Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Emmanuel Adamson Mwakasaka (76 total)

MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Pamoja na majibu mazuri ya Waziri, ninaomba kumuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa kwenye bajeti ya Serikali mwaka huu moja ya vitu vilivyoainishwa mle ni pamoja na kufanya review ya mikataba mingi kwa hawa waliobinafsishiwa viwanda. Sasa ni lini Serikali itafanya review ya kujua uwezo wa huyo mwekezaji kuhusu kuwekeza Tabora Mjini?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa kuna tuhuma zinazomuhusu mwekezaji huyo wa kiwanda cha Nyuzi kwamba kuna mashine mbalimbali ambazo aliziuza kama vyuma chakavu, ambazo zilikuwa mle kwenye kiwanda na kwamba kuna mashine nyingine ambazo tayari zilishasafirishwa, hazipo kabisa pale;
Je, ni lini Serikali itafanya ukaguzi ili kujiridhisha kwamba mwekezaji yule kweli hajaziuza mashine hizo au kuzihamisha nje ya nchi?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu review, sina sababu ya kukuficha, review ilishaanza kuhusu Tabotex, nimeshakwenda kumuona hata aliyekuwa Meneja, ambaye sasa hivi ni Meneja Mwatex. Aliyekuwa Meneja wa kiwanda hiki sasa yuko Mwatex Mwanza, nimemfuata nikamuhoji. Ngoja nikueleze, kuna mambo mengine anapoteza muda, kuna majibu amenipa anapoteza muda na iko kwa Msajili wa Hazina na atamshughulikia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu namba mbili, kwamba kuna mashine zimeuzwa, ile tathmini nzima ndiyo itakuja kuhitimisha kwamba alipotoa mashine hii na kuleta mashine nyingine aliitoa kwa misingi gani. Niwaeleze ukweli ambao nimeushuhudia, mitambo ya viwanda vyetu vya nguo, viwanda vingine vilikuwa na mitambo ya mwaka 1963, kwa hiyo mwekezaji makini anapoingia ile mitambo ya mwaka 1963 ataiondoa. Nimeona mashine moja imeagizwa kutoka Swiss, kwenye kiwanda kimojawapo, mashine moja ina uwezo wa kufanya kazi kuliko mitambo 10 ya zamani ukiunganisha. Kama amefanya kwa nia hiyo tutamhukumu kwa alivyotekeleza, lakini kama nilivyosema maslahi yetu ni kwamba kiwanda kifanye kazi, kitoe ajira, kizalishe bidha na hatimaye alipe kodi, akitimiza hayo sina tatizo naye.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kumuuliza Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa mazungumzo na hawa wawekezaji mahiri wa kusindika tumbaku na mambo ya sigara yanaendelea. Je, mazungumzo hayo yakifanikiwa, ana uthibitishia Mkoa wa Tabora kwamba utapata upendeleo kwa kujengwa Kiwanda cha Tumbaku? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa Mheshimiwa Rais ameonesha nia ya Serikali kuwashirikisha mashirika ya kijamii kama NSSF kushiriki kwenye ujenzi wa viwanda na biashara, je, ni lini mazungumzo hayo, Serikali itaanza na haya mashirika ya kijamii?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, ujenzi wa Kiwanda cha Tumbaku Tabora ni la wadau wa Tabora ambao walikaa pamoja na ninyi Wabunge. Nimewaeleza kwamba tunahangaika kutafuta wawekezaji, siku ya Jumapili mwekezaji kutoka China atafika Tabora. Kwa hiyo, Wabunge wa Tabora tukimaliza kikao tukutane kusudi ninyi mtangulie kumpokea Jumamosi halafu tujadiliane. Masharti ni yale yale, kama mtatoa eneo bila kuweka vikwazo vya fidia za ajabu mtapata upendeleo, hali ndivyo ilivyo, utakavyotoa vivutio utapata upendeleo. Ujumbe wa China unakwenda Tabora na Precision Jumapili, tangulieni, Jumamosi tukakutane kule tuweze kuwakaribisha wawekezaji. Kwa hiyo, Tabora nimewafanyia kazi, ni jukumu langu pia ni jukumu lenu.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, uwekezaji wa hizi Social Securities, maelekezo ya Mheshimiwa Rais nimeyasikia, nilichofanya nimemwagiza Katibu Mkuu anayeshughulikia biashara na uwekezaji Wizarani kwangu, akutane na Makatibu Wakuu wa Wizara ya Kazi inayosimamia haya mashirika, akutane na Makatibu Wakuu wa Wizara ya Kilimo, wote wakae, wabainishe ni wapi kwenye shughuli zenye tija ambako hizi Social Securities zinaweza kuwekeza na kuweza kurudisha pato lake. Kwa hiyo ,watalaam watafanya kazi hiyo na nimewaambia kabla ya tarehe 26 waniletee orodha na nitaitangaza hapa Bungeni kwako.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii niweze kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa, tatizo linalowakabili wananchi wa Maswa Magharibi kuhusu bwawa lao, linafanana kabisa na tatizo la bwawa la Kazima Mjini Tabora ambalo maji yake yanapungua mara kwa mara hasa wakati wa kiangazi, kutokana na tope pamoja na mchanga uliojaa pale. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha lile tope pamoja na mchanga linaweza kuondolewa ili wananchi wa maeneo yale waweze kupata maji ya kutosha?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa bahati nzuri bwawa la Kazima nimelitembelea ni bwawa kubwa na kweli nimelikuta lina matatizo. Moja, kipindi cha kiangazi kutokana na miti mingi iliyoko kwenye lile bwawa maji yanabadilika rangi, lakini pia bwawa lile linajaa tope kutokana na shughuli za kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, tayari tumeshaongea na Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji wa Tabora, kuhakikisha kwamba tunashirikisha jamii. Nimwombe pia Mheshimiwa Mwakasaka, shida kubwa inayojitokeza ni kwamba wananchi wanalima sehemu ambayo maji yanatoka; baada ya kulima mvua zikinyesha zinabeba zile tope kuleta kwenye bwawa. Kwa hiyo, suala la msingi ni kwamba kwa kushirikiana na Halmashauri, tujaribu kuhakikisha kwamba tunaacha eneo la kutosha kuja kwenye bwawa, wananchi wasifanye shughuli za kilimo pamoja na ufugaji ili tuweze kulilinda bwawa letu lisijae mchanga.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa wakulima wa tumbaku wamekuwa wakikopwa na pesa zao zinachukua muda mrefu sana kuja kulipwa, Serikali ina utaratibu gani wa kuwasaidia wananchi hawa wanaolima tumbaku hasa Mkoa wa Tabora kuhakikisha kwamba wanalipwa pesa yao na riba kama wanavyofanya mabenki?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa utaratibu wa tumbaku kuchukuliwa na baadaye ndipo wakulima hulipwa kumesababisha matatizo makubwa sana na ndicho hasa chanzo cha kurundikana kwa madeni mengi ya wakulima kutoka kwenye Vyama vya Ushirika. Tunafahamu kwamba mfumo mzima wa ushirika siyo kwenye tumbaku tu lakini katika mazao mengi una changamoto na ndiyo maana Bunge hili lilifanya uamuzi mzuri sana wa kuleta Sheria mpya ya Tumbaku, Sheria Na.6, 2013 ili kuondokana na changamoto hizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaendelea kuimarisha ushirika ili isitokee tena kwamba wakulima wanachukuliwa tumbaku yao na wanakaa miaka mingi bila kulipwa. Kwa hiyo, tunaamini kwamba kwa mfumo huu wa ushirika ambao tunauleta sasa haitawezekana tena wananchi kukopwa lakini tunahakikisha kwamba tumbaku ya wananchi inakuwa inalipwa moja kwa moja. Badala ya kuchukua kwanza na kulipa baadaye ni kwamba tutakuwa tunatumia mfumo kama ule wa korosho ambapo tumbaku ikishakusanywa kwenye Vyama vya Msingi wanunuzi wanakuja kununua pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inafahamu changamoto hii, inafanyiwa kazi na tunaamini katika mfumo uliokuja wa Vyama vya Ushirika utarekebisha matatizo makubwa ambayo yametokea. Vilevile sheria hii imeweka mazingira mazuri sana ya kuwabana na kuwafikisha katika vyombo vya sheria si tu wafanyakazi wa Vyama vya Ushirika lakini vilevile hata Maafisa Ushirika ambao wanashirikiana katika kuwahujumu wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilieleze tu Bunge lako Tukufu kwamba changamoto kubwa iliyoletwa na mfumo wa ushirika ambao tunauondoa ni kwamba kumejengeka utatu usio mtakatifu kati ya viongozi wa Vyama vya Ushirika, mabenki na watendaji wa Serikali. Kwa hiyo, tunahakikisha kwamba utatu huu ambao umeleta matatizo kwa wananchi unavunjwa ili wananchi waweze kupata haki yao na kusiendelee kutokea changamoto katika zao la tumbaku.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Raphael Michael, Mbunge wa Moshi Mjini ametoka nje, naomba nitumie nafasi hii kwa sababu swali alilouliza linafanana kabisa na suala ambalo liko Tabora katika Hospitali yetu ya Mkoa ya Kitete, naomba niulize swali kwa Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, Hospitali yetu ya Mkoa wa Tabora ya Kitete ina tatizo lile lile la mlundikano wa wagonjwa kama ambavyo iko Moshi Mjini. Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Hospitali ya Wilaya inajengwa Tabora ili kuweza kupunguza huu mlundikano wa wagonjwa?
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, Hospitali ya Mkoa wa Tabora ya Kitete ina upungufu mkubwa sana wa Madaktari, tuna Daktari Bingwa mmoja tu. Serikali inajipanga vipi kuhakikisha Hospitali ya Mkoa wa Tabora ya Kitete inapata Madaktari Bingwa wa kutosha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, watu wanasema hata katika mpira vilevile, ikitokea mpira unapigwa golini halafu mtu kaondoka wewe piga goli tu. Kwa hiyo, naomba nimpongeze kwa hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Tabora ya Kitete aliyoizungumzia kwamba kwa sababu changamoto ni nyingi tuna mpango gani wa kuanzisha Hospitali ya Wilaya. Katika hili naomba nielekeze, tuweke vipaumbele katika Manispaa zetu kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Serikali iko tayari kabisa kushirikiana na wananchi wa Tabora ili kuhakikisha wananchi wa Tabora wanapata afya njema.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, napenda kuwashukuru wana Tabora kwa ujumla wao, kwa sababu nilipopita kule Tabora nimeona shughuli mbalimbali za kusimamia miradi. Nilitembelea Kituo cha Afya cha Itobo na kile kingine cha Bukene nimeona vifaa vya upasuaji vimewekwa kwa ajili ya akinamama. Kwa hiyo, juhudi zile wakati tukifanya mpango wa pamoja sasa kuimarisha Mkoa wa Tabora, kwa sababu tukiangalia sehemu ile hata watu kutoka Kigoma watakaopata matatizo wanaweza wakaja pale, ni vema kabisa tukaendelea kuweka nguvu. Katika mpango wetu mkakati wa Serikali kuimarisha Hospitali za Mikoa kupitia ule mradi mkubwa, nadhani tutaelekezana hapo baadaye jinsi gani tutafanya na Tabora ipewe kipaumbele kikubwa zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala la watumishi kwamba hatuna Madaktari Bingwa, bahati nzuri katika mchakato tutakaoufanya ni pamoja na kuhakikisha Madaktari Bingwa wanafika katika kanda mbalimbali. Imeonekana mara nyingi sana Madaktari Bingwa wanaishia katika maeneo ya miji mikubwa sana hasa Dar es Salaam. Katika maeneo ya pembezoni Madaktari Bingwa hasa madaktari wa magonjwa ya akinamama (gyno) wanakosekana.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili nililigundua hata nilipofika katika Mkoa wa Singida, kuna hospitali nzuri lakini Madaktari Bingwa wamekosekana na hata nilivyofika Songea jambo hili nililiona. Mpango wetu ni kwamba kupitia Wizara ya Afya vilevile tutafanya mkakati sasa kuweka mipango vizuri ili Madaktari Bingwa waweze kufika maeneo mbalimbali ikiwemo na Tabora, lengo kubwa wananchi wetu wapate huduma bora.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, TAMISEMI, napenda kumthibitishia Mheshimiwa Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini kwamba, Tabora ni mojawapo ya mikoa tisa ambayo Wizara ya Afya imeifanyia tathmini kwamba inayo uhaba mkubwa wa Madaktari Bingwa pamoja na Mikoa ya Kigoma, Mara, Katavi, Rukwa na Simiyu. Kwa hiyo, tutakapopanga Madaktari kwa mwaka huu wa fedha, tutatoa kipaumbele kwa Mkoa wa Tabora na mikoa mingine nane.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe Madaktari wote na wataalamu wa afya ambao mnatarajia kuomba kazi Serikalini kwamba tutawapanga katika mikoa hiyo tisa ndiyo kipaumbele chetu. Kwa hiyo, kama wanataka kukaa Dar es Salaam wajue hatutachukua daktari ambaye anataka kukaa Dar es Salaam. Nakushukuru.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa kutokana na msongamano huo wa magereza na mahabusu ambao hata Mheshimiwa Waziri ameukiri hapa, kunasababisha magonjwa mengi hasa ya mlipuko; nimewahi kutembelea Gereza la Uyui pale Tabora, kulikuwa na wagonjwa wengi wa upele; na sasa hivi kuna tatizo kubwa sana la upatikanaji wa madawa sijui Serikali ina mkakati gani wa kufanya upendeleo kuhakikisha wale mahabusu na wale ambao ni wafungwa wanapata dawa za kutosha?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge Mwakasaka amefuatilia mara nyingi sana jambo hili na hata kuna kipindi tumekaa, yeye pamoja na wenzangu wa Wizara ya Afya. Jambo lake tulishalipokea, kadri mtiririko wa fedha unavyokuja tutalifanyia kazi kwa sababu ni jambo ambalo alishalifuatilia hata kwa ngazi ya Wizara na tulimuahidi kwamba tunalifanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge, naomba uendelee kuvuta subira na niwapongeze wana Tabora kwa kukuamini kwa sababu kwa kweli umeendelea kulifuatilia hilo pamoja na mambo ya uhalifu ambao mara nyingi mmekuwa mkiusemea na sisi tunachukua hatua.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tatizo lililopo kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara, linafanana kabisa na tatizo ambalo lipo kwenye Hospitali ya Mkoa wa Tabora ya Rufaa ya Kitete. Kuna tatizo kubwa sana la wagonjwa na hasa akinamama wanapoenda kujifungua, wodi ile ni ndogo na wengi wanalala chini wakiwa hata wale wachache wanakuwa wana-share kitanda kimoja:-
Je, Serikali inajipanga vipi kutatua hili tatizo la muda mrefu la msongamano wa akinamama wanapojifungua pale Hospitali ya Mkoa wa Tabora ya Kitete?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Hospitali ya Kitete pale Tabora ina changamoto kubwa na ndiyo maana ukifanya rejea ya majibu yangu mbalimbali niliyoyatoa hapa Bungeni, tumesema kwamba catchment area ya Mkoa wa Tabora, ukubwa wake na jiografia yake ilivyo ina kila sababu tuweke nguvu. Ndiyo maana katika bajeti ya mwaka huu sitaki kutaja figure hapa exactly, tuna fungu ambalo tumelitenga kwa ajili ya suala zima la ukarabati pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tutaangalia ni kipi kilichotengwa katika mwaka huu. Lengo ni kwamba ile fedha ipatikane tu ikafanye kazi na value for money ionekane. Naamini ule ukarabati utaanza mara moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nikuhakikishie kwamba katika majibu yangu ambayo nayakukumbuka hapa Bungeni niliyoyatoa ni suala zima la Hospitali ya Kitete; naomba tuwasiliane kwa karibu zaidi ili tujue ni fungu kiasi gani limetengwa, lakini tuhimize sasa ile fedha ili iweze kufanya kazi vizuri.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mkoa wa Tabora hususani Tabora Mjini tuna mabwawa makubwa mawili, Bwawa la Igombe na Bwawa la Kazima, pia tuna mradi wa bwawa ambalo lipo Kata ya Ndevelwa ambalo limeigharimu Serikali zaidi ya shilingi bilioni moja ambalo mpaka sasa hivi halifanyi kazi kwa sababu linavuja.
Mheshimiwa Spika, sijui Serikali ina mkakati gani wa kufanya mradi huu ambao kwanza umekwama, lakini pamoja na haya mabwawa mengine yaweze kutumika katika kilimo cha umwagiliaji ili wananchi kwa ujumla waweze kupata ajira pamoja na kuweza kupata mazao kwa ajili ya kujikimu kutokana na hali mbaya ya chakula ambayo inaikabili nchi yetu kwa sasa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, mabwawa mawili ya Igombe na Kazima yanatumika kwa ajili ya maji ya matumizi ya binadamu na Bwawa la Igombe limeshaboreshwa tayari lina maji ya kutosha, sasa kuangalia uwezekano kwamba yanaweza yakatumika kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji basi tunalichukua tuweze kulifanyia kazi.
Mheshimiwa Spika, kuhusu bwawa hili ambalo limebomoka, hili kwa sasa tayari tumejikita kuhakiksha kwamba mabwawa yote ya zamani yanaboreshwa ili yaweze kufanya kazi zilizotarajiwa.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa
kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Naibu
Waziri, nauliza swali ambalo kama ilivyo Rungwe ule mradi wa Masoko, Tabora
Mjini ule mradi wa Ziwa Victoria, kuna vijiji ambavyo niliviorodhesha kwenye swali
Na. 57 lililojibiwa hapa Bungeni ambavyo ni Vijiji vya Itetemla, Uyui, Ntalikwa,
Kabila, Mtendeni, Itonjanda na baadhi ya maeneo ambayo ni ya Kata za Tumbi.
Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji hivi na hizi Kata havijaorodheshwa kwenye
huu mradi wa Ziwa Victoria na vina shida sana ya maji. Sijui vitapitiwa lini na
mradi huu wa Ziwa Victoria? Naomba swali langu lipatiwe majibu. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika,
kwanza kabisa Tabora Mjini kuna mradi mkubwa wa maji ambao umekamilika
kutoka bwawa la Igombe na kwamba maji yanayozalishwa ni lita milioni 30 kwa
siku wakati mahitaji ni lita milioni 24. Kwa hiyo, kwa maana ya Tabora Mjini tayari
imeshakamilisha huduma maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tupo na mradi ambao sasa hivi upo kwenye
zabuni ambao utatoa maji kutoka Ziwa Victoria kupeleka Nzega, Tabora na Igunga. Kwa hiyo, nina hakika kabisa kwamba sasa Tabora itakuwa na maji
mengi na ndiyo maana tunataka hayo maji yakishafika tuyaelekeze yaende
mpaka eneo la Sikonge. Kwa hiyo, Vijiji vyote Mheshimiwa Mbunge ambavyo
havina maji nje ya Manispaa ya Tabora kupitia mradi huo tutakuwa na maji ya
uhakika kuhakikisha sasa kata na vijiji vyote vinapata maji ikiwemo na sehemu ya
eneo la Uyui.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, kwa kuwa huu mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria unaonekana unaendelea kusuasua na hauna uhakika exactly lini utaanza na wananchi wa Tabora wanaendelea kuteseka kwa shida ya maji na sisi pale Tabora Mjini tuna bwawa kubwa la Igombe ambalo lina-access ya maji kwa maana ya lita za ujazo ambazo Serikali kama itaweka mpango mkakati wa kusambaza maji yale ya Igombe na kwa unafuu, Wananchi wa Tabora Mjini watapata nafuu ya tatizo la maji.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba yale maji ya Igombe yaweze kusambazwa kwa bei nafuu kuliko kusubiri huo mradi wa Ziwa victoria ambao haujulikani utaanza lini? Hilo la kwanza
Swali la pili, moja ya tatizo lingine linalosababisha ile Mamlaka ya Maji (TUWASA) Tabora inapata matatizo katika uendeshaji wake ni pamoja na kutolipa deni ambalo Mamlaka ya Uendeshaji ya Maji - TUWASA pale Tabora inaidai Serikali kwa muda mrefu zaidi ya shilingi bilioni 2.3 ambazo zinadaiwa hasa kwenye taasisi zetu za majeshi pamoja na taasisi zingine za Serikali.
Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha TUWASAwanalipwa pesa hizo ili Tabora iweze kupata maji ambayo yatakuwa ni ya uhakika? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka tuweke kumbukumbu sawa. Katika mradi huu wa Tabora-Sikonge ambao katika bajeti yetu mwaka huu nadhani tulipitisha pamoja hapa. Tulitenga takribani shilingi bilioni 29 ukiangalia kitabu cha maendeleo lakini kwa juhudi kubwa zilizofanywa na Serikali kupitia ufadhili kutoka India ndiyo maana nimesema ile figure zaidi ya shilingi bilioni 500 ambayo Serikali imeshaweka commitment hiyo. Hivi sasa mchakato wa manunuzi upo katika hatua mbalimbali na lengo la mradi huu kati ya mwezi Aprili mpaka mwezi Mei mradi huu utakuwa umeanza, kwa hiyo, ndugu yangu, mtani wangu, Mnyamwezi wa Tabora naomba ondoa hofu katika hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala zima la jinsi gani tutumie bwawa la Igombe, wataalam wetu wameshaanza kufanya tathmini pale. Takribani ule mradi utagharimu shilingi bilioni 1.5 na hili ndiyo maana tumeona kwamba jambo hili kama Ofisi ya Rais - TAMISEMI lakini na kushirikiana na wenzetu ambao ni Wizara mama wa Wizara hiyo tutaangalia jinsi gani tutafanya kwa pamoja katika mchakato wa pamoja wakati tunasubiri mradi mkubwa wa maji wa hizo shilingi bilioni 500, jinsi gani tutafanya hizo back up strategy ya mradi mwingine huu mdogo katika bwawa la Igombe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo lengo letu kama Serikali ni kuweza kutatua shida ya maji katika Mkoa wa Tabora na ndiyo maana nimesema mradi huu siyo Tabora peke yake, kuna watu wa Tinde pale, kuna watu wa Kahama, kuna watu wa Shinyanga mradi huu utakuja kujibu matatizo ya watu wote wa ukanda ule. Niseme, Wasukuma na Wanyamwezi wa eneo hilo mmepata bahati kubwa sana kwa Serikali kuwaona kwa jicho la karibu kuwatengea takribani shilingi bilioni 580.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hata hivyo, suala zima la bili ya maji; suala la bili ya maji ni kwamba tumetoa maelekezo mbalimbali hapa kwamba bili ya maji kupitia Waziri wa Maji ameshatoa maelezo mbalimbali, sasa naomba niziase taasisi mbalimbali; kila taasisi inayodaiwa deni la maji liweze kulipa deni la maji siyo Tabora peke yake lakini katika maeneo yote ya nchi hii, kama taasisi inayodaiwa na maji, miradi hii ya maji au hizi mamlaka za maji zitashindwa kutupatia maji kwasababu watu wanashindwa kulipa bili za maji.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongezana ninaomba kuiuliza Serikali kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali imekiri kwamba hii migogoro kweli ipo na ni ya muda mrefu, Jimbo la Tabora Mjini linazungukwa na kambi nyingi za Jeshi ambazo migogoro mingi inapelekea kuhatarisha amani miongoni mwa wanajeshi pamoja na raia. Ni lini sasa Serikali au Serikali ina mpango gani wa kuwakutanisha wanajeshi wahusika ili waweze kukaa na wananchi kuweza kutatua migogoro hiyo ya ardhi iliypo Tabora Mjini?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Serikali inafanya uhakiki mbalimbali kuanzia watumishi wa Serikali na mpaka leo tumeona wale wa vyeti, lakini ni lini Serikali itafanya uhakiki wa hawa Maafisa wa Ardhi ambao wanaingiza migogoro kwa makusudi kati ya wananchi pamoja na Serikali kwa kufanya mpango wa kugawa viwanja; kwa mfano kiwanja kimoja kutolewa zaidi ya mtu mmoja (double allocation). Maafisa hao wapo na hawajafanyiwa uhakiki ili wachukuliwe hatua. Ni lini Serikali itafanya uhakiki wa hawa maafisa wanaoleta migogoro ili na wao wachukuliwe hatua?
NAIBU WAZIRI ARDHI, NYUMBA, MAENDELEO NA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kwanza niseme tu ni kweli alichokisema kwamba maeneo mengi ambayo yamezungukwa na Majeshi na wala si majeshi tu hata watu wengine wa kawaida, kumekuwa na migogoro baina ya wananchi na pande ya pili inayomiliki wakiwemo Jeshi. Kuhusu zoezi alilouliza, mimi nimwambie tu kwamba naomba wananchi wa Tabora wawe na subira kwa sababu tayari zoezi la kuhakiki maeneo ambayo yana migogoro na yale ambayo yanamilikiwa na Jeshi limeshaanza. Upande wa wenzetu Wizara ya Ulinzi wameshaunda kamati ambayo imeanza kupitia katika maeneo na mimi nikiri tu wazi na ni-declare interest kwamba hata kwenye Wilaya yangu pia kulikuwa na tatizo hilo lakini tayari Kamati ile imeanza kupita na wanafanya uhakiki wa mipaka.
Mheshimiwa Spika, na wanapofika katika maeneo
yale wanahusisha uongozi wa eneo husika. Kwa hiyo, wakifika pale lazima uongozi wa Wilaya na uongozi wa Mitaa au Vijiji vinavyohusika watahusishwa ili kuweza kubaini ile mipaka iliyokuwepo toka mwanzo. Wenzetu Jeshi wameenda mbali zaidi, kwa yale maeneo ambayo watakuwa hawayahitaji baadae watasema nini cha kufanya katika eneo hilo, ikiwa ni pamoja na kuyarejesha pia kwa wananchi; lakini ni baada ya uhakiki kwasababu mengine yako strategically huwezi kuyaondoa leo na kuwapa wananchi. Kwa hiyo, uhakiki huo Mheshimiwa nikuhakikishie umeshaanza, unafanyika na Tabora watafika na tatizo litakuwa solved.
Mheshimiwa Spika, swali la pili amezungumzia suala la uhakiki wa maafisa ambao wanaingiza mgogoro kati ya Serikali na wananchi. Mimi niseme tu kwamba katika ziara ambazo tunafanya mimi pamoja na Mheshimiwa Waziri kila tunapopita tukikuta kuna tatizo hatua zinachukuliwa palepale. Ni juzi tu hapa alikuwa Lindi ambako tumekuta kuna mtu kamilikishwa eneo kubwa la wananchi zaidi ya ekari 4,000 lakini Mheshimiwa Waziri ame-declare pale pale kwamba ardhi ile irudi kwa wananchi na yule mtumishi amesimamishwa. Hata hivyo mimi pia nilipopita katika maeneo yale kuna wafanyakazi idara hiyo tumewatoa katika eneo lile na kuweza kutafuta wale wengine wanaohusika.
Mheshimiwa Spika, niseme kwa upande wa Maafisa Ardhi wale ambao ni wateule ni jukumu la Halmashauri, tukiona kwamba huyu mtu hafanyi kazi yake vizuri ni lazima tumuondoe na tunaleta jina lingine kwa maana ya ku-propose ateuliwe kuwa Afisa Ardhi Mteule; kwa sababu wale nao wasipofanya kazi yao vizuri hawa wadogo wa chini wanaharibu kazi zaidi. Kwa hiyo, ni jukumu letu sote katika maeneo yetu kuona wasiofanya kazi vizuri wachukuliwe hatua kwa sababu mamlaka ya ajira yako pale pale katika maeneo yao, kwa maana ya Mkurugenzi. (Makofi)
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Matatizo yaliyopo Kwera yako sawasawa kabisa na matatizo ambayo yapo kwenye Manispaa ya Tabora kwenye barabara ile ya Mambali ambayo inapita Misha, Kata ya Kabila, Kata ya Ikomwa mpaka kutokea Bukene. Barabara hii kwa kiwango kikubwa eneo kubwa lipo eneo la halmashauri na haijapandishwa daraja pamoja na maombi ya muda mrefu. Hata hivyo, kwa kuwa Halmashauri ya Tabora uwezo wa kuitengeneza barabara hii kwa lami unaonekana haupo kabisa, Serikali ina mpango gani kuhakikisha barabara hii inawekwa kiwango cha lami ili iweze kuwa endelevu katika uchumi wa Mkoa wa Tabora? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mwakasaka ni mjumbe wa Kamati yangu ya Miundombinu. Tumeliongea sana hili katika Kamati na naomba tu nirudie kumhakikishia, kama ambavyo tulikuwa tumeongea katika Kamati, kwamba Serikali muda si mrefu itakamilisha kupitia maombi yote ya barabara ambazo zimeombwa kupandishwa hadhi na matokeo ya maombi hayo yatatangazwa kwenye Gazeti la Serikali hivi karibuni.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa Serikali inakiri kwamba ujenzi wa bwawa hili ulikamilika mwaka 1958, kwa maana hiyo ujenzi huu uliwakuta wananchi wengi ambao walikuwepo pale kwa miaka mingi kabla ya hapo na kwa kuwa wananchi wanaendelea kunyanyasika maeneo yale na hasa kwa kukosa sehemu ya kilimo; na kwa kuwa kuna wananchi ambao wao ni waaminifu na hawaharibu mazingira.
Je, Serikali iko tayari angalau kuwapa wananchi maeneo mbadala ya kuweza kufanya shughuli zao za kilimo maeneo yale?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa maeneo yale kumekuwa na matatizo ambayo yanahusiana pia na mifugo ya wananchi hao hao wamekuwa wakikamatiwa mifugo yao na maafisa wa wanyamapori na wengine wala siyo maafisa wa wanyamapori wamekuwa wakiwanyanyasa wananchi, wakikamata ng’ombe zao na wengine kuwapiga fine ambazo hazina hata receipt.
Nini tamko la Serikali kuhusu hawa maafisa wa wanaymapori hewa ambao wanakuwa wanafanya uhalifu ndani ya maeneo yale?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, mwaka 1958 eneo la Hifadhi ya Igombe halikuwa na wati wowote waliokuwa wanaishi pale katika kipindi hicho, kwa hiyo wote wameingia baada ya huo mwaka kwahiyo hakuna uhalali wowote kusema kwamba wananchi wameingiliwa na Mkoa wa Tabora bado ni mkubwa kwa hiyo watu wanaweza wakatafuta maeneo mengine kwenda kuendeleza maisha yao.
Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la unyanyasaji, ni kwamba mifugo na wewe Mheshimiwa Mbunge unafahamu kwamba sasa hivi Serikali inajitahidi. Tumekuwa kwamba watu hawakuwa na maeneo kwa ajili ya mifugo yao, lakini tumeendeleza kuongeza mifugo bila kutafakari ni jinsi gani ambavyo tunaweza tukamiliki maeneo yetu kwa ajili ya mifugo, kwa hiyo, ni kwamba mifugo imeingia katika lile eneo. Hata hivyo ni lazima tu-balance, ni kwamba lile bwawa likipotea, Tabora haina chanzo kingine cha maji.
Mheshimiwa Spika, sasa hivi angalau tunatoa maji kutoka Ziwa Victoria lakini kabla ya hapo hatukuwa na chanzo kingine. Hebu tujionee huruma sisi kam binadamu. Mifugo imeingia pale, tuache lile bwawa kwa ajili ya matumizi ya binadamu watu wa mifugo watafute eneo lingine. Mimi niseme hakuna unyanyasaji wa aina yoyote lakini mnyanyasaji ni yule mfugaji ambae anaingia katika lile eno halafu anasingizia watu wa Serikali.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tatizo la kutolipa wakandarasi au wazabuni katika sehemu mbalimbali za nchi hasa wale ambao wanatoa huduma kwenye vituo vya polisi limekuwa ni kubwa kwa muda mrefu. Kwa mfano, mkoani Tabora kuna wazabuni wengi ambao wanaidai polisi malimbikizo ya muda mrefu ya huduma wanazotoa na hasa utengenezaji wa magari.
Kwa mfano Tabora yapo malalamiko ya muda mrefu ya mzabuni ambaye anatengeneza magari ya polisi hajalipwa sasa hivi ni zaidi ya miaka mitatu, anadai zaidi ya shilingi milioni 222. Sijui Mheshimiwa Waziri anazo taarifa hizi na kama hana, atasaidiaje mkandarasi huyu ambaye ndiye anatengeneza magari ya polisi pale Tabora Mjini alipwe fedha zake?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninazo taarifa anazozisemea Mheshimiwa Mbunge. Nakumbuka nilivyotembelea Mkoa wa Tabora nililetewa jambo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi, ni utaratibu wa Serikali tulioweka wa kuhakiki kwanza madeni yote. Baada ya kuwa tumeshafanya uhakiki, yale madeni ambayo yamehakikiwa ndiyo yanalipwa kukiwa na kumbukumbu sawa za kazi iliyofanyika na fedha zinazodaiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, kwa jambo hili ulilolileta Mheshimiwa Mbunge, mhakikishie mtoa huduma huyo kwamba baada ya uhakiki huo ambao ulishafanyika nitawaelekeza watu wangu waweke kipaumbele katika kulipa madeni hayo ili kutokuwakwamisha wazabuni wetu kuweza kuendelea na shughuli zao na kutoa huduma hizo ambazo wametoa hata huko kwetu.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tabora Manispaa tuna tatizo kubwa la msongamano wa wagonjwa katika Hospitali Teule ya Kitete na kwa kuzingatia hilo, Tabora Halmashauri kwa kushirikiana na Madiwani pamoja na wananchi wengine tumetenga eneo kwa ajili ya kujengwa Hospitali ya Wilaya ambayo mpaka sasa hivi ujenzi wake unasuasua kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Je, Serikali inajipanga vipi katika kusaidia uwezeshaji wa kuweza kujenga hospitali hiyo ya wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimshukuru Mheshimiwa Mwakasaka pamoja na Waheshimiwa Madiwani katika Manispaa ya Tabora kwa kutenga eneo la kujenga Hospitali mpya kwenye Manispaa ya Tabora ambayo itakuwa Hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msingi huohuo, kwa kuzingatia kwamba Hospitali ya Kitete ni kweli imezidiwa na mzigo maana yake ndiyo hospitali pekee ya rufaa ya mkoa, Serikali inaahidi na namwomba ushirikiano wake, wakati tutakapokuwa tunaweka kwenye bajeti tushirikiane ili tuweze kupitisha kwa pamoja. Ahsante sana.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nukipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Mkoa wa Tabora una vivutio vingi vya utalii ukiwemo uwandaji. Ni lini Serikali itafanya uhakiki wa vitalu vya uwindaji vilivypo Tabora? Kwa sababu kuna taarifa kwamba vitalu vya uwaindaji vilivyopo vinasomeka ni vichache kuliko uhalisia wa vitalu vilivyopo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa kuna vitalu viko vingi katika nchi yetu na kazi yetu kubwa ambayo tunaifanya sasa hivi, tunapitia upya vitalu vyote ili tuweze kuvibaini na kuona vipi vinafaa na vipi havifai. Kwa hiyo badaa ya kukamilisha hilo zoezi ni wazi kabisa Mheshimiwa Mbunge atafahamu ni vitalu vingapi ambavyo vinapatikana katika Mkoa wa Tabora.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Tabora Manispaa imeathirika sana na migogoro ya ardhi. Kuna kata ambazo zinapakana na maeneo ya jeshi, ambazo ni Kata za Cheyo, Mbugani, Tambuka Reli, Uyui na Micha. Maeneo yale yamekuwa na migogoro ya mipaka ya muda mrefu. Je, Wizara ya Ardhi imejipangaje kwa kushirikiana na Wizara ya Ulinzi ili waweze kuoanisha sasa mipaka halisi ili kuweza kutatua migogoro hii ya mipaka katika kata hizo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Tabora kama nilivyosema manispaa imekuwa na migogoro mikubwa ya ardhi na hasa bomoa bomoa. Tabora imeathiriwa sana na zoezi la bomoa bomoa; si maeneo ya reli tu lakini hata maeneo mengine yanayopaka na mashule kama Tabora Girls…
Wananchi wale na maafisa kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri wengine si waaminifu. Je, Serikali kwa kuwa hawa wananchi wengi waliobomolewa hayakuwa makosa yao, inawachukulia hatua gani hawa ambao wamesababisha wananchi wamepata hasara kubwa na sasa hawana hata amani na wamekuwa katika hali isiyoeleweka?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza amezungumza habari ya mipaka kuathiri maeneo yaliyopakana na Jeshi na ametaja kata ya Cheyo, Tambuka Reli na nyingine. Naomba tu nimthibitishie Mheshimiwa Mwakasaka kwamba Wizara ya Ulinzi ilishachukua hatua ya kuunda Kamati ambayo imepitia katika maeneo yote ambayo yana migogoro ya Jeshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo hayo walikuwa wakifika wanaongea na watu wa eneo lile na kuweza kubainisha mipaka; kwa sababu kuna mengine ambayo wananchi lakini maeneo mengine Jeshi liliingia ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kabla ya kuanza kuweka mipaka upya au kuipitia kwanza wanachambua yale maeneo. Wakishamaliza shughuli hiyo ndiyo Wizara itaingilia kati katika suala la kupanga. Hata hivyo, kwanza tuitambue tuibaini ili kuondoa ile migogoro. Zoezi limeshaanza katika baadhi ya wilaya na Kamati ile inafanya kazi vizuri kwa sababu inashirikisha uongozi wa maeneo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la bomoa bomoa katika maeneo ambayo yamevamiwa au watu wamebomolewa pengine hawakuwa na tahadhari; kwanza naomba nitoe tahadhari kwa wananchi wengi, kwamba maeneo mengi ya taasisi za umma yamevamiwa sana na wananchi na wengine wamejenga nyumba za kudumu kwa muda mrefu. Hata hivyo, unapoangalia kisheria na taratibu na ukubwa wa shule yanayotakiwa kuwa unakuta sehemu nyingi yamevamiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa makosa ya watendaji wetu kuna wengine pia walithubutu kutoa hati katika maeneo ambayo ni ya shule. Kwa hiyo zoezi hili linafanyika ili kuhakikisha kwamba maeneo yote yanapimwa na yanatambulika na wale wote walioingia ndani basi sheria inachukua mkondo, wake kwa maana ikiwa ni pamoja na kuvunjiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wale ambao watakuwa wamevunjiwa kimakosa ni lazima uhakiki ufanyike tuweze kujua pengine hata ile hati aliyonayo si sahihi. Kwa hiyo kama tukikuta mtu amevunjiwa katika utaratibu ambao ni wa kimakosa basi tutaona namna ya kuweza kumpatia kiwanja mbadala. Nitoe rai tu kwamba wale wote walioko kwenye maeneo ya umma ni vizuri wakayaachia.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza, tatizo la akina mama kujifungua mara nyingi wakati mwingine linaletwa pia na matatizo ya baadhi ya ma-nurse ambao huwa wanawanyanyapaa akina mama wenzao wanapotaka kujifungua.
Sasa sijui Serikali ina mpango gani au huwa inachukua hatua gani kuwadhibiti hawa akinamama ambao wana tabia za kuwanyanyasa akina mama wenzao wanapotaka kujifungua? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa na tatizo la baadhi ya watoa huduma kutoa lugha zisizokuwa sahihi kwa wagonjwa ambao wanafika katika hospitali, na hili ni jambo ambalo ni kinyume kabisa na maadili na taaluma za afya ikiwa ni pamoja na ma-nurse.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeendelea kuimarisha mabaraza yetu na hivi karibuni, wiki iliyopita tu, Mheshimiwa Waziri alitoa kauli ya kuhakikisha kwamba watoa huduma wote, ikiwa ni pamoja na madaktari na ma-nurse, wanakuwa wanatoa huduma nzuri ambayo inazingatia maadili na miiko ya kazi ambayo wanayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naendelea kulisisitiza hilo, na tumeendelea kuimarisha mabaraza yetu na tumeanza kuchukua hatua kwa wale ambao wanakiuka taratibu hizo.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Mamlaka ya Maji ya Tabora Mjini (TUWASA) ina matatizo makubwa ya malimbikizo ya madeni zaidi ya bilioni mbili ambayo inawadai Taasisi za Serikali na hasa majeshi yetu na kwa kuwa Mheshimiwa Waziri amesema katika majibu yake ya msingi kuna pesa zimetengwa kulipa katika miradi mbalimbali. Je, ni lini Mamlaka ya Maji Tabora watalipwa pesa zao ambazo zinawafanya sasa wasifanye kazi kwa ufanisi?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, madeni ya maji ambayo Taasisi za Serikali zinadaiwa katika mwaka wa fedha zitalipwa moja kwa moja kwenye Fungu la Hazina. Kwa hiyo, tutakapoanza kutekeleza Bajeti hii ambayo mmeipitisha tutaangalia tuweze ku-manage fedha zile, tuweze kulipa kwenye mamlaka husika ili waweze kuendelea kutoa huduma za maji.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza. Kwa kuwa hii biashara ya vyuma chakavu inavikumba pia viwanda vilivyobinafsishwa kwa muda mrefu sasa kikiwemo Kiwanda cha Nyuzi Tabora, na kwa kuwa kuna taarifa kwamba mashine nyingi mle ndani zimeuzwa kama chuma chakavu na kimefungwa kile kiwanda, je, Mheshimiwa Waziri, kwa sababu nimewahi kulalamika hapa Bungeni na kutoa taarifa kuhusu kufanyika kwa vyuma
chakavu, ni lini tunaweza tukaenda tukakagua kile kiwanda kwa sababu sasa hivi umetoka kusema utakula nao sahani moja, tuweze kujua kama vile zile mashine hazijauzwa kama vyuma chakavu?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kiwanda cha Nyuzi cha Tabora kina mwenye nacho (owner) kwa hiyo, mwenye mali anapoibiwa mimi siwezi kwenda kuangalia mali yake yule, lakini taarifa nilizonazo kutoka kwa mwenye kiwanda ameniambia amepata soko la nyuzi na kiwanda hicho kitaanza kazi. Kwa hiyo, mimi naweza kumbana yule kwa kupitia msajili wa hazina kwamba aanze kazi na ndio wajibu wangu. Sasa kama alizembea, mali ikaibiwa mle hilo nadhani ni suala la kila abiria achunge mzigo wake.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Chama cha Mapinduzi inatekeleza mradi mkubwa sana wa maji wa kutoka Ziwa Victoria kwenda Tabora na mradi huo kuna kipindi vifaa vya ujenzi vilikuwa vina mikwamo kwamo. Swali langu ni dogo tu, je, mradi huo umefikia kwenye hatua gani ya utekelezaji na wananchi wa Tabora wategemee kupata maji hayo lini? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji unaendelea vizuri sana, tulikuwa na matatizo machache ya kuhusu masuala ya msamaha wa kodi lakini tumeshayamaliza, na Mheshimiwa Mbunge wewe mwenyewe ni shahidi; wakandarasi wote watatu wameshaanza kazi, mabomba wanaendelea kuleta na sasa hivi kama unaenda barabara ya kwenda Dar es Salaam utakutana na malori yanabeba mabomba kupeleka Tabora; kwa hiyo mradi unaendelea vizuri. (Makofi)

MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lililopo Chamwino ndiyo tatizo lililopo Manispaa ya Tabora. Ofisi mpya ya Halmashauri imekwama kwa muda mrefu sasa kukamilika kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Kwa kuwa ombi maalum kupitia Hazina Serikali iliahidi kutoa shilingi bilioni mbili ili kuweza kukamilisha ujenzi huo pamoja na kumlipa mkandarasi anayedai karibu shilingi bilioni moja Masasi Construction.
Je, Serikali ni lini italeta pesa hiyo kwenye Halmashauri ya Manispaa ya Tabora ili jengo hili liweze kukamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli lilikuwa ombi maalum, lakini tutaenda kulifanyia kazi. Siwezi kutoa commitment hapa lakini tutaenda kulifanyia kazi tuangalie kwamba lile ombi la awali limefikia wapi halafu tutapeana mrejesho nzuri na Mheshimiwa Mbunge, kwa sababu najua ni kweli Manispaa ya Tabora wanapata shida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tutakwenda kuangalia jinsi gani tutafanya.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Katika Jimbo la Tabora Mjini, Kata ya Ikomwa maeneo ya Kapunze; Kata ya Kabila, maeneo ya Igosha; Kata ya Ndevelwa, maeneo ya Ibasa; na mengine ambayo kwa muda mrefu hayana mawasilino, Halotel inaonekana inasuasua hata kwenda kufanya survey tu maeneo yale. Sijui Serikali ina mkakati gani kuhakikisha hawa Mameneja wa Mikoa wa Halotel wanafanya kazi ipasavyo ili maeneo hayo yapatiwe huduma ya mawasiliano? Serikali ina mkakati gani kwa kuwa hiyo pesa inalipwa na Serikali kuhakikisha hawa Mameneja wa Mikoa wa Halotel wanafanya kazi yao kwa ufanisi.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa taarifa hiyo, lakin nataka tu niweke record sawa, Kampuni ya Halotel haijengi kwenye vijiji kwa kutumia fedha za Serikali ni fedha zao ila tumekubaliana na Serikali kwamba tuwape unafuu fulani wa kupata wayleave bila kulipa fidia ili waweze kufikisha mawasiliano katika vijiji vingi zaidi Tanzania, tuliwapa vijiji 4,000. Kwa hiyo ni fedha zao siyo hela za Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda tu nimhakikishie kwamba tutaliangalia na hilo eneo, tuone kama Halotel wataweza kufikisha mawasiliano mapema au tuviingize hivi vijiji katika mpango wa Mawasiliano kwa Wote, ambapo hapo ndiyo tunatoa fedha za Serikali kwa makampuni ambayo yanashinda tenda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana kwa juhudi zake za kufuatilia masuala ya wananchi wake na mkutano wetu uliotukutanisha mimi na Waziri wangu kuyaongelea haya masuala, nimhakikishie kwamba tutatekeleza yale ambayo tulikubaliana kwenye kikao pamoja na kwamba leo amerudia kuliuliza hilo, labda kwa sababu ni muda mzuri wananchi wasikie. Hata hivyo, tunatambua juhudi zake na kwa namna ambavyo amelifuatilia sana suala hilo ofisini kwetu. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Walimu ndiyo wanaowalea watoto wetu shuleni na ndiyo wanaotegemewa zaidi kuwa walinzi wa watoto hawa wanapokuwa shuleni. Hata hivyo, baadhi ya Walimu ndiyo wamekuwa na tabia za kuwadhalilisha watoto kwa vitendo mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa kuwa kuna suala la elimu, mtoto yule anakuwa mwoga kutoa taarifa pale anapodhalilishwa na Mwalimu. Serikali ina mkakati gani wa kuwapa watoto elimu ili wawe na ujasiri wa kuripoti vile vitendo ambavyo wanafanyiwa na baadhi ya Walimu? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Serikali imeweka utaratibu shuleni wa kuwawezesha watoto wa kike kuwa na ujasiri wa kuripoti matukio ya udhalilishaji ambayo yanafanyika yaani life skills na pia tumeanzisha club mbalimbali za kuwawezesha watoto kuwa na ujasiri wa kuweza kuripoti matukio hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitumie fursa hii kuomba na kuwasihi watoto wasiwe na uwoga wowote kwa sababu Serikali yao inawalinda. Pale ambapo anafanyiwa vitendo ambavyo ni kinyume na matakwa ya Serikali, watoe taarifa na hatua kali zitachukuliwa dhidi ya wote wanaodhalilisha watoto na kuwasababishia wasisome shuleni kwa amani. (Makofi)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa hawa baadhi ya maaskari wetu ambao wamekuwa wakiwakamata hawa bodaboda wakiwa kwenye mwendo na kuwasababishia ajali ambapo wengine wamepata ulemavu mkubwa na hata kusababisha kifo. Sijui Serikali pale inapokuwa imethibitisha kwamba uzembe ulikuwa ni wa askari na yakatokea madhara kwa muendesha bodaboda, sijui huwa wanakuwa na mpango gani wa kuwapa fidia hawa waendesha bodaboda? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini swali langu la pili, kuna malalamiko mengi ya waendesha bodaboda kwamba mara nyingi wanapokuwa wamekamatwa huwa wanabadilishiwa mashtaka wanapofika kituoni. Sasa kwa kuwa hatuna CCTV camera za kuangalia hasa yule wa bodaboda alikamatwa kwa kosa gani, je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba kosa lile alilokamatiwa yule mhusika ndilo analoshtakiwa nalo? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kuleta swali hili kwa sababu ni kweli ni jambo ambalo linajitokeza katika baadhi ya maeneo na linaleta malalamiko.
Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba maisha ya vijana wetu yakipotea hayana fidia ya kusema umeweza kufidia maisha. Kwa hiyo, jambo ambalo tunafanya kama Wizara kwa kweli sisi kiutawala tunaelekeza utaratibu wa kiustaarabu wa ukamataji wa vijana hawa ili isisababishe ajali ambazo zinapoteza maisha kwa vijana wetu. Pia, tumeendelea kuwaelezea vijana wetu kwa sababu wamekuwa na uongozi kwenye vituo vyao kuhakikisha kwamba nao wanatoa ushirikiano, kwa wale ambao wamefanya makosa ni haki yao kufika kwenye adhabu ili kuweza kupunguza makosa hayo yanayojitokeza.
Mheshimiwa Spika, kuhusu yale ya kubambika kesi hilo ni kosa la kimaadili na sisi kama Wizara wale wote wanaofanya haya kwa wananchi wanachukuliwa hatua kwa mujibu wa utaratibu wa ufanyaji kazi wa Jeshi la Polisi.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na taarifa mbalimbali kuhusu baadhi ya halmashauri kutoa mikopo hii ya vijana na akina mama kwa upendeleo. Serikali imewahi kulifanyia uchunguzi jambo hili na inasema nini kuhusu suala hili kama kweli lipo katika baadhi ya halmashauri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ngazi yetu sisi ya Wizara hivi karibuni hatujawahi kupokea malalamiko ambayo ni ya msingi kabisa kutoka katika halmashauri yoyote, kwamba kuna upendeleo katika utoaji wa mikopo. Kwa sababu utaratibu uliopo kila halmashauri inatakiwa iwe na Kamati ya Mikopo ambayo ndiyo hupitisha mikopo ile na miongoni mwa Wajumbe wa Kamati ya Mikopo ni Waheshimiwa Madiwani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nijibu tu kwamba, kwa kweli utaratibu uliopo inawezekana kuna baadhi ya vikundi vikawa havijaguswa kwa mwaka ule husika kwa sababu fedha zenyewe zinakuwa hazitoshi, ni kidogo. Kwa mfano, unaweza ukawa na shilingi bilioni moja ukataka kutoa mikopo kwa vikundi 80 katika halmashauri, lakini halmashauri ina vikundi 600 kwa hiyo ni wazi kwamba kuna baadhi ya vikundi vitakosa. Kwa hiyo, jambo la msingi ambalo nataka nishauri halmashauri ni kwamba wasirudie kuvipa mikopo vikundi ambavyo vilipata mikopo mwaka jana na mwaka huu vikapata, bali vipate ambavyo mwaka jana havikupata. Huo ndiyo utaratibu mzuri zaidi na hiyo ni kupitia Kamati ya Mikopo ya Halmashauri.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Halmashauri nyingi ikiwemo ya Tabora Manispaa uwezo sasa wa kifedha hasa zile zinazotokana na own source umepungua kutokana na baadhi ya mapato ya Halmashauri kwenda kwenye Serikali Kuu na hii imesababisha huduma nyingine kama za afya na hasa vituo vya afya Halmashauri kushindwa kupeleka fedha kule kutokana na upungufu huo. Serikali ina mpango gani wa kuziba pengo hilo ili zile Halmashauri ambazo hazina uwezo ziweze kupata fedha ambazo zinaweza kusaidia vituo vya afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakasaka, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata fursa ya kutembelea Manispaa ya Tabora na katika nafasi ile tulitembelea na kuona vyanzo vya mapato vya Manispaa ya Tabora. Nilikuwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge na tukawashauri, vile vyanzo vilivyopo kwanza ni vizuri wakavisimamia wakahakikisha kwamba hakuna hata senti tano ambayo inapotea. Tulitembelea eneo la stendi, jinsi ambavyo wanakusanya hatukuridhika na jitihada ambazo zinatumika katika kukusanya, lakini pia kuna vyoo pale na maeneo mengi ambayo hakika wakisimamia vizuri, bado ni maeneo oevu ambayo pesa zinaweza zikakusanywa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kushirikiana na Halmashauri pamoja na TAMISEMI, nguvu yetu tukiweka pamoja hakika huduma katika vituo vya afya na hospitali zitaweza kuboreshwa. Naye mwenyewe ni shuhuda, ameona jinsi ambavyo bajeti ya afya imeongezeka kutoka shilingi bilioni 31 mpaka shilingi bilioni 269. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, ni azma na nia ya Serikali kuhakikisha kwamba tunaboresha vituo vya afya.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza, nianze kwa kuishukuru hii Wizara ya Nishati chini ya Dkt. Kalemani pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Subira kwa kazi nzuri mnayofanya, hongereni sana. Ninaomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Manispaa ya Tabora kwa kuitamka inaonekana kama hata vile vijiji vinavyozunguka ni kama vipo karibu sana, lakini vijiji vingi vipo mbali na maeneo ya mjini. Huu mradi ambao unafadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika kwa ajili ya kusambaza umeme unaonekana unasuasua maeneo mengi ya vijiji hivi ambavyo vimetajwa. Kama kuna uwezekano naomba Serikali iangalie uwezekano wa kuingiza vijiji hivyo kwenye mradi huu wa REA III ili viweze kupatiwa umeme haraka, hilo la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nilipata taarifa kwamba Mheshimiwa Waziri anaweza kufanya ziara Tabora wiki ijayo sehemu za Urambo, kwa kuwa Tumbi hii ninayoizungumzia ipo njiani, anapokuwa Mheshimiwa Waziri anaelekea Urambo lazima atapita Tumbi pale. Je, Waziri yupo tayari kusimama maeneo yale hata kwa dakika chache ili asikilize kero za wananchi pale zinazohusiana na hilo suala la usambazaji umeme?
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Mwakasaka, kwanza hilo la pili nipo tayari kusimama, nitasimama na nitafanya kazi pale, Mheshimiwa Mbunge nakupongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na vijiji kweli kabisa Jimbo la Tabora kwanza lina kata 29 na kata 15 zipo mjini na kata 14 kimsingi zipo vijijini ingawa ni za Manispaa. Nimpe tu taarifa Mheshimiwa Mbunge kwa niaba ya wananchi wake zile kata 14 ambazo kimsingi zipo vijijini tumezipelekea kwenye miradi ya REA kwenye mpango wa Peri-Urban. Kwa hiyo, wananchi wake wataendelea kupata umeme kama kawaida. (Makofi)
MHE. ADAMSON E. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Katika hii Mifuko ambayo wanakopeshwa vijana, kumekuwa na tatizo kubwa la wale wanaokopeshwa kurudisha mikopo hiyo ili na wengine waweze kukopa. Je, Serikali ina mpango gani mahsusi kuhakisha wale wanaokopeshwa wanarudisha ile mikopo ili na wengine waweze kukopeshwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA) Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tunao Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ambao umekuwa ukitoa fedha za mikopo kwa makundi mengi ya vijana na kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge wapo baadhi ya vijana kupitia makundi hayo wameshindwa kurejesha fedha hizi kwa wakati. Tunachokifanya ni kuwasiliana na Halmashauri husika ambao tunafanya kazi kwa pamoja kuhakikisha kwamba wanaendelea kutoa elimu kwa makundi haya ya vijana kwa sababu fedha ile si fedha ambayo inatakiwa tu watu wapewe na ibaki hivyo hivyo, ni pesa ambayo ni revolving. Kwa hiyo, tunaendelea kutoa elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tumekuwa tukifanya kaguzi za mara kwa mara kuwahimiza vijana hawa kuendelea kurejesha fedha, mpaka ninavyozungumza hivi sasa makundi makubwa ya vijana wameelewa na wameanza kurudisha fedha hii kwa ajili ya kuwafanya vijana wengine waweze kukopeshwa pia.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA. Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza. Tabora hasa Manispaa imezungukwa na kambi za jeshi kwa eneo kubwa. Kutokana na hali hiyo kumekuwa na migogoro mikubwa ambayo inapelekea wananchi ambao wamekuwa wakitumia maeneo kwa muda mrefu kufikia hata kupigwa wanapokuwa wanafanya shughuli zao. Kwa mfano, kuna eneo ambalo kuna barabara inapita katika kata nne eneo la Uyui, kuna eneo la Rada, barabara hii ni ya miaka mingi na ni hiyo tu ambayo wananchi wa kata hizo nne wanaitumia, ikifika saa moja na nusu mpaka saa mbili usiku, wananchi wakipita maeneo maeneo yale wamekuwa wakipigwa na wakati mwingine hata kunyanganywa vifaa vyao vya usafiri zikiwemo baskeli. Je, Serikali ina mpango gani kuhusiana na eneo hilo ambalo wananchi wamekuwa wakitumia kama barabara?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa shughuli nyingi zimesimama katika maeneo hayo hasa za wananchi ambao walikuwa wakitumia maeneo hayo kwa kulima ambayo wamekuwa wakilima muda mrefu, lakini wengine na shughuli zao za kiutamaduni kwenye mapori ambayo wamekuwa hata hawayapi athari yoyote. Je, kutokana na hali hiyo ambayo ni ya muda mrefu Mheshimiwa Waziri yupo tayari sasa kuja Tabora ili tuweze mimi na yeye kwenda kukagua maeneo haya na kuyapatia utatuzi ambao ni mgogoro wa muda mrefu? (Makofi)
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara inayopita kuelekea eneo la Rada la jeshi na kwamba wananchi wanapopita hapo wanapigwa, suala hili nitalifuatilia ili niweze kupata taarifa rasmi ya nini hasa kinachoendelea. Hakuna sheria inayoruhusu wananchi kupigwa, lakini kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge nitakuwa tayari kwenda kufanya ziara katika eneo hili la Tabora Mjini ili nijionee mimi mwenyewe hali ilivyo pale na tutafute ufumbuzi, suluhu kwa ajili ya maslahi ya pande zote. Ni vema wananchi watambue kwamba, yale mapori yanayoonekana kama hayana kazi, ni maeneo ambayo wanajeshi wanafanya mazoezi, kwa hiyo yana kazi maalum. Tukifanya hii ziara, tutaweza kuambatana na viongozi wa jeshi ili tuone ni ufumbuzi gani ambao unaweza ukapatikana.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa vijana wengi hasa wa kizazi hiki kipya hawaelewi vizuri umuhimu wa kuuenzi Muungano, Je, Serikali ina mkakati gani wa kutoa elimu ya kutosha hasa kwa vijana wa sasa na hata wale wa zamani ili kujua umuhimu wa kuuenzi Muungano?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue fursa hii kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakasaka kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nimdhihirishie tu kwamba Serikali inaendelea na mchakato na imeendelea kutoa elimu juu ya faida za Muungano na labda kama bado ziko changamoto ambazo elimu hii haiwafikii vijana walio wengi, nadhani ni wakati muafaka sasa wa kuendelea kuhimiza kuhakikisha kwamba elimu hii inawafikia vijana wote.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa kuwa, hili swali limekuwa la muda mrefu na maeneo mengi ya Tabora Mjini zikiwemo Kata za Itetemya maeneo ya Kipalapala, lakini pia maeneo ya Ndevelwa, Ikomwa, Kakola, Uyui na mengine bado yana matatizo mengi sana ya mawasiliano ya simu. Namuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa kuwa hili Bunge lina muda mrefu na tutakuwa na siku za katikati za mapumziko ya wiki, ni lini atakuwa tayari kuongozana na mimi angalau tukakague pamoja miradi hii aweze kuona shida ya wananchi wa sehemu hizo kwenye mambo ya mawasiliano?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Adam Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mwakasaka kwa juhudi nyingi sana anazozifanya katika kushughulikia kero za wananchi katika Jimbo la Tabora Mjini. Mwenyewe nimekwishafika pale, Mheshimiwa Mwakasaka na unakumbuka tulikuwa wote tukazungukia baadhi ya maeneo niliyozungumza yamefungiwa minara na nakuhakikishia kwamba niko tayari wakati wowote twende kutembelea maeneo mengine na nitaambatana na timu ya watalaam kutoka Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote pamoja na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania, ahsante.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Shule ya wasichana ya Tabora (Tabora Girls) ni shule kongwe sana hapa nchini ambayo pia ina vipaji maalumu. Shule hii kwa muda mrefu imetelekezwa kuhusu uzio. Ile shule haina uzio kabisa kwa miaka mingi na tayari juhudi za viongozi mbalimbali nikiwemo mimi mwenyewe tumeshaanza mkakati wa kujenga uzio huo.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutusaidia katika kukamilisha uzio huo wa Shule ya Wasichana Tabora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa
Mwenyekiti, nakushukuru. Namwomba Mheshimiwa Mbunge tuonane tuone. Kama wananchi wameanza kujitolea na wadau mbalimbali akiwepo Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri ya wananchi wake anaowawakilisha hapa Bungeni, basi tuonane tuone ni changamoto gani zilizopo na sehemu gani ya kuweza kusaidia kumalizia uzio huo.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, la kwanza, kwa kuwa madeni haya ni ya muda mrefu na imetokea mara nyingi Serikali imekuwa ikilipa madeni yaliyokuja baadaye wanaacha yale ya nyuma. Sijui ni vigezo gani vinatumika kuacha madeni yale ya muda mrefu na kulipa yale ambayo yamekuja baadaye?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; wazabuni wengi wanaodai magereza kwa maana wale wanaofanya zabuni ya chakula wengi sasa wana hatari ya kuuziwa nyumba zao hasa wale ambao wamekopa katika taasisi mbalimbali za fedha. Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha hawa wazabuni mbalimbali inawakomboa wasiweze kuuziwa nyumba zao na taasisi za kifedha?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, madeni ambayo yanalipwa ni miongoni mwa madeni ambayo tumeshalipa kama ambavyo nimeeleza katika jibu la msingi pia yako madeni ya zamani na nilieleza kwamba madeni mengine ambayo hayajalipwa ni kutokana na kwamba mengine yameshahakikiwa na hivyo basi pale fedha ambapo zitapatikana yatalipwa. Naamini kabisa yatakapokuwa yamekamilika madeni hayo kulipwa kama ambavyo nia ya Serikali ilivyo basi yale matatizo ambayo yanakabiliwa na hawa wazabuni yataweza kupatiwa ufumbuzi. Ni dhamira ya Serikali kuhakikisha madeni haya yanalipwa ili kuepusha usumbufu wowote kwa wazabuni wetu.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nami niweze kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nilikuwa na swali kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Tabora mjini pamoja na kwamba liko mjini lina Vijiji vipatavyo 41 ambavyo mawasiliano yake si mazuri na Mheshimiwa Naibu Waziri Nditiye hivi karibuni tulitembea wote baadhi ya sehemu.

