Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Khamis Mtumwa Ali (4 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. MTUMWA ALI KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia, aidha napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Kiwengwa kwa kunichagua kwa kura nyingi kuwa Mbunge wa Jimbo hili tiketi ya Chama cha Mapinduzi. Pia napenda kuwashukuru Watanzania kwa kumchagua Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, kuwa Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania na Mheshiimwa Dkt. Ali Mohamed Shein kuwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri, naomba niguse mambo mawili, matatu ambayo yamezungumzwa katika hotuba ya Upinzani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wapinzani katika hotuba yao wamezungumza kwamba wana hofu ya kuvunjika kwa Muungano, mimi napenda kusema kwamba hofu hii wataendelea kuwa nayo lakini Muungano huu hauvunjiki utaendelea kuwepo, kwa maslahi ya Watanzania wakiwemo Wazanzibari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kusema ukweli Muungano huu umeleta faida nyingi kwetu, wengine tunaozungumza hapa tumekuwepo kwa tiketi ya Muungano kama siyo Muungano maana yake tusingekuwemo humu na tusingefika hapa kuzungumza na kuchangia mambo mbalimbali ambayo yanahusu mustakabali wa nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wameendelea kusema eti Muungano huu unalindwa na CUF na Maalim Seif, kama siyo wao Muungano huu usingekuwepo. Nataka niwahakikishie kwamba, Muungano huu unalindwa na Watanzania wote, Watanzania wa Zanzibar na Watanzania wa Tanganyika ndiyo wanaoulinda Muungano huu, siyo Maalim Seif na wana-CUF. Kusema ukweli Upinzani Muungano huu hawautaki, iweje leo waulinde, sisi tutasema Serikali ya CCM ndiyo itaulinda Muungano huu na tutahakikisha kwamba unadumu kwa maslahi ya Tanzania na kwa maslahi ya Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba yao hii, wamezungumzia haki za binadamu, eti wamesema Serikali ya Muungano imeivamia Zanzibar kijeshi na Polisi kwenye uchaguzi wa marejeo. Hivi Zanzibar ina Serikali yake ivamiwe kijeshi kivipi, wao wanachotaka kufanya wanataka kufanya vurugu, lakini nafasi hiyo hawakuipata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nalipongeza Jeshi la Polisi na Jeshi la Wananchi wa Tanzania kwa kusimamia uchaguzi wa marudio, kurejewa kwa hali ya ukimya, hali nzuri ya ulinzi na usalama wa hali ya juu. Wananchi wote walipewa fursa ya kushiriki katika uchaguzi ule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wale ambao wamekataa wenyewe wasisingizie kwamba Zanzibar imevamiwa, waseme ukweli kwamba walishindwa kushiriki kwa sababu wanajua kwamba hawawezi kurejea katika uchaguzi ule kwa sababu CCM tutawashinda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, njama zao za kuiba kura tulizibaini na bahati nzuri Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar kupitia Jecha alwatan akafutilia mbali uchaguzi ule na hatima yake tukarudia uchaguzi ambao halali na hatimaye wameshindwa kuingia uwanjani wametia mpira kwapani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nawaambia zile pesa za posho na mshahara wanaopata wawasaidie wale wenzao waliouza mashamba yao ya mikarafuu kwa ajili ya kugombea baadaye wakakaa nyumbani wakaambiwa eti wapumzike sasa hivi wanajuta kwa nini hawakuingia katika uchaguzi ule. Iliyobaki ni kelele na kuwapa matumaini mabovu Wazanzibari kwamba kesho eti Jumuiya ya Madola itamtangaza Maalim Seif itakuja kumuapisha, yaguju. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wamekaa wanasema eti wapewe nafasi wapumue, sasa hivi ndiyo wakati mzuri tumeshawapa nafasi wapumue nje ya Serikali. Kwa sababu walikuwepo ndani ya Serikali hakuna walichokifanya, walikuwa wanaijejea Serikali, hawana maendeleo waliyoyaleta. Wamepewa Wizara ya Afya wameshindwa kuleta hizo huduma walizokuwa wanasema, maana walikuwa wanasema hata panadol hakuna, hatimaye wameshindwa kufanya hivyo. Kwa hiyo, hawa bora wakae nje waone sasa hivi Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein ikifanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze katika kutoa mawili, matatu kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Kwanza nampongeza kwa hotuba yake nzuri na mwonekano mzuri ambao aliusema hasa kwa nia ya kuyarekebisha yale mambo ambayo yanahusiana na Muungano yanayohusu masuala ya kifedha. Huu mgao wa fedha ni vyema sasa ukaangaliwa kwa makini.
MHE. MTUMWA KHAMIS ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mgao huu ukiangaliwa kwa makini utasaidia zaidi kudumisha Muungano wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika naomba nizungumzie Mfuko wa Jimbo. Mfuko huu unakuja Zanzibar kama ulivyo na ni vyema ukapangiwa utaratibu mzuri ili tuweze kuupata katika wakati mzuri kama wanavyoupata wenzetu huku Bara. Kwa sababu pesa zikifika kule zinakuwa zinachelewa, kwa hiyo, tunamuomba Mheshimiwa Waziri afuatilie na apange utaratibu mzuri wa fedha hizi ziweze kupatikana kwa wakati mzuri ili kuweza kuhakikisha maendeleo ya wananchi wetu yanapatikana kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ajira za Muungano, ni jambo muhimu sana kuangalia ajira hizi zinapatikana kwa usawa. Tukiwa tunapata ajira hizi kwa usawa hata wale vijana ambao wana mihemko na hawaelewi kuhusiana na suala la Muungano wataweza kuelewa. Ikiwa kuna utaratibu mzuri wa upatikanaji wa ajira hizi katika hizi taasisi za muungano itasaidia sana kuhakikisha kwamba Muungano wetu huu unadumu kwa sababu upungufu mdogo mdogo uliokuwepo ukifanyiwa kazi utaweza kusaidia kuhakikisha kwamba Muungano wetu huu unaimarika na unadumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mazingira, naomba nimpongeze Waziri kwa jitihada ambayo ameichukua kwa kuanza kwa kasi mpya kuhakikisha kwamba masuala ya mazingira yanafanyiwa kazi vizuri. Napongeza pia hatua anazozichukua sasa hivi kwa kutembelea Zanzibar kwa kwa kuwa Kisiwa cha Zanzibar…
MHE. MTUMWA KHAMIS ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. KHAMIS MTUMWA ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, muumba mbingu na ardhi kwa kuniwezesha kuwa mzima wa afya na kuweza kuchangia hotuba ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na Mama Samia Suluhu Hassan kwa kufanya kazi nzuri ya kusimamia Taifa letu hili. Pia napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanazozifanya katika kusimamia amani ya nchi hii. Kwa kweli bila amani hatuwezi kufanya jambo lolote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi linakabiliwa na changamoto mbalimbali nitaanza kuzungumzia makazi ya askari. Kwa kweli makazi ya askari ni duni sana pamoja na Mheshimiwa Waziri kuelezea kwamba wana mpango mzuri wa kujenga nyumba za askari. Hata hivyo, kiuhalisia ukiangalia zile nyumba za askari ambazo zipo hivi sasa zinatisha. Ukienda central tu hapo utakuta nyumba za askari zina mabati, ndani hazina ceiling board hata yule askari akinunua mayai akayaweka ndani baada ya wiki utaona yameshatoa watoto yaani zile nyumba zimegeuka incubator. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo hizo nyumba za askari zilizopo ambazo hazina hata ceiling board, zimejegwa kwa udongo ambapo siku za mvua ukipata maji zinaporomoka. Kwa kweli Mheshimiwa Waziri ni lazima aangalie hali hii kwani mazingira wanayoishi askari wetu si mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikifika wakati wa usiku baridi iliyokuwemo ndani ya nyumba zile ni kama wapo katika mafriji. Wale ni binadamu, wanataka nyumba nzuri ili waishi kama binadamu wengine ili waweze kufanya kazi vizuri. Naomba sana Serikali kupitia Wizara hii waweze kuangalia hizi nyumba wanazojenga na hizi