Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Livingstone Joseph Lusinde (11 total)

MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE aliuliza:-
Mradi wa Maji wa Kijiji cha Manzase ulishalipiwa nusu ya gharama za mradi na Uongozi wa Serikali ya Awamu ya Nne.
(a) Je, Serikali ya Awamu ya Tano ina Mpango gani kuukamilisha ili wananchi wa Kijiji hicho wapate huduma ya maji safi na salama;
(b) Kijiji cha Chinoje kilipata Mradi wa World Bank na kuchimbwa visima 10 lakini maji hayakupatikana. Je, Serikali ina Mpango gani?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Livingstone Joseph Lusinde, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutekeleza Miradi ya Maji ya Vijiji Kumi kwa kila Halmashauri, Halmashauri ya Chamwino inatekeleza miradi kwenye vijiji saba ambapo miradi katika Vijiji vitano vya Mvumi Makulu, Itiso, Mvumi Mission, Chamuhumba na Membe imekamilika na wananchi wapatao 49,000 wanapata huduma ya maji. Mradi wa Wilunze unaendelea kutekelezwa na upo asilimia 60.
Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa mradi wa maji katika Kijiji cha Manzase umefikia asilimia 40. Kazi zilizofanyika hadi sasa ni ujenzi wa vituo 11 vya kuchotea maji, ujenzi wa nyumba ya mashine na ujenzi wa tanki lenye ujazo wa lita 80,000. Gharama ya ujenzi wa mradi ni shilingi milioni 355, ambapo hadi sasa kiasi cha shilingi milioni 71 kimeshapelekwa kwenye Halmashauri hiyo kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huu. Serikali itaendelea kupeleka fedha ili kukamilisha mradi huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji katika Kijiji cha Chinoje ni kati ya miradi iliyokosa chanzo cha maji wakati wa utekelezaji wa awamu ya kwanza ya Program ya Maendeleo ya Maji. Utafiti wa chanzo kingine cha maji unafanyika na ujenzi wa mradi utafanyika katika mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE aliuliza:-
Rais wa Awamu ya Nne alipotembelea Jimbo la Mtera katika Kijiji cha Mvumi-Misheni aliahidi kutujengea barabara ya lami kutoka Mlowa Barabarani hadi Mvumi-Misheni kwenye Hospitali Teule ya Wilaya ya Chamwino. Pia Rais wa Awamu ya Tano katika kampeni zake alipofika Mvumi-Misheni alisisitiza kuwa barabara hiyo itajengwa haraka iwezekanavyo. Je, ujenzi huo utaanza lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Livingstone Joseph Lusinde, Mbunge wa Mtera, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Rais wa Awamu ya Nne alipotembelea Jimbo la Mtera katika Kijiji cha Mvumi – Misheni aliahidi kujenga barabara ya lami kutoka Mlowa Barabarani hadi Mvumi- Misheni kwenye Hospitali Teule ya Wilaya ya Chamwino. Aidha, ni kweli kuwa wakati wa Kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, Rais wa Awamu ya Tano, naye aliahidi kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumfahamisha Mheshimiwa Mbunge kuwa, Serikali inatambua umuhimu wa barabara hii kwa jamii na hususan katika kusaidia wagonjwa wanaoenda kupata huduma ya matibabu katika Hospitali ya Mvumi Misheni.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia umuhimu huo, azma ya Serikali ya kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami iko pale pale na itatekelezwa kulingana na upatikanaji wa fedha. Kwa sasa barabara hiyo itaendelea kuhudumiwa na Serikali kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kufanya matengenezo ya aina mbalimbali kwa kiwango cha changarawe kwa kutumia fedha za Mfuko wa Barabara ili iendelee kupitika majira yote ya mwaka.
MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE aliuliza:-
Upo mradi wa kilimo cha umwagiliaji katika Kijiji cha Mpwayungu kwa jina maarufu Mgangalenga wa muda mrefu na Serikali imegharamia fedha nyingi sana.
Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha mradi huo ili wananchi waweze kunufaika nao?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Livingstone Joseph Lusinde, Mbunge wa Mtera, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, scheme ya umwagiliaji ya Mpwayungu ilijengwa kupitia Mradi Shirikishi wa Kuendeleza Kilimo cha Umwagiliaji (PIDP) mwaka 2005/2006. Ujenzi wa scheme hii ulihusisha ujenzi wa banio na kuchimba mifereji ya kufikisha maji mashambani. Scheme hii ina eneo linalofaa kwa kilimo cha umwagiliaji lenye hekta 160. Eneo lililoendelezwa kwa kufikiwa na mifereji ya udongo linafika hekta 140 ambalo ni kwa ajili ya kilimo cha mpunga lakini kwa sasa eneo linalotumika ni chini ya hekta 25. Kwa sasa Serikali inaendelea na juhudi za kuhamasisha wakulima kulitumia eneo hilo ambalo limeshaendelezwa kwa kilimo cha umwagiliaji.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Tume ya Umwagiliaji itafanya mapitio ya usanifu wa mradi huu katika mwaka wa fedha 2016/2017 kwa nia ya kuongeza ufanisi wake.
MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE aliuliza:-
Rais wa Awamu ya Nne alipotembelea Jimbo la Mtera katika kijiji cha Mvumi Misheni aliahidi kutujengea barabara ya lami kutoka Mlowa barabarani hadi Mvumi Misheni kwenye Hospital Teule ya Wilaya ya Chamwino. Pia Rais wa Awamu ya Tano katika kampeni zake alipofika Mvumi Misheni alisisitiza kuwa barabara hiyo itajengwa haraka iwezekanavyo.
Je, ujenzi huo utaanza lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimwa Livingstone Joseph Lusinde, Mbunge wa Mtera kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa Rais wa Awamu ya Nne alipotembelea Jimbo la Mtera katika Kijiji cha Mvumi Misheni aliahidi kujenga barabara ya lami kutoka Mlowa barabarani hadi Mvumi Misheni kwenye Hospitali Teule ya Wilaya ya Chamwino. Aidha, ni kweli kuwa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, Rais wa Awamu ya Tano naye aliahidi kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumfahamisha Mheshimwa Mbunge kuwa Serikali inatambua umuhimu wa barabara hii kwa jamii na hususan katika kusaidia wagonjwa wanaoenda kupata huduma ya matibabu katika hospitali ya Mvumi Misheni. Kwa kuzingatia umuhimu huo, azma ya Serikali ya kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami iko pale pale na itatekelezwa kulingana na upatikanaji wa fedha. Aidha, kwa sasa barabara hiyo itaendelea kuhudumiwa na Serikali kupitia Ofisi ya Rais - TAMISEMI kwa kufanya matengenezo ya aina mbalimbali kwa kiwango cha changarawe kwa kutumia fedha za Mfuko wa Barabara ili iendelee kupitika majira yote ya mwaka.
MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE aliuliza:-
Serikali iliunda chombo kinachosimamia barabara za Vijijini na Mijini kinachoitwa TARURA:-
Je, chombo hicho kitaanza lini kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa kwani barabara hizi ni mbaya sana hasa wakati wa masika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Livingstone Joseph Lusinde, Mbunge wa Mtera, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) ilianzishwa kwa Sheria za Wakala za Serikali, Sura 445 na kutangazwa katika Gazeti la Serikali Na. 211 la tarehe 12 Mei, 2017. TARURA imeanza rasmi tarehe Mosi Julai, 2017, kwa ajili ya utekelezaji wa matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilometa 108,946.2 katika mwaka wa fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Naibu Spika, TARURA imeidhinishiwa shilingi bilioni 230.8 kwa ajili ya matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilometa 34,024. Kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 98.5 zimetolewa na kutumika kujenga barabara zenye urefu wa kilometa 4,188.31, madaraja 35, makaravati makubwa 43 na makaravati madogo 364.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018, barabara zilizojengwa katika Jimbo la Mtera zina urefu wa kilometa 93.3 kwa gharama ya Sh.356,737,115.80. Barabara hizo ni:-
Handali – Chanhumba – Igandu - Nghahalezi (kilometa nne); Nghahalezi – Miganda – Idifu - Iringa Mvumi - Mlowa barabarani (kilometa tano); na Nagulomwitikila - Huzi - Ilangali (kilometa 17) kwenda Nhinhi - Wiliko (kilometa 20); Mlowa barabarani - Makangw’a (kilometa 12); Manzase – Sasajila - Ilowelo (kilometa 21.3); Chipogolo - Loje - Igungili (kilometa 14). Wakandarasi wanaendelea kufanyakazi na wanatarajia kukamilisha kazi hiyo Mei, 2018.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2018/2019, TARURA imeomba kutengewa kiasi cha shilingi bilioni 243.3 kwa ajili ya ujenzi wa barabara zenye urefu wa kilometa 23,465.05, ukarabati wa madaraja 117, mifereji ya mvua yenye urefu wa mita 67,844 na makaravati 1,881 kwa nchi nzima.
MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani juu ya wanyama waharibifu hususan tembo ambao wamesambaa hovyo katika Jimbo la Mtera na kufanya uharibifu mkubwa pamoja na kuua watu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii napenda kujibu swali la Mheshimiwa Livingstone Joseph Lusinde, Mbunge wa Jimbo la Mtera kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la wanyamapori wakali na waharibifu limekuwa likijitokeza kwenye Wilaya zaidi ya 80 hapa nchini. Wanyamapori wakali na waharibifu ambao kwa kiwango kikubwa wamekuwa wakileta madhara kwa maisha ya binadamu na uharibifu wa mazao yao kisheria ni tembo, mamba, nyati, kiboko, simba, fisi na faru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ongezeko la watu limesababisha kuzibwa kwa shoroba za wanyamapori pamoja na maeneo ya mazalia na mtawanyiko wao. Kuzibwa kwa shoroba hizo kumeongeza migogoro baina ya binadamu na wanyamapori. Hali hiyo kwa ujumla wake imeongeza ukubwa wa tatizo la mwingiliano kati ya binadamu na wanyamapori hususan tembo na hivyo kusababisha matukio mengi ya uharibifu wa mali na upotevu wa maisha ya binadamu katika maeneo mbalimbali likiwemo Jimbo la Mtera.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukabiliana na changamoto hiyo, Serikali itaendelea kufanya doria za kudhiti wanyamapori katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Chamwino. Pia Wizara itaendelea kutoa elimu ya njia nyingine za kudhibiti tembo zikiwemo matumizi ya mizinga ya nyuki, uzio wa kamba uliopakwa mchanganyiko wa pilipili na oil chafu kuzunguka mashamba na kuchoma matofali ya kinyesi cha tembo kilichochanganywa na pilipili. Moshi unaotokana na uchomaji wa matofali ya kinyesi chenye pilipili ni mkali na hivyo hufukuza tembo mashambani kwa mafanikio makubwa. Njia hizi mbadala zimeonesha mafanikio makubwa pale zinapotumika vizuri na kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na mikakati hiyo, Serikali itaendelea kutoa fedha za kifuta jasho kwa uharibifu wa mali, yaani mazao na mifugo na kifuta machozi kwa wahanga waliouwawa au kujeruhiwa na wanyamapori hao. Kwa mfano, mwaka wa fedha 2017/2018 Wizara yangu imelipa jumla ya shilingi 7,520,000 kwa wananchi 27 wa Wilaya ya Chamwino walioathirika na wanyamapori.
