Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Emmanuel Adamson Mwakasaka (38 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, jina langu kamili naitwa Emmanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini. Nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hotuba nzuri ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli. Naomba ili kule mbele ya safari nisije nikasahau kuunga hoja, kabla sijaanza kuchangia niseme naunga mkono hoja asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kutoa rai kwanza kwa ndugu zetu kwa Waandishi wa Habari haya wanayofanya ndugu zetu hawa wapinzani nilikuwa naona leo magazeti mengi yameandika kimenuka, na lugha kama hizo naomba waandike pia kwamba hawa wenzetu pamoja na kwamba kimenuka wanaondoka wakiwa wamesaini pesa za walipa kodi ili wananchi waweze kuwaelewa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba pia nisirudie ya wenzangu kwa sababu Mkoa wa Tabora tuna kitu ambacho ni common interest kama Kiwanda cha Tumbaku na wenzangu walishaongelea. Lakini naomba niongelee Kiwanda cha Nyuzi katika hotuba ambayo ni ya Mheshimiwa Rais. Kiwanda kile tulikwenda kukikagua na Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya kama mwezi mmoja umepita, Kiwanda cha Nyuzi Tabora sasa hivi ni godown.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kubinafsishwa tulikwenda ili wakakifungue lakini tukaambiwa mimi na DC kwamba kiwanda kile funguo zake maana yake tuliambiwa kwamba ile mitambo ya mle ndani ilishauzwa kama vyuma chakavu, tukataka tushuhudie lakini tukaambiwa kwamba funguo ziko India. Sasa kwamba mwekezaji kaondoka na funguo kwenda India hili ni jambo ambalo Mheshimiwa Mwijage, Waziri wa Viwanda na Biashara tuna tatizo hilo, kiwanda kile kimfungwa funguo ziko India. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kama Mbunge wa Tabora Mjini niweze kuongelea suala la hospitali yetu ya Mkoa ambayo ndiyo ya Rufaa ya Kitete. Pale kama alivyoainisha Mheshimiwa mmoja aliongelea suala la Kitete, hospitali ya Kitete ina changamoto nyingi na ndiyo hospitali tunayoitegemea kama ya rufaa. Kweli ina tatizo kubwa la wataalam, Madaktari Bingwa pale wanahitajika madaktari kama nane, nilitembelea ile hospitali kama mwezi mmoja pia umepita, niliongea na Mganga Mkuu, kuna Daktari Bingwa mmoja tu katika Madaktari Bingwa nane wanaohitajika katika hospitali. Lakini niliuliza kwani kuna changamoto gani, nikaambiwa suala ni kwamba hawapendi kukaa pale Tabora kwa sababu ya mazingira, nilimuuliza Mganga Mkuu unadhani ni mazingira gani akaniambia hawapendi kukaa Tabora kwa sababu kwanza maslahi ni kidogo, hawawezi pia kupata nafasi za kufanya kazi zile za ziada part time kama wanavyoweza kufanya Madaktari wengine wa Miji mikubwa kama Dar es Salaam, Mwanza, Mbeya na Arusha. Kwa hiyo, ningeomba Wizara iweze kuangalia kwa makusudi ili kuweza kuboresha zile huduma lakini pia kuboresha maslahi ili hao wataalam watakapopatikana waweze kukaa kama hospitali yetu ya Kitete bila kuona kwamba wamesahauliwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna matatizo pia ya Wauguzi wako wachache sana hospitali yetu ya rufaa na wale wachache ambao wanafanya kazi, nichukue nafasi hii kuwapongeza kwamba wanafanya kazi katika mazingira ambayo maslahi siyo mazuri, lakini inapofika suala la muda wao wa ziada manesi wale wanafanya kazi nzuri Madokta lakini muda wao wa ziada amekuwa haupati pesa kutoka Serikalini kwa ajili ya kulipa zile overtime, kwa hiyo, hii inakatisha tamaa, naomba Wizara husika muweze kuliangalia jambo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye suala la maji nitakwenda haraka haraka kwa sababu ya muda, Tabora tuna bwawa la Igombe linatoa maji lakini tuna bwawa pia la Kazima ambalo sasa limejaa tope, lakini bado kuna maji ambayo yanaweza kutosha hata vijiji vya jirani au kata za jirani kama Manoleo, Itonjanda na Ifucha ambazo zinazunguka lile bwawa. Lakini bwawa lile limeachwa tu kiasi ambacho sasa halihudumii zile sehemu ambazo zina matatizo ya maji.
Mimi ningeishauri Serikali kwamba katika kipindi hiki ambacho bado tunasubiri maji ya Ziwa Victoria waweze kuchukua njia angalau kutoa lile tope, maji yale ni mengi kuliko tunajenga bwawa jipya, tuna bwawa jipya linajengwa sehemu za Inara, Kata ya Ndevelwa, bwawa lile hata maji ya safari hii lile bwawa lilikuwa linakamilika lakini sasa linavuja maji hayakai, na limegharimu zaidi ya shilingi bilioni moja na kitu. Lakini Idara yetu ya maji pale TUWASA bili nyingi hazilipwi na hasa na taasisi za Serikali na ile TUWASA pale Tabora ni moja ya taasisi ambazo zinajitegemea hazipata ruzuku yoyote. Ile taasisi inadai zaidi ya shilngi bilioni 1.3 na wadeni wakubwa ni pamoja na taasisi za Serikali lakini pamoja na shule mbalimbali. Kwa hiyo, naomba Wizara ya Maji muweze kuliangalia hili kwamba tunafanyaje, kwa sababu sasa suala la maji limekuwa ni tatizo kubwa Tabora.
Lakini pia naomba niongelee suala la wenzetu hawa askari na hasa polisi kwa kweli hali za askari wetu hasa polisi kwenye kambi zao zile nyumba zao kwa kweli hata ukiziangalia hazilingani na Jeshi la Wananchi, JWTZ sasa hivi ukiangalia nyumba zao angalau zinavutia. Naomba Wizara inayohusika basi tuwakumbuke na ndugu zetu wa polisi kuwawekea mazingira mazuri wanapokaa pamoja na maslahi yao ili kuweza kufanya kazi zao kwa ufanisi.
Mwisho naomba niongelee kuhusu reli, wenzetu walishaongelea. Kuhusu reli kwanza kabla sijaongea kwa sababu sijajua kama nitafika huko mimi nina interest, tumeambiwa tu-declare interest kama unayo kwenye shirika. Mimi nimekuwa ni mfanyabiashara mmoja wa reli, lakini kuna kitu kimoja kinanishangaza kuhusu reli, kila siku ni Godegode. Kila tunaposikia treni haiendi ni Godegode, sasa pale Godegode kuna nini? Kama imewezekana kujenga daraja la Malagalasi kubwa kiasi kile, kila siku kambi ya reli ni Godegode, naomba Wizara husika tuangalie pale Godegode kuna nini, isije ikawa ni mradi…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwakasaka muda wako umekwisha!
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Ahsante naomba kuunga hoja mkono asilimia mia moja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA – MWENYEKITI KAMATI YA BUNGE YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE: Mheshimiwa Spika, kwa mara ya kwanza humu Bungeni kama kuna hoja ambazo sijawahi kuona hazipingwi na Mheshimiwa Mbunge yeyote ni hii ambayo ipo mbele yetu. Wachangiaji walikuwa Waheshimiwa 10 na wote wameunga mkono hoja ya Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchangiaji wa kwanza alikuwa Mheshimiwa Omari Kigua ambaye yeye alizungumza namna Mheshimiwa Josephat Gwajima, ambavyo hakuweza kutoa ushirikiano kwenye Kamati na hata kwenye Taarifa ni kweli Kamati hii nyinyi Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi hata kwa zile clip chache mlizoziona maana yake zingine zilirushwa.

Mheshimiwa Spika, tulijitahidi kuwa waungwana vitendo vilivyokuwa vinafanyika ndani ya ile Kamati, nimeshangaa kidogo wakati Mheshimiwa Shally Raymond alivyosimama nilitegemea angeweza kusema hata jinsi ilivyokuwa siku moja kwenye Kamati Mheshimiwa Askofu Gwajima alivyoharibu hali ya hewa ya mle ndani mpaka Mheshimiwa Shally Raymond akasema kama kungekuwa na uwezekano wa kumrushia mtu ngumi humu, leo ingekuwa hivyo lakini wacha tumvumilie. Tulifanya uvumilivu mkubwa sana. Kwa hiyo, alichozungumza Mheshimiwa Omari Kigua ni kweli kuhusu Mheshimiwa Gwajima na hakuonyesha kujutia chochote.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu Mheshimiwa Jerry Silaa kama alivyosema Mheshimiwa Kigua ni kweli. Yeye alisema amezua tafrani kwa wananchi kuhusu kusema Wabunge hawakatwi kodi. Lakini akasema naomba radhi kwa hilo lakini hakuna mahali ambapo alisema naomba radhi kwa kusema uongo kuhusu Wabunge kutokatwa kodi. Lakini Mheshimiwa Shally Raymond yeye alipoongea Habari ya Mheshimiwa Gwajima aliunga mkono hoja. Lakini alisema kwa nini Mheshimiwa Gwajima hakugusia nchi zingine amegusia tu Tanzania na wakati yeye anajinasibu anawaumini zaidi ya milioni 2,400,000 dunia nzima.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, inaonekana Mheshimiwa Josephat Gwajima yeye aliilenga moja kwa moja Serikali kwa matamshi yake ambavyo yanakwenda. Lakini kwenye hili suala la Mheshimiwa Shally Raymond Waheshimiwa Wabunge si lazima mtu umtaje kwa jina unapomlenga. Wanasheria pia mnafahamu kuna neno linaitwa innuendo ni mahali ambapo unamuelezea mtu lakini humtaji jina lakini yale maelezo unayoyaeleza hata mtoto mdogo mwenye ufahamu atasema huyu unamlenga fulani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Josephat Gwajima yeye alilenga moja kwa moja kwa kutumia neno hilo la kisheria kwa sababu inaonyesha wazi Serikali ndio ilituhamasisha kuchanja na Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan ndio alianza kuchanja na kutuhamasisha. Sasa ukisema wamepewa fedha wanaoshabikia chanjo unasema indirect lakini unailenga Serikali. Kwa hiyo, ni kweli alikuwa anachonganisha na kugonganisha Mihimili.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Tunza Malapo yeye amethibitisha hapa kwamba, Mheshimiwa Gwajima pamoja na kwamba aliuaminisha umma kwamba ninakwenda kwenye hiyo Kamati nitapeleka ushahidi mwingine ambao hata sikuusema hata Kanisani. Lakini Mheshimiwa Tunza Malapo aliposimama hapa ni kweli Mheshimiwa Gwajima hakuwa na ushahidi wowote ambao aliowaaminisha watanzania wote.

Mheshimiwa Spika, na kuhusu suala la Mheshimiwa Jerry Silaa ni kweli hata kwenye kikao alikiri kwamba hata yeye anakatwa kodi kwenye mshahara wake. Sasa tunajiuliza alikuwa na nia gani kuwaambia wananchi jambo ambalo sio la kweli.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Joseph Tadayo aliongelea suala la Mheshimiwa Gwajima kushindwa kuthibitisha suala la Viongozi kupewa fedha ili wachanjwe alishindwa kabisa. Tulipomuuliza unaweza ukatutajia Kiongozi hata mmoja ambaye kapewa fedha? tena alibabaika sana mpaka akafika mahali akasema wanakamati mnakumbuka na Hansard zipo, ile fedha ni misaada. Lakini tukamuambia kwenye kauli zako hakuna mahali uliongelea suala la misaada lakini ulisema Viongozi wanaoshabikia chanjo wamepewa fedha.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu Mheshimiwa Jerry Silaa, Mheshimiwa Tadayo alichangia kwamba Mheshimiwa Jerry Silaa alishindwa kuthibitisha kwamba, Wabunge hawakatwi kodi kwenye mishahara yao.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Ali King aliunga mkono hoja kama wengine na yeye alisema kwamba ili ukitaka umaarufu unatakiwa uende tofauti na wenzio na hapa alisema, uende kinyume na akatoa ile mifano sikumbuki vizuri alisema nini, mchambawima ndio alitolea huo mfano.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hiyo ndio hoja ya Mheshimiwa Ali King hata hapa Bungeni kama kwa mfano mtu akiamua tu kutafuta umaarufu akipanda hapa juu ya meza ataandikwa na vyombo vyote mbalimbali. Lakini atakuwa ametenda kosa ambalo sio la kawaida lakini alikuwa anatafuta umaarufu, hiyo ndio hoja ya Mheshimiwa King.

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Agnes Hokororo aliunga mkono hoja kama wenzie. Aliunga mkono hoja zote mbili, lakini akaongelea Kanuni ya 85 ya Kanuni za Kudumu za Bunge za 2020 ambazo zinaongelea utovu wa nidhamu uliokithiri na akazungumzia kwamba hakuna uhuru usiokuwa na mipaka. Na hili ni kweli Waheshimiwa Wabunge hakuna uhuru ambao ni absolute timilifu kabisa, haupo hata kwenye sheria kila uhuru una mipaka yake.

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, yeye alikwenda zaidi mbali kwa ku-quote vifungu mbalimbali vya Biblia ikiwemo Marko 6, Waefeso 6:12, na akasema hata kwenye Biblia hakuna madhara ya kitu ambacho huamini hata kama utakuwa umepata chanjo, umepata tiba na kitu chochote. Na kwa kuwathibitishia hili wanakamati nadhani mliona kwenye mitandao wakati amekuja Mheshimiwa Josephat Gwajima hata kwenye Kamati kabla hajaitwa, wakati tunamuita alichelewa kidogo. Tukauliza kwa nini anachelewa kuingia wakati tumemuita? Wakasema anaona amezidiwa ghafla kabla ya kuingia kwenye Kamati ameomba akaletewe dawa kwanza anywe. Kwa hiyo, hata Mheshimiwa Josephat Gwajima anakunywa dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchangiaji wa tisa alikuwa Mheshimiwa Mariam Ditopile yeye alinukuu maneno ya Mheshimiwa Rais kuhusu Wabunge kutulia. Ni kweli wako Wabunge wanatafuta kick kwa jinsi alivyochangia, lakini kick zenyewe za namna gani? Kwa maana nyingine isiwe kick ambazo zinaharibu hadhi, heshima ya Bunge na pia kuchonganisha.

Mheshimiwa Spika, lakini pia na suala lingine aliloongelea Mheshimiwa Mariam Ditopile ni hili suala la kwamba Viongozi wetu wamepewa fedha. Kwa kweli hii imewachanganya sana wananchi Waheshimiwa Wabunge na nyinyi mnafahamu. Wananchi wengi hawachanjwi wengine kwa imani ya kwamba waliochanjwa wamepewa fedha.

Mheshimiwa Spika, sasa maneno haya kama yanatolewa na Kiongozi ni kweli yanawachanganya wananchi na yanaleta kitu ambacho sio utulivu katika nchi. Na kwa suala la Mheshimiwa Jerry Silaa, Mheshimiwa Mariamu Ditopile kasema amesikitishwa na drama zake na ule ubishoo ambao alikuja nao kwenye Kamati yakiwemo yale mavitabu aliyokuja nayo rundo.

SPIKA: Ahsante, malizia sasa.

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA – MWENYEKITI KAMATI YA BUNGE YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE: Mheshimiwa Spika, ingawa uliuliza vile vitabu hakuweza kuvitumia vyote. Aliweza kutumia kitabu kimoja tu Biblia katika lile rundo lote ambalo alikuja nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na la mwisho ni la Mheshimiwa Elibariki Kingu naye ame-quote vifungu vya Biblia na amelaani yote ambayo yamekuwa yakiendelea lakini ameuliza jambo moja Waheshimiwa Wajumbe. Kwamba, je, enzi za Hayati Mheshimiwa Dkt. Magufuli kwa mfano vitu ambavyo anafanya Mheshimiwa Gwajima angefanya? Waheshimiwa Wabunge na hasa akina mama tunaongea mambo ya gender na kwamba sisi tunaheshimu gender. Katika muda mfupi tu, anatokea mwanaume mmoja tena Mheshimiwa Mbunge, anaanza kuzungumza jambo ambalo hata mtoto mdogo yeyote ambaye ana akili timamu atasema hivi huyu mbona anamdharau mwanamke?

WABUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, ndiyo.

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA – MWENYEKITI WA KAMATI YA BUNGE YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE: Enhee! ndiyo maana yake, anamdharau mwanamke ndiyo hoja ya Mheshimiwa Kingu! kwamba je, wakati wa Mheshimiwa Hayati Magufuli angefanya haya? Maana yake kwa nini ayafanye wakati anaetawala ni mwanamke? Hii haikubaliki Waheshimiwa Wajumbe ninawaomba sana, Bunge zima liweze kuridhia maazimio yote mawili kwa ajili ya hizi hoja zote mbili ambazo tumeziwasilisha hapa kwa ajili ya majadiliano ambayo mmemaliza. Nirudie tena kuwaomba Wabunge wote waridhie maazimio yote mawili.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii ya kuchangia bajeti. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Mwigulu na timu yake kwa bajeti nzuri sana waliyoiwasilisha. Kwa mara ya kwanza, mimi ni kipindi changu cha pili Bungeni hapa. Nimeona Wapinzani wakianza kuisifu Serikali. Hii ni dalili ya kwamba kwa kweli Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, anafanya kazi nzuri. Muda mchache tu umemsikia Mheshimiwa Esther Matiko akizitaja Ibara, akitaja vifungu vya Katiba, akitaja Ilani yetu ya Chama Cha Mapinduzi kwa vifungu, lakini amesifu mpaka ile tozo ya asilimia sita ya elimu ya juu. (Makofi)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Adam kuna Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa tu nimpe taarifa Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili, kwamba kazi ya Mbunge ni kuisimamia na kuishauri Serikali. Ndio maana ukiapa haijalishi umetoka chama gani kwa sababu CCM ipo madarakani sasa hivi ina Ilani yao lazima tusome na niwaombe tu hizi Ilani msikae nazo kama mapambo. Kasomeni mfanye rejea muweze kuishauri na kusimamia Serikali vizuri. Ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwakasaka unaipokea hiyo taarifa.

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tena naipokea kwa mikono miwili, kwa sababu, narudia kwa mara ya kwanza, Ilani yetu kwanza inasifiwa na upinzani; lakini inasomwa. Kila miradi ambayo tulikuwa tunaipanga na inasomwa hapa. (Makofi)

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Taarifa.

T A A R I F A

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa kiongozi mzoefu wa kipindi cha pili. Upinzani sio uadui ni jicho la pili la Serikali. Kazi ya upinzani sio kukubali mambo yote ambayo Serikali inafanya vinginevyo wote tungekuwa chama kimoja. Kwa hiyo nampa taarifa, wajibu wetu sisi; sisi tunagonga muhuri sehemu ikifanywa vizuri, ikifanya vibaya tutapinga na nchi yetu itasonga mbele. Nampa taarifa. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwakasaka.

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea.(Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado point iko pale pale, sasa hata taarifa zao tunazipokea kwa sababu zina mashiko. Miradi ile ya nyuma ambayo kila mradi ulikuwa ukiletwa Bungeni ilikuwa inapingwa. Naunga mkono hoja. (Makofi)

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ridhiwani una taarifa gani tena? Haya karibu.

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mchangiaji hoja kwamba, shida iliyotokea hapa ni kwamba kuna mtu kasoma Biblia kuliko Mroma Mwenyewe. Ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwakasaka.

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mi taarifa za leo zote nazikubali. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kumpongeza Mheshimiwa mama Samia Suluhu Hassan kwa jinsi alivyoanza. Kwa kweli sasa hili Bunge tunakwenda vizuri, hata humu ndani sasa kumetulia, zile hoja tulizokuwa tunapingana pingana hazipo, lakini wakati tunasifia, tunamsifia Mheshimiwa Rais pia kwa teuzi mbalimbali.