ambazo zipo ili kuziboresha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuongelea posho za askari wetu hawa. Kwa kweli inasikitisha sana, askari wadogo hawapati posho stahiki na kwa wakati na hali hii inapelekea kuwa na imani potofu na duni. Ikiwa kama kuna matabaka ya kupata hizi posho stahiki au kucheleweshewa kupelekwa posho hizi kwa wakati itapelekea askari hawa kuvunjika moyo na hatimaye kutofanya kazi zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana hapa wakati wa bajeti tulimwambia Mheshimiwa Waziri kwamba askari wanalipia umeme kwenye mifuko yao wenyewe kutoka katika mishahara yao. Mheshimiwa Waziri akasema hili atalisimamia lakini inafika hatua wanastaafu pesa za umeme ambazo wametumia kutoka kwenye mifuko yako hawajalipwa hadi sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana sana Mheshimiwa Waziri na hili aliangalie aweze kuhakikisha askari hawa wanapewa posho zao straight kama ilivyo kwa Jeshi la Wananchi (JW). Kwa sababu wakipewa hivyo itapunguza malalamiko wakati wa kustaafu ya kutopewa posho au pesa ambazo wanazitumia kwa ajili ya kulipia nyumba au umeme. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja aweze kutuelezea vizuri mkakati huu kafikia wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie kuhusu mafunzo mbalimbali ya Jeshi la Polisi. Ni ukweIi usiopingika kwamba bila mafunzo Jeshi la Polisi haliwezi likafanya kazi vizuri. Ikiwa mafunzo haya yanatolewa kwa askari wa headquarter tu bila kuwashirikisha wale askari wadogo wadogo waliopo mikoani itakuwa ni vigumu askari hawa kufanya kazi kwa weledi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri aweze kuhakikisha kwamba askari wadogo nao wanakwenda mafunzo siyo waliopo headquarter tu mikoani mafunzo hamna, hivi sasa mafunzo yamepungua kabisa. Kama kutakuwa na upungufu wa bajeti basi Serikali ipeleke fedha kikamilifu ili mafunzo haya yaweze kupatikana vizuri zaidi kwa askari wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ujenzi wa Vituo vya Polisi kama alivyosema Mhesimiwa Raza pale vipo katika hali ngumu. Katika Jimbo langu kuna Kituo cha Polisi kimoja tu, unapotokea uhalifu inakuwa ni shida sana. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri kwamba katika Shehia yangu ya Kilombero tungepata Kituo kimoja cha Polisi kwa sababu anapotokea mhalifu inakuwa ni vigumu kumfikisha Kituo cha Mahonda ambapo ni mbali zaidi kutoka eneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri amekuja hapa akasema kwamba viatu vyake vizuri sana kuliko vya wengine, ni kweli. Hata hivyo, askari wake viatu wanavyotumia ni vile vya UN! Namwomba sana Mheshimiwa Waziri ajitahidi viatu vya askari wake viwe kama vyake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. KHAMIS MTUMWA ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuzungumza. Awali ya yote napenda kuchukua fursa hii kwanza kumshukuru kwanza Mwenyezi Mungu, muumba wa mbingu na ardhi, kwa kutuwezesha kuwa wazima wa afya na kuweza kusimama katika Bunge lako hili Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri ambayo anafanya ya kutuletea maendeleo katika Taifa letu na kusimamia amani ya nchi yetu hii. Kwa kweli Mheshimiwa Rais anastahiki pongezi sana tena sana kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kazi nzuri ambazo wanazifanya za kuweza kuhakikisha Taifa letu hili linasimama kwa amani na Jeshi la Polisi linatekeleza majukumu yake ipasavyo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri na IGP na Makamishna wote, hongera sana kwa kazi ambayo wanaifanya ya kuhakikisha kwamba Taifa letu linakuwa na amani sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia sasa kuhusiana na hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani katika kipengele cha hali ya usalama nchini. Katika taarifa yake ukurasa wa tano, Mheshimiwa Waziri amesema