Swali kwa kuwa tayari andiko lilishaandikwa la kuomba minara ya simu kwa TTCL sijui zoezi hilo limefikia wapi kuhakikisha Vijiji hivyo vinapata mawasiliano ikiwepo eneo tulilokwenda pamoja Mheshimiwa Waziri linaloitwa Iteteme?
WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Mbunge Mwakasaka kama ifuatavyo. Kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake kuhusiana na masuala ya tenda, lakini kwa nyongeza ni kwamba nchi yetu kwa sasa ina usikivu wa asilimia 94, imebakiza asilimia 6, na kama alivyozungumza kwamba tumetangaza tender nyingine ambayo Vijiji 1222 sasa vitapata minara.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Mwakasaka na ndugu zangu majirani zangu wana Tabora baada ya hii tenda tunakamilisha minara kwenye maeno yote usikivu utakuwepo maeneo yote pamoja na eneo la delta.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri yaliyotolewa na Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, wazabuni wengi na nina imani hii ni kwa nchi nzima lakini hapa niwe specific kwa Tabora, ni wafanyabiashara wadogowadogo na wengi wapo sokoni wamekuwa waki-supply vyakula mbalimbali Serikalini kwa maana ya magereza na hata shuleni. Wengi wa wazabuni hao pamoja na kuhakikiwa madeni yao, hawajalipwa kuanzia mwaka 2013, inafika miaka sita (6) sasa na wazabuni hawa wengi wamekopa kwenye mabenki. Leo hii wengine wameuziwa nyumba zao na wengine wana kesi mbalimbali mahakamani. Serikali inasemaje kuhusu suala hili la kuwalipa wazabuni hawa kwa sababu madeni yao ni ya muda mrefu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kumekuwa na mtindo wa walipaji ambao wapo kwenye malipo mbalimbali hayo ya wazabuni kulipa madeni ya karibuni yaani wao kwa mfano deni ni la mwaka huu au la mwaka jana wanalipa hayo kwanza, yale ya miaka mingi ambayo watu wamekuwa na madeni haya ambayo yamepelekea mpaka kuuza nyumba zao hawalipi. Serikali inasemaje kuhusu hilo suala hilo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mwakasaka, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la kwanza kwamba wapo wazabuni tangu 2013 hawajalipwa. Naomba kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Serikali yetu kama nilivyosema kwenye jibu la msingi imekuwa ikilipa madeni haya kila mwaka. Kuanzia mwaka 2016/2017 tulitenga bajeti ya shilingi bilioni 625 na tukalipa shilingi bilioni 746. Mwaka 2017/2018 tulitenga shilingi trilioni 1 kwa ajili ya ulipaji wa madeni na tukalipa shilingi trilioni 1.096. Mwaka 2018/2019 tumetenga shilingi bilioni 600 na tukalipa shilingi bilioni 600.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tumeendelea kulipa madeni haya. Sasa linalonishangaza ni kusema kuna wazabuni wadogowadogo wa tangu mwaka 2013. Naomba nitoe wito wangu kwa Makatibu Tawala wa Mikoa wote waweze kuwasiliana na wazabuni kwenye mikoa yao ili wahakikishe kama madeni yao bado ni halali kwa sababu madeni yote ambayo ni halali tumekuwa tukiyalipa mpaka mwaka 2020/2021 tutakuwa tumekamilisha kulipa madeni yote na deni lililopo sasa ni shilingi bilioni 325 tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili ni kwa nini wanalipa madeni ya karibuni. Tuna vigezo vya ulipaji wa madeni haya, kigezo kimojawapo ni kuhakikisha kuwa madeni ya zamani yanapewa kipaumbele kwenye kulipwa. Kwa hiyo, nitoe wito wangu kwa Maafisa Masuuli wote wanapopelekewa fedha za kulipa madeni wafuate vigezo walivyopewa na Mlipaji Mkuu wa Serikali ili tuweze kuwasaidia wazabuni wetu.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kumekuwa na vitendo vingi vya unyanyasaji na hasa kwa watoto wadogo ambavyo haviripotiwi kabisa na akina mama kwa sababu ya kuogopa wakati mwingine usalama wao, lakini wengine pia kwa sababu ya kutojua haki zao za Kisheria. Sijui Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha akina mama wanapata elimu hiyo ili watoto wanapopata matatizo ya kudhalilishwa waweze kuwa na ujasiri wa kuripoti vitendo hivyo?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini kwa swali lake la nyongeza kuhusu uwepo wa vitendo vya ukatili dhidi ya watoto. Swali lake kwa ujumla anasema tuna mkakati gani wa kutoa elimu, nimetoa maelezo wakati najibu swali la Mheshimiwa Sonia Magogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kubwa tutaendelea na jitihada za kutoa elimu kwa jamii kupitia vyombo vya habari hata ukiangalia TV, ukisikiliza radio na vipeperushi mbalimbali, tumekuwa tukichapisha juu ya suala hili la vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto. Mkakati mwingine Mheshimiwa Mwakasaka ambao tunautumia, tuna namba ya simu bure 116 ambayo inatoa fursa kwa mtu yeyote na nitumie fursa hii kuliarifu Bunge lako tukufu kwamba mwananchi yeyote ambaye ana tatizo la vitendo vya ukatili dhidi ya watoto mnaweza mkajaribu hata sasa hivi kupiga namba 116 itapokelewa na taarifa dhidi ya vitendo hivyo inafika katika mahala, vyombo vya Serikali na kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuameanzisha Madawati ya Jinsia na Watoto katika Jeshi la Polisi. Tuna madawati zaidi ya 350 ambayo kazi yake pia ni kutaka kutoa uhuru kwa wanawake na watoto kwenda kutoa taarifa juu ya vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto bila vikwazo vyovyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema suala hili kwa kweli tutaendelea kulifanyia kazi, nikiwa kama Waziri ninahusika na masuala ya haki na ustawi wa mtoto. Kwa kweli kuna ongezeko kubwa la vitendo vya ukatili dhidi ya watoto, ubakaji na ulawiti umeendelea kuongezeka katika jitihada zetu. Kwa hiyo, tuanze sisi ndani ya familia, kwa sababu vitendo hivi vinatokea pia katika familia husika, watu wa karibu ndiyo wanajihusisha kwa kiasi kikubwa na vitendo hivi vya ukatili dhidi ya watoto.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nilikuwa naangalia kwenye haya majibu ya Serikali naona wametenga pesa kwa ajili ya ujenzi wa hospitali, lakini pamoja na vituo vya afya, lakini kwenye majibu haya sijaona pesa ambayo imetengwa kwa mwaka 2019/2020 kwa ajili ya maboma ambayo yako mengi sana sehemu mbalimbali ambayo wananchi wamejitolea nguvu zao kwa ajili ya kukamilisha maboma hayo hasa ya zahanati, ujenzi wa zahanati.

