Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Doto Mashaka Biteko (25 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Naomba na mimi nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii ya kuzungumza mbele ya Bunge lako.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nianze moja kwa moja, nina miradi ya barabara ambayo iko kwenye Wilaya yetu ya Bukombe ambayo namuomba Mheshimiwa Waziri aiangalie kwa jicho la pili kwa sababu Wilaya ya Bukombe kwa ramani yake jinsi ilivyo, upande wa Kusini imepakana na hifadhi kwa hiyo hakuna namna ya kupita. Namna pekee ya kufungua Wilaya ya Bukombe ni kufungua barabara za upande wa Kaskazini. Kwa hiyo, ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri utuangalie Wilaya ya Bukombe utuunganishe na Wilaya nyingine za Mkoa wa Geita na mikoa ya jirani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, iko barabara inayotokea Ushirombo inapita Katome, inapita Nyang‟orongo, inapita Nanda, inapita Bwelwa, inapita Iboya, inapita Bwendamwizo, inapita Ivumwa, inapita Wigo, inatokea Nyaruyeye Wilaya ya Geita, inakwenda Nyarugusu inatokea Buyagu hadi Geita Mjini. Barabara hii ni muhimu sana kwa sababu inawasaidia wananchi wa Wilaya ya Bukombe kusafirisha mazao yao kuyapeleka Geita. Barabara hii ni muhimu sana kwa sababu inawaunganisha wananchi wa Wilaya ya Bukombe pamoja na wananchi wa Wilaya ya Nyang‟hwale kwenda mkoani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba pia, Mheshimiwa Waziri aingalie barabara ambayo inatuunganisha Bukombe pamoja na Wilaya ya Chato. Barabara hii ni muhimu sana kwa uchumi wa wananchi wa Geita, kwa wananchi wa Chato, pamoja na wananchi wa Bukombe. Barabara yenyewe ni hii inayopita Bulega, inatokea Kavoyoyo, inaenda Shisabi, inaenda Mwabasabi, inaenda Matabe, inatokea Bwanga kwa Dkt. Kalemani, tunaunganishwa na Daraja moja la Nyikonga. Mheshimiwa Waziri tunakuomba sana hii barabara ni muhimu sana, uiweke na yenyewe iweze kutusaidia kwenye kukuza uchumi wa watu wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Lunzewe Bwanga, leo ni miaka miwili imesimama haijengwi. Ni barabara ambayo inajengwa kwa kiwango cha lami, kwa muda wote huu haijafanyiwa kazi, lakini mbali na hivyo wananchi wa Lunzewe pale hawajalipwa fidia kwa miaka yote hiyo. Hawawezi kuendeleza nyumba zao, hawawezi kufanya chochote kwa sababu wanasubiri fidia kutoka TANROADS. Ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri utusaidie barabara hii ijengwe, lakini vilevile wananchi wale waweze kupata fidia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba vilevile, Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni aliwaahidi wananchi wa Bukombe; na hii ni sauti ya wananchi wa Bukombe inakulilia Mheshimiwa Waziri, kilometa tano za lami kwenye Mji wa Ushirombo tunaziomba. Sijaona mkakati wa aina yoyote wa kutekeleza ahadi hii, ninakuomba sana, wananchi wanaamini kwamba ahadi hii itatekelezwa na tuanze sasa hivi. Kilometa tano tu na sisi pale tupate lami Mheshimiwa Waziri, ili siku ukija na suti yako usitoke na vumbi, uje uko smart, utoke ukiwa smart kwa sababu utakuwa umetuleta barabara ya lami. Ninakuomba sana uzingatie hilo Mheshimiwa Waziri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, uwanja wa ndege wa Geita. Mkoa wa Geita ndio mkoa unaotoa dhahabu na madini, Wizara ya Nishati na Madini mapato yake makubwa yanatokea Geita, lakini jambo la kusikitisha ni kwamba pamoja na upya wake hatuna uwanja wa ndege. Uwanja wa ndege tuanaotumia ni ule wa Geita Gold Mine. Ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri, umeonesha hapa kuwa ziko fedha ambazo zimepangwa kwa ajili ya uwanja wa Geita, tunaomba fedha hizo zitolewe, uwanja wa Geita ujengwe kwa haraka ili wananchi wetu waweze kupata maendeleo na usafiri wa anga. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ninaomba vilevile nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, ile barabara inayotoka Katoro kuja Ushirombo, inapita Nyang‟hwale, barabara hii ni barabara kubwa inapitisha magari makubwa. Barabara hii tunaomba na yenyewe uiwekee lami kwa sababu, hii barabara ukiiwekea lami, utapunguza mizigo kwenye barabara ya Bwanga ambayo kwa vyovyote vile haiwezi kuhimili mizigo ya magari mengi yanayopita pale.
Mimi ninafahamu kwa Serikali hii ya Awamu ya Tano mambo haya yanawezekana. Ninakutia moyo Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, ninakutia moyo nikiamini kwamba maneno haya niliyoyaomba na sauti ya Wanabukombe utaizingatia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, Mungu akubariki sana. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi nyingi sana kwa Wizara kwa hotuba nzuri sana. Pamoja na mambo mengine, naiomba Wizara iangalie na isaidie wananchi wa Bukombe kwa mambo kadhaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo kubwa la Wilaya ya Bukombe ni la hifadhi ya Kigosi Muyowosi. Nashauri Wizara iwe na mpango wa kuwashirikisha wananchi katika uhifadhi na kuweka mahusiano mazuri kati ya wananchi na wahifadhi
Kwa kuwa eneo kubwa la Wilaya ya Bukombe ni hifadhi, naiomba Wizara na kuishauri iweke Ofisi ya Maliasili Wilayani Bukombe. Kwa sasa wananchi wanafuata huduma Wilayani Kahama ambako ni mbali kwa kilometa 96. Nawatakia kazi njema Waheshimiwa Waziri na Naibu Waziri
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Kabla sijasema, namshukuru Mungu kwa nafasi hii ambayo amenipa ili niweze kusimama kwenye Bunge hili na kusema machache.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kuwapongeza sana watoa hoja, Waziri wetu wa TAMISEMI pamoja na Waziri wa Utumishi, Mheshimiwa Simbachawene pamoja na Mheshimiwa Kairuki kwa kuwasilisha bajeti yao vizuri na bajeti ambazo kwa kweli zimebeba mambo mengi sana ambayo tunayaendea kwa mwaka wa fedha unaokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana tunatofautiana kutazama kitu kimoja, mimi nianze kwa kutoa shukrani kwa Serikali kwa kazi kubwa inayofanyika Bukombe. Wewe ni shahidi, kwa muda mrefu fedha za dawa zilikuwa hazipatikani kwenye zahanati, vituo vya afya na hospitali zetu, leo ninavyosimama hapa Wilaya ya Bukombe tulikuwa na mahitaji ya fedha za dawa kwenye vituo vya afya na zahanati zaidi ya shilingi milioni 600 na tunafurahi kusema kwamba sasa hivi tumeshapata shilingi milioni 512. Hii ni kazi kubwa sana, inahitaji kushukuriwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile hatukuwa na magari kwa ajili ya wagonjwa, Wilaya yetu ya Bukombe tumepata magari mawili kwa ajili ya wagonjwa yatakayokuwa yanahudumia kwenye Kituo cha Afya cha Uyovu pamoja na cha Ushirombo. Tumepata fedha kwa ajili ya kupanua shule ya msingi Ibamba, shule ambayo imeandikisha watoto wa darasa la kwanza peke yake 1,200. Wasikivu hawa, tulipowafuata
kuwaomba pesa, wametupa pesa shilingi milioni 92 kwa ajili ya kupanua shule hiyo. Naomba nichukue nafasi hii kuwashukuru sana kwa niaba ya wananchi wa Wilaya ya Bukombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna shule maalum mbili Wilaya ya Bukombe, shule zenyewe ni shule ya msingi Uyovu pamoja na Ushirombo. Nafurahi kusema kwamba Serikali wametusikiliza, wametupatia fedha kwa ajili ya shule hizi shilingi milioni 100 tumekwisha patiwa kwa ajili ya kuhudumia watoto hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapojaribu kuhangaika kuona vijana tunawasaidia vipi kwenye nchi yetu, Wilaya ya Bukombe maombi tuliyopeleka kwa ajili ya Mfuko wa Maendeleo ya Vijana, tayari Serikali imetusikia imetupatia, imetupatia shilingi milioni 51 za kuanzia kuwapatia mikopo vijana wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mambo ni lazima tuyaseme, usipoweza kushukuru kwa kidogo, huwezi kushukuru kwa kikubwa hata kama utapatiwa. Naomba kwa moyo wa dhati, niishukuru Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya na Mawaziri wake ambao kwa kweli Wabunge wote hapa na wananchi ni mashahidi, tunawaona wanavyohangaika kuona
Tanzania inapata maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo, niseme machache ambayo sasa yanahitaji kuangaliwa na Serikali ili tuweze kuboresha. Jambo la kwanza, kwenye Wilaya yetu ya Bukombe tumekuwa tukiomba watumishi kwenye Idara ya Afya, hatujapatiwa watumishi wa kutosha na bahati mbaya sana hata hao wachache waliopo, wanapewa uhamisho bila kuletwa watumishi wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano, Wizara ya TAMISEMI wamehamisha madaktari saba wa Hospitali ya Wilaya ya Bukombe. Nimeuliza hili jambo hapa Bungeni, nimewafuata na ofisini kuwauliza, jamani mnapohamisha madaktari saba kwa mara moja kwenye Wilaya ya Bukombe mnatarajia nini kwa wananchi wetu? Ninaomba kupitia bajeti hii, Waziri wa TAMISEMI utusaidie, madaktari wetu saba wale
mliowahamisha mara moja mnatuletea lini fidia ya madaktari hao? Kwa sababu hali iliyopo kule siyo nzuri, wananchi wanahitaji huduma, lakini watoa huduma ni wachache sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeomba vile vile Hospitali yetu ya Wilaya ya Bukombe ambayo ni Hospitali ya Wilaya ipanuliwe, theatre yake ni ndogo. Ilikuwa ya mwanzo, kwa ajili ya kutumika kwa muda tu, baadaye watajenga theatre nyingine. Nasikitika, toka miaka hiyo ya 1990 haijawahi kupanuliwa. Naomba hili jambo na lenyewe liangaliwe ili wananchi hawa waweze kupata huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo madai ya watumishi wa Idara ya Afya, wanadai fedha nyingi, on-call allowance. Wanadai allowance zao hizi hawalipwi, wanadai mishahara yao na malimbikizo yao, tunaomba na hili Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI utakapoanza kuhitimisha hoja yako, utuambie watumishi hawa wanaanza kulipwa lini? Kwa sababu bila hawa, wananchi wetu hawawezi kutibiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niongelee suala la elimu na kwenye hili nitaongelea elimu yenyewe lakini nitaongelea walimu. Hakuna muujiza wa kukomboa elimu hii kama hatuwezi kuwaangalia walimu wa Tanzania. Fanya kila unachoweza, unaweza ukawa na darasa lina vigae, masofa na television, lakini kama hakuna mwalimu aliyepewa motisha, kazi inayofanyika pale haiwezi kuleta matokeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walimu wa Tanzania wana malalamiko yao mengi, tusipoweza kuyapatia majibu kwa awamu hii, dawa ya elimu ya nchi hii hatuwezi kuipata. Walimu 80,000 wa nchi hii wamepandishwa madaraja, hawajarekebishiwa mishahara yao. Leo nakuomba Waziri wa TAMISEMI utusaidie, uwape tumaini walimu wa Tanzania, madaraja yao haya mnaanza kuyarekebisha lini na kuwalipa mishahara yao?
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo walimu ambao wamepandishwa madaraja, baada ya kuwa wamepandishwa madaraja, wameonja mshahara mpya, mmewarudisha nyuma kwa sababu ya uhakiki. Mheshimiwa Waziri tunakuomba utuondoe kwenye kitendawili hiki. Wale waliopanda madaraja, wapatiwe mishahara yao ili waweze kiushi sawa sawa na jinsi ambavyo walikuwa wanatarajia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri
hili aliangalie. Wakati mwingine unaweza usiwe na fedha, lakini lugha nzuri kwa watu inaweza kuwapa
motisha wa kufanya kazi. Wapo watendaji wa Serikali na nichukue nafasi hii kumshukuru sana na
kumpongeza sana Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Amos Makalla, nilimuona kwenye television, anawatia moyo
walimu wa Tanzania. Wapo watu wengine wanafunzi wakifeli, analaumiwa Mwalimu Mkuu, unamvua madaraka
Mwalimu Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya mwanafunzi kufeli siyo kama kufyatua tofali kwamba utaweka udongo kwenye kibao cha tofali, tofali litatoka, haiwezekani! Nataka nikwambie unaweza kumlazimisha mwalimu kuhudhuria kazini, huwezi kumlazimisha mwalimu kufundisha. Suala la kufundisha ni suala la mapenzi. Walimu wakati sisi tupo nyumbani tunaangalia television, wao wamejifungia kwenye vyumba vyao wanajiandaa kwa ajili ya watoto wetu kesho yake. Walimu hawa hawana mishahara mikubwa, wanajinyima fedha zao waweze kuchukua fedha hizo wakanunue vifaa vya kufundisha na maandalizi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapowavunja moyo kwa kuwaambia maneno ya kejeli, ninaomba Mheshimiwa Waziri unaposimama, ulikemee jambo hili walimu wa Tanzania wasikie. Walimu hawa wanahitaji kuthaminiwa, kuheshimiwa, unamvua Mwalimu Mkuu madaraka kwa sababu ya kufeli mwanafunzi, mwalimu pekee sio sababu ya mwanafunzi kufeli, zipo sababu nyingi zinazosababisha mwanafunzi kufeli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ya kwanza inaweza kuwa mzazi, sabab ya pili inaweza kuwa mazingira ya kazi na ya tatu inaweza kuwa mwanafunzi mwenyewe na sababu nyingine anaweza kuwa mwalimu. Unachukua sababu moja ya mwalimu peke yake, unamvua madaraka!

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya walimu wa Tanzania na kwa niaba ya walimu wa Bukombe naomba nipaze sauti yao, tabia hii iachwe ya baadhi ya watu, wanaichafua na wanaigombanisha Serikali na walimu wa Tanzania, hatuwezi kukubali kama Bunge tukaona walimu ambao sisi wametufikisha hapa wanaendelea kudharauliwa na kuonewa kwa maneno ya kutungwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Mheshimiwa Waziri wa Utumishi ukemee hili kwa sauti kubwa, watendaji kule chini wasikie na mimi nafahamu wewe Mheshimiwa wa Utumishi unafahamu ni watu gani wamefanya haya. Walimu wa Tanzania hatuwezi tukakubali wakaendelea kuonewa kwa kiwango hiki.
Tuwasaidie walimu kwa kuwapatia vifaa vya kufanyia kazi kwa kuwapatia fedha za kutosha, zile stahiki zao kama kupanda madaraja yao walipwe kwa wakati, mambo ya kuwapiga danadana inatosha, sasa hivi nao wanahitaji wapate chao mkononi na wafanye kazi kwa kujituma zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie Mfuko wa Barabara. Wilaya yetu ya Bukombe upande wa Kusini tunapakana na milima, maeneo ya Imalamagigo, Mchangani na Nifa, maeneo yote haya tumeomba fedha kwa ajili ya Mfuko wa Barabara turekebishe barabara hizo hatuwaji kupata hata shilingi moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekwenda TAMISEMI mara kadhaa kuwaomba ndugu zangu watusaidie, watu wanateseka, wanafunzi wanashindwa kwenda...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii nikushukuru sana kwa nafasi hii ya kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Elimu kwa hotuba yake hii aliyoileta kwenye Bunge letu hili. Nampongeza vilevile Mheshimiwa Naibu Waziri wa Elimu kwa kazi kubwa anayoifanya kwa ajili ya kuinua elimu ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naipongeza sana Kamati ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa taarifa yao ambayo kwa kweli ilikuwa inajieleza vizuri, sana na nimetoa ushauri ambao mimi binafsi nauona ni ushauri wa msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Confucius ambaye ni Mwanafalsafa wa Kichina aliwahi kusema maneno haya, akasema kwamba ukitaka kupanga kwa ajili ya mwaka mmoja, basi panda mpunga. Ukitaka kupanga kwa ajili ya miaka 10 basi panda miti na ukitaka kupanga kwa ajili ya miaka 100 ijayo, basi mwelimishe mwanao au mtoto wako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ndiyo moyo wa Taifa hili. Taifa lolote ili liweze kuendelea na tafiti zimeonesha, kuna uhusiano wa moja kwa moja wa ukuaji wa elimu na ukuaji wa uchumi; hivi vitu vinakwenda pamoja. Taifa ambalo limeendelea kielimu kwa vyovyote vile linajikuta linaendelea vilevile kiuchumi. Kwa hiyo, tunajadili Wizara ambayo ni muhimu sana kwa nchi yetu; na kwa kweli namwomba Mheshimiwa Waziri aendelee kuchapa kazi kwa sababu bila hivyo Taifa letu hili tutachelewa sana kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa uamuzi wake wa kutoa elimu bure kwa Watanzania. Uamuzi huu, unaweza ukaonekana wa kawaida kwa sababu ni kawaida, hata mbuzi huwa haoni umuhimu wa mkia wake mpaka uondoke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikupe taarifa kwamba kabla ya elimu bure, Wilaya ya Bukombe watoto waliokuwa wanaandikishwa darasa la kwanza mpaka la saba walikuwa 45,000 peke yake. Baada ya kuanzishwa kwa elimu bure, sasa hivi watoto walio darasa la kwanza kwa elimu ya msingi yote, wanafika 75,000. Maana yake ni nini? Maana yake ni kwamba wapo watoto wengi zaidi ambao walikuwa wanaacha shule, walikuwa wanashindwa kwenda shule kwa sababu ya michango na ada hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunahitaji kumtia moyo Mheshimiwa Rais, tuitie moyo Serikali iendelee kuwekeza zaidi kwenye elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefuatilia hotuba ya Mheshimiwa Waziri na yako mambo ambayo nataka nichangie kidogo. Jambo la kwanza ni ukaguzi wa elimu. Suala la ukaguzi wa elimu lilishaelezwa kwa kila aina ya lugha, hapa Bungeni na nje ya Bunge. Ukaguzi wa Elimu wa Tanzania una hali mbaya sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi ku-suggest na vyombo vingine viliwahi kupendekeza kwamba ili ukaguzi wa elimu uweze kuwa imara ni lazima tuutoe kwenye mikono ya Wizara uwe wakala wa kujitegemea. Serikali ilishawahi kuahidi hapa Bungeni kwamba inaanzisha mchakato wa kufanya ukaguzi kuwa wakala wa ukaguzi. Ahadi hiyo nimesoma kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Elimu sasa hivi, wala hakuna kinachozungumziwa, kana kwamba hakuna kitu kilichowahi kusemwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakupa mfano. Kwenye kijarida cha elimu (ninacho hapa), cha Januari hadi Machi, mwaka 2013, ukurasa wa nne, Mheshimiwa Waziri wa Elimu alisema yafuatayo: “Katika jitihada zake za kuipa mamlaka zaidi na uwezo na hivyo kuongeza ufanisi katika ukaguzi wa shule na Vyuo vya Ualimu, Serikali inakusudia kuibadili Idara ya Ukaguzi wa Shule iliyoko chini ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, kuwa Wakala wa Kujitegemea. Imeandikwa humu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haitoshi, Kamati ya Bunge lako iliyokuwa inaongozwa na Mheshimiwa Margaret Sitta mwaka wa fedha 2013/2014, ilikuja na mapendekezo hayo hayo ya kuifanya ukaguzi kuwa Wakala Maalum wa Elimu na Waziri wa Elimu wakati huo, mimi sijawa Mbunge, nilikuwa nje, kwa sababu mimi ni mdau wa elimu, aliahidi kuwa jambo hilo linafanyiwa kazi. Nataka kujua Mheshimiwa Waziri, hivi hili jambo limeishia wapi? Hivi hili jambo lilikuwa tu ni kwamba tumalize kipindi hicho cha bajeti hiyo, halafu maisha yaendelee? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukaguzi wa elimu hauwezi kuendelea kwa mfumo tulionao. Wakaguzi wana hali mbaya; Wakaguzi hawana kila kitu, kuanzia rasilimali mpaka uwezo wa rasilimali watu. Wakaguzi ni wachache, shule ni nyingi. Lazima sasa tuangalie utaratibu mpya wa kuhakikisha kwamba Walimu hawa na wao tunaweza kuwapatia fursa ya kukaguliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, iliwahi kusemwa iwepo Bodi ya Wataalam wa Walimu. Hii Bodi kwenye kitabu cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri sijaiona. Hivi hata hivi vyeti feki tunavyozungumza, kama kungekuwa na Bodi ya Kudhibiti Walimu ingekuwa imeweza kuligundua hilo mapema. Hili lilishawahi kuahidiwa humu humu Bungeni na Mheshimiwa Shukuru Kawambwa wakati ule akiwa Waziri kwamba Serikali ipo katika hatua za mwisho za kuanzisha Bodi ya Walimu. Hii bodi iko wapi? Mbona na yenyewe siioni! Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anakuja kujibu, atusaidie kutupa majibu sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo limezungumzwa na wengi ni suala la vitabu. Nami nataka nizungumze kidogo hapa, nimevisoma hivi vitabu. Mheshimiwa Waziri ameeleza kwenye hotuba yake ukurasa wa 21, amesema kwamba vitabu hivi vina makosa ya kimaudhui na hivyo uchambuzi wa kina unafanyika ili vitabu vilivyochapishwa mwaka 2016/2017, kubaini endapo vina dosari; nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri, vitabu hivi siyo tu kwamba vina makosa ya kimaudhui, vina makosa mengi, wala havifai kupelekwa sokoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa sababu tu aliyechapisha pengine ni Serikali, anapata kigugumizi. Mwaka 2016, Mei hapa hapa Bungeni, Mheshimiwa Waziri alitueleza kwenye hotuba yake ukurasa wa 55, kipengele cha tatu, akasema hivi:

“Mheshimiwa Spika, vimeandikwa na kuchapishwa vitabu nakala 6,862,000. Akasema hivi, katika vitabu hivyo, vitabu 2,807,000 vimebainika kuwa na makosa na kwa hiyo, wamemwambia aliyevichapisha avirudishe akavichape upya.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi vilivyochapishwa na Serikali vina makosa lukuki. Nitakupa mfano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitabu cha kwanza cha English, Form Four, kina makosa 34 kwa uchambuzi wangu. Kina makosa ya mpangilio; yaani ukurasa wa kwanza kwenye jedwali (table of content) lenyewe lina makosa. Anasema Preface iko roman (ii) ukienda kwenye kitabu iko roman (iii), ukiangalia chapter one, anasema iko ukurasa wa nne, ukienda kwenye kitabu ndani, iko ukurasa wa kwanza. Ni makosa mengi ambayo siwezi kuyaeleza! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kitabu cha Kidato cha Tatu, kina makosa 12 ya kimantiki na nimwambie Mheshimiwa Waziri, siyo makosa ya kimaudhui, ni makosa ya kimantiki, makosa ya kimaudhui, makosa ya kiuandishi. Kwenye mwongozo wao walionao, huu hapa ninao. Unataka kitabu chochote kilichozidi kurasa 100 kifungishwe au kiwe binded kwa kutumia gundi, lakini ninacho kitabu kiko hapa, kina zaidi ya kurasa 100 lakini kimegundishwa kwa pini. Hata ubora wa vitabu vyenyewe haupo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais anahangaika kutafuta fedha kwa ajili ya watoto wa Tanzania. Haiwezekani Mheshimiwa Rais atenge shilingi bilioni 18.77 kila mwezi kwa ajili ya watoto. Baba anatoa fedha kwa ajili ya watoto wake wapate chakula kizuri, wanaenda kupewa matango pori! Nyumba hii ambayo ni ya kwetu sisi Wabunge, Nyumba hii ya Mheshimiwa Ndugai na Mheshimiwa Tulia Ackson ikubali mambo haya yatendeke mbele yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atuambie, ni shilingi ngapi zimetumika? Tumeambiwa zaidi ya shilingi bilioni 100 zimetumika kuchapisha vitabu vibovu hivi. Hizi fedha ni kama zimepigwa kiberiti na sasa hivi viko kwenye mzunguko vinafundisha watoto kuwapatia maarifa ambayo ni substandard. Tunapeleka wapi Taifa hili? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikwambie, Walimu wa Tanzania baada ya kuliona hili waliweka pembeni vitabu vyenu wakaachana navyo, wakaanza kufundisha kwa maarifa yao wanayoyajua. Hivi hata wingi wa neno sheep; neno sheep peke yake, kuna wataalam ambao wanakaa kupitia vitabu hivi, nimewasoma. Kuna mtaalam wa curriculum, kuna wataalam wa kutoka Vyuo vya Ualimu, kuna wataalam wanaotoka NECTA, kuna wataalam wa… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii na naomba nimshukuru Mungu kwa kunipa kibali cha kusimama tena ili niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijasahau, naomba nitangulie kuunga mkono hoja iliyowasilishwa na mkwe wangu, Mheshimiwa Dkt. Tizeba, Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Kwa kweli nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, kwa hotuba yake nzuri aliyoiwasilisha hapa Bungeni. Kama tutakuwa wakweli, tutaona kwa vitendo kile ambacho Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni alikiahidi Tanzania nzima wakati anazunguka; lile jambo la kuondoa tozo za kero na ushuru mbalimbali wa kero kwa wakulima. Jambo hili watu wengine walikuwa wanadhani ni ndoto, sasa limekuwa kweli kwa sababu leo Mheshimiwa Waziri ametuletea orodha ndefu sana ya tozo mbalimbali ambazo zimefutwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Bukombe, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutekeleza jambo hili, kama kawaida yake, mambo mengi ambayo ameyaahidi yamekuwa yakitekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Bukombe wanashukuru sana kwamba Wizara hii kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu tumejengewa soko kubwa sana la kisasa kwa ajili ya wakulima wa muhogo ambalo liko Namonge. Soko hili litasaidia sana wananchi wa Wilaya ya Bukombe na Mkoa wa Geita na nchi jirani, kwa sababu ni soko kubwa sana, linawasaidia hawa wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, ile mbegu ya mihogo inayoitwa mkombozi, inazalishwa kwenye Wilaya ya Bukombe, multiplication yake inafanyika kwenye Wilaya ya Bukombe ambapo Kata nne na vikundi 52 vinafanya kazi hii. Kazi nzuri sana hii imefanywa na Wizara ya Kilimo kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe. Tunawashukuru sana, kwa kweli hili jambo litatusaidia kwa sababu mihogo tuliyokuwa nayo mbegu yake ilikuwa imechoka, isingeweza kuwapatia tija wakulima wa Wilaya ya Bukombe na Mkoa wa Geita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, natamani nizungumze kidogo juu ya zao la pamba. Tanzania tuna potential ya kuzalisha pamba takriban tani milioni moja, lakini kwa sasa kwa taarifa ambayo Mheshimiwa Waziri amewasilisha hapa, tunazalisha pamba kwa mwaka mzima tani 122,000 peke yake. Kwa hiyo, pamba kwa kweli ambalo lilikuwa ndilo zao muhimu sana kwa wananchi walilokuwa wanalitarajia sana kubadilisha maisha yao, limeanguka na kila mwaka ukiangalia graph ya trend inashuka kila wakati. Kwa mfano, msimu wa mwaka 2012/2013 tulipata pamba tani 350,000; mwaka 2013/2014 tukapata pamba 249,000; mwaka wa 2015/2016 tukapata tani 149,445; na mwaka huu 2017/2018 Mheshimiwa Waziri ametuonesha dhahiri pale tumepata tani 122,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini tumefika hapo? Tumefika hapo kwa sababu tunaona kama zao hili limetelekezwa na wananchi wengi wamekata tamaa ya kulima pamba. Ukienda kwenye Mkoa wa Geita, kwa mfano, msimu wa mwaka 2015/2016 jumla ya ekari 119,701 zililimwa, lakini msimu uliopita pamba imeshuka. Wakulima wengi wamehama kulima pamba, wamelima ekari 73,546 peke yake. Wananchi wamekata tamaa kwa sababu yako maudhi madogo madogo ambayo naomba Mheshimiwa Waziri ayaangalie kwa haraka ili tuweze kuyatatua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, mbegu ya pamba tuliyonayo (UK 91) ni mbegu ya zamani sana, ya miaka 24 iliyopita, bado iko kwenye circulation, matokeo yake mbegu hii haiwezi kuhimili magonjwa, haiwezi kuhimili mabadiliko ya tabianchi na mbegu hii haitupi tija. Sasa hivi Tanzania ekari moja tunazalisha pamba kiasi kidogo sana ukilinganisha na wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitatoa mfano; wastani wa kuzalisha pamba duniani kwa heka, ni tani 2.2. South Africa wanazalisha tani tisa; Burkina Faso wanazalisha tani 1.2; Syria tani 4.9; Egypt tani 2.9; na Tanzania 0.7 na Mheshimiwa Waziri anafahamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningekuwa naruhusiwa na Kanuni za Bunge, nikasema Wabunge wote ambao wamesoma kwa pamba wasimame hapa na wapige kelele, waseme ndiyo! Utapata kazi sana kuwanyamazisha. Kwa sababu wengi waliomo humu wameishi na wamesomeshwa kwa zao la pamba. Hata hivyo kwa sasa zao hili limekuwa yatima! Kuna kiongozi mmoja kule Wilaya ya Bukombe aliwahi kuwaambia wananchi kwenye mkutano wa hadhara, kwamba achaneni na pamba limeni viazi kwa sababu hakuna mtu anayehangaika nayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri atuhangaikie zao letu la pamba. Mauzo ya nchi kwa mujibu wa taarifa ya BOT yameshuka. Hata hayo yenyewe, utaweza kuona kwa taarifa ya mwezi wa Nne iliyopita, mauzo ya pamba tumeuza dola milioni 43 peke yake, wakati mwaka uliopita tu tuliuza 53.1. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri aje na mkakati wa kuwasaidia wakulima juu ya upatikanaji wa pamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, najaribu kujiuliza, hivi kwa nini mkulima huyu asiingizwe kwenye value chain ya pamba? Tujenge ginnery hizo, mkulima aende akauze pamba yake pale; akiwa pale auze sufi, mbegu, achukue mashudu yake akafanyie kazi nyingine. Hivi inakuwaje mkulima anabeba pamba, humo ndani ya pamba anauza na byproduct nyingine zote zinakwenda nje ya nchi?

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaambiwa pamba yote inayozalishwa Tanzania 70% inakwenda nje ya nchi. Maana yake ni nini? Maana yake ni kwamba tunapeleka ajira nje ya nchi, tunapeleka uchumi kwa watu wengine. Saa imefika Mheshimiwa Waziri tuje na mkakati, hizi ginnery, tupeleke pamba yetu kama mkulima anavyopeleka alizeti kule Singida. Mashudu yawe ya mkulima, mafuta yawe ya mkulima na mbegu iwe ya mkulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, mbegu hii tunayotumia ya UK 91, hapa leo atuambie tunaachana nayo lini? Tunahitaji mbegu ya UK M08 ambayo imethibitishwa kitaalam ambayo GOT yake ni 44%. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri hili na lenyewe tuliangalie.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo lingine limezungumzwa hapa kuhusu habari ya ushirika. Ushirika ndiyo ilikuwa dawa ya kumsaidia mkulima wa Tanzania. Ushirika umekufa kwa sababu ya wajanja wachache. Kipindi kilichopita Serikali ilipeleka fedha kwa ajili ya kufufua ushirika, ikapeleka management kwa ajili ya kuinua ushirika. Leo ushirika huu badala ya kuwasaidia wakulima na wao wamebadilika kuwa wanunuzi wa pamba kama ginneries wengine. Nyanza ananunua pamba kama ambavyo sijui shirika gani linanunua pamba; haiwezekani kuwasaidia wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakulima wana shida ya pembejeo. Ndiyo maana msimu uliopita wakulima walipatiwa mbegu ya pamba ambayo haikuota, wakulima wakapatiwa madawa ambayo hayakuua wadudu, lakini ikashangaza ginners bila aibu wakaenda siku ya kununua pamba wanahitaji kukata fedha kutoka kwa wakulima kwamba walichukua madawa na mbegu. Madawa gani ambayo hayakuua?

Mheshimiwa Naibu Spika, nani alikwamisha? Kwenye mlolongo mzima wa kuagiza pembejeo ni mrefu mno! Kuna producer huko juu, kuna agent hapa katikati, kuna mtu mwingine ni quality assurance ambaye ni TPRI. TPRI wakati ule tuko kwenye mgogoro wa madawa, tulihangaika naye sana. Bodi ya Pamba wanaonesha kwamba TPRI hajawahi kuleta majibu, kwa nini mbegu haioti? Kwa nini madawa hayakuua wadudu?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri awaonee huruma wananchi hawa, wananchi hawa walisomesha watoto wao kwa pamba na benki yao iliyokuwepo pekee kwa wananchi wa Kanda ya Ziwa na hasa Mkoa wa Geita na Wilaya ya Bukombe kila shilingi waliyokuwa wanaipata walikuwa wananunua mifugo. Mifugo kwa sasa na yenyewe ina changamoto yake. Sasa hivi kila mtu anayezunguamza anaiona kama jambo baya, jambo ambalo ni laana, mharibifu wa mazingira mkubwa. Wafugaji hawajasaidiwa, kwa namna gani waweze kufuga kisasa?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna watu wanazungumza, punguzeni mifugo; hivi wanapunguza vipi mifugo wakati hata viwanda vya kuchakata nyama hatujavijenga? Namwomba sana Naibu Waziri atusaidie.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nataka kuzungumzia ni kuhusu matrekta...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini
NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. DOTO M. BITEKO): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili na mimi nitoe mchango wangu kwa ajili ya hoja ambayo imewekwa mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijasema, naomba nichukue nafasi hii vilevile nimshukuru sana Mungu, mwingi wa rehema ambaye ametupa uzima na afya mpaka kuifikia siku ya leo na kwa kweli bila yeye tusingekuwa hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba vilevile nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa imani kubwa ambayo alinipatia na kuniteua kuwa Naibu Waziri wa Madini. Naomba niseme tu kwamba nafasi hii ambayo ameniteua nitafanya kazi hii kwa nguvu zangu zote, kwa weledi mkubwa na kwa kumtanguliza Mungu mbele ili ndoto ambayo yeye anaiona kwa ajili ya nchi hii niweze kumsaidia kuifikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba vilevile nimshukuru Mheshimiwa Waziri wa Madini, mtoa hoja, dada yangu, Mheshimiwa Angellah Kairuki, ambaye kwa kweli pamoja na mambo mengine amekuwa mwalimu mzuri sana kwangu. Mtafahamu mimi nimeteuliwa mwishoni, nimeingia Wizarani nikiwa mgeni. Mheshimiwa Waziri huyu, pamoja na kwamba yeye ni Mbunge mwenzangu, amekuwa mwalimu mzuri sana kwangu. Mimi naweza kuwa shahidi na Wabunge wengine ambao wameshafanya kazi na Mheshimiwa Angellah Kairuki watakuwa mashahidi, ni mtu wa pekee ambaye anapenda kuona kila mmoja anatumia kila talanta aliyonayo kutekeleza majukumu yake na yeye anakusaidia kufanya kazi yako kwa urahisi. Kwa kweli ningekuwa na muda wa kusema ningesema sana kwa bahati kubwa ambayo Mungu amenipa ya kufanya kazi na Mheshimiwa Waziri huyu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nimshukuru sana Mheshimiwa Stanslaus Nyongo, Naibu Waziri wa Madini. Huyu tunaitana pacha; yeye alitangulia kuteuliwa pale Wizarani, amenipokea, ameni-orient vitu vingi, nimejifunza mambo mengi sana kutoka kwake kwa namna ya utendaji lakini kuifahamu Wizara kwa sababu nilikuwa mgeni na yeye alinitangulia kufika hapo. Kaka yangu nakushukuru sana, Mungu akubariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kuishukuru sana familia yangu; mke wangu mpenzi Bernadetha Biteko kwa kuendelea kunivumilia, yeye pamoja na watoto wetu, wakati natekeleza maukumu haya. Naomba niwashukuru sana wananchi wa Bukombe ambao wao ndio walinichagua na kunituma kuwawakilisha kwenye nyumba hii. Naomba niwahakikishie kwamba kazi ambayo walinipa kuifanya kwa niaba yao ntaendelea kuifanya kwa nguvu zangu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo ya utangulizi, naomba sasa nitangulie kusema naunga mkono hoja. Kwa kweli hoja hii imeletwa muda mwafaka kwa sababu Wizara hii ni mpya na Waziri tuliyenaye ni Waziri mpya na tangu Wizara hii imeundwa ndio Waziri wa kwanza mwanamke, kwa hiyo, ni Wizara ya kipekee sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme tu kwamba mambo mengi sana ambayo yamewasilishwa na Waheshimiwa Wabunge ni ya msingi sana. Mchangiaji wa kwanza hadi wa mwisho, kama atakavyokuja kueleza mtoa hoja, wote ukiwasikiliza utaona mambo mengi wanayozungumza ni ushauri mzuri ambao unatuelekeza namna bora ya kutekeleza majukumu yetu ili sekta hii iweze kukua na iwe na mchango mkubwa kwa pato la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli champion wa kubadilisha sekta hii ya madini hapa Tanzania ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Yeye ndiyo ametoa uongozi na uelekeo wa namna gani tusimamie sekta hii ili madini ambayo Mungu ametupa yaweze kuwanufaisha Watanzania. Rais wetu ametamani kwa muda mrefu na hicho ndicho anachotaka sisi wasaidizi wake tufanye, kuwasaidia Watanzania waweze kunufaika na rasilimali hizi. Naomba niseme juhudi kubwa ambayo Mheshimiwa Rais ameifanya na sisi chini ya Waziri, Mheshimiwa Angellah Kairuki, tutaifanya kwa mioyo yetu na nguvu zetu zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba nijielekeze kwenye michango michache ambayo Waheshimiwa Wabunge wameeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ambalo limeelezwa hapa ni kuwasaidia wachimbaji wadogo. Nieleze kwamba, historia ya wachimbaji wadogo Tanzania na Afrika kwa ujumla, ni ndefu sana. Sisi Tanzania wachimbaji wadogo ni wengi sana lakini tunazo changamoto ambazo tumezikuta na hizo ndizo tutakazozishughulikia ili tuhakikishe kwamba wachimbaji wadogo hawa wanakua, wanatoka kwenye uchimbaji mdogo wanakwenda kwenye uchimbaji wa kati; wanatoka kwenye uchimbaji wa kati wanakwenda kwenye uchimbaji mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo mtoa hoja amesema kwenye hotuba yake, uchimbaji mdogo ni hadhi ya muda mfupi. Sisi kama Wizara tunatoa msukumo mkubwa kuwasaidia wachimbaji wadogo. Ndiyo maana utaona tunahama kwenye majina ambayo wachimbaji wadogo kwa miaka mingi wamekuwa wakiitwa; mara wanaitwa wavamizi, wasio halali, wachimbaji haramu na majina mengine mabaya. Tunatamani tuwaone wachimbaji wa Tanzania wale wadogo wanakuwa wachimbaji ambao wanarasimishwa, wanachimba kwa kufuata sheria, wanachimba katika mazingira ya kutunza mazingira ili madini wanayochimba yaweze kuwa na manufaa kwao wenyewe na watoto wao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mzuri tumeuona. Kuna watu wengine wanadhani wachimbaji wadogo ukiwasaidia hawana tija. Tulikwenda Mundarara, Jimbo la Longido kwa Mheshimiwa Dkt. Kiruswa, tumekuta Wamasai kule ni wachimbaji wadogo wa ruby na Mbunge wa Longido naye amesema hapa; wamefanya maendeleo makubwa, wamejenga nyumba za kisasa, wamehama kwenye matende, wanaishi maisha mazuri. Tulipofanya mkutano pale wote wanafurahia kuona kwamba Serikali ya Awamu ya Tano inawapa fursa ya kunufaika na rasilimali zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hii si nguvu ya soda, tutaifanya kwa nguvu zetu zote. Ndiyo maana kila mahali mnapotuona tunakutana na wachimbaji wadogo; kazi kubwa tunayoifanya ni kuwatia moyo na kuwapa miongozo ya Kiserikali namna gani watende kazi zao kwa uadilifu na walipe kodi za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja hii, sisi kama Wizara, sisi kama Serikali ya Awamu ya Tano kazi yetu itakuwa hiyo; kuwalea, kuwasaidia na kuwahamisha wachimbaji wadogo kwenye uchimbaji wa kubahatisha na kuwapeleka kwenye uchimbaji wa uhakika ili waweze kujikwamua kimaisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine iliyozungumzwa hapa ni habari ya STAMICO na kwa sababu tuko wengi wenzangu watakuja kuzungumza hapa lakini mimi nieleze eneo moja la madeni ya STAMIGOLD.

STAMIGOLD ni kampuni iliyoanzishwa na Shirika la Taifa la STAMICO na ikarithi mgodi mmoja wa Tulawaka. Shida tuliyoipata pale ni suala la management. Watu wamekwenda pale bahati mbaya sana baada ya kufika pale wametengeneza utaratibu kana kwamba tayari wamekwisha ku-break even. Wamejilipa mishahara mikubwa, wameweka gharama kubwa za uendeshaji, wazabuni wamefanya tendering kwa bei kubwa sana, imetokea sasa mgodi ule hauwezi kutengeneza faida.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yetu pamoja na mambo mengine tumechukua hatua tisa za kwanza za kufanya. Moja, kuhakikisha kwamba tunabadilisha management yote ya STAMIGOLD na kuweka management ya watu ambao ni waadilifu. Pili, tunatafuta wazabuni ambao bei zao ni bei shindani, bei nafuu, bei za soko. Tunataka tuhame kwenye exaggerated prices twende kwenye bei ambazo ni halisi za soko na hili jambo tunalifanya kwa nguvu zote. Kwa mfano, kwenye mzabuni anayetupatia mafuta tumempata Puma ambaye bei yake anayotuuzia ina upungufu wa Sh.159, lakini zamani ungeweza kuona kwamba bei ya mafuta tuliyokuwa tunanunua ilikuwa kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niwaombe Waheshimiwa Wabunge watuamini, Wizara hii ni mpya tunafanya kila tuwezalo kuhakikisha kwamba hatuliangushi Bunge hili na zaidi sana hatumuangushi Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Watanzania wote ambao wameiamini Serikali ya CCM iweze kuwaongoza. Naomba niwaombe mtupe muda, kuna kazi kubwa tunaifanya kwa STAMIGOLD, baada ya muda mtaona mabadiliko na matokeo makubwa kama ambavyo mmeshauri. Naomba niseme kwamba ushauri wa Waheshimiwa Wabunge juu ya STAMICO na STAMIGOLD tunauchukua na hatupuuzi ushauri wa aina hata mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine imezungumzwa juu ya kuwasaidia wachimbaji wadogo kwa kufanya utafiti. Hapa nataka nitoe mfano mmoja kwa hoja ya Mheshimiwa Kanyasu, Mbunge wa Geita ambaye alizungumzia habari ya utafiti wa GST kwenye Wilaya ya Bukombe ambako na yeye ana wananchi wake wanachimba kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba utafiti uliofanyika kule Bukombe ni wa awamu ya mwanzo, lakini kuna utafiti unaotakiwa kufuata ambao ni geochemistry, tulikuwa hatujawahi kuufanya; tumefanya geophysics, tukimaliza tunakwenda kwenye geochemistry ili tuweze kujua miamba iliyoko pale ina madini ya namna gani na yenye dhahabu kiasi gani. Namuomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira baada ya muda tukipata fedha tutapeleka GST waende wakakamilishe utaratibu ule walionao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Nachuma amezungumza mambo mengi juu ya Kamati, kwamba Kamati ya Tanzanite ya Mheshimiwa Spika iliyoundwa hapa ilikuwa na mapendekezo mengi haoni matokeo. Naomba nimhakikishie, kama ambavyo Mheshimiwa mtoa hoja alivyotoa kwenye hotuba yake, dira yetu pamoja na mambo mengine ni pamoja na hizo taarifa za Mheshimiwa Spika. Naomba nimhakikishie na kwa uhakika kabisa, mapendekezo yote ya Kamati zote zilizoundwa, kuanzia zile za Mheshimiwa Rais pamoja na za Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara tumezitengenezea matrix na time frame ya kuweza kuzitekeleza, hata hiyo One Stop Centre nayo tunaijenga ndani ya ukuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la tanzanite hatuna mzaha, tunatamani kuona madini haya yanawafurahisha Watanzania. Tutoke kwenye aibu ya kuona madini haya yanapatikana kwenye nchi nyingine na hapa Tanzania sisi tunakuwa wageni. Naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba kazi hii tunaifanya na tumeshaanza na tuko mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata haya mabadiliko, mimi nilidhani wakati huu Mheshimiwa Mbunge angetupongeza na angempongeza Mheshimiwa Rais kwa sababu moja ya mapendekezo yaliyokuwepo ni kujenga ule ukuta, ameona tumeujenga. Tunakwenda kwenye hatua nyingine ya udhibiti, tunakwenda kwenye kuhakikisha kwamba tunakuwa na eneo moja la kuuzia madini hayo ili kila mtu anayechimba madini yale aseme nina madini ya namna hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kudhibiti madini, moja ambayo ni ya msingi sana ni kuondoa urasimu, hutakimbiza mwekezaji lakini la pili ni kupigana na rushwa, uondoe rushwa kwenye mfumo. Ndiyo kazi ambayo Mheshimiwa Angellah Kairuki anahangaika nayo kwenye hii Wizara. Bahati nzuri wafanyakazi wetu tunakubaliana kwamba tuna wajibu wa kujenga image ya Wizara yetu kwa kufanya kazi kwa nguvu lakini kuwaondolea urasimu watu wanaohitaji huduma ofisini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama kuna jambo anahitaji mtu kulipata leo mpe leo kama amekidhi vigezo, hakuna sababu ya kumwambia njoo kesho wakati anastahili kupata ili utengeneze mazingira binafsi. Hili jambo tutapigana nalo kwa nguvu zote na kwa hili hatutaangalia mtu usoni. Tunataka Mtanzania yule mwenye haki apate haki yake, tunataka Mtanzania anayekuja Ofisi yetu ya Madini asiwe na mazingira ya aina yoyote ya kuomba rushwa au kiashiria, hata kukonyezwa tu kwamba mtu anataka rushwa, tunataka kuondoa hali hiyo. Tupeni muda, tumejipanga, Waziri wetu anatupa maelekezo kila siku. Sisi watendaji, Katibu Mkuu na Tume ya Madini tutafanya kazi hii kwa nguvu zetu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Alhaj Bulembo amezungumza habari ya wachimbaji wadogo kuwapatia leseni, hili ndilo jambo tunalolifanya. Kila mahali kunakotokea rush tukawakuta wachimbaji wadogo, tukiangalia tukakuta hakuna leseni ya mtu kazi ya kwanza tunayoifanya na tunawashirikisha Waheshimiwa Wabunge, tunawarasimisha wale wachimbaji wadogo waliogundua hayo madini ili wachimbe kihalali, watoke kwenye uchimbaji wa kubahatisha wawe na nyaraka ili mtu yeyote akija kuwaona akute ni watu halali. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, tumefanya hayo mambo maeneo mengi na Mheshimiwa Alhaj Bulembo angekuwepo ni shahidi, kule alikokuwa anazungumzia Geita tumerasimisha, ukienda Nyakavangala kule Iringa tumerasimisha, hata Mundarara, kule alikozungumza Mheshimiwa Kalanga na kwenyewe tunawarasimisha. Lengo ni kuhakikisha kwamba wanafanya kazi katika hali ambayo ni rasmi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Joel ameeleza habari ya CSR kwenye jimbo lake na kwenye ule Mgodi wetu wa Itiso ambako wanachimba dimension stones. Nimekwenda mwenyewe Itiso, kampuni ile inafanya kazi kubwa, ina deposit kubwa ya mawe, tena yenye gharama kubwa na wao tuliwaambia na wanafanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kule Itiso kampuni hii imewachimbia maji wananchi, wanapata maji ya kunywa, lakini imekuwa ikitoa michango mbalimbali kwenye jamii. Lengo ni kurudisha huduma kwa wananchi ili kupata kile kitu kinachoitwa license on operation, upate kukubalika kwa wanajamii ili wakati unafanya kazi yako iwe rahisi kwako.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo limezungumzwa hapa ni jambo ambalo Mheshimiwa Ndassa amelieleza. Naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Ndassa, yeye anawatetea wachimbaji wakubwa na wawekezaji. Mimi niseme, Serikali ya Awamu ya Tano nia yake ni kuhakikisha kwamba wawekezaji wote wenye nia njema ya kuja kuwekeza Tanzania kwa hali ya win-win situation wanakaribishwa milango iko wazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwatoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge, mimi toka nimeteuliwa ukikaa pale ofisini wawekezaji wanaokuja ofisini kuomba appointment waweze kuzungumza mambo ya uwekezaji ni wengi huwezi kuwamaliza. Ndiyo maana kuna Mbunge mmoja amesema tunakaa mpaka saa mbili usiku, si kwamba tunakaa tunaangaliana, hapana, tunakutana na wawekezaji wa kila namna. Tunachotamani kukiona kwenye Wizara yetu na wawekezaji wetu, wawe wawekezaji ambao ni genuine, si wawekezaji wajanja wajanja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwekezaji ambaye anakuja kwetu hana hata mtaji anataka kuja kutumia rasilimali za Tanzania kutafuta mtaji kisha awekeze hapa, hao hawana nafasi. Mwekezaji ambaye amejipanga kuja kufanya kazi Tanzania tunamkaribisha, tunatamani uwekezaji wa fedha za kigeni ndani ya nchi na hii ndiyo dira ya Mheshimiwa Rais wetu, tunataka tuwaone Watanzania wanafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwenye Mgodi wa Magambazi nini kilichotokea? Pale kulikuwa na wachimbaji wadogo zaidi ya 5,000, wale wachimbaji wadogo wamechimba wametengeneza marudio lakini ile leseni ilikuwa ya mtu mwingine, tukawaondoa wachimbaji wadogo wampishe mchimbaji mkubwa mwekezaji. Bahati mbaya kumbe yule mchimbaji mkubwa yeye hakuwa na huo mtaji wa kuwekeza pale, yeye akaja kuchukua yale marudio ya wananchi anachenjua hayo anapata pesa. Sasa hatuwezi kutumia nguvu ya Watanzania kwa ajili ya mwekezaji wa kigeni kwa kigezo kwamba eti ni mwekezaji. Hawa ni Watanzania wametumia nguvu yao, wamesaga mawe, wametengeneza marudio, kama ni mchimbaji kweli akachimbe naye kama wao walivyochimba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumetuma timu ya kwenda kukagua kule, wametuletea mapendekezo, zaidi ya sheria 19 zimevunjwa, sasa tunampa maelekezo namna gani afanye ili aweze kutekeleza sheria yetu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Ndassa Wizara yetu iko tayari kumsaidia mwekezaji yeyote ambaye yuko tayari kufuata sheria. Kama kuna mwekezaji mwingine yeyote, sio wa Magambazi tu, wa pande kuu nne zote za Tanzania ambaye anadhani anaweza kuja Tanzania na briefcase bila mtaji akaupata hapa akarudi kwao akiwa tajiri, zama hizo zimepitwana wakati. Tunataka mtu aje awekeze mtaji, tumsaidie sisi apate leseni na yeye apate kitu cha kuacha hapa kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba nirudie tena kukushukuru sana kwa kunipa nafasi, lakini nirudie kusema namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa imani kubwa aliyonipa, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa namna anavyoendelea kutufundisha kufanya kazi. Ni bahati mbaya tu Mheshimiwa Waziri amekaa nyuma, nilitamani niseme maneno haya ninamuona ilia one sura yangu inachokisema ninakusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja, nakushukuru sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kusimama, naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mungu kwa nafasi hii na nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa imani aliyonipatia na kuniteua kuwa Waziri wa Madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile namshukuru sana mtangulizi wangu, Mheshimiwa Angellah Kairuki ambaye amekuwa Mwalimu wangu mzuri sana kwenye nafasi hii. Wakati nikihudumu kama Naibu Waziri wa Madini, amekuwa Mwalimu mwema, aliyenifundisha, aliyeni-expose kwa kweli kwa kila namna ya kujifunza namna ya kusimamia Sekta ya Madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru vile vile Mheshimiwa Nyongo ambaye pia ni Naibu Waziri kwa ushirikiano mkubwa ambao walinipatia wakati nikiwa Naibu Waziri mwenzake na hata sasa ambapo tunaendelea kushirikiana pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo ya utangulizi, kama walivyoanza wengine, nami naomba nimpongeze sana Mwenyekiti wa Kamati yetu ya Nishati na Madini, Mheshimiwa Dunstan Luka Kitandula na Makamu wake, Mheshimiwa Mariam Ditopile pamoja na Wajumbe wote wa Kamati kwa kazi kubwa wanayoifanya na kwa maelekezo ambayo kwa kweli wanatupa kila wakati tunapokutana nao kwenye vikao vya Kamati na kwenye mashauriano mbalimbali wanapoona kuna mambo yanayohitaji kufanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba, binafsi naona fahari kubwa kufanya kazi pamoja na Kamati hii kwa sababu ya umakini wao na ubunifu wao, lakini vilevile kujali kwao na kufuatilia mambo mbalimbali ambayo yako kwenye Sekta ya Madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijasahau nami niseme naunga mkono hoja iliyoletwa hapa na Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini. Nami nitoe mchango mdogo tu kwenye mambo mbalimbali ambayo yamezungumzwa kwenye taarifa lakini vilevile na Waheshimiwa Wabunge mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, itashangaza sana kama nitasema hakuna changamoto kwenye Sekta ya Madini. Changamoto zipo na hazikuwepo leo, zimekuwepo kwa muda mrefu. Ninyi mnafahamu kwamba hapa Afrika Sekta ya Uvunaji wa Madini sisi tumeanza miaka ya 1990 kwa kuleta mitaji mikubwa kutoka nje. Huko nyuma waliokuwa wanachimba madini walikuwa wachimbaji wadogo. Ukianza mwaka 1987 mpaka mwaka 1997, miaka kumi ile wachimbaji wadogo peke yao ndio walikuwa wanachimba kwa asilimia 94, hapakuwa na mtaji wa mgeni hata mmoja, tulikuwa sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, walikuja wenye mitaji miaka hiyo ya 1990 na hapo sasa Sekta ya Madini ikawa ndilo jambo linalojadiliwa. Bunge hili linafahamu, kama kuna sekta ambayo imeundiwa Kamati nyingi mno ni Sekta ya Madini. Kamati za Ushauri za Bunge ziliundwa kwenye Sekta ya Madini, Kamati za uchunguzi ziliundwa kwenye Sekta ya Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, toka mwaka 2002 iliundwa Kamati ya Kipokola, mwaka 2004 ikaundwa Kamati ya Masha; mwaka 2006 ikaundwa; zimeundwa Kamati nyingi na hata Bunge hili na lenyewe limeunda Kamati mbalimbali. Nia ilikuwa moja tu, kuondoa changamoto zilizomo kwenye Sekta ya Madini; na Serikali imekuwa ikifanya hivyo hatua kwa hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunavyoendelea kufanya kazi ya kusimamia Sekta ya Madini, tunagundua changamoto zilizomo, tunatafuta mbinu za kuziondoa. Namna mojawapo ya kuondoa changamoto hizo, ipo kwenye sheria. Ndiyo maana mnaona Sheria ya Madini imekuwa ikibadilika miaka hadi miaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 1998 ilibadilika, mwaka 2010 ilibadilika na baadaye 2017 tukafanya marekebisho makubwa sana ya mwelekeo wa Sheria yetu ya Madini. Nia ni kuleta tija kwa nchi kwenye Sekta hii ya Madini. Bado tunaendelea kukabiliana na hizo changamoto pamoja na kwamba tumeshapiga hatua kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesikiliza michango ya Waheshimiwa Wabunge hapa na nianze kueleza mchango mdogo tu ambao umeelezwa na ndugu yangu, Mheshimiwa Frank Mwakajoka, sijui ni kwa nia njema au ni kwa sababu ya kunogesha, anasema Sekta ya Madini mchango wake umeshuka. Naomba niweke taarifa sahihi kwenye Bunge hili; mchango wa Sekta ya Madini kwenye nchi ya Tanzania toka tumeanza kuchimba haujawahi kushuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitampa rekodi kidogo hapa; mwaka 2013, Sekta ya Madini ilikuwa inachangia asilimia 3.3; mwaka 2014, Sekta ya Madini ilikuwa inachangia asilimia 3.7; mwaka 2015, ilichangia kwa asilimia 4.0; mwaka 2016, imechangia constantly na mwaka uliofuata 2017, kwa asilimia 4.8. Haijawahi kuchangia kwa asilimia tano na ikashuka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukuaji wa Sekta yenyewe ya Madini ni ule ambao ni very promising. Mwaka 2013, ukuaji wa Sekta ya Madini ulikuwa asilimia 6.9; mwaka 2014, ukuaji wake ulikuwa asilimia 9.4; mwaka 2015, ulikuwa asilimia 9.1. Mwaka juzi, mwaka 2017, sekta iliyoongoza kwa ukuaji katika sekta zote sio mchango wa sekta, ni Sekta ya Madini, ilichangia kwa asilimia 17.5. Nadhani tusivunjane moyo, tutiane moyo, tuna safari kubwa ya kufanya. Kazi ya kudhibiti madini kutoroshwa sio kazi ya mtu mmoja, Wizara ya Madini, ni kazi ya Watanzania wote. Leo nataka niwaambie tunapokamata wanaotorosha madini hatukuti wageni peke yao, tunawakuta na Watanzania wenzetu wamo wakisaidia utoroshaji wa madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haiwezekani Serikali iwe yenyewe peke yake bila Watanzania wenyewe kutengeneza mindset ya kuwa na wivu na rasilimali zao. Naomba nipaze sauti kwenye Bunge hili kuwaomba Watanzania; madini tuliyonayo kuna siku yataisha, lazima tuone wivu, tuyalinde kwa nguvu zote. Wanaokamatwa wote wawe wenyeji, wawe wageni, ukienda utakuta aliyetengeneza huo mchongo ni Mtanzania mwenzetu aliyekuwa anachimba nao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda naomba nieleze vilevile, wameeleza hapa Waheshimiwa Wabunge kwamba sasa wachimbaji wadogo waanze kurasimishwa na wameeleza maoni waliyoyatoa kwenye mkutano tulioufanya, tukamwalika Mheshimiwa Rais, kwamba tuyasikilize. Naomba niwaondoe wasiwasi; mapendekezo yao yote yako 22, yote tunayafanyia kazi kama Serikali, yote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mapendekezo waliyoyatoa yanayohusiana na sharia, Serikali inayafanyia kazi lakini yapo mengine ya kiutendaji kwa mfano kuwapatia maeneo ya kuchimba; baada ya wiki inayokuja nitatoa taarifa ya leseni ngapi tunazifuta kwa sababu tunazo leseni nyingi kwa kweli, zaidi ya 2,038, zimeshikiliwa na watu ambao hata humu nchini hawamo. Zinadaiwa fedha zaidi ya dola milioni 42, zimekalia maeneo wachimbaji wadogo wakienda kule wanafukuzwa, tunakwenda kuzifuta zote hizo tuwapatie wachimbaji wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo limeelezwa hapa juu ya TEITI, kwamba TEITI haijafanya kazi yake; naomba niweke rekodi sawasawa, ni kweli kwamba TEITI kazi inayofanya ni reconciliation kati ya kile kilichotolewa kwenye mgodi na kile kilichoingia Serikalini, hakuna fedha yoyote


