamasai. Kwa hiyo, tulikubaliana kabisa kwamba eneo hili tupate bwawa kwa ajili ya kutunza maji kwa ajili ya shughuli za kilimo, lakini pia maji haya yasaidie kunywesha mifugo, kwa sababu katika kata tatu za Jimbo la Lushoto ambazo ni tambarare ni pamoja na eneo hili ambalo ninalizungumza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunakusudia kwamba yatakapopatikana mabwawa katika eneo hili yatasaidia kutatua pia tatizo la wafugaji kuingiza mifugo katika Hifadhi ya Mkomazi na ndiyo maana nasema watu wangu wanateketea kwa sababu ya kukosa maarifa. Kwa hiyo sasa sisi tutumie maarifa haya ili kutatua kero hizi za wafugaji kuingiza mifugo katika hifadhi, lakini tutatue kero hizi za kuacha maji yakiwa yanapotea bila kuwa na matumizi yoyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi naomba nipendekeze eneo ambalo Wizara hii inaweza ikapata fedha, wenzangu wengi wamezungumzia kuongeza tozo katika tozo ile ya mafuta, mimi naunga mkono sina tatizo na hilo, lakini hivyo bado kuna eneo la simu. Mitandao ya simu hii wakati mwingine inatumika vibaya nadhani kwa sababu labda hatujasimamia hili eneo vizuri. Ni eneo ambalo na lenyewe tunaweza tukaja na wazo zuri tukapata tozo kiasi kutoka kwenye mitandao ya simu ili likaweze kutunisha mfuko wetu huu wa maji vijijini. Kwa hiyo niombe sana Wizara ya Fedha ijaribu kuliangalia hili tuone namna gani tunaweza tukapata chochote katika mifuko hii ya simu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mamlaka ya Udhibiti wa Maji na Nishati (EWURA) huwa wanachukua asilimia katika Mamlaka za Maji lakini pia wanachukua asilimia tatu nadhani katika bili za TANESCO. Pesa hizi zingewekewa ukomo kwamba labda asilimia 40 ya pesa hizo wanazozikusanya kutoka mamlaka za maji na kwenye madini pamoja na TANESCO angalau asilimia 40 iingie katika mfuko huu wa maji ili kwenda kutunisha mfuko wa maji na kumtua mama ndoo kichwani kama ambavyo ilani inatuelekeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala zima la maji ni suala ambalo kwa kweli ni jambo kubwa sana ambalo ni ahadi ya ilani na wote hapa hakuna Mbunge ambaye hajaahidi. Kwa hiyo ninaiomba sana Wizara izingatie hilo. Ninaomba kuunga mkono hoja kwa asilimia 100. Ahsante sana, nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na mimi naomba nitoe mchango wangu katika hoja iliyoko mezani kwenye Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri ambayo inaendelea kufanyika katika mbuga yetu ya Hifadhi ya Mkomazi. Kuna wataalam kule wameenda kutatua matatizo yale ya mgogoro, kwa hiyo tunaamini kwamba kwa upande wa Lushoto, Korogwe na Mkinga, sasa maeneo yale ambayo wananchi walikuwa wanasigana na hifadhi majawabu yatakwenda kupatikana kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala lingine nilizungumza juzi kwenye semina naomba nilirudie kwamba Msitu wa Shagayu ambao ndiyo unatiririsha maji yanayokwenda kwenye Hifadhi ya Mkomazi uliungua mwaka 2012 takribani hekta 49 na zilizopandwa miti ni hekta 11 tu. Kwa hiyo, ikolojia ya msitu ule imeharibika. Niombe sana kwamba tukapande miti katika eneo lile ili angalau maji yaendelee kutiririka na kufaidisha Mbuga hii ya Mkomazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nimezungumza katika Bunge lililopita kuhusu usawa katika rasilimali za Taifa. Katika Halmashauri ya Lushoto hatuna mlango wa kuingia hifadhi ya Mkomazi, lakini hali kadhalika kwa Korogwe na Mkinga. Eneo pekee ambalo mtalii anaweza akaingia Hifadhi ya Mkomazi ni kupitia Wilaya ya Same. Sasa naomba na sisi wa Mkoa wa Tanga tupate mlango katika eneo lile la Kamakota ambayo iko katika kata ya Lunguza. Tumeshazungumza mwaka jana lakini mpaka ssa hakuna utekelezaji.

Sasa naomba sana kwamba sisi Lushoto tuna utalii wa misitu, tuna utalii wa mazingira na utalii wa miamba. Kwa hiyo ili mtalii aweze kuacha pesa ni lazima awe na siku nyingi za kukaa katika eneo fulani. Lakini anapotumia siku moja na kuondoka ina maana wananchi wa maeneo yale hawafaidiki na kuwepo kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba sana kuwa tuongeze itinery ya matukio ambayo watalii watakuwa wanayaona katika maeneo yetu. Kwa hiyo naomba suala hili la kupata geti katika eneo la Kamakota lifanyiwe kazi ili na sisi tuweze kuchangia uchumi wa Taifa.

Lakini suala lingine ni suala hili la uhifadhi na ujirani kwamba kumekuwa na matatizo kati ya wafugaji, lakini pia na maeneo haya ya hifadhi. Sisi kule tunajitahidi angalau kujenga malambo nje ya hifadhi kwenye zile kata ambazo zinapakana na hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawaomba TANAPA watuunge mkono katika majaribio haya ya kujenga haya malambo na majosho ili tupunguze kasi ya mifugo kuingia katika hifadhi kwa sababu kama tunavyojua hizi hifadhi zimeanza kuhifadhiwa tangu wakati wa ukoloni. Ina maana wakoloni waliona thamani zaidi kuliko labda hata sisi Tanzania huru sasa hivi tunataka kwamba kila mahali tufanye kuwa ni sehemu ya kuchungia wanyama. Ni vizuri tukaweka mipango yetu mizuri. Sisi tumepewa maarifa ya kuweza kutatua na kupanga rasilimali ardhi vizuri, lakini bila kuathiri nia njema kabisa ya kuhifadhi na kutunza rasilimali hizi za Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la concession fees kwenye mbuga zetu. Hili nalo lazima liangaliwe na kuleta pia hamasa sio tu kwa watalii wa nje lakini kwa watalii hawa wa ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na ahsante sana kwa kunipa dakika hizi tano.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii hasa kwenye eneo la uwezeshaji na uwekezaji. Katika Jimbo la Mlalo, Halmashauri ya Lushoto, wakulima wadogo wameanzisha kilimo cha mazao ya mchaichai ambacho kina tija kubwa kwa sababu ni malighafi ya bidhaa mbalimbali. Tatizo kubwa ni udhaifu mkubwa wa Idara ya Biashara ya Halmashauri kuziona fursa za kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa soko pekee tunalolitegemea ni Kisiwani Pemba ambalo ni soko la kati na siyo soko la moja kwa moja kwa mlaji. Tunaomba kwa dhati, Wizara hii iwatafutie wananchi wa Mlalo masoko ya moja kwa moja ya bidhaa ghafi ya mchaichai ili waweze kukuza uchumi na kipato chao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia mdau wa ndani wananchi wa Mlalo wamethubutu kukopa mtambo wa kusaga na kukamua majani ya mchaichai kuepuka adha ya kusafirisha majani ghafi kwenda Pemba ambako kwa sasa ndiko soko la kati lilipo. Kupitia kampuni ya kukopesha mitambo ya EFICA mdau ameweza kukopa mtambo na sasa wananchi wamepata hamasa kubwa ya kuchangamkia fursa hii adhimu tatizo pekee sasa ni soko la moja kwa moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha Kusindika Chai cha Mponde kule Bumbuli bado ni changamoto. Wawekezaji teule wa Mfuko wa Hifadhi wa LAPF bado hawajaonyesha dhamira ya dhati ya haraka ya kufanikisha zoezi hili. Kata zaidi ya 15 zinategemea chai kama zao kuu la kiuchumi, tozo za Halmashauri zinapatikana kupitia chai, tunaiomba Serikali ilione hili kwa jicho la huruma sana kuwasaidia wananchi wa Bumbuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha AFRITEX Tanga kinachotengeneza nguo pale Tanga mjini kimefungwa kwa sababu ya kodi. Tafadhali naomba tufuatilie ili kuona tatizo hili ambalo limefanya ajira zaidi watu 2,000 za moja kwa moja ziwe hatarini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda cha RHINO CEMENT kimeshusha uzalishaji baada ya kukosa malighafi za kutosha za makaa ya mawe kutoka Liganga na Mchuchuma. Napendekeza sana wapewe mrahaba kama waliopewa wawekezaji wa Dangote ile waweze kupata malighafi ya kutosha. Kiwanda kina uwezo wa kuzalisha saruji tani 20,000 kwa mwezi lakini upatikanaji wa malighafi ni chini ya tani 1,000 kwa mwezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na nia njema ya Serikali ya kuelekea uchumi wa kati unaotokana na uchumi wa viwanda, bado hatupaswi hata kidogo kupuuza matatizo ya viwanda vilivyopo. Kiwanda cha Sabuni cha Foma, TIP Soap Industries vyote vimekufa, Tanga kunani?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nami nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia katika hoja iliyoko katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naanza kwa kuwapongeza Mawaziri wenye dhamana; Waziri na Naibu wake kwa kazi nzuri ambayo wameifanya. Hili suala la tozo kwa kweli ni jambo ambalo lilikuwa linawarudisha nyuma wakulima wetu, kwa sababu hizi tozo zote zilikuwa zinakwenda kwa mkulima. Kwa hiyo, tunaamini kabisa kwamba kwa kuondoa hizi tozo zitaongeza tija pia zitaongeza uzalishaji pamoja na ari kwa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la utafiti hasa kwenye vyuo vyetu vile kikiwemo kile cha MATI - Mlingano. Kwa dhati kabisa tunaiomba Wizara itafute namna ya kuboresha tafiti mbalimbali za mazao ya kilimo. Sasa hivi kutokana na mabadiliko ya tabianchi, mazao mengi yameanza kukataa katika baadhi ya maeneo. Kule Lushoto sisi tulikuwa ni wakulima wazuri sana wa Kahawa, lakini sasa hivi kutokana na mabadiliko ya tabianchi, Kahawa imeanza kupotea. Hali kadhalika na Kilimanjaro hali pia siyo nzuri kama ilivyokuwa mwanzo. Kwa hiyo, tuombe hivi vyuo vifanye tafiti kuona namna gani wanaweza wakabadilisha mbegu ambayo itakuwa inaendana na mazingira ya wakati huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kule katika Jimbo la Mlalo kuna scheme ya kilimo cha mpunga, kinaitwa Mng’aro Irrigation Scheme. Scheme hii imeanzishwa mwaka 1985, wakati huo ilikuwa chini ya ufadhili wa Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO). Linafanya vizuri sana kwa sababu tunalima mpunga lakini pia tunalima mahindi. Scheme hii ina uwezo wa kuzalisha mahindi mara tatu ndani ya msimu mmoja wa mwaka. Kwa hiyo, inasaidia sana kupunguza tatizo la upungufu wa chakula katika maeneo ya Mkoa wa Tanga, lakini na Mkoa wa Kilimanjaro kwa baadhi ya maeneo, hasa Wilaya ya Same na Mwanga. Tatizo kubwa ni mpunga. Mpunga unaolimwa katika bonde lile hauna thamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi ukaamini hivi ninavyozungumza, gunia moja la mpunga kutoka Mng’aro ni shilingi 42,000. Kwa hiyo, unakuta mwananchi anatumia gharama kubwa sana wakati wa kulima, lakini wakati anauza mpunga huu hauna thamani. Kwa hiyo, naomba Wizara itusaidie kufanya utafiti ili tupate mbegu bora zaidi ambayo inaweza ikasaidia wakulima hawa waweze kupata soko zuri la kuweza kushindana na mpunga kutoka Kyela, Shinyanga, Ifakara na maeneo mengineyo. Kwa hiyo, tunaomba sana katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la malambo na majosho ya kuosha mifugo. Katika Halmashauri ya Lushoto tuna kata tatu ni tambarare; na hizi kata ndizo ambazo zina jamii ya wafugaji. Mwaka 1954 kabla ya Tanganyika huru, wakoloni wa Kijerumani walikuwa wamejenga lambo na josho mahali fulani na mpaka sasa hivi lipo. Pamoja na tatizo hili la kuchakata vyuma chakavu, lakini lile lambo bado lipo. Kwa hiyo, naiomba Wizara, na sisi katika Halmashauri tumeshaandika mpango wa kulifufua lile lambo ili tuwasaidie wafugaji hawa wasiingize mifugo katika Hifadhi ya Mkomazi, kwa sababu wakati mwingine hii migogoro ya wafugaji na hifadhi tunaisababisha sisi wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumsaidia Mheshimiwa Waziri kwamba tusiweke huu mzigo moja kwa moja kwake, tumeanza katika ngazi ya Halmashauri. Kwa hiyo, tunaomba mtuunge mkono ili josho lile liweze kutumika, tuwapunguzie wafugaji hawa adha ya kuingiza mifugo kwenye hifadhi na kupigwa faini ambazo ni kubwa sana. (Makofi)

Pia nataka nimwelekeze Mheshimiwa Waziri kwamba katika Kata hizi nazozingumza ambazo zina wafugaji, pia tumeanzisha kilimo cha mazao ya mchaichai. Sasa hivi mchaichai una thamani kubwa sana duniani. Tumeanza majiribio katika ekari kama nne hivi na tumepata soko zuri, lakini soko lenye liko Pemba. Baada ya kuona kwamba zao hili linaweza likawa na tija, mwekezaji mmoja wa ndani ameagiza mtambo kutoka India na sasa hivi tunaweza tukakamua mchaichai katika Tarafa hii ya Umba ambayo ina Kata karibia nne ambazo zinalima mchaichai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe rai kwako kwamba unaweza ukaja ukajifunza huu ubunifu ambao tumeupata kule tukausambaza maeneo mengine ya nchi kwa sababu mchaichai hahutaji sulpher, hauhitaji pembejeo mbalimbali. Ni suala tu la kupanda, kunyweshea, baada ya muda unakata. Tani moja ya mchaichai ni shilingi 250,000. Kwa hiyo, naomba aje alichukue hilo kama shamba darasa la kueneza hiki kilimo maeneo mbalimbali katika nchi yetu. (Makofi)

Suala ambalo lingine ambalo nilikuwa nalizungumzia ni suala bulk procurement ya mbolea. Hili ni jambo ambalo linakuja kutibu tatizo sugu ambalo tulikuwa tunakumbana nalo. Sisi kule Lushoto ni wakulima wa mboga mboga na matunda, lakini mara nyingi tulikuwa tunaulizwa mbona sisi wakulima wa mboga mboga hatupati ruzuku ya kilimo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaelewa kwamba ruzuku hii ilikuwa inaenda katika maeneo yale ya uzalishaji wa chakula. Sasa kwa kuanzisha bulk procurement, maana yake ni kwamba mbolea itapatikana kwa bei ya chini na nadhani kwenye bajeti ya mwaka 2016 Waziri aliyekuwa na dhamana wakati huo alituahidi kwamba lengo ni kuhakikisha kwamba mbolea inapatikana kama vocha ya simu; au akatumia lugha nyingine kwamba ipatikane kama ambavyo unanunua CocaCola dukani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naamini kwa utaratibu huu wa kununua kwa pamoja kama ambavyo tumejifunza kwenye mafuta, utaleta tija kwa sababu kutakuwa na bei maalum, lakini pia itasaidia kuhakikisha kwamba hata wale wafanyabiashara wa ndani wanaweza sasa wakaingia kwenye fair competition. Sasa hivi siyo rahisi sana kwa mwekezaji mdogo wa ndani ku-compete na makampuni yale makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutumia bulk procure- ment maana yake ni kwamba hata hawa wafanyabishara wadogo wadogo ambao ni wazawa wa ndani wanaweza sasa na wao wakaingia katika mfumo huu, wakaagiza kiasi cha tani wanazohitaji katika maeneo yao na itawasaidia pia kukuza mitaji lakini pia kukuza dhana nzima ya uchumi kwa maana ya upande wa wazawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusu tangawizi. Halmashauri ya Lushoto tunalima tangawizi, Halmashauri ya Same wanalima tangawizi, kule Njombe na Madaba wanalima tangawizi na Kigoma na Rukwa nadhani pia wameanza, lakini changamoto ipo kwenye bei. Kwa sababu mara nyingi sana tangawizi inavunwa katika muda ambao unafanana bei yake huwa inashuka kutokana na suala la demand na supply. Kwa hiyo, nimsihi Mheshimiwa Waziri tuone namna ya kuwasiliana na Wizara ya Viwanda Biashara na Uwekezaji kupitia TIRDO na SIDO tupate mashine ndogo ndogo za kuweza kui-process na kuikausha kwa sababu tunauza ikiwa mbichi, hatuwezi tukaitunza muda mrefu. Hii itasaidia kuongeza tija lakini pia tukifanya hizi pro- cessing pamoja na packaging nzuri tunaweza tukaanza kuvuka kwenye masoko ya kimataifa na kuweza kuwasaidia hawa wakulima waweze kuona tija katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu ulikuwa ni huo, nitoe tu rai kwamba Wizara hii inafanya kazi kubwa, ina ma-Extension Officer mpaka kule kwenye vijiji, tunawaomba muwatumie vizuri. Hii ndiyo Wizara pekee ambayo ukifika katika ngazi ya kijiji unaikuta lakini nadhani kuna tatizo la connection kutoka kwenye Halmashauri na kuja kwenye Wizara. Hebu tuitumie nafasi hii vizuri ku- coordinate na kuhakikisha kwamba ikitokea agizo la kitaifa basi huku chini wote wanawajibika. Tunapopita katika maeneo yetu tunagundua wakati mwingine hawa Maafisa Ugani hata hajui kwa nini yuko mahali pale. Kwa hiyo, nitoe sana wito kwamba kwa sababu mnayo hii rasilimali watu ya kutosha tuitumie vizuri kuhakikisha kwamba Wizara hii tunaitendea haki kama ambavyo tunaizungumza kwamba ndiyo uti wa mgongo wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Amani na Usalama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nami nachukua nafasi hii niungane na Waheshimiwa Wabunge pamoja na Mheshimiwa Spika, kutoa pole kwa mwenzetu kwa jambo ambalo limempata na tunamuomba Mwenyezi Mungu amjaalie ili afya yake iweze kurejea katika hali ya kawaida.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nami nitoe mchango mbele ya Bunge lako Tukufu juu ya Azimio la Bunge kuridhia Mkataba wa Kuanzishwa Kamisheni ya pamoja ya Bonde la Mto Songwe sambamba na kuridhia Azimio la Itifaki ya Amani na Usalama kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, miaka ya hivi karibuni suala la maji limekuwa ni suala ambalo linaelezwa kuweza kusababisha Vita Kuu ya Tatu ya Dunia. Maji yamekuwa ni tatizo, lakini chanzo kikubwa cha ukosefu wa maji ni uharibifu wa mazingira. Pamoja na mabadiliko ya tabia nchi ambayo kimsingi yanashahibiana moja kwa moja na mabadiliko ya tabia za binadamu hasa pale ambapo tunaharibu mazingira, basi maazimio kama haya yakija kwenye Bunge letu Tukufu, hakuna namna zaidi ya kuridhia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe rai tu kwamba pamoja na nia nzuri ya Serikali kuridhia hili, lakini sasa iwe ni mwanzo wa changamoto pia kuhifadhi mabonde mbalimbali yaliyoko katika Taifa letu. Kwa mfano, tumeona hivi karibuni kulikuwa na wadau wa Bonde la Mto Ruaha Mkuu lakini pia kule Mkoani Rukwa na Katavi kuna bonde pia, nimeona Mheshimiwa Waziri anayehusika na mazingira walikuwa wanafuatilia pia uhifadhi wa lile bonde; na kuna mabonde mengine kama Malagarasi, bonde la Mto Pangani nayo pia bado hayako katika hatua nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitoe rai kwamba tunapokwenda kuridhia mikataba hii ya Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kwa maana kwa nchi ya Tanzania na Malawi, basi pia tuone umuhimu wa kuangalia kwa mapana haya mabonde mengine ambayo yanazunguka katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe rai, kama ambavyo kwenye Kamati wameshauri kwamba nchi yetu haikuwa na mahusiano mazuri sana na Malawi hasa katika eneo hili la ziwa, lakini nadhani kwamba itifaki hii iende pia kuamsha ari mpya katika kutengeneza mahusiano, siyo tu ya kidiplomasia lakini ya kiuchumi, ya kijamii na ya kimazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini kwamba mkataba huu ukiridhiwa utoe tija ambayo inategemewa kwa wananchi wa pande zote mbili. Pia ni kipaumbele kwamba kwa kuwa hata Mkoa huu wa Songwe ni mkoa mpya, tunaamini kwamba fursa mbalimbali zitakazopatikana kupitia uanzishwaji wa hii Kamisheni utasaidia hata kusukuma maendeleo mengineyo hasa katika Sekta za Kilimo na uzalishaji wa umeme; tumeona hapa takriban megawatt 180 zinaweza zikazalishwa kupitia bonde la Mto Songwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine ambayo naiona ni suala zima tu la eneo kwa wananchi juu ya utunzaji wa jumla wa mazingira hasa tunavyoona kwamba mto huu unatiririsha maji kuelekea katika Ziwa Nyasa na mara nyingi shughuli za kilimo wakati mwingine zinachangia kusababisha uharibifu na kusababisha vina vya maziwa kupanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitoe rai kwamba pia wananchi waelimishwe ili wale ambao wanalima pembezoni mwa mabonde haya, wawe waangalifu kiasi kwamba tuweze kulinda siyo bonde peke yake, lakini pia hata mtiririko wa maji kuelekea katika Ziwa Nyasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili nizungumzie kuhusu kuridhia kwa Itifaki hii ya Amani na Usalama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Napenda kupongeza kwa hatua hii. Pia natoa rai kwamba naunga mkono moja kwa moja Azimio hili, kwa sababu tumeona kwamba sasa hivi nchi hizi za Afrika Mashariki tuna tatizo la ugaidi. Tumeona mara nyingi kule upande wa Kenya hasa eneo la Garissa na Mombasa mara kwa mara wamekuwa wakishambuliwa na magaidi hasa hawa wanaotokana na wenzetu wale wa kutoka Somalia, Al-Shabaab.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni, mwaka mmoja uliopita, hata katika Mkoa wa Tanga katika maeneo ya Mapango ya Amboni kulipatikana vikundi ambavyo vilikuwa na dalili zote kwamba ni vikundi vya kigaidi na hata hali inayotokea pale katika eneo la Kibiti, Mkuranga ni viashiria ambavyo siyo vizuri sana kwa ustawi wa amani na usalama katika nchi zetu za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme wazi kwamba protocol hii itatusaidia ili tuwe na ulinzi wa pamoja kama ambavyo tunafanya na hata juzi hapa, tuliona kule Tanga kulikuwa na zoezi la pamoja kwa nchi za SADC. Kwa hiyo, tutafarijika sana kwamba zoezi hili sasa nje ya SADC lifanyike pia kwa nchi hizi za Afrika Mashariki hasa kwa kuzingatia kwamba sisi mipaka yetu hii karibu nchi zote tano ukiondoa Sudan Kusini ambayo ni mwanachama mpya, lakini nyingine zote tunapakana nazo kila mahali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hii itasaidia kama hapa ambapo wamezungumza pia kwamba wakati mwingine kuna minada ya mifugo inafanyika katika hizi nchi, hata mimi katika Jimbo langu la Mlalo pia ni mwathirika wa hii minada. Ni kwamba katika Bonde la Mkomazi ambako kuna wafugaji ambao wanapatikana katika Wilaya za Same, Lushoto Mkinga na Korogwe, mara nyingi kule hatuna minada katika haya maeneo kwa upande wa Tanzania. Kwa hiyo, hawa wafugaji huwa wanapeleka kuuza mifugo katika upande wa Kenya. Kwa hiyo, kwa kupitia itifaki hii, naamini kwamba suala hili litaimarisha mahusiano haya na tunaweza hata tukawa na masoko mazuri yenye amani na usalama na kusaidia biashara hizi ziweze kufanyika vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, nitoe rai kwamba ipo mipaka katika Jumuiya ya Afrika Mashariki ambayo siyo mipaka rasmi, lakini kwa Serikali hizi kwa kushindwa kuirasimisha, inachochea sasa hata vitendo vya uhalifu kufanyika na biashara za magendo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, pamoja na kwenda kusaini Azimio hili la Amani na Usalama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, lakini pia Serikali sasa ione pia chachu na ione pia mwanya wa kwenda kurasimisha ile mipaka, hata isiwe katika ngazi za Kimataifa lakini angalau katika ngazi zile zile za ujirani mwema kwamba tuwe tunaweza kubadilishana mazao ambayo yanapatikana katika nchi hizi tunazopakana. Tofauti na hivyo, bado unabaki mwanya kwa wananchi wa kawaida kuitumia kuvusha kwa njia za magendo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitoe rai kwamba tunapokuwa na maazimio mazuri kama haya ni vizuri pia tukayatumia haya haya kuongeza tija nyinginezo za kiuzalishaji, isibaki tu kwa ulinzi na usalama, lakini pia za uzalishaji na kuinua uchumi wa wananchi katika maeneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono Maazimio yote mawili. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami naomba nitumie fursa hii kumpongeza Waziri mwenye dhamana pamoja na Naibu wake, wanafanya kazi nzuri sana, kazi ambayo haiwezi ikatiliwa shaka na Mbunge yeyote makini humu ndani.

Vilevile naomba nimpongeze Katibu Mkuu wa Wizara ndugu yangu Kayandabila nae anafanya kazi nzuri sana, tumeona jinsi tatizo la ardhi katika nchi yetu linavyozidi kutatuliwa siku hata siku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo kuna tatizo kidogo katika eneo langu la Halmashauri ya Lushoto, kuna Mwekezaji mmoja wa nchi jirani ya Kenya amemilikishwa mashamba matatu lakini ameshindwa kuyaendeleza.

Sasa katika Halmashauri yetu tuna uhaba mkubwa sana wa ardhi na ardhi hii hekari 4,019 zimekaa tu domant. Kwa hiyo, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, kwamba huyu Mwekezaji anapita na anatoa lugha za kashfa mitaani kiasi kwamba anajifananisha kwamba yeye mmoja ni sawa na Watanzania watano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa tafsiri rahisi ya yeye mmoja na Watanzania watano ni kwamba hapo kuna Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Waziri mwenye dhamana na Mbunge. Kwa hiyo, sisi watano ni yeye mmoja. Sasa naomba nimwachie hilo Mheshimiwa Waziri aangalie namna gani tunafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba la kwanza lina hati namba 41/44,hekari 562; shamba la pili ni hati namba 17/ 146, hekari 1188; shamba la tatu ni namba 11/247, hekari 2,442; na tumeshatoa notice ya revocation kuanzia tarehe 14 Julai, 2016 na hakujibu na tarehe 9 Desemba, file limeshafika kwa Kamishna wa Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Kamishna wa Ardhi Kanda ya Kaskazini kwa masikitiko makubwa yule mama ambaye alikuwa pale kabla hajahamishwa amekalia file na kila tukiuliza analeta sababu ambazo siyo za kiofisi. Jambo lolote la kiofisi linapaswa kujibiwa kwa nyaraka za kiofisi, lakini mama huyu kila wakati ukiuliza anatoa majibu kwamba file halijakamilika, sijui notice zimekosewa. Sasa haya ni mambo ya technical ambayo wananchi hawapendi kuyasikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, kwenye barua yetu Afisa Mteule wa Ardhi ameandika wazi kwenye hitimisho, mwekezaji katika mashamba ya katani Mnazi ameshindwa kwa kiasi kikubwa kuyaendeleza mashamba anayoyamiliki. Katika hekari 4,192 ni hekari 500 tu ndizo ambazo ameziendeleza kwa kupanda mkonge na kuvuna, hekari 1,942 mkonge uko porini kwenye vichaka hautunzwi kabisa. Hekari 1023 ni msitu mtupu ambao unatumiwa na wafugaji wa kijamii ya kimasai kwa malisho ya mifugo yao. Pia mmiliki huyu hajalipa kodi ya ardhi tangu 2004/2005 mpaka sasa na anadaiwa zaidi ya shilingi milioni 42.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wawekezaji kama hawa kwa kweli sidhani kama wana nafasi katika Serikali hii ya Awamu ya Tano. Namsihi sana Mheshimiwa Waziri tuchukue hatua stahiki. Wananchi hawa wa Lushoto kama nilivyotangulia kusema wana uhaba mkubwa wa adhi. Kwa hiyo ardhi hii ndio angalau tukipata na sisi tunaweza tukaingia na wenzetu hawa kuingia katika economic zone tukapata angalau mahali pa kuwekeza. Kwa hiyo, namsihi sana, namwamini Mheshimiwa Waziri, sijawahi kutilia shaka uwezo pamoja na mama yangu pale Angelina Mabula nawapongeza sana, ahsanteni sana.
Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Kazi za Ubaharia wa Shirika la Kazi Duniani na Azimio la Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Vitambulisho vya Mabaharia Na. 185 wa Mwaka 2003 wa Shirika la Kazi Duniani
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nataka nipongeze Serikali kwa kuleta mkataba huu, niseme tu kwamba mkataba huu umechelewa sana. Sisi kule Tanga tumepoteza vijana wengi sana kwa sababu ya kuchelewa kusaini mikataba kama hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vijana wengi walikuwa wanajihusisha na shughuli za madawa ya kulevya wanapozamia kwenye meli kwa ajili ya shughuli za ubaharia. Kwa mkataba huu naamini sasa kwamba kwa kuwa kazi za ubaharia zinaenda kutambuliwa rasmi ndio utakapoona tofauti kwa kazi ambazo ni rasmi na zile kazi za kishoka utaweza kuona kwamba tukiwa na mikataba rasmi kama hii basi shughuli nyingi zitakazofanyika zinalinda pia maslahi mapana ya usalama wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kushauri Serikali kwamba kwa kuwa mkataba huu ni wa Kimataifa na pia tunayo maziwa katika mipaka yetu na mipaka hii tunapakana na nchi mbalimbali. Kwa upande wa Ziwa Victoria tuna Kenya na Uganda; Ziwa nyasa kuna Malawi na Zambia; na Tanganyika kuna Burundi na Congo na hapa nimeona Congo wameridhia mkataba huu mwaka 2015. Nitoe rai kwamba kwa kuwa nao kwenye maziwa haya pia kuna vyombo hivi vya usafirishaji basi tujaribu ku-harmonies na hizi sheria pia zitumike kwenye vyombo ambavyo vinasafiri katika maziwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumejifunza kwenye Kamati kwamba wenzetu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar wana chombo maalum cha kusajili vyombo vya majini, sasa huku kwetu tuna SUMATRA ambao wanasajili vyombo vya majini na vyombo vya nchi kavu. Ningependa sasa kuishauri Serikali kwamba ifikie mahali tutenganishe hivi vitu kwa sababu tunaona mara nyingi sana kwenye maziwa huku kunatokea maafa makubwa labda ni kutokana kwamba SUMATRA wako busy zaidi na vyombo vya nchi kavu kuliko vyombo vya majini. Kwa hiyo, nitoe rai kwamba kwa kutumia mkataba huu sasa tuweze kupanua wigo wa kutoa huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo niseme kwamba hii ni fursa nzuri sana kwa vijana wetu kupata ajira, lakini ni fursa nzuri pia kwa utambuzi wa Kitaifa kama alivyomalizia msemaji wa mwisho hapa kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilikuwa inatumia wakala kusajili meli na ndiyo maana unakuta wakati mwingine hata hizi meli zinahusishwa na uharamia, lakini pia zinahusishwa na mambo mabaya ambayo yanachafua taswira ya Taifa. Sasa ni imani yetu kwa mkataba huu kila kitu kitawekwa katika utaratibu ambao ni mzuri kwa ajili ya kulitangaza Taifa letu katika Mataifa ya nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naunga mkono azimio hili.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Naomba kabla sijaendelea niwaambie wenzangu Waheshimiwa Wabunge waende katika Kitabu cha Maendeleo Fungu Namba 21 Hazina wataona pale kuna shilingi bilioni 60 kwa ajili ya Village Empowerment hapa ndio kwenye zile shilingi milioni 50 kwa kila kijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nijaribu tu kumsahauri Mheshimiwa Waziri, kwa kuwa hili ni agizo la Ilani ya Chama cha Mapinduzi na humu ndani tuko vyama vingi ni vema hizi shilingi bilioni 60 ungeanza katika Majimbo yale ya Chama cha Mapinduzi ambao kimsingi ndio wameahidi kwenye Ilani yao, hizi Ilani nyingine ambazo hatujawahi kuziona ungeweka pembeni kwanza, kwa hiyo shilingi bilioni 60 ambayo iko kwenye Fungu Namba 21 Kitabu cha Maendeleo hiki hapa wote msome Village Empowerment.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii adhimu kabisa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya, kazi hii ya kuzuia makinikia, ni kazi ambayo ni ya ujasiri mno haijawahi kufanywa na kiongozi yeyote wa Taifa hili tangu Awamu ya Pili, ya Tatu na ya Nne. Kama tunasema zimeundwa tume lakini zimeishia kuwa ni Tume ambazo labda zimeweka makabrasha pembeni lakini huyu amechukua hatua ya kwenda hata kuzuia.

