Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla (182 total)

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika ahsante, nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza, Waziri amekiri hapa kwamba kati ya mwaka 2011/2014 waliandaa mpango wa majaribio wa kuwaondoa watoto hawa wanaoishi katika mazingira hatarishi, na suala la watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi linaeleweka, na ni kubwa ndani ya nchi hii. Ni kwa nini Serikali hii ya CCM mnafanya mipango ya majaribio ambayo inatumia muda mrefu, fedha nyingi na yenye matokeo machache au matokeo kidogo?

Swali la pili, umekiri katika majibu yako kwamba meaandaa Mpango Kazi wa kuweza kuwaondoa watoto hao wanaoishi katika mazingira hatarishi. Ni kwa kiasi gani Mpango Kazi huu umekuwa shirikishi kwenye Serikali zetu za Mitaa kwa maana ya Halmashauri, ili na wao waziweke katika bajeti yao, ili kwa pamoja waweze kuona watoto hawo wanaondoka katika mazingira hatarishi?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Asante, nakushukuru Mheshimiwa Spika kwa kunipa nafasi hii, na ninakushukuru Mheshimiwa Paresso kwa kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza kwamba ni kwa nini Serikali inaandaa mpango wa majaribio ni kwa sababu za kitaalamu. Hauwezi ku-embark kwenye mradi mkubwa utakaolihusisha Taifa zima kwenye Mpango Mkakati wa kuwaondoa watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu bila kufanya pilot study. Labda kiswahili tu kinaweza kikawa kinasumbua lakini kwa namna yoyote ile kwenye operational research na kwenye programming huwa tunaanza kwa kufanya pilot study ambayo ikifanikiwa tutakuwa tumejifunza changamoto zilizopo na baada ya hapo sasa tunaweza tuka scale up kwenye eneo kubwa zaidi. Kwa hiyo, kuanza na pilot study ni taratibu za kawaida tu kwenye programming.

Swali la pili, ni kwa namna gani mpango huu umekuwa shirikishi, majibu ni kwamba wakati unafanya pilot study jambo la kwanza ambalo unalolifanya ni kufanya table research. Ni kufanya utafiti wa mezani, unasoma tafiti mbalimbali, unaangalia nyaraka mbalimbali lakini baada ya hapo unatengeneza dodoso ambalo unawashirikisha wadau mbalimbali, na mwanzoni sasa unafanya formative assessment maana yake unawakusanya wadau, unawashirikisha kwenye utafiti wako wa awali ambao umeufanya kwa kutumia nyaraka mbalimbali na baada ya hapo sasa wale wadau waliopo watakupa, mawazo utajifunza changamoto kutoka kwao, utaziona fursa kutoka kwao, utaweza kupanga mbinu kwa pamoja na wao na kwa maana hiyo wanakuwa sehemu ya mradi husika.

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza;

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini ujenzi ule kimsingi umesimama na hakuna kinachoendelea pale Hospitali ya Mitengo.

(a) Je, ni lini sasa Serikali itaanza kuendeleza ule ujenzi wa Hospitali ya Kanda pale Mitengo?

(b) Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ujenzi wa hospitali hii bado umesimama na wananchi wa Kanda ya Kusini na hasa wale wa Mtwara Mjini wana changamoto za kupata matibabu bora ya tiba, lakini kimsingi kwamba Hospitali ya Ligula, hospitali ambayo ni Hospitali ya Mkoa hakuna x-ray, x-ray zimeharibika na ni muda mrefu hivi sasa wananchi wanahangaika kutembea umbali mrefu kwenda kufuata x-ray Mkoa wa Lindi na Dar es Salaam. Je, Serikali ipo tayari hivi sasa kuleta x- ray mpya ambazo zitaweza kutumika kwa ajili ya kuboresha tiba za wananchi wa Mtwara?
NAIBU WAZIRI WA AFYA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwanza, kwamba ujenzi umesimama siyo kweli, kwa sababu mara tu baada ya mimi kupewa heshima hii ya kuhudumu kwenye Wizara hii kama Naibu Waziri nilipoanza kazi tarehe 19 Disemba, 2015 nilifika mimi mwenyewe binafsi kwenye Hospitali hii ya Kanda ya Kusini kwenye eneo la Mikindani.

Nilifika na nilijionea mimi mwenyewe na nilifanya ziara ya kushtukiza kwa maana hiyo hakuna hata mtu mmoja Mkoani Mtwara ama Lindi aliyekuwa anafahamu kwamba siku hiyo kuna Naibu Waziri wa Afya angefika, na wala hata Mkuu wa Mkoa hata RMO hawakujua. Nilifika na nikapitiliza mpaka site na nilikuta kuna mafundi wapo site wanaendelea na ujenzi. Kwa maana hiyo siyo siasa tu na ndiyo maana tukisema hapa kazi tu, tunamaanisha tupo kazini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili kuhusu x-ray nimpongeze Mheshimiwa Nachuma kwa jitihada zake anazozifanya kufuatilia uwepo wa vifaa tiba, vifaa na vitendanishi kwenye hospitali hii. Alifika kwenye ofisi zetu akiulizia lakini pia Mbunge mwingine wa Nachingwea naye alifika mpaka ofisini kwangu na bahati nzuri alinikuta na tukazungumza, labda niseme tu kwamba kuna matatizo ya hapa na pale kwenye vifaa vya imagine, x-ray, Ct-Scanner, MRI na vitu vingine kama hivyo.

Mheshimiwa Spika, lakini tupo kazini tunayafanyia kazi, tunabuni mbinu mbadala za namna ya kuziwezesha hospitali zote nchini kuwa na vifaa vya uhakika kupitia mipango mbalimbali na muda si mrefu mikakati yetu ikiiva nchi hii, matatizo ya Ct scanner, matatizo ya MRI, matatizo ya x-ray yatakuwa historia.

Mheshimiwa Spika, mtupe muda kidogo tu mkakati huu utakapo kamilika Tanzania mpya mtaiona ikiwa imefika na mtaanza kufaidi matunda ya uwepo wa Serikali ya Awamu ya Tano ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri Kigwangalla, kwa niaba ya wananchi na wanawake wa Zanzibar, tunapenda kuishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuridhia kufungua Benki ya Wanawake, Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kumshukuru Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kukubali kutoa ofisi yake. Ahsante sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa baadhi ya Wabunge wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tulikuwa ni miongoni mwa waanzilishi wa benki hii kwa kutoa hela zetu kuweka hisa, lakini mpaka hii leo hatujui chochote kinachoendelea na hatujapatiwa gawio la hisa kutokana na Benki hii ya Wanawake.
Je, Serikali itaanza lini au inasema nini kuhusu gawio letu la hisa la wananchi wote, sio lazima Wabunge tu na wananchi wote? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kabla sijajibu swali lake, nitumie nafasi hii kwa namna ya kipekee kumpongeza sana aliyekuwa Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Mheshimiwa Sophia Mnyambi Simba, kwa chachu ya kuanzisha benki hii. Pia nimpongeze aliyekuwa Naibu Waziri wa Wizara hiyo ambaye sasa ni bosi wangu, Mheshimiwa Ummy Ally Mwalimu, kwa kutia chachu ya kukua kwa kasi ya benki hii. Zaidi nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, kwa kujitolea kufanya uamuzi makini wa kuchangia mtaji kwenye benki hii wa shilingi bilioni mbili kila mwaka. Naamini Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ataendelea kuipa uwezo benki hii kwa kuendelea kutekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwapongeze Wabunge wote wa Viti Maalum ambao nao kwa dhati kabisa waliamua kujitolea michango kwa kununua hisa kwenye benki hii. Kilichokwamisha wao kupata hisa hizi rasmi kwa maana ya utaratibu wa kisheria ni kwamba wakati benki inaanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Makampuni ya mwaka 2002, Cap. 212, ilikuwa imesajiliwa kama Private Limited Company. Kwa maana hiyo ilikuwa na benki binafsi ya wanahisa binafsi ambao walikuwa wameteuliwa kuianzisha benki hiyo na Mheshimiwa Rais wa wakati huo na kwa maana hiyo Wabunge walipochangia michango ile kwa maana ya kununua hisa kwa ajili ya kujiunga kwenye benki hii haikuweza kurasimishwa kwa haraka kwa sababu ya utaratibu wa kisheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumbukumbu za Wabunge wote walionunua hisa pale awali wakati benki inaanzishwa zipo. Machi, 2012 baada ya kutambua michango hii ya Waheshimiwa Wabunge wote wa Viti Maalumu bila kujali itikadi zao, ilionekana kwamba usajili wa benki kwa mujibu wa sheria ubadilike, badala ya kuwa private sasa iwe public kwa maana ya kuwa Public Limited Campany ambapo kwa mujibu wa sheria sasa inaruhusiwa kuongeza wanahisa wengi zaidi. Lakini benki imeenda mbele, sasa hivi itakuwa benki ya wananchi wote kwa maana ya kwamba tuna mkakati wa ku-issue IPO, kufanya Initial Public Offering kwenye Soko la Hisa ili wananchi wengi zaidi wanunue hisa na iweze kuwa na mtaji mkubwa na kufika kwa wananchi wengi zaidi. Kwa maana hiyo, wale Wabunge walionunua hisa wakati huo, watapewa hati rasmi za hisa zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kupewa hati rasmi za hisa na wananchi wengine watakaonunua hisa nao pia watapewa hati za hisa hizo. Sasa benki kwa kuwa imeanza kupata faida kuanzia mwaka jana na mwaka huu, itaweza kutoa gawio. Huo ulikuwa ni utaratibu wa kisheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakusukuru kwa kunipa nafasi hii.
MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba kuuliza kama ifuatavyo.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kauli chafu za baadhi ya wahudumu zinatuumiza sana mioyo yetu sisi wanawake hasa pale tunapokwenda kujifungua. Nikisema mfano hapa utalia, sitaki niseme mfano maana yake mambo mengine aibu. Je, Serikali inawachukulia hatua gani wahudumu kama hao na wako wengi tu? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa, katika Tanzania kuna wale Wakunga wa jadi ambao hasa hasa vijijini wanatusaidia sana sisi wanawake wakati tunapojifungua. Naomba kujua kwamba, je, Serikali inawathamini vipi Wakunga hawa wa jadi ili kuwaweka katika mazingira mazuri au mazingira rafiki? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba tu Mheshimiwa Dada yangu Mheshimiwa Faida Mohammed Bakar asitoe machozi na naomba nimjibu kama ifuatavyo; kwamba Serikali inawachukulia hatua gani wahudumu ambao wanatoa lugha chafu kwa wateja. Kwanza Serikali imeweka utaratibu mzuri sana wa kukusanya maoni na malalamiko ya wateja kwenye mahospitali yote. Pia Mheshimiwa Waziri wa Afya, Mheshimiwa Ummy Ally Mwalimu ambaye ni champion wa haki za uzazi na watoto hata kabla hajawa Mbunge amefika tu Wizarani na ameanzisha utaratibu wa kuwa na namba maalum ambapo maoni ya wateja kutoka popote pale, kona yoyote ya nchi yetu wanaweza wakayawasilisha kwenye namba hiyo na sisi moja kwa moja tukayashughulikia.
Mheshimiwa Spika, sambamba na jitihada hizo Mabaraza ya Weledi kwa maana ya Mabaraza ya Wauguzi, Mabaraza ya Madaktari, Mabaraza ya Wafamasia yana utaratibu wa kimaadili wa kuchukua hatua dhidi ya wataalam ambao wamesajiliwa na Mabaraza hayo pindi ushahidi utakapopelekwa kwenye mabaraza hayo na wana nguvu ya kimahamaka wakikaa kwenye Baraza la Kimaadili pale wanakuwa na nguvu ya Mahakama ya Hakimu Mkazi na kwa maana hiyo wanaweza kuchukua hatua za kisheria ikiwemo kuwaadhibu wataalam hawa kwa kuwapeleka jela.
Swali la pili, kwamba Serikali ina mikakati gani ya kuboresha huduma hizi? Tumejipanga vizuri Wizarani kuboresha huduma za akinamama wajawazito na watoto na hasa kuanzia ngazi ya kwenye jamii, kwa maana ya kuwatumia vizuri wakunga wa jadi. Serikali inawawezesha vipi jibu ni kwamba Serikali yetu ina utaratibu wa kuwapa mafunzo wakunga hawa wa jadi kwa maana ya traditional birth attendant kule kule kwenye maeneo yao, lakini pia kuwapa vifaa.
Mheshimiwa Spika, wanapewa vifaa kama gloves, pia kama wakigundua kuna tatizo kwa mama mjamzito mapema kabla hata siku ya kujifungua haijafika, wamepewa maelekezo ya namna ya kuwapa rufaa kuingia kwenye mfumo rasmi ya kutoa huduma za afya ya uzazi kwa akinamama. Kwa maana hiyo, wanapewa mafunzo wanathaminiwa, wanapewa vifaa na wanapewa maelekezo ya kuwa absorbed kwenye mfumo rasmi wa huduma ili akinamama hawa waondokane na hatari za kutibiwa katika hali ya complications na watu ambao hawana special skills za kuweza kutoa huduma hizo.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nataka tu kumthibitishia Mheshimiwa Faida na Waheshimiwa Wabunge na Watanzania tumeshatoa maelekezo kwa watumishi wetu wote katika sekta ya afya kuvaa vitambulisho. Kwa hiyo, pindi unapohudumiwa kitu cha kwanza ni vizuri uangalie anayekuhudumia ni nani, ni Ummy Ally Mwalimu na pale unapopata matatizo, tuletee jina la huyo mhudumu na tumesema hatutavumilia lugha chafu kwa wahudumu wetu kwa hiyo, tuletee jina na tutawapeleka katika Baraza la Wauguzi na Wakunga Tanzania na nimeshalielekeza baraza liongeze jitihada katika kuhakikisha tunarudisha nidhamu na maadili katika utumishi wa sekta ya afya. Kwa hiyo, Mheshimiwa Faida naomba usilie suala lako tunalifanyia kazi. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwenye swali langu la msingi nimeelezea dhahiri kwamba hospitali ya Mji wa Tarime inatoa huduma kwa Wilaya nzima ya Tarime na baadhi ya wananchi wa Serengeti na Wilaya ya Rorya. Serikali imekuwa ikileta fedha za OC na bajeti ya dawa, kwa kufuata population ya Mji wa Tarime ambayo ni watu 78,000. Ppia imekuwa ikileta, fedha la kapu la pamoja kwa maana ya basket fund, milioni 106 tu ambayo haikidhi haja na zamani tulikuwa tukipokea zaidi ya milioni 500 bado huduma za afya zilikuwa siyo dhahiri.
Mheshimiwa Spika, swali langu ni kwa nini Serikali sasa, isiweze kuleta fedha za OC na za basket fund kwa kufuata population walau ya Tarime Rorya na siyo ya Mji wa Tarime, ukizingatia kwamba tunatoa huduma kote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wananchi wanaopata huduma ya afya kwenye hospitali ya Mji wa Tarime, wamekuwa wakitozwa sh. 6,000 lakini wakifika ndani hawapati madawa, hawapati huduma zinazostahili, ni kwa nini sasa Serikali kwa maana katika Hospitali ya Mji wa Tarime tayari tuna jengo ambalo liko tayari, kuweza kufungua duka la dawa kwa maana ya MSD ni kwa nini sasa Serikali isiweze kuja na kufungua hilo duka pale kwenye hospitali ya Mji wa Tarime ili wananchi waweze kupata huduma ya madawa wanavyoenda kutibiwa pale kuliko kuhangaika tena wanatoa sh. 6,000 halafu akitoka nje anaambiwa hamna dawa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, swali la kwanza ni kwa nini Serikali, isichukulie takwimu kwamba Hospitali hii ya Mji wa Tarime inatibu pia wateja kutoka Rorya na maeneo mengine ya jirani. Jibu ni kwamba Serikali siku zote inapopanga Mpango wake wa Bajeti kwa ajili ya kuzihudumia hospitali zote nchini ina formula maalum ambayo inazingatia kigezo anachokisema cha idadi ya watu wanaohudumiwa katika hospitali. Pia, pesa zote zinazotoka kwa wafadhili zinapangwa kwenye bajeti kutokana na burden of desease, mzigo wa magonjwa ambao unahudumiwa katika eneo la kijiographia ambapo hospitali hiyo inatoa huduma.
Kwa hivyo, watu wote wanaofanya planning kwenye sekta ya afya, wanazingatia kigezo cha idadi ya watu, lakini pia mzigo ambao hospitali husika inaubeba kwa maana ya kutoa huduma zake. Kwa maana hiyo, niseme tu maelezo ya ziada hapa kwa Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo:
Mheshimiwa Spika, kwamba changamoto ya kuwahudumia Watanzania kwenye eneo hili la dawa, vifaa na vifaa tiba ni kubwa sana, kwa maana ya mzigo wa kibajeti ambapo Sekta ya Afya inabeba. Changamoto hiyo itaweza kutatuliwa kwa jitihada ambazo tunazifanya sasa hivi za kuhakikisha Watanzania wote wanakuwa na bima ya afya, hili ni jambo ambalo lipo kwenye Ilani ya Uchaguzi pesa tulizonazo sasa ni ndogo haziwezi kubeba mzigo wa kutibu Watanzania wote kama ambavyo tunatamani iwe, sasa tunakuja na jitihada mpya ya kuhakikisha Watanzania wote wanaingia kwenye Mfuko wa Bima ya Afya ili hospitali zenyewe ziweze kukidhi mahitaji ya madawa, vifaa tiba na vitendanishi kama ambavyo zinajipangia.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, kuhusu duka la dawa la MSD. Nimpongeze Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko na wataalam wetu wa sekta ya afya kwenye hospitali ya Mji wa Tarime, kwa kuandaa eneo kwa ajili ya kuanzisha duka la MSD. Kwanza nitumie nafasi hii kwa namna ya kipekee kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli. Kwa kuanzisha mkakati, wa kufungua maduka ya MSD yaani MSD Community outlets.
Maduka haya kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais yanatoa huduma kwenye hospitali ya Taifa na hospitali za Kanda kwa maelekezo yake, lakini kwa kuzingatia mahitaji ya Mikoa na Wilaya zote nchini kwamba wangependa kuwa na maduka ya MSD, ili waweze kuhakikisha wananchi wanapata dawa kwa ukaribu na kwa gharama nafuu zaidi, ndani ya hospitali kuliko kuzifuata nje ya hospitali. Wizara yetu imewaelekeza MSD waandae Mpango Mkakati wa kutoa utaalam wa kiufundi wa namna ya kuanzisha maduka ya dawa, katika mfumo huu wa MSD community outlets. Taasisi yetu ya MSD, imejipanga kuwasaidia Milkoa.
Pia Taasisi yetu ya NHIF imejipanga kuingia kwenye mkakati wa kuwakopesha hospitali yoyote ile iwe ya Mkoa ama ya Wilaya, fedha kwa ajili ya kuanzisha maduka haya na MSD itatoa technical support, ikiwepo mifumo ya kuendeshea maduka haya kama mifumo ya computer ili kuweza kuyaendesha kisasa zaidi na katika mtindo ule ule ambapo maduka yetu ya MSD community outlets yanaendeshwa.
MHE. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Kwa kuwa tatizo hili la Rorya linafanana na tatizo la Iringa Mjini, baada ya kujua tatizo la hospitali ya Rufaa ya Iringa Mjini, Manispaa tumejenga hospitali ambayo inafanya kazi. Hata hivyo, tuna tatizo la vifaa tiba kwa mfano, akinamama wanavyofanyiwa operation wanahitaji wapange foleni kusubiri yale mashuka yakaoshwe kwenye hospitali ya Rufaa, ni lini sasa Serikali itatatua tatizo hili ambalo akinimama kwa kweli wanapata matatizo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Peter Msigwa, Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini kwa swali lake na majibu ya Serikali ni kwamba yeye ni Mjumbe kwenye Halmashauri ya Mji wa Iringa Mjini. Kwa maana hiyo, anashiriki kikamilifu katika uendeshaji kuanzia kwenye kupanga na hata kusimamia utekelezaji wa sera ya afya na sera ya maendeleo ya jamii kwenye eneo lake.
Namshauri ashirikiane vizuri na Halmashauri yake waweze kupanga bajeti kwa ajili ya kununua mashine za kufulia nguo hizo, ambapo zinakosekana kwenye hospitali moja ili aweze kutoa hiyo huduma kwa ukaribu na kwa urahisi zaidi kwa wananchi wanaohitaji.
Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo naomba niseme tu kwamba. Uendeshaji wa hizi hospitali una changamoto kubwa ya kifedha, kama nilivyosema awali, na kwa maana hiyo, Waheshimiwa Wabunge wote wakitaka kutatua matatizo yanayozikabili hospitali zao ni lazima wawe makini kwenye kuelekeza mapato yanayotokana na own source collection za pale kwenye Halmashauri, kwenye eneo hili la huduma za afya.
Maana kila Mbunge sasa amekuwa anatuletea maswali sisi watu wa Wizara ya Afya wakati sisi kazi yetu ni kutoa technical support, kazi yetu ni kusimamia ubora na vitu vingine lakini wao wenyewe Wabunge, wakishirikiana na Madiwani na Halmashauri zao wana jukumu la kutoa huduma bora zaidi kwa Wananchi wanaowaongoza. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Serikali kuamua kufanya tathmini kwenye Mabaraza ya Watoto ni kwamba kuna changamoto ambazo zipo na kuyafanya Mabaraza hayo yasitetee haki za msingi za watoto hasa za watoto yatima.
Je, tunatambua kwamba kuna center za watu binafsi ambazo zinahudumia watoto yatima na zinafanya kazi kwenye mazingira magumu sana nchi nzima ikiwepo na Jimboni kwangu Bunda. Serikali ina mkakati gani wa kusaidia center hizi ili kusaidia watoto yatima waweze kulelewa vizuri na kupata huduma sahihi hasa za elimu kama wanavyopata wengine?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, mmesema Rais aliweka sahihi tarehe 22 Mei, 2015 na kwamba mpaka sasa hivi hamjakamilisha taratibu za kanuni. Ni jambo gani linawakwamisha, hamuoni kwamba kuna haja ya kukamilisha hizi kanuni mapema na mwaka huu wa fedha tutenge bajeti ili Baraza ili lianze na vijana wawe na chombo chao cha kuibana Serikali na kutetea vijana wao katika nchi hii?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nitumie nafasi hii kumpongeza muuliza swali Mheshimiwa Ester Amos Bulaya na aliyeuliza swali la msingi Mheshimiwa John John Mnyika kwa kuendelea kufuatilia haki na maslahi ya vijana wa nchi yetu. Pamoja na pongezi hizo naomba kujibu maswali yake ya nyongeza kama ifuatavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwamba kuna changamoto zinazowakabili watu wenye taasisi ama vituo binafsi vinavyolea watoto yatima na kwamba Serikali inawasaidiaje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina majukumu ya kutengeneza mfumo wa kisheria ambao utaziwezesha taasisi mbalimbali zikiwemo za Serikali na za watu binafsi kutekeleza majukumu yake ya kutoa huduma kwa wananchi kama ilivyopangwa kwa mujibu wa sheria hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo mfumo huo sasa upo na tunatengeneza Mabaraza haya kwa malengo ya kutoa ushauri kwa Serikali juu ya namna bora ya kuendesha taasisi mbalimbali za binafsi ama za Serikali zinazotoa huduma kwa watoto yatima ama watoto wanaoishi katika mazingira magumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwamba tumechelewa kuunda kanuni. Ni miezi takriban sita tu toka sheria ile imesainiwa na Mheshimiwa Rais na sidhani kama tumechelewa. Imani yangu ni kwamba, kanuni zitatengenezwa haraka na zitaanza kufanya kazi kwa sababu mwaka 2015 ulikuwa ni mwaka wa Uchaguzi Mkuu na watu wengi walikuwa busy na kwa kipindi kirefu, hivyo Mawaziri wasingeweza kufanya kazi ya kutunga kanuni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali ipo kazini, naomba atuamini, tutatunga kanuni hizo haraka na tutawashirikisha wadau wote ili mawazo yao yaweze kuwemo humo ndani na mwisho wa siku tutunge kanuni zilizo bora ambazo zitaweza kuleta ustawi wa vijana wa nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu, najua kwamba vyanzo vya kipindupindu hasa ni uchafu na hasa katika maeneo ya mikusanyiko kama vile kwenye masoko. Kwenye haya masoko huwa watu wanalipa kodi, lakini Serikali inashindwa kufanya usafi au kuzoa takataka. Je, Serikali sasa haioni kwamba yenyewe ndiyo chanzo cha kipindupindu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa sasa hivi kuna tahadhari kubwa sana ya ugonjwa wa homa ya zika ambayo homa hii sasa hivi iko kule Marekani ya Kusini, lakini Tanzania siyo kisiwa na wote tunajua kwamba zika ilianzia Uganda kwenye Milima ya Zika miaka hiyo ya 1920 au 1930 huko. Kwa hiyo, bado jana nimemsikia mtendaji mkuu wa World Health Organization akisema kwamba, kuwe na tahadhari.