Nakumbuka Mheshimiwa Mwigulu wakati anasoma bajeti yake alituambia kuhusu kadi ya njano na nyekundu; kwamba mama anazo zote mbili na tumeziona. Moja imetumika juzi juzi tu na kwenye mpira kuna kadi unapewa moja kwa moja nyekundu bila kuonywa, lakini nyingine unaonywa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mwenyekiti wa Maadili kama alivyokuwa anasema Mheshimiwa Matiko, ninapoona maadili yanamomonyoka huwa najisikia vibaya na hasa ya viongozi. Kwa sababu sisi moja ya kazi yetu ni kuishauri Serikali kama Bunge na sisi Kamati ya Maadili tupo pia kwa niaba ya Bunge zima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Mama Samia kwa kuonesha kadi nyekundu kwa Kiongozi mmoja wa Serikali ambaye ametumia ulimi wake vibaya. Moja ya maadili ya kiongozi ni pamoja na kutumia lugha ya staha. Sasa huyu mwenzetu mmoja aliweka comedy akazidisha akatumia lugha ambayo si ya staha, mama alimwonesha kadi nyekundu moja kwa moja. Mimi nampongeza sana na hiyo italeta heshima kwenye Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mwigulu kwenye eneo ambalo alilizungumza Mheshimiwa Munde, ameongea vizuri sana kuhusu lile suala la land rent. Tunahitaji kodi, kodi lazima ikusanywe na ni kweli kila nchi inaendelea duniani kwa kukusanya kodi. Naomba kuna vipengele kama viwili hebu Mheshimiwa Mwigulu akaviangalie au hata atakapoanza kuhitimisha hoja yake aje atufafanulie kidogo ni kweli kuna mkanganyiko kwenye eneo fulani. Kwa mfano, kuna wazee ambao walipata msamaha wa jumla kwenye kodi. Sasa itakapoingia ile tunalipa kwenye LUKU moja kwa moja wale wazee ule msamaha sijui itakuwaje. Pia na lile eneo ambalo utakuta kwa mfano mtu kwenye kiwanja kimoja ana mita tatu ambazo zote zipo kwenye kiwanja kimoja sasa wakati analipia LUKU ile sijui kama hakutakuwa na contradiction nyingine yoyote, basi hiyo Mheshimiwa Mwigulu atatufafanulia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwa upande wa TRA. Wananchi wengi wangependa kuwa na kampuni wanapotaka kufanya biashara, lakini mlolongo wa namna ya kufungua kampuni, mimi ni mjasiriamali na-declare interest. Kwa mtu wa kawaida kufungua kampuni kuna shida. Ile milolongo ya kuanzia kujaza fomu huko, ukishamaliza uende kwa Mtendaji, uende kwa Bibi Afya, uende kwa watu wa Chakula wa TFDA, sehemu mbalimbali haina shida. Hata hivyo, kuna eneo moja ambalo kabla hujaanza process yoyote unatakiwa ufanyiwe hesabu na mtaalam wa mahesabu. Sasa wengi unakuta kwamba hawawezi kutoa ile fedha kumpa Mhasibu ambaye unakuta gharama yake ni kubwa labda Sh.600,000 au Sh.700,000 na mtu ndio anataka kufungua kampuni. Naomba aliangalie eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia sehemu ya uhakiki. Tulishawahi kuzungumza huku, sehemu ya uhakiki wa madeni ni kichaka kabisa cha kuficha vitu mbalimbali. Maeneo yale kwa mfano, natolea mfano wa mwananchi mmoja wa jimbo langu ambaye anadai toka mwaka 2014/2015 madeni yake mpaka 2020 niliambiwa kwamba ameshahakikiwa. Nikawapigia mpaka Hazina wakasema wamekudanganya, hakuna katika majina hayo, huyo hawajaleta jina lake na huyu alihudumia Ofisi ya RPC na maandishi yao yapo, uhakiki sasa hivi una miaka karibu saba. Wanaendelea kuhakiki kwa hiyo ni kichaka cha watu kuficha haki za watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la sensa, namshukuru Mheshimiwa Mwigulu, amezungumzia suala la sensa. Naomba kwenye suala hili waje kutoa elimu ya kutosha, Tabora limetuponza. Ukiangalia kwa mfano Jimbo la Tabora Mjini alisema hapa Mheshimiwa wa Viti Maalum kuhusu ukubwa wa jimbo lile na idadi ya watu, ni tofauti kabisa. Tabora Mjini ina watu wasiopungua 500,000 inaenda 600,000 huko. Ni jimbo kubwa nilisema hapa wakati nachangia asubuhi, lina kata 29, lakini kutokana na baadhi ya watu kutojitokeza kwenye sensa, ile iliyopita hawakuweza kukidhi mahitaji ya sensa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninavyofahamu, huwezi kupanga maendeleo bila kujua una idadi ya watu kiasi gani. Kwa hiyo, naomba sana waje kutoa elimu ya kutosha, Jimbo la Tabora Mjini ni kubwa na pale itakapofika kugawa majimbo, Tabora Mjini wasije wakaisahau ni kubwa ina kata 29, vijiji 41, ni jimbo ambalo sehemu nyingine ukienda ni masaa mawili kwenye jimbo moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee suala la urasimishaji kwa kumalizia. Wako watu ambao waliaminiwa, kampuni mbalimbali kwa ajili ya urasimishaji kwenye ardhi. Wamekusanya fedha za wananchi; wananchi wanasubiri kupimiwa na zile kampuni zimechukua muda mrefu na sehemu nyingi hazijarasimishwa rasmi. Hizi kampuni zinaonekana nyingine za kitapeli. Serikali iangalie kama kuna uwezekano wakizigundua wazifute kabisa ili kampuni zingine ziweze kuchukua hiyo kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya machache, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ADAMSON E. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia kwenye huu Mpango uliowasilishwa na Waziri wetu wa Fedha. Kwanza nauunga mkono kwa asilimia moa moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa hapa nilipofika. Maandiko yameandikwa kwamba Mwenyezi Mungu humpa amtakaye na kumnyima amtakaye. Kwa hiyo, nashukuru kwamba wenzetu ambao wanapiga kelele sana Mwenyezi Mungu aliamua tu kwamba hawa hawafai kwa sasa. (Makofi)
MBUNGE FULANI: Kwa kuiba.
MHE. ADAMSON E. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niwashukuru wananchi wangu wa Tabora kwa kunichagua kuwa Mbunge wa Tabora Mjini. Pia hawa ndugu zetu wanapoongelea suala la Hapa Kazi Tu, nashindwa kuelewa sijui hawaoni au hata hawasikii kwa sababu unapoongelea kauli mbiu ambayo wewe unaona kwa vitendo inafanyika, mimi nashangaa kama hawaoni hata kama kuna mabadiliko hata ya ukusanyaji kodi tu nayo hawaoni. Kama tunakwenda kwa kauli, mnaelewa kuna viongozi ambao walisemwa kwenye Bunge hili hili, wakatukanwa sana, lakini leo wakaja na kauli mbiu ya siku 100 nyumba za nyasi hamna wakati kwao kuna nyasi nyingi tu lakini leo wanakumbatiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba mimi nianze kuchangia kwa suala la reli. Sisi ambao tuko Kanda ya Ziwa, suala la reli kwetu ni muhimu sana na siyo tu Kanda wa Ziwa lakini kwa uchumi wa nchi yetu ya Tanzania. Reli ya kati kwa jinsi ilivyo sasa kuanzia Dar es Salaam kuja Tabora lakini kutoka Tabora kwenda Mwanza, kwenda Kigoma na Mpanda ni chakavu sana na ndiyo maana mara kwa mara reli hii imekuwa na matatizo ya kukatika vipande vipande. Kwa hiyo, lile suala la standard gauge, naiomba Serikali iipe kipaumbele reli hii kwa sababu inasaidia vitu vingi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la viwanda, kwa mfano Tabora tulikuwa na Kiwanda cha Nyuzi nimeshawahi kuzungumza hapa ambacho sasa kimekufa kwa sababu ya mwekezaji ambaye hakuwa mkweli. Sasa Mheshimiwa Waziri mhusika nadhani nilizungumza niliongee kwa ufupi kidogo, kile kiwanda yule aliyebinafsishiwa sasa amegeuza godown lakini pia kakifunga. Kwa hiyo, naomba Waziri wa Viwanda, Tabora tunahitaji sana viwanda kwa sababu raw materials zipo, tunahitaji pia Kiwanda cha Tumbaku kwani inalimwa zaidi Tabora kuliko mkoa mwingine wowote, hakuna sababu ya Kiwanda cha Tumbaku kuwa Morogoro. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Wanatabora tunaomba katika kuweka vipaumbele mkikumbuke Kiwanda cha Tumbaku Tabora kwa sababu ndiko zao linakolimwa zaidi. Kwa sasa tuna vile viwezeshi vingi vya kufanya hata ile tumbaku yenyewe ifikiwe kiurahisi. Barabara hii inayokatisha Manyoni maeneo ya Chaya imebaki kama kilomita 82 kufika Tabora Mjini. Kama barabara ile itakuwa imekamilika basi Tabora mtakapokuwa mmetuwezesha Kiwanda cha Tumbaku mtakuwa mmetusaidia. Siyo suala tu la kama wameisaidia Tabora, lakini na uchumi kwa sababu hata wale ambao wanasafirisha tumbaku ile kuitoa Tabora kuipeleka Morogoro ni gharama kubwa lakini pia gharama zile zinafanya wakulima wa tumbaku wanaumia zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tabora wamekuwa waaminifu sana wote mnafahamu, imekuwa ni ngome ya Chama cha Mapinduzi hata kama wapinzani wanajaribu kubeza lakini ile imekuwa ngome ya Chama cha Mapinduzi. Mkoa wetu wa Tabora watu huwa hawasemi sana wanaenda kwa vitendo. Kwa kuwa hawasemi sana naomba tusiwachukulie upole wao kwa kuwacheleweshea vitu ambavyo vinaonekena kwa macho. Nadhani mnaelewa Tabora ukiwaudhi kidogo unakaa miaka mitano unatoka nje ya ulingo. Tabora katika miaka thelathini haijawahi kumrudisha Mbunge zaidi ya miaka mitano na hizi ni hasira zao. Pamoja na hayo bado hawachagui mpinzani, watamtoa wa CCM wataweka wa CCM kwa maana ya kwamba bado wanaimani na Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
MHE. ADAMSON E. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Tabora pia tunarina asali kwa kiwango kikubwa. Naomba tunapoweka mipango hii tuweze kukumbuka hata kuwa na kiwanda kidogo cha kusindika asali Tabora. Si hilo tu, Tabora pamoja na Shinyanga na mikoa inayofuata wafugaji ni wengi sana, ngozi inayopatikana kule, viwanda kama leather goods lakini pia viwanda vya kusindika nyama vinahitajika kule. Maana ili uwe na viwanda pia ni vizuri kama kile kiwanda kiwe ni kiwanda ambacho kina faida kwa uchumi wa Tanzania na siyo siasa zaidi. Kitu cha kujiuliza raw materials zinapatikana maeneo yale, Tabora zinapatikana. Kwa hiyo, naomba mtukumbuke kwa hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna suala lingine ambalo linahusiana na reli hiyohiyo ya kati kutoka Isaka kwenda mpaka Keza na kutoka eneo la Uvinza kwenda Msongati hii ni reli mpya. Reli hii tunaihitaji kwa ajili ya uchumi, tunaihitaji kwa ajili ya kupata maendeleo katika maeneo hayo ambayo kwa kweli ni ngome ya Chama cha Mapinduzi kama nilivyosema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie reli upande wa hapa Morogoro hasa maeneo haya ya Godegode. Kila mara imekuwa pale ndiyo pana matatizo makubwa, tatizo ni nini kama Malagarasi imeshajengwa? Kama Malagarasi daraja limeweza kufanya kazi nina imani Serikali hata pale Godegode inawezekana. Hata hiyo standard gauge tutakayoitengeneza kwa mujibu wa mpango huu basi isije ikawa tena kufika Godegode yakawa yaleyale. Naomba Waziri anayehusika na hilo aweze kulitilia maanani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini naomba nizungumzie…
TAARIFA
MHE. MAULID S. A. MTULIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.
MWENYEKITI: Haya taarifa Mheshimiwa Mtulia.
WABUNGE FULANI: Aaaaah.
MHE. MAULID S.A. MTULIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nimpe taarifa mazungumzaji kwa kutumia Kanuni ya 64(1) (a) amezungumza maneno ambayo siyo sahihi na katika Bunge hili Tukufu Mbunge yeyote hatakiwi ama hapaswi kuzungumza uongo. Mzungumzaji aliyekaa ametoa taarifa za uongo ya kwamba Tabora hakuna Mbunge wa Chama cha Upinzani isipokuwa ni CCM tu wakati humu ndani tuna Mbunge wa Chama cha Wananchi (CUF) kutoka Tabora. (Makofi)
MBUNGE FULANI: Huko siyo Tabora ni Kaliua.
MHE. ADAMSON E. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niliweke sawa hili labda pengine unajua Kiswahili kina matatizo yake. Mimi ni Mbunge wa Tabora Mjini na hawa wanaongelea sijui Kaliua mimi sijaongelea Kaliua. Nimezungumzia miaka 30 ambayo inahusiana na mjini na huu ni ukweli.
MBUNGE FULANI: Ulisema Tabora.
MHE. ADAMSON E. MWAKASAKA: Narudia Tabora Mjini haijawahi kutokea katika miaka 30 Mbunge akarudi mara mbili. Naomba nieleweke sijaongelea Kaliua kwa hiyo sikusema uongo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ulinde zile dakika zangu ambazo imeingia hoja ambayo nayo haikuwa ya kweli. Tunapoongelea hii reli, reli ina matatizo mengine ambayo Serikali bado nadhani haijakaa sawa. Ni vizuri kukumbuka suala la wafanyakazi wa reli, reli hii imekuwa ikihujumiwa mara nyingi sana. Kile kipindi cha transition wakati reli imechukuliwa na wale wawekezaji wa India, wafanyakazi wale walipokuwa wanarudi kujiendesha wenyewe waliahidiwa kulipwa mafao yao ambayo yatakuwa tofauti na mkataba wa mwazo ambayo mpaka leo hayajalipwa kwa wafanyakazi wale. Wafanyakazi wengi wa reli kwa muda mrefu wamekuwa katika kipindi cha malalamiko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iweze kufikiria kulipa wale wafanyakazi haki zao stahiki ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi na waweze kuipenda kazi yao. Kwa sababu mengine yanatokea inakuwa ni hujuma tu kwa sababu mtu hajaridhika na kitu anachokipata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, reli kuna matatizo wafanyakazi hawajalipwa haki zao ambazo ziliahidiwa na Serikali kwamba akishatoka yule mwekezaji wa Kihindi basi kuna maslahi ambayo watalipwa ambayo wanayapigania mpaka sasa. Nina imani wale wafanyakazi watakapokuwa wamelipwa zile staili ambazo waliahidiwa basi ufanisi katika Shirika letu la Reli la Tanzania utakuwa umeboreka na utakuwa wa kupendezesha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono kwa asilimia mia moja Mpango huu kama ulivyowasilishwa, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mimi naomba kwanza nianze kwa kuipongeza Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli pamoja na timu yake yote ya watendaji wakiwemo Mawaziri wote kwa kazi nzuri ambayo wameendelea kuifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuunga mkono hoja ili nisije nikasahau ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mheshimiwa Charles Mwijage na nampongeza kwa hotuba yake na uwasilishaji wake mzuri wa Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa fedha wa 2016/2017. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuanza na utangulizi huo, nianze kuchangia kuhusiana na wafanyabiashara wadogo. Wafanyabiashara wadogo kama ambavyo Mheshimiwa Mwijage, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji alivyooanisha kwenye kitabu chake kwamba nchi kama Korea Kusini, Singapore na Malaysia wakati sisi tunapata uhuru nchi hizi tulikuwa tunalingana kiuchumi, sasa leo wenzetu wako mbali mno, sijui sisi tatizo letu ni wapi. Moja ya tatizo ninaloliona ni urasimu kwa wafanyabiashara hawa wadogo ambao tumekuwa tukiimba kwamba kwetu wako karibu asilimia 99 na hata nchi zingine ambao kwa kiasi kikubwa ndiyo wanachangia pato kubwa la Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikisema mfanyabiashara mdogo mdogo, tunaanzia na wale wanaopata leseni za kawaida, mtu ana mtaji wake wa shilingi laki mbili, tatu mpaka milioni moja. Kwa urasimu ambao tunao kwenye biashara, kwa mfano, mfanyabiashara anakata leseni ya kawaida shilingi elfu themanini, anataka kuja kuomba tender ya Serikali, kuna viainishi vingine anatakiwa kuwa navyo. Kwa mfano, awe na cheti kutoka Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) wakati anataka kuomba tender hapo hajapata, hii nayo ina gharama yake. Kwenye Sheria ya Manunuzi (PPRA) kuna GPSA, ukitaka kujisajili GPSA kununua kitabu chao tu kile cha kuomba kujisajili siyo kupata biashara ni shilingi laki moja. Mimi nina mashaka makubwa mfanyabiashara wa mtaji wa shilingi laki mbili mpaka tano au milioni moja ataweza kufanikisha milolongo hii yote. Pia huwa kunakuwa na mwingiliano wa kazi kati ya PPRA na TFDA (Mamlaka ya Chakula na Dawa). Unaweza ukakuta hawa PPRA nao wanakagua chakula, sijui kwa mamlaka yapi, mimi nashindwa kuelewa kwa sababu TFDA na hawa PPRA wanachanganyana. Kwa hiyo, ile Sheria ya Manunuzi kama walivyosema wenzangu nadhani sasa imepitwa na wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nichangie suala la gharama ambayo wafanyabiashara wanakutana nayo hasa pale bandarini. Kuna ushuru wa uzembe unaofanyika zile damage charges, ule uzembe unaofanyika pale haumhusu mteja. Vitu vinavyoendelea pale kwa mfano wengine waliongelea mambo ya magari lakini kuna mizigo pia, mteja unafuatilia toka siku ya kwanza unajua meli imeingia na ina gari lako, sijui wengine lakini mimi nimetoa magari mara nyingi pale, haijawahi kutokea zile siku wanazokupa kama free ukaweza kutoa gari. Wao wana kisingizio, wakati wewe unataka kwenda kulipia wanakuambia system iko down.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo wasafirishaji kwa mfano wa mabasi na reli, tunaona kabisa kwamba kama gari kwa mfano limekwama njiani wataleta basi lingine kwa gharama zao kwa sababu siyo kosa la msafiri. Vivyo hivyo hata kwenye reli tumeona reli ya kati hapa ikitokea matatizo wanakodisha magari kwa gharama zao.
Sasa hawa TRA mitandao yao inapokuwa iko down kwa nini gharama zile aingie mteja? Mimi nadhani gharama zile zilikuwa zinapaswa kubaki TRA. Hili ni jipu kwa sababu kama kweli kila siku mitandao iko down, mtu anataka kwenda kulipia pesa wanasema kuna tatizo la mitandao sasa hivi huwezi kulipia, ni mapato ya Serikali yanachelewa kukusanywa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kwenye suala la Sera hii ya Viwanda. Kama alivyoainisha Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni kwamba nchi yetu itakuwa ya viwanda kwa asilimia zisizopungua 40, hapa nirudi kwenye Mkoa wangu wa Tabora, mimi ni Mbunge wa Tabora Mjini, nimeshasema mara nyingi mwamba ngoma anavutia kwake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tabora ni mkoa wa kihistoria hata kura zile za uhuru tatu zilifanyika Tabora. Tabora inalima tumbaku kwa wingi kuliko sehemu yoyote Tanzania hii. Tabora ilikuwa na kiwanda cha nyuzi lakini Kiwanda hiki cha Nyuzi, siku moja Mheshimiwa Mwijage wakati anajibu swali moja hapa alisema kwamba wame-respond vizuri wale watu kwamba wanasema nyuzi hazina soko. Siyo kweli Mheshimiwa Mwijage, naomba siku ukipata nafasi katembelee Tabora pale na mimi nikiwepo, kimefungwa na mitambo iliyopo mle ndani inasadikiwa imeuzwa kama chuma chakavu kama walivyosema wengine na huwa hawakufungulii unapokwenda pale. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mwijage hii sababu wanayotoa si kweli, kile kiwanda aliyebinafsishiwa siyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini si hivyo tu kuna asali Tabora. Naomba Mheshimiwa Mwijage hata kama viwanda itashindikana kama niko sahihi hapa Tanzania hatuna maabara ya kupima ubora wa asali kwa maana ya maabara. Naomba basi hata tutakapojenga maabara tujenge Tabora ili wale wanafunzi ambapo vyuo viko vingi pale waweze kupata hiyo ajira ambayo tunasema sasa tutakuwa watu wa viwanda na biashara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia naomba nimalize kwa hizi taasisi ambazo ni za utafiti kama TIRDO, TEMDO na CARMATEC. Naomba wanapofanya utafiti waikumbuke na Tabora. Kwa mfano, wanapotengeneza matofali ya saruji ambayo yamechanganyika na udongo, wanatoa matofali ambayo unajenga nyumba za kisasa, mafunzo yale yakifanyika Tabora yatawawezesha pia vijana kupata ujasiriamali kwa kutumia taasisi hizi za utafiti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya machache, narudia kuunga mkono hoja na ahsante kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kwanza nimshukuru Mbunge mwenzangu kwa kunipa nafasi hii ya dakika tano, lakini naomba pia nianze kwa kumpongeza Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano pamoja na Uchukuzi kwa hotuba yake nzuri. Mimi naomba niongee suala moja ambalo hili limekuwa ni tatizo kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba sana Mheshimiwa Waziri, kwa kuwa kampuni hii ya kuhodhi mali ya reli (RAHCO) iliundwa kisheria atuletee muswada hapa Bungeni ili tuweze kufanya marekebisho waweze kuungana. Kuna tatizo kubwa sana la hii RAHCO. RAHCO ni moja ya tatizo katika uendeshaji wa Shirika la Reli Tanzania na ushahidi upo. Hawa RAHCO ndiyo waliokuwa wanauza hata mabehewa yale ambayo waliuza kwa chuma chakavu ni hawa RAHCO. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine, kuna tatizo la conflict of interest (mgongano wa maslahi) kati ya RAHCO na TRL unafanya lile shirika lisiende vizuri. Naomba labda nimwambie Mheshimiwa Waziri kwamba achunguze vizuri ile Godegode imesemwa sana na Gulwe; yale mabilioni yanayopelekwa pale kila siku na RAHCO yanakwenda wapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, TRL inashikilia reli, inaangalia reli na kinachopita juu ya reli. RAHCO wao wanaangalia reli tu, wafanyakazi karibu asilimia 95. Hata wa RAHCO wenyewe wako Shirika la TRL kwa hiyo, ili kuondoa huu mgongano wa kimaslahi haya makampuni ni vizuri yaunganishwe. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufanya majumuisho kesho kwa kuwa huu pia ni msimamo wa Kamati ya Miundombinu kwamba haya Mashirika yaunganishwe aweze kutupa majibu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine kuna suala la mishahara. Hawa RAHCO ndiyo wanapelekewa pesa zote na wanajilipa mishahara mikubwa kweli kweli tofauti na TRL, wakati uendeshaji wao ulikuwa mmoja, hata Mheshimiwa Rais ameongelea sana hili suala la mishahara kupita kiasi kwa watu ambao wanafanya kazi zinazofanana. Sasa lile suala la kwamba RAHCO wana hodhi kila kitu lina matatizo sana. Kwa hiyo, ningeomba hii kama tulivyokubaliana hata kwenye Kamati ya Miundombinu, ulete muswada wa kuirudisha RAHCO pamoja na TRL. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine kuna mkataba ule wa mwaka 2014 ambao ulikuwa umesainiwa kati ya Afrika Kusini na Tanzania kuhusu kutengenezwa vichwa kumi na moja vya treni. Vichwa tisa viko tayari, sasa ningemuomba Mheshimiwa Waziri sijui hili suala la kulipia vile vichwa tisa, tulipata taarifa ni karibu shilingi bilioni 57 zinatakiwa ili waweze kulifanyia hilo, lakini pia maslahi ya Wafanyakazi ambayo yanafika karibu 7.5 au 6 billion; malimbikizo ya madai yao mbalimbali; haya yanaleta migogoro kila mara katika Shirika la Reli Tanzania.
Naomba Mheshimiwa Waziri wakati unajumuisha majumuisho yako na hili uweze kuliona, ni moja ya matatizo ambayo kila mara yanaleta migogoro katika Shirika letu la Reli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia naomba nizungumzie suala katika…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga Mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa uwasilishaji mzuri wa mpango wa makadirio ya mapato na matumizi ya fedha kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina hoja chache za kuandika au kutoa ushauri kwa maandishi, ili zifanyiwe kazi na Wizara kama ifuatavyo:-
(i) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tetesi kuwa moja ya sababu inayosababisha kukawia au kucheleweshwa kwa uunganishaji upya wa mashirika mawili ya reli ya kati yaani TRL na RAHCO, ni tetesi au madai kuwa kuna baadhi ya watendaji ndani ya Wizara ambao wana maslahi ya binafsi ya kibiashara kupitia miradi inayosimamiwa na RAHCO. Naomba Mheshimiwa Waziri uchunguze hili.
(ii) Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali ifanye juhudi kubwa katika kuzifufua upya na kuziimarisha karakana za TRL za Morogoro na Tabora ili ufanisi wa kiufundi na kuimarisha vichwa na mabehewa ya treni uweze kuwa wa uhakika.
(iii) Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Taarifa ya Utekelezaji wa Miradi ya Mfuko wa Maendeleo wa Mawasiliano kwa Wote hadi Aprili, 2016, Jimbo la Tabora Mjini lenye jumla ya kata 29, kata za Kalunde katika vitongoji vya Ulundwa na Ilamba, kata ya Ifucha, vitongoji vya Miziwaziwa, Usuhilo na Ugurudu, kata ya Ntalikwa, kitongoji cha Shimo la Udongo, kata ya Uyui, kitongoji cha Imala Mihayo na Kakulungu na kata ya Ndevelwa, vijiji vya Ibasa na Izenga, hakuna kabisa mawasiliano ya simu. Ninaomba Wizara iwakumbuke wananchi hawa katika uwekaji wa minara ya simu ili nao waweze kupata mawasiliano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi hii ili nami niweze kuchangia hii hotuba ya bajeti. Naomba kwanza nianze kwa kusema naiunga mkono hotuba hii kwa asilimia mia moja. Nianze pia kumpongeza Waziri wa Mipango, Mheshimiwa Philip Mpango, kwa bajeti yake nzuri, lakini pia na Serikali yote kwa ujumla inayoongozwa na Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli, kwa utendaji mzuri wa kazi pamoja na Mawaziri wote na watendaji wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze na suala la muhimu katika uchumi wa nchi yoyote ambalo linatokana na afya. Napenda kuipongeza Wizara ya Afya, kwa takwimu ambazo zimeonekana humu katika kitabu zinazoonesha kwamba vifo vya mama na mtoto vimepungua kwa kiwango kikubwa, naipongeza sana Wizara ya Afya. Hata hivyo, kuna data imenishtua kidogo, data hii inahusiana na ongezeko la mimba au ujauzito usiotarajiwa kwa watoto wa miaka 19 na ambao wanafanana na hiyo kutoka asilimia 23 mwaka 2010 mpaka asilimia 27 mwaka 2015, hii data kwa kweli inatisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, nachelea kujua ni nini hasa tatizo, pengine ni elimu, lakini pengine kuna tatizo lingine. Sasa tusipoangalia, hata tunapojadili bajeti ambayo inahusiana na uchumi na hasa tunapokwenda kwenye uchumi wa kati ambao ndiyo matarajio yetu, kama kutaendelea kuwa na ujauzito usiotarajiwa kwa vijana wetu kwa kiwango kikubwa cha namna hii, basi hata ile nguvukazi yenyewe tunayoitarajia tutakuwa na mashaka nayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia labda nielekeze hili kwa Mheshimiwa Waziri wa Afya. Suala la elimu kwa ajili ya hawa vijana wetu ambao sasa wanaongezeka kupata mimba zisizotarajiwa, vijana wadogo. Pengine suala la elimu sasa limekuwa limefifia na hasa njia hizi za kujikinga na matatizo mbalimbali yakiwemo haya ya kupata mimba za utotoni pamoja na magonjwa mengine. Kulikuwa na kampeni mbalimbali miaka ya nyuma na nadhani sasa zinaendelea ila inaelekea zimepoa.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kupoa huko sasa watoto data zinaanza kupanda kupata ujauzito utotoni. Nitolee mfano, kwa mfano suala linaloongelewa zaidi na Wizara na watu mbalimbali ni kuwaambia watu namna ya kujikinga kwa kutumia njia mbadala,kwa mfano njia za uzazi wa mpango zinaongelewa sana. Nadhani tuna aibu kidogo, mimi sioni sana likiongelewa suala la watoto hawa ambao tayari wameshakuwa watu wazima, kutumia njia kwa mfano kama mipira ya kiume (condoms), watu wanaona ni aibu kuzungumza hili wakati nchi tunazojilinganisha nazo, nchi zilizoendelea kwa mfano kama Uingereza, Marekani na nyingine, hili ni suala la wazi kabisa huwa wanajadili, wanawaambia vijana wao kwamba njia mbadala ili muweze kujikinga na mimba za utotoni lazima mtumie vitu kama mipira.
Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumzia hilo kwa sababu kuna wengine wanadhani hili suala la kuongelea masuala kama condom ni aibu fulani na hapa tunafanya makosa makubwa sana. Kuna watu wanatembea na silaha kwa ajili ya kujikinga, si kwamba wanategemea kwamba labda watakumbana na majambazi wakati huo, hapana.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo hivyo hata watoto hawa ambao tayari ni watu wazima, wanapotembea na mipira kama hii kwa ajili ya kujikinga, si aibu. Nakumbuka kipindi fulani cha nyuma kuna Waheshimiwa Wabunge fulani walipokuwa wanasachiwa wakakutwa kwenye mabegi yao kuna condoms, watu wakasema hii ni aibu, mimi sioni kwamba ile ilkuwa ni aibu. Hawa wanaonekana kabisa wanajali na wako tayari kujikinga, ile ni silaha, ni anti-missile ya kupata ujauzito, ni anti-missile ya kupata magonjwa yasiyotarajiwa, kwa hiyo nadhani elimu ni kitu muhimu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee suala hili ambalo ni la hivi karibuni kuhusu kuitoa kwenye halmashauri kodi ya majengo na kuipeleka kwenye Serikali Kuu. Hili suala, halmashauri zetu nyingi zinatumia kodi hii…
Mheshimiwa Naibu Spika, naona kengele kama imegonga mapema sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kodi hii ndiyo inategemewa na halmashauri nyingi saa hapa nchini, sasa kuifuta kuna halmashauri ambazo zitakufa kifo kinachoitwa natural death. Kuna halmashauri ambazo kipato chake kinategemea zaidi kodi hizi, naipongeza sana Serikali kwa kuondoa kodi nyingi za mazao ya kilimo, lakini kuna halmashauri ambazo hata kwa mwaka mzima haifikishi zaidi ya milioni 100, kwa mfano ile halmashauri ya Gairo, Morogoro. Ile halmashauri, nilikuwa kwenye Kamati ya LAAT, ile halmashauri ina kipato kidogo sana kwa mwaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee pia hili suala la hizi kodi za simu. Nina mashaka, pamoja na kwamba Serikali inatuambia haitatuathiri watumiaji wa kawaida, wale wa makampuni ya simu ni wajanja, lazima kodi zile zita-back-fire kwa mtumiaji wa kawaida, atakuja kuathirika na kodi zile.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hizi kodi pia za usajili wa magari na usajili wa pikipiki, imepandishwa kutoka 150,000/= mpaka 250,000/= kodi ya magari, hii itasababisha watu wengine kuanza kukwepa suala la ku-transfer gari, watu wengi watatumia majina ya wenzao. Hiki kitu kitawakosesha Serikali mapato, bora utoze kidogo lakini uwe na uhakika wa kupata kodi ile kuliko kuikosa kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kupanda kwa hii kodi ya pikipiki kutoka 45,000/= mpaka 95,000/= ni kodi kubwa mno. Kodi hii itatufanya tuweke uadui ambao si wa lazima kati ya wamiliki wa pikipiki (bodaboda) ambao walitetewa na Bunge hili. Miaka iliyopita, bodaboda hawa ndiyo walitetewa kuhusu kodi, wakatetewa zikaja pikipiki nyingi nchi hii, sasa leo wanapandishiwa kodi kwa zaidi ya asilimia 100, sijui tunawaweka katika hali gani. Inaweza ikapelekea hawa wasiwe na imani na Serikali yao; naomba kodi za namna hii ziangaliwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni hili suala la maagizo elekezi kutoka Wizara ya Ardhi. Kuna maagizo elekezi kutoka Wizara ya Ardhi kuhusu kusimamisha kwa muda usiojulikana uuzwaji wa viwanja…
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kujadili bajeti hii ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji. Nami nianze kwa kuwapa pole wale wote ambao wamepata majanga mbalimbali yakiwemo haya ya ajali ambazo zimewakumba watoto wetu kule Arusha, lakini na zingine mbalimbali ambazo zimetokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nitumie fursa hii kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na Baraza lake lote la Mawaziri kwa jinsi wanavyotutendea haki kwa jinsi sisi wawakilishi. Kipekee niipongeze Wizara hii na hasa Waziri wake Engineer Lwenge pamoja na Naibu, Katibu Mkuu wake kwa kutukumbuka sisi wana Tabora.

Sisi Tabora kwa muda mrefu tumekuwa na matatizo ya maji na tatizo hili tumekuwa tukiliimba hapa kila mara na hata waliotangulia ni tatizo lililokuwa sugu. Sisi wana Tabora tunaendelea kusema tunaomba mtufikishie salamu za shukrani kwa Mheshimiwa Rais kwa kutimiza Ilani na Sera za Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo pale Tabora kwenye upande wa maji juzi juzi tu tumetoka kushuhudia mkataba wa mradi wa Ziwa Victoria wa bilioni 600 ambazo zimesemewa semewa hapa; nazidi kuishukuru Serikali. Pia siku chache zilizopita Makamu wa Rais Mama Samia Suluhu Hassan alikuwepo pale kwa ajili ya kuzindua mradi wa maji kule Mabama Mkoani Tabora. Tunasema ahsante Serikali kwa kuijali Tabora.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna matatizo ya maji ambayo kwa kutumia lile ziwa moja la Igombe maji yetu yamekuwa hayana uhakika na hasa yamekuwa ni maji machafu ambayo hata rangi yake mara nyingi utaona ni ya kijani. Sasa tumepata fursa hii tunasema ahsante. Hata hivyo, nitakuwa sijaitendea haki nafsi yangu na hata wananchi wa Tabora kama sitazungumzia hili lililojitokeza leo kwa baadhi ya Wabunge wenzetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Mbunge mwenzetu tena naomba ku-declare interest kwamba nipo naye kwenye Kamati ya Miundombinu, bahati mbaya hayupo hapa, Mheshimiwa Kitwanga, alizungumzia suala la kwa nini ule mradi wa Tabora umepewa hela nyingi kiasi hicho, amesahau kwamba Tabora ilikuwa imesahaulika miaka mingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, napata mashaka Mheshimiwa ambaye ameshakuwa hata Waziri, kauli alizozitumia hapa hazipaswi kabisa kutumiwa na mtu yoyote ambaye ni kiongozi wa Serikali, ambaye amewahi kuwa kiongozi wa Serikali na pia ni Mbunge. Unapo sema kwamba mradi ule umepita kwao, kule Kolomije na kwamba mradi ule kwa kuwa unakuja Tabora, yeye yuko tayari kuhujumu mradi ule kuzima mitambo. Kwanza huu ni uasi, lakini si tu uasi ni kuchochea mambo ambayo katika nchi yetu hatujayazoea kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyofahamu kuna miradi mingi imepita nchi hii ambayo haijawanufaisha watu ambao wanaokaa maeneo yale, kwa mfano mradi wa REA, hata nguzo za umeme zinapita mahali pengine ambapo watu hawapati mradi huo, lakini sijawahi kusikia wakisema watang’oa nguzo za umeme. Sasa yeye akisema yuko tayari ule mradi aweze kuzima zile mashine huu ni uchochezi ambao haukubaliki kabisa. Pia unaposema kwamba mimi nikiwa Waziri kule ndani nilikuwa sisemi nitasema nje anataka kutupa message gani? Kwamba wakiwa kule ndani wanakuwa waoga? Sidhani kwamba lile suala linapaswa kuzungumza namna hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kutokana na mradi huu, kuna Mheshimiwa Mbunge mwingine ameongelea mpaka mchakato wake wa mradi wa maji wa Tabora kwamba mchakato wake ana taarifa kwamba haukwenda vizuri na kwamba kulikuwa na waombaji watano na kwamba wengine hawakutendewa haki. Nashangaa pilipili usiokula inakuwashia nini?