Kwa hiyo, ni jitihada za kijasiri sana ambazo zinapaswa kuungwa mkono na kila mzalendo wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimshauri na kwa bahati nzuri Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Katiba na Sheria yuko hapa kwamba kuna watu wanatutisha kwamba tutashitakiwa. Lakini kwa bahati nzuri Mwenyekiti wa Barrick ameshakuja kuonesha kwamba anahitaji maridhiano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili kwa sababu siyo jinai ni madai, madai yanaanza kwanza kuzungumza ninyi wenyewe, inaposhindikana ningeshauri kwamba tusiogope tuende kwenye Mahakama ya Kimataifa (International Court of Justice - ICJ), kule tunapelekana baada ya kushindwa kuelewana. Kwa hiyo hii ni mahakama huru kabisa tunakwenda kule tunashitaki na tunaweza tukapata haki zetu stahiki, kwa sababu kuna dispute imefanyika ndani ya mkataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nataka niseme hata kwenye Mahakama zetu, kuna ile alternative dispute resolution ambayo kabla hamjaamua kushtakiana mnaweza kwanza mkakaa ili kutafuta amicable way ya ku-solve matatizo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri najua wewe huna makeke ni mtulivu na ni mwanasheria ambaye umebobea, kwa hiyo hili naamini litakwenda vizuri.

T A A R I F A

HE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hii kwa kuwa amesema ndugu yangu Khatib kwamba naye anaelewa kwamba mwelekeo ni kulipa basi naipokea, safi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kwenye tozo ya shilingi 40 kwenye mafuta, naomba niwaambie Waheshimiwa Wabunge kwamba tunapozungumza hii tozo, kwanza inaanza kutozwa kwenye ushuru, yale makampuni yanayoingiza mafuta ndio kwanza wanawekewa hii tozo. Mafuta yakishalipiwa ushuru yakishatoka, yakishaingia kwenye usambazaji hakuna tena kodi pale, mafuta hayana VAT ndio maana EWURA wako pale kwa ajili ya kuweka bei kikomo. Sasa hivi kwa sababu tunaingiza mafuta kwa njia ya bulk procurement maana yake ni kwamba hata EWURA wataangalia competitive price na kwenye price stabilization ya mafuta REA ipo, reli ipo, kwa nini tushangae mafuta leo? Hata hiyo shilingi 50 ya maji ipo, mbona gharama hazikuongezeka? Kwa hiyo hili ni suala la kitaalam. Mambo haya ya mafuta niwaambie hata hayo mafuta ya taa sasa hivi tunaagiza kiasi kidogo sana, yako makampuni 23 yanayoingiza mafuta hapa nchini, lakini hayazidi matano yanayoingiza mafuta ya taa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mafuta ya taa yanatumika kwa kiasi kidogo sana sasa hivi, tusidanganye, ni lazima Watanzania tutanue wigo wa walipa kodi. Walipa kodi walikuwa ni wachache sana ndio maana hao hao kila siku wanakamuliwa, lakini tunavyotanua wigo wa walipa kodi maana yake ni kwamba hata huyu mtu mdogo ambaye anatumia lita mbili atuchangie shilingi 80. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii niseme kwa dada yangu Mheshimiwa Majala, wewe ni Muislam na katika uislam kuna Zakatul - Mal (zaka ya mali) kila shilingi 100 unatakiwa uilipie japo shilingi mbili na nusu, hii haikwepeki. Hata katika Wakristo fungu la kumi lipo, kodi haijawahi kumpendeza yeyote. Tunasema hapa lazima watu walipe ushuru, lazima walipe kodi, kama ambavyo kanisani watu wanatoa sadaka na kama ambavyo kanisani watu wanatoa fungu la kumi na kule misikitini watoza Zakatul- Mal na hata huu mwezi wa Ramadhan wewe unatakiwa utoe Zakatul- Fitr kabla ya kuswali sala ya Idd. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mamlaka hii ya Magufuli ni mamlaka inayotoka kwa Mungu na haya ndio maagizo kwa mujibu wa vitabu. Kwa hiyo, lazima tutanue wigo wa ulipaji kodi, kodi inapolipwa na watu wengi kwanza inakuwa ni rahisi kulipika, inapungua, pia tunaongeza katika mfuko wetu tunapata kodi nyingi zaidi. Nani aliyewaambia kodi ya road licence ilikuwa inaenda kununua maandazi ya wafanyakazi wa TRA? Ilikuwa inaenda kwenye huduma. Kwa hiyo, hata hii ya tozo ya mafuta inakwenda kwenye huduma, hivyo tusubiri mwakani kama utekelezaji haupo, tuwaambie mmechukua shilingi 40 kwenye kila lita utekelezaji wake uko vipi, lakini suala la kodi halikwepeki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee suala la viwanda. Kule Tanga viwanda vyetu vingi vimefungwa kwa sababu ya mambo ya kodi pia wengine ni kwa sababu ya ushindani wa kibiashara. Naomba nitoe rai Kiwanda cha Afritex cha nguo kimefungwa, nimeshazungumza sana Mheshimiwa Waziri, pia wenzetu wale wa Tanga Fresh wanapewa deni ambalo haliwahusu. Nikuombe Mheshimiwa Waziri ulisimamie deni hili ili wawekezaji hawa waweze kuona comfort ya kufanya biashara katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la kiwanda cha Chai cha Mponde, umeshazungumza kwamba wawekezaji kupitia Mfuko wa LAPF watakwenda kuwekeza pale, lakini sasa ni mwaka wa tatu bado tunaona mambo hayaendi. Nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Waziri kwamba katika Halmashauri ya Bumbuli, Jimbo la Bumbuli, Kata 14 zinalima chai, kwa hiyo, kufungwa kwa kiwanda hiki ni msiba mkubwa wale wananchi kwa kweli tumewakosea sana, wanashindwa kuzalisha mali na wanashindwa kuongeza pato la Taifa kupitia uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni usambazaji wa umeme vijijini. Ninashukuru kwamba Wizara ya Nishati na Madini imetoa vijiji 146 katika Mkoa wa Tanga, ni vijiji vichache sana ukifananisha na Mikoa mingine. Nimuombe Waziri mwenye dhamana aliangalie hili kwa umakini sana, kwa sababu kama katika Halmashauri ya Lushoto na Halmashauri ya Handeni, Halmashauri pekee zina Majimbo mawili mawili…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nikuombe sana Mheshimiwa Naibu Waziri wa Nishati na Madini pamoja na Waziri mwenye dhamana tuangalie hili kwa kina sana kuhakikisha kwamba tunapata viwanda vya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, basi nashukuru naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa shukrani za dhati kwa Waziri mwenye dhamana, Mheshimiwa William Lukuvi pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Angeline Mabula, sambamba na timu nzima ya Wizara chini ya Jemadari Kayandabila.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe malalamiko yangu kuhusu hatua ambazo zinachukuliwa na Idara ya Ardhi Kanda ya Kaskazini; tunalo shamba letu la Mnazi Sisal Estate ambalo kwa sasa linamilikiwa na mwekezaji wa Kenya kupitia kampuni ya Le-Marsh Enterprises ambayo inamiliki mashamba matatu yenye hati zifuatazo; tittle No.44144, ekari 562; tittle No. 17146, ekari 1188, pamoja na tittle No. 11247,
ekari 2442.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Lushoto ilitoa barua ya Notice of Revocation yenye Kumb. Na. LDC/ L.10/VOL.111/245-09/12/2016 kwenda kwa Kamishna wa Ardhi Kanda ya Kaskazini. Naomba nitoe masikitiko yangu kuwa barua hii inakaribia kumaliza mwaka lakini hadi sasa hakuna kinachoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikichukua hatua za ufuatiliaji mara kwa mara kwenye Ofisi ya Kanda, lakini mara zote nilikuwa napata ushirikiano hafifu, ikiwemo mara ya mwisho, Mheshimiwa Waziri tulivyofanya mazungumzo, walitujibu kuwa kuna matatizo ya kiufundi kwenye taarifa ya notisi. Hili kwetu tunaliona kama ni hujuma kwa kuwa barua za Kiserikali hujibiwa kwa taratibu zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama walivyo wawekezaji wote wababaishaji huyu Le Marsh Enterprises ni miongoni mwao na amekuwa akiwahadaa wananchi, Halmashauri na sasa anaonekana na baadhi ya Maafisa wa Ardhi Kanda, wanamlinda hivyo kusababisha chuki kubwa kwa wananchi husika wa Kata za Mbaramo, Mnazi, Lunguza ambao wanazungukwa na mashamba hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuna nia ya kumuonea mtu lakini tunahitaji kuona wananchi wanafaidika na rasilimali zao na pia kuona mapato ya Halmashauri yanapatikana bila kikwazo chochote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hitimisho; mwekezaji katika Mashamba ya Katani ya Mnazi ameshindwa kwa kiasi kikubwa kuyaendeleza mashamba anayoyamiliki. Kati ya ekari 4192 ni ekari 500 tu ndizo ambazo ameziendeleza kwa kupanda mkonge na kuvuna, ekari 1942 mkonge upo porini, kwenye vichaka hautunzwi kabisa. Ekari 1023 ni msitu mtupu ambao unatumiwa na wafugaji wa jamii ya kimasai kama malisho ya mifugo yao. Pia mmiliki huyo hajalipia kodi ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia hoja hii iliyopo mbele ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia RCC ya Mkoa wa Tanga na vikao vya Mfuko wa Barabara vya Mkoa (Road Board)kwa miaka miwili mfululizo tulikuwa tukipanga fedha kwa ajili ya kuifanyia upembuzi yakinifu (feasibility study) pamoja na detailed design barabara ya Lushoto hadi Mlalo kilometa 45. Hata hivyo, kwa mara zote ombi letu lilikuwa halipokelewi mara linapofika kwa Afisa Mtendaji wa Wakala wa Barabara wa Taifa (TANROADS).

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ni muhimu sana kwa uchumi na ustawi wa maendeleo ya Mlalo. Ikumbukwe kwamba uchumi wa wananchi wa Mlalo unategemea sana kilimo cha mboga mboga na matunda. Matunda na mboga mboga ni bidhaa ambazo zinaoza kwa haraka sana. Hivyo basi, ili kujenga uchumi imara, tunahitaji barabara madhubuti ambazo zitafikisha mazao yetu sokoni kwa haraka zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara kwa mara barabara zetu zimekuwa zikijifunga nyakati za mvua kutokana na landslide (maporomoko) hivyo kwa dhati kabisa tunaiomba Serikali yetu sikivu isikie kilio chetu tupate barabara ya kiwango cha lami. Eneo hili ni kilometa 45 tu kutoka Lushoto Mjini hadi Mlalo ambapo ndiyo kituo cha mwisho cha mabasi yaendayo maeneo tofauti ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya kutoka Mlalo – Mng’aro kilometa 20, imepandishwa hadhi hivi karibuni miaka ya 2012 na Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete. Baadhi ya nyumba zilizopo pembezoni mwa barabara hiyo zimewekwa alama ya “X”, tunapenda kujua tafsiri ya alama hizo kwa sababu wananchi wanashindwa kuelewa hatma ya nyumba zao na wanashindwa kuziendeleza. Hivyo, tunaomba Serikali itoe tafsiri ya alama hizo ili wananchi waweze kujipanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, mawasiliano ya simu za viganjani bado siyo rafiki sana, yapo maeneo ambayo yapo katika mabonde na yamefunikwa na vilele vya milima, mfano katika Kata ya Malindi hasa Kijiji cha Makose na kata ya Rangwi eneo la Longoi Mtaa wa Bustani na katika eneo lote la Mliifu Kata ya Manolo. Tunahitaji msaada huu kwa wananchi wa maeneo niliyoyataja ili kuongeza tija na ufanisi katika shughuli za kijamii na kiuchumi kwa wananchi wa Jimbo la Mlalo hususani Makose, Longoi, Mliifu, Hambayo na Viti.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Kwanza nitoe pongezi kwa dada yangu Mheshimiwa Ummy kwa kazi kubwa anayoifanya, kazi inaonekana, chapa mwendo tuko pamoja na wewe. Lakini shukrani za pekee nizitoe mimi kama Mbunge wa Jimbo la Mlalo kwa msaada mkubwa wa mabati ulichotupatia katika kituo chetu Mwangoi, tunashukuru sana. Nitoe pia pongezi kwa Mheshimiwa Naibu Spika kama Balozi wa Afya katika Jimbo la Mlalo, umefanya mambo makubwa sana, Mwenyezi Mungu aendelee kukubariki na ile wodi ambayo tumeipa jina lako sasa tuko katika hatua za usafi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwa haraka sana nichangie katika hoja iliyopo mbele ya Bunge lako Tukufu, nikianza katika ukurasa wa 112, vipaumbele vya Wizara kwa mwaka 2018/2019, kipengele namba mbili, kuimarisha huduma ya kinga dhidi ya magonjwa yanayotokana na kutokuzingatia kanuni za usafi na usafi wa mazingira kama magonjwa ya kuhara, kuhara damu, kipindipindu na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ipo kampeni inayoendelea sasa hivi ya “usichukulie poa nyumba ni choo” hapa kuna jambo la msingi saa ambalo Wizara inatakiwa ilifanyie kazi. Nimefanya utafiti mdogo katika Jimbo langu nimegundua kwamba watoto wengi wa shule ndio ambao wanaugua ugonjwa wa UTI na sababu kubwa inayosababisha tatizo hili ni ukosefu wa vyoo bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ninaitaka sasa Wizara kwa kushirikiana na TAMISEMI watengeneze mkakati mahsusi wa kuhakikisha kwamba shule zetu za msingi na sekondari zinakuwa na vyoo bora kabisa. Inawezekana kabisa kila mwaka tunasema bajeti ya Wizara ni kubwa, haiongezeki lakini inawezekana tukawa tunahitaji bajeti kubwa kwa kuwaaminisha kwamba Watanzania ni wagonjwa sana kumbe tatizo siyo ugonjwa labda tukipata elimu inawezekana bajeti hii ikapungua kabisa wala hatuhitaji kuwa na mabilioni mengi katika eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba sana hii kampeni ya “usichukulie poa maisha ni choo” tuiendeleze na hata kule kwa wenzetu Wasukuma kule Mwanza tunaona nyumba ziko milimani kule na hatujui hata vyoo wanachimbia maeneo gani, naamini katika hili tutapunguza fedha nyingi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye report ya CAG amezungumzia deni la Wizara ya Afya katika hospitali zile za nje hasa kule India. Niiombe Wizara ilifanyie kazi eneo hili. Wapo Watanzania wengi sana ambao wanahitaji rufaa za kwenda kupata matibabu nje, lakini wanashindwa kwenda kwa sababu tunadaiwa fedha kule.

Kwa hiyo, nikuombe dada yangu Ummy, wewe ni shahidi kuna mgonjwa mmoja nilikuomba angalau umsaidie alikuwa ameshapata kibali na alikuwa ameshapata kibali na alikuwa yuko tayari hata kujilipia nauli tatizo lilikuwa fedha za matibabu na natumia nafasi hii kukwambia kwamba Mwenyezi Mungu yule mgonjwa amempenda zaidi. Kwa hiyo, huoni kwamba ni Watanzania wengi wanapoteza uhai kwa kukosa fursa hii? Kwa hiyo, nawaomba sana Wizara isimamie hili ili liweze kupata ufumbuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni suala la Kituo cha Saratani cha Ocean Road; wanafanyakazi nzuri sana lakini kwa kweli kuna msongmanao mkubwa. Nitoe rai kwa Wizara hii; hebu tutengeneze mkakati wa kuwa na hospitali kwa kanda, tunaweza tukaanzia Kanda ya Ziwa pale Bungando, tukaenda Mbeya angalau pale hospitali ya Rufaa ya Mbeya tukatengeneza vituo vya saratani ili tupunguze ule msongamano pale Dar es Salaam. Wananchi wengi wanapata shida sana kwa kwenda mpaka Dar es Salaam kupata hii huduma ambayo sasa hivi sasa saratani imekuwa ni ugonjwa wa kawaida sana kwa ndugu zetu hawa.

Mheshimiwa naibu Spika, lingine nizungumzie huduma za hospitali katika Hospitali yetu ya Rufaa ya Mkoa Bombo pale Tanga, najua Mheshimiwa Waziri wewe ni mwenyeji vizuri pale, lakini siyo wakati wote unapata muda wa kuembelea pale. Huduma zetu bado zinahitaji kuboreshwa sana . Tunaye Daktari Bingwa nadhani ni mmoja tu, kwa hiyo bado tunahitaji tupate Madaktari Bingwa wa kutosha. Kama unavyojua jiografia ya Mkoa wetu wananchi ni wengi sana wanaohitahi huduma katika hospitali hii, kwa hiyo, nikuombe sana na hili nalo ulizingatie.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, ahsante sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa maelezo yangu kwa Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi. Nina masikitiko makubwa kwamba huenda kama nchi yetu isingekuwa na maziwa makubwa kuzungukwa na bahari basi tusingekuwa na sekta hii ya uvuvi. Hii ni kwa sababu Wizara haioneshi kujali na kuthamini kusambaza huduma za uanzishaji wa mabwawa ya samaki kwenye maeneo ambayo hayana maziwa na mito mikubwa. Hivyo kutokuwa na tija inayokusudiwa kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wa Tanga wenye Wilaya nane ni Wilaya nne zilizoko pembezoni mwa Bahari ya Hindi ndio zinazopata samaki, Wilaya hizo ni Mkinga, Tanga, Pangani na sehemu ndogo ya Wilaya ya Muheza. Aidha, Wilaya ya Lushoto, Korogwe, Handeni na Korogwe hazina mito mikubwa wala mabwawa ya kuwezesha wananchi kupata kitoweo cha samaki.

Mheshimiwa Spika, jambo hili limekuwa likileta madhara makubwa ya kiafya kwa wananchi hasa wa Lushoto kutokana na upungufu wa madini ya chuma (iron) ambayo yanapatikana katika jamii ya samaki. Naomba kuishauri Serikali itujengee mabwawa ya samaki ili iweze kutibu madhara makubwa ya kiafya ya wananchi wa Lushoto.