MHE. OMARY A. BADWEL (K.n.y. MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE) aliuliza:-
Je, ni lini barabara ya kutoka Mpunguzi kupitia Nagula, Mpwajungu, Ituzi hadi Ilangali itapandishwa hadhi kuwa ya Mkoa ambayo itasimamiwa na Mkoa kwa maana ya TANROADS?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Livingstone Joseph Lusinde, Mbunge wa Jimbo la Mtera, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ya Mpunguzi – Ilangali yenye urefu wa kilometa 88.3 ni barabara mjazo yenye tabaka la changarawe na udongo, ambayo inaunganisha Wilaya ya Dodoma, Bahi, Chamwino na kwa upande mwingine inaunganisha Mkoa wa Dodoma na Mkoa wa Iringa, Wilaya ya Iringa Vijijini. Upande wa Dodoma Jiji ina kilometa tatu, Bahi kilometa 18.3 na Chamwino kilometa 67.
Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, Serikali ilitengeneza sehemu ya Mpunguzi hadi Nagulo kwa kiwango cha changarawe yenye urefu wa kilometa 21.3 kwa gharama ya shilingi bilioni 3.032 katika mwaka wa fedha 2015/2016 kwa ufadhili wa DFID. Aidha, barabara ya Mpunguzi – Ilangali katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali kupitia TARURA iliifanyia matengenezo ya sehemu korofi kwa urefu wa kilometa 17 yaliyogharimu shilingi milioni 86.2 na katika mwaka wa fedha 2018/2019, TARURA Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino imetenga shilingi milioni 170 za kuifanyia matengenezo ya muda maalumu kwa urefu wa kilometa 8.5 na kazi hii ipo katika hatua za manunuzi.
Mheshimiwa Spika, maombi ya kupandishwa hadhi barabara ya Mpunguzi – Ilangali kwa sasa yapo ngazi ya Mkoa. Pindi yatakapowasilishwa kwa Waziri mwenye dhamana na kuonekana kwamba yanakidhi vigezo vilivyowekwa na sheria, barabara hii itapandishwa hadhi.
MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE aliuliza:-

Wakazi wa Kitongoji cha Mafulungu kilichopo katika Kijiji cha Ilangali, Kata ya Manda wanajishuhgulisha na uchimbaji wa madini.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwawezesha wakazi hao ili shughuli zao za uchimbaji ziwe za ufanisi na zenye tija?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, naomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Livingstone Lusinde, Mbunge wa Mtera, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kata ya Manda, Kijiji cha Ilangali, Kitongoji cha Mafulungu, Wizara ilishatoa leseni 16 za wachimbaji wadogo wa madini ya jasi (gypsum) zilizotolewa kuanzia mwaka 2014 hadi 2016. Hadi sasa Tume ya Madini imepokea maombi 32 ya leseni za uchimbaji mdogo wa madini ya jasi kutoka katika eneo hilo. Maombi 16 yapo katika hatua za mwisho za kutolewa leseni na maombi 16 bado hayajakamilisha vigezo vya kupatiwa leseni.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuwahamasisha wakazi wa Mafulungu kujishughulisha na uchimbaji wa madini sambamba na kutunza kumbukumbu za uzalishaji na mauzo ili waweze kuaminika na kukopeshwa na taasisi za fedha. Aidha, nawashauri wachangamkie fursa ya uwepo wa madini hayo katika kitongoji chao kwani mahitaji yake ni makubwa hasa katika viwanda vya saruji nchini na nchi za nje baada ya Serikali kuzuia uingizaji wa madini hayo kutoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Madini inaendelea kutoa elimu kwa wamiliki wa leseni kuhusu uchimbaji bora wa madini ya jasi na kuwataka kuchangia miradi ya maendeleo katika jamii kwenye maeneo yanayowazunguka katika migodi yaani kwa maana ya Corporate Social Responsibility kwani ni takwa la kisheria kama inavyoelekezwa katika kifungu cha 105 cha Sheria ya Madini ya mwaka 2010 kama ilivyorekebishwa mwaka 2017.
