Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Yussuf Salim Hussein (27 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na mimi kupata nafasi kwa siku ya leo kuchangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu na mimi kuweza kusimama kwa mara ya kwanza leo kuchangia katika bajeti ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Mimi sitaki nikupongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri nataka nikupe pole, mzigo huu ni mkubwa na nadhani Serikali ya Chama cha Mapinduzi hamjajipanga katika kutekeleza na kuwatumikia Watanzania ipasavyo katika suala hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo, mifugo na uvuvi imebeba sehemu kubwa kama siyo yote ya maisha ya Watanzania. Watanzania wote utawakuta asilimia kubwa wanaogelea katika taasisi hizi tatu. Kwa hiyo, sidhani kama mmejipanga vya kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba Serikali nzima kutokuwa na vision tunakwenda wapi ndiyo tatizo ambalo linapelekea kilimo chetu na masuala yetu yote ndani ya nchi hii hatufikii pale ambapo tunakusudia na inakuwa ni ubabaishaji tu. Hatuna vision tunataka kulima nini, tulime wapi, tupeleke wapi na kwa namna ipi, hakuna!
Kwa hiyo, unakuta Rais anayekuja ana mipango yake katika kichwa, Waziri anayemweka ana mipango yake katika kichwa, hatuna vision ambayo kama nchi tumepanga kwamba tunataka kulima kitu hiki ili tukipeleke kwenye kiwanda hiki au tusafirishe, hakuna hiyo vision. Ni kila anayekuja, anakuja na mawazo yake na fikra yake ndio maana ndugu ni kawapa pole.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama hatuna vision, tunataka kulima nini, tulime wapi, tuelekee wapi, hatuwezi kupata maendeleo ya kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni mipango ya Serikali si mipango ya kifamilia, si mipango ya mtu binafsi, lazima tuwe na vision, tuwe na mpango ambao tumejipanga. Hatuwezi kupata mafanikio ya Kitaifa kwa miaka miwili au mitatu yakaweza kuonekana, hii siyo sunsumia bwana. Kuendesha Serikali ni lazima watu wajipange, wawe na vision ili mafanikio yale yataonekana baada ya miaka 10, 15 lakini kwa mfumo huu hatuwezi kwenda na itakuwa kila siku tunacheza chakacha tu hapa. Ni lazima tuwe na vision ambayo itakuwa inatuonesha tunataka kwenda wapi, kila Rais na Waziri ajaye awe anaelekeza nguvu zetu hapo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2013/2014 nchi hii imevuna mahindi mengi sana. Natoa mfano wa kuthibitisha kwamba Serikali haina vision. Kila ukipita humo mikoani unakuta rumbesa za mahidi yamefunikwa maturubai kwa sababu Serikali haikuwa na mpango, haikujipanga mvua ikanyesha mahindi yale yakaharibika yote. Mwaka jana tayari nchi hii unasikia baadhi ya mikoa ina njaa, kwa nini ni kwa sababu hatukujipanga. Hebu kama Serikali kaeni mjipange tunataka kulima nini, kwa wakati gani, tupeleke wapi, tuuze wapi? Tukifanya hivyo tutakuwa tumefanikiwa na haya maendeleo tunayoyazungumza leo kutoka hapa kwenda kwenye uchumi wa kati yataonekana vinginevyo itakuwa tunakata viuno tu hapa. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee suala la pili la mifugo. Nchi ya Tanzania imebahatika kuwa na mifugo mingi zaidi ya wananchi wake, lakini tukijiuliza hii mifugo imetusaidia nini, imetupeleka wapi, imesaidia nini katika Pato la Taifa? Matokeo yake badala ya kutupa mafaniko chanya inatupa mafanikio hasi. Leo wananchi kwa wananchi wenyewe kwa wenyewe Watanzania wanapigana kwa sababu ya mifugo yao, kwa sababu ya kilimo chao. Leo wafugaji wanaonekana kama ni maadui ndani ya nchi hii, leo wafugaji mifugo yao haijawasaidia chochote, haijawanufaisha chochote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu Serikali basi ituambie ni mkakati gani wa muda mrefu ambao imepanga ili kuweza kuona kwamba mifugo hii, tena hapa ametaja vizuri tu katika ukurasa wa kumi idadi ya mifugo ile ambayo inamilikiwa na watu tu inazidi idadi ya Watanzania mbali ya hiyo ambayo ipo katika mapori. Sasa itatusaidiaje au sisi tunalewa sifa tu kwamba Tanzania ni nchi ya tatu katika Bara la Afrika kuwa na mifugo mingi lakini inatusaidia nini, tumejipanga vipi? Kwa hiyo, sisi ni sifa tu Watanzania tupo hivi na hivi. Akili za kupanga mapinduzi ya kupindua Serikali ya Zanzibar ya wananchi mnayo lakini akili ya kukaa mkapanga sasa namna gani tutumie rasilimali hii Mwenyezi Mungu aliyotupa ili tuwaletee wananchi wetu maendeleo hiyo hakuna, ni ubabaishaji tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hii ambayo unatupa mwaka huu na mwakani kipindi kijacho cha bajeti utakuja kutupa taarifa hii. Hata hivyo, tuseme ukweli kama bajeti iliyotengwa kwa Wizara ya Kilimo wanapewa asilimia 38 tunategemea nini? Tusitegemee kitu chochote kwa sababu asilimia 38 hawawezi hawa kutekeleza majukumu yao, kwa hiyo, atakuja hapa iwe sababu yake sikuwa na bajeti na kweli tutamlaumu nini? Hebu tuacheni kuongeza kimo kwa kinu tupange bajeti kulingana na ule uwezo ambao tunao halafu tumkamate Waziri tumekupa kiasi hiki na hukuweza kufikia yale malengo. Leo unampa asilimia 38, kwa hiyo, badala ya kufanya kazi unampa mzigo sasa wa kufikiri atumie vipi kiwango kile kidogo cha pesa uliyompa kwa ajili ya kufanikisha majukumu yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa sekta ya uvuvi, hapa ndipo kwenye mtihani mkubwa. Waziri hapa katika hotuba yake amesema nchi ambayo inatarajiwa angalau tuwe na wavuvi milioni mbili tuna wavuvi laki moja, hatujaitumia hata kidogo sekta ya uvuvi, bahari kuu hatujaitumia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya 2013/2014, Waziri alisema kwamba wamezalisha vifaranga vya samaki milioni 20 na hivyo ndivyo vitagawanywa kwa wakulima ili iwe ni kichocheo cha kuongeza samaki. Vifaranga milioni 20 Tanzania, haitoshi hata mboga ya siku moja, kweli Serikali mpo serious kwamba mnataka kuongeza samaki? Mwaka uliofuata mwaka jana hajatuambia hivyo vifaranga milioni ishirini vingapi vimepona, vingapi vimekufa na imepatikana faida gani. Kwa hiyo, hakuna kitu chochote ni usanii tu ambao unapita hapa tunapigana usanii, tunakuja hapa tunajidanganya, tunawadanganya na Watanzania kuona kwamba tuna bajeti ya trillions of money lakini mwisho wa mwaka faida hakuna. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunazungumzia kwamba kuna uvuvi haramu, tumefanya nini sasa kukomesha uvuvi haramu, unapiga nyavu moto. Hawa wavuvi umewasaidiaje, umewapa elimu gani na umewapa mbadala gani? Je, ni nani kaingiza hizo bidhaa, zimepita wapi, zimelipiwa kodi au hazikulipiwa? Tumlaumu nani, are you serious Serikali ya CCM? Hamjawa serious jamani, hebu kuweni serious halafu tuone baada ya miaka mitano, kumi tutayazungumza haya? Sasa wapinzani tunaposema tunasema kwa sababu tuna uchungu, tunaumia na ndiyo maana tunasema hebu kaeni pembeni tuwaonyeshe namna gani Serikali inaendeshwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukosefu wa vifaa, huwezi kwenda kuvua katika bahari kuu na kidau, lazima…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)
Azimio la Bunge la Kuridhia Makubaliano ya Paris chini ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie katika azimio hili lililopo mbele yetu.

Kwanza nisikitike tu kwamba Azimio lenyewe ni kubwa sana na kwa lilivyopangwa na litakavyojadiliwa sioni kama tumelipa thamani hiyo au uzito huo ambao inalo. Ni kitu kikubwa sana na ndiyo kinagusa maisha yetu sasa kujadiliwa hapa kwa siku moja sidhani kama tunalipa uzito huo, naomba tulipe uzito sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Azimio hili nasema linagusa maisha yetu kwa sababu gani? Wamezungumza hapa katika paragraph ya nne kwamba kuna kupotea, sasa nitazungumza hii habari ya kupotea kwa visiwa na maeneo ya namna hiyo, sea erosion.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuna upoteaji mkubwa sana, lakini siyo kwamba vile visiwa vinaisha tu au ardhi inamegwa na bahari kwa sababu ya nguvu ya maji, hatuishii hapo tu lakini kuna na viumbe vinapotea ambavyo vimo katika vile visiwa au katika bahari na vikiendelea kupotea viumbe na mimea ndiyo na sisi maisha yetu yanapotea vilevile.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitatoa mifano michache tu, kuna miti ambayo inapotea kwa kasi kubwa sana, xylocarpus moluccensis na xylocarpus granatum hii ni mitonga, mtonga mweusi na mtonga mwekundu inapotea sasa ikipotea hiyo ina maana kizazi chetu watakuja kuona au watakuja kusikia ni historia.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna heritiera littoralis (msikundasi) nayo inapotea. Kizazi chetu kinachokuja hii miti hawataikuta, watakapokuja hawakuti hii miti ni hisotoria itakuwa nini? Itakuwa tumewajengea faida gani? Lakini siyo hivyo tu ni mazalia ya viumbe vingine hii kama kaa, chanje kama hii miti haipo katika bahari ina maana na hivyo viumbe vingine navyo vinapotea.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika visiwa vilevile kuna ndege ambao ni endemic, ni ndege muhimu hapa duniani wanapotea vilevile. Kwa mfano white eyes (chigi manjano) sisi kule Zanzibar tunaita tayari wamepotea hawapo, sawa. Kuna ndege hawa Javaspirous tayari wanapotea hawapo na yote ni kwa sababu ya kwamba mabadiliko haya ya tabianchi yanapotea. Kwahiyo kupotea na kuondoka kwa visiwa siyo kwasababu tu kwmaba tuna ardhi inaondoka, lakini tunapoteza na hizo mnaita wenyewe sasa bioanuai sijui na nini, vitu vyote vinapotea tutakuwa hatuna na kizazi chetu kitakujakurithi nchi ambayo mimea na ndege hawapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee mbele kuna tatizo linasema kwamba mvua hizi tunapata tunaita mabadiliko ya tabianchi, lakini hatuwezi kuwa na mabadiliko ya tabianchi mazuri tunayoyategemea kama sisi wenyewe hatujabadilika. Mwenyezi Mungu ametuleta duniani kuitawala dunia na vilivyomo ndani yake, je, sisi wenyewe tunalijua hili? Tumebadilika? Kama hatujabadilika na tunachokitawala katika dunia hii kitaendelea kuharibika, hakitakuwa katika namna tunayoitaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania tulikuwa tunapata mvua nne kwa mwaka, leo tunapata mvua mbili kwa taabu na zikija hizo mvua basi ni laana maana yake ni mafuriko, uharibifu. Likitoka jua ni hivyo hivyo, kwanini? kwamba sisi wenyewe hatujabadilika kwa hiyo na sisi wenyewe lazima tubadilike. Oman ilikuwa jangwa, walikuwa miaka miwili hawaoni mvua, mvua ikinyesha ni ajabu leo wanapata mvua nne, kwanini? Wao wenyewe wamebadilika. Kwa hiyo na sisi lazima tubadilike na tuelewe kwamba tumeletwa ulimwenguni kwamba tuvitawalie hivi, Je tumebadilika nafsi zetu? Tunalijua hilo? Kwa hiyo na sisi wenyewe lazima tubadilike na ndiyo maana sasa mvua hizi zinaleta mafuriko, zinaleta athari kubwa, kilimo kinaharibika, matokeo yake sasa ni hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini siyo hapo tu wadudu hawa kuna wadudu sasa hivi matunda haya yote kuna vidudu dudu hivi mapapai yanaharibika, maembe, ndizi, wale wadudu weupe sijui mnawaitaje sijui sigatoka, sijui wenyewe wataalam mnawaitaje. Wataalam wa kilimo kwa miaka nenda miaka rudi hakuna mabadiliko yoyote. Yote haya yanasababishwa na kubadilika kwa haya mabadiliko ya tabianchi ambayo tunayasababisha sisi wenyewe.

Waheshimiwa Wabunge, tunasema kwamba theluji inayeyuka katika Mlima Kilimanjaro, wenyewe Wachaga wa Kilimanjaro wanaita Kibo. Sasa kwa maana ile Kibo ikipotea maana yake na Mlima Kilimanjaro unapoteza thamani yake tutakuwa tunajivunia nini kama Watanzania? Kwa hiyo, vyote hivi ni vitu ambavyo tunatakiwa tuviangalie sana. Lakini jangwa linaongezeka kwasababu sisi wenyewe ambao tumeambiwa tuitawale dunia ndiyo wakataji wakubwa wa miti, ndiyo wachomaji mkaa, ndiyo wachomaji wa moto kwenye misitu, kwa hiyo, ni sisi wenyewe na ndiyo maana nikasema tunalichukulia uzito kiasi gani? Sisi kama wananchi, kama binadamu ambao tmeletwa tuvitawale hivi tunalichukulia hili suala la mabadiliko ya tabianchi kwa thamani kiasi gani, kwa nguvu kiasi gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni nini athari yake? Wanaoathirika sana ni wakulima na wavuvi. Tabianchi ikibadilika, wakulima hawa watalima hawavuni kwa sababu hizo nilizozitaja ama kwa mafuriko ama za jua ama za wadudu waharibifu hawatavuna na matokeo yake sasa tutakuwa tunawasema watalaam wa kilimo, sijui madawa, sijui hatuna watu ugani lakini ni tabianchi tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tabia hizi zikibadilika, mazingira yakibadilika, hali ya hewa ikibadilika na maradhi yatakuja. Zanzibar nime-check mara hii pale mwezi Januari na Februari ongezeko la wagonjwa wa pressure hospitali pale ni kubwa sana, kwa sababu gani? Ya joto tu limeongezeka. Kwa hiyo, hizo ni athari za moja kwa moja tunaziona lakini wavuvi pia samaki watakosekana, wakikosekana samaki inamaana hao nao wanaathirika. Kwa hiyo, ikifa hii ecosystem yote ina maana na kizaizi chetu kinachokuja hakitaona mimea na ndege na wanyama ambao walikuwepo wa asili hapa kwa hiyo, lazima tuwe serious na hili ili tuone kwamba kizazi chetu kinakuja kufaidika kwa kiasi gani, nini tufanye?

Mheshimiwa Naibu Spika, waathirika wa masuala haya duniani asilimia 20 ni wale watu maskini kabisa na ndiyo hao wanaoathirika kwa sababu wao ndiyo wanaoishi huko kwenye miti, kwenye misitu na huko vijijini kwa hiyo, hao ndiyo watakaoathirika. Sasa hili suala linalozungumzwa la global warming basi ionekane sasa kwamba inafanyakazi vizuri na iwafikie wale walengwa. Nitatoa mfano, kwa mfano, kuna hizi kaya maskini ambazo zinasaidiwa sijui shilingi 20,000 kwa mwezi hivyo inamsaidia nini mtu wa kaya maskini? Yeye ni masikini unampa shilingi 20,000 kwa mwezi inamsaidia nini? Pesa ambayo hata mtoto wangu na mtoto wako Mheshimiwa Naibu Spika haimtoshi kwa mwezi kwenda shule tu.

Sasa unamsaidia mtu wa Kaya maskini sasa nadhani hizi pesa Mheshimiwa Waziri hebu zipangiwe sasa utaratibu ili kama tuna tatizo sehemu fulani twende tuka-solve hilo tatizo na hizi pesa tusiwe tunazigawanya kisiasa siasa tu, kupendezeshana pendezeshana tu hali ni mbaya ni lazima tuwe commited katika kuyatafutia suluhisho masuala haya vinginevyo itakuwa tunapoteza muda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nadhani natoa mfano tu hapa wa TASAF kwamba hizi shilingi 20,000 hizi hazisaidii kuondoa yale matatizo na badala yake zinaleta mizozo tu zaidi, mnawapa mnaowajua, mnawapa watu mnachangua na nini kwa hiyo, hebu hii pesa ndogo ambayo
tutaipata katika kufanya haya basi tuipeleke katika eneo ambalo lina tatizo tuondoe tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna masuala haya ya social protection (kinga za kijamii) je, tuna alternative gani? Maana yake tusiwe tunasema tu wkamba kuna hili, Je, alternative yetu ni ipi? Juzi nilikuwa namuangalia Dkt. Kilahama amepunguza yaani wamefanya utafiti, wamepata miti kutoka miaka 14 kuvuna mkaratusi sasa ni miaka nane unavuna katika ubora. Kwa hiyo, solution ziwe hizi na tuzieleze sasa kwa jamii moja kwa moja kwamba solution ni hii. Kwa hiyo, tufanye vitu vya namna hii na tuwatumie wasomi na watalaam wetu katika tafiti zao tufanye katika kukabiliana na hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, lazima tujitathmini kama Watanzania. Kama haya tunayaona leo na haya dunia inayasema leo tunachukua hatua gani? Tuna gesi lakini bado asilimia 80 ya Watanzania wanatumia mkaa na kuni kama nishati. Kwa hiyo, tuendeleze elimu na tuwasaidie, tuboreshe kurahisisha matumizi ya gesi ili tupunguze sasa hizi athari zinazotkana vinginevyo itakuja kuwa kama hadithi ya biashara ya utumwa. Wazungu ndiyo walioanzisha biashara ya utumwa, wakafaidika, walipopata teknolojia wakawatupia watu wengine wao wakasema ni biashara haramu. Kwa hiyo, na sisi tusipoliangalia hili tutakujakuishia katika historia za namna hiyo.

Kwa hiyo, naomba katika matumizi sasa gesi tunayo tuhamasishe sana ili tuepuke ukataji wa miti na utumiaji wa mkaa na kuni kama nishati na badala yake tuweze kuyatunza mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, Bismillah Rahman Rahim.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya mwanzo siku ya leo kuchangia hotuba iliyo mbele yetu ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nami nitajikita zaidi katika ukurasa wa 10 - 12 katika hotuba yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nianze na historia fupi ili wale ambao wana mtazamo finyu waweze kuelewa historia ilisemaje au historia inasemaje. Nasema Taifa la Zanzibar lilianza miaka mingi sana, ni Taifa lenye historia ndefu na ilianza kabla hata ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo miaka 2,000 iliyopita. Ukitaka kuipima historia ya Zanzibar basi itakuchukua muda mrefu, lakini mimi nitaanza hapa kwenye karne ya 18 na 19 ambapo walio wengi wanaweza kukumbuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watakumbuka kwamba Zanzibar ilikuwa ni center ya biashara kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati, Zanzibar ilikuwa ni Taifa lenye Mabalozi wake miaka hiyo lakini Zanzibar ilikuwa na mfumo madhubuti wa kiuchumi na kiulinzi. Kwa hiyo, Zanzibar lilikuwa Taifa kubwa na litaendelea kuwa Taifa, historia inasema hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwarejeshe kidogo waelewe ninaposema kwamba Zanzibar lilikuwa Taifa na lilikuwa na nguvu za kijeshi na kiuchumi. Zanzibar katika karne ya 18 ilikuwa tayari ina jeshi lake kubwa na ina manuwari za kivita. Zanzibar ilikuwa na Jeshi la Ardhini lililokuwa linaongozwa na Jenerali Sir Lloyd William Matthews ambaye alifariki na kuzikwa Zanzibar na kaburi lake lipo pale pale Zanzibar na jeshi hilo lilikuwa linaitwa Blue Jacket.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kulikuwa na Jeshi la Baharini ambalo lilikuwa na manuwari kumi za kivita. Kulikuwa na manuwari inaitwa Liverpool ambayo ilitengenezwa India mwaka 1826 ikiwa ina uwezo wa kuchukua mabaharia 150 na mizinga 74 lakini kulikuwa na Prince Regency, Victoria, Shaalam, Coral lean, Rahman, Pied Montez, Mustapha, Atenamise na Crew. Zote hizi zilikuwa ni manuwari za kijeshi, katika karne ya 18, Zanzibar tayari ni nchi na ina vifaa kama hivyo vya kijeshi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Zanzibar ilikuwa na majemedari wa kivita ambao walipigana vita. Waliosoma historia wanaweza kukumbuka kwamba Zanzibar kulitokea vita baina ya kabila la Mazrui na mpaka kufikia Kisiwa cha Pemba kikatekwa, lakini majemedari hawa ni miongoni mwa majemedari waliopigana vita hiyo na kukikomboa Kisiwa cha Pemba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na jemedari wa mwanzo Jenerali Mohamed Juma, Jemedari Khalef bin Nassor, Jenerali Mohamed bin Nassor, Jenerali Hamad bin Ahmed, Jenerali Abdallah Sleyum, Jenerali Khalid bin Said, Jenerali Nassor Sleyum, Jenerali Hemed Sleyum na Jenerali Jen Tagai. Wote hawa walikuwa ni majemedari wa kivita ambao walikuwa katika majeshi ya Taifa la Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiuchumi Zanzibar ilikuwa ni Taifa ambalo linajiendesha kibiashara. Mpaka karne ya 18 na 19 Zanzibar ilikuwa inaweza kufanya biashara zake na Bara Hindi, Uarabuni, Uchina, Japan na walikuwa na mikataba ya kibiashara katika nchi hizo. Kwa upande wa Afrika Mashariki na Kati Zanzibar ndiyo ilikuwa kitovu cha biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naileta historia hii ili tuelewe na kwamba Zanzibar wakati huo ilikuwa tayari na sarafu yake ikitumia sham, rupia, noti zake zenyewe shaba, pesa ya Mnyasa, blue butter, shanga, mtama pamoja na cowrie. Kwa hiyo, Zanzibar ilikuwa ni eneo kubwa la kibiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tujiulize wakati huo Tanganyika ilikuwa wapi? Hata hilo jina Tanganyika lilikuwa halipo. Tanganyika imezaliwa tarehe 4 Mei, 1885 na baada ya Mjerumani kuchukua eneo la maili 600 la eneo la Mrima. Kwa hiyo, hapo ndiyo jina Tanganyika likapatikana wakati huo Tanganyika jina halipo hawana hata ngarawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilitaka kuyaeleza haya ili kuiweka historia sahihi. Nakuja sasa kwenye hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwenye ukurasa wa 11 hapa alipozungumza kwamba katika kutatua kero za Muungano vikao vimefanyika baina ya Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kuweza kutatua changamoto katika masuala hayo hususani masuala ya fedha, biashara, ajira katika taasisi za Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile akaendelea kwamba, wamekutana na kuzungumza katika sekta zinazohusu fedha, biashara, viwanda, uwekezaji, ujenzi, uchukuzi, maliasili na utalii. Kama haya yamezungumzwa na kero za muungano zimeanza karne na karne ni lipi ambalo limepatiwa ufumbuzi katika haya? Hakuna hata moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri ni juzi tu, Mawaziri na kamatio zao za viwanda wa Zanzibar na wa Tanganyika hapa, wamekutana wameshindwa kutatua tatizo la sukari. Kuna tani 460,000 Zanzibar za sukari zinataka kuuzwa, Serikali ya Muungano imekataa, lakini wakati inakataa kununua sukari ya Zanzibar Serikali hii inaenda kuagiza sukari Brazil. Ndugu zetu wa damu, ndugu zetu ambao tumeungana hawawezi kununua sukari kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, wanaenda kununua sukari Brazil. Kisingizio eti ukinunua sukari ya Zanzibar wataagiza sukari kutoka nje na badala yake watachanganya wauze Tanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi hata kama ni hivyo, iwe kweli ni hivyo, kwani kuna ubaya gani kununua hiyo wakati unaangalia wewe ile marker price tu. Kama bei ya Brazil na bei ya Zanzibar ni sawa kuna ubaya gani? Lengo la hili si kweli kama hapa hotuba ilivyoeleza kwamba, wana nia ya kutatua, lakini lengo lake ni kuikandamiza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar isiwe na mapato yake ya ndani, hili ndio lengo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu, mwangalie market price, kwanini usinunue sukari? Mbona sukari inayotengenezwa Mtibwa mnanunua wakati kile ni kiwanda vilevile ambacho kinatokana na kiwanda cha sukari cha Zanzibar? Sasa hii kwa nini mnunue? Mtoto halali, lakini mama haramu, kwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lengo hapa la hii hakuna lengo la kutatua kero ya Muungano na lengo lake ni kuhakikisha kwamba, Zanzibar haipati mapato. Matokeo yake ni nini…

T A A R I F A . . .