Mheshimiwa Spika, ili kuwa na afya bora kwa wananchi wetu wa Tanzania na hata kupunguza bajeti ya Wizara ya Afya, Serikali ni lazima ichukue jukumu lake la kujengea uwezo watu wa Lushoto wapate mabwawa lakini pia na nchi nzima kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Spika, mifugo katika nchi yetu imekuwa haina faida zaidi ya kuonekana kama laana. Tunaomba sana mifugo ijengewe malambo, majosho ili kuongeza thamani ya mazao ya mifugo. Katika Jimbo la Mlalo, Kata za Mnazi na Mng’aro zina wafugaji wengi hasa ikizingatiwa zipo jirani na Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi ambalo ni eneo rafiki kwa ustawishaji wa mifugo. Nitoe rai kwa Serikali kupitia Wizara hii ili kusaidia wananchi wa maeneo haya ili waweze kuboresha mifugo yao. Nashauri pia Serikali iangalie kwa kina sekta ya maziwa hasa eneo la kodi kwa maziwa yanayoingizwa kutoka nje ya nchi. Nawasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nadhani ninazo dakika kumi hapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Waziri mwenye dhamana, Mheshimiwa Profesa Makame Mbarawa pamoja na wasaidizi wake Engineer Atashasta Nditiye na Mheshimiwa Kwandikwa kwa kazi nzuri wanayoifanya. Tuombe Mwenyezi Mungu aendelee kuwabariki na jukumu letu sisi ni kuwatia nguvu na kuishauri Serikali katika yale ambayo wanayatekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na suala la gati katika eneo la Mkinga ambalo tumepata mwekezaji wa kiwanda kikubwa sana cha saruji. Niombe sana Wizara hii ihakikishe kwamba jambo hili linakwenda kutokea. Tunazungumza mara kwa mara humu ndani ya Bunge kwamba tunahitaji kuwa na miradi ya PPP.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii japo sio PPP lakini private sector moja kwa moja ameamua kuwekeza kujenga gati katika eneo hili la Mkinga ili aweze kurahisisha shughuli zake katika kiwanda cha saruji ambacho kitakuwa kikubwa zaidi kuliko viwanda vyote vilivyopo nchini na kitakuwa kinazalisha sana. Kwa hiyo, niombe sana wizara hii iharakishe kutoa vibali vyote vinavyohusika ili jambo hili litokee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wote tunatambua uwepo wa reli ya Tanga - Arusha kwenda mpaka Musoma, reli hii ilikuwa inazungumzwa mara kwa mara lakini sasa tunaomba pamoja na jitihada ambazo zimeanza kufufua reli ya zamani na nimpongeze sana Mkurugenzi wa Shirika la Reli, Ndugu Masanja Kadogosa kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya lakini tunaomba sasa kwenye huu mpango wa standard gauge uchukue hatua za haraka na sisi tuweze kuwa na reli hiyo ya kiwango cha kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wewe ni miongoni mwa mashahidi ambao wamepita barabara ya kutoka Mlalo kwenda Lushoto kilometa 45. Barabara hii tumekuwa tukiiombea fedha mara kwa mara katika mfuko wa barabara wa mkoa lakini mara nyingi tunakwamishwa na wenzetu wa Wakala wa Barabara Taifa (TANROADS). Engineer Mfugale ninafahamu kwamba upo katika majengo haya na unasikia, barabara hii ya Lushoto – Mlalo ni muhimu sana kwa shughuli za kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, shughuli kubwa ya uchumi ya wananchi wa Lushoto ni kilimo cha mboga mboga na matunda. Kwa hiyo, utagundua kwamba bidhaa hizi zinatakiwa zifike sokoni kwa wakati. Sasa kama hatuna barabara madhubuti maana yake ni kwamba wananchi wanapata hasara kwa sababu kwa kuwepo kwa barabara ambazo sio rafiki mazao yanaharibika yakiwa njiani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana tumeshaomba mara mbili kufanyiwa upembuzi yakinifu pamoja na detailed designing ya barabara hii na kila mara tukiomba wenyewe hawaleti mrejesho.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana safari hii barabara hii iingizwe katika mpango, najua mwaka huu tumeshachelewa lakini katika mwaka wa fedha unaokuja tafadhali sana kilometa hizi 45 tupate barabara ya kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la mawasiliano ya simu, katika Halmashauri ya Lushoto maeneo mengi tunashukuru kwamba simu zinapatikana. Changamoto ipo kwa sababu jiografia yetu ni milima baadhi ya maeneo ya mabondeni hakuna mawasiliano mazuri. Kwa hiyo, niwaombe tu wizara pamoja na wadau wote wanaohusika katika eneo hili waweze kuona kwamba namna gani tutaboresha mawasiliano ili wale ambao wapo katika maeneo ambayo yamefunikwa na vilima waweze kupata mawasiliano ambayo yataweza kufanya shughuli zao kwa ufanisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Tanga – Pangani mpaka Bagamoyo ni barabara ya siku nyingi sana na ni barabara ya kimkakati kwa maana ipo katika ramani ile ya Afrika Mashariki. Tumeanzia kutoka Horohoro kuja mpaka Tanga sasa tunataka kilometa 45 zile za Tanga – Pangani, lakini pamoja na kuunganisha na kipande cha Mwela – Sakula – Madanga – Saadan mpaka Bagamoyo ili tuweze kusaidia pia kuimarisha shughuli za kiuchumi pamoja na kutangaza mbuga zetu za Saadan kwa upande wa Bagamoyo na Tanga, lakini pia Mbuga ya Mkomazi ambayo ipo katika Mikoa ya Kilimanjaro na Tanga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la ATCL hasa suala la ndege kwamba watu wengi wanazungumzia ndege kama biashara ya chai kwamba asubuhi anapika maandazi na chai, jioni atapata faida, hili ni suala ambalo lina multiplier effect. Yapo mambo mbalimbali ambayo uwepo wa ATCL umesababisha hata bei ya ndege kushuka, tulikuwa tunaona hapa FastJet na ndege nyingine binafsi zilikua zinatoza gharama kubwa sana kutoka eneo moja kwenda lingine, lakini uwepo wa ATCL na bombardier hizi umesaidia hata ku-regulate bei kiasi kwamba sasa hivi wananchi wanatoka maeneo mbalimbali kwa gharama nafuu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia inasaidia kuondoa… kuna rasilimali moja ambayo Watanzania wanaisahau, rasilimali muda. Sisi shughuli zetu zinapoteza muda mwingi sana kwa sababu ya kutumia muda mrefu kusafiri, lakini uwepo wa usafiri wa anga unarahisisha mambo mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi ndugu zangu Wangoni hawa walizoea kushinda barabarani kutoka Dar es salaam kwenda mpaka Peramiho, lakini sasa hivi kwa uwepo wa bombardier ni saa moja anaruka kutoka Dar es Salaam kwenda Songea. Kwa hiyo, ninaomba sana tuimarishe shirika letu la ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika bajeti iliyopo mbele ya Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku moja Mheshimiwa Rais aliwahi kusema kwamba anadhani kuna baadhi ya Mawaziri hawamuelewi, lakini mimi nataka niseme kwamba inawezekana Mheshimiwa Tizeba na Mheshimiwa Mwijage ni miongoni mwa Mawaziri ambao hawamuelewi Mheshimiwa Rais anataka nini. Hili nalizungumza katika Tanzania ya viwanda pamoja na mapinduzi ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nitajikita katika zao la mkonge. Jana sindano zilikuwa za pamba leo zihamie kidogo kwenye upande wa mkonge. Mkoa wa Tanga peke yake una mashamba 27 ya mkonge, nchi nzima ya Tanzania inayo mashamba 53, mashamba 14 yapo katika Mikoa ya Pwani, Morogoro, Kilimanjaro na shamba moja liko Mkoa wa Arusha. Lakini mashamba haya mengi yametelekezwa na mpaka sasa ninavyozungumza hapa hata mkonge wa kusafirisha korosho na mazao mbalimbali tunaagiza duty kutoka nje ya nchi. Kwa hiyo, hapa utaona moja kwa moja kwamba kama tunakusudia kuwa na Tanzania ya viwanda bila kubainisha tunakusudia kuwa na viwanda vya namna gani, itakuwa hii ni hadithi ambayo itakwenda kukumbana na kifo muda si mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati nchi hii ilipopata uhuru Mwalimu Nyerere alianzisha maeneo mbalimbali na mazao mbalimbali ya kimkakati ya kukuza viwanda vya ndani, miongoni mwa viwanda hivyo vilikuwa ni viwanda ambavyo vinachakata mazao ya mkonge ikiwemo TANCORD, ambayo wakati huo iko Tanga, kuna Amboni Spinning, kuna Ubena Spinning iko Morogoro na TPM ambacho kiko Morogoro na mpaka sasa hivi ndichoo kiwanda pekee ambacho kinazalisha magunia ya mkonge. Kiwanda kingine kiko Moshi, Kiwanda cha Magunia cha Moshi. Sasa utaona kwamba sasa hivi mkonge unaozalishwa nchini kwa mujibu wa takwimu za Wizara ni tani 26,495 na mwaka huu wanataraji kwamba tutazalisha mpaka tani 43,127, lakini viwanda hivi havipati malighafi za kutosha kwa singa nyingi zinasafirishwa kwenda nje kama malighafi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo viwanda vya ndani vinakosa material na miongoni mwa viwanda vinavyokosa ni pamoja hii TPM ya Morogoro, hawa wana uwezo wa kuzalisha magunia mpaka milioni 10 kwa mwaka, lakini sasa hivi uwezo wao ni kuzalisha maguni milioni moja peke yake, na soko la ndani peke yake lina uwezo wa kupata magunia milioni tatu ambayo tunaweza tukasafirisha mazao mbalimbali ikiwemo korosho. Hapa tatizo lipo wazi kwamba tatizo ni kwamba ni kwenye kodi, viwanda hivi vinavyozalisha ndani vina kodi mbalimbali corporate tax, kuna VAT na kadhalika. Wanaoagiza duty kutoka nje hawalipi kodi kwa sababu hivi ni vifungashio ambavyo tumeridhia katika Common Market Protocol kwamba vifungashio vinavyokuja kufungasha mazao havitozwi kodi, matokeo yake ni kwamba tunakosa kodi kwa viwanda vya ndani kushindwa ku-supply bidhaa zao kupitia malighafi ambazo zinatoka na mazao ya ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana uliangalie hili kwa jicho la karibu sana kwamba ili kujenga uwezo wa viwanda vya ndani na kuelekea Tanzania ya viwanda ni lazima viwanda vinavyochakata mazao ya mkonge viweze kusimamiwa ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili nizungumzie suala la kilimo cha kahawa. Kahawa ilikuwa ni zao ambalo kule Kilimanjaro ni zao la wanaume, lakini sasa hivi wanaume wa Kilimanjaro wanashindana na wanawake kwenye ndizi, Baba Paroko pale ni shahidi kwamba hata wanawake wanaenda kutafuta purchasing power nje ya nchi kwa sababu wanaume wa Kilimanjaro pesa hazipo! Ni kwa sababu ya kilimo cha kahawa kimekufa na hapa tunahitaji tufanye utafiti, mabadiliko ya tabianchi sasa hivi yameikumba nchi yetu maeneo mengi kahawa haizalishwi tena. Kule Lushoto tulikuwa tunazalisha kahawa tani 300 mpaka tani 500 kwa mwaka, sasa imeshuka mpaka tani 150. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hesabu ziko sawa tu kwamba tulikuwa na shamba Kwehangala ambayo iko Jimbo la Bumbuli heka 450 sasa hivi shamba lile limekuwa ni viwanja vya kawaida tu watu wamerasimishiwa. Kwesimu heka 350 yote haya yalikuwa ni mashamba ya Usambara Coffee Growers sasa hivi hayatumiki tena kama mashamba ya kuzalisha kahawa. Kata sita Jimbo la Mlalo zinalima kahawa, Kata 14 Jimbo la Bumbuli zilikuwa zinalima kahawa, Kata nne Jimbo la Lushoto zilikuwa zinalima kahawa. Karibu Kata 25 ambazo zilikuwa zinalima kahawa sasa hivi hazilimi kahawa pia imeathiriwa na mabadiliko ya tabianchi. Kwa hiyo tunawaomba sana TaCRI wafanye utafiti ili kuweza kuboresha zao hili liweze kurudi katika kama ilivyokuwa zamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo Lushoto peke yake hata maeneo mengine ya Tarime walikuwa wanalima kahawa, Mbozi walikuwa wanalima kahawa, Ileje - Mbeya kule walikuwa wanalima kahawa sasa hivi uzalishaji wa kahawa umeshuka sana ni lazima mazao haya yaweze kurejeshwa kama ilivyokuwa zamani na yatarejeshwaje? Ukurasa wa 69 hapa tumeona kwamba Wizara inazungumzia kwamba TaCRI watakuwa moja kwa moja wanawajibika kwenye Wizara na miongoni mwa majukumu yao itakuwa ni kufanya utafiti pia kugawa mbegu na kutoa elimu kupitia Maafisa Ugani, sasa hili la Maafisa Ugani ndiyo ambalo mimi ningeshauri muanze nalo. Maafisa ugani walioko huko hawaelewi kabisa hata huko Usambara kulikuwa kuna kahawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, TaCRI pia wafanye utafiti kutokana na mabadiliko ya tabianchi ni aina gani ya mbegu ambayo inaweza ikawa bora kwa hali ya hewa iliyopo sasa. Sambamba na hilo ni lazima sasa AMCOS za kahawa pia ziboreshwe. Vile vyama vyetu vya Ushirika vya zamani, Usambara Cooperative, TARECU na kadhalika vimekufa, kwa hiyo tunahitaji sasa kutoa elimu mpya ya ushirika kwa wakulima hawa wa kahawa kwa kule Usambara ili kuongeza tija lakini kuongeza uzalishaji na sisi tuweze kushiriki katika uchumi huu wa Tanzania ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika kwamba Waziri mwenye dhamana bado sijaona kama ana jitihada maksudi za kufufua zao la kahawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na semina mbalimbali zinazoendelea lakini tunahitaji sasa hizi semina ziweondoke maofisini, zihamie kwenye maeneo kahawa inakozalishwa. Kumekuwa na miaka miwili ya kuendesha semina maofisini, sasa naomba uanze kwenda site, acha kuvaa suti ni wakati wa kuvaa gumboot na kuingia site kuhakikisha kwamba wakulima huko wanazalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni tozo kwenye nguo ambazo zinaingizwa nchini ili kunusuru viwanda vyetu vya nguo. Viwanda vya nguo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa mchango wangu mbele ya Bunge lako Tukufu. Kwanza nianze kuipongeza Wizara, Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nawapongeza Jeshi la Polisi; IGP Sirro pamoja na Makamishna na Makamanda wote katika ncni yetu. Tuko katika kipindi ambacho tunaona kabisa kwamba kuna transformation kubwa imefanyika. Matukio mengi tuliyozoea kuyaona hata katika ajali, lakini pia uhalifu kwa maana ya wizi katika mabenki, lakini pia ujambazi wa kutumia silaha, kwa kweli yamepungua kwa kiasi kikubwa sana. Sasa hatuwezi tukabeza hizi jitihada pamoja na kwamba changamoto zipo na sitarajii sisi kama viongozi tuamini kwamba changamoto zitakwisha kwa wakati mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunawapongeza na tunawaomba waongeze weledi katika kushughulikia matatizo mbalimbali hasa kwa maana ya kwamba sasa hivi kutokana na ukuaji wa teknolojia, uhalifu nao unakua. Tukisema tunajiunga katika kanda na uhalifu na wenyewe pia wanajiunga, wana kanda zao; tukisema tuko katika block fulani na wenyewe pia uhalifu unazidi kuongezeka. Kwa hiyo, tuhakikishe kwamba tunakuwa na jeshi lenye weledi na kuhakikisha kwamba mambo yanakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la kushauri kwa sababu ndiyo kazi yetu ya msingi kama Wabunge, kushauri na kuisimamia Serikali. Katika eneo la ushauri nianze na Jeshi la Zimamoto. Jeshi la Zimamoto bado liko karne nyuma zaidi ya karne tuliyokuwanayo. Bado vifaa wanavyotumia kuzima moto haviendani na teknolojia ilivyokua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona sasa hivi tunayo majengo marefu sana hasa katika Majiji; Jiji la Dar es Salaam, Mwanza na Arusha ambako kuna majengo marefu, lakini utashangaa bado Zimamoto wana magari ambayo hayawezi kuzima moto hata ambao uko ghorofa ya pili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe rai kwamba kikosi hiki cha Zimamoto kiboreshwe, kiwe na vifaa vya kisasa ambavyo vinaendana na wakati tulionao. Pia, katika Jiji kama la Dar es Salaam ambalo linazidi kupanuka, hatutarajii kuwaona Zimamoto bado wakiwa pale pale walipokuwa tangu Serikali ya Awamu ya Kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunatarajia kuwaona Zimamoto wakiwa na vituo labda maeneo kama Mbezi, Mbagala, Kigamboni, Bunju na maeneo mbalimbali ambayo hata ikihitajika huduma ile gari linafika kwa wakati. Sasa hivi bado wako maeneo yale ya kule Mjini Ilala ambapo hata akiitwa kuzima moto Mbagala, anatumia hata saa mbili kufika huko na hiyo tija haiwezi ikaonekana. Kwa hiyo, suala la msingi kwanza tuboreshe hii huduma kwa maana ya kuwapa vifaa vinavyoendana na wakati, lakini pia wajaribu ku-decentralize hii huduma kuelekea huko ambako makazi ya watu yapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni la breakdown. Unapopata ajali katika Jiji la Dar es Salaam wanatumia breakdown, hizi Land Rover za zamani. Zile Land Rover sidhani kwamba hata zinalipa kodi kwa maana ile ni biashara, lakini sidhani kama wako katika mfumo rasmi kwamba wanalipa hata mapato ya Serikali. Kwa sababu umbali ambao hauzidi kilometa moja wanachukua Sh.80,000/= kuvuta gari ambalo limeharibika ama lime-park eneo ambalo haistahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wasiwasi wangu hapa ni kwamba je, kwa vijana hawa tuliokuwa nao kama Mawaziri, Mheshimiwa Mwigulu, Mheshimiwa Engineer Masauni, bado Taifa hili tuna haja ya kuwa na breakdown aina ya Land Rover zile kweli? Yaani Land Rover ile ikaanze kuvuta BMW ya shilingi milioni 200 inavutwa na gari ambalo thamani yake haifiki hata milioni 12?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani hapa kuna tatizo. Lazima tuje na ubunifu kwa sababu hii wanaifanya kama biashara. Basi tujaribu kuitangaza hii biashara watu wenye uwezo watuletee breakdown za kisasa ambazo unapakia gari juu ya gari. Hili tuliangalie kwa makini sana. Breakdown hizi, zenyewe zinaharibu hayo magari wakati wa kuyapakia au wakati wa kuyavuta. Wanatumia minyororo ambayo ni teknolojia ya zamani sana kiasi kwamba utakapoona lile gari linavyovutwa, japokuwa wewe ni binadamu, lakini unaumia kwamba hapa kitu kinachofanyika siyo sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba na eneo hilo waliangalie, wao ni vijana lazima walete ubunifu kwenye hii Wizara. Tumeona Mheshimiwa Augustine Mrema aliwahi kukaa kwenye Wizara hii na akatengeneza jina, nao tunatarajia wafanye vitu ambavyo vinaonekana ili viweze kuwatangaza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, nizungumzie suala la Gereza la Kilimo, Mnaro. Nimeshamwambia Mheshimiwa Waziri mara kadhaa kwamba Gereza hili ni miongoni mwa Magereza machache ya kilimo katika nchi hii na kule kuna scheme za umwagiliaji, lakini Gereza hili ni chakavu kwa sababu ni la siku nyingi mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu Serikali ya Awamu ya Kwanza nadhani mwaka 1973 ndiyo Gereza hili limejengwa. Kwa hiyo, wanahitaji kuboresha miundombinu ya Gereza. Pia, nimewahi kumwambia Mheshimiwa Waziri kwamba ikama ya wafungwa pale ni ndogo. Hili ni Gereza la Kilimo, tunahitaji tuone wanalima. Tunahitaji tuone wanazalisha; ni kilimo na ufugaji unaendelea pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Gereza lina uwezo wa kuchukua wafungwa mpaka 100, lakini walioko pale ni wafungwa 38. Siku moja Mheshimiwa Matiko hapa alisema kuna msongamano Gereza la Tarime, Rorya, nikamwambia sasa si awahamishie kule watusaidie kwenye shughuli za kilimo Lushoto? Hii iwe tu wazi kwamba kwa nini wafungwa ni wachache, ni kwa sababu watu wa Lushoto sio watu wa matukio. Kwa hiyo, ndiyo maana kule Magerezani huwezi hata kuwakuta Wasambaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni Kituo cha Polisi cha Mlalo. Kuna wakati kulitokea suala hili la ugaidi katika maeneo ya Mapango ya Amboni na wale watu walifika katika Milima ya Usambara. Kituo cha Polisi Mlalo kilikuwa hakijajenga amari, kwa hiyo, hatukuwa na sehemu ya kuhifadhia silaha. Sasa tumeshajenga tunaomba kikaguliwe...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha maelezo yangu binafsi kuhusu hoja iliyopo mbele ya Bunge Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, takriban mwaka mzima nimekuwa nikiomba Jeshi la Polisi likague Kituo cha Polisi Mlalo ili baada ya kukaguliwa tuweze kupata silaha. Nimejaribu kufuatilia jambo hili kwa muda mrefu lakini Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya na Mkoa hakuna hatua zozote zilizochukuliwa. Niombe sasa Wizara, jambo hili lifanyike kwa wakati ili kuimarisha ulinzi na usalama katika eneo letu la Wilaya ya Lushoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Mlalo lenye Tarafa tatu, Kata 18, Vijiji 78 na Vitongoji 600 lina vituo viwili vya Polisi, lakini kwa bahati mbaya vituo hivyo havina silaha. Ni jambo baya sana hasa ikizingatiwa kuwa Jimbo lenyewe liko katika mpaka na nchi jirani ya Kenya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Gereza la Kilimo Mng’aro limechakaa sana kwa sababu limejengwa wakati wa Serikali ya Awamu ya Kwanza. Pia, gereza hili lina upungufu wa wafungwa chini ya ikama. Uwezo wa gereza ni kuweza kuweka wafungwa 100 lakini kwa sasa wafungwa wapo 38 hivyo kulifanya gereza hili kufanya kazi zake chini ya ufanisi hasa ukizingatia ni gereza la kilimo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa mchango wangu katika Wizara ya TAMISEMI kuhusu elimu. Katika halmashauri ya Lushoto na Bumbuli kuna takribani shule za msingi 168 ambazo ni kiasi kikubwa sana. Tunao uhaba mkubwa wa vyumba vya madarasa vipatavyo 228 kwa Halmashauri ya Lushoto, lakini pia kuna uhaba mkubwa wa Walimu wapatao 836. Hivyo kukosa ikama bora kwa mujibu wa taratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Lushoto na Tanga kwa jumla kuna shule nyingi sana kulinganisha na mikoa mingine. Wakati Mkoa mzima wa Tanga una shule za msingi 1,032 mikoa kama Simiyu zipo 571, Katavi 177 ambao ni zaidi ya Wilaya ya Lushoto kwa shule tisa tu, Songwe 406, Njombe 499, Lindi 502 utaona uwiano huu hauwezi kuleta tija na ulinganishi kwa sababu mamlaka za usimamizi zinapata mzigo mkubwa kusimamia, itapendeza kama Mkoa wa Tanga utapewa uangalizi maalum ili kusimamia elimu kutokana na ukubwa huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utawala; lengo la ugatuzi wa Serikali za Mitaa ni kuboresha utawala bora na kupeleka madaraka karibu na watu. Mkoa wa Tanga ni mkoa pekee wenye halmashauri nyingi ambazo ni 11. Hivyo kuhitaji muda, rasilimali fedha na watu ili kusukuma maendeleo. Halmashauri 11 wilaya nane (8) na majimbo 12 ni mzigo mkubwa hivyo kuhitaji kutazamwa kwa jicho la kipekee ili kuboresha maeneo ya utawala na kuleta utawala bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mikoa kama ya Geita ina halmashauri sita (6), Katavi tano ()5, Iringa tano (5), Lindi sita (6), Rukwa sita (6) utaona kwamba Mkoa wa Tanga sasa unahitaji angalau kugawanywa na kupata mkoa wa zaidi. Wilaya ya Muheza, Kilindi na Korogwe ni kubwa mno kuweza kuzalisha wilaya ya ziada. Hali kadhalika Wilaya ya Lushoto inaweza kupatiwa halmashauri tatu yaani Mlalo, Lushoto na Bumbuli kwa sababu takribani robo ya wakazi wa Mkoa wa Tanga wanaishi Lushoto, idadi kubwa ya watu huhitaji usimamizi wa huduma za kijamii ni suala linalohitaji jicho la karibu kutafakari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, performance based audit, napendekeza ufanyike ukaguzi mahsusi juu ya utendaji wa Maafisa Ugani (Extension Officers) katika halmashauri zetu nchini. Watumishi hawa wanaonekana wenye kuzurura hawajulikani wanafanya kazi gani, hivyo kuwa mzigo kwa Taifa kuwalipa mishahara wakati hakuna tija yoyote inayopatikana kutokana na uwepo wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA; Mamlaka hii mpya iishie pale ambapo halmashauri zimeishia, hata hivyo shughuli zao ziendane na mpango wa Taifa wa mwaka mmoja na miaka mitano ili kuleta uwiano wa usawa kuweza kwenda pamoja na sekta nyingine (mfano lengo la usambazaji umeme kijijini (REA) ni ifikapo 2020/2021 ifike mwisho. Je, kwa vijiji visivyokuwa na barabara TARURA wanahusianishaje zoezi hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika halmashauri ya Lushoto hakuna hata gulio moja ambalo lina miundombinu ya vyoo wala vizimba vya kuhifadhia bidhaa, hivyo kuleta kero kwa wananchi na kusababisha magonjwa ya milipuko kwa nyakati tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa mchango wangu wa shukrani za dhati kwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama na watendaji wake kwa kuridhia na kuanzisha ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Mtae - Mlalo, Lushoto. Hii ni hatua muhimu kwa ujenzi na utoaji wa haki katika Mhimili huu. Nafarijika sana kuona jambo hili limekamilika na sasa ujenzi upo katika hatua za upauzi na usafi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mahakama hii itahudumia kata sita za Tarafa ya Mtae na kata za jirani na itapunguza kwa kiasi kikubwa tatizo la wananchi kujichukulia sheria mkononi kwa kukosa sehemu sahihi za kutafsiri haki katika ngazi hii ya msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia kutoka katika Idara ya Mahakama kupitia Chuo cha Sheria Lushoto tuweze kupata msaada wa kisheria katika maeneo yetu ya uwakilishi. Tunaamini hili litasaidia sana katika kuwapa uwezo vijana wetu wanaosoma katika chuo hiki, lakini pia kuwasaidia wananchi kwenye mashauri mbalimbali katika maisha yao ya kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Law School; kumekuwa na uhitaji mkubwa wa wanafunzi waliomaliza katika vyuo mbalimbali vya hapa nchini katika Shahada ya Sheria, hata hivyo, linapokuja suala la kupata ujuzi wa elimu ya Uwakili Chuo pekee kinachotoa taaluma hii ni University of Dar es Salaam. Tunaomba Mtendaji Mkuu wa Mahakama kuona namna bora ya kuweza kupanua wigo ili Taaluma hii ya Uwakili iweze kupatikana katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho la ushauri ni kuhusu azma ya mahakama kutaka kujenga mahakama kila kata ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Naomba kushauri jambo hili lipitiwe upya na lifanyiwe utafii wa kina kwani kwa maoni yangu kushusha mhimili wa Mahakama katika ngazi ya kata itakuwa ni mzigo na gharama kubwa kwa mhimili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, napendekeza kwamba ni bora mahakama hizi zikaishia katika ngazi ya tarafa. Yapo maeneo ikiwemo Lushoto eneo la tarafa ni rafiki kufikika kwa urahisi hivyo kutokuwa na uhitaji wa kuweka mahakama katika ngazi ya kila kata. Tunazo tarafa tano zinazounda Halmashauri ya Lushoto, hivyo ni vyema angalau kila tarafa ikapata Mahakama ya Mwanzo ili kuleta ufanisi katika kutafsiri sheria na kutoa haki. Katika Halmashauri ya Bumbuli, Lushoto kwenyewe zipo tarafa tatu lakini kuna Mahakama ya Soni na Bumbuli pekee, Tarafa ya Tamota na Mgwashi hazina mahakama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kupongeza mhimili huu wa Mahakama lakini pia Viongozi Watendaji Wakuu wa Wizara ya Katiba na Sheria kwa utendaji wao na kuipa heshima Wizara hii, hasa katika eneo hili la usimamizi na utoaji wa haki. Nawasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia katika Wizara hii mpya kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nami niwapongeze Mawaziri wote wanaohudumu katika Wizara hii. Pia nimpongeze sana Katibu Mkuu Profesa Msanjila kwa kazi kubwa ambayo anaifanya na nipongeze dhamira njema kabisa ya Mheshimiwa Rais kutenganisha Wizara hii kutoka Nishati na kuifanya sasa kuwa Wizara kamili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na suala hili la Corporate Social Responsibilities. Tumeona miradi mingi sana ya madini bado haijaweza kuleta manufaa kwa wananchi wanaozunguka maeneo ambayo madini yanatoka. Hapa tunaona tatizo liko kwenye sheria. Sera ya Madini iko wazi kabisa inaeleza umuhimu wa makampuni ambayo yanachimba madini katika maeneo husika kuweza kusaidia katika jamii zile zinazozunguka, lakini Sheria yetu ya Madini iko kimya katika jambo hili. Nataka Waziri mwenye dhamana na Wizara kwa ujumla waje na majibu yanayoonesha namna sera na sheria zinavyoweza kuungana na kuweza kuleta harmonization kiasi kwamba wananchi wanaotoka katika maeneo ambayo madini yanachimbwa waweze kufaidika na huduma hizi za kijamii na tusiachwe na mahandaki kama walivyofanya Mgodi wa Resolute kule Nzega. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napenda nilizungumzie ni suala la madini ya ya madini ya bauxite ambayo yanapatikana katika Milima ya Usambara, Wilaya ya Lushoto. Tunayo madini mengi sana kule yanapatikana katika Kata za Malindi, Magamba, Soni eneo la Shashui pia na eneo la Makanya kule Lushoto. Madini haya inawezekana kwa kutofahamu tunayatumia kama sehemu ya kifusi barabarani lakini kwa kuwa sasa Wizara hii ina Mawaziri wa kutosha ambao wanaweza wakatembelea maeneo tofauti tofauti niwasihi sana wafike Lushoto waweze kuja kutoa elimu kwa wananchi wa Lushoto ili pamoja na rasilimali nyingine ambazo tunazo basi tuanze kufaidika na rasilimali hii ya madini ya bauxite ambayo ni madini muhimu sana na ambayo yana thamani sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, wapo wachimbaji wachache ambao wanachimba madini haya lakini bado katika Halmashauri hatujafaidika kwa kiasi kikubwa na upatikanaji wa rasilimali hii ya madini. Kwa sababu wanayachukua katika malori makubwa na wengi wanapeleka katika nchi jirani ya Kenya, naamini kwamba hata Serikali pia inakosa mapato. Kwa hiyo, pamoja na elimu hiyo watakayokuja nayo lakini watutafutie wawakezaji ambao wanaweza wakaja wakayachenjulia kule Lushoto ili angalau kile ambacho ni stahiki wachukue na yale mabaki yetu basi tubaki nayo tuendelee kutengenezea barabara zetu kwa sababu pia Lushoto tuna uhaba mkubwa wa ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la Tume ile ya Makinikia ambayo iliundwa, lakini nimejaribu kupitia katika kitabu sijaona mahali popote zile dola milioni 300 zimeandikwa. Sasa namuomba sana Waziri mwenye dhamana atakapokuja kujibu hapa aniangalizie kwamba zile dola milioni 300 ziko katika eneo lipi. Natambua kwamba Mheshimiwa Prosefa Palamagamba Kabudi ndiyo alikuwa mkubwa wa ile Timu ya Maridhiano, hivyo hili jambo nalo tungeweza kupata majibu lingetusaidia sana kuondoa sintofahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nizungumzie suala la madini ya urani ambayo yanapatikana katika Hifadhi ya Taifa ya Selous haswa katika eneo la Wilaya ya Namtumbo. Zipo tetesi mitaani zimeenea kwamba yale madini yanachimbwa kwa siri. Ningependa kujua kutoka Serikalini kwamba jambo hili lina ukweli kiasi gani kwa sababu ile ni rasilimali yetu wote na hata kama iko ndani ya hifadhi, bado hifadhi hizi zipo kwa mujibu wa sheria na sheria hizi tunazitunga sisi. Yapo mambo yanaweza yakafanyika na tunaweza tukapata muafaka wa eneo hili lakini siyo vizuri kama Wabunge tukaendelea kupata maneno haya kwa siri kwamba urani inachimbwa katika Hifadhi ya Selous haswa katika eneo la Wilaya ya Namtumbo, ingependeza sana kama tungepata majibu kwa uhakika zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo pia ni pongezi kwa Jeshi letu la Ulinzi ni suala la ujenzi wa ukuta katika machimbo ya Mererani, kila Mbunge amesimama hapa amelipongeza ni jambo nzuri. Nataka niseme pamoja na dhamira nzuri ya Rais na jitihada hizo ambazo Jeshi wamefanya, bado kuna jitihada za makusudi zinatakiwa ziangaliwe katika eneo linalogusa kodi, ni kwa nini madini haya yanatoroshwa kupitia nchi jirani ya Kenya, hapa lazima Wizara iende mbali zaidi kulitafutia ufumbuzi. Kujenga ukuta ni jambo moja lakini kutengeneza sera na miongozo mbalimbali inayotoa incentive nzuri kwa wasafirishaji hawa wa madini inaweza ikapendeza zaidi ili kuwavutia wasiwe na hamasa ya kupitia nchi jirani katika mipaka ambayo siyo rasmi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo liendane pia na madini katika Kanda ya Ziwa kwamba madini mengi yanatoroshwa kupitia Kenya. Wafanyabiashara wa Kenya wanawaambiwa kabisa hawa wafanyabiashara wadogo wadogo bwana wewe ukishafikisha hapa tayari ni suala
dogo yanakwenda huko duniani. Kwa hiyo, tuziangalie pia sheria zetu haswa katika maeneo ya kodi kwamba kodi zetu ni rafiki kiasi gani kwa wachimbaji hawa wadogo wadogo lakini pia wachimbaji wakubwa ili ziweze kutoa nafasi kwa kuruhusu mambo haya kufanyika ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine kwa ujumla ambalo limezungumzwa ni STAMICO. STAMICO kweli ni janga kama ambavyo Wabunge wengi wamesema. Katika vitu ambavyo unawea ukawashangaa STAMICO kwamba pia wameshindwa ni katika hata migodi hii ya chumvi. Kutengeneza chumvi ni kazi rahisi sana, ni kuchukua maji ya bahari na kuyaweka katika mabwawa na baada muda tayari chumvi imetengenezwa. Hivi ninavyozungumza Mgodi ule wa Salt Mining kule Saadani umekufa, kule Uvinza umekufa, lakini STAMICO hawa ndiyo ambao wametufikisha hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Mheshimiwa dada yangu Angellah haya maoni ya Wabunge hebu yachukulie kwa kina, sidhani kwamba ni vema sana kufufua hili Shirika la STAMICO. Tungekwenda mbali zaidi tukatafuta solution nzuri ili angalau tusije tukaingia tena kwenye mtego huu ambao umetufikisha hapa tulipo. Hii migodi midogo midogo ya kokoto na chumvi kama imewashinda sidhani bado tunaweza tukawapa jukumu kubwa hili la haya madini ya uranium, nickel na madini mbalimbali ambayo yanaendelea kugunduliwa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe rai kwako Waziri kwamba alichukue jambo hili kama ni angalizo kwa Waheshimiwa Wabunge na kama anadhani kuna namna pekee ya kutushawishi basi siyo vibaya akatungenezea semina na hao watu wa STAMICO tukajadili na tukachakata na tukajiridhisha kwamba kweli wanaweza wakabadilika. Kama walivyo sasa naamini kabisa kwamba hili ni janga na tusingependa hela za Serikali ziendelee tena kupotea katika shirika hili.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Kwanza naomba nichukue nafasi hii kwa dhati kabisa kuzipongeza Kamati zote mbili kwa namna ambavyo wamechambua na kuleta ripoti zao ambazo ziko mbele ya Bunge lako Tukufu. Kipekee kabisa, nimesimama mbele ya Bunge lako Tukufu kutoa shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kupitia Waziri wa Ardhi, Mheshimiwa Lukuvi, pamoja Naibu Waziri Mheshimiwa Mabula na sisi kule Mlalo tulikuwa na shamba la Mnazi Sisal Estate ambalo lilikuwa linamilikiwa na Kampuni ya Lemashi Enterprises, wawekezaji hawa kutoka Kenya, shamba hili lilitelekezwa kwa muda mrefu sana takribani miaka 15.

Mheshimiwa Spika, wewe ni mkongwe humu kulikuwa na Mbunge wa Jimbo la Mlalo, Mheshimiwa Charles Kagonji ndiye mtu wa kwanza kupigania shamba hili kurudishwa kwa wananchi. Kwa kipindi chake chote cha Ubunge wa Jimbo la Mlalo alishindwa. Hali kadhalika akaingia Mheshimiwa Brig. Ngwilizi naye amepambana lakini Mkenya yule pamoja na mianya mbalimbali ambayo alikuwa anaitumia kupitia watumishi ambao siyo waaminifu katika Halmashauri, Mkoa na Wizara kwa wakati huo mambo hayakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kipekee natoa pongezi hizi kwa Mheshimiwa Lukuvi, Waziri wa Ardhi, kwa kazi kubwa sana ambayo amefanya ndani ya kipindi cha mwaka mmoja na nusu tulifanikiwa kurudisha shamba lile mikononi mwa Halmashauri ya Lushoto. Hivi navyozungumza tayari tumeweka mwekezaji mwingine, sisi kwa bahati nzuri tumechukua shamba kwa mwekezaji na tukatafuta mwekezaji mwingine na tumepata mwekezaji mpya amelipa kodi zote stahiki Serikali zaidi ya shilingi bilioni 2.8 na ameshaanza kuwekeza zaidi ya trekta tano mpya ziko ndani ya shamba, ameweka excavator na kila aina ya mashine. Mashine zote ambazo zilikuwa zina process na kuchakata mkonge kwa maana ya kuanzia kukata mpaka mwishoni kutengeneza mchakato wa brushing amefufua mashine zote zile za Kijerumani ambazo zilikuwepo tangu miaka ya 1936. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, natoa pongezi hizi kwa sababu sasa wananchi wote wanaozungukwa na shamba lile ambalo linazunguka takribani kata tatu wamepata ajira za kudumu zaidi ya wananchi 330 lakini ambao wapo wamepata ajira siyo za kudumu za kwenda kukata mkonge wengine kwenda kupalilia kulima na kadhalika. Kwa hiyo, unaweza ukaona kwamba ni kwa kiasi gani uchumi wa Halmashauri ya Lushoto ulikuwa umelala kwa kipindi kirefu kwa sababu tu ya kumpata mwekezaji ambaye hakuwa sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba hili nilizungumze kwa uwazi sana, mashamba ya mkonge tunapoyazungumza ni makubwa sana, kwa mfano hili Shamba la Mnazi ni takribani heka 4,100 lakini mwekezaji huyu alikuwa amewekeza katika heka 500 tu. Kwa hiyo, shamba lingine lote likageuka pori ambalo limekuwa makazi ya nyoka baadhi ya wafugaji kulitumia kwa ajili ya shughuli ya ufugaji. Hata haya mashamba tunayoyazungumza katika Mkoa wa Tanga kwa maana ya Wilaya ya Korongwe na Muheza ambapo bado kuna mashambapori mengi unakuta hawa wawekezaji wanalima katika upande wa barabara. Kwa hiyo, unapopita huku barabarani unaona kuna shughuli zinaendelea lakini kimsingi zile shughuli ni kiini macho wanaweka tu hekari za mwanzoni barabarani lakini huko pembezoni ni machaka makubwa sana ambayo yamegeuka kuwa msitu. Kwa hiyo, nitoe rai sana kwa Wizara kwamba iendelee bado tunayo mashamba zaidi ya 36 ambayo hayaendelezwi katika Mkoa wa Tanga.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia katika Wizara hii ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Kwa masikitiko makubwa nimepitia hotuba ya Wizara hii lakini sikuona mahali ambapo wamepongeza jitihada za wananchi wa Kata ya Mtae, Tarafa ya Mtae Wilaya ya Lushoto ambao kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo wameweza kukarabati jengo la Serikali ya kijiji na kuwa Kituo Kidogo cha Polisi katika Tarafa. Wananchi kwa kushirikiana na Mbuge pamoja na Kamanda wa Polisi Mkoa na Wilaya kwa pamoja kituo kimeanza kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, aidha, vilevile kwa kuzingatia utawala bora na utawala unaozingatia sheria, wananchi wa Mtae wamewapatia nyumba ya kuishi familia mbili za Askari kati ya watatu waliopo katika eneo la kituo hiki. Napenda kuona Wizara hiii ikitoa japo neno la shukrani kwa wananchi hata kama ni wajibu wao katika kujiletea maendeleo.

Mheshimiwa Spika, mimi Mbunge wa Mlalo na timu yangu kupitia Mfuko wa Jimbo tumeweza kuchimba kisima katika Gereza la Kilimo Mng’aro ambalo lina uhaba mkubwa wa maji. Tumeweza kutumia takribani shilingi milioni 20 kuwawekea kisima kirefu pamoja na tanki la kuhifadhia maji lenye ujazo wa lita 5000. Tunatamani kuona Wizara ikishirikiana nasi katika kuboresha miundombinu ya Gereza hili ambalo limejengwa kwa tope na miti. Tunaomba Wizara itembelee Gereza hili la Kilimo cha Mpunga na Mbogamboga lenye uwezo wa kulisha wafungwa walioko katika Magereza ya Mkoa wa Tanga kwa asilimia 75.

Mheshimiwa Spika, bado jengo la Polisi katika Makao Makuu lipo katika hali mbaya na ujenzi wa jengo jipya ulisimama kwa muda mrefu. Tungependa kuona ni kwa kiasi gani jambo hili linafikia mwisho.

Mheshimiwa Spika, mwisho, napenda pia kushauri kuhusu Katibu Mkuu wa Wizara hii kusimamia mafungu mengi, hivyo kushindwa kuleta ufanisi katika Wizara hii. Afisa Masuuli wa Wizara hii ambaye ni Katibu Mkuu anasimamia Idara ya Uhamiaji, Idara za Zimamoto, Jeshi la Magereza, Jeshi la Polisi pamoja na NIDA.

Mheshimiwa Spika, naomba niwasilishe haya kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Mlalo, basi angalau Wizara hii iweze kuwaunga mkono katika jukumu hili zito la ulinzi wa raia na mali zao.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa nafasi hii, nami niweze kushiriki katika hoja iliyopo katika Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimefarijika sana kuona Mheshimiwa Waziri wa Fedha yupo hapa, lakini Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji yupo pale kwa sababu mambo ambayo nakusudia kuyazungumza yanagusa sana katika maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumza uchumi wa viwanda kwa maana ya kulipeleka taifa kwenye uchumi wa kati ni lazima tuwe na models ambazo zinatupeleka huko. Hatuwezi tu kuwa na model ya viwanda ambavyo hatuelewi ni viwanda vya namna gani vitatupeleka huko. Kwa maoni yangu nadhani kwa kuwa nchi hii asilimia zaidi ya 70, 75 ni wakulima basi model nzuri itakuwa ni ya viwanda ambavyo vinahusianisha au vinajifungamanisha na kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ulizuka mjadala wa kuhusu matumizi ya ndege, lakini inawezekana labda tu ni kwa sababu vitu hivi sisi kama Watanzania tumechelewa kuvitumia na ndiyo maana wakati mwingine hata tukiona mizigo inapanda ndege tunaona kama ni israafu, lakini nataka nikwambie kwamba sehemu mojawapo itakayosaidia kukuza Sekta ya Kilimo ni kuwepo kwa ndege ambazo zinabeba mizigo, hasa mazao haya ambayo ni perishable. Tunapozungumza mazao kama maparachichi, mazao ya kilimo ya matunda, mbogamboga, green beans, French beans, broccoli, coriander, lakini pia na mazao ya maua, haya yanahitaji ndege ili yaweze kufika kwenye masoko kwa haraka sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tatizo kubwa katika nchi yetu ni kwamba hatuna ndege nyingi za mizigo zinazotua katika viwanja vyetu. Sio katika Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam, sio Kilimanjaro wala sio kule Songwe, kidogo kwa watu wa Kaskazini wanatumia Uwanja wa Ndege wa Nairobi kwa kupeleka maua na bidhaa hizi za matunda na mbogamboga.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niiombe sana Wizara ya Fedha iangalie hapa kwa sababu kuna tatizo moja. Kwanza ni airport charges zetu ziko juu, lakini pia landing fee ya kutua katika viwanja vyetu ziko juu sana. Sambamba na hilo, wakiweza kuangalia pia mafuta ya ndege kwamba angalau yasiwe na tozo nyingi, najua yako zero lakini ingekwenda mbali zaidi kwamba angalau tuyapate kwa bei ya nafuu sana ili yavutie ndege ambazo ni za mizigo ziweze kutua katika viwanja vyetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi hapa nilimwona Mheshimiwa Waziri wa Fedha yuko kule Rungwe, nadhani alikuwa na Waziri wa Uwekezaji, wakiwa wanaangalia uwezekano wa kusafirisha maparachichi kupitia Uwanja wa Songwe. Sasa kama tutakuwa na ndege za mizigo zinazoweza kutua katika viwanja vyetu hivi maana yake hii itaongeza thamani ya uzalishaji kwa wakulima wetu. Kwa hiyo hili naomba tulitazame sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili katika eneo hilohilo la viwanda, hasa vinavyofungamanishwa na kilimo, ni suala zima la vifungashio. Tanzania bado tuna tatizo la vifungashio, ndiyo maana unakuta maparachichi yanayolimwa Njombe, Iringa na kwingineko yanapelekwa Nairobi yakifika kule yanafungwa katika vifungashio ambavyo ni bora na yanapelekwa kwenye masoko ya Ulaya na Marekani ambapo wanauza kwa bei kubwa zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana Wizara hii iangalie eneo hili, kwamba tutafute wawekezaji ambao watawekeza katika viwanda vya vifungashio ili mazao yetu yanapotoka moja kwa moja kutoka Tanzania yawe yako katika ule ubora ambao unaweza kuyafanya yakashindana kimataifa. Unaweza ukaona mfano maparachichi ambayo tunauziwa hapa Tanzania kwa shilingi labda 1,400, huko kwenye masoko ya dunia inafika mpaka dola kumi, kwa hiyo utaona kwamba ni kiasi gani cha pesa ambacho tunapoteza kwa sababu tu hatuyaandai vizuri wala hatuyawekei mpango madhubuti wa ku-process katika ubora ambao unatakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine linalojifungamanisha pia katika kilimo ni suala zima la majokofu ama hizi cold boxes za kusafirishia haya mazao. Mazao ya mbogamboga, matunda, yanahitaji kupata ubaridi wa kutosha kutoka kule kwenye mashamba kwenda katika hivyo viwanja tunavyozungumza au kwenda katika masoko. Katika eneo hili unakuta kwamba wakulima hawawezi kuyasafirisha yakiwa katika hali ya ubaridi. Kwa hiyo niiombe sana Wizara ya Fedha wakati tunatoa misamaha kwenye vifaa vingine vinavyosaidia kwenye uwekezaji katika kilimo kama matrekta na pembejeo nyingine, hebu tuangalie na hili suala la cooler boxes na cold rooms ambazo zinasaidia sana wakati wa usafirishaji wa haya mazao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wale ambao wamepata bahati ya kuwa na miradi ile ya MIVARF katika maeneo yao watakuwa ni mashahidi kwamba MIVARF wameweza kujenga cold rooms ambazo zinaweza kubeba mazao hata kwa tani 15 mpaka 20, lakini tatizo lipo kwenye kuyatoa kule kwenye vijiji kuyaleta kwenye vile vituo ambavyo ni post harvest centers, pale lazima wananchi wetu waweze kupata incentive kwenye kodi ili waweze kuwa na hivi vifaa na waweze kuongeza uzalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kilimo bado tuna uwezo sasa wa kuhakikisha kwamba tunapata viwanda ambavyo vinakwenda kuongeza thamani kwa maana ya kupata pembejeo na madawa pamoja na viuadudu katika mazingira yetu hapahapa, lakini pia sambamba na uzalishaji wa mbegu. Tatizo la mbegu limekuwa ni tatizo kubwa sana kwa sababu mbegu zetu nyingi zinatafitiwa kutoka nje. Kwa hiyo niombe sana Serikali iongeze pesa katika vituo vyetu vya utafiti ili kutokana na mabadiliko haya ya tabianchi ambayo yameendelea kuikumba nchi yetu wananchi waendelee kubadilisha aina ya mazao kwa sababu bado mpaka sasa hivi wananchi wengi wanapanda mazao mengi kwa mazoea lakini kiuhalisia kwa kweli hayana ubora ule ambao unaweza ukashindana katika soko.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nataka kulizungumzia ni la madawa; juzi Kamati ya PAC tulitembelea Bohari Kuu ya Madawa (MSD) na tukakutana na wenzetu wa Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC), karibu nchi 16 walikuja pale kufunga mkataba na MSD ili iweze kuagiza madawa kwa niaba ya hizo nchi 16 na kufanya deliveries.