MHE. FELISTER A. BURA (K.n.y. MHE. LIVINGSTON J. LUSINDE) aliuliza:-

Kwa kuwa Serikali imehamia Dodoma, je, kwa nini Serikali isijenge Maktaba yenye kumbukumbu za kazi za Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambayo pia itakuwa sehemu ya utalii kwa watu wa ndani na nje ya Mkoa wa Dodoma?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, napenda kjibu swali na Mheshimiwa Livingstone Lusinde, Mbunge wa Mtera, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kuzingatia umuhimu wa kuhifadhi kumbukumbu za Waasisi wa Taifa ambao ni Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Hayati Abeid Aman Karume, ilitunga Sheria ya Kuwaenzi Waasisi ya mwaka 2004. Sheria hii inaelekeza uhifadhi wa kumbukumbu hizo na kuanzishwa kwa kituo cha kutunza kumbukumbu. Aidha, Umoja wa Afrika uliiteua Tanzania mwaka 2011 kuwa Mratibu wa Programu ya Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika ambayo, pamoja na mambo mengine, imetoa kipaumbele katika uhifadhi wa kazi ambazo alifanya Baba wa Taifa na mashujaa wenzake katika ukombozi wa Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni katika msingi huo Serikali kwa kushirikiana na UNESCO, imekarabati studio za iliyokuwa Redio Tanzania Dar es Salaam zilizopo barabara ya Nyerere na kuwa kituo adhimu cha kuhifadhi na rejea ya kazi za Baba wa Taifa. Serikali vilevile, inaunga mkono juhudi za taasisi kadhaa nchini katika kuhifadhi amali za urithi wa kumbukumbu za Baba wa Taifa. Baadhi ya taasisi hizo ni kama ifutavyo:-

Maktaba ya Taifa, Dar es Salaam; Makumbusho ya Taifa, Dar es Salaam; Makumbusho ya Mwalimu Nyerere, Butiama; Ofisi ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa; Taasisi ya Mwalimu Nyerere; na Vituo vya Television vya TBC na ITV.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji wa Programu ya Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika, Serikali imeteua Wilaya ya Kongwa, Dodoma kuwa Kituo Kikuu cha Kumbukumbu za Ukombozi wa Nchi yetu ambapo miundombinu kadhaa ya uhifadhi wa historia itajengwa zikiwemo kazi adhimu za Baba wa Taifa. Ahsante.
MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE aliuliza:-

Je, ni lini barabara ya Mvumi Mission itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Livingstone Lusinde, Mbunge wa Mtera kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mfuko wa Barabara wa mwaka wa fedha 2019/2020 imetenga kiasi cha shilingi milioni 375 kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Mvumi Mission kwa kipande chenye urefu wa kilometa moja kwa kiwango cha lami. Maandalizi ya ujenzi yameshaanza na ujenzi unatarajia kukamika ifikapo mwezi Agosti, 2020.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kujenga na kuboresha miundombinu ya barabara na madaraja katika Jimbo la Mtera kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Ahsante.
MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga kituo kikubwa cha polisi katika Jimbo la Mtera hususani katika Kijiji cha Mvumi Misheni ili kukabiliana na wimbi kubwa la uhalifu katika Jimbo la Mtera?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Livingstone Lusinde, Mbunge wa Mtera kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, maeneo mengi ya vijijini nchini yameongezeka idadi ya watu, shughuli zao za kiuchumi na mambo mengine ambayo yanahitaji huduma ya ulinzi na usalama toka Jeshi la Polisi ikiwa ni pamoja na Kijiji cha Mvumi Misheni.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi inao mpango wa kuboresha na kujenga Vituo vya Polisi katika ngazi ya Tarafa na Kata nchi nzima ambavyo vitasaidia kusogeza huduma kwa wananchi hadi waliopo katika maeneo ya vijijini ikiwemo Kijiji cha Mvumi Misheni katika Jimbo la Mtera.