Je, Tanzania kama nchi imejiandaaje hasa ukizingatia kwamba, wakati ugojwa wa ebola umetokea zile specimen zilipelekwa Nairobi, je, sasa hivi ukitokea hapa Tanzania tumejiandaje kama Serikali?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza Serikali yenyewe ndiyo chanzo cha kipindupindu si kweli na naomba niseme tu jukumu la usafi, ni jukumu la kila mtu, kuanzia usafi wa mwili wake, usafi wa nyumba yake, usafi wa mahali pake pa kazi,ni jukumu la kila mtu na si jukumu la Serikali. Serikali ni mratibu kwenye uteketezaji wa taka ambayo ni hatua ya mwisho ya usafi kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuhusu ugonjwa wa zika Serikali imejiandaaje? Serikali imekwishachukua hatua za awali za kufanya matayarisho ya kujikinga na ugonjwa huu. Kwanza, nitumie nafasi hii kuwatoa hofu Watanzania wote kwamba ugonjwa huu bado haujaingia kwenye nchi yetu wala kwenye nchi za jirani. Tahadhari kubwa ambayo tumechukua ni kwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwanza kutoa tamko la uwepo wa ugonjwa huu kwenye nchi nyingine. Hiyo ni hatua ya kwanza ya kiepidemolojia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya pili, ni kutoa taarifa za ukweli kuhusu ugonjwa yaani fact sheet, ambayo tayari Waziri wa Afya kwa mamlaka yake amekwishatoa taarifa sahihi zinazohusu ugonjwa wa homa ya zika na zimetawanywa nchi nzima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, ni kuweka mikakati ya kuripoti mtu yeyote yule ambaye atafika kwenye vituo vya kutolea huduma na ikaonekana ana dalili zinazofanana na ugonjwa wa homa ya zika kuleta taarifa hizo centre ili tuweze kuangalia kama anaweza akawa ameambukizwa na ugonjwa huu ama la.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ndio taratibu za kiepidemolojia za kufanya udhibiti wa ugonjwa wa mlipuko katika hatua ya awali ambapo ugonjwa bado haujangia nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuwatoa hofu Watanzania kwamba ugonjwa huu sio hatari katika viwango vya ugonjwa kama wa ebola, denge, ama West Nile fever kwa sababu ugonjwa huu unasababisha tu homa ndogo ndogo lakini una madhara makubwa kwa akinamama wajawazito walio kwenye first trimester, wenye mimba changa, kwamba wanaweza wakazaa watoto wenye vichwa vidogo. Nakushukuru.
MHE. HALIMA ALI MOHAMMED: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa ya Naibu Waziri nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tafiti zinaonyesha kwamba wanawake wanaathirika zaidi na maradhi ya moyo kuliko wanaume.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia wanawake hawa ambao ndiyo walezi wa familia hasa wale waliopo kule vijijini?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, je, Serikali ina mkakati gani wa kudhibiti uingizwaji wa vyakula vibovu ambavyo havina kiwango katika nchi yetu? Ahsante (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Swali la kwanza Serikali ina mkakati gani wa kupunguza kiasi cha magonjwa haya kwa wanawake ambao wanaathirika zaidi kuliko wanaume.
Mheshimiwa Naibu Spika, tofauti ya upatikanaji wa magonjwa haya, kwa jinsia kwa maana ya baina ya wanawake na wanaume ni ndogo sana na kwa maana hiyo, mkakati wa kupambana na kuenea kwa magonjwa haya hauwezi kutofautishwa kwa jinsia. Hivyo mkakati wetu utakuwa ni wa pamoja na tayari Wizara ya Afya imeanza kutekeleza mkakati huo, kwanza kwa kutia umuhimu wa kipekee kwenye kuimarisha Kitengo cha NCD yaani Kitengo cha Magonjwa Yasiyo ya Kuambukiza pale Wizarani chini ya Kurugenzi ya Tiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, kitengo hiki tayari kimeishaaza mkakati wa kuandika mkakati wa kupambana na magonjwa haya na mkakati huu utawafikia hao akinamama wa vijijini na watu wote kwa ujumla wake kuanzia ngazi ya huduma za afya kule vijijini, kwa maana ya ngazi ya zahanati, ngazi ya vituo vya afya na ngazi ya hospitali za Wilaya, Mikoa na hata ngazi ya Kanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ni kweli kumekuwa na hisia kwamba kuna vyakula visivyo na viwango vinaingia nchini mwetu kutoka nchi za mbali. Serikali kwa kushirikiana kwa maana ya Wizara yetu Wizara ya Afya, ambayo ina kitengo cha TFDA (Tanzania Food and Drugs Authority) ambacho kipo chini ya Wizara yetu ya Afya, pamoja na Kitengo cha Viwango (TBS), wanaendelea kushirikiana kwa pamoja, kukagua mizigo yote ambayo inaingia nchini kwa njia za halali.
Lakini pia vyombo vingine vya kusimamia Sheria kama Majeshi ya Polisi na Uhamiaji, wataendelea kuwa makini kwenye mipaka yetu yote, katika njia zilizo halali na hata zile ambazo siyo halali kudhibiti uingizwaji wa vifaa hivi ikiwemo vyakula na dawa ambavyo havijapitishwa kwa viwango vinavyostahili, kwa mujibu wa Sheria za nchi yetu. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ni kwamba hadi sasa hivi katika Hospitali ya Mkoa wa Dodoma pesa ambayo imeidhinishwa mwaka 2014/2015 haijatolewa na pia ya 2015/2016 haijatolewa:-
(i) Je, ni lini pesa hizi zitatolewa ili kukamilisha ujenzi huo?
(ii)Je, Serikali haioni kwamba inaingia gharama za ziada inapochelewesha miradi na kuathiri mipango ya wale wakandarasi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni lini Serikali itakuwa tayari kutoa pesa hizo, jibu kwa ufupi ni kwamba pesa hizo kwa kuwa zipo kwenye bajeti, zitatolewa pindi Serikali itakapopata pesa za kutosha na ambazo zitakuwa tayari kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kuhusu variation ambayo inatokana na kuchelewa kwa miradi, kwa bahati mbaya sana kuna gharama nyingine haziepukiki kutokana na uwezo mdogo wa kiuchumi wa nchi yetu. Nia thabiti ipo na utekelezaji utafanyika tu pale ambapo tutaweza kuwa na fedha hizo. Kwa bahati mbaya sana kama tutakuwa tumeshaingia gharama hatutakuwa na namna ya kuzikwepa kwa kuwa ndiyo hali halisi ya uchumi wetu.
MHE. FELISTER A BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Dodoma ilijengwa mwaka 1923 na ilipojengwa ilikuwa na wakazi wasiozidi elfu hamsini lakini kwa sasa Dodoma ina wakazi takribani laki sita na majengo yako vilevile wala hayajaongezeka. Bima ya Afya waliamua kujenga jengo kwa ajili ya kupunguza wingi wa watu katika Hospitali ya Mkoa wa Dodoma ambalo lina miaka mingi halijakamilika, limekabidhiwa lakini hakuna samani ndani yake.
MWENYEKITI: Uliza swali sasa.
MHE. FELISTER A. BURA: Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kuishawishi Bima ya Afya ambayo ipo chini ya Wizara yake kuleta samani na kukamilisha jengo lile ili lianze kutumika kwa wagonjwa wa Dodoma?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Bura kwa swali lake la nyongeza. Sisi hatuna shida na kuishawishi taasisi ya NHIF kuwakopesha Hospitali ya Mkoa wa Dodoma, lakini ukweli utabaki palepale, narudia tena ukweli utabaki palepale kwamba hospitali hizi za mikoa zipo chini ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Naomba Waheshimiwa Wabunge tunapohudhuria vikao vya RCC tuikumbuke sekta ya afya kwa kushawishi bajeti maalum za mikoa na hata bajeti za kawaida za mikoa kwa kiasi kikubwa zielekezwe kwenye kuboresha hospitali zetu ikiwa ni pamoja na utanuzi wa majengo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia suala la mikopo NHIF ni suala la kibiashara zaidi. Kama hospitali husika ina makusanyo na vigezo vinavyotosha kuwezesha kupata pesa kwa mkopo kutoka NHIF basi uongozi wa hospitali husika utafanya mazungumzo ya kibiashara ambayo yana faida kwa pande zote mbili baina ya wao wenyewe. Hili wala siyo suala la sisi kama Wizara kwenda kuishawishi NHIF kwa sababu mambo haya yanahusu fedha na fedha zinataratibu zake.
MHE. ABDALLAH N. MAFTAHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Naomba niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kwa muda mrefu Serikali ilikuwa na mpango wa kuhakikisha inatoa huduma za afya bure kwa wazee, lakini kumekuwa na mkakati na utaratibu wa kutoa bima ama kadi za matibabu kwa wazee ambazo zina mipaka. Kwa mfano, mzee wa Mtwara Mjini akienda Mtwara Vijijini kule hana nafasi ya kutibiwa japokuwa ana zile kadi. Je, Serikali ina mkakati gani sasa hivi wa kuondoa mipaka ya kadi za matibabu za wazee? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na namshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kuuliza swali hili la muhimu sana. Takribani mwezi mmoja umepita Mheshimiwa Waziri wa Afya alinipa jukumu la kutengeneza Kikosi Kazi ambacho kitawashirikisha wadau mbalimbali kwenye Mfuko wa Afya kwa Umma (CHF) na Bima ya Afya kwa ujumla wake. Kikosi Kazi kimeshakaa na tumepanga mpango kazi wa namna mpya ya kuboresha huduma za afya kutokana na kadi ya CHF.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo tutakayoyafanya ni pamoja na kuweka utaratibu mzuri wa cross subsidization, dhana unayoisema Mheshimiwa inaitwa cross subsidization. Pia tutashughulikia suala la portability ya kadi kwa maana ya kutoka kwenye level moja kwenda kwenye level nyingine kwa maana ya kutoka kwenye level pengine ya wilaya kwenda kwenye level ya rufaa ya mkoa ama kutoka wilaya moja kwenda wilaya nyingine ama kutoka zahanati kwenda kituo cha afya, hiyo inaitwa portability ya hiyo kadi. Hili ni jambo mojawapo ambalo tunalifanyia kazi na tutaliwekea mkakati mahususi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, ni lazima kutakuwa na ongezeko la uchangiaji kwa sababu unapotoka level ya chini kwenda level ya juu gharama za huduma pia zinaongezeka. Tutakapoleta mpango huu tutawashirikisha Wajumbe wa Kamati yetu na Wabunge wote kwa ujumla ili kwa pamoja twende kuwahamasisha wananchi wakubaliane na mpango huu mzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango huu utakuja sambamba na kutafuta namna bora zaidi kwa kulekule kwenye halmashauri kutenga fedha mahsusi kwa ajili ya kulipia Bima ya Afya kwa wazee ili waweze kupewa Kadi za Bima za Afya bure kama ambavyo sera inasema. Kwa maana ya kwamba ni lazima tuwabane walionacho ili tuweze kuwahudumia ambao hawana uwezo wakujihudumia, hiyo ndiyo mikakati ya Serikali. (Makofi)
MHE. JUMA S. NKAMIA: Mheshimwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza kwa rafiki yangu Mheshimiwa Dkt. Hamisi Kigwangalla, Naibu Waziri wa Afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri wakati anajibu swali anasema, Serikali ilifanya maamuzi lakini swali langu lilikuwa Serikali ina mpango gani wa kununua mashine kwa ajili ya Hospitali ya Taifa ya Muhimbili? Mashine anayoizungumzia Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla ni mashine ambayo imechukuliwa kutoka Hospitali ya Benjamin Mkapa ya Dodoma, katika Chuo Kikuu cha Dodoma, ikahamishiwa Muhimbili. Swali la kwanza, je, anaweza kukiri kwamba ni kweli hiyo mashine anayoizungumzia ni ile iliyochukuliwa kutoka Hospitali ya Benjamin Mkapa katika Chuo Kikuu cha Dodoma kupelekwa Muhimbili? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Dodoma pia kuna wagonjwa. Unapohamisha mashine ya CT-Scan kutoka Dodoma kupeleka Muhimbili na unakuja hapa unasema ziko mbili sasa, unataka watu wa Dodoma wafe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSI, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza, nitumie nafasi hii kumshukuru na kumpongeza Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuonyesha mapenzi ya dhati na kuwajali watu wa Dodoma na Kanda ya Kati kwa ujumla wake kwa kujenga hospitali kubwa ya kisasa inayoitwa Benjamin Mkapa Ultra-Modern Hospital hapa Dodoma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muktadha huo pia nitumie nafasi hii kwa namna ya kipekee kumpongeza Rais wa Awamu ya Tano, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, kwa ziara ya kushtukiza aliyoifanya kwenye Hospitali yetu ya Taifa Muhimbili ambayo ilibaini upungufu mwingi wa vipimo na namna ya kuchunguza magonjwa kwenye hospitali hii kubwa ya Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najibu swali ya Mheshimiwa Nkamia kama ifuatavyo. Kwanza, nakiri kwamba mashine ambayo imefungwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ni mashine ambayo ilikuwa ifungwe kwenye Hospitali ya Benjemin Mkapa. Kwa sababu mbalimbali za kitaalamu ndani ya Serikali, majengo ambapo ilikuwa ifungwe mashine hii kwenye Hospitali ya Benjamin Mkapa iliyopo Dodoma yalikuwa bado hayajakamilika wakati huo hospitali kubwa kabisa ya Taifa pale Muhimbili kulikuwa kuna mahitaji ya mashine kwani mashine iliyokuwepo ilikuwa imeharibika. Mheshimiwa Rais alifika pale Muhimbili akajitolea fedha na matengenezo yakaanza lakini huduma ikawa haiwezekeni kutolewa kwa kuwa mashine haikupona kwa wakati. Kwa hivyo, ndani ya Serikali tuliona ingekuwa ni vyema kwa kuwa tuna uwezo wa kununua mashine nyingine mpya na tulikuwa tayari kununua mashine mpya kwa ajili ya kufunga Muhimbili tu-switch ile ambayo imeshafika nchini ambayo ilikuwa ifungwe hapa Dodoma ifungwe sasa Muhimbili. Sasa hivi tupo kwenye mchakato wa kununua mashine mpya kwa ajili ya kuja kufunga Benjamin Mkapa na majengo ya kufunga mashine hiyo kwa sasa yanaelekea kukamilika. (Makofi)
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Naomba niulize swali kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Mlalo kama ifuatavyo:-
Je, ni lini Serikali itatuletea huduma za X-ray katika Kituo cha Afya cha Mlalo ambacho kinahudumia zaidi ya wakazi elfu sitini wa Jimbo la Mlalo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na namshukuru Mheshimiwa Rashidi Shangazi, Mbunge wa Jimbo la Mlalo, kwa swali lake la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu ni kwamba, Serikali yetu ya Tanzania imeingia mkataba na Serikali ya Uholanzi ku-embark kwenye mradi mkubwa unaojulikana kama mradi wa sekta ya afya wa ORIO ambapo Serikali yetu itakuwa tayari kuchangia nusu ya Euro 22,000,000 kwa ajili ya kununua vifaa vya kufanyia uchunguzi wa magonjwa na kusambazwa kwenye hospitali zote nchi nzima. Tulikuwa tumelazimika kuchangia takribani Euro milioni 2.2 na mpaka tunavyoongea tulikuwa tumepungukiwa na kama Euro 818,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wiki iliyopita, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dokta John Pombe Magufuli amemwelekeza Waziri wa Fedha kwamba fedha zilizokuwa zitumike kwa ajili ya semina elekezi kwa Mawaziri zielekezwe kwenda kukamilisha deni hilo la Euro 818,000 kwa ajili ya kukamilisha mchango wetu kwenye mradi huu mkubwa wa kununua vifaa. Hivyo, naamini kwamba hospitali mbalimbali nchini ikiwemo Hospitali ya Mlalo zinaweza zikapata vifaa hivyo pindi tutakapoanza utekelezaji wa mradi huu.
MHE. RASHID ALI ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pamoja na majibu ya Naibu Waziri, nitakuwa na maswali mawili kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, makundi ya Watanzania ambao wapo Ocean Road kusubiri matibabu ya ugonjwa hatari wa saratani, wagonjwa hao, ukifika pale Ocean Road utatokwa na machozi. Daktari hawezi kufanya matibabu kama hajafanya planning baada ya kuwekewa x-ray. Kuna mashine ya C-Arm ambayo ni mbovu haifanyi kazi. Hiyo ndiyo ambayo inamfanya daktari aweze kujua mgonjwa huyu ameathiriwa kiasi gani.
Je, ni lini Wizara itachukua hatua za dharura na za muhimu kabisa kuweza kuhakikisha mashine hii inafanya kazi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, wapo watumishi katika Kitengo cha Saratani mmoja anaitwa Christopher; huyu amehamishwa Temeke; na mwingine ni Sefue ambaye amehamishwa Hospitali ya Amana. Hao walikuwa ni wataalam wazuri, wamesomeshwa katika Kitengo cha Mionzi. Watu hawa wamehamishwa, wamepelekwa katika Hospitali ambazo hawafanyi kazi wanayotakiwa kwa mujibu wa taaluma yao! Ni lini Waziri anayehusika atalifuatilia suala hili ili hatua zinazostahili zichukuliwe?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza hatua za dharura. Serikali tayari imekwishachukua hatua za dharura kufanya matengenezo ya mashine anayoizungumzia. Kwa maana hiyo, hapa ninapozungumza hakuna mashine hata moja ambayo haifanyi kazi pale Ocean Road. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, Serikali kupitia agizo alilotoa Mheshimiwa Waziri wa Afya, mara ya kwanza tu alipoenda kujitambulisha kwenye Hospitali hii, imetenga shilingi bilioni nne kwa ajili ya kukamilisha ununuzi wa mashine ya LINAC (Linear Accelerator) pamoja na CT Simulator ambayo inapanga utaratibu wa matibabu ya saratani kwa wagonjwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, juzi hivi shilingi bilioni 2.5 zimeahidiwa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa ajili ya kuanza mchakato wa ununuzi wa mashine hizo. Hivyo, ile kero anayoizungumzia Mheshimiwa Rashid Ali Abdallah ya matibabu, tunaifahamu na Mheshimiwa Waziri alitoa machozi mara ya kwanza alipokuwa pale na ametoa maelekezo ambayo tunayatekeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kuhusu hawa watumishi waliohamishwa. Ni kweli walihamishwa, lakini walihamishwa kwa taratibu za kiutumishi, suala hilo tunalifahamu na tayari tumechukua taratibu za kuunda Kamati Maalum ambayo inachunguza kama walihamishwa kwa fitina ama walihamishwa kwa taratibu za kiutumishi ambazo zilifuatwa. Kwa maana hiyo, kama itabainika kuna matatizo yalijitokeza tutachukua hatua za kuwarudisha.
Hata hivyo, kuondoka kwao pale hakujaleta upungufu wowote wa matibabu katika Hospitali ya Saratani ya Ocean Road.
MHE. MARIA N. KANGOYE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza napenda kusema kwamba nasikitika sana kwani sijaridhishwa na majibu ya Naibu Waziri, ukizingatia kwamba ametoa mfano mmoja mmoja kwa kila kipengele cha swali langu wakati NGOs zipo nyingi ndani ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nijielekeze katika kuuliza maswali yangu mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa vijana na wanawake ndio engine ya maendeleo ya nchi yetu: Je, ni lini Serikali itaanza kutoa elimu ya ujasiriamali kwa vikundi vya wanawake na vijana kabla ya utoaji wa milioni 50 kwa kila kijiji? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kwa kuwa zipo Taasisi za Kitanzania ambazo zimekuwa zikisaidia vijana wanaoathirika na madawa ya kulevya na tasisi hizi zimekuwa ni chache kulingana na wingi wa vijana hawa, je, Serikali ina mpango gani wa kusaidia taasisi hizi ili ziweze kupanuka na kusaidia vijana wengi zaidi?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Maria Ndila Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Serikali ina mpango gani wa kutoa elimu kwenye taasisi hizi mbalimbali?
Serikali haina tu mipango, Serikali imeshaanza utekelezaji wa anachokisema kupitia taasisi mbalimbali. Wizara mbalimbali zinatoa elimu kwenye vikundi mbalimbali ambavyo wanafanyanavyo kazi, lakini pia sisi kwenye Wizara yetu specifically tuna Benki ya Wanawake ambayo imeanzisha utaratibu wa kuanzisha siyo matawi ya benki, lakini kuanzisha vikundi kwenye kila mkoa ambapo wanawake wajasiriamali na hata wanaume na vijana wanapewa elimu ya ujasiriamali na pia wanawezeshwa mitaji kupitia utaratibu ambao wamejiwekea.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, kwamba Serikali ina mpango gani kuhusu kuwawezesha na kuwajengea uwezo vijana? Tayari Serikali inafanya jambo hilo. Namwomba Mheshimiwa Mbunge asiwe na shaka na kazi inayofanywa na Serikali kwa kuwa inafanywa kwa ustadi wa hali ya juu.