Hata hivyo, changamoto kubwa ni kwamba hapa ndani uwezo wa viwanda vya ndani katika soko la madawa ni asilimia nne peke yake na bado napo kuna tatizo la kwamba hatuna viwanda vya kutosha vya madawa, hata dripu tunaagiza nadhani kutoka Uganda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimwombe sana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana hii ya uwekezaji kwamba sasa tujaribu kupata incentive nzuri kwa ajili ya kuhamasisha viwanda vya madawa vijengwe hapa nchini ili tuweze sasa kupata hili soko la Kusini mwa Afrika. Kama nchi 16 leo zinachukua madawa kutoka Bohari Kuu ya Madawa maana yake ni kwamba hayo madawa yangekuwa yanazalishwa hapa nchini moja kwa moja hii ingekuwa ni faida kwetu, lakini leo MSD anageuka tu kama agent wa kuagiza kwa makampuni mengine ya nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kabisa ni kwa Bandari ya Dar es Salaam; bado Bandari yetu na Mamlaka ya Mapato Tanzania sio rafiki sana kwa uwekezaji, kuna mambo mengi ambayo yanafanyika pale kila siku tunarudi nyuma, kila siku wanaanzisha mambo mapya. Kwa hiyo tunapozungumza suala zima la uwekezaji ni lazima Serikali nzima iwe inazungumza, Wizara zote zizungumze na kuwe na connection kwamba mizigo inapotoka nje inapofika katika bandari zetu ichukue muda mfupi na iweze kwenda kule ambako inakusudiwa. Kama tutakuwa tuna bandari ambayo inachelewesha mizigo, basi hata ile dhana nzima ya kwamba nchi yetu inavutia wawekezaji itakuwa haifanyi kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa muda wako. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii ili niweze kutoa mchango wangu kwenye hoja iliyopo mbele ya Bunge letu Tukufu.

Mheshimiwa Spika, ningependa kuanza na nukuu ya Katiba kwenye Ibara ya 18 ambayo ndio inayoleta mjadala mpana humu ndani kuhusu haki na uhuru wa mawazo. Hata hivyo, Wabunge wengi wakisoma kipengele hicho hawaendi kwenye Ibara ya 30(1) ambayo naomba niisome; haki na uhuru wa binadamu ambavyo misingi yake imeorodheshwa katika Katiba hii havitatambuliwa na mtu mmoja kwa maana ambayo itasababisha kuingiliwa kati au kukatizwa kwa haki na uhuru wa watu wengine kwa maslahi ya umma.

Mheshimiwa Spika, sasa ndugu zangu ni sahihi kabisa kwamba tunao uhuru lakini uhuru wetu una mipaka na mipaka yenyewe ni pale uhuru wa kwako unapoanzia kuna mahali unaishia na uhuru wa mtu mwingine unaendelea. Kwa hiyo, ni lazima tunapolizungumza hili tujielekeze katika ibara zote mbili za Katiba.

Mheshimiwa Spika, kwa muktadha huo huo, naomba nianze na suala hili la vyombo vya habari kuishauri Serikali kwamba ni kweli tulipitisha sheria ndani ya Bunge letu Tukufu lakini jukumu la kutengeneza kanuni tumeliacha kwa Waziri mwenye dhamana tukiamini kwamba atawashirikisha wadau wote katika kutengeneza kanuni. Sasa kwa kuwa sheria kidogo ni ngumu kurudisha mara kwa mara lakini tunaamini kwamba kanuni zikionekana kwamba kwa nyakati tofauti haziendani na sheria tuliyopitisha, basi nimwombe Waziri kwamba sio vibaya kuitisha tena vikao na wadau kuweza kujadili ili kuondoa hizi sintofahamu ambazo tunaziona na zinazungumzwa.

Mheshimiwa Spika, changamoto ya hili lote ni kwamba sasa hivi karibu kila Mtanzania ni mwanahabari kwa sababu ya mitandao hii ya kijamii Instagram, WhatsApp na Facebook, chochote mtu anachofanya ana-post matokeo yake baadaye kinaenda kwenye jamii na tunaona kwamba ni jambo la kawaida. Ni vizuri sana hasa kwa kuwa tumeanzisha maudhui ya hizi online broadcast, tuwe makini sana katika eneo hili la kila Mtanzania kuwa Mwanahabari.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, ni lazima pia hawa Waandishi wa Habari wanaandaliwa kwa namna gani, hili nalo ni jambo la msingi sana. Tumeona vyuo vyetu vingi vya habari vinavyoandaa Waandishi wa Habari ni vya kawaida sana mtaani, ni vya kawaida mno kiasi kwamba hatutarajii kwamba vyuo hivi vije kutengeneza Wanahabari mahiri. Kwa hiyo na lazima hili nalo Serikali ilione kwa sababu yenyewe ndio yenye jukumu la kuhakikisha kwamba tunapata habari ambazo zinalinda mila na desturi zetu kama Watanzania lakini pia zinazingatia uhuru wa Taifa letu na pia kuzingatia usalama wa Taifa.

Mheshimiwa Spika, sasa leo inawezekana ukakutana na mwandishi wa habari hata hizo sheria zinazoongoza mambo ya usalama wa Taifa hazijui, lakini ni kwa namna ambavyo vyuo vinavyowaandaa ndio ambavyo nadhani tatizo linaanzia hapo. Kwa hiyo, ni vyema Serikali ikatengeneza mitaala kwa kushirikiana na wadau, lakini pia kuboresha vyuo vile ambavyo vinatoa maudhui ya habari ili tuweze kupata Waandishi ambao ni mahiri katika nyanja mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, juzi tulipata wageni kutoka Chama cha Waandishi wa Habari Duniani (IPI) na nilipata bahati ya kuzungumza nao. Wakati tunazungumza walikuwa wamejaribu kulishwa hii dhana kwamba Tanzania hakuna uhuru wa vyombo vya habari, wakaeleza baadhi ya maeneo. Nami katika kujadili tukawa tunazungumza mmojawapo alikuwa anatoka India, nikamuuliza kwamba kwa mfano sasa hivi India ina mgogoro mkubwa sana na Pakistan, nikamwambia inawezekana kweli Mwandishi wa Habari wa India aka-side na Pakistan akiwa ndani ya India kuhusu labda ule mgogoro unaoendelea pale katika eneo la Kashmir. Alivyonijibu tu akasema hiyo wala inawezekana kama yupo kwenye chombo cha habari wala hatatoka hata ndani ya chombo cha habari.

Mheshimiwa Spika, hii ina maana kwamba sisi tunadhani kwamba uhuru wa habari ni kila kitu unaweza ukaandika, lakini hawa wenzetu ambao tunatoa mifano kwao na wao wana miiko. Mwingine alikuwa anatoka Ujerumani, wakati tunazungumza naye akasema hivyo hivyo kwamba hata kule Ujerumani kuna mwandishi mmoja aliwahi kuandika habari akatoa picha ambayo inaonesha kifaru cha Ujerumani jinsi ambavyo kilikuwa kimechakaa kwamba je, ikitokea sasa hivi wanagombana na nchi fulani, kwa kifaru hiki tunaweza tukashinda vita? Basi mwandishi yule wala hakuweza kuonekana tena, alikuja kuonekana baada ya mwezi mmoja. Kwa hiyo, utaona kabisa kwamba sio kwamba hakuna uhuru ambao hauna mipaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine kwa uchache sana nielezee habari ya michezo kwamba kwenye michezo nako kuna tatizo. Ni kweli kwamba tumefuzu kwenda AFCON 2019, lakini lazima tujione kwamba kwanza nchi zimeongezwa ambazo zinashindana, zamani zilikuwa 16 sasa hivi zimefika 24. Kwa hiyo, inawezekana labda ni baada ya kutanua goli ndio tukapata nafasi. Jambo la msingi hapa ni kwamba lazima tuwe na mikakati ya dhati kabisa ya kukuza michezo. Chuo cha Michezo kule Malya ni kwa kiasi gani kinasaidia kutengeneza kama sio Walimu wa michezo kwenye shule lakini hata Makocha ambao wanakuja kufundisha vilabu vyetu.

Mheshimiwa Spika, tumeona kwa mfano nchi jirani ya Burundi hapa ina Makocha kwenye Ligi Kuu ya Tanzania Bara karibu sita kutoka Burundi na wote ni wa kizazi ambacho kinalingana. Kina Ndailagije, Masoud Juma kuna yule Ramadhan wa Mbeya City lakini hapa kwetu Tanzania kuna programu gani ya kupeleka Makocha wetu hawa au vijana wakapate exposure ya kujifunza mbinu/medani mbalimbali nje ya nchi. Kwa hiyo, nadhani hili ni eneo ambalo linatakiwa lifanyiwe kazi.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo pia michezo shuleni, bado michezo shuleni haifanyiki kwa kiwango kile ambacho tulikitarajia na vile ambavyo huko nyuma kilikuwa kinafanyika. Mheshimiwa Mwakyembe amesoma Shule ya Wavulana Tabora na ameona ni shule ambayo ilikuwa imejiimarisha kwenye kila aina ya mchezo, alikuwepo pale, nadhani mchezo pekee ambao haukuwepo pale ni netball. Hivi leo katika tasnia hii ya michezo, hapa mpira wa pete huuoni ukifanya vizuri, kurusha tufe na mkuki hatuoni.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaona michezo ile ile ambayo jamii imeikubali ndiyo ambayo tunaiona lakini bado kuna michezo mingi ya kukimbia na kadhalika hatuoni ikipewa kipaumbele sana na Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaomba sana, nimeuliza swali wakati mmoja kuhusu Sera ya Maendeleo ya Michezo ya Taifa, hebu tupitie hii sera kwa uharaka ili tuweze kutengeneza sera nzuri ambayo pamoja na kushirikisha sekta binafsi, lakini pia Serikali itachukua jukumu lake la msingi la kuhakikisha kwamba sio tu kwamba michezo inakuwa ni sehemu ya burudani, lakini pia michezo inakuwa ni sehemu ya ajira kama ambavyo sasa hivi tumeona duniani kote michezo inaajiri watu wengi sana.

Mheshimiwa Spika, la mwisho lakini sio kwa umuhimu, ni vifaa duni vya TBC. Ni kweli shirika letu la Utangazaji TBC linafanya kazi nzuri sana sasa hivi na limezidi kujenga imani kwa Watanzania, lakini vifaa hawana. Mfano mzuri upo hapa hapa ndani ya Bunge, ukienda kwenye Studio ya Bunge ile ambayo TBC wanarekodi ile mic lazima wanapokezana, kuna wakati mwingine imefungwa na rubber band.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe sana kwamba ili tuweze kuwa na shirika ambalo linalofanana na Taifa letu kwamba Taifa linapiga hatua, lakini pia Shirika la Utangazaji la Taifa tulione kwamba ni shirika ambalo linaweza kushindana na vyombo vingine vya Kimataifa lakini pia na vyombo binafsi ambavyo tunaona vinafanya vizuri katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuwa mchangiaji wa kwanza katika Wizara hii muhimu sana kwa maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeskiliza vizuri hotuba zote tatu, lakini kipekee napenda sana niwapongeze Wizara hii ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na Makatibu wao Wakuu pamoja na watendaji wote wa Wizara hii, kwa kazi kubwa ambayo wameifanya. Ipo kazi kubwa ya kuboresha miundombinu ya shule zetu zile kongwe ambayo imefanyika, kila mwenye macho anaona, kazi kubwa imefanyika, tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia taasisi ambazo wanazisimamia zipo taasisi ambazo zinafanya kazi nzuri, tunawashukuru sana. Na miongoni mwa taasisi hizo ni Bodi ya Mikopo; bodi hii tunaona kabisa kwamba sasa hivi inafanya kazi nzuri sana, tumeona kabisa wanafunzi sasa wanajielekeza kwenye masomo peke yake, hakuna mambo yale ya kugomea au ya kutafuta fomu za mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunawaomba pamoja na pongezi hizo lakini wazidi kuboresha kama ambavyo tumeendelea kushauri miaka yote, kwamba kwa kuwa hii ni Bodi ya Mikopo na ni mikopo, kama hata Mheshimiwa Rais amezungumza mara nyingi, basi ni vizuri hii mikopo isiwe na ubaguzi kwa maana ya mwanafunzi yeyote aweze kuwa na stahiki ya kuweza kupata mikopo kwa vigezo vile tu vya kitaaluma lakini visiwepo kwamba huyu sijui baba yake ni nani, huyu baba yake ni nani. Hii itakuwa ni nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwapongeze TCU; wamekuwa wanasimamia eneo hili vizuri, tumeona maboresho ya vyuo mbalimbali vikielekezwa kuboresha maeneo yao mbalimbali. Lakini niwashauri kwamba wasiwe sana wanafanya kazi kama matarishi, kama migambo, ni vizuri kwa kuwa hapa wanasimamia elimu wakae na wale wadau, haswa vyuo hivi ambavyo viko chini ya taasisi za dini, wazungumze nao, wawaelekeze na wawaelekeze mwelekeo wa Serikali unakotaka twende, lakini kuvifungia tu ama kuvinyang’anya baadhi ya kozi na kadhalika sio jambo zuri. Kwa hiyo, ni vizuri sana wakae na wadau hawa vizuri, hawa ni wadau wa maendeleo ambao wanasaidia katika Sekta hii ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Sera ya Elimu; juzi hapa niliuliza swali katika eneo hili linalogusa Sera ya Elimu, lakini majibu ambayo nimeyapata bado kwa kuwa ilikuwa kwenye swali nahitaji nipate ufafanuzi zaidi. Sera ya Elimu ya Mwaka 2014 imeweka bayana kwamba elimu ya msingi itaishia Darasa la Sita na Naibu Waziri wakati analijibu akasema sera sio msahafu, lakini sasa japokuwa sio msahafu lakini hata mitaala inayotengenezwa inaishia Darasa la Sita. Maana yake ni kwamba wanafunzi wa Darasa la Saba ni kama wanakwenda kuota jua tu kwa mwaka mzima, wanapoteza muda. Kwa hiyo tunapenda tupate majibu yanayoeleweka; ni lini hii sera itatekelezwa kwa mujibu wa sera yenyewe ilivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili, kwenye Sera ya Elimu vitabu bado ni tatizo. Hivi ninavyozungumza hapa Darasa la Tano mpaka sasa hivi bado vitabu vya huu mtaala mpya havijakwenda. Kwa hiyo, Serikali ituambie, hawa wanafunzi wa Darasa la Tano watasoma kwa vitabu gani? Maana wanaendelea sasa hivi tuko kwenye mwezi wa nne sasa, wanasoma vitabu gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema juzi, kwamba sera sio msahafu inawezekana tukafika mpaka Darasa la Saba; sera hii mpya imefafanua kabisa kwamba mitaala ya elimu itaishia Darasa la Sita, hao Darasa la Saba watakuwa wanasoma mtaala upi maana hakuna kitu ambacho kimeandaliwa kwa ajili ya Darasa la Saba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo kwenye hiyo Sera ya Elimu pia tupate majibu ni mitaala ya shule za mchepuo wa Kiingereza. Mpaka sasa hivi kuanzia Darasa la kwanza mpaka la tatu bado hawana vitabu, inabidi wachukue vitabu hivihivi vya Kiswahili wafanye direct translation ambacho sio kitu kizuri. Kwa hiyo, tunapenda kuona kwamba kuna vitabu vya mchepuo wa Kiingereza ambavyo vimeandaliwa kwa ajili ya watoto hao wanaosoma mchepuo huo. Na Waheshimiwa Wabunge, kwa taarifa yenu hapa tunazungumza watoto wengi ambao ni watoto wetu sisi Wabunge na watu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine katika suala la elimu nizungumzie suala zima la watoto hawa wanaosoma shule hizi za private, watoto wetu. Ukisoma Katiba, Ibara ya 13(4) – wewe ni mwanasheria mbobezi – inasema ni marufuku kwa mtu yeyote kubaguliwa na mtu au mamlaka yoyote inayotekeleza madaraka yake chini ya sheria yoyote au katika utekelezji wa kazi au shughuli yoyote ya mamlaka ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hapa kuna ubaguzi wa wazi tunawafanyia watoto wanaosoma katika shule za private. Kwa sababu sasa hivi tuna elimu bila malipo kwa watoto ambao wanasoma shule za Serikali, lakini huku kwenye private wazazi tumekubali tunalipa ada, lakini kwa kuwa kuna ruzuku ambayo Serikali inatoa kusaidia watoto hawa wa shule za Serikali kwenye mitihani, basi hii iende pia kwenye shule za private kwa sababu na hawa ni watoto wa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa bahati mbaya sana – Mheshimiwa Waziri ulitazame hili kwa kina – katika utoaji wa elimu kuna wadau wakuu kama watatu; kuna Serikali yenyewe na wewe kama Wizara na TAMISEMI lakini na hawa private secor, hizi private schools nyingi ni shule za dini na kwenye shule za dini mara nyingi wanatoa elimu hii kwa watoto wale wegine ni yatima kabisa ambao hawana uwezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa watoto hawa hawana uwezo, mashirika ya dini yanasaidia kuchukua gharama zile za ada, Serikali ichukue jukumu tu hizi gharama ndogo ya kwenye ada za mitihani tuwasaidie ili waweze kuwa na usawa. Lakini hii haitakuwa haki kabisa kwamba hawa wanapata haki hawa wengine hawapati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu hii Taasisi ya Elimu Tanzania; nimesoma hapa katika hotuba ya Wizara, ukurasa wa 147 kipengele kidogo cha (4) anasema “Kuendelea na uandishi wa vitabu vya kiada kwa Darasa la Sita, Saba, Kidato cha Kwanza mpaka cha Sita na moduli kwa ajili ya Elimu ya Ualimu pamoja na kuandaa maudhui ya kielektroniki”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa changamoto iliyoko hapa ni kwamba mpaka sasa hivi mamlaka hii pia sisi tunadhani kwamba imeshindwa kwenye hili eneo la uchapishaji wa vitabu. Na hili eneo huko nyuma lilikuwa linafanywa na private sector, tumepitisha Sheria hapa ya PPP. Sasa nasikitika kuona kwamba mamlaka hii kwa maoni yangu bado haijafanya vizuri katika eneo hili, kwa nini msikae na hao wadau wa sekta binafsi ninyi mkawa tu kama mwongozo kama ilivyokuwa kwenye ile Bodi ya EMAC zamani ambapo wachapishaji binafsi walikuwa wanapewa miongozo wanaandaa, EMAC inafanya approval na mwisho wa siku kitabu kinakwenda sokoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake sasa hii ndiyo imetutia hasara kubwa ile ya vitabu ambavyo vimeondolewa katika mfumo, kwamba mamlaka yenyewe imechapisha vitabu, imeharibu na vimeondolewa katika mfumo. Lakini mpaka leo hatuambiwi ni hasara kiasi gani tumepata na nani amewajibika kwa hasara ile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mheshimiwa Waziri hebu hili lione kwa sababu tumepitisha Sheria ya PPP tuboreshe hii idara vizuri, Taasisi hii ya Elimu Tanzania iwe na majukumu mahususi ili majukumu mengine tuwaachie sekta binafsi waweze kufanya ili kama kutatokea hata kama kuna makosa tunaondoka kwenye risk. Maana yake sasa hivi tatizo ni kwamba taasisi inapofanya yenyewe inachukua pia na risks zinapotokea. Kwa hiyo, nikuombe sana kama mwanzo kulikuwa na nia njema lakini kwa nia njema hiyo hiyo tukae na hao wadau tuwashirikishe tuone katika eneo hili tunatokaje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika hotuba iliyoko mbele ya Bunge letu Tukufu. Kwanza nitoe pongezi za dhati kwa Waziri mwenye dhamana pamoja na Manaibu Waziri kwa kazi kubwa na nzuri sana wanayoifanya. Pia pongezi hizi ziende kwa Watendaji wa Wizara na Mashirika yote yaliyoko chini ya Wizara hii kwa maana kwamba tunajua bila wao utekelezaji wa Ilani ya Chama ni jambo ambalo ni gumu. Kwa hiyo tunatoa pongezi na jukumu letu sasa ni kushauri kwa yale maeneo ambayo tunaona kwamba yanaweza yakawasaidia kufanya kazi yao kwa ufanisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipekee kabisa naomba kwanza nitoe pongezi za dhati kwa Meneja wa TANROAD Mkoa wa Tanga, Injiania Ndumbaro kwa kazi kubwa sana anayoifanya. Mkoa wa Tanga hususan Wilaya ya Lushoto, Korogwe na Muheza ni za milima, kwa hiyo mara nyingi sana barabara zinasumbua hasa nyakati za mvua, lakini injinia huyo amekuwa halali na kuhakikisha kwamba barabara hizi wakati wote zinapitika. Mvua za mwaka jana zilileta mafuriko makubwa sana katika eneo la Lukozi lakini ndani ya kipindi kifupi aliweza kutujengea daraja pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo, lakini pia nitoe masikitiko kidogo kwa watendaji wa TANROAD hasa ngazi ya Taifa kwa sababu barabara yetu ya kutoka Mlalo kwenda Lushoto, lakini pia kutoka Mlalo kwenda Mng’aro hadi Maramba kule Mkinga kila mwaka kwa kipindi cha miaka mitano mfululizo tumekuwa tukipanga katika vipaumbele vyetu kwenye RCC kwamba ifanyiwe upembuzi yakinifu, lakini pia ifanyiwe na usanifu wa kina. Mara zote inapofika kwenye meza ya Watendaji wa Kitaifa kwa maana ya Injinia Mfugale, walikuwa hawaipangii fedha. Kwa hiyo niombe sana kwamba barabara hii ni muhimu kwa sababu inaelekeza eneo muhimu sana la kiuchumi hasa kwa mazao ya mbogamboga na matunda ambao ndiyo uzalishaji mkubwa katika eneo letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sasa naomba nitoe mchango wangu katika eneo zima la usafirishaji hasa usafirishaji wa anga. Kwanza kabisa kipekee nimpongeze sana Mtendaji Mkuu wa ATCL ndugu yangu Ladislaus Matindi amekuwa akifanya kazi kubwa sana na kazi nzuri ya kuhakikisha kwamba shirika hili linasimama. Pongezi hizi pia zimuendee Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa ununuzi wa ndege hizi nane ambazo kwa kweli zinafanya vizuri katika soko la ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunataraji kuiona ikifanya vizuri zaidi ATCL katika soko la nje kwa maana kushiriki katika ushindani. Tumeona hapa yapo maeneo kadhaa wameanzisha safari lakini bado tunataka kuiona ATCL ikifanya kazi vizuri, itafanyaje vizuri; kwanza ni lazima tusiiweke ATCL kwenye mikono ya Wizara peke yake, ATCL lazima tuichukue kama ni mradi wa kimkakati wa nchi, tuone kama nchi tunataka kwenda wapi na shirika hili la ndege. Utaona wenzetu wa mashirika kama ya Turkish ya Uturuki, Rwanda Air na Qatar ya Doha kule wameyaweka kama ya kimkakati ni ya nchi nzima inayabeba haya mashirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano ukifika pale Kigali leo, wanaitangaza Kigali kama kituo cha kibiashara cha mikutano, kwa hiyo nchi mbalimbali tunaona kabisa katika forum mbalimbali za kimataifa wanafanya mikutano Kigali lakini kwa kupitia Rwanda Air. Ukifika Doha pale Qatar ni mji mkubwa sana wa kibiashara sasa hivi, lakini umechagizwa kabisa na uwepo wa Qatar Air, lakini pia ukifika kule Istanbul, Uturuki utaona kabisa sasa hivi imekuwa ni kituo kikubwa cha kibiashara kati ya Asia na Ulaya kupitia hili Shirika la Ndege la Turkish.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yanafanikiwa tu kwa sababu wenzetu hawa wameweza kutoa ruzuku kwenye haya mashirika kwa sababu yamechukuliwa kama ni miradi ya kimkakati ya nchi na hayajaachiwa kwenye Wizara kama ambavyo tunafanya sisi. Utaona kwamba gharama kama za landing na navigation charges ziko chini au wamezitoa kabisa kwamba yanaruhusu sasa biashara kufanyika kwa wepesi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo ATCL ni kweli wamenunua ndege nane, lakini mpaka sasa hivi tunavyozungumza hawana hata ndege moja ya kubeba mizigo. Sasa tunapozungumza Tanzania ya viwanda ambayo pia tuna mazao ambayo tunataka tuyapeleke kwenye masoko ya kimataifa, bila kuwa na ndege za kubeba mizigo jambo hili litakuwa ni gumu. Kwa mfano, tu hapa tuna viwanda zaidi ya kumi na nne katika Kanda ya Ziwa ambavyo vinachakata minofu ya samaki, lakini kwa masikitiko makubwa viwanda vyote hivi vinasafirisha minofu kwenda uwanja wa Nairobi ama uwanja wa Entebbe kiasi kwamba sisi hatuonekani kama tuna-export hii samaki kutoka katika eneo letu. Sababu kubwa ni kwamba hatuna viwanja, hatuna ndege za kubeba mizingo lakini pia viwanja vyetu vya ndege gharama za kutua ndege za mizigo ni kubwa sana kiasi ndege hazivutiki kuja kutua katika viwanja vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaona hata juzi hapa Waheshimiwa Wabunge wanalalamika kwamba maparachichi yanapelekwa Kenya halafu Kenya ndiyo wanayapeleka kwenda Uchina. Hili tunaweza tu tukaliepuka kama tutakuwa na gharama rafiki kwenye viwanja vyetu, lakini pia tutakuwa na ndege zetu ambazo ni za mizigo, ili sasa hata hivi viwanja tunavyoendelea kupanua huko Songwe, huko Mwanza na kadhalika viweze kutumika kama sehemu mojawapo ya kuchochea uchumi wa nchi yetu na ndiyo maana katika hatua ya awali nilizungumza kwamba bila kuifanya ATCL kuwa ni mkakati wa kitaifa tukaiacha peke yake kwenye Wizara hii moja, ile tija ambayo tunaikusudia itakuwa haijafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumza, ni suala zima la kupanua Bandari ya Tanga. Tumeona katika kitabu, ukurasa wa 117, kuna upanuzi wa Bandani ya Tanga. Hii ni bandari muhimu sana kimkakati na ndiyo maana nadhani hata Wakoloni wa Kijerumani walianza kujenga bandari Tanga kabla ya maeneo mengine na hata reli ya Tanga nadhani ndiyo reli ya kwanza kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe sana Serikali kwamba ni muhimu sana bandari hii iboreshwe kwa wakati. Pia itasaidia kwa sabau sasa hivi tumeona hata wenzetu Wazanzibar kuna baadhi ya bidhaa wanazipitishia Mombasa lakini tukiboresha Bandari ya Tanga kutakuwa na uwezo mkubwa wa kupitisha mizigo hata ya Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo ni ukarabati wa reli ya Tanga – Moshi - Arusha - Musoma. Hili nalo tunamshukuru sana ndugu yetu Kadogosa, jitihada zimeanza lakini jitihada hizi zisiishie kufufua reli hii ya zamani. Tunatamani na sisi pia tuone SGR ikiwa katika maeneo haya, inachukua mkondo huo wa reli za kimataifa ili kuboresha sasa huduma za usafiri na kuunganisha usafiri wa reli na usafiri huu wa majini. Hii ni kwa sababu kuna mizigo mingi ambayo inaenda nchi jirani ikiwemo Uganda na Kenya ikiweza kupita katika bandari hii na kupitia reli kwenda mpaka Musoma inaweza ikasaidia hata sisi kama nchi pia kuwa na mkakati wa kushindana katika soko la Sudani Kusini kwa kupitia Bandari ya Tanga na reli hii ya kwenda Moshi – Arusha - Musoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho lakini siyo kwa umuhimu ni suala zima la mawasiliano. Ndugu yangu Mheshimiwa Eng. Nditiye tumezungumza mara kadhaa kwamba kuna maeneo katika Jimbo la Mlalo bado mawasiliano ya simu hayapatikani. Kwa hiyo, naomba sana Wizara ihakikishe yale maeneo mahsusi niliyowaandikia yanafikiwa na huduma hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia hoja hii kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Mkinga – Maramba – Mng’aro, Mlalo hadi Lushoto ipo chini ya Wakala wa Barabara ya Mkoa. Barabara hii inaunganisha Wilaya za Mkinga na Lushoto, lakini pia na pacha ya kwenda Korogwe na wilaya jirani ya Same Mkoani Kilimanjaro.

Mheshimiwa Spika, mara zote kwa kipindi cha miaka mitano mfululizo barabara hii tumekuwa tukiipitisha katika vikao vyetu vya RCC ili itengewe fedha kwa ajili ya upembuzi na usanifu wa kina (detailed design) mara zote inapofika katika ngazi ya Taifa, budgets inakatwa. Tunataka kujua kulikoni? Tanga - Lushoto tunakosea wapi? Barabara hii Lushoto - Mlalo yenye kilometa 45 ni muhimu sana na kiungo kikubwa cha uchumi kwa wananchi wa Usambara. Tunataka kujua kwa nini?

Mheshimiwa Spika, sisi tunaipanga barabara hii katika mipango yetu kwa kuzingatia vipaumbele. Tunapenda kupata taarifa rasmi kutoka Serikalini. Hivyo Serikali itoe umuhimu wa kipekee kwa barabara hii angalau hata ijengwe kwa kiwango cha lami hata kwa awamu za kilomita 10 kwa kila mwaka. Vinginevyo kutokana na jiografia ya Lushoto ilivyo, ikibaki kwa kiwango cha changarawe, Serikali inapoteza pesa nyingi sana katika periodic maintenance.

Mheshimiwa Spika, nchi yetu ina viwanda 14 vinavyochakata samaki katika Mikoa ya Mara, Mwanza na Kagera, lakini kwa bahati mbaya kutokana na kutokuwa na ndege za mizigo, minofu hii inasafirishwa kwenda Nairobi na Entebe hata Kigali ambako wenzetu wanapata mapato ya export.

Mheshimiwa Spika, hivyo, nashauri, pamoja na ndege za abiria, Serikali iweke mkazo kuanzisha mchakato wa kununua ndege za mizigo ili pia viwanja mbalimbali vinavyoboreshwa viweze kutumika kusafirisha mazao mbalimbali kwenda nje ya nchi kwa masoko.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali itazame upya gharama zetu za viwanja vya ndege ili viweze kuvutia hata ndege za mizigo kuweza kutua katika viwanja vyetu.

Mheshimiwa Spika, shirika letu la ndege ATCL linafanya vizuri sana lakini bado linakumbana na ushindani mkubwa kutoka mashirika ya ndege ya Kimataifa.

Mheshimiwa Spika, kwa bahati mbaya sana hata wenzetu katika Kanda ya Afrika Mashariki miradi hii wanaichukulia kama miradi ya kimkakati, hivyo kusimamiwa na Serikali nzima tofauti na hapa kwetu ambapo jukumu hilo imeachwa kwa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi pekee.

Mheshimiwa Spika, Mashirika kama Emirates, Turkish, RwandAir ni sehemu ya kukuza utalii na biashara ya Kimataifa katika nchi zao. Mfano, RwandAir inatumika kuitangaza Kigali kuwa kituo cha utalii wa mikutano ya Kimataifa. Ethiopian Airways inajulikana kwa kuchangia pato la nchi hiyo kupitia sekta hii ya usafirishaji. Turkish Airline inasifika kwa kuifanya Uturuki kuwa kituo kikubwa cha biashara katika Bara la Ulaya na Bara la Asia. Qatar Airways imeubadili mji wa Doha na kuwa kituo kikubwa cha biashara cha Asia na kuhakikisha kuwa mji wa Doha unakuwa kiunganishi muhimu cha ndege zote za Kimataifa kwenda maeneo tofauti duniani.

Mheshimiwa Spika, kwa mtazamo na mifano hiyo, ATCL inawezaje kuhimili ushindani na mashirika haya ikiwa huko kwao yana misamaha ya kodi, hayalipi gharama za kutua viwanjani na uongozaji wa ndege yanaendesha au ni sehemu ya mfumo wa uendeshaji ya viwanja vikubwa vya ndege (mfano, Dubai Kigali, Doha na Addis Ababa) yanamiliki kampuni za kutoa huduma viwanjani (ground handling company), yanamiliki kampuni za kutayarisha vyakula vinavyotumika ndani ya ndege (inflight catering) na hata kumiliki shule za kutayarisha wafanyakazi wa karakana za utengenezaji wa ndege kwa mashirika mengine ya ndege. Kwa bahati mbaya gharama zote hizi hapa kwetu zimeachwa chini ya Shirika la ATCL.

Mheshimiwa Spika, gharama za uendeshaji wa ATCL ambazo zinatokana na utoaji wa huduma zinazotolewa na mashirika ya Serikali ambazo zinaweza kutazamwa kama walivyofanya wenzetu kwa mashirika yao.

Mheshimiwa Spika, tusipoitazama ATCL kama uwekezaji wa kimkakati wa Kitaifa wenye nia ya kuwezesha sekta nyingine, hapo baadaye tutakwama, suala linaweza kuchukuliwa kwamba ni biashara ya muda mfupi, lakini tukilipa mtizamo wa Kitaifa litakuwa na tija ambayo ndiyo dhumuni kubwa ya kulifufua Shirika hili.

Mheshimiwa Spika, hivyo, badala ya kung’ang’ania tozo la gharama za kutua uwanjani na uongozaji ndege (landing and air navigation charges) ni vyema kuitazama ATCL kama sehemu ya utoaji huduma hizo isiyohitaji kulipiwa.