matukio ya uhalifu yamepungua na kutoka mwaka 2017 kutoka matukio ya 56,913 yamepungua hadi kufikia matukio 47236 mwaka 2018. Hongera sana kazi nzuri ambayo wanaifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kushauri zaidi kwamba ili matukio haya yapungue zaidi ni vyema sasa Mheshimiwa Waziri Wizara yake ikaendelea kuimarisha vifaa vya utendaji kazi katika Jeshi la Polisi na hasa kwenye kipengele cha mafuta ili kuhakikisha maeneo yote ambayo yanatokea matukio mbalimbali, Jeshi letu la askari la Polisi liweze kufika vizuri na kuweza kufanya kazi katika maeneo hayo ili kupunguza haya matukio yetu ya uhalifu ambayo yanaendelea kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kuchangia kuhusiana na suala la basic training za polisi. Hawa kuruta wanapofanya mazoezi wakati wapo katika training zao wanakimbia kwa kutumia viatu vya kiraia pamoja na tracksuit hizi za kiraia. Sasa unapofika wakati wa field yenyewe utamkuta askari amevaa lile bullet proof ambalo halipungui kilogramu 10 au amechukua mashine ya SMG isiyopungua kilogramu saba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni vyema hawa askari wakaweza ku-cope na haya mafunzo ambayo wanayapata. Kwenye mafunzo hawachukui hivi vifaa lakini kwenye field utakuta wanabeba hivi vifaa na utawakuta wamevaa mabuti na helment karibu masaa yote ya kazi wanatakiwa vifaa vile wawe navyo. Kwa kweli ili kuwajengea mazingira mazuri ya kuweza kupambana zaidi na kuweza kuzoea vile vifaa ambayo wanavitumia ni vyema wakati wa training vilevile waweze kupata hivyo vifaa ili waweze kufanya mazoezi vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile naomba nichangia kuhusiana na suala la ujenzi wa nyumba za askari na vituo vya polisi. Mwaka jana tumemwambia Mheshimiwa Waziri kwamba hizi nyumba za askari hasa katika iji letu hili la Dodoma zimakaa kama incubator ambapo ukapeleka mayai yako pale baada ya muda utapata vifaranga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni aibu kweli kwa sababu askari wetu wanafanya kazi nzuri, lakini wanapoenda kulala siku za joto inakuwa balaa, siku za baridi inakuwa balaa, maana yake juu kuna bati, pembeni kuna bati na chini kuna bati. Sasa kama mtu ana mke ana watoto sijui wanaishi katika mazingira gani katika nyumba zile ni vyema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni vema nyumba hizi tukazifanyia ukarabati zikaendana na hadhi ya Jiji la Dodoma. Pia nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kutenga zile bilioni 10 za kuhakikisha kwamba askari waweze kuishi vizuri na ningewaomba sana hizi nyumba 400 kila mkoa ambazo zimewekwa humu katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ziweze kuonekana kwa vitendo. Kwa sababu mwaka huu umetuambia nyumba 400 kila mkoa ningeomba sana mwakani nyumba tusije tukazizungumza tena hasa katika hili Jiji la Dodoma askari wetu kukaa kwenye nyumba za incubator za kuzalishia vifaranga vya kuku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, kuna suala la huduma za maji na umeme. Mwaka jana nilimshauri sana Mheshimiwa Waziri, hizi huduma ni bora wangekopi katika Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JW) wanafanyaje na wao wakachukua hizi wakafanya, kwa sababu huduma za maji na huduma za umeme kwa kweli ni gharama kwa askari mwenyewe kulipa. Imefika mahali miaka iliyopita wanafika askari wanastaafu wanakopesha pesa zao mfukoni kulipia huduma za maji na umeme katika vituo vya polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri askari wetu hawa pesa ambayo wanapata ni ndogo sana halafu pesa hiyo hiyo takribani huduma ya maji Mheshimiwa Waziri anaijua, haipungui shilingi 50,000 au 60,000 kwa mwezi na huduma ya umeme karibu 50,000 au 60,000. Ukiangalia mishahara yao ni midogo, kidogo linakuwa ni suala gumu zaidi kwa askari wetu hao. Naomba sana Mheshimiwa Waziri suala hili akalichukua akalifanyia kazi endapo mwakani akija atuambie kwamba amefanya kama JW wanavyofanya kuhusu suala la maji na suala la umeme kwenye huduma hizi za malipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala pia la uniform, askari wetu wananunua wenyewe, ni nadra sana kupewa viatu bure kama ulivyokuwa unavaa wewe, ni nadra sana kupewa hizi uniform bure kama ambavyo wanavyopata kwa mgao ambao wanapopewa mara nyingi wanakuwa wanatumia pesa zao za mshahara sasa kujinunulia hivi vifaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri amezungumza vizuri tu kwenye hotuba yake, kuna viwanda ambavyo vinatengeneza viatu na kuna viwanda ambavyo vinatengeneza nguo. Naomba sana Mheshimiwa Waziri hili alibebe ili sasa migao itakapotoka itoke kwa wakati na nguo hizi na vifaa wasiwe wananunua wenyewe waweze kununuliwa na jeshi letu la polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mishahara na posho za askari nalo hili imekuwa ni shida sana, ningeomba sana Mheshimiwa Waziri aziangalie kama alivyosema kwenye maelezo yake wakati anahutubia hapa, kwamba yale masuala madogo madogo amezungumza nao. Mwakani naamini yale masuala madogomadogo hatosema amezungumza nao atakuja hapa atatuambia masuala madogo madogo tulishamalizana nao ili na wao waweze kufanya kazi vizuri kama Jeshi letu la Polisi ambao wanatulinda sisi tunalala kwa amani, wao wanapata shida, lakini mishahara yao bado na hali zao za mambo madogo madogo ambayo yapo zinakuwa vilevile zipo katika hali ngumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri suala hili alichukue serious kweli kwa sababu wenzetu hawa wanafanya kazi kubwa sana ya kulinda amani ya nchi yetu lakini posho zao na maslahi yao yanakuwa na shida. Hata wenzangu wamezungumza kuhusiana na suala la askari anapandishwa cheo anakaa miaka chungu mzima hapati matunda ya kile cheo ambacho anakipata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri na namwelewa utendaji wake mzuri na Mheshimiwa Naibu Waziri watalizingatia hili, tuone sasa haya madeni ambayo askari anadaiwa yakamilike na hayo mambo mengine mazuri yapatikane vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala pia katika Kitengo cha Upelelezi, Mheshimiwa Waziri upelelezi hauwezi ukafanyika bila fedha, lazima zipatikane fedha, hawa askari wetu waweze kufanya upelelezi vizuri, vinginevyo kitengo hiki kitakufa kabisa. Information is money, huwezi ukaenda kwa mtu ukamwambia akupe taarifa au uka-collect information bila kuwa na fedha, lazima uwe na pesa kidogo umpatie maji ya kunywa kidogo, umpatie mtu kidogo vitu fulani ili aweze na yeye kumtengeneza ili akupe information Mheshimiwa Naibu Waziri anajua sana kazi hizi wameshazifanya sana wanazielewa. Kwa hiyo, nawauomba sana Kitengo hiki cha Upelelezi ili kiweze kufanya kazi vizuri…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. KHAMIS MTUMWA ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie Wizara hii ya Muungano na Mazingira. Pia naomba nichukue fursa hi kumpongeza kwa dhati kabisa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Rais wa Zanzibar Dkt. Ali Mohamed Shein kwa kuhakikisha kwamba wanaulinda, kuuhifadhi na kuutetea muungano wetu huu mpaka sasa unafika miaka 55. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Waziri Mkuu na Makamu wa Rais kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuhakikisha kwamba wanazikusanya kero hizi za Muungano na kuweza kuzifanyiakazi hatua baada ya hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wake pamoja na Katibu Mkuu kwa kuweza kuzichanganua na kuzitafuta kero hizi na hatimaye tunaona matokeo yake ya kuweza kutatuliwa moja hadi moja kwa kadri ya siku zinavyokwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze sasa kwenye suala zima la umuhimu wa Muungano wetu. Muungano wetu huu ni wa historia na unatusaidia sana pande zote mbili ya Tanzania Bara na ya Zanzibar na hasa kwenye suala zima la kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia mambo mbalimbali ya kibiashara yanafanyika pande mbili hizi na watu hunufaika, lakini bado kuna kikwazo kikubwa cha kufanya double taxation ambayo inafanyika Zanzibar ukipeleka kitu ukileta Tanzania Bara ulipie tena ushuru mara ya pili. Hii bado ni kero na tunaipigia kelele sana na Wabunge wengi wa Zanzibar wanaipigia kelele hii kwa sababu bado inaonekana haitendi haki kwa pande zote mbili za Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kuzungumza kuhusiana na suala la ushiriki na ushirikiano mdogo kuhusu masuala ya Kitaifa na kikanda. Kama Mheshimiwa Waziri alivyoelezea katika kitabu chake hiki, amefanya juhudi za kuunda Kamati ya kuweza kuhakikisha kwamba changamoto hizi zinafanyiwa kazi za kielimu, nafasi za masomo na vilevile amezungumza kuhusiana na suala la utafutaji wa fedha kwa masuala ya mambo ya nje ya misaada na mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile ametuambia masuala mbalimbali yameundiwa Kamati ambayo atahakikisha kwamba soon tunaona matokeo yake. Napenda sana kumshauri Mheshimiwa Waziri tutakapokuja kwenye bajeti ya mwakani, changamoto hizi tusiwe tunazirejea tena kila siku katika Bunge letu hili Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nizungumzie kuhusiana na suala la Elimu ya Muungano. Wenzangu wametangulia kusema kwamba ipo haja ya kutoa taaluma kwa yale ambayo yanatatuliwa katika Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusiana na zile kero za Muungano, kwa sababu vijana wanaoamkia sasa hivi bado wana mentality kichwani kwamba Muungano siyo mzuri, au unatunyonya sana kule Zanzibar. Kiukweli Muungano una faida kubwa sana za kiuchumi, kisiasa na kijamii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kukiwa na utoaji wa elimu katika maeneo mbalimbali hasa kule Zanzibar juu ya changamoto ambazo zinatatuliwa na umuhimu wa Muungano wetu, mimi nina imani kwamba muungano huu utazidi kudumu zaidi ya miaka 100 badala ya miaka 55 hii tuliyofikia sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kuzungumzia suala la ushirikiano kuhusiana na masuala mbalimbali ya Muungano hasa katika Taasisi hizi za ukaguzi. Tumeshuhudia kwamba Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu (CAG) hufanya ukaguzi katika Taasisi mbalimbali au katika Taasisi za Ubalozi bila kushirikiana na Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu Zanzibar. Suala hili tumeshalizungumza sana kwamba wale wenzao ni vyema kwamba wakashirikiana nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, madhali hili suala siyo la Muungano lakini ni vyema zaidi wakaenda kukagua katika Taasisi za Muungano ambazo zipo nje hasa Ubalozi wawashirikishe na wenzetu kule ili wapate exposure na mambo mengine ambayo wataweza kujifunza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri aliniahidi siku moja kwamba tutafuatana mimi naye twende kule Zanzibar, tuone, tukae na Taasisi ambayo inahusiana na Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi kuangalia zile changamoto zao ambazo zinawakabili, lakini alitingwa na kazi. Naamini baada ya Bunge hili au baada ya kujibu hoja zetu hizi tutafuatana ili tuone tatizo hili pia linatatuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Mheshimiwa Waziri; baada ya kauli ya Meshimiwa Waziri Mkuu kusema kwamba ikifiuka tarehe 1 Juni, 2019 suala la mifuko ya plastic ni marukufu, Mheshimiwa Waziri na Naibu wake na Katibu Mkuu wake wamefanya jitihada ya haraka kuonana na wadau na kuweza kuzungumzia mambo mbalimbali ambayo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante kwa mchango mzuri. Mheshimiwa Juma Kombo, ajiandae Mheshimiwa Mtolea.

MHE. KHAMIS MTUMWA ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)