MHE. MGENI JADI KADIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza, kwa kuwa Daktari amehakikisha kuwa chanzo cha ugonjwa huu hakijulikani, je, yuko tayari kutenga fedha ili uchunguzi uendelee? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kwa kuwa wanawake wengi hawajui ugonjwa huu, je, Serikali ina mpango gani sasa wa kutoa mafunzo au elimu hasa vijijini ili kujua dalili za ugonjwa huu pale unapojitokeza?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Serikali kutenga fedha, tayari Serikali inatenga fedha kwa ajili ya kutoa huduma za afya nchini kwa magonjwa yote siyo tu ugonjwa huu wa leiomyomata uteri. Ugonjwa huu siyo hatarishi kiasi cha kusema utengewe programu maalum na bajeti maalum kwa sababu kuna vipaumbele vingine vya magonjwa mengine hatari zaidi kuliko huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili kuhusu kutoa elimu kwa akinamama hususan wa vijijini, hili ni jambo ambalo Serikali ya Awamu ya Tano itakuwa ikilitekeleza kwa kasi zaidi kuliko Serikali zilizopita kutokana na uwepo wa Mpango Maalum wa kuajiri Wahudumu wa Afya Vijijini (Community Health Workers) ambao watakuwa wakitoa elimu kwenye kaya na kwenye jamii kila siku. Zamani walikuwepo wahudumu hawa lakini walikuwa wakitoa huduma hiyo kwa kujitolea (voluntary) lakini sasa Serikali ya Awamu ya Tano imeanzisha mpango wa kuwaajiri kabisa na tunawafundisha kwa wingi sana katika kipindi hiki.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba niulize swali moja dogo kwa Mheshimiwa Naibu Waziri. Mheshimiwa Naibu Waziri anasema kwamba ugonjwa huu siyo hatari, lakini kwa sasa hivi hapa Tanzania tunalo tatizo kubwa sana la uzazi. Ndoa nyingi zinavunjika kwa sababu akinamama hawapati mimba na inasemekana kwamba hiki ni chanzo mojawapo cha kuzuia akina mama kupata mimba. Pamoja na kuwa anasema kwamba siyo ugonjwa hatari lakini haoni kwamba tatizo la familia kutokupata watoto ni tatizo kubwa hapa nchini?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na nashukuru kwa swali la Mheshimiwa Magdalena Hamis Sakaya, Mbunge wa Kaliua na nitalijibu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, tunaposema ugonjwa fulani ni hatari tunaangalia ni kundi kubwa kiasi gani linapata ugonjwa huo. Hatusemi tu ni hatari kwa sababu ameupata mmoja na ameathirika, hizi ni taratibu za kitaalam, za epidemiology na labda niseme tu hili ndilo eneo nililobobea kitaaluma, epidemiology and public health.
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi, kwa ugonjwa huu wa uterine fibroid, kiwango cha akinamama wanaoathirika na ugonjwa huu hakifiki 20%.
WABUNGE FULANI: Aaaah.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Hakifiki 20% ya akinamama wote na kwa maana hiyo hatuwezi kuweka programu maalum ya ugonjwa huu wakati tuna vipaumbele vingine vya magonjwa yanayowasibu akinamama kila siku.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tatizo la akinamama kupata shida ya kujifungua, ni kweli linahusiana na ugonjwa wa fibroid lakini sababu siyo ugonjwa wa fibroid, actually, akinamama wanapochelewa kushika mimba ndiyo wanaingia kwenye hatari zaidi ya kupata ugonjwa wa fibroid. Kwa sababu ugonjwa wa fibroid unawapata akinamama wakiwa wanakaribia kipindi cha menopause yaani kati ya miaka 35 na kuendelea na siyo chini ya hapo...
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Inatarajiwa kibaiolojia akinamama wengi zaidi wawe wameshika mimba katika kipindi hicho.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama kusema kwamba Daktari amejibu siyo tu kama ni Naibu Waziri bali amejibu kama mtaalam.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Kwa hiyo, amejibu na anajua anachokisema.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niahidi kitu kimoja, tutafanya semina kwa Wabunge ili kueleza suala hili na tuwape takwimu halisi ugonjwa huu unaathiri wanawake kiasi gani na tunayo maelezo hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nilitaka kuliweka hilo vizuri.
MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIB: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri wa Afya, je, ni lini Serikali itahakikisha imeondoa changamoto zilizopo katika huduma ya afya na wananchi kuweza kupata huduma zilizo bora katika vituo hivyo?
MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIB: Mheshimiwa Munira Khatib tafadhali rudia swali lako uikaribie microphone.
MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIB: Mheshimiwa Naibu Spika, je, ni lini Serikali itahakikisha changamoto zilizopo katika huduma ya afya zinaondoka na wananchi wanafurahia huduma hizo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kila siku Serikali inafanya kazi ya kuondoa changamoto zilizopo kwenye mfumo wa sekta ya afya. Serikali ya Awamu ya Tano kupitia maelekezo ambayo tunayapata kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015-2020 inajielekeza kwenda kuanzisha mfumo wa bima ya afya ambapo Watanzania wote watapaswa kuwa na kadi ya bima ya afya kwa lazima. Azma hii ya Chama cha Mapinduzi ya kuweka utaratibu wa Bima ya Afya kwa kila mtu tunaamini itaondoa changamoto kwa kiasi kikubwa zinazoukabili mfumo wa afya nchini kwetu.
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba, kwa vile, Halmashauri yangu ya Wilaya ya Itilima imeweza kulipa MSD zaidi ya milioni 120, hivi sasa tunavyozungumza vituo hivyo havijaweza kupata dawa, vituo hivyo ni Mwaswale, Nangale, Chinamili, Nkoma, Sunzura na Sawida. Je, ni lini sasa vituo hivyo vitapata dawa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante. Ni kweli tumepokea fedha za dawa kutoka Mfuko wa Pamoja kutoka kwenye vituo walivyovitaja vya Mwaswale ambapo tuna milioni 17.7, Lugulu milioni 16.2, Nyamalapa milioni 13.8, Chinamili milioni 13 na vituo vingine takribani zaidi ya shilingi milioni 50. Vituo hivi vitapata dawa kutoka kwa wale washitiri wa ndani (prime venders) ambao nimewazungumzia, nimesema mpaka sasa tuna Washitiri 13 na tunaendelea kufanya jitihada za kuongeza Washitiri wengine. Lengo likiwa ni kupunguza time ya Washitiri hawa ku-supply dawa kwenye vituo hivi. Washitiri tulionao kwa sasa kwa faida ya Waheshimiwa Wabunge wote ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, tunao Astra Farmer, Jill Came, Salama Pharmacy, Anuther, Planet Farmer, Bahari Pharmacy, Samiro Pharmacy, Hashi Pharmacy, Pyramid, Mac Medics, Shukuru, Abakus na Philips. Washitiri hawa wanatusaidia kwa kiasi kikubwa kuziba pengo pale ambapo kwenye Bohari ya Taifa ya Dawa hatuna dawa na tuna fedha kutoka Halmashauri basi Halmashauri zinapokosa dawa zinapaswa kuandikiwa kibali maalum kutoka kwenye Bohari ya Dawa ya Kanda na kwenda kununua dawa hizo kwa Washitiri hawa wa ndani ambao wana mikataba na MSD.
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo likiwa ni kuhakikisha Halmashauri zetu zinanunua dawa kwa watu waliothibitishwa na dawa ambazo zina viwango vya ubora vinavyohitajika.
MHE. SULEIMAN M. NCHAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, wabheja sana. kwa niaba ya wananchi sharp wa Jimbo Sharp, namwomba Mheshimiwa Naibu Waziri, Jimbo la Kishapu limekamilisha ujenzi wa hospitali ya kisasa kabisa ya Wilaya, tena ni hospitali ya mfano na kujivunia ambayo Serikali ya Chama cha Mapinduzi, imeijenga kwa kushirikiana na wananchi wa Jimbo la Kishapu pamoja na Wawekezaji.
Kwa kuwa, hospitali hiyo ina upungufu mchache, imekamilika takribani kwa asilima 78 na upungufu huo katika swali la nyongeza hauwezi kunoga kuueleza, nimwombe Naibu Waziri, yuko tayari kufuatana na Mbunge sharp, kwenda kwa wananchi sharp, kuiona hospitali sharp, inayotoa huduma sharp sharp, ili mambo yaendelee kuwa sharp wakati wowote atakapotamka kwamba yuko tayari? Wabheja Sana.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa majibu sharp, kwa Mbunge sharp wa wananchi sharp wa Kishapu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa na mimi ni Naibu Waziri sharp, namuahidi Mbunge sharp kwamba nitakuwa sharp, kuandamana naye ili tufanye safari ya sharp sharp, kwenda Kishapu kwa ajili ya kuwahudumia wananchi sharp wa Kishapu.
Mheshimiwa Naibu Spika, weekend ijayo baada ya hii, namuahidi Mheshimiwa Suleiman Nchambi kuandamana naye kwenda Kishapu kwenda kuitembelea hospitali hii na naomba Waheshimiwa Wabunge wengine wawe sharp kutekeleza mambo sharp sharp kwa ajili ya wananchi wao kama Mbunge wa Kishapu.
MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Napenda kuuliza ni lini wodi ya wazazi katika Hospitali yetu ya Mkoa ya Mawenzi itakamilika kwa sababu imejengwa kwa zaidi ya miaka mitano na inakuwa ni kero kwa wanawake wa Mkoa wa Kilimanjaro?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kukamilika kwa wodi ya wazazi katika hospitali ya Mawenzi, Moshi ni suala la kipaumbele kwenye Serikali ya Awamu ya Tano. Wiki takribani tatu zilizopita nilifika pale na kuona hatua ya ujenzi iliyofikiwa na tukashauriana na uongozi wa hospitali ile na kukubaliana kwamba kwa mwaka huu wa fedha waombe wapewe bajeti maalum kwa ajili ya kukamilisha sehemu ya jengo hilo ambayo itatoa huduma kwa akina mama wajawazito na watoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile watumie mikopo inayopatikana kwenye taasisi mbalimbali za kifedha ili wakamilishe ujenzi huo mara moja sasa hivi kuliko kusubiria huu utaratibu wa kutumia bajeti. Tayari wameanza mchakato huo kupitia Mkuu wa Mkoa, Mheshimiwa Said Meck Sadick kwa kufanya mazungumzo na Benki ya TIB.
MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mbali na suala hili kwamba Serikali inachukua muda mrefu kusema kwamba haijapatikana ushahidi, lakini ushahidi anaweza akautoa mtoto kwamba ni fulani ndiyo kanifanyia kitendo hiki, lakini Serikali inasema bado ushahidi.
Pia kuna baadhi ya wazazi huwa wanaficha makosa haya, ama sijui kwa kuona aibu ama kwa kuoneana sijui vipi, labda huwa wanapewa hela na wale watuhumiwa. Je, Serikali inawachukulia hatua gani wazazi kama hawa wanaoficha ukatili huu dhidi ya watoto wao? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, endapo mtoto ameathirika kiafya, yaani yule ni mtoto mdogo ujue, lakini kaathirika kiafya, maumbile yake yameathirika, Serikali inamsaidiaje mtoto kama huyo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Utaratibu wa kesi ni utaratibu wa kisheria na haijalishi sana jambo lenyewe lina maumivu kiasi gani kwa watu wanaohusika kwenye kesi hiyo. Hivyo, utaratibu wa kisheria unataka ushahidi ufikishwe Mahakamani na Mahakama ishawishike bila kuwa na shaka kwamba kosa kweli limetendeka. Kwa sababu raia wote wana haki ya kutendewa sawa mbele ya macho ya sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, haiwezekani Serikali hata kama ina uchungu kiasi gani na watoto wanaofanyiwa vitendo vya ukatili, basi ikalazimisha tu hatua zichukuliwe dhidi yao bila utaratibu wa Kimahakama kufuatwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo nitoe wito, wazazi watoe taarifa kwenye vyombo vya sheria kuhusiana na vitendo vya ukatili wanavyofanyiwa watoto pindi vinapotokea. Kwa sababu pia jambo lingine ambalo linajitokeza kutokana na utafiti uliofanywa kwa kushirikiana na Wizara yetu pamoja na Chuo kikuu cha Muhimbili, ni kwamba maeneo hatarishi ya vitendo vya ukatili kwa zaidi ya asilimia 60 ni nyumbani ambapo watoto wanaishi, ikifuatiwa na shule kwa zaidi ya takriban asilimia 56.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama hayo ndiyo mazingira ambayo watoto wanafanyiwa vitendo hivi, basi wazazi wakishirikiana na Walimu watoe taarifa kwenye mamlaka za kisheria na watoe ushahidi na wawe tayari kwenda kutokea Mahakamani ili kutoa maelezo yatakayowezesha watuhumiwa kuwekwa hatiani.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza Naibu Waziri kwa majibu mazuri aliyoyatoa. Nataka tu kuongezea na kutoa rai kwa wazazi na kutoa onyo kwamba pale ambapo mtoto atatoa ushahidi na ikidhihirika kwamba amefanyiwa vitendo vya kikatili, tukigundua mzazi ama jamaa analegalega kwenye kutoa ushahidi, tutamuunganisha na wahalifu na hatua zitachukuliwa bila kujali kwamba yeye ni mzazi wake.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru nami kuweza kunipatia nafasi ya kuuliza swali fupi la nyongeza. Je, ni kwa nini Serikali isiwapeleke watoto hawa kwenye makambi ya JKT kwa ajili ya kupatiwa mafunzo ya stadi za kazi?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Bila shaka Mheshimiwa Khadija Binti Nassir alikuwa anamaanisha watoto wa Mitaani. Kama anamaanisha watoto wa Mitaani, hawawezi kupelekwa kwenye makambi ya majeshi ya JKT
kinyume na matakwa yao, kwa sababu watoto wana haki za msingi za kupatiwa ulinzi na Serikali yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, wataendelea na sisi kama Serikali tunapenda waendelee kukaa kwenye familia; na kama kwenye Vituo vya Kulelea Watoto hawapati malezi stahiki, sisi utaratibu tunaoufanya kwenye Serikali ni kujaribu ku-trace familia wanazotoka na kuwapeleka kule ili waweze kuunganishwa na jamii yao.
MHE. ANNA R. LUPEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa Hospitali ya Wilaya ya Mpanda kuna vifo sana vya akina mama wajawazito na kwa kuwa Madaktari wetu pamoja na Manesi ni wachache:
Je, ni lini Serikali itaongeza Madaktari katika Wilaya ya Mpanda ili vifo vya akina mama wajawazito viweze kupungua?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kwa kuwa Hospitali ya Wilaya ya Mpanda ni kama vile Hospitali ya Mkoa, hatuna Daktari Bingwa wa akina mama: ni lini Serikali itatuletea Daktari bingwa ili akina mama vifo vyao vipungue?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwa sasa, hatuna uhakika ni lini tutakamilisha utaratibu wa ndani ya Serikali wa kutoa vibali kwa ajili ya kuajiri watumishi kwenye Sekta ya Afya. Hivyo naomba avute subira mpaka hapo tutakapokuwa tayari kufanya hivyo.
Swali la pili, kuhusu Daktari Bingwa wa magonjwa ya akina mama wajawazito na watoto, kwenye Hospitali ya Mpanda, naomba kumshawishi Mheshimiwa Mbunge kwenye vikao vyao vya Halmashauri vya Bajeti kwenye Bunge linalokuja, wajipange kuanzia chini, kwenye Halmashauri yao kuweka kasma ya watumishi wa aina hiyo, lakini pia sambamba na kuweka kasma ya kuajiri Daktari Bingwa, waandae mazingira yatakayovutia Daktari huyo kuja kwenye hospitali hiyo na akifika, basi akae.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itafanya utaratibu wa kupanga watumishi kwenda kwenye hospitali hiyo kadri ambavyo watakavyokuwa wameomba.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize Sali dogo tu la nyongeza. Kwa kuwa njia mojawapo ya kupunguza hivi vifo vya mama na mtoto ni pamoja na kuboresha mfumo wa referral, yaani kutoka kwenye Vituo vya Afya, ama kwenye Hospitali za Wilaya kwenda kwenye Hospitali ya Mkoa; na kwa kuwa vituo vyetu vingi sana katika Mkoa wetu wa Iringa havina magari ya kubebea wagonjwa na vipo katika miundombinu mibaya sana ya barabara: Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kila Kituo cha Afya kinapatiwa gari ili kupunguza hivi vifo vya mama na mtoto?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba taarifa hizi zimfikie Mheshimiwa Ritta Kabati na Wabunge wote ambao wangependa kupata magari ya ambulance kwenye Halmashauri zao, kwamba kwanza jukumu la kununua magari haya lipo kwenye Halmashauri zenyewe. Waheshimiwa Wabunge kwa kuwa ni sehemu ya Halmashauri hizi, kwenye mipango yao ya bajeti tayari tutakapomaliza Bunge hili utaratibu wa mchakato mzima wa bajeti utaanza, basi Wabunge wahudhurie vikao hivyo na waweke ambulance kama kipaumbele cha kwanza kwenye bajeti zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hivyo, sisi Wizara ya Afya, tutaendelea kuwaomba na kuwashirikisha wadau wa maendeleo watupe ufadhili. Kama tutafanikiwa kupata ambulance, basi tutazigawa kwenye hospitali zetu nchini.
MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa kunipatia nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza baada ya majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi juzi tu, gazeti moja la Mwananchi lilitoa habari kuwa, huduma za dawa zitatolewa yaani kwa kununuliwa katika hospitali kuu ya Muhimbili. Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusiana na habari hizo?
Swali la pili, kwa kuwa ajali ni jambo baya sana, na ajali huweza kutokea kwa mtu yeyote na wakati wowote ule, na kwa kuwa watu wanaopata ajali huwa wanalipishwa dawa hata kama ni kwa baadae. Je, Serikali itakubaliana nami kwamba sasa ni wakati muafaka wa kuingiza katika mfumo kwa hao watu wanaopata ajali, kutolipa malipo ya huduma na dawa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NAWATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya MheshimiwaFaida Mohammed Bakar, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kuhusu taarifa za Hospitali ya Taifa ya Muhimbili imetoa tamko kwamba itaanza ku-charge dawa zote; naomba nirejee maelezo niliyoyatoa hapa juzi, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Mrisho Kikwete, Mbunge wa Chalinze. Kuhusu jambo hilo hilo ambalo leo tena Mheshimiwa Faida Mohammed Bakar analiuliza,kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, haijafanya mabadiliko yake kwenye Sera ya Taifa ya Afya ya mwaka 2007; na nimeeleza kwenye majibu yangu ya msingi kwamba kuna magonjwa ambayo yanapewa msamaha kwa mujibu wa sera hiyo, kwenye ile Ibara ya 5.4.8.3 cha sera hiyo ambapo tunaelezea makundi ambayo yanapaswa kupata huduma za afya kwa msamaha.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitarudia tena kuyataja kwa faida ya Wabunge lakini pia kwa faida ya watanzania wote. Kwamba wagonjwa wote wanaoumwa magonjwa ya muda mrefu, yaani chronic illnesses, wanapewa msamaha na Sera ya Taifa ya Afya; na kwa kutaja machache tu nitasema kuna magonjwa ya moyo, magonjwa yote ya akili, magonjwa ya saratani, kifua kikuu, ukoma, UKIMWI, pumu, sickle cell, magonjwa yote haya yanapewa msamaha kwa mujibu wa Sera ya Afya. Lakini pia kuna makundi maalum machache nayo yanapewa msamaha na Sera ya Afya na makundi hayo ni makundi ya wazee wenye umri wa miaka zaidi ya 60, watoto wenye umri chini ya miaka mitano, akina mama wajawazito na watu wenye uwezo mdogo wa kifedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama kuna gazeti liliandika taarifa hizo, basi gazeti hilo linapotosha na taarifa hizo haziwezi kuwa sahihi, na mimi kama Naibu Waziri mwenye dhamana ya kusimamia utekelezaji wa sera ya afya hapa nchini, ninarejea tena kutoa msimamo wa Serikali kwamba sera yetu haijabadilika na kwa maana hiyo makundi haya ambayo yanapewa msamaha na Serikali kwa mujibu wa sera yataendelea kupata msamaha huo kwa mujibu wa sera yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, kuhusu ajali. Matibabu yote ya dharula kwa mujibu wa Sera ya Afya hapa nchini ni bure, mtu akiugua ghafla achilia mbali kupata ajali; akiugua tu ghafla, akaanguka, jambo la kwanza akifika hospitalini atapewa tiba hiyo bure bila kuulizwa gharama yoyote ile. Huo ndio utaratibu na ikitokewa mahala mtu akawa-charged naomba azifikishe taarifa hizo kwangu na mimi nitachukua hatua hapo hapo.
MHE. ASHA A JUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa mwingiliano baina ya wananchi na kambi ni mkubwa, sasa pamoja na hatua za miti na kuta, ni kwa kiasi gani au ni tahadhari gani ya ziada zilizochukuliwa kukabili matokeo ambayo hayatarajiwi ya bahati mbaya kama yale yaliyotokea Gongolamboto na Mbagala? Na nataka nithibitishiwe hapa kwamba wahanga wote wa Gongolamboto na Mbagala kama walishapata fidia?
Swali la pili, ni kwamba Jeshi linapopanua sehemu zake hizo huwa linatoa fidia. Je, katika suala hili limejipanga kiasi gani katika mpango wa kulipa fidia kwa wananchi ambao inawahamisha? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (Kn.y WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA): Mheshimiwa Naibu Spika, majibu ya Serikali kwa swali lake la kwanza ni kwamba mpaka hivi tunavyoongea hapa tayari ndani ya Jeshi kuna mikakati ya kujenga maghala mapya na kwa kiasi kikubwa maghala mapya ya kuhifadhia ilaha yamekwisha kamilika kwenye vikosi mbalimbali, kambi mbalimbali. Japakuwa sitovitaja ni vikosi gani kwa sababu za kiusalama, lakini tayari mabomu na vifaa vyote vya milipuko vya Jeshi vimekwishahamishwa kwenye kambi ambazo zipo karibu zaidi na wananchi na kuwekwa kwenye maghala hayo mapya ili kuondoa uwezekano wa matatizo kama yale yaliyojitokeza pale Mbagala na kule Gongolamboto.
Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa fidia tayari naamini utakuwa ulishaanza na pengine ulishamalizika sina uhakika sana na hilo, naomba nisiseme lolote.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali lake la pili, kuhusiana na wananchi kupatiwa fidia kwenye maeneo ambayo Jeshi linaonekana limevamia. Kiukweli ni kinyume chake. Jeshi limekuwepo katika maeneo haya ya makambi kwa kiasi kikubwa lakini wananchi ndiyo wamekuwa wakivamia maeneo ya majeshi. Lakini kwa kuwa Jeshi hili ni la wananchi na ni rafiki kwa wananchi, japokuwa wananchi wanavamia Jeshi mara kadhaa limekuwa hata likilazimika kuhamisha mipaka yake kutoka kule waliko wananchi na kuingiza ndani zaidi kwenye maeneo yake. Pamoja na kwamba wanayahitaji hayo maeneo lakini Jeshi kwa sababu ni la wananchi na ni rafiki kwa wananchi limekuwa likifanya hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba niwasihi wananchi wote ambao wapo karibu na maeneo ya Jeshi wasiendelee kuwa na tabia ya kuvamia maeneo ya majeshi na tayari sasa hivi Serikali imeshaanza kubaini mipaka yote ya kambi za majeshi na kupanda miti kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi na kwenye kambi hizi ndogo ndogo kuweka fence aidha ya wavu ya ukuta. Ninaamini tunapoelekea matatizo kama haya ya mwingiliano baina ya wananchi na Jeshi hayatojitokeza.
MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina maswali mawili ya ngongeza. Kwa kuwa mbali na matatizo ya Madaktari hatari feki ambao wameenea katika baadhi ya hospitali zetu, lakini pia kuna tatizo sugu la dawa feki ambazo zinateketeza ama zinaleta athari kwa watumiaji wa dawa hizo. Je, Serikali inalishughulikiaje tatizo hilo la dawa feki? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Waganga wa Tiba Asilia wameenea katika maeneo mengi ya nchi yetu ya Tanzania na kwa kuwa baadhi yao hutumia dawa feki ambazo hazijathibitishwa.
Je, kwa nini Serikali inawaruhusu Waganga hao wa Tiba za Asili kufanya kazi zao na baadhi yao kutoa dawa feki kwa watumiaji? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza kuhusu dawa feki, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Faida Mohamed Bakar, Waheshimiwa Wabunge wote na wananchi kwa ujumla kwamba uwezekano wa kuwa na dawa feki kwenye vituo vya kutolea tiba hapa nchini ni mdogo sana, almost hakuna kwa sababu tuna utaratibu mzuri wa kuhakiki viwango vya ubora wa dawa ambazo zinatolewa kwa ajili ya matumizi ya binadamu na hata zile za mifugo hapa nchini kwetu, utaratibu huu ni mgumu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kusajili dawa ambayo itaingia kwenye soko inachukua muda mrefu, inachukua Mamlaka mbalimbali za uchunguzi kuichunguza dawa hiyo na hatimaye kuiruhusu iweze kutumika katika vituo vyetu. Kama ikijitokeza kukawa kuna walau fununu tu za uwepo wa dawa feki basi, Serikali kutumia mamlaka zake za uchunguzi hutuma kikosi cha ukaguzi kwenye eneo hilo ili kuweza kuthibitisha kama kweli maneno hayo yanayosemwa kuhusu uwepo wa dawa feki ni ya kweli ama laa. Mara nyingi hatua kali huchukuliwa dhidi ya mtu yoyote yule ambaye atakutwa na dawa feki.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusu waganga wa tiba asili, waganga wa tiba asili wapo kisheria, wanatambuliwa kwa mujibu wa sheria na wanasajiliwa kwa mujibu wa sheria ya waganga wa tiba asili na tiba mbadala ya mwaka 2002.
Mheshimiwa Naibu Spika, hawa ni kweli baadhi yao wanatoa dawa ambazo ni feki na siku zote tumekuwa tukiwabaini na tukichukua hatua za kuwadhibiti. Napenda kutumia Bunge lako Tukufu kuwaeleza waganga wote feki ambao hawajasajiliwa kuchukua hatua za kufika kwenye Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala mara moja, kwa ajili ya kusajiliwa pia kutumia utaratibu mpya ambao tumeuanzisha baada ya lile tukio la Dkt. Mwaka nilipoamua kumtembelea kwa ghafla. Tumeanzisha utaratibu mpya sasa wa kusajili dawa zote ambazo zinatolewa na waganga wa tiba asili na tiba mbadala hususani zile ambazo zinafanyiwa packaging kisasa. Utaratibu huo na wenyewe utakuwa mgumu kama ulivyo huu wa dawa hizi za tiba ya kisasa ili kuweza kudhibiti uwezekano wa uwepo wa waganga wa tiba asili ambao wanaweza wakawa wanatoa dawa ambazo zina sumu ndani yake.
MHE. HAFIDH ALI TAHIR: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza, kwa sababu Watanzania huwa wanasafiri kati ya Bara na Zanzibar kwa ajili ya kutafuta matibabu, na kwa sababu Wizara hizi mbili siyo za Muungano. Mheshimiwa Waziri unaweza kutuambia nini kuhusu ushirikiano wa pamoja kati ya Bara na Zanzibar kuhakikisha waganga hao feki wanapigwa vita ili wananchi waende vizuri.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yetu ya Afya inafanya kazi kwa karibu sana na Wizara ya Afya ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kwenye mambo yote yanayohusu afya, ikiwemo tiba asili na tiba mbadala. Hivyo kama kuna tatizo hilo kule Zanzibar kuna fursa ya wataalamu kushirikiana, kuna fursa ya viongozi wa hizi Wizara mbili kushirikiana na utamaduni huo umekuwepo toka hata sisi hatujaingia humu kwenye Serikali. Kwa hiyo, asiwe na shaka kama kuna tatizo huwa tunawasiliana na tunashirikiana kwa ukaribu.
MHE. HALIMA A.BULEMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya madhara ya Madaktari feki wamekuwa wakisababishia wagonjwa hawa vilema vya maisha au kupoteza maisha kwa ujumla.
Je, kuna utaratibu wowote wa fidia kuwafidia watu hawa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, japo kuwa Mheshimiwa Halima Bulembo ni jirani yangu ungenitonya kwamba utaniuliza swali. Kwanza hakuna tukio lolote lile ambalo limewahi kuripotiwa ambapo Daktari feki amesababisha madhara kwa mgonjwa. Madaktari feki hawa mara nyingi kwa matukio ambayo tunayafahamu wamekuwa wakitoa huduma kisanii tu kwa malengo ya kutaka kukusanya pesa hususani zile wa rushwa kutoka kwa wateja. Lakini haijatokea wakafanya haswa kitendo cha kwenda kutoa tiba kwa mgonjwa, hususani labda kufanya operesheni ama kufanya procedure. Kama ingewahi kutokea hivyo pengine labda kungekuwa kuna sheria ambayo ingekuwa inatuongoza kwamba nini kiwe fidia kwa mteja yoyote yule ambaye atakuwa amesababishiwa madhara kutokana na Madaktari feki.
MHE. LUCY T. MAYENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa uchumi wa nchi yetu umekuwa ukiimarika na mikakati ambayo imeendelea ambayo imekuwa ikifanywa hivi sasa inaonyesha kwamba nchi yetu itakuwa ni Taifa bora. Lakini vilevile kwa kuwa idadi ya watu inazidi kuongezeka na kwa miaka mingi ya nyuma Serikali yetu imekuwa ikisomesha Watanzania wengi katika nchi mbalimbali lakini baadhi ya Watanzania ambao ni Madaktari waliamua kuondoka hapa Tanzania na kwenda nje kwa ajili ya sababu kuwa zikiwa ni maslahi.
Je, Serikali ina mkakati gani maalum wa kuweza kuwarejesha Madaktari hawa ambao sasa wamepata uzoefu mkubwa.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kweli kwamba Serikali yetu imekuwa ikiongeza udahili kwa ajili ya kufundisha Watanzania wenzetu kwenye fani za tiba kwa kiasi kikubwa sana katika miaka ya hivi karibuni. Hivi tunavyozungumza hapa kwa mwaka mmoja tuna uwezo sasa hivi wa kuzalisha takribani Madaktari wa tiba 1,000. Hiki ni kiasi kikubwa sana na ni uwekezaji mkubwa sana ambao umefanywa na Serikali yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kutambua uwekezaji huu mkubwa uliofanyika ni kweli nakiri kwamba tumekuwa na uwezo mdogo wa kuwa- absorb kwenye system wale wote wanaohitimu kwenye fani za tiba na utabibu kwa ujumla wake. Serikali ya Awamu ya Tano tayari ina mkakati mahsusi wa kuhakikisha tunaongeza kiasi cha Madaktari ambao wanakuwa absorb kwenye system ya kutolea huduma za afya ili tuwe na Madaktari wengi zaidi ambao wanafanya kazi kwenye Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu maslahi mpaka hivi ninavyoongea hapa Madaktari ni mojawapo ya fani za kitaalamu hapa nchini ambao wanalipwa vizuri sana kuliko wengine. Hivi ninavyoongea Daktari anayemaliza masomo yake ya Degree analipwa vizuri sana kuliko ukilinganisha na fani zote zile kwenye Serikali na tunavyoongea kwenye sekta binafsi sasa wanaanza kupata shida kuajiri Madaktari ambao wamehitimu kwa kuwa ndani ya Serikali maslahi ni mazuri zaidi kuliko hata yale ya kwenye sekta binafsi na ni jambo la kujivunia. Kwenda nje pia siyo jambo la kusema ni baya, kwa sababu wa navyoenda wengi wao wanakaa miaka mitatu, miaka sita wanarudi nchini kuja kutoa tiba hapa na tayari wanakuwa wameshapata uzoefu wa kufanya kazi nje ya nchi. Kwa hivyo, ni fursa na hatuwezi kuwabana kwa njia nyingine yoyote ile zaidi ya kusema tuboreshe maslahi ndani ya Serikali ili Madaktari waweze kutoa huduma kwa Watanzania wengi hapa nchini.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza maswali mawili ya nyongeza;
Swali langu la kwanza ninataka tu nipate ufafanuzi kutoka kwa Mheshimiwa Naibu Waziri, hii project ya Road to Independence, nimepitia bajeti zote za Wizara ya Ulinzi, nimepitia bajeti ya Wizara ya Utamaduni, sijajua kama anaweza akaweleza wananchi wa Nachingwea ni kipindi gani haswa inaenda kutekelezwa hii program ili tuweze kujua kwa sababu miundombinu ya eneo lile bado inaendelea kuharibika mpaka sasa hivi tunavyozungumza, ikiwemo eneo ambalo ameisha Mheshimiwa Samora Machel.
Swali la pili ambalo ninapenda kuuliza, ni nini kazi za Mabalozi wetu katika nchi hizi ambazo zilinufaika na maeneo haya, ukienda Msumbiji leo hii kuna Chuo Kikuu kinaitwa Nachingwea University kinapatikana pale Msumbiji. Je, hawaoni umuhimu wa kushirikisha Balozi zetu na nchi zilizohusika kuweza kusaidia maeneo haya ili kuweza kuweka kumbukumbu za Viongozi ambao waliishi katika maeneo haya? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza nitatoa utangulizi kwamba historia ya ukombozi wa Bara la Afrika haiwezi kutenganishwa na ushiriki mahiri na wa kujitoa wa nchi yetu Tanzania. Haiwezi kutenganishwa na uwepo wa Viongozi mashuhuri kama Mwalimu Julius Kambarage Nyerere lakini pia na Viongozi wengine wa Bara la Afrika kama kina Nkwame Nkurumah na hao wapiganaji wenyewe wakina Samora Machel wakina Robert Mugabe na wengine. Kwa maana hiyo, hii historia japokuwa ni chungu na japokuwa ni ngumu hatuna sababu ya kusema tunaweza tukadharau kutunza maeneo ambayo historia hiyo inayathamini, kwa maana hiyo eneo hili la Nachingwea ambalo Mheshimiwa Mbunge analizungumzia litapewa kipaumbele kwenye program hiyo ya Road to Independence ambayo nimeizungumzia hapa. Program hii kama anavyosema kwenye bajeti haionekani, naomba mimi na yeye tushirikiane kwa pamoja baada ya kikao hiki cha Bunge kufanya utafiti kwenye vitabu vya bajeti ili tuone ni wapi haswa bajeti hii ya Road to Independence inapatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, inawezekana usiwe mradi ambao unatokana na bajeti ya ndani ukawa ni mradi ambao pengine una ushirika wa hawa wabia anaowasema wakiwemo wafadhili wa maendeleo ama Vyuo Vikuu ambavyo vinapenda kufuatilia historia ya ukombozi wa Bara la Afrika.
Swali la pili, kwamba hatuoni kama Balozi zetu zinaweza zikashirika nchi hizo, Tanzania tulikuwa na jukumu kubwa tu ambao tulijitolea kulibeba la kutafuta ukombozi wa Bara la Afrika na kuwapa nyumba na makazi, mafunzo, chakula na malazi zaidi ya wapiganaji kutoka nchi zaidi ya 12 za Afrika zilizokuwa zinapambana na ukoloni na kwa maana hiyo, hiyo ni heshima ya kipekee ambayo sisi tuliipata kupata wapiganaji wa ukombozi kwenye nchi zao kuja kukaa katika nchi yetu. Heshima hiyo tunaendelea kuipata leo na mwaka jana Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alitunukiwa heshima ya kipekee pale AU kwa kupewa jengo la Peace and Security katika Mkutano wa Marais wa Afrika na hivi tunavyoongea hapa katika watu watatu mashuhuri wa Bara la Afrika ambao wanatambuliwa na wamewekewa alama za kipekee pale Addis Abba kwenye Makao Makuu ya AU ni pamoja na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, wengine wakiwa ni Nkwame Nkurumah na mwingine akiwa ni Nelson Mandela.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, Tanzania itaendelea kuwapokea na kuwapa ushirikiano wapiganaji wote ambao wanapenda kuja Tanzania kwenye maeneo waliyowahi kuishi kama vile kufanya hija na kukumbukia siku ambazo walikuwepo hapa nchini wakipigania uhuru wa nchi zao, ambazo sasa zimekuwa huru.
MHE. RUTH H. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumuuliza Mheshimiwa Waziri swali la nyongeza. Pale Muhimbili tumepata vifaa vya kisasa vizuri sana lakini gharama za vifaa hivyo kwa mfano pacemaker ni kama shilingi milioni tano mpaka milioni sita na kitu kama angiography ni kama shilingi milioni mbili. Je, Serikali kwa nini haitoi ruzuku ili kuwawezesha wagonjwa wanaokwenda pale kupata tiba kwa bei nafuu pamoja na Hospitali ya Ocean Road ambapo chemotherapy ni ghali sana? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ni lini Serikali itaendeleza utaratibu wa kuleta Majopo ya Madaktari kwa ajili ya magonjwa mengine ambayo yanawapeleka wagonjwa nje?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naanza na la pili kwamba ni lini Serikali itaendeleza utaratibu wa kuleta Majopo ya Madaktari kwa ajili ya kutoa tiba. Jibu lake ni rahisi tu kwamba, tunaendelea kuleta Majopo ya Madaktari kutoka nchi mbalimbali rafiki na nchi yetu kwa ajili ya kutoa huduma hizi kwa Watanzania walio wengi. Mfano mzuri ni Ijumaa iliyopita nilikwenda kuwashukuru na kuwapongeza Madaktari kutoka nchi za Qatar na Saudi Arabia ambao walifanya operesheni 75 kwa watoto wa Kitanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mara ya kwanza katika nchi yetu tumefanya operesheni ya coronary bypass ambapo tunapindisha mzunguko wa damu kwenye mishipa midogo midogo ya juu ya moyo, inaitwa coronary arteries na tumefanya kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi yetu. Kwa hiyo, utaratibu huo upo na unaendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mkurugenzi wa Mkuu wa Taasisi ya Jakaya Kikwete (JKCI), Profesa Mohamed Janabi na timu yote ya wataalam kwenye hospitali ile kwa jitihada mbalimbali wanazofanya kuhakikisha huduma za matibabu ya moyo zinapatikana hapa hapa nchini kwa kiwango cha juu na kwa maana hiyo kuipunguzia Serikali gharama na kuwapunguzia wananchi wa Tanzania usumbufu wa kusafiri nje ya nchi kufuata huduma hizo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza ni kuhusu gharama za vifaa na kwamba Serikali haitoi ruzuku hiyo siyo sahihi. Gharama za afya ni kubwa mno na hivi tunavyoongea hapa Serikali inapaswa kupongezwa tu kwa kuendelea kutoa ruzuku kwenye huduma za afya nchini. Nalisema hili kwa sababu moja, asilimia 70 ya Watanzania wanaokwenda kutafuta huduma za afya kwenye vituo vya kutolea huduma hizo kwa kiasi kikubwa wanazipata bure, hawalipi chochote na kwa maana hiyo ni subsidize services za Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivi tunavyoongea, tunaweka utaratibu mpya kwenye bajeti hii kwa ajili ya vifaa alivyovisema kama vya angiogram pamoja na pacemaker viweze kutolewa kwa ruzuku na Serikali. Juzi Mheshimiwa Waziri amewaelekeza Taasisi ya Jakaya Kikwete waweke utaratibu huo na naamini kwenye mwaka huu wa fedha sasa hakutokuwa na kulipia gharama za pacemaker na vitu kama hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Taasisi ya Ocean Road, matibabu yake niliyaeleza hapa jana vizuri sidhani kama Mheshimiwa Mbunge hakunisikia, naomba nitunze muda wako tu. Tumetenga shilingi bilioni saba kwa ajili ya chemotherapy kwenye bajeti hii.
MHE. RITA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba kuuliza swali fupi tu. Kwanza niipongeze Serikali kwa kuanzisha Kitengo cha Matibabu ya Figo katika Hospitali ya Benjamin Mkapa hapa Dodoma. Hata hivyo, nimeona Hospitali ya Muhimbili pia ina kitengo kinashughulikia matibabu ya figo. Ni kwa nini Serikali isiweke eneo moja, kwa mfano hapa Dodoma washughulikie tu mambo ya figo na kule Muhimbili washughulikie tu mambo ya moyo? Pia nimeona tengeo katika bajeti, sasa hapa ni kama kuharibu rasilimali, naomba jibu.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, majibu ni kwamba, tayari Serikali ndicho inachokifanya, hospitali ya kisasa kabisa ya Benjamin Mkapa Ultra-Modern Hospital itabobea zaidi kwenye kutoa tiba mahsusi ya magonjwa ya figo. Tutaanzia kwenye hizi tiba ambazo sasa hivi tunazo kwenye hospitali nyingine za dialysis kwa maana ya kusafisha figo na tunakwenda mbele zaidi hadi kuanza kufanya huduma za kupandikiza figo (transplant) na hayo yatafanyika kwenye Hospitali ya Benjamin Mkapa hapa Dodoma.
MHE. MWANTUMU DAU HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri swali la nyongeza. Kupitia misaada mbalimbali ambayo Wizara inapokea kutoka kwa wafadhili, haoni kuwa, kuna haja hususan Hospitali ya Mnazi Mmoja, ya kuisaidia Wizara ya Afya ya Zanzibar kwa kuwapatia dawa kwa ajili ya kuwahudumia wagonjwa wanaosumbuliwa na magonjwa hayo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, katika mambo yaliyopo kwenye Orodha ya Mambo ya Muungano afya si mojawapo. Kwa maana hiyo sisi kama Wizara ya Afya hatuwajibiki moja kwa moja kushughulikia mambo yanayohusu afya kule Zanzibar. Hata hivyo, katika utaratibu na ushirikiano na umoja tulionao tunafanya kazi kwa karibu sana na wenzetu pacha Wizara ya Afya ya kule Zanzibar na hivyo ushirikiano huu tutaendelea kuudumisha.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kunipa fursa ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri amezungumzia suala la uhaba wa bajeti lakini naomba kuuliza; Benjamin Mkapa Foundation wamejenga vituo vya afya kule mkoa wa Rukwa ambako kuna matatizo makubwa sana; kwa mfano kuna Zahanati ya Kala - Nkasi, Milepa – Sumbawanga, Ngorotwa – Kalambo pamoja na ile ya Kishapu na wamekabidhi kwa Halmashauri toka Juni 2014, lakini mpaka leo havijatumika wakati kuna matatizo makubwa sana, ni kwa nini Serikali haijaweza kuvitumia vituo hivyo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Pamoja na majibu mazuri naomba nimsaidie Mheshimiwa Naibu Waziri mwenzangu kwamba suala hili ni kwa nini, ni kwa sababu taratibu za makabidhiano bado zinaendelea. Pindi taratibu hizo zitakapokamilika tutakabidhi majengo hayo kwa Halmashauri.
MHE. PROSPER J. MBENA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Kwa kuwa tatizo hili ni kubwa sana nchini kwetu na kwa kuwa wahusika Wizarani wanaonekana kutolitambua vizuri ukubwa wake pamoja na kwamba watoto wa mitaani wanaonekana kila siku; je, Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari kuanzisha register pale Wizarani kwake ambako itapokea majina ya wanaume pamoja na wanawake wachache ambao wanatelekeza watoto wao ili aweze kuwa na kumbukumbu nzuri? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, Mheshimiwa Waziri atakubali kupokea ushauri binafsi kutoka kwa wadau wanaokerwa na tatizo hili ili ushauri huo aweze kuutumia katika kuleta mapendekezo ya kurekebisha Sheria Namba 21 ya Watoto?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti naanza na la (b), Serikali iko tayari sana kupokea ushauri kutoka kwa mtu yeyote Yule.
Lakini (a) kwamba Serikali kuanzisha registers pale Wizarani namba nijibu kwamba Serikali kupitia Sheria ya Mtoto Namba 21 ya mwaka 2009 ambayo ilitungwa na Bunge lako Tukufu, kwenye kile kifungu cha 94 inatoa mamlaka kwa Halmashauri yaani Serikali za Mitaa kuwabaini watoto wote wa mitaani na kuwahudumia.
Kwa maana hiyo Waheshimiwa Wabunge tusikwepe jukumu hili kusimamia utekelezaji wa sheria hii kwenye Halmashauri zetu. Lakini kusema jambo hili litashughulikiwa centrally pale Wizarani wakati watoto wako kwenye Serikali za Mitaa ni kujaribu kuweka urasimu ambao hauhitajiki.
Hivyo Waheshimiwa Wabunge wote na Halmashauri zetu tukiwa kama viongozi wajumbe kwenye Halmashauri hizi, tuweke mikakati mahsusi ya kuwahudumia watoto hawa kule kule kwenye Halmashauri zetu.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Napenda kuuliza swali la nyongeza kwa Mheshimiwa Waziri. Kumekuwa na ongezeko kubwa la akina mama wanaojifungua kwa operesheni, na suala hili lilikuwa linahusishwa pia na maadili ya madaktari wetu. Je, Serikali ina tamko gani kwamba suala hili ni suala la kitaalam au ni mmomonyoko wa maadili miongoni mwa madaktari? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, kujifungua kwa operation ni jambo ambalo haliwezi kuwa la kukiuka maadili, bali ni jambo la kitaalamu. Kuna sababu na vigezo mahususi ambavyo hupelekea daktari akafanya uamuzi wa kumpeleka mama mjamzito kwenda kujifungua kwa njia ya operation (caesarean section) na kitu chema sana kufanya uamuzi huo kwa sababu huokoa maisha ya mama na mtoto kuliko kusubiria kujifungua kwa njia ya kawaida ambapo mama mjamzito anaweza akaingia kwenye hali hatarishi.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Katika majibu ya msingi ya Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba benki hii kwa sasa inajikita katika kutoa huduma kwa kutumia vituo vya mikopo. Sasa nataka nijue kwamba ni lini wanawake wa Mkoa wa Songwe watapata kituo angalau kimoja ili waweze kujiinua kiuchumi?
Swali la pili, kwa kuzingatia kwamba madhumuni ya uanzishwaji wa benki hii ni kuwainua wanawake wanyonge, hususan wanaoishi vijijini, ambao hawana uwezo wa kumiliki ardhi wala nyumba kama ilivyo kwa wanawake wangu wengi wa Mkoa wa Songwe, lakini masharti ya mikopo ya benki hii kimsingi hayatofautiani sana na masharti ya benki nyingine. Je, Serikali haioni kwamba kuna umuhimu wa kurekebisha masharti haya ya mikopo ya benki ili basi wanawake wa Mkoa wa Songwe waweze kunufaika?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda nimpongeze kwa kuwajali wanawake wa Mkoa wa Songwe, yeye akiwa kama Mbunge wa eneo hilo na mimi nikiwa kama Balozi wa Wanawake.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza ni lini tutafungua angalau kituo kimoja cha mkopo kwenye Mkoa huo. Naomba nimpe taarifa kwamba tayari tuna kituo kimoja Songwe, maeneo ya Tunduma na kwamba tayari tumemwambia kwenye jibu letu la msingi kwamba tunauweka Mkoa wa Songwe katika mpango wetu wa kufanya kazi wa mwaka 2017/2018. Hivyo mtaji utakaporuhusu basi tutaufikiria mkoa huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, naomba na yeye atuhurumie kwa kutambua kwamba tayari benki yetu inajitanua kidogo kidogo na kwa sababu Songwe imemeguka kutoka Mkoa wa Mbeya, ambao tayari una vituo 11 vya kutolea mikopo, atuhurumie twende na maeneo mengine, kama kumwongezea basi tutamwongezea kidogo sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, kuhusu masharti ya mikopo kwenye Benki ya Wanawake; tayari Mheshimiwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto alikwishatoa maelekezo Siku ya Wanawake Duniani mwezi wa Machi mwaka huu, kwamba Benki ya Wanawake iweke utaratibu mpya wa kushusha masharti na gharama za kutoa mikopo kwa wanawake ili wanawake wenye kipato cha chini waweze kumudu gharama za kurejesha mikopo hiyo bila usumbufu wowote. Tayari maelekezo haya ya Mheshimiwa Waziri yanafanyiwa kazi na Benki yetu ya Wanawake.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye bajeti ya mwaka huu tayari tumeweka provision, ambapo kutakuwa kuna fungu maalum la pesa litakalokwenda moja kwa moja kwa wanawake wenyewe, badala ya kutumika katika administrative activities za benki.
MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Kwa kuwa, kumekuwa na uhitaji mkubwa wa upatikanaji wa mikopo yenye riba nafuu, hususan Mkoa wangu wa Iringa na Wilaya ya Mufindi tuna Community Bank, sasa Serikali haioni kuwa hii ni opportunity nzuri kufungua dirisha pale kwa Benki ya Wanawake ili wanawake wote wa Mkoa wa Iringa waweze kunufaika na hii mikopo yenye riba nafuu? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nampongeza Mheshimiwa Rose Tweve kwa kuendelea kuwaseme wanawake, mtu yeyote yule akiwasemea wanawake maana yake anarahisisha kazi yangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, majibu ya swali lake ni kwamba, wazo hilo la kufungua dirisha kwenye benki ya Mufindi Community Bank pale ni zuri sana na Serikali tunalichukua. Natumia jukwaa lako hili kutoa maelekezo kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Wanawake kufanya jitihada za haraka kabisa za kuweza kutumia fursa hii ya pendekezo linalotolewa na Mheshimiwa Rose Tweve na kuangalia maeneo mengine yote nchini ambako kuna Community Banks.
Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu kuna Meru Community Bank, kuna Mwanga Community Bank; tuna uwezo wa kufanya nao ushirikiano kwa kufungua madirisha maalum ya wanawake ili tuweze kuwafikia wanawake wengi zaidi katika nchi yetu. Hivyo, wazo lake tunalichukua.
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nami nimuulize swali dogo Mheshimiwa Naibu Waziri.
Kwa kuwa, toka Bunge lililopita niliiomba Serikali itufungulie dirisha dogo la Benki ya Wanawake katika Mkoa wa Tabora na kwa kuwa, Mkoa wetu uchumi wake ni duni sana, yeye anafahamu, je, yuko tayari yeye au Waziri wake kwenda Tabora na mimi au kuja Tabora kuongea na wanawake wa Tabora, kuwapa ahadi ya ukweli yeye mwenyewe, kwa sababu mimi nilishaahidiwa hapa Bungeni litafunguliwa dirisha dogo mpaka leo halijafunguliwa, ili uwaambie ni lini sasa Serikali itakuwa tayari na benki hiyo, kuwafungulia dirisha dogo wanawake wa Mkoa wa Tabora ili nao waweze kufaidika na keki hii ya Taifa letu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Munde Tambwe Abdallah kwa swali lake la nyongeza na hapo naona ananitega tu kwa sababu mimi mwenyewe natokea Tabora. (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni ahadi ya Serikali toka awamu iliyopita kufungua matawi Mkoani Tabora kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge anasema, naomba nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Benki ya Wanawake Tanzania, afanye haraka sana kwenda kufungua madirisha hayo Mkoani Tabora ili kutekeleza ahadi za Mawaziri waliokuwepo kabla yetu sisi hapa Bungeni, kwa sababu Serikali inaendelea kuwepo hata kama Mawaziri wanabadilika.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Kwanza nilitaka kufahamu ni mikakati gani iliyowekwa na Serikali katika kuongeza vifaa tiba na wataalam katika Hospitali zote za Jeshi zikiwepo za Zanzibar?
Pili, ni lini Waziri atafanya ziara katika vituo hivyo ili kuona hali halisi ya utendaji kazi katika vituo hivyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, mikakati ya Serikali katika kuongeza vifaa tiba, dawa na watumishi kwenye Vituo vya Afya vya Kijeshi ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza Serikali kwenye bajeti zake kila mwaka imekuwa ikiongeza bajeti ya huduma za afya kwa ajili ya makamanda na wapiganaji wetu kwa sababu wanapewa umuhimu wa kipekee katika nchi yetu, lakini sambamba na kuongeza bajeti Serikali pia imeongeza mikakati ya kufundisha wataalam mahsusi kwa ajili ya majeshi na hivi karibuni tumepata wafadhili kutoka Ujerumani kupitia Serikali ya nchi hiyo ambao ni marafiki zetu ambapo wametujengea chuo kikubwa na cha kisasa cha kijeshi kwa ajili ya kutoa wataalam kwenye sekta za tiba na chuo hiki nikupe taarifa Kamati yako ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama inayoongozwa na Mheshimiwa Adadi mwezi Aprili, 2016 ilitembelea kwenye chuo hiki ambacho kimejengwa kwa msaada wa Serikali ya Ujerumani na wakajionea namna kilivyo kizuri na cha kisasa.
Mheshimiwa Spika, pia Kamati ilitupa ushauri kwamba kituo kile badala ya kuishia kutoa stashahada kiende mpaka ngazi ya degree na Jeshi likachukua ushauri ule na limekubali kukipandisha hadhi chuo hicho na mkakati wa kukiweka sawa inaendelea.
Sambamba na mkakati huo ili kutatua changamoto ya upatikanaji wa dawa, vifaa tiba na vitenganishi kwenye jeshi kwa sababu ya umuhimu wao tayari mikakati ya kuajiri wataalam wapya wakimemo madaktari bingwa na madaktari wa kawaida pamoja na wataalam wengine imeendelea kutekelezwa. Mpaka kufikia mwezi Machi madaktari takribani 143 waliajiriwa mahsusi kwa ajili ya kutoa huduma majeshini.
Mheshimiwa Spika, lakini pia kupitia chuo hiki ambacho kimeaznishwa tunaamini katika miaka ya karibuni kutakuwa hakuna changamoto ya watumishi lakini pia kupitia kwenye kuongeza bajeti yetu tunaamini changamoto ya upatikanaji wa dawa, vifaa tiba na vitenganishi nayo itakuwa imepatiwa ufumbuzi. Lakini suluhisho la kudumu ambalo Serikali inalifanya kwa sasa ni kutengeneza Bima ya Afya mahsusi kwa ajili ya makamanda na wapiganaji wetu na bima hii tayari imeshapata baraka za Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli na sasa hivi ndani ya Serikali mchakato wa kuirasimisha unaendelea ili ufike katika ngazi ya Baraza la Mawaziri na utekelezaji ufanyike.
Swali lake la pili, kwamba je Waziri itakuwa tayari kwenda kufanya ziara ninaomba nilichukue na nilifikishe kwa Waziri mwenye dhamana ili aweze kuzungumza na Mheshimiwa Mbunge na pengine kumpa majibu mahsusi kwamba ni lini ataenda kuvitembelea vituo hivi.
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Napenda niulize maswali mawili tu ya nyongeza kwa Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, mambo alioyasema Waziri nakubaliana nayo, lakini bado katika nchi yetu watoto wanaendelea kuteseka na wengine wanarandaranda mitaani. Je, Serikali haioni kwamba, imeshindwa kuweka maandalizi kwa ajili ya kutoa huduma sahihi kwa watoto? (Makofi)
Swali la pili, moja ya kazi za Serikali ni kuandaa kizazi chake kutoka kizazi kimoja hadi kingine na ndiyo maana nchi nyingine wanatenga mifuko kama hiyo na wanadiriki hata kulipa wanawake wanapokuwa wajawazito pesa kidogo kidogo ambazo baadaye umsaidia mzazi pale mambo yanapokuwa magumu kule mbele.
Je, sasa Serikali haioni ni wakti muafaka wa kufikiria kuanzisha mfuko huo ili kuweza kulinda watoto wetu wakue vizuri?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili, kuhusu mfuko, naomba arejee majibu yangu kwenye jibu la msingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la kwanza, napenda tu kusema kwamba jukumu la malezi ni jukumu letu sote kama wazazi na linaanzia moja kwa moja kwenye familia. Sisi wanaume na wake zetu, tuchukue jukumu la kulea watoto tuliowazaa wenyewe. Kwa tamaduni za Kiafrika, extended family ina wajibu kwenye kulinda ustawi na kutoa ulinzi kwa watoto wote ambao wanaachwa na ndugu zetu, ambao pengine wametangulia mbele ya za haki ama wamepoteza uwezo wa kutoa malezi kwa mtoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mamlaka za Serikali za Mitaa ambazo Wabunge ni Wajumbe, zina majukumu ya msingi ya kuhakikisha ulinzi na ustawi wa watoto kwenye maeneo yao. Hivyo, ninatoa wito kwa Wabunge wote na jamii kwa ujumla tuweke mikakati madhubuti katika Mamlaka za Serikali za Mitaa tunakoishi kwa ajili ya kutoa ulinzi na ustawi kwa watoto.
NAIBU SPIKA: Waheshimiwa muda wetu umeenda sana. Tunaenda kwenye swali la mwisho, Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mheshimiwa Peter Joseph Serukamba, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, sasa aulize swali lake.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa mahitaji ya Sekta ya Afya hapa nchini yapo, yalikuwepo na yataendelea kuwepo, ni kwanini Serikali mlikubali kuingia mkataba huu au makubaliano haya ya fedha hizo asilimia 33 zinaenda tu kwenye ununuzi wa dawa na asilimia 67 inaenda kwenye fedha hizo zinaenda kwenye masuala ya usimamizi na ufuatiliaji kwa maana ya administrative cost, ni kwanini mliingia makubaliano haya amabyo hayana manufaa kwa Sekta ya Afya hapa nchini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Serikali imesaini Abuja Declaration ya kutaka asilimia 15 ya bajeti yake iende katika sekta ya afya. Ni ukweli usiopingika kwamba sekta ya afya hapa nchini kwenye zahanati zetu, vituo vya afya, hospitali za wilaya ina changamoto kubwa sana ikiwemo ukosefu wa dawa, lakini leo hatujui kipaumbele cha Serikali ni nini. Serikali leo inang‟ang‟ana kuhamia Dodoma wakati kwenye hospitali zetu hakuna dawa hata kidogo. Ni kwanini hamuwi na vipaumbele vya afya ya Watanzania kwanza kuliko haya mengine? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwamba kwanza ni kwanini Serikali iliingia makubaliano haya? Jibu ni rahisi tu, kwamba fedha za Health Basket Fund ni fedha za ziada za nyongeza ambazo tunapewa na wafadhili wetu. Sasa haiwezi kutokea mtu akaja akasema nakuongezea kitu kutatua changamoto inayokukabili halafu ukakataa. Kwa hivyo kulikuwa hakuna sababu ya Serikali kusema eti ijiulize maswali mara mbili mbili wakati imepata wafadhili na wafadhili wanakuja kuongeza tija kwenye kutoa huduma za afya kwa Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini zaidi ya hapo, fedha hizi kutengwa, kwamba asilimia 33 iingie kwenye dawa na asilimia 67 iende kutumika kwa ajili ya ku-administrate mfumo mzima wa afya kwamba sio jambo la muhimu; pengine Mheshimiwa Cecilia Daniel Paresso ungejifunza kwa ukaribu zaidi namna ya ku-administrate mambo ya mfumo wa afya. Mfumo wa afya ni katika mifumo complex ambayo unaweza ukaikuta hapa duniani, na si kazi rahisi ku-administrate utoaji wa huduma za afya. Wewe unapokwenda hospitali unaona ni kitu kirahisi tu unapoonwa na daktari na ukapewa dawa, lakini nyuma ya hiyo visit yako moja ambayo unaenda kuipata kwa daktari ukae ukijua kuna mchakato mrefu sana wa ku-administer mfumo mzima mpaka kufikia hapo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo wa afya unaendana na mambo kama ufuatiliaji, tathmini, tafiti, surveillance za muda mrefu pamoja na kukusanya takwimu. Haya ni mambo mhimu sana ambayo Serikali yetu kwa kweli haikuwa ikiwekeza kabla ya kupata hizi pesa za Health Basket Fund.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzipata wafadhili wakasema kwamba ni lazima watusaidie katika eneo hili kwa kiasi kikubwa. Lakini hata hivyo kwenye jibu langu la msingi nimesema tunaangalia uwezekano kwa maelekezo ya Mheshimiwa Waziri wakati akisoma hotuba yake ya bajeti hapa katika mwaka wa fedha unaokuja tufanye mapitio ili sehemu kubwa zaidi ya fedha hizi ziweze kuwekezwa kwenye dawa kama ambavyo tumefanya mabadiliko kwenye pesa zinazotokana na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kuhusu Abuja Declaration. Abuja declaration kweli ni commitment ambayo nchi yetu iliingia kwenye miaka ya mwanzo ya 2000, kwamba tutatenga asilimia 15 ya bajeti yote kubwa kwenye sekta ya afya. Serikali yetu kwa nyakati mbalimbali imekuwa ikifanya jitihada hizo za kuongeza bajeti kwenye sekta hii, lakini bahati mbaya sana ukuaji wa uchumi haukuweza kuendana na kasi ya mahitaji yetu makubwa ya kuwahudumia Watanzaia kwenye sekta ya afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ifahamike hapa kwamba huduma za afya ni katika huduma zenye gharama kubwa sana kwenye taifa lolote lile; na kwa maana hiyo kusema uchumi wetu huu mdogo unaweza ukakidhi mahitaji yote si jambo la rahisi na si jambo la kusema linaweza likafikiwa leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana Serikali ya Awamu ya Tano kupitia maelekezo yaliyopo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM tumejikita kwenye kuitafsiri Ilani ile kwa kuhakikisha tunaanzisha Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya ambao utamlazimisha kila Mtanzania kuwa kadi ya Bima ya Afya ili wananchi washiriki kwenye kuchangia huduma kabla ya kuzitumia, tukiamini kwamba kama kila Mtanzania atakuwa na Bima ya Afya maana yake atakuwa na uhakika wa kupata huduma hizo pale ambapo anazihitaji bila kupata changamoto ya kifedha, na hii ni njia mojawapo ya kukusanya pesa kwa watu wengi zaidi ambayo kwa kiasi kikubwa inaendana na misingi ya Sera ya Ujamaa na Kujitegemea ambayo sisi wa Chama Cha Mapinduzi tunaisimamia.
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Nakushukuru Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kunipa fursa hii. Watafiti Joel Lugala na Jesse Mbwambo katika andiko lao la kitafiti linalosema au lililoandikwa street children and street life in urban Tanzania; the culture of surviving and its implication for children health la mwaka 2013; watafiti hawa katika hitimisho lao wanasema, Serikali ya Tanzania hailijui tatizo la watoto wanaoishi katika mazingira magumu. Na kwa majibu ya Serikali ni dhahiri tatizo hili halieleweki na hitimisho hili ni thabiti. Je Serikali itachukua hatua gani kulielewa tatizo hili kwani linazidi kukuwa siku hadi siku? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali inatambua mfumo wa uchumi umebadilika hayo yanayosemwa kwamba watoto watalelewa na ndugu, au walezi hayapo kwa sasa. Watoto yatima wamekuwa wakinyanyaswa, wakidhulumiwa mali zao na ndugu wa wazazi; je, Serikali ipo tayari kubadili mtazamo wake kuhusu watoto wanaoishi katika mazingira magumu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Halima Abdallah Bulembo, Mbunge wa Viti Maalum kwa swali lake zuri la nyongeza aliloliuliza, lakini pili akiwa Mbunge mdogo kuliko wote hapa Tanzania amekuwa siku zote mstari wa mbele kutetea haki za vijana na watoto. Ni Mbunge wa kutiliwa mfano na ninakupongeza na ninaomba uendelee kufanya hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kujibu swali Lake…
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Nalijibu Mariam haraka za nini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kujibu swali lake napenda kusema na narudia tena kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, kwamba mtazamo na msimamo wa Serikali uko wazi na hautotetereka. Kwamba sehemu ya kwanza na ya muhimu na ya lazima kwa malezi ya mtoto wa Kitanzania ni kwenye familia yake. Kama imetokea kwa sababu moja ama nyingine wazazi wamefariki ama hawana uwezo wa kutoa malezi yanayohitajika kwa mtoto, familia pana (extended family) inapaswa kuchukua jukumu hilo na kama haiwezekani jamii pana inapaswa kuchukua jukumu hilo. Yote haya yakishindikana, sasa inakuwa ni wajibu wa Serikali kuwachukua watoto hawa na kuwatunza kwenye makao maalum kwa ajili ya malezi ya watoto, huo ndio msimamo wa Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na msimamo huu haimaniishi kwamba Serikali hailielewi tatizo hili, tatizo hili tunalifahamu, Serikali imefanya tafiti mbalimbali, na pamoja na hiyo tafiti ya akina Joe Lugala na wenzake tunaifahamu, na tumeifanyia, kazi na haimaanishi kwamba tafiti hiyo basi ndio hiyo hiyo tu hakuna tafiti nyingine na kwamba inatoa mwongozo wa kila kitu hapana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tafiti nyingi zimefanyika na zote tunazichambua na tunazifanyia kazi. Naomba nimtoe shaka Mheshimiwa Halima Bulembo kwamba Serikali iko macho kuhusiana na suala hilila malezi ya watoto, na kwamba tutaendelea kusimamia msimamo wetu, kwamba kisaikollojia, kijamii, na kwa maana ya kutoa ulinzi stahiki na mapenzi yanayohitajika kwa watoto wa nchi hii Serikali itakuwa mstari wa mbele. Nitoe rai kwenu nyote Waheshimiwa Wabunge na watanzania wote kwa ujumla mnaonisikiliza tujitahidi kuwalea watoto na kuhamasisha jamii ziwalee watoto kwenye unit ya family.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri sana, lakini nataka kuongeza suala moja. Kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto ya Mwaka 2009, kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri, jukumu la kwanza la malezi ya mtoto liko chini ya wazazi la pili familia. Lakini kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto, kifungu cha 94 kinasema ni jukumu la Serikali za Mitaa kuhakikisha kinachukua hatua zote za kuhakikisha watoto wanaoishi katika mazingira magumu haki zao zinatekelezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama kusisitiza Wabunge wote, ni Wajumbe wa baraza la Madiwani. Sisi Wabunge tumechukua hatua gani ya kuhakikisha watoto yatima katika wilaya zetu, katika halmashauri zetu wanapata haki ya elimu, wanapata haki ya elimu ya ufundi wanapata malazi, na wanapata chakula.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili jambo si la Serikali kuu ni jambo letu sisi wote Wabunge, tunapokaa kwenye mabaraza ya madiwani tujiulize mmechukua mikakati gani ya kupambana na tatizo la watoto yatima na watoto wa mitaani. Niliona niiweke hivyo wazi, wakisubiri Wizara ya Afya wao wakae tu kama si kipaumbele chenu haliwezi kuwa kipaumbele cha Watanzania kama sisi Wabunge hatutatia mkazo suala la watoto yatima,
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa Wilaya ya Kibondo ni Wilaya ambayo ilikaliwa na wakimbizi na kwa kuwa kuna majengo ambayo yamekaa kwa muda mrefu ya IOM ambayo Serikali ya Wilaya na Mkoa ilisharidhia kwamba yatumike kwa ajili ya chuo hicho. Je, Waziri haoni sasa ili kubana matumizi ya Serikali afike na kutoa ushauri ili yale majengo yatumike kwa ajili hiyo?
Mheshimiwa Mwenyekiti swali la pili, kwa kuwa makampuni mengi ya ujenzi baada ya kujenga barabara yamekuwa yakiacha miundombinu ya majengo mazuri. Sasa haoni ni wakati muafaka wa kupunguza upungufu wa wauguzi zikiwepo Wilaya nyingi pamoja na Kilolo kwa kuweza kuyatumia yale majengo vizuri ili Serikali iweze kupata manufaa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwamba nifike Kibondo ili nikashauriane na Serikali ya Mkoa ambao wameshapitisha azimio la kutaka kutumia majengo yaliyoachwa na IOM namwahidi nitafika mara baada ya Bunge la Bajeti kukamilika ili nishirikiane na Serikali ya Mkoa nione kwa ushirikiano na Wizara ya Mambo ya Ndani ambayo wana dhamana ya mali na maeneo yote ya wakimbizi, ni nini Serikali itafanya ili kuwezesha azimio lao hilo mkoani kutekelezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kuhusiana na majengo yaliyoachwa na miradi mbalimbali ya ujenzi; taratibu kwa kweli zimekuwa ni hivyo kama anavyopendekeza Mheshimiwa Mbunge. Hivyo, wafuate taratibu za kuzungumza ndani ya vikao vyao vya kufanya maamuzi kwenye halmashauri husika, ili walete mapendekezo Serikali Kuu tuone kama yanaweza yakapitishwa na wanaohusika na mradi huo kutumika kwa ajili ya shughuli ambazo wanazipendekeza.
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Ni lini Serikali italeta marekebisho yaliyoahidiwa na Mheshimiwa Mwakyembe wakati wa bajeti yake ili kuzuia ndoa za watoto wa shule?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nayaunganisha yote mawili kwenye jibu langu hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeanza mchakato wa white paper toka mwaka 2008 na lengo likiwa ni kutafuta namna ya kuwashirikisha wananchi kwa ujumla wao kwenye kufanya maamuzi juu ya suala hili ambalo limegubikwa na misingi ya dini, lakini pia limegubikwa na misingi ya mila zetu kwenye makabila mbalimbali hapa nchini. Kwa maana hiyo, suala hili Serikali imeonelea isilichukue kwa haraka haraka na ndiyo maana ikaanzisha mchakato wa white paper.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa bahati mbaya mwaka 2010 Mheshimiwa Rais, niseme kwa bahati nzuri pia, aliamua kuanzisha mchakato wa Mabadiliko ya Katiba na ndani yake akidhani kwamba, ile Tume itakapokuwa inakusanya maoni ingewezekana kupata maoni ambayo yangehusisha nia ya wananchi ya kutaka kufanya mabadiliko kwenye sheria mbalimbali ikiwemo Sheria ya Ndoa na Sheria ya Mirathi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya baada ya mchakato ule kukamilika, maoni yanayohusiana na suala hili hayakuonekana kama ni miongoni mwa mambo ambayo yalipendekezwa na wananchi. Hivyo, sasa hivi Serikali kupitia Wizara ya Sheria na Katiba imeamua kuanza upya jitihada za kuipeleka mbele white paper ili kupata maoni ya wananchi na hatimaye tuweze kuchukua maamuzi kama Serikali.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniona. Nina swali dogo tu, nawaunga mkono wanaharakati wote kuhusu suala hili muhimu, sasa nauliza Serikali, je, itakuwa tayari kuingiza kipengele kwenye sheria ambacho kinazuia kuzaa kabla ya kufikisha miaka 18? Maana wapo watoto wanazaa wana miaka 13 au 14, lakini hawachukuliwi hatua yoyote. Je, Serikali itaweka kipengele kuzuia? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni suala lenye utata kidogo na katika hatua hii kwa kweli, hatujalifikiria hilo. Naomba tuchukue wazo lake tulifanyie kazi tuone kama ni jambo ambalo angalau linaweza hata likafikiriwa kwa sababu lina utata sana.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, kwa kweli nasikitika sana kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri, najua hizi habari alipewa akiwa ofisini kwake.
Mheshimiwa Spika, hii guest house anayoizungumzia kwanza imepitwa na wakati sana, imejengwa miaka 56 iliyopita, lakini ambacho kimempita asione ni kwamba kituo hiki ni kikubwa sana na ni kizuri sana, kina eneo takribani zaidi ya heka tatu, kina mandhari mazuri sana, kina majengo mengine yote ya maabara, nyumba ya daktari, nyumba ya manesi na wodi za wagonjwa.
Sasa swali langu ni kwamba, je, kwanza Naibu Waziri atakuwa tayari tuende akajiridhishe kwamba jibu lake hili ambalo alizungumza kana kwamba kuna nyumba tatu tu, halitoshelezi maana ya kuwa na kituo kama hiki?
Pili, nataka Waziri aniambie kutokana na kwamba kituo hiki sasa hivi hakitumiki vizuri kama kituo cha utafiti kwa vile inaweza kuisha mwaka, miaka miwili hakujafanyiwa utafiti hata mtu mmoja; je, haoni kwa nini kituo hiki kiongezewe kiwe kituo cha afya ili pale watakapopenda kufanya utafiti wafanye, lakini kwa vile kuna majengo ambayo Serikali imetumia hela nyingi sana kukitengeneza na mandhari mazuri na kuna mlinzi, kuna gardener, kuna msafishaji, kuna tv, kuna maji, kuna umeme lakini kituo hiki sidhani hata hiyo guest house inapata watu wawili kwa mwezi maana mwenyewe nilienda nikalala pale kujiridhisha.
Mheshimiwa Spika, naomba Naibu Waziri aniambie; je, Serikali iko tayari kukifanya kituo hiki kiwe Kituo cha Afya ili kisaidie Kata tatu za Vuje, Maore na Bombo ambazo zina wananchi zaidi ya 50,000 ukichukulia kwamba Jimbo langu ni kubwa sana na ukichukulia kwamba jiografia ya kwangu ni mbaya sana na vituo vipo viwili tu na viko mbali mno? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Namshukuru Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka kwa maswali yake mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, majibu ya Serikali kwa swali lake la kwanza kwamba Waziri atakuwa tayari kwenda kukitembelea kituo hiki, ndiyo tupo tayari na baada ya Bunge hili tutakwenda na tutamtaarifu Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo hili aongozane na sisi tutakapokwenda kukitembelea kituo hicho.
Mheshimiwa Spika, jibu la pili ni kwamba ninachokiona Mheshimiwa Kaboyoka ana uchu wa kupata kituo cha afya zaidi kuliko matatizo yaliyopo pale kwenye Kituo hiki cha Utafiti cha Gonja. Sasa mahitaji ya vituo vya afya huwa yanaibuliwa na wananchi kwenye Halmashauri yao wenyewe. Ninamshauri Mheshimiwa Mbunge ashirikiane na Watendaji kwenye Halmashauri yake na wananchi kwenye Halmashauri yake waweze kuanzisha mchakato wa namna ya kupata Kituo cha Afya kwa ajili ya kukidhi mahitaji yao.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na kwamba kituo hiki kimekaa kwa muda mrefu na kwamba hakitumiki, hapana siyo kweli. Nakubaliana na yeye kimejengwa zaidi ya miaka 50 iliyopita lakini mwaka 2007/2008 kituo hiki kilifanyiwa ukarabati mkubwa kwa ajili ya maandalizi ya utafiti wa mabadiliko ya prevalence ya ugonjwa wa malaria ambao unaendana na tabia nchi. Wakati mchakato wa kuanza utafiti ule ikaonekana kwamba prevalence ya malaria imeshuka kwa kiasi kikubwa katika nchi za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara na kwa maana hiyo utafiti ule haukuendelea. Kwa sasa utafiti mwingine unaendelea kwenye kituo kile unaendeshwa na Taasisi yetu ya Utafiti ya NIMR kupitia kituo chake cha Amani kilichopo Tanga kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Muhimbili kuhusiana na namna ya kutumia teknolojia ya habari na mawasiliano katika kufikisha ujumbe unaohusiana na kupambana na maambukizi ya ugonjwa wa UKIMWI.
Kwa hiyo, siyo kwamba kituo kile hakitumiki, kituo kile kinatumika kwa matumizi yake ya awali ya utafiti, kama nitakapokitembelea kutakuwa kuna haja ya kuangalia namna ya kuweza kukifanya kitoe huduma nyingine mbali na zile huduma mahsusi tutashauriana ndani ya Serikali kuona kama tunaweza tukalichukua wazo hilo.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Afya nina maswali mengine kwake.
Kwa kuwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida ndiyo tegemeo kubwa kwa wananchi wa Mkoa wa Singida hususan wanawake katika kupata huduma za afya, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha Hospitali hii ya Rufaa inapata wataalam na madawa ya kutosha pamoja na vifaa tiba kama MRI, ultra sound na x-ray pamoja na gari la kubebea wagonjwa. (Makofi)
Kwa kuwa tayari kuna jengo ambalo limeainishwa kwa ajili ya kuanzishwa duka la madawa karibu na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida na kinachokosekana ni fedha za ukarabati wa jengo hilo?
Je, ni lini Serikali itapeleka fedha za kutosha kwa ajili ya ukarabati wa jengo hilo ili lianze kufanya kazi mara moja?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Namshukuru Mheshimiwa Aysharose Ndogholi Mattembe, Mbunge wa Viti Maalum, kwa maswali yake mawili ya nyongeza.
(a) Jibu letu la kwanza ni kwamba Serikali ina mikakati mingi kama ambavyo tulieleza wakati wa kipindi cha bajeti hapa Bungeni, miongoni mwa mikakati hiyo ni pamoja na kuongeza bajeti yetu ya dawa, vifaa, vifaa tiba na vitendanishi kwenye bajeti hii ya mwaka 2016/2017 kutoka takribani bilioni 26 zilizokuwepo kwenye bajeti ya mwaka uliopita mpaka bilioni takribani 252 kwenye bajeti hii mpya. Kwa hiyo, tukishakuwa na fedha za kutosha tutaweza kukidhi mahitaji ya hospitali zote nchini.
Mheshimiwa Spika, pili tunaendelea kuzishauri Halmashauri na Mikoa yote nchini watumie vizuri pesa wanazopata kutokana na user fees wanazo-charge kwa wagonjwa wakati wanaenda kupata huduma kwenye hospitali, pia pesa wanazopata kutoka kwenye Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya ili waweze kuzitumia vizuri kwa ajili ya manunuzi ya vifaa tiba, kwa sababu tunalenga katika muda mrefu kuhakikisha hospitali zetu za Wilaya na hospitali za Mikoa zinajitegemea zenyewe na ndiyo malengo ya Decentralisation by Devoluton.
(b) Kuhusiana na ukarabati, hili nimuachie Mheshimiwa Mbunge akashauriane na Katibu Tawala wa Mkoa wake, waone ni namna gani wanaweza wakafanya ukarabati wa hospitali hii wa jengo hili la theater na maabara na vitu vingine.
Mwisho nimtoe shaka Mheshimiwa Mbunge pamoja na Wabunge wote kwamba katika mwaka huu unaoendelea tuna mradi mkubwa wa vifaa tiba unaoitwa ORIO ambapo tutaweza kupata vifaa kama MRI, CT Scan, ultra sound na x-ray machines ambavyo amevitaja Mheshimiwa Mbunge na tutavigawa kwenye hospitali mbalimbali nchini.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nimshukuru Naibu Waziri kwa majibu. Nataka tu kuongeza sehemu ya pili ya swali la Mheshimiwa Aysharose Mattembe kwamba ni lini tutapeleka wataalam.
Mheshimiwa Spika, nataka kumthibitishia Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi karibuni tutaanza kutangaza nafasi kwa hiyo tutapeleka wataalam katika hospitali za Rufaa za Mikoa.
Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili tumekubaliana kwamba tunataka kuzifanya kweli hospitali za Rufaa za Mikoa ziwe Hospitali za Rufaa kwa hiyo tumetangaza nafasi tutafundisha wataalam watano katika kila Mkoa kwenye masuala ya usingizi, magonjwa ya akina mama, magonjwa ya watoto, upasuaji na mifupa.
Kwa hiyo niwaombe Waheshimiwa Wabunge kuwahamasisha Madaktari walio katika mikoa yao walete maombi, hatutampeleka mtu ambaye hatoki katika hospitali hizi za Serikali na Mashirika yasiyo ya Kiserikali.(Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Licha ya kupata majibu mazuri kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa Mkoa wa Morogoro hauna hata hicho kituo cha kutolea mikopo na mafunzo ya ujasiriamali, je, kuna mikakati gani ya kuanzisha kituo hicho kwenye Mkoa wa Morogoro?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, je, kituo hicho kitaanzishwa lini? Ahsante
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya 2016/2017, benki imetengewa shilingi bilioni 950. Kwa hiyo, nimuahidi kwamba katika mkoa ambao tutaupa kipaumbele ni Mkoa wa Morogoro ili tuweze kufungua dirisha la kuwawezesha wanaweke kupata mikopo. Hata hivyo, siyo katika Mkoa wa Morogoro tu tumepanga kwamba katika mwaka wa fedha wa 2016/2017 tufungue dirisha maalum ambalo litawawezesha wanawake kupata mikopo yenye riba nafuu angalau kati ya asilimia 10 mpaka 12. Kwa hiyo, hili jambo tutaweza kulianza mara tu utekelezaji wa bajeti ya 2016/2017 utakapoanza.
MHE. KHADIJA HASSAN ABOUD: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri. Napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, baada ya ushahidi kutolewa na mhukumiwa kupata adhabu, je, kuna mikakati gani au mipango gani inayochukuliwa kuwasaidia hawa watoto hasa wa jinsia ya kiume ili kuwaepusha na unyanyapaa pia kuathirika kisaikolojia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali namba mbili; naomba kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba ni hatua gani zinachukuliwa kuharakisha kesi hizi za udhalilishaji wa watoto ili kuepusha kukosekana au kupotoshwa kwa makusudi ushahidi na vielelezo muhimu na pia kwa sababu mtoto huyu anakuwa mdogo kupoteza kumbukumbu zake yeye mwenyewe binafsi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Swali la kwanza kwamba baada ya ushahidi kukamilika na hatua za kisheria kuchukuliwa kwa mujibu wa sheria na Mahakama dhidi ya mtuhumiwa, nini kinafanyika kwa mtoto aliyeathirika.
Mheshimiwa Naibu Spika, mtoto aliyeathirika na familia yake kwa ujumla kwa utaratibu wa kitaalam uliopo kwa sasa huchukuliwa na kurudi kwenye familia yake, pia huunganishwa na wataalam wa kutoa ushauri nasaha katika vituo vyetu mbalimbali vya kutolea huduma za afya. Anaweza akaunganishwa na Wataalam wa Ustawi wa Jamii ili aweze kurudi kuwa katika hali yake ya kawaida, lakini pia ataunganishwa na Wataalam wa Saikolojia na Wanasihi aweze kujengewa confidence ya kuweza kurudi sawa kama alivyokuwa zamani kabla hajafanyiwa vitendo hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kwamba ni nini Serikali inafanya. Serikali ina mikakati mingi ikiwemo hiyo kwanza kuwa na Sera ya Kuwalinda Watoto ya mwaka 2008, pili Sheria na tatu kuwa na utaratibu mahsusi wa kuweza kutoa ulinzi kwa watoto. Kwa maana hiyo, sasa hivi tunakwenda kukazia kwa kutunga sheria nyingine ya kudhibiti vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto. (Makofi)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSI, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, nataka kuongeza kwenye sehemu ya pili ya swali la Mheshimiwa Khadija Aboud kwamba, mikakati ya Serikali ni ipi katika kuhakikisha kesi hizi za udhalilishaji dhidi ya watoto zinaharakishwa. Tumeanza majadiliano na wenzetu wa Mahakama kwamba sasa Mahakama iwe na vipindi maalum ambavyo Mahakama itakuwa inasikiliza kesi tu za udhalilishaji dhidi ya watoto na wanawake.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na mawazo kwamba tutengeneze Mahakama Maalum za Watoto, lakini tumeona hapana, tunaweza tu tukawa katika kipindi fulani cha mwaka Mahakama inakaa na kusikiliza kesi za udhalilishaji wa watoto, maana yake tutaweza kuhakikisha wabakaji na walawiti wa watoto wote wanachukuliwa hatua haraka iwezekanavyo.
MHE. JOSEPHINA T. CHAGULA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Naomba nimwulize swali moja tu la nyongeza. Kwa kuwa kumekuwa na ongezeko kubwa sana la wagonjwa wa kisukari katika jamii yetu na inavyoonekana, jamii bado haijapata uelewa mkubwa kuhusu kujikinga na ugonjwa huu wa kisukari. Je, Serikali haioni ni muda muafaka kuja na mpango mkakati wa kutoa elimu kwa jamii ili kuweza kujikinga na baadhi ya vyakula pamoja na kubadilisha staili ya maisha yetu tunayoishi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda kumshukuru Mheshimiwa Josephina Tabitha Chagula, Mbunge wa Viti Maalum kwa swali lake la nyongeza. Nalijibu kwanza kwa kutambua ushiriki wake yeye mwenyewe kwenye mazoezi kila siku asubuhi na baadhi ya Wabunge. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, napenda kuwatambua Waheshimiwa Wabunge wote wanaounda timu ya Bunge Sports Club kwa jitihada wanazozifanya kuamka asubuhi na mapema na kwenda kushiriki kwenye mazoezi. Natoa rai kwa wananchi wote kufuata mfano mzuri anaouonesha Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge wote na mimi mwenyewe kwa kushiriki kwenye mazoezi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, siyo tu tunajenga afya zetu lakini pia sisi kama viongozi tunatoa mfano bora kwa wananchi wote kushiriki kwenye shughuli mbalimbali za kijamii, lakini pia kufanya mazoezi kwa ajili ya kulinda afya zetu. Kufanya hivyo, siyo tu kunajenga miili yetu, lakini pia kunaipunguzia gharama Serikali. Takwimu zinaonesha kwamba kufikia mwaka 2020 mzigo wa magonjwa duniani utakuwa mkubwa kiasi cha kufikia kiwango cha asilimia 73 na katika mzigo huo nchi za Afrika zinatarajiwa kuchukua share kubwa kuanzia mwaka huo wa 2020 niliyoutaja.
Mheshimiwa Naibu Spika, sababu ya hayo ni kwamba dynamics za maisha ya binadamu kwenye nchi zinazoendelea kama ya kwetu zimebadilika sana, hususan kwenye maeneo ya mijini ambapo lifestyle sasa imekuwa ni watu kukaa kwenye magari, watu kutokujishughulisha na shughuli mbalimbali ambazo ni physical ambazo zinaweza zikapunguza sukari mwilini na matokeo yake mzigo wa magonjwa ya kuambukiza unaongezeka siku hata siku.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto inaendelea kuwaelimisha wananchi kupitia vyombo mbalimbali vya habari, lakini pia ikishirikiana na wadau mbalimbali kama Tanzania Diabetes Association ambayo napenda kuitambua kwa mchango wake mkubwa kwenye kupambana na ugonjwa wa kisukari.
Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge tushiriki kwenye kuelimisha jamii kwenye majimbo yetu na ku-support michezo ili kuwaokoa watu wetu. (Makofi)
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali kuhusu vyuo hivi viwili vilivyoko Wilayani Mbulu, nami naomba kuuliza maswali madogo ya nyongeza. Kwa kuwa katika Chuo cha MCH - Mbulu hadi sasa wanafunzi wetu wamesitishiwa huduma ya chakula kutokana na madeni makubwa walionayo wazabuni. Je, ni lini Serikali itarudisha huduma hiyo ya chakula ili wanafunzi wetu wasome kwa amani? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa katika Hospitali ya Wilaya ya Mbulu kuna jengo la ghorofa lililojengwa takribani miaka mitatu na liko chini ya kiwango na kwa sasa halitoi huduma iliyokusudiwa. Je, Serikali inachukua hatua gani kuja kubomoa hilo jengo na kujenga jengo lingine jipya ili liweze kutoa huduma kwa hospitali yetu na chuo kwa ujumla?
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza linahusu chakula kwa wanafunzi wa Chuo cha Mbulu. Kwa mwaka mmoja uliopita, Serikali iliondoa utaratibu wa kupeleka bajeti ya chakula kwenye vyuo vyote vya MCH nchini na vyuo vyote ambavyo viko chini ya Serikali na badala yake huduma hizo zimekuwa zikitolewa na sekta binafsi kwa makubaliano na miongozo maalum inayotolewa na Serikali. Kwa maana hiyo, chuo hiki kinapaswa kifuate utaratibu huo mpya wa Serikali ili wanafunzi wapate huduma hiyo kutoka kwa washitiri binafsi.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili la jengo, kwa sababu ni swali jipya na jengo hilo silifahamu vizuri, naomba nisitoe commitment yoyote ile, ila nimuahidi tu Mheshimiwa Issaay kwamba tutaongozana ama nitamkuta Jimboni baada ya Bunge la bajeti ili nilitembelee jengo lenyewe, nijue ni mradi wa nani, chanzo cha fedha za kutekeleza mradi huo ni kipi na niweze kujua nitamshauri vipi yeye pamoja na uongozi mzima wa Halmashauri ya Mbulu ili tuweze kuona mradi huo ukitekelezeka kwa manufaa ya umma.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Pamoja na majibu hayo ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, katika Jimbo la Mafinga wananchi wa Kijiji cha Lungemba wamepisha eneo kwa ajili ya upanuzi wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii Lungemba na uthamini umeshafanyika. Je, ni lini sasa Serikali itawalipa wananchi wale ambao wamejitolea ardhi yao kwa ajili ya upanuzi wa Chuo cha Maendeleo ya Lungemba?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri kabla ya Bunge la bajeti nilifika Jimboni kwa Mheshimiwa Chumi na nafahamu miradi mbalimbali ambayo inatekelezwa pale. Kama kumbukumbu zangu ziko sahihi tayari zimetengwa shilingi milioni 200 kwa ajili ya kuwalipa fidia wananchi wa eneo lile. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kulikuwa kuna mgogoro kidogo, kuna baadhi ya wananchi walikubali kuchukua hiyo fidia ambayo walikuwa wanapewa, lakini kuna baadhi ya wananchi hawakukubaliana na fidia ambayo ilikuwa inatolewa na hivyo hawakuzichukua na ulipaji wa fidia ukawa kama umesimama. Hivyo, namsihi Mheshimiwa Mbunge, akishirikiana na viongozi wenzake kwenye Halmashauri, watumie jitihada za kuwashawishi wananchi wakubaliane na fidia ambazo zinatolewa na Serikali ili chuo hicho kiweze kuendelezwa na wananchi waweze kupata huduma inayostahili. Nitoe rai kwa wananchi wa eneo lile kwamba miradi ya maendeleo inapokuja kwenye maeneo yao waikumbatie na badala ya kukwepa fidia washirikiane na Serikali ili kuendeleza miradi husika.
MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Katika Wilaya yangu ya Kibondo, Jimbo la Muhambwe, kuna Chuo cha MCH ambacho kwa muda mrefu sasa karibu miaka mitano wamejaribu kujenga maabara, wamekwishafikia mpaka ngazi ya kupaua, wamekwishaweka mbao mwaka wa pili na nusu sasa na hakijapauliwa. Ni lini Serikali itapeleka pesa kwa ajili ya kupaua jengo hilo la maabara?
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini? Ni pale ambapo uwezo wetu wa kibajeti utaruhusu.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Naomba niulize swali la nyongeza, kwa kuwa, hali ya Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Tango, FDC inafanana na kile cha Mtawanya, kilichopo Mkoani Mtwara, je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuboresha miundombinu ya chuo hicho lakini pia kuboresha utoaji wa taaluma katika Chuo hicho cha Maendeleo ya Wananchi Mkoani Mtwara?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, Serikali ina mpango mkakati mpya kabisa wa kufanya maboresho kwenye Vyuo vyote vya Maendeleo ya Wananchi hapa nchini. Mpango wetu ni kwamba, tayari tumeanza mazungumzo na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ili tuweze kuvihamishia kwenye Wizara hiyo badala ya kubaki navyo sisi kwenye Wizara yetu. Lengo hasa ni kuboresha mitaala inayotolewa kwenye vyuo hivi lakini kuboresha administration ya vyuo hivi na kuongeza bajeti. Kwa maana hiyo, Mheshimiwa Chikota, mpango tulionao ndiyo huo.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Hata hivyo, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, NHIF wamekuwa wakitafuta viwanja kule Mtwara kwa ajili ya kujenga kituo kwa ajili ya kutolea huduma za kisasa. Kwa nini wasishirikishwe katika ujenzi huu wa Hospitali ya Kanda ya Kusini badala ya kufanya duplication ya kujenga huduma ambazo zinafanana?
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa nini Serikali isitenge pesa zake yenyewe kwa kiasi cha kutosha ili kuhakikisha kwamba ujenzi huu unakamilika kwa haraka kwa sababu umeanza tangu mwaka 2009 na sasa hivi tuko 2016, ni karibia mika saba sasa. Je, wako tayari kutenga pesa zake za kutosha katika bajeti ya mwaka 2017/2018 badala ya kuendelea na mazungumzo ambayo yanaonyesha kutokuzaa matunda?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii, pia namshukuru sana Dada yangu, Mheshimiwa Hawa Abdulrahman Ghasia, Mbunge wa Jimbo la Mtwara Vijijini kwa maswali yake mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nitumie nafasi hii kumpongeza sana kwa jitihada anazofanya kufuatilia ukamilishaji wa mradi huu wa hospitali, yeye pamoja na Mheshimiwa Abdallah Chikota wamekuwa wakinisumbua sana kuhusu utekelezaji wa mradi huu.
Kwa msingi huo mimi mwenyewe nilifanya ziara kwenye mradi huu na mpaka sasa nimekwisha kufanya ziara mbili za kazi na katika ziara moja tuliongozana na wenzetu wa NHIF ambao ni Mfuko wa Bima ya Afya ya Taifa ambao upo chini ya Wizara yetu na kuwapa ushauri badala ya wao kujenga hiyo Center of Excellence ambayo wamekusudia kuijenga kule Kusini wafanye tathmini na watazame namna ya kutumia fedha zile ambazo walizikusudia kwa mradi wao kuwekeza kwenye kukamilisha mradi huu wa Hospitali ya Kanda ya Kusini, hivyo wazo lake na sisi tulikwishaanza kulifanyia kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lile swali la pili kwamba kwa nini Serikali haitengi pesa za kutosha kwenye bajeti yake; ni kwamba tayari mradi huu umekuwa ukitekelezwa kwa kasi kidogo na Serikali na majengo kwa sehemu kubwa ya kuanzia yamekwisha kukamilika yako takribani asilimia 95 kuanza kutumika na mimi katika ziara zangu nimewaelekeza namna ya kuanza utekelezaji wa mradi wenyewe hivyo hivyo ulipofikia kuliko kuusubiria mpaka ukamilike ili walau huduma za mapokezi, huduma za dharura lakini pia huduma za out patients (huduma za wagonjwa wa nje) zianze kutolewa kwa kutumia majengo ambayo tayari yanaelekea kukaimilika kwa sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa tumekwisha kuwekeza takribani shilingi 1,782,000,000, na katika Bajeti ya mwaka 2016/2017, Serikali kwenye bajeti yake imetenga shilingi bilioni mbili kwa ajili ya mradi huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimuahidi kwamba tutaendelea kuitazama hospitali hii Ili kwenye bajeti ya mwaka 2017/2018 tuweze kutenga fedha za kutosha kwa ajili ya awamu ya tatu ya utekelezaji wa mradi huu.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaitwa Susan Lyimo. Nashukuru kwa majibu mafupi sana ambayo hayana uelekeo; nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Kamati ya UKIMWI ilipotembelea MSD, pamoja na mambo mengine ilipata taarifa kwamba kuna shehena kubwa sana ya dawa za UKIMWI ambayo ilikwama bandarini kwa sababu ya kutokulipa VAT, nataka kujua kama dawa zile tayari yameshaondoka bandarini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; natambua kwamba wafadhili wengi walisema watajitoa na hivyo Serikali ikaanzisha Mfuko wa UKIMWI, nataka kujua mpaka sasa hivi mfuko huo una kiasi gani cha fedha hasa ikizingatiwa kwamba wagonjwa hawa au waathirika hawa wakishaanza kutumia madawa wanapaswa kuendelea kuyanywa mpaka mwisho wa maisha yao. Nataka kujua mfuko huo toka umeanzishwa mpaka leo una kiasi gani cha fedha na tusipewe ahadi za uongo kama ambavyo tumesikia?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kumtoa hofu kwamba Serikali haishindwi kuwahudumia wagonjwa wa UKIMWI katika nchi hii, lakini ni utaratibu wa kawaida tu wa kujenga mahusiano mema na marafiki ambao wanajitokeza kutusaidia kubeba mzigo mzito wa kutoa huduma za afya kwa watu wetu. Na huu ni utamaduni wa nchi zote duniani na haitarajiwi hata mara moja kwamba itafika siku wataamua ghafla kusitisha misaada hii ambayo wanaitoa kwa wagonjwa wa UKIMWI, lakini kama tutafika huko tayari tumeandaa fall back position kwa kuanzisha Mfuko wa UKIMWI anaouzungumzia, na mfuko huo tumeanza kuuwekea bajeti kwenye bajeti hii iliyopita na tumeanza kwa kiwango kidogo cha shilingi bilioni sita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaendelea kuwashirikisha wadau mbalimbali wa maendeleo waweze kuchangia fedha kwa ajili ya kuwekeza kwenye mfuko huu. Na nitoe rai kwake Mheshimiwa Mbunge na kwa Waheshimiwa Wabunge wote kwa ujumla tujitolee kuchangia Mfuko wetu wa UKIMWI kadri tutakavyoweza na pia hata kuvutia marafiki wawekeze kwenye mfuko huo ili iwe fall back position ambayo ina uwezo wa kutosha huko mbeleni kwa ajili ya kuwahudumia wagonjwa wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisahau kuhusu shehena ya dawa, hakuna shehena ya dawa mpaka hivi sasa ambayo imekwama popote pale na kwamba dawa zinapatikana nchini kwa asilimia mia moja. Kwa sababu taarifa za dawa za UKIMWI na miradi misonge yote tunazipata kila wiki, kwa update niliyonayo kufikia Ijumaa iliyopita hakukuwa na shehena ya dawa iliyokwama bandarini, lakini dawa zote zipo kwenye bohari zetu za mikoa na bohari za kanda kwa kiwango cha asilimia mia moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nizungumzie jambo la kitaalam, tukisema kuna availability ya dawa kwa asilimia mia moja, tunamaanisha kwenye Bohari ya Taifa kuna dawa zinazojitosheleza kutumika kwa miezi sita mbele na kwenye bohari za mikoa tuna dawa za kujitosheleza kwa matumizi ya miezi mitatu mbele na kwenye bohari za wilaya tuna dawa za kujitosheleza kwa mwezi mmoja mbele hiyo ndiyo availability tunayoizungumzia ya asilimia mia moja, sasa kwenye dawa zote za miradi misonge zikiwemo dawa za UKIMWI tuna availabaility a hundred percent.
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa majibu yasiyoridhisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama za vipimo ni kubwa mno kwa wananchi wetu maskini ambao tunawawakilisha. Nafikiri ni vizuri Waziri akatamka ni lini ataruhusu watu binafsi kuweka x-ray na vipimo vingine kwenye hospitali za binafsi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii x-ray ziko madukani, Waziri yuko tayari kwenda kufunga hospitali ya mtu lakini hayuko tayari kuamrisha x-ray zilizoko madukani ziende kwenye hospitali za Serikali ili zihudumie wananchi wetu wanaokufa kila siku.
Kama kwa nchi nzima suala hili haliwezekani, namuomba Mheshimiwa Naibu Waziri lifanyiwe majaribio kwenye Halmashauri ya Mji wa Kahama ambapo hospitali hiyo inahudumia zaidi ya Halmashauri 15 ikiwemo na Halmashauri ya kwake mwenyewe. Naomba majibu.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Namshukuru kaka yangu Mheshimiwa Jumanne Kibera Kishimba kwa swali lake la nyongeza na nimpongeze kwa kazi nzuri anayoendelea kuifanya kuwahudumia wananchi wa jimbo lake la Kahama Mjini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ubunifu anaouzungumzia wa kutumia watu binafsi kutekeleza miradi mbalimbali ya kufunga vifaa na vifaa tiba vya kutolea huduma za afya hususani vya uchuguzi wa magonjwa kama x-ray na ultra-sound kwenye hospitali za Serikali ni ubunifu ambao tunaukubali. Anasema ni lini mimi nitaruhusu kwenye Wizara yetu; napenda kumtaarifu tu kwamba Serikali tayari inaruhusu ubia wa sekta binafsi na Serikali (Public Private Partnership – PPP) na ina sheria mahususi ambayo ilitungwa na Bunge hili miaka kadhaa iliyopita kwa hivyo siyo jambo jipya; sema modality ya mikataba hii iweje na nani afunge lini na mkataba na nani na kwa sababu zipi ndizo taratibu ambazo tunazitazama siku hata siku na tunazitazama kwa kesi kadri zinavyokuja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo kama Halmashauri ya Kahama Mjini inapenda kufanya mikataba ya namna hiyo Mheshimiwa Mbunge azungumze na wataalam kwenye Halmashauri yake, wafuate taratibu za ndani ya Serikali za kuingia mikataba ya PPP ili waweze kupata vibali kutoka Hazina, Wizara ya Afya na TAMISEMI waweze kutekeleza mipango hiyo ila ni jambo ambalo tunalikubali.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri amefika katika hospitali ya Hydom, lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa Naibu Waziri amekiri kwamba hospitali hii imepandishwa hadhi miaka sita toka 2010 hadi leo ya kuwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa na haijapata hata siku moja ile haki ya kibajeti ya hospitali ya Mkoa. Je, sasa ni lini hospitali hii itatengewa bajeti ili ifanane na hospitali zote za Rufaa za Mikoa ya Tanzania?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa kwenye majibu ya msingi amesema hospitali hii ina tatizo la miundombinu na watumishi. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuijengea uwezo na kuipatia watumishi ili hospitali ya Haydom iweze kutoa huduma kwa sababu na yeye amekiri kwamba inafikika na maeneo ya jirani na mikoa hii?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Flatei Massay kwa ufuatiliaji anaoufanya kiasi kwamba amenilazimisha kufika kwenye hospitali hii katika ziara zangu mara mbili toka nimeteuliwa katika nafasi hii. Katika mara zote nimefika na kutatua changamoto mbalimbali ambazo zimekuwa zikiikabili hospitali hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli ni kwamba, pamoja na kwamba hospitali hii ingependa iwe Hospitali ya Rufaa ya Kanda bado haijakidhi vigezo. Pili, kuteuliwa kuwa hospitali ya ngazi ya Kanda hakuifanyi hospitali kudai haki ya kupewa fedha kibajeti wakati haimilikiwi na Serikali. Serikali inashirikiana na mashirika ya hiyari kama KKKT kutoa huduma kwa wananchi kwa kuwawezesha kupata michango ya health basket fund pamoja na watumishi ambao wanapelekwa by secondment na Serikali kwenye hospitali husika. Kwa sasa, Mkoa wa Manyara una hospitali yake ya rufaa ya mkoa na Serikali inaijengea uwezo hospitali hii ili iweze kutoa huduma ambazo zinaendana na hadhi ya hospitali ya rufaa ya mkoa.
MHE. MUNIRA MUSTAFA KHATIBU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Kwanza, nakushukuru Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa majibu yake mazuri ambayo amenijibu, lakini napenda kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Je, ni utaratibu gani uliotumika kugawa hivi vifaa katika hospitali zetu za wilaya na mikoa kwa sababu vifaa hivi ndani ya hospitali zetu za wilaya na mikoa havionekani?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, je, ni utaratibu gani unaotumika kuwapa elimu akinamama wajawazito kuweza kuwalea watoto hawa?
NAIBU WAZIRI, WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Kangaroo Mother Care haihitaji vifaa vyovyote vile, kwa sababu ni huduma ambayo inatolewa na aidha mzazi mama, baba, ama mtoa huduma yeyote yule ambaye atakuwa amechaguliwa na familia kutoa huduma hiyo. Huduma hii inahusisha kumchukua mtoto kumweka kifuani ngozi kwa ngozi na mzazi huyo, mara nyingi inakuwa ni mama. Kwa maana hiyo, hakuna vifaa vinavyohitajika pale zaidi ya mashuka na mablanketi ambayo yanagawanywa kwenye hospitali zote nchini kwa utaratibu wa kawaida wa kila siku.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa sasa kupitia Wizara ya Afya ina encourage zaidi kutoa huduma kwa kutumia njia hii ya Kangaroo Mother Care na ndiyo maana hatuwekezi sana kwenye kujenga vituo maalum pembeni kwa ajili ya kuwatenga watoto na wazazi wao, kwa sababu imeonekana wakikaa na wazazi wao wanajengwa afya zao kisaikolojia zaidi.
MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa lengo la Serikali la kuanzisha benki hii ni kuwasaidia wanawake wanyonge waliopo vijijini; na kwa kuwa masharti ya Benki ya Wanawake haina tofauti na masharti ya mabenki mengine; na kwa kuwa riba inayotozwa na benki hii pia haina tofauti na riba inayotozwa na mabenki mengine. Je, lengo la Serikali la kuanzisha benki hii kuwasaidia wanawake wanyonge limefikiwa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa wanawake wengi wao wapo vijijini na benki hii haijaweza kuwafikia wanawake hao wa Tanzania waliopo vijijini. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba wanawake wengi wanyonge waliopo vijijini wanafikiwa na huduma ya benki hii?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, (a) swali lake linahusu riba ya benki hii kuwa sawa na riba inayotolewa na mabenki mengine. Majibu yetu ni kwamba mwezi Machi mwaka huu wakati tukisherehekea sherehe ya Siku ya Wanawake Duniani, Waziri wa Afya alitoa agizo tena kwenye mkutano wa hadhara kwa Mkurugenzi wa Benki hii kwasababu kipindi hicho hakukuwa na bodi, waweze kulishughulikia suala hilo, ili kutengeneza dirisha maalum ambalo litawafikia wanawake wa nchi hii na mikopo yenye riba nafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa msimamo wetu ni kwamba bodi ambayo tayari Mheshimiwa Waziri ameiunda inalishughulikia suala hilo na tutatoa majibu baada ya kupata mwongozo kutoka kwa bodi husika ni namna gani wametekeleza agizo la Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wanawake wa vijijini watafikiwa na benki hii lakini pia pamoja na benki nyingine lakini pia pamoja na schemes nyingine za kuwawezesha wanawake kujiendeleza katika shughuli mbalimbali za kiuchumi. Na ndiyo maana kwenye Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015/2020 Serikali imeanzisha mpango wa kupeleka shilingi milioni 50 kwenye kila kijiji kwa ajili ya kuwafikia makundi mbalimbali ya kujijenga kiuchumi. Benki yetu itaendelea kushirikiana na benki nyingineza kijamii kama hizi community banks na benki nyingine kubwa ili kuweza kutoa mikopo kwa wanawake.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naitwa Sophia Mwakagenda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na nataka kujua commitment ya Serikali juu ya benki hii ya wanawake ni lini itaiongezea ruzuku ili hiyo riba ambayo imekuwa ni kubwa iweze kuwa ndogo kuweza kusaidia kuwakopesha wanawake hasa wa vijijini?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, commitment ya Serikali inajionesha wazi kwa Serikali kutenga bajeti ya shilingi bilioni moja kwenye mwaka huu wa fedha kwa ajili ya kuiwezesha benki hii kufungua dirisha maalum kwa ajili ya mikopo kwa wanawake. Hiyo ndio commitment yetu tunasubiri utekelezaji tu.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba niulize swali moja dogo la nyongeza.
Kwa kuwa walengwa ni wakina mama ambao wengi wao bado wako Vijijini kama muuliza swali alivyosema. Lakini ukiangalia riba wanatozwa ni sawa sawa na wafanyabiashara wa kawaida na wao wanategemea kilimo. Sasa je, benki hii ili wafikie akina mama wakulima walipo maeneo tofauti na kule Kilolo inaonaje sasa ikiwapa mkopo uwe wa muda mrefu badala ya kuwapa kama wafanyabiashara ndogo ndogo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la riba ni suala ambalo linazingatia masharti yanayotolewa na regulator ambaye ni Benki Kuu na kutokana na masharti hayo benki yetu haiwezi kukiuka masharti ambayo yanawekwa na Benki Kuu ili tu kuwafikia akina mama na ndiyo maana Waziri wa Afya aliagiza tutengeneze scheme maalum kwa ajili ya kuwafikia akina mama wa vijijini na akina mama wajasiriamali wadogo wadogo ili riba itakayotolewa na benki hii iwe ni mahususi na iwafikie akina mama hawa waweze kupata mikopo nafuu zaidi kuliko ilivyo sasa. Kwa hiyo, suala hili tunaliangalia.
MHE. SILAFU J. MAUFI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri katika suala, hili ninapenda kuuliza maswali ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la vifaa hivyo anavyovizungumzia ambavyo vinasambazwa katika maeneo yetu ya zahanati, kwa Wilaya yetu ya Sumbawanga, Wilaya ya Nkasi, Wilaya ya Sumbawanga Vijijini pamoja na Kalambo vifaa hivi havipo. Kama vinasambazwa vinasambazwa lini? Na je, Serikali itachukua mpango upi mkakati wa kuweza kufuatilia na kuhakikisha kwamba vifaa hivi vimesambazwa katika maeneo yetu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni kwamba Mkoa wa Rukwa ni Mkoa uliopo pembezoni; ni Mkoa ambao hauna Hospitali za Wilaya. Hata juzi Mheshimiwa Malocha alizungumzia suala la Hospitali ya Wilaya, kwa maana ya kituo cha Rahela kipasishwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini bado Mkoa wa Rukwa hauna Hospitali ya Wilaya, kwa hiyo ndio maana hospitali yetu ya Rufaa ya Rukwa inakuwa na msongamano wa wagonjwa wengi katika eneo lile.
Sasa ni lini Serikali itahakikisha zahanati zetu, vituo vyetu vya afya vinakuwa katika ukamilifu wake na vifaa tiba vyake ili kuondoa msongamano katika Hospitali yetu ya Mkoa wa Rukwa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwamba vifaa vitasambazwa lini? Mpaka sasa tunavyozunguza, hatujaanza kuvisambaza vifaa hivi kwa sababu vifaa hivi 500,000 vinatokana na tamko alilolitoa Mheshimiwa Waziri wa Afya wakati wa bajeti kama mpango maalum. Bajeti imeanza kutekelezwa mwezi Julai na bado hatujapokea fedha kwa ajili ya kutekeleza mpango huu mzuri ambao Waziri wa Afya ameuanzisha kwa majaribio mwaka huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vifaa ambavyo vinapaswa kuja kwa utaratibu wa kawaida vimeendelea kupelekwa kwenye vituo vyote vya kutolea huduma za afya nchini na hivi 500,000 ni kwa ajili tu ya kufanya majaribio ya kuona kama tukiwapa delivery packs akinamama wanaoenda kujifungua, pengine inaweza ikasaidia kupunguza changamoto mbalimbali zilizopo kwenye mfumo. Kwa hiyo, huu ni mpango mpya na maalum na bado haujaanza kutekelezwa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge asiwe na shaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuhusu Vituo vya Afya na Zahanati kuweza kutoa huduma kwenye Mkoa wa Rukwa; kwanza, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya Bunge hili, ziara yangu ya kwanza ni Mkoa wa Rukwa. Mwezi uliopita kabla ya bajeti hii ya Bunge hili nilifika kwenye Mkoa wa Katavi. Baada ya Bunge hili nitafika kwenye Mkoa wa Rukwa kuona ni namna gani tunaweza tukashirikiana nao kuwawezesha kuanzisha huduma za upasuaji na huduma za maabara kwenye vituo vyote vya afya vilivyopo kwenye mkoa huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na Hospitali za Wilaya, yeye kama Mbunge akishirikiana na Wabunge wa Majimbo, wanapaswa kukaa kwenye vikao vyao vya Halmashauri na kupanga mpango kabambe wa kujenga hospitali hizi na Serikali Kuu itawasaidia pale ambapo watakuwa wamekwama. Napenda watambue kwamba jukumu hili ni lao kama Halmashauri kuanzisha miradi ya ujenzi wa Hospitali za Wilaya na sisi Serikali Kuu tunawajengea uwezo tu.
MHE. AYSHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona na kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tatizo lililopo katika Mkoa wa Rukwa halina tofauti na tatizo lililopo katika Mkoa wa Singida.
Swali; je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha Hospitali za Wilaya za Mkoa wa Singida na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida inapata vifaa tiba vya kutosha kama vitanda vya kujifungulia ili kuwasaidia wanawake wajawazito ambao hutumia muda mrefu wa kutembea kufuata huduma hizo za afya?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba Mheshimiwa Aysharose atambue kwamba, mimi kama daktari na kama baba wa wanawake na kama mume wa mwanamke, nina passion ya kipekee na mambo yote yanahusu wanawake na ndiyo maana nikapewa jina la Balozi wa Wanawake. Kwa msingi huo, toka nimeteuliwa kwenye nafasi hii, nimezunguka kwenye zaidi ya vituo 120 vinavyotoa huduma za afya nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ziara zangu nimekuwa nikihamasisha ujenzi wa theatre na maabara ambazo zitakwenda kuboresha huduma ya mama na mototo kwenye vituo vyote vya kutolea huduma za afya nchini. Hivyo, namhakikishia kwamba vifaa tiba ni sehemu muhimu ya mpango huu ambao tumeuanzisha wa kuboresha huduma za upasuaji na huduma za akinamama wajawazito kwa ujumla wake. Kwa hiyo, Mkoa wa Singida nimeshafika mara mbili toka nimeteuliwa na katika ziara zangu nimekuwa nikihamasisha mambo haya yatekelezwe na Halmashauri zenyewe, maana mpango huu siyo wa kwetu.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Kwa kuwa lengo la Serikali ni kutoa huduma za afya kwa mama wajawazito bure, hiyo ni nia nzuri; lakini katika Mkoa wa Mwanza, baadhi ya visiwa vimekosa huduma za afya kwa sababu ya ukosefu wa Vituo vya Afya pamoja na Zahanati; Visiwa hivi viko katika Wilaya ya Buchosa ambavyo ni visiwa vya Soswa, Nyamango, Chamagati, Gembale, Nayonzwa pamoja na Kata ya Buryaheke kule Wilayani Buchosa. (Makofi)
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba katika visiwa hivyo kunajengwa Vituo vya Afya ili kuwasaidia akinamama wajawazito wasitembee umbali wa zaidi ya kilometa 40 kupata huduma za afya?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mkakati wa kwanza, kila mwaka tunatenga fedha kwenye bajeti kwa ajili ya kuboresha huduma za akinamama wajazito na watoto. Mkakati wa pili, tayari Serikali inafanya mkakati wa ku-optimize huduma zinazotolewa kwenye Vituo vya Afya, ndiyo huo niliouzungumza wakati nikijibu swali la Mheshimiwa Aysharose, kwamba tunahakikisha vituo vyote ambavyo vimesajaliwa kama Vituo vya Afya, vinatoa huduma optimally, yaani huduma za upasuaji na huduma za kimaabara kama ambavyo Sera ya Afya inaelekeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wa tatu umetangazwa juzi na Mheshimiwa Waziri wa Afya wakati wa Mkutano wa Global Financing Facility (GFF), ambapo tutajenga vituo 100 vipya vya afya na kufanya maboresho kwenye vituo hivyo kwa ajili ya kuboresha utoaji wa huduma za akinamama wajawazito na watoto.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa sababu ambazo Madaktari Wakuu au Waganga Wakuu wamekuwa wakitoa kwa suala zima la ukosefu wa dawa katika hospitali zetu ni kwamba, kundi hili la msamaha la wazee, akinamama wajawazito na watoto ni wengi na wanaugua mara kwa mara. Naomba nifahamu, Serikali mmefanya utafiti kwa kiasi gani ili kuona kwamba hili kundi halilemei makundi mengine na kusababisha ukosefu wa dawa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kundi la wazee linapewa kipaumbele cha kipekee kwenye Serikali ya Awamu ya Tano, ndiyo maana kuna portfolio maalum ambayo iko chini ya Waziri wa Afya inayosimamia mambo yanayohusu maslahi ya wazee. Kwa msingi huo, huduma hizi za afya kwa wazee zimepewa kipaumbele na Waziri na ndiyo maana alipoteuliwa tu, alitangaza kwamba wazee wapewe dirisha lao maalum, lakini pia wazee wapate haki ya kutibiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakoelekea, tumezielekeza Halmashauri zote nchini ziwakatie Bima ya Afya, aina ya CHF (Mfuko wa Afya ya Jamii), wazee wote waliopo kwenye Halmashauri zao ili wazee hawa badala ya kusema tu wanatibiwa bure, watibiwe kwa kutumia kadi zao za CHF.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kwanza niulize swali linalohusiana na Halmashauri yangu ambayo inavyo Vituo vya Afya, cha Mahurunga na Kitere, ambavyo vinavyo vyumba vya upasuaji na vifaa vyote vinavyohitajika; lakini mpaka sasa hivi havijaweza kufanya kazi kwa sababu hakuna watalaam wa kuweza kufanya hizo huduma suala ambalo linakatisha tamaa kujenga vituo vingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika bajeti iliyopita tuliiomba Serikali itenge pesa kupitia mafuta kwa ajili ya kujenga Zahanati na Vituo vya Afya, Serikali ikatuahidi kwamba tuipe muda ifanye tathmini nchi nzima ili kujua mahitaji halisi na kujua majengo mangapi hayajakamilika. Tulitaka kufahamu, je, Serikali sasa imeshakuwa tayari, imeshafanya hiyo tathmini ili iweze kuingizwa katika bajeti inayokuja?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Napenda kujibu maswali matatu; kwanza, la Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti, Mheshimiwa Hawa Ghasia la kuhusu Kituo chake cha Afya, ambacho kina kila kitu, lakini hakina watalaam; ana vituo viwili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba, sekta ya afya ina upungufu wa watalaam takriban asilimia 48, lakini tayari Mheshimiwa Rais juzi amezungumza kwamba tutaajiri watalaam katika Sekta ya Afya, kwa hiyo, tutapanga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunasubiri kuajiri watalaam, nitumie Bunge lako Tukufu kuwaelekeza Makatibu Tawala wa Mikoa wawapange upya watalaam walionao. Unaweza ukaenda katika Kituo cha Afya ukakuta kina watalaam 18, lakini kituo kimoja cha afya katika Wilaya hiyo hiyo kina watalaam watatu. Kwa hiyo, hili ni jukumu la Makatibu Tawala wa Mikoa kufanya redistribution.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili la Mheshimiwa Hawa Ghasia kwamba, je, ule mpango wa kufanya tathmini ya maboma ya Vituo vya Afya, tumefikia wapi? Ni kweli Wizara ya Afya pamoja na Ofisi ya Rais (TAMISEMI), baada ya kupitisha bajeti ya mwaka 2015, tulifanya tathmini na tumesha-identify kuna maboma mangapi ya Zahanati, kuna Vituo vya Afya vingapi ambavyo havijakamilika; na tayari Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango yuko hapa, tumekubaliana badala ya kusema tunaenda kuvimaliza vyote katika mwaka mmoja, ndiyo narudi katika swali la Mheshimiwa Zacharia. Tuta-pick angalau Kituo cha Afya kimoja katika kila Halmashauri badala ya kusema tutafanya Kituo cha Afya katika kila Kata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mkakati wetu kila mwaka angalau Kituo cha Afya kimoja kwa kila Halmashauri baada ya miaka mitatu tutakuwa na Vituo vya Afya takriban 500, asilimia 100 zaidi ya Vituo vya Afya 500 ambavyo vimekuwepo nchini miaka 50 baada ya uhuru, sisi tutavipata katika kipindi cha miaka mitatu. Kwa hiyo, tutaleta katika bajeti ya mwakani hivyo, kituo kimoja cha afya kwa kila Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la Mheshimiwa Gekul, ni kweli hii sera ya msamaha kwa wajawazito, wazee na watoto chini ya miaka mitano, ndiyo mojawapo ya sababu ya changamoto katika upatikanaji wa dawa, vifaa na vifaa tiba katika Vituo vya Afya vya Umma. Sasa ni takriban asilimia 60 kwa kweli ya watu ambao wanahudumiwa katika hospitali zetu za umma, ni hawa watu wa msamaha. Kwa hiyo, hawachangii wakati Sera ya Afya inasema, huduma za afya ni kuchangia. Mkakati wetu ni upi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri amesema, nilitaka kuongeza, tunazungumzia financing for the health sector, jinsi gani tutatengeneza, jinsi gani tutagharamia Sekta ya Afya. Kwa hiyo, tunaenda kwenye Bima ya Afya kwa kila Mtanzania; maana yake, Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya kuwakatia Bima ya Afya wanawake, wazee na watoto wa chini ya miaka mitano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi wa Pili tutakuja kwako Bungeni, tulete mapendekezo yetu na tunategemea moja ya vyanzo vya fedha hizi ni zile kodi zinazotokana na mambo ya madhambi; sin taxes. Kwa mfano, pombe, sigara na bia na naamini Waziri wa Fedha na Mipango atatukubalia kwa ajili ya kufikia Universal Health Coverage itakapofika mwaka 2020.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina swali moja la nyongeza.
Je, Serikali imeandaa utaratibu wowote wa kuwakagua watoto ambao wapo chini ya umri wa miaka mitano katika kliniki au wasiohudhuria kliniki ili kuweza kupata takwimu sahihi za watoto ambao wamekeketwa chini ya miaka mitano ili kufahamu ukubwa wa tatizo ukoje? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ni kwamba katika mfumo wa kutoa huduma za afya nchini watoto wote chini ya umri wa miaka mitano wanapaswa kuhudhuria kliniki ya RCH ili wapate chanjo mbalimbali lakini pia wazazi wao waweze kufikiwa na elimu mbali mbali ambazo zinatolewa kila siku kabla ya kuanza kwa kliniki hizo.
Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na utaratibu huo watoto wote wachanga sasa hivi kuna mpango maalum chini ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto wa kuwaelimisha wauguzi wote nchini kufanya ukaguzi maalum wa watoto hususani wa kike kuhusiana na mambo ya ukeketaji ili tuweze kuwabaini wazazi ambao wamewapeleka watoto wao wachanga kufanyiwa ukeketaji.
Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo huduma hiyo sasa ipo na inaendelea kutolewa nchini. Nitoe onyo kwa wazazi wote ambao wanaendelea na vitendo hivi, kwamba wakikamatwa hatua kali zitachukuliwa dhidi yao kwa sababu kufanya hivyo ni kinyume cha sheria.
Mheshimiwa Spika, kwa sababu sasa hivi utaratibu umehama badala ya kuwakeketa mabinti wakubwa, sasa hivi wazazi wamegundua kwamba wawakekete watoto wachanga. Jambo hili halikubaliki na tutachukua hatua kali, na ndiyo maana tumeweka sasa mkakati wa kutoa elimu kwa wauguzi wafanye ukaguzi maalum kwa watoto wa kike kama wamekeketwa ama la, kwa hiyo utaratibu upo.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina maswali mawili ya nyongeza. Ni wazi kwamba suala la Palliative Care yaani Tiba Shufaa hapa nchini halijaeleweka kabisa, naamini hata wewe labda huelewi na vilevile Wabunge wengi sana hawaelewi. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri sasa yuko tayari, kutoa semina kwa Wabunge wote ili wapate uelewa wa maana ya Palliative Care? Vilevile, elimu hii pia itolewe kwa wananchi wote ili waweze kulielewa na waweze kuwasaidia wagonjwa wetu ambao wanakufa katika mazingira magumu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa, Mheshimiwa Naibu Waziri anakiri kwamba tuna tatizo kubwa la wahudumu wa afya, ambao pia hawana huo uelewa. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri atakubaliana na mimi kwamba, kuna haja kubwa sasa ya kuhakikisha kwamba tunakuwa na curriculum ya Palliative Care katika courses za undergraduate kama wanavyofanya wenzetu wa Kenya na Uganda ili sasa tuwe na wataalam wa kutosha kwa hii huduma, hasa tukizingatia sasa kwamba kuna magonjwa mengi ya kusendeka (chronic diseases) ambayo yako nyingi na kwa maana hiyo, wagonjwa ni wengi na hawapati huduma hiyo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Swali la kwanza, Waziri alikuwa ananinong’oneza hapa, uzuri Waziri wangu anakaa nyuma ya kiti cha kujibia maswali, kwamba yuko tayari kuleta semina kwa Wabunge wote kwa ajili ya kutoa elimu ya Tiba Shufaa (Palliative Care).
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ufupi Palliative Care ni nini? Kwenye mfumo wa afya, Palliative Care ni huduma ambayo inatolewa kwa wagonjwa ambao ni terminally ill, yaani wagonjwa ambao wanaumwa magonjwa ambayo sasa imefika wakati sayansi ya tiba haiwezi kuyatibu. Kinachofanyika sasa ni kutoa huduma ya kupunguza maumivu, lakini pia huduma ya ushauri nasaha na huduma ya kiroho (Spiritual Services). Kimsingi ni kumtibu mgonjwa holistically kwa kumtazama kwa ujumla wake, mgonjwa kama mgonjwa kama binadamu na sio kutazama ugonjwa ambao mgonjwa anaumwa.
Mheshimiwa Niabu Spika, swali lake la pili, kuhusu curriculum naomba kwanza nieleze jitihada za Serikali kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, tayari tuna Sera ya Taifa, ambayo inatoa mwongozo kwenye huduma za tiba shufaa, ambayo mwezi Juni, 2016 imeanza kutumika. Sera hii inaelekeza sasa kuanzia mwaka huu vyuo vyote vinavyofundisha masomo ya Udaktari, Uuguzi, Ufamasia na Kada nyingine za afya waweke mtaala kwenye courses zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie jukwaa hili la kwako, kuwaagiza watu wote wanaoendesha vyuo vinavyotoa taaluma mbalimbali za kwenye sekta ya afya, kufuata mtaala ambao tayari umeandaliwa na Wizara yetu na waanze kuutumia kwenye masomo yanayoanza mwaka huu. Kwa hiyo, mtaala tunao tayari na nimeshaagiza sasa wautumie kufundishia.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru.
Kwa kuwa akina mama wengi wajawazito hususani vijijini wamekuwa wakipoteza maisha wakati wa kujifungua kwa sababu ya kukosa huduma ya kupangiwa kufanyiwa operation kabla ya siku ya kujifungua, hii imekuwa ikitokana na kwamba akina mama hawa hawapati elimu pale wanapokuwa wanakwenda katika vituo vya afya kwa ajili ya kliniki, hawaambiwi kwamba inawezekana kama mtu anakuwa na matatizo basi afanyiwe operation ya kupanga. Serikali imekuwa ikisisitiza operation za dharura, na hata katika majibu ya Waziri, amesisitiza sana katika huduma za vituo vya afya kutoa upasuaji wa dharura.
Je, Serikali haioni umuhimu sasa wa kutoa mwongozo katika vituo vya afya kwamba wanapotoa elimu kwa akina mama wajawazito wawaelimishe juu ya elimu ya kupata upasuaji wa kupanga ili kuokoa maisha ya mama na mtoto?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante.
Kwanza, napenda yeye mwenyewe pamoja na Wabunge wote wafahamu kuwa suala la kupunguza vifo vya wanawake wajawazito wakati wa kipindi cha uzazi ni suala systemic, hakuna mkakati mmoja unaoweza kulipatia ufumbuzi. Nikisema ni suala la kimfumo ninamaanisha kwamba ni lazima mfumo mzima uweze kufanya kazi ndipo tuweze kushusha vifo vya akina mama wajawazito katika kipindi cha kujifungua. Kwa maana hiyo ni rai yangu kwamba sisi Waheshimiwa Wabunge kwenye Halmashauri zetu tushiriki kwenye vikao vya kufanya maamuzi ili tuweke kipaumbele kwenye kujenga vyumba vya upasuaji, maabara, na Serikali tutatimiza wajibu wetu wa kupeleka watumishi wenye ujuzi wa kutoa huduma ambazo zitawezesha vituo vyetu vya afya nchini viweze kutoa huduma za upasuaji wa kupanga kama anavyozungumza Mheshimiwa Kiteto.
Mheshimiwa Spika, kwamba elimu inatolewa ama haitolewi, elimu inatolewa kila siku kwa akina mama wote wanaofika kliniki, pia niwapongeze akina mama wote nchini kwa kuelewa umuhimu wa kuhudhuria kwenye kliniki za uzazi kipindi wanaposhika ujauzito kwa sababu kiwango cha mahudhurio kimeongezeka sana kutoka takribani asilimia 56 miaka kumi iliyopita mpaka kufikia kiwango cha asilimia 86 kwenye miaka ya karibuni. Hivyo ni kwamba uelewa sasa umeongezeka, akina mama wanadai huduma za kliniki ziwepo, sasa kazi ni kwetu kuzitoa huduma hizo.
Mheshimiwa Spika, napenda kulipa taarifa Bunge lako Tukufu kwamba Tanzania ina vituo vya afya vipatavyo 489 tu, katika hivyo ni 113 tu vinavyotoa huduma za upasuaji na hii ni changamoto ambayo ipo kwenye Halmashauri zenyewe kwamba zikamilishe katika vituo hivi 489 vianze kutoa huduma za upasuaji na ndiyo kazi ninayoifanya kila siku kwenye ziara zangu.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, juzi Mheshimiwa Waziri wa Afya na Naibu wake walijibu kuhusu suala hili la makundi maalum (akina mama wajawazito, watoto na wazee), walisema kwamba sasa wameiagiza Halmashauri zetu waorodheshe wazee ili wapatiwe kadi za bima ya afya. Naomba nifahamu kama Serikali ipo serious huo mwongozo umeshatolewa na TAMISEMI katika Halmashauri zetu ili Madiwani wapange fedha hizo za kuwalipia wazee bima ya afya katika bajeti inayofuata?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza mwongozo ulikwishatoka na Halmashauri tayari zimeanza kutekeleza mpango huo wa kuwakatia CHF wazee wote waliopo katika maeneo yao.
Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kuwaomba Wabunge wote washiriki kwenye vikao vya bajeti vya mwaka huu ili wasimamie suala hili, kwa sababu utekelezaji wake upo kwenye Halmashauri. Pesa za kuwakatia kadi za CHF wazee wa nchi yetu waliotumikia ujana wao kuletea maendeleo Taifa letu zipo kwenye own source, kwenye vyanzo vya ndani vya Halmashauri ambavyo sisi kama Wabunge ni Madiwani tushiriki kwenye vikao hivyo, tuweze kuwakatia kadi za CHF wazee wetu.
Mheshimiwa Spika, mwongozo ulikwishatoka na kuna baadhi ya Halmashauri zimeanza kutekeleza mfano mzuri ni Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama kwa rafiki yangu Mheshimiwa Allan Kiula, wao wanatekeleza na wazee wengi wamefaidika na mpango huu.
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa swali la msingi kipengele (b) linafanana kabisa na tatizo tulilonalo Mkoa wa Tabora. Mkoa wa Tabora tulipata mamilioni ya pesa tukajenga chuo cha nursing na theatre ya kisasa, mpaka sasa tumekamilisha kwa asilimia 90 sasa hivi tuna miaka minne bado asilimia 10 tu jengo lile na theatre ya kisasa vianze kufanya kazi.
Mheshimiwa Spika, nilikuja hapa Bungeni nikamuuliza Naibu Waziri Mheshimiwa Kigwangalla akaniambia ataleta wataalam na yeye atakuja na atalifuatilia kwa sababu ni kama milioni 40 na kidogo tu ndiyo zinasababisha lile jengo liharibike na lishindwe kufanya kazi na theatre ya kisasa ishindwe kufanya kazi.
Je, Mheshimiwa Naibu Waziri kwa mara ya pili leo, anawaeleza nini wananchi wa Mkoa wa Tabora kuhusu chuo chao nursing na theatre yao ya kisasa? Na atupe majibu ya ukweli.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante.
Mheshimiwa Spika, nimepokea concern yake nitafika pale Tabora wakati natoka kumzika mzee wetu Mzee Sitta, nitapita pale kukagua na kuona progress imekuwa ni nini kwa sababu tayari suala hili nilikwishaanza kulishughulikia na ninaamini kwamba lingekuwa limepatiwa ufumbuzi kufikia sasa. Kwa kuwa anasema bado naomba nitumie fursa hii ya kwenda mazishi ya Mzee Sitta kupita pale ili niweze kuona hali halisi.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi niulize swali moja dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, pamoja na maagizo mbalimbali na matamko mbalimbali yanayotolewa hapa Bungeni na hata nje ya Bunge na Serikali kuhusiana na kutoa huduma bure kwa makundi haya muhimu, bado tumeshuhudia akina mama wanaojifungua hospitali wanazuiliwa na vichanga vyao kwa sababu tu wameshindwa kulipa gharama za kujifungua.
Je, Serikali inasemaje kuhusiana na haya yanayofanywa na uongozi wa hospitali kama Muhimbili, hospitali kubwa kumzuia mwanamke ndani ya hospitali zaidi ya wiki kwa sababu ameshindwa kulipa huduma za kujifungua. Serikali haioni kwamba inakwenda kinyume na sera zake?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa kuna matukio ya baadhi ya vituo vya kutolea huduma nchini kukiuka utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Afya ya mwaka 2007. Nakiri kuwepo kwa mapungufu hayo, lakini tayari kwa kuwa tulipata taarifa tulikwisha kutoa maelekezo na hapa Bungeni katika Bunge lililopita nilieleza na kufafanua wazi kwamba Sera ya Afya inaelekeza wakina mama wajawazito wote na watoto wote chini ya miaka mitano watibiwe bure, pamoja na makundi mengine mabayo nilitaja kwenye jibu la msingi.
Mheshimiwa Spika, ninaagiza kwa mara nyingine tena, ninaagiza watoa huduma wote wa afya wa Serikali ama wenye mikataba na Serikali watoe huduma hizi bure kama Sera ya Afya inavyosema. Nikikuta ama nikipata taarifa kituo chochote kile cha kutolea huduma hakifuati misingi hii inayoagizwa na sera nitachukua hatua kali dhidi ya viongozi wa taasisi husika.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize maswali madogo ya nyongeza.
Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa kuwa ugonjwa huu ni wa kitaalam zaidi na kwa kuwa elimu yake haijatolewa kikamilifu; je, Serikali iko tayari kutoa elimu kwenye vituo vya afya, zahanati na Wilaya wanapohudhuria kliniki wakina mama. Kwa sababu waathirika wakubwa ni wakina mama, je, Serikali inasema nini? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili kwa kuwa ugonjwa huu dawa zake zina gharama sana, je, Serikali iko tayari kuzitoa dawa hizo bure ili akina mama na wananchi wote waweze kupata huduma hiyo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA,WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante.
Mheshimiwa Spika, kwanza kuhusu elimu Serikali tayari inatoa elimu kuhusiana na ugonjwa wa sicklecell na magonjwa mengine yote kwa kina mama kwenye kliniki ya uzazi pindi akina mama wanapokwenda kuhudhuria, aidha wao wenyewe kwa mahitaji yao mbalimbali ama watoto wao walio chini ya umri wa miaka mitano, kwa hiyo, elimu inatolewa.
Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa kwenye kutoa elimu ipo kwenye kutoa elimu kwa vijana ambao wanatarajia kushika mimba siku za usoni. Changamoto hii ni kwamba bado katika nchi yetu hatubajeti sana fedha kwa ajili ya kinga zaidi kwa kweli tunatumia fursa ya kliniki na watu wanaokwenda hospitalini ama fursa ya shule kutoa elimu ya afya kwa umma, kama tungepata fursa ya kibajeti ya kuweza kufanya hivyo tungeweza kufanya.
Sasa tunashirikiana na wadau mbalimbali kama Chama cha Kitaifa cha Sickle Cell ambacho kinatoa elimu nchi nzima kuhusiana na ugonjwa huu, pia kuna taasisi ya utafiti iko pale Muhimbili nayo inatoa elimu kwa umma nchi nzima kuhusiana na ugonjwa huu. Kwa vijana ambao wanatarajia kwenda kujifungua ama wanapata mwenza ni vema wakapima kama wao ni carriers wa sickle cell ama laa. Kwa sababu carrier wa sickle cell akiona na carrier wa sickle cell wakashika mimba maana yake mtoto ana hatari ya asilimia zaidi ya 25 ya kupatwa na ugonjwa huu kama homozygous yaani kuwa na sickle cell ambayo imekomaa.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusiana na gharama za matibabu ya sickle cell hapa nchini, ugonjwa wa sickle cell napenda kumpa taarifa yeye, Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwa ujumla kwamba ni miongoni mwa magonjwa ambayo kwa mujibu wa Sera ya Afya ya Taifa ya mwaka 2007 ugonjwa wa sickle cell unatibiwa bure. Tiba ya sickle cell ni bure kwenye vituo vyote vya kutolea huduma za afya, sasa hivi kuna taasisi imetufuata inataka kutekeleza huo mradi wa kutoa elimu kwa umma nchi nzima ili kuwa-screen watu wote wajue hali zao kuhusiana na sickle cell kama wao ni carrier ama siyo carriers.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa chuo kile hakikukidhi haja ya kukikarabati na kwa kuwa katika majibu ya msingi yamesema kwamba eneo la chuo lilikuwa dogo. Je, Serikali haioni haja ya kujenga chuo kipya kwa sababu Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ina maeneo mengi ambayo yangeweza kujengwa chuo hicho? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ina upungufu mkubwa sana wa wafanyakazi katika Idara ya Afya kwa zaidi ya 70%. Ni kwa nini sasa Serikali isitoe upendeleo maalum kwa ajili ya Wilaya ya Tunduru na kwa vijana wa Tunduru ili waweze kuhudhuria mafunzo hayo katika vyuo ambavyo vimefufuliwa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inayo haja ya kujenga vyuo vipya kwa ajili ya kutoa mafunzo ya watumishi kwenye sekta ya afya, si tu kwa Tunduru lakini ni kwa nchi nzima. Bahati mbaya sana Mpango wa MCH Aider Training ulipoanzishwa mwaka 1973 ulilenga kuzalisha wataalam wa kutoa huduma za uzazi kwa akinamama vijijini kwenye zahanati ambazo zilikuwa zinaanzishwa kwenye mpango ule kutokana na Azimio la Alma-Ata miaka hiyo na Azimio la Afya kwa Wote enzi za miaka ya 70.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango ule umebadilika na hatuwezi kujenga tena chuo kwenye kila mkoa kwa sababu mpango wa kujenga Vyuo vya MCH Serikali iliazimia kujenga chuo kwenye kila mkoa ili kuwazalisha hawa MCH Aider kwa kuwapa kozi ya mwaka mmoja na nusu kwa haraka ili tuwapate kwa wingi zaidi waweze kuwahi kwenda kuokoa maisha ya akinamama wajawazito na watoto. Mpango ule haupo tena na kwa maana hiyo vyuo vya afya sasa hivi haviwezi kuwa ni vyuo vya afya kwa kila mkoa bali vinakuwa ni vyuo vya afya vya kitaifa na utaratibu sasa hivi tunashirikisha pia sekta binafsi ambao nao wanaanzisha vyuo kwa ajili ya kutoa mafunzo ya taaluma mbalimbali za kwenye sekta ya afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ni kwamba Tunduru wapate watumishi kwenye sekta ya afya, hili ni katika mipango ya Serikali ambayo ni endelevu. Kadri ambavyo tutapewa vibali vya kuajiri watumishi kwenye sekta hii ndivyo ambavyo tutaendelea kuajiri watumishi wapya na kuwatawanya si Tunduru peke yake bali ni kwenye wilaya zote hapa nchini.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Mbali na changamoto ambayo inakikabili Chuo cha Maendeleo ya Jamii - Kisangwa kuhusiana na kutopata fedha za uendeshaji, karakana na kadhalika lakini chuo hicho pia hakina gari. Hivi tunavyozungumza aliyekuwa Mkuu wa Chuo alijiuzia VX kwa Sh. 600,000/= na kufanya Mkuu wa Chuo wa sasa hivi asiwe na gari na kusababisha shughuli za chuo zisiende. Je, Serikali iko tayari kushughulikia ufisadi huu kwa sababu hakuna VX inayouzwa Sh. 600,000/= na kupeleka gari ili chuo hicho kiendeshe shughuli zake vizuri?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa swali kutoka kwa rafiki yangu Mheshimiwa Ester Amos Bulaya kuhusu kile anachopenda kukiita ufisadi. Majibu ya Serikali ni kwamba kwenye kuuza mali za umma ambazo zimemaliza muda wake na ama zimekuwa classified kama ni dilapidated ama mali zilizochoka unajulikana na umeandikwa. Kwa hivyo, kama Mheshimiwa Mbunge ana ushahidi kwamba utaratibu huu ambao umeandikwa kwenye sheria mbalimbali za kuuza mali za Serikali zilizochakaa haukufuatwa, naomba anikabidhi nyaraka alizonazo ili niweze kufuatilia na kuchukua hatua kwa mujibu wa sheria za nchi yetu.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa sasa wanafunzi wa vyuo vikuu wamekuwa wengi ukizingatia Chuo hiki cha Maendeleo ya Jamii Tengeru kimeanza kujaa. Je, Serikali ina mpango gani wa kupandisha vyuo vidogo vya diploma kama vile vya Monduli CDTI ili kuwa university kuweza kuwa-accommodate vijana waweze kusoma kwa wingi maana elimu inayotolewa na vyuo hivi ni nzuri sana kwa ajili ya Taifa letu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza Serikali haina utaratibu wa kuendelea kuvipandisha vyuo vya taaluma za kati kuwa vyuo vya kutoa degree kwa sababu Serikali ya Awamu ya Tano haiamini kwamba inahitaji watu wengi zaidi wenye degree kwenye soko la ajira, hapana! Serikali ya Awamu ya Tano inahitaji watu wengi zaidi wenye ujuzi kwa ajili ya ku-support uchumi wa viwanda na maendeleo ya kilimo na maendeleo ya biashara na ujasiriamali vijijini. Kwa hivyo, tutaendelea kuvijengea uwezo vyuo vyetu vya CDTI nchi nzima ili viendelee kutoa kozi kwenye ngazi hii ya wanataaluma na watu wenye ujuzi wa kati ili ku-support uchumi wa viwanda ambao tunaujenga kwa sasa.
MHE. USSI SALUM PONDEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Afya, naomba kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka nyuma kulikuwa kuna utaratibu wa Wizara zetu mbili hizi kukutana na kubadilishana uzoefu na vikao hivyo vilivyokuwa vinafanyika vilikuwa vina