Sisi ambao ndio wenye mradi ule tunaona kila kitu kimekwenda vizuri na ule mradi tayari na ule mradi tayari umesainiwa na watu sasa hivi karibu wanaanza kazi. Atuachie sisi wana Tabora tuamue kwamba wale waliopewa ule mradi hawapaswi kuwa na ule mradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Tabora tuna tatizo moja wakati tuanasubiri huo mradi wa Ziwa Victoria. Tabora ile mamlaka yetu ya maji TUWASA imekuwa na madeni makubwa wanaidai Serikali zaidi ya shilingi bilioni 3.3 ambazo ni malimbikizo ya madeni ya muda mrefu. Sasa naiomba Serikali, ili kuwe na ufanisi na ile Mamlaka ya Maji Tabora, basi deni hili lilipwe ili angalau tuweze kuwa na huduma ya maji ya uhakika.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanasema asiyeshukuru kwa dogo hata kwa kubwa hawezi kushukuru. Mimi kwa upande kwa Mkoa wa Tabora kwa hapa ambapo Wizara na Serikali yetu imetufikisha kwenye suala la maji, niendelee kuipongeza Wizara pamoja na Chama chetu cha Mapinduzi kwa sababu tunatekeleza sera yake na Ilani pamoja na ahadi mbalimbali zilizoahidiwa kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante.
TAARIFA YA KAMATI YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE KUHUSU SHAURI LA KUDHARAU NA KUDHALILISHA BUNGE LINALOMKABILI MHE. GODBLESS JONATHAN LEMA (MB)
EMANUEL A. MWAKASAKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE: Mheshimiwa Spika nakushukuru kwa kupewa nafasi ya kuhitimisha hii hoja. Labda kuja jambo moja ambalo amelisema Mheshimiwa. Kuna hili ambalo alikuwa analizungumzia Mheshimiwa Mnyika la kunukuu Ibara ya 63, lakini pia akanukuu kanuni ya 5 na amenukuu kanuni hizi ili kujaribu kutafuta uhalali kwamba ametumia vifungu na kujaribu kutaka kuonesha jamii au hata wananchi kwa ujumla wadhani kwamba ulichokifanya pengine umekiuka Katiba au kifungu chochote cha kanuni, kitu ambacho si kweli.

Mheshimiwa Spika, Kanuni ya 74, kanuni ya 72(1) inakupa mamlaka ya kuangalia amani na utulivu Bungeni, ninaomba kwa ridhaa yako nisome 72(1) inasema:

“Spika atakuwa na wajibu wa kuhakikisha kuwa, utaratibu bora unafuatwa Bungeni, na uamuzi wa Spika kuhusu jambo lolote la utaratibu utakuwa ni wa mwisho.” Hii ni kanuni ya 72(1) ya kanuni zetu za Kudumu za Bunge.

Kanuni ya 74(1) inasema:

“Spika anaweza kutaja jina la Mbunge kwamba amedharau mamlaka ya Spika na kisha kupeleka jina hilo kwenye Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge ikiwa

(a) kwa maneno vitendo, Mbunge huyo anaonesha dharau kwa mamlaka ya Spika; au

(b) Mbunge huyo atafanya kitendo chochote cha makusudi au Mbunge yoyote anayeongoza shughuli hiyo.”

Mheshimiwa Spika, kitu ambacho Mheshimiwa Lema alikifanya hapa. Kwa hiyo, hakuna mahali popote ambapo umekiuka kanuni yoyote.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Lema jana alisema kitu cha ajabu sana, kwamba yeye alichokisema humu Bungeni na kipo kwenye hansard cha kudhalilisha Bunge na kuliita dhaifu ni msimamo wa Kambi ya Upinzani na leo tunaweza kuthibitisha kwa jinsi walivyoweza kutoka wote hapa, kumbe kweli wao msimamo wao ni kulidhalilisha, kulidharau Bunge. Kwa mantiki hiyo, kwa kuwa tayari tumeshamtia hatiani Mheshimiwa Lema kwa kutohudhuria Mikutano mitatu ya Bunge, Waheshimiwa wengi wote wameweza kuunga mkono pia hoja hii.

Mheshimiwa Spika, naliomba Bunge lako Tukufu liweze kupokea taarifa hii ya Kamati ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge, lakini pia kuridhia azimio la adhabu ya Mheshimiwa Lema ambayo imependekezwa na Kamati ya Haki Kinga na Mamlaka ya Bunge.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji wa pili katika Wizara hii. Nami kama Msemaji aliyetangulia nianze kwanza kupongeza kwa jinsi ambavyo Mheshimiwa Lukuvi pamoja na Naibu Waziri wake Mheshimiwa Angelina Mabula wanavyokwenda na kasi ya kuweza ku-solve migogoro mbalimbali ya ardhi katika nchi hii, kitu ambacho tulikuwa hatujazoea kukiona mara kwa mara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lukuvi amekwenda sehemu nyingi sana na pengine kama alivyosema Mheshimiwa Ndugulile, kwa kawaida alikuwa anapinga mambo mengi ya ardhi lakini leo anaunga mkono hoja, basi na mimi nianze kwa kuunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo kuna changamoto chache ambazo nyingi tumeshazifikisha ambazo zinahusiana na Mkoa wetu wa Tabora na hasa Tabora Manispaa. Tabora Manispaa sijui niseme ina bahati mbaya au nzuri, lakini kwa ulinzi ni bahati nzuri kwamba tumezungukwa kwa kiwango kikubwa na Kambi za Jeshi. Sasa kumekuwa na mwingiliano mkubwa sana baina ya wanajeshi pamoja na wananchi na hili mara kwa mara nimekuwa nikilizungumzia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na migogoro mikubwa ambayo tayari imeripotiwa mara nyingi, ningemwomba Mheshimiwa Waziri watafute utaratibu wa Wizara ya Ardhi pamoja na Jeshi kwa maana ya Ulinzi ili kuweza kutatua migogoro ile kwa sababu inahatarisha amani. Maeneo mengi ambayo ni ya Jeshi kwa madai yao, wameweka zile beacon ambazo wanazitambua wao, lakini wananchi sehemu nyingi hasa maeneo ya Usule, Kata za Mbugani, Tambukareli, Cheyo, Mtendeni na Malolo wanazo beacon za muda mrefu ambazo walipimiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Jeshi wanapokuja na wao wanasema wana alama zao, hili suala limekuwa na mgogoro wa muda mrefu, naomba Wizara iweze kulishughulikia suala hilo ili wananchi pamoja na Jeshi wasiwe na mgogoro na kwa kuzingatia kwamba Jeshi mara nyingi hawatumii maeneo yale, wananchi wamekuwa wakiyatumia kwa kilimo. Sasa wale wananchi waweze kupewe ruhusa, tunaongelea kilimo, sasa Jeshi eneo kubwa hawalimi kabisa na wananchi wamekuwa wakilima muda mrefu basi watatue hili suala ili wananchi waweze kuyatumia maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo lenyewe sitalizungumzia kwa undani ila kwa kuwa nimesikia hapa pia yupo Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi Dkt. Yamungu, tuna Chuo cha Ardhi pale Tabora Mheshimiwa Waziri cha Ardhi kina changamoto nyingi sana, kuna upungufu mwingi ikiwemo na vitendea kazi. Chuo hiki cha Ardhi ni cha miaka mingi na changamoto zile walimwakilishia Dkt. Yamungu akiwa ni mgeni rasmi kwenye mahafali ya Chuo cha Ardhi yaliyopita ambayo na mimi nilihudhuria, nina imani kama hajamfikishia Mheshimiwa Waziri changamoto zile basi amfikishie rasmi, kwa sababu yuko hapa waliorodhesha changamoto nyingi, basi nisiziorodheshe sasa hivi yeye atampatia ili aweze kuzifanyia kazi.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu nije kwenye hivi viwango maalum wanavyolipa wamiliki wa nyumba na majengo. Tabora Manispaa ndiyo peke yake ambayo imekuwa inalipa Sh.25,000/= kwa mwaka ilikuwa ni flat rate. Tofauti kabisa na Manispaa na Halmashauri zingine ambazo nyingi zilikuwa zinalipa kwa mfano, Morogoro Sh.10,000/=, Temeke Sh.15,000/=; Mwanza Sh.10,000/=; Manispaa ya Songea Sh.12,500/=, lakini Tabora Mjini Sh.25,000/=. Sasa sijaelewa ni vigezo gani pamoja na kwamba kitu kinachotumika wanadai kwenye ile valuation wanatumia ile 0.25 thamani ya nyumba wana calculate kwa hiyo 0.25 kupata thamani au tozo ambayo anayotakiwa kutozwa huyu mmiliki wa nyumba au jengo. Hata hivyo, katika sehemu nyingi imekuwa ni Sh.10,000/=, haijafika Sh.20,000/= kwa nini Manispaa ya Tabora ni Sh.25,000/=? Naomba Mheshimiwa Waziri hilo aweze kuliangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne naomba nizungumzie nyumba zinazojengwa na National Housing. Nia ni njema kwamba waweze kuzikopesha nyumba hizi kwa watu mbalimbali na hasa wanyonge pia ikiwezekana, lakini kuna mchezo mchafu unafanyika kwenye hizi nyumba. Kuna wenzetu ambao wana uwezo mkubwa wa kifedha huwa wanazinunua hizi nyumba wao, wanazinunua kwa wingi na wakati mwingine kwa majina mbalimbali halafu wanakuja kuzipangisha. Sasa naomba wafanye uchunguzi watu wa namna hiyo waweze kudhibitiwa ili kweli lile lengo la kwamba watu wapate nyumba nafuu liweze kutimia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba niongelee hili suala la Wathamini wa Ardhi (Valuers) wamekuwa hawawatendei haki wananchi wengi hasa wanyonge, siyo wote lakini baadhi yao. Wanapofanya valuation, hapa kwenye valuation huwa ndiyo kuna harufu hapa ya rushwa. Unaweza ukakuta kwa mfano kiwanja ambacho labda au nyumba ambayo ingekuwa na thamani ya Sh.50,000,000/= huyu Valuer kwa sababu hajaongea kwa matamshi ambayo angeyataka yeye ana-valuate ile labda kwa Sh.2,000,000/=. Sasa yule mnyonge anashindwa afanye nini kwa sababu huyu mtu wa valuation ndiye anayetambulika kisheria kwamba akifanya valuation basi hiyo ndiyo itafuatwa. Mheshimiwa Waziri naomba hawa Valuers siyo wote lakini baadhi yao siyo waaminifu na eneo hilo lina mambo mengi ya rushwa. Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa kuongelea suala la Sheria ya Mabaraza ya Ardhi Namba mbili (Na.2) ya mwaka 2002. Ni kweli uanzishwaji wake ulikuwa ni wa muhimu kwa sababu kila Wilaya ikiwa na Baraza la Ardhi angalau migogoro mingi ya ardhi itapungua. Naiomba Wizara fedha ambayo inatakiwa kwa ajili ya kuanzisha Mabaraza ya Ardhi kila Wilaya ipelekwe kwa wakati unaotarajiwa ili sehemu nyingi kuwe na Mabaraza haya ya Ardhi kwa ajili ya kuweza kutatua migogoro mingi ya ardhi katika sehemu mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya machache, narudia kuunga mkono hoja na nasema ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia hii hoja. Mimi ni Mjumbe pia wa Kamati hii ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge. Kwanza naipongeza Kamati hii kwa kazi ambazo imekuwa ikizifanya pamoja na ugumu wake na changamoto zake, lakini imekuwa ikifanya kazi bila kumwonea mtu yeyote kama taarifa ambavyo imeweza kusomwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Bunge hili liweze kuelewa Kamati ile ya Maadili ina Vyama vyote, tuko mle ndani Vyama vyote na hatujawahi kupiga kura kutoa hukumu yoyote ile, tumetoa hukumu zote tukiwa tumekubaliana na hii inamaanisha kwamba hukumu zile hazikuwa na upendeleo wa aina yoyote. Kama ingekuwa siyo Kamati ile ya Maadili ambayo Mheshimiwa Naibu Spika unaielewa kazi mnayotuletea pamoja na Mheshimiwa Spika, kusingekuwa na Kamati ile sijui Bunge hili lingekuwaje.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtakumbuka hasa sisi ambao ni Wabunge wageni, Bunge hili wakati tunaanza nidhamu ilikuwa siyo kabisa ambayo Mheshimiwa Mbunge anapaswa kuwa nayo kwa baadhi ya Wabunge wenzetu. Hata hivyo, baada ya mashauri mbalimbali leo hii hata ukiliangalia Bunge lina nidhamu kubwa. Nawashukuru sana Wabunge pia kwa kutuwezesha sisi kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hata unaona hata ukimwambia mtu anayevunja taratibu labda ukimwambia kaa chini, hurudii hata mara mbili, mara tatu, anakaa. Haikuwepo hiyo mwanzoni na nawashukuru pia Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwamba mmeona umuhimu wa kuwa na nidhamu humu ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kwamba hakuna uhuru usiokuwa na mipaka hata uhuru wa kuzungumza kama ambavyo watu wamekuwa waki-quote Katiba kwamba wana uhuru wa kuzungumza. Uhuru wowote ule siyo absolute, kwa maana kwamba siyo timilifu kuna mipaka yake hata katika kuongea, sasa ukiwa umetumia vibaya uhuru huo basi unajikuta unafika mahali ambapo sipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona hata wakati Mbunge mmoja anaongea hapa jana, Mheshimiwa Mbunge mmoja alikuwa anaongea suala ambalo limekatazwa hata kwenye vifungu hivi vya Kanuni zetu huruhusiwi kutumia lugha ambayo ni ya matusi au ya dhihaka hata kwa Mbunge mwenzio, siyo Mheshimiwa Rais tu kama ambavyo kila kitu Mheshimiwa Rais amekuwa over protected siyo kweli, hata kwa Mbunge mwenzio huruhusiwi kwa mujibu wa Kanuni zetu hizi na hasa hiyo ya 64(1)(f) na (g), inakataza kabisa hata kwa Mbunge mwenzio. Kwa hiyo siyo Rais tu hata sisi tunapaswa kuheshimiana. Pia kuzungumza uongo imekatazwa, kila jambo unalozungumza humu basi uwe una ushahidi nalo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, Mheshimiwa Mbunge mmoja hapa amezungumza suala la kwamba Mheshimiwa Rais alimwita Mheshimiwa Lowasa kumrudisha kwenye Chama cha Mapinduzi. Sijaiona hata kwenye clip yoyote kama ambavyo huwa mnatuma clip, je, mtu angekwambia uje Kamati ya Maadili uthibitishe unayo clip hiyo au mtu anaongea tu ili kufurahisha na kujaribu kutaka wananchi waamini hivyo. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge tuwe tunaangalia tunachokizungumza ili msije mkajikuta mnaletwa kwenye Kamati hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama kusingekuwa hata na Code of Conduct unaweza ukaona humu ndani kwenyewe, hivi mavazi ya humu ndani yangekuwaje! Sasa kwa sababu kuna Code of Conduct Waheshimiwa Wabunge wanachagua mavazi ya kuvaa. Hata hizi sheria kama tunavyosema hatuhitaji kumwonea mtu yeyote, tunafanya kazi kwa ajili ya kuweka mambo sawa Bungeni kama ambavyo sasa tumeendelea kufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna baadhi ya watu ni wachochezi wapo humu, lakini Waheshimiwa Wabunge wale ambao wanawachochea wenzao natoa rai tu kwamba jaribuni kuwaangalia wale mnaowachochea, wengine wanachochea anayepewa adhabu ni mwingine, sasa wewe unapata faida gani?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA; Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii nichangie kidogo kwenye hii bajeti ya Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa dakika ni chache sana na mimi nitaongea machache mengi wengi wameshazungumza. Kwanza, naunga mkono hoja asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, naomba kama mimi binafsi au mtu wa maadili nitoe ushauri kidogo. Kuna madeni mengi ambayo yamekuwa yakizungumzwa; madeni ya wakandarasi mbalimbali ambayo yanaongezeka kila siku kwenye sekta ya ujenzi waangalie namna gani watapunguza madeni haya kwa sababu kila siku kuna shida lakini Ofisi ya Waziri Mkuu inafanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Spika, nilisema nitatoa ushauri wa kimaadili kidogo. Ni vizuri kumsema mtu akiwa yupo ili aweze kujibu lakini unapomsema mtu hayupo na hawezi kujibu kunakuwa na mashaka na ndimi mbili huwa si nzuri. Nchi sasa hivi imetulia sana huko nje maana yake wananchi wana imani na Serikali iliyopo ya Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan. Sasa wanaanza kutokea baadhi ya Waheshimiwa wenzetu kuponda vitu ambavyo vilifanywa katika awamu iliyopita, si vizuri. Kama kitu ulikisifia jana, leo ukaanza tena kukiponda wananchi wanachanganyikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, miradi yote hii iliyoanzishwa ndiyo ilitufanya Wabunge wengi turudi leo humu Bungeni nikiwemo na mimi. Unafahamu kwamba Tabora Mjini haijawahi kurudisha Mbunge mara mbili ni mimi niliyesimama hapa Mwakasaka, ni kwa sababu ya mafanikio ya Awamu iliyopita chini ya Mheshimiwa Hayati Dkt. Magufuli pamoja na Mheshimiwa Mama Samia. Miradi ile ile iliyotupitisha leo tunapoanza kuiponda tunawachanganya wananchi.

Mheshimiwa Spika, tusiwe na ndimi mbili na hata kwenye Biblia sijafahamu ni kitabu gani lakini nadhani ni Mithali, Mwenyezi Mungu anasema kheri uwe moto au baridi, ukiwa uvuguvugu utatapikwa maana yake huna msimamo. Tuwe na msimamo, wananchi wana imani na Serikali iliyopo ya Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, tusiwachanganye kwenye miradi ambayo inaendelea. Bahati nzuri Mheshimiwa Samia ana uwezo mkubwa, miradi hii itaendelea na tuna imani kabisa kwamba nchi yetu itasonga mbele. Tuache kuwachanganya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi yangu ni machache tu, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Hotuba ya Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa namwangalia kidogo mwenzangu mmoja Mheshimiwa mmoja hapo nje alikuwa ananiita anasema ninyi CCM mmekuwa timu pongezi kazi yenu kupongeza tu. Sasa nikamwambia mimi kwa upande wangu Tabora au Tabora Mjini nina mambo mengi tu ya kuipongeza Serikali. Kwa hiyo hata kama anaita timu pongezi tutaendelea kuwa tunatoa pongezi kwa yale mambo mazuri ambayo yanafanywa chini ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano Tabora tumebahatika tuna mradi mkubwa wa maji wa zaidi ya bilioni 600 ambao sasa unaendelea; Kiwanja chetu cha ndege kinaboreshwa; alisimama Mheshimiwa Ntimizi hapa aliongelea kile kipande Chaya ambacho kimebaki katika barabara ya kuunganisha kuanzia Itigi mpaka Tabora kwa lami, Mkandarasi yuko anaendelea na kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo sisi Tabora zao la tumbaku kama ambavyo wamekuwa wakiongea wenzangu ni zao la kimkakati. Tulikuwa na matatizo sana ya tumbaku kununuliwa. Mheshimiwa Waziri Mkuu ameshakuja Tabora mara nyingi na matunda yake yanaonekana, tumbaku nyingi imekwishanunuliwa, kwa hiyo naipongeza sana Serikali kwa namna ambavyo inatimiza ahadi zake. (Makofi)

Mheshiimiwa Mwenyekiti, tunazo changamoto kwenye suala la afya. Kwenye suala la afya sisi pale Tabora Hospitali yetu ya Rufaa ya Kitete, Madaktari Bingwa yupo mmoja tu mpaka sasa hivi na tunahitaji Madaktari Bingwa tisa. Kwa hiyo, naiomba Serikali iweze kutupatia Madaktari Bingwa ili hospitali ile iweze kuwa inajitosheleza kwa ajili wagonjwa ambao wanakwenda rufaa Bugando, Muhimbili na sehemu zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tangazo pia lilitolewa Bungeni hapa kuhusu madawa au maduka ya madawa ambayo yanazunguka hospitali zetu na kwamba yangefuatiliwa na pengine kuondolewa kabisa. Kwa mfano pale Tabora Hospitali ya Kitete, imezungukwa na maduka ya dawa ambayo yenyewe dawa karibu zote unapata na imekuwa ni kawaida hata dawa ambazo ni za kawaida wagonjwa wamekuwa hawazipati kwenye hospitali, lakini wanapokwenda pale nje wanapata dawa zile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunajiuliza zile dawa je zinatoka mle ndani au namna gani kwa sababu wale wanao miliki zile dawa au yale maduka ya dawa wengine ni wauguzi na wengine ni madaktari. Sasa naiomba Serikali lile tamko la kufuatilia ule mlundikano wa haya maduka ya dawa yanayozunguka hospitali zetu wafuatilie isije ikawa ndicho chanzo cha dawa kupotea kutoka mahospitali yetu na kupelekwa kwenye pharmacy ambazo zipo jirani na hospitali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la pembejeo. Tabora wengi ni wakulima kama ilivyo sehemu nyingine, lakini mara nyingi pembejeo haziendi kwa wakati. Kwa mfano, mwaka jana wakulima walipata mbolea katika kipindi ambacho ilikuwa sasa na mazao yameshakuwa kiasi ambacho mengine yalishakuwa yameharibika na hata ilipokuwa imekuja mbolea haikuwa na faida kwa wakulima wengi. Kwa hiyo, naiomba Serikali yetu sikivu kuangalia suala hili la pembejeo za kilimo, ziwe zinawafikia wakulima kwa wakati unaostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna suala la migogoro ya ardhi. Migogoro ya ardhi imekuwa ni changamoto nadhani kwa nchi nzima katika sehemu mbalimbali. Hata hivyo, kwa Tabora kwa sababu ilisemekana au ile Tume ambayo ilipita kwa ajili ya kuchunguza migogoro ile bado hatujapata jibu la migogoro ya ardhi hasa kwa Tabora Mjini. Tabora Mjini imezungukwa na Kambi za Jeshi na migogoro mingi ni kati ya wananchi na jeshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Ardhi iliahidi kwamba itaongea na Wizara ya Ulinzi ili kuangalia ni nani hasa alivamia eneo la mwenzake; kwa sababu wananchi wanadai kwa muda mrefu kwamba maeneo hayo ni ya kwao miaka na miaka na Jeshi la Wananchi wanasema kwamba maeneo yale ni yao. Sasa kwa sababu Serikali ilishaamua muda kwamba itangalia upya ramani, haijajibiwa mpaka sasa hivi na mgogoro ule bado unaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naihimiza Serikali kwamba ili kuondoa matatizo ambayo sasa yamekuwa sugu kwenye kata mbalimbali za Jimbo la Tabora Mjini na maeneo mengine, basi wawahishe ule mchakato wa kuangalia upya ramani ili waweze kuweka alama ambazo zitaepusha migogoro ambayo si ya lazima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria. Tulifanya ziara juzi juzi katika Mkoa wa Shinyanga, tulikwenda Mikoa ya Simiyu, Geita na tulikutana na changamoto nyingi. Ukiangalia Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ukurasa wa 62 kuna suala la kesi karibu asilimia 96.3 ambazo zimekwisha, kwa maana kwamba mashauri yake yalishamalizika, lakini uwiano huu ni kwa nchi nzima. Sasa kama ni uwiano kwa nchi nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama ni uwiano kwa nchi nzima kuna sehemu zingine ambazo bado kuna mlundikano wa kesi kutokana na uhaba wa Majaji pia na Mahakimu wa kawaida. Kwa mfano sehemu hizi nilizozitaja; ukichukulia Shinyanga Mjini wanatakiwa Majaji sita lakini kuna Majaji wawili tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule Simiyu yuko Hakimu mmoja ambaye anashindwa kuzimudu kesi zote kwa sababu kuna upungufu mkubwa wa Mahakimu. Sasa kesi nyingi zinarundikana kwa sababu ya upungufu wa Mahakimu na Majaji pia. Kwa hiyo, naomba Serikali iweze kufuatilia hiyo ili hii figure iliyotolewa hapa ya asilimia 96.3 iendane na wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna suala la wenzetu hawa ambao wana matatizo ya uathirika wa UKIMWI kama alivyozungumza mwenzangu mmoja hapa. Nadhani tuwape upendeleo katika pato letu lile la ndani angalau asilimia moja kwenye zile percentage ambazo ni own source katika halmashauri waweze kuchangiwa hawa wenzetu ili kuwawezesha kumudu maisha; kwa sababu wako waathirika ambao kwa kweli bila kusaidiwa hawawezi kujisaidia wenyewe. Nina imani Serikali yangu ni sikivu inaweza ikaliangalia hilo na ikalifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya machache, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye hii Wizara muhimu na nyeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabla ya mchango wangu nianze kuipongeza hii Wizara kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. Wizara ya Ardhi kwa kweli kuna changamoto nyingi, lakini Mheshimiwa Lukuvi na Mheshimiwa Mabula wanafanya kazi nzuri, nawapongeza sana. Hamuiangushi Serikali ya Awamu ya Tano. Pamoja na pongezi hizo, naomba niende kwenye changamoto moja kwa moja ambazo zimekuwa zikiikabili Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya ardhi kwakweli imekuwa ni mingi. Pamoja na kwamba mingine inapungua lakini mingine imekuwa ni ya kawaida. Kwa mfano, tunapoongelea suala la watu kupewa ardhi, watu wawili au watatu au wateja wawili au watatu yaani (double allocation) hili jambo ni la muda mrefu, lakini wanaosababisha hivyo ni hao hao watendaji wetu wa ardhi ambao wameaminiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi wasiwasi au mashaka yangu ni zile hatua wanazochukuliwa hawa watendaji ambao wamekuwa wakisababisha hii Wizara kupata matatizo mengi sana hasa haya ya double allocation. Sioni kama ni sahihi kumuhamisha mtu baada ya kufanya matatizo sehemu fulani anapelekwa kwingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona wangechukuliwa hatua ambazo zitawafanya hata wengine wasiwe na ile kwamba atafanya makosa kama hayo ya (double allocation) halafu anajua kabisa kwamba mimi hapa watakachofanya kama sio kuniteremsha cheo, watanihamishia sehemu nyingine. Hawa wachukuliwe hatua kali kwa maeneo waliyopo ili kuwapunguzia wananchi matatizo haya yanayojitokeza mara kwa mara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna suala hili la wenye uwezo. Wamekuwepo watu mbalimbali ambao wanavamia maeneo ya watu ambao hawana uwezo. Mtu anakwenda, anajenga eneo la mtu ambaye anajua hana uwezo kwa kutegemea kwamba; anasema huyu ataenda Mahakamani na akienda Mahakamani anajua yeye kwamba kwa uwezo wake aidha anaweza kukawiza kesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu kuna mahali inafika mtu anamdhulumu mzee ardhi halafu anaanza kumhesabia miaka. Mathalani, mtu ana miaka kama 60, mtu anasema muache tu aende Mahakamani, akienda Mahakamani huyu hata kabla kesi haijakwisha huyu atakuwa ameondoka. Sasa vitu vya namna hii vinafanyika, naomba Wizara waweze kuviangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nije kwenye wangu wa Tabora na hasa Tabora Manispaa. Katika eneo hili, Mheshimiwa Lukuvi na Mheshimiwa MAbula, wamekuja Tabora mara nyingi, nawapongeza kwa hilo. Migogoro mingi ya ardhi iliyopo Tabora wanaifahamu, lakini ile migogoro mingi pia imesababishwa na watendaji wa ardhi pale Tabora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo naomba lifanyiwe uchunguzi, waporaji wengine wa ardhi ni miongoni mwetu, kwamba ni viongozi tena wengine ni viongozi wa chama ambao nadhani Mheshimiwa Lukuvi anakumbuka alipokuja Tabora hata Mheshimiwa Mabula walikumbana na kitu cha namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa nini basi isifike mahali Serikali ikaanza kufanya uhakiki kama kunavyofanyika uhakiki mwingine. Uhakiki wa wamiliki halali wa viwanja vile. Inawezekana na sioni ugumu kwa sababu kuwatambua watu ambao wamefoji viwanja vile ni kufanya uhakiki. Ningependekeza hicho kwamba ufanyike uhakiki wa maeneo yenye migogoro ili ionekane ni nani hasa wamiliki wa vile viwanja kwa sababu hili tatizo lipo nchi nzima. katika maeneo mbalimbali viongozi wanajitwalia ardhi kwa kutumia vyeo vyao lakini wanaandika majina tofauti tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati viwanja kwa mfano vinagaiwa tuseme kwenye halmashauri au manispaa viongozi wanajitwalia viwanja vingi tu. Mtu mmoja anaweza akachukua viwanja hata 30 kwa majina tofauti halafu baadaye anaanza kuviuza kidogo kidogo kwa bei kubwa ya kuwaumiza wananchi. Sasa kwa nini lisifanyike zoezi la uhakiki kuwabaini hawa ili vile viwanja vingine wanapobainika pamoja na hatua za kisheria kuchukuliwa kwa wao kufoji majina mbalimbali lakini pia kuwapa wale ambao hawana uwezo wa kumiliki hivyo viwanja?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kwa pale sisi Tabora Manispaa tuna bahati mbaya, kwa upande mwingine bahati nzuri kwamba tunazungukwa na majeshi lakini pia tunazungukwa na hifadhi. Kumekuwa na migogoro ya muda mrefu ya ardhi kati ya wananchi pamoja na wanajeshi, kwa maana ya mipaka ile ambayo kwa muda mrefu haijaoanishwa sawasawa, ni nani hasa ambaye anastahili kuwa na eneo lile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, wananchi wamekuwa wakilima muda mrefu, wale ambao wanapakana na maeneo ya majeshi, lakini hivi karibuni imetokea suala la jeshi kudai kwamba yale maeneo ni yao, ambayo wananchi wamekuwa wakilima zaidi ya miaka 40 pale. Sasa naiomba Wizara ya Ardhi kwa kushirikiana na Wizara ya Ulinzi, waweze kufanya haraka zoezi la kupata ramani zile ili kujua ni nani hasa ni mmiliki wa maeneo gani na kwa mipaka gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba hili suala la hifadhi, hifadhi wote tunazihitahiji, wote tunahitaji utalii, tunahitaji kutunza misitu, lakini kuna sehemu kubwa ambayo wananchi wanafanyiwa uonevu. Wako wananchi miaka na miaka kabla hata ya hayo maeneo ya hifadhi hayajatamkwa bayana. Leo hii wanaondolewa maeneo ambayo hawajua sasa watakwenda wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba pia Wizara hii kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii waweze kuona ni wapi wananchi wale sasa haki yao ipo. Nadhani baada ya haya machache ambayo yanajitokeza kwenye suala hili, kama yakifanyiwa kazi nadhani tutaweza kuwa tume-solve hili suala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya machache, naunga mkono hoja.
TAARIFA YA KAMATI YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE KUHUSU SHAURI LA KUDHARAU NA KUDHALILISHA BUNGE LINALOMKABILI NDUGU PROF. MUSSA ASSAD, MDHIBITI NA MKAGUZI MKUU WA HESABU ZA SERIKALI
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru ninaomba niweze kujibu kidogo baadhi ya hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na Mheshimiwa Catherine Magige yeye aliongelea suala la uzalendo. Ni kweli, duniani kote uzalendo kwanza. Nashukuru ameunga mkono Kamati, lakini naomba niende kwenye hoja za Mheshimiwa Mbowe ambaye alianza kwa kusema kwamba Azimio lilikuwa limefanyiwa maamuzi kabla.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii siyo kweli kwa sababu Mheshimiwa Mbowe kwanza ni Mjumbe katika Kamati ya Uongozi na wakati tunajadili ratiba ya kwanza alikuwepo na hata hii ya pili, pamoja na kwamba hii ya pili alichelewa amekuta ndiyo kwanza imeisha, lakini alifika. Ni kwamba hoja hiyo ililetwa kwenye Kamati yetu na Kamati ile wamo pia wa Vyama vya Upinzani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbowe anapoongelea composition, uwiano wa wale Wajumbe wanaoingia kwenye Kamati ya Maadili, huu uwiano umewekwa kwa taratibu na kanuni za Kibunge. Pia tusije tukawa tunajisahau, Chama cha Mapinduzi ndiyo chenye Wabunge wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tusipoangalia hoja nyingine zinazotolewa kwa mtu wa kawaida anayesikiliza anaweza akadhani kwamba hizi Kamati zinapangwa tu. Hizi Kamati zinapangwa kwa uwiano wa Wabunge. Kwa hiyo, siyo rahisi na sioni kama mnaelekea huko, labda kama mnaweza nanyi mkawa na Wabunge wengi kama Chama cha Mapinduzi, pengine uwiano huo utakuwa sawa, lakini kwa hapa ilipo ndiyo kanuni zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Mheshimiwa Mbowe anaposema Kamati ile inakuwa haitendi haki, siyo kweli. Mheshimiwa Mbowe alikidhalilisha kiti pamoja na Bunge na aliitwa kwenye Kamati ya Maadili na Madaraka ya Bunge. Baada ya kumsikiliza hoja zake na kuomba msamaha tulimsamehe. Sasa leo Mheshimiwa Mbowe kama anamtetea Mheshimiwa Profesa Assad ambaye hakuomba hata msamaha na pamoja na kwamba aliambiwa maana ya udhaifu, neno “dhaifu” kwa mtu wa kawaida anavyoweza kulichukulia, bado hakuomba msamaha, anamtetea, hii haijakaa sawa sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, la Mheshimiwa Hassan anasema no one is perfect. Ni kweli, hata Mheshimiwa Profesa Assad sio perfect katika kila jambo. Nashukuru katika hili umetuunga mkono. Sisi tuliliona hilo, lakini unapokuwa ni kiongozi ambaye unaaminiwa na Taifa, hata hayo Mataifa makubwa tunayoyasema ambayo tunayatolea mfano, yamekuwa hayakubali mtu kutoa taarifa za nchi yake nje ya nchi. Mfano ni Wamarekani, wanamtafuta mtu mmoja kama sikosei anaitwa Slowden na bado hajaropoka chochote, lakini wana wasiwasi kwamba kuna taarifa mbalimbali za nchi anazijua, wanamtafuta wamkamate wakati wowote.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine uhuru aliouzungumzia Mheshimiwa Mbowe, ni kweli anapozungumza kwamba Ibara ya 18 ya Katiba imetoa huo uhuru anaouzungumza yeye, mimi nilidhani angeenda akasoma pia na mipaka ya uhuru huo, kwa sababu Waheshimiwa Wabunge hakuna uhuru wowote ambao ni timilifu. Uhuru wowote unaopewa, not absolute, siyo timilifu. Kuna mipaka imewekwa kwenye Katiba hiyo hiyo, Ibara ya 30 kila uhuru una mipaka yake. Sasa mtu akivuka mipaka hiyo, ndio mambo kama haya ya Mheshimiwa Profesa Assad yanatokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Vuma amem-quote Mwalimu, Baba wa Taifa kwamba amewahi kusema, uhuru bila nidhamu unakuwa kama ni wazimu. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wajumbe, kila jambo na hasa jambo ambalo linahusiana na uhuru wa chombo kingine, kuna mipaka yake; Bunge, Mahakama lakini pia na Executive. Hizi kanuni tumejiwekea wenyewe, anayezivunja, ndio ataletwa kwenye Kamati ya Maadili. Siyo kila mmoja anayeletwa kwenye Kamati ya Maadili anapewa adhabu. Kwa hiyo, maneno ya Mheshimiwa Mbowe siyo ya kweli.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine Mheshimiwa tunayemwongelea hapa, Mheshimiwa Profesa Assad alikuwa na nafasi ya kuzungumza yale ambayo alizungumza nje, alikuwa na nafasi ya kuja kuyazungumza hapa kwa sababu anahudhuria vikao vya Kamati zetu mbili. Anayo sehemu ya kuyasemea hayo, lakini siko alikosemea. Anayo nafasi ya kuyasemea, kwa hiyo, uhuru wake aliutumia vibaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Mbowe alisema kikao cha ambacho kimekaa Kamati ya Maadili ni kama kikao cha Chama cha Mapinduzi. Hii siyo kweli, kwa sababu kama nilivyosema mwanzo, wamo pia Wajumbe wa Kamati ambao wanatoka Vyama vya Upinzani.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo yangu, naomba sasa Bunge likubali taarifa pamoja na Azimio.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. DKT. CHRISTINA G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
TAARIFA YA KAMATI YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE KUHUSU SHAURI LA KUDHARAU NA KUDHALILISHA BUNGE LINALOMKABILI MHE. HALIMA JAMES MDEE (MB)
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba niweze kujibu baadhi ya hoja ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge kuhusiana na shauri hili la Mheshimiwa Halima Mdee.

Mheshimiwa Naibu Spika, naanza na Mheshimiwa Masoud, yeye aliongelea zaidi suala la nidhamu katika Bunge kwamba nidhamu lazima iweze kupewa kipaumbele ili sisi tuwe mfano pia kwa wale wanaowaangalia Wabunge na aliunga mkono hoja. Nashukuru na sina la kuweza kuzungumzia zaidi ya hapo, huo ndiyo ukweli wenyewe kwamba nidhamu ni kitu muhimu na ndiyo maana kuna Kamati hii ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia suala la Mheshimiwa Godbless Lema siwezi kulizungumzia kwa kuwa yeye tayari anasubiri kuitwa kwenye hii Kamati hii hii ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge kwa maneno ambayo kayatumia humu ndani ambayo ni kinyume na maadili.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mlinga amezungumzia kwamba tuna viongozi wetu humu mbalimbali upande wa Chama cha Mapinduzi lakini pia na upande wa Upinzani yupo Kiongozi wa Upinzani. Hawa ndiyo wanatakiwa wawe viongozi katika kuelekeza mambo yanayohusiana na maadili kwa Waheshimiwa Wabunge mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia siyo kweli kwamba Wabunge ambao wamekuwa siku zote wanapewa adhabu ni wa Upinzani peke yake. Katika nyaraka/kesi mbalimbali ambazo sisi tumezipitia katika kumbukumbu ya kesi zilizopita (precedents) hata Wabunge wa Chama cha Mapinduzi wapo ambao kwa miaka ya nyuma wamewahi kupewa adhabu na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kwa kusimamishwa vikao mbalimbali akiwemo Mheshimiwa Richard Ndassa ni wa Chama cha Mapinduzi miaka ya nyuma amewahi kusimamishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nizungumzie suala ambalo amelisema Makamu Mwenyekiti, Mheshimiwa Dkt. Ishengoma. Ni kweli ukiangalia mwenendo wa Mheshimiwa Halima Mdee kwa muda mrefu, Kamati kwa kiwango kikubwa imempunguzia adhabu na hasa kwa kuzingatia muda mfupi wa uhai wa Bunge uliobaki. Kwa hiyo, Kamati ile hatukai tu kwa ajili ya kukomoa watu mbalimbali, ndiyo maana nimetoa majina ya Waheshimiwa mbalimbali ambao waliletwa kwenye Kamati hii na wakasamehewa akiwemo Mheshimiwa Aikael Mbowe ambaye ni Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, siyo kwamba inamtia hatiani kila mmoja lakini Mheshimiwa Halima Mdee ameletwa mara nyingi sana. Hata hii adhabu tuliyompa ni kwamba tuliangalia pia na body language yake alivyokuja kwenye Kamati, tunaangalia vitu mbalimbali. Hata yeye alikuwa anaonyesha kabisa hali ya wasiwasi kwanza kutokana na muda wa Bunge uliobaki mpaka ilifika mahali akasema mimi kweli nimekuja tena humu. Hata yeye mwenyewe anaona kabisa kwamba sasa amezidi kuletwa kwenye Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge. Kwa hiyo, adhabu hii tuliyompa kwa kweli ni ndogo lakini pia kuna huruma kama alivyosema Makamu Mwenyekiti kwa sababu tu ya uhai wa Bunge ambao umebakia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Bunge likubali taarifa pamoja na Azimio linalohusu Mheshimiwa Halima Mdee. Naomba kutoa hoja.

MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.8) wa Mwaka 2019 (Toleo la Kiingereza)
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba nianze kwa kuipongeza Serikali kwa kuleta mabadiliko haya ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Namba 8 ya mwaka 2019. Ni kweli toka mwaka 1954 ni muda mrefu tulikuwa tunahitaji marekebisho haya ningeomba nipitie maeneo machache tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba nianze na hili la Sheria ya Mawakili Sura 307 hata kwenye Kamati eneo hili lilikuwa na mambo mengi sana, lakini wakati tupo kwenye Kamati kulikuwa na tatizo la baadhi ya wadau ambao walikuwa wakihoji kwanini kuwe na Sheria ya Uwakilishi, kwa kawaida hawa ma-advocate wanakwenda kwa kura moja moja hata kwenye hiyo General Meeting yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ni kwamba pamoja na mambo ya gharama hata kama serikali haichangii bado ile fedha inahitajika kwenye shughuli zingine. Uwakilishi siyo kwenye vyama tu hivi au TLS peke yake, hata sisi kama vyama vya siasa hatuendi wote kwenye mikutano yetu mikuu, uwakilishi upo siyo kwa TLS peke yake, kwa hiyo, suala kwamba TLS labda kuna ajenda labda imefichwa hiyo kitu sidhani kwamba ni sahihi. Lakini pia serikali imeridhia mapendekezo mengi ya kamati ambayo yanaonekana kwenye Jedwali la Marekebisho, kwa hiyo, naipongeza sana Serikali kwa kuzingatia hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuonesha kwamba Serikali haina nia mbaya na Muswada huu kwenye marekebisho ya sheria hizi ukienda kwenye Sura 16 ambayo inarekebisha kifungu cha 138(c) cha kuwalinda watoto wa kiume kwa kawaida sheria ambayo ipo ilikuwa ni ya mtoto wa kike, hapa tunaongelea mtoto wa kiume chini ya miaka 18, wengine maarufu wanaita vi-ben ten, wapo kwenye sheria hii, kwamba sheria iwepo kwa sababu tulikuwa hatuongelei chochote. Kweli kuna wavulana wanakuta wana miaka 16, 17 wanadhalilishwa na mambo haya ya kujamiana na mambo mengine, haikuwepo sheria ya kuwalinda. Sasa Serikali imeleta sheria hii ya kuwalinda watoto wa kiume wa namna hiyo, naipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna Ibara ya 13 ya Tasnia ya Maziwa lakini pia Ibara 38 ya Tasnia ya Nyama tulikuwa tunachanganya kidogo kwenye zile bodi tulijaribu kuuliza kwanini Bodi hizi Mwenyekiti wao atokane na mapendekezo ya Waziri wa uteuzi wa Waziri kwanini bodi hizi zisiwe kama bodi zingine ambazo Mwenyekiti wake anateuliwa na Mheshimiwa Rais, lakini Serikali ilitoa maelezo mazuri kwamba hawa watakuwa ni washauri zaidi na siyo kama kwenye bodi zingine.

Kwa hiyo, naishukuru Serikali kwa mapendekezo hayo na sisi kama Kamati tuliridhia na naomba niseme kwa hoja hizi chache naunga mkono hoja ya mapendekezo haya kwa asilimia mia moja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nami nafasi ya kuweza kuchangia hii hotuba ya Makadirio ya Bajeti kwa Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kabla sijaanza ili nisije nikasahau, naomba kwanza kuunga mkono hoja ya makadirio katika Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kuipongeza Serikali kwa miradi mbalimbali ambayo imekuwa ikiendelea hapa nchini. Miradi mingi kwa kweli ambayo hatukutegemea miaka ya nyuma, sasa inakwenda vizuri. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na suala la kilimo. Tunaposema uchumi wa viwanda Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia ni kutilia kwanza mkazo kwenye suala la kilimo. Bila kilimo kwa kweli hata hayo meendeleo ya uchumi wa viwanda itakuwa ni ndoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Waheshimiwa Mawaziri katika sekta hii, lakini kilimo kina changamoto zake. Kwa mfano, ukiangalia sasa hivi kuna miradi hii ambayo iko chini ya Wizara, miradi kama ya greenhouse au vitalu nyumba. Tumefanya ziara tumeona baadhi ya hii miradi. Kwa kweli katika kilimo Wizara hii niwapongeze sana Waheshimiwa Waziri, wanafanya vizuri sana. Mheshimiwa Jenista Mhagama, Mheshimiwa Angellah Kairuki pamoja na Naibu Mawaziri wenu, Mheshimiwa Ikupa na Mheshimiwa Mavunde, tumeona hiyo miradi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli miradi hii inakwenda vizuri na hasa ajira kwa vijana. Vijana wengi sana wameajiriwa katika miradi hii ya vitalu nyumba na wanafanya vizuri katika kujiingizia kipato. Tatizo linalojitokeza ni kwamba hii miradi hasa ya vitalu nyumba bado ni ghali. Mathalan, kama unataka upate kitalu nyumba cha mita 30 kwa nane unahitajika uwe na shilingi milioni 12 mpaka 15 kitalu nyumba kimoja. Sasa kwa mtu wa kawaida kuwa na uwezo huo ni vigumu. Naiomba Wizara katika eneo hili ione uwezekano wa kupunguza hi gharama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vifaa vingi kwa jinsi tulivyokuwa tunahoji vinatoka Kenya, vichache ndiyo vinatoka hapa Tanzania na hasa zile wavu zake kwa ajili ya kuezekea vitalu nyumba vinatoka nje kwa mujibu wa maelezo ya wataalam. Sasa naiomba Wizara, kama inawezekana, kukawepo na uwezekano wa kuweza kupata hizi malighafi hapa hapa Tanzania ili kila mmoja aweze kumudu kununua au kutengenezewa hivi vitalu nyumba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Sekta hiyo hiyo ya Kilimo naomba nisome eneo dogo kwenye ukurasa wa 27 kwenye kitabu cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Linasema: “upatikanaji wa chakula kwa mwaka 2018/2019 umeendelea kuimarika kutokana na hali nzuri ya mvua katika maeneo mengi ya nchi.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, mashaka yangu hapa, data hizi sijui zimetoka wapi? Kwa hawa wataalam wetu, tumetembea kidogo Kamati ambayo mimi nipo ya Katiba na Sheria, maeneo mengi bado hali ya chakula siyo nzuri. Maeneo mengi ambayo tumetembea, mazao mengi yamekufa, hata hapa tu jirani Gairo mahindi mengi ukiangalia na mazao mengi yalifika maeneo yanataka kubeba, lakini sasa yanakufa na maeneo mengi. Sasa hii hali nzuri, sijui, labda kuna Mikoa ambayo mimi sijatembea inawezekana kuna hali nzuri ya mvua. Ila mimi sijaona sehemu nilizotembelea au tulizotembea nikaona kuna ongezeko au kuna mvua ambazo ni nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee suala la ulinzi kwa wanawake na watoto ambapo katika kitabu hiki ni ukurasa wa 59. Kuna changamoto kubwa hapa. Juzi juzi tulikuwa Mkoa wa Mara, tuliufanya ziara ya kukagua miradi ya Makahama. Tulipomtembelea Mkuu wa Mkoa, Ndugu Malima alitupa report moja ambayo siyo nzuri kabisa kuhusiana na usalama wa wanawake na watoto. Kuna ongezeko kubwa sana la udhalilishwaji wa wanawake na watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, pale Mara, tulikuta kesi ambayo kuna mtoto wa miaka kama minne alibakwa lakini siyo kubakwa tu, akaambukizwa na UKIMWI baada ya kwenda kupimwa. Mama wa mtoto yule baada ya kuona kesi haiko vizuri, akapewa shilingi milioni mbili akawa anakwenda kuomba kwamba kesi isiendelee kwa sababu mtoto wake tayari ameshaharibiwa na hakuna kitakachoweza kubadilika. Hii inaonyesha kabisa kwamba bado wananchi wengi na hasa akina mama hawajapata elimu ya kutosha kuona namna gani wanapaswa kulinda watoto wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, udhalilishaji huo upo wa watoto lakini hatua zinachukuliwa. Sheria zetu bahati nzuri na wewe ni Mwanasheria; Sheria ya ubakaji haijakaa vizuri. Hii sheria kuna umuhimu wa kuipitia upya, kwa sababu ili idhihirike kwamba mtu alibaka, zile elements za kuhakikisha mtu atiwe hatiani kwa kubaka ni ndefu na siyo rahisi kuithibitisha. Nadhani hii haijakaa vizuri, inatakiwa ifanyiwe marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende upande wa Mahakama. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria. Tumekagua miradi mingi ya Mahakama, lakini kuna sehemu nyingi sana ambazo bado zinahitaji kuwepo na Mahakama. Sehemu nyingi Mahakama wanapanga, zile ambazo kunakuwa na mashauri mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tulikwenda Mkoa wa Arusha tukaenda mpaka kule Longido. Kuna sehemu tulifika yale maeneo ya mpakani pale, bado wanakodi kwenye sehemu za watu. Ile katika utoaji haki kunakuwa na tatizo kidogo, kwa sababu kama Hakimu au Mahakama zipo kwenye nyumba za watu, hata utaoji haki unakuwa hauko sawa sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miradi hiyo ya Mahakama, kuna miradi mingi ambayo sasa inakamilika; na hili nimewahi kulizungumza. Shida inayokuja ni kwamba fedha zile za kuwalipa Wakandarasi sehemu nyingine bado hazijafika. Sasa wasiwasi wangu ni kwamba Mahakama ambayo inasimamia haki pale itakapotokea kwamba pesa hazijapelekwa kwa wakati, Mahakama hiyo hiyo nayo itashitakiwa. Sasa hili jambo halijakaa sawa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye hifadhi ya jamii. Mifuko yetu mingi imekuwa ikifanya vizuri, lakini kuna changamoto. Baadhi ya mifuko hii kuna kadi kwa mfano za NHIF hospitali nyingine zinakataa kupokea. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mwakasaka.

MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi hii ambayo nimeweza kuipata kwa ajili ya kuchangia hii hoja iliyopo mbele yetu ya hotuba ya Mheshimiwa Rais. Nami kama wengine walivyoanza naomba pia nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa hotuba yake nzuri ambayo imejenga na ina dira ambayo ni muhimu sana kwa maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nina hoja chache sana kwa sababu nyingi zimeshazungumzwa na waliotangulia, nitachangia kidogo kwenye kilimo kwa sababu naona wengi wameongelea kilimo; upotevu wa baadhi ya mazao ya kutoka kwenye kilimo yameongelewa zaidi, sehemu za kuhifadhia kwamba ni moja ya sehemu inayofanya kuwe na hiyo harvest loss ya 30 percent to 40 percent ambayo imetajwa kwenye ukurasa wa 14 wa hotuba ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, pia nadhani mbegu zinachangia sana katika upotevu wa mazao. Kwa mfano kwenye mahindi kuna mbegu ambayo ipo sasa hivi ambayo hata kama imekomaa yule mkulima akichelewa kidogo tu kuivuna anakuta kwamba tayari yale mahindi anavuna yakiwa yameoza, lakini ile ni ubora wa ile mbegu. Wizara hii ya Kilimo inafanya kazi nzuri sana lakini kwenye suala la mbegu bado kuna changamoto kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la reli; ni kweli sasa hivi reli inajengwa kwa kasi kubwa na hasa SGR, lakini pia tunahitaji ile reli ya zamani kuendelea kuwepo kwa sababu nafahamu kwamba hii reli ambayo sasa hivi ni ya kisasa hata kama itakuwa imekamilika, bado kuna shughuli za usafirishaji zitaendelea kuwepo kwa kutumia reli ya zamani. Kwa hiyo kuna umuhimu sana wa kuimarisha reli ile ya zamani na hasa maeneo ambayo tumekuwa kila siku tukiyasikia miaka na miaka, maeneo ya Kilosa yale nadhani ni Gulwe na maeneo mengine ya Godegode, kila mara reli inachukuliwa na maji na inaigharimu Serikali hela nyingi sana.

Mheshimiwa Spika, sasa nadhani wakati umefika Serikali ibuni namna gani itafanya hata kama itatumia fedha nyingi sana kuinua matuta makubwa kwenye hii reli ya zamani ambayo ile treni itapita juu kabisa isikutane na yale maji, kitu ambacho kitakuwa sustainable, sio hii ya kila siku zinapelekwa billions za fedha pale, lakini kila mwaka mvua ikija eneo lile reli inachukuliwa.

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee suala la miradi ambayo Mheshimiwa Rais amekuwa akiisimamia ambayo kwa kweli hata Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi ufanyaji kazi wa Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli na miradi ambayo imeibuliwa na inaendelea imetubeba sana hata kwenye uchaguzi uliopita.

Mheshimiwa Spika, hii miradi ni endelevu, sina uhakika kama miradi yote hii kwa mfano ya nishati ile ya Bwawa la Mwalimu Nyerere kule lakini nimetoka kuzungumzia SGR na miradi mingine mikubwa; miradi hii sijui kama inaweza ikaisha yote kabla Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, hajamaliza kipindi chake. Kwa kuwa Mheshimiwa Rais anaiheshimu sana Katiba na ameshazungumza kwamba yeye hatoongeza kipindi, ataondoka, sasa yeye yuko very strong lakini ile miradi iko protected namna gani, ile miradi mikubwa aliyoianzisha itaendelezwa kinamna gani?

Mheshimiwa Spika, hapa hoja yangu ni kwamba tunatakiwa tujifunze kutokana pia na matukio ya wenzetu. Hivi karibuni baada ya uchaguzi wa Marekani, siku ya kwanza tu Joe Biden alisaini executive orders za ku-revise vitu alivyovifanya Trump, the same day ambayo aliapa alisani. Kwa hiyo ina maana yeye katika kipindi chote kuna vitu ambavyo alikuwa hakubaliani navyo, alikuwa anasubiri tu akiingia avibadilishe.

Mheshimiwa Spika, sasa naongelea hili kwenye miradi mikubwa ambayo Mheshimiwa Rais ametuanzishia na inakwenda vizuri na ni muhimu sana kwenye kujenga uchumi wa nchi yetu; iko protected namna gani? Ili asije akaingia mtu, maana yake kwa sasa Mheshimiwa Rais yuko madarakani kila mmoja anam-support, lakini mioyo yetu tunaifahamu wanadamu, kubadilika ni wakati wowote. Hatujui, je, miradi hii itaendelezwa akiondoka? Sasa mimi pendekezo langu hapa ni kwamba ikiwezekana ziimarishwe institutions ambazo zitalinda hii miradi ili isije ikaguswaguswa na wengine watakaokuja mpaka iishe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukizungumza hivyo unaigusa kidogo Katiba, lakini nimewahi kusema hapa kwamba Katiba sio Msahafu au Biblia, hata Mheshimiwa Rais wakati anaingia nakumbuka kwenye hotuba yake ya kwanza alipokuja hapa aligusia Katiba na hakuna mahali aliposema kwamba labda Katiba ile haifai. Labda ninukuu kidogo kwenye ukurasa wa 12 wa Hotuba ya Mheshimiwa Rais ya mwaka 2015; naomba ninukuu, anasema; “Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la mchakato wa Katiba Serikali yangu imepokea kiporo cha mchakato wa Katiba ambao haukuweza kukamilika katika Awamu iliyopita kutokana na kutokamilika kwa wakati kwa zoezi la uandikishaji wapiga kura.

Anaendelea, anasema; napenda kuwahakikishia kuwa tunatambua na kuthamini kazi kubwa ya kizalendo iliyofanywa na wananchi walioshiriki hatua ya awali ya ukusanyaji wa maoni kuhusu Katiba mpya. Pia tunatambua kazi nzuri ya Tume ya Marekebisho ya Katiba na Bunge la Katiba lililopita lililotupatia Katiba inayopendekezwa. Tutatekeleza wajibu wetu kama ulivyoainishwa katika Sheria ya Marekebisho ya Katiba; napenda mtuamini hivyo.”

