Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Mary Pius Chatanda (2 total)

MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Mheshimiwa Waziri Mkuu TARURA imekuwa ikifanya kazi kubwa ya kutekeleza miradi ya barabara mijini na vijijini. Na kwa kuwa umuhimu wa barabara hizi ndizo zinazochangia kwa kiasi kikubwa uchumi katika usafirishaji. Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa bahati mbaya sana TARURA wanakumbwa na bajeti ndogo. Je, Serikali itakuwa tayari sasa kuiongezea bajeti TARURA ili iweze kutekeleza majukumu yake haya makubwa ambayo imekabidhiwa? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Chatanda Mbunge wa Korogwe Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, tunacho chombo kinachosimamia ujenzi na ukarabati wa barabara vijijini; TARURA kwa sasa; ambacho tumekipa mamlaka ya kufanya kazi karibu kwa pamoja na Mamlaka ya Serikali za Mtaa kwa maana ya halmashauri za wilaya. Sasa kila TARURA iliyoko kwenye halmashauri hiyo jukumu lake ni kufanya mapitio ya barabara zote zilizopo ndani ya wWilaya hiyo kuona mahitaji ya ujenzi wake, ukarabati wake na matengenezo ya kila siku pale ambako panahitaji ukarabati huo na kutenga fedha na kuomba fedha kulingana na mahitaji yake. Kwa hiyo kila TARURA katika kila halmashauri inayo bajeti yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, inawezekana pia TARURA Wilaya ya Korogwe haitoshelezi mahitaji ya ukarabati wa barabara zake. Si rahisi kupata bajeti yote kwa asilimia 100 kulingana na mahitaji hayo lakini bado kipindi tulichonacho sasa mwezi wa pili tukiwa tunaelekea kwenye Bunge la Bajeti kuanzia mwezi wa nne basi TARURA ile kwenye halmashauri husika ioneshe mahitaji ya fedha kulingana na mahitaji ya barabara zao ili sasa tuanze kuingiza kwenye mpango wa fedha kwa ajili ya matumizi ya mwaka ujao wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niseme Serikali iko tayari kupokea maombi ya TARURA zote nchini za mahitaji ya fedha halafu tutazigawa sote kwa pamoja; na kupitia Kamati yetu ya Miundombinu inaweza kusimamia pia TARURA kupata fedha ya kutosha ili iweze kujenga barabara zake kwenye maeneo yake kama ambavyo halmashauri inahitaji kuboresha barabara zake. Ahsante. (Makofi)
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba kumuuliza Waziri Mkuu, Serikali imekuwa ikipeleka fedha nyingi katika Halmashauri zetu kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji na kukamilisha, lakini miradi hiyo imekuwa haitumiki kama ilivyokusudiwa kutokana na usanifu mbovu wa miradi na kutokamilika kwa miradi hiyo.

Je, Serikali ipo tayari kuchunguza na kuchukua hatua kwa wale wote watakaobainika kwamba, walisababishia hasara Serikali na kuwasabishia Wananchi kutopata huduma ambayo walikuwa wamekusudiwa kupewa na Serikali?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Chatanda, Mbunge wa Korogwe Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, upo ukweli kwamba, miradi yetu mingi ya maji ambayo inatekelezwa kwenye maeneo mbalimbali iko mingine haitekelezwi kwa viwango na kwa hiyo, haina thamani ya fedha kama ambavyo tumekusudia iweze kutekelezwa. Lakini pia kama ambavyo Waziri mwenye dhamana alipokuwa ameleta bajeti yake mbele yetu Wabunge alieleza hatua mbalimbali zilizochukuliwa dhidi ya miradi yote ambayo imetangazwa na haina thamani kama ilivyokusudiwa kwa fedha iliyotolewa. Na moja kati ya hatua ambazo amezifanya, alieleza hapa kwenye hotuba yake na ndio hasa kazi ambayo inafanywa, ameshaunda timu inayopita kukagua miradi yote nchini kwa kujiridhisha miradi hiyo kupitia BOQ zake kuona matengenezo yake na kama inakidhi thamani ya fedha kwa fedha zilizotolewa kwa mradi huo.

Mheshimiwa Spika, na pale ambapo sasa hakuna thamani ya fedha hizo hatua ambazo Mheshimiwa Mbunge anataka kujua zinachukuliwa. Na ninataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge tumewasikia ushauri wenu kwenye sekta ya maji ikiwemo na kuchukua hatua kali kwa watendaji wetu ambao wanasimamia miradi ya maji na maji hayapatikani, lakini mradi wenywe haujatengenezwa kwa viwango kwamba, hatua kali zitachukuliwa. Na Wizara sasa imeanza kupitia, Wizara yenyewe pale Makao Makuu, na inashuka ngazi ya Mikoa mpaka Wilayani ili kujiridhisha kwamba, tunakuwa na watumishi wenye weledi wa kutekeleza miradi hiii na kusimamia thamani ya fedha kwa manufaa ya Watanzania, ili huduma ziweze kutolewa kwa Wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaendelea na kazi hiyo na Wizara inaendelea kukagua miradi pamoja na ile tume, itakapokamilisha kazi itakuwa na majibu. Wale wote watakaothibitika hatua kali dhidi yao itachukuliwa. (Makofi)