Mheshimiwa Spika, sijui Serikali ina mpango gani wa kusaidia kukamilisha ujenzi wa maboma mbalimbali ambayo yamo katika sehemu mbalimbali za majimbo yetu? Swali la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Tabora Manispaa jengo la Halmashauri limechakaa sana mpaka linavuja, sehemu nyingi zinavuja, lakini Halmashauri kwa mapato yake ya ndani imejitahidi kuligharamia jengo hilo na imelipa mpaka sasa hivi zaidi ya shilingi bilioni 1.5 kwa mapato ya ndani na toka ujenzi umeanza mwaka 2014 Serikali imewahi kutoa shilingi milioni 450 tu katika kusaidia ujenzi wa jengo hilo. Sasa sijui Serikali ina mkakati gani wa kusaidia ujenzi wa jengo hilo ambalo ujenzi wake unafikia shilingi bilioni tano ambayo kwa mapato ya Halmashauri kama ya Tabora Mjini si rahisi kukamilisha, Serikali ina mkakati gani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, katika swali lake la mwanzo anauliza haoni fedha ambazo Serikali imetenga kwa ajili ya kumalizia maboma ambayo wananchi wametumia nguvu katika kuyajenga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, msingi wa majibu katika majibu yangu ya msingi yametokana na swali alilouliza Mheshimiwa Mbunge kwa sababu katika swali lake la msingi ni kama vile hakuona jitihada ambazo zinafanywa na Serikali katika kuhakikisha ujenzi wa vituo vya afya, hospitali pamoja na zahanati na ndiyo maana katika majibu ambayo nimempa nimeonesha idadi ya fedha ambazo zimetolewa na Serikali na nia njema ya Serikali ambayo inaongozwa na CCM na sisi katika Ilani yetu tumeahidi pale ambapo wananchi wanatoa nguvu yao na Serikali tunapeleka mkono kusaidiana na wananchi ili kuhakikisha nguvu ya wananchi haipotei na yeye mwenyewe Mheshimiwa Mbunge ni shuhuda nguvu kubwa ambayo inapelekwa na Serikali kuhakikisha kwamba tunaboresha huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini katika swali lake la pili kuhusiana na ujenzi pale Manispaa ya Tabora ambao unatakiwa ugharimu kama kiasi cha bilioni tano ni ukweli jengo limeanzishwa ni kubwa kweli kweli na katika hali ya kawaida kwa bajeti ya Serikali inavyotengwa si rahisi kwamba jengo hili litakamilika lote kwa mara moja na ndiyo maana tumekuwa tukiwashauri ni vizuri tukaanza upande ambao tunaweza tukaukamilisha ukaanza kutumika wakati ujenzi mwingine unaendelea kwa kadri bajeti itakavyokuwa inaruhusu. (Makofi)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nichukue nafasi hii kuipongeza Wizara ya Afya kwa kazi nzuri chini ya Mheshimiwa Dkt. Gwajima, lakini hivi karibuni Mheshimiwa Dkt. Mollel alifanya kazi nzuri pale Mount Meru Hospitali kwa ajili ya kurudisha zile fedha ambazo alitozwa yule mama ambaye alikuwa ametoka kujifungua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; Hospitali ya Kitete Tabora bado inatoza fedha kwa akinamama ambao wamejifungua normal delivery na ushahidi upo. Je, msimamo wa Serikali ukoje ukizingatia katazo ambalo alilitoa Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli akiwa Songwe na hiyo Sera ya Afya ambayo ametoka kuitamka Mheshimiwa Naibu Waziri? Nini msimamo wa Serikali kuhusu kuendelea kutozwa akina mama hao?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; akinamama ambao wanashindwa kutoa hizo fedha ambazo zinaanzia Sh.30,000/= mpaka Sh.50,000/= katika normal delivery, huwa wanazuiliwa pale Hospitali ya Kitete Tabora Manispaa. Je, Serikali ina msimamo gani kuhusu wale akinamama ambao bado wanazuiliwa na watoto wao wachanga, hakuna kutoka mpaka watoe fedha hizo ambazo ni za kujifungulia? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wake huo mzuri kwa ukaribu kwenye eneo hili la Huduma ya Mama na Mtoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, msimamo wa Serikali bado ni ule ule wa kisera na miongozo na maelekezo ya Serikali, kama ambavyo nilishasema kwamba Waganga Wakuu wa Mikoa na Waganga Wakuu wa Wilaya wahakikishe wanasimamia utekelezaji wa sera hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini msimamo wa Serikali? Ukienda kwenye hospitali ambayo Mheshimiwa Mbunge anasema, mapato yao kwa mwezi huu wa Januari, 2021 ni shilingi milioni 73; mapato kutokana na Bima ni shilingi milioni 133, lakini Serikali imepeleka OC ya shilingi milioni 54 kwa mwezi wa Januari, 2021. Maana yake mapato yao kwa mwezi ni shilingi milioni 260. Ukitoa na matumizi ya akinamama na watoto, hizi za kutoa bure, ni milioni 13 point, ndiyo matumizi yao kwa mwezi Januari, 2021. Maana yake ukitoa matumizi mengineyo ni shilingi milioni 134, ukija ukijumlisha, wanabakia kuingia mwezi huu wa Februari, 2021 na shilingi milioni 120. Kwa maana nyingine hakukuwa na sababu yoyote ya kum-charge mama na watoto pesa yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ikipeleka OC ya shilingi milioni 54 kwenye hospitali hiyo kila mwezi, maana yake imeshawalipia hawa akinamama. Ukiondoa shilingi milioni 13 ina maana imebaki fedha nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaondoka pamoja na Mheshimiwa Mbunge kwenda Kitete, tukae site pamoja tupige hesabu na tuone. Tutakubaliana pamoja, tutakuja na way forward. (Makofi)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali; kwa kuwa tulishawahi kupata mafanikio katika kuunganisha baadhi ya shughuli za taasisi fulani kwa mfano tuliunganisha TRL pamoja na RAHCO, lakini pia kwa ufanisi kabisa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii imeweza kuunganishwa.

Je, Serikali haioni sasa kwamba imefika mahali kwamba tulete mabadiliko ya sheria ambayo tutaunganisha sasa TARURA pamoja na TANROADS ili waweze kufanya kazi pamoja tuweze kuondoa hii kero ambayo hii kila siku kunakuwa na mapungufu ya fedha?

Mheshimiwa Spika, Tabora Mjini ina kata 29 na vijiji visivyopungua 41, imeathirika sana pembezoni Kata za Tambuka Reli, Ntarikwa, Uyui, Ifucha na kata nyingi za pembezoni.

Je, Serikali haioni sasa kwamba ni muda muafaka pamoja na kwamba imetenga bajeti ya nyongeza kuweza kufanya haraka kutengeneza zile barabara kwa sababu nyingine hazipitiki? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kwanza niseme dhumuni la Serikali kuanzisha Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini ilikuwa ni kuiwezesha Mamlaka hii kuwa karibu zaidi na wananchi na barabara za vijijini na mijini ili tathmini ya kina na ya haraka iweze kufanyika na kuhakikisha kwamba barabara hizi zinajengwa mapema iwezekanavyo kuliko ilivyokuwa inasimamiwa na TANROADS kutokana na ukubwa wa nchi na majukumu ambayo TANROADS ilikuwa nayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba TARURA inafanya kazi yake vizuri na kwa kushikirina kwa karibu sana na TANROADS tunaendelea kuhakikisha barabara zetu za mijini na vijijini zinapitika vizuri na changamoto ya fedha haitakuwa na suluhu kama tutaunganisha TANROADS na TARURA kwa sababu Serikali ni moja na vyanzo ni vilevile. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kuhakikisha kwamba TARURA inafanya kazi ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, pili, kuhusiana na suala la barabara za Tabora Mjini; ni kweli nchini kote tumepata changamoto ya uharibifu wa barabara nyingi na nimhakikishie kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, tayari fedha zimetengwa zaidi ya mara moja na nusu ya fedha za mwaka wa fedha uliopita ili kuhakikisha kwamba fedha zile zinatumika kurekebisha miuondombinu mingi ya barabara na katika Jimbo la Tabora Mjini barabara Mama Onyango, Kilimbika, Jobodo, Mkoani, Lubatuka, Manolelo, Inala, Shule ya Msingi Jamhuri na nyingine tayari kazi za mrekebisho zinaendelea na nimhakikishie zitaendelea kufanyiwa marekebisho, ahsante sana. (Makofi)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali; kwa kuwa tulishawahi kupata mafanikio katika kuunganisha baadhi ya shughuli za taasisi fulani kwa mfano tuliunganisha TRL pamoja na RAHCO, lakini pia kwa ufanisi kabisa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii imeweza kuunganishwa.

Je, Serikali haioni sasa kwamba imefika mahali kwamba tulete mabadiliko ya sheria ambayo tutaunganisha sasa TARURA pamoja na TANROADS ili waweze kufanya kazi pamoja tuweze kuondoa hii kero ambayo hii kila siku kunakuwa na mapungufu ya fedha?

Mheshimiwa Spika, Tabora Mjini ina kata 29 na vijiji visivyopungua 41, imeathirika sana pembezoni Kata za Tambuka Reli, Ntarikwa, Uyui, Ifucha na kata nyingi za pembezoni.

Je, Serikali haioni sasa kwamba ni muda muafaka pamoja na kwamba imetenga bajeti ya nyongeza kuweza kufanya haraka kutengeneza zile barabara kwa sababu nyingine hazipitiki? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kwanza niseme dhumuni la Serikali kuanzisha Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini ilikuwa ni kuiwezesha Mamlaka hii kuwa karibu zaidi na wananchi na barabara za vijijini na mijini ili tathmini ya kina na ya haraka iweze kufanyika na kuhakikisha kwamba barabara hizi zinajengwa mapema iwezekanavyo kuliko ilivyokuwa inasimamiwa na TANROADS kutokana na ukubwa wa nchi na majukumu ambayo TANROADS ilikuwa nayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba TARURA inafanya kazi yake vizuri na kwa kushikirina kwa karibu sana na TANROADS tunaendelea kuhakikisha barabara zetu za mijini na vijijini zinapitika vizuri na changamoto ya fedha haitakuwa na suluhu kama tutaunganisha TANROADS na TARURA kwa sababu Serikali ni moja na vyanzo ni vilevile. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kuhakikisha kwamba TARURA inafanya kazi ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, pili, kuhusiana na suala la barabara za Tabora Mjini; ni kweli nchini kote tumepata changamoto ya uharibifu wa barabara nyingi na nimhakikishie kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, tayari fedha zimetengwa zaidi ya mara moja na nusu ya fedha za mwaka wa fedha uliopita ili kuhakikisha kwamba fedha zile zinatumika kurekebisha miuondombinu mingi ya barabara na katika Jimbo la Tabora Mjini barabara Mama Onyango, Kilimbika, Jobodo, Mkoani, Lubatuka, Manolelo, Inala, Shule ya Msingi Jamhuri na nyingine tayari kazi za mrekebisho zinaendelea na nimhakikishie zitaendelea kufanyiwa marekebisho, ahsante sana. (Makofi)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Jimbo la Tabora Mjini lina kata 29 na
vijiji 41, na katika vijiji hivyo vingi havina mawasiliano ya simu na vijiji vingine vipo karibu kabisa, kilomita mbili tu kutoka mjini lakini bado ni vigumu kupata mawasiliano; mathalani kata ya Itetemya. Ninaomba kuuliza;

Je, ni lini Serikali itatufanyia mpango wa kuongeza angalau minara ili mawasiliano yaweze kuwa mazuri? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA
HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakasaka kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya mawasiliano ni takriban nchi nzima ina changamoto mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto ambazo zinatokana na teknolojia iliyowekwa katika eneo husika, lakini pia mnara uliowekwa pale inategemea kwamba uliwekwa katika wakati upi, kwamba iawezekana kulikuwa na population ya watu wachache na sasa wameongezeka sasa mnara unaweza ukazidiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunafahamu kabisa kwamba kuna maeneo ambayo kutokana na sababu za kijiografia unakuta kwamba katika kata moja mawasiliano yapo katika vijiji sita lakini Kijiji kimoja kinakuwa kinakosa mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali kupitia Wizara yetu imeanza kufanya utafiti wa kujiridhisha ili tuweze kupata teknolojia ambayo tutakuwa tunafikisha huduma ya mawasiliano katika zile sports ambapo unakuta kwamba ni Kijiji kimoja tu ambacho kimekosa mawasiliano lakini tufikishe kwa teknolojia ambayo ni nafuu na yenye gharama nafuu. Waheshimiwa Wabunge pia tuweze kusaidiana kuhakikisha kwamba tunawaelewesha wananchi wetu kujua kwamba mawasiliano yatafika kwasababu bahati nzuri mmetusaidia kupitisha bajeti ambayo itatufikishia mawasiliano katika vijiji vyetu.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Wizi wa kimtandao unaongezeka kila kukicha; kwa kuwa TCRA kwa maana ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania wana uwezo wa kujua namba fulani inayofanya wizi ipo mahali fulani: Je, kwa nini Serikali sasa haioni kwamba uwepo utaratibu maalumu wa Jeshi la Polisi pamoja na TCRA kuzuia watu kabla hawajaibiwa kwa sababu wana uwezo wa ku-trace hiyo namba? Hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, pale namba inapotumika ambapo namba ile siyo ya kawaida kwa mfano hizi namba zinazoanzia 15000 na kuendelea ndiyo namba ambazo ni za mitandao yenyewe, unakuta zinatuma ujumbe kwa mfano umeshinda labda shilingi milioni 600, umeshinda shilingi milioni sita, umeshinda kiasi kadhaa; anatuma mtu anaendelea kukatwa fedha zake. Sasa nauliza je, pale mwananchi ambapo anakuwa hana kosa na kosa ni la hawa wenye mitandao wenyewe kwa mfano TiGO au Vodacom, kuna mkakati gani wa Serikali ili wananchi ambao hawakufanya makosa yoyote waweze kubanwa hizi kampuni za simu kulipa fedha zao? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba nimpongeze Mheshimiwa Emmanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kwa kazi kubwa anayoifanya kwa maslahi ya wananchi wa Jimbo lake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, naomba niwashukuru na kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge wote kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wakiifanya kwa kushiriki katika michakato mbalimbali ya kuishauri Serikali ili tuweze kuboresha huduma kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo ambalo Mheshimiwa Mwakasaka ameliongelea ni kwamba Serikali inamkakati gani wa kujaribu kuzuia wizi kabla hata haujatokea? Sheria ya makosa ya Kimatandao ya Mwaka 2015 ambayo ilianzishwa mahususi kwanza kutambua makosa yenyewe ya kimtandao ni yapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kikubwa ni kwamba kupitia Kamati ambayo imeshaundwa, kwa nafasi hiyo, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuisimamia vizuri Kamati hiyo, kazi yake kubwa ni kwenda kutoa elimu kwa Umma. Inapotoa elimu kwa Umma ni pale ambapo sasa Mtanzania anajua kabisa kwamba ni kosa lipi ambalo linahusika na sheria hii na kulihalalisha kwamba nikilifanya basi hatua za kisheria zitachukuliwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ni kujenga uwezo kama ambavyo nimesema kwamba kuna kitengo maalum cha makosa ya kimtandao, ambayo ni Cybercrime Unit ambayo inashughulika na makosa haya. Lakini kuwajengea uwezo na kuleta vitendea kazi ambavyo…

NAIBU SPIKA: Elekea kwenye jibu la pili hilo ameshaelewa Mheshimiwa Mwakasaka. Jibu swali lake la pili. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Swali la pili anaongelea kuhusu message ambazo wanakuwa wanatumiwa. Nalo hili linaangukia katika makosa yale yale ya kimtandao tunasema unsolicited messages. Hili tayari tumeshakaa na watoa huduma tumeshaanza kuweka mkakati wa kuhakikisha kwamba, tunawasaidia na kuelewa kwamba namna gani message hizi hazitakiwi kutumwa kwa watanzania ambao hawajaziomba. Matokeo yake wanakuwa na makosa ambayo hawajahusika moja kwa moja. Ahsante. (Makofi)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Rufaa ya Kitete, kama neno rufaa linavyoonesha, ndio hospitali tegemezi kwa Mkoa wa Tabora. Hospitali ile inahitaji Madaktari Bingwa wasiopungua nane na kama alivyojibu Mheshimiwa Waziri kwamba, kuna Madaktari watatu, ingawa mimi nafahamu kuna Madaktari Bingwa wawili yani kama ilivyo jibu lake la msingi, kwa watoto na akinamama; hatuna Madaktari wa upasuaji, hatuna Madaktari wa mifupa, hata physician hawapo kwa hiyo, hatuna Madaktari wengi na hii ni hospitali ya rufaa. Niseme namshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kutupa shilingi hizo bilioni 10.5 kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya dharura pamoja na majengo ya watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, baada ya Mheshimiwa Rais kutoa fedha zote hizo na majengo tayari yamekamilika, hayana Madaktari Bingwa kwa muda mrefu, Wizara ya Afya hamuoni mnaanza kudidimiza hata juhudi za Mheshimiwa Rais kwa kutoleta madaktari bingwa katika majengo hayo mazuri ambayo yanajengwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa, sehemu zingine kuna Madaktari Bingwa wengi sana, ikiwemo Dar-es-Salaam. Na kwa kuwa, Madaktari wengi hawaendi kwenye mikoa mingine kama Tabora kwa sababu ya vivutio. Je, Wizara imejipangaje kuweka vivutio kwa madaktari hawa bingwa ili waweze kuvutiwa kufanya kazi sehemu kama Tabora Mjini? ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja amesema Madaktari ni wawili sio watatu; mimi ninachoweza kumwambia mpaka mwisho wa mwaka huu maana yake wanaenda kuongezeka Madaktari sita. Wanapoongezeka maana yake watakuwa, tulitegemea wawe tisa, lakini maana yake unasema watakuwa nane, lakini nataka kukuhakikishia watakuwa tisa mpaka tunapofika mwisho wa mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, specifically ametaja baadhi ya magonjwa na matatizo yanayowasumbua zaidi kwenye eneo lao; tayari Waziri wa Afya ameshaelekeza upembuzi yakinifu ufanyike nchi nzima kujua maeneo yenye Madaktari wengi kuliko mahitaji halisi, ili kuweza kuwapeleka katika yale maeneo ya pembezoni ambayo yana uhitaji zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia amezungumzia suala zima la kwamba, la watumishi kwa ujumla kwamba, majengo yanakwenda kwisha na wakati mwingine majengo yanakuwa mazuri, lakini ndani yake hakuna watumishi wa kufanya kazi hiyo; lakini nimwombe Mheshimiwa Mbunge suala la watumishi wa afya kuwa wachache sio suala tu la Tabora peke yake ni suala la nchi nzima na ni tatizo ambalo hata wanapokwenda shuleni kuwa recruited wanakuwa vilevile wachache, kwa hiyo kwenye soko kuwapata aina ya kada unayotaka wakati mwingine ni changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme kwamba tumechukua; na hata wakati fedha hizi shilingi trillion 1.3 ambazo Mheshimiwa Rais wetu ameipa Sekta ya Afya shilingi bilioni 495, alielekeza kwamba wakati ujenzi huu unaendelea, vile vile tukae na TAMISEMI na kwa wakati huo huo tukae na Wizara ya Utumishi kujipanga kuhakikisha majengo yanapoisha na ujenzi huo unapoisha, watumishi wanapatikana wa kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Mwakasaka usiogope jinsi fedha na ikama inavyotoka. Tutahakikisha kila mahali kunakuwepo na watumishi wanaoweza kutoa huduma. Pia tunapunguza hilo tatizo kwa kuhakikisha vilevile madaktari bingwa walioko Dar es Salaam na mikoani wanaweza wakachukua wale wagonjwa wanaotakiwa kupelekwa rufaa Dar es Salaam au kwingine au kuletwa Benjamin, wakawafuata huko huko Kitete na kutibiwa huko huko ili kupunguza wananchi kuja Benjamin au kwenda Dar es Salaam. Ahsante sana.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kumekuwa na mashindano makubwa sana katika bandari za majirani zetu hasa Mombasa, Kenya na Beira, Msumbiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sijui Serikali ina mkakati gani wa kuimarisha bandari yetu ya Dar es Salaam ili iweze kuweza kushindana na Bandari hizo za nchi za jirani?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nimpongeze pia Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa Bandari ya Dar es Salaam ni lango la uchumi wa nchi yetu. Sasa anataka kujua je, tuna mikakati gani ya ushindani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli katika sekta hii ya usafirishaji hususan bandari tuna washindani ambao ni Beira, tuna Durban pamoja na Mombasa. Hivi ninavyosema, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais awali alitoa shilingi bilioni 210 kwa ajili ya kununua vitendea kazi katika ile Bandari ya Dar es Salaam, lakini vifaa vile vilikuwa bado havitoshi na ameongeza shilingi bilioni 290 na kufanya bilioni 500 kwa ajili ya kuongeza ufanisi katika Bandari yetu ya Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo vifaa hivyo kwa kuwa tayari tumeshaagiza na nina hakika kuingia Dar es Salaam tayari, pia tunatengeneza njia za reli kwa ajili ya kwenda kuchukua mzigo na kupeleka katika Bandari hizo ambazo nimezitamka hapo kama Isaka pamoja na nchi jirani za kwenda Zambia. Kwa hiyo tunagemea kwamba ushindani utaimarika zaidi mara tu baada vifaa hivi kuja ili tuwe bora katika nchi zetu za Afrika Mashariki. (Makofi)
MHE. EMMANUEL MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Magereza zetu zimekuwa na tatizo ambalo linatokana na hili swali la msingi kwamba kwa kuwa hawa watu wanakosa faragha, wengine wanafanya vitendo wenyewe kwa wenyewe mle magerezani. Je, Serikali ili kupunguza hivyo vitendo vya watu kugeuzana wenyewe kwa wenyewe magerezani, inachukua hatua gani kupunguza vitendo hivyo ambavyo vinasababisha kuwa kinyume hata na mila na desturi zetu?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuna njia nyingi ambazo Serikali inachukua, la kwanza ni kuhakikisha tunaimarisha ulinzi katika magereza na kuimarisha ulinzi kuna njia nyingi vilevile, tuna mifumo ya ki-intelligence kupata taarifa kabla matukio hayajajitokeza. Pia kuna utaratibu ambao kuna askari waliopo katika magereza kuangalia mienendo na mazingira ya wafungwa katika magereza na tabia zao vilevile.

Mheshimiwa Spika, kubwa zaidi ni kwamba kupitia Serikali ya Awamu ya Sita, kuna mikakati kabambe ya kufanya maboresho makubwa katika vyombo vyetu vya usalama. Moja ni kuhakikisha tunaimarisha na kuboresha miundombinu ya magereza ili kutenganisha kati ya wafungwa kwa mfano, kutenganisha wafungwa wenye umri fulani mpaka umri fulani, wenye historia ama rekodi ya uharifu zaidi kuliko wengine na mambo mengine, ili kutoa nafasi kwa kuweza kupeleka nguvu zaidi ya uangalizi katika maeneo ambayo yanastahili kulingana na uzito na changamoto ya mfungwa husika.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, wafanyabiashara wengi hawa ambao walikuwa wanategemea kuuza nyamapori walishajenga mabucha kwa ajili ya kuuza nyamapori, kama ambavyo Serikali ilikuwa imewahamasisha. Mpaka sasa hivi vibali havijatolewa kwa muda mrefu na hasa kwa hawa wawindaji wa kawaida ambao wanalipa na leseni. Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba hawa wafanyabiashara wa nyama ya pori wanapata hivyo vibali ili waweze kufungua mabucha yale ambayo walishayajenga?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; hata pale nyama hiyo inapokuwa imepatikana kwa hao wachache ambao wanauza, bei yake inakuwa ni ghali sana, na wananchi wengi wa kawaida wangependa kula hii nyama ya porini. Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka mazingira mzuri kwa ajili ya kufanya hii nyama ya pori nayo iwe na bei ya kawaida ambapo kila mmoja anaweza kununua? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Emmanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba tu niwatoe wasiwasi Watanzania na Mheshimiwa Mbunge kwamba vibali hivi vitatolewa baada ya mapitio ya Kanuni kukamilika. Tulikuwa na changamoto ya namna ya ugawaji wa vibali hivi kwa kuwa tuliweza kuanzisha makampuni ambayo tuliyakaribisha ili yaweze kuomba vibali vya uwindaji wa kienyeji. Lakini tumegundua changamoto inayojitokeza ni namna ambavyo tunaweza kuwanyima haki ya Kikatiba wananchi kuweza kupata kitoweo ambayo iko ndani ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tumepata maoni kutoka kwa wadau na sasa tumepitia Kanuni hizi, tunatarajia sasa kuzirejesha kwa maana tutoe ile haki ya wananchi, nao wawe na haki ya kuweza kupata kitoweo hiki.

Mheshimiwa Spika, kuhusu bei ya nyamapori, suala hili baada ya kuwa tumepitia Kanuni hizi na wananchi kuruhusiwa nao kuwinda uwindaji wa kienyeji, basi tunatarajia bei ya nyamapori kushuka kuliko ilivyo sasa ambapo tulikuwa tumependekeza makampuni pekee yaweze kuingia katika biashara hii. Ahsante.(Makofi)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kata ya Mbugani katika Jimbo la Tabora Mjini ina uhitaji mkubwa sana wa zahanati. Sijui Serikali ina mpango gani wa kuisaidia Kata hiyo ya Mbugani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata hii ya Mbugani ambayo ina uhitaji wa zahanati, nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora, kufanya tathmini kujiridhisha na vigezo vya kujenga zahanati ya kimkakati na baada ya hapo kuona mapato ya ndani, na pia kuleta maombi Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili kwa kutumia mapato ya ndani na Serikali kuu tuone uwezekano wa kutekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tabora ya Kitete bado ina upungufu mkubwa wa dawa, je, Serikali imejipangaje kuhakikisha inapunguza tatizo hilo la upungufu wa dawa katika Hospitali ya Kitete?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwa sababu kwa asilimia na kwa rekodi ambazo zimetoka MSD kwa sasa upatikanaji wa dawa ni asilimia 78 maana yake tuna upungufu wa asilimia 22. Moja ya namna ya kufanya ni kuchukua mapato ya ndani ambayo Hospitali ya Kitete inapata itumie kununua dawa palepale Tabora kama hazitakuwepo pale MSD.
MHE. EMMANUEL E. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Tabora Mjini wananchi kwa nguvu zao wamejitahidi sana kujenga vituo vya afya ambavyo vingi viko kwenye maboma lakini wengine wamekusanya mawe na kujitolea nguvu zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango gani wa kusaidia kumalizika kwa hivi vituo vya afya ambavyo wananchi wamejitoa nguvu zao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Serikali inatambua maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Tabora Mjini wananchi wameshiriki kwa nguvu zao kuchangia ujenzi wa vituo vya afya na maboma yako mengi karibu kila Mbunge hapa anaweza kuyaainisha. Kwa hiyo, wakati wa sasa ukiwa ni mpango wa kuhakikisha kwamba Halmashauri zote zinapata hospitali za Wilaya, ambapo tulikuwa na Halmashauri 28 hazikuwa na hospitali za Halmashauri ambapo mwaka huu wa fedha Serikali imepeleka fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa pili ilikuwa ni kumaliza Tarafa zote nchini, tulikuwa na Tarafa 570, karibu Tarafa 233 zilikuwa hazina ambapo Serikali tumepeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa maeneo hayo. Kwa hiyo, mpango wa tatu utakuwa sasa ni kwenda kumalizia katika yale maeneo ambayo wananchi wameweka nguvu zao. Kwa hiyo, haya masuala ni yanakwenda kwa mipango na kwa muda kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inalitambua hilo na tutatenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunapeleka fedha ku-support wananchi nguvu zao walizozitoa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa na mimi nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Tabora Mjini lenye kata 29 ambalo ni kubwa sana kata nyingi za nje ambazo ni za vijijini zina upungufu mkubwa wa vituo vya afya, hasa katika Kata ya Uyui ambayo ina zahanati ambayo ingeweza Serikali ikaiboresha kuiweka kuwa kituo cha afya.

Je, Serikali inaahidi nini katika jambo hilo la kuzisaidia hizo kata za nje ya Mji wa Tabora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka Mbunge wa Tabora Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika Manispaa ya Tabora kama ilivyo katika halmashauri zote kote nchini kuna upungufu wa vituo vya afya kwa baadhi ya kata. Dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kwanza tunakamilisha ukamilishaji wa vituo vya afya vilivyoanza ujenzi na kupeleka vifaa vifaa tiba na watumishi ili vianze kutoa huduma za afya. Baada ya hapo tutafanya tathmini ya maeneo ambayo ni kimkakati kwa ajili ya kujenga vituo vya afya vingine ikiwemo katika eneo hili la Uyui.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, assante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wetu wa Tabora na hasa Tabora Manispaa, bado wagonjwa wengi wa rufaa wanakwenda Bugando kwa sababu ya kuwa na upungufu mkubwa wa Madaktari Bingwa katika hospitali yetu ya rufaa ya Kitete, sijui Serikali ina mpango gani wa kutuletea Madaktari Bingwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetangulia kujibu swali la Mheshimiwa Rwamlaza, mkakati wa Serikali ni kuhakikisha hospitali zetu za Rufaa za Mikoa zinakuwa na Madaktari Bingwa. Kwa hivyo, nimhakikishiwa Mheshimiwa Mbunge kwamba Hospitali ya Mkoa wa Tabora nayo ni kipaumbele na tutahakikisha tunapata wataalam hao kwa ajili ya huduma katika hospitali ile.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kiwanda cha Nyuzi pia Tabora kina matatizo kama ambayo yapo kule Ukonga. Wafanyakazi waliachishwa muda mrefu lakini wengi hawakupata mafao yao. Nilikuomba Mheshimiwa Waziri kama utakuwa tayari tuambatane ukawa umeniahuidi lakini mpaka leo naona bado sijui lini utakuwa tayari ili ukawasikilize wale wafanyakazi, kwa kweli hali zao ni mbaya sana, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru. Naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakasaka ambaye kimsingi ameeleza pia hali ya changamoto zilizo katika viwanda vilivyokuwa kama Kilitex pamoja na Sunguratex, hali hiyo ipo pia kwenye Kiwanda cha Nyuzi kule Tabora. Mimi nipo tayari kuweza kushirikiana naye hata kuambatana nae ili kuweza kutatua changamoto hiyo lakini katika hatua ya awali pia tutapata nyaraka na idadi ya majina hayo ili tuweze kuona urahisi zaidi wa kuwahudumia wananchi wetu, ahsante. (Makofi)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Katika kata 29 zilizopo katika Jimbo la Tabora Mjini kuna upungufu mkubwa kwenye vituo vya Polisi vilivyoko kata za nje. Kata ya Kazima haina kabisa Kituo cha Polisi na uhalifu mwingi unafanyika maeneo yale katika Jimbo la Tabora Mjini: Ni lini Serikali itaweza kuweka mkakati wa kujenga Kituo cha Polisi katika kata hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge Mwakasaka kwa dhamira yake ya kujenga vituo vya Polisi kwenye maeneo ya Tabora. Unajua Tabora wakati fulani ilikuwa na wimbi kubwa sana la uhalifu, hapo katikati wakapoa sana, tukaamini pamekuwa eneo lenye utulivu. Sasa kama wameanza matukioya uhalifu, namwomba Mheshimiwa Mbunge, kupitia Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Tabora, waangalie maeneo yanayoweza kuwekwa vituo vya kimkakati kama Kazima, basi wayaingize kwenye mpango wao ili Serikali Kuu kupitia Jeshi la Polisi iweze kuwasaidia kukamilisha vituo hivyo. Wakifanya hivyo, tutawaunga mkono, nashukuru sana.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa suala hili la kugawa Mkoa wa Tabora na kuwa na Mkoa unaitwa Manonga ni la muda mrefu sasa na michakato mingi ilishafanywa ikiwemo jina lenyewe la Manonga. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, Je, hicho kikao cha tarehe 22 kama alivyosema Mheshimiwa Waziri cha RCC kikifanyika, Serikali iko tayari kuugawa Mkoa huu wa Tabora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imetoa maelekezo na sheria kwamba lazima taratibu hizo zifuatwe na kisha maombi hayo yawasilishwe rasmi Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili iweze kuwasilishwa kwenye mamlaka husika baada ya tathmini. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge baada ya wao kuwasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ofisi itafanya tathmini na kuwasilisha mamlaka husika ili maamuzi yaweze kufanyika kwa kadri itakavyoona inafaa, ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Uyui ambayo ndiyo kata kubwa kuliko kata zote katika Jimbo la Tabora Mjini haina kabisa kituo cha afya na tulikwishaomba muda mrefu ili iweze kupata kituo cha afya.

Je, ni lini Serikali itatupatia kituo cha afya katika Kata hiyo ya Uyui?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kata zote ambazo zina vigezo vya kujengewa vituo vya afya zitaingia kwa awamu baada ya kukamilisha vituo vya afya ambavyo vinaendelea kujengwa. Serikali imekwishatoa maelekezo kwa Halmashauri zenye mapato ya ndani yanayozidi bilioni tano, kuanza ujenzi wa vituo hivyo kwa kutumia ile asilimia 60 na asilimia 70 ya mapato ya ndani. Kwa hiyo, nitoe maelekezo pia kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Tabora kuanza kutenga fedha kwa awamu, wakati Serikali pia inatafuta fedha kwa ajili ya kupandisha hadhi lakini pia kujenga kituo cha afya katika kata hii, ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, mwaka jana Bunge la Bajeti kama hili niliuliza swali kama hili hili na Mheshimiwa Naibu Waziri Dkt. Mollel mwenyewe aliniahidi mwaka jana kwamba ifikapo mwezi Novemba, mwaka jana wangekuwa wametuletea Madaktari Bingwa pale Kitete kwa sababu kuna upungufu wa Madaktari Bingwa wasiopungua 11.

Je, ahadi hiyo wale wananchi wa Tabora Mjini na especially kwa hiyo Hospitali yetu ya Kitete lini watapelekewa hao Madaktari Bingwa ambao niliahidiwa mwaka jana?

Swali la pili, hospitali ya Kitete ambayo ndiyo Hospitali yetu ya Rufaa ina upungufu mkubwa wa vifaa kwa ajili ya kuwahudumia wagonjwa zikiwemo oxygen cylinders kwa wale wenye mahitaji maalum ya kupumua na vitu vinavyofanana na hilo.

Je, ni lini Serikali itatusaidia vifaa hivyo katika Hospitali yetu ya Rufaa ya Kitete? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mheshimiwa Mbunge aliuliza swali kama hili na Mheshimiwa Waziri wa Afya alielekeza kwamba wakati tunasomesha hawa, Madaktari wengine watafute sehemu zingine ili wapelekwe na ilishafanyika upembuzi yakinifu na wamepatikana Madaktari wa kusambazwa siyo tu Kitete ni maeneo mengi ya nchi ambayo kuna tatizo kama hili la Tabora.

Mheshimiwa Spika, sasa tupo kwenye stage ya kutafuta fedha kwa ajili ya uhamisho ili waweze kupelekwa kwenye maeneo yale, kwa kweli tumefikia karibia hatua za mwisho ili jambo hili liweze kutekelezwa ambalo ulitaka lifanyike.

Mheshimiwa Spika, swali lako la pili, kwanza ninakupongeza wewe na Wabunge wa Tabora kwa sababu mmepigana, lakini Rais wetu kwa mwaka huu kwa miaka yake hii miwili zimepelekwa Bilioni 13 kwenye hospitali yenu ya Mkoa. Maana yake unapozungumzia oxygen, kimejengwa kiwanda cha kuzalisha oxygen chenye thamani ya milioni 800 na sasa imeshawekwa miundombinu yote jengo limejengwa, kiwanda kimejengwa na imebaki tu filling pump ambayo mpaka tarehe 25 itakuwa imekamilika ili oxygen iweze kupatikana kwa ajili ya watu wetu wa Kitete.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, mwaka jana mwezi Aprili ilikuwa, wakati tuko kwenye Bunge la Bajeti kama hivi, niliuliza the same question na Mheshimiwa Dkt. Godwin Oloyce Mollel bahati nzuri naye ndiyo bado Naibu Waziri wa Afya, walinijibu mpaka mwezi wa Kumi na Moja ule upungufu wa Madaktari Bingwa 11 ambao ulikuwepo mwaka jana hospitali ya Kitete na mpaka sasa hivi bado upo, kwamba wangeweza kuwa wameweza kutupunguzia mpaka mwezi wa Novemba, 2022 bado mpaka sasa hivi.
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, ninamshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu mazuri na nimshukuru sana Mheshimiwa Mwakasaka kwa swali lake kuhusu ni lini Serikali itapeleka Madaktari Bingwa katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Kitete.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana tulipata kibali cha ajira cha kuajiri Madaktari Bingwa lakini hatukuwapata sokoni, kwa hiyo mkakati tunautumia Serikali ni kama alivyoeleza Naibu Waziri ni wale ambao tayari ni Madaktari katika hospitali husika tunawapeleka kuwasomesha, na bahati mbaya hawajamaliza kusoma. Hatua ya haraka ambayo tumeifanya Mheshimiwa Mwakasaka, tumefanya tathmini ya Madaktari Bingwa tumegundua katika baadhi ya hospitali za Rufaa za Mikoa kuna Madaktari Bingwa wengi kuliko katika baadhi ya hospitali nyingine. Kwa hiyo, tunafanya re-distribution tunawatawanya upya, tumekwama tu kidogo kwenye fedha.

Mheshimiwa Spika, mwaka huu pia tumepata kibali cha ajira, tutaajiri Madaktari Bingwa na pia tutawasambaza katika Hospitali za Rufaa za Mikoa. Changamoto waliomaliza kidogo ni wagumu kuingia sokoni kwa hiyo mkakati tunaoutumia ni kuhamasisha Madaktari katika hospitali zetu za Rufaa za Mikoa wakasomee Udaktari Bingwa halafu wakirudi wabaki pale pale katika hospitali zao.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri ahsante sana kwa majibu yako. Naomba kuelewa wanasomeshwa na Serikali ama wanatiwa moyo ili wakajisomeshe wenyewe kwenye huo utaalam wa ziada.

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, ni swali zuri. Kipekee tunampongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa mara ya kwanza tumeanzisha utaratibu unaitwa Samia Suluhu Super Specialist Program tunasomesha Madaktari Bingwa zaidi ya 400 ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, tumeenda mbali hatuwasomeshi mmoja mmoja tunawasomesha katika utaratibu wa set, kama ni Daktari Bingwa kwa ajili ya upasuaji wa mifupa kwa hiyo anakwenda Daktari Bingwa Upasuaji wa Mifupa, anakwenda Nurse kwa ajili ya ICU - Intensive Care Unit, anakwenda Mtu wa Usingizi na anakwenda Mhudumu. Kwa hiyo, tunasomesha katika ngazi ya set na tunampongeza sana Rais Samia, tunayo bajeti ya kama bilioni nane na wiki ijayo tutakuja Bungeni kuomba tena bajeti Wabunge mtupitishie kwa ajili ya kusomesha Madaktari Bingwa nchini, ahsante sana.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Tabora Mjini lenye kata
29 na wakazi sasa katika sensa hii nadhani hawatapungua 500,000 kwenye jimbo moja, na tulishawasilisha maombi ya kuligawa jimbo hilo kwa muda mrefu: -

Lini Serikali itaweza kuligawa jimbo hilo ili liweze kuwa na majimbo angalau mawili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE NA
URATIBU): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, tunatambua ukubwa pia wa Jimbo la Tabora Mjini. Lakini vilevile niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote na Mheshimiwa Mwakasaka kwamba muda utakapofika, tume tayari tumeanza maandalizi ya uchaguzi wa mwaka 2025, tutashirikiana kwa ukaribu kuona namna ambavyo tunaweza tukagawa majimbo hayo kwa mujibu wa vigezo na masharti. Na niwaambie kwamba tutazingatia pia suala la idadi ya watu, hususan iliyotokana na Sensa yetu ya Watu na Makazi, itaendelea pia kutuongoza kwenye kipengele hicho namna ambavyo tunaweza kufanya, ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii nami niulize swali la nyongeza. Pamoja na kwamba Mji wa Tabora unaitwa Toronto kwa sababu ya ubora wake, lakini kuna kata nyingi ambazo zina shida pale mjini kwenye barabara, hasa Kata ya Ng’ambo, Kata ya Isevya, Kata ya Kitete, na kata nyingine; je, Serikali lini ita…
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Barabara kadri upatikanaji wa fedha hizo katika Kata za N’gambo, Isevya na Kitete katika Manispaa ya Tabora Mjini.

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa takwimu za Bohari ya Madawa, sasa hivi upatikanaji wa dawa ni asilimia zaidi ya 80, lakini ukienda kwenye uhalisia, hicho kitu ni tofauti kabisa. Kumekuwa na shida kubwa ya dawa sijui tatizo ni nini? Hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili ni kwamba, sasa kumekuwa na tatizo sugu kabisa kwenye hospitali zetu nyingi; wagonjwa kila wanapokuwa wameandikiwa dawa nyingi huwa wanaambiwa wakanunue kwenye maduka ya watu binafsi: Je, Serikali ina mpango gani wakutatua tatizo hili la wagonjwa kila mala kuandikiwa kwenda kununua dawa katika maduka ya watu binafsi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza amesema kwenye takwimu za Bohari ya Dawa upatikanaji wa dawa ni asilimia 80, lakini ukienda kwenye uhalisia unakuta kuna jambo tofauti. Labda nimwambie Mheshimiwa Mbunge, ni kweli kwamba ukiangalia kwenye hospitali zetu za Taifa mpaka hospitali zetu za mikoa, upatikanaji wa dawa ni asilimia 97, kwa sababu wanatumia dawa zinazotoka Bohari ya Dawa na pia wanatumia mapato ya ndani kununua dawa wenyewe. Kwa hiyo, asilimia yao ni kubwa kuliko hata ile ambayo ipo Bohari ya Dawa. Pia kwenye hospitali zetu za wilaya, ni kweli kwamba sasa upatikanaji wa dawa kwa sasa ni asilimia 68, maana yake kuna asilimia 32 ya watu ambao bado wanakosa dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge ni shahidi kwamba ukilinganisha mwaka jana 2022 na sasa kuna ongezeko la upatikanaji wa dawa. Kama ambavyo sasa MSD inaenda kupata mtaji kutoka Serikalini ili waweze kununua dawa mapema, sasa hilo tatizo litaisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Mbunge amesema kuna tatizo sugu la wananchi kukosa dawa na wanatakiwa kununua kwenye maduka ya watu binafsi. Hilo hilo linajibu, kwa sababu kama ndani ya hospitali zetu za wilaya na vituo vyetu kwenye hospitali za mikoa kwenda Taifa ni asilimia 97, maana yake kuna upungufu wa asilimia tatu. Ukija kwenye hospitali zetu za wilaya kushuka chini asilimia 32, kwa hiyo, ni lazima watanunua.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumwambia Mheshimiwa Mbunge, kwa mkakati ambao umewekwa hapa na Serikali kwa maana ya kutoa mtaji MSD, tutaenda kutatua hilo tatizo kama ambavyo anategemea litatuliwe. (Makofi)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na malalamiko miongoni mwa baadhi ya vijana kwamba hizi programu za mendeleo kwa vijana na hasa zile za kwenda nje zinavyotolewa kunakuwa na upendeleo. Sijui Serikali inasemaje kuhusu tatizo hilo ambalo linalalamikiwa sana? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nakuhakikishia kwamba Serikali hii haina upendeleo kabisa. Serikali ya Awamu ya Sita imeweka wazi vigezo vya vijana kuweza kupata fursa hizi. Tumekuwa tukizitangaza kwenye vyombo vya habari, tumekuwa pia tukiwaambia Waheshimiwa Wabunge fursa zilizopo. Kuhusu fursa za kwenda nje, tumeingia katika billeteral agreement, na mikataba ya kuhusiana na namna gani vijana wanaweza kupata fursa za ajira tulishaieleza.

Mheshimiwa Spika, wapo Mawakala wa Ajira za nje ya nchi ambao wamesajiliwa chini ya Ofisi ya Kamishna wa Kazi. Pia kupitia TaESA pamoja na SUGECO tumekuwa tukitafuta wahitimu wanaofanya vizuri kwenye vyuo vyote vikuu ikiwemo Chuo cha Kilimo (SUA). Wanafunzi ambao wanafanya vizuri kwenye maeneo mbalimbali wanapata fursa za kwenda kufanya masomo nje ya nchi kwa mfano nchini Israel. Sasa hivi wataenda vijana takriban 600 katika programu hizo.

Mheshimiwa Spika, tunachagua vijana ambao wamefanya vizuri na reccomendation hii inafanywa kwa usaili kwa kupitia Chuo Kikuu chenyewe na kuangalia yale matokeo ya nani amefanya vizuri. Kwa hiyo, hakuna Mtanzania ambaye anazuiwa kufanya vizuri na yeyote anayefanya vizuri anachukuliwa na Serikali kwa ajili ya kwenda kupata masomo hayo nje ikiwa ni sambamba na kupata fursa mbalimbali kulingana na sifa na vigezo ambavyo vimewekwa kwa mujibu wa sheria bila upendeleo, ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nilikuwa na maswali mawili ya nyongeza. La kwanza, kwa kuwa sasa Serikali imekiri kwamba kuna tatizo kubwa la upungufu wa madawa kwenye zahanati;

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapa wazee bima maalum ya afya ambayo inaweza ikawasaidia kupata dawa katika maduka ya watu binafsi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa sasa kuna mmomonyoko wa maadili miongoni mwetu kijamii wazee wakiwa wanaenda hospitali wengi hawawapishi katika zile foleni wanawaacha wazee wanapata shida.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kila hospitali inakuwa na madirisha maalum ya wazee kupata huduma haraka?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake hili muhimu sana kwa ajili ya afya za wazee wetu. Kwanza nianze kwa kumwambia Mheshimiwa Mbunge, moja tuliposema tunakuja na Bima ya Afya kwa Wote, ndilo lilikuwa suluhisho la hili jambo, na unajua kwamba kwenye Muswada wa Bima ya Afya kwa Wote tulikuwa na kipengele cha kuwalipia watu wasio na uwezo, kwamba wanakuwa na bima ya afya, maana yake na kuwa wazee wako sehemu ya hili. Lakini suala la kusema kwamba wapate bima maalum ili wakikosa ndani ya hospitali zetu dawa waweze kupata kwenye maduka binafsi; mimi nafikiri cha msingi hapa ni hospitali zetu, kwa maana ya vituo vya afya, hospitali za wilaya na zahanati zetu ziwe na dawa zote ambazo zinaweza kuwasaidia wazee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mikakati imefanyika; nafikiri Mheshimiwa Mbunge unajua jinsi ambavyo sasa hivi dawa zikifika kuna kamati za vijiji za kupokea dawa, Waheshimiwa Wabunge wanapewa ripoti na kila mtu anashiriki kwenye mchakato huu. Nina hakika hakutakuwepo na upungufu mkubwa na wazee watapata dawa zao.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye miradi mingi ya REA katika baadhi ya vijiji hawa Wakandarasi wamekuwa hawawalipi vibarua na kuna malalamiko mengi. Serikali inachukua hatua gani kuhakikisha hawa Wakandarasi wanawalipa wale vibarua ambao wanafanya kazi hizo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama anavyosema Mheshimiwa Mwakasaka, tumekuwa na changamoto hiyo ya Wakandarasi ama kuchelewa sana au kutolipa kabisa malipo ya vibarua wanaofanya nao kazi. Tumelichukulia hatua kwa kuwa tunawasiliana na wale watumishi wa hao Wakandarasi na kuwashauri wanapokuwa wanaingia katika engagement hizi watengeneze vikundi na wawasiliane na Ofisi zetu za Serikali zilizopo kwenye maeneo husika ili changamoto inapotokea tuibaini mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Mkoa wa Tabora tumeendelea kushughulikia matatizo hayo nasi ofisini tumeshapata watu mara kadhaa ambao wamekuja na tumewapeleka REA pesa yao imeweza kulipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaahidi Waheshimiwa Wabunge kwenye maeneo yetu yote wale wote wanaofanya kazi ujira wao halali utalipwa kwa sababu Serikali inamlipa Mkandarasi na Mkandarasi lazima alipe kwa wale vibarua ambao amefanya nao kazi. (Makofi)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante nami kwa nunipa swali la nyongeza. Kituo cha afya cha Misha katika kata 29 za Tabora kimekamilika lakini bado hakina vifaa vya Afya vya kutosha;

Je, ni lini serikali itapeleka vifaa hivyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakasaka kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya hiki Misha kipo pembezoni mwa Manispaa ya Tabora na tayari katika mwaka wa fedha 2022/2023 ambao tunaenda kuumaliza Serikali ilikuwa imetenga fedha kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba katika kituo hiki cha afya, nitakaa na Mheshimiwa Mwakasaka ili tuweze kupitia hivi na kuona tunapeleka hivi vifaa tiba kwa haraka sana.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa na mimi nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara inayotoka Tabora Mjini kupitia Mwanza Road ambayo inapita Bwawa la Igome mpaka kwenda Mambari - Nzega, ni muda mrefu haina lami na imekuwa ikisuasua: Lini Serikali itajenga barabara hiyo kwa lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli alichosema Mheshimiwa Mbunge wa Tabora. Nataka tu nimjulishe Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii ipo kwenye ilani na tumeitengea fedha kwa ajili ya kuanza maandalizi ya kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Jimbo la Tabora Mjini lenye kata 29 lina matatizo kama hayo, lina shule nyingi sana za msingi ambazo ni kongwe na wananchi wamekuwa wakifanya juhudi ya kuzikarabati kwa juhudi zao wenyewe. Je, ni lini hasa huo mpango utaanza huu wa kuzisaidia kukarabati hizi shule kongwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu umeanza mwezi Aprili mwaka huu na utakamilika mwezi Julai mwaka huu. Mara baada ya kukamilika, tunaanza utekelezaji. Nimhakikishie tu kwamba tuko ndani ya mwaka wa utekelezaji na tutafikia shule zote ikiwemo hizi ambazo yeye ameziainisha. Ahsante sana.

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa, kiwanda cha nyuzi Tabora mpaka kinafungwa wafanyakazi wengi walikuwa hajalipwa mafao yao ya kustaafu. Ni lini Mheshimiwa Waziri upo tayari tuiongozane kwenda kuwasikiliza wale wastaafu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwakasaka kama alivyouliza kuhusiana na wastaafu wa kiwanda hicho cha Tabora, nipo tayari kumpa ushirikiano kuwasikiliza, pia Serikali itatoa fursa hiyo kuweza kuhakikisha kwamba haki zao hazipotei. (Makofi)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Jimbo la Tabora Mjini lenye Kata 29 kuna Kata ya Tumbi pamoja na Kata ya Misha tayari vituo vya afya vimeashaanza kujengwa na vipo katika hali ile ya kumalizia. Ni lini Serikali italeta fedha hizi za kumalizia vituo hivyo vya afya viwili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba kata nyingi bado zinahitaji vituo vya afya, lakini Kata za mkakati tumekwishaziainisha na Waheshimiwa Wabunge, walileta Kata za kipaumbele tatu kila Jimbo, niwahakikishie kwamba Serikali inaendelea kuandaa bajeti kwa ajili ya kuendelea na ukamilishaji wa vituo hivi vya afya, vikiwemo hivi vituo vya afya viwili ambavyo vipo katika Jimbo la Tabora Mjini.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Jimbo la Tabora Mjini lenye Kata 29 kuna Kata ya Tumbi pamoja na Kata ya Misha tayari vituo vya afya vimeashaanza kujengwa na vipo katika hali ile ya kumalizia. Ni lini Serikali italeta fedha hizi za kumalizia vituo hivyo vya afya viwili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba kata nyingi bado zinahitaji vituo vya afya, lakini Kata za mkakati tumekwishaziainisha na Waheshimiwa Wabunge, walileta Kata za kipaumbele tatu kila Jimbo, niwahakikishie kwamba Serikali inaendelea kuandaa bajeti kwa ajili ya kuendelea na ukamilishaji wa vituo hivi vya afya, vikiwemo hivi vituo vya afya viwili ambavyo vipo katika Jimbo la Tabora Mjini.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa wananchi wengi wanapata tatizo na eneo hili la uhakiki kwa ajili ya kupata hivyo Vitambulisho vya Taifa. Sijui Serikali inasemaje kuhusu muda hasa ni muda gani ambao uhakiki unachuku ili wananchi waweze kupata vitambulisho vyao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, uhakiki hautakiwi kuchukua muda mrefu sana, lakini tunafanya uhakiki ili tujiridhishe kwamba wanaopewa vitambulisho hivi ni raia wa Tanzania. Kwa hiyo, itakapotokea taarifa yoyote hasa wananchi wakatia mashaka juu ya mtu aliyetambuliwa inabidi tufanye uhakiki kujiridhisha.

Sasa juu ya muda gani itategemea pale itakapokamilisha, lakini aombe maafisa wetu wasichukue muda mrefu kwa sababu wanapaswa kushirikiana na vyombo vingine vikiwa Kamati za Usalama za Wilaya na Idara za Uhamiaji ili kujiridhisha na kumpa jibu yule ambaye anatafuta kitambulisho. Nashukuru.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nami nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kama ilivyo Wilayani Chemba, Jimbo la Tabora Mjini lenye Kata 29 wananchi maeneo mbalimbali katika kata hizo wamejenga kwa kujitolea zahanati ambazo sehemu nyingi wamefikia kwenye maboma. Sasa je, ni lini Serikali itasaidia hizo juhudi za wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, maboma haya ya zahanati ambayo yamejengwa na wananchi katika Jimbo la Tabora Mjini ni sehemu ya mkakati wa Serikali kuendelea kuyatambua kwa awamu na kuyatengea fedha kwa ajili ya kuyakamilisha. Ni sehemu ya bajeti ya maboma 300 katika mwaka ujao, tunajua hatuwezi kumaliza yote, lakini tutakwenda kwa awamu katika majimbo yote likiwepo Jimbo hili la Tabora Mjini. Ahsante.

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa na mimi nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Skimu ya umwagiliaji ambayo inaendeshwa na umoja wa umwagiliaji katika Kata ya Magoeko katika Jimbo la Tabora Mjini ilitengewa fedha mwaka 2022/2023; fedha hizo sasa zimehamishiwa kwenda wilaya nyingine ya Uyui na Mheshimiwa Waziri nilishakukabidhi malalamiko hayo. Sijui Serikali inasemaje kuhusu wanakijiji hao ambao tayari wameshachanganyikiwa kwa sasa hivi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Mheshimiwa Mbunge amewasilisha jambo hili mezani na kwa sababu amelileta wiki iliyopita tu Alhamisi, naomba anipe muda, tutakaa mimi na yeye pamoja na tume ili tutafute ufumbuzi wa kudumu na mwisho wa siku tuweze kuwahudumia wananchi wote wa Mkoa wa Tabora.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kituo kipya cha Afya ambacho kipo katika Kata ya Misha katika Manispaa ya Tabora Mjini kina upungufu mkubwa wa watumishi lakini pamoja na vifaa. Sijui Serikali inajipangaje kukisaidia kituo kile?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakasaka, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini, kama ifuatavyo. Katika kipindi cha mwaka huu wa fedha 2023/2024, tayari Manispaa ya Tabora imeshapokea zaidi ya shilingi 750,000,000 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba katika vituo vya huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, nimuhakikishie kwamba, katika eneo la vifaatiba, Serikali inaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha vituo vyetu vilivyokamilika lakini na vituo vya zamani vinapata vifaatiba vya kutosha kwa ajili ya kuwahudumia wananchi.

Mheshimiwa Spika, pili, ni kweli kituo ambacho amekitaja kina upungufu wa watumishi lakini kama ilivyo utaratibu wa Serikali, tunaendelea kupeleka watumishi kwa awamu, na tutahakikisha pia kituo kile kinapata watumishi ili waweze kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi, ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa na mimi nafasi ya kuuliza swali la nyongeza: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara nyingi za Tabora mjini zimeharibika, hasa hizi za pembezoni zikiwemo Kata za Ng’ambo, Kidongo Chekundu, pamoja na Kata za Mwinyi na nyingine. Lini Serikali itatoa fedha za ukarabati, hata kwa kukarabati kwa kutumia changarawe na moram?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuondoe hofu na yeye, kwamba bahati nzuri sehemu ya baadhi ya barabara ambazo ameziainisha hapa zimetengewa fedha katika bajeti yetu na zitatekelezwa katika mwaka wa fedha unaokuja. Ahsante sana.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Jimbo la Tabora Mjini lina Hospitali ya Rufaa ya Kitete. Hospitali hii ina upungufu wa Madaktari Bingwa wasiopungua tisa na ni ahadi ya muda mrefu Serikali kutuongezea Madaktari Bingwa. Sijui Serikali itatuletea lini hao Madaktari Bingwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna shida ya Madaktari bingwa; japo wapo, lakini hawatoshi. Niendelee kumwomba Mheshimiwa Mbunge tushirikiane mimi na yeye kwa sababu kuna ambao wako shuleni sasa hivi, tena wengine wanatokea pale Kitete. Vile vile jinsi ambavyo wanamaliza tuendelee kuwapangia na kwa sababu sijaiangalia Kitete specifically, tutaangalia kwenye mgao huu kama kuna kilichofanyika kwenye eneo la Kitete.