Mheshimiwa Spika, naomba ili miradi hii asije akaichezea atakayekuja tuangalie utaratibu, hata kama utakuwa ni wa Azimio la Bunge.

SPIKA: Mheshimiwa Mwakasaka.

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, naam!

SPIKA: Hii ajenda ya sijui nani ataondoka, nani atakuja siipendi sana kwa sababu tunaishia kuwatia hofu wananchi; tuamini Mungu ni mwema na tupo na Rais yupo. (Makofi)

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, mimi hoja yangu hapo ni kwenye namna gani tutailinda hii miradi ili isije ikaishia njiani. Ndiyo maana nilitoa mfano huu wa Marekani, kwamba kwa mfano Trump angekuwa amepewa wigo mpana wa kugusa vitu vingine, maana yake aligusa vidogovidogo tu, zile executive orders, Biden akaweza kuzibadilisha, lakini Trump hakuwa mtu wa kawaida, lakini kuna vitu alizuiliwa kwenye Katiba asiviguse. Kwa hiyo, maana yangu hapa ni kuzi-strengthen institutions kwa mfano Mahakama na Bunge.

Mheshimiwa Spika, leo kwa mfano Bunge tukiazimia hapa kwamba miradi fulani ambayo ni ya kimkakati hata likija Bunge lingine isibadilishwe au isisimamishwe na kama itakuwa iko kwenye Katiba yule mtu hatogusa hii ndiyo concern yangu. Kwa sababu hii ni legacy kubwa Mheshimiwa Rais atakapoondoka ataiacha, miradi hii aliyoianzisha ni very productive kwenye economy lakini…

SPIKA: Yaani hoja yako naielewa, tunaielewa vizuri sana.

MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru.

SPIKA: Kwa mfano Makao Makuu ni Dodoma, hatutarajii tena aje mtu mwingine aseme ana Makao yake Makuu Sumbawanga au mahali pengine.

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, iko protected wapi? Akija mtu akisema anataka kurudisha Dar es Salaam?

SPIKA: Ahsante sana, bahati mbaya sasa na muda nao umekuwa…

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naunga mkono hoja.
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kupata nafasi hii kuchangia Maazimio yote mawili. Ni kweli tumepata msiba mzito sana kwa nchi lakini pamoja na mataifa mengini, ni pole kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan lakini pamoja na sisi sote.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kawaida watu wakipatwa msiba hata katika familia zetu ni lazima watayumba sembuse msiba mkubwa kama huu ulioupata taifa, ndiyo maana wengine wameanguka, wengine walikosa matumaini, ni kawaida misiba inapotokea. Pia na matendo ya aliyetutoka, matendo ya Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ambayo amelitendea Taifa hili hasa katika nyanja za maendeleo, miradi mingi imetajwa pamoja na kudhibiti mapato na matumizi ya Serikali, ndicho kitu ambacho Watanzania wengi sana waliweza kulia na kunguka.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kunukuu maneno ya Mheshimiwa Rais Kenyatta, Rais wa Kenya, wakati amekuja kutoa rambirambi na salamu za mwisho alimuambia Mheshimiwa Rais mama Samia Suluhu Hassan kwamba hata wao Kenya wanaona Mheshimiwa Rais hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ameshafungua njia. Kwa hiyo, kazi yetu sisi ni kufuata njia ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi sina mashaka yoyote na mama Samia Suluhu Hassan ambaye ni Rais wetu wa sasa. Tumeshaanza kuona kwa vitendo namna gani ameanza kazi. Msiba kwa sasa tunao kwa siku zile 21 lakini na kazi zinaendelea. Nampongeza sana Mheshimiwa mama Samia Suluhu Hassan kwa jinsi alivyoanza kufanya kazi zake. Ameanza kidogokidogo kutusahaulisha hata yale machungu na mashaka ambayo watu walikuwa nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sipendi sana kuongelea huyu ni mwanamke, huyu mwanaume, napenda sana kuangalia utendaji wa kazi. Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ameanza kazi vizuri sana kwenye kikao kile ambacho kilikuwa cha kupokea ripoti ya CAG na wengine walitajwa kidogo baada ya kusomwa ile ripoti siwezi kusema aliondoka na mtu lakini kuna kitu alikiona hakijakaa sawasawa haraka sana aliweza kuchukua hatua na haya ni matarajio ya wananchi wengi katika utendaji wa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, mara nyingi sana vitu vinavuja kwa viongozi mbalimbali hasa katika kazi za utendaji, kitu kinaweza kikawa ni siri lakini kinavuja. Leo hii watu waliongelea watu wa mitandao hapa, kuna mmoja akamtaja Kigogo na wengine, kwa mara ya kwanza kina Kigogo leo hawakujua hata jina ambalo litaletwa humu. Walitaja majina mbalimbali ambayo wanayajua wao siye hatukuliona humu. Pia nikipongeze Chama changu cha Mapinduzi katika hili kwa sababu Mheshimiwa mama Samia Suluhu yeye ndiye Mwenyekiti wa Chama chetu cha Mapinduzi mpaka tunaingia humu hatujui jina ni la nani litakuja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan ameanza vizuri mama yetu tuendelee kumuombea. Kazi hii ni ngumu na ni nzito halafu imekuja ghafla, sisi tuendelee kumuombea ili aweze kufanikiwa katika majukumu yake na aweze kuliongoza Taifa letu vizuri na mimi sina shaka hata kidogo na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba niunge mkono Maazimio yote mawili kwa asilimia mia moja, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala Za Mikoa Na Serikali Za Mitaa
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii ya TAMISEMI. Kwanza nianze kwa kusema naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja nisije nikasahau.

Mheshimiwa Spika, kilio kikubwa kila mahali kwa kweli ni TARURA na waathirika nadhani ni sisi wote Wabunge ambao tupo humu. Nilikuwa na wazo moja, hivi haiwezekani kuunganisha Wakala wa barabara TANROADS na TARURA? Maana yangu ni kwamba wangeunganishwa hawa halafu labda Waziri akawa mmoja na watendaji kama Makatibu Wakuu wakawa tofauti ili center ya fedha iwe moja kwa ajili ya ufanisi wa hii TARURA.

Mheshimiwa Spika, maana yake TARURA kwa kweli bajeti yake pamoja na kwamba imetengwa, lakini bado ni ndogo ukilinganisha na matatizo ya TARURA yaliyoko kila mahali. Kwa mfano, Tabora tunaitwa Toronto; ni pale mjini. Ni kweli Tabora ukitelemka usiku ni kama Toronto kweli, lakini ni mjini. Ukienda vijijini hali ni mbaya, barabara ni mbaya kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala la walimu. Walimu wengi wamejaa mijini na hasa kwenye Shule za Msingi. Wengi wamejaa mijini na shule za mjini zimefurika. Vijijini kuna shida sana ya walimu kukaa. Sasa najiuliza ni kwa nini? Moja ya sababu ni mazingira yenyewe ya maeneo ya vijijini ambayo walimu wanakimbia kukaa huko. Nilikuwa naishauri Serikali iangalie ni njia gani mbadala watafanya kuweza kuwashawishi walimu wapende kukaa vijijini kama ambavyo wanakaa mjini. Vinginevyo huu wimbo wa upungufu wa walimu vijijini utaendelea kuwepo.

Mheshimiwa Spika, pia kwenye vituo vya afya kuna juhudi kubwa zinafanyika, nyingine ni za wananchi wenyewe kujitolea kujenga vituo vya afya. Hali bado siyo nzuri, nadhani ni katika nchi nzima ingawa kwa mfano Tabora tunacho Kituo cha Afya cha Maili Tano; kituo kile, kile chumba chake cha upasuaji theater kuna kitanda tu ambacho alitoa mdau mmoja. Hakuna vifaa vingine vyovyote vile vya kuwezesha kile kituo kiweze kufanya kazi. Kwa hiyo, naomba Wizara iweze kutusaidia katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, lingine kwa idhini yako, nimejaribu kuangalia kwenye kanuni kama ningeweza kuomba mwongozo kwenye kanuni, nimeona siyo jambo ambalo limetokea leo, lakini kwa idhini yako hata hii Wizara naomba uniwezeshe au unipe ruhusa niweze kuchomekea jambo. Kuna vijana wale ambao wamefukuzwa, walikuwa wanajenga Ikulu, wapo kama 854. Vijana wale walikuwa miongoni mwa wale 2,400.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mkuu wa Majeshi ameshatoa ruling ya vijana wale kuondolewa au kufukuzwa, maana yake wamesharudishwa makwao. Nilikuwa na ombi, siyo kwamba naunga mkono vitendo ambavyo wamefanya wale vijana vya kutaka kugoma, lakini naangalia pia impact yake kule walikokwenda kwenye maeneo yao na sehemu mbalimbali. Hawa vijana wamefanya kazi kwa miaka karibu mitatu na kweli waliahidiwa ajira na Mheshimiwa Rais ambaye sasa ni Hayati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninahisi ni pamoja na mkanganyiko wa mawazo. Kwanza kwa kuondokewa na Mheshimiwa Rais, lazima watakuwa walichanganyikiwa. Walisahau kwamba na Mheshimiwa Rais ambaye yupo sasa majukumu yale atayatekeleza kama kawaida. Nadhani iliwachanganya; nahisi, mimi kama Mwakasaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nawaombea vijana hawa kwa Amiri Jeshi Mkuu ambaye ni Mama Samia Suluhu Hassan, kama wanaweza kusamehewa, ni kweli wamefanya jambo ambalo kijeshi wanaita ni uasi, walitaka kuandamana, lakini tuangalie na fate zao wenyewe na familia zao wanakoenda. Namwomba sana Mheshimiwa Rais kama itampendeza kuwasamehe vijana hawa wamejitolea sana kujenga Ikulu yetu na nina hakika waliko wanajutia kile walichotaka kukifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii ya Mawasiliano. Wenzangu wamechangia zaidi kwenye maeneo mengi ambayo ni mazuri lakini mimi nitachangia katika maeneokama matatu. Kwanza nianze kwa kuipongeza Wizara hii kwa namna ilivyoweza kudhibiti hasa wizi unaotokana na fedha ambazo zimekuwa zikiibiwa kwenye simu za kimataifa. Naipongeza sana Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Wizara imeweza kudhibiti kwa kiwango kikubwa wizi unaotokana na mitandao. Wizi wa ndani kwa sasa hivi umeongezeka kwa kiasi kikubwa na kwa sababu kuna TCRA vile vitengo vya Cibber crime vina uwezo wa ku-tress hawa wezi. Kwa sababu sasa hivi mtu anakuibia kama alivyosema mchangiaji nadhani alikuwa ni wa pili. Watu wanaiba kwa kutumia mitandao na zile simu zinajulikana na wale watu wanaendelea kutumia zile simu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano nikisikia Tigo wamepiga wameniambia hapa ni customer service huwa nakata pale pale sisikilizi chochote, kwa sababu mimi ni mmoja wa wahanga. Nilipigiwa customer service ya Tigo walivyoniambia tu ni customer service nikawaambia kwamba nitawaaminije kama ni ninyi? Wakanipa data zangu zote ambazo nimefanya ile miamala ya mwisho. Kwa hiyo nikawaambia hakuna shida, wakaniambia tumekuongeza kutoka kutuma shilingi 3,000,000 sasa utatuma shilingi 5,000,000 kuna ujumbe unakuja hapo utabonyeza okay. Ujumbe kweli ulikuja nilipo bonyeza okay nikaambiwa nimetuma shilingi 711,000 na kila kilichopo nikabaki na zero balance.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninavyoamini ni kwamba inawezekana hawa wengine pia ni watumishi wa mitandao hii au ni wale ambao wanafundisha wenzao namna ya kutuibia. Wasiwasi wangu ni kwamba inaweza ikafika mahali kwa advancement hii ya watu wa mitandao, unaweza ukajikuta hujafanya transaction yoyote lakini huko tunakokwenda unaweza ukajikuta unaangalia balance yako kwenye simu hakuna senti tano. Kwa hiyo naishauri Wizara awa wenzetu upande wa polisi ambao tunaambiwa kwamba ndio tuwe tunaripoti tunapotapeliwa, wawe karibu sana na watu wa TCRA ili waweze ku-trace hizo namba ambazo zinafanya wizi huo wa kimtandao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine hili ni la kiusalama mimi na kerwa sana, unapiga simu yako na hili ni mitandao karibu yote. Unapiga simu, kabla haijaanza kuita wewe unapewa matangazo, simu yako inaunganishwa, bonyeza sijui, hash sijui, yanaanza matangazo halafu simu ndio inaita. Sasa mimi najiuliza kama ulikuwa unapiga simu ya emergency labda mtu kavamiwa labda na majambazi,
anapiga simu ili labda Polisi wapokee ile simu, yanaanza matangazao yao ambayo sisi hatujawaomba kama tunataka hayo matangazo kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake wewe wakati unasikiliza matangazo yale, unaweza ukapata hasara, kwa nini wasiendelee na matangazo yao kwa mitindo mingine, lakini mteja yeye akipiga ile simu iite moja kwa moja kuliko kuikawiza kwa sababu ya mambo ya kiusalama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Minara ya Simu; miji inaendelea sana, kwa mfano mimi nime-experience kitu kimoja na ni wengi hapa Dodoma na sasa muda mrefu kunakuwa na shida ya simu zetu wenyewe either kupiga au hata kupatikana. Nahisi ni conjunction ya mitambo yenyewe, yaani kwa maana ya minara. Wakati mji kama Dodoma haujawa Jiji, minara ilikuwa ni hiyo hiyo iliyopo na kama imeongezeka ni michache sana. Sasa matokeo yake kunakuwa na foleni kubwa sana ya simu na meseji. Unaweza ukatuma meseji leo ikawa delivered kesho. Pia unapopiga simu kunakuwa na shida ya kupatikana kwa simu. Kwa hiyo, nawaomba Wizara waweze kuongeza minara hii ya simu ili mawasiliano yaweze kuwa mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, naomba sana Ndugu yangu Waziri Ndugulile, jiografia ya Tabora anaijua, kwa mfano, Jimbo langu la Tabora Mjini linaitwa mjini tu, lakini lina vijiji 41. Vijiji vingi havina mawasiliano ya simu, ukienda kwa mfano, Kata za Ndevelwa, Uyui, Kabila, Ntarikwa, Tumbi hizo ni kata za nje, ukienda Ikomwa ambayo inapakana na Nzega kule mawasiliano ya simu ni magumu sana. Hata hivyo, pale pale mjini eneo la Kipalapala ambapo halizidi kilometa mbili, kuna shida ya mtandao wa simu. Kwa hiyo naomba ndugu yangu Ndugulile atufikirie kupeleka minara mingine ya simu katika maeneo yale ili mawasiliano yaweze kuwa mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja. (Makofi)
Hoja ya Dharura kuhusu Mikopo ya Elimu ya Juu Nchini
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii muhimu. Nianze kwa kusema naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Ezra kuhusiana na watoto wetu ambao wanakosa mikopo.

Mheshimiwa Spika, kama muda wa saa moja tu uliopita nilikuwa naongea na Mheshimiwa Venant wa Jimbo la Igalula. Juzi jumapili nilikuwa natoka Tabora nimepita pale nikasimama, kuna mgahawa fulani nikasimama. Nikakutana na suala kama hili hili ambalo tunajadili hapa, kuna mtoto amefaulu vizuri pale anakwenda Mzumbe. Sasa nilikuwa namsimulia na michango iliyopita pale nami ni mmoja wa waliochanga pamoja ya kwamba nilikuwa on transit. Ni mtoto wa kike ambaye na yeye amekosa mkopo na hajui kama atapata mkopo na amefaulu viuzuri sana.

Mheshimiwa Spika, huwa najiuliza kuna ile wanasema unauziwa mbuzi kwenye gunia. Hii Bodi ya Mikopo imekuwa ikitoa takwimu nyingi sana za namna wanavyokopesha wanafunzi mbalimbali. Vilevile tukienda kwenye uhalisia hasa vijijini wanafunzi wengi waliofaulu vizuri wanakosa mikopo hiyo. Sasa sijui huu utoaji wao wanaangalia vigezo gani? Sawa wanasema ufaulu na vitu kama hivyo, lakini hawa wanaofaulu wengi wanakosa mikopo.

Mheshimiwa Spika, hii inakatisha tamaa sana. Tume-promote sana watu kusoma, kuna shule mpaka kwenye kata sasa zimekuwa promoted watu wanasoma kwenye kata. Watoto wakike na hasa vijijini, vijiji kama vya kule kwetu kanda ya ziwa ambako watoto wengi wa kike walikuwa wanaolewa kabla ya umri wao, kwa sabbu walikuwa hawaendi shule. Sasa tumewa-promote wasome na kweli wanasoma na wanafaulu kweli, lakini hawapati mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ni nini maana yake? Tunaanza kuwajengea tena ile tabia ya kuanza kurudi kulekule ambako sasa wazee watakuwa wanasema sasa hiyo shule yenyewe ina faida gani kwa sababu hata sasa mwanangu ukifaulu uwezi kwenda kokote? Kwa hiyo tunaanza tena kuwakatisha tamaa sisi wenyewe kwa kukosa utaratibu mzuri wa kuwapa mikopo. Hizi takwimu za juzi ambazo tayari sensa inaonyesha akinamama wako wengi zaidi, akinababa tuko wachache. Kwa maana nyingine muda sio mrefu nadhani akinababa watakuwa bidhaa adimu sana, kwa mujibu wa takwimu za sensa.

Mheshimiwa Spika, sasa watoto wa kike hawa ndio watakuwa wengi, ambao tunatakiwa tuwalinde vizuri kwa sababu huko mbele kwa data hizi, wapo watoto wa kike ambao watakosa hata kuolewa, lakini sasa wakose hata kazi au wakose elimu? Bora sasa hata wakipata elimu, elimu hiyo itawasaidia hata kama atakosa mwenza wake huko mbele, lakini ana kazi yake nzuri, huyu mtoto wa kike atakuwa yupo protected. Kwa hali hii tunayokwenda nayo sasa hivi si nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna malalamiko na hasa vijijini kwamba wamekuwa wakipewa upendeleo zaidi watu ambao wapo mijini, watoto ambao wapo mijini na ambao pengine ndugu zao wana uwezo ndiyo wamekuwa wakipata mikopo, malalamiko haya yapo. Sasa Bodi ya Mikopo wanapotoa taarifa zao, basi ikiwezekana watupe na za vijijini kwamba vijijini ni watoto wangapi ambao walikuwa wana-qualify mikopo, wameweza kupewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nazungumza hivyo kwa sababu malalamiko haya ya kwamba mijini na wale ambao wana uwezo watoto wao ndio wanapewa mikopo, itatusaidia sana kama Bodi ya Mikopo itakuja na data za wale wa vijijini, watoto wa mtu masikini kabisa ambao wameweza kupata hiyo mikopo ili tuendelee kuwa-promote watoto wetu waendelee kujua kwamba wakisoma watapata mikopo hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nirudie tena kuunga mkono hoja ya Mheshimiwa Ezra, kwamba Bodi ya Mikopo iangalie kwamba kweli hicho kinachosemwa ndicho kinachofanyika? Malalamiko ni mengi na yanakatisha tamaa kwamba watoto wengi bado hawafaidiki na mikopo hiyo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja hiyo, ahsante sana (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante na mimi leo kuwa wa kwanza kuchangia bajeti ya Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nianze kwanza kwa kuishukuru Serikali ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa miradi mikubwa ambayo inaendelea hapa nchini kwetu.

Mheshimiwa Spika, jana nilikuwa Tabora tulikuwa na ufunguzi wa mradi mkubwa wa reli iendayo mwendo kasi (SGR). Kwa kweli tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuweza kutujali wananchi katika miradi ambayo ni mingi sana kwa kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze pia Mheshimiwa Waziri Mkuu kwenye ofisi yake hii kwa jinsi ambavyo anachapa kazi na Watendaji wake. Nitakuwa na machache ya kusema, kwenye suala la kuwawezesha vijana kuna miradi ile ya vitalu nyumba na wengine wamewahi kuongelea hapa. Vile vitalu nyumba gharama yake ni kubwa, vitalu nyumba vya kawaida vinafika mpaka Milioni 12 ambavyo vijana wa kawaida hata wakimaliza kujengewa ule ujuzi hawana uwezo wa kumudu kununua vile vitalu nyumba. Kwa hiyo, ninaomba Serikali iangalie hawa vijana watawezeshwa kwa nchi nzima namna gani wanaweza kupata vile vitalu nyumba kwa bei ambayo ni affordable, hawa vijana kila wakimaliza mafunzo wasikae tu bila kazi yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulizungumzia suala pia la bajeti ya wenzetu upande wa DPP, wenzangu wengi waliongelea, kwenye ukomo wa bajeti tuliomba waongezewe hata Shilingi Bilioni 10 kwa ajili ya kuwezesha hizo Ofisi za DPP ziweze kufanyakazi, kwa sababu kwa kweli mashtaka mengi yanakawia kusikilizwa ni kwa sababu ofisi nyingi Mikoani hazina hawa wenzetu wa ofisi ya DPP. Kwa hiyo, mara nyingi wanatumika Askari wale wale wafanye upelelezi, Askari hao hao na waendeshe mashtaka. Sasa nimewahi kusema hawa Askari wakati mwingine wakifika vituoni wanapangiwa kazi zingine, inakuwa siyo rahisi wakafanyakazi za aina mbili. Kwa hiyo, Ofisi ya DPP kwa kweli inahitajika kuwa na usaidizi wa kutosha.

Mheshimiwa Spika, nitakuwa sijatenda haki kama sintalisema hili ambalo nimelikuta jana Tabora. Nimekwenda Tabora kushuhudia uwekaji wa jiwe la msingi la SGR nimekuta bomoa bomoa ambayo siyo ya kawaida, kwa kweli wananchi wa Tabora Manispaa Mheshimiwa Waziri Mkuu wamebomolewa sana vibanda vyao, hatukatai mimi siungi mkono Miji yetu kuwa michafu, siungi mkono kabisa, Serikali kuisafisha Miji yetu inafanya vizuri ninaunga mkono kabisa kuweka Miji yetu katika hali ya usafi. Kitu ambacho kinanisikitisha ni namna mazoezi yenyewe yanavyoendeshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano Tabora Manispaa, kwanza wale wa kubomoa wameenda usiku, asubuhi wananchi wale wajasiriamali na wengine wanaamka wanakuta vibanda vimebomolewa, yanatumika matingatinga usiku lakini hata kipindi chenyewe, sasa hivi watu wako kwenye mfungo wa Ramadhani, watu wako kwenye Kwaresma wanamalizia, hivi kulikuwa na haraka gani hawa wananchi wakiwa katika hali hii Mheshimiwa Waziri Mkuu, bado tuna majibu ambayo tunatakiwa kuwajibu ugumu wa maisha unaoendelea kipindi hiki na Waheshimiwa Wabunge wengi wameongelea hilo suala, maisha yamepanda tunafahamu vita ya Russia, tunafahamu hiyo Ukraine tunajua kinachoendelea, maisha yamepanda, sasa wananchi wanapobomolewa bila hata kusubiri basi huu mfungo basi upite. Hili limekuwa na haraka gani katika kipindi hiki? Watoto wao wanaowategemea hawa wajasiriamali wamekosa nini sikukuu wote zitakuwa ni mbaya kwao, hawa watoto wamekosa nini?

Mheshimiwa Spika, nafikiri hii approach Mheshimiwa Waziri Mkuu tuiangalie kwamba hawa tunawasaidiaje, mbona tunawasaidia hata wahalifu?

Mheshimiwa Spika, niliuliza Mtaalam mmoja wa Manispaa alinijibu kwamba walishirikishwa walikuwa wabishi kwa hiyo tumeamua tena tuwabomolee usiku, kwani kumshirikisha mtu Mheshimiwa Waziri Mkuu ni nini? Wangapi wanashirikishwa hapa wanaambiwa msiue, msizini, msifanye hiki na wanaendelea kama kawaida, lakini tunawawekea mpaka Mawakili kuwatetea. Kwa mfano, kesi za mauaji bado zipo tunawawekea Mawakili, kwa nini hawa akina Mama Lishe tusiwatetee? Tuangalie approach ya namna gani tunaweza tukafanya, hawa ni Watanzania wenzetu, nchi hii ni ya kwetu sote, tuangalie approach ambayo haitakuwa ya kuwaumiza kiasi hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maana yake sisi wengine tofauti na Watendaji wa Serikali hawa waliokuwa wananiambia jana wao ni Watendaji wa Serikali tena mmoja ni Mteule wa Rais, mimi siyo Mteule mimi wanaonifanya niwepo hapa ni wale wananchi lazima niwasemee. Kwa hiyo, ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, hatukatai kutenga maeneo kwa ajili ya wafanyabiashara.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, Tabora Manispaa walioomba wanafika zaidi ya Elfu Moja, maeneo yametengwa yako kama 500, ni kama nusu tu, hawa wengine wanapelekwa wapi? Matokeo yake sasa kila siku tutakuwa ni kuombwa mitaji tu, Wabunge hawa ndiyo wanaoombwa mitaji, maana yake wale sasa kwa kuwabomolea hawana tena mitaji.

Mheshimiwa Spika, kwenye huu mradi ambao unaendelea nchi nzima huu wa SGR kwenye ripoti ya watu wa reli watajenga sehemu mbalimbali majengo na hasa kwenye vituo vikubwa yatakuwepo majengo ya biashara, mpaka shopping malls zitakuwepo mle, ninaomba Mheshimiwa Waziri Mkuu imekuwa ni kawaida hata kwenye Halmashauri kunapotengwa maeneo ya nyumba za kufanyia biashara au vibanda vya kufanyia biashara, wanaanza wao wenyewe Watumishi wa Serikali kuanza kujigawia vile vibanda.

Mheshimiwa Spika, ninakuomba Mheshimiwa Waziri Mkuu kwenye huu mradi mkubwa hawa wananchi ambao mradi huo wa reli wa SGR utapita basi, wapewe kipaumbele kwenye maeneo ya vile vyumba ambavyo vitakuwepo kwa ajili ya biashara ili vijana wetu nao wapate ajira, kuliko hawa wenzetu wenyewe wa Serikali kuanza kuandika majina mbalimbali na kuchukua vile vibanda halafu wao ndiyo wanafanya biashara.

Mheshimiwa Waziri Mkuu nirudie kusema kwamba ofisi yako inafanyakazi nzuri na nchi yetu kwa kweli kwa kiwango kikubwa inakwenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuimarisha demokrasia nchini na kukuza diplomasia ya uchumi
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi niweze kuchangia Azimio hili la Bunge. Nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuwa miongoni mwa Marais wachache sana hapa duniani wanaoheshimu Katiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Katiba ya nchi yoyote ile huwa inakuwa na mapungufu yake. Na katika mapungufu hayo kwa kwaida wengi wa viongozi huwa wanaziogopa Katiba zao, lakini mama ameweza kuwa shujaa wa sasa kuruhusu hata mikutano ya vyama vingi, sio kitu rahisi kabisa, kukaa kiti kimoja na mtu ambaye ni hasimu wako huwa ni kitu kigumu sana. Tunaona hata katika michezo Yanga na Simba tu ni michezo ya kawaida, lakini watu wanavyoweza kupigana vijembe, sasa katika hilo nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuheshimu Katiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Katiba yetu iko wazi, inasema nchi hii ni ya vyama vingi kwa hiyo, kwenda kinyume cha hapo ni kwamba, mtu anakuwa haheshimu Katiba. Kwa hiyo, namshukuru na ninampongeza sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, lakini nchi hii imeingia kwenye mikataba mingi ya haki za binadamu, ikiwemo ile ya human rights ya mwaka 1984 ambayo Tanzania tulisaini mkataba ule. Sasa kwenda kinyume na mikataba ile tunakuwa hatutendi haki kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Rais, lakini Mheshimiwa Rais amekuwa kimataifa sasa anajulikana kila pembe kwa namna anavyofanya kazi yake katika kuhakikisha sisi sasa tunajikomboa kiuchumi na tunasonga mbele.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni unakumbuka Mheshimiwa Rais alipata tuzo ambayo ilitolewa kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu, tuzo ile inaitwa BABAKAR NDIAYE AWARD. Alipata ile tuzo kwa sababu, ya ule mchango wake unajulikana sasa kimataifa jinsi anavyofufua uchumi wa nchi yetu kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Rais Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini lingine, hivi juzi tu tulikuwa kwenye Kamati ya PAC, tumezunguka sehemu nyingi tumeona miradi mingi ambayo sasa inaendeshwa ten ana wenzetu wawekezaji kutoka nje wengi sana sasa wanakuja Tanzania kwa sababu, sasa Mheshimiwa Rais ameifungua nchi na kila siku tunaona vikwazo vinaendelea kuondolewa kwa ajili ya wawekezaji kutoka nje. Kwa hiyo, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini na wengine wamesema hapa, Mheshimiwa Rais juzijuzi hapa alikuwa ametuletea ugeni mkubwa sana wa Makamu wa Rais wa Marekani. Nchi ya marekeni kupata ugeni mkubwa kama ule, yeye Mheshimiwa Makamu wa Rais kufika tu hapa Tanzania, ujio wake sisi Tanzania tumejulikana dunia nzima kwa sababu, Marekani kiongozi wake anapokwenda mahali popote duniani ni karibu dunia nzima inafuatilia kwa hiyo, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa ujio wa Makamu wa Rais wa Marekani.

Mheshimiwa Spika, lakini pia na yale ambayo wameweza kuzungumza kuhusiana na mambo ya kiuchumi na namna ambavyo Marekani wanaweza kusaidia katika kuendeleza uchumi wa nchi yetu, tunamshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nimalizie kwa kusema Katiba, ambayo nimesema Mheshimiwa Rais anaiheshimu sana, nchi nyingi hata ambazo zimekuwa zikisifiwa kwamba, zina Katiba nzuri tumeona hata majirani zetu fulani hapa, siwezi kuwataja jina lao, siwezi kutaja hiyo nchi, pamoja na kusifu kwamba, Katiba yao ni nzuri, watu wanaendelea na maandamano. Kwa hiyo, narudia kusema Mheshimiwa Rais kuruhusu maridhiano ya kisiasa hapa Tanzania ule ni ushujaa mkubwa sana kauonesha na sisi tutamuunga mkono, kilichobaki sasa hivi tuendelee kushindana kwa hoja, tuende tuwapalekee wananchi nini kimefanyika katika awamu zetu zote katika utawala wetu wa Tanzania. Tukashindane kwa hoja milango kwa kuwa iko wazi sasa hakuna vile visingizio vya kwenda kutukanana hadharani.

Tuendelee kushindana kwa hoja, twende tuwapelekee wananchi nini kimefanyika katika awamu zetu zote katika utawala wetu wa Tanzania. Tukashindane kwa hoja, milango kwa kuwa iko wazi sasa hakuna vile visingizio vya kwenda kutukanana hadharani.

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kusema kwamba na mimi naunga mkono hoja azimio hili kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii muhimu ya Afya. Nakushukuru sana. Nianze kwa kupongeza Serikali na hasa kwa jinsi ambavyo imekuwa ikileta fedha nyingi katika eneo hilo la huduma ya afya. Kwa kweli namshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anaangalia kwa ukaribu afya za wananchi, lakini Mheshimiwa Ummy pamoja na Ndugu yangu, Mheshimiwa Dkt. Mollel, nawapongeza kwa kazi nzuri sana wanayoifanya pamoja na timu yao ya Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa pongezi hizo hizo, sisi Mkoa wa Tabora na hasa Hospitali yetu ya Kitete ambayo ni ya Rufaa na sisi ni miongoni mwa waliopata ile CT-Scan ambayo inagharimu karibu shilingi bilioni 1.8. Tunawashukuru sana Wizara na imeshaanza kufanya kazi na inategemewa na wilaya zote kuanzia Kaliua, Nzega, Uyui na sehemu zingine katika eneo hilo, kwa kweli tunaishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze pia Serikali kwa kuweza kuona ule udanganyifu ambao umekuwa ukifanywa na wenzetu wa NHIF na zile hatua ambazo wamechukua, Mheshimiwa Ummy na timu yako tunawashukuru, lakini wasiishie hapo. Katika hotuba ya Waziri amekiri bado kwenye zahanati kuna upungufu mkubwa wa dawa. Waangalie kwa nini MSD wanaongezewa bajeti na dawa wanapeleka, lakini kwa nini kuendelee kuwa na upungufu kwenye zahanati na hospitali zetu za mikoa na za wilaya nazo zina matatizo ya upungufu wa dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika yale maduka ambayo Mheshimiwa Ummy kipindi fulani alisema mita 500 na nini, anafuatilia na vitu kama hivyo, maduka haya ya dawa yamejaa dawa siku zote. Ukichunguza sana sio kwamba wale wa maduka ya dawa wote wanaagiza hizo dawa, wanazipata hapa hapa nchini na hatuelewi wanazipataje, wakichunguza mtajua. Nina imani hizo dawa kuna mahali zinachepuka, badala ya kwenda kwenye hospitali, wanazipata hawa wa maduka binafsi. Umekuwa ni mtindo wa kawaida mwananchi hata kidogo tu anaumwa anaambiwa akachukue dawa kwenye duka la dawa, naomba wafanye uchunguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo ambalo ulilisema hapa kuhusu gharama za mtu wa kawaida kwenda kutibiwa. Wiki iliyopita tu Mheshimiwa Ummy hata akitaka kuona ninayo hapa meseji ya Benjamin Mkapa, consultation fee kwa mtu ambaye hana uwezo kabisa, yaani ule ushauri tu 630,000 ninayo hapa. Consultation fee narudia yaani ule ushauri tu 630,000 ninayo bill yake hapa na imeandikwa ina-expire within 24 hours. Ndani ya masaa 24, huyu tena hapati tena hiyo huduma, awe amelipa hiyo 630,000. Sasa anawezaje mtu wa kawaida kupata matibabu. Kwa kweli hicho ni kitu kigumu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara kwa mara nimekuwa nikisimama kwa ajili ya Hospitali ya Kitete kuhusu upungufu wa Madaktari. Madaktari Bingwa ambao wanahitajika kwa mujibu wa ikama ni 21, lakini tuna Madaktari Bingwa watano tu. Kwa mujibu wa taarifa za Wizara ni kwamba sita sasa wamekwenda kusoma, kwa ajili ya Udaktari Bingwa lakini bado mashaka yako pale pale. Kwanza hawa sita wote watarudi Hospitali ya Mkoa wa Kitete? Kwa sababu wanaweza ku-diverge wakatoka pale wakaenda kwingine, wameshakuwa mabingwa. Madaktari Bingwa wengi wanapenda kufanya kazi katika mikoa ambayo, kwa mfano Dar es Salaam, wamefurika wako wengi ni kwa sababu ya maslahi. Sasa wana mkakati gani kama Wizara kuhakikisha hata hawa ambao wanawasomesha wanarudi kufanya kazi pale kitete ili na sisi tuanze kuona sasa kwamba tunaanza kupata Madaktari Bingwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mwenzangu mmoja jana, Mheshimiwa mmoja alikuwa ananiambia kwa nini huchangii Wizara ya Maji, mbona ni muhimu sana. Nikamwambia nitawapotezea muda wenzangu bure, mimi maji ninayo ya kutosha, kwa hiyo nitachangiaje? Sana sana kule Tabora Mjini sisi tuna maji ya Ziwa Victoria, tunaishukuru sana Serikali na tuna maji in excess. Sasa kilichobakiwa ni ile distribution na nini, ndio maana nikasema siwezi kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata kwenye huduma ya nishati sisi tuko vizuri sana na huduma zingine, kasoro tu Kitete. Ndio maana kila nikiinuka Kitete, Kitete na Tabora Mjini haiitwi Toronto hivi hivi Mheshimiwa Ummy ameshafika mara nyingi. Shida yetu sisi kwenye afya hapa. Naomba atusaidie ile Toronto sasa isiwe mtu anatoka Toronto halafu anaenda kutafuta huduma zingine za afya sehemu nyingine ni eneo tu la Mheshimiwa Ummy, akitusaidia basi atakuwa kwa kweli ametutendea haki sana. Vinginevyo Waziri anafanya kazi nzuri sana, tunamshukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kitete hospitali hiyo hiyo ya mkoa, kuna wanaojitolea katika kada mbalimbali wako 91, hao wanajitolea 91 ni watu wengi sana. Sasa tunarudi kule kule kwamba pale watakapotoa ajira wasianze kuwaleta watu ambao wametoka huko, hatukatai kuleta watu wengine, lakini wawape kipaumbele hawa ambao wanajitolea kwa sababu kazi ya uuguzi ni kazi ambayo kwa kweli ni ya kujitolea na kweli wanajitolea, 91 ni wengi sana. Kwa hiyo watakapotoa nafasi zile ambazo wataanza kuajiri naomba waweze kuwakumbuka hawa ambao wanajitolea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna sera ya watoto wa chini ya umri wa miaka mitano kwamba wanapewa matibabu bure. Hiki kitu kwenye sera kipo, lakini kiuhalisia sehemu nyingi hakifanyiki. Mwaka mpya nilikwenda kutembelea Hospitali ya Kitete tena nilikuwa na timu pia nilikwenda na baadhi ya viongozi wa Chama cha Mapinduzi kwa ajili ya kuona wagonjwa lakini na kuweza kutoa vifaa mbalimbali. Tulimkuta mtoto wa miaka mitano ambaye alikuwa amepataa referral, sio tu rufaa lakini pia alikuwa anatakiwa kulipia matibabu. Sasa nikawa namuuliza kwa sababu tuliongoza na Muuguzi Mkuu kwamba imekuaje hawa watoto ambao ni chini ya miaka mitano, sera inasema matibabu ni bure. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, akaniambia kuhusu ugonjwa wake. Sasa namwomba Mheshimiwa Waziri kwenye hili suala la watoto wa umri wa miaka mitano wawe wawazi kama kuna magonjwa ambayo hayawi covered kwenye hiyo sera ya kwamba matibabu ni bure kwa mtoto wa chini ya miaka mitano, wayaeleze wazi bayana, watu wawe wanafahamu. Vinginevyo wakienda pale akinamama na watoto wao wanajua tu kwamba mtoto wangu kwa sababu yuko chini ya miaka mitano atapewa matibabu bure, anapofika pale anapewa bill ya kulipa, inawachanganya sana wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Ummy lingine ni kuhusu suala la udhibiti wa hizo dawa. Kama dawa zinapelekwa kwa mfano hospitali fulani, inajulikana kabisa kwamba package ni hii, mnadhibiti vipi hizi dawa? Maana yake tumeona sehemu zingine baadhi ya Manesi siyo wote na baadhi ya watumishi wa hospitali ambao wamekuwa wakikamatwa na hizo dawa wakipeleka kwenye maduka ya madawa binafsi? Hizi dawa wanazitoaje? Udhibiti wa dawa ukoje? Naomba eneo hilo muweze kuliangalia kwa ajili ya kudhibiti upotevu wa dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia madirisha ya wazee na watu wenye mahitaji maalum. Bado kuna hospitali nyingi hapa nchini ambazo hazina madirisha ya wazee wenye umri mkubwa ambao wanahitaji huduma za afya lakini pia na wale wenye mahitaji maalum kwa mfano, wenzetu ambao wenye ulemavu kwamba waweze kupata huduma hizo haraka kutokana na mahitaji yao ya kimwili.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mimi kusema haya na kushukuru sana naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nami nafasi ya kuchangia katika Wizara muhimu hii ya Nishati na mimi nianze kumpongeza Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan hasa kwa hili la leo kwamba hata mafuta sasa yamepungua bei kwa kiasi fulani. Lakini Mheshimiwa January Makamba unafanya kazi nzuri hongera sana. (Makofi)

Mimi nadhani nianze na hili la leo kupungua bei ya mafuta, hili liende na kwenye Wizara zingine. Wakati mafuta yamepanda bei na vitu vingi vilipanda bei kwa kisingizio cha haya mafuta. Kwa mfano, Wizara nyingine litachukua hata hili kwamba kwa mfano kwenye kilimo sasa mazao nayo, yaonekane yanaanza kupungua bei kwa maana ya kwamba vitu tuvione vinaanza kupungua bei. Kama vitu mitaani vitazidi kuwa na hali ile ile wananchi hawawezi kuona unafuu wa kupungua bei ya mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia usalama wa mafuta wapo ndugu zetu Kampuni mbalimbali na mashirika ambayo yanashughulika na usalama wa mafuta. Vituo vingi vya mafuta vina mafuta mazuri, lakini baadhi ya vituo vinaharibu sana magari ya watu. Kuna vituo ambavyo ukishaweka mafuta sijui huwa wanachanganya au namna gani, lakini baada ya hapo unakuta umeweka mafuta gari imekuwa na matatizo, kwa hiyo, wananchi pia wanapata tatizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwenye suala la REA; maeneo mengi yalishaahidiwa na Serikali kwamba yatapewa umeme wa REA katika mwaka huu mpaka mwaka kesho kwamba karibu vijiji vyote vitapata umeme, nchi hii ni kubwa na kuna majimbo mengine ni ya mjini kama mimi Tabora Mjini ni mjini, lakini kwa kutamka ni mjini, ila Tabora Mjini ina vijiji 41 na vijiji vile vingine vinakwenda mpaka masaa mawili kufikia hivyo vijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna baadhi ya watendaji wakishaona neno mjini wanasema wote hawa kuunganishiwa REA ni shilingi 27,000 kitu ambacho wanakuwa hawajawatendea haki wananchi. Mheshimiwa Makamba uzuri Tabora umeshafika, umefika Nisha kule na sehemu zingine, lakini kuna Mawaziri wawili akiwemo Mheshimiwa Mgalu kuna siku moja nilikuwa nataka nimpeleke kijiji kimoja Itema, alivyofika njiani wakati ule akiwa Naibu Waziri akasema huku kote pia ni Tabora Mjini, naomba tuishie hapa hapa, hatukuweza kufika kwa sababu ni mbali sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna mwongozo mlitoa kwamba hata vijiji vile viweze kupatiwa umeme wa REA. Sasa nina taarifa kwamba kwa sababu neno mjini linasemwa wananchi wa vijijini kule wanataka kupewa umeme kwa gharama ambayo sio ya REA. Kwa hiyo, naomba hili Mheshimiwa Waziri January uliangalie sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna suala hili la uunganishwaji umeme, nimesikia hata kwenye taarifa ya Kamati ya Nishati, hawa wakandarasi ambao wanaunganisha umeme kwenye nyumba mbalimbali gharama zao ni kubwa sana. Nadhani ni vizuri Serikali ikaangalia namna ya kuwa-control hao wakandarasi, hakuna faida Serikali ipunguze namna ya kufanya installments za umeme, halafu hao wakandarasi wawe wanazidisha bei, yale makali ya fedha za uunganishwaji umeme yatabaki pale pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna hawa waratibu ambao watakuwa wanatoa taarifa hizi za uunganishwaji wa umeme hasa katika suala hili la REA. Naomba ndugu yangu January katika hili hao waratibu wenu ambao watakuwa wanatoa hizi taarifa muwafuatilie ili kuona kwamba taarifa zao je, zitakuwa sahihi? Maana yake mara nyingi hamuambiwi taarifa ambazo ni sahihi. Vijiji vingi kweli na vitongoji havijapata umeme na wananchi muda tuliowaahidi kwamba ukifika muda fulani watapata umeme, wanasikiliza tu muda ule ukifika hawakupata huo umeme Mheshimiwa January tutakuwa katika hali mbaya sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna suala hili la kubadilisha nyaya za umeme sehemu mbalimbali nchini, Tabora kuna shida sana ya kukatikakatika umeme kama walivyosema wenzangu hapo. Wananchi wanapata shida ya umeme lakini pia kwa wafanyabiashara ambao ni walipakodi wazuri kwa Serikali, mitambo yao muda mrefu inapokuwa haifanyi kazi wanapata wao hasara, lakini pia na Serikali inapata hasara kwa kutopata zile kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ni-declare interest katika eneo hili na mimi ni mhusika. Mimi nina mashine mbalimbali za kusaga, kukoboa na ku-grade, lakini muda mrefu unaweza kukuta kwa wiki mara nne hazijafanya kazi kabisa umeme haupo. (Makofi)

Kwa hiyo, unapata hasara mfanyabiashara, lakini pia Serikali inapata hasara, lakini umeme ule unaporudi mara nyingine unaunguza vyombo mbalimbali, kwa sababu unarudi ukiwa hauja-stabilize na gharama hiyo TANESCO kulipa sio rahisi huwa hawalipi, kwa hiyo wananchi na wafanyabiashara wanapata hasara sana, kwa hiyo naomba muangalie katika hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mheshimiwa January aliongelea hapa suala kuhusu mkataba ule wa gesi ambao umesema mazungumzo yameendelea vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hii gesi watakapokuwa wamefanikiwa ionekane kweli ina faida kwa wananchi kwa sababu inaweza ikaletwa gesi lakini gharama zake ni kubwa na huku tunasema tuondoe utumiaji wa nishati hizi halisia kama miti na nini kwa sababu ya uharibifu wa mazingira, lakini kama hii gesi ambayo wanaendelea kufanya mchakato wake itaendelea kuwa ghali itakuwa hakuna faida, wananchi wataendelea kukata miti na vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya machache, naunga mkono hii hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii. Nianze kwanza kwa kuipongeza Serikali kwa bajeti nzuri sana ambayo kwa kweli imeleta matumaini makubwa kwa Watanzania na hasa wanyonge. Pia nimpongeze Mheshimiwa Rais mama Samia Suluhu Hassan, kwa jinsi ambavyo amekuwa akituletea maendeleo. Vile vile niwapongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Mwigulu pamoja na Naibu wake kwa kutusomea bajeti nzuri sana yenye matumaini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi siyo mchumi, lakini nizungumze kidogo kuhusu mambo ya inflation. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Mwigulu, Waziri wa Fedha ni kwamba hali ya uchumi sasa hivi kidunia imepungua kwa asilimia 3.1, badala ya matarajio ambayo ilikuwa ni asilimia 6.0. Katika hilo hilo suala la inflation wanasema kwamba mpaka hapa tulipo katika soko la dunia bidhaa nyingi zimepanda kwa asilimia 24, lakini mfumuko wa bei kwenye soko la dunia kwamba umeongezeka kwa asilimia 5.7 kwa nchi zilizoendelea na kwa nchi zinazoendelea ni asilimia 8.7, maana yake ni kwamba bidhaa zitaendelea kupanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa zimetolewa sababu nyingi ambazo kwamba mojawapo ni hii ambayo ni ya vita ya Ukraine na Russia, lakini na suala la UVIKO 19, tunashukuru Mheshimiwa Spika alituletea wale wataalam jana ambao wengine walikuwa wametoka BoT na wengine wa Serikalini kwa ajilli ya kutupitisha sehemu mbalimbali katika kuangalia mambo ya uchumi. Moja ya kitu ambacho kinahitaji elimu ya kutosha, ni pale waliposema kwamba hata kusingekuwa na vita ya Ukraine na Russia, bado bei kwa mfano za bidhaa zilizopo sasa zingeendelea kuwepo hapa zilipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa mwananchi wa kawaida inatakiwa kutolewa elimu ya kutosha ili ajue tunafikaje hapo, kwa sababu hawa wataalam wetu pia ndiyo wanapita na mitaani na wananchi pia wanawasikiliza, kwa hiyo siyo kitu cha ajabu kumwona mwananchi wa kawaida akisema uchumi huu kudorora au bei kupanda siyo kwa sababu ya vita ya Russia na Ukraine, ni kwa sababu ya elimu kama hii. Kwa hiyo kuna umuhimu wa kutoa elimu ya kutosha ili watu waelewe maana ya mfumuko wa bei ni nini, lakini pia kuwapa wananchi njia mbadala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha kuna suala pia la umwagiliaji kwenye kilimo. Kwa kuwa hali ya hewa si nzuri sana kwa nchi yetu na huenda kukawa pia hatutarajii lakini pengine sehemu zingine zikapata upungufu kidogo wa chakula, kuna umuhimu sana wa kuimarisha hizi skimu za umwagiliaji ili tuweze kufanikiwa katika kujihami na suala la chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Sekta ya Afya Mheshimiwa Mwigulu alituambia kwamba sasa hivi baada ya miundombinu kuboreshwa, tatizo kidogo limekuwa kwenye upungufu wa wahudumu wa afya. Tunaomba hiyo miundombinu ambayo tayari imejengwa kwa muda sasa na iko kwenye mafanikio mazuri, ili iweze kuwa na ufanisi, basi Serikali ifanye jitihada za kutosha kupatikana kwa hawa wahudumu wa afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la elimu, Serikali imefanya vizuri, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuwarudisha mashuleni wale watoto wa kike ambao walikuwa na changamoto mbalimbali zikiwemo za ujauzito. Hata hivyo, pia kumekuwa na changamoto, kwenye elimu pia kuna upungufu mkubwa sana wa Walimu na hasa vijijini. Sehemu nyingi vijijini bado kuna upungufu wa Walimu, Serikali ifanye mkakati wa kutosha na ikiwezekana hata kurekebisha baadhi ya kanuni au Sheria za kuwalazimisha Walimu wakae vijijini. Vinginevyo hili tatizo litakuwa ni la kudumu na tutaendelea kuliimba kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu elimu bure mpaka kidato cha sita tunaipongeza sana Serikali kwa kuamua hivyo. Hata hivyo, Serikali iangalie uwezekano wa kutoa chakula, kama haiwezekani kwa shule zote, basi angalau shule ambazo ziko kwenye remote areas ambako wanafunzi kupata chakula inakuwa siyo rahisi. Miaka ya nyuma iliwezekana, mimi binafsi shule ya msingi nilisoma chakula kilikuwepo shuleni, wale ambao mmesoma miaka ambayo na mimi nimesoma, ile ya 1970, tulikuwa tunakula chakula shuleni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tunakula chakula ambacho kama mnakumbuka, tulikuwa tunakula mpaka ngano, tulikuwa tunaita bulga. Kulikuwa na siku maalum ya kula bulga lakini pia tulikuwa tunaletewa chakula na watu wale wa chakula barafu walikuwa wanatuletea samaki wale ambao wamegandishwa. Kwa hiyo tulikuwa tunapata elimu ya namna hiyo, lakini hata madaftari likiisha ulikuwa unampelekea Mwalimu, anaangalia kama limejaa anakupa daftari lingine. Kwa hiyo tunaomba pia Serikali iangalie kutoa nafuu za namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nizungumzie suala hili la utalii, utalii ndugu zangu ni muhimu na nchi yetu imepiga hatua kubwa sana sasa hivi kuhusu utalii. Mheshimiwa Rais ametuongoza vizuri katika eneo hili. Utalii wetu umekua kwa kiwango kikubwa, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais mama Samia Suluhu Hassan na hasa hili suala la Royal Tour. Kama ilivyo kawaida penye mafanikio hapakosi changamoto, wenzetu wameanza kutuchafua ili tusifanye vizuri. Katika hili niko tofauti kidogo na wenzangu kwenye kuchangia eneo hili. Naona hapa nia siyo watu kuhamishwa au watu kuhama, hapa wanalenga utalii wetu ili wale wenzetu ambao wanakuja kwenye kufanya huo utalii waone kule Tanzania kuna sehemu haina amani. Hawa wenzetu Wzungu na watalii wengine, mara nyingi hawaendi sehemu ambayo wanajua kuna machafuko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo wenzetu hawa wanaotumia lugha hizi mbalimbali za kwamba kuna kitu fulani kinafanyika watu wanahamishwa, tena watu wenyewe wanahamishwa kwa hiyari yao wala siyo vurugu, lakini bado wanaingilia kutupakazia. Nchi hii siyo mara ya kwanza kuhamisha watu, kulikuwepo na suala la operation vijiji miaka ya 70, watu walihamishwa mpaka kupelekwa Gezaulole na Mwanadilatu, hatukuona watu wakiingilia na kusema hawa wamehamishwa kinyume cha sheria. Vile vile bomoa bomoa nyingi zimepita, ardhi ya nchi hii ni mali ya umma chini ya udhamini wa Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wanahamishwa kwa kutumia taratibu na wanakuwa compensated. Sasa leo anapotokea mtu anaingilia kitu ambacho ni cha nchini mwetu; na ninaomba kidogo ninukuu, hii ni sovereign. Hii term inatumika kimataifa na maana yake naomba noisome. Maana yake ni the supreme absolute uncontrollable power by which an independent state is governed and from which or specific political powers are delivered. Inaendelea kusema, the international independence of a state, combined with rights and powers of regulating its internal affairs without foreign interference. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sisi tuna regulate mambo yetu wenyewe na tuna taratibu ambazo hatujakiuka any international law yoyote. Kwa hiyo, ndiyo maana nimesema wanalenga utalii wetu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu na hasa Wizara yetu ya Utalii, hapa tunachafuliwa, kulenga namba ya wale watalii ambao wanaongezeka hapa nchini. Hata hili alilolianzisha Mheshimiwa Rais, la Royal Tour, haya ndiyo yanayolengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuwe waangalifu, wanataka paonekane kwetu hapana utulivu ili waweze kutupunguzia idadi yetu ya Utalii… (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mwakasaka. Muda mrefu kengele ilishagongwa.

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Mamlaka ya Nchi kuhusiana na Umiliki wa Maliasili wa Mwaka 2017.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nami nafasi ya kuchangia hili jambo muhimu sana kwa maslahi ya nchi yetu, kwa kuletwa marekebisho haya ya sheria mpya ya The Natural Wealth and Resources Act of 2017. Naipongeza sana Serikali kwa kutuletea huu Muswada mpya tuweze kuupitia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba ninukuu vifungu vichache tu kwa jinsi vilivyo. Tumekuwa kweli tukiibiwa sana na nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuliona hilo na kuliwekea mkakati ambao kama nchi ni lazima tunatakiwa tuwe pamoja kwa ajili ya maslahi ya Taifa letu kwa ujumla. Ile Sheria yetu Na. 10 ilikuwa haina vitu vingi ambavyo sasa vimeletwa kwenye hii sheria mpya. Kwa mfano, Waziri sasa ambaye alikuwa ndiye Waziri wa Nishati na Madini amepunguziwa madaraka mengi, yamepelekwa kwenye Commission.

Mheshimiwa Naibu Spika, Commission ile ina watu mbalimbali ambao wana utaalam mwingi lakini Commission hii imewekwa ili kuondoa ule upungufu ambao ulikuwepo kwenye sheria ya kwanza na sasa zile discretionary powers za Waziri alizokuwa nazo zimepelekwa kwenye Commission ambapo sasa Commission hii itakuwa na uwezo wa kufikiria kutoa leseni na hata kuifuta leseni ya madini kitu ambacho hakikuwepo mwanzoni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa na mikataba ambayo kwa mfano, hawa wenzetu wawekezaji walikuwa wakishaingia mikataba, huwezi kubadilisha chochote hapa katikati mpaka mkataba utakapoisha hasa kwenye masuala ya kodi, lakini sasa kuna vipengele vya kuweza ku-review mikataba hiyo, kitu ambacho kitaisaidia sana nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Kifungu namba 10 (1) na (2), pale kuna masuala ya pesa ambazo zinatakiwa kuhifadhiwa na hawa wawekezaji. Pesa nyingi walikuwa wanapeleka nje, lakini sasa sheria hii mpya inawataka wawekezaji wote kwamba sasa pesa zao, isipokuwa dividend waweke hapa nchini. Sasa kwa kuweka pesa nchini, pesa hizi zikiwa kwenye mabenki yetu zitasaidia hata mzunguko wa kifedha wa nchi katika mabenki yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nasikiliza kwenye Kambi Rasmi ya Upinzani walikuwa wanaongea kwamba usimamizi wa Serikali unatakiwa uwe mbali katika masuala ya madini. Nasikitika sana kwa usemi huo, sikuutegemea kabisa! Wakati nchi imeingia kwenye matatizo makubwa, Hansard ipo, usimamizi wa Government uwe mbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nashangaa! Tumefika hapa tulipo kwa sababu na kutokuwa na close supervision; tulikuwa hatuna, kiasi ambacho tumeibiwa sana. Sasa Serikali inabana, wenzetu wanasema Serikali isiwe moja kwa moja. Hilo la kwanza.

KUUSU UTAATIBU....

Mheshimiwa Naibu Spika, narudia kwamba nimesikia na Hansard zipo. Lipo la pili, wameongelea hii certificate kuletwa under emergence kwamba nchi haiko kwenye vita, imeongelewa hapo pia. Vita gani wanaitaka wao? Hapa tupo kwenye vita kubwa ya kuokoa rasilimali zetu za nchi. Wao wanaposema kwamba nchi haiko kwenye vita, wanaongelea vita gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ridhaa yako naomba nifute hilo, labda nitakuwa nimei-misheard lakini ninaomba pia Hansard zirejewe kwa sababu nilikuwa nimelisikia, ila nafuta ili niweze kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye hili la pili la kwamba nchi hii haiko kwenye vita, kwa hiyo, hii certificate of emergence haikutakiwa kuletwa hapa Bungeni. Hiki siyo kweli kwa sababu suala hili la sisi kuibiwa hizi rasilimali zetu siyo tu kwamba sisi tumetikisika, hata wenzetu waliotuhumiwa tuliona wamekuja hapa kwa sababu ilikuwa ni suala ambalo limegusa wengi. Linagusa kodi za wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nawashangaa wenzetu wakisema wao wanataka certificate of emergence zije wakati kuna vita. Vita gani zaidi ya hii ambayo tunapigania uchumi wetu? Kwa hiyo, wasiendelee kuwadanganya wananchi kwa vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna suala hili la Kifungu Na. 12; kuna suala la wao wenzetu kulazimisha kwamba tuweke neno “shall” badala ya “may” kwenye suala la Bunge kupitia hii mikataba. Ninavyofahamu ni kwamba Bunge kazi yake kubwa ni kuishauri Serikali. Sasa Bunge likiwa lenyewe ni part of decisions, sijui litaishauri vipi Serikali wakati na Bunge lenyewe lilishiriki kwenye kutoa maamuzi?

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tutakubaliana na wao ina maana kwamba Bunge sasa litakuwa halina nguvu kuja ku-review mambo ambayo na lenyewe lilikuwa miongoni mwa kujadili. Kwa hiyo, nadhani ibaki vile vile kama ilivyo.

Hili neno “may” libaki kwa sababu kisheria linatoa muda wa Bunge kujiridhisha halafu ndiyo kuitisha ku-review; siyo kila kitu kiwe reviewed na Bunge halikutani kila mara na ndiyo maana vyombo vingine vimepewa mamlaka kuweza kushughulikia vitu ambavyo haviwezi kuletwa Bungeni kila mara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hiki Kifungu Na. 11 kuhusiana na hizi kesi ambazo kukitokea dispute yoyote na hawa wawekezaji kwamba kesi hizi ziendeshwe ndani ya Mahakama zetu. Naunga mkono kifungu hiki kwa sababu kwanza sisi tuna Prominent Lawyers wengi tu, nchini kwetu. Siyo lazima kila kesi, kuna mgogoro kidogo tu uende nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii International Court of Arbitration, kwanza ni kesi chache sana zinazokwenda kule. Pia kwa nini tuzidharau Mahakama zetu ambazo zina uwezo mkubwa sana wa kisheria? Kwa hiyo, napenda kifungu hiki kibaki ili pia kuzipa hadhi Mahakama zetu. Tunao Majaji, tunao Wanasheria ambao wanakwenda kuhudhuria kesi nyingine nje ya nchi yetu. Kwa hiyo, tunao Majaji, tunao Mahakimu wazuri sana nchini mwetu ambao wanaweza wakashughulikia kesi hizi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kusema kwamba nchi ni kweli kwa sasa hivi ilikuwa inazihitaji sana hizi sheria zilizoletwa hapa kwa sababu ya hali halisi ambayo ipo nchini kwetu na kwamba wananchi wasidanganywe na wenzetu kwamba kila siku Serikali ya CCM ndiyo imekuwa ikileta hizi certificate of emergence hapa. Labda niwakumbushe kwamba hata huko kwao, leo kuna viongozi ambao walishiriki kwenye maamuzi haya, huku nyuma, wako kwao leo ambao leo wao wanawaona wa maana. Sasa wasiwachanganye wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya machache, naomba kusema, naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Mapitio na Majadiliano kuhusu Masharti Hasi katika Mikataba ya Maliasili za Nchi wa Mwaka 2017.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nami nafasi ya kuchangia hili jambo muhimu sana kwa maslahi ya nchi yetu, kwa kuletwa marekebisho haya ya sheria mpya ya The Natural Wealth and Resources Act of 2017. Naipongeza sana Serikali kwa kutuletea huu Muswada mpya tuweze kuupitia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba ninukuu vifungu vichache tu kwa jinsi vilivyo. Tumekuwa kweli tukiibiwa sana na nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuliona hilo na kuliwekea mkakati ambao kama nchi ni lazima tunatakiwa tuwe pamoja kwa ajili ya maslahi ya Taifa letu kwa ujumla. Ile Sheria yetu Na. 10 ilikuwa haina vitu vingi ambavyo sasa vimeletwa kwenye hii sheria mpya. Kwa mfano, Waziri sasa ambaye alikuwa ndiye Waziri wa Nishati na Madini amepunguziwa madaraka mengi, yamepelekwa kwenye Commission.

Mheshimiwa Naibu Spika, Commission ile ina watu mbalimbali ambao wana utaalam mwingi lakini Commission hii imewekwa ili kuondoa ule upungufu ambao ulikuwepo kwenye sheria ya kwanza na sasa zile discretionary powers za Waziri alizokuwa nazo zimepelekwa kwenye Commission ambapo sasa Commission hii itakuwa na uwezo wa kufikiria kutoa leseni na hata kuifuta leseni ya madini kitu ambacho hakikuwepo mwanzoni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa na mikataba ambayo kwa mfano, hawa wenzetu wawekezaji walikuwa wakishaingia mikataba, huwezi kubadilisha chochote hapa katikati mpaka mkataba utakapoisha hasa kwenye masuala ya kodi, lakini sasa kuna vipengele vya kuweza ku-review mikataba hiyo, kitu ambacho kitaisaidia sana nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Kifungu namba 10 (1) na (2), pale kuna masuala ya pesa ambazo zinatakiwa kuhifadhiwa na hawa wawekezaji. Pesa nyingi walikuwa wanapeleka nje, lakini sasa sheria hii mpya inawataka wawekezaji wote kwamba sasa pesa zao, isipokuwa dividend waweke hapa nchini. Sasa kwa kuweka pesa nchini, pesa hizi zikiwa kwenye mabenki yetu zitasaidia hata mzunguko wa kifedha wa nchi katika mabenki yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nasikiliza kwenye Kambi Rasmi ya Upinzani walikuwa wanaongea kwamba usimamizi wa Serikali unatakiwa uwe mbali katika masuala ya madini. Nasikitika sana kwa usemi huo, sikuutegemea kabisa! Wakati nchi imeingia kwenye matatizo makubwa, Hansard ipo, usimamizi wa Government uwe mbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nashangaa! Tumefika hapa tulipo kwa sababu na kutokuwa na close supervision; tulikuwa hatuna, kiasi ambacho tumeibiwa sana. Sasa Serikali inabana, wenzetu wanasema Serikali isiwe moja kwa moja. Hilo la kwanza.

KUUSU UTAATIBU....

Mheshimiwa Naibu Spika, narudia kwamba nimesikia na Hansard zipo. Lipo la pili, wameongelea hii certificate kuletwa under emergence kwamba nchi haiko kwenye vita, imeongelewa hapo pia. Vita gani wanaitaka wao? Hapa tupo kwenye vita kubwa ya kuokoa rasilimali zetu za nchi. Wao wanaposema kwamba nchi haiko kwenye vita, wanaongelea vita gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ridhaa yako naomba nifute hilo, labda nitakuwa nimei-misheard lakini ninaomba pia Hansard zirejewe kwa sababu nilikuwa nimelisikia, ila nafuta ili niweze kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye hili la pili la kwamba nchi hii haiko kwenye vita, kwa hiyo, hii certificate of emergence haikutakiwa kuletwa hapa Bungeni. Hiki siyo kweli kwa sababu suala hili la sisi kuibiwa hizi rasilimali zetu siyo tu kwamba sisi tumetikisika, hata wenzetu waliotuhumiwa tuliona wamekuja hapa kwa sababu ilikuwa ni suala ambalo limegusa wengi. Linagusa kodi za wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nawashangaa wenzetu wakisema wao wanataka certificate of emergence zije wakati kuna vita. Vita gani zaidi ya hii ambayo tunapigania uchumi wetu? Kwa hiyo, wasiendelee kuwadanganya wananchi kwa vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna suala hili la Kifungu Na. 12; kuna suala la wao wenzetu kulazimisha kwamba tuweke neno “shall” badala ya “may” kwenye suala la Bunge kupitia hii mikataba. Ninavyofahamu ni kwamba Bunge kazi yake kubwa ni kuishauri Serikali. Sasa Bunge likiwa lenyewe ni part of decisions, sijui litaishauri vipi Serikali wakati na Bunge lenyewe lilishiriki kwenye kutoa maamuzi?

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tutakubaliana na wao ina maana kwamba Bunge sasa litakuwa halina nguvu kuja ku-review mambo ambayo na lenyewe lilikuwa miongoni mwa kujadili. Kwa hiyo, nadhani ibaki vile vile kama ilivyo.

Hili neno “may” libaki kwa sababu kisheria linatoa muda wa Bunge kujiridhisha halafu ndiyo kuitisha ku-review; siyo kila kitu kiwe reviewed na Bunge halikutani kila mara na ndiyo maana vyombo vingine vimepewa mamlaka kuweza kushughulikia vitu ambavyo haviwezi kuletwa Bungeni kila mara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hiki Kifungu Na. 11 kuhusiana na hizi kesi ambazo kukitokea dispute yoyote na hawa wawekezaji kwamba kesi hizi ziendeshwe ndani ya Mahakama zetu. Naunga mkono kifungu hiki kwa sababu kwanza sisi tuna Prominent Lawyers wengi tu, nchini kwetu. Siyo lazima kila kesi, kuna mgogoro kidogo tu uende nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii International Court of Arbitration, kwanza ni kesi chache sana zinazokwenda kule. Pia kwa nini tuzidharau Mahakama zetu ambazo zina uwezo mkubwa sana wa kisheria? Kwa hiyo, napenda kifungu hiki kibaki ili pia kuzipa hadhi Mahakama zetu. Tunao Majaji, tunao Wanasheria ambao wanakwenda kuhudhuria kesi nyingine nje ya nchi yetu. Kwa hiyo, tunao Majaji, tunao Mahakimu wazuri sana nchini mwetu ambao wanaweza wakashughulikia kesi hizi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kusema kwamba nchi ni kweli kwa sasa hivi ilikuwa inazihitaji sana hizi sheria zilizoletwa hapa kwa sababu ya hali halisi ambayo ipo nchini kwetu na kwamba wananchi wasidanganywe na wenzetu kwamba kila siku Serikali ya CCM ndiyo imekuwa ikileta hizi certificate of emergence hapa. Labda niwakumbushe kwamba hata huko kwao, leo kuna viongozi ambao walishiriki kwenye maamuzi haya, huku nyuma, wako kwao leo ambao leo wao wanawaona wa maana. Sasa wasiwachanganye wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya machache, naomba kusema, naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Reli wa Mwaka 2017
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami kuweza kuchangia hoja iliyopo mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kusema naipongeza sana Serikali kwa kuleta Muswada huu wa Sheria ya Reli wa mwaka 2017. Sheria hii tumekuwa tukizungumza muda mrefu sana namna gani mashirika haya mawili yaani RAHCO na TRL wanaweza kuungana kwa ajili ya ufanisi wa Shirika letu la Reli. Naipongeza Serikali kwa kutuletea muswada huu na ninaunga mkono hoja ya muswada huu kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo ninayo machache ya kuongelea kwenye muswada huu, Naomba nianze na suala hili la wafanyakazi wa lililokuwa Shirika la Reli (TRC) baadaye likaenda RAHCO na sasa tunarudi tena kwenye TRC. Wenzangu wameshaongelea lakini na mimi ninapenda tu kuwekea mkazo kwamba sasa hii inakuwa kama ni danadana, hawa wametoka TRC, wale wafanyakazi wengi bado hawajapata haki zao, lakini wamekuja TRL na sasa Serikali wanatuambia kwamba madeni haya yote yatahamishiwa tena kwenye shirika jipya. Sasa ifike mahali Serikali iwe serious na jambo hili kwa sababu wafanyakazi wanapokuwa hawajaridhika huwa kunatokea matatizo mengi yakiwemo haya ya hujuma mbalimbali ambazo zinarudisha nyuma uendeshaji wa shirika hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna matatizo yalitokea mengi, kwa nini shirika lililokuwa TRC lilivunjika. Moja ya matatizo hayo yaliletwa na wafanyakazi wenyewe, lakini pia na baadhi ya sheria ambazo hazikuwa nzuri ambazo sasa nyingine zinafanyiwa marekebisho madogo. Kwa mfano udhibiti wa tiketi za abiria kwenye ile TRC haukuwa mzuri sana kiasi ambacho kilipelekea shirika kupata hasara nyingi. Pia udhibiti wa wizi wa mafuta, shirika lilikuwa likipoteza sana mafuta kwa sababu ya wizi ambao ulikuwa unafanyika na baadhi ya wafanyakazi ambao walikuwa si waaminifu wa Shirika hilo la Reli lililopita. Sasa ninamuomba Mheshimiwa Waziri pamoja na wale ambao watakuwa wanamsaidia waweke uzito mkubwa katika jambo hili kwa sababu ni moja ya vitu vilivyosababisha kuanguka kwa iliyokuwa TRC.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba na mimi niende kwenye suala hili ambalo sasa limekuwa ni kama janga, na ni janga kwa wananchi, hasa hili la bomoabomoa. Niseme mimi Tabora Mjini ni mmoja wa wahanga wakubwa wa bomoabomoa. Tabora Mjini wako wananchi ambao wamejenga ndani ya maeneo ya reli, yaani nikisema mita 30 kwa 30, maeneo yale ya kawaida, lakini pale stesheni 75 kwa 75, wapo wananchi ambao walijenga ndani ya maeneo ya reli.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme mimi kama Mbunge wa Tabora Mjini, lakini pia kama Mjumbe wa Kamati ya Miundombinu, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kusimamia ujenzi huu wa standard gauge, pamoja na Mheshimiwa Profesa Makame Mbarawa kwa kutuletea ujenzi huu, tunahitaji sana maendeleo. Tunahitaji maendeleo kwa ajili ya kupata hii standard gauge, lakini maendeleo wakati mwingine yanakuja na vilio, vilio hivi ni pamoja na hii bomoabomoa. Pale Tabora Mjini hivi ninavyoongea wale ambao wamejenga ndani ya maeneo ya reli wengi wameanza wenyewe wananchi kubomoa na kuondoka, nawapongeza sana wananchi wale.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna suala la sintofahamu kwa wale ambao wamepimiwa maeneo yale na mamlaka ambazo nazo zimesajiliwa na Serikali. Kwa mfano ambao wamepewa maeneo kuanzia maafisa mipango miji wa manispaa walipima wakapitisha ramani zao na zikawa approved Wizara ya Ardhi na wakapewa hati, wananchi hawa ni wengi sana na wamekumbwa na zoezi hili, na ni kweli wengine ukipima wanakuwa ndani ya maeneo ya reli sasa hivi kwa sababu kuna ramani ya reli na ramani iliyopo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hawa waliowapimia ambao ni manispaa, wananchi hawa ni very innocent hawajui chochote. Ninaiomba Serikali ione namna gani itawafikiria wananchi hawa. Naelewa Mheshimiwa Rais ana huruma, tumewahi kuona wamachinga wakionewa huruma pamoja na kwamba sehemu nyingine hawakupaswa kuwepo lakini walipewa sehemu nyingine ya kwenda kujihifadhi. Sasa wananchi hawa kwa kuwa walipewa na vyombo halali, na wengine wako mpaka mita 500 nje ya reli, ninaomba Serikali ione itafanyaje kuhusu wananchi hawa kwa sababu kwa kweli wengi ni maskini, kama walivyosema wenzangu na ni wengi mno na hawajui pa kwenda baada ya hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi mamlaka zilizowapa, mbona Dar es Salaam kule nakumbuka kuna baadhi ya watendaji ambao waligawa maeneo sehemu mbalimbali lakini Serikali ilizungumza kwamba wale ambao waliwapa hawa na wao wawajibike. Kwa eneo hili la bomoabomoa, tunapenda pia Serikali itufahamishe kwamba wale ambao wamewagawia wananchi hawa maeneo hayo na bado wapo na hawajasema chochote, sijui inakuaje? Vilevile kwa kuwa wamegawiwa na manisapaa, pale ambapo Serikali haiwezi kutenga fedha kwa ajili ya kuwafidia hawa, basi manispaa zile ziwajibike kulipa fidia kwa wananchi ambao walitoa ile ardhi na mpaka wananchi wakapewa hati.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, na mimi niseme kile kifungu namba 26 pamoja na vifungu vingine ambavyo vimependekezwa na Kamati yetu ya Miundombinu, basi Serikali iweze kuzingatia kwa sababu vifungu vingine vina mapungufu makubwa, na hasa hiki kifungu namba 26 ambacho kinamruhusu Mdhibiti wa TRL au wa Shirika la Reli kwenda kukagua peke yake bila kuishirikisha Serikali, ile ni hatari.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ile reserve ya reli iweze kuongelewa vizuri kisheria, reserve ya reli imekaaje, iweze kuwa sawasawa na barabara, barabara kuna beacon. Anaonekana kabisa mtu hata akitaka kuvamia anaona zile alama kwamba hili sasa ni eneo la barabara katika reli haiko hivyo. Sasa ninamuomba Mheshimiwa Waziri kwamba hili waliwekee kipaumbele kwa sababu ni kweli, leo unaweza ukawa unabomoa huku kesho ulikobomoa mwingine anajenga…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja, ahsante.
Muswada wa Sheria ya Wakala wa Meli Tanzania wa Mwaka 2017
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia huu Muswada wa The National Shipping Agencies Act, 2017.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kusema naunga mkono, kama ilivyokuwa kwenye Kamati, uanzishwaji wa hii sheria na pia naipongeza Serikali kwa kuona umuhimu sasa wa kuendelea kudhibiti rasilimali zetu mbalimbali kwa kupitia hizi sheria upya na kuweza kuzifanya ziwe mpya na hasa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dokta John Pombe Magufuli, kwa jinsi anavyosimamia hili suala la kudhibiti rasilimali zetu. Vile vile nampongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kutuletea Muswada huu. Nianze kwa ku-declare kwamba mimi ni mmoja wa Wajumbe wa ile Kamati ya Miundombinu.

Mheshimiwa Spika, Muswada huu ni mzuri, lakini kwenye Kamati kulitokea vitu vichache ambavyo tuliona kwamba vinapaswa kufanyiwa marekebisho na ambavyo naishukuru Serikali kwamba vingi imeona na imefanya marekebisho. Kilitajwa kile kifungu 2(2) ambacho kilikuwa kinaleta mgongano kwa Tanzania Mainland pamoja na Zanzibar, lakini naishukuru na kuipongeza Serikali kwa kuliona hilo na kukiondoa.

Mheshimiwa Spika, lakini tumepata changamoto pia, ambayo nadhani na Kamati nyingine huwa wanapata inapoletwa Miswada mbalimbali hapa Bungeni. Tunapotunga sheria, sheria ni kitu ambacho kwa kweli ni nyeti na kinachukua muda mrefu kuja kukitungia tena sheria mpya au kufanya marekebisho. Kwa kweli muda wa kupitia hivi vifungu ulikuwa ni mchache.

Mheshimiwa Spika, natoa pendekezo kwa Serikali kwamba wanapoleta Miswada mbalimbali basi yale mapendekezo ya Kamati ya kuomba muda kabla ya kipindi cha Bunge kuanza kupata muda wa kutosha, angalau wiki moja, kupitia Miswada hiyo ni kitu muhimu sana. Vinginevyo tutakuwa tunapitisha kitu ambacho kwa kweli kitakuwa kimepitiwa harakaharaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, pamoja na muda huo mfupi, Kamati iliweza kubaini upungufu ambao mwingine umetajwa hapa, kikiwemo hicho kifungu 2(2), lakini pia na kwenye suala la kupendelea wazawa kwenye suala la utoaji wa leseni kama ilivyo kwenye Sera ya Ardhi ya Mwaka 1999; kwamba wazawa kwenye suala la ardhi wamepewa upendeleo ambao ni tofauti na mtu ambaye si mzawa. Kamati ililiona hilo na nashukuru pia Serikali ilizingatia mapendekezo hayo.

Mheshimiwa Spika, tuje kwenye mapendekezo haya ya jina; kama ilivyosomwa hapa ripoti ya Kamati, kwamba jina lile NASAC bado Kamati haikuridhia, lakini kulikuwa na sababu. Kuna majina ambayo tuliridhia kutokana na historia yake. Kwa mfano, tuliridhia kwenye Sheria ya Reli kurudi kwenye jina la zamani TRC, lakini ulikuwepo mchakato wa kuridhia jina hilo kutokana na utendaji wa nyuma wa ile TRC. Jinsi TRC ilivyokuwa imeporomoka ni tofauti kabisa na NASACO ilivyokuwa imeporomoka. Ndiyo maana tukasema kwamba jina hili pengine libadilishwe na ndiyo msimamo wa Kamati, ili kufuta ile taswira ya nyuma ya NASACO.

Mheshimiwa Spika, kuna majina ambayo ukitajiwa yanakukumbusha jambo ambalo si zuri. Kwa wale ambao wanakumbuka Vita ya Kagera; mtu yeyote miaka ile, hata leo, ukimtajia lile neno Mutukula, Kyaka au Mbare, unamkumbusha Vita ya Kagera, kwa sababu ya majina yanayotumika. Vilevile leo ukitaja jina Shauritanga watu wanaokumbuka nyuma, unakumbuka majanga yaliyotokea kwenye ile shule.

Mheshimiwa Spika, sasa tunaporudi na NASAC, NASACO inajulikana ilikufaje. Mimi sioni kwa nini Serikali inapata ukakasi wa kubadilisha hilo jina. Pamoja na kwamba wamesema maudhui, kwani maudhui ni nini, maudhui si unabadilisha tu. Kuendelea na hili jina NASAC, bado tutaendelea kutamka NASACO na wengi watauliza NASACO imerudi? Ni kipi kipya ambacho Serikali imeona kuirudisha NASACO? Watauliza hivyo, lakini itakuwa shida sana kusema hii inaitwa NASAC. Jina ni kama ni lilelile.

Mheshimiwa Spika, tuje kwenye suala la namna gani NASACO ilikufa. Mheshimiwa Waziri kwenye ufafanuzi wake alitueleza na tukaridhika, lakini kuna suala moja ambalo hii sheria mpya inatakiwa unapozungumzia kuanzisha shirika jipya, kwa jina karibu lilelile uoneshe basi hasa kitu gani kimebadilika. Kwa mfano hiki kinachozungumzwa na Waheshimiwa Wabunge wengi hapa, kwamba Serikali itakuwa inacheza mpira yenyewe, referee atakuwa ni mwenyewe.

Mheshimiwa Spika, kilio hiki kimezungumzwa mpaka na wadau ambao wameitwa, lakini tulipata majibu ya Serikali kwamba wamefanya marekebisho ya kuibana Serikali ili isije ika-abuse zile powers zake au ikawa biased katika kutoa maamuzi kuhusu hawa washindani wake wengine. Serikali kwa kufanya hivyo, basi itakuwa imeutendea Muswada huu mema kuliko wangeacha kama ilivyo, kwamba wao Serikali wadhibiti kwa asilimia mia moja na wakati huohuo wawe wanafanya biashara. Kwa kuwa Serikali imesema imefanyia marekebisho vifungu hivyo ili kuibana isiwaonee wengine, basi Muswada utakuwa umekaa sawasawa, lakini mwanzoni ulikuwa haujakaa sawasawa.

Mheshimiwa Spika, kuna jambo najiuliza; hata tukitunga sheria nyingi humu Bungeni, bila kuangalia ni akina nani ambao wanatufanya kila siku tunatunga sheria upya au kuwabana, tutabaki vilevile. Ni ukweli usiopingika kwamba Wakala wa Meli sio anayekagua mzigo ambao unakuwa kwenye kontena, mathalan; wakala ni yule anayekabidhiwa documents zile za mzigo lakini wanaokagua wanakuwa ni wale watumishi ambao wameaminiwa na Serikali, kwa mfano TRA kama wengi walivyozungumza.

Mheshimiwa Spika, sasa hoja yangu ni kwamba hata tukibadilisha hii sheria, je, wale wamedhibitiwa vipi; hawa ambao wanaitia hasara Serikali. Kwa sababu kuna mfano mmoja ametoa Mheshimiwa Mbunge mmoja, ule wa suala la bangi, ni kweli mfano huo tulipewa, lakini wakala hakuona ila aliyeshiriki kwenye kuangalia ni kitu gani kilikuwa kwenye lile kontena alikuwa ni mwakilishi wa Serikali ambaye ni TRA. Sasa kwa kubadilisha hii sheria sijui hawa wa TRA ni walewale. Kwa hiyo isipokuwepo nia madhubuti ya kuwadhibiti hawa watendaji wetu, hata tukitunga sheria nyingi namna gani, tutabaki tuko palepale.

Mheshimiwa Spika, nina mfano mmoja wa watendaji hawa wa Serikali, pamoja na kwamba sisi tunatunga sheria. Nashukuru katika wale ambao ulikuwa umewateua kwenda kwenye makinikia mimi nilikuwa mmojawapo; kuna jambo moja ambalo tuliliona kule ambalo linafanana kabisa na hili la udhibiti wa vitu ambavyo vipo bandarini kwa mfano au vinavyoingia melini, wanaosimamia utathmini wa rasilimali zile za Taifa, hasa kwa mfano almasi, ni viongozi wa Serikali. Wanakuwepo wakati wa tathmini, wakati wa kufungwa na mpaka mzigo unaondoka, tena sio chini ya wanne, wanakuwa wanne mpaka sita. Ule wizi au ubadhirifu, wao wanakuwepo kuubariki kwa sababu huwa wanakuwepo wakati wa kufunga.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, napendekeza kwamba pamoja na hizi sheria tunazozipitisha, udhibiti mkubwa uwe wa kielektroniki kwa maana kwamba zitumike zaidi CCTV cameras kuwadhibiti hawa ambao wanaaminiwa na Serikali, maafisa hawa mbalimbali. CCTV cameras ziwe sehemu nyingi ili ndiyo ziweze kutumika zaidi katika kudhibiti rasilimali zetu za nchi kwa sababu tumeibiwa sana. Wizi ule unafanyika zaidi kwa sababu sehemu nyingi hakuna CCTV cameras, unaweza ukaona hata yule ambaye anakagua mzigo anavyoweza ku-conspire na mwingine na anaweza kuchukuliwa hatua kuliko ilivyo sasa, sehemu nyingi tunategemea mageti na watu haohao ambao wanatuibia kila siku.

Mheshimiwa Spika, kwa haya machache, naomba kurudia tena kwamba naunga mkono Muswada huu.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 2) wa Mwaka 2018
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia huu Muswada wa Sheria Wa Marekebishowa Sheria Na. 2 wa mwaka 2018 yaani the Written Laws Miscellaneous Amendment Act, No. 2 of 2018.

Kwanza nianze kwa kuipongeza Serikali kwa kuleta muswada huu ambao una marekebisho ambayo ni ya muhimu sana, lakini la pili nampongeza Waziri, Mwanasheria Mkuu wa Serikali na timu yenu kwa jinsi ambavyo mlikuwa mmejipanga mlipokuwa mkija kwenye Kamati mlionesha ushirikiano wa hali ya juu mpaka tumefikia hapa tulipo.

Mheshimiwa Mweyekiti, mimi sina mengi sana kwenye muswada huu kwa sababu mambo mengi tulikubaliana kwenye Kamati baada ya Serikali kama nilivyosema ilionesha ushirikiano mkubwa katika kurekebisha vifungu mbalimbali kwa hiyo, nntakuwa na machache.

Mheshimiwa Mweyekiti kwa mfano kwenye sehemu ya sita ya marekebisho ya muswada huu inahusianana Sura ya 89 ambayo inahusiana na ukomo ambayo ni The Law of Limitation Act, Cap. 89. Naipongeza Serikalikatika eneo hili
sana kwa sababu tumekuwa na matatizo mbalimbali na hasa kwenye kesi za msingi ambazo zimekuwa zikitupwa na Mahakama kwa sababu tu ya kitu kinachoitwa legal technicalities. Kesi ya msingi inakuwa inatupwa, muda unakuwa umepita, lakini sasa kwa kifungu hiki kinamruhusu sasa Mheshimiwa Waziri anayehusika na Wizara husika kufungua mashauri nje ya muda. Tumekuwa tukipoteza kesi nyingi hasa kwenye Halmashauri zetu kwa sababu ya kifungu hiki. Kwa hiyo, naipongeza Serikali sana kwa kuleta kifungu hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye sehemu ya 13 ya Marekebisho ya Sheria ya Urejeshwaji wa Mali, Sura ya 256 mali zinazopatikana kwa njia ya uhalifu. Ni kitu ambacho kimetokea mara nyingi sana kwamba hata katika mazingira ya kawaida sio Wabunge tu hata wananchi wa kawaida unaangalia kitu au unaangalia mali za mtu ambazo ukiangalia mazingira ya kawaida ile circumstantial evidence unaona kabisa kwamba mali hizo hazikupatikana kwa njia iliyo halali. Kwa hiyo, kwa kuleta kifungu hiki ni vizuri sana ila isipokuwa tu kwamba kifungu hiki kinapotekelezwa basi mali zile isije ikawa mtu labda ana hinda tu au mtu kaona tu kwamba huyu kwa nini ana mali nyingi basi kifungu hiki kitumike kuhakikisha kwamba haki inatendeka kama ilivyokusudiwa na asionewe mtu kwa sababu haki ya kumiliki mali ni haki ya Kikatiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ibara za 14 mpaka 19 kwenye masuala ya urejeshwaji wa wahalifu yaani extradition. Katika kifungu hiki kulikuwa na takwa hili ambalo lilikuwa linahitaji kwamba mhalifu akae siku 15 kabla hajapelekwa mahali au hajasafirishwa kwenda kukabiliana na tuhuma au shitaka linalomkabili. Hizo siku 15 kuna washitakiwa ambao wanahitajiwa kwa haraka, sasa kwa kuboresha kifungu hiki kwamba mshitakiwa aweze kuletwa hata kabla hazijafika hizo siku 15 basi kitapelekea ufanisi wa kesi pia kwenda haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna ibara ya tisa ambayo inarekebisha kifungu 57 kinachohusu utaratibu wa kurekodi mahojiano. Kifungu kipo vizuri lakini mimi wasiwasi wangu hapa vile vinasa sauti sijui vitakuwa specified namna gani, kwa sababu viko vifaa vya aina nyingi na vingine ni rahisi sana kuwa tempered, sasa sijui Wizara katika hili imejipanga hasa kuwa na vifaa. Je, vitakuwa ni vifaa maalum ambavyo vitakuwa vinafahamika kwamba kifaa hiki hasa ndicho kinachotumika, lakini pia na ubora wa vifaa hivi ili ule utoaji wa ushahidi kwa kutumia vifaa hivi basi usije ukawa una mapungufu.

Mheshimiwa Mweyekiti, lakini kuna sehemu ya sheria hii ya Chama cha Mawakili, mimi naunga mkono kama ambavyo inapendekezwa ingawa kuna vitu vichache na naomba nikatae hii hoja ya kwamba kuna watu specific wanalengwa hapa. Kwa kutungwa sheria hii hapa hakuna specialization yoyote ya mtu kwa sababu wote tunahusika na sheria hii na mara nyingi kwenye practice sheria, haijawahi kutokea kwamba sheria hiyo inafanya kazi kwa Wapinzani imefanya kazi hata kwa Chama Tawala na mifano ipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niseme tu kwenye lile suala la kazi au majukumu ya Baraza la Mawakili pamoja na ile secretariat wakati inaanzishwa sheria hii mwaka 1954 kwa wakati ule ilikuwa ni sawasawa kabisa, lakini mazingira kwa sasa yamebadilika sana, nadhani kuna umuhimu wa kuboresha baadhi ya majukumu ya Baraza, kwa mfano ukiangalia kwenye hii sheria secretariat inaonekana imepokwa majukumu mengisana yamepelekwa kwenye Baraza. Sasa mimi nadhani wayaangalie upya suala la lile ripoti za mwaka kuzipeleka kwenye Baraza hii ilikuwa ni kazi ya secretariat kabisa ukiangalia. Kwa hiyo, mimi naomba Serikali iangalie upya ya katika yale majukumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya machache naomba kuunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa wa Mwaka 2018
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa na mimi nafasi niweze kuchangia huu Muswada ulio mbele yetu wa Sheria ya Vyama vya Siasa. Kwanza nianze ku-declare interest kwamba ni mmoja wa Wajumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria, kabla sijasahau huko nitakakohitimisha nianze kwa kusema naunga mkono Muswada huu kwa asilimia 100, (Makofi).

Mheshimiwa Spika, naomba nianze na Ibara ya 4(2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwa ruhusa yako naomba niisome kwa sababu sio ndefu sana, inasema hivi; “Vyombo vyenye mamlaka ya utendaji vitakuwa ni Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar; vyombo vyenye mamlaka ya kutekeleza utoaji haki vitakuwa ni Mahakama ya Serikali ya Muungano na Mahakama ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, na pia namalizia kwa kusema na vyombo vyenye mamlaka ya kutunga sheria na kusimamia utekelezaji wa shughuli za Umma vitakuwa ni Bunge na Baraza la Wawakilishi.”

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nasoma utangulizi kwanza nilisoma utangulizi, nilisoma wote lakini kwenye utangulizi hapa wenzetu wanajaribu kuwashawishi sio Bunge tu na hata ambao waliopo nje kwamba Muswada huu unapitishwa wengine wakiwa ndani, kuna wengine wako ndani, kuna Viongozi wako ndani wamewataja majina.

Mheshimiwa Spika, sijaona best practice yoyote ambayo wameiandika hapa kwamba kuna Serikali duniani ambayo hata kama mtu ana uhalifu uko nje basi siku kuna Muswada basi anaachiwa aje achangie halafu arudi kule ndani, sijawahi kuona. Ndio maana nimesoma hii Ibara ili kuangalia hivyo Vyombo vitatu kila moja ana madaraka yake, sasa Bunge hili, haliwezi kuingilia wale walioko ndani, hatujui wamefanya nini, ili waweze kuchangia na hiyo haifanyi muswada uwe batili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini, niseme kifungu 6A(3) ambacho kinazungumzia kukasimu Madaraka. Wakati wachangiaji wengine wakizungumza hapa mmoja wa wachangiaji hapa alikuwa anasema mbona Vyama vingine vinaruhusu Kamati Kuu ya Vyama vyao Kukasimiwa Madaraka na Halmashauri Kuu ya Chama.

Mheshimiwa Spika, ni kweli lakini kinachoongelewa hapa kuna vyama vingine tumeona hiyo Kukasimu Madaraka wanaweza wakawa ni watu wawili tu au watatu wamejifungia basi wamekasimiwa Madaraka, hiki ndio kinachoongelewa hapa. Kwa sababu chama ni cha watu wengi, na wanachama wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini Serikali imefanya marekebisho mengi ya Muswada ambao walikuwa wameleta mara ya kwanza tulikaa na Serikali kama ambavyo Serikali wamezungumza, lakini pia na Waheshimiwa Wabunge mbalimbali. Kuna sehemu nyingi sana ambazo tulikubaliana na wenzetu wakiwepo kwa mfano, Kifungu cha 7(6A) (6B) hiki cha pressure groups tulikubaliana kitoke kikatoka Serikali ni sikivu ikasikia ikatoa. Lakini tulikuwa na vifungu ambavyo Kifungu kwa mfano cha Sheria hii Kifungu 24(7) cha kuhusu hati, hati chafu, na vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Spika, tulikubaliana tutoe neno qualified tubaki na disclaimer tulikubaliana, lakini vitu vingi, na kimoja ameongelea mwenzangu hapa ametoka kuongea Mheshimiwa Ally Saleh ambacho nacho kimetoka cha kuunganisha vyama iki-merge Kifungu hiki nacho tulipinga pamoja. Sasa hawa wenzetu wanakwenda nje wanaenda kusema eti, sisi Chama cha Mapinduzi tumekubali ushauri wao, kutoka wapi? Kwa sababu haya yalikuwa ni mawazo yetu sisi kwenye Kamati, na sio kutoka Upinzani, kitu hiki si kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niseme kuna jambo moja, kuna andiko moja nimelisoma mahali kuna mahali andiko lile shetani anawangaa wanadamu, shetani anasema mimi nawashangaa wanadamu, wanadamu hawa ukiwapa kitu cha moto wanakipooza, lakini ukiwapa tena kitu cha baridi nacho wanakipasha moto. Sasa shetani haelewi kwamba wanadamu wanataka nini, wenzetu wameleta mawazo yao kwenye Kamati yamekuwa absorbed tumejadili tukakubaliana. Leo wanaanza kusema haya ni mawazo yao, la kwanza, kitu ambacho si kweli. Lakini la pili tulikubaliana sasa leo mtu anapokuja kusema hii Sheria haifai, nashindwa kuelewa hicho kitu ametoa wapi.

Mheshimiwa Spika, lakini kitu kingine ni suala hili la mali za chama, kwanza nilidhani wenzetu katika Kifungu hiki, ndio wangeunga mkono kwelikweli kwa sababu hapa sisi Chama cha Mapinduzi unajua kabisa hili suala la mali ya chama hata kwetu Chama cha Mapinduzi, mali za chama zinahakikiwa, sasa hapa kuna ubaya gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili linakwenda sambasamba na suala la ruzuku, kama mtu anataka kusaidia au kikundi kinataka kusaidia kudhibiti kitu ambacho ni cha watu wengi, leo mtu anakataa, huyu ana ajenda ya siri. Unataka mali zako zisijulikane kwa nini? Unaficha nini, nashangaa kwa sababu nilifikiria Kifungu hiki wangeweza kukifurahia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wengine wameongelea suala la mwenge. Wenzetu katika kitabu chao wanaandika kwamba wao wanadhani mwenge kazi yake yake iliisha lakini niwakumbushe Bunge hili, siku moja nadhani kama sio Mheshimiwa Haonga lakini kuna Mheshimiwa hapa alizungumzia nembo ya Taifa na akamsema yule ambaye inasemekana au inasadikika kwamba yeye ndiye alianzisha au aliyechora nembo na akasema hapa Bungeni jamani tuenzi vitu vyetu vinavyotuweka pamoja, tumkumbuke na huyu aliyebuni hiki, leo wamegeuka wanasema mwenge tena hauna maana.

Mheshimiwa Spika, mtu anazungumza hapa kwamba tena hii ni ripoti ya chama kwamba mwenge umekwisha kazi yake, lakini hata pale kwenye nembo yetu iliyoandikwa uhuru na umoja mwenge upo pale na wanauona. Sasa leo wanaposema kwamba mwenge umekwisha kazi zake na nembo yake isiwepo, mimi nashindwa kuelewa ideology yao ni ipi, hapa ni kutaka kutupotosha.

Mheshimiwa Spika, naomba niseme la mwisho, suala la ulinzi. Ulinzi wanaouongelea wao ambao ukiuangalia ulinzi huo kwenye taarifa yao wanazungumzia kwamba ulinzi huo lazima uhalalishwe, lakini kwenye ibara ya 20(2)(c) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inakataza vyama vya siasa ambavyo vina vikundi ambavyo vina mwelekeo wa kutumia nguvu. Sasa mtu anapoendelea kung’ang’ania vikundi viwepo wakati Jeshi la Polisi lipo mimi nashindwa kuelewa ana ajenda gani ya siri.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi kifungu hiki nakiafiki kibaki kama kilivyo na hivi vikundi visiwepo kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sheria hizi haziathiri vyama vya upinzani tu, hakuna mahali ambapo sheria hizi tunasema Chama cha Mapinduzi iwe exceptional, hakuna wote tutaathiriwa na sheria hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nasema kwa sheria hii tulipotoka sasa, maana, tukumbuke hii sheria imerekebishwa mara ya mwisho mwaka 2009 miaka kumi sasa, hapa ni mahali pake sheria hii itatuathiri wote, ni nzuri sana, na nasema hivyo kwa sababu ya uzoefu wa kwenye hivi vyama.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, kuhusu hili suala la ufadhili. Wenzetu wamesema kwenye vifungu mbalimbali hata nchi ambazo wamezitaja kwa mfano Ghana na Kenya kuna udhibiti. Leo uanze ufadhili ambao hauwezi kudhibitiwa hiyo ni hatari kwa usalama wa nchi lakini pia ni hatari kwa usalama wa vyama vyetu vya siasa. Mimi naunga mkono ufadhili wa kutoka nje uendelee kudhibitiwa na haitaathiri vyama vya upinzani tu, hata chama tawala kitaathirika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 7) wa Mwaka 2019 (Toleo la Kiingereza)
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa dakika ni chache, nilikuwa na vifungu vingi vya kuzungumzia, lakini naomba niongelee tu kimoja zaidi kwenye hii sehemu ya sita kwenye hii Sura 431, kifungu cha 15 ambayo inahusiana kwa ujumla na suala hili la watoto wadogo kufanya self-testing kwenye mambo haya ya UKIMWI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na data; kwa kuwa nchi nyingi hapa zimetajwa ikiwemo Lesotho, South Africa, Uganda na zingine, mimi nakwenda kwenye hii iliyoendelea zaidi yaani kwa maana ya Afrika Kusini. Kwa data zilizopo ni kwamba Afrika Kusini mwaka 2012 walikuwa na maambukizi kwa asilimia 12.2 lakini mpaka 2018 wamekuwa na maambukizi kwa asilimia 24.7, imepanda karibu mara mbili na hawa ndiyo ambao wanatolewa mfano mzuri huo wa miaka 12.

Kwa hiyo, napenda niishukuru Serikali kwa kuleta Muswada huu lakini pia kuleta ufafanuzi wa e-age of consent kwa sababu pamoja na Afrika Kusini kwamba ni nchi imeendelea sana lakini pia imetolewa mfano, baada ya wao kuruhusu hii miaka 12 kwamba ndiyo iwe ya kupima, haijaonesha improvement yoyote. Afrika Kusini sasa maambukizi yameongezeka maradufu, na kama walivyosema wenzangu naunga mkono, mtoto yule bado ni mdogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtoto wa miaka 12 wa kwetu sisi huwezi kumlinganisha na mtoto kwa mfano wa kizungu, hata appearance yake ni tofauti kabisa, ni katoto kadogo sana. Kwa data hizo hizo, watoto ambao wanaathirika kuanzia maika 10 mpaka 14 kwa ripoti zetu za ndani ni asilimia 0.03 kwa mujibu wa data zilizopo. Wengi wa watoto hawa wanapata maambukizi kupitia kwa wazazi wao na hasa wakati wa kujifungua, ndo data zilizopo. Kwa hiyo, suala la kusema watoto wapime katika umri huo haliwezi kuwa justified katika miaka 12, miaka 15 inatosha kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa sababu muda ni mfupi nitoe tu ushauri, mara nyingi tunasema moja ya maambukizi ni pamoja na watu kutumia madawa mbalimbali, ni kweli data zile zinatisha za watu kutumia hizi dawa mbalimbali, lakini kwanini wanazitumia! Kwa mfano watu wanapotumia hizi dawa za kuongeza nguvu na nyingine, tunasema wengine ni kwa ajili ya chakula na style yetu ya maisha, lakini hatuongelei sana akili, hatuongelei jinsi ubongo wetu unavyooathirika. Sasa hivi kuna tatizo moja linawapata vijana wadogo sana na hasa wenye umri mdogo kutumia hizi dawa mbalimbali. Kwa ushauri wangu watu wa afya wanapotoa ushauri mbalimbali, vijana wengi wanakutwa na msongo wa mawazo wengine kwa sababu ya maombi tu mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata mtoto mdogo, kama mmemuona mtoto mdogo anapokuwa anajisaidia ile haja ndogo, anapokojoa kwa mfano ukimstua yule mtoto ule mkojo unarudi ndani, haendelei. Sawa sawa na kijana leo ana mshahara mdogo labda wa 1,000,000 ukitoa makato mbalimbali anabaki labda na 500,000, 600,000 ghafla anakuja, anaweza kuwa mvulana au msichana analeta ombi la 1,000,000. Huyu hizi nguvu anatoa wapi! Ni lazima awe na mfadhaiko wa mawazo, lakini athari za kutumia hizi dawa tuwe wakweli, tuambiane kwa data.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kuna nchi moja ya hapa karibuni ya…

MWENYEKITI: Ahsante, Mheshimiwa Mollel.

MHE. EMANUEL A.MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 3) wa Mwaka 2019
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuanza kuchangia hoja. Kwanza nimpongeze Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kutuletea hii Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Na.3 (Written Laws Amendment Bill of 2019).

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wangu kwanza naona haya marekebisho kama yalikawia kidogo. Huu ndiyo wakati wake muafaka kuletewa haya marekebisho, kwa hiyo naipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaanza kuchangia moja kwa moja, nilikuwa nasoma maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kuhusu Muswada huu nikianzia na pale alipotoa mifano msomaji kwamba Muswada huu kwa uharaka wake haukupata baadhi ya maoni ya wadau na akawataja wale ambao ni Wakala wa Meli.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimkumbushe msoma taarifa wa Kambi Rasmi ya Upinzani kwamba kwa mujibu wa Ibara ya 64 (1) ya Katiba yetu ya Nchi, Bunge ndiyo lenye mamlaka ya kutunga sheria mbalimbali kwa niaba ya wananchi, lakini pia kwa mujibu wa Kanuni yetu ya 84 ya Kanuni za Kudumu za Bunge, Kamati hailazimiki kupokea hayo maoni ya wadau kama ambavyo ameainisha yeye, lakini pia kwa taarifa yake tu ni kwamba tulipata maoni ya wadau wengi sana ikiwemo na Benki ya Dunia ilileta mwakilishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza pia Serikali kwamba imekuwa sikivu sana kwenye ushauri wa Kamati. Kwenye sehemu mbalimbali ya Muswada huu, Serikali imeridhia maoni mengi ya Kamati, kwa mantiki hiyo, naipongeza sana Serikali. Nikianza na suala la definition kwenye Sheria ya Makampuni, Sura 212, Kamati ilikuwa imependekeza kwamba kuwe na ile tafsiri ya zamani kwa ajili ya kuweka wigo mpana kwenye masuala ya biashara, lakini nashukuru pia kwamba Serikali imeweza kuchukua maoni mengi ya Kamati.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia Kifungu hiki cha 6 ambacho kinahusiana na suala la ku-comply kwa makampuni yale ambayo yalikuwa registered chini ya Sheria ya Makampuni na yanatakiwa kuhamia kwenye sheria zingine, ule muda wa miezi miwili, Kamati sisi tulipendekeza iwe miezi mitatu kwa sababu ni suala tu la compliance kwamba wafuate sasa taratibu ambazo zinawaondoa kwenye Sheria ya Makampuni kwenda kwenye sheria zingine kwa mfano Non-Government Organization Act. Kama kampuni itakwenda kule basi Kamati tulipendekeza kwamba kuwe na suala tu la Mheshimiwa Waziri kuweza kuweka kwenye schedule of amendment ili yule mtu ambaye anahamia kwenye sheria zingine aweze kupata muda wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sitaongelea vifungu vingi ili na wenzangu waweze kuchangia, nitakwenda katika vifungu vichache na hasa vile vilivyopata malalamiko mengi. Kwa mfano, ukienda kwenye kifungu cha 10 cha Sheria ya Makampuni, Sura 212 ambayo imelalamikiwa sana kuanzia kwenye Kifungu 400(1), Serikali pia katika sehemu hii tunashukuru ilipokea mapendekezo yetu. Pia kuna terminology ambayo imekuwa imeleta shida sana ambayo ukisoma ile 400A(1) hili neno reasonable cause to believe lilileta shida sana kwamba pengine maeneo haya Msajili anaweza kuwa biased, Msajili anaweza tu kuamua anavyotaka yeye, lakini Serikali katika kifungu hiki ilituhakikishia kwamba kutakuwa na room ambayo yule ambaye hakuridhika na kile ambacho kipo pale anaweza kukata rufaa na hiyo inakwenda mpaka kwenye kifungu 400A(2)- (7), vifungu hivyo vitamfanya Yule ambaye hakuridhika aweze kukata rufaa. Katika hili kama Kamati tuliomba Ibara ya 13(6)(a) iweze kuzingatiwa ili yule ambaye atakuwa anakata rufaa aweze kuona amepata haki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna sheria hii ambayo inausiana na taasisi zisizokuwa za Kiserikali, (Non-Government Organization), Cap. 56, hili suala pia hapa lilileta shida sana kwenye mjadala wa Kamati kwa sababu wengi wa wadau walikuja na hoja ya kwamba miaka 10 kusiwepo na hiyo renew ya registration, lakini wadau wale kwa sababu walikuwa wanajirudiarudia tuliwaomba pia watupe best practice ya nchi zingine katika hili kwamba je, wanataka sheria hiyo idumu moja kwa moja kwamba mtu asiwe hata anakuwa reviewed na vitu kama hivyo. Wadau wengi katika sehemu hii walishindwa kufafanua best practice kwamba ni nchi gani hizo ambazo zinaaachia tu mtu anakwenda kwa sababu alisajili NGO, basi hata kama anakwenda kinyume cha matakwa basi aendelee kuachiwa tu. Wadau wengi walishindwa kufafanua, kwa hiyo sisi kama Kamati, eneo hili tunaiunga mkono kabisa Serikali kwa marekebisho ambayo wameleta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala hili la Sheria za Takwimu, Sura 351. Kuna kifungu kile 37(4) ambacho kinapendekeza adhabu kwa mtu yeyote ambaye atatoa takwimu ambazo hazijapata kibali kutoka Ofisi ya Takwimu ya Taifa. Sisi Kamati tunaunga mkono eneo hili kwa sababu bila kudhibiti hizi takwimu zinaweza kutuletea madhara makubwa sana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Muswada wa Sheria ya Usimamizi wa Maafa, 2022
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia huu Muswada wa Sheria ya Maafa. Naipongeza sana Serikali kwa kuona kwamba kuna umuhimu wa kuboresha hii Sheria ya Maafa hasa baada ya kufuta ile Sura 242 ambayo ndio tulikuwa tunaitumia kabla ya hii mpya. Hata hivyo, nina mchango mdogo kwamba tunapofuta ile sura 242, je, kwenye hii mpya tutakuwa na kitu gani kipya ambacho kinaweza kuboresha hii Sheria yetu ya Maafa.

Mheshimiwa Spika, maafa ambayo yanaleta majanga ni kitu cha ghafla, ni kitu cha dharura, mara nyingi huwezi kujua kinatokea wakati gani. Bado nasema ni muhimu sana kuzuia kabla ya jambo lenyewe halijatokea. Kwa mfano, kuna majanga ambayo tunayaona kabisa kwa macho na watu wanapita, kama vile mtu kuchimba kwenye daraja mchanga na tunajua kabisa, watu wa mamlaka mbalimbali wanapita pale kwa mfano madaraja ambayo na treni inapita, inachimbwa michanga pale.

Mheshimiwa Spika, sasa treni itakapokuja kuanguka kwa bahati mbaya katika maeneo yale, yale ni majanga ambayo tungeweza kuyazuia kabisa. Sasa kitengo hiki ambacho kiko chini ya Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu hii Division ya Maafa ni vizuri sana wakawa wanaangalia kwanza kuzuia kuliko kuangalia namna gani watashughulikia hayo maafa.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa napitia best practice kwenye nchi za wenzetu, sana kwenye kamati tuliangalia nchi karibu mbili; tuliangalia ya India kama alivyosema Mwenyekiti wetu wa Kamati kwenye ripoti, lakini pia na Afrika Kusini. Kwa mfano wenzetu wa Afrika Kusini wana kitu kinaitwa Disaster Management Act ya mwaka 2005, ndani yake kuna Mpango wa Taifa wa namna ya kushughulikia mikakati maalum ambayo mingine kama itampendezesha Mheshimiwa Waziri, kuna sehemu ambazo ni muhimu sana kwa mfano chapter 12 kwenye hizo guidelines zao, kuna minimum standards za relief kunapotokea majanga.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, yale majanga ambayo yako kwenye ile magnitude kubwa kabisa, kuna watu wanakuwa wamekopa fedha benki kwa mfano na kipindi kile cha majanga hawa hawawezi kulipa tena benki, lakini wakati huo benki zinaendelea kuwachaji interest na vitu vingine.

Mheshimiwa Spika, sasa wao wana-relief standards za kuangalia magnitude ya ile disaster yenyewe watawasaidia watu namna gani, lakini ukiangalia hiyohiyo ya wenzetu wana special provisions kwa watu ambao ni wajane, lakini pia na kwa orphans. Wanaangalia kwamba sasa watu hawa tutawasaidiaje katika kipindi kama hiki cha majanga makubwa kwamba hawa yatima pamoja na wajane wanasaidiwa kuna special unit kwa ajili ya kuwasaidia hawa. Kwa hiyo na sisi ni vizuri pamoja na kutunga vizuri hii sheria yetu tuangalie na wengine wanafanikiwa namna gani ikiwemo hiyo ya wenzetu wa Afrika Kusini.

Mheshimiwa Spika, niipongeze Serikali kwa kuondoa mlolongo wa Mheshimiwa Waziri kwenye ile Sura Na.6 kipengele (c) kuondoa yale mamlaka ya Mheshimiwa Waziri ya kukamata mali ya mtu yeyote ambayo ingeweza kutumika wakati wa majanga. Kulikuwa na shida na hasa majanga yanapokuwa yamepita au yamepungua kwa kuwa na shida kubwa inatokea namna ya kuwa-compensate, kuwalipa fidia hawa ambao mali zao zilikuwa zimechukuliwa kwa ajili ya kutumika kwenye majanga. Sasa kwa kuwa pia na Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wameondolewa madaraka hayo zimebaki taasisi peke yake, naishukuru sana Serikali kwa kukubali ushauri wetu Wanakamati na kuondoa vipengele vya namna ile.

Mheshimiwa Spika, lingine limeongelewa hata kwenye ripoti yetu kulikuwa na mlolongo wa kamati watu ni wengi mno, inatokea janga inaanza mikutano ya wale wanakamati ni wengi kweli, mpaka watu wanakwenda kwenye tukio mambo yalishaharibika zamani kwa sababu ya wingi wake na kwa kadri watu mnavyokuwa mko wengi mnaangalia na akidi nayo vilevile inakuwa shida, lakini kwa kukubaliana na ushauri wa Kamati kupunguza idadi ya hawa ambao wanashughulikia maafa, naipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Spika, hii Sera ya mwaka 2004 ambayo tunaitumia ya mambo ya Sera ya Taifa ya Maafa, sera ile ni nzuri ingawa tumependekeza iboreshwe, sasa shida ya sera ni moja hata ingekuwa nzuri sana mara nyingi sera kwenye sheria not enforceable yani ile sera yenyewe uwezi ukaifanyia kazi moja kwa moja kisheria hata ingekuwa ni nzuri kiasi gani. Sasa waangalie katika kuendelea kuboresha hizi sheria zetu za maafa yale mambo ambayo ni mazuri sana kwenye sera zetu tuweze kuyaingiza kwenye sheria kamili.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya machache, naunga mkono hoja na ahsante kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)