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, mie Mwongozo wake wala siusikilizi kwa sababu, hata masuala ya biashara hajui, wala hiyo Zanzibar haijui, wala hajui chochote huyu, huyu aljununi fununu humu ndani humu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama suala sukari ya Zanzibar haiwatoshi Wazanzibari wenyewe anajuaje yeye? Zanzibar inatumia sukari tani ngapi? Usinipotezee muda, huna unalojua, unataka sifa wala Uwaziri hupewi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Mheshimiwa Naibu Waziri nakuheshimu sana, unajua fedha hujui biashara. Kwa nini mnaagizia mitumba wakati mnazalisha pamba hapa Tanzania na inawatosha kuzalisha nyie? Njoo kwenye biashara tukufundishe biashara, wewe ni mtu wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachosema hata kama sisi tunaagiza sukari kutoka nje, tunaiuzia Tanganyika muangalie market price. Ikiwa market price ni sawa kwa nini msinunue Zanzibar mkanunue sukari Brazil wakati Zanzibar ipo imejaa kwenye ma-godown? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ndio hoja yangu. Kwa hiyo, lengo ni kuikandamiza Zanzibar isipate mapato yake kiuchumi. Kwa hiyo, ajenda hii iliyozungumzwa hapa kwamba, mnakaa SMZ na SMT kuzungumzia kero za Muungano, halina ukweli wowote na lengo lake hii ni kuikandamiza Zanzibar isipate maendeleo kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake ni nini? Serikali ya Zanzibar sasa hivi ime-stuck na wanailazimisha ZRB kukusanya mapato ya milioni 200 kila mwezi kutoka kwenye vyombo vya moto tu, hivi Zanzibar kuna magari mangapi, vespa ngapi, pikipiki ngapi ambazo watatozwa faini wapate milioni 200? Matokeo yake kuwa na chombo cha moto Zanzibar sasa hivi ni laana. Ndugu zetu wa damu hawa kuinunua sukari ya Zanzibar hawataki ma-godown yamejaa pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, amezungumzia hapa, katika ukurasa wa 17 na ukurasa wa 18 kwamba, Msajili wa Vyama anasimamia vizuri suala la demokrasia ya vyama vingi, ili iimarike. Siamini katika hili na ninaamini kama Msajili wa Vyama ndiye anayeuwa Vyama vya Siasa hapa Tanzania na hususan Vyama vya Upinzani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Msajili wa Vyama anaiandikia CHADEMA kwamba, wajieleze kwa nini asikifute kwa sababu wameandamana. Kwani kuandamana haramu kwa mujibu wa Katiba ya Tanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa yeye badala ya kusimamia vyama vikaenda mbele yeye ndio anavikandamiza vyama, CHADEMA amewafanya hivyo, CUF amepandikiza mgogoro yeye mwenyewe, CUF haina mgogoro, yeye ndiye anayesababisha mgogoro huu. Yeye msajili alivyo mnafiki kamwandikia Katibu Mkuu kwamba, hatatoa ruzuku kwa sababu, ana mgogoro. Akamwandikia Ibrahim Lipumba kwamba, hatatoa ruzuku kwa sababu chama kina mgogoro.

M W O N G O Z O . . .

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, neno mnafiki, namuomba Mheshimiwa Waziri kama hajui arudi katika Biblia, arudi katika Qur-an, arudi katika tafsiri, neno unafiki maana yake ni nini. Arudi huko ataona, kama hajui. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unafahamu vizuri maana ya unafiki, nitafsirie; mmoja kati ya alama za mnafiki ni anapoahidi asitekeleze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudi kwenye hoja kwamba, Msajili huyu kamwandikia barua lipumba kwamba, hatatoa ruzuku kwa sababu chama kina mgogoro. Akamwandikia barua hiyohiyo Seif Sharrif Hamad kwamba, hatatoa ruzuku kwa sababu, chama kina mgogoro. Kwa nini leo msajili huyu anarudi anampa Ibrahim Lipumba zaidi ya bilioni 1.3 pesa za ruzuku wakati alishaandika kwa maandishi kama hatoi? Kama sio unafiki ni nini? Kaandika yeye mwenyewe, sasa hiyo ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hajengi siasa za vyama na badala yake anaua vyama na lazima tumwambie…

T A A R I F A . . .

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hiyo siipokei kwa sababu, huyu yakuuluna maala yafaaluuna. Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa haipokelewi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilichokisema mimi ni kuandika barua yeye mwenyewe halafu akarudi akatoa pesa. Kama aliandikiwa barua kwa nini, asirudishe barua zake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, yeye mwenyewe ndiye alisema; mimi nazungumzia hoja yake mwenyewe, maandishi yake mwenyewe.
Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama mchana huu. Aidha, ninakushukuru na wewe kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Spika, wachangiaji wa leo ni wakali sana, kule kwetu tunasema moto umepata magogo sijui kwenye chanja utawaka! Wapemba wana methali inasema; “ukilima patosha utavuna pashakwisha” na ukilima usipo palilia ukivuna utalia. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, namshukuru mchangiaji aliyemaliza amemuonyesha chanzo kimoja cha mapato ambacho Mheshimiwa Waziri akikitumia anaweza kuongeza pato katika Wizara yake. Sasa na mimi nataka nimuonyeshe chanzo ambacho kama atakitumia basi Jeshi letu litakuwa ni chanzo kikubwa cha mapato hata pengine kuliko utalii au vyanzo vingine vya mapato katika nchi yetu kwenye Pato la Taifa.
Mheshimiwa Spika, Jeshi letu limesifiwa sana na linasifiwa sana na ndiyo ukweli kwa utendaji kazi na weledi na nidhamu ya hali ya juu ndani ya nchi yetu na nje ya nchi yetu, ni ukweli kwamba Jeshi letu linashiriki katika UN - Mission nyingi. Tunaomba leo, Mheshimiwa Waziri utakapo kuja hapa utuambie Jeshi letu linashiriki katika mission nyingi za UN; je, ni kiasi gani cha fedha tunazopata kutoka katika mission hizo? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, katika Mission hizo kuna dry lease ambazo tunapeleka wanajeshi na logistic nyingine zinafanywa na UN, lakini wet lease ambazo tunapeleka wanajeshi na vifaa, kila kifaa kinalipiwa kwa dola. Kwa mfano gari moja tu linalipiwa kati ya dola 500 hadi dola 800, na inalipwa katika vipindi vya miezi mitatu, mitatu. Tumeshiriki katika UN Mission nyingi, utuambie Mheshimiwa Waziri ni kiasi gani cha fedha za kigeni ambazo Jeshi letu linapata katika mission hizo au pato letu sisi ni yale majeneza tu yanayokuja na maiti hapa tunazika? (Makofo)
Mheshimiwa Spika, hapa lazima tujipange, dunia ya leo, missions hizi za UN ni mtaji. Nchi kama Bagladesh, India, South Africa, Ukraine, wamewekeza sana katika UN Missions majeshi yao na silaha, kwa sababu zinaingiza pato kubwa katika Jeshi la Wananchi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri tunaiomba Serikali sasa, nilisema wakati nachangia Wizara ya Kilimo hapa kwamba Serikali haina vision, tunaiomba Serikali sasa ikae, ipange hapa ili Jeshi letu lisiwe linaenda kule kupigana vita tu, lakini liwe linaenda kule linapigana vita kwa faida ya wao wenyewe, lakini na kwa faida ya nchi yetu na Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Serikali lazima ipange tujuwe ni vifaa gani vinatakiwa vinunuliwe viwepo pale na katika ubora wake ili lile pato katika nchi yetu liwe ni pato kubwa na tusiwe tunapeleka askari wetu na kupoteza maisha tu kule! (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa kweli inasikitisha, Serikali hii ya CCM kwamba hata jeshi mnalipatia asilimia ndogo ya bajeti ambayo inapitishwa. Jeshi ambalo linalinda mipaka ya nchi yetu, Jeshi ambalo limekomboa nchi zote hizi za Kusini, Jeshi ambalo ni waaminifu, ni waadilifu, ni wasikivu.
Mheshimiwa Spika, Jeshi ambalo linafanya kazi katika mazingira magumu, yakitokea maafa sasa hivi hapa daraja limekatika ni wao huko, mvua, jua huko, leo katika bajeti yao wanaambiwa kwamba wanapata asilimia 18 katika bajeti ya maendeleo, hivi jamani kweli!
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika naendelea, kama kuna Mbunge hajaridhika anione kwa wakati wake nimsomeshe. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tunapopeleka Wanajeshi wetu katika mission hizi kuna Chapter Seven kuna Chapter Six, namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atuambie namna gani askari wetu wanalipwa wanapoenda katika Chapter Seven na wanapoenda katika Chapter Six. Atuambie ni namna gani wanalipwa. Kwa sababu Chapter Seven ni ulinzi wa amani, lakini Chapter Six ni vita kamili. Kwa hiyo, tunaomba Mheshimiwa Waziri utupe ufafanuzi.
Mheshimiwa Spika, lakini pia utuambie Mheshimiwa Waziri kwa mfano, kama hawa waliokwenda DRC hivi karibuni tu, tumepoteza askari wawili muhumu sana! Luteni Rajabu na Meja Mshindo ni askari ambao ni muhimu sana katika jeshi letu, wamepotea katika kuisambaratisha M23 wamefanikiwa; je, waliporudi askari wale ambao walirudi na roho zao, Serikali imewathamini vipi? Wale ambao wamepoteza maisha katika vita ile ya kuisambaratisha M23 hadi leo ni vita ya kawaida tu pale na wao familia zao zitaenziwa vipi?
Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali iwaangalie askari wetu hawa angalau wawe na bima ya afya, wawe na bima ya ajali, wawe wana bima ya kazi hatarishi zile wanazo zifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ni aibu leo kusikia askari mstaafu tena pengine alikuwa na cheo kikubwa anamaliza jeshi anakuwa fundi baiskeli au mziba pancha mtaani au mlinzi, ni vitu vya kusikitisha kwa kweli! Kwa hiyo, angalau basi wapatiwe hizi bima za afya askari wote wawe na bima za afya, wawe na uhakika angalau na maisha yao.
Mheshimiwa Spika, namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa, katika ukurasa wa 24 wa hotuba yake amesema miongoni mwa kazi walizozifanya ni kutoa mafunzo katika jeshi, lakini pia na Jeshi la Akiba. Kwa hiyo atuambie hilo Jeshi la Akiba ambao wamepata mafunzo ni askari wangapi na mafunzo ya aina gani ili tuweze kujua hawa askari wetu wa akiba wamepata mafunzo ya aina gani.
Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kusema kama hatutowathamini wanajeshi wetu na kama tutaendelea na usanii huu wa kwamba tunapitisha bajeti hapa katika Bunge, halafu bajeti zile haziendi hata kwa Jeshi, tunajipalia makaa wenyewe! Tunajipalia makaa sisi wenyewe pamoja na uaminifu na uadilifu waliyonao, lakini hawa ni wanadamu kama wanadamu wengine. Kwa nini bajeti ya Bunge ikamilike, kwa nini bajeti ya Serikali, Mawaziri na Maafisa wengine wapewe kwa ukamilifu, lakini bajeti ya Jeshi iende robo, kwa nini? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hata hawa wanaofanya kazi hizi tunashindwa kuwakamilishia bajeti! Ninaiomba Serikali sasa, tumepita katika Awamu Nne tumebabaisha sana, hii Awamu ya Tano ya hapa kazi tu na mmesema kwamba Awamu ya Tano hii ni nzuri sana, sisi tuna imani hiyo kwamba inaweza ikawa nzuri, basi mkae kama Serikali, mpange ili tuone Serikali inaendeshwaje.
Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, Bismillah Rahman Rahim.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na leo nilikuwa nichangie kwa ukali sana, lakini Mheshimiwa Waziri ashukuru kwamba hotuba yake imekuja katika siku Tukufu na katika siku ya leo sisi Waislam huwa tunahusiana uusi kum ibada-Allah wanafsi-bitaquwa-Allah. Kwa hiyo, nitamshauri zaidi kuliko kwenda katika yale mambo ambayo nilikuwa nimeyapanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumza sana katika nchi yetu kuhusu kuporomoka kwa maadili. Maadili yanaporomokaje? Vijana wetu tunasema hawana maadili, nyimbo hazina maadili, michezo haina maadili; sasa nani hana maadili? Ni sisi wenyewe ndio hatuna maadili. Hatuna kwa sababu gani? Kwa sababu tumekubali kuwa watumwa tukaacha mila na utamaduni wetu na tukaiga mila nyingine. Mheshimiwa Waziri pale kila siku anaenda na nyimbo za kizazi kipya, sijui nini, lakini hujamsikia akihamasisha ngoma za asili au tamaduni zetu za kiasili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wakati wa ngoma zile jando na unyago, misondo, akinamama wanavunja ungo wanawekewa ngoma, wanafundishwa, pale ndiyo tunafundishwa maadili. Leo katika hao wasanii wa kizazi kipya, ukimwondoa Mr Ebbo ni nani anavaa kivazi cha asili cha Mtanzania kuitangaza Tanzania yetu? Hakuna. Wote wanaiga. Ni suruali chini ya matako, anajishika hapa, anajikunjakunja; kwa nini tusiende katika mila na destuli zetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri ahamasishe ngoma zetu za asili ili vijana wetu angalau wajue mila na desturi na asili yao. Leo humu ndani ya Bunge ukiondoa katika hawa watoto wangu, ukimwondoa Mheshimiwa Mtemi Chenge, ukimwondoa Mheshimiwa Musukuma labda na Mheshimiwa Ndassa, ni Mnyamwezi gani anayeweza kucheza Lizombe humu? Mheshimiwa Kigwangalla hawezi.

TAARIFA . . .

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana shemeji yangu. Napokea taarifa yake. Mwenyezi Mungu amweke Mr. Ebbo mahali panapostahili kwa kazi yake aliyoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, turudi katika mila na desturi zetu. Hata utalii tunapoutangaza huko nje, tunapotumia mila na desturi zetu, basi watalii wanavutika zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa katika utalii. Wageni wanapokuja, tunapowawekea ngoma za kiasili wanafurahi zaidi, wanacheza na mpaka wanakwambia sasa tutafutie tena utuwekee. Wanapenda mchezo wa ng’ombe, wanapenda ngoma za kiasili, lakini leo sisi tumeingia katika kizazi tu hiki. Sasa unasema maadili yamepotoka, ni sisi wenyewe ndiyo tunayapotoa. Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kila mwanamichezo hapa amelalamika kwamba michezo inakufa, tunapeleka watu haturudi na medali, tunarudi na aibu, tunatoka kwa shangwe, tunarudi na msiba; ndiyo. Kwa sababu wanamichezo wazuri walikuwa wanapatikana mashuleni. Leo katika shule hakuna huo utamaduni wa hii michezo kuendelezwa, ikafika kipindi ikafungiwa kabisa ikawa haipo, mara inarudishwa. Kwa hiyo, hatujui tunafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la michezo katika mashule jamani, michezo ni afya. Watoto wanapocheza, utakuta wale watoto wanaofanya michezo mashuleni ndiyo wanakuwa active vilevile katika masomo. Kwa hiyo, pale ndiyo sehemu ambapo tunajenga michezo, lakini ndiyo sehemu ambapo tunapata vipaji. Sasa hapo Mheshimiwa Waziri ukishapata kutoka shuleni: Je, una vyuo vya kuwapeleka na kuwaendeleza? Hili nalo ni swali ambalo Mheshimiwa Waziri aliweke katika kichwa chake, leo nimemwambia na namsaidia tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, limezungumzwa sana, Mheshimiwa Waziri anafungia nyimbo, lakini nyimbo inafungiwa baada ya kuwa imeshatoka baada ya mwaka mmoja, mwaka mmoja na nusu au miezi sita. Tayari kile kibaya ambacho unakiona wewe kipo pale anakifungia kimeshakwenda huko katika Jamii. Sasa kwa niniaunafungia nyimbo? Mimi sijui labda atanisaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati nilipokuwa shuleni nilikuwa msanii vilevile. Nilikuwa siendi hewani mpaka kuna Board of Sensor inapita, inasikiliza kile ambacho nitakipeleka hewani na panafanywa marekebisho; aah, hili ondoa, hili peleka, hili fanya hivi. Nikimaliza wanarudi tena ndiyo unaruhusiwa sasa kutoka hewani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo anakwenda kumfungia msanii ameshapata gharama, nyimbo imeshatoka, kama ni maadili yamepotoka, ndiyo leo anakuja kuifungia nyimbo wakati ujumbe umeshatoka? Sasa Mheshimiwa Waziri katika hili naomba hizi Board of Sensors ziwe zinafanya kazi zake kabla ya wimbo kutoka kama ni mavazi, kama ni maneno yenyewe yaliyotumika, kama ni kitu gani, kifanyike kwanza. Sasa unakuja kufunga banda, farasi ameshatoka, sijui unafanya nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, anafungia magazeti, redio; sasa hivi vitu kwetu ni vipya. Hapa ilikuwa magazeti ni ya Serikali tu, Redio ni za Serikali tu, hata hiyo television yenyewe ilikuwa hakuna, alikuwanayo Mwalimu pekee, anaangalia, kesho anakwambia nimeota Urusi kuna vita. Sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi vitu Mheshimiwa Waziri anatakiwa avilee. Sasa wakati anavilea hivi vitu anatakiwa aweke utaratibu, havikuwa katika tamaduni zetu. Sasa kama havikuwa katika tamaduni zetu, ni kitu kipya, lazima Mheshimiwa Waziri akae, atulie, aone namna gani atakwenda navyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni changamoto ambazo zitakuwepo nyingi kwa sababu vyombo vilikuwa vinamilikiwa na Serikali, leo watu binafsi wanamiliki vyombo, kila mmoja ana mtazamo wake, ana fikira yake, unaona? Kwa hiyo, Waziri ambaye anasimamia hili anatakiwa avilee. Sasa leo Mheshimiwa Waziri mwenyewe amegeuka kama kuku mvia; anataga yai lake, halafu analila mwenyewe. Sijui tunakwenda wapi? (Makofi)


Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kitu kingine ambacho kimetokea hapa, kimezungumzwa na wachangiaji baadhi hapa kwamba Waandishi wa Habari wanapotea; Serikali haitoi taarifa yoyote. Sasa akitokea mtu na mtandao wake, akatoa taarifa, hata kama ni ya upotoshaji, hiyo ndiyo itaaminika, kwa sababu wewe kama Waziri hujafanya kazi yako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namshauri kwamba linapotokea tatizo kama hilo, wakati hao ni watu wake, tuwahi kutoa taarifa hii. Sasa taarifa nyingine itakayokuja itakuwa hiyo sasa ni ya upotoshaji au Serikali imeshasema, lakini kama Mheshimiwa Waziri ananyamaza, akitokea mwingine akisema, anakwenda kusema huyo ni mchochezi, huyo fisadi, huyo hivi; nani hakufanya kazi yake? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshauri Mheshimiwa Waziri atoe taarifa kwa wakati. Waandishi wa Habari wanapotea na Waandishi wa Habari hawa, kusema na kuandika ndiyo kazi yao. lazima watasema! Sasa wakisema sivyo, kosa siyo lao, kosa ni lako ambaye hukutoa taarifa kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kitu kingine ambacho nataka kukizungumza cha mwisho kuhusu mapato ya TFF na ZFA. Kuna mgao ambao huwa TFF inapata kila mwaka kutoka FIFA. Zanzibar ukiondoa kiwanja cha Gombani kuwekewa nyasi tokea kuanzishwa haya, ikaondolewa Zanzibar, inategemea TFF haijawahi kupata mgao mwingine. Kwa hiyo, hizi pesa zinakwenda wapi? Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, tunalotaka kujua, hapo zamani tulikuwa tunapata Dola laki 2.5 kwa mwaka kutoka FIFA, lakini hapo katikati hizi pesa wakazizuia, wakawa hawazileti kwa sababu ya mambo yaliyojitokeza hapo, ufisadi, accounts zenyewe haziko sawa na kadhalika, kwa hiyo, hizi pesa zikazuiwa. Je, hizo pesa zimeanza kurudi? Sasa zimefikia hiyo laki 7.5 tunayoambiwa au vipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mambo yote yanatakiwa kuwekwa wazi. Mheshimiwa Waziri atakapoweka wazi; atakapozungumza haya mambo kwa wakati, hawezi kusikia malalamiko. Hata yakitoka yale malalamiko, itakuwa tayari Mheshimiwa Waziri ameshayasema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, leo nimezungumza kwa upole sana na Mheshimiwa Waziri kumwonesha namna gani aweze kufanya kazi vizuri katika hii Wizara. Hii Wizara inaonekana kama ni Wizara tu hivi nyepesi nyepesi na nini, lakini Wizara hii ndiyo inabeba maisha yetu. Kinapopotea kizazi chetu, inapotoka taarifa ya upotoshaji, inaweza ikaligharimu Taifa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Bismillah Rahman Rahiim.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi jioni ya leo, Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango na Naibu Waziri wake na kwa sababu bado tunaendelea na swaumu basi nitazungumza kwa upole na kuwashauri zaidi. Hivi Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri hawa watu wanaposimama wakalalamika kwamba hakuna fedha huko mitaani, Mawaziri wanaposimama kwamba hawajapelekewa fedha, fedha za halmashauri haziendi, fedha zinatumika vibaya hazionekani, hivi wao kama waungwana haya hayawaumi? Kwa nini hawajitathimini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitawashauri leo kwa nini wanakosa fedha, watu wa fedha wataaalam wa mambo ya mahesabu ya pesa wametuambia hapa, kwamba tuna upungufu ya trilioni 1.2 ili kuweza kukidhi mahitaji yetu. Sasa kwa nini hawazipati? Hawazipati kwa sababu wakiwa katika mipango yao bado hawajapanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme hivi siku zote huwa nazungumza humu, Tanzania kamwe tusitegemee maendeleo kama nchi wakati hatuna National vision, hatuna tunataka nini? Leo wanaizungumzia Tanzania ya viwanda, nikimuuliza Waziri Mheshimiwa Dkt. Mpango katika kipindi cha miaka kumi na Waziri wa Viwanda yuko hapo, katika kipindi cha miaka kumi tunataka viwanda vya aina gani? Vikubwa vingapi? Viwanda vya aina gani, vya kati vingapi? Viwanda vidogo vya aina gani vingapi na mkakati wake upi? Hamna.

T A A R I F A . . .

MHE. YUSSUF S. HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru namheshimu sana msanii huyu. Nazungumza tena atuambie suala la maendeleo ya nchi huwezi kulipima kwa mwaka mmoja au miwili au mitatu. Tukubaliane hapa nawasaidia tukubaliane huwezi kupima maendeleo ya nchi kwa miaka miwili, mitatu, sasa ndani ya mwaka mmoja hadi miaka 10 utuambie tunataka viwanda vidogo hamsini na mkakati wake huu na vitapatikana hivi, hivi, hivi. Tunataka viwanda vya kati ya ishirini vitapatikana hivi na mkakati wake huu. Tunataka viwanda vikubwa vitano vitapatikana hivi, hamna hicho kitu ni usanii tu, sawa. Sasa nawapa really mifano wakajifunze.

T A A R I F A . . .