Mheshimiwa Spika, mwisho, lakini siyo kwa umuhimu, uwanja wa ndege wa Tanga unapaswa kufanyiwa ukarabati ili nasi tuweze kusafiri na kusafirisha bidhaa zetu kwenda kwenye masoko ya Kimataifa.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, asante sana kwa nafasi hii, na mimi niweze kutoa mchango wangu katika kamati zote mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwapongeze Wenyeviti wote kwa kazi nzuri ambayo wameifanya. Kipekee kabisa nianze na Kamati ya UKIMWI; na niwapongeze sana wewe pamoja Mheshimiwa Spika kwa ubunifu mkubwa wa kamati hii ambayo hapo mwanzoni Kamati hii wajumbe walikuwa wanaikimbia. Sasa hivi imekuwa ni kamati moja muhimu sana, tumepata semina za kutosha. Ni kamati ambayo imetoa madarasa mengi na imefanya mambo makubwa na kwa kweli Mwenyekiti wake Mheshimiwa Oscar Mukasa anahitaji pongezi za ziada kabisa katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo kamati zimeeleza kwenye eneo hili la Kamati ya UKIMWI pamoja na madawa ya kulevya bado kuna changamoto hasa katika eneo zima la udhibiti wa madawa ya kulevya lakini pia tumeona katika kifua kikuu bado nguvu si kubwa kama ambavyo tunaiona katika UKIMWI.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ningeomba sana Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu isaidie katika eneo hili, na haswa katika suala lile la Tume ya Madawa ya Kulevya, ili kuhakikisha kabisa kwamba tunaongeza ufanisi ili katika hali ambayo tumeona sasa hivi kwamba kumekuwa na udhibiti mkubwa wa madawa basi taifa letu liendelee kunusurika na hii hali ambayo tunaiona.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo ningetamani nilichangie ni katika eneo hili la elimu haswa kwa kupitia Kamati ya Huduma za Jamii. Suala la elimu ni suala ambalo linahitaji tafakuri mpya kama taifa. Tumeona maoni na ushauri umekuwa ukitolewa, na mara ya mwisho Mheshimiwa Benjamin Mkapa, Rais Mstaafu naye alitoa wazo hili la kupitia mfumo wetu wa elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo wetu wa elimu bado unazalisha watu ambao wanashindwa kushindana katika dunia hii ambayo artificial intelligence imechukua nafasi kubwa. Kwa hiyo, sisi kama taifa tunao wajibu wa kuhakikisha kwamba tunaitizama upya elimu yetu. Na tunaposema hapa maana yake tuanzie katika Sera lakini pia katika sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mambo ambayo bado hatufanyi vizuri katika elimu na mara nyingi tunajificha katika kichaka cha Sera na sheria. Kwa mfano, hivi ninavyozungumza wanafunzi ambao wapo darasa la saba mwaka huu, Sera ya Elimu ilikuwa inatuelekeza vitabu mwisho ni darasa la sita lakini wapo darasa la saba; ina maana hakuna vitabu, sasa tunaweza tukaona kwamba wanapoteza mwaka mzima bure shuleni kwa kitu ambacho walishakisoma wakiwa katika darasa la sita.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni uzalishaji wa mitaala; Taasisi ya Ukuzaji wa Mitaala kwamba mitaala yetu sasa tuiboreshe zaidi ili iweze kuendana na dunia ya sasa. Kama ambavyo tumeona kupitia SADC tumepata fursa ya Kiswahili kuwa bidhaa katika nchi 16 za SADC. Ili Kiswahili kiwe bidhaa ni lazima sasa mitaala na yenyewe ilitamaze eneo hili; kwa maana huwezi ukaenda kufundisha nchi ambazo zinazungumza Kireno kama lugha ya asili bila hawa tunaowategemea wakafundishe Kiswahili katika nchi hizo bila kujua lugha ya Kireno ama lugha nyinginezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nata anitoe rai kwamba kwa kuwa ndio tunaelekea katika maandalizi ya bajeti basi eneo hili lionekane ni mahususi kabisa katika bajeti ili Taasisi ya Ukuzaji wa Mitaala iweze kuendana na soko hili la SADC ambalo tunakusudia kwenda kulifikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni uhaba wa watumishi hasa katika kada ya elimu. Katika Halmashauri ya Lushoto tuna uhaba wa walimu 1,200. Utaona kabisa kwamba kule Lushoto mwalimu mmoja anafundisha vipindi 40 hadi 46 kwa wiki, tofauti kabisa na mapendekezo ambayo ni vipindi 24 hadi 26 kwa wiki. Kwa hiyo, utaona ni tatizo kubwa sana; lakini wakati Taasisi ya Mitihani inapotangaza matokeo huwa haiangalii maeneo ambayo hayana walimu, inatangazwa kwa usawa nchi nzima; wenye walimu na wasio na walimu wote mnawekwa katika kapu moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ningetaka pia tuangalie kwamba wakati wa kutangaza matokeo ya mitihani mbalimbali kuanzia shule za msingi, sekondari za kawaida na high school basi wazingatie pia kwamba kuna Halmashauri hazina walimu wa kutosha. Kama ambavyo umeona hapa kwamba kwa wiki moja mwalimu anafundisha vipindi 40 hadi 46 maana yake ni kwamba hapa huwezi ukatarajia kwamba utapata ufanisi wa kutosha sawa na shule za seminari.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, eneo hili ni muhimu sana tunapoelekea katika bajeti na Wizara ya Utumishi, na wametuahidi kwamba wanakusudia kuajiri watumishi wengi, basi eneo la elimu liwe ni eneo mahususi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine pia ni katika usimamizi katika elimu. Nitatoa mfano wa Halmashauri ya Lushoto ina shule za msingi 169, ni Halmashauri ya nne kwa kuwa na shule nyingi za msingi hapa nchini. Halmashauri inayoongoza ni ya Moshi Vijiji, hii pamoja na kwamba inaitwa vijijini lakini ipo mjini, zinazofuata ni Ubungo na Kinondoni, hizi zipo mijini; utaona hata miundombinu yake ya kufikia shule ni rahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, unapozungumza Halmashauri ya Lushoto jiografia yake ya milima, mabonde, maporomoko na majabali ni ngumu sana kufikika kiasi kwamba hata ukaguzi hauwezi ukafanyika vile inavyopaswa, vilevile pia ndiyo maana unakuta hata upungufu huo wa walimu unachangiwa na kutokuwepo na miundombinu wezeshi ikiwemo ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitoe rai tu kwamba Wizara pamoja na TAMISEMI kuangalia maeneo fulani fulani ikiwezeka pia tutengenezewe kanda maalumu. Zisiwe tu zinatengenezwa kanda maalum za mambo ya uharifu lakini hata mambo haya ya elimu; kwa sababu Halmashauri yenye shule 169 maana yake ni kwamba kuna mwamko mkubwa sana wa kujenga hizi shule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa sitaki kuamini kwamba kwa mwamko huo wa kujenga shule kusiwe na mwamko wa kupata faida inayotokana na elimu. kwa hiyo, sisi kwetu shida sio vyumba madarasa, kwetu shida sisi ni ubora wa elimu ambayo inapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni suala zima la TBC. TBC wanafanya kazi nzuri, tumeona maboresho mbalimbali yanaendelea upatikana lakini bado usikivu na upatikanaji wa TBC ni katika maeneo ya mjini; kiasi kwamba sasa TBC sasa hivi inashindana na redio hizi za kawaida. Kwa hiyo, tungetamani kuiona TBC ikienea nchi nzima hasa katika maeneo ya pembezoni. Hii itasaidia sana haswa katika vipindi vile ambavyo vinatoa elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kipindi kile cha lishe; sasa hivi vipindi vizuri kama hiki wananchi hawapati faida ya kuvisikia kwa sababu TBC haisikiki. Naamini kwa namna ambavyo Tanzania tunazalisha na vyakula vilivyo vingi, wananchi wakipata elimu hizi za lishe na mambo mengineyo kupitia TBC itasaidia sana kuhakikisha kwamba hata huu udumavu ambao tunausema utapungua kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe, pamoja na kazi kubwa ambayo anaifanya pale TBC, lakini tunaomba shirika letu hili lipate uboreshaji mkubwa. Tunaomba sana kuwa na Televisheni ya Taifa ambayo ndiyo msingi wa kulinda maadili, mila na desturi za Kitanzania, aweze kusaidia katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja za Kamati zote mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi hii ya kuwa mchangiaji katika bajeti hii ya Waziri Mkuu. Binafsi nianze na pongezi kwa Serikali yetu ya Awamu ya Tano chini ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa ambayo inafanyika na inaendelea kufanyika na pia wasaidizi wake wa karibu, Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, kiranja mkuu wa shughuli za Serikali, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa anafanya kazi kubwa sana ambayo kila mwenye macho anaona na asiye na macho anaweza akapapasa hatua kubwa za maendeleo ambazo zimefikiwa katika awamu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee pia nakupongeza wewe mwenyewe kwa namna ambavyo unaendesha Bunge letu Tukufu. Mara nyingi sana binadamu mpaka asiwepo ndiyo sifa zake zinaelezwa kedekede, lakini ni vizuri zaidi tukazieleza sifa hizi wakati wewe mwenyewe ukiwa unashuhudia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika awamu hii ambayo tumekuwa na Bunge mtandao, kwa kweli nilikuwa nataniana na ndugu yangu Musukuma hapa, alikuwa anasema, hivi huyu mtani wako naye ana utabiri kidogo? Maana alituletea falsafa hii ya Bunge mtandao, halafu mwaka huu tukakutana na changamoto ya Corona. Sasa unaweza ukapata wateja safari hii kuhusu utabiri wa uchaguzi unaokuja, kwa sababu umeonekana katika eneo hilo ni mahiri. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nianze kuchangia bajeti iliyoko mbele yetu katika eneo la fungu 37 - Ofisi ya Waziri Mkuu haswa suala la linalohusu Mfuko wa Maafa.

SPIKA: Eh, Nilikuwa namsikiliza vizuri sana Mheshimiwa Shangazi alipokuwa hasa anatamka neno Corona, kwa sababu wao kule wanasema Coona. Mheshimiwa endelea. (Kicheko)

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa. Kule tunazo Coona za kuchakata mkonge.

Mheshimiwa Spika, Fungu Na. 37 - Ofisi ya Waziri Mkuu linahusu maafa, lakini kwa muda mrefu sasa hatuoni ukiwekewa fedha kiasi kwamba limekuwa ni tatizo kubwa sana. Mwaka huu tumepata neema ya mvua nyingi katika nchi yetu na hasa mikoa ya kaskazini na mashariki. Kwa kweli watumishi wa Serikali wamekuwa wakipata shida sana katika eneo hili la maafa kwa sababu hakuna hata zile pesa za mwanzo za kufanya intervention. Hata Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba na Sheria Mheshimiwa Mchengerwa, tumeona wiki mbili hizi akiwa amepanda kwenye boti anazunguka katika maeneo mbalimbali huko Rufiji, lakini unamwona yeye kama Mbunge, hata huwezi kumwona DC wala watu wengine. Kwa hiyo, unaona kabisa ni tatizo la kutokuwa na fedha katika Mfuko huu wa Maafa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri eneo hili tulitafutie mwarobaini wa kudumu. Tutafute vyanzo vya uhakika vya kuweza kuweka pesa katika Mfuko huu wa Maafa. Tena ikiwezekana zipatikane hata kwa asilimia, kwa sababu majanga ni mengi yanayotokea nchi hii. Tumeona tu kwa mfano kwa mwaka huu wa fedha ambao tunaenda kuukamilisha, tulianza na tatizo la nzige; kulikuwa na tishio la nzige, lakini Mwenyezi Mungu ameepushia mbali, hawakuingia katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tumekutana na changamoto ya mvua, hali ya barabara zetu siyo nzuri huko vijijini, kiasi kwamba kwa ile asilimia 30 TARURA wanaipata naamini katika eneo hili mwaka huu haiwezi ikatosha, hivyo inaweza ikaadhiri hata namna ya usafirishaji wa vifaa mbalimbali wakati wa uchaguzi. Kwa hiyo, tunaomba eneo hili tulitizame kwa kina sana.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ningetaka nilizungumze ni eneo la kuhusu anuani za utambulisho wa makazi (post code). Hili ni eneo ambalo limeanza Dar es Salaam kama pilot study, lakini eneo hili nalo limefika mwisho na waliokuwa wanasimamia mradi huo ambao ulikuwa ni pilot ni TCRA kupitia Wizara ya Mawasiliano na Uchukuzi.

Mheshimiwa Spika, sasa tungeweza kuoanisha Mfumo wa Utambuzi wa Makazi pamoja na Vitambulisho vya Taifa, ingekuwa na maana sana; kwa maana kwamba mtu anakuwa anatambulika kwa anuani ya makazi lakini pia na kitambulisho cha Taifa, kiasi kwamba hata kuzuia uhalifu inakuwa rahisi kwamba unafahamu kwa kupitia kitambulisho hiki, huyu mtu anaishi maeneo gani na mambo mengine hata katika mifumo ya kibiashara na mambo mengineyo.

Mheshimiwa Spika, pia katika eneo hili tumeona kabisa kwamba kwa mfano kwa Mkoa wa Dar es Salaam, wenzetu wale wenye utaratibu wa taxi zile za UBA unasaidia sana kiasi kwamba mtu popote alipo kwa sababu kwa Dar es Salaam wameshaingiza kwenye mtandao na ipo mpaka kwenye google unapata, inasaidia hata kurahisisha biashara.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunatamani sana kwamba hili eneo la utambuzi wa makazi liwe eneo la nchi nzima ikiwezekana, eneo hili liendelee lakini pia liunganishwe na mfumo wa vitambulisho ili hata mtu anapohama eneo moja kwenda lingine, inaweza kuwa ni rahisi kufuatilia vitambulisho vya Taifa na pia kupitia anuani za makazi.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo ningetaka kuzungumza ni hili la NIDA, katika eneo la watumishi. NIDA wana watumishi wachache sana nitatoa mfano kwa Wilaya ya Lushoto ambayo ina takribani watu 600,000 inao watumishi watatu tu wa NIDA katika wilaya nzima. Sasa utaona kwamba wale wazee walioko vijijini watu wenye shida mbalimbali zikiwemo za ulemavu hawawezi kufika Lushoto au wengine inabidi watumie gharama kubwa kwenda kufatilia vitambulisho hivi sasa tungependa kuona kwamba angalau hili liangaliwe ikiwezekana waongeze idadi ya watumishi lakini pia wapatikane hata watumishi wa kuwasaidia wasaidizi maana tumezungumza hili eneo la wasaidizi na wenyewe wanajitetea kwamba hawana mafungu. Kwa hiyo, ni vizuri wakawekewa mafungu ya kutosha ili na eneo hili nalo waweze kutusaidia vizuri.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo ningependa kushauri ni katika uanzishwaji wa mfuko wa ugharamiaji elimu kwa maana ya student loan fund tunatumia pesa nyingi sana kila mwaka ambazo ni lazima zitengwe kutoka hazina lakini kama tutaanzisha mfuko mahususi wa kugharamia elimu maana yake Serikali pamoja na wadau mbalimbali katika taasisi za kifedha kama mabenki lakini pia ni mifuko ya hifadhi wanaweza wakatengeneza mpango wa ku-capitalize pesa katika mfuko hata kwa muda fulani na baadaye sasa mfuko huu ukawa unakopesha wanafunzi kwa ngazi hata ya diploma na degree lakini pia hata wa digrii ya pili na hata wa udaktari. Ili sasa tuondokane na hii hali ya kuweka pesa kila mwaka shilingi bilioni 500 nakadhalika nadhani tukiweza kutengeneza eneo hilo tukalitengenezea mpango mahususi hata kwa kutumia mikopo nafuu kutoka vyanzo vingine vya kimataifa mikopo ya muda mrefu inaweza likawa ni eneo ambalo tunaweza tukaondoka na hii adha ambayo kila mwaka lazima tutenge bilioni 500 kwa ajili ya kusaidia wanafunzi katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, lakini katika nukta hiyo ningependa sana kupongeza Benki ya Dunia kwa kutuachia ule mkopo wa milioni 500 US Dollar ambao kwa kweli ni kazi kubwa sana imefanywa na Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana Mambo ya Nje tunakupongeza sana pia watanzania kwa pamoja tunashukuru sana kwa mkopo huu kwa sababu hapo mwanzo ulikuwa na figisu nyingi za baadhi ya watu kukosa uzalendo lakini kwa nukta hii tunashukuru sana kwa msaada huu tunaamini kwamba msaada huu utaenda kuongeza tija katika utoaji wa elimu yetu hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana ahsante sana kwa nafasi hii. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nami nashukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kutoa mchango wangu katika hoja iliyoko mezani ambayo ni Hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa katika vipindi viwili kwa maana ya wakati anafungua Bunge la 2015 na Bunge hili la sasa la 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu utajikita zaidi katika eneo la diplomasia ya uchumi. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais, ametembea katika maono na dira ile ambayo ameizungumza katika hotuba zake mbili na kuonyesha umahiri na ujasiri mkubwa wa kusimamia kile ambacho anakielekeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kipindi cha miaka mitano, 2015 - 2020 Tanzania imeweza kufungua Balozi nane ambazo zinafikisha Balozi takribani 43 duniani kote. Ongezeko hili la Balozi nane kwa kipindi kifupi cha miaka mitano inaonyesha dhamira ya wazi kabisa kwamba Mheshimiwa Rais anataka sasa aipeleke Tanzania huko duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii maana yake nini? Maana yake sasa ni kwamba Wizara za kisekta zinatakiwa zifanye kazi mahsusi ili hizi Balozi ambazo tumezifungua zikawe fursa za kibiashara na fursa nyingine kutoka kwao kwa maana ya kutuletea teknolojia pamoja na mitaji. Kwa mfano, sasa hivi tumefungua Ubalozi kule Havana, Cuba, tunajua wenzetu wale ni wajuzi sana wa kilimo hasa cha umwagiliaji. Kwa hiyo, tunatarajia kuiona Wizara ya Kilimo ikifungamanisha sasa uanzishwaji wa Ubalozi Havana, Cuba pamoja na kusaidia sekta ya kilimo hapa nchini kwa maana ya kubadilishana utaalam na ujuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo hilo hilo la diplomasia ya uchumi, Mheshimiwa Rais ameahidi kwamba tunanunua ndege ya mizigo kwa ajili ya kusafirisha mazao hasa ya mbogamboga na matunda. Hii maana yake nini? Maana yake ni kwamba ni lazima sasa tujiandae kwamba hayo mazao tunayotaka yaende kwenye ulimwengu mwingine, tumeyaandaa kwa kiasi gani? Ndiyo hiyo hoja ambayo alikuwa anaizungumza Mheshimiwa Humphrey Polepole hapa kwamba ng’ombe wetu tutaendelea kuwaacha wazurure huko halafu baadaye tuseme kwamba wanaweza kwenda kushindana kwenye masoko mengine ya dunia? Ni lazima sasa Wizara zichukue hii kama changamoto ili ndege hii isije ikapaki airport haina shughuli za kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu lugha ya Kiswahili. Sasa hivi lugha ya Kiswahili ni miongoni mwa lugha 10 zinazozungumzwa zaidi ulimwenguni. Hapa kuna haja ya dhati kabisa kwa Wizara ya Elimu kupitia mtaala upya. Tunataka kukipeleka Kiswahili katika nchi za Kusini za Afrika (SADC), nchi 16. Huwezi ukapeleka Kiswahili hiki ninachozungumza hapa kwenye nchi ambazo zilikuwa zinatawaliwa na Mreno. Maana yake ni kwamba ni lazima sasa tutengeneze mtaala mpya, tuandae wataalam mbalimbali wa kusoma lugha, wawe na ujuzi wa kujua Kireno, Kifaransa, Kiingereza, Kiarabu, Kichina na lugha nyingine zote ili watakapokwenda kuipeleka bidhaa ya Kiswahili katika hayo maeneo, basi kusiwe na shida ya kuwa na ukalimani. Kwa hiyo, nawafumbua macho Mawaziri kwamba ikishazungumzwa kwenye Hotuba ya Rais sisi turudi katika sekta zetu kuchakata na kuweka hiyo mipango ili mambo haya yaweze kwenda vile ambavyo tunakusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuhusu biashara. Wizara ya Mambo ya Nje ina mpango wa kufungua Ubalozi Mdogo pale Lubumbash, hili ni eneo la kibiashara. Tumeona nchi yetu tunajitahidi sana katika uzalishaji, tunatakiwa tutumie fursa hii ya Balozi tunazozifungua na Balozi Ndogo kuhakikisha kwamba mazao ya Watanzania yanapata masoko. Siyo ya Watanzania tu na bidhaa zinazotoka nchi za wenzetu na zenyewe ziweze kuja hapa kwetu na kutunufaisha katika maeneo yote ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaposema diplomasia ya kiuchumi, hili ni jambo kubwa tunalotakiwa tulitazame kwa jicho la kimkakati. Balozi hizi nane ambazo zimeanzishwa, zote ukizipitia ni za kimkakati. Tukizungumza mahusiano yetu na Uturuki, ni eneo la kimkakati la kibiashara; tukizungumza na Algeria, ni eneo la kimkakati; tukiwaangalia Jamhuri ya Korea Kusini nalo ni eneo la kimkakati. Tusibweteke, tutumie fursa hii, tupitie upya Hotuba ya Mheshimiwa Rais, kila sekta ambayo imeguswa, basi ifungamanishe kila jambo linalopatikana kwa kuzipitia upya sera zetu na miongozo yetu mbalimbali kuhakikisha kwamba tunakwenda kuipeleka Tanzania katika uchumi huo wa kati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii. (Makofi)
The Written Laws (Miscellaneous Amendment) Bill, 2016
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba nitoe mchango wangu kidogo kwenye suala lililopo mbele ya Bunge lako Tukufu. Kwanza nami nipongeze mapendekezo haya yaliyoletwa na AG, amefanya kazi nzuri, japo yapo maboresho madogo, lakini dhamira yake inaonekana ni njema kabisa kwa Taifa letu hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niongelee kwenye Division ya Mahakama hii ya Uhujumu Uchumi ama Mahakama ya Mafisadi kama ambavyo imezungumzwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nami concern yangu mwanzoni ni kwenye shilingi bilioni moja kama ndiyo kianzio, lakini kwa kuwa niko kwenye Kamati ya Sheria na Katiba hata wale wadau ambao tumewaita pale kama Tanganyika Law Society wamekuja na wazo angalau ifike milioni 500. Sisi kwenye Kamati tukasema basi, kwa kuwa ufisadi umejaa zaidi katika Halmashauri zetu na huko wakati mwingine pesa zilizoko kule inawezekana ni milioni 100, 50, inaweza ikawa bado na athari kubwa sana za uchumi kwa wananchi wa maeneo husika, basi tutake tu kwamba Ofisi ya DPP, iweze kuangalia hata kesi ambazo hazijafika kiwango cha bilioni moja, lakini zina madhara makubwa kwenye jamii, basi zipate nafasi kwenye Mahakama hii Maalum.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni separation of power. Suala hili pia lilikuwepo kwenye Kamati na bado naamini kwamba, tunaposema kwamba Rais atashauriana na Mkuu wa Mahakama, haimaanishi kwamba Rais, anaingilia uhuru wa Mahakama. Kwa sababu hapa ni suala la kisera na ni suala la kiuongozi na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hii ya mwaka 77 ambayo tuko nayo, Ibara ya 33 inasema:-
(1) “Kutakuwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano.
(2) Rais atakuwa ni Mkuu wa Nchi…
Sasa unaposema Mkuu wa nchi; ina maama mihimili yote hii ipo chini yake. Hapa ndiyo Rais anapokuwa Mkuu wa Nchi. Kipengele hicho hicho kinaendelea
….. Kiongozi wa Serikali na Amiri Jeshi Mkuu.”
Sasa hapo tunamzungumzia Rais kama Mkuu wa Nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Ibara ya 34(4) inasema:-
“Bila ya kuathiri masharti mengineyo ya Katiba hii, madaraka ya Rais wa Jamhuri ya Muungano yatatekelezwa ama na Rais mwenyewe moja kwa moja au kwa kukasimu madaraka hayo kwa watu wengine wenye madaraka katika Utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano.”
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ndipo tunapoona nafasi ya Mwanasheria Mkuu, nadhani pia hata uwepo wake humu Bungeni ni ku-coordinate kati ya Serikali, Bunge na mhimili mwingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka nitoe mchango wangu katika eneo hilo, kwamba hapa lazima suala hili litaanzia kwenye sera na huko kwenye sera linaanzia kwenye majukwa wakati mwingine ya kisiasa na hata hii Mahakama ya Mafisadi ni suala ambalo Rais alikuwa analizungumza kwenye Mikutano ya Uchaguzi, ina maana ni suala ambalo limetokana na Ilani ya Chama ama limetokana na matakwa ya kisiasa, siyo kwamba Mahakama ndiyo iliyoomba yenyewe kwamba sasa imezidiwa na shughuli pale waanzishe Mahakama hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, huo ndiyo ulikuwa mchango wangu katika eneo hilo. Nakushukuru sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi hii na mimi niweze kutoa mchango wangu kwenye hoja iliyoko mbele ya Bunge letu tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wananizonga nyuma hapa, lakini naomba niendelee kwa sababu kama ulivyotueleza kama Kiti kwamba mamlaka zitatoa taarifa rasmi, sasa naomba Waheshimiwa Wabunge tuvumiliane kwa sababu mamlaka hizi zinatoka kwake na lazima tuziheshimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma mpango ambao unatuelekeza mpango wa mwaka mmoja lakini pia mpango wa miaka mitano na ninaomba nitoe mchango wangu katika eneo dogo la sekta ya afya, hasa kwenye eneo zima la uwekezaji katika sekta hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge awamu iliyopita nikiwa Mjumbe katika Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali tulitembelea Medical Stores Department (MSD) na kuona namna ambavyo wanafanyakazi, lakini wakati tuko pale kukawa na delegation kutoka nchi za SADC ambayo imekuja kufanya uchunguzi ili kuweza kuwapa MSD jukumu la kusambaza dawa katika nchi 16 za Kusini mwa Afrika (SADC), lakini tulijiridhisha kwamba kwa Sheria ya Uanzishwaji wa MSD walikuwa hawana mamlaka ya kuzalisha dawa isipokuwa ni kununua na kusambaza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nimeleta hoja hii? Nimeileta kwa sababu dawa za binadamu zinazozalishwa hapa nchini ni asilimia nne peke yake katika dawa asilimia 100 ambazo tunazitumia. Ni asilimia nne tu ya dawa ndiyo zinazalishwa nchini; dawa nyingine zote tunazinunua kutoka nje ama Ujerumani au India. Sasa hoja yangu ni kwamba Wizara inayohusika na uwekezaji ni wakati mwafaka sasa kuhakikisha kwamba inavutia wawekezaji katika sekta hii ya dawa za binadamu ili kama tutapata soko la usambazaji wa dawa katika SADC dawa hizi ziwe zinatoka hapa hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Wizara ya Afya iweze kuleta muswada Bungeni wa kuweza kubadilisha sheria iliyoanzisha Mamlaka ya MSD ili sasa iweze kuzalisha, lakini pia kusambaza kwa maana kwamba dawa zikiwa zinazalishwa hapa nchini itakuwa rahisi hata kuzisambaza katika hizi nchi za SADC tuweze kupata uwezo wa kwamba dawa zitakuwa zinazalishwa ndani ya nchi, lakini pia kwa kuwa MSD inaweza ikawa ndiyo msambazaji katika nchi za Kusini mwa Afrika basi tukapata multiplier effect kwenye uchumi wetu kwa mana ya uzalishaji na usambazaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini eneo lingine ambalo ninataka kuchangia ni eneo la bandari; kwamba bandari yetu ni hub ya kiuchumi kwa nchi za Kusini mwa Afrika. Tunaomba iendelee kuboreshwa kwa maana kwamba kuweza kushindana na bandari nyingine zilizoko Kusini mwa Afrika hasa ile ya Beira na ya Johannesburg, Cape Town lakini pia na bandari ya kule Angola.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanini nazungumza hivi? Ni kwa sababu sisi tuko katika Ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ambapo tunakumbana na changamoto za protocol mbalimbali za Afrika Mashariki, lakini wakati mwingine hizi protocol hazigusi Kusini mwa Afrika. Kwa hiyo, ni lazima tuwe makini sana pindi tunaposaini protocol za Ukanda wa Bahari wa Afrika Mashariki, tuzingatie kwamba sisi soko letu kubwa tumelielekeza Kusini mwa Afrika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine na la mwisho ambalo ninapenda kutoa mchango ni eneo la viwanja vya ndege; gharama za kutuana gharama za ku-park katika viwanja vyetu vya ndege bado ni kubwa. Kwahiyoili kuwezesha mamlaka hizi za viwanja tuweze kupokea ndege nyingi kwa wakati mmoja, ni lazima tutazame eneo hili la Mamlaka za Viwanja vya Ndege kwa maana ya landing fees na parking fees ili ziweze kushawishi ndege za mashirika mbalimbali kuweza kutua hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nakushukuru kwa nafasi. (Makofi)
The Written Laws (Miscellaneous Amendments) (No. 3) Bill, 2023
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi. Kwanza nimpongeze Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kutuletea Muswada huu ambao madhumuni yake ameyaeleza lakini pia kwenye Hotuba ya Kamati pia tumeeleza madhumuni ya mabadiliko haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mabadiliko haya ya Sheria Mbalimbali Namba Tatu wa Mwaka 2023 yanalenga kwenda kuleta ufanisi katika Wizara mpya ya Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji. Kwa sababu tangu Mheshimiwa Rais ameunda Wizara hii maana yake Waziri mwenye dhamana tumemfunga mikono, hawezi kufanya kazi kwa sababu hati idhini ambazo zinamruhusu kufanya kazi kwenye Wizara hii ziko katika Wizara ya Viwanda na Biashara. Mabadiliko haya yanalenga kuleta ufanisi lakini kuifanya sasa Wizara mpya hii ikafanye kazi hasa kwa kupitia mabadiliko katika Sheria Namba 373 ambayo ni The Export Processing Zone kwa maana ya Kanda Maalum za Uwekezaji kwa Ajili ya Mauzo Nje ya Nchi (Special Ecnomic Zone).

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili ni muhimu sana kwa sababu ndilo ambalo linaipa uhalali Wizara hii kufanya kazi. Sasa kama tusipofanya marekebisho haya maana yake Wizara itakuwa bado haijaanza kutekeleza wajibu wake ambao ndio umefanya iundwe. Lakini pamoja na sababu hizo sisi kwenye Kamati tumejadili kwa kina tumeridhika na madhumuni ya mabadiliko haya na kimsingi tumeunga mkono. Hata hivyo tunashauri baadhi ya mambo kadhaa ikiwemo eneo la kwanza ambalo tunapenda kushauri ni kwenye Ibara ya 14 ya Sheria hii ya Export Processing Zone, kanda maalum hii ya kiuchumi. Kwenye Ibara ya 14(1) imetaja muundo wa Bodi ya EPZA. Kwenye muundo huu wa bodi Mtendaji Mkuu wa Bodi ndiye anakua Katibu wa Bodi, na huko nyuma Waziri ndio alikuwa Mwenyekiti wa Bodi. Lakini kwenye composition kwenye muundo huu wako Makatibu kadhaa wanaingia kwa nafasi zao katika Bodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, yupo Katibu Mkuu anayehusika na Wizara ya Fedha, Katibu Mkuu Waziri ya Maji, Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, wote ni Wajumbe kwenye Bodi hii, lakini kwenye mabadiliko bado hawajaleta. Tunatamani kuona kwamba na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji naye aingie kwenye Bodi kwa sababu Makatibu wenzake wote wanakuwa ni Wajumbe wa Bodi, kwa hiyo ni vizuri na yeye akawepo hapo kwenye Bodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo tungependa kuipongeza Serikali ni hii dhana nzima ya kuitoa sasa kwenda kuondoa hiki Kifungu cha 4, kuondoa neno “Minister responsible for industries”. Kwa maana kwamba kwa kuliondoa hili neno linafanya sasa kwamba wakati wowote Mheshimiwa Rais anapoweza kutoa hati idhini kwenda Wizara yoyote, anaweza akahamisha majukumu ya Special Economic Zone ama Export Processing Zone kwenda mahali popote bila kuleta mabadiliko ya sheria. Kwa sababu tayari eneo hili limefanyiwa marekebisho ya jumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa nafasi ili nami niweze kuchangia mpango huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka tu niseme kwamba tumepata somo zuri kutoka kwa Profesa, amezidi kutufundisha kwamba kuna maeneo ambayo sisi kama Taifa ni lazima tuongeze umakini na tuyafanyie kazi kwa uharaka ili tuweze kwenda kufanana na wenzetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, na nikianzia pale alipoishia alipokuwa anazungumzia uwezo wa NDC kuweza kuendesha mradi mkubwa kama ule ya kule Liganga na Mchuchuma. Ni kweli wasiwasi huo si yeye tu anao lakini naamini Wabunge wengi hasa wanaotoka maeneo hayo wanajiridhisha hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi leo mchango wangu ulikuwa ujikite sana kwenye suala zima la sera, Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alipata kusema kwamba ili tuendelee tunahitaji mambo manne. Tunahitaji ardhi, watu, siasa safi na uongozi bora. Hapa kwenye siasa safi ndipo ambapo tunapata zile sera (policy).

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Taifa letu katika kipindi cha miaka mitano ya Serikali ya Awamu ya Tano, Serikali iliyopita tumefanya mabadiliko mengi sana ya sheria mbalimbali, na nyingine pia kuziboresha kupitia Miscellaneous Amendments lakini hatukugusa kwenye sera; na ili tuwe na sheria tunaanza kwenye sera.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mawaziri wote hapa wa sekta hakuna hata mmoja ambaye sera yake ni ya wakati tuliokuwa nao, sera nyingi Serikalini zimepitwa na wakati sera nyingi zimekuwa kuukuu kiasi kwamba hata mipango mizuri tunayoipanga kwa sera zilizopo bado itakuwa ni vigumu kutekelezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakupa mfano tu kwenye eneo hilo la viwanda na biashara Sera ya Maendeleo Endelevu ya viwanda (Sustainable Industry Development Policy) 1996 hadi 2000. Leo tuko mwaka wa 2021, miaka 21 hakuna sera wala hakuna mabadiliko yoyote yanayofanyika huko, ama wamelikalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukija kwenye Sera ya Maendeleo ya Viwanda Vidogo na Biashara Ndogo (Small and Medium Enterprises Development Policy 2003), hii Wizara imeikalia tangu 2011 wameanza mchakato mpaka tunavyozungumza mchakato bado unaendelea, kwa hiyo hilo ni tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukienda kwenye Sera ya Taifa ya Biashara (National Trade Policy – NTP 2003) nayo ni hivyo hivyo, mchakato unaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa, kwa bahati mbaya sana sheria iliyoanzisha viwanda ni ya mwaka 1967 tukiwa katika ujamaa mkongwe kabisa. Sasa hivi tupo katika angalau utandawazi hata sekta za viwanda inashikiliwa zaidi na sekta binafsi siyo viwanda vile ya umma ambapo wakati huo mashirika kama TIRDO kama SIDO na halikadhalika ndiyo yalikuwa yanaweza ku-back up. Kwa hiyo utaona kabisa kwamba ndiyo maana hata eneo la viwanda na biashara kipindi hiki hatufanyi vizuri, kwasababu sera bado imepitwa na wakati lakini sheria yenyewe iliyoanzisha, Sheria ya Viwanda pia imepitwa na wakati sana, ya 1967.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ningependa sana na eneo hili nadhani ni Ofisi ya Waziri Mkuu ndio wanaosimamia sera, ebu tuwape hawa Mawaziri wa Kisekta muda kabisa wa kuhakikisha kwamba sera hizi zinaenda kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, na nimefurahi sana, juzi Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan alipotoa angalau muda wa miezi mitatu kwa Waziri wa Uwekezaji kwenda kutengeneza Wizara, hilo ni jambo zuri, kwamba ni lazima tuwape muda. Tusiishie tu kwamba Waziri amepewa nanii anaondoka bila kumpa muda kwamba tunataka kipindi fulani tuwe tumeona sera ambayo imekamilika ili mambo yetu yaweze kwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sera ya Ajira ni ya mwaka 2008. Hivi tunavyozungumza tunataka ajira milioni nane, ziko katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi, lakini Sera ni ya mwaka 2008 inawezekana kabisa kuna mpishano kubwa kati ya Sera na mipango yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ni lazima tuone kwamba mipango tunayoiweka na sera tuliyokuwa nayo ni kwa kiasi gani vinashabihiana ili kuweza kuzalisha zile ajira 2008. Sera ya Vijana ni ya mwaka 1998 Sera ya Michezo ya mwaka 1995. Sanaa ya Michezo ambayo sasa hivi tunaona kwamba eneo hili linachangia pato, nadhani ni la pili baada ya utalii, lakini sera yake ni ya mwaka 1995 ndiyo maana tunaona hata wasanii au kwenye michezo wanajiendesha wenyewe wenyewe hakuna mpango ambao Taifa kama Taifa tunaweza tukaona kama katika eneo la Michezo tunakwenda kwa mwelekeo upi. Kwa hiyo ni lazima Mheshimiwa Bashungwa fanyia kazi eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na ndiyo maana hata Club ya Simba inapata taabu katika kuingia kwenye uwekezaji kwasababu michezo bado inaonekana ipo katika ridhaa, ilhali sasa hivi michezo ni sehemu ya Uwekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sera ya Mambo ya Nje, diplomasia ya uchumi haijaandikwa popote, tunazungumza tu. Tupo katika diplomasia ya uchumi, lakini hakuna mahali popote kwamba kuna sera inaelekeza hivi, tutakuwa na waambata wa kibiashara katika balozi zetu tutakuwa na hiki, hakuna! Tunaizungumza mdomoni lakini lakini kwenye Makabrasha hakuna (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hili nalo ni eneo muhimu sana, tulitazame, hasa katika eneo hili la Kilimo ambapo tunatamani kuona kwamba mazao ya wakulima wetu yanavuka mipaka na kwenda kushindana na maeneo mengine. Sasa ni lazima sera hizi zisimamiwe na tuwape muda tuhakikishe kwamba tunakuwa na sera madhubuti zinazoweza kusimamia mpango wetu wa maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwenye elimu huku nako kuna double standard. Kuna wakati Waziri anatumia sera ya mwaka 1995, kuna wakati anatumia 2004, inategemea tu umembana katika angle gani, kwa hiyo anatafuta upenyo kwa kupitia sera. Kwa hiyo ni lazima tuwe specific, kwamba kwa elimu yetu tunatumia sera ya mwaka gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ya 2004 ndiyo ilituelekeza kwamba elimu ya Msingi iishie darasa la Sita, lakini hata Mtaala wa elimu ukaelekeza hivyo ndiyo maana miaka miwilli mitatu huko nyuma hakukuwa na vitabu vya darasa la saba. Baada ya kuanza kuhoji hili jambo nadhani wamenyofoka katika maeneo fulani fulani wametengeneza Mtaala wa Darasa la Saba; lakini kimsingi ilikuwa kwamba elimu ya msingi iishie darasa la saba katika kuboresha suala zima la elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe sana kwamba eneo hili Serikali tunaomba kwamba tuboreshe sera zetu katika sekta zote ili ziweze kuendana na mipango hii mizuri ambayo tunaiweka ili ziweze kusaidia Taifa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa nafasi hii ya kuweza kutoa mchango katika hoja ambayo iko mbele ya Bunge lako Tukufu. Nianze kwa kumpongeza sana dada yangu Mheshimiwa Ummy Ali Mwalimu ambaye hapo nyuma alikuwa ni Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Tanga na sasa tumemkabidhi Jimbo la Tanga Mjini na kazi inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze rafiki yangu Mheshimiwa Silinde na Ndugu yangu Dugange kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya, lakini kipekee nimpongeze sana Katibu Mkuu Profesa Riziki Shemdoe. Huyu ni kijana wangu anatoka kabisa pale Mlalo, kwa hiyo, hayo ni matunda ya Mlalo. Pia niwapongeze Ndugu Magembe na Ndugu Gerald Mweri kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba mchango wangu ujikite sana kwenye eneo zima la elimu na nitaanza katika ngazi ya Halmashauri ya Lushoto ambayo ni halmashauri ya nne nchini kwa kuwa na shule nyingi za msingi. Halmashauri ya Lushoto ina shule za msingi 168, shule hizi ni nyingi sana ambazo nadiriki kusema kwamba kwa ngazi ya Halmashauri tunashindwa kuziendesha sisi wenyewe, hivyo, tunaiomba Wizara na Mheshimiwa Ummy yeye alikuwa Mbunge wa Viti Maalum anajua, watusaidie tutengeneze Kanda Maalum ya Kielimu ya Lushoto, vinginevyo mara zote mtatuona shule za Lushoto zikiwa za mwisho katika mitihani mbalimbali kwa ngazi zote kuanzia msingi mpaka sekondari.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Lushoto imetawanyika sana kwa sababu ya safu ya Milima ya Usambara, kwa hiyo, hata jiografia yake ni ngumu sana kufikika kila mahali na hiyo pia inachagiza hata watumishi mara zote wanapoletwa Lushoto, hasa Wlimu, wanahama na kuhamia Wilaya nyingine za bondeni ama mkoani kwa ujumla. Kwa hiyo, tatizo kubwa ni jiografia ambayo sasa inaathiri utoaji wa elimu na upatikanaji wa elimu bora, kwa hiyo, niombe sana, ukiangalia mgawanyo wa baadhi ya halmashauri, kwa mfano nitasema Mafinga Mjini kwa ndugu yangu, shemeji yangu, Mheshimiwa Chumi, shule za msingi katika Halmashauri ya Mafinga ni 28, ukienda pale Korogwe Mji ni 36, ukienda Pangani ni 36, lakini ukienda Mlele kwa Mheshimiwa Kamwelwe pale wana shule 13 katika halmashauri nzima, utawezaje kutoa mgao sawa na halmashauri yenye 168? Hii kwa kweli ni dhahiri kwamba, jambo hili lazima liratibiwe upya na tuweze kuwa na mgawanyo ambao unaeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukija kwenye Walimu; Walimu waliokutwa na vyeti fake katika Halmashauri ya Lushoto walikuwa 216, lakini hatujarejeshewa idadi hiyo, isipokuwa tulikuwa tunapata tu mgawo huu wa kawaida wa Walimu 16, Walimu 24, Walimu 60 na katika awamu hizi zote tatu za nyongeza ya Walimu. Kwa hiyo, niombe sana kwamba, wale ambao wametoka kwa sababu ya vyeti fake 2016 tungepata idadi kamili ile irudi ili iweze kusaidia katika eneo hilo. Hivi ninavyozungumza tuna uhaba wa Walimu 1,274 katika Halmashauri ya Lushoto kwa hiyo, utaona kwamba ni tatizo kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niingie katika eneo lingine ambalo hili ni la kitaifa. Kuna tatizo kubwa ambalo tunalo katika mgawanyo wa hizi fedha ambazo zinakwenda kwenye capitation. Serikali imeweka utaratibu mzuri tu ambao tangu mwaka 2016/2017 tulitenga zaidi ya shilingi bilioni 219, lakini mwaka 2017/2018 bilioni 220, mwaka 2018/2019 shilingi bilioni 286, mwaka 2019/2020 shilingi bilioni 288 na mwaka 2020/2021 shilingi bilioni 298. Ni jambo jema kabisa kila mwanafunzi kati ya wanafunzi milioni kumi n amia tano wa shule za msingi wanapata Sh.10,000, lakini pia wanafunzi milioni 2,200,000 wa shule za sekondari pia wanapata shilingi 10,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hoja iko pale kwenye ile pesa kuna shilingi 4,000 hii inakatwa kwa ajili ya vitabu, inayokwenda shuleni ni shilingi 6,000 ambayo na yenyewe ina mgawanyo wake; kuna ambazo zinakwenda matumizi ya ofisi asilimia 35 kwenye ile shilingi 6,000; taaluma asilimia 30 kwenye shilingi 6,000; mitihani asilimia 15 kwenye shilingi 6,000; huduma ya kwanza asilimia 10 na ukarabati asilimia 10 ambapo ukiangalia asilimia 10 hizi ni kama shilingi 600. Sasa sijui ukarabati wa Sh.600 tunakarabati nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hoja yangu iko kwenye zile shilingi 4,000 ambazo zinakuwa retained kwa ajili ya ununuzi wa vitabu. Ni masikitiko makubwa kwamba, ndani ya kipindi cha miaka hii mitano vitabu vimeanza kusambazwa takribani miezi mitatu iliyopita, mimi ndio nimeona vitabu kwenye Halmashauri ya Lushoto. Bahati mbaya sana vitabu vyenyewe vimekuja kwa ratio ya wanafunzi watatu kwa kitabu kimoja. Sasa ninajiuliza kwamba, hizi hela zote zilizotengwa kwa miaka mitano ambazo ni takribani shilingi 200,000,000,000, zimefanya kazi gani na zilikuwa zimewekwa kwenye akaunti gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama vitabu vimechapishwa kwa mara moja tu, tutaona kabisa kwamba hapa kwenye Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kuna tatizo, lakini pia kwenye Wizara inayosimamia sera, kwa maana ya Wizara ya Elimu, kuna tatizo. Tukumbuke kwa mara ya kwanza walichapa vitabu vya shilingi 144,000,000,000 ambavyo vilikuwa vimekosewa na vikaondolewa kwenye mzunguko. Hatujawahi kuambiwa ndani ya Bunge hili kwamba, wale waliotia ile hasara wamechukuliwa hatua gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaendelea kuchukua hatua mbalimbali huko za watu, wahujumu uchumi na kadhalika, lakini katika eneo hili hatujawahi kuona shilingi 144,000,000,000 ambazo vitabu vimechapishwa havina ubora, lakini pia vimekosewa, havikuwa na maudhui, wala havikuwa vinafuata hata mtaala husika, vimeondolewa katika mzunguko kimya kimya na vimewekwa kwenye maboksi vimeachwa huko huko kwenye shule wala hawajavikusanya, hatuambiwi hasara hii ambayo Taifa tumeipata ni watu wangapi wamewajibika kwa kosa hili? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana hizi ni zama za kuambiana ukweli. Tunaomba kabisa kwamba tusicheze na elimu, kwa sababu haya matatizo yote tunayoyaona sasa hivi ni kwa sababu tulikuwa tunaifanya elimu kama ni jambo ambalo sio la msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana tupate majibu na hizi ni takwimu sahihi kabisa kutoka Serikalini huko. Watueleze pesa zetu hizi za vitabu kwa miaka mitano na vitabu vimepelekwa katika awamu hii, tena miezi mitatu iliyopita na bado vimepelekwa kwa ratio ya watoto watatu kwa kitabu kimoja kwa mujibu wa halmashauri yangu. Ningependa sana kuona kwamba kama tunasema kila mwanafunzi anapata Sh.4,000 kwenye capitation, tulitaka kuona kwamba wanafunzi nchi nzima wanapata vitabu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo kwa kuwa sasa tunakwenda katika ulimwengu wa TEHAMA ningeomba sana kwamba kwenye capitation hii tuangalie sasa uwezekano wa kuanza kwenda kupeleka ipad ama computer mpakato kwa wanafunzi ili waanze kusoma kwa kujifunza mambo ambayo yanabadilika katika dunia hii ya leo. Tunakwenda katika artificial technology ambayo TEHAMA ndio inayotawala ulimwengu sasa tutakapokuwa tunaendelea kupeleka hela za vitabu, lakini tuone pia umuhimu wa kuangalia eneo zima hili la teknolojia kwa sababu sasa hivi umeme vijijini umeendelea kwenda na maeneo mbalimbali sasa umeme upo. Kwa hiyo, naamini kabisa kwamba, tukiweka hivyo tutawasaidia hawa vijana wetu kujifunza kwa vitendo kwenye dunia ambayo wanakuja kuitawala siku za usoni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru dada yangu Jacqueline Msongozi kwa kunitunuku cheo ambacho amekitamka muda si mrefu hapa Bungeni. Nami naahidi nitatenda mema kulingana na ukubwa wa cheo alichonipatia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ambayo ndiyo imekipatia chama hiki ushindi ukurasa wa 177 tunayo barabara yetu ambayo imewekwa pale kwa ajili ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kilometa 278 kutoka Same – Mkomazi – Umba Junction ambapo unaipata Tarafa ya Umba kwa Kata za Lunguza, Mng’aro na Mnazi kwenda Mabokweni kwa ndugu Kitandula, kufika Maramba kuunganisha na barabara inayokwenda Horohoro kwenda Mombasa na kurudi Tanga Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ni muhimu sana na ni barabara ya kimkakati. Kwanza iko pembezoni mwa mpaka wa Tanzania na nchi jirani ya Kenya. Lakini pia iko pembezoni kabisa inazunguka hifadhi ya Taifa Mkomazi. Na huku ndiko kule kwenye mazalia pekee ya vifaru ambao tunawatumia katika Taifa letu hili kama kielelezo miongoni mwa vielelezo vya urithi wa Kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninamuomba sana Waziri mwenye dhamana kwamba wakati tunajadili barabara hii huko nyuma ulikuwa ni Katibu Mkuu wa Wizara unayoiongoza sasa. Sasa unakwenda kusimamia Sera na Chama Cha Mapinduzi kitakuja kukuuliza ni kwa namna gani umezitekeleza sera zinazotokana na Ilani ya Chama chake. Kwa hiyo, tuanomba uweke msisitizo sana katika hili eneo la upembuzi na usanifu wa kina ufanyike kwa haraka ili tangawizi kutoka Mambamlyamba, tangawizi kutoka Mbaramo, na Mnazi ziweze kwenda kwenye masoko ya Mombasa na Tanga Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Mombo – Lushoto kilometa 36 na wewe umeipita lakini ninafaharika pia kusema kwamba na Mheshimiwa Rais wa Awamu hii ya Sita amepita katika barabara hii alivyokuja Mlalo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, barabara hii ni nyembamba mno na sasa hivi Wilaya ya Lushoto imekuwa na magari mengi sana ya usafirishaji wa mboga mboga na matunda lakini pia na mabasi. Kwa hiyo, barabara hii magari lazima yapishane kwa kusimama kwenye makona ili anayeshuka na anayepanda aweze kupishana vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sasa, tumeshazungumza mara nyingi kwenye vikao vyetu vya RCC na tunavyopitisha bajeti katika RCC, tunavyopeleka Serikali Kuu, Engineer Mfugale mara zote alikuwa anaziondoa hizi bajeti zetu. Tunaomba sasa zisimamiwe. Barabara hii ni barabara muhimu sana. Watanzania wanajua kwamba ukiondoa Ikulu ya Dar es Salaam kabla ya hii tuliyojenga Chamwino juzi, Ikulu kubwa nyingine tangu wakati wa mkoloni wa Kijerumani ni ile iliyoko Lushoto. Kwa hiyo, barabara hii ni muhimu sana kwa sababu hapa ndipo penye Ikulu kubwa ukiondoa Dar es Saalm kabla ya hii ya Chamwino. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya kutoka Lushoto – Magamba – Mlalo kilometa 33. Hii imekuwa na ahadi nyakati zote lakini pia ikiwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu hii ya Sita alivyokuja Mlalo alituahidi kwamba barabara hii tutahakikisha kwamba inajengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wameshaanza lakini walikuwa wanafanya awamu ya kilometa tano, tano. Mwaka jana yalitokea mafuriko ambapo Naibu Waziri mwenye dhamana hiyo ambaye sasa hivi ni Waziri wa Ulinzi Mheshimiwa Kwandikwa alikuja pale na akaahidi kwamba Mwaka huu wa Fedha angalau ataijenga kwa kiwango cha kilometa 10. Ninaomba sana kwamba bajeti hii kabla haijapita lazima eneo hili mliangalie kwa kina. Tunapozungumza mazao yanayolimwa Lushoto ni mazao yanayoharibika kwa wepesi. Viazi, karoti, matunda na mboga mboga. Hivi viazi ambavyo vinafanya wale wa mjini wanaitwa ‘baby’ japo ni wazee wazima vinatoka Lushoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo. Engineer tunakuomba sana kwamba uende ukatenge hii fedha kama ambavyo ilikuwa ni ahadi ya Serikali ya Awamu ya Tano lakini kazi inaendelea. Tunaamini kabisa kwamba Serikali ya Awamu ya Sita itatekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuwa mzungumzaji wa kwanza katika Wizara hii ya Teknolojia ya Habari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitumie nafasi hii kukupongeza wewe binafsi kwa imani ambayo Wabunge wamekuwa nayo juu yako na kukurudisha katika kiti cha enzi, na ninaamini kwamba utatuombea dua na siku ya Jumamosi mambo yatakuwa mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Waziri mwenye dhamana ya Wizara hii, lakini pia nimpongeze Naibu Waziri, Mheshimiwa Eng. Andrea Mathew Kundo pamoja na Katibu Mkuu, Dkt. Chaula, lakini pia na Naibu Katibu Mkuu Jim Yonazi, kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii bado ni mpya kwa maana ya kuundwa hivi karibuni lakini mambo ambayo inafanya ni mambo ya siku nyingi. Na Wizara hii imeundwa mahususi kabisa kuja kuwasaidia Watanzania na hususan vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Ilani ya Chama chetu Cha Mapinduzi katika ukurasa wa 96, imezungumzia suala la uwekezaji na kuwezesha mashirika kimitaji na kimenejimenti. Kwa bahati nzuri sana menejimenti iliyopo sasa chini ya Mtendaji Mkuu wa TTCL Waziri Kindamba, anafanya kazi nzuri sana, na kama Serikali ikimpa ushirikiano tunaoutaraji ambao umeelekezwa katika ilani wa uwezeshaji wa kiuchumi na kimenejimenti, maana yake shirika hili litakwenda mbali sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa masikitiko makubwa kama ambavyo mmesikia ripoti ya Kamati hapa inaonesha kwamba madeni makubwa ambayo TTCL anadai yamesababishwa na Serikali. Kwa hiyo, Serikali yenyewe imekuwa sasa ndio muuaji wa mashirika yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo katika eneo hili hatutakubali kwa sababu tumekukabidhi tools za kusimamia Wizara hii kupitia ilani ya chama, kwa hiyo chama tutakuuliza; tumekupa ukaue shirika au ufanye shirika lifanye kazi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa ripoti ya CAG, takribani bilioni 40 zinadaiwa kupitia Mkongo wa Taifa. Kamati hapa imeeleza kwamba na yenyewe inaona takribani dola milioni 68 za Mkongo wa Taifa ni deni kutoka TTCL. Kwa hiyo, tunaomba sana kwamba eneo hili tulisimamie vizuri ili shirika hili liweze kushindana na mashirika binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe hatujaweka mtaji wowote mkubwa kwa kipindi cha takribani miaka kumi mpaka kumi na mbili wakati kampuni hizi binafsi karibia kila mwaka zinaweka mtaji wa dola 100,000 mpaka 150,000. Katika hali ya kawaida hatuwezi kufanya Shirika hili lishindane. Kwa kweli tunaomba sana Shirika hili lijengewe uwezo, uwezo wa management upo na tunaridhika nao lakini uwezo wa mtaji ndiyo jukumu la Serikali hasa kupitia madeni …

MWENYEKITI: Mheshimiwa Shangazi makampuni binafsi hayaweki dola laki moja wanaweka dola milioni mia moja kila mwaka. (Makofi)

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa sahihisho hilo, sasa nadhani Mheshimiwa Ndugulile amekaa kwa kutulia pale unaweza ukaona kwamba makampuni binafsi wanaweka dola milioni mia moja sisi miaka 12 mpaka 15 hatujaweka chochote. Hata hicho wanachozalisha tunaendelea kukivuna, madeni yale ambayo Serikali inazalisha hatuyalipi. Kwa hiyo, tunaomba suala hili lishughulikiwe na jioni hapa kwenye shilingi tunakuandaa kabisa uwe tayari vinginevyo leo utaondoka bila mshahara hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka nilizungumzie ni kwamba Shirika hili tunataka liwezeshwe kimenejimenti kwa maana kwamba liwe huru kibiashara. Yapo mashirika kama haya kwenye nchi za wenzetu, kwa mfano, kuna Deutsche Telecom Ujerumani, China Telecom, Telecom Egypt, Telecom Namibia, ni Mashirika ya Umma lakini yanajiendesha kibiashara moja kwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa huku tunakoendesha sana kwa kisiasa hivi ndiyo maana wakati mwingine sasa tunayanyang’anya hata mitaji ya kujiendesha na kuyafafanisha na makampuni binafsi, hii siyo sawa. Kwa kuwa vijana tuliowakabidhi wana uwezo wa kuliendesha kimenejimenti ni lazima tulipe sasa kazi ya ziada na tupate shirika ambalo linakuwa la matokeo, result oriented. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo napenda kuchangia ni TCRA. Hapa napo kuna shida, sisi kama Taifa ni lazima tutangaze utamaduni wetu kimataifa na hili eneo zile TV za kulipia (Pay TV) zinafanya kazi nzuri sana, lakini zinazuiliwa kuweka matangazo katika zile channel zao ambazo zipo katika Pay TV. Kwa mfano, Azam Media kupitia Cinema Zetu ambapo wote tunafahamu kwamba tasnia ya Bongo Movie na Bongo Fleva wanaitumia sana ku-promote muziki wao, hawaruhusiwi kuweka matangazo wala kuwa na wadhamini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Pay TV ndiyo TV pekee ambazo zinaonekana ndani na nje ya nchi kwa maana kwamba zinakuwa katika ving’amuzi vya ndani na vya nje, kule ndiyo utamaduni wetu unaweza ukaonekana. Utamaduni huu ukionekana kupitia wadhamini na matangazo maana yake uzalishaji wa hizi sinema utakuwa bora zaidi na vijana wengi watapata ajira ya kutosha hapa na matokeo yake na Serikali nayo itapata kodi kupitia matangazo na udhamini. Sasa Serikali inakwama wapi kuziruhusu hizi Pay TV kuweka matangazo na wadhamini? Hii siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, TV kama ya Wasafi, kijana mdogo yule anajaribu kukua, lakini tunamuwekea vizingiti vya namna hii, tunatarajia tuwe na Wasafi nyingi, ni watu wangapi wameajiriwa ndani ya Wasafi Media. Unapowanyima fursa ya kuweka matangazo na kuwa na wadhamini atatokaje huyu kwenda kuzalisha vijana wengine watengeneze maudhui mazuri ili yauzike kimataifa na sisi utamaduni wetu uzidi kukua huko lakini mwisho wa siku Serikali mtapata kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi Azam Media ndiyo inaonyesha mpira katika Ukanda huu wa Kusini mwa Afrika inashindana na TV nyingi za Kimataifa DSTV, GTV na nyinginezo, lakini ile ni sifa ya Watanzania. Mwaka huu wameweka uwekezaji mkubwa, nadhani tutatangaziwa hivi karibuni kupitia ligi ya VODACOM mkataba wa miaka kumi shilingi bilioni 190, haijawaji kutokea. Hiki ni chombo cha Watanzania, hizi ni bidhaa za Watanzania lazima tufaharike nazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapowawezesha hawa ndiyo wanaongezeka akina Baraka Mpenja kule ambapo wanapata ajira, akina Ally Kamula watapata ajira tutakuwa nao, lakini wakina Gift Macha watapa ajira tutakuwa nao. Sasa TCRA hili eneo la kwenye Pay TV matangazo na udhamini tatizo lenu ni nini? Mbona Serikali wakati mwingine mnakuwa na wivu ambao hauna sababu? Kwa sababu kwa kupitia matangazo na huo udhamini tutapata kodi na tukipata kodi ndiyo tutazidi kutanua hii tasnia na itakuwa kubwa zaidi, itaajiri vijana wengi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kabisa kwamba katika ukuaji wa pato la Taifa ina sehemu kubwa sana ya mchango wa sanaa, sasa sanaa yetu itakuwa tu endapo itakuwa inaonekana katika ving’amuzi vya kimataifa na vya ndani kwa sababu sasa ndani tumejitosheleza twende nje, tuwaruhusu hawa waweke matangazo. Utalii wetu pia tutautangaza kupitia hizo Pay TV tukiweka matangazo pale Nigeria, Ivory Coast na kila mahali wataona. Tunalalamika hapa kwamba hatutangazi utalii wetu tunaweza tukautangaza kupitia Pay TV.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii, huo ndiyo ulikuwa mchango wangu kwa siku ya leo. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHES. RASHID SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa nafasi hii. Naomba nichukue nafasi hii kuipongeza sana Wizara, Mheshimiwa Waziri, pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri wanafanya kazi nzuri sana ambayo imeanzia kwenye kule ku-plan jezi ya wekundu wa Msimbazi kwa kuweka lile jina la Visit to Tanzania, naamini kabisa kwamba tutaona athari chanya za neno lile muda si mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kushauri mambo kadhaa katika Wizara hii. Jambo la kwanza nataka niwaarifu Wizara kwamba, Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi inapakana na wilaya nne; Wilaya ya Mwanga, Same kwa Mkoa wa Kilimanjaro, lakini kwa Mkoa wa Tanga, kuna Wilaya ya Lushoto pamoja na Wilaya ya Mkinga. Sasa mara zote Mawaziri wanapofanya ziara wanakwenda Mkoa wa Kilimanjaro pekee. Sasa nataka niwaambie na Tanga ipo kwa maana ya Lushoto na Mkinga, inapatikana Hifadhi ya Taifa Mkomazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule tuna changamoto ya tembo wamevamia katika miji kadhaa hasa katika Tarafa ya Umba, Kata ya Mnazi na Kata ya Lunguza, Vijiji vya Mkundi Mbaru na Mkundi Mtae kule tembo wanasumbua sana. Juzi wamemwona Naibu Waziri yuko Kilimanjaro wakasema huyu Mheshimiwa Naibu Waziri mpaka asikie tumevuna tembo ndiyo afike hapa. Kwa hiyo namwomba sana afike eneo lile akatatuwe matatizo ya wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine nataka nichangie kuhusu soko la utalii. Wizara hii kuna maeneo ambayo inakosea, tunasubiri watalii waje wenyewe Tanzania kwa kutumia tour operators wa Kitanzania. Nataka niwaambie kwenda kwa stahili hiyo ya kuvua samaki walioko kwenye kapu haitatusaidia, ni lazima tujitahidi twende kule ambako wanapotoka. Kuna festival kubwa mbili zaidi duniani; ya kwanza iko kule South Africa ambayo wanaita Indaba, iko kama ile Karibu Festival ya Arusha, lakini hii ya South Africa inakusanya Mataifa ya Afrika, Ulaya pamoja na Mataifa ya Amerika ya Kusini. Hali kadhalika kule Ujerumani Berlin, nako kuna shoo kubwa sana ya mambo ya utalii. Kule ndiko Wizara inapaswa kwenda kukutana na tour operators wa kimataifa wale ndio wanaosukuma watalii kuja katika nchi zetu, lakini tutakapokuwa tunasubiri huku itakuwa sio kazi rahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tumwombe sana Mheshimiwa Waziri sana, yeye ni Mngoni na ame-migrate kutoka South Africa, sasa asikae Wizarani,atoke aende huko duniani akatuletee watalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine nataka kuchangia kwenye eneo la vitalu vya uwindaji. Uwindaji ni sekta ambayo imefifia. Mwaka 2013 tulipata wawindaji takribani elfu 1,550, lakini mwaka 2018 kabla hata ya covid walishuka mpaka 473. Kuna mambo fulani tuliyafanya pale ambayo tulikosea, ikiwa ni pamoja na kuongeza ile tozo ya leseni ya vitalu kutoka dola 30,000 kwenda dola 85,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe sana sisi nchi yetu jiografia imetawanyika sana, mwindaji anapotoka Ulaya, anakuja aidha Kilimanjaro International Airport, Dar es Salaam ama Zanzibar, anahitaji tena kuchukua charter flight kwenda Selous, kwenda Katavi, kwenda Burigi wakati huo kabla haijawa hifadhi kwa ajili ya kufanya huu uwindaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuna gharama nyingine ambazo wanazipata. Hivyo, sasa tutengeneze inclusion ya kupunguza gharama hizi ili tuweze ku-facilitate hizi shughuli za uwindani katika maeneo ambayo yako scattered.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Sekta nzima ya Utalii nataka niwaambie, tuna advantage kwa mwaka huu kwa sababu hata Zanzibar watalii waliopatikana mwaka uliopita na mwaka huu ni wengi zaidi kuliko historia ya utalii Zanzibar. Hii ni kwa sababu covid kote duniani wanajua Tanzania ndio sehemu ambayo ni covid free, kwa hiyo wenzetu Wazanzibari kwenye eneo la utalii watakuwa mashahidi, miaka hii miwili wamepokea watalii wengi sana.

Kwa hiyo na sisi tuboreshe tu mazingira tuangalie tozo zetu zimekaaje tuweze kupata hiyo advantage ya kuwa covid free kwa ajili ya kuvutia watalii wengi sana kuja kutalii katika nchi yetu. Otherwise nawapongeza wanafanya kazi nzuri, waendelee hivyo hivyo. Namshukuru pia hata akienda pale uwanja wa Taifa yeye kama yeye magoli huwa yanakuwa mengi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru kwa nafasi hii. Kabla ya kusema lolote nipongeze kwanza Kamati zote mbili kwa taarifa ambazo kimsingi ndizo kazi tunazozifanya katika Kamati na ndizo kazi za Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninayo machache ya kutoa mchango wangu katika Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa. Ninaomba nishauri jambo; tumepokea miradi mingi sana ya maendeleo katika maeneo yetu kupitia Serikali za Mitaa lakini kuna changamoto kubwa kwamba wataalam wetu walioko katika Wizara hii ya TAMISEMI wamekuwa wakigawa mafungu haya kwa ulingano, kwa maana ya kwamba kama tunajenga shule ya msingi au darasa la shule ya msingi ama sekondari, tunaletewa pesa ambayo inafanana nchi nzima, lakini mazingira ya nchi nzima hayafanani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, Wilaya za Lushoto, Makete, Kyerwa nadhani na Tarime, yale maeneo ambayo zaidi yanalimwa kahawa ni maeneo ambayo ni ya milima. Ukiwapa pesa sawa na sehemu ambayo ni tambarare maana yake haziwezi zikawa na tija ile iliyokusudiwa. Kwa hiyo, tuwaombe sana wataalam wetu waangalie haya wakati wanapanga mipango hii ya Serikali wazingatie jiografia ya baadhi ya maeneo ili tusipewe pesa ambayo inalingana na maeneo mengine hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo lingine ambalo ningependa kutoa mchango wangu ni eneo la mapato ya halmashauri kwa maana ya mapato ya ndani asilimia 20 ambazo zinapaswa kurudi kwenye Serikali za Vijiji. Fedha hizi zilikuwa kipindi cha nyuma wakati halmashauri nyingi zilikuwa zinawajibika kuwalipa Madiwani, zilikuwa hazipatikani vizuri kurudishwa katika vijiji. Sasa kwa kuwa Serikali imebeba mzigo wa kulipa posho za Madiwani tungependa kuona sasa asilimia 20 ikisimamiwa kurudi kwenye Serikali za Vijiji. Maana huko ndiko ambako miradi hii ya Serikali inakwenda kutekelezeka na wasimamizi wakubwa ni Wenyeviti wa Serikali za Vijiji pamoja na Wenyeviti wa Vitongoji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu hawa na ambao wenyewe wanachaguliwa kama sisi, wanakuwa hawapati ruzuku yo yote kutoka Serikalini. Hata hivyo, tunaamini kwa mwongozo uleule uliopo ambao mwanzoni ulikuwa unatumika kulipa Madiwani na sasa dhamana ya Madiwani imekwenda Serikali Kuu hii asilimia 20 basi ni vyema ikarudishwa kwenda kulipa Wenyeviti kwa msisitizo na kusimamiwa kwa mujibu wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningependa kulichangia katika mchango wangu ni suala la asilimia 10 ya fedha hizi za halmashauri ambazo zinakwenda kwenye Mfuko wa Vijana na Wanawake na zile asilimia mbili kwa Wenye Ulemavu. Eneo hili bado lina changamoto, nipo katika Kamati ya LAAC ambako mara kadhaa tumekuwa tukizihoji halmashauri. Unaona mara zote fedha hizi zinaonekana zinaendelea tu kutoka japokuwa kwa tafsiri Mfuko huo unaitwa Revolving Fund, ni fedha ambayo inatakiwa itoke kisha irudi, lakini mara zote tukija tunaona tu kwamba zinatoka zile zinazorudi halmashauri zimekuwa na usimamizi hafifu katika kusimamia sheria na kufanya zile fedha zirudi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi ningependekeza, kwamba hili jambo kwanza msisitizo uwepo kwenye Revolving Fund kwamba fedha zikishakopesha zirudi. La pili, Serikali itazame model nzuri zaidi ya kuja na jambo hili. Sasa hivi halmashauri zote zinatenga sawa asilimia 10, lakini hazilingani mapato, nadhani wangetumia model ya Mfuko wa Jimbo ambao unatumia population.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli inawezekana Wilaya ya Lushoto ina population kubwa lakini mapato yake ni madogo na kuna wilaya nyingine ni ndogo, lakini mapato yake ni makubwa. Sasa huu wingi wa vijana ukawa unatofautiana, hivyo wa Lushoto pamoja na wingi wao wakapata kidogo kwa sababu mapato yao ni madogo. Kwa hiyo ni lazima kuja na mpango wa ku-centralize haya mapato yote labda katika Mfuko Maalum halafu sasa yaende kwenye makundi haya ya vijana kwa kuzingatia hata fani ambazo wanasoma katika Vyuo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mathalan, sasa hivi tuna vyuo ambavyo wame-graduate mainjia wengi, tunaweza tukaanzisha kampuni ndogo za mainjinia, wakapelekwa katika miradi midogo midogo labda ya barabara, ya usambazaji umeme vijijini, ya maji na kadhalika kwa kupitia Mifuko hii na baadaye tunaweza tukaiona tija kubwa zaidi kuliko ambayo tunayoiona sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba niunge mkono hoja Kamati zote mbili. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii ili na mimi niweze kutoa mchango wangu katika hotuba iliyoko mbele ya Bunge letu Tukufu.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze napongezi kwa ofisi ya Waziri Mkuu kwa kazi nzuri sana ambayo wameifanya. Tumeona utekelezaji wa miradi mbalimbali ambayo hivi punde tumetoka kuikagua katika maeneo tofauti tofauti katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kipekee kupitia hotuba yangu ningependa pia nitoe mchango katika eneo la ukusanyaji wa mapato, nikitoa pongezi kubwa sana kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa namna ambavyo wameendelea na zoezi zuri kabisa la kukusanya mapato bila kutumia mitutu ya bunduki wala bila kufunga biashara za watu. Hii inaonyesha wazi dhamira ya Mheshimiwa Rais, kwamba yeye ana mentality ya kibiashara na ana amini kwamba kupitia biashara ndivyo tunaweza kupata kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningependa kuchangia eneo la mfumuko wa bei lakini nikigusia eneo zima la mafuta. Kama ambavyo mzungumzaji wa mwisho ametoka kusema, ni kweli mafuta yanapopanda bei, maana yake kila kitu kitakwenda kupanda bei; kwa sababu gharama za usafiri, usafirishaji mitambo na kadhalika kwenye maeneo yote ya udhalishaji inategemea nishati ya mafuta.

Mheshimiwa Spika, sasa ni nini muarobaini wa hili jambo? Kwa sasa kwa hali tuliyokuwa nayo ambayo imetokana na vita, baina ya Ukraine na Russia, namna pekee ambayo inaweza kutusaidia ni Serikali kuweka ruzuku katika eneo zima hili la uagizaji wa mafuta ili angalau sasa kuweza ku-stabilize bei.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mfumo wa uagizaji mafuta kwa pamoja, eneo hili ningeomba sana kwa ridhaa yako uwasiliana ikiwezekana na Wizara ya Nishati, angalau tupate semina ya uelewa wa pamoja. Hatuwezi tukakwepa mfumo wa bulk procurement system ambao ndio unaotufanya leo tunatamba kuwa na storage ya mafuta ya siku 36. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama tungeruhusu kila mmoja aagize mafuta kwa wakati wake, tusingeweza kuwa na control hii ambayo leo tunayo na mfumo huu umeanzishwa mwaka 2011 kupitia Bunge lako Tukufu likiwa ni sehemu la mwanzo wa mfumo huu.

Mheshimiwa Spika, mfumo huu umetusaidia sana kudhibiti baadhi ya mambo. Maana yake nini; kwenye mfumo huu wa uagizaji wa pamoja wafanyabiashara wa mafuta wanakutana na viwanda ambavyo vinasambaza mafuta kwa maana ya refineries; tunaangalia bei shindani, na kwenye mamfuta vitu vitatu ni muhimu sana kuzingatia; kwanza reliability, availability, na affordability; hivi ndivyo vitu vitatu vya msingi vya kuangalia wakati wa kuagiza mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapokwenda kupata sasa tonnage watu wote tunapeleka oda zetu kwa yule ambaye ameshinda tenda na anasafirisha mzigo wote kwa wakati mmoja. Anaposafirisha mzigo kwa wakati mmoja maana yake hata shipping cost zinakuwa zimeshuka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zamani wakati kila mmoja alipokuwa anaagiza kutoka kwenye kila kichochoro chake maana yake hata demurrage pale bandarini ilikuwa inaongezeka kwa sababu unasubiri mafuta yako katika meli kumi tofauti tofauti. Lakini leo tunaagiza mzigo katika meli moja kubwa inaleta, hata kama ni metric ton 600,000 zinatua kwa pamoja; demurrage imeshuka kutoka dola 30 hadi 45 kwa siku, sasa hivi dola moja mpaka tatu kwa siku. Kwa hiyo, haya ni mapinduzi makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umuhimu wa mfumo huu ili tuelewe, ndiyo maana nasema lazima tupate semina ya kuelewa hili jambo vizuri. Leo nchi zote zinazotuzunguka hapa zimejiunga katika mfumo wa bulk procurement system. Uganda wamo, Burundi wamo, Rwanda wamo, Malawi wamo, Zambia wamo na DR Congo wimeingia. Hata nchi Mauritius imekuja kujifunza namna bora ya kuingia katika mfumo huu wa manunuzi ya pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kusema, makampuni yanayozalisha mafuta duniani yanafahamika. Kwa hapa kwetu tuna Trafigura au DAX Energy; ya kizawa, tuna GBP ambapo mmiliki ni mwenyeji kutoka Kigoma, anashusha katika Bandari ya Tanga. Kuna Hans Energy, mwenyeji wa Mara, wakati mwingine anashusha katika Bandari ya Dar es Salaam, wanapata hizi tenda. Kwa hiyo, hakuna shida ya kuwa na wasiwasi kwamba eti kuna meli sijui zimepaki Bandarini huko kwenye bahari zina mafuta. Huko ndiko tulikotoka wakati ule tulipokuwa tunaletewa mafuta machafu, ambayo yalikuwa hata ukiweka kwenye magari, kila siku magari yanakufa pampu barabarani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumetoka huko, hakuna businessman mzuri, smart akaweka meli kwenye bahari. Biashara yote inafanyika kwenye mtandao na hii ni kama zilivyo kwenye Bureau De Change, bei ya mafuta kila siku ukiingia kwenye mtandao unaiona. Nasi source yetu ni Arab Gulf ndiko tunakochukulia mafuta zaidi. Ukiangalia kwenye mtandao pale unaona bei ya mafuta kila siku kama ilivyo kwenye stock exchange, hakuna namna kwamba eti utakuta meli imekaa kwenye deep sea huko ambayo siyo ya wizi au siyo ya maharamia iletwe kwenye nchi ambayo ni ya kistaarabu kama Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachoshauri, Serikali iwe na mpango mkakati madhubuti wa kuongeza storage facility katika TIPER. Sasa hivi TIPER tunapokea mafuta lakini bado kwa hali hii ambayo tunayo, ni lazima tuongeze storage capacity ili tuweze kuwa na ujazo wa kuwa na mafuta hata wa miezi mitatu mpaka minne. Ila katika mfumo mzima wa kodi, mfumo huu ndiyo unaotusaidia zaidi. Kwa sababu gani? Pale ambapo makampuni haya ya mafuta yanapotoa order zao, tayari TRA anajua kabisa kwamba kampuni ‘X’ itaingiza metric ton kiasi fulani na kodi yetu tutakusanya kiasi fulani. Hata kama yatapita kwenye mita, lakini tayari mchakato wa awali wa kujua kwamba Serikali inapata kodi kiasi gani unajulikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, niwaambie, mafuta ndiyo bidhaa pekee ambayo inalipiwa kodi zote kabla hata hayajaanza kutumika. Inapoanza kuwa discharged kutoka kwenye meli kwenda kwenye matenki yale ya kuhifadhia, tayari pale kodi zote za Serikali zinakuwa zimelipwa. Kwa hiyo, huo mfumo umetusaidia sana kama Taifa na ningeomba sana wala tusiuguse. Kama kuna maboresho yanaweza kufanyika, lakini kwa tunavyokwenda mpaka sasa uko vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo ningetaka kuchangia ni MSD. Bohari ya Madawa haifanyi kazi vile inavyopaswa. Tuna shida kubwa sana katika Bohari ya Madawa kwa maana kwamba Halmashauri nyingi tumeweka fedha pale ili tuletewe vifaatiba na vitendanishi, lakini hivi tunavyozungumza ni zaidi ya miezi sita hakuna vifaa ambavyo vinapatikana katika hospitali zetu. Sasa jukumu la Bunge ni kusimamia na kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Spika, tunaomba Bunge lako Tukufu lielekeze Serikali kama MSD kazi imewashinda, basi atafutwe mtu ambaye anaweza kwenda kusimamia ile kazi vizuri. Huko nyuma tumeona walikuwa na mpango mzuri sana. Walikuwa na mpango mzuri kiasi kwamba waliwahi kupata tender ya kusambaza dawa katika nchi zote za SADC, lakini nadhani kwa haya yaliyotokea hapa nyuma na kushindwa kufanya kazi zao kwa ufanisi, hata ile kazi ambayo ingeweza kuingizia Taifa kipato sasa imekwenda kwenye eneo likinge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno hayo, nakushukuru sana. Ahsante sana kwa nafasi hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji wa kwanza katika Wizara hii. Kipekee sana nampongeza sana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana katika Wizara hii. Sambamba naye nampongeza pia Naibu Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya bila kuwasahau Makatibu Wakuu wote wawili na Watendaji wote wa Wizara hii ambayo ni nyeti sana kwa kuhudumia shughuli mbalimbali za Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo ni mwaka mmoja tangu Mheshimiwa Rais alihutubie Bunge lako Tukufu, maana alihutubia Bunge hili tarehe 22 mwezi wa Nne 2021. Kwa hiyo, leo ni mwaka mmoja tangu hotuba yake aitoe ndani ya Bunge hili na katika mchango wangu nitapenda nianze na nukuu ambayo ameitoa wakati anahutubia Bunge. Alisema: “Serikali itaendelea kutekeleza kwa vitendo dhamira yake ya kuwa Serikali anayoiongoza na itaendeleza jitihada za kuimarisha maadili, nidhamu, uzalendo, uchapakazi na uwajibikaji.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia aliahidi pia kusimamia haki na stahiki za watumishi wa umma na watendaji Serikalini ili kuongeza ari ya kufanya kazi kwa bidii na kukuza uwajibikaji wa hiyari katika utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais na mara zote Mheshimiwa Rais alikuwa anatembea katika vitendo vyake. Na tumeona, baada ya ahadi hii alianza kazi kubwa ya kwanza kupandisha madaraja jambo hili ambalo lilikuwa limesimama kwa muda mrefu sana tangu mwaka 2016/2017 lakini kwa mkupuo alikuja kupandisha madaraja watumishi takribani 190,761. Hali kadhalika kuna watumishi wengine takribani 926,190 watapandishwa madaraja na wako katika hatua mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mchango wangu nilipenda pia kusema eneo moja kwamba katika upandishaji huu wa madaraja kwa mkupuo, tunashukuru kwamba una faida hii; kwamba tumewapandisha kwa mkupuo lakini katika ule mkupuo kuna wale ambao sasa walikuwa wamecheleweshwa sasa kwa kuwapandisha kwa mkupuo maana yake inabidi wale wachache ambao sasa wana sifa za ziada ambazo walicheleweshwa nao tuwabaini ili waweze kusongezwa mbele zaidi ya madaraja. Hii itasaidia pia kuwapatia stahiki zao kwa mujibu wa sheria na baadhi yao wengi wanakaribia kuelekea kustaafu. Maana yake ni kwamba hata mafao yao yaweze kupangwa kulingana na madaraja hayo mapya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo tumeona pia upandishaji wa vyeo, kwamba tumeona wanaendelea kupanda vyeo katika nafasi mbalimbali; na sasa wanakaribia kufikisha watumishi takribani 25,000 ambao wamepandishwa nafasi mbalimbali katika utumishi wa umma.

Mheshimiwa Spika, jambo hili linaonesha ile dhamira ya dhati ya Mheshimiwa Rais ya kuongeza ari na uwajibikaji Serikalini, na hii pia inachagiza, ni sehemu ya motisha, ya watumishi ya kuendelea kujitoa na kuendelea kuwajibika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nataka niseme moja ambalo ninaamini kabisa kwamba kwa ninavyomwamini Mheshimiwa Rais hawezi akaacha lipite hivi hivi; hili la kuhusu kupandisha mishahara ya watumishi wa umma. Hili ni jambo ambalo muda mrefu sana halijafanyiwa kazi, takribani sasa ni miaka sita. Lakini kwa ahadi hizi ambazo ameendelea kuzitimiza hata hili ninaamini siku ile ya Meimosi ambayo ndiyo aliyotoa ahadi na haya yote ameweza kuyatekeleza ndani ya kipindi cha mwaka mmoja naamini kabisa kwamba inawezekana kabisa kwa bajeti hii iliyotoka, Trilioni 36 mwaka 2021/2022 na hii ya mwaka 2022/2023 ambayo tunasoma takribani Trilioni 41 sitaki kuamini kwamba fedha zote hizi zinakwenda kwenye miradi, ninaamini kabisa kwamba na watumishi safari hii na wenyewe watatoka kifua mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo hili ni muhimu sana, kuongeza motisha ya wafanyakazi kupitia mishahara kwasababu kwanza tutambue watumishi hawa ni sehemu ya kodi za Serikali, kupitia mishahara yao Serikali inakusanya kodi; kwa hiyo tunapowaongeza maana yake pia tutaongeza kodi hapo baadaye kupitia mishahara ya watumishi, kwa hiyo kwa hali ilivyo sasa ya mfumuko wa bei na upandaji wa gharama mbalimbali za maisha, mimi naamini kabisa kwamba ni wakati sahihi kabisa kwa watumishi nao sasa kuweza kuonwa kwa jicho hili la huruma la Mheshimiwa Rais na wenyewe sasa waweze kupambana na hali hii ya kimaisha, lakini pia kuongeza tija na uwajibikaji katika utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo ningependa kulichangia ni katika fungu 40 ambalo sasa hili ni fungu maalum kwa ajili ya Ofisi ya Rais Ikulu; hili fungu ni muhimu sana. Na katika bajeti hii ambayo imepita tumetenga takribani Shilingi bilioni 24.5 na hadi mwezi Machi zimeshatumika bilioni 18.3. Hili ni eneo muhimu sana Waheshimiwa Wabunge, hizi ndio fedha ambazo zinamwezesha Rais kufanya kazi hizi kubwa ambazo tumeziona katika kipindi hiki kifupi. Hii ndiyo kazi kubwa ambayo zile trilion zilizokuja kwenye madarasa kwenye maji, kwenye afya na maeneo minjini yote zimetokana na fungu hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni vizuri sana tumtengee Rais fedha hizi za kutosha aweze kuzunguka maeneo mbalimbali katika dunia; lakini pia zimesaidia hata kukuza mitaji na uwekezaji, kwasababu tumeona hata hivi karibuni Mheshimiwa Rais alikuwa katika Falme za Kiarabu amefanya kongamano kubwa la expo kule ambako amekutana na wafanyabiashara na wawekezaji kutoka maeneo mbalimbali. Hii yote ni mitaji ambayo inatokana na kazi nzuri sana ya fungu hili. Kwa hiyo fungu hili ni vizuri sana hata wakati wa kupitisha tupitishe kwa sauti kubwa ili sasa tumpe funguo Mheshimiwa Rais ya kwenda kututafutia mafungu mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, halikadhalika Filamu ya Royal Tour ambayo ameizindua hivi karibuni kule Marekani, na tutaanza sasa uzinduzi wake katika Taifa letu, hili nalo ni eneo mahsusi sana la kimkakati kwa ajili ya kukuza utalii wa Watanzania. Tunaona kabisa kwamba dhamira njema hii ya Mheshimiwa Rais kupitia kazi ambayo ameifanya katika filamu ile yeye mwenyewe kuwa kama ndiye tour guide namba moja wa Taifa sasa iwe wake up calls kwa tasnia nzima ya utalii, lakini pia na Wizara nyingine zote kufungamanisha eneo hili la utalii, na pia kukuza uwekezaji na mitaji katika maeneo mengine kwa sababu sasa Tanzania inatangazika katika maeneo mbalimbali duniani kupitia hiyo loyal tour. Kwa hiyo hapa ndipo nilipotaka nielezee kumuhimu mkubwa sana wa fungu hili la 20 ambalo ni ofisi mahsusi ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Eneo la mwisho ambalo nilitaka kulichangia ni eneo la uhaba wa watumishi katika maeneo mbalimbali ya huduma za kijamii hasa elimu na afya. Tumeona kwamba kuna ahadi ya ajira mpya takribani 32,000. Tunaomba sana hivi ajira zitangazwe kwa haraka na zibainishwe vizuri, maana wametokea matapeli ambao wanachanganya vijana wetu. Kwa hiyo ni vizuri kwenye tovuti za Serikali mambo haya yawe hadharani ili wananchi waweze kupata fursa ya kuomba ajira hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii. Nami naomba kwanza niunge mkono hoja ya Mheshimiwa Omari Kigua kwa namna ambavyo hali ipo huko mtaani ni lazima sasa Wabunge tunao wajibu wa kuishauri Serikali kuona namna bora sana ambayo tunaweza ikatusaidia kutoka katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wote tunakubaliana kwamba miongoni mwa sababu ambazo zinachangia ongezeko hili la mafuta ni sababu za nje, lakini sisi kama nchi lazima tutafuta maeneo ya matumaini kwa watu wetu kwa sababu Serikali hii ni yao na imeahidi kuwatumikia, kwa hiyo, ni vyema itakatafuta namna bora ya kuweza kuondoa changamoto hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo ambalo ningeshauri kwanza ni sisi kwa mwezi matumizi yetu ya ndani ya mafuta ni kama lita Milioni 300, hiki ni kiasi ambacho tunakitumia ndani japo uagizaji tunafika mpaka kwenye lita Milioni 600 lakini haya mengine yanakwenda nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, ningependa kuishauri Serikali kwamba katika eneo hili tungekuja na mpango wa stabilization fund ambayo itakwenda ku-stabilize bei ya mafuta. Maana yake Serikali ije iombe kibali kwa Bunge, wakakope japo bilioni 300 kwa maana kwamba angalau kila lita moja ya mafuta tuiwekee ruzuku ya shilingi 1,000 ili mafuta haya yaweze kushuka bei. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii itatusaidia kwamba hatutakwenda kugusa hizi tozo pamoja na kodi nyingine zilizopo pale, kwa sababu hizi tozo zilikuwepo miaka sita iliyopita na hazijawahi kuwa tatizo. Kwa hiyo, leo siyo kwamba kwa kuwa mafuta yamepanda bei tatizo ni hizi tozo, hizi tozo zinatusaidia maeneo megine kama kupeleka umeme vijijini, barabara, maji na kadhalika. Kwa hiyo, ni lazima kuje na maarifa mengine ya ziada ambayo yataendelea kuhakikisha kwamba tozo zinaendelea kuwepo ili miradi ya maendeleo iendelee kufanyika kwa sababu ni wajibu wa Serikali kupeleka miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, bila kufumua bajeti ya Serikali ambayo imeshapita kupitia hizo tozo, solution hapa ni kuja na price stabilization fund, tuweke ruzuku katika kila lita moja ya mafuta tunaweza tukajipa kipindi cha miezi mitatu mitatu, kwamba labda miezi mitatu hii tutazame, tu-pump shilingi bilioni 300 katika mwezi wa kwanza wa uagizaji, mwezi wa pili, lakini baadaye tuangalie na hali huko duniani inaendelea vipi. Hilo ni jambo la haraka ambalo Serikali linaweza likalitazama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili, jana kulikuwa na kikao kizuri sana ambacho Mheshimiwa Waziri Mkuu alikiitisha, tunampongeza kwa jitihada hizi, lakini katika kutazama sana pale sikumuona Waziri wa Viwanda na Biashara na mimi naamini yeye ndiye mwathirika mkubwa sana katika eneo hili, kwa sababu hapa eneo ambalo tunalizungumza zaidi ni kwenye usafiri, lakini tunasahau eneo muhimu sana la uzalishaji.

Mheshimiwa Spika, huko kuna viwanda ambavyo vinatumia mafuta haya haya kuzalisha bidhaa maana yake bila kuangalia eneo hili la price stabilization fund, mfumuko wa bei kwenye baadhi ya bidhaa utakuwa mkubwa sana na wananchi hawataweza kuhimili hiyo hali. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Serikali kwa ujumla kwamba ni vizuri sana katika hatua hii kumshirikisha kwa dhati kabisa Waziri wa Viwanda na Biashara ili aweze kuangalia sekta hii yote ya kibiashara na viwanda kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho lakini sio kwa umuhimu...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuwa mchangiaji wa kwanza katika hoja hii iliyoko katika Bunge letu Tukufu. Kwa dhati kabisa nianze kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa nzuri sana ambayo ameendelea kuifanya kwa Taifa letu. Naamini Waheshimiwa Wabunge wote watakubaliana nami kwamba kwa kipindi hiki kifupi cha miaka miwili, miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo yetu katika halmashauri, manispaa, majiji na miji ni kwa kiwango kikubwa sana. Lakini pia nichukue fursa hii kumpongeza Waziri mwenye dhamana ya Wizira ya Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI na Wasaidizi wake Manaibu Waziri na Makatibu na watumishi wote kwa ujumla wao katika kumsaidia Mheshimiwa Rais kazi hii kubwa ya utekelezaji wa majukumu ya Wizara husika.

Mheshimiwa Spika, mimi nitaanza kuchangia katika eneo zima la barabara za vijijini, kwa maana ya Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (Tanzania Rural Urban Road Agency - TARURA). TARURA wanafanya kazi nzuri sana, kazi ambayo katika ile programu ya SDP wana component ya kutengeneza barabara kutoka maeneo ya uzalishaji kuyapeleka katika masoko na magulio. Kazi hiyo wanaifanya vizuri, mafungu yanaenda vizuri na usimamizi ni mzuri, kwa kweli tunaona tofauti kubwa sana tangu tulivyokuwa tunazisimamia hizi barabara kupitia halmashauri; na sasa tangu mamlaka hii imeingia tunaona kwamba kuna ufanisi umeongezeka kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nauliza hapa kwamba mamlaka kama ya DAWASA imepata ithibati ile ya ubora wa Dunia, lakini ninaamini kabisa kwamba sitashangaa siku moja nikiona kwamba TARURA nao wanapata ile International Standard Organisation kwa maana ya ubora wa kazi ambayo wanaifanya, lakini pia sitashangaa Engineer Victor Seff akitunukiwa udaktari wa heshima kwa kazi kubwa ambayo anaifanya kwa namna ambavyo ameifungua Tanzania hasa katika maeneo ya vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika,pamoja na sifa hizo lakini kuna changamoto ndogo ambayo naiona. Changamoto iko katika disbursement ya pesa hasa zinazotokana na Mfuko wa Barabara. TARURA ina vyanzo vikuu vitatu, chanzo cha kwanza ni jimbo cha pili ni tozo na cha tatu ni Mfuko wa Barabara. Sasa fedha za jimbo na za tozo zinaenda kwa wakati lakini fedha hizi zinazotokana na Mfuko wa Barabara zinachelewa, hivyo zinasababisha baadhi ya wakandarasi kuto omba zabuni za barabara ambazo fedha zake zinatokana na barabara. Kwa hiyo nimuombe sana Mheshimiwa Waziri na Serikali kwa ujumla, kwamba tujitahidi kupeleka mafungu ya hizi fedha zinazotokana na mfuko wa barabara kwa wakati

Mheshimiwa Spika, lakini kwakule Lushoto ambako kazi kubwa imefanyika tunachangamoto kubwa mbili. Changamoto ya kwanza ni kwamba TARURA hawana ofisi, ofisi waliyokuwa nayo sasa hivi inavuja kiasi kwamba wakati wa mvua wanaingia na miamvuli ndani ya ofisi, hili si jambo zuri. Sisi tumefanya jitihada kubwa, tumewapa kiwanja jirani kabisa na ofisi ya Mkuu wa Wilaya, ni eneo zuri mno ambalo linafaa kwa ujenzi wa ofisi ya TARURA.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili Wilaya ya Lushoto ni wilaya ambayo asilimia 95 ni milima; magari waliyokuwa nayo yamechakaa sana kila siku yanafanyiwa ukarabati. Inafikia hatua ili waweze kutimiza wajibu wao wakati mwingine lazima hata sisi Wabunge tunawaazima magari yetu, hii si sawa. Tunaomba wapatiwe magari ya kuhudumia majimbo yote matatu ya Wilaya ya Lushoto kwa sababu Wilaya ya Lushoto ni milima na mabonde hivyo inahitaji magari ambayo ni madhubuti sana ili waweze kufanya kazi hizi kwa ufanisi mkubwa.

Mheshimiwa Spika, naomba nihame katika eneo hili niende katika eneo la elimu. Tuna changamoto kubwa sana ya watumishi katika Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto, na mara kadhaa nikisimama hapa ndani ya Bunge lako nimekuwa nikizungumza jambo hili. Kipekee nipongeze jitihada hizi za Mheshimiwa Rais kutangaza ajira takriban 21,200. Mimi niombe, hizi 200 ambazo zimekaa pale juu zenyewe azielekeze Lushoto; na azielekeze Lushoto kwa sababu hizi zifuatazo.

Mheshimiwa Spika, sisi katika Idara ya Elimu Sekondari mahitaji ya walimu ni walimu 1000, waliopo ni walimu 841 tunaupungufu 159, kidogo hapo kuna uhafadhari. Hata hivyo, mwaka 2022 wamehama walimu 35, 2023 wamehama 25 na bado wanaendelea.

Mheshimiwa Spika, lakini wanahama huku hatujawahi kuona wakihamishwi kutoka maeneo mengine kuja Lushoto, hili ndilo tatizo kubwa. Ukienda kwenye idara ya elimu msingi mahitaji ni 2,250 waliopo ni 1333 upungufu ni 917; 2020 wamehama 34; 2021 wamehama 34 tena; 2022 wmehama 23; 2023 bado sijapata takwimu zake, lakini wanaohamia kuja Lushoto hatuwaoni kila unaye muuliza anakwambia changamoto ni baridi. Sasa mimi nauliza mbona wakipewa viza za kwenda Ulaya hawakatai na Ulaya na kwenyewe kuna baridi?

Mheshimiwa Spika, hizi sababu hatutaki kuzisikia, kwenye ajira hizi mpya zinazotangazwa tunataka tuletewe watumishi ambao wako committed kufanya kazi popote katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; na ikikupendeza tuletee ambao wako single, kama ni wanawake wawe hawajaolewa na kama ni wanaume wawe hawajaoa ili wasianze kuleta sababu za kuanza kuhama. Kule wako mabinti wa kisambaa wazuri weupe, watapata wachumba wazuri kule kule.

Mheshimiwa Spika,katika zoezi lile la vyeti fake tumepungukiwa na zaidi ya watumishi 216 ambao walikutwa na tatizo la vyeti; lakini hatuja pata ile compensation ya ile idadi ambayo walipunguzwa. Niombe sana, pamoja na mapungufu haya ninayo yataja basi angalau tupate wale 216 katika mkupuo mmoja ili kuziba lile gape ambalo limetokana na wenye matatizo ya vyeti.

Mheshimiwa Spika,eneo lingine ambalo ningetaka kulisemea pia, wapo walimu ambao wanajitolea katika shule zetu; na katika halmashauri ya Lushoto tunao walimu 97 ambao wanajitolea. Ningependa sana kuomba kwa ridhaa yako Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana, hebu tutafute hawa ambao wanajitolea, hawa wamekaa zaidi ya miaka miwili wanajitolea lakini leo wanakuja kushindanishwa na wengine ambao walikuwa wanafanya shughuli nyingine na inawezekana wakakosa. Nikuombe sana hawa hebu tuwapeni kipa umbele. Hii iwe pia ni zoezi endelevu, Serikali inaweza ikawa na data base ya Watumishi wote na tukawa na utaratibu kwamba kila mwalimu anaye maliza chuo basi apate angalau mwaka mmoja wa kujitolea na hata ikiwezekana muundo wa kuwaajiri ubadilike sasa waajiriwe wale ambao wako katika maeneo ambayo tayari wanajitolea kwa kipindi fulani.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo ningependa kuchangia ni kuhusu afya. Kama ambavyo tuna changamoto ya watumishi katika sekta ya elimu na afya ni vivyo hivyo. Ikama katika halmashauri ya Lushoto ni watumishi 662 ndio wanaohitajika waliopo ni 391 sawa na asilimia 59, upungufu 270 sawa na asilimia 41. Ungufu huo uko katika kada hizi zifuatazo;

i. Madaktari mahitaji ni 29 waliopo ni 11 upungufu ni 18 sawa na asilimia 38,

ii. Madaktari wasaidizi wanao hitajika ni 39 waliopo ni 2 ungufu 37 sawa na asilimia 5,

iii. Maafisa Wauguzi wanaohitajika 24 walipo ni 2 tu upungufu 22 sawa na asilimia 8,

iv. Wauguzi wako 132 wanaohitajika walipo ni 63 upungufu ni 69.

Mheshimiwa Spika, naomba sana, bajeti za miaka miwili, mitatu huko nyuma tumepeleka pesa nyingi sana kwenye miundombinu. Haitakuwa na maana yoyote tutakapokuwa na miundo mbinu lakini ikakosa watumishi.

Mheshimiwa Spika, niombe sana kwa ridhaa yako tuendelee kuhakikisha kwamba maeneo haya yanapata watumishi. Hivi tunapozungumza hivi ni kwamba wakati mwingine si lazima zitokee ajira mpya, hata kufanya restructuring katika muundo mzima wa ajira. Yako maeneo hasa mijini unakuta wamejaa katika maeneo ya miji lakini huku vijijini hakuna wanao hudumia Watanzania. Sasa nchi hii ni yetu sote tungependa kuona regional secretariat zifanye kazi ya ziada kuangalia katika maeneo ya miji lakini na maeneo ya vijijini yawe na usawa wa ikama ya watumishi.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kufungua dimba katika uchangiaji wa bajeti ya Ofisi ya Utumishi na Utawala Bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, ambaye kimsingi ndiye Waziri kwenye Wizara hii kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya na kazi hii anaifanya. Nimewahi kusoma maandiko matakatifu kutoka kwenye vitabu vyetu vitukufu kwamba Mtume Muhammad Swallallahu Alayhi Wasalaam alifundishwa biashara na Bi Hadija ambaye ndiye alikuwa mke wake. Huyu ndiye aliyemfundisha bihashara pamoja na Utume wake lakini biashara hiyo alifundishwa na mwanamke.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna Bibi mmoja anaitwa Elizabeth ambaye ni Mama yake Yohana mbatizaji ndiye aliyegundua kwamba Bi. Mariamu, Mama yake Yesu ana ujauzito. Kwa hiyo utagundua kwamba mwanamke kwa nafasi hii ambayo tumemkabidhi Rais majukumu haya hatukumkabidhi kwa bahati mbaya ni kiumbe ambaye amebarikiwa kutoka kwa uumbaji wa Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, theories mbalimbali, wanazuoni wengi wanatanabaisha kwamba kitovu cha matumizi sahihi ya rasilimali ni rasilimali watu. Rasilimali watu katika nchi yetu tumeikasimisha katika Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, inafanyika kazi nzuri sana na tunawapongeza sana. Sera zote za Utumishi wa Umma, Sheria lakini miongozo mbalimbali yote inasimamiwa na Ofisi hii ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Mheshimiwa Naibu Spika haya mambo yaweze kufanyika na kukamilika ni lazima kuhakikisha kwamba wakati wote haki za watumishi zinasimamiwa ipasavyo na hili Mheshimiwa Rais ameonyesha kwa vitendo haswa baada ya kuwapandisha madaraja watumishi wote kwa wakati, lakini kulipa malimbikizo yote ya pesa ambazo watumishi wa umma walikuwa wanadai. Hali kadhalika amebadilisha kada ya utumishi na hili amelifanya kwa kutoa Muongozo wa kupandisha madaraja kwa watumishi wapya ambao wapande madaraja kwa miaka minne na wale watumishi wa muda mrefu kwa miaka mitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatakiwa ifanye kazi katika maeneo kadhaa ambayo ningeomba kutoa ushauri. Eneo la kwanza ni maadili, katika idara zote zinazosimamia maadili ya utumishi wa umma ni vizuri sana zikazingatia misingi ya utumishi wa umma. Hapa nitatoa mfano kwamba, sisi tunapokea Ripoti ya CAG ambayo Bunge linaipokea na linajadili. Ningependa kuona na Sekretarieti hii ya Maadili ya Viongozi wa Umma na yenyewe ianze kufanya hivyo kupitia ile Tume ya Utumishi kwamba Tume ya Utumishi inaleta ripoti ndani ya Bunge, lakini kwa bahati mbaya sana ripoti ile hatuijadili.

Mheshimiwa Naibu Spika kwa hiyo ningependa kushauri kwamba ifike mahali sasa angalau na Tume ile ya Utumishi ikileta ripoti ndani ya Bunge, tuifanyie mjadala ili tuweze kuona ufanisi uko kwa kiwango gani katika maeneo yote ya utumishi wa umma? Tunaweza tukagundua upungufu katika utendaji, lakini pia kuangalia haki za watumishi na msawazo wa ujumla wa utumishi katika nyanja mbalimbali za utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna mfumo ule wa Upimaji Utendaji Kazi kwa Watumishi (OPRAS) mfumo ule una changamoto. Sasa ni vizuri wakaja na mfumo bora zaidi ambao utakuwa unapima quantity na quality. Tunaweza tukasema ubora lakini pia na wingi wa kazi ambazo mtumishi mmoja anafanya na hapa tuwashirikishe vizuri watu wa e– government. Hii mifumo tunaizungumza tu, lakini ukienda kwenye uhalisia huoni namna inavyofanya kazi na ndiyo maana wakati mwingine inazua maswali mengi hata kutoka kupoteza imani hasa linapokuja suala la ajira. Kwa hiyo niombe sana kwamba tutumie e–government kuhakikisha kwamba tunaboresha mifumo iweze kusomana vizuri, tuwe na kanzidata ambayo inaweza ikajua mfanyakazi mmoja anafanya kazi kwa kiasi na mwingine anafanya kazi kwa kiasi gani. Pia na usambazaji mzima wa hao watumishi katika halmashauri zetu, katika idara na katika mashirika kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina jambo lingine ambalo ningetaka nishauri na hili ni jambo ambalo kwa kweli kama Taifa inabidi tuliangalie kwa umakini mkubwa sana, suala zima la ajira. Nitatoa tu mfano katika kada moja ya elimu, kama kuna mahali tumekosea ni pale tulipoua Tume ya Mipango. Tume ile ya Mipango ndiyo ilikuwa inaweza kupanga mipango yetu ya muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu. Tumeiunganisha Tume ya Mipango kwenye Wizara ya Fedha, sasa hivi ufanisi wake huuoni na huko mbele ya safari tutakwenda kukumbana na tatizo ambalo ndiyo hili naomba niliseme.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kwenye kada moja tu ya elimu; tunavyo Vyuo 35 vya Elimu hivi ni katika ngazi hii ya diploma na certificate ambavyo ni vya Serikali. Kila chuo kinadahili wanafunzi 400 kwa mwaka, kwa maana kwa vyuo 35, tunapata wanafunzi 14,000 wanadahiliwa kwenye ualimu kwa mwaka mmoja. Ukichukua na wanafunzi walioko kwenye vyuo binafsi vya elimu viko 23, hivi vinachukua wastani wa wanafunzi 11,000, ukichanganya unapata ni wanafunzi wastani wa 25,000 wanadahiliwa kila mwaka. Kwa hiyo kwa vyuo hivi vinavyochukua wanafunzi kwa miaka mitatu maana yake una wanafunzi 75,000 wanadahili sasa hivi wako kwenye vyuo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukija kwenye Vyuo Vikuu UDOM, St Augustine pamoja na University of Dar es Salaam, DUCE na vinginevyo vina wanafunzi, mpaka sasa hivi ninavyozungumza hapa 56,183. Jumla yake ni wanafunzi 131,183 hawa wanadahiliwa, wanaandaliwa kwa ajili ya soko la elimu. Soko lenyewe halipo, ajira zilizotoka ni 21,000 elimu na afya ambazo ni wastani wa kwenye elimu ni 12,000, hawa wanafunzi tutawapeleka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishauri, hapa sasa ndiyo tunakuja kwenye Tume ya Mipango lakini pia eneo la utawala bora. Kuna umuhimu gani kuendelea kuzalisha walimu kama kwenye soko hatuwahitaji? Ifikie mahali tupunguze utitiri vya vyuo hivi vinavyotoa kada za elimu kama hatuna nafasi ya kweza kuajiri ili watoto wetu wasome masomo ambayo watakapokwenda kwenye soko wanaweza wakayafanyia kazi na ualimu kwasababu ni ambalo ni mahususi maana yake akishasoma hawezi akafanya kazi nje ya eneo hilo. Kwa hiyo niombe sana jambo hili tulifanyie kazi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, inakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Azimio la Bunge kuhusu Mapendekezo ya Kuridhia Itifaki ya Biashara ya Huduma ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ya Mwaka 2012
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kutoa mchango wangu katika Azimio hili ambalo liko mbele ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nampongeza sana Waziri mwenye dhamana ya Viwanda na Biashara kwa kuleta Itifaki hii. Kipekee nawapongeza Kamati kwa namna ambavyo wamechakata na kutoa maoni ambayo na sisi tunaweza kupata mwanga wa kuweza kushauri katika kuridhia Itifaki ya Biashara ya Huduma ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika ya Mwaka 2012.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina wasiwasi kidogo kwa nini Itifaki hii imechelewa, lakini sio jambo geni kwa Tanzania, mara nyingi mambo mengi huwa tunachelewa, ila sasa kwa sababu sasa hivi dunia inakwenda kasi, ni vizuri tukipata fursa nzuri kama hizi, tukajitahidi kwenda nazo kwa haraka zaidi. Ninachotaka kusema ni kwamba sisi kabla ya mwaka 2000 Sera yetu ya Mambo ya Nje ilikuwa ni ukombozi wa Bara la Afrika na tulijikita zaidi Kusini mwa Afrika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, karibu nchi zote hizi ambazo tunazozizungumzia, ukiacha zile ambazo zimepata uhuru kabla yetu au karibu na sisi, nyingine zote tumeshiriki kwa jasho na damu kusaidia kuzikomboa. Jambo hili lilikuwa na maana sana kwamba baada ya ukombozi ule wa kupata uhuru, basi wakishakuwa huru ni lazima tutengeneze utengemano kama huu wa kufanya biashara, kwa hiyo kwa hatua hiyo naipongeza Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningetaka niliseme ni kwamba, Sera yetu ya Mambo ya Nje wakati huo ilikuwa ni ya ukombozi, kwa hiyo ni vizuri tukaipitia upya Sera yetu ya Mambo ya Nje ya sasa ya Economic Diplomacy yaani Diplomasia ya Uchumi kwa sababu bado kuna maeneo mengi ya kiuchumi ambayo hatujayatumia vizuri kama Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi nchi tunazozizungumzia hapa ukiacha nchi mbili kwa maana ya Afrika Kusini na Angola, hizi nyingine zote GDP per capita tunawazidi, kwa maana sisi uchumi wetu uko juu zaidi. Sasa kwa jiografia ilivyo na utamaduni ulivyo ni kwamba nchi hizi karibu sehemu kubwa hata kabla ya kuridhia hii Itifaki tunazihudumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya mambo ambayo yametajwa kwenye Itifaki kwa mfano huduma za kifedha, zipo nchi kama DR Congo tayari kuna huduma za kifedha kwenye hizo nchi, kwa maana mikataba ya nchi na nchi, tayari kuna Benki ya CRDB ina-operate pale Lubumbashi. Ukienda Comoro tayari kuna Benki ya Exim nadhani na CRDB pia wana-operate pale Comoro. Kwa hiyo, utaona kwamba zile bilateral treaties tayari zinafanya kazi nje ya Itifaki hii kwa maana ya nchi na nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija katika mawanda mazima ya mawasiliano, kwenye mawasiliano tunazungumzia suala zima la uchukuzi na suala zima la logistics. Hii inafanyika, hata kwa kampuni moja moja lakini pia kwa nchi kwa maana kwamba tunaposafirisha bidhaa kutoka katika bandari zetu kwenda katika Nchi hizi za SADC bado kuna eneo ambalo tayari tunafanya. Kwa hiyo Itifaki hii iende ikaboreshe na kutengeneza mnyororo mzima wa kuthaminisha Itifaki hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo ambalo hatukufanya vizuri na ambalo tunataka Itifaki hii ambayo tunairidhia baada ya miaka 11, twende tukaisimamie ni suala zima la elimu. Kama ambavyo nimetangulia kusema kwenye utangulizi ni kwamba kwa kuwa tumeshiriki katika ukombozi wa hizi nchi maana yake tumezisaidia kwa namna moja ama nyingine hasa katika eneo la ulinzi na usalama (peace keeping). Ukifika huko mara nyingi askari polisi na jeshi kwa ujumla wake wamepewa mafunzo na Watanzania na ndiyo maana ukifika kwenye nchi hizo ukikutana na maaskari wanajua vizuri hata Kiswahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la elimu tunatakiwa tuingie hapo kupeleka huduma. Kwa mfano, huduma za elimu ya uhandisi, bado tuna wahandisi wengi hapa ndani ya nchi na hakuna ajira, ni lazima tutengeneze mkakati wa kuhakikisha tunasukuma watu wetu wa kada hiyo kwenda kufanya kazi katika nchi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la afya, Wahadhiri wa vyuo tunatakiwa tuwapeleke huko kwa sababu sisi tuna idadi kubwa na wenzetu hawa baadhi ya nchi bado hazijajitosheleza, ni lazima tutumie fursa hiyo kupeleka watu wetu kutoa huduma hiyo ya elimu katika hizi nchi. Kwa sababu za kidiplomasia nashindwa kuzitaja, lakini tumefanya utafiti wa kina zipo nchi bado zinahitaji huduma ya Madaktari, zipo nchi zinazohitaji huduma ya Wahandisi na zipo nchi zinahitaji huduma ya Manesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo Watanzania wamethubutu wenyewe kwenda kwenye hizo nchi, lakini Tanzania haiwatambui, kwa maana Balozi zetu zilizopo kule haziwatambui kwa sababu wameenda wenyewe. Kwa hiyo, tunachotaka kumshauri Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana, aitumie vizuri Wizara ya Mambo ya Nje tuhakikishe kwamba Mabalozi wetu kwenye diplomasia ya uchumi kwa Nchi za SADC tuna-capitalize kwenye hili eneo la kuweza kusaidia Watanzania ambao wamesoma na ndani ya nchi tumeshindwa kuwaajiri, lakini kuna fursa hiyo nje ya Tanzania, basi waipate kupitia eneo hili la SADC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo liko kwenye Ibara ya 16 ni suala zima la afya. Afya hapa imetajwa kwa ujumla na nimeshataja katika maeneo hayo ya kitaaluma, lakini kwenye logistic chain ya usambazaji wa madawa, hapa nataka niweke wazi kwamba hata MSD waliwahi kupata zabuni ya kusambaza dawa katika nchi zote za SADC wakati huo zikiwa 13 na sasa zimefika 16.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba sana kwamba tunaweza tukahakikisha pia tunaishirikisha vema Wizara ya Afya kupitia MSD kwenda kutumia fursa hiyo ya kusambaza madawa katika hizo nchi. Imeonekana kwamba usambazaji wa dawa unaofanywa na MSD ndani ya Tanzania ni usambazaji wa kiwango cha kimataifa, hivyo wenzetu hawa wamevutiwa. Kwa hiyo, tutumie fursa hiyo ya kwenda kutengeneza logistic ya kwenda kusambaza dawa katika SADC, lakini wakati huo huo tukiitumia kama advantage ya kuhakikisha kwamba tunafungua viwanda vingi vya madawa katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dawa nyingi ambazo tunazisambaza katika nchi yetu hazizalishwi Tanzania. Source kubwa ya madawa yetu yanatoka Ujerumani na India. Kwa hiyo, maana yake kama SADC watamchukua MSD kwenda kusambaza madawa katika nchi zao inawezakana kabisa kwamba na dawa ambazo zitapita Tanzania au zitazalishwa Tanzania soko letu litakuwa kubwa zaidi. Tukiwekeza katika viwanda vya madawa maana yake dawa zetu zitakuwa ni sehemu ya kwenda kusambazwa katika Nchi za SADC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningetaka kushauri ni suala zima la ukuzaji wa Lugha ya Kiswahili. Hapa napo ni lazima tuwe na mkakati madhubuti. Kiswahili hiki tunachozungumza leo sio cha kwenda kufundishia. Ni lazima tujipange upya, BAKITA na Wizara inayohusika tuanze kuandaa wataalam, Linguists ambao watakwenda kufundisha hicho Kiswahili katika nchi ambazo tunakusudia. Haitawezekana kumfundisha Kiswahili kama hujui lugha yake. Zipo nchi zinazungumza Kireno, zipo nchi zinazungumza Kifaransa na zipo nchi zinazungumza Kiingereza. Kwa hiyo, ni lazima tuwaandae watu wetu watakaokwenda kufundisha Kiswahili wawe wanazijua hizo lugha ili waweze kurahisisha uwasilishaji na mawasiliano kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho lakini sio kwa umuhimu nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, lakini tunataka kuona mabadiliko makubwa katika eneo hili la SADC kwa sababu kwa jiografia ya nchi yetu ndiyo eneo kubwa zaidi ambalo linaingiza pato kubwa baada ya India. Sehemu nyingine ambayo tuna soko kubwa la watu hawa zaidi ya milioni 360 ni ukanda wa SADC. Kwa bahati nzuri ni kwamba ukanda huu unatutegemea zaidi sisi, kwa hiyo sisi katika Itifaki hii maana yake tunakwenda kupiga comparative advantage ya uwepo wetu katika SADC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema maneno hayo, nakushukuru sana kwa nafasi, naunga mkono Itifaki hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami niweze kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana katika eneo hili la kilimo pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Anthony Mavunde. Kwa kweli wanafanya kazi kubwa na nzuri sana ambayo imeanza kuonekana. Tunataka kuona sasa kazi hii itoke kwenye zile suti ambazo wameziandaa ielekee kwenye vitendo na uhalisia zaidi ili mwisho wa siku tusifanye tathmini kwa mavazi, bali kwa tija ambayo itaonekana kupitia kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu nitaulekeza katika zao la kimkakati la kahawa. Mkoa wa Tanga ni miongoni mwa mikoa takribani 15 ya nchi yetu ambayo inalima kahawa na hususan katika milima ya Usambara kwa maana ya Wilaya za Muheza, Korogwe pamoja na Lushoto. Zao hili kwa muda mrefu Serikali imekuwa haitoi motisha kwa wakulima kiasi kwamba zao hili sasa linakwenda kupotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama utakumbuka, hata jana Mheshimiwa Anne Kilango Malecela alikuwa anaongelea zao la tangawizi, na hali ya hewa ya Same na Lushoto zinafanana kwa asilimia kubwa, lakini watu wamehama kutoka kilimo cha kahawa kwenda kilimo cha tangawizi kwa sababu ya changamoto mbalimbali zikiwemo huduma hafifu za ugani, uchakavu au umri mkubwa wa mibuna, upatikanaji wa pembejeo; madawa na mbolea na matumizi ya mbegu bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kwenye mbegu bora ndiko ambako nataka niweke msisitizo. Ni kwamba Bodi ya Kahawa (TCB) ifanye kazi ya ziada kuhakikisha kwamba kunakuwa na miche mingi ya kahawa hasa katika mikoa hii ambayo nimeitaja hapo awali. Mkoa wa Kagera ndiyo unaoongoza kwa uzalishaji wa kahawa hapa nchini ambapo wanazalisha takribani kwa mwaka tani za kutosha tu, ambazo kwa ujumla wa tani zote nchi nzima, wao wanachangia asilimia 45.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkoa unaofuata ni Mkoa wa Mbeya, Kigoma na Songwe nako kahawa inazalishwa. Yapo maeneo ambayo wanazalisha kwenye baadhi ya wilaya ikiwemo Ruvuma ambako ni Mbinga pamoja na Nyasa, pia Mkoa wa Arusha, Mara, Njombe, Iringa, Manyara, Katavi, Morogoro na Mwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo langu hapa ni kuishauri Serikali kwamba sasa tuweke ruzuku katika zao hili la kahawa. Tunaona kabisa kwamba zao la kahawa kwa ripoti za mwaka 2021 tumeuza nje takribani dola milioni 142. Ni kiasi kikubwa sana ukilinganisha na pesa ambayo tumeuza kwenye tumbaku ambapo tumbaku ina ruzuku, lakini kahawa haina ruzuku. Kwa hiyo, tunaamini kabisa kwamba tukiongeza uzalishaji katika kahawa, hata hili pato litaongezeka kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetazama hapa kwenye takwimu, nchi ya Ethiopia ambayo inaongoza kwa uzalishaji wa kahawa, inazalisha takribani tani 457,000. Yenyewe tangu mwaka 1959 mpaka tunavyozungumza sasa, haijawahi kupunguza uzalishaji. Kadri mwaka unavyoongezeka ndivyo na uzalishaji unavyoongezeka, maana yake wao walilichukuwa hili kama ni zao mahususi, zao la kimkakati ambalo linaibeba nchi ya Ethiopia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri pamoja na Serikali kwa ujumla nawaomba sana kwamba pamoja na mazao mengine yote ya kimkakati tunayoyajadili, tuweke nguvu ya ziada katika zao hili la kahawa ambalo sasa linaelekea kupotea. Matarajio yetu ni kuzalisha wastani wa tani laki moja kwa mwaka, lakini mpaka sasa hivi tumefika tani 68,000 tu. Hizi ni chache sana kwa ukubwa wa nchi yetu ukilinganisha na nchi jirani ambazo kahawa inalimwa lakini siyo kwa ardhi kubwa kama ambayo tunayo hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao la kahawa, tofauti na mazao mengine ya kimkakati, ukishapanda una uwezo wa kukaa miaka 30 mpaka 40 kutegemea na aina ya kahawa. Kwa mfano, Arabika, kubadilisha mti uliochoka unahitaji miaka 50 mpaka miaka 60. Hata hii ambayo sasa hivi tunaendelea kuvuna huko, ni kahawa ambayo imeanza kulimwa na wakoloni na baadaye ikalimwa na babu zetu. Sasa sisi kama kizaki kipya tunatakiwa tupeleke mbegu, tuanzishe vitalu vya miche ya kahawa katika maeneo yote niliyoyataja ili sasa tuongeze uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, aina ya Robusta, mche unaweza kukaa hadi miaka 40, ndiyo unakwenda kuzeeka kiasi cha kupunguza uzalishaji. Kwa hiyo, naomba sana katika eneo hili tufanye maboresho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine la uzalishaji, nikitoa tu mfano wa eneo la uzalishaji wa kimkakati ambalo tumejifunza katika Wilaya ya Mbinga kule Ruvuma; kupitia ushirika wa MBICUFARM tumejifunza jambo kubwa sana. Kahawa yote tunaiona inakobolewa katika mashine ambazo ziko chini ya Vyama Vya Ushirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge, tukitaka kwenda kujifunza ushirika wa ukweli, ni vizuri tukaenda kujifunza kwenye Chama cha Matengo kule ambacho sasa hivi kinaitwa MBICUFARM. Wanafanya kazi nzuri sana na tumeiona kahawa yote ikiwa kwenye maghala imehifadhiwa. Hapa ndipo tunapopata somo kwamba haya maghala na yenyewe tukiyawekea takwimu yanaweza yakasaidia hata kuvutia wateja kutoka nje kwa sababu watakuwa na uhakika kwamba akifika mahali fulani kwenye ghala namba fulani anaweza akapata tani za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana na nitoe rai kwamba tuige mifano mizuri ya wenzetu kama hawa ambao tumezikuta tani takribani 15,000 ziko kwenye maghala na tayari mnunuzi amepatikana kutoka nje ya nchi. Halmashauri haikamatani na wafanyabiashara kwenye mageti, hela yote inapatikana kupitia mfumo sahihi wa stakabadhi. Halmashauri inachukua mrabaha wake, Vyama Vya Ushirika vinachukuwa mrabaha, AMCOS zinachukua kilicho chao; na tumeona AMCOS zikitoa CSR hata kwa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika AMCOS moja inaitwa Kimuli, imeweza kutoa makalavati kwa TARURA ili waweze kuboresha miundombinu ya barabara. Sasa hii ni dhana pekee unayoweza kuipata kupitia ushirika nje ya ushirika itakuwa ni kukimbizana na wachuuzi wadogo hawa ambao baadaye pia wanasaidia kutorosha mazao hata kwenda nje ya nchi na mwisho wa siku inaonekana turnover ya nchi ni ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho lakini siyo kwa umuhimu, ni hili ambalo limezungumzwa kuhusu leseni za maghala. Tumejifunza jambo kwenye maghala haya ya mafuta kwamba baada ya kupata mfumuko huu wa mtikisiko wa soko la mafuta duniani, kila wakati Wizara ya Nishati ilikuwa inatoa takwimu za mafuta yaliyoko katika maghala ya mafuta. Ningetamani kuona jambo hili nalo likitokea katika kila aina ya bidhaa ambayo tunayo hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili litawezekana tu kama tutakuwa na takwimu sahihi na ghala lilipo na linahifadhi kitu gani? Maana yake hapa tunachotafuta ni takwimu siyo jambo lingine. Mambo ya ubora na mambo mengine yatasimamiwa na idara zinazohusika, lakini angalau kujua kwamba nchi yetu ina sukari kiasi gani? Nchi yetu ina ngano kiasi gani? Nchi yetu ina mafuta ya kupikia kiasi gani? Hili linahitaji takwimu na sehemu sahihi ambayo tunaweza tukafanya hili, ni kupitia wakala wa maghala nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu, kwanza nimpongeze sana Waziri mwenye dhamana Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa kwa kazi nzuri sana ambayo anaifanya katika Wizara hii, lakini sambama na naye nimpongeze Naibu Waziri Mheshimiwa Pauline Gekul kwa kazi nzuri sana unaifanya mama endelea tupo nyuma yako tunaunga mkono, lakini kipekee niwapongeze watendaji wa Wizara hii ndugu yangu Dkt. Abbas lakini pia Naibu Katibu Mkuu kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi mchango wangu utajikita sana katika mambo ya soka, lakini nikiangalia zaidi eneo la mapato. Nilikuwa ninamuuliza Mheshimiwa Mwijage hapa kwamba kuna wakati wa Yesu, kuna yule Zakayo ambaye alikuwa ni mtoza ushuru, sasa kwa bahati leo tupo na Mkurugenzi wa Singida Big Stars ambaye pia ndio mtoza ushuru wetu hapa Tanzania na kwa babati nzuri na yeye ana timu inacheza ligi kuu katika msimu huo unaokuja, sasa nikakumbuka ile methali ya mwenda tezi na omo marejeo ngamani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilabu vya Simba na Yanga vimeanishwa muda mrefu sana, lakini vilabu havijiendeshi kibiashara, bado ni vilabu ambavyo vinategemea ruzuku za wanachama, lakini michango mbalimbali na kwa bahati mbaya sana huko nyuma walikuwa na mfumo ambao sio mzuri sana wa usajili kiasi kwamba walikuwa wanasajili wachezaji, hasa wachezaji wa nje…

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa taarifa.

T A A R I F A

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba vilabu ambavyo havijiendeshwi kibiashara sio vyote, Young Africans sasa hivi ipo kwenye kumalizia kujiendesha kibiashara na muda mfupi tu watakamilisha mpango huo na itakuwa inajiendesha kibiashara sawa sawa. Kwa hiyo nampa taarifa na aipokee, ahsante sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Shangazi sidhani kama ni taarifa, lakini ni …

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, sio taarifa, kwanza angetega sikio asikie nazungumza nini ndio ataelewa kwamba kuna biashara inafanyika au hakuna biashara. Simba na Yanga peke yake hadi sasa hivi zinadaiwa na Mamlaka ya Kodi Tanzania bilioni kumi na hizi ni fedha ambazo zinatokana na…

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waziri wa Fedha.

T A A R I F A

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa mbili mzungumzaji; moja sikuwa najua…

NAIBU SPIKA: Taarifa moja tu.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji sikuwa najuwa anavyoongea Zakayo anamaanisha mimi, lakini nilitaka nimpe taarifa kwamba mimi similiki timu ni mdau tu wa michezo ya hapa Tanzania, kwa hiyo… (Makofi)
NAIBU SPIKA: ahsante lakini sidhani kama ulitajwa. (Makofi/Kicheko)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPAGO: Mheshimiwa Naibu Spika, niliona anaongelea Zakayo. (Kicheko)

NAIBU SPIKA: Naona unajishuku, haukutajwa popote hapa yametajwa mambo ya Yanga na madeni ya TRA nilifikiri unasimama kuhusu unasamehe madeni ya TRA ya vilabu vikubwa. Haya Mheshimiwa Shangazi endelea.

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naona mambo yanakuwa mazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Simba na Yanga kwa umoja wao wanadaiwa takribani shilingi bilioni kumi na Mamlaka ya Kodi Tanzania na fedha hizi zinatokana na pays as you earn, lakini skills development levy ambazo hawakukusanya tangu wakati ule ambapo walikuwa wanaendesha katika mfumo ambao sio rasmi sana kama ambavyo sasa hivi angalau wanaelekea kwenye mfumo ambao unaeleweka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunawomba sana Wizara ya Fedha hivi vilabu kwasababu havijiendeshi kibiashara, havina mahali popote vinaweza kuja ku-retire hivi amount, basi wasamehe hizi kodi ili sasa virudi katika mfumo wa kuweza kuwa na compliance wakati huu ambapo sasa vimeanza kujiendesha katika mfumo ambao ni rasmi. Lakini bila kusamehe hili deni ipo siku Mamlaka ya Mapato ikiamua kuvifungia hivi vilabu hatutakuwa na kitu kinachoitwa Simba wala Yanga kwa sababu wana deni kubwa ambalo haliwezi kulipika. Kwa hiyo, nikuombe sana Waziri wa Fedha lakini nikuomba Waziri wa Michezo ufuatilie hili jambo ili vilabu vyetu viweze kupata hiyo nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini eneo lingine ambalo nilitaka kulichangia pia ni kwenye eneo ambalo sasa linawahusu hata wale wamiliki wa Singida Big Stars, lakini wengine ni wa Namungo, Simba, Azam na kadhalika. Hili ni eneo ambalo lina kodi ya zuio (withholding tax); TFF wameingia mkataba na Kampuni ya Azam ya kuonesha matangazo ya mpira, lakini kulikuwa kuna kipengele cha withholding tax ambacho vilabu vilikuwa havikuambiwa, kwa hiyo wakati sasa vilabu vinapewa fedha na Azam inabidi sasa wa-retire ile amount ya withholding tax kitu ambacho kimepunguza kile kiwango ambacho tumetangaziwa pale awali.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii inavifanya vilabu sasa vikose fedha za kutosha za kuweza kujikimu kama ambavyo mdhamini alikusudia kwa hiyo tunaiomba Wizara ya Fedha, lakini pia Wizara ya Michezo ikae ikae katikati iangalie, kwa sababu vilabu vyote tunavyozungumza hapa havina mahali ambapo mwisho wa mwaka wanaweza wakaonesha hesabu ili waweze kurudishiwa hizi fedha, kwa sababu vilabu vyetu bado vipo katika mfumo wa ridhaa, kwa hiyo namna pekee ya kuwasaidia ni kuwasamehe hii kodi ya zuio katika hii biashara ya matangazo kupitia Azam TV.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo ningependa kulichangia ni suala la kwenye michezo ya kubahatisha (betting). Ningeomba sana kwanza nawapongeza sana SportPesa kwa kazi nzuri ambayo wanafanya, wameweza kudhamini Simba na Yanga takribani miaka mitano na wametoa zaidi ya shilingi bilioni 6.6. Lakini pia walikuwa wanadhamini vilabu vingine kama Singida United, wamedhamini Namungo tumeona wakiwa na msaada mkubwa. Lakini nitoe rai sasa kwa Wizara ya Michezo iweze kuongea na kampuni nyingine za michezo ya kubahatisha kwa maana ya betting sasa hivi tunazo kampuni zaidi ya 20 twende kuwaeleza kwamba ili aweze kupata leseni ni lazima angalau adhamini pia japo timu moja, kama ambavyo tumeona kuna 10Bet wanadhamini timu ya Dodoma Jiji hapa, basi na hizi kampuni nyingine za betting zichukue japo timu moja ya ligi kuu au kama sio ya ligi kuu basi hata ya ligi daraja la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii itasaidia sana kwa sababu maudhui wanayokwenda kushindania yanatokana na mpira, kwa hiyo ni lazima wawekeze pia katika kuendeleza tasnia nzima ya mchezo ili waweze pia kupata malighafi ya kuzalisha kwa ajli ya hizo kampuni zao za ku-bet. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo ningependa nilisemee ni eneo la kwa ujumla kuwapongeza wale ambao wanafanya vizuri katika udhamini kwa maana ya Azam kupitia Azam Sports wanafanya kazi nzuri sana. Lakini wadhamini wengine kama SportPesa wadhamini wengine kama Mohamed Dewji kupitia kampuni yake ya MO29 wanafanya vizuri kiasi kwamba sasa tumeona namna ambavyo Simba inaendelea kufanya vizuri katika Taifa hili, takribani kipindi cha miaka mitano tumeingia katika hatua ya robo fainali na tumeliwakilisha vyema Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia hata katika hii Royal Tour, Simba ndio tumeanza kwa sababu katika kuweka jezi ya Simba ile ya Visit Tanzania hao watalii ambao tunawaona kuna mchango mkubwa sana wa Simba Sports Club. Kwa hiyo ninakubaliana na wewe sasa kwamba na michezo nayo iingie hapa i-chip in kwenye hii Royal Tour kwenye sports ili tuweze kufanya michezo yetu iweze kuwa na msaada mzuri kwa vijana wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali, 2017
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kupata fursa hii. Nianze na maneno matakatifu aliyoyasema Nabii Issa au baba yetu Yesu wakati yupo msalabani pale alisema baba wasamehe kwa sababu hawajui wanalolitenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba niendelee. Ni kweli kama alivyosema mama yangu Mheshimiwa Riziki Shahari Mngwali, mwanzoni tulikuwa hatukuelewa vizuri hii sheria ambayo imeletwa mbele ya Bunge lako Tukufu, lakini kadri tulivyokuwa tunaendelea Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Waziri mwenye dhamana wamekuja kutoa somo katika Kamati yetu na imefika mahali bila unafiki tunasimama hapa tukiwa na mind nzuri kabisa tukiamini kwamba, sheria hii inakwenda kufanya kazi ambayo ndiyo mara nyingi tunailalamikia hata humu Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge karibu wote hapa huwa tunalalamika kila siku kwamba bajeti ya Serikali sio realistic, kwa nini tunaweka projection kubwa lakini mapato yanakuwa madogo; kwa sababu ni makisio na haya makisio yanaanza kufanywa katika Halmashauri zetu. Halmashauri inafanya makisio ndani ya miezi mitatu inapeleka kunako husika na mwisho wa siku wanapokusanya mapato halisi yanapishana na yale makisio.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ili tutengeneze utaratibu na kuwa na mwanzo mzuri wa realistic budget ni lazima sasa tuipe Serikali muda mrefu wa kuanza kukusanya na kuleta ripoti baada ya miezi sita. Huu wala sio utaratibu mgeni, ni utaratibu ambao hata South Korea wanautumia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaona kabisa katika vyanzo vyetu vya mapato kwenye Halmashauri nyingine vinategemea zaidi mazao, upo wakati kati ya mwezi mmoja hadi mitatu unakuta Halmashauri fulani haina mazao yoyote. Kwa hiyo, utarajie kwamba kwa kipindi hicho Halmashauri hii haitakusanya chochote.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, Mheshimiwa Mwita waitara kule Jimboni kwake wengi ni wafugaji wa kuku, sio kwamba akishaanza kuku pale dakika hiyo hiyo atapata mayai; ni baada ya muda fulani mayai yatapatikana labda ndani ya wiki mbili au tatu na kama kuna ushuru ndio ataanza kulipa. Kwa hiyo, hizi projections zote zinakwenda kuwekwa kwenye maduhuli ya Serikali na vyanzo mbalimbali vinavyotokana na mapato ambayo sio ya kodi kama kwenye mahakama na kadhalika. Kwa hiyo, ndani ya miezi sita ndio tupate ripoti. Hizi ripoti ambazo tunapata sasa hivi ndani ya miezi mitatu ni ripoti ambazo ni premature kwa sababu hazina approval ya Baraza la Mawaziri, lakini hii ya miezi sita inakwenda kupata ridhaa ya Baraza la Mawaziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hebu tuone kwa concern hiyo. Tusiende mbali kusema kwamba Bunge linanyang’anywa madaraka yake; madaraka ya Bunge yapo kimsingi kwa mujibu wa Ibara ya 63(2) yapo wazi kabisa yamewekwa pale, lakini pia tunakutana katika Mabunge manne na kila Bunge hapa lina kazi yake Waheshimiwa Wabunge. Bunge hili tulilokula nalo ni kwa ajili ya kupitisha bajeti ya Serikali; Bunge la mwezi wa Tisa tukija hapa ni kwa ajili ya kutunga sheria ndio muktadha; la mwezi wa Kumi na Moja lile ni la uchunguzi na kupokea ripoti za CAG, LAAC na kadhalika na mwezi wa Tatu ni oversight na hii oversight ndiyo hizi pesa ambazo tunapeleka mwezi wa Tatu ndio tunaenda kuziangalia zimefanyaje kazi, tunakwenda kuisimamia Serikali pale imetekeleza vipi. Kwa hiyo, ninaposema upotoshaji ndio hili ambalo namaanisha, kwa hiyo naamini kwa muktadha huo tutakuwa tumeelewana vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunachozungumza hapa pia ni suala zima la kwamba kama nilivyotangulia kusema kwamba lengo mahususi ni kuhakikisha kwamba sasa Serikali inapata bajeti ambayo ni realistic, tusije hapa tukapendezeshana tu kwamba bajeti inasomwa lakini haiendeni na mapato tuliyokusanya. Pia hata mwaka jana mpaka Novemba Serikali ilikuwa bado haijapeleka pesa kwenye Halmashauri zetu na tukaja hapa tukalalamika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukamlalamikia sana Waziri mwenye dhamana ya afya kwamba madawa hayapatikani, lakini chanzo chake ni hiki hiki tunachokisema kwamba hata sheria, tumebadilisha hapa Finance Bill na imeanza kufanya kazi tarehe moja, sio kwamba inapoanza kufanya kazi moja kwa moja kuna taratibu nyingine za kiofisi bado hazijakaa vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, unakuta Serikali mpaka ijipange tuanze kubadilisha majedwali na kadhalika mpaka mwezi wa 11 pesa bado hazijaingia kwenye Halmashauri zetu. Kwa hiyo, niwaombe Waheshimiwa Wabunge tunapojadili mambo haya tuache kutumia akili za vikao vyetu vya pembeni pembeni, tujaribu kutumia akili za
kawaida kabisa kwa muktadha wa shughuli za Kibunge ili tuweze kuishauri na kuisimamia Serikali vile inavyopaswa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ya kwangu ndio hayo, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana.