Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Ali Salim Khamis (2 total)

MHE. ALI SALIM KHAMIS aliuliza:-
(a) Je, Shirika la Ndege Tanzania ni Shirika la pamoja kati ya Tanganyika na Zanzibar?
(b) Kama ndiyo je, Zanzibar ina asilimia ngapi katika Shirika la ATCL?
(c) Je, ni lini ATCL italipa deni la kodi ya kutua (landing fee) kwa Mamlaka ya Ndege Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ali Salim Khamis, Mbunge wa Mwanakwerekwe, lenye vipengele (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Kampuni ya Ndege ya Tanzania, Air Tanzania Company Limited ilianzishwa mwaka 2002 chini ya Sheria ya Makampuni (The Companies Act). ATCL ilichukua majukumu ya lililokuwa Shirika la Ndege la Tanzania (Air Tanzania Corporation) ambalo lilibinafsishwa kwa mujibu wa Sheria Na. 16 ya 2002 (Air Tanzania Corporation Reorganisation and Vesting of Assets and Liabilities Act, 2002).
(b) Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria nilizozitaja hapo juu ATCL inamilikiwa kwa asilimia 100 na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Umiliki wa ATCL haujatenganishwa kuonyesha asilimia za hisa zinazomilikiwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(c) Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Kiwanja cha Ndege cha Zanzibar inaidai ATCL kiasi cha shilingi 230,767,986.00 kama deni la tozo za kutua (landing fee). Madai haya ni sehemu ya orodha ya madeni ya siku nyingi ya ATCL ambayo yamewasilishwa Serikalini. Deni hili ni moja ya madeni ambayo yanahakikiwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na Serikali italipa deni hili mara baada ya kupokea taarifa ya uhakiki ambayo itathibitisha kuwa ni deni halali.
MHE. HAFIDH ALI TAHIR (K.n.y. MHE. ALI SALIM KHAMIS) aliuliza:-
Kisiwa cha Shungimbili kilichopo Wilaya ya Mafia kinamilikiwa na mwekezaji ambaye amekibadilisha jina na kukiita Thanda, mmiliki wake ni Kampuni ya Utalii ya Zululand ya Afrika Kusini. Aidha, kuna madai kuwa kisiwa hicho kimeuzwa kwa mwekezaji huyo; kwenye kisiwa hicho kuna hoteli yenye hadhi ya dunia na ndicho kisiwa ghali duniani kuishi kwani kwa siku ni USD 10,000 na ili upate chumba ni lazima ufanye booking kwa muda usiopungua siku saba:-
(a) Kama kisiwa hicho kimeuzwa: Je, kimeuzwa shilingi ngapi na hoteli hiyo inalipa kodi kiasi gani kwa Serikali?
(b) Je, Wizara ya Maliasili na Utalii inashirikiana vipi na Wizara ya Utalii Zanzibar hasa ukizingatia Wizara ya Mambo ya Nje ni ya Muungano katika Mikataba ya Kimataifa?
NAIBU WAZIRI WA MALISILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ali Salimu Khamisi, Mbunge wa Mwanakwerekwe, lenye vipengele (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kisiwa cha Shungimbili ni moja ya visiwa vitatu vilivyopo katika Wilaya ya Mafia. Visiwa hivyo vitatu na vingine 12 vinafanya jumla ya visiwa 15 ambavyo ni maeneo tengefu yanayosimamiwa na Taasisi ya Hifadhi za Habari na maeneo tengefu yaliyopo nchini, chini ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.
Kimsingi Taasisi hii ilianzishwa kwa Sheria ya Bunge Namba 29 ya mwaka 1994 ambapo miongoni mwa majukumu yake ni kusimamia maeneo yote yaliyotangazwa kuwa hifadhi za habari (Marine Parks) na maeneo tengefu ya bahari (marine reserves).
Mheshimiwa Naibu Spika, Kisiwa cha Shungimbili hakijauzwa na baada yake kimeingizwa katika uwekezaji kupitia Kampuni ya Thanda Tanzania Limited inayojenga Lodge ya kitalii ikiwa ni majawapo ya mipango ya Taasisi ya MPRU ya kuimarisha uwekezaji katika maeneo inayosimamia ili kuongeza mapato ya Serikali na kutekeleza Sera ya Utalii ya mwaka 1999. Aidha, uwekezaji huo umepita taratibu zote za Serikali na utakapokamilika mwekezaji atatekeleza wajibu wake ikiwemo kulipia tozo zote kwa mamlaka zinazohusika kwa mujibu wa sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, ndiyo yenye dhamana ya kuingia mikataba yote ya Kimataifa, yenye maslahi kwa nchi nzima Bara na Visiwani. Hata hivyo, pamoja na kwamba nyongeza ya kwanza ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 haijaorodhesha Sekta ya Utalii kama moja ya maeneo ya Muungano, haijazuia Wizara zinazosimamia Sekta ya Utalii kutoka pande hizi mbili kuendelea kushirikiana.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushirikiano kati ya pande mbili za Muungano unaozungumziwa unajumuisha maeneo ya utangazaji wa vivutio vya Tanzania Kimataifa kama nchi moja, utayarishaji taarifa na ujenzi wa mifumo imara ya ukusanyaji wa takwimu kupitia Kamati inayojulikana kama The Steering Committee of the Tanzania Tourism Sector Survey na mikutano mbalimbali ya ushirikiano kati ya Tanzania Bara na Zanzibar na ile ya uwezeshaji utalii (Tourism Facilitation Committee) ya wadau wa utalii. Wizara yangu itaendelea kudumisha na kuuboresha uhusiano huu kwa sababu mtawanyiko wa vivutio vya utalii unagusa Tanzania kama nchi moja.