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Wewe tatizo lako hata kufunga hukufunga. Pilipili usiyoila wewe yakuwashia nini? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaambia hivi, tuwe na huo mkakati. Sasa nawapa mfano mmoja na waende wakajifunze. Huyu Waziri wa mafuta wa Oman alipoingia pale, wale walikuwa wanazalisha mafuta lita 600,000. Alipoingia akakuta wachimbaji wa mafuta yote ni makampuni ya kigeni. Akataka wazawa wachimbe yale mafuta ili ile fedha izunguke ndani ya nchi yao. Akaenda kwa mfalme akamwomba kiasi cha fedha, akawaita matajiri akawaambia kaeni mchimbe mafuta kwa kiwango hiki kinachotakiwa. Asilimia 50 Serikali itawakopesha na asilimia 50 watoe wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi makampuni yanayochimba mafuta Oman ya kizalendo ni 15. Wanazalisha wenyewe, wafanyakazi ni wao wenyewe na kabla ya hapo hawajaanza wao, walitoa vijana wao kwenda kusoma, wakaja wakasimamia, leo wanasimamia uchumi wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii kama Serikali wametenga fedha kiasi gani kuwaita wafanyabiashara kwamba wao wanaweza kiwanda kikubwa, waweke kiasi hiki na Serikali itawakopesha kiasi hiki? Tukiwa na viwanda vitatu au vinne kama kile cha Kagera Sugar, kina wafanyakazi zaidi ya 3,000 pale, tukawa na hivyo kumi, tutakwenda wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa na chini ya vile ambavyo vina wafanyakazi 2,500, tutakwenda wapi? Tukiwa na hivi vidogo tutaenda wapi? Leo unasema wapiga matofali ni kiwanda? Kwa hiyo, ni lazima tufanye hivyo. Tukifanya hivyo, fedha itarudi katika muda mfupi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, huwa nazungumza kwa jazba, achukua mantiki ya ninayozungumza, asichukue ukali wa maneno yangu, huwa nazungumza kwa jazba kwa sababu nazungumza kwa uchungu sana, kwamba kwa nini wenzetu waendelee, sisi tushindwe kuendelea? Kwa hiyo, huo ni mfano mmoja ambao nimetoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano wa pili, hapa wanashindwa kukusanya kodi kwa sababu wameharibu biashara; nchi zote hizi. Mozambique, Malawi, Zambia, Uganda, Rwanda, Burundi na Kenya zilikuwa zinakuja Tanzania kununua bidhaa. Sasa kwa sababu wameharibu biashara, kwa sababu hawajui biashara, wamepandisha kodi, wanataka kukusanya kingi kwa wakati mmoja, badala ya kukusanya kidogo kidogo na Waswahili walisema: ndogo ndogo nyingi, si kubwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo toka hapo nje, hao wajasiriamali, hao wadada wanaouza hapo, wanaenda kuchukua bidhaa Uganda. Kwa nini wakati nchi zote hizo zilikuwa zikija Tanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wakija Tanzania kununua maana yake nini? Maana yake hoteli, gesti, migahawa, magari, tunaingiza fedha. Leo wamepandisha kontena hapa hailipiki. Kwa hiyo, bidhaa zile zile zinapita Dar es Salaam, zinaenda Zambia, halafu zinarudi Tanzania zinauzwa. Sisi tunafanya nini? Hivyo ndivyo biashara inavyoendeshwa? Sisi tunazaliwa, hatuna fedha, kwetu siyo matajiri, lakini baba yangu anauza dagaa kwa fungu, anauza malimao, kitunguu na binzari; biashara tunajua. Ndogo ndogo nyingi, si kubwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wao wamepandisha ushuru, wafanyabiashara wameacha kuleta biashara, nchi zote hizi za Maziwa Makuu zilikuwa zinakuja Tanzania kununua biashara, l eo hawaji tena, ni Watanzania wanatoka kwenda kuchukua mashuka na mashati wanakuja kutuuzia Wabunge hapa. Kwa nini? Ni kiasi gani cha fedha tunapoteza? Kwa hiyo, hebu wakae chini wampange, tuone kwa namna gani tunaweza kupata fedha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumzia suala lingine ambalo litawasaidia kwa haraka kupata fedha. Wameanzisha Reli ya Kati, Bombardier na Stiegler’s Gorge, itawachukua miaka mingapi kurudisha fedha? Nawapa njia nyingine ambayo ni urahisi tu, wataweza kurejesha fedha, ndani ya mwaka mmoja wataanza kuzalisha na kupata fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ukanda huu wa bahari; Tanga mpaka Mtwara. Wahamasisheni wawekezaji wa ndani, wawawezeshe, waweke miundombinu bora, wahamasishe nje wajenge na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Utalii yupo hapa, tujenge hoteli angalau 20 katika ukanda ule. Ndani ya mwaka mmoja, tumejenga hoteli rooms 50, 50 tu, sawa? Baada ya mwaka mmoja, hoteli hizo tayari wageni wanaingia, pesa ile itaanza kurudi. Sasa tunachukua fedha nyingi tunaenda kuikwamisha! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuchukue mfano mwingine hapa, Bunge lililopita hilo wanalosema hao tulikuwa tunazungumzia gesi, gesi, gesi. Ni dola milioni ngapi tumekopa tukawekeza kwenye gesi? Leo gesi tayari tumeiacha, tunaenda kwenye Stiegler’s Gorge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake ni nini sasa? Baya zaidi ni pale n ninaposema hatuna vision ni kwamba yale aliyoyaanzisha Mheshimiwa Rais Dkt. Kikwete leo tumeyaacha na ni mamilioni ya pesa, tumeshayaacha tunaanzisha mengine; na haya baada ya miaka 10 akija Rais mwingine yanaaachwa, tunaanzisha mengine. Hili deni la Taifa kila mwaka litaendelea kukua. Wanalaumiwa hivyo, Waheshimiwa hawaoni aibu? Hawaoni tabu kila siku, watu wazima kunyooshewa vidole? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lazima tujipange, tufanye kitu kwa uwezo wetu, tusiongeze kimo kwa kupanda kinu. Hatujafikia huko ambako wanataka kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawapa mfano wa utalii, Dubai tu hapo, wanataka kutoka watalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuchukulie Dubai, wanataka kutoka watalii 5,000,000 hadi watalii 10,000,000; wamewawezesha katika same bank na plan yao wajenge hoteli 150 ikifika 2020. Wana-import kila kitu. Kwa hiyo, baada ya miaka mitano ikifika 2020 ndani ya mwaka 2021 wanaanza kuzalisha. Kwa hiyo, kwa nini hatuigi haya mambo mazuri?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashauri, waangalie mfumo wa biashara, kwa nini wafanyabiashara wetu waende Uganda na nchi zote za Maziwa Makuu wakati walikuwa wanakuja hapa? Leo hawaji, tunapoteza kiasi gani cha fedha? Warudini katika kujenga angalau hoteli 20 au 30 katika ule ukanda, tutazalisha baada ya mwaka mmoja na fedha nyingi tutapata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa kunyooshewa vidole kila siku, watu wazima, sisi wengine inatuuma. Kwa hiyo, nawashauri tuyafanye hayo na tuangalie namna bora. Nami nawaambia tena, katika viwanda hawajajipanga wazee wangu, wajipange vizuri watuambie.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya leo. Mwenyezi Mungu amesema katika Quran, Sura ya 41, aya ya tisa mpaka ya 11 katika juzuu ya 24 kwamba ameitandika ardhi na akaipa neema mbalimbali za ndani ya ardhi na juu ya ardhi, akaipa milima na mabonde, akaipa mito na maziwa, akaipa misitu, akaipa na viumbe hai na madini ili kwayo ituneemeshe na itufaidishe wanadamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kusikitisha katika ardhi hii ya Tanzania imekuwa kama ni laana sasa kwetu, badala ya heri inakuwa shari. Mwenyezi Mungu ametuambia hayo na turudi katika vitabu vyake ili tujifunze. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi katika uchangiaji wake, Mwenyekiti wangu Mchakachuliwa, Mheshimiwa Dkt. Mary Mwanjelwa, alikariri falsafa ya Baba wa Taifa, kwamba ili tuendelee tunahitaji mambo manne; watu, ardhi, siasa safi na uongozi bora.
Watanzania tuna ardhi kubwa, tunamshukuru Mungu. Tupo wengi, tunakaribia milioni 50 sasa Alhamdulillah, lakini kwa nini tunagombana, tunahasimiana, tunapigana mpaka tunauwana? Ni kwa sababu ya ardhi. Ni kwa sababu ya ama ya siasa safi, uongozi bora ama yote mawili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali ya Chama cha Mapinduzi, kwa muda wa miaka 54, bado inawaomba tena mkae chini mtafakari, tatizo letu ni nini mpaka iwe ardhi hii haijatuletea tija? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kitu ambacho kinaleta matatizo katika ardhi na kusababisha maafa makubwa ni kukosekana kwa kile kinachoitwa Integrated Land Information Management System. Pamoja na mipango mizuri iliyopangwa na Mheshimiwa Waziri na timu yake, pamoja na World Bank kutoa pesa zaidi ya Dola milioni 20 kwa ajili ya kazi hii, pesa hizi kwa zaidi ya miaka miwili zimezuiliwa katika Ofisi ya Waziri Mkuu, hili halijatendeka. Watanzania wanauana, wanaumizana, wanahasimiana, kwa nini? Siasa safi, au uongozi bora? Tatizo ni nini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana nikasema kwa miaka 54 hebu wenzetu kaeni chini kuwe na vision, leo kila mchangiaji anasimama anakwambia tunamshukuru Mheshimiwa Lukuvi tokea awe Waziri, amejaribu kutatua migogoro. Mheshimiwa Lukuvi ni mwanadamu, ni kiumbe. Hivi akiondoka Mheshimiwa Lukuvi, tunarudi kule kule?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kaeni chini Serikali ya CCM tuwe na vision, yeyote atakayekuja katika Wizara hizi, awe anaanza pale anakwenda mbele. Leo akiondoka Mheshimiwa Lukuvi iwe Wizara hii haipo; akiondoka Mheshimiwa Mwigulu, Wizara ya Kilimo, kwisha! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jamani mnyonge mnyongeni, haki yake mpeni. Namshukuru Mheshimiwa Profesa Muhongo. Ukienda katika ile Wizara, unajua hasa kwamba anatoka wapi anakwenda wapi, step by step. Amejipanga! Kwa hiyo, pale unajua namna gani mtu amejipanga, anatoka wapi, anakwenda wapi. Jamani ukweli lazima usemwe! Kwa hiyo, tunaomba Serikali ya CCM katika Wizara zote tujipange, tuwe na vision tujue tunakwenda wapi, siyo kusema kwamba aah, Lukuvi! Lukuvi kiumbe! Lukuvi ni binadamu huyu! Akiondoka huyu jamani, tuwe tunarudi kule? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naliomba Bunge hili, leo hii, wakati bwana mkubwa anawasilisha huyo, tujue fedha hii iliyotolewa na World Bank itatoka lini, wapewe wafanye kazi ili Watanzania wasiuwane na wasihasimiane kwa neema waliyopewa na Mwenyezi Mungu. Hilo la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije la pili. Namwomba Mheshimiwa Waziri Lukuvi, pamoja na kutushawishi sana Wajumbe wa Kamati yake, pamoja na maelezo mazuri sana aliyotutolea, lakini bado tuna wasiwasi na bado mimi binafsi sijakubaliana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi cha miaka nane wananchi wa Kigamboni wamekuwa mayatima, wamekuwa na hofu juu ya hatima ya ardhi yao, Mji wa Kigamboni utakavyokuwa. Pamoja na kupunguza eneo likarejeshwa kwa wananchi, hilo lililobakia la hekta 6000, hadi leo Serikali hii haikupi fedha ya kwenda kufanya hizi shughuli ambazo zinatakiwa kufanywa. Hii miundombinu. Sasa kama hupewi fedha na ardhi ile tayari imezuiwa na wananchi wale wamepewa tu maelezo kwamba mwingie kwenye uwekezaji, mwingie hivi, mwingie hivi, lakini kwa muda wa miaka nane sasa hakuna fedha inayotoka, pale tunategemea nini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana tunasema jamani, Serikali ya CCM tunapanga; lakini tunajitekenya wenyewe, mkicheka wenyewe, kama hamjampa fedha huyo Lukuvi, atafanya nini? Kwa hiyo, kama fedha haijatengwa, wale wafanyakazi na ile Ofisi; wafanyakazi warudi Wizarani na Ofisi ifungwe, mpaka atakapopewa fedha ile itarudi ikae kwa miundombinu, ili ule Mji wa Kigamboni uje katika hilo linalotakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika nyumba za gharama nafuu. Kuna wazo zuri, mipango mizuri na kwa kweli namshukuru sana. Kama analipwa hiyo shilingi milioni 40, basi ni haki yake, alipwe Mkurugenzi wa Nyumba na Makazi, kutokana na kazi anayoifanya. Kwa sababu mtu kama anafanya kazi, basi mwache apewe kwa namna anavyofanya kazi. Anafanya kazi na anastahiki. Tunaiomba Serikali waondoe suala VAT katika nyumba za gharama nafuu ili wananchi wanyonge waweze kununua hizi nyumba ziwafaidishe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi jamani mtu anayelipwa mshahara wa sh. 150,000/=, ataweza kweli kununua nyumba yenye thamani ya shilingi milioni 45 kwenda juu? Kama hakuna wizi huko nyuma, ataweza? Sasa tunaiomba kodi hii VAT iondolewe katika hizi nyumba ili nyumba hizi, lile lengo lililokusudiwa la wale wanyonge kuweza kununua na kuishi katika nyumba hizi ziwafikie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, Mheshimiwa Waziri, Tanzania imekua, Watanzania wanaongezeka, mahitaji ya ardhi yanaongezeka, lakini na teknolojia ya kutumia ardhi inaongezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kasi ya upimaji wa ardhi ni ndogo sana. Pamoja na kuruhusu taasisi binafsi, wakawapa vibali wapime ardhi, lakini bado kasi ni ndogo sana hususan huko vijijini. Namwomba Mheshimiwa Waziri, hii kasi iongezeke ili upimaji uendelee kwa kasi na wananchi wa vijijini wamiliki ardhi ziwasaidie waweze kukopesheka kwa faida yao na kwa faida ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Awali ya yote nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha jioni ya leo kusimama hapa. Jioni ya leo nataka kumshauri tu Mheshimiwa Waziri na kuishauri Serikali. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri awe makini, atulie bardan wasalaman, laa takhaf wa laa tahzan. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na hadithi ndogo wakati nasoma miaka ya 70, darasa la tatu kulikuwa na kitabu kidogo cha Kiswahili maarufu tukikiita Haji na Selele, kilikuwa na hadithi nyingi ndogondogo. Sasa tukisoma tukimaliza mwisho wake tunaulizwa hiyo hadithi imekufunza nini? Moja kati ya hadithi iliyokuwemo ni ile ya mtu aliyekuwa na kuku wake kila siku akitaga yai moja la dhahabu. Siku hiyo akaamua kumchinja ili apate mayai mengi ya dhahabu matokeo yake akakosa yote. Hadithi hii inatufunza nini? Tamaa nyingi mbaya. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza na-declare interest kwamba ni Mjumbe wa Kamati ya Wizara hii, lakini pia nimeshawahi kutumikia Idara ya Misitu na Utalii, kwa hiyo nazungumza kitu ambacho kinaelea katika kichwa changu, nakifahamu. Binafsi wakati nilipoteuliwa kuwa Mjumbe wa Kamati hii na nikakutana na viongozi wa Wizara nilieleza waziwazi baada ya taarifa kwamba sifurahishwi na TFS na nikawa na mashaka nayo sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimefarijika zaidi baada ya kupata semina na ile hofu yangu ikathibitishwa na mtaalam aliyebobea katika masuala ya misitu kwa utafiti wake alioufanya kwa muda wa miaka mitatu juu ya TFS. Nakushauri nini Mheshimiwa Waziri? Kwa sababu ameyakuta haya lakini kwa sasa yeye ndiye mwenye dhamana na Wizara hii, kwa hiyo, mwaka huu namshauri tu ila mwakani nitambadilikia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, TFS ni nzuri katika ukusanyaji wa kodi lakini namwomba Mheshimiwa Waziri alinganishe sasa tunachokipata na athari tunayoipata, vinalingana? Misitu ya asili inapotea na itazidi kupotea na kwa mujibu wa mtaalam baada ya miaka 10 Tanzania hii itakuwa jangwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda niwakumbushe wale wanaokumbuka mwishoni mwa miaka ya 80, kazi kubwa tuliyoipata Watanzania na dunia kwa suala la HASHI na HADO kwa Mikoa ya Dodoma na Shinyanga ilivyokumbwa na janga la ukame, kazi iliyofanyika ndani na nje ya nchi. Binafsi nilifika Dodoma hapa kwa ajili ya kupanda miti kutokana na hali iliyokuwepo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Waziri aichambue TFS, aone udhaifu wake. Udhaifu wa TFS ni menejimenti, ni lazima ahakikishe kwamba anabadilisha, wanakusanya vizuri, wanapanda vizuri, lakini katika misitu ya asili suala la kuelekeza nguvu tu kwamba wakusanye kodi wanatumalizia misitu kitu ambacho kitakuja kuwa ni hatari kubwa kwa Taifa hili. Badala ya rehema hii misitu itakuja kuwa nakama kwetu, Mheshimiwa Waziri namshauri hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo hatuwezi kuwa na misitu endelevu, hatuwezi kuwa na misitu yenye tija, hatuwezi kuwa na misitu ambayo itatuletea faida sisi na kizazi chetu kama hatuna wataalam katika fani hiyo ya misitu. Leo nchi hii ina Chuo kimoja tu cha Misitu Olmotonyi, lakini Serikali imekitelekeza. Chuo kile kimekuwa kama yatima, hakina ruzuku yoyote kutoka Serikalini.
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri kile chuo kiangaliwe, kipewe ruzuku, kisimamiwe, kisomeshe wataalam wengi zaidi ili warudi katika misitu yetu ambayo iko chini ya Wizara, Halmashauri na Vijiji ili iwe ni misitu endelevu kwa faida yetu na faida ya kizazi kijacho. Huo ndiyo ushauri wangu kwa Mheshimiwa Waziri kwa siku ya leo katika upande wa misitu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye utalii. Amezungumza na kutoa ufafanuzi mkubwa juu ya nia yake ya kutoka kwenye watalii milioni moja na zaidi kwenda milioni tatu. Ni wazo zuri, tunaliunga mkono kwa sababu tunafahamu ongezeko la watalii litaleta faida gani kwenye nchi yetu, lakini lazima tujue tunataka aina gani ya watalii katika nchi yetu? Kwanza iwe ni kwa ajili ya kukuza mila na desturi zetu lakini wawe ni watalii wenye faida siyo watalii vishuka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nataka nimshauri Mheshimiwa Waziri, ili kupata watalii wazuri lakini kuwa na wawekezaji wazuri katika sekta ya utalii na kuondoa tofauti baina ya watalii, wawekezaji na jamii inayozunguka hivi vituo vya kitalii lazima kuwa na triangle ambayo itahusisha investors, Serikali na community.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutakapokuwa na triangle hiyo na wakawa pamoja na kujua mwekezaji anahitaji nini, Serikali inahitaji nini na jamii inahitaji nini, mkawa mnasimama katika kitu kimoja, mwekezaji akija hapa katika muda mfupi atakuwa amepata idhini ya kuwekeza lakini pia itakuwa uwekezaji huo una faida kwa sababu kila mmoja atakuwa anajua majukumu yake na yamepangwa yapo. Kwa hiyo, hilo namshauri Mheshimiwa Waziri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kubwa zaidi mtalii anachohitaji ni huduma. Inasikitisha unapokwenda katika hoteli zetu au katika vivutio vyetu vya kitalii kwa zile huduma zinazopatikana pale. Mtalii hahitaji jengo zuri ambalo labda lina ma-AC na kadhalika, anachohitaji hata kama ni kibanda cha nyasi lakini kiko katika kiwango gani? Je, tumeviweka katika viwango vile ambavyo wao wanavifurahia?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli watalii wanafurahia sana tradition yetu lakini je, watendaji wetu ambao wanafanya kazi hiyo, wanafanya kazi wakiwa na uweledi huo? Ndiyo maana katika Kamati nikakikamata sana Chuo kile cha Utalii, je, mnafundisha kulingana na mahitaji tunayoyahitaji ndani ya nchi yetu? Kwa hiyo, chuo kile kitoe wataalam ambao watakuwa ni wale wanaohitajika kulingana na mazingira yetu na matakwa yetu na lengo letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ana mwaka mmoja wa kuondoa yale yote mabaya ambayo leo tunamwambia ambayo ameyakuta na mwakani hapa atakapokuja katika bajeti tuje tuone improvement. Kama ipo mimi tutakuwa pamoja, kama haipo Mheshimiwa Waziri kwa kweli mimi nitakuwa adui namba moja katika hili. Kwa sababu ninayoyazungumza nayazungumza nikiwa nayajua na najua kuna nini. Leo nazungumza tu hapa vizuri lakini siku nyingine nikiamua kuzungumza vibaya atakuja kuelewa kwamba kweli hiki kitu ninachokizungumza nakifahamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri tunataka kile chuo kinachotoa vijana…
MWENYEKITI: Ahsante.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN:Bismillah Rahman Rahim.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na kwa sababu ya dakika kumi ulizonipa basi niende haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya kwanza ni kuhusiana na ufinyu wa bajeti. Kamati yetu sisi imeshindwa kutembelea maeneo ambayo hasa yana migogoro na kuweza kuishauri vizuri Serikali. Mgogoro wa Ngorongoro kila Mtanzania anaufahamu, Loliondo, lakini uvamizi katika mapori ya akiba ya Kigosi, Moyowosi, Burigi, Kimisi na kadhalika, kote huko tumeshindwa kufanya kazi kwa sababu ya ufinyu wa bajeti, Wizara yenyewe hadi hapa tunazungumza bado robo moja kumalizia ina chini ya asilimia 30 ya bajeti ambayo imetengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niliombe Bunge hili, mtu anaonyeshwa njia wakati wa kwenda siyo wakati wa kurudi, bajeti ijayo tuhakikishe tunaweka fedha ya kutosha katika Kamati zetu na katika Wizara zetu ili tuweze kufanya kazi vizuri na kuishauri Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mweyekiti, suala la pili, tuna tatizo kubwa sana katika nchi yetu lakini tunalidharau na tukiendelea kulidharau kwa mujibu wa tafiti zinazofanywa na wataalam baada ya miaka 20 nchi hii tutalia kilio cha kusaga meno. Waheshimiwa misitu yetu inapotea kwa kasi kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana ndugu yangu Mheshimiwa Kiwanga alilia machozi kama mtoto mdogo alivyokuwa anatembea katika Kamati akaona misitu inavyoathirika. Labda nitoe mfano, uchomaji wa mkaa ni chanzo kikubwa sana cha nishati na asilimia 90 ya Watanzania wanategemea nishati ya mkaa na kuni kwa ajili ya matumizi yao ya nyumbani, lakini vitu hivyo havina sheria, kanuni na hakuna sera ya uchomaji wa mkaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano, kuna vijiji kumi Kilosa vimefanyiwa utafiti, wamepanga matumizi ya ardhi pamoja na matumizi ya misitu, wamegawa vile vijiji katika block 24 na kila mwaka wanatumia block moja kwa kuni, mkaa na matumizi yao. Kwa hiyo, miaka 23 wanaacha zile block zina-regenerate zenyewe. Kwa hiyo, pale tatizo lile limeondoka, faida yake nini? Hakuna uvamizi katika yale maeneo mengine, kijiji kinapata faida zaidi kutokana na mapato yanayopatikana, lakini pia kuna na ile teknolojia iliyowekwa pale ya uchomaji mkaa ile miti inatumiwa vizuri pamoja na majiko yale bunifu waliyonayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tusijidanganye, tujiulize, hivi ni miti mingapi inayokatwa kwa mwaka mmoja ndani ya nchi yetu na ni miti mingapi inayopandwa kwa mwaka ndani ya nchi yetu, inawiana? Huo mti utakaopandwa utakaa miaka mingapi ili tuje tukate tena? Kwa hiyo, tusijidanganye mtu anaweza akasema yeye hatumii mbao kwa sababu sasa hivi kuna teknolojia atatumia vioo kutengeneza milango, meza na kadhalika lakini akifa, nani ambaye haendi na ubao?
Kwa hiyo, tusijidanganye hii ni kwa wote Mkristo utaenda na sanduku, Muislam utawekewa ubao, kila mtu siku ya mwisho utaondoka na ubao. Kwa hiyo, miti ina faida kubwa ukiondoa zile tangible na intangible benefit kutoka kwenye miti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la tatu, hili ni janga, ni kubwa lakini bado Watanzania tunalifumbia macho. Hivi hatuumii kila siku kusikia ndugu zetu wanauana kwa sababu ya tatizo la wafugaji na wakulima?
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, Bismillah Rahman Rahim.Nakushukuru kwa kunipa nafasi kuwa mchangiaji wa mwanzo katika siku ya leo katika hotuba iliyo mbele yetu ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu, kama walivyotangulia wenzangu na mimi napenda nikukumbushe kwamba kama ambavyo tuliagizwa kwamba tukumbushe hakika ya ukumbusho unawafaa wanaoamini.
Mheshimiwa Waziri Mkuu ulipoapa kuwa Mbunge ulishika Msahafu na kauli yako ya mwisho ukamwomba Mwenyezi Mungu akusaidie na ulipoapishwa kuwa Waziri Mkuu ulishika tena Msahafu na kauli yako ya mwisho ikawa unamwomba Mwenyezi Mungu akusaidie. Na sisi
tunamwomba Mwenyezi Mungu akusaidie inshaallah. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu katika hotuba yako ukurasa wa 52 na 53 umezungumzia suala la amani, lakini amani haiwezi kuwa amani ya kweli kama haijasimama kwenye nguzo zake na nguzo kubwa ya amani ni haki, Katiba na kufuata sheria. Ni dhahiri Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali ambayo sasa wewe ndiye Kiongozi Mkuu wa Serikali hiyo kwa maana ya Mtendaji Mkuu wa Serikali, Serikali
yako au nchi yako unayoisimamia sasa hivi, siyo salama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nje ya mipaka yetu hatuna vita, lakini ndani ya nchi yetu wananchi hawaishi kwa amani kabisa. Kila mmoja wetu ana hofu ya nini kitatokea baadaye? Kuanzia Mawaziri na watendaji wote wa Serikali hakuna mmoja anayefanya kazi yake akiwa na amani ndani ya nafsi yake akiamini kwamba jua litatua hajatumbuliwa. Wafanyabiashara kuanzia wakubwa na wadogo, hawana amani na biashara zao wakiona kwamba wakati wowote biashara zao zitapotea. Wafanyabiashara wakubwa, wamachinga wenye vibanda vidogo vidogo, anaweza
akaamka asubuhi, biashara yake haipo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bomoa bomoa za nyumba, mtu ana nyumba yake amejenga kwa miaka 20, 30 anaishi inakuja kubomolewa ndani ya dakika tano. Watanzania hawaishi kwa amani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia vifo vinavyotokana na
watu wenyewe kupigana, wakulima na wafugaji, wanyama kufa kwa kukatwa mapanga ama sumu, vimezidi kuendelea katika nchi yetu, lakini njaa inayoendelea kwa sababu mbalimbali za ukame, mafuriko ama wanyama waharibifu na ndege, inazidi kuendelea katika nchi yetu na wananchi wakisema wana njaa majibu ya Serikali yanakuwa hayaeleweki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi sana, nchi hii siyo salama. Baya zaidi hivi sasa kinachotia hofu ni hii kamata kamata, utekaji na uuaji unaoendelea katika nchi yetu. Wilaya za Mkuranga na Rufiji sasa hivi watu wanapigwa risasi, viongozi wa Chama cha Mapinduzi ambao ni Wenyeviti wa Vijiji wanapigwa risasi, hakuna hatua yoyote inayochukuliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, inanishangaza sana kuona polisi wanatumia nguvu kubwa kuondoa mashamba ya bangi huko, lakini watu wanakufa kwa risasi ndani ya nchi hii. Kwa umri wangu wa miaka 54 sasa sishangai suala la utekaji, wala uwekwaji ndani wa watu, wala kupotea watu
wasionekane kama Ben Sanane, sishangai na sitashangaa. Waheshimiwa Wabunge, haya yalianza Zanzibar. Miaka ya 1964 mwanzoni, akina Abdallah Kassim Hanga, Mlungi Ussi, Abdulaziz Twala, Othman Sharrif na Twaha Ubwa walipotea katika mazingira ya kutatanisha na hadi leo
hawajaonekana. Mwaka 1972 mwasisi wa Jamhuri ya Muungano Abeid Aman Karume amepigwa risasi, akauawa. Kesi ikawa inaoneshwa live katika televisheni ya Zanzibar wakati huo ndiyo televisheni ya mwanzo kwa Afrika, ikionesha kesi ile. Mshtakiwa Mr. ‘X’ hajulikani ni nani, kesi ile ikaishia. Wanaotuhumiwa kuwa wauaji wakahifadhiwa na Jamhuri ya Muungano hadi kufa kwao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeshuhudia kifo cha Edward Sokoine kimeacha maswali mengi sana. Kifo cha Imran Kombe aliyekuwa Mkuu wa Usalama wa Taifa, kapigwa risasi kama ngedere katika shamba lake, lakini pia Horace Kolimba alipotea katika mazingira ambayo yameacha maswali mengi; Balali aliyekuwa Gavana Mkuu wa Serikali kapotea, lakini Wazanzibari hadi leo tunajiuliza kifo cha Dkt. Omar Ali Juma kupotea kule na familia yake imetelekezwa hadi leo. Kwa hiyo, sishangai Ben Sanane, sishangai kukamatwa kwa Wabunge na watu wengine kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Haya ni mazoea! Naona ni utamaduni, kwa hiyo, hili silishangai. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri Mkuu, ninayasema haya kukwambia kwamba Serikali yako pamoja na kwamba unazungumzishwa hapo hunisikilizi, lakini sishangai na napenda tu nikwambie kwamba Serikali yako unayoisimamia ndani ya mwaka mmoja na nusu, haina amani ndani ya nchi
yako na ujue kama wewe ukiwa Mtendaji Mkuu wa Serikali iko siku utaulizwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni mtihani, uongozi ulionao ni mtihani; uzima ni mtihani; watoto ni mtihani; madaraka ni mtihani; na iko siko utaulizwa juu ya neema hii aliyokupa Mwenyezi Mungu umeitumia vipi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadithi fupi tu; Nabii Nuhu aliishi katika dunia kwa miaka 950. Siku anakufa, Mwenyezi Mungu anampelekea malaika wawili kuzungumza naye, anaulizwa, Yaa Nuhu, hebu tupe habari za duniani? Nuhu akasema yeye asiulizwe mambo ya duniani, kwa sababu
hakika ya dunia ni kama nyumba, ameingia kwa mlango wa mbele akatoka kwa mlango wa nyuma. Hajui kilichomo ndani. Miaka 950, seuze sisi wenye miaka 60 na 70.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili nizungumzie suala hili linaloitwa mgogoro wa Chama cha Wananchi CUF. Chama cha Wananchi CUF hakina mgogoro. Mimi ni kiongozi ndani ya Chama cha Wananchi CUF, naingia katika vikao vyote vya Chama cha Wananchi CUF, Chama cha Wananchi CUF kinaendesha vikao na shughuli zake kama kawaida. Unaoitwa mgogoro ambao umepandikizwa na system kwa kutumiwa Msajili wa Vyama vya Siasa na Profesa Ibrahim Lipumba, huu sisi hatuuiti mgogoro. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo lake kubwa huu unaoitwa mgogoro kwa kutumia watu hao ni kuzuia haki ya Wazanzibari ya tarehe 25/10/2015. Hawawezi kuzuia haki hii Profesa Ibrahim Lipumba na Msajili wa Vyama na mwingine yeyote kwa sababu ni haki na maamuzi halali ya wananchi wa Zanzibar na haki ya WazanzibarI itapatikana muda mfupi unaokuja. Msijidanganye wala wasijidanganye katika hili, hamuwezi kuzuia haki ya Wanzibari ya tarehe 25. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimalizie kwa kumwambia bosi wangu, keshakimbia eeh, Mheshimiwa Magdalena Sakaya juzi wakati anachangia hapa alisema anawashangaa Wabunge kwamba ni wanafiki. Nataka nimuulize na kwa sababu kakimbia lakini yupo kibaraka
mwenzie atamfikishia huu ujumbe, ni nani mnafiki? Yeye akikaa na Profesa Ibrahim Lipumba anasema kwamba…
KUHUSU UTARATIBU....
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa mwongozo wako. Ninachotaka kusema, hii pilipili usiyoila sijui yakuwashia nini Mheshimiwa Jenista. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachosema, anapokaa na Profesa Ibrahim Lipumba anasema kwamba Profesa Ibrahimu Lipumba anamuunga mkono na wako pamoja. Akiondoka Profesa Ibrahim Lipumba anawaita Wachungaji anawaambia nimechoka kutumia pesa yangu, Mwenyekiti
akija hapa akiondoka analeta masuala mengine. Nawaomba Wachungaji mwende mkaongee na Seif Sharif suala hili limalizike ili mimi nisitumie pesa zangu, mnafiki ni nani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nawaambia tena Msajili wa Vyama vya Siasa, mpango wake alioupanga taarifa tunazo asitegemee kwamba…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Bismillah Rahman Rahim. Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie jioni ya leo, Mheshimiwa Waziri naomba unisikilize vizuri, nataka kuendelea kukushauri kwa mwaka wa pili mfululizo.

Mheshimiwa Waziri, Wizara yako ni ngumu sana na unapaswa kuwa mvumilivu sana, tenda wema uende zako usingoje shukrani.

Naanza na utalii, Waheshimiwa Wabunge wengi humu walikuwa wanachangia kila mmoja katika Jimbo lake, katika Wilaya yake anataja vivutio vya utalii ambavyo vipo katika eneo lake, lakini bado havijaanza kufanya kazi. Wengine wamesifia kwamba Rais ameleta ndege na idadi ya watalii wameongezeka, lakini hatuwezi kuvaa koti bila kuvaa shati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushauri kwamba ili kupata watalii wengi ni lazima tuwe na hoteli za kutosha, tuwe na facilities za kutosha kwa hiyo tuongeze number of rooms katika nchi yetu ili idadi ya watalii iongezeke na hilo litafikiwa baada ya kuwa na mahoteli mengi lakini pia baada ya kuweka miundombinu ya kutosha ambayo itawafanya wawekezaji wavutike kuja kuwekeza katika sekta hii ya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni aibu kwa nchi yetu ya Tanzania ukiangalia vivutio vya utalii tulivyonavyo ni natural siyo artificial, lakini unaambiwa nchi yetu inaingiza watalii milioni 1,200,000 ni aibu kubwa sana. Ukiwagawa hawa kwa vivutio tulivyonavyo labda kila mtalii anaweza kwenda katika kivutio kimoja tu. Kwa hiyo, nakushauri tuwe na lengo katika kipindi cha miaka kumi ya Serikali ya hapa kazi tu, basi angalau tuwe tunaongeza milioni moja baada ya miaka 10 tuwe na watalii milioni kumi na hili linawezekana kama tutakuwa na mipango madhubuti ya kuongeza mahoteli na kuboresha miundombinu katika sekta ya utalii kule chini, hizi ndege zitakuwa hazina maana yoyote kama mgeni akifika hapa hapati huduma za kutosha kule chini, hilo la kwanza. (Makofi)

Pili, Mheshimiwa umezungumzia tu suala la utalii wa fukwe, lakini limezungumzwa sana hapa utalii wa baharini, sijaona hasa mkakati madhubuti ambao unatupeleka kwamba katika kipindi kijacho tutakuwa na hoteli ngapi za kitalii au tutakuwa na utalii wa fukwe wa aina gani. Naomba tuweke mikakati, tuweke mpango hasa madhubuti, haya maneno yasikutishe tuweke mpango madhubuti ili ukiondoka tuseme Mheshimiwa Maghembe na Naibu wake mlifanya nini, kwa hiyo maneno yasikutishe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, toba sikio, narudia toba sikio, nasikia kuna fees zinataka kuongezwa baada ya Bunge hili, hizo fees kama mtakubali na wataalam wako sijui kama mmeshauriana ziingie zitaua sekta ya utalii. Sidhani kama TRA ni wataalam wa sekta ya utalii, siwakatazi kupandisha kodi lakini wakae na wataalam wa sekta ya utalii waone.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikia kuna fees za hunting block fees, wanataka kuweka fees asilimia 18. Kuna hunting block application fees, kuna application for hunting block transfer fees, kuna hunting permit fees, kuna conservation fees for hunters, kuna conservation for hunting observer’s fees, kuna intercompany permit fees, kuna travel handling fees, kuna professional hunting licence fees, kuna examination fees, game fees, fees for non consumptive wildlife utilization photographic tourism.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama utakubali asilimia 18 katika haya unaenda kuua utalii. Naomba watalaam wa utalii wakae pamoja na watu wa TRA mkubaliane kwenye fee hizi, zikiingia zitaenda kuua utalii. Nakushauri hilo kama mtaalam ambaye nimefanya kazi katika sekta hii. Nafahamu kama mwekezaji, nafahamu kama mzalendo, nakushauri kitaalam kabisa. Serikali mkae mliangalie upya, fees hizi zikiingia zitaua sekta ya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia kwenye hoja ya utalii, suala la makumbusho, suala la Makumbusho ya Taifa limetajwa sana hapa, watu wamezungumza sana, bado halijafanyiwa kazi. Nakuomba uwaangalie wafanyakazi, stahiki zao, mazingira wanayofanyia kazi, tumetembelea makumbusho, tumezungumza na wafanyakazi, mfanyakazi anafanya kazi pale miaka mitano hajapanda cheo, hajaongezwa mshahara, hajaenda kusoma. Wakati mwingine anafanya kazi, masaa ya kazi yanamalizika bado kuna wageni hawezi kuondoka, hana hata malipo ya over time, hili nalo liangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kuhusu suala la misitu na nyuki. Watu wengi hapa wameshauri kwamba tuangalie suala la mkaa, wametoa mfano wa Kilosa. Kilosa imefanikiwa lile kwa sababu wana wataalam. Ule mradi kuna wataalam wa misitu pale ndani, kwenye Halmashauri wana wataalam wa misitu pale ndani, kwa hiyo, ule mradi wa kuchoma ule mkaa endelevu ni kwa sababu wana wataalam wa misitu. Nakushauri Mheshimiwa Waziri ufanye linalowezekana Chuo cha Misitu Olmotonyi kifufuliwe ili kuweza kuzalisha wanamisitu ambao wataweza kuendeleza misitu yetu. Bila kuwa na wataalam wa misitu ambao watakuonyesha hasa mti huu unakua mahali gani, una faida gani na kwa maslahi gani? Hatuwezi kufikia hayo malengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko Kilosa mlikofanikiwa, mlifanikiwa kwa sababu wale Maafisa Misitu wanawaeleza wale wanakijiji kwamba mti huu ukiukata unatoa coppice, mti huu usiukate kwa sababu ndege ni mazalia yake. Mti huu ni mti wa asili ubakie, lakini mtu ambaye hajui yeye
atakata tu kila akiuona mti mnene ndiyo anauona huu nitapata mkaa zadi. Kwa hiyo, Chuo cha Olmotonyi kifufuliwe kitoe wataalam zaidi na siyo wanafunzi wajisomeshe wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la wanyamapori. Mgogoro huu wa Loliondo, Ngorongoro naiomba Serikali kwa dhati kabisa ikae chini iamue inataka nini. Kama Serikali wanataka uhifadhi na maliasili zetu za Taifa zibaki kwa ajili yetu na kizazi kijacho basi iamue kutaka hivyo, kama Serikali inataka siasa iendelee na mchezo huu wanaoendelea nao. Suala la Ngorongoro, Loliondo linasababishwa na wanasiasa, tuwe wazi tuseme pale watu wana interest zao binafsi na hawaangalii, wakati hiyo mifugo ipo pale ilikuwa ni mifugo mingapi? Walikuwa ni watu wangapi wanaishi pale na leo ni wangapi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, Bismillah Rahman Raheem, nakushukuru kunipa fursa ya kuwa mchangiaji wa mwanzo kwa siku hii ya leo kwenye hotuba iliyo mbele yetu. Nisiwe mwizi wa fadhila nami niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na Watendaji wote wa Wizara ya Ardhi. Pongezi hizi zinatolewa kwa usimamizi mkuu wa wawili hawa au watatu hawa lakini wameshirikiana vizuri na watendaji wao ndiyo maana wakaweza kupongezwa na kila Mbunge anayesimama leo hii. Ni ombi langu kwao isije ikawa sifa ya mgema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la migogoro ya ardhi, kuna migogoro mingi sana ya ardhi hapa nchini, sina haja ya kuitaja lakini nataka nimshauri tu Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake sasa hizi sifa zao basi ziende katika kutatua haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama eneo la ardhi ndani ya nchi hii liliopimwa ni asilimia 15 ndiyo eneo ambalo limepimwa na kupangiwa matumizi ni dhahiri kwamba mna kazi kubwa ya kufanya ili kuweza kupima eneo kubwa zaidi na kupangiwa matumizi ili kupunguza hii migogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa faida za kupima ardhi na kupanga matumizi zimeonekana wazi, mimi kama Mjumbe wa Kamati nilipoenda Kilombero pale imeonekana tumejifunza, tumeona na wananchi wanafaidika sana, kwa sababu ile faida ya kupata Hati Miliki ya yale maeneo yao inawafanya wao sasa kuenda mbele kiuchumi na kufaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili sasa tatizo liko wapi, sasa hapa Mheshimiwa Waziri nadhani utanielewa wewe unaelewa vizuri zaidi lakini kwa mtazamo wangu mimi ninawaomba katika Serikali ni vizuri Waziri Mkuu leo yupo mkae katika Serikali, huu mkanganyiko wa kwamba watumishi wengi wa ardhi wako kwenye Halmashauri au wako chini ya Halmashauri ama TAMISEMI wako kule, na wewe sasa unataka kuipima ardhi ili wananchi wapate hati miliki pamoja na kupanga mipango ya ardhi na hawa watu sasa hawawajibiki moja kwa moja kwako, nani atawapatia vifaa vya kufanya hiyo kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri bajeti hii iko kwako, bajeti hii iko TAMISEMI, bajeti hii iko wapi? Sasa hili kama Serikali mkae ili kusiwe na conflict of interest hapa kwenye hii Wizara ama katika eneo hili ili vifaa vya kupimia ardhi vipatikane, wataalam wapatikane, ardhi ipimwe ili kuondoa matatizo. Serikali mpo Waziri Mkuu yupo mkae kama Serikali muondoe haya mambo ya kupeleka hawa TAMISEMI, hawa wapi, hawa wapi, mimi kwa mtazamo wangu ni mipango ya kiujanja ujanja iliyokuweko hapo, wekeni wazi hii Serikali ya Hapa Kazi Tu mfanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili niendelee kukupongeza kwa namna ambavyo umeweza kutumia busara na hekima kubwa kuwahamasisha wamiliki wa ardhi wakaweza kulipa kodi ya pango, ni kitu kimoja kizuri sana kimeleta tija na kila mmoja ameona faida yake. Tunakuomba uendelee kutumia approach hii ya kuwaelimisha na siyo nguvu, wanaomiliki ardhi kama ambavyo unatumia waendelee kulipa kwa faida ya nchi hii na pato la Taifa liongezeke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa utakapokuja kujumuisha utuambie wale ambao wanamiliki mashamba makubwa, wanamiliki ranchi lakini hawajaziendeleza, hawazifanyii kazi ni wangapi na je Serikali ina mpango gani? Pamoja na hayo nipendekeze kabisa kwamba mashamba yale makubwa ambayo hayajaendelezwa pamoja na ranchi yatumike sasa kuwagawia au kuwaazima kwa muda hawa wafugaji wakati mkiendelea kufikiria ili kupunguza migogoro na vita vya wakulima na wafugaji wakati kuna maeneo kama haya ambayo hayajaendelezwa na watu wanayamiliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuongelea suala la Kigamboni, ni takribani miaka tisa sasa wananchi wa Kigamboni kwenye ule mradi wa Kigamboni nyumba zao hawawezi kuziuza, hawawezi kutengeneza, hawawezi kufanya kitu chochote wanasubiri mradi, lakini ni miaka tisa mradi haujaanza, Mheshimiwa Waziri hatujui kwamba huu mradi utaendelea kuwepo au hautakuwepo. Kama hautakuwepo wananchi wale kwa muda wa miaka tisa mmewazuia kufanya chochote mtawafidiaje na kama utakuwepo katika kipindi chote hiki mtawafidiaje. Naomba Serikali ijipange hapa ili wananchi wale muwaondoe katika ugumu ule ambao mmewapa hivi sasa, wanakaa wanasubiri mradi, miaka tisa ni mingi sana kwa maendeleo ya mtu binafsi, kwa Serikali ni kidogo, lakini kwa maendeleo ya mtu binafsi ni miaka mingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la National Housing, ninaomba Serikali pia ipo, National Housing inafanya kazi moja kubwa sana na kila Mtanzania leo hii anaona kazi inayofanywa na National Housing, wanastahili sifa kweli, wanajitahidi sana. Kuna nyumba za gharama nafuu ambazo wananchi maskini wanatakiwa wanunue zile nyumba lakini ukiziangalia siyo za gharama nafuu kulingana na patol mwananchi wa Tanzania uwezo wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba hizi siyo za gharama nafuu kwa sababu ya mambo mengi, moja kama kodi ya VAT kwa vifaa vya ujenzi itaondolewa kwa watu hawa wa National Housing wataweza kujenga nyumba hizo na Mtanzania yeyote ataweza kununua, lakini kama kodi ya VAT haitaondolewa basi suala hili litaendelea kuwa gumu kwao. Vilevile gharama nyingine zinaongezeka wao wanapojenga zile nyumba wanaweka gharama za kuweka maji, umeme, barabara ambazo wao wanapaswa kuweka wenyewe. Sasa Serikali ipo, kama mmeamua kujenga nyumba hizo sehemu fulani, kwa nini Serikali haipeleki maji, ikapeleka umeme, ikapeleka barabara kwenye eneo lile kabla ya watu wa National Housing hawajaanza kujenga? Serikali ni moja lakini kwa nini kunakuwa na conflict of interest?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nchi za wenzetu wanafanya hivyo, ukienda nchi zote za Arabuni na Ulaya kabla ya lile eneo kuendelezwa huduma muhimu za barabara maji na umeme zinapelekwa kwanza, barabara, maji, umeme, shule, masoko yanapelekwa kwanza halafu ndiyo nyumba zinajengwa wananchi wanaenda kuhamia pale ikiwa huduma zote muhimu zipo. Kwa nini kwenye nchi yetu inashindikana?

Kwa hiyo, nikuombe tu Mheshimiwa Waziri kwamba hili nalo mliangalie katika Serikali ili watu hawa wafanye hiyo kazi kwanza kabla ya kupeleka ujenzi katika eneo basi huduma hizi muhimu ziende ili kupunguza gharama. Mkiendelea kwamba watu wa National Housing walipe gharama za kuvuta maji, walipe gharama za kuvuta umeme, walipe gharama za kutengeneza barabara, wananchi wa Tanzania kwa kipato chao wataendelea kushindwa kuzinunua nyumba hizi na mtazijenga mtaziweka zitakuwa hazileti ile faida iliyokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaunga mkono hoja ya Kambi Rasmi ya Upinzani, lakini niendelee kukupongeza Mheshimiwa Waziri nikuambie kaza kamba, narudia isije kuwa sifa ya mgema, tunategemea kipindi kijacho tuendelee kukusifu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Bismillah Rahman Rahim.

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na kabla sijaanza nina maombi, naomba uniongezee dakika kumi ili nitoe somo leo humu Bungeni. Pili, nakusudia kusema ukweli ili tuondoke hapa tulipo twende mbele na ukweli unauma kwa hiyo nakuomba univumilie na Wabunge wa pande zote wanivumilie. Kama umeniruhusu uniambie ili nijue najipanga vipi katika hoja zangu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nawaomba Wabunge kwanza tuache ushabiki wa kufuata ngoma. Naomba mnisikilize vizuri nitakayoyasema. Kama nchi yetu inapita katika kipindi kigumu au ilishawahi kupita, nchi yetu sasa hivi inapita katika kipindi kigumu sana. Vita hii ambayo Rais John Pombe Magufuli anaendelea nayo ni vita moja ngumu sana na yeye peke yake kama yeye hawezi kufaulu katika vita hii ni lazima Watanzania tushirikiane tukiwa kama Watanzania na siyo CCM, Wapinzani au nani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vita hii ni kubwa kwa sababu ni vita ambayo imekamatana na kitu ambacho ni fitna, kitu ambacho ni mali/fedha. Kwa hiyo hii ni vita moja kubwa sana ambayo ni lazima kama Watanzania tukae pamoja, Waheshimiwa ni lazima tuondoe tofauti zetu. Suala la wana CCM kutuona sisi Wapinzani kama maadui au wakoloni tunaotoka nchi nyingine tunataka kuitawala Tanzania halitatufikisha. Suala la sisi Wapinzani kuwaona CCM ni maadui, ni wezi, ni nani, ni nani halitatufikisha lazima tukawe kitu kimoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpasuko uliopo ndani ya nchi yetu hivi sasa kama hatujatumia busara, hekima na akili zetu, wallah wabillahi wataalah na hii Ramadhan, Tanzania ndiyo imefika mwisho wake hapa. Nayasema haya leo, wenye kuweka kumbukumbu waweke. Tulipo ni pabaya sana kuliko

kipindi chochote kile ambacho nchi yetu imepitia. Vita hii ni ngumu na vita hii inahitaji umoja wa kweli kweli. Tufanye nini ili tutoke katika mkwamo huu tuliokwama? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lazima turejeshe umoja wa Kitaifa. Hatuwezi kuondokana na matatizo haya kwenye nchi hii lazima tukae pamoja kama Taifa, tuache kubaguana kwamba huyu Mpinzani, huyu Chama Tawala ana nguvu au ana hiki! Tukae pamoja tuweze kuweka mfumo mmoja wa Kitaifa, tuwe na National vision, tunataka nini kama Taifa ili Rais Magufuli leo vita hii anayoyoiendeleza najiuliza baada ya miaka kumi akiondoka anayekuja ataiendeleza? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama hakuendeleza anayekuja tutakuwa tumefanya nini? Leo anakamatwa Chenge, anakamatwa Ngeleja, anakamatwa mwingine tunawatoa kafara. Mheshimiwa yaliyotokea ni mfumo na lazima Chama cha Mapinduzi kikubali kubeba lawama hii, tufike mahali tusameheane, tufike mahali tukae pamoja, ndiyo kwa sababu Chama cha Mapinduzi ndio kinachoongoza dola. (Makofi)


Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni lazima wakubali kubeba msalaba huu kwamba jamani tumekosea na tulipofika sasa tukae pamoja kama Taifa tuzungumze tuwe na mfumo mmoja wa Kitaifa ambao utatuondoa hapa tulipo kutupeleka mbele. Malumbano haya tunayoendelea nayo hatutafika hata siku moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpasuko huu, hawa wanaotajwa tajwa ni wanadamu, wanadamu, wana nyongo, wana fikra na wana watu nyuma yao, wanaumia, wanavumilia lakini ipo siku watasema, mwisho wa siku Taifa hili tutakuwa tunalipasua sisi wenyewe. Ni wakati sasa tukae pamoja kama Taifa, tuangalie tunataka nini katika kila sekta tuwe na vision tunataka nini.

Mheshimiwa Spika, leo akiwa Mheshimiwa Magufuli ndio Rais aende hapo atupeleke katika vision hiyo, kesho akija

Mlinga ndiyo Rais wa Tanzania atupeleke hapo, sitaki ushabiki nimesema Waheshimiwa, sio kwamba Mlinga amekuja anasema yeye kwa sababu ni mpenzi wa mpunga tunaondoka katika hapa leo tulime mpunga ili tusafirishe nje ya nchi, hapana! (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, tusiwe hivyo tuwe na National Vision ambayo kila Kiongozi anayekuja awe wa Chama Tawala, awe wa Upinzani anatupeleka hapo, tutakuwa tumeondokana na hili, vinginevyo narudia tena Wallah wabillah watallah vita hii hatutashinda na tutagawanyika na kama Taifa hili litatawanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa kuna fitna na mali ni fitna na hili Mwenyezi Mungu amesema hii ni fitna na tusipokuwa makini Taifa hapa ndio linafikia mwisho wake.

Mheshimiwa Spika, niseme hivi, namuunga mkono Mheshimiwa Rais Magufuli, katika vita hii na namuunga mkono kwa sababu ameamua kujitoa muhanga, nilikuwa nafikiri Rais Magufuli yupo katika zile sifa za unafiki lakini hayumo na ndio maana nikasema ni mfumo. Alipotoka kwa sababu kipindi kilichopita alikuwemo katika Baraza la Mawaziri, alikuwemo ndani ya Serikali na haya yote yanayotendeka leo yeye alikuwemo alisema? Alitakiwa aondoe kwa mkono wake wakati ule hathubutu, alitakiwa aseme hathubutu, lakini alichukia, leo amefika mahali anaweza kuondoa kwa mkono wake anaondoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, waliopo hawa Mawaziri hawa tusidanganyane hakuna mmoja anayeweza kumwambia Rais hili usifanye, hakuna!

Mheshimiwa Spika, mfumo ambao ulijengeka haumwezeshi Waziri yeyote aliyepita au Mwanasheria Mkuu au yoyote kuweza kumwambia Rais usifanye hili hayo ni makosa yametendeka na mwanadamu yeyote lazima afanye makosa ndio akawa binadamu, ambaye hafanyi makosa ni Mwenyezi Mungu. Kwa hiyo niwaombe, niwaombe ndugu zangu wa CCM mbadilike, mkubali kwamba Taifa hili ni letu sote tukae pamoja tuseme nini vision ya Taifa katika kila idara, katika kila sekta ili tujenge nchi yetu kwa pamoja. Malumbano hayatatusaidia, nguvu zenu za dola hazitasaidia na hapa Taifa litagawanyika na tutagawana mbao kuanzia hapa.

TAARIFA .....

MHE: YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa kwa sababu tatizo lililopo inapoletwa sheria hapa Bungeni, unapoletwa Muswada wowote hapa unakuja

na maagizo, inatakiwa Wabunge waachwe huru, wawe huru kujadili, wawe huru kuishauri Serikali, yasiletwe maagizo kwamba Caucus ya CCM ikutane twendeni hivi, Caucus ya UKAWA ikutane twendeni hivi, tuwe huru kujadili mawazo, kujadili masuala ya Taifa letu, mhimili huu usiingiliwe, Rais abaki na Muhimili wake, atuache Wabunge tuweze kusaidia Taifa hili. Tukienda na tabia hii tutalimaliza Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sehemu ya pili, naenda kwa Mheshimiwa Waziri, nimwombe Mheshimiwa Rais a-pause kidogo huko kwenye madini, kwa sababu huu uchafu na uozo huu upo nchi nzima, katika Wizara zote na Idara yote na Taasisi zote. Baada ya pato ambalo litapatikana huko kwenye madini na sehemu nyingine, upotevu na wizi wa namna hiyo hizo fedha zikipatikana zinaenda wapi? Zitakwenda Hazina, Wizara ya Fedha huko ndio kumeoza ndio kwenye wizi ndio kwenye ubadhirifu mbaya kupita wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Waziri waanze hapa, nataka tuiangalie Benki Kuu kuna matatizo, sitaki kuingia kwenye mambo ya watu sana hapo. Ninachotaka kusema tu, tuiangalie ndoa ya Benki Kuu na Bureau de Changes kuna nini hapa? Pia tuangalie ndoa ya TRA na hawa watu wa clearing and forwarding, kuna upotevu mkubwa wa fedha katika eneo hilo, Mheshimiwa Waziri aangalie tusafishe hapo ili fedha yetu itakapotoka hapo sasa kwenye madini, kwenye uvuvi, kwenye maliasili, kwenye kilimo ikienda pale Hazina tuwe na uhakika fedha yetu ni salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba univumilie nitapiga nikilegeza kidogo mshipa si msumari, lakini tunahitaji kuwa katika umoja huo ili tuondokane na hili tulilonalo. Naiomba Serikali kwa heshima zote, kwa heshima zote tuachane na kubaguana, tuachane na Rais leo kutuona sisi Wapinzani kama maadui, tukae pamoja tuweke mustakabali wa Taifa letu ili tuondoke hapa tulipo twende mbele.

Mheshimiwa Spika, nije kwenye kuchangia na kuielekeza Wizara katika mapato, suala la kukuza kilimo, ufugaji na uvuvi. Mheshimiwa Waziri amezungumza tu lakini hakueleza na ndio pale niliposema tunahitaji vision, je tunataka kukuza kilimo, lakini ni kilimo gani?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, Bismillah Rahman Raheem, nakushukuru kunipa fursa ya kuwa mchangiaji wa mwanzo kwa siku hii ya leo kwenye hotuba iliyo mbele yetu. Nisiwe mwizi wa fadhila nami niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na Watendaji wote wa Wizara ya Ardhi. Pongezi hizi zinatolewa kwa usimamizi mkuu wa wawili hawa au watatu hawa lakini wameshirikiana vizuri na watendaji wao ndiyo maana wakaweza kupongezwa na kila Mbunge anayesimama leo hii. Ni ombi langu kwao isije ikawa sifa ya mgema.

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la migogoro ya ardhi, kuna migogoro mingi sana ya ardhi hapa nchini, sina haja ya kuitaja lakini nataka nimshauri tu Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake sasa hizi sifa zao basi ziende katika kutatua haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama eneo la ardhi ndani ya nchi hii liliopimwa ni asilimia 15 ndiyo eneo ambalo limepimwa na kupangiwa matumizi ni dhahiri kwamba mna kazi kubwa ya kufanya ili kuweza kupima eneo kubwa zaidi na kupangiwa matumizi ili kupunguza hii migogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa faida za kupima ardhi na kupanga matumizi zimeonekana wazi, mimi kama Mjumbe wa Kamati nilipoenda Kilombero pale imeonekana tumejifunza, tumeona na wananchi wanafaidika sana, kwa sababu ile faida ya kupata Hati Miliki ya yale maeneo yao inawafanya wao sasa kuenda mbele kiuchumi na kufaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili sasa tatizo liko wapi, sasa hapa Mheshimiwa Waziri nadhani utanielewa wewe unaelewa vizuri zaidi lakini kwa mtazamo wangu mimi ninawaomba katika Serikali ni vizuri Waziri Mkuu leo yupo mkae katika Serikali, huu mkanganyiko wa kwamba watumishi wengi wa ardhi wako kwenye Halmashauri au wako chini ya Halmashauri ama TAMISEMI wako kule, na wewe sasa unataka kuipima ardhi ili wananchi wapate hati miliki pamoja na kupanga mipango ya ardhi na hawa watu sasa hawawajibiki moja kwa moja kwako, nani atawapatia vifaa vya kufanya hiyo kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri bajeti hii iko kwako, bajeti hii iko TAMISEMI, bajeti hii iko wapi? Sasa hili kama Serikali mkae ili kusiwe na conflict of interest hapa kwenye hii Wizara ama katika eneo hili ili vifaa vya kupimia ardhi vipatikane, wataalam wapatikane, ardhi ipimwe ili kuondoa matatizo. Serikali mpo Waziri Mkuu yupo mkae kama Serikali muondoe haya mambo ya kupeleka hawa TAMISEMI, hawa wapi, hawa wapi, mimi kwa mtazamo wangu ni mipango ya kiujanja ujanja iliyokuweko hapo, wekeni wazi hii Serikali ya Hapa Kazi Tu mfanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili niendelee kukupongeza kwa namna ambavyo umeweza kutumia busara na hekima kubwa kuwahamasisha wamiliki wa ardhi wakaweza kulipa kodi ya pango, ni kitu kimoja kizuri sana kimeleta tija na kila mmoja ameona faida yake. Tunakuomba uendelee kutumia approach hii ya kuwaelimisha na siyo nguvu, wanaomiliki ardhi kama ambavyo unatumia waendelee kulipa kwa faida ya nchi hii na pato la Taifa liongezeke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa utakapokuja kujumuisha utuambie wale ambao wanamiliki mashamba makubwa, wanamiliki ranchi lakini hawajaziendeleza, hawazifanyii kazi ni wangapi na je Serikali ina mpango gani? Pamoja na hayo nipendekeze kabisa kwamba mashamba yale makubwa ambayo hayajaendelezwa pamoja na ranchi yatumike sasa kuwagawia au kuwaazima kwa muda hawa wafugaji wakati mkiendelea kufikiria ili kupunguza migogoro na vita vya wakulima na wafugaji wakati kuna maeneo kama haya ambayo hayajaendelezwa na watu wanayamiliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuongelea suala la Kigamboni, ni takribani miaka tisa sasa wananchi wa Kigamboni kwenye ule mradi wa Kigamboni nyumba zao hawawezi kuziuza, hawawezi kutengeneza, hawawezi kufanya kitu chochote wanasubiri mradi, lakini ni miaka tisa mradi haujaanza, Mheshimiwa Waziri hatujui kwamba huu mradi utaendelea kuwepo au hautakuwepo. Kama hautakuwepo wananchi wale kwa muda wa miaka tisa mmewazuia kufanya chochote mtawafidiaje na kama utakuwepo katika kipindi chote hiki mtawafidiaje. Naomba Serikali ijipange hapa ili wananchi wale muwaondoe katika ugumu ule ambao mmewapa hivi sasa, wanakaa wanasubiri mradi, miaka tisa ni mingi sana kwa maendeleo ya mtu binafsi, kwa Serikali ni kidogo, lakini kwa maendeleo ya mtu binafsi ni miaka mingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la National Housing, ninaomba Serikali pia ipo, National Housing inafanya kazi moja kubwa sana na kila Mtanzania leo hii anaona kazi inayofanywa na National Housing, wanastahili sifa kweli, wanajitahidi sana. Kuna nyumba za gharama nafuu ambazo wananchi maskini wanatakiwa wanunue zile nyumba lakini ukiziangalia siyo za gharama nafuu kulingana na patol mwananchi wa Tanzania uwezo wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba hizi siyo za gharama nafuu kwa sababu ya mambo mengi, moja kama kodi ya VAT kwa vifaa vya ujenzi itaondolewa kwa watu hawa wa National Housing wataweza kujenga nyumba hizo na Mtanzania yeyote ataweza kununua, lakini kama kodi ya VAT haitaondolewa basi suala hili litaendelea kuwa gumu kwao. Vilevile gharama nyingine zinaongezeka wao wanapojenga zile nyumba wanaweka gharama za kuweka maji, umeme, barabara ambazo wao wanapaswa kuweka wenyewe. Sasa Serikali ipo, kama mmeamua kujenga nyumba hizo sehemu fulani, kwa nini Serikali haipeleki maji, ikapeleka umeme, ikapeleka barabara kwenye eneo lile kabla ya watu wa National Housing hawajaanza kujenga? Serikali ni moja lakini kwa nini kunakuwa na conflict of interest?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nchi za wenzetu wanafanya hivyo, ukienda nchi zote za Arabuni na Ulaya kabla ya lile eneo kuendelezwa huduma muhimu za barabara maji na umeme zinapelekwa kwanza, barabara, maji, umeme, shule, masoko yanapelekwa kwanza halafu ndiyo nyumba zinajengwa wananchi wanaenda kuhamia pale ikiwa huduma zote muhimu zipo. Kwa nini kwenye nchi yetu inashindikana?

Kwa hiyo, nikuombe tu Mheshimiwa Waziri kwamba hili nalo mliangalie katika Serikali ili watu hawa wafanye hiyo kazi kwanza kabla ya kupeleka ujenzi katika eneo basi huduma hizi muhimu ziende ili kupunguza gharama. Mkiendelea kwamba watu wa National Housing walipe gharama za kuvuta maji, walipe gharama za kuvuta umeme, walipe gharama za kutengeneza barabara, wananchi wa Tanzania kwa kipato chao wataendelea kushindwa kuzinunua nyumba hizi na mtazijenga mtaziweka zitakuwa hazileti ile faida iliyokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaunga mkono hoja ya Kambi Rasmi ya Upinzani, lakini niendelee kukupongeza Mheshimiwa Waziri nikuambie kaza kamba, narudia isije kuwa sifa ya mgema, tunategemea kipindi kijacho tuendelee kukusifu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na kwa sababu ya muda itabidi niende haraka haraka sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naunga mkono taarifa ya Kamati zote mbili kwa asilimia mia moja. Pili, suala hili amelizungumza mwanangu Ndassa lakini kalizungumza kwa Kisukuma sikulielewa vizuri. Tunachokitaka maazimio tuyayoyapitisha katika Bunge hili yaundiwe Kamati ambayo itayasimamia. Kwa sababu hivi sasa tunapitisha tukiondoka hapa yamepita, tukirudi tena hakuna aliyenayo, hayasimamiwi, hatujui Serikali imetekeleza lipi na imeacha lipi. Kenya wana mfumo huu, kwa hiyo, iundwe Kamati ya Bunge ambayo itakuwa inasimamia maamuzi na maazimio yanayopitishwa na Bunge, hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine niseme tu mimi sijui tuna laana gani sisi Watanzania na miaka 60 ya Uhuru sasa tunayokwenda nayo bado tuna matatizo ambayo sisi wenyewe tunajitakia. Wizara ya Ardhi sasa hivi na hii Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi na Maji tutaendelea kuzilaumu kila siku kama hatuzipatii fedha zikafanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi anafanya kazi vizuri, lakini anakwama kwa sababu ya fedha. Sasa atalaumiwa kila siku, watu watapigana, watauana kwa sababu anashindwa kupima ardhi kwa sababu ya fedha, apewe fedha afanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii Wizara hii ya Kilimo ya Mpina kama hawajapewa fedha hawa za kutosha hatuwezi. Kama hatujapanga leo maana niseme sijui tuna laana gani Libya walikuwa wanachukua maji kutoka Mto Nile ambao umeanzia kwetu wanajitosheleza kwa chakula na matunda yote siye Tanzania tuna mito na maziwa mangapi hapa tunashindwa, tupange fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabadiliko ya tabia nchi yanayojitokeza katika nchi yetu, mwaka huu mahindi hayana bei, mbaazi hazina bei, tumbaku haina bei na vitu vingi tu. Mwakani hapa mabadiliko ya tabia nchi tutakuwa na dhiki ya chakula kama wangepewa fedha hawa wakanunua hivi vyakula wakaweka katika Hifadhi ya Taifa vingetufaa mwakani kukitokea tatizo, hakuna, fedha tunakusanya hatujui. Kwa hiyo, hebu tukaeni chini sasa kama Watanzania jamani tunataka nini, tujipange miaka 60 inatosha si watoto tena katika Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni misitu. Naomba Serikali misitu yote nchini isimamiwe na taasisi au mamlaka moja, halafu hiyo mingine iendelee tu, ile ya kijiji ibaki kuwa ya kijiji, ya Halmashauri ibaki kuwa ya Halmashauri lakini kuwe na msimamizi mmoja ili zile sheria zinazohusiana na masuala haya ya misitu zisimamiwe. Tanzania nadhani tunapoteza hekta laki tatu na nusu kila mwaka kwa matumizi tofauti lakini upandaji wetu sidhani kama tunafika hata hekta laki moja kwa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukichukulia hilo na hiyo miti ambayo ni fast growing trees ukiipanda inaweza ikachukua zaidi ya miaka sita ndiyo unaanza kuvuna, nchi yetu baada ya miaka 20 ijayo tutakuwa katika hali gani? Sasa kama sisi tunavimba kichwa kusema kwamba tuna asilimia 35, sijui 52 ya misitu katika nchi yetu lakini na matumizi ni makubwa, ongezeko kubwa la watu mahitaji ni makubwa.

Kwa hiyo, ni lazima matumizi yetu yaendane na upandaji wetu na tuone kwamba mti tukiupanda leo hatuvuni leo rahisi kabisa ni baada ya miezi sita, kwa hiyo, lazima tuwe makini katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala lingine, Mheshimiwa Musukuma kamzungumzia sana Waziri Mpina, mimi nampa tena ushauri Mheshimiwa Waziri wa Maliasili. Mheshimiwa Waziri nilikupa ushauri ndani ya Kamati, nakupa ushauri leo ndani ya Bunge. Nikwambie Wizara hii ya Maliasili na Utalii ni yai viza. Yai viza lina matumizi mazuri sana kwa wanaolitumia lakini yai viza ukilikosea linanuka vibaya sana. Nikushauri tu Mheshimiwa Waziri uwe mtulivu, hii Wizara haitaki amri, haitaki nguvu, haitaki ubabe na haitaki hasira, hii Wizara ni lazima utulie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwa nawashauri humu ndani kwamba ndani ya Wizara hii lazima mkae mafiga matatu. Community iseme inataka nini, Serikali iseme inataka nini, mwekezaji aseme anataka nini, nyote watatu mkae mseme mnataka nini ili mwende kwa pamoja. Sasa ukichukulia nguvu ukasema leo kwamba kwa mfano tu, nafunga vitalu vya uwindaji, kesho unasema nawaachia mwaka mmoja, kesho kutwa nawaachia miaka miwili, hii biashara ni nyepesi sana kuharibika na ndiyo nikasema ni yai viza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lazima utulie vizuri sana na hizi figure tatu, hii triangle zikae kuweka mkakati wa tunakwenda vipi vinginevyo utakuwa ni Waziri ambaye umetumikia Wizara hii muda mfupi sana. Kwa sababu imebeba uchumi wa Taifa letu, ukikoroga kidogo tu katika sekta hii unakoroga system nzima ya utalii na ukikoroga system nzima ya utalii umekoroga uchumi wa nchi yetu ambao asilimia sasa hivi zaidi ya 20 inatokana na utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nikushauri ukae vizuri, uwe makini, tupo ambao tumeshafanya kazi katika sekta hii, tupo ambao tumesoma, tutakushauri vizuri kwa nia safi kabisa ili twende mbele. Suala hili la kutumia nguvu ukaona labda ni sifa unapotumia nguvu si sifa unajiharibia na ukijiharibia wewe, unaliharibia Bunge, unaiharibia Serikali na unaiharibia nchi yote ya Tanzania. Kwa hiyo, nakushauri tu kwamba utulie vizuri sana sisi tutakusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala lingine la wawekezaji. Mtu ameshapewa vibali vyote vya kujenga lakini kuna tatizo la hii Environmental Impact Assessment inachelewa, mwekezaji anakaa miaka miwili, mitatu hajapewa hiyo, sasa atajenga lini huyu? Kwa hiyo, hili benchi la kutoa vibali vya ujenzi bora lote likae pamoja ili mwekezaji akipata kitu apewe kwa pamoja anaenda kuwekeza tujue kwamba mwekezaji…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, mwekezaji akishawekeza labda kwa miaka mitatu amejenga anahitaji tena miaka miwili kufanya marketing kupata wageni hapa. Kwa hiyo, naomba sana Serikali itulie vizuri, ijipange, muda unatosha, tuko tayari kuishauri vizuri Serikali kwa minajili ya faida ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Bismillah Rahman Rahim. Nataka kumshauri tena Mheshimiwa Waziri na naomba anisikilize vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1979 nikiwa na umri wa miaka 14, nilifika katika uwanja wa mapambano ambapo wanajeshi wetu walipambana na majeshi ya Iddi Amin. Miaka 40, mwaka huu mwezi Machi, nilifika tena katika maeneo yale, nikamwomba Mwenyekiti wangu tutembelee maeneo ya makaburi kule Kaboya. Nikatembea na Kamati. Tulitoka Kaboya, baada ya kumaliza mpaka barabarani, hakuna mtu anaongea na mwenzake ndani ya gari. Sasa asiyejua kufa, aangalie kaburi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, anaposema kwamba kuna usalama ndani ya mipaka yetu, sikubaliani naye unless yeye na Jeshi lake na makamanda wake, wanipe tafsiri ya usalama ni nini? Maana labda kufa mtu mmoja mpaka 54 kwao bado ni amani. Mimi sikubaliani kabisa kama kuna amani. Haiwezekani Mtanzania afe ndani ya ardhi yake kwa sababu ya mali yake, halafu watuambie kuna amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Waziri wa Maliasili. Kama mimi ndio ningekuwa Waziri siku ile, ningetoa kauli mbaya zaidi kuliko ile. Haiwezekani Watanzania wenzetu wanauliwa ndani ya ardhi yao kwa mali yao halafu tunasema tuna amani. Kwa sababu gani? Mimi sikubaliani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, anapaswa ajipange, hii ndiyo nchi. Hii Wizara anayoiongoza yeye hii ndiyo nchi, jeshi ndiyo nchi, haya maringo na kujidai kwetu ni kwa sababu ya hawa. Sasa bila hawa, hatuna amani, hatuwezi kuwa na nchi. Sikubaliani kabisa na Mheshimiwa Waziri na namwomba sana, hawa makamanda, miaka 40 hiyo iliyopita, mimi nimeenda kule wengine hawakuwa Wanajeshi na wengine ndiyo wanaanza Jeshi. Awapeleke kule wakaone yale makaburi, ndiyo watajua jeshi ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna matatizo kwenye mipaka yetu. Namwomba Mheshimiwa Waziri na Wizara, wadau wenzake, zile barabara, kilometa 54 za mpakani, ile barabara ijengwe ili Wanajeshi wetu na Kamati ya Ulinzi na Usalama katika Wilaya ile ya Misenyi iweze kufanya patrol ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Waziri, akae na Wizara zote, kama ni Ardhi, Miundombinu na kadhalika, wajenge ile barabara. Tumekwenda kule, huwezi kufika. Sasa likitokea lolote, wanajeshi wetu watakufa, hawajapata usaidizi. Haiwezekani, hakuna amani. Namwambia Mheshimiwa Waziri, hakuna amani, lakini kwa sababu ya muda, sitasema sana, ningechambua sana hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, bajeti iliyopita nilimwonesha vyanzo vya fedha nikamwambia UN Mission ni fedha. Kuna nchi kama Bangladesh zinaendesha nchi zao kwa UN Mission tu. Mheshimiwa Waziri, anunue vifaa. Kila kifaa kinalipwa katika UN Mission. Tuna Wanajeshi wetu katika UN Mission, kwa nini tunakosa fedha za kuendesha Jeshi? Haiwezekani. Hilo moja la mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile vifaa hakuna. Wanajeshi wetu walioko katika vita hawana vifaa. Ushahidi ni huu wa DRC. Haiwezekani Wanajeshi wetu wavamiwe, ndani ya masaa 13, wanapigana hakuna mawasiliano, hakuna rescue. Thirteen hours Wanajeshi wanapambana mpaka wanaishiwa risasi, wanakuja kufa, ni uzembe. Inauma kweli kweli! Sisi ambao tumeshuhudia maeneo yale ya vita, inatuuma. Mtanzania mmoja kufa, inatuuma! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani, ule ni uzembe. Mheshimiwa Waziri akituambia kwamba sijui walivamiwa, mimi sikubali, najua ni uzembe. 13 hours Askari wa kulinda amani anapigana, ana silaha ya kawaida tu, ana risasi 90. Anapigana kwa uadilifu, wamejipanga kwa sababu ni weledi, 13 hours, hakuna rescue, halafu Mheshimiwa Waziri anatuambia nini hapa? Sikubaliani na hili, Mheshimiwa Waziri, anunue vifaa, Wanajeshi wetu waende wafanye kazi kwa uangalifu, lakini pia ni faida vile vile kwa Taifa. Hivyo, Mheshimiwa Waziri anunue vifaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ambalo nataka niliseme na hili tutakuja kupambana sana kwenye mshahara wa Mheshimiwa Waziri. Nilisema Wanajeshi hawa, wapatiwe angalau bima basi. Haiwezekani, mwanajeshi anastaafu anadhalilika, anasawajika.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, Bismillah Rahman Rahim. Kwanza ni-declare interest ni Mjumbe wa Kamati kwa hiyo naunga mkono hoja za Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, sina kawaida ya kupongeza lakini leo nitampongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake na watendaji wake kwa namna ambavyo Mheshimiwa Waziri na timu yake anakuja sasa kuielewa hii Wizara na kufanya kazi inavyotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ni-declare interest kwamba ni mtaalam wa misitu, nimesoma na nimefanya kazi, pia ni mtaalam wa mambo ya hoteli, nimesoma na nimefanya kazi. Kwa hiyo, nitachangia kitaalamu zaidi kuliko kisiasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania inapoteza hekta 370,000 za misitu kila mwaka kutokana na matumizi mbalimbali. Ukilinganisha na hekta 10,000 zinazopandwa kwa mwaka hujatoa hapo loss percentage, miti inayokufa na itachukua muda gani, utaona ni kwa kiasi gani Tanzania baada ya miaka mingapi tutakuwa hatuna misitu katika nchi yetu na tutapoteza maliasili hii. Maliasili hii ikipotea ndiyo kusema wanyama na wanadamu wa Tanzania watatoweka kwa sababu kutakua hakuna malisho, maji na hakuna kitu chochote. Kwa hiyo, jukumu la upandaji miti na utunzaji wa misitu ni la kila Mtanzania na siyo la Wizara peke yake. Kwa hiyo, Wabunge, taasisi na kadhalika ni lazima tuhakikishe kwamba tunapanda miti ya kutosha na tunaitunza na tunaitumia vizuri kwa faida yetu na faida ya kizazi kijacho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufanikisha hili, nimwombe Mheshimiwa Waziri sasa, kwa upande wake haya ni majukumu yake, tuna vijiji zaidi ya 13,000 Tanzania na vijiji na Serikali za Mitaa huko ndiyo zinamiliki 52% ya misitu, nani anaitunza, anashauri na anawaelekeza matumizi endelevu ya misitu? Tunapaswa kuwasomesha watu na kuhakikisha kwamba kila kijiji na halmashauri ina mtaalamu wa misitu ili atoe elimu inayofaa ya matumizi mazuri ya misitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania idadi yetu inaongezeka na mahitaji yanaongezeka kila siku. Kwa hiyo, ni lazima tuhakikishe kwamba miti hii tunaitunza vizuri kwa faida yetu. Mtu akikwambia hajui faida ya msitu huyo anajidanganya maana yake mlango katika nyumba yake ni misitu, lakini nije mwisho tu siku anapoondoka duniani awe Muislamu, awe Mkristu ataondoka na ubao tu. Kwa hiyo, ni lazima suala hili tuliangalie vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mabibi na mabwana misitu 672, imeelezwa katika ukurasa wa 45 wa kitabu hiki. Mheshimiwa Waziri ni dhahiri kwamba bado tuna kazi kubwa ya kufanya. Tuboreshe Chuo cha Misitu Olmotonyi, Chuo cha Nyuki Tabora na Chuo cha Mbao pale FITI Moshi ili kupata wataalam wengi wa masuala haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nije katika sekta ya utalii ambayo ni sekta ngumu sana. Ni sekta tete sana na ndiyo maana nimekupongeza kwa sababu umetulia na ukataka kujua sasa katika sekta hii kuna nini. Tanzania tumeelekeza nguvu zetu katika utalii kwenye mbuga tu. Katika kitabu hiki amegusagusa tu utalii wa fukwe, lakini tujiulize siku ikitokea interaction ndogo tu katika mbuga watalii wakakaa mwezi mmoja au miwili hawataki kwenda huko kwa sababu yoyote tu, tunategemea wapi wakati asilimia kubwa ya pato la Taifa tunategemea kwenye utalii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri na Serikali naomba mkae na mpange namna gani mtawekeza katika ukanda wa bahari kuanzia Mtwara mpaka Tanga kuona tunaweka hoteli na tunaboresha vituo vya kitalii pale. Kuna utalii wa fishing, kuna diving, kuna snorkeling, lakini kuna utalii ule wa fukwe ambao ni mkubwa sana, hatujawekeza huko tunaelekea upande mmoja. Biashara ya utalii ni biashara ambayo inaweza ikayumba wakati wowote kwa sababu ndogo sana. Kwa hiyo, ni lazima tuwekeze sehemu zote kwa usawa kabisa vinginevyo tutakuja kujikuta tumetumbukia katika dimbwi ambalo siyo zuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini biashara hii inahitaji wataalam. Kwa hiyo, nasisitiza tena Chuo kile cha Utalii lazima kitoe wataalam wa kutosha ambao wataweza kuwahudumia wageni wetu. Mtalii anapokuja hapa haangalii amelala katika hoteli ya ukubwa gani, anaangalia ile service anayopewa hata kama amelala katika chumba kimeezekwa makuti lakini anaangalia ile service. Bila ya kuwa na wataalam waliofundishwa, ni dhahiri kwamba wageni wetu watakapokuja hapa watakosa zile huduma zinazotakiwa na wakizikosa itakuwa hatupati ile tija tuliyoitaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunategemea tufike watalii 2,000,000 au 3,000,000 ikifika 2020-2030, linawezekana hilo kama tutahamasisha utalii wa baharini. Ukanda wa bahari tukihamasisha basi tunaweza kufikia hapo katika kipindi kifupi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuwekeza huko katika ukanda, katika kuhamasisha ndiyo Mheshimiwa Waziri na Naibu wako, Katibu Mkuu, mtoke sasa muende nje, lazima tupate serious investors. Tukipata serious investors wakawekeza katika ukanda huo na wakahamasisha hilo maana yake wale wageni watakaowaleta ni wa daraja la kwanza na daraja la pili. Hivyo, idadi ya fedha tutakayopata itakuwa ni kubwa zaidi kulingana na wageni labda milioni tano, sita ambao watakuja, hawa wageni vishuka wanaokula mihogo ya kuchoma barabarani. Kwa hiyo, tuwe na serious investors ili walete wageni ambao wataleta fedha nyingi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kengele umeshanipigia nimalizie kwa kumshauri Mheshimiwa Rais kajenga Uwanja wa Ndege Chato, ni vizuri sana na navyoamini utatanua utalii katika ukanda ule na hiyo ndiyo nia lakini kujenga uwanja wa ndege tu kama hataboresha zile barabara…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya tatu asubuhi ya leo, mbele ya ma-sterling. Lakini nashukuru leo nachangia mpango wakati Waziri Mkuu yumo humu ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikisema mara nyingi na tumekuwa tukiishauri Serikali mara nyingi juu ya nchi yetu twende vipi, lakini Waheshimiwa kabla sijachangia nataka niwaeleze Waheshimiwa Wabunge kwamba tunailaumu Serikali hii na zaidi Serikali ya Awamu ya Tano lakini mimi naona wa kulaumiwa ni sisi Wabunge, je, Wabunge tunatimiza wajibu wetu? Kazi yetu sisi Wabunge kwa mujibu wa sheria kwa mujibu wa Katiba ni kuisimamia Serikali, je, tunaisimamia Serikali hii? (Makofi)

Kwa hiyo Bunge hili limeshindwa kutekeleza wajibu wake na ndio maana Serikali ikayumba hiyo, hiyo Serikali kama inayumba haifanyi vizuri ni kwa sababu sisi Wabunge tumeshindwa, kwa hiyo, Bunge hili limepoteza nguvu yake, limepoteza hadhi yake, tunashindwa kuisimamia Serikali na ndio maana Serikali inafanya itakavyo. Haiwezekani Bunge hili tupitishe bajeti, sisi sheria inasema, Katiba inasema kwamba tukishapitisha bajeti tuisimamie Serikali, Serikali haifanyi halafu tunaiachia tu hiyo Serikali. Wabunge hatujiamini, tumegawanyika, hatujui wajibu wetu na sidhani kama tunafaa kuwa katika Bunge hili wote humu ndani. Haiwezekani huo ndio wajibu wetu sisi kuisimamia hii Serikali na hatuisimamii, kwa hiyo, Serikali inafanya itakavyo kwa sababu msimamizi ambao ni sisi Wabunge hatufanyi kazi yetu. Tujitathmini sisi wenyewe.

Mheshimiwa Mpango mimi nakushauri tena, na naiambia tena Serikali na Waziri Mkuu yupo, ubaguzi huu tunaokwenda nao kwenye nchi hii kubaguana, kutoshirikiana hatuwezi kufikia maendeleo kamwe na kama nchi. Ni lazima tukae kama nchi, tuwe na mpango angalau wa miaka 50 tutakaokubaliana kwamba huu ndio Mpango wa Taifa, hii ndio vision ya Taifa, Rais yeyote, Waziri yeyote, Mkuu wa Mkoa yeyote, kiongozi yeyote anaekuja aende hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwa natoa mifano mara zote, Serikali ya awamu ya nne tulikopa fedha nje ya nchi kwa sababu ya gesi. Leo kaja Rais ana interest nyingine gesi tumeacha Deni la Taifa, hatuwezi kwenda na huwa nasema huwezi kupima maendeleo ya nchi kwa miaka miwili, mitatu, mitano au kumi ni lazima tuwe na mpango ambao kwa muda wa miaka 50 Rais yeyote anayekuja, Waziri yeyote anayekuja, kiongozi yeyote anayekuja ataenda hapo. Sasa kama hatuko hivyo sisi tunaendelea kubaguana tu hapa, tunaendelea kuwawinda wapinzani, tunaendelea kusema huyu mbaya, huyu hivi, hatuwezi kufikia maendeleo, ni lazima tuache tofauti zetu kama Watanzania tunataka maendeleo tukae kitu kimoja tuweke vision tunataka nini ndani ya nchi yetu. Ubaguzi huu unaoendelea hatuwezi kufika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nikwambie kama kitabu hiki cha Bunge maana yake ushauri wa Kamati ya Bunge ndio Bunge lenyewe kama huu tutaufuata haya yaliyomo humu tu basi nchi yetu itaondoka hapa ilipo na kupiga hatua mbele. Lakini niulize vitabu kama hivi vimeandikwa vingapi na kipi kimetekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi nikuombe pamoja na kwamba nazungumza hunisikilizi, nikuombe Bunge hili tukitoka tuseme kwamba hili Bunge limeiagiza Serikali moja, mbili, tatu. Tukija Bunge la Januari hapa katika Mkutano wa Kumi na Nne kama Serikali, turudie kwanza yatokanayo na Bunge la Kumi la Tatu je, Serikali tulitaka mfanye hivi mmefanyaje? Kama Serikali haikufanya basi sisi tuchukue hatua kama Bunge kama tunataka maendeleo. Hatuwezi hivyo Waheshimiwa hii ni mark timer tunadanganyana. Ukisoma hiki kitabu cha Kamati watu wamekaa, wameandika vitu vizuri, vitu vya maana, vitu ambavyo vitatupeleka kwenye maendeleo ya kweli ya nchi yetu, lakini hakuna hata kimoja kinachofanyika.

Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Dkt. Mpango, hebu kaeni, hebu Waziri Mkuu tuondoeni hizi tofauti zetu za kisiasa tulizonazo tukae kama Taifa moja tupange mipango ya nchi yetu tujueni tunakwenda vipi, anayekuja kiongozi yeyote aende hapo isiwe kila mtu anakuja na interest zake hatuwezi kufika. Huwa siku zote naisema na nakuomba hebu tuweke majaribio tu Bunge hili tuliagize Serikali halafu Bunge lijalo tuiulize Serikali kama itakuwa imefanya. Kwa hiyo, hatuwezi kwenda katika mfumo huo tukapata maendeleo kama Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiyumkiniki nchi zina miaka 48 ya Uhuru wao wana chumi 2 wana mafuta na dhahabu, lakini wametupita mara 5930 sisi tuna miaka 57 ya Uhuru bado tunapiga mark time eti leo Tanzania asilimia 16 ya ardhi ya Tanzania maji, lakini Mbunge anasimama hapa anaomba maji kwa Waziri wa Maji si aibu hiyo? Nchi hii kuna mikoa inalalamika njaa wakati asilimia 53 ya nchi hii ni ardhi ambayo ni productive land.

Kwa hiyo, hatujajipanga sisi wenyewe na tunakaa sisi wenyewe na kutegemea labda misaada, mikopo na ufadhili lakini sisi wenyewe kama nchi hatujajipanga na hatuwezi kufikia hapo kwa mfumo huu wa kubaguana, kwa mfumo huu wa kunyoosheana vidole lazima tukae kama Taifa Waheshimiwa mimi naomba tujiulize tuna laana gani kwenye nchi hii kila kitu tunacho kila kitu tunacho labda tunapitwa na kwa Afrika tunapitwa na DRC tu, labda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nchi nyingine zote tena kwa item moja moja tu lakini vitu vyote tunavyo tuna misitu ya kutosha, tuna maji ya kutosha, tuna ardhi ya kutosha ya kilimo hasa nini tunakuwa hivi ni kwa sababu Serikali hamjaamua sasa na kwa sababu sisi Wabunge tupo hivi labda tuiombe Serikali sasa tuwapigie tena magoti muamue kukaa chini ebu mje tuweke Mpango wa Taifa ambao utatupeleka.

Narudia atamaliza miaka kumi Rais Magufuli pamoja na nguvu yote anayoitumia ataacha hivi hivi katika lawama, lakini ebu tujeni akiondoka Rais Magufuli kama ameazisha hiyo reli ya kati atakayekuja aendeleze asije akaiacha hapa Dodoma kama itakuwa imefika ili tufikie sasa ile lengo, lakini hivi tunavyokwenda hatuwezi kwenda. Mimi napenda kumshauri Waziri katika mambo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, pato letu dogo kama nchi mahitaji makubwa mahitaji ni makubwa, kwa nini tunaenda kwenye miradi mikubwa ambayo inagharimu pesa nyingi na itachukua pesa nyingi na itachukuwa muda mrefu kuanza kuzalisha tusiende katika miradi midogo ambayo itazalisha kwa muda mfupi? Nilisema hapa kwa mfano kama tutajenga mahoteli 100 katika ukanda ule wa bahari Dar es Salaam au Mtwara mpaka Tanga tukajenga mahoteli 100 hali yanachukua mwaka moja kuyajenga baada ya mwaka tunaanza kuzalisha tunaanza kupata fedha ambazo tutazipeleka kwenye Stiegler’s Gorge, tutazipeleka kwenye reli na mambo mengine. Leo tunaanza kufanya miradi ambayo inachukua labda miaka mitano, miaka 10 haijamaliza inakula fedha halafu hatuna njia nyingine ya kupata fedha kwa nini tunaunga kimo kwa kwa kinu? Mheshimiwa hebu twendeni kwenye miradi midogo midogo ili tupate tija kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Azimio la Bunge la Kuridhia Ubadilishaji Hadhi Mapori ya Akiba ya Biharamulo, Burigi, Kimisi, Ibanda na Rumanyika – Orugundu kuwa Hifadhi za Taifa
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata dakika tano na bila kupoteza muda niunge mkono maamuzi haya ya Serikali, niipongeze Serikali, niipongeze Wizara kwa uamuzi huu.

Mheshimiwa Spika, katika mchango wangu kwa sababu ni mtaalam na mimi katika sekta ya Maliasili na Utalii basi nitatoa angalizo na ushauri zaidi na dakika tano ulizonipa ni kidogo lakini nitajaribu kuzitumia vizuri.

Mheshimiwa Spika, la kwanza, naomba Serikali iiangalie hii TANAPA kwa macho mawili sasa kwa sababu tunaiongezea mzigo TANAPA, ni sawasawa na gari unaliongezea shehena ya mzigo, kwa hiyo ulaji wake wa mafuta, tyres na break utaongezeka zaidi. Kwa hiyo, TANAPA iangaliwe kwa macho mawili kwa sababu matumizi yake yatakuwa ni makubwa zaidi. Tukumbuke kwamba TANAPA ina hifadhi 16 na ni tano tu ndiyo zinazojitegemea zilizobakia zote zinategemea huku. Kwa hiyo, uwezo wa TANAPA kurudisha kwenye Serikali utakuwa mdogo na lazima tuiangalie kwa macho mawili.

Mheshimiwa Spika, kitu cha pili ambacho naiomba Serikali hiki ikifanye kwa umakini mkubwa na kitapunguza gharama, ni ushirikishwaji wa wananchi katika zoezi hili. Ningependa hifadhi hii iwe ni hifadhi ya mfano sasa katika Taifa ili kuondoa yale malalamiko yote yaliyokuwepo katika hifadhi. Sitaki kuamini kwamba ushirikishwaji wa wananchi umekamilika au wameshirikishwa kikamilifu. Sijui approach iliyotumika, nimesoma kabrasha lote sijaona, lakini niseme tu kwamba kama wananchi watashirikishwa kikamilifu na wakapewa alternative nyingine za maisha yao, wao ndiyo watakuwa walinzi wa kulinda hili.

Mheshimiwa Spika, nimeshamshauri Mheshimiwa Waziri mara nyingi, Zanzibar katika mapori tulikuwa na walinzi zaidi ya 30 sasa hivi kila pori linalindwa na walinzi watano kwa sababu wananchi wenyewe ndiyo wanaolinda maeneo yao, lakini wamepangiwa na wameshirikishwa. Sasa sijui samples maana yake nimesoma ameshirikisha Kamati za Ulinzi na Usalama, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya lakini hajataja kijiji hata kimoja ambacho ameshirikisha na ametumia approach gani kuwashikirikisha wananchi na kwa kiasi gani na wao wametoa maoni yao na kukubali, kwa sababu ni lazima itapishana, vijiji 48 kila kijiji kina mahitaji yake tofauti.

Mheshimiwa Spika, uthibitisho katika hilo ukisoma ukurasa wa 15 na ukurasa wa 17, kwenye fungu lile 314 na fungu 332 litakupa uthibitisho kwamba ushirikishwaji wa wananchi umekuwa mdogo wasingeweza kuvunja beacons ambazo zimewekwa. Kwa hiyo, waliwashirikisha katika kuonesha ile mipaka ya asili lakini hawajawashirikisha katika zoezi hili zima ambalo wanataka kulifanya nao watafaidika vipi na watakuwa na sehemu gani. Wananchi wakishirikishwa vizuri nasema tena kwamba ulinzi ambao TANAPA watapata kazi kubwa ya kulinda utakuwa umekatika kwa sababu wananchi wenyewe ndiyo watakaolinda wakijua watafaidika vipi katika hili. Katika hili pia sijaona kama ametaja WMS, je, katika vijiji hivi 48 vyote hakuna kijiji ambacho kina WMS ambayo ipo pale na imeshiriki vipi na imetoa maoni gani.

Mheshimiwa Spika, la mwisho kabisa, uwekezaji wowote, baada ya sasa umeshawekeza kazi kubwa sana iliyopo na ya gharama kubwa ni marketing. Sasa Serikali pamoja na TANAPA sijui imejipanga vipi kwa sababu hiki ni kitu kipya kinaanzishwa katika suala zima la marketing. Marketing ni gharama kubwa, inahitji watu wenye weledi, watu ambao wanaujua undani wa yale mapori na kilichomo mule ndani na namna gani wamejipanga kuitangaza hii ili sasa lile lililokusudiwa liweze kufikiwa. Marketing kwa maana mbili; marketing kwa maana ya wale wawekezaji watakaokuja kuwekeza pale, namna gani wamewahamasisha, wamewatengenezea miundombinu ya kuhamasika kuwekeza pale, lakini marketing na ya wageni ambao sasa waje kutembelea pale.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya dakika tano, nakushukuru sana.
TAARIFA YA KAMATI YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE KUHUSU SHAURI LA KUDHARAU NA KUDHALILISHA BUNGE LINALOMKABILI NDUGU PROF. MUSSA ASSAD, MDHIBITI NA MKAGUZI MKUU WA HESABU ZA SERIKALI
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie katika hoja iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Profesa Assad kwa kuwa mkweli. Profesa Assad kawa mkweli, kasema ukweli wake, kasimama na ukweli wake na kasimama na anachokiamini katika taaluma yake. Pia nampongeza kwamba hakuisumbua Kamati kwa sababu kasema alichokisema na kasema mbele ya Kamati anachokiamini kwa mujibu wa taaluma yake. Kwa hiyo, mimi nampongeza sana Profesa Assad. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimemsikiliza msomaji hapa wa taarifa sijaona sehemu yoyote ambayo Profesa Assad ana sababu ya kutiwa hatiani. Kama mtu kakiri alichokisema na kasema hicho nimesema na ndivyo taaluma yangu inavyosema, nyie mnamtia hatiani kwa sababu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi sioni sababu ya Profesa Assad kutiwa hatiani kwa hiki alichokisema kwa sababu hajabadilisha neno na wala hajakataa, kasema. Kuona sisi Wabunge kwamba tunaweza au tunajua kila kitu ni kosa. Tukiambiwa dhaifu lazima tukubali, sisi ni wanadamu hatujakamilika lazima tuna madhaifu yetu. Kwa hiyo, tunapokosolewa lazima tukubali kukosolewa. Sasa kama kuna udhaifu na ni wanadamu sisi si Mungu lazima tukubali kuna udhaifu, no one is perfect. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwamba sisi tusikosolewe, hii tutakuwa sasa tumekiuka mipaka. Kwa hiyo, mimi nampongeza sana Profesa Assad na Kamati sijaona kama imetutendea haki kwamba sisi tusikosolewe, sisi ni nani mpaka tusikosolewe? Sisi ni wanadamu kama mwanadamu mwingine yeyote. Awe ni raia wa kawaida, Mbunge, Waziri, Rais kama ni mwanadamu lazima atakosea na huo ndiyo uanadamu, ile kutenda makosa ndiyo uanadamu wenyewe. Kwa hiyo, lazima tukubali kama ni udhaifu basi kweli tunao kwa sababu sisi ni wanadamu, tuangalie sasa udhaifu huu uko wapi na nini tufanye. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama tuna watu kama hawa anaweza akasimama akakwambia hapo umekosea wewe unamhukumu kwa kukwambia hilo wakati umekosea kweli, hatutendi haki. Kuna mifano mingi, tumetunga sheria ngapi humu zimekwenda huko, zimerudi tunazifanyia amendment, je, tuko perfect? Kwa nini kila tunachokifanya kikienda huko kisiende smoothly, kwa nini kirudi tufanyie amendment? Ni kwa sababu sisi ni wanadamu tuna udhaifu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwasilishaji kasema kwamba hakuwasiliana na Spika alipoondoka kwenda huko, kwani yeye aliambiwa akienda huko Marekani ataongea na waandishi wa habari na watamuuliza swali hili? Hakujua!