iliyopotea. Kinachofanyika makampuni yanayoshughulika na Sekta ya Madini na Gesi, mafuta, ni makampuni 2,087. Wao wakatengeneza utaratibu wa kuyachambua baadhi kama sampuli, wakachukua yale yenye threshold ya mtaji wa milioni 300 ndiyo yakafika hayo 50. Sio kweli kwamba tulipaswa kukagua 2,000 sasa tumekomea 50, hapana, ni wale MCG waliamua wenyewe kuchambua kwamba tukague wale ambao wana mtaji mkubwa kuanzia dola milioni 300, ndiyo tukapata kiasi hicho.

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo fedha anayozungumza imepotea sio fedha iliyopotea, ni reconciliation, kwamba ukienda kwenye mgodi unakuta anakwambia nimelipa shilingi 10, ukija huku Serikalini unakuta pengine hiyo hela haijawa recorded au unakuja huku Serikali unakuta kuna fedha fulani haijawa recorded, ukienda kwenye mgodi unakuta hiyo fedha. Kwa hiyo, hiyo kazi unachukua hizo anomalies zote, unampelekea CAG ili aweze kuhakiki kujua kama kweli kuna fedha zimepotea, kwa hiyo hakuna pesa iliyoibiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati njema Mheshimiwa Mwakajoka ni Mjumbe kwenye Kamati, majibu haya tulimpatia kwenye Kamati, lakini kwa sababu ni lazima tunogeshe, ruhusa tunaendelea, lakini nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mwakajoka; hakuna mtu ataiba fedha kwenye Sekta ya Madini akabaki salama, hakuna mtu atatorosha madini kwenye Sekta ya Madini atabaki salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, wachimbaji wamelalamikia kodi, wamelalamikia masoko. Nilikuwa na mkutano hapa juzi wa Wakuu wa Mikoa yote Tanzania, tumeshaanzisha maeneo na kuyatenga kwa ajili ya masoko ya madini. Hata ule utaratibu wa kusema mtu anayetaka kuleta madini hapa nje awe na mlolongo mrefu, mlolongo huo tumeuondoa, sasa watu wanaotoka Congo, Msumbiji, wale wanaotaka ku-trade madini yao ndani ya nchi, ruhusa, ilimradi waseme kwamba tunataka kuja kufanya biashara. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Doto Biteko, muda wako umekwisha.

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Madini
WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, kabla ya kuanza kujibu hoja mbalimbali zilizowasilishwa na Waheshimiwa Wabunge napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa tumefarijika sana kama Wizara kutokana na michango mbalimbali ambayo Waheshimiwa Wabunge wameitoa kwa kusema na kwa kuandika. Tumepata ushauri na maoni ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, ushauri na maoni hayo yalikuwa ya msingi na sisi tunaamini ushauri huu ni muhimu sana kwetu katika kutekeleza majukumu yetu.

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile tumesikia hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ambao nao wametoa ushauri mbalimbali ambao kwa kiasi kikubwa Serikali kwa hatua mbalimbali imekuwa ikiufanyia kazi. Pia Waheshimiwa Wabunge wapatao 10 wametoa michango yao kwa kusema; michango yao hiyo yenye maoni na ushauri tunayachukua kwa uzito wake na itatusaidia sana katika kuboresha utendaji wa kazi Wizarani. Aidha, Waheshimiwa Wabunge 18 wamechangia kwa maandishi ambao pia michango yao hiyo tumeichukua kwa umuhimu wa kipekee na itatusaidia sana katika kuboresha utendaji wetu.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kulifahamisha Bunge lako Tukufu kwamba hoja zote zilizowasilishwa na Waheshimiwa Wabunge sisi kama Wizara tunazichukulia kwa uzito wa kipekee na mimi nimesimama hapa kutolea ufafanuzi baadhi ya hoja zilizotolewa. Hata hivyo kutokana na ufinyu wa muda tulionao yawezekana hoja zote hizi nisipate nafasi ya kuzieleza moja baada ya nyingine. Itoshe tu kusema kwamba tutaziwasilisha kwa maandishi kwa Waheshimiwa Wabunge ili pamoja na mambo mengine majibu yetu yawe rejea kwa siku za usoni.

Mheshimiwa Spika, Kabla sijaanza kujibu naomba na mimi nirudie tena kumshukuru tena na tena Mheshimiwa Rais kwa imani kubwa aliyotupa kwa kuanzisha Wizara hii ya Madini, na kwa kweli Wizara hii pamoja na kwamba inaweza ikaonekana inazo Taasisi chache ina mambo mengi ya kufanya kwa sababu shughuli zake zinasaidia sana ukuaji wa uchumi. Mheshimiwa Rais msukumo alioutoa ni wa kusababisha Wizara hii mchango wake utoke kwenye asilimia 4.8 ya kuchangia Pato la Taifa sasa uwe mchango wa walau asilimia 10 ifikapo 2020. Lakini namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa yeye mwenyewe amekuwa kinara mkubwa sana wa kutusimamia na kutupa maelekezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utakumbuka wakati tunaanzisha utaratibu wa kuanzisha masoko hapa nchini Mheshimiwa Waziri Mkuu yeye mwenyewe ndiye aliitisha kikao cha Wakuu wa Mikoa wote nchini lakini soko la kwanza la masoko tuliyolianzisha yeye mwenyewe wala hakutuma mtu wa kufanya kazi hiyo kwa niaba yake alifanya mwenyewe. Kwa kweli tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa msukumo wake huo na sisi Wizara ya Madini tunapata imani kubwa na nguvu kutoka kwake.

Mheshimiwa Spika, naomba nimshukuru pia Naibu Waziri wa Madini Mheshimiwa Nyongo kwa ushirikiano mkubwa anaonipa, yeye pamoja na wenzangu Wizarani, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wengine.

Mheshimiwa Spika, lakini nitakuwa mchoyo wa fadhila kabisa kama sitakushukuru wewe mwenyewe binafsi. Tulifanya semina moja hapa Bungeni kwa ajili ya kuangalia masuala la madini na wewe ulikuwa mgeni rasmi nakumbuka kwenye hotuba yako maneno uliyoyazungumza, ni kwamba Wizara ya Madini lazima mtuondolee aibu ambayo imezunguka sekta ya madini. Maneno haya ni nyongeza tu ya msukumo mkubwa ambao wewe mwenyewe umekuwa ukiutoa kwenye kusimamia sekta hii. Uliunda Kamati mbili kama Waheshimiwa Wabunge watakavyokumbuka na zote hizi zilikuwa na nia ya kuhakikisha kwamba tunasimamia vizuri sekta ya madini.

Mheshimiwa Spika, ninaweza kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote, Kamati yetu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa michango yao, ushauri wao lakini sana kwa kufuatilia kwa karibu mambo mbalimbali yaliyoko. Mwisho lakini si kwa muhimu niwashukuru Wakuu wa Mikoa wote, vyombo vya habari na wadu wa madini; na wengine umewaona wako hapo wamekuja kutuunga mkono. Baada ya kusema shukurani hizo naomba sasa nijielekeze kwenye hoja chache ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezieleza.

Mheshimiwa Spika, kuna hoja hapa imezungumzwa juu ya wananchi wa Tarime; na hoja hii imezungumzwa na Msemaji wa Kambi ya Upinzani kwenye eneo la madini na ambaye pia ndiye Mbunge wa Tarime. Lakini mimi nilikuwa najaribu kutafakari, jambo hili tumelifanyia kazi kwa karibu sana. Mheshimiwa mtoa hoja atakumbuka jambo hili mgogoro wake haujaanza leo umeanza mwaka 2009, 2012. Mimi nimekwenda na Mheshimiwa Heche Jimbo kwa kwake tumekwenda kushughulikia jambo hili la fidia ambalo limekuwa la muda mrefu. Mheshimiwa Heche nilitamani sana leo asimame hapa asema kwa kweli Serikali mnajitahidi kwa kuchukua hatua kwa sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumekuta wananchi waliofanyiwa uthamini kwenye awamu ya 47 walio kwenye hati ya kulipwa na mgodi wako 66. Tumekwenda na Chief valuer kuangalia nyaraka mbalimbali tumekuta wananchi ambao walikuwa wamefanyiwa uthamini ni zaidi ya 117 wengine wamekatwa kwa hila; na fedha walizokuwa wametengewa kulipwa zilikuwa ni shilingi milioni 224 peke yake; tukakataa tukiwa na Mheshimiwa Heche tukasema hapana Watanzania hawa walichagua Serikali ya Chama Cha Mapinduzi ili iwasemee, haiwezekani atokee mtu tena kwenye ardhi yao wakatiwe maeneo na wengine wapunguzwe na fedha waliupwe kidogo. Tumeamuru uthamini urudiwe upya. Hili jambo Mheshimiwa Heche nilidhani leo kwa niaba ya watu wa Nyamongo angeweza kufika hapa akapongeza Serikali kwa kufanya jambo hili kwa faida ya watu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa mbunge anafaamu, jambo la utiririshaji wa maji kwenye mgodi wa North Mara limeanza kwa muda wa miaka 10 iliyopita. Tumeanza kwa awamu ya kwanza, huu ni mgodi mkubwa, ni kweli tunahitaji fedha kutoka nje, ni kweli tunahitaji ajira kutoka kwa watu wetu kwa ajili ya watu wetu lakini afya za watu ni muhimu kuliko jambo lolote. Nimekwenda mwenyewe na Mheshimiwa Mbunge pamoja na Mheshimiwa Mbunge mwingine aliyenialika Mheshimiwa Agness Marwa, tukafanya mkutano na wananchi wa Nyamongo tukawaambia warekebishe kasoro ifikapo tarehe 30 Machi hawakurekebisha kasoro; hatua ya kwanza kwa mujibu wa sheria tunapiga faini; na tumewapa wiki tatu baada ya wiki tatu kama kasoro hizo hazijarekebishwa tutachukua hatua inayofuata ambayo imetajwa kwenye sharia. Nilitarajia Mheshimiwa Heche angefika akapongeza walau kwa faida hiyo, kwa sababu sisi wenyewe ndio tumeamua sasa kuwasimamia wananchi wa Nyamongo bila kupepesa macho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, limezunguzwa jambo lingine hapa kwenye eneo hili, kwamba je, haya mambo fedha mlizotoza faini warudishiwe wananchi? AG amelieleza vizuri sana na nilitamani sana Mheshimiwa Heche pamoja na sisi Waheshimiwa Wabunge ambao ni wawakilishi wa wananchi tuchukue nafasi hii ya kuwaelimisha wananchi utaratibu ulivyo. Inawezekana kabisa tunatamani walipwe fidia ya fedha walizotoza faini, lakini unalipa against kitu gani kwa sababu tathimini ya madhara hayo haijawahi kufanyika? Lazima ikishafanyika tukajua ndio tunaweza kwenda kwenye hatua nyingina kama AG alivyozunguzma.

Mheshimiwa Spika, ninaomba nikuhakikishie wewe pamoja Bunge lako, Serikali inayoongozwa na Chama cha Mapinduzi chini ya Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kipaumbele chake cha kwanza ni watu wake na maisha bora ya watu wake waweze kunufaika na rasilimali hizi, tutasimama kidete kulinda uhai wa watu wetu kwa gharma yoyote ile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ameelze hapa Mheshimiwa Neema Mgaya juu ya taarifa ya GST na kuwafanyia utafiti wachimbaji wadogo. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu, Wizara ya Madini baada ya marekebisho makubwa ya sheria na kuifanya GST sasa kuwa taasisi inayojitegemea na si wakalaa, tunaenda kufanya utafiti kwa ajili ya maeneo ya wachimbaji wadogo. Na hatua ya kwanza ili uweze kufanya utafiti ni lazima ununue hivyo vifaa vya kufanyia utafiti; tumenunua mtambo maalum kwa ajili ya kuwafanyia utafiti wachimbaji wetu. Niwaombe wachimbaji wa Tanzania wawe na subira tunapoendelea kufanyia kazi mambo haya.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Magige ameeleza vizuri sana na ameeleza kwa uchungu tabia ya baadhi ya watu kuendelea kutoza tozo ambazo Bunge hili limezifuta. Nilieleza hapo wakati najibu swali na naomba nirudie tena. Bunge hili halifanyi maigizo hapa, linatunga sheria na sheria hizo lazima zifuatwe, mtu yoyote anayetoza tozo ambazo Bunge hili limezifuta kwa mujibu wa sheria anatenda kosa. Ninaomba Mheshimiwa Magige atuletee mfano wa watu waliotozwa sisi tutachukua hatua. Nimewasiliana na Wizara ya Fedha wamesema hakuna maelekezo hayo.

Mheshimiwa Spika, wakati mwingine ni tabia ya mtu mmoja tu, huyo mtu mmoja kwa vitendo vyake anavyofanya inaonekana Serikali nzima inanyanyasa watu. Nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Catherine Magige hakuna mtu atatozwa tozo hizo ambazo Serikali imeshaziondoa, na mimi nikuhakikishie kwamba tutaendelea kulifanya kazi kwa nguvu zetu zote.

Mheshimiwa Spika, limeelezwa jambo la urasimu kwenye baadhi ya ofisi zetu na ikatajwa specific ofisi ya Geita, na Mheshimiwa Mbunge Ammar. Inawezekana ukaonekana urasimu, lakini tukubali kazi ya kusimamia Sekta ya Madini ndugu zangu imejaa mambo mengine, usipokuwa makini kosa moja la dakika moja unaweza ukaisababishia Serikali hasara ya mabilioni ya shilingi. Hawa vijana tulionao ni wachache lakini jambo la msingi sana; tumefanya kazi Wizara nzima ya kupruni watu wengine ambao tulikuwa tunaona sio waaminifu tumebakiza watu ambao wanafanya kazi . (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninawaomba waheshimiwa Wabunge hawa ni vijana wenu, hawa ni watoto wenu, hawa ni wanadamu pia wanahitaji kutiwa moyo; wamefanya kazi kubwa sana. Tunaangalia trend ya mapato inavyokwenda kwa sasa ni tofauti sana na miezi mitatu iliyopita, kazi hii wanafanya vijana hawa. Nikuombe sana Mheshimiwa Ammar, kama kuna specific case, ya mtu mmoja anayesababisa urasimu kwenye ofisi zetu sisi tutachukua hatua. Hata hivyo ombi lako la kuomba ofisi pale Nyang’wale naomba nikuhakikishie kwamba tunaendelea kufanya tathimini kwenye maeneo mbalimbali. Si tu Nyang’wale yako na maeneo ya Mbogwe kuna shughuli nyingi zinafanyika, tunaangalia kama tutapata uwezekano wa kupata human resource ya kutosha tutafungua ofisi ili watu wetu waweze kuhudumiwa kwa urahisi kuondoa mizunguko isiyokuwa na maana.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, Mheshimiwa Amar anafahamu, maeneo mengi ambayo yalikuwa yameshikiliwa na makampuni makubwa yote tumeyapelekea default note na tuko kwenye utaratibu wa mwisho wa kuyafuta ili tuwapatie wachimbaji wadogo. Niwaombe wachimbaji wa Nyangh’wale na wachimbaji wa maeneo mengine Tanzania, wajiunge kwenye vikundi, lakini niwaombe pia wachimbaji wa Tanzania mfumo wa kuanza kuchimba wakianza kupata wanagombana hizo zilipendwa. Mheshimiwa Amar ni shahidi, wachimbaji hawatunawa-mobilise tunawaweka kwenye vikundi, wakianza tu kupata pesa migogoro inaanza. Niwaombe tushikamane tunapokuwa tunapata fedha kama ambavyo tunashikamana wakati tunatafuta leseni.

Mheshimiwa Spika, limeongelewa pia eneo hapa na Mheshimiwa Kapufi, juu ya makinikia na usafirishaji wake. Mheshimiwa Kapufi tumeshawahi kulizungumza hili jambo sio mara moja, sio mara mbili, tunayo changamoto ya kisheria, tunaiangalia changamoto hiyo; tunakisikia kilio chake na sisi tunatamani tumuondolee kero hiyo. Tunahitaji mapato kwenye mgodi wake, lakini tunahitaji pia na yeye fedha aliyowekeza iweze kurudi. Hii ni Serikali inayotaka kuona Mtanzania kwenye nchi yake anawekeza na anapata pesa anawekeza kwenye mambo mengine zaidi. Nimwombe Mheshimiwa Kapufi awe na subira tumalize hili jambo, ni jambo la kisheria, lakini kama nilivyomwambia mimi na yeye hapa ninavyozungumza moyo wangu na moyo wake inawasiliana kwa sababu tulizungumza, anajua ni wapi tumekwama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa hata nikisimama nikasema kesho aanze kusafirisha atakutana na kikwazo ambacho kitampa hasara kubwa zaidi. Naomba awe na subira Mheshimiwa Kapufi, mimi naumia, nimekwenda mwenyewe kwenye mgodi wake na wenzangu Wizarani tunalifanyia kazi, likikamilika tutampa utaratibu utakaofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Maftaha ameeleza hapa juu ya One Stop Centre, hii inafanyikaje. Naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge; One Stop Centre ni mfumo tuliouanzisha wa kufanya biashara ya madini kwenye dari moja. Tunataka kuwaondolea urasimu wachimbaji wetu wa kutoka point moja kwenda point nyingine kwa ajili ya kutafuta huduma. Kwenye One Stop Centre ni jengo kubwa ambalo ndani ya jengo hilo ofisi zote zinazohusika kwa ajili ya utoaji huduma kwenye madini zitakuwepo kwenye ukuta huo. Jengo hilo ni kubwa, Uhamiaji watakuwa hapo, Valuers watakuwa hapo, watu wa kupima ubora wa madini watakuwa hapo, benki zitakuwa hapo, ukienda na madini yako vitu vyote unafanya kwenye eneo moja na kutoka na utaratibu wako unavyojua kwa ajili ya matumizi yako. Kwa hiyo, One Stop Centre sio refinery wala sio smelter wala sio kitu kinachofanya kazi ya kuchenjua, ni jengo kwa ajili ya kutolea huduma. Tutakapokwenda kulizindua nitamwomba Mheshimiwa Maftah tuandamane naye akaone One Stop Centre ilivyo ili aweze kujua tunafanya vitu vya namna gani.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Musukuma amezungumzia habari ya watu wanaofanya kazi kwenye Ofisi ya Madini, uaminifu wao. Hilo tunalichukua, ni jambo ambalo tutaendelea kulifanyia kazi kila siku, lakini jambo la maana sana.

Mheshimiwa Spika, Mgodi wa GGM, toka mwaka 2017 tumekuwa na mgogoro na mipasuko kwenye maeneo ya Nyamalembo, nyumba 80 zilifanyiwa tathmini, lakini na sisi tukapeleka timu nyingine kwenda kuangalia. Tumetoka kwenye nyumba 800 tumekuta nyumba zilizoathirika ni zaidi ya nyumba 3,000 na mgodi umekubali baada ya timu ambayo tumeipeleka kule inayohusisha ofisi zote, mgodi walikuwemo, Halmashauri walikuwemo, Ofisi ya Ardhi walikuwemo, watu wa Madini walikuwemo, watu wa RS walikuwemo, ilikuwa timu kubwa imefanya kazi kwa muda ambao kwa kweli, ulizidi hata kiwango cha muda waliokuwa wamepewa.

Mheshimiwa Spika, wamekuja na ripoti nzuri sana juu ya fidia ya maeneo hayo. Nimwombe Mheshimiwa Musukuma, GGM wameanza kulipa fidia, inawezekana hizo fidia mtu mwingine anaweza kusema ndogo, lakini ndogo ukilinganisha na nini na ukilinganisha na tathmini gani? Sisi tunasema fidia hizi zimeanza kulipwa. Kama kuna mwananchi anadhani hajalipwa inavyostahili tuwasiliane na sisi tutampa vigezo.

Mheshimiwa Spika, wametokea watu wengine hapohapo Geita ambao walilipwa kipindi cha nyuma, wako wananchi kama watatu mmoja amelipwa milioni 74. Pamoja na kulipwa milioni 74 kwenye orodha hii tena ya kulipwa upya jina lake limo. Pamoja na kwamba huu mgodi ni wa mwekezaji lakini lazima na sisi tumwonee huruma. Watu ambao wanafikiri wanaweza kupata fedha kwa ujanja ujanja, nashauri tu watafute shughuli nyingine ya kufanya.

Mheshimiwa Spika, tumewaambia hata watu wa Nyamongo wale walotegesha hawawezi kulipwa hata iweje kwa sababu, wametegesha. Hata wale ambao Mheshimiwa Heche anawajua wa awamu ya 21 na wenzao waliokuwa wanadai fedha, watu 1,934 1,800 walichukua cheki, watu 134 wakaacha cheki, tuliwaambia na wao wakachukue cheki. Tunapokuwa tunawatetea Watanzania ni lazima pia tuwalinde wawekezaji na baadhi ya watu wachache ambao sio waaminifu kwa sababu, pia ni wajibu wa Serikali kuwalinda wawekezaji.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Millya ameeleza hapa juu ya foleni kubwa kwenye ukaguzi wakati watu wanaingia mgodini. Ushauri wake tunaupokea na tunaupokea kwa heshima kubwa na tunauzingatia. Namwomba awe na subira, tunatafuta kibali cha kuajiri watumishi wengine. Mara baada ya kukamilika, tukipata watu tutaongeza workforce pale kwa ajili ya kuangalia watu wanavyoingia pale mgodini.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Maige ameeleza maeneo mbalimbali ambayo wachimbaji wake wana mgogoro. Ameeleza eneo la Bushimangira. Ni kweli mimi na yeye tulikwenda. Eneo la Mwazimba ni kweli mimi na yeye tulikwenda na kuna changamoto zilizokuwepo hapo za utoaji wa leseni. Wale waliohusika kwenye utoaji wa leseni hizo kwa kukiuka utaratibu walichukuliwa hatua na Wizara. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Maige wananchi wa Mwazimba na wananchi wa Bushimangila kwa Serikali hii wawe na amani, hawatapoteza leseni yao, watapewa leseni yao. Kwa sababu leseni ile ilitolewa katika mazingira ambayo ni tata, sisi Wizara tumechukua hatua moja kubwa zaidi kwa kufuata utaratibu tumeiandikia default notice ili tuweze kuzifuta tuwapatie wachimbaji wadogo.

Mheshimiwa Spika, nimwombe Mheshimiwa Maige kama ambavyo yeye anasema ni mtetezi wa wanyonge, aendelee kuwatetea wananchi wa Mwazimba na wa Bishimangila. Nataka nimhakikishie Wizara ya Madini tutam- support kwa mambo yote hayo. Ameeleza habari ya fidia, jambo hili tunalifanyia kazi tupewe muda, lakini baada ya muda tutalimaliza na watu wanaohusika.

Mheshimiwa Spika, yako maeneo mengine ambayo nataka nimalizie. Jambo lililozungumzwa hapa ni habari ya Mgodi wa TANCOL, ameelieleza vizuri sana Mheshimiwa Naibu Waziri wa Viwanda. Tumeshapeleka barua kutoka NDC, Wizara ya Madini; NDC na yeye analalamika kwenye ubia ule anapunjwa. Tarehe 11 Mei, ametuletea barua na sisi baada ya bajeti hii tunapeleka timu ya wakaguzi maalum kutoka Tume ya Madini kwa ajili ya kwenda kujiridhisha na mambo yote yaliyomo kwenye barua iliyoletwa na NDC.

Mheshimiwa Spika, naomba nikuhakikishie hili jambo tumeanza kulifanyia kazi mapema. Hapa ninapozungumza TANCOL alikuwa analipa kodi kwa kutumia Sheria ya Madini ya mwaka 1998. Analipa kwa kutumia Net Back Value, kwa maana gani? Kwamba, yeye akishachimba makaa ya mawe, kodi anayotoza anatoza pale site kwa hiyo, wakati sisi tunachukua kodi kwa tani moja dola 53 yeye anasafirisha hayo makaa ya mawe anapeleka kwenye destination yake anauza tani moja dola 220. Sasa kodi tunachukua kwenye dola 53 badala ya dola 200 na kitu. Tumekuwa na ubishani mwingi wa kisheria, lakini hatimaye AG ametupa mwelekeo. Naomba niwahakikishie kwamba, jambo hili tunalifanyia kazi kabisa na Waheshimiwa Wabunge watapata matokeo baada ya taarifa yetu hii kwenda kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa niendelee tena kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge. Waheshimiwa Wabunge niwaombe kazi ya ulinzi wa rasilimali madini sio kazi ya Wizara ya Madini peke yake, ni kazi yetu wote. Niwaombe tuungane wote na kwa kweli, wachimbaji wadogo wa Tanzania kama hatuwezi kuwapongeza kwa kipindi hiki hatutawapongeza tena, wamekuwa watu wema mno, ndio wanaotupa taarifa. Nimeeleza hapa watu ambao tumewakamata wakitorosha madini wanaotupa taarifa ni wachimbaji wenyewe.

Mheshimiwa Spika, naomba kwa heshima na taadhima na kwa niaba ya Wizara ya Madini niwashukuru sana wachimbaji wa madini Tanzania kwa kuitikia wito, kwa kuona wivu na rasilimali zao. Nataka niwahakikishie Wizara ya Madini itawapa kila aina ya support watakayoihitaji.

Mheshimiwa Spika, pia niwashukuru sana vyombo vya habari nchini. Uelewa wa sekta ya madini hapa nchini unasaidiwa sana na vyombo vya habari, wamekuwa mstari wa mbele kueleza udhaifu uko wapi, wengine wameandika makala za kiuchunguzi ambazo zimetusaidia kujua ukweli. Kwa mfano kule Mahenge, ilianza makala ya gazeti moja, tulivyokwenda tukakuta mambo mengi yaliyokuwa yameelezwa kwenye makala ile yalikuwa ya kweli. Naomba nirudie tena kuwashukuru sana waandishi wa habari kwa uzalendo wao, kwa kuipenda nchi yao na kwa kweli kwa kuona sekta yetu hii ya madini inakua.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa, nikushukuru tena kwa kunipa nafasi hii na naomba nitoe hoja. (Makofi)

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kukushukuru tena kwa kunipa nafasi ya kuhitimisha hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Madini kwa mwaka wa fedha 2021/2022. Wizara imepokea michango mbalimbali ambayo Waheshimiwa Wabunge wameitoa kwa matamshi na Wabunge wengine kwa kuandika. Pia tumepata ushauri na maoni na mapendekezo ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini ambayo ni muhimu kwetu katika kutekeleza majukumu yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla ushauri na maoni pamoja na mapendekezo ya Waheshimiwa Wabunge kwetu sisi ni muhimu kwa ajili ya kuendeleza Sekta ya Madini.

Napenda kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliopata nafasi ya kuchangia hotuba yetu. Jumla ya Waheshimiwa Wabunge 22 wamechangia hotuba hii kwa kuzungumza na wajumbe wawili wamechangia kwa kuandika. Nichukue fursa hii kulifahamisha Bunge lako Tukufu kwamba, hoja zote zilizowasilishwa hapa na Waheshimiwa Wabunge, sisi kama Wizara tunazichukua kwa uzito wa aina yake na kwamba itakuwa ni tool nyingine ya kufanyia kazi katika kipindi hiki cha mwaka wa fedha.

Mheshimiwa Spika, naomba niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliosema, hata waliotuandikia na hata wale tuliokutana nao tukazungumza nje ya Bunge. Tunaheshimu michango yao, na tutaifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, baada ya utangulizi huo sasa naomba nijielekeze kutoa ufafanuzi kwa hoja kidogo tu zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge kutokana na muda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kueleza kwamba usimamizi wa Sekta ya Madini hautegemei mtu mmoja kwa maana ya Wizara ya Madini, unawategemea sana Waheshimiwa Wabunge ambao wao ndio wawakilishi wa watu mahali huko tunapofanya shughuli za uchimbaji madini. Tumefanya ziara maeneo mbalimbali, tumeona kiu ya Watanzania walio wengi ya kutaka kuwekeza kwenye Sekta ya Madini na tumewaona Waheshimiwa Wabunge wengi walivyo na kiu ya kuona madini yanawanufaisha Watanzania.

Mheshimiwa Spika, hiyo spirit peke yake kwangu mimi ni kiashiria tosha kwamba usimamizi wa Sekta ya Madini ni wetu sote. Kwa kweli naomba niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge, hakuna hoja hata moja ambayo sisi tutaichukulia kama hoja substandard. Hoja zote zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge ni tool yetu ya kufanyia kazi na kuanzia leo nataka niwahakikishieni kwamba hoja zote walizozitoa tutaziandikia majibu na tutaziwasilisha kwako ili Waheshimiwa Wabunge waweze kuzipata.

Mheshimiwa Spika, suala la kwanza nieleze kwa kifupi ni suala la local content. Suala hili limeongelewa kwa hisia kubwa sana na Waheshimiwa Wabunge, local content huko ndiko uliko mzunguko wa fedha kwenye Sekta ya Madini. Ukiruhusu mzunguko ulioko kwenye local content uende kwa watu wa nje ukawaacha watu wa ndani, manufaa hayo hayaweza kupatikana.

Mheshimiwa Spika, tulipotoka mbali, tumetoka kwenye mazingira ambayo mchele wa kulisha migodi ulikuwa unatoka nje ya nchi, nyanya zilikuwa zinatoka nje ya nchi, vitunguu vilikuwa vinatoka nje ya nchi, walinzi wanatoka nje ya nchi, Wahasibu wanatoka nje ya nchi, watu wa manunuzi wanatoka nje ya nchi, watu wa Human Resource wanatoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia biashara zilizokuwa zinafanywa na migodi, volume kubwa ya fedha zile ilikuwa bado inarudi nje ya nchi na kwa gharama kubwa sana. Tumefanya mabadiliko hapa tukatoa mamlaka kwa Tume ya Madini ku-approve kila aina ya manunuzi, mgodi sasa hivi hata ukitaka kununua kikombe cha chai, ni lazima upate kibali cha Tume ya Madini. Kwa sababu hiyo nataka nitoe taarifa kwa Bunge lako Tukufu, tulipofika tumepiga hatua kubwa. Leo wakati manunuzi ya Mgodi wa GGM yaliyofanyika kwa mwaka huu tulionao jumla ya Shilingi bilioni 849.9 ni fedha zilizofanyiwa biashara kwa local content kwa wazabuni wa ndani na Shilingi bilioni 182 peke yake ndizo zilizofanyiwa na watu kutoka nje.

Mheshimiwa Spika, Mgodi wa Buzwagi bilioni 105.8 ni zabuni zilizofanyiwa biashara na Watanzania wa hapa ndani na wakati huo huo bilioni 95 ni watu wa nje. Mgodi wa Shanta bilioni 106.5 ni bidhaa za ndani na huduma zimetolewa ndani, bilioni 30 peke yake ndizo bidhaa kutoka nje au huduma kutoka nje. Mgodi wa WDL bilioni 53.6 ni biashara iliyofanyika ndani na bilioni 5.4 peke yake ni biashara iliyotoka nje. Hatua hii ni kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, hata bidhaa kubwa ambazo walikuwa wanazungumza Waheshimiwa Wabunge mfano mafuta, vipuri, consumables na vitu vingine vyote kwa kiwango kikubwa ni biashara zinazofanyika hapa ndani. Biashara ya mafuta kwa mfano, kwa Geita, mtu anayefanya biashara ya kupeleka mafuta kwenye mgodi wa GGM ni Mtanzania yupo Geita kwa asilimia 30. Ukiangalia biashara ya kupeleka nguo, kupeleka vitu vyote unavyoviona zaidi ya asilimia 70 biashara hii inafanyika hapa ndani.

Mheshimiwa Spika, CSR inayozungumziwa, tulipotoka tukiangalia Mheshimiwa Musukuma na Mheshimiwa Kanyasu watakuwa mashahidi; kabla hatujarekebisha sheria hapa CSR fedha zilizokuwa zinatumika zilikuwa nyingi na tena hazina uhalisia na wala ile miradi iliyokuwa inatumika hayakuwa mahitaji ya watu wanaozunguka migodi, matokeo yake yakawa ni nini? Matokeo yake ni kwamba fedha nyingi zinaonekana zipo traded kwenye migodi, lakini watu wanaozunguka ile migodi bado ni maskini wa kutupwa, bado watoto wao wanakaa chini hawana madarasa, bado watu wale hawana maji.

Mheshimiwa Spika, tukafanya mabadiliko kwenye sheria hiyo Mheshimiwa Musukuma atakumbuka shule moja pale Geita ilijengwa kwa bilioni tisa wakati shule ile haina ghorofa tulivyokwenda kufanya valuation tukakuta fedha hizo hata nusu yake isingeweza kutosha tumefanya marekebisho. Leo mpango wowote wa CSR unaotaka kufanywa na mgodi mtu aliye na wajibu wa kuusimamia mpango huo ni halmashauri husika na halmashauri yenyewe ina kazi mbili, baada ya kuwa imejiridhisha na mpango huo unaendana na mahitaji ya halmashauri kazi ya pili ni kuangalia value for money.

Mheshimiwa Spika, kuna wakati fulani kuna miradi ilikuwa inatengenezwa, wanakwambia mfuko mmoja wa simenti unauzwa Sh.30,000 wakati ukienda kwenye soko unakuta mfuko mmoja unauzwa Sh.15,000. Mambo hayo yote tumeyabadilisha sasa hivi value for money inaangaliwa na manufaa haya yanaonekana. Mheshimiwa Kanyasu hapa atakuwa shahidi Geita ilivyokuwa kabla ya kusimamia sheria hii na sasa hivi ni tofauti sana, imebadilika kwa sababu miradi mingi halmashauri wanasimamia.

Mheshimiwa Spika, yako matatizo tunayapokea ya usimamizi na nidhamu ya matumizi ya fedha; sisi kama Wizara Madini ambao tuna wajibu wa kusimamia local content pamoja na TAMISEMI, tutaendelea kusimamia matumizi ya fedha hizi ili yaweze kuwa na tija.

Mheshimiwa Spika, limezungumzwa jambo moja la Mradi wa Niobium. Naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Njeza, hili jambo linaweza likaonekana Wizara tunachelewesha, nimwombe Mheshimiwa Oran Njeza awaambie wale wawekezaji tuliokuwa tunaendelea nao waje tupo tayari.

Mheshimiwa Spika, bado tumemaliza mambo mengi tunabishana mambo mawili tu; madini ya niobium, wao wanataka tuya-treat kama madini ya viwandani ambayo yanatozwa mrabaha wa asilimia tatu, sisi tuna ya-group yale madini kama madini ya metal na yenyewe yanatozwa asilimia sita. Sasa ubishani huo hatuwezi kuu-resolve kwa kuzungumza tu, ni lazima waje tuzungumze.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine tunalozungumza nao ni kwamba wanataka wachimbe kwenye Kilima cha Pandahill wakishachimba processing ya madini hayo wayaondoe kwenye Kilima waende wakafanye kwenye process ya EPZA. Sheria ya Madini inaeleza uchimbaji wa madini ni chain nzima, kuanzia uchimbaji na process. Sasa tunawaambia tukifanya tendo la kutenganisha huu mradi, uchimbaji ukafanyika kwenye mgodi na process ikafanyika mahali pengine, kwanza tutakuwa tumevunja Sheria ya Madini, lakini pili kwenye EPZA kuna misamaha mingi sana ya kodi.

Mheshimiwa Spika, kodi ya mapato ya asilimia 30 itakuwa na msamaha kwa muda wa miaka 10; kodi ya zuio na kodi nyingine pamoja na kodi ya pango, bado tunaendelea kujadiliana nao. Bahati mbaya baada ya kuwa tumewaambia hoja hizi hawakurudi tena. Kwakuwa Mheshimiwa Mbunge anaweza kuwa sasa...

SPIKA: Waheshimiwa wote mnaokuja kukaa na kuongea Mheshimiwa Waziri Mkuu nilishatoa maelekezo, lakini basi nawaagizeni mtakaa kiti kile kama AG hayupo, mumlinde angalau afya yake na yeye. Haiwezekani watu 50 au 60 kila siku wanakutana naye hapa kwa hapa, hebu jaribuni sana kupunguza, hata kama ni Mawaziri kama hauna shida ya maana usiende pale, kwa sababu ana wajibu wa kuwasikiliza Wabunge na wale mnaokwenda basi kaeni kiti cha mbali pale kidogo ili kuweka ile distance ambayo ni salama. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri, endelea.

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo milango yetu ipo wazi Kampuni ya Panda Hill wakaribie wakati wowote tuzungumze, lakini watusaidie na wao ni lazima tulinde manufaa ya nchi yetu kwenye rasilimali madini, kwa sababu hizi rasilimali kuna siku zitakwisha.

Mheshimiwa Spika, kuja jambo lingine hapa limeelezewa la TEIT, kwamba TEIT hajapata fedha. Naomba kutoa taarifa hapa mbele ya Bunge lako Tukufu kwamba TEIT walishapata fedha za maendeleo Sh.850,000,000 ambazo wamekwishapata kwenye bajeti yao. Hata hivyo, kuna mzozo mmoja unaozungumzwa hapa wa reconciliation ya bilioni 30 ambao Mheshimiwa Jesca alikuwa akiueleza sana. Ni bahati njema kwamba Mheshimiwa Jesca amekuwa consistent na jambo hili Bunge lililopita kwenye bajeti alieleza tulitoa majibu, lakini sijachoka tutatoa ufafanuzi.

Mheshimiwa Spika, kilichotokea, hakuna hata shilingi moja iliyoibiwa wala kupotea, kilichotokea TEIT wanachofanya wanakwenda kwenye mgodi X wanaomba malipo waliyolipa Serikalini, wanapewa iwe orodha ya malipo. Wanakwenda Serikalini wanaomba kile walichopokea, wanafanya reconciliation. Kilichotokea ni kwamba reporting ya Serikali na reporting ya migodi miaka yao ya fedha inatofautiana, ndio maana tulivyomtuma CAG Novemba, 2019 alituletea taarifa ya hoja hiyo, hizo fedha zote zilionekana hata kwenye bank statement zipo.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa kuwa bado linaendelea kuzungumzwa, nataka nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Jesca na Watanzania hakuna shilingi hata moja itakayoliwa kwenye migodi, inasimamiwa kwa uwazi na kwa ukweli na hata kwenye Semina tuliyoifanya uliyotupa kibali, Mheshimiwa Jesca nilimwambia, nadhani hapa leo aliamua kutuchangamsha kidogo kulirudia jambo hili, lakini majibu anayo.

Mheshimiwa Spika, limeongelewa jambo lingine la blacklisting ya wafanyakazi, ni kweli wapo wafanyakazi kwenye migodi wanakuwa blacklisted na nilishatoa maelekezo pamoja na wenzangu Wizarani kwamba, watu wanaoweza kuwa blacklisted ni wale waliotenda makosa makubwa sana. Mtu amechelewa kazini siku mbili unamfukuza kazi, halafu una m-blacklisting asiajiriwe kwenye migodi mingine, tulishatoa maelekezo ni marufuku na kuna Watanzania wawili waliokuja kwangu waliokuwa na kesi za namna hiyo niliwaambia wawaondoe kwenye orodha yao ya blacklisting.

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii niwaombe Watanzania wale wote walioajiwa kwenye migodi, wajenge image ya nchi yetu, tunapambana kuhakikisha kwamba Watanzania wanachukua ajira zote kwenye migodi, hivyo ni lazima wawe waaminifu. Leo ninavyozungumza migodi mikubwa ya GGM asilimia 97 ya wafanyakazi wote ni Watanzania. Migodi ya North Mara asilimia 98 ni Watanzania hata Country Manager wa Mgodi wa North Mara kwa maana ya group nzima ya BARICK hapa Tanzania ni Mtanzania anaitwa Georgia na ni mwanamama yupo, amekuja hapa. Yule mgeni aliyekuwepo hapa tumemaliza mkataba wake ameondoka Georgia sasa…

SPIKA: Meneja wa mgodi huo unaohusika hebu asimame. Makofi kwake waheshimiwa. Hongera sana dada yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri, unaweza ukaendelea.

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo…

SPIKA: Mheshimiwa Meneja hawajakuona kamera hizi hazijakuonesha. Hata Mheshimiwa Waziri wa Fedha anaona, hata mavazi yake enhe! (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Waziri wa Madini, endelea.

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Labda wengine, lakini mimi niliwahi kwenda kwenye mgodi mmoja nitatoa mfano, nikazungumza maneno mengi na wenye mgodi. Baadaye wakaniomba side meeting, wakaniambia tunaomba na wasaidizi wako tukae kule chumbani, jambo walilokuwa wanalalamika ni uaminifu wa baadhi ya watu wetu, kwa kweli wanatuchafua wote, wanatuondolea heshima wote. Wale wanaopata nafasi ya kusimamia migodi hii wasimamie kwa haki na weweze…

SPIKA: Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa vile anaongelea neno la uaminifu. Nilizungumza hapa siku moja nimepigwa na mitandao yote, kwamba ninaongea kitu cha kufikirika. Leo Waziri anasisitiza. Endelea Mheshimiwa Waziri jambo hili, uaminifu unalipa. (Makofi)

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, lingine wale Watanzania kama kina Georgia wanaopata nafasi za kuendesha migodi hii, wawasaidie Watanzania wengine. Wanaowa-blacklist Watanzania hawa ambao wapo kwa kuwaonea wala sio Wazungu tusiwasingizie, ni sisi wenyewe. Nataka niwahakikishie jambo hili haliwezi kufanyika tena tumeshatoa maelekezo kwa watu wote wahakikishe wale waliofanya makosa makubwa ndio wanakuwa blacklisted, lakini makosa madogo madogo ya kawaida mtu amechelewa kazini, hayo haya-qualify mtu kuwa blacklisted. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii vile vile tumekuwa na changamoto ya utoaji wa fedha kutoka kwenye benki zetu. Huko tulipotoka makampuni makubwa yalikuwa yanasema benki za ndani ya Tanzania haziwezi ku-finace miradi ya uchimbaji madini. Nataka nitoe taarifa kwako na ndio maana tuliwaalika watu wa CRDB na NMB, hivi leo mradi uliokuwa umekwama kwa miaka mingi kotokana na corona, wawekezaji wamekwenda ku-list huko nje kutatufa finance wamekosa, wameamua kurudi kwenye benki za ndani na sisi tukawaita ili tuweze kuzungumza nao na Mheshimiwa Waziri Mkuu akaweka mkono wake wa kutusaidia kuzungumza na benki hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nafurahi kusema kwamba mradi mmoja wapo mkubwa wa uchimbaji wa graphite hapa nchini wa Ruangwa huko Lindi Jumbo tayari CRDB wametoa fedha zote za kuendesha huo mradi. GGM wana mkopo wanapewa na Benki ya NMB zaidi ya bilioni 250, uwezo huo uko ndani. Sisi tunachowaambia mabenki inawezekana huna fedha zote za ku-finance hii miradi, tufanye synergy ya benki mbili au tatu. Mbona kwenye miradi mingine wanatuletea, unakuta Exim ya China imeungana na Barclays ya London wamefanya synergy wana-finance mradi uko Tanzania na mabenki yetu yanaweza kufanya hivyo na hilo wametuelewa, sasa miradi mingi inatolewa fedha hapa ndani.

Mheshimiwa Spika, hata wachimbaji wadogo wengi ningekuwa na muda ningekuletea orodha ya wachimbaji wadogo waliokopeshwa na mabenki ya ndani. Jambo hili mabenki wametupa heshima kubwa kwasababu wameona trust iko kwenye madini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho najua kwasababu ya muda yako mambo mengine ni ya kiusimamizi mdogo wangu Mheshimiwa Maganga la Nyakafuru Pamoja na loyalty kwamba ukiweka tu milioni 100 tunakata hapana sheria haiku hivyo. Loyalty utalipa baada ya kuwa umevuna lakini hatuwezi kukata kodi kwenye mtaji tukifanya hivyo tutakuwa tunamuibia Mtanzania.

Mheshimiwa Spika, na hilo la Nyakafuru tutakwenda lina hadithi zake ndefu Mheshimwa Mkuu wa Mkoa aliunda kamati, kamati imeshatoa majibu alilieleza wakati tuko kwenye ziara na nimemhakikishia kwamba hakuna mtanzania hata mmoja atadhulumiwa wala hakuna mtanzania hata mmoja ataonewa.

Mheshimiwa Spika, lakini la kweli tuchukue muda mwingi kuwaeleza watanzania ukweli kuna drama nyingine watu wanafanya ambazo ukweli ukienda kwenye detail unakuwa wao wanatudanganya viongozi na tunachukua maamuzi ya kuumiza wawekezaji bila sababu ya msingi. Wawekezaji wakubwa tunawahitaji jamani kwenye uchimbaji madini tunahitajiana wote wachimbaji wadogo tunawahitaji, wachimbaji wa kati tunawahitaji na wachimbaji wakubwa tunawahitaji akitokea mmoja katika group hizi akapata matatizo basi tunakuwa na fallback position tukiwaondoa wachimbaji wakubwa kwa kisingizio cha wachimbaji wadogo, mwisho wa siku hatuwezi kukuza hii sekta.

Mheshimiwa Spika, leo tunafurahi tunasema kwamba uchimbaji mdogo na wachimbaji wadogo wamechangia kwenye pato la Taifa kwenye ile gross asilimia 30. Tulikotoka wachimbaji wadogo hawakuwa na maana walikuwa wanachangia chini ya asilimia tano hatua hiyo tumeifikia kwasababu tumewapa heshima lakini heshima hiyo tunayowapa wachimbaji wadogo isigeuke kuwa fimbo ya kuwaumiza wachimbaji wakubwa na wa kati ambao nao wanaweka fedha zao tuheshimiane hatuwezi kutumia kigezo cha uchimbaji mdogo na uchimbaji mdogo

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Waziri malizia.

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie uchimbaji mdogo ni hadhi ya muda mfupi haiwezekani mchimbaji mdogo yeye ha-graduate mtoto anasoma darasa la kwanza yeye ni mdogo mdogo lakini ukienda kuangalia finance zake na vitabu vyake ana mtaji mkubwa lazima tuwafundishe Watoto kuona Fahari kuitwa wachimbaji wakubwa ili uchimbaji wa ndani uwe wa kwetu naomba nikushukuru sana. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa tafadhali nisaidie suala la Nyanzaga likoje.

SPIKA: Ameshamaliza hapana hapana hamna taarifa vurugu hiyo hapana Mheshimiwa. Mheshimiwa Waziri huja toa hoja

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, kwa kuhitimisha naomba sasa Bunge lako likubali kujadili na kupitisha makadirio ya matumizi ya Wizara ya Madini kwa mwaka wa fedha 2021 naomba kutoa hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi nichangie Wizara hii. Kabla sijafanya hivyo nimshukuru sana Mungu kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kusimama tena hapa na kuchangia Wizara hii muhimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama walivyoanza walionitangulia naomba nianze kwa kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na timu yake ya Maliasili na Utalii kwanza kwa kutuletea hotuba hii nzuri, detailed na imegusa kila sekta kwenye Wizara yake. Naomba vilevile niwapongeze sana Wajumbe wa Kamati inayosimamia Wizara hii nao kwa hotuba yao nzuri ambayo imetoa maoni na ushauri ambayo kwa kweli yanatusaidia sisi tunaochangia kuweza kujua maeneo gani yatafanyiwa kazi na Kamati iliona. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda mrefu tumemwona Mheshimiwa Waziri anavyohangaika na kupambana na ujangili nchini. Waziri na Wizara imeonyesha nguvu yake yote kwenye jambo hili. Nataka niwatie moyo kupitia mchango wangu huu kwamba kazi wanayoifanya ni kwa faida ya nchi, waendelee mbele na wasivunjike moyo. Tumeona wale majangili wote waliotungua ndege wamekwishakamatwa. Juzi niliona video moja kwenye mitandao ya kijamii maaskari wetu wamekamata majangili haya yaliyokuwa yanafanya kazi ya kuua wanyama wetu. Naomba niwatie moyo na kuwaombea kwa Mungu waendelee bila shaka wanyama hawa ni kwa faida ya nchi yetu na vizazi vyetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Bukombe asilimia 40 ya ardhi ya Bukombe ambayo ni kilometa za mraba 8,055.59 ni hifadhi. Wananchi wanaoishi Bukombe wana maingiliano ya karibu na hifadhi ya Kigosi Moyowosi lakini mahusiano ya Kigosi Moyowosi hayajawahi kuwapatia faida na hapa nataka niseme kwa uchungu kidogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi walio wengi wa Wilaya ya Bukombe wana majonzi makubwa na hifadhi hii. Nimesimama hapa kumwomba Mheshimiwa Waziri atakaposimama na kuhitimisha aje na majibu ambayo yatawapa tumaini watu wa Bukombe juu ya mahusiano mabaya ya Wahifadhi na wananchi wa Wilaya ya Bukombe. Nenda Ngara, nenda Biharamulo, njoo Bukombe, pita Mbogwe, nenda Kahama, nenda Ushetu kwa jirani yangu Kwandikwa kila Mbunge aliyemo humu ambaye anawakilisha maeneo haya hana habari njema ya kuelezea juu ya mahusiano ya Maliasili pamoja na wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, yako manyanyaso makubwa ambayo yamefanyika ukiambiwa hapa unaweza ukatokwa na machozi. Leo nataka niyazungumze haya na niseme hadharani ikiwa sitapata majibu, watu wa Bukombe watanishangaa kuunga mkono bajeti hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, Kitongoji cha Idoselo kilichoko kwenye Kijiji cha Nampalahala, watu wa Maliasili wameingia hapo, wamechoma moto nyumba za wananchi 40, kijiji ambacho kina GN ya Serikali kwa maana hiyo kimetambuliwa na Serikali! Katika kijiji hicho tumefanya uandikishaji wa BVR, kampeni tumepiga kule, walishachagua Mwenyekiti wa Kijiji, kilishasajiliwa, kina GN ya Serikali, watu wametoka nyumbani wamekula chai wameshiba vizuri, wana magari na mafuta ya Serikali, wana kiberiti na bunduki, wanaenda kuchoma nyumba za wanachi ambao hawana uwezo wa kujitetea, wamepiga na wameharibu mazao ya watu, watu hao wapo wanaendelea kutamba na kusema kwamba mtatufanya nini. Jambo hili lisipopata majibu leo namwambia Mheshimiwa Waziri hapa hapa nakufa na yeye. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, haiwezekani wananchi wale ambao wamelima mashamba yao, mazao yao yamekua yamefikia mahali fulani wanatumaini kwamba baada ya miezi fulani tunakwenda kuvuna tulishe familia zetu, tusomeshe watoto wetu, ananyanyuka mtu mmoja tu au wawili kwa sababu wana nembo ya Serikali kwa maana ya Maliasili wanakwenda kuchoma nyumba zao na baadaye wanatamba kwenye vyombo vya habari tumechoma vibanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikuhakikishie ikiwa wao wana maghorofa, hivyo vibanda vya wananchi wao ni maghorofa yao. Ikiwa wao wanakula vizuri hayo waliyosema ni vi-plot wao ndiyo mashamba yao ambayo yanalisha familia zao. Lazima nipate majibu kwenye Bunge hili, lazima wananchi wa Bukombe wafutwe machozi kwa jambo la ukaidi, kwa jambo hili kubwa lililofanyika Wilaya ya Bukombe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Bukombe pamoja na mambo haya, kuna manyanyaso makubwa yamefanyika. Wako wananchi wamevunjwa miguu, wako wananchi wamevunjwa mikono, wako wananchi wamefanywa kuwa walemavu wa kudumu, walikuwa wanalima kwa ajili ya familia zao, leo watu hawa hawawezi kufanya hivyo kwa sababu wamekuwa walemavu, aliyefanya ni nani? Baadhi ya Askari wasio waaminifu wa Maliasili wamewaumiza watu hawa. Nataka majibu wananchi hawa mnawafanyia nini?
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara hii imepiga risasi ng‟ombe za wananchi, nataka majibu ni kwa nini. Ng‟ombe waliopigwa risasi ni wa Ndugu Masanja Njalikila, ng‟ombe sitini (60); Ndugu Hamisi Ngimbagu, ng‟ombe wanane (8); Ndugu Manzagata Mang‟omb,e ng‟ombe mmoja (1); Ndugu Fikiri Masesa, ng‟ombe wawili (2); Ndugu Sikujua Majaliwa, ng‟ombe kumi na nane (18); Ndugu Blashi Ng‟wanadotto, ng‟ombe arobaini na tatu (43); Ndugu Juma Masong‟we, ng‟ombe kumi na mbili (12); Ndugu Mussa Seni, ng‟ombe wawili (2); Ndugu Serikali Andrea, ng‟ombe wawili (2); Ndugu Juma Langa, ng‟ombe kumi na nane (18) na Ndugu John Mashamba, ng‟ombe wawili (2); jumla ng‟ombe 215. Ndugu Jofrey Omboko punda wake wane (4) wamepigwa risasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa leo nataka majibu hatma ya watu hawa inapatikanaje. Kama inabidi nisimame kwenye Bunge hili nilie machozi kwa ajili ya wana Bukombe nitafanya hivyo, lakini watu wangu wapate majibu. Haiwezekani niwepo Mbunge hapa nimekaa kwenye kiti hiki cha kuzunguka, wananchi wangu wana mateso na nijione Mbunge mwenye furaha, hilo sitafanya. Naomba nipatiwe majibu, vinginevyo sitaunga mkono hoja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo lingine limetokea na hili ni la kisheria na naunga mkono usimamiaji na utii wa sheria. Iko tabia ya watu kupewa adhabu ya kutaifishwa mifugo yao. Leo ninavyosimama hapa jumla ya ng‟ombe 603 za wananchi wa Bukombe wametaifishwa, wamechukuliwa kuanzia siku ile ni mali ya Serikali. Nataka niseme kwenye kundi la wale waliopelekwa Mahakamani wenye ng‟ombe walikuwa watano (5), watatu (3) walikubali kutoa fedha, wakapelekwa Mahakamani wakadanganywa kwamba wakiwa huko wataachiwa Mahakamani.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme fedha zao wamekula na ng‟ombe zao zimetaifishwa lakini wako wawili (2) waliokataa kutoa fedha kujumuishwa tu kwenye mashtaka yale wakati wanadai ng‟ombe wao Maliasili wamekataa kuwaweka. Wamekwenda kuhukumiwa wale ng‟ombe kama ng‟ombe wasiokuwa na mwenyewe. Watu hawa wamekwenda Polisi, wameripoti Maliasili wakawaambia tunaomba mtufanyie jambo moja mtuingize kwenye mashtaka na sisi tushtakiwe wamekataa kuwapeleka wanasema hawa ng‟ombe hawana mwenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, unyanyasaji huu una-turnish image ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Unyanyasaji huu hauwezi kumfanya Mbunge wa Bukombe afurahie Wizara ya Maliasili na utalii. By the way kwenye Sheria zao za Maliasili na Utalii sisi tunaopakana na hifadhi tunapaswa kupata asilimia 25% ya mapato yale. Toka nimekuwa Bukombe pale sijawahi kuona hata shilingi moja inapelekwa Bukombe. Naomba na hiyo hela Mheshimiwa Waziri na yenyewe aniambie naipataje kwenye Halmashauri yetu?
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii na naomba niseme ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nami nichukue nafasi hii nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kusimama hapa, nichukue nafasi hii kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Bukombe kwa kunichagua na kunituma niwe mwakilishi wao katika nyumba hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza sana aliyewasilisha Mapendekezo ya Mpango ambao tunaujadili hivi sasa. Mapendekezo ya Mpango huu tumeletewa ili tuweze kuyaboresha, nami naomba niboreshe katika maeneo kadhaa kwa sababu ya muda, ili tuweze kuboresha zaidi Mpango huu kwa masilahi ya watu wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, naomba sana, tunapokuwa tunaangalia namna ya kukuza uchumi wa nchi, ni lazima tuangalie zaidi upatikanaji wa ajira kwa vijana. Nchi hii ina vijana wengi sana, asilimia zaidi ya 40 ni vijana ambao wanaweza kuajiriwa au ni nguvu kazi ya nchi hii. Hawa wasipowekwa maalum kwenye Mpango, namna gani watapatiwa ajira na tukafanya projection ni wangapi watapata ajira kwa Mpango huu, tutakuwa tunachelewesha kukua kwa uchumi wa nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namna pekee ya kuweza kuwapatia vijana hawa, mathalan wa Bukombe ili uweze kuwapatia ajira, ni lazima uwatengee maeneo ya kuchimba dhahabu. Bukombe ndilo eneo pekee katika Mkoa wa Geita ambapo maeneo mengi yana dhahabu nyingi, lakini vijana wa Bukombe hawajapatiwa maeneo ya kuchimba dhahabu. Vijana hawa hawawezi kuielewa Serikali kama hawajapatiwa maeneo ya kuweza kufaidi rasilimali za nchi ambazo Mungu amewapatia na wamezaliwa wamezikuta hapo. Wakati umefika Mheshimiwa Waziri tuje na Mpango wa kuangalia namna gani vijana wanapatiwa maeneo ya kuchimba dhahabu katika Mpango wetu huu tulionao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la umeme. Watu wengi hapa wamezungumza, wamepongeza uwepo wa umeme wa REA. Sisi tuna REA I na REA II, mpaka sasa, lakini Wilaya ya Bukombe haijawahi kupata hata awamu moja ya umeme wa REA.
Nakuomba sana Mheshimiwa Profesa Muhongo na Naibu Waziri wako, nafahamu ninyi ni watu wasikivu, mtusaidie Bukombe na sisi tupate umeme wa REA. Haina maana nimesimama hapa kama Mbunge, wenzangu wanashangilia umeme na wewe Mheshimiwa Profesa Muhongo ulisema, sitaenda REA III mpaka viporo vya REA I na REA II viishe, wakati mimi hata REA I na REA II sijawahi kuiona! Mheshimiwa Profesa Muhongo nakusihi sana, Bukombe uitazame kwa jicho la huruma. Tunahitaji umeme kwa ajili ya maendeleo ya watu wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Uyovu kuna Kituo cha Afya, kinafanya huduma kubwa ya kuhudumia watu, kinahudumia Wilaya ya Bukombe, kinahudumia Wilaya ya Chato, kinahudumia Wilaya ya Biharamulo, lakini hakuna umeme pale. Madaktari wangu pale wanafanya operation kwa tochi. Jana nimepigiwa simu, wanazalisha mama mmoja wanatumia tochi. Mheshimiwa Waziri, nakuomba sana utusaidie umeme kwa ajili ya watu wa Bukombe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, naomba niipongeze sana Serikali kwa kuja na Mpango wa elimu bure kwa Watanzania. Mpango huu kwa maoni yangu naona kama ukichelewa. Kuanzia sasa watoto kuanzia darasa la kwanza mpaka la kumi na mbili watapata elimu bure. Ninafahamu wako watu wengine ambao wanaweza wakapuuza Mpango huu kwa kuona kwamba ni siasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikisheni, tulipoanza na Mpango wa kujenga Shule za Kata, watu walitokea hapa wakapuuza namna ile ile, lakini leo ninavyosimama hapa na kuongea mbele yako, Shule za Kata ndiyo zimetusaidia kupata Wataamu wengi wa nchi hii. Nitakupa mfano kwenye Wilaya yetu ya Bukombe, Shule ya pili kwa kufanya vizuri Kidato cha Sita ni Shule ya Kata ya Lunzewe Sekondari, ambayo watu wakati tunaanza walianza kupuuza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali, tusukume na namwomba sana Mheshimiwa Simbachawene, endelea kutuelimisha Watanzania. Tunavyoanza siyo rahisi! Siyo rahisi tunavyoanza tukaenda na mafanikio ya moja kwa moja. Tutapata setbacks hapa na hapa, lakini kadri tunavyoendelea ndivyo tutakavyokuwa tuna-improve ili twende mbele zaidi kwa maslahi ya Watanzania.
Mheshimwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Mawaziri, naomba sana, sasa tumeshafanya vya kutosha; tumejenga madarasa, sijawahi kuona Mpango wa kuwasaidia Walimu, kuwa-motivate Walimu kufanya kazi vizuri. Walimu wa Tanzania wanafanya kazi katika mazingira magumu. Walimu wa Tanzania bado wanalipwa kwa viwango ambavyo havikidhi maisha yao kwa siku 30. Walimu wa Tanzania bado wana waajiri wengi na wanawajibika kwa watu wengi wakati wao ni watu wale wale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeomba na tumelia kwa muda mrefu Walimu wapatiwe Tume ya Utumishi wa Walimu. Wamepatiwa, sasa ninaomba Serikali iharakishe mfumo wa kurekebisha Kanuni hizo zinazotengenezwa ili Tume ya Utumishi wa Walimu ianze kufanya kazi tuwahudumie Walimu wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Mfumo wa Elimu ndugu zangu umegawanyika katika sehemu tatu, sehemu ya kwanza ni Mtaala, sehemu ya pili ni udhibiti wa ubora na sehemu ya tatu ni Examiner au Mtahini yule anayeangalia matokeo ya kile walichojifunza Wanafunzi. Upande wa mtaala ambako Mwalimu ndiko yupo, hakuna nguvu kubwa iliyowekwa kwa muda mrefu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaangalia madarasa, ndiyo! Tunaangalia madawati, amina! Tunaangalia chaki, sawa! Lakini lazima tumwangalie Mwalimu ambaye ndiye mhusika Mkuu na msimamizi mkuu wa Mtaala wa Elimu katika nchi hii. Walimu hawa wanapokuwa wanalalamika na kulia, msitarajie tutapata matokeo ya uhakika. Tunaweza tukawalazimisha wakae darasani, watafanya kazi lakini nataka niwaambieni, motivation ya Walimu wa nchi hii bado iko chini. Iko kazi tunapaswa kufanya, tuje na Mpango Waziri wa Fedha, mpango maalum wa kutengeneza frame work ya motivation ya Walimu. Nchi nyingine zimeshafanya jambo hilo na zimefanikiwa sana. Naomba sana Mheshimiwa Waziri, jambo hili tuliangalie kwa jicho la pili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi pale Bukombe kuna zao maarufu sana. Asali bora nchi hii inatoka Bukombe. Asali inayovunwa Bukombe na watu wamejiunga kwenye vikundi, wanafanya kazi kama yatima. Wako kwenye Vikundi watu 6,000, wanavuna asali zaidi ya lita milioni moja kwa mwaka, lakini hakuna hata Kiwanda kimoja cha kusindika asali. Nakuomba Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara na tulishazungumza, tuangalie namna ya kupata Kiwanda cha Kusindika Asali ya watu wa Bukombe ili asali yao ipate bei kubwa, ipate soko la uhakika, tubadilishe maisha yao kwa kuwapatia fursa ya kuendeleza maisha yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba, vile vile Wilaya ya Bukombe tuna mifugo mingi, lakini mifugo hiyo haichangii kwenye pato la Taifa. Nchi hii ina mifugo milioni 25, lakini ukiangalia takwimu kwa hali ya uchumi, kwa taarifa ya hali ya uchumi ya Juni, 2015, utaona nchi hii pamoja na kuwa na mifugo milioni 25, tumeuza nje ya nchi mifugo 2,139 na tumepata Shilingi bilioni 34 peke yake. Tuna mbuzi milioni 15, lakini tumeuza mbuzi 264; tumepata Shilingi bilioni 1.7.
Nakuomba Mheshimiwa Waziri wa Mifugo, utakapokuja kujumuisha, uje na Mpango wa kutusaidia wafugaji hasa wa Kanda ya Ziwa, wafugaji wa Tanzania, tupate malisho, tumechoka kukimbizana na Wahifadhi wa Wanyamapori, ma-game kupigana kila siku na kuanza kuhangaishana kutozana vifedha vidogo vidogo hivi, wakati tuna uwezo wa kuchangia kwenye Pato la Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, nimekuwa na Naibu Waziri, Mheshimiwa Engineer Ramo, mtu msikivu sana. Alikuja Jimboni kwangu, akazungumza na wafugaji pamoja na Waziri wa Mifugo, walituambia mambo mengi ya kufanya, lakini cha ajabu, baada ya kauli zao kutoka, siku mbili, tatu, kauli ile ikabadilika kabisa. Wale wafugaji sasa hivi huko ninavyoongea wanatimuliwa kama wakimbizi kwenye nchi yao. Naomba Serikali tuangalie namna ya kuwasaidia watu hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba tatizo la maji, Wilaya ya Bukombe bado tuko nyuma sana. Watu wanaweza kusema kwenye makaratasi asilimia 30 ya watu wanapata maji, hapana. Wanaopata maji Bukombe ni chini ya asilimia 30 na actually ni chini ya asilimia kumi. Miradi iliyopo mingi imeshasimama. Mradi wa Msasa haufanyi kazi, Mradi wa Kilimahewa haufanyi kazi ipasavyo, pale Ruhuyobu tuna miradi miwili; mradi mmoja peke yake ndiyo unaofanya kazi, mradi mwingine umesimama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi hii ni kazi ambayo tunahitaji tuione. Nami namwomba Mheshimiwa Waziri wa Maji, unapokuwa na kale kampango ka kupeleka maji Tabora, Nzega, Bukombe pale ni karibu, ukipitia Mbogwe, tunapata maji ya Ziwa Victoria, biashara hii inaisha. Nitakapokuwa nikisimama hapa, Mheshimiwa Waziri wa Maji, nitakuwa nazungumza mambo mengine, siyo maji. Saa imefika, naomba mtusaidie wananchi wa Bukombe tuweze kupata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, najua muda wangu umekwisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi nyingi kwa Mheshimiwa Waziri Mwigulu kwa kazi yake nzuri ya kutusaidia sana kutatua changamoto mbalimbali Jimboni kwangu, nina mchango ufuatao kwa Wizara:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo cha zao la pamba kimekuwa kikisuasua sana kutokana na uwepo wa changamoto nyingi kwenye zao hili. Ubora wa mbegu ya pamba unakatisha tamaa. Tunaiomba Serikali sasa iweke kipaumbele kwenye uzalishaji wa mbegu bora za pamba.
Mheshimiwa Naibu Spika, msimu uliopita Wilaya ya Bukombe ilikuwa na mnunuzi mmoja tu wa pamba, jambo lililofanya bei ya pamba kukomea sh. 800/= kwa kilo. Naiomba Serikali itoe maelekezo ili uwepo wa soko huria wauone pia Wanabukombe.
Mheshimiwa Naibu Spika, wapo wakulima ambao waliingia kilimo cha mkataba, lakini kutokana na hali ya hewa, kuna mazao yaliharibiwa na hivyo kuwafanya wakulima hawa wawe na deni ambalo itakuwa vigumu kulilipa. Naiomba Serikali iweke utaratibu wa kutoa fidia kwa wananchi ambao mazao yao yameharibiwa na mvua.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Geita ni miongoni mwa mikoa mipya, lakini Ofisi ya Kilimo Mkoa, haina gari. Naiomba Serikali itupatie gari la Idara ya Kilimo Mkoa wa Geita.
Mheshimiwa Naibu Spika, usambazaji na utoaji wa pembejeo uzingatie majira halisi ya kilimo. Kumekuwa na mazoea ya kuleta pembejeo nje ya muda wa msimu wa kilimo. Nashauri Wakala wa Mbegu uimarishwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, ufugaji wa samaki ni jambo linalopaswa kupewa kipaumbele sana. Serikali sasa ianze kutoa ruzuku kwa ufugaji wa samaki. Aidha, Serikali pia ianzishe utoaji wa elimu ya ufugaji samaki.
Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta ya Mifugo ina changamoto nyingi. Mifugo haina maeneo ya malisho, Wilaya ya Bukombe haina maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya mifugo. Naomba Wizara ishirikiane na Wizara nyingine kutenga maeneo ya wafugaji. Huduma za ki-veterinary sasa zifufuliwe ili mifugo mingi iweze kupata huduma ipasavyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nipongeze sana Wizara kwa kazi kubwa inayofanywa ya kuinua elimu ya Tanzania, bado kuna kama kazi ya kufanya ambayo ninaamini kwa uwezo wenu mtaikabili na kuimaliza mapema. Naomba kuchangia machache yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Buhombe ina changamoto ya uwepo wa Chuo cha VETA, Wilaya hii ipo kwenye rasilimali nyingi zikiwemo misitu (mbao), madini, mifugo (ngozi) ambazo zinaweza kurahisisha kwa kiwango kikubwa ujifunzaji na upatikanaji wa ujenzi (skills) wa kutumia rasilimali hizi ili ziwe zenye faida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya yetu ina changamoto ya high school kama nilivyokuja ofisini kwako, naomba sana Mheshimiwa Waziri, shule yetu ya sekondari ya Businda iongezewe mabweni na mabwalo, madarasa na maabara ili shule iwe high school. Kwa sasa hali tuliyonayo wanafunzi wetu wengi wanalazimika kusafiri umbali mrefu kufuata elimu ya kidato cha tano na sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ukaguzi wa shule, idara ziimarishwe na ninaomba kushauri upatiwe rasilimali za kutosha kwa maana ya miundombinu, rasilimali fedha na watu, nashauri pia wakaguzi walipwe mishahara inayowapasa kama ilivyo kwa Wakuu wa Idara (LSS). Aidha, naomba idara hii, ifanywe kuwa wakala wa kujitegemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, napongeza sana ushirikiano wa Wizara na Watendaji wake wanaonipatia wakati wote.


Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizi, naomba pia nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na Naibu Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara kwa miongozo wanayotupatia Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe. Naomba kutoa mchango wangu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe imeleta Wizarani maombi ya kupatiwa vibali vya kujenga miradi ya maji kwenye Wilaya yetu. Kwa mijini, tunaiomba Wizara iharakishe miradi ya Mji wa Ushirombo kwani Wilaya hii pamoja ukongwe wake haina mtandao wa maji mjini hasa kwenye Kata za Igulwa, Kateute, Bulaugwa na Ushirombo. Wananchi kama ilivyo kwenye maeneo mengine ya Wilaya, wanapata shida kubwa sana ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kata ya Uyovu tuna chanzo cha maji kikubwa ambacho kama kitapatiwa fedha, kinaweza kusambaza maji kwenye mji mdogo wa Runzewe ambako maeneo ya Kabuhima, Azimio, Kanembwa na baadhi ya maeneo ya Kabagale. Naiomba Wizara itusaidie kupata fedha kwa ajili ya kupanua mradi huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ya umwagiliaji iliyopo Bukombe imesimama muda mrefu. Mradi wa Nampangwe na Bugelenga imesimama. Pamoja na kutumia fedha nyingi za Serikali lakini fedha ya kukamilisha haijatolewa jambo ambalo hadi leo wananchi wanaona halina manufaa. Naomba miradi hii ipatiwe fedha ili ikamilike na wananchi wa maeneo haya waweze kulima kwa tija katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo haya yakipewa kipaumbele yataondoa kabisa tatizo la njaa kwenye Mkoa wa Geita na Mikoa ya jirani.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini
WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kukushukuru tena kwa kunipa nafasi hii kuhitimisha hoja ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Madini Mwaka wa Fedha 2022/2023. Wizara imepokea michango mbalimbali ya Waheshimiwa Wabunge ambayo wameitoa kwa kusema, pia tumepata ushauri na maoni ya mapendekezo kutoka kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati ya Madini ambayo kwa kweli ni muhimu sana kwetu.

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla ushauri na maoni yaliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge ni ya msingi sana. Huo ni ushahidi mwingine kuwa Bunge lako ni Bunge ambalo kwa kweli linasimamia maslahi mapana ya wananchi wetu wa Tanzania. Ukiwasikiliza kwa kiwango kikubwa yale wanayoyazungumza ni yale ambayo ama yanaathiri uchimbaji ama biashara yenyewe ya madini na hivyo kufanya sekta hii isikue. Kwa hiyo, tumeyachukua kwa uzito mkubwa na sisi kama Wizara tutaenda kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, naomba tu nifafanue kwa kifupi hoja mbalimbali ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezielezea. Nieleze kwamba Wizara ya Madini kwa vyovyote vile ili uweze kufanya maendeleo kwenye sekta na kuifanya sekta ikue haiwezi kuwa na monopoly ya mawazo au ya fikra, ni lazima ichukue mawazo ya Waheshimiwa Wabunge, mawazo ya wadau wengine waliomo kwenye sekta na kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mmeona hapa hoja zinazozungumzwa kwa kweli ni zile ambazo zinatufundisha au zinatuelekeza kwenye kuboresha zaidi, zinaweza kuzungumzwa kwa tone tofautitofauti lakini bottom line ya kila hoja iliyosemwa ni kuhakikisha kwamba manufaa ya madini haya yanakuwa kwa Watanzania na kwa nchi yetu na kwakweli ndiyo kiu yetu sisi Watanzania wote.

Mheshimiwa Spika, sasa limezungumzwa eneo la wachimbaji wadogo, nataka nilielezee hilo kwa kifupi tu. Ni kweli kwamba yapo maeneo watu wamepewa leseni na toka wamepewa leseni inawezekana hawafanyi chochote kwa namna ya kuonekana kwa macho, lakini uchimbaji wa madini wenyewe ulivyo si kila atakayepewa leseni leo leo ataanza kuchimba, mwingine ataanza kufanya utafiti, mwingine ataanza kutafuta hizo data na baadaye aanze kuchimba.

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie kwamba Wizara ya Madini toka tumeanza kuwapa nguvu wachimbaji wadogo hizo ndizo hatua tunazochukua. Tunapata lawama hapa na pale kwamba tunafuta leseni, ni kwa sababu tunatekeleza maelekezo ya Bunge, lakini tunatekeleza maelekezo ya viongozi wetu kwamba ni lazima wachimbaji wadogo wapewe kipaumbele. Hivi nilivyosimama hapa tumeshafuta zaidi ya leseni mia mbili ambazo ni dormant na zipo nyingine nyingi zaidi ya 400 ambazo zina-default notice, process ya kufuta inaendelea.

Mheshimiwa Spika, process ya kufuta leseni ina lawama nyingi, sisi Wizara ya Madini tumekubali kubeba lawama hiyo kwa niaba ya wachimbaji wadogo, kwa sababu wapo watu wengine ambao ni kweli watashika yale maeneo kufanya udalali, nitakaa na leseni kutegeshea kuona ni nani anakuja. Wengine wanasubiri wachimbaji wadogo waende kwenye hile leseni wachimbe, halafu aseme hapa ni kwangu awaondoe wale wachimbaji wadogo. Nataka niwahakikishie wale wenye leseni kwamba wale ambao wanatekeleza matakwa ya sheria, Wizara tutawalinda lakini wale ambao hawatekelezi matakwa ya kisheria, maeneo hayo tutayachukua tuwapatie wale ambao wanahitaji kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, jambo ambalo limeelezwa hapa kwa uchungu mkubwa ni jambo la CSR. Inawezekana kuna migodi mingine haifanyi vizuri. Nieleze kwa ujumla kwamba migodi mikubwa hii inatekeleza kwa kiwango kikubwa matakwa ya sheria ya kutenga fedha kwa ajili ya CSR. Sasa tunachogombea hapa siyo uwepo wa fedha, tunagombea matumizi ya fedha na nadhani hili ni jambo zuri. Tulikotoka tulikuwa tunagombea uwepo wa fedha zenyewe, sasa hivi hiyo siyo story tena, story ni namna gani hizo fedha zinavyotumika.

Mheshimiwa Spika, Sheria yetu ya Madini, section ya 105 imetoa utaratibu mzuri sana kama ambavyo Mheshimiwa Makamba ameeleza kwamba ni lazima mipango ile ya CSR ipelekwe kwenye Halmashauri. Kazi ya Halmashauri kubwa ya kwanza ni kuthibitisha au ku-approve hiyo mipango. Una- approve kwa kuangalia value for money. Kuna wakati fulani miradi mingine ilikuwa inatekelezwa; mfuko mmoja wa cement unatekelezwa kwa CSR lakini mfuko wa cement unauzwa shilingi 80,000/=. Sasa kama hali ndiyo hiyo, kazi ya Halmashauri ni kuhakikisha kwamba mfuko wa bei ya soko ni huu au bidhaa inayotakiwa kununuliwa kwa ajili ya kutekeleza bei ni hii.

Mheshimiwa Spika, mgodi tuliokuwanao kwenye framework, mgodi ambao CSR yake unaweza kuiona kuanzia day one, ni migodi inayosimamiwa na Twiga, ukiwemo Mgodi wa Bulyanhulu pamoja na Mgodi wa North Mara. Hii CSR yake iko packed kwenye uzalishaji wa dhahabu. Kila wakia moja ya dhahabu unachukua dola sita unaziweka pembeni kwa ajili ya CSR.

Mheshimiwa Spika, hata North Mara, tunavyozumza, fedha zipo Shilingi bilioni 5,600 hazijafanyiwa kazi. Kuna Shilingi bilioni moja nyingine ya mwaka 2021 ipo haijafanyiwa kazi. Kinachotokea ni kwamba kuna matatizo ya usimamizi wa fedha za CSR. Kwa hiyo, kuna wakati mwingine tunafanya auditing, tunachukua muda mrefu na auditing hizo wanaoumia siyo sisi, ni wananchi, lakini kuja kumlaumu mgodi kama mtu ambaye hajatoa hizo fedha, na penyewe kwa kweli tuwatendee haki kidogo. fedha hizi wao wamezitoa na tayari ziko kwenye utaratibu wa kutekelezwa.

Mheshimiwa Spika, hata kule Bulyanhulu, tunazungumza kujenga barabara; ni kweli, mgodi umeshatenga Dola za Kimarekani milioni 40; na barabara ambayo tunabishana, tujenge kutokea Mwanza kuja Kakola au kutokea Kakola kwenda Kahama, hilo ndiyo bado tunabishana. Ila kazi ya mgodi, tayari hela zake ameshatenga, anasubiri uamuzi wetu wenyewe.

Nawaomba wale wote tuliopewa wajibu wa kusimamia mambo haya, tufanye haya mambo kwa haraka ili huduma zipatikane kwa wananchi ili imani ya wananchi kwamba sekta hii inawasaidia kwenye maisha yao iweze kupatikana.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, nami nisingependa kuchukua muda mrefu, ni jambo lililozungumzwa kuhusiana na Merelani. Nimesikia concern ya Waheshimiwa Wabunge, lakini lazima tukubali, maeneo mengi yanayochimbwa madini, watu wamebadilisha maisha yao. Ukienda Mahenge, kabla hatujapasimamia vizuri na leo hali yake ni tofauti; ukienda Geita hali ni tofauti, ukienda Kahama hali ni tofauti, lakini bila kuficha Mererani hali yake ni tofauti sana.

Mheshimiwa Spika, hali ya Mererani ni mahali pa ukiwa. Watu wana hali ngumu, lakini watu wanapishana na magari, wanakuja Mererani, wanaondoka. Ndiyo Serikali ikaja na utaratibu kwamba tuongeze manufaa kwa kujenga soko Mererani. Nafurahi kwamba fedha zilizotengwa kwa ajili ya kujenga lile soko ni Shilingi bilioni tano na bilioni moja imeshatolewa kwa ajili ya kujenga lile soko.

Mheshimiwa Spika, yako matatizo tutakutana nayo kwenye kutekeleza, ni kwamba ni kweli pengine biashara itashuka, kutakuwa na turbulence ya hapa na pale, isituvunje moyo. Kazi yetu kama Serikali, yale yote aliyosema hata Mheshimiwa Gambo na Wabunge wengine wa Manyara, tutayaangalia yote kwa ujumla wake, tuje na utaratibu mzuri zaidi ambao utafanya sekta hii iweze kukua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie la mwisho kabisa kwamba, katika uchimbaji madini wanawake wamechangamkia fursa sana. Naomba nichukue nafasi hii niwapongeze sana wanawake wa Tanzania na ndiyo wamekuwa walipa kodi wakubwa sana.

Mheshimiwa Spika, Wizara tumeona hiyo ni fursa ya kuwatumia wanawake kwenye sekta ya madini. Tunataka tuwahamishe wanawake kwenye utoaji wa huduma kwenye midogo waende kwenye utendaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kazi hii hatuwezi kuifanya wenyewe, tunahitaji Waheshimiwa Wabunge na wenyewe watusaidie. Kwa msingi huo, Wizara tumekaa, na tumeona kwamba tunahitaji tupate ma-champion Wabunge wanawake watakaotusaidia kuhamasisha wanawake wengine kushiriki kwenye uchumi wa madini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hali hiyo tunaomba Waheshimiwa Wabunge wafuatao watukubalie, watusaidie kwenye jambo hili; Mheshimiwa Munde Tambwe, Mheshimiwa Mhandisi Stella Manyanya, Mheshimiwa Ritta Kabati, Mheshimiwa Janejelly Ntate James na Mheshimiwa Asia Abdukarimu Halamga. Hawa wawe mabalozi wa wachimbaji madini wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja. Naomba Bunge likubali kutupitishia makadirio ya fedha tulizoomba ili tukafanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kukushukuru tena kwa kunipa nafasi hii kwa ajili ya kuhitimisha Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Madini kwa mwaka wa fedha 2023/2024. Wizara imepokea michango ya Waheshimiwa Wabunge waliyoitoa kwa kuzungumza na walioandika. Tumepata ushauri na mapendekezo ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini ambayo ni muhimu kwetu katika utekelezaji wa majukumu yetu kama Wizara na katika usimamizi wa Sekta yetu ya Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla ushauri na maoni yaliyotolewa au mapendekezo yaliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge ni ya muhimu sana kwetu na yana lengo moja tu kuimarisha Sekta ya Madini na kuifanya sekta hii ichangie zaidi kuliko inavyochangia hivi sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliyopata nafasi ya kuchangia Hotuba yangu. Jumla ya Wabunge 30 wamechangia Hotuba hii kwa kusema na kwa kuandika, ambapo Waheshimiwa Wabunge 29 wamechangia kwa kuzungumza na Mbunge mmoja amechangia kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii vilevile kulifahamisha Bunge lako Tukufu kwamba hoja zote zilizowasilishwa na Waheshimiwa Wabunge kwenye mjadala uliokuwepo hapa toka jana, Wizara tumezichukua kwa uzito wa aina ya pekee na kwa kweli hakuna hoja hata moja tunayoipuuza au tunayoifanya kuwa ndogo, zote tumezichua kwa uzito wake na kwetu sisi wametupa kazi ya kwenda kufanya katika kipindi hiki cha mwaka fedha ujao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo kutokana na ufinyu wa muda sitaweza kuzitolea ufafanuzi hoja zote kwa sababu iliyo dhahiri kwamba muda hautoshi, hoja ni nyingi na maelezo yaliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge yote ni ya msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe ufafanuzi mchache kwa mambo ya jumla na mambo mahususi pengine kwa mifano tu. Kabla sijafanya hivyo naomba tena nimshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniamini na kunipa jukumu la kusimamia Sekta hii ya Madini. Nimshukuru sana Dkt. Philip Isdori Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao wao kwa nyakati tofauti wamekuwa wakituelekeza kutekeleza mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepata pongezi nyingi katika michango ya Waheshimiwa Wabunge. Tunazichukua pongezi hizo kwa tahadhari kubwa ya mgema kusifiwa tembo asije litia maji, lakini kuwaeleza tu Waheshimiwa Wabunge, kama kuna watu wanastahili pongezi ya mafanikio ya Sekta hii ya Madini, wa kwanza ni Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania; wa pili ni Dkt. Philip Isdory Mpango, Makamu wa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania; na wa tatu ni Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu kazi zote tunazozifanya zinatokana na maelekezo ya viongozi hawa ambayo nia yao ni kuiona sekta hii inakwenda mbele na sisi tunafanya kazi ile ambayo wametutuma. Kwa kweli naomba niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa pongezi hizo. Nataka niwahakikishie kwamba pongezi walizotupa na changamoto walizotupa zitatuongezea nguvu zaidi ya kufanya kazi ili tutakaporudi hapa mwakani Mungu akipenda, basi sekta hii ije ieleze mambo yaliyo bora zaidi ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyashauri katika michango yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nisije nikasahau kuwashukuru sana sana wasaidizi wangu Wizarani. Nikianza na Naibu Waziri, Mheshimiwa Kiruswa, Katibu Mkuu Wizara ya Madini, Naibu Katibu Mkuu, Kamishna wa Madini, Watendaji wote wa Taasisi za Wizara zilizoko hapa ambao kwa kiwango kikubwa wao ndiyo wasimamizi wakuu wa mambo yote ambayo tumeyafanya Wizarani. Naomba niwashukuru wafanyazi wote wa Wizara kuanzia kada ya chini mpaka ya juu kwa kuwa naamini bila wao tusingefika hapa. Nawashukuru sana kwa support wanayonipa Wizarani na nawaombea kwa Mwenyezi Mungu awabariki sana wao na familia zao ili waendelee kuchapa kazi hii kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wameendelea kutamani itokee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niongelee mambo ya jumla machache. Jambo la kwanza limeelezwa na Waheshimiwa Wabunge wengi. Kwanza, tunapaswa kufanya zaidi ya hiki tunachofanya, wote tunakubaliana, ni kweli tunaweza kuhubiri kwamba tuna mafanikio, lakini maoni ya Waheshimiwa Wabunge na Watanzania ni kwamba bado hatujafanya vizuri zaidi. Tufanye vizuri zaidi kwa kuongeza mchango wa Sekta ya Madini, lakini tuwasaidie wachimbaji wadogo na tuvutie uwekezaji mwingi zaidi nchini ili tuweze kupata zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wameenda mbali zaidi, wamekuja na mfumo mwingine wanaopendekeza na nakubaliana nao kwamba ni muhimu sasa Serikali na yenyewe iwe mwekezaji. Tukubaliane hapa jambo moja ile dhana ya zamani ya kuwaona Watanzania wao kazi yao ni kuuza vitunguu, juisi, madini ni ya watu wengine Bunge hili leo limethibitisha tumehama. Wote tunawaona Watanzania kama watu wanaostahili kupewa fursa na wakipewa fursa tutapata mapato kutokana na wao na hiki ndicho kinachotupa ujasiri wa kusimama hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaona watu wanasema leseni zisizoendelezwa zifutwe wapewe watu wengine, hiki ndicho tunachotaka ku–empower watu wetu na leo nawaambia wenzangu pale Wizarani kwamba ni vizuri tukaweka maono makubwa hadi tuogope if you have a vision that doesn’t scare you hiyo vision ni ndogo sana. Tuwe na maono makubwa yatutishe wote mpaka tufike mahali tuseme hili ninaloliweka kweli nitalifikia? Ili litupe kazi ya kwenda kulisimamia kwa nguvu zote bila kupumzika na nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge sekta hii kama Wabunge wanavyosema, itachangia zaidi kwa sababu potential ipo na nitawaambia baadhi ya maeneo ambayo tunayaona ni potential yapo kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, kwa kipindi cha zaidi ya miaka 15 iliyopita hatukuwahi kufungua mgodi mkubwa, tunaingiza kwenye pipeline migodi mipya mingine ambayo Wabunge wameona tumesaini mikataba na niwatoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge wale wanaosema kwamba tumeingia mikataba, free courage interests hatuwezi kupata, nataka niwaambie iko migodi imeanza kulipa free courage interests hapa sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie pia kwenye Bodi ya Makampuni yote tuliyoingia ubia siyo kweli kwamba hatuna Wajumbe kwenye Bodi. Tunao kwenye bodi na kwenye mikataba ile hata kwenye management kuna watu tunateua kuwaingiza na kuna baadhi ya watu ili mgodi uweze kumteua ni lazima awe approved na Serikali, huko nyuma haikuwa hivyo, ilikuwa mtu mwenyewe mwenye leseni anateua watu wanaendesha shughuli halafu wewe huwezi kujua. Hata financial model tunafanya joint financial modeling hafanyi peke yake mwekezaji, tunajua kila aina ya madini, kila aina ya kitakachochimbwa na faida tutakazozipata ndiyo maana tunaweza tuka-project tutapata kiasi gani. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan iko makini sana kulinda mali za Watanzania, kuhakikisha kwamba hatuwezi kuona tunapoteza hata milimita moja. Nafahamu yako mambo mengine ambayo kadri tunavyoendelea tutaona tuna mahali fulani pa ku– improve. Hili nilieleze kurekebisha sheria kwa maoni yangu mimi si dhambi, kurekebisha sheria ni uungwana, kwamba huwezi kukomaa na jambo ambalo practically halifanyiwi kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana tukiliona jambo ambalo tukienda site halifanyi kazi tunarudi hapa kwa wale wanaotunga sheria tunawaambia jamani mtusaidie hili jambo huko site halifanyi kazi na tunazungumza kwa haki kabisa na Waheshimiwa Wabunge wamekuwa rahimu wanatukubalia, tunarekebisha. Lengo ni kuifanya sekta hii ikue, hatufanyi jambo lolote la kuonyesha kwamba Serikali ina mabavu zaidi tufahamu Waheshimiwa Wabunge, asilimia kubwa ya Sekta ya Madini inaendeshwa na sekta binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta binafsi ili iweze kufanya kazi, ni lazima uiwekee mazingira rafiki ya kibiashara, upunguze userikali, uwe mfanyabiashara na wewe, STAMICO yuko hapo anafanya kazi ya kuwekeza kwa niaba ya Serikali, anafanya biashara kwa niaba ya Serikali, lazima akili yake na yeye afikiri kibiashara. Leo tunapata kandarasi kwa mara kwanza toka tumepata uhuru, STAMICO anapata kazi za kufanya uchorongaji anapambana na makampuni makubwa ya nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa huku ndani ukija STAMICO anataka kununua kipuli kwa mfano rig machine imeharibika kitu kidogo kinahitaji labda dola laki moja spea. Wewe ukirudi huku ndani unataka ufate Sheria ya Manunuzi ambayo itatangaza tenda siku 14, wakati kuna mkandarasi mwingine kifaa kimeharibika leo, kesho saa tisa kimekuja amefunga, biashara inaendelea, hawezi kufanya biashara, ndiyo maana Mheshimiwa Rais akasema tuiangalie na Sheria ya Manunuzi ile ambayo inazuia biashara, tuirekebishe. Nataka niwahakikishie Wizara ya Fedha wanafanyia kazi hiyo ili tuwe na sheria ambayo ni rafiki itakayoruhusu biashara hapa nchini ili mwisho wa siku sekta hii iweze kukua. (Makofi)

Mheshimwa Mwenyekiti, kwa habari ya GST, asingeweza kufanya utafiti kwa sababu ya sheria aliyokuwa nayo, kazi yake ilikuwa ni ku– rospect peke yake anaishia hapo, explorations haikuwa kazi yake, tulikuja hapa baada ya maoni ya Waheshimiwa Wabunge, tukaleta hoja wakatukubalia, tumebadilisha sheria tumempaka Mamlaka GST, sasa kwa Bunge hili aweze na yeye kufanya utafiti hasa kwa madini mkakati kwa sababu lazima tukubaliane dunia inaelekea huko. Sasa hivi GST anafanya explorations na ataingia mikataba na makampuni mengine binafsi na Serikali itaweka fedha pale kwa ajili kuweza kumpa mamlaka zaidi ya kufanya utafiti. Nataka niwaambie hili jambo ni jipya, twende nalo taratibu, lakini mwisho wa siku tutaona kile tulichokusudia kukipata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Gambo na wengine wamezungumza juu ya minada, naelewa concern ya kubadilisha kanuni ile ya Mererani controlled area ni ya kuzuia madini yote kuuzwa nje ya Mererani. Lengo lilikuwa ni kufanya Mererani uwe Mji wa kuchangamka. Mheshimiwa Rais ameshatupa maelekezo na tumelifanyia kazi. Nataka niwaambie tunarejesha minada ya madini, tunarejesha maonyesho ya madini ya vito hapa nchini kama ilivyokuwa huko nyuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliacha kufanya hivyo nadhani ilikuwa mwaka 2017, tunarejesha sasa na tunaweka utaratibu na hivi ninavyozungumza tuna timu ya wataalam ambayo imekwenda kuangalia minada mingine inavyofanyika Thailand, India ili tuweze kufanya jambo hili na wale wote wanaoendesha minada huko duniani wako wengi wamekubali kuja kutuendeshea minada hii ili tuweze kuwapa bei nzuri zaidi wachimbaji wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusilaumiane, tuamini kwamba kila jambo tunalolifanya nia yetu ni njema kuifanya sekta hii ikue. Nataka niwahakikishie Wabunge kwamba mambo yote haya yatakwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo moja limezungumzwa la migogoro na kwamba Wizara kunapotokea mgogoro hatua ya kwanza tunaenda kuwafukuza watu na kwamba kuna mahali pengine wachimbaji wakipata madini wanakwenda kuwafukuza. Tuweke rekodi sahihi, toka Serikali ya Awamu ya Sita sikumbuki eneo lolote ambalo wachimbaji wadogo wamefukuzwa. Nataka niwaambie eneo ambalo wachimbaji wadogo wanaweza kusimamishiwa biashara ya uchimbaji kunakuwa na sababu za kiusalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Getere amezungumza hapa Kinyambwiga, Kinyambwiga usingeweza kuruhusu waendelee kuchimba kwa sababu ni eneo ambalo watu wenyewe walitaka kuonyesha wana nguvu kuliko hata wasimamizi wenyewe. Tumepeleka Polisi pale, Polisi amepigwa, tumepeleka walinzi, walinzi wamepigwa. Hatua ya kwanza, ni ku–restore peace ili uweze kuchimba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kuchimba mahali penye mapigano na lazima niwaombe wachimbaji wetu nchini waelewe kwamba Serikali hii inatoa mazingira yote ya kuchimba, tunafuta maeneo mengi ambayo Serikali inalaumiwa tuwapatie wachimbaji wadogo, haiwezekana tena hata wale wanaokuja kusimamia pale na wao waweze kufanyiwa vurugu. Tulifanya hivyo kwa sababu moja na baada ya amani kurudi mgodi ule tuliufungua na biashara inaendelea. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge tuendelee kutoa elimu kwa wachimbaji wetu kwamba, madini haya ni yetu tuyachimbe kwa amani yaweze kutupatia manufaa na mwisho wa siku tuweze kupata faida ambayo tunakusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie jambo la refinery kwa sababu ni jambo kubwa. Katika Sheria tulizorekebisha mwaka 2017, Serikali ilielekeza au Bunge lilielekeza kwamba sasa madini yote yaongezwe thamani hapa nchini. Kazi ya kwanza ilikuwa ni kuvutia watu waje wajenge mitambo ya kusafisha dhahabu ili tupate refinery. Refinery ili uweze kupata certifications process yake ina inachukua muda mrefu, wako waliyofikia hatua ya ISO, wako wengine wanakamilisha taratibu ili mambo haya yaweze kufanyika. Sasa tumefanya nini sisi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulichoamua na Benki Kuu walikuja kwenye Kamati ya Mheshimiwa Kitandula, wakatoa taarifa, kanuni ya kununua dhahabu tayari imekamilika na wameanza kununua dhahabu na hivi ninavyozungumza wameshanunua kilo mia nne kama Benki Kuu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachotaka sasa tunakamilisha taratibu zilizoko kwenye refinery ili tuweze kuanza kununua dhahabu kama Serikali na kuanzisha hicho kinachoitwa National Gold Reserve kwa ajili ya kuhimarisha currency yetu. Tutaenda taratibu lakini tunataka twende kwa uhakika ili makosa yaliyotokea huko nyuma yasije yakajitokeza. Wale wenye refinery nawaomba wenye mabenki wawape muda, kwa sababu kuna mambo mengine ambayo ni kisera ambayo bado tunayarekebisha. Kwa mfano ni lazima kwenye refinery uweke incentive, tumepunguza kupitia Bunge hili mrabaha kwa wale wanaouza dhahabu kwenye refinery kutoka asilimia sita hadi asilimia nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaangalia gharama ya ku– refine, isiwe kwa mchimbaji iwe kwa BOT na Benki Kuu wamekubali kuchukua gharama, lakini tunaangalia vile vile kama inspection fee tunaweza tukaona kiasi fulani kibaki kwa ajili ya refinery ili mchimbaji anapopeleka madini yake asipate gharama yeyote. Kwa kufanya hivyo dhahabu itakuja. Mwisho wa siku kwa sababu sheria inaturuhusu, tutazuia kabisa kama nchi nyingine kusafirisha dhahabu ambayo haijasafishwa kwa sababu viwanda vya kufanya hivyo viko hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda nirudie tena kuwashukuru sana sana Waheshimiwa Wabunge wote kwanza kwa namna wanavyotusaidia kusimamia Sekta ya Madini. Mimi huwa nawaambia wenzangu sekta hii hatusimamii Wizara, tunasimamia wote, maoni na michango ya Waheshimiwa wabunge ndiyo inayotufanya sisi twende kwenye drawing table tuone jambo gani turekebishe na jambo gani tulifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata haya mambo mengine, Mheshimiwa Hassan amezungumza habari ya cyanide na mercury, nilieleze tu tulishapitisha azimio hapa la kupiga marufuku matumizi ya mercury na matumizi ya cyanide na mercury ni tofauti, lakini vile vile recovery ya dhahabu labda tu kwa taarifa ya faida ya Bunge, recovery ya mercury ni ndogo ni chini ya asilimia ishirini wakati cyanide hutumii kwa mkono kama unavyotumia mercury, yenyewe unatumia either kwa VAT leaching au kwa CIP au CIL. Hii ni ya kiwanda kabisa siyo uchenjuaji wa kawaida kama wa wachimbaji wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe nchi nyingi sana na wanaotuzunguka wamehama kwenye matumizi ya zebaki kwa sababu ni hatari zaidi kwa afya za watu, tuwa-support watu wetu kwamba waanze kutumia teknolojia ya kisasa kwa ajili ya uchenjuaji wa dhahabu badala ya kutumia kemikali ambayo ina athari kwa mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti baada ya kusema maneno hayo nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi, lakini vile vile nikushukuru sana kwa namna ulivyotusimamia pamoja na Mheshimiwa Spika, Naibu Spika kwa namna ambavyo mnatuongoza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, naomba sasa Bunge lako likubali kutupitishia fedha hizi ili tuweze kwenda kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii, na mimi nichangie Bajeti Kuu ya Serikali. Kabla ya kufanya hivyo, naomba tena nimshukuru Mungu kwa nafasi hii, ambaye amenipa uhai niweze kusimama tena mbele yako ili niweze kusema machache.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikupongeze sana wewe binafsi kwa namna unavyoliendesha Bunge letu. Wewe umekuwa kamanda wa makamanda; tumeona hapa makamanda wanakukimbia kila ukitokea; na hiki ni kiashiria kwamba wewe hutishiki, uko imara. Na mimi nakuhakikishia tu kwamba sisi Wabunge wenye nia njema tuko pamoja na wewe. Endelea kutuongoza kwa kufuata kanuni zetu na taratibu tulizojiwekea, bila shaka na Mungu atakubariki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa bajeti aliyoiwasilisha. Bajeti hii bila shaka inatutatulia changamoto nyingi, lakini yako mambo ambayo nadhani yanahitaji kuboreshwa kidogo; na kwa maoni yangu ndiyo haya yaliyonifanya nisimame. Nianze na sekta ya elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sekta ya elimu imetengewa jumla ya bajeti ya shilingi trilioni 4.8 na unafahamu kwamba kwenye Azimio la Dakar tulikubaliana kwamba kila nchi itenge 6% ya GDP yake ipelekwe kwenye elimu. Ukiangalia hapa, pesa ambazo tunapeleka kwenye elimu shilingi trilioni 4.8, fedha nyingi kati ya hizo tumesema, zinazokwenda kwenye maendeleo ni shilingi bilioni 897.7 na shilingi bilioni 427.6 zinakwenda kwenye matumizi mengineyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha hizi za maendeleo zilizotengwa; 50% yake inakwenda kwenye mikopo ya wanafunzi. Kwa maoni yangu naona inaondoa dhana ya maendeleo, inaingia kwenye dhana ya matumizi mengineyo. Na mimi ninadhani, hizi fedha ambazo zimepekwa kwa ajili ya mikopo ya wanafunzi, zilipaswa zitoke kwenye kifungu cha maendeleo zije kwenye kifungu cha matumizi kwa sababu zenyewe zinakwenda kutumika kwa ajili ya kuwapatia mikopo wanafunzi. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri aje atueleze kwa nini fedha hizi zinapelekwa kwenye maendeleo badala ya matumizi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumezungumza miaka mingi, na mimi kabla sijawa Mbunge nilikuwa nafutailia Bunge hili. Kwa muda mrefu tumekuwa tukihangaika na kuifanya Idara ya Ukaguzi kuwa Wakala wa Ukaguzi wa Elimu Tanzania. Elimu ya Tanzania hii dawa yale iko kwenye ukaguzi; elimu ya Tanzania ili iwe bora lazima kuwe na mtu ambaye anaiangalia kila siku. Idara ya Ukaguzi ambayo iko chini ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, leo Sayansi na Teknolojia; fedha inayopewa ni kidogo sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nenda kila kona ukaangalie, Idara ya Ukaguzi wana hali mbaya ya kifedha. Magari yao hata matairi hayana; magari yao hata mafuta hayana; uwezo wa kukagua kwa maana ya capacity ya wafanyakazi ni kidogo. Leo kwenye bajeti hii ukaguzi wametengewa 20% peke yake; fedha hizi ni kidogo sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa tunadhani kwamba tunapiga hatua, tunakwenda mbele kwa kuifanya Idara hii kuwa Wakala Maalum wa Ukaguzi wa Elimu nchini ili quality assurance tunayoizungumza kila mara iweze kuwa na uhakika zaidi, lakini leo ninaona tunarudi nyuma badala ya kwenda mbele. Naomba sana Idara hii iangaliwe, wafanyakazi wake, miundombinu pamoja na vitendea kazi, wapatiwe ili tuweze kukagua elimu ya nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka nilizungumzie ni kilimo. Kilimo kimetengewa shilingi trilioni 1.6 na kimebeba 4.9% ya Bajeti yote ya Serikali ukiondoa madeni. Mwaka wa 2014 walikopesha matrekta 118; mwaka 2015 wamekopesha matrekta 74 peke yake na mwaka huu tunarudi nyuma tena. Tulikuwa tunaamini kwamba kilimo ndiyo sekta ambayo inaajiri Watanzania wengi zaidi, tulipaswa kuweka nguvu zaidi pale kuliko kuiangalia kwa namna ambayo tunaiangalia hivi sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikwambie mwaka huu wa kilimo na msimu huu wakulima wa pamba hawana habari njema wanayoielezea. Mbegu waliyopewa haijaota. Nenda Bukombe pale, wakulima wanalalamika mbegu waliyopewa 73% tu ndiyo iliyoota, haikuota. Wamepewa dawa za kuua wadudu, hazikuua wadudu, lakini wakulima hawa hawana namna ya kufidiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Bunge hili tuiombe Serikali, wakulima ambao walipelekewa dawa ambazo hazikuua wadudu, wakulima ambao walipelekewa mbegu ambazo hazikuota, Serikali ije na commitment ya kuwafidia watu hawa kwa sababu, wametumia nguvu kubwa kuwekeza pale; na kilimo hiki ni mara moja baada ya mwaka mmoja. Tusipowapa kifuta machozi watu hawa, nataka nikuhakikishie mwaka mzima watu hawa watakuwa maskini kwa sababu kile wanachokitarajia hawatakipata. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumzie vilevile kwenye eneo la wachimbaji wadogo wadogo. Wilaya yetu ya Bukombe na Mkoa wa Geita, kama unavyofahamu, ni Mkoa ambao una dhahabu nyingi. Uchumi wa Geita unategemea dhahabu na ndiyo maana hata Mheshimiwa Serukamba alivyosema katika mikoa maskini, indicators au vigezo walivyovitumia kuifanya Geita kuwa mkoa wa pili kwa umaskini Tanzania hata mimi ilikuwa inanisumbua.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakuomba sana na Mheshimiwa Waziri wa Fedha, fedha za ruzuku kwa ajili ya wachimbaji wadogo wadogo tuzipeleke. Shilingi milioni 900 hizi tulizozitenga zisiishie kwenye makaratasi, ziende kwenye reality, tuwapalekee wachimbaji wetu wadogo wadogo waweze kuchimba kisasa ili waweze kujikwamua kiuchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Geita vijana wengi uchumi wao na hasa wa Bukombe, wanategemea uchimbaji wa dhahabu. Ukienda huko kila mmoja anakuuliza ni lini mnatuletea maeneo? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimemsikia Mheshimiwa Naibu Waziri anasema kuanzia mwezi wa saba. Ninaomba mwezi wa Saba iwe kweli, wachimbaji wadogo wadogo waanze kuchimba. Tusianze tena kuambiwa bado tuko kwenye michakato. Jamani wamesubiri michakato muda mrefu, sasa hivi wanahitaji kuona matokeo ya kuchimba na wanapatiwa eneo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kidogo ufugaji wa nyuki. Ufugaji wa nyuki ni eneo ambalo kwa Wilaya ya Bukombe limeajiri Watanzania wengi sana. Wako watu zaidi ya 6,000 wameajiriwa kwenye sekta ya ufugaji wa nyuki, lakini watu hao hawana mtu wa kuwasaidia, wanafanya kwa mizinga ya kienyeji. Nimeangalia takwimu kwenye Hali ya Uchumi wa nchi, kuanzia mwaka 2010 sekta ya ufugaji wa nyuki inashuka. Mwaka 2010 tani 428 tu; mwaka 2011 tukashuka, tukavuna tani 343; mwaka 2012 tukashuka, tukavuna tani 103; mwaka 2013 tukashuka, tukavuna tani 83.
Mheshimiwa Naibu Spika, wafuga nyuki hawa wakipewa fedha kidogo tu kwa ajili ya kuwa na mizinga ya kisasa, kwa ajili ya kufuga nyuki kwa namna ya kisasa, nataka nikuhakikishie, inatoa ajira kubwa sana kwa Watanzania na hasa wananchi wa Bukombe.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Uyovu, ukienda Namonge, kule kote wananchi wa kule wanategemea ufugaji wa nyuki ili waweze kupata mapato yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakuomba sana, mazingira haya wezeshi tuyafanye kote. Nchi yetu, amezungumza Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwenye bajeti yake kwamba kazi tuliyonayo sasa hivi ni kutengeneza mazingira wezeshi ya wawekezaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nasoma kwenye taarifa moja ya urahisi wa kufanya biashara duniani; nchi yetu ni ya 139 kwa urasimu. Ukitaka kufungua biashara Tanzania, unahitaji siku siyo chini ya 19 ili uweze kufungua biashara. Mazingira haya ambayo siyo wezeshi hayawezi kuwavutia wawekezaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia vilevile kwenye compliance, hivi tunawalindaje wawekezaji kama nchi? Nchi yetu ni nchi ya 64. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu tuna kazi kubwa ya kufanya, namwomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha arekebishe haya, tuweze kuwasaidia Watanzania…

NAIBU SPIKA: Ahsante.
Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo
MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana kwa nafasi hii lakini vilevile niwashukuru sana Wajumbe wa Kamati ya LAAC pamoja na PAC kwa taarifa yao nzuri ambao kwa kweli wamefanya kwa niaba yetu sisi Bunge zima. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ya LAAC imekuja na mapendekezo tisa kwa mujibu wa tarifa hii. Mimi naomba nitangulie kusema nayaunga mkono mapendekezo yote hayo ambayo imeyatoa. Kwa kweli ukisoma taarifa hii utaona Kamati hii imechukua muda mwingi sana kufanya kazi. Sisi kama Wabunge kwa sababu kazi hii wamefanya Wabunge wenzetu tunawajibika kuwapongeza sana Wajumbe na uongozi wote wa Kamati hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza lililozungumzwa kwenye Kamati hii na mimi nataka nichangie kidogo kwenye maeneo hayo ni upelekaji wa fedha kwenye Halmashauri zetu. Kila Mbunge aliyesimama hapa amezungumza kwa namna tofauti tofauti namna ambavyo kutokupelekwa kwa fedha za maendeleo kwenye Halmashauri kunavyoathiri miradi ya maendeleo kwenye Halmashauri zetu. Wewe unafahamu na Bunge linafahamu shughuli nyingi tunazofanya sisi Wabunge zinatekelezwa kwenye ngazi ya Halmashauri, kama Halmashauri hizi hazipatiwi pesa bila shaka mwisho wa siku hatutakuwa na jambo la maana la kujivunia kwamba tumefanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kwenye Wilaya yetu ya Bukombe tumepeleka maombi mbalimbali ya fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Barabara nyingi zilizopo kule kwa muda mrefu hazipitiki kwa sababu maeneo mengi ya Wilaya yetu ya Bukombe yapo kwenye milima, barabara zile zimekatika, hazipitiki. Barabara kama za Maghorofani, Mchangani, Imalanguzu, Nifa, Rulembela na Kelezia hizi zote hazipitiki kwa sababu hazijawahi kufanyiwa matengenezo mwaka uliopita na mwaka huu vilevile hatujawahi kupata fedha. Kwa hiyo, naunga mkono mapendekezo ya Kamati ya kwamba sasa Serikali iharakishe kuzipeleka pesa kwenye Halmashauri ili tuweze kupata maendeleo haya na ukarabati wa miradi hii uweze kukamilika.
kufurahi. Wilaya ya Bukombe na Wilaya nyingine kwenye Mkoa wa Geita na hili nimeliuliza humu Bungeni, nimekwenda TAMISEMI nimewauliza fedha za walimu waliosimamia mtihani wa kidato cha nne mwaka jana ziko wapi? Wengine wakaniambia uende kwa watu wa Wizara ya Elimu, wengine wanasema hapana nenda TAMISEMI, shilingi milioni 35 walimu wa Bukombe kila tukikutana ndiyo jambo wanaloniuliza. Kila tukionana wananiambia Mheshimiwa pamoja na maneno mazuri uliyonayo kahela ketu kako wapi? Naomba hapa kahela haka kapatikane, watu hawa wapewe chao, watu hawa wajijue na kahela kao haka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumesimamisha kupandisha vyeo vya walimu kwa sababu tulikuwa tunashughulikia watumishi hewa, tumesimamisha mishahara iliyokuwa imepandishwa ikarudi ili tumalize jambo la watumishi hewa, hata haka ka kusimamia mitihani na kenyewe kanasimama, hapana! Naomba sana walimu hawa walipwe fedha zao ili waweze kufanya kazi yao kwa juhudi wakiwa wanajua kwamba Serikali inawapenda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ajira ya mwaka jana iliandikwa barua TAMISEMI kwenda kwenye Halmashauri zote walimu wapya walioajiriwa fedha zao zile Halmashauri zichukue kwenye akaunti yoyote pesa zilipe nauli. Wilaya ya Bukombe shilingi milioni 58 zilichukuliwa ni fedha za wakandarasi zikalipa nauli walimu wapya waliokuwa wameajiriwa, zikalipa subsistence allowance kwa ajili ya walimu wale wapya, fedha hizo hazijalipwa, wakandarasi wanatafuta hela, Halmashauri inahaha ipate wapi pesa ya kuweza kuwalipa wakandarasi hawa. Halmashauri hii ikishtakiwa na ambavyo hatuna fedha imani yangu ni kwamba hatuwezi kutoboa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba TAMISEMI kwa barua ile mliyoandika ya kwamba wachukue fedha kwenye akaunti yoyote mtarudisha, rudisheni hizi fedha sasa hivi Halmashauri kule hali ni mbaya. DT hata kukaa kwenye kiti anaona shida, Mkurugenzi kukaa kwenye kiti anaona shida kwa sababu wakandarasi hajui watakuja kwa wakati gani. Naomba Wizara ya TAMISEMI tuhakikishe kwamba madai haya tunayashughulikia haraka iwezekanavyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lipo lililosemwa hapa na watu kwenye Waraka tmezungumzia asilimia kumi ya vijana na akina mama, naomba hili jambo tuanze…
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. DOTO M. BITEKO – MWENYEKITI WA KAMATI YA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa
Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii nikushukuru sana wewe kwa kunipa fursa hii, lakini
vilevile niwashukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri wa Nishati na Madini pamoja na Waziri wa
Nishati na Madini na Wabunge wote waliochangia hoja hii. Kwa kweli michango yao imekuwa
mizuri na imeboresha sana taarifa yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, wachangiaji kwenye hoja yetu walikuwa 32, hawa wote 32
wamechangia kwa kusema, lakini Waheshimiwa Wabunge tisa wamechangia kwa kuandika.
Katika kujumuisha hoja yetu nitaelezea tu mambo machache ambayo yamejitokeza kwenye
michango ya Waheshimiwa Wabunge na wachangiaji wengine kwa ujumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo kubwa ambalo Waheshimiwa Wabunge wengi
wamelichangia ni suala la umeme, na suala la umeme hili wamelijadili katika maeneo yote
mawili – upande wa TANESCO na upande wa REA, hoja hii imechangiwa na Wabunge 27. Kwa
upande wa TANESCO, Waheshimiwa Wabunge wengi wameeleza masikitiko yao, wameeleza
msisitizo wao, wametoa maoni yao juu ya madeni ya TANESCO na kuomba kuwepo kwa
namna ambayo TANESCO itaweza kutoka kwenye mkinzano huu wa madeni makubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye upande wa REA, Waheshimiwa Wabunge wengi
wamezungumzia juu ya usimamizi wa miradi ya REA, wamezungumzia vilevile upelekaji wa
fedha za miradi ya REA na na wakandarasi kuwashirikisha viongozi wakati wakandarasi hao
wanapokwenda site na kuongeza ule wigo (scope) kwenye maeneo ambako miradi hii
inakwenda. Mambo haya yote kwenye taarifa yetu tuliyaeleza na Waheshimiwa Wabunge
nawashukuru sana kwa michango yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa madini jumla ya Wabunge 19 wamechangia
hoja hii, na mambo yaliyojitokeza kwenye michango yao ni pamoja na suala la wachimbaji
wadogo wadogo. Kwanza wachimbaji wadogo wadogo kupatiwa maeneo ya kuchimba, lakini
vilevile wachimbaji hawa wadogo wadogo kupatiwa ruzuku ili iweze kuwasaidia kuchimba
kisasa. Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia vilevile hili jambo la wachimbaji
wadogo wadogo kuvamia leseni za wachimbaji, jambo hili kwenye Kamati pia na Serikali ilitupa
ufafanuzi wa kutosha.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia wamezungumzia suala la Tanzanite. Tanzanite
kupatikana Tanzania na Tanzania isiwe ya kwanza kwenye muuzaji wa Tanzanite linawakera
Waheshimiwa Wabunge wengi kama ambavyo linawakera Watanzania wengi. Lakini naomba
tu nitoe taarifa, Serikali jambo hili imelichukua kwa uzito wake na kwenye kamati tulipewa
taarifa kwamba Serikali imepeleka ukaguzi maalum (special audit) na nilidhani tusizungumze
sana hili kwa sababu baada ya taarifa ile kuja tutakuwa na mahali pa kuanzia kuishauri Serikali
vizuri. Kwa hiyo, nadhani hili tuiachie Serikali kwa sababu imeshalichukua kwa uzito wa aina
yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia STAMICO,
Wabunge sita wamechangia juu ya STAMICO na wameelezea juu ya kuhodhi maeneo mengi
ya STAMICO. Hili ni kweli, lakini hata kwenye kamati wajumbe walilizungumza kwa uchungu sana
kwa sababu STAMICO ana maeneo mengi ambayo ameyashikilia lakini hachimbi, ameingia
ubia na wawekezaji, wale wawekezaji kwa miaka karibu 12 hakuna wanachofanya. Tunaitaka
na kuiomba Serikali kwamba sasa ifike mahali hawa wabia walioingia JV na STAMICO waanze
kufanya kazi, vinginevyo itakuwa ni kupoteza muda.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wanaovamia yale maeneo ambayo yako dormant
utakosa sababu ya kuwaondoa kwa sababu wewe hilo eneo umelishika. Kwa mfano
Mheshimiwa Bukwimba amezungumzia suala la Bacllif. Pale kuna leseni 12 ambazo STAMICO
wameingia mkataba pamoja na TANZAM 2000; lakini toka wameingia makubaliano hayo
hakuna kinachoendelea. Kwa hiyo, wananchi wale wanaweza kuvamia kwa sababu hawaoni
jambo lolote linaloendelea, na Serikali imechukua hatua juu ya jambo hili, inaielekeza STAMICO Mheshimiwa Naibu Spika, na niwaombe Waheshimiwa Wabunge waliopendekeza
kuifuta STAMICO, mimi nadhani tui-capacitate STAMICO. Itakuwa ni jambo la aibu sana sisi
wenyewe, Serikali, Watanzania tunaanzisha shirika letu wenyewe tunaliua halafu tunaanzisha
lingine, kwani Watanzania tutawatoa wapi? Si ni hawahawa tutakaowapata kuunda shirika
lingine? Mimi nilikuwa naomba tuipe nguvu, tuisimamie vizuri STAMICO iweze ku-deliver kwa
wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kinachopungua pale STAMICO ni mambo mawili; jambo la
kwanza ni upelekwaji wa fedha lakini jambo la pili ni usimamizi ulio madhubuti. Mimi naomba
nichukue nafasi hii kuwapongeza sana Wizara, kila mara wanapitishapitisha mikono yao pale
STAMICO. Ninaamini baada ya muda fulani pengine tunaweza tukaona matokeo yanabadilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, upo mgodo wa Serikali ambao ni wa Stamigold. Mgodi huu
unasimamiwa vizuri sana na Watanzania, kuanzia mfagizi, mlinzi mpaka MD wa mgodi ule ni
Mtanzania, mswahili mwenzetu. Nao wana changamoto ambazo wamezieleza. Changamoto
ya kwanza wanayoizungumzia hawana MDA, ile Mining Development Agreement,
tumewaomba Serikali wahakikishe wanafanya kazi ya kuwapatia hiyo MDA.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile mitambo waliyonayo yote ni ya kukodi hawana
mtambo hata mmoja wa kwao, jambo ambalo linasababisha gharama ya uendeshaji wa
mgodi ule kuwa kubwa sana, zaidi ya asilimia 31.7 ya gharama za uendeshaji zote zinakwenda
kwenye ukodishaji wa mitambo. Tumeiomba Serikali na katika hili nitumie nafasi hii kuiomba
Wazara ya Fedha kama migodi mikubwa ya kigeni tunaipa exemption ya mafuta, kwa nini
mgodi wetu wenyewe wa Stamigold ambao kwa asilimia mia moja ni wa Serikali, na wenyewe
tusiupe exemption ili na wao wapunguze gharama za uendeshaji, tuapte faida haraka?
Tunatoa fursa hii kwa wageni, migodi ya ndani tunaibinya, nilikuwa naomba jambo hili
lichukuliwe kwa uzito wake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wamezungumza juu ya mafuta, ujenzi wa farm tank na hili
tumelipata kutoka kwa wadau wote tuliokutana nao, wameeleza umuhimu wa kuwa na
Central Storage System ya mafuta baada ya kuwa yamepakuliwa kabla ya kusafirishwa
kwenda kwa watumiaji wengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, nirudie tena, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa
michango yao na kwa kweli niseme toka nimekaa kusikiliza mchangiaji wa kwanza mpaka wa
mwisho mimi binafsi nimejifunza vitu vingi. Wameona mambo haya kwa macho ya tofauti
pengine na kamati tulivyoona. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, ninaomba sasa Bunge lako likubali
kuipokea taarifa hii na kuwa Maazimio ya Bunge.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii. Nami kabla sijazungumza maeneno mengi naomba niounge mkono hoja, lakini nimpongeze sana mtoa hoja Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na wasaidizi wake Mawaziri; Mheshimiwa Jenista Mhangama pamoja na Mheshimiwa Angella Kairuki na Manaibu Waziri kwenye Wizara hii kwa kazi kubwa waliyoifanya na kwa namna kwa kweli ambavyo wamewasilisha hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa umakini mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba kwenye sekta ya madini yapo maeneo ambayo yamezunguzwa kwa urefu kidogo na Waheshimiwa Wabunge na moja ya jambo ambalo limeongelewa hapa ni habari ya kudhibiti utoroshaji wa madini, kwamba Wizara ionge msukumo kwenye utoroshaji wa madini. Mheshimiwa Waziri Mkuu amekuwa champion mkubwa sana kwenye jambo hili, kama mtakumbuka aliitisha mkutano na Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa wote nchini kwa ajili ya uanzishwaji wa msoko ya madini nchini. Tulikaa kwa siku mbili nzima na yeye mwenyewe alitoa msimamo mkubwa na hata wakati kwa kwenda kuzindua soko la madini kule Geita, yeye Mwenyewe Mheshimiwa Waziri Mkuu alichukua kazi hiyo ya kuzindua soko. Pia akatoa maelekezo kwa Waheshimiwa Wakuu Mikoa wote kwamba ifikapo Juni 30 mwaka huu, kila Mkoa kuwa na masoko ya madini mbalimbali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu ambaye ndiye mtoa hoja wetu leo kwa kweli amekuwa msimamizi mkubwa sana wa jambo hili. Hata hivyo, Wizara ya Madini tunafanya kazi ya kubwa ya kusimamia utoroshaji wa madini kama tulivyoeleza. Kwanza mambo yaliyokuwa yanasababisha utoroshaji wa madini ni kodi ambazo sio rafiki. Watu walikuwa wanaona nafuu kwenda kuuza kwenye masoko yasiyojulikana kwa sababu ya uwepo wa kodi nyingi ulikuwa unawafanya waogope kwenda kwenye masoko hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kodi hizo ambazo zilikuwa kero kama ambavyo wao walisema Serikali imechukua hatua kubwa kabisa ya kuziondoa; VAT withholding tax zimeondolewa ili kuwaruhusu sasa wachimbaji wetu waweze kufanya biashara katika mazingira rahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tunaongeza sasa Vituo vya Ukaguzi wa Madini. Sasa hivi tunavyo vituo 87 kote nchini, tunataka tuviongeze mpaka vifike 166 na kazi tunaanza kuifanya mapema ili tuweze kusimamia vizuri madini haya ambayo yanasafirisha nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kapufi ameelezea habari ya wachimbaji wadogo wanapongia mikataba na wageni kwenye uchimbaji. Nataka nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Kapufi na Waheshimiwa Wabunge na wachimbaji wote nchini, Serikali imewapa fursa Watanzania kutafua mbia au mtu wa kushirikiana naye kwenye kazi ya uchimbaji kutoka mahali popote. Wajibu ambao anao huyu anayetafuata mbia, kwanza lazima huo mkataba wanaoingia waulete Serikalini ili Serikali iweze kuagalia kama unakinzana na sheria zetu za ndani, lakini kuangalia kama Mtanzania huyu hatanyonywa. Tunayo mifano mahali pengi Watanzania wamengia mikataba na wageni, ukienda kuangalia mwenye leseni ni Mtanzania, lakini kila anachopata Mtanzania ni asilimia tano hadi kumi. Hatuwezi tukakubali Watanzania wakanyonywa na Serikali yao ipo kwa ajili ya kuangalia maslahi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwatoe wasiwasi na niwaombe wale wote wanaopata wawekezaji toka nje, wawalete na mikataba yao ofisi kwetu kwenye Wizara ya Madini, mikataba ile iweze kusajiliwa ili ipate nguvu za kisheria kwa ajili ya kusimamiwa, sisi tutawapa kila aina ya support watakayoihitaji kutoka kwetu. Naomba vile vile niwatoe wasiwasi Watanzania kwamba kuna utaratibu wa watu wanaofanya kazi ya utafiti kutengeneza taarifa za kupika ili waweze kuziuza kwa bei kubwa kwa watu kutoka nje. Jambo hilo kama Wizara linatufedhehesha sana, lakini zaidi sana linatuondelea imani kwa wawekezaji kutoka nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeamua Wizara ya Madini, tunataka tuanzishe mchakato wa kuanzisha Bodi itakayowasajili Wajiolojia wote hapa nchini ili kila mmoja anapofanya kazi ya utafiti na kutoa geological report aweze kubanwa na sharia, asiweze kupika matokeo kwa ajili ya kutafuta fedha.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa…

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019
WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii nikushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia hoja ya kamati. Na ninaomba vilevile nimpongeze sana Mwenyekiti wa Kamati, Mheshimiwa Mama yangu Mama Kaboyoka, kwa kazi kubwa yeye pamoja na kamati yake akisaidiana na Mheshimiwa Aeshi Hilal kwa kuendesha kamati ile vizuri na kuja na taarifa nzuri ambayo kwa kweli, imesheheni mambo mengi ya kufanyia kazi, nawapongeza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumetokea hoja tatu zinazohusu Shirika la madini Nchini (STAMICO). Na hoja hizo zote kwa ujumla wake kama Wizara tunazipokea na ni hoja za msingi sana ambazo zinahitaji kufanyiwa kazi. naomba tu nitoe taarifa kwa kamati kwamba, yako mambo ambayo tayari tumeshaanza kuyafanyia kazi. ni kweli kwamba, shirika hili lilikuwa linakumbwa na tatizo kubwa sana la utendaji na hivyo kulifanya kutokufanya kazi nzuri zaidi ya kuzalisha kama ambavyo lilikusudiwa toka kuanzishwa kwake mwaka 1970.

Mheshimiwa Naibu Spika, STAMICO toka wakati ule haijawahi kufanya kazi yoyote ya kuipatia faida isipokuwa siku za hivi karibuni baada ya mabadiliko ambayo nitayaeleza hapa:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza utendaji uliotajwa kwenye kamati ni utendaji ambao tumeshaanza kuufanyia kazi. Shirika kwa muda mrefu halikuwa na Mwenyekiti wa Bodi. Nafurahi kusema kwamba, Mwenyekiti wa Bodi amekwishakuteuliwa na alivyoteuliwa na sisi tukaangalia menejimenti nzima ya shirika, tumeifanyia maboresho mengi sana na kumpata mtendaji ambaye kwa sasa kwa kweli, mabadiliko yanaonekana sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, shirika lilikuwa linazalisha hasara na madeni mengi sana. Wakati tunaingiza bodi mpya na kubadilisha uongozi shirika lilikuwa limekwishakuzalisha madeni yanayozidi bilioni 35; ninafurahi kuripoti mbele ya Bunge lako Tukufu kwamba, sasa shirika linafanya biashara bila kuzalisha hata deni la shilingi moja. Na mwezi uliopita shirika limefanya biashara ya bilioni 24 na ndio maana umeona hata mwaka huu ulioisha tumeweza kutoa mchango kwa Serikali, jambo ambalo halikuwahi kufanyika toka shirika kuanzishwa miaka ya 70.

Mheshimiwa Naibu Spika, limeelezwa jambo hapa la mikataba ambayo shirika linaingia na ubia na mikataba miwili ambayo imeelezwa hapa, Mkataba wa kwanza ni wa Tanzanite One pamoja na Mkataba wa Bacliff:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa taarifa kuwa mikataba hii yote imekwishakupitiwa na ule mkataba ambao ulikuwa unatusumbua wa Bacliff tayari tumekwishakutoa notice ya kimakosa ya kileseni, ili tuweze kufuta leseni hiyo baadaye irudi Serikalini, ili Serikali iweze kujua namna gani itaifanyia kazi leseni hiyo. Kwa kweli, ubia ule ulikuwa sio ubia wa kutupatia faida maana ilikuwa ni leseni ile inatumika na mbia mwenzetu kukopa fedha nje ya nchi na anakwenda kuwekeza mahali pengine ambapo sisi hatujui. Sasa tumeshachukua hatua na tayari tumeshatoa default notice kwa ajili ya kufuta hiyo leseni, ili Serikali iweze kuifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ama kuhusu Mkataba wa TML tarehe 23 Disemba, mwaka wa Mheshimiwa Naibu Spika, tayari tumeshatoa Surrender Certificate ya leseni ile na sasa ninavyozungumza hapa ni mali ya Serikali. Serikali itaangalia utaratibu mzuri wa namna ya kuisimamia leseni hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hapa kwenye mkataba wa TML ndio pametuopatia matatizo mengi sana. Hata hiyo disclaimer opinion ambayo CAG ameipata ni kutokana na mbia huyo kutokuandaa vitabu vyake vya kihasibu na kutokuweka rekodi zake vizuri na kwa hiyo, CAG akienda wakati wote anakuta hakuna taarifa yoyote; kwa kweli, ulikuwa ubia ambao tusingeweza kupata faida hata tungekaanao kwa muda wa miaka 1,000. Serikali imechukua hatua baada ya maoni mbalimbali ya Serikali yakiwemo ya Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini tumefanyia kazi na tayari leseni hiyo imerudi mikononi mwa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu ambalo Kamati imeeleeza ni kufanya tathmini ya kujua mali za shirika:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nafurahi kuieleza kamati na Bunge lako tukufu kwamba, kazi hiyo tayari imekwishakufanyika na hata muundo wenyewe wa shirika tumeanza kuupitia upya. Tulikuwa na kurugenzi nyingi ambazo hazina kazi, tumezi-consolidate ili zibaki chache ziweze kuongeza tija kwa shirika na hatimaye tuweze kupata faida.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe tu taarifa kuwa, shirika hili tukilipa nafasi kwa kipindi hiki na turn arround tuliyoifanya kwa kweli, imani yetu ni kwamba, tutaanza kupata faida muda si mrefu. Hata yale madeni ambayo yalikuwepo miaka mingi tuliyoyarithi na yenyewe tumeanza kuyalipa kidogokidogo kadiri ya faida tunayoifanya. Asset tuliyonayo ni kubwa na utajiri tulionao ni mkubwa, kazi iliyopo ni kuweka akili kidogo ya kuweza kugeuza hizo assets kuwa mali na baadaye kuweza kulipa faida shirika letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nisingependa kuzungumza mengi, Kamati naipongeza tena kwa michango yake na kwa yale waliyotuelekeza. Wizara yetu kwa kweli, iko tayari kuyafanyia kazi na tunawatakia kila la heri baada ya kusema hayo. Nakushukuru sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia, lakini niseme tu kwamba hoja, michango na maoni ya Waheshimiwa Wabunge kwenye mpango huu sisi Wizara ya Madini tunayapokea yote na kuahidi kwamba tutakwenda kuyafanyia kazi kwa nguvu zetu zote. Hili linatokana na ukweli kwamba sekta yetu ya madini Waheshimiwa Wabunge hawa wamekuwa walezi wakubwa wa kushauri mahali ambako tunaona hatuendi sawa, wamekuwa wepesi haraka kutufikia na kutuambia turekebishe wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa spirit hiyo hiyo nataka nikuhakikishie na bila kupoteza muda wa Bunge lako, kwamba maoni yote waliyoyatoa Waheshimiwa Wabunge kwenye mpango huu tunaamini mtoa hoja ameyapokea na sisi Wizara ya Kisekta tumeyapokea na tutayafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda mmoja tu, la kutoa comfort kwa Waheshimiwa Wabunge, ni kwamba wamesema wengi kwamba GST ipewe mamlaka ya kufanya utafiti wa kina juu ya upatikanaji wa madini hapa nchini. Jambo hili ni la kweli, na hivi karibuni Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi tumefanya marekebisho makubwa kwenye sheria ya madini ambayo sasa imewapa mamlaka GST kufanya utafiti wa kina. Kwa sheria iliyokuwepo huko nyuma ni kwamba GST alikua anakomea kwenye kuchora ramani na kutoa taarifa za awali za madini, lakini uchambuzi na utafiti wa kina GST hakuwa na mamlaka hayo. Marekebisho tulioyafanya juzi hapa sasa yamempa mamlaka GST kufanya utafiti wa kina na kutupa taarifa za kina za madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hilo mtaona tofauti baada ya kuwa sheria imeanza kufanya kazi na Serikali imejipanga. Mheshimiwa Rais, ameshakubali kabisa kwamba ni lazima tufanye utafiti wa kina kwa nchi yetu. Hali tuliyonayo sasa hivi, utafiti tulionao wa ki-jiofizikia wa high resolution ni asilimia 16 tu ya nchi yetu. Sasa ni lazima tufanye zaidi angalau tufike asilimia 50-60 ili tujipatie uhakika zaidi wa rasilimali hii kutambua ziko wapi; na hata kama tunapata wawekezaji wanaokuja kwetu basi tuwe na uhakika bila shaka yeyote kuwaambia kwamba tuna hiki na kiko mahali gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni madini mkakati, Waheshimiwa Wabunge wengi wameelezea habari ya madini mkakati. Nataka niwahakikishieni Waheshimiwa Wabunge kwamba tumeweka utaratibu mzuri sasa, kwa sababu madini mkakati ndio yanayohitajika dunia kwa ajili ya mabadiliko ya kiteknolojia. Watu wanahama kutoka kwenye matumizi ya mafuta na kwenda kwenye matumizi ya betri. Ni lazima kama Taifa tusibaki nyuma na sisi tuchangamkie hiyo fursa. Mataifa makubwa yanakuja kwetu kutafuta madini hayo, kwa sababu tumerekebisha sheria hii, tutakacho kwenda kufanya sasa ni kuangalia mapping ya kujua madini mkakati haya yako wapi. Yametajwa ya aina nyingi na; ndiyo maana mtaona miradi mingi mikubwa ambayo inachimba madini mkakati kama nickel. Sasa hivi imeanza kuchimba kule Kabanga lakini na mahali pengine. Madini kama rare earth elemets tunakamilsha majadiliano na PRG ili madini yale yaanze kuchimbwa. Kule Niobium kwenye eneo la Panda Hill na kwenyewe tunakamilsha majadiliano ili madini yaanze kuchimbwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilitaka niseme hayo machache ili Waheshimiwa Wabunge wapate comfort kwamba mawazo yao na maoni yao yote kwa pamoja tumeyapokea na nikushukuru sana kwa nafasi hii. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Kama walivyosema wengine nichukue nafasi hii kwa kweli kuipongeza sana Kamati yetu ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, kwanza kwa umakini wao. Nimefanya nao kazi kwa muda sasa, ni Kamati ambayo kwa kweli weledi wake kwenye uchambuzi wa masuala ya madini hautiliwi shaka na ni watu ambao wanaenda kwenye details kwenye haya mambo yanayohusiana na Sekta ya Madini. Kwa kweli wametusaidia sana kama Wizara kuona namna gani tuipeleke mbele sekta ya madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kwa niaba ya wenzangu Wizarani kumshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mheshimiwa Kitandula na Makamu wake Mheshimiwa Gulamali pamoja na Wajumbe wote kwa namna ambavyo wamekuwa wakitusaidia sana katika kutusimamia kwenye kuendeleza Sekta ya Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, yamesemwa mambo kadhaa na nisingependa kuonekana kama najibu. Nataka tu kuchangia hoja ya Kamati na nataka nizungumze mambo matatu. Jambo la kwanza, imeelezwa hapa juu ya upatikanaji wa malighafi kwa ajili ya viwanda vyetu vya uchenjuaji au refinery zetu za dhahabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imefanya kazi kubwa kwa msaada wa Bunge hili. Wakati tunaanza kujenga refinery hapa nchini, changamoto na matishio ya refinery hizi kupata malighafi ilikuwa je, hawa refiners watapata dhahabu kutoka kwa wachimbaji? Kwa sababu bei wanayoweza kununua inawezekana kwenye soko ikawa ya juu zaidi kuliko wanayonunulia wenyewe. Kwa hiyo tulichofanya na tulileta hapa Bungeni tukapitishiwa na Bunge ni kutoa vivutio kwa ajili ya refineries hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kivutio cha kwanza tukashusha mrabaha wa dhahabu. Dhahabu ukitaka kwenda kuuza kwenye refinery, badala ya kuchajiwa 6% ya mrabaha, yule anayeuza kwenye refinery anachajiwa 4% peke yake na hii inatusaidia kuwapa nafasi wachimbaji wale kupeleka dhahabu na kulipa mrabaha kidogo zaidi na viwanda hivi viweze kupata malighafi.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ambalo ni muhimu Bunge tukalielewa na tusiliogope. Kwa kawaida kama una kiwanda kutafuta malighafi kutoka nje ya nchi siyo dhambi, actually ni jambo zuri sana. Kiu yetu ni kuifanya Tanzania kuwa hub ya biashara ya madini. Ni vizuri tukatengeneza mazingira rafiki ya kuwavutia majirani zetu walete madini yao hapa ndani waweze kufanya refinery na mwisho wa siku waweze kusafirisha. Advantage tuliyonayo sisi kama Taifa ni kwamba madini yanayochimbwa Tanzania kwenye masoko ya kimataifa hayatiliwi mashaka kwenye ethics zake. Yamechimbwa kwa kufuata utaratibu kwa kuzingatia haki za binadamu na kwa hiyo ukienda kwenye masoko ya kimataifa duniani yananunuliwa kirahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nataka nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaangalia rasilimali zetu za ndani, lakini hatutaacha kuwavutia wengine kwa ajili ya kuja kuuza madini yao hapa kwetu. Yako Mataifa hayana hata shimo moja la dhahabu lakini yana refinery na yanatumia rasilimali za Mataifa mengine kwa ajili ya kufanya biashara. Fursa kama hiyo hatuwezi kujifungia tu ndani tukasema kwamba sasa sisi tutatumia madini yetu peke yetu halafu tufanye refinery mengine tuyaache. Ndiyo maana tunatoa wito na mataifa mengi yamekuja hapa kujifunza, tunatoa wito kwa majirani zetu kuleta madini yao kwa ajili ya kuja kufanya refining kwetu hapa nchini kwa sababu kwanza watapata bei ya uhakika. Wanunuzi wapo, masoko yapo na mifumo ambayo ni rahisi zaidi ipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, liko lingine limezungumzwa juu ya leseni ya Peak Resource. Peak Resource wako Ngwara na Mheshimiwa Mulugo pamoja na Mheshimiwa Neema wanalizungumza kila wakati. Ni kweli kwamba tuliwahi kuwaalika kwa ajili ya kwenda kufanya signing. Tulivyofika siku ya signing wenzetu wakataka tubadilishe kipengele kimoja kwenye mkataba na kipengele ambacho tulikuwa tunabishania ni kimoja tu, kwamba uchimbe hapa uongeze thamani ya madini hayo hapa nchini. Wao wakawa wanataka wachimbe hapa wakaongeze thamani na tayari walishanunua eneo la kujenga hicho kiwanda London. Tukakubaliana Hapana, tunahitaji hicho kiwanda kijengwe hapa ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, imetuchukua muda, baadaye tumekubaliana. Naomba niwape taarifa watu wa Ngwara, Mheshimiwa Neema na Mheshimiwa Mulugo. Habari njema tuliyonayo ni kwamba timu ya majadiliano imemaliza hiyo kazi, mikataba hiyo sasa iko kwa Mwanasheria Mkuu kwa ajili ya vetting na muda siyo mrefu tutafanya ceremony ya signing kwa ajili ya mkataba huo wa rare-earth element.

NAIBU SPIKA: Haya Mheshimiwa Waziri malizia sekunde 10.

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, nataka nimalizie tu lile la STAMICO na kuwasaidia wachimbaji wadogo. Ni kweli amesema Mheshimiwa Manyinyi, wachimbaji wetu wadogo wameongeza tija kubwa sana kwenye uzalishaji. Wametoka kwenye 4% ya mapato yote tunayopata mpaka 40%. Tumeamua kuwasaidia kwa kuwanunulia mitambo kwa ajili ya kuwafanyia utafiti kwenye maeneo yao na kuwapatia leseni ili waweze kuchimba.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kuwashukuru Kamati na kwa kweli tutaendelea kuwapa ushirikiano na tunaomba Kamati waendelee kutupa ushirikiano ili tuweze kusukuma sekta yetu hii mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Azimio la Bunge kuhusu Wakala wa Kimataifa wa Kimataifa wa Nishati Jadidifu (International Renewable Energy Agency - IRENA) na Azimio la Bunge kuhusu mapendekezo ya kuridhia Mkataba wa Kuanzisha Taasisi ya Dawa ya Afrika wa Mwaka 2019 (Treaty for the Establishment of the African Medicine Agency - AMA)
NAIBU WAZIRI MKUU NA WAZIRI WA NISHATI (MHE. DKT. DOTO M. BITEKO): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nomba nikushukuru tena kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuhitimisha hoja hii.

Pili, naomba niwashukuru sana Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, chini ya Mwenyekiti wetu Dkt. David Mathayo kwa umakini wao na uchambuzi mzuri sana walioufanya wakati tumewasilisha mapendekezo ya kuridhiwa kwa mkataba huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ilifanya kazi kubwa sana na kwa kweli imeturahisishia sana hata sisi Wizara wakati wa kupitia mambo mbalimbali. Kamati ilifanya kazi kubwa ya kuwatafuta na kuwasikiliza wadau, kuona maoni yao, mashaka na wasiwasi walio nao kwenye Azimio hili. Kwa kweli, niwashukuru sana ubunifu wao umetusaidia. Wadau waliofika kwama TPSF na Jumuiya ya Nishati Jadidifu walitoa maoni ambayo kwa kweli yalikuwa yamewekwa kwa umakini mkubwa. Yaliandikwa kabisa na wengine walisema kwa michango yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kifupi, michango ya Waheshimiwa Wabunge wengi waliozungumza kuhusiana na Azimio hili, ni michango iliyounga mkono sisi turidhie na hoja kwamba, tulichelewa ni hayo waliyoyasema kwamba, wasiwasi ni akili na kwamba kawia ufike, bora tumechelewa tuwe na uhakika wa kile tunachoingia. Nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote waliotoa michango yao tunawashukuru sana, sana kwa sababu wamefanya kazi hii iwe rahisi na tutakapokuwa tunapitia sera zetu hasa za nishati jadidifu, tutazingatia kwa umakini mkubwa maoni waliyoyatoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu Waheshimiwa Wabunge wengi wameunga mkono, niseme wote wametuunga mkono kwenye jambo hili. Hivyo, nisingependa kuchukua muda wako kutoa maelezo marefu. Naomba tena nikushukuru wewe na niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao. Nataka niwahakikishie kwamba, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliposema anaifungua nchi ni pamoja na sisi kuingia kwenye Majukwaa ya Kimataifa kama haya, ambapo tunaweza kupata fursa mbalimbali za kujua taarifa mbalimbali hasa kwa sababu dunia ipo kwenye stress ya nishati na nishati jadidifu ndiyo kimbilio la kila mmoja hapa duniani, kwa sababu ya masuala ya kimazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwatoe wasiwasi kwamba Mkataba huu hautufungi kwa namna yoyote. Mkataba huu hata gharama ya kulipa ni ndogo, lakini muhimu zaidi tukiona kuna jambo haliendi sawa tuna uwezo wa ku-call off na kuweza kuendelea na maisha mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba niwasilishe Azimio kwa kusema yafuatayo:-

Kwa kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni miongoni mwa nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa;

Na kwa kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni miongoni mwa Nchi Mwanachama wa Taasisi za Ushirikiano wa Kiuchumi Kikanda wa Jumuiya mbalimbali hapa Afrika;

Na kwa kutambua kuwa malengo yaliyomo katika mkataba wa IRENA iliyoanzishwa tangu tarehe 26 Januari, 2009 yana lengo ambalo sisi kama Taifa tunahitaji pia kujiunga;

Na kwa kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inazo rasilimali za nishati jadidifu katika maeneo mbalimbali hapa nchini na yaliyotajwa katika Sera yetu ya Mwaka 2015 na madhumuni yaliyoko kwenye Mkataba huu nimeyaeleza kwa kina kwenye maelezo yangu ya awali pamoja na manufaa tutakayoyapata,

Hivyo basi kwa kuzingatia manufaa ambayo Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itakayoyapata, naliomba Bunge lako lipitishe Azimio hili kuhusu Mapendekezo ya Tanzania kuridhia Mkataba wa Wakala wa Kimataifa wa Nishati Jadidifu wa Mwaka 2009.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria mbalimbali (Na. 2) wa Mwaka 2019 (Toleo la Kiingereza).
WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii. Nitumie nafasi kuunga mkono hoja na nimpongeze sana mtoa kwanza kwa kuwasilisha, lakini kwa kazi kubwa aliyoifanya. Nawashukuru sana Kamati ya Bajeti ambao walishughulikia Muswada huu, tumefanya nao kazi kwa karibu sana, chini ya Mwenyekiti, Mheshimiwa Simbachawene. Kwa kweli ni Kamati makini, wamefanya kazi kubwa sana. Kama walivyosema, tumefanya nao mpaka usiku wa manane; na kwa kiasi kikubwa yale yote ambayo wao walipendekeza yaweze kurekebishwa, wameyarekebisha.

Mheshimiwa Spika, nataka kuongelea jambo moja tu. Jambo lenyewe ni kumpongeza sana Mheshimiwa Rais. Mabadiliko haya yaliyoletwa, kwa kweli champion wake aliyesababisha tufike hapa ni Mheshimiwa Rais. Kwenye Mkutano ule ambao tulikutana na wadau wa madini pale Dar es Salaam, tulipomwalika Mheshimiwa Rais kuja kutufungulia Mkutano, yeye aliamua ku-dedicate siku zima kukaa na kuwasikiliza wachimbaji wadogo. Hatua hii ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sifa ya Serikali inayotokana na watu, ni kuwasikiliza watu wake. Ndiyo maana mnapoona tunaleta mabadiliko ya sheria hizi, ni kwa sababu sifa hiyo Serikali ya Chama cha Mapinduzi inayo, kwamba inawasikiliza watu wake. Sheria hizi ziko kwa ajili yetu, kutuhudumia sisi. Wakati wa kutekeleza tukiona kuna ugumu mahali fulani siyo dhambi kurekebisha. Hiki ndicho kilichofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kiashiria kikubwa kabisa kinachoonesha kwamba tunawasikiliza watu, kwanza ni ule mkutano wenyewe tuliofanya na wadau. Kiashiria kingine kikubwa ni ulr mwitikio ambao Serikali imekuwa nao wa kuja kurekebisha sheria hizi ili kuondoa kero zilizokuwepo kwenye Sekta ya Madini. Naomba nitoe nafasi nimpongeze na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutoa nafasi hiyo ili wachimbaji wadogo waweze kuongeza mchango kwenye Sekta ya Madini.

Mheshimiwa Spika, limesemwa neno moja hapa, nami naamini aliyelisema alikuwa anazungumza kwa maana ya kutania tu kwamba tumeamua kubadilisha kwa ajili ya ku- change gear angani. Wadau wa madini wamekaa hapo juu. Kwa muda mrefu walikuwa na mambo ambayo wanalalamikia na ambayo sisi wenyewe wasimamizi wa sheria tulikuwa tunayaona kweli ni changamoto. Tumeamua kurekebisha ili tuweze kuongeza tija ili tuweze kudhibiti utoroshaji. Kwa mara ya kwanza kwenye historia ya nchi hii, marekebisho haya yanatengeneza masoko ya madini kwenye nchi yetu, hatukuwahi kuwa nayo. Kila mtu alikuwa anachimba, anajua atapeleka wapi. Sasa wamewekewa utaratibu, wapi watakwenda kuuza, wamewekewa utaratibu wa namna gani watasimamiwa pale kwenye masoko ya madini.

Mheshimiwa Spika, wito wangu kwa wachimbaji wadogo ni kwamba fursa hii tumeipata, tuitumie vizuri ili tuweze kuongeza manufaa. Yameongelewa maneno hapa kwamba sasa wale wenye Dealer License, kwa sababu ya uwepo wa masoko haya, watazuiwa ku-export, hapana. Wale Dealership License wataendelea ku-export kwa mujibu wa sheria. Kwa sababu kifungu hicho kinachowaruhusu ku- export bado kipo.

Mheshimiwa Spika, ilikuwepo changamoto ya kuwazuia kusafirisha madini ghafi. Tumerekebisha kifungu hicho cha sheria na sasa tumetoa mwongozo ambao kila mtu mwenye madini atapaswa kuongeza thamani kwa kiwango fulani. Kama alivyosema Mheshimiwa Millya, tayari tumeanza kutoa vibali vya watu wanaotaka ku-export.

Mheshimiwa Spika, wachimbaji wadogo wamekaa kwenye gallery yako, tatizo hilo tumeliondoa. Nawaomba sana wachimbaji wadogo watumie fursa hii waweze kuomba vibali, waweze kusafirisha madini ili walipe kodi. Kodi ambayo ilikuwa inawaudhi ni hizo ambazo zimezungumzwa. Naamini Mheshimiwa Waziri wa Fedha atakuja kuziongelea.

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kuwahakikishia wachimbaji wadogo wote Tanzania, Serikali ya Awamu ya Tano ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, ipo kwa ajili yao, ndiyo maana tunachukua muda mwingi wa kuwasikiliza. Hata siku waliyopendekeza uwepo wa Siku ya Madini Nchini, sisi tumeshaanza kuifanyia kazi kwa kushirikiana nao.

Mheshimiwa Spika, hata ukiwauliza wachimbaji wadogo kama wanasikilizwa ama hawasikilizwi, wao ni mashahidi tunawasikiliza sana, tena hatuwasilikizi ofisini tu, tunawafuata huko waliko kwenye migodi. Pia tunazungumza nao kwenye vikao, tunazungumza nao kwa kuandikiana na mapendekezo yao ndio tutakayowatumia hata wakati wa utengenezaji wa kanuni tutawashirikisha kwa sababu ni takwa letu kwamba twende pamoja, hakuna mtu anayetaka kumvizia mwenzie, tunachotaka ni wote tuwe kwenye boti moja ili tuweze kuimarisha sekta ya madini.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na nakushukuru kwa nafasi hii. (Makofi)