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Yussuf unachangia ukiwa umeweka mikono mfukoni. Hapa ni Bungeni unajua! Eeh, hapa ni Bungeni na kengele imeshagonga.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Naibu Spika, kengele ya kwanza.

NAIBU SPIKA: Kengele ni moja tu Mheshimiwa Yussuf.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, Bismilah Ramahan Rahim, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nataka nianze leo makatibu angalieni dakika mnatukata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kupongeza na kuunga mkono Hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani, lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri nilipongeze na Jeshi letu kwa kazi ngumu wanayoifanya na nawapa hongera sana siwapi pole kutokana na kazi ngumu na ugumu kwa sababu mwanajeshi hapewi pole akifanya kazi ngumu ndio kazi yake anapewa hongera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme kile ambacho kinatukwaza sisi kama raia. Juzi nadhani ilikuwa siku ya Jumatatu kuna Msemaji wa Jeshi la Polisi sikupata jina lake, lakini alikuwa ni Luteni Kanali alikuwa anatoa taarifa juu ya clip inayoendelea katika mitandao ya jamii ikionesha jinsi wanajeshi walivyofyeka mazao ya mtu ambaye amevamia katika eneo la Jeshi. Akatoa maelezo, akatoa vielelezo na akathibitisha kwamba hilo ni eneo la jeshi ambalo limenunuliwa na wale raia wamelipwa, well hatuna tatizo katika hilo. Kinachotuumiza sisi kama eneo ni la kwenu wanajeshi kihalali maana yake nini, maana yake na kilichomo ndani ya eneo lile ni cha kwenu. Sasa ninyi mlikuwa mumuondoe yule yale mazao myaache kwa sababu mazao hayo ni ya kwenu, kwa kweli sisi wakulima na watu wa mazingira inatuumiza sana tunapoona Jeshi linatumia nguvu zake tunaita utemi kufyeka mazao ya kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Amiri Jeshi Mkuu Awamu ya Pili wa nchi hii Mzee Ali Hassan Mwinyi ni mhamasishaji m kubwa wa kilimo cha papai. Leo akikuuliza Jeshi lako linatumika kufyeka mipapai utamjibu nini? Tunaliomba Jeshi letu kama eneo ni lenu tumieni taratibu na sheria kuhakikisha mnadhibiti maeneo yenu kwa sababu kiusalama ni maeneo yenu, lakini muwe waungwana kwa sababu mazao hayana kosa lolote, tumuogope Mwenyezi Mungu yale mazao ninyi mngeyatumia mapapai ni lishe bora kabisa kwa nini myafyeke, ile hamtoi picha nzuri tumeambiwa hapa na Kambi ya Upinzani kwamba Jeshi liwe-think tank ya Taifa hili, tunataka muwe mfano bora kwa wananchi na vijana wetu. Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo labda limewaumiza sasa nawapeni asali kidogo hiyo ilikuwa shubiri kwenu. Wanajeshi wetu wanafanya kazi masaa 24 lakini katika hali ya kawaida minimum wanafanya kazi masaa 12 ondoa ule muda wa kusafiri. Sasa kama anafanya kazi masaa 12 kwa nini hawalipwi overtime lakini baya zaidi kinachoumiza kwa nini mishahara yao haiwi-specific ikawa hii ni tofauti na wafanyakazi wengine. Lakini kwa nini wanajeshi hawa kama halipwi over time, hawana mishahara ambayo ni tofauti na wafanyakazi wengine wanaofanya masaa tisa, lakini bado wanaendelea kukatwa kodi ndani ya mishahara yao hii si haki, kama Wabunge tunatakiwa kuisimamia Serikali kuhakikisha kwamba wanajeshi hawa wanalipwa kulingana na namna wanavyofanya kazi, ndio maana wanajeshi hawa anapostaafu anadhalilika sana muda mfupi tu.

Kwa hiyo, tunaiomba Serikali na Mheshimiwa Waziri ulisimamie hili kuona kwamba wanajeshi hawa wanapata stahiki kulingana na kazi ngumu wanayoifanya. Minimum 12 hours ukimwangalia mtu amesimama pale halafu anakatwa kodi kwenye mshahara wake hii siyo fair kabisa kabisa, lazima hili liangaliwe na marekebisho yafanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine wanajeshi hawa wanafanya kazi katika mazingira magumu sana, ameligusia Mheshimiwa Anatropia, limegusiwa hata katika hotuba zote hawana insurance, hawana bima ya afya, sasa hili nalo ni tatizo. Tatizo ni nini? Kwa hiyo, tunaiomba Serikali ihakikishe kuwapatia wanajeshi hawa bima za afya kwa faida yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la nne ambalo nataka kulizungumzia hili ni lako kama Mwenyekiti wa Kamati hii lakini kama ambaye leo uko kwenye kiti tunaiambia Serikali, Jeshi nilisema hapa na leo naendelea kusema linaweza likawa chanzo kikubwa cha kuiletea mapato Taifa hili na kuingiza fedha nyingi katika pato la Taifa kulikoni Wizara nyingine yoyote. Inaweza ikashindana na Wizara ya Maliasili na Utalii kama Jeshi letu tutalitumia vizuri kuingiza fedha za kigeni katika nchi yetu.

Niiombe Serikali kwa nini tunanunua ndege hizi tunazonunua ambazo kwa mujibu wa taarifa toka ziliponunuliwa tunapata hasara kila mwaka kwa nini? Kwa nini fedha hii isitumike kununua ndege na vifaa vya kijeshi ambapo nchi yetu tumeingia katika US Missions vifaa hivi vikatumika kule ambako tunapata fedha moja kwa moja hakuna ujanja wa namna yoyote. Kwa nini isitumike hivyo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna nchi kama Bangladesh, Pakistan, India, Rwanda, China, Nigeria, Uruguay na Ukraine zinaendesha nchi zao kwa sababu ya huyu UN Mission tu, sisi tunashindwa nini? Kwa mfano katika pale UN ukiingia tu unalipwa iwe ni dry lease, iwe ni wet lease unalipwa pesa yako kila baada ya miezi mitatu. Risasi inalipwa, bunduki inalipwa, hanga linalipwa, gari linalipwa, ndege inalipwa sasa kwa nini inashindikana hivyo? Kwa mfano gari moja ukiingiza katika US Mission inalipwa dola za Kimarekani 4000 kwa gari moja. Sasa kama tumeingiza gari 100 pale tutakuwa tunapata kiasi gani achalia mbali ndege na hivyo vifaa vingine, kwa hiyo huo ni mfano na US Mission wanalipa kila baada ya miezi mitatu hiyo fedha hakuna ujanja ujanja kwamba wamewaambia watu wapake rangi ndege wanakwambia milioni 200 kumbe ni milioni tano.

Kwa hiyo, tunaiomba Serikali badala ya kuelekeza fedha katika miradi ambayo inaleta hasara iwekeze katika Jeshi ili Jeshi litukusanyie hii fedha. Tulishasema kwamba Jeshi likitumika vizuri nithink tank na linaendelea Jeshi hili kutuzalishia fedha nyingi za kigeni kadri inavyowezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tujiulize leo tuna miaka zaidi ya 10 nchi yetu iko katika ulinzi huu wa amani kule Sudan, DRC lakini tumepata nini? Tumepata fedha kiasi gani labda Mheshimiwa Waziri kama unazo data unaweza ukatuambia ni fedha kiasi gani, lakini bado tunaishauri Serikali iangalie namna ambayo tutalitumia Jeshi letu kama kitega uchumi na ni kuliwezesha tu tukanunua vifaa hivi badala ya kuingia katika miradi ambayo ukweli haileti tija kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho nataka kukizungumzia katika Jeshi, wanajeshi hawa kuna malalamiko makubwa namna ambavyo wanakaa muda mrefu ndani ya Jeshi bila ya kupanda vyeo. Mtu anatumikia cheo kwa miaka 12 hajapanda cheo kingine hii kwa kweli inaumiza wanajeshi wetu, lakini si inawaumiza personally inaumiza mpaka na familia zao. Kwa hiyo tunaomba huo muda ambao wanajeshi wanakaa pale jeshini uangaliwe vizuri na isiwe mtu anakaa zaidi ya miaka 12 bila kupanda cheo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine wanapoenda katika mafunzo Serikali ihakikishe kwamba inawapatia stahiki na malipo yao mapema kabla ya kuingia katika mafunzo kwa sababu wanaziacha familia nyumbani, zinahitaji huduma yeye yupo kwenye mafunzo usipomlipa kwa wakati concentration yake itakuwa ni kuangalia familia na kuangalia mafunzo matokeo yake ikija ile akiwa katika mafunzo yale ya hatari ndio unakuta tunapata majeruhi katika mafunzo. Tuiombe Serikali kuhakikisha kwamba inawalipa wanajeshi wetu stahiki zao kwa wakati kabla ya kuanza kwa mafunzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema kwamba Jeshi ni kioo katika jamii yetu, Jeshi linatakiwa liwe mfano bora la kufundisha wananchi wote tabia nzuri na mwendo mzuri. Jeshi letu linafanya kazi katika mazingira magumu liongezewe bajeti, lakini hata hii bajeti finyu itoke na itoke kwa wakati ili waweze kufanya kazi zao kwa ukamilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitaki kupigiwa kengele kwa sababu nimeweka stop watch leo nimeona ni dakika yangu ya tisa namalizia kwa kusema kwamba nampongeza Mheshimiwa Waziri na wanajeshi kwa kazi ngumu na nawatakia kila la heri, ahsante. (Makofi)
Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji Hadhi Sehemu ya eneo la Pori la Akiba la Selous kuwa Hifadhi ya Taifa ya Nyerere
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nami niungane na wenzangu kuunga mkono azimio lililo mbele yetu, ila niendelee kuishauri Serikali katika hili kwamba, eneo hili sisi tunapendekeza lote eneo la Selous liwe Nyerere Conservation Area. Kwa nini tunapendekeza eneo lote liwe conservation area; ni kwa sababu hili eneo tutalilinda lote na hatutaligawa ikawa sehemu moja tunaithamini zaidi nyingine tunaidharau, lakini pia tutaifanya Serikali iweze kuwekeza miundombinu na kuwahamasisha wawekezaji kuja kuwekeza mle ndani ili pato la Taifa liwe kubwa zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kuigawa vipande vipande utakichukua kipande kimoja utakithamini zaidi na kingine utakichukua kama ni cha kwako tu. Kwa hiyo, tunapendekeza hii Selous iwe Nyerere Conservation Area yote na isiwe vipande vipande, ili uhifadhi uwepo zaidi, lakini tuweze kuiendeleza zaidi kwa maana ya kwamba, tuone faida na pato la Taifa linakua.

Mheshimiwa Spika, napendekeza vilevile kama tunalipa jina la Nyerere basi tusimkate, Mwalimu alikuwa na heshima yake kubwa sana hapa Tanzania, Afrika na duniani kote, kwa nini tusiliite Mwalimu Nyerere Conservation Area? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, neno Mwalimu linaleta heshima na hadhi yake kwa Baba wa Taifa. Kwa hiyo, tusikate tu ikawa Nyerere, nadhani itakuwa, kwa mimi nahisi kama kutakuwa kuna mapungufu fulani hivi katika kumpa ile heshima ambayo amekusudiwa kupewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la tatu ambalo nataka kuchangia ni suala la marketing. Tunapoipa jina la Mwalimu Nyerere Conservation Area au Mwalimu Nyerere National Park, whatever na inatoka kutoka Selous wakati duniani Selous ni worldwide inajulikana itabidi hapo Wizara isimame vizuri sana kufanya suala la marketing kwamba unapoisema hii Mwalimu Nyerere Conservation Area au Mwalimu Nyerere National Park wale wageni kule au wanaokuja kutembelea waelewe kwamba ni ileile Selous na imebadilishwa jina tu.

Sasa hiyo kazi ya marketing kubadilisha inachukua muda kidogo; nafahamu ugumu wa marketing katika biashara hii ya utalii. Kwa hiyo, lazima Serikali iwe makini sana katika kulipeleka suala hili huko kuiuza hiyo Selous.

Mheshimiwa Spika, la mwisho Mheshimiwa Waziri wakati mnabeba jukumu hili la kubadilisha Selou kutoka kuwa pori la akiba na kuifanya kuwa national park na sisi tunapendekeza kwamba liwe conservation area basi tulikuwa tunaomba ile miundombinu kama ambavyo ameeleza Mbunge anayetoka katika mikoa hiyo kwamba, ile miundombinu mle iboreshwe. Utakapoboresha ile miundombinu mle na ukafanya vilevile marketing kuwahamasisha wawekezaji kuja kuwekeza mle ndani basi, lile suala zima la kuhifadhi lile eneo na lile suala zima la kwamba tunataka kuikusudia kuitangaza hii Stiegler’s ambayo inajengwa pale itakuwa imepata maana kamili maana wawekezaji watakapoongezeka mle ndani baada ya kuboreshwa kwa miundombinu maana yake ni kwamba, pato la Taifa litaongezeka na uhifadhi utaongezeka zaidi kuliko kuacha tu sehemu ikawa inahifadhiwa na sehemu ikaachwa kuwa nini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunapendekeza iwe Mwalimu Nyerere Conservation Area eneo lote la Selous badala ya kuchukua kipande tu. Hii tunapendekeza sana kitaalamu Mheshimiwa Waziri na tunaomba Serikali ikae ilifikirie hili na hili eneo tusiligawe vipandevipande itakuwa tunaliharibu ule uasilia wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukumbuke kwamba Selous ni worldwide, kwa hiyo, tukiigawa tunaanza kuipotezea ile heshima yake. Jina kubadilika tu sio tatizo, lakini ile heshima ya Selous ibaki kama ilivyo na tunapendekeza iwe Mwalimu Nyerere Conservation Area, ili iweze kukidhi mahitaji na matakwa ya dunia, lakini mahitaji na matakwa yetu na pato la Taifa liongezeke. Nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kwa kupata nafasi.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa masikitiko makubwa, na naomba katika hili utusaidie. Juzi nilimpa tatizo hili kabla ya kuwasilisha hotuba yao jana Mhehsimiwa Naibu Waziri kilio cha Wazanzibar kuhusiana na usafirishaji wa dagaa. Wazanzibar wanasafirisha dagaa kutoka Zanzibar kupeleka Congo, wana vibali vyote kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kusafirisha, lakini wanapofika ndani ya Tanganyika Tunduma wanakamatwa, wakishakamatwa dagaa wao wanazuiliwa wanalipishwa faini ya milioni mbili kila mtu mmoja na gari inapigwa faini ya milioni kumi; evidence zote hizo nimempa Mheshimiwa Naibu Waziri kabla ya kuwasilisha hotuba yao jana. Kama hilo halitoshi wanawekwa ndani wanapouliza kwa nini, sisi tuna vibali, hii ni transit tu tunapita kwa nini tunakamatwa? Wanawekwa ndani. Kuna msafirishaji anaitwa Ameir maarufu Mchezo amewekwa ndani kwa kuuliza swala hilo, kuna huyu agent wao pale Tunduma anaitwa Kibona amewekwa ndani kwa kuuliza swali kama hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaposema sisi Wazanzibar kuhusu masuala haya tunaambiwa tunasema maneno ya uchochezi. Mmetuzuilia sukari tusilete hapa tumenyamaza, mmetuzuilia maziwa yasiletwe hapa tunanyamaza, basi hata kupita? Kwa kweli hili linaumiza sana; na huu ni mwezi wa Ramadhan sitaki kusema sana lakini ni kitu kinachoumiza sana.

Mheshimiwa Spika, mimi nimwambie, na nilisema katika Bunge hili, kwamba Serikali ya Awamu ya Tano hii kuanzia Mheshimiwa Rais na Mawaziri hawa wanafanya kazi vizuri sana, wanakwenda mbio sana Mawaziri hawa kutatua changamoto hizi, lakini hapa katikati hapa ndipo penye matatizo, mpaangalie. Sasa hata magari yanakamatwa, kwa mfano kuna magari tisa yamekamatwa Mbeya yamepelekwa Tunduma; huko Tunduma kuna nini? Kwamba gari imekamatwa Mbeya, kama ni watu wa Fisheries wako pale, kama ni watu wa TRA wako pale lakini yapelekwe Tunduma, kuna nini huko?

Mheshimiwa Spika, sasa Wizara inajisifu imekusanya makusanyo mengi sana zaidi ya mpango wao kumbe ni dhuluma, maana hii mimi ninaiona kuwa ni dhuluma; Inauma, inauma, inauma kweli kweli. Tunaomba yale mambo wanayofanya hawa ndugu zangu hawa wa Kinyamwezi, yaani kila mnapotugusa sisi tunanyamaza, tunawaangalia tu; mnatugusa na hapa tunanyamaza tunawaangalia tu, tunataka ushahidi kamili.

Mheshimiwa Spika, naomba hili utusaidie; hawa ni watani wangu; we tulia wewe. Naomba niendelee. Naishauri Serikali katika suala la uvuvi wa bahari kuu. Kuna meli nyingi sana zinazokuja kuvua katika bahari yetu. Niko katika uwekezaji kandokando ya barabara Ukanda ule wa Kaskazini ya Pemba.

Mheshimiwa Spika, meli nyingi sana zinakuja zinafanya fishing, diving, na snorkeling lakini hakuna kazi yoyote, hakuna utaratibu wowote unaopatikana. Wakati huo huo Zanzibar inataka kusajili meli kwa ajili uvuvi kuna tatizo hili la kodi ambalo wamewekewa inakuwa ni tata.

Mheshimiwa Spika, tunaomba, kama sisi hatuwezi kulinda bahari yetu nani atatulindia? Na shida iliyopo hawa Askari wetu wa Marline Park, hawa wanaofanya, hawawezi kuzifikia, zile meli, zile meli ni kubwa vyombo walivyonavyo wao kuwafikia wale ni vyombo vidogo. Kwa mfano iko siku moja watu wa TRA, ZRB na KMKM walienda na fiber boat, kuna meli ilikuwa inavua karibu sana na Manta Resort zote wakaenda. Walipokaribia wale waliwaambia tu huko huko mliko ishieni huko, waliwatangazia kwa spika lao kubwa lile wakafanya ubishi wakaenda. Ile meli ilizungushwa tu wale karibu wazame, kwa sababu kile ni ki-fiber boat na lile ni wimbi la kuzungusha meli.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tuiombe Serikali katika suala hili lazima tujipange. Watu wanatoka huko, wanakuja Tanzania kwenye bahari yetu wanavua wanaondoka na samaki halafu samaki hao hao wanarudi tunakuja kuuziwa tena hapa hapa. Katika hili hatujajipanga; hii bahari ni rasilimali moja moja kubwa sana na ambayo inatuletea tija kubwa sana kama tutajipanga lakini bado hatujawekeza vya kutosha. Niiombe Serikali iwekeze vya kutosha katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, achana na hapo sasa, hiyo ni bahari kwa upande huu wa Magharibi, lakini sasa nenda upande wa Mashariki ya bahari yetu. Kule kwetu sisi kuna upande wa Mashariki wa vile Visiwa, sasa hapo ndipo utaona meli ambazo zinavua haswa. Hizo meli kubwa zinakuja, zinavua kwa mwezi mmoja kisha zinaondoka; hakuna kule kwa sababu hata hizo fiber bolt haziwezi kwenda.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Yussuf.

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kunipa nafasi na kwa sababu ya dakika tano itabidi niende in a point form kwa sababu ni mjumbe muhimu sana katika Wizara hii. kwanza nianze kwa kuwapa pole ndugu zetu wa Pemba ambao ni wadau wakubwa katika utunzaji wa rasilimali hizi za Maliasili na Utalii wa Kisiwa cha Fundo ambao wamepata ajali jana mashua kama 34 zimepotea na tano hazijaonekana mpaka sasa hivi na watu zaidi ya 30 hawajulikani walipo. Kwa hiyo, wale Kasa na Makobe wanaowatunza kwa ajili ya Utalii na watalii watapata shida, kwa hiyo, tunawapa pole kwa tukio hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilisema mwaka jana wakati anachangia Wizara hii kumwambia Mheshimiwa Waziri kwamba ni Wizara moja ngumu sana ni Wizara yenye changamoto nyingi sana, ni Wizara ambayo inahitaji umakini mkubwa sana na nikamuonya Mheshimiwa Waziri kwamba asipokuwa makini anaweza kuwa ni Waziri atakayehudumu kwa muda mfupi. Lakini nitaanza kusema kwamba Mheshimiwa Waziri katika kipindi kifupi ameonesha umahiri na umakini na ameenda vizuri sana na haya mafanikio yanayopatikana sasa hivi basi ni kwa umahiri wake na kubwa zaidi au siri ya mafanikio yake ni ile namna anavyoshirikiana na walio chini yake na watalaam pamoja na wadau wa Sekta hii. Kwa hiyo, nikupongeze Mheshimiwa Waziri na timu yako kwa kufanya kazi vizuri. Niseme pia ni Mbunge nina miakasita humu Bungeni wewe ni Waziri wa nne katika Wizara hii tokea niingie humu lakini kwa uelewa wangu na nilivyoona nathubutu kusema kwamba ni Waziri bora kulikoni hao waliokutangulia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisemi haya kwa utashi nasema kwa mifano. Kuna meli zaidi ya 12 za watalii za kitalii na watalii ambazo zimeingia katika kipindi hichi. Kuna Waisraeli 1000 wameingia hapa, Wachina 349, kuna kukuzwa hizi hifadhi za Biharaulo, Burigi, Kimisi, Ibanda na Rumanyika lakini kuanzishwa kwa Jeshi Usu vyote ni vitu ambavyo ni uthubutu wa Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake ambavyo ameweza kuvifanya, kwa hiyo, sisemi kwa utashi nasema kwa mifano ambayo iko wazi kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niache katika hilo kwa sababu ya muda niseme tu kwamba Mheshimiwa waziri ili tuweze kupata watalii wengi basi ni lazima kuna mambo lazima yatendeke, na kuna mambo Serikali lazima ijipange, wewe kama Waziri hutaweza ni mambo ya Kiserikali, Political stability transparent democracy hivi vitu lazima viwepo katika nchi, lakini pia kuboreshwa kwa miundombinu ya maji, umeme na barabara katika maeneo ya uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuwe na sheria na sera pamoja na kanuni za uwekezaji ili ziweze kuwavutia wawekezaji kuja kuwekeza katika nchi yetu. Kwa hiyo hatuna haja ya kuona watalii 2,000,000,000; 3,000,000,000 hiyo sio issue hoja ni kupata serious investors tukipata serious investors wakawekeza maana yake tutapawa watalii wa daraja la kwanza na daraja la pili na tukipata watalii wa daraja la kwanza na daraja la pili maana yake mtalii mmoja anaweza ku-spend from 1000 Dollars kwenda mbele, kwa hiyo, hata tukipata hao watalii 1,500,000 lakini watalii wenye maana ambao tuna serious investors wamewekeza basi tutaweza kupata fedha nyingi zaidi kulikoni kuwa na namba kubwa ya watalii lakini Pato dogo.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia watalii ili waje kwa wingi na wajirudia kuja na kuja kila mwaka lazima huduma zetu ziwe nzuri, kwa hiyo lazima uboreshe Vyuo vya Utalii ili vijana wetu waweze kusomeshwa na kuhitimu vizuri waweze kutoa service nzuri. Wageni wanaokuja wanakuwa na mila tofauti, tabia tofauti, madhehebu tofauti sasa ni sisi kazi yetu kuweza kuhakikisha kwamba tunawapatia huduma iliyo nzuri ili waweze kuja na mara nyingine tena. Kwa hiyo, lazima tuboreshe vijana wetu wasome.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu a muda nikuombe Mheshimiwa Waziri kuna sheria zinazokinzana sheria hizi zinahatarisha Maliasili zetu, kwa hiyo tukuombe kwamba Mheshimiwa Waziri uwe initiator ukae na Mheshimiwa Waziri wa Madini, Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Mheshimiwa Waziri wa Ardhi ili muweze kupitia sheria zote zile ambazo zinakinzana zinaleta ukakasi katika kutunza rasilimali zetu ili sasa tuweze kutunza. Mheshimiwa Waziri kuna sheria zinakinzana na zinahatarisha Maliasili zetu, hususani wanyamapori, tunakuomba katika hili basi wewe uwe initiator katika hawa Mawaziri muweke hiyo timu mupitie zile sheria na mlete hapa Bungeni ili tuzifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri …

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa ahsante sana, sekunde 30.

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Naibu Spika, dakika moja tu. Niiombe Wizara ya Fedha hili suala la tozo zilizowekwa kwa ajili ya TANAPA basi ziondoshwe, kwa nini ziondoshwe kwa sababu TANAPA imepewa mzigo mkubwa sana inahudumia zaidi ya mbuga 11 sasa hivi ambazo hizo haziji nini na zimeongezwa na nyingine tano, sasa na hii fedha ambayo inakusanywa kama kodi inarudi kwa wananchi kupitia ujenzi wa barabara, shule na hospitali wakti TANAPA wanafanya kazi hiyo. Sasa kwa nini wakiingiza Magreda, Makatapila, Magari walipishwe kodi? Kwa hiyo naomba Wizara ya Fedha… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Yussuf, umeshaeleweka.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuwa mchangiaji wa mwanzo katika Wizara hii. Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ndiyo inayobeba maisha yetu sisi wananchi wote tuliomo ndani ya Tanzania na Wizara hii inajukumu kubwa sana. Kwa hiyo, nitachangia kwa kadiri ya uwezo Mungu aliyonipa.

Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri kijukuu changu, Katibu Mkuu na Watendaji wote kwa namna ambavyo wanafanya kazi na sisi Kamati wanatushirikisha katika utendaji wa kazi yao. Pongezi hizi ziendane sambamba na utendaji ambao umetukuka ambao wanao Mungu awajalie waende mbele zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ardhi haiongezeki, lakini idadi ya watanzania inaongezeka, idadi ya mifugo inaongezeka, shughuli za kibinadamu zinaongezeka, mahitaji ya vitu vilivyopo juu ya ardhi na chini ya ardhi yanaongezeka lakini ardhi yetu inabaki pale pale. Sasa ni lazima tuishauri Serikali iangalie namna bora ya kupanga matumizi bora ya ardhi kwa haraka ili tuwe na kilimo cha kisasa, tuwe na ufugaji wa kisasa lakini pia tutumie maliasili zetu kama misitu na maeneo yaliyohifadhiwa vizuri kwa sababu hayo yatabaki hivyo hivyo.

Mheshimiwa Spika, hebu tujenge picha ya miaka 50 ijayo, watanzania ambapo wanaweza kufikia idadi ya milioni 100 hali itakuwaje na ardhi yetu ni ile ile. Ama inazidi kupungua kwa sababu ya erosion na mambo mengine ya mabadiliko ya tabia nchi. Kwa hiyo, ni lazima Wizara iwezeshwe kupewa fedha kwa ajili ya kupanga matumizi bora ya ardhi ili tuweze kukabiliana na changamoto ilinayokuja hapo mbele ya ongezeko la idadi ya watu, idadi ya wanyama, idadi ya matumizi yale tuweze kuendana na hali halisi ilivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiangalia miaka mitano tu au kumi tusipoangalia zaidi ya hapo tutakuja kukuta tunaachia vizazi vyetu matatizo makubwa sana ya ardhi. Kwa hiyo, tuiombe Serikali kwa heshima kubwa na taadhima kubwa na mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani, itoe fedha kumuwezesha Waziri wa Ardhi na Watendaji wake waweze kupima ardhi na kupanga matumizi ya ardhi na yasimamiwe kwa faida yetu na maisha yetu na kizazi kijacho. Vinginevyo tutajikuta katika hasara kubwa sana sana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo nataka nilizungumzie ni suala la migogoro ya ardhi. Hili litaendelea kuwepo lakini inaumiza kichwa kuona bado kuna migogoro ya ardhi ya wilaya na wilaya, kuna migogoro ya ardhi baina ya kata na kata, kuna migogoro ya ardhi baina ya kijiji na kijiji. Kwanini, wakati yote hayo yanasimamiwa na taasisi moja, au vitu vyote hivyo viko chini ya Serikali. Ninavyoona na ninavyojifunza tukiwa kwenye Kamati tunapokwenda huko ni kwamba, suala la ardhi, sera na mambo mengine yako chini ya Wizara. Huko chini mmiliki wa ardhi ni halmashauri, ni kijiji, wao ndiyo wenye maamuzi, sasa hapa kutakuwa na mvutano. Waziri anasema sera inasema hivi, lakini mwenye ardhi ambaye ni kijiji au ni halmashari yeye anataka hivi. Kwa hiyo, huu mvutano tuiombe Serikali ikae pamoja ione namna bora ambavyo masuala ya ardhi yatakuwa katika sehemu moja na yataweza kufanyiwa kazi kulingana na ardhi yetu ilivyo.

Mheshimiwa Spika, lingine niombe, migogoro yote inasababishwa na kutopangwa kwa matumizi ya ardhi, ardhi kutokupimwa. Haijulikani maeneo ya mifugo, haijulikani maeneo ya kilimo, haijulikani maeneo ya hifadhi, maana yake hifadhi nazo zimevamiwa, wananchi wanagombea maeneo ya hifadhi, wananchi wanagombea maeneo ya misitu. Yatakapopimwa na hili ndiyo suala ambalo litaleta msukumo mkubwa sana wa kutatua matatizo hayo. Kwa hiyo, haya yatakapopimwa yote na matumizi yakapangiwa na hali halisi ikaenda kama ilivyopangwa, basi haya yatatatuka.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuiombe Serikali, namshukuru Mheshimiwa Rais ameunda Kamati ile ya Wizara nane; Mawaziri nane, wamepita wamekwenda kuangalia hizo changamoto zilizopo huko, sasa waje hapa na hiyo taarifa baada ya kuipeleka kwa Mheshimiwa Rais ili na sisi kama kuna mvutano wa sheria na upo, kwa sababu tunaona sheria zinavyovutana. Sheria ya ardhi haioani na Sheria ya wanyamapori, kwa hiyo migongano ya sheria hizi ili tuzifanyie marekebisho kwa haraka ziweze kuendana na wakati na tuone sasa ardhi hii badala ya kuwa neema kwetu inakuwa balaa ili tatizo hili liondoke. Leo watu wanauana, watu wanapigana kwa sababu ya ardhi. Haiwezekani katika nchi ambayo watu tuko na amani na tunaweza tukakaa, tukazungumza na tukarekebisha sheria zetu kulingana na mahitaji na matumizi ya ardhi tuliyonayo.

Mheshimiwa Spika, kingine ambacho nataka nikizungumze ambacho binafsi hakinipi raha ni kuona kwamba kuna baadhi ya watu wanamiliki ardhi kubwa sana na hawaitumii. Kuna baadhi ya watu wanamiliki viwanja kumi na tano, ishirini, thelathini, wakati watu wengine hawana. Sasa haya maadam yanajulikana, ni miongoni mwa haya matatizo ambayo yanasababisha watu kwa watu kupigana. Kwa hiyo, tuiombe Serikali sasa kupitia Wizara yako Mheshimiwa Waziri ili kila mtu aliyepewa ardhi aweze kuitumia, na kama haitumii basi tutumie taratibu za kisheria kuona kwamba kama ardhi huitumii basi wapewe wanaoweza kutumia ili kuondoa hii migogoro ambayo inasababisha siku hadi siku kuleta hatari katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nataka nizungumzie kidogo kuhusu National Housing. National Housing ilikuwa inakwenda vizuri sana na mpaka sasa Shirika hili lilikuwa linatoa picha kwamba ni shirika moja zuri ambalo linatuletea tija lakini katika kipindi cha mwaka mmoja takriban sasa au zaidi kidoho shirika hili linasua sua. Tunaomba kabisa…

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, dakika moja tu nimalizie sentensi yangu. Tunaomba kabisa Serikali iruhusu ile mikopo waliyokuwa wanachukua shirika hili ili waweze kuchukua mkopo wamalizie yale majengo waliyonayo lisipate hasara. Nakushukuru sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba nianze kwa maneno ya mshairi yafuatayo na naomba Waheshimiwa Mawaziri wanisikie namna gani mshairi huyu aliiiasa nafsi. Alisema; huku giza lajikita nafsi yangu inuka, inuka uje nakuita nafsi yangu itika, sikuiti kwa kukuteta nafsi yangu isijeshituka. Akasema, nakuita uje na zibo nafsi yangu isijezibuka, kama hakiyo ni robo, nafsi yangu kilo epuka, siwe na matobotobo nafsi yangu utaaibika, nakuita uje na fungo nafsi yangu isijefunguka, umeumbwa kwa udongo nafsi yangu utaondoka, basi uache maringo nafsi yangu jua tauka. Unijie na stara nafsi yangu umesitirika, uje ukitia idhara nafsi yangu utaumbuka, maisha ni msafara nafsi yangu unakumbuka, usinijie na hasira nafsi yangu utaathirika, usinije na papara nafsi yangu utanichoka, bali uje na subira nafsi yangu utatukuka, kama waja na kiburi nafsi yangu bora geuka, kwangu uje na hadhari nafsi yangu utasalimika, yadhahiri ama siri nafsi yangu yameandikwa. Haya basi, anasema haya kuwa msikivu nafsi yangu semezeka, dunia mti mkavu mara waweza kung’oka, huwabwaga wenye nguvu nafsi yangu utanusurika…

SPIKA: Mheshimiwa Yussuf bajeti sasa.

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, nimeanza maneno haya kusudi madaktari wetu hawa wa uchumi wanisikie. Kwa muda wa miaka mitatu mfululizo tulikuwa tunaionesha Serikali namna gani uchumi wetu unaanguka, namna gani tunapata hasara, namna gani maisha ya Watanzania yanakuwa magumu lakini kiburi, dharau na jeuri kikawa ndiyo kimewatawala madaktari wetu hawa wa uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulisema mfumo wao wa kodi zilizopitiliza kiasi zinaua biashara, tukasema binafsi nimesimama kwa microphone hii na kiti hiki nilichokaa mwaka jana nikawaambia zaidi ya hoteli 56 pale Kariakoo zimefungwa na majumba yamebadilishwa matumizi. Kwa hiyo, hakuna wageni wanaoingia, mabasi yaliyokuwa yanaleta wageni wale hayana kazi, wafanyakazi waliokuwa pale hawana ajira, porters waliokuwa wakifunga mizigo hawana, restaurant zile hazifanyi kazi, wakawa hapa wanakuja na maneno ya kwamba wao wamejidhatiti na wapo vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya miaka mitatu Mwenyezi Mungu ameleta rehema zake, Rais ameona kwamba nchi inadidimia, amekutana na wafanyabiashara tuliokuwa tukiyaeleza sisi kwa muda wa miaka mitatu, lipi ambalo wafanyabiashara hawakumweleza Mheshimiwa Rais?
(Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wajitathmini madaktari hawa wana haki ya kuwepo pale kama ni waungwana, kama ni waungwana wajiuzulu kwa sababu kila kitu tuliwaeleza na tukawashauri na wakaleta dharau kwamba wao wamejipanga katika uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jana mchangiaji mmoja amesema kwamba miradi hii tunayofanya mikubwa ni mizuri na inatakiwa ifanywe; well, ndivyo, lakini katika uchumi wetu huu? Niliwapa mfano kwa sababu wameleta mtaalam wao mmoja hapa akatupa semina anatupa mifano kutoka Wizara yao hiyo ya Biashara anatupa mifano tunamuuliza maswali anakwepa. Tukawaeleza namna gani Sweden/nchi za Scandinavia zinakuza uchumi wao tukawaeleza Waheshimiwa Mwenyezi Mungu mkubwa, juzi kuna shirika moja hili la mawasiliano limempa Rais shilingi bilioni tatu, Airtel wamempa Rais shilingi bilioni tatu.

Mheshimiwa Spika, sasa tuchukulie mashirika yote ya simu yafanye vile, tuwe na viwanda 20 vifanye vile, tuwe na makampuni ya kilimo na wachimba madini wafanye vile, ndiyo Sweden inavyoendesha uchumi wake. Ile bajeti yao yote ni zile donations zinazotokana na wafanyabiashara na zinatokana kwa sababu wameweka mazingira sawa/wezeshi na uwazi katika biashara zao. Kwa hiyo, mfanyabiashara hana hofu ya kufanya biashara yake, anafanya biashara, inapofika mwisho wa mwaka anafanya hesabu anaichangia Serikali yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa fedha ile inatosha wao kwa bajeti yao na surplus ile ndiyo wanatusaidia sisi katika nchi zetu. Kwa hiyo, ile income inayotokana na makusanyo ya Serikali ndiyo wanakuja kwenye miradi yao mikubwa kama ya kwetu hii ya Stiegler’s au SGR na ndege. Sasa sisi tunaichukua bajeti ndogo tunayokusanya ambayo haitoshelezi tunaiingiza kwenye miradi mikubwa, unawakuta Watanzania leo wana-suffer katika maisha ni kwa sababu ya mipango yenu mibaya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na tulikuwa tukiwashauri humu ikawa hapa Mheshimiwa Dkt. Ashatu anakuja hapa anatushikia kiuno anakwambia Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Tano imejidhatiti, hatuna hofu, tutakwenda hivi na hivi. Leo baada ya miaka mitatu kwa nini mnaramba matapishi yenu? Kilekile tulichokuwa tunakieleza mnakikataa leo mnakirudia, kwa nini mnaramba matapishi yenu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wataalam hawa ndio kweli wanamshauri vibaya Rais na wanatupeleka kubaya…

SPIKA: Mheshimiwa Yussuf, mimi naona unalaumu lakini husemi concretely ni maeneo gani, ni kitu gani, yaani unapiga lawama za jumla tu.

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, nimesema, nilisema mwaka jana hapa kodi ya kontena moja milioni 40 pale bandarini inatuulia biashara yetu na wafanyabiashara wanachukua kontena hilo hilo, linapita as a transit likifika Uganda wanalipa milioni kumi biashara ile ile inarudi, haya mashati na vitenge tunavyouziwa hapo nje na mashuka vinatoka Uganda, vinapita hapo, niliyasema hayo. Jeuri na kebehi ikaja hapa hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nataka kuwashauri tena wachumi wetu hawa, wapi tutapata fedha ili kuokoa hapa tulipo. Kuvunja ni mara moja, lakini kujenga inakuchukua muda mrefu, wametuulia uchumi kwa muda wa miaka mitatu, si kazi rahisi kuujenga uchumi. Nilisema huwezi kuona maendeleo ya Taifa kiuchumi kwa miaka mitano au kumi, siyo rahisi, nilisema. Kwa sababu kama Taifa kujenga uchumi ni kitu kimoja kinahitaji mipango na muda mrefu, nilisema hivyo.

Mheshimiwa Spika, sasa nawaonesha; la kwanza, Mheshimiwa Mattar siku zote anapiga kelele kuhusu uvuvi wa bahari kuu. Meli moja ya uvuvi kwa utafiti uliofanywa inaweza ikaingizia Serikali yetu dola milioni 65 kwa mwaka. Hayo yanazungumzwa tu, hayajafanywa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama tutaimarisha utalii katika ukanda wa bahari huu, utalii wa fukwe, tukafanya diving, snorkeling, fishing, utalii wa historia, utalii wa kiutamaduni, pato la utalii, GDP ya Taifa inaweza kutoka asilimia 17 hadi asilimia 40 kwa muda mfupi sana. Kinachohitajika hapa katika utalii ni triangle, vitu vitatu tu; waweke pamoja jamii, iweke pamoja wawekezaji (serious investors), ikae na Serikali waweke mfumo ili sheria zisigongane, serious investors waje wawekeze tuta-boost uchumi wetu. Tunawaeleza hilo la pili tunapiga kelele mwaka wa tatu, bado hakuna mkakati wowote wa utalii uliopangwa katika ukanda wa bahari kuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, biashara ni lazima uweke mazingira wezeshi, uweke mazingira ya uwazi. Mtanzania awe ana uwezo wa kujua nakwenda kuchukua simu hii China, nainunua shilingi ngapi, ntailipia kodi shilingi ngapi awe anaweza kufanya kulekule…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Yussuf, malizia.

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Spika, mimi nimewashauri na wakiwa tayari ntawashauri wataalam wao waliosoma Amerika wametudanganya na tuliwauliza maswali wakajibu, tutawapa mifano ya nchi mbalimbali. Sisi hatukusoma, na Mheshimiwa Marehemu Karume alituambia tumesoma hatukujua, tumejifunza tumetambua. Tukienda huko kwa wenzetu tunajifunza kwa nini waendelee sisi tukwame; kwa nini, tunajifunza hayo mambo. Kwa hiyo tunapowashauri Waheshimiwa tunaomba muwe wasikivu. Nakushukuru. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi wa Mwaka 2018
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na mimi kunipa nafasi jioni ya leo nichangie kidogo katika mada iliyopo mbele yetu. Mheshimiwa Waziri Mpango kwa mara nyingine nataka kukusaidia pamoja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano kama mtanisikiliza na kunielewa, mimi siyo mtalaam wa sheria na sijui sheria, lakini katika mambo ya uwekezaji sidanganyiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wengi humu ndani wamechangia na wanahofu juu ya suala hili kwamba huko mbele litatuletea matatizo, leo tunalitungia sheria na mimi kwa uzoefu wangu katika uwekezaji hili litaleta matatizo huko mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inavyoonekana tunatunga sheria leo bila kujua tunataka kuja kufanya nini huko mbele, hatujui undani wa nini tunataka kuja kufanya tunatunga sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Omari Kigua mchangiaji wa pili leo alikuwa anachangia nawasilikiliza vizuri anasema hii ni new idea na ni kweli suala la uwekezaji kwa nchi yetu ni new idea tunaliingiaje. Sasa hapa ndio nataka unisikilize vizuri nikusaidie ukiona utafanya marekebisho ya sheria falakhala kheri huko haifai basi twendeni tu tuko katika jahazi moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uwekezaji ni suala moja kubwa sana na ni lazima uandae miundombinu ambayo utahakikisha unamvutia mwekezaji na wewe mwenyewe unajihakikishia na ile jamii iliyokuzunguka unaihakikishia mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwa nasema mara zote, ili uwe na uwekezaji wenye tija usio na mashaka hapo mbele lazima kuwe na triangle. Serikali ikae na mwekezaji mkae pamoja na jamii mkae pamoja, bila ya hivyo uwekezaji huo baadae utaleta matatizo. Hii migogoro inayozungumzwa yote leo ndani ya nchi hii miradi iliyoanzishwa inaleta migogoro ni kwa sababu hamkukaa, ni upande mmoja uliamua, hilo moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni lazima mu- identify hicho mnachotaka kufanya hiyo PPP, hiyo miradi muiseme bayana kutoka leo kwamba mradi huu na huu ndiyo tunataka iingie katika hilo. Maana yake nini na hili ndiyo tatizo ambalo Mheshimiwa Rais Magufuli atapata shida sana mpaka wakati mwingine anatamka maneno unamuonea huruma, katika level ya yenu ya Uwaziri labda hapo mtakuwa vizuri, lakini Waziri, Katibu Mkuu tatizo la Serikali ya Awamu ya Tano, kuanzia Wakurugenzi kuja chini ndiyo tatizo na hao ndiyo watendaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika level yenu ninyi mpaka kufikia Makatibu Wakuu mnapokea vizuri mnafanya vizuri, mnapanga vizuri lakini nyie siyo watendaji. Kuanzia level ya Wakurugenzi kuja chini hapa ndiyo penye matatizo na ndiyo hili tatizo ambalo mnalipata katika Serikali ya Awamu ya Tano lazima mpaangalie vizuri hapo katika mkiona na maana hilo chukueni mfanyie kazi, mkiona siyo la maana liacheni tuzame pamoja.(Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine katika suala la uwekezaji na miradi hii ambayo mnaikusudia ni ya PPP lazima muwe na bajeti. Kama Serikali mkisha-identify hiyo miradi ambayo hii tunataka tuingie ubia, ninyi wenyewe sasa muwe na bajeti ambayo mmeitenga kwamba bajeti hii ndiyo itatupeleka katika hiyo miradi, bila ya kuwa na bajeti ninyi wenyewe kama Serikali mkategemea tu huyo mtu aje hapa, hapo hamuingii ubia na hapo mnanunuliwa na mwisho wa siku tunakwenda katika hayo matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo lazima Serikali ijipange na ndiyo maana nikasema mu-identify, haya masuala nimeyasomea Waheshimiwa! Lazima mu-identify ile miradi mkisha-identify muweke bajeti kwamba kwa uwezo wetu kama nchi miradi hii miwili ndiyo mnataka kuingi katika PPP na bajeti yetu sisi ni hii kama Serikali, msipofanya hivyo mkitegemea tu huyu akija mtu mnaenda kuingia katika matatizo kwa sababu yeye akija na fedha yake atawachukua kwa namna anavyotaka yeye.

Kwa hiyo, hilo Waheshimiwa naomba nalo mliweke katika vichwa vyenu muone namna gani mnalitungia sheria.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu kuhusu miundombinu, ameligusia mzungumzaji aliyemalizia kabla yangu, ni lazima ile sehemu ambayo mnataka kufanya hiyo miradi mtangulize kuweka miundombinu, kuwe na barabara hapo, kuwa na maji, kuwe na umeme na miundombinu yote ambayo inahitajika lazima iwepo kabla. Mkifanya hivyo kama Serikali hapo itakuwa tayari hili suala mmelifanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la nne au la tano ni uwazi. Katika vitu ambavyo tunalaumu ni kwamba hakuna uwazi katika masuala haya, wenzetu hawa wao wana utaalam na ndiyo maana Mheshimiwa Kigua akasema hii ni new idea, atakapokuja huyo mwekezaji tayari ana utaalam ana uzoefu ameshafanya, kwetu ni kitu kipya tunataka kukianza sasa, tuna rasilimali tu, sasa anapokuja tayari ana uzoefu, ana utaalam, ana kila kitu, sisi hatuna tunaanza sasa, tunaingiaje na mtu huyo? Ndipo pale niliposema ni lazima mkae ule utatu, kwa sababu pale ninyi mtasema yale yenu na yeye atasema yake kwamba anataka ule mradi wote awazunguke uwe wa kwake, tumeshafanya na hawa tunawajua vizuri sana, wenzetu hawa ni wazuri sana kwenye kuandika ni wazuri sana kwenye kujieleza, sasa kama hakuna uwazi mkazungumza pale halafu mkaweka kitu kimoja basi watatuzidi huko mbele na kama hawakutuzidi matokeo yake baadae ndiyo zinakuja hizo kesi wanakuja kutufilisi, kwa hiyo, lazima kuwa na uwazi katika masuala haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kujipanga hivyo, hizi siku kutoka siku 15 hadi siku 21 ni nyingi sana katika suala la uwekezaji, mkisha-identify ile miradi mkishaitangaza ina maana wataalaam waliopo chini yenu wafanye kazi sasa, tunataka kiwanda cha maziwa, kwa hiyo, wataalam wanaohusiana ng’ombe, maziwa, majani na nini watoe ushauri sasa pale hapa je tukiwekeza hapa kama Serikali tunataka nini na nini ili sasa mkija mkikaa na huyu mwekezaji ninyi mnajua mnachokitaka, mnatetea hoja zenu, mna- negotiate mpaka mnafikia makubaliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipofanya hivyo tukiingia tu kichwa kichwa tutashindwa, sasa wawekezaji wanapokuja ukimwambia baada ya siku 21 wao wanakata tamaa. Kwa hiyo, tuweke mazingira tujipange tuwe tayari, tujitayarishe kwamba tunataka kuingia katika PPP iwe tumejitayarisha, kwa hiyo akija investors anataka ku-join iwe tuko tayari, kwa hiyo, ndani ya siku tatu, ndani ya wiki moja hardly siku 10 tumemaliza biashara shughuli inaanza, iwe tayari tumejipanga vinginevyo Waheshimiwa tunaenda kuingaia katika matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano katika hili, tumeingia kweye biashara ya utalii tu hii tunalalamika kwamba wafanyakazi wengi katika sekta ya utalii au katika mahoteli ni watu kutoka Kenya, kwa nini na Tanzania vijana tunao wamesoma na nini kwa nini hawaajiriwi? Ukiimuuliza investors anakwambia hawaajiriki, hasa ukikaa katika mambo hayo unakuta kweli haajiriki, kwa sababu Kenya walijitayarisha kuingia katika biashara, wakawatayarisha vijana wao kuingia katika hiyo biashara, tujitayarishe kabla hatujaingia katika PPP tuwe tumejitayarisha, tumejipanga vya kutosha ili tukiingia tuwe tunajua. Changamoto zitakuwepo kibinadamu, lakini tuhakikishe kwamba tumejipanga vizuri na tunaingaia katika kitu ambacho tunakielewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ukitaka nikusaidie zaidi katika haya nitakusaidia, nimejifunza vya kutosha, nawafahamu wenzetu namna ambavyo wanakuwa wajanja mnapoanzisha kitu na baadae wanakuzunguka, kwa sababu ni new idea kwetu ni lazima tuwe makini sana, nakutakia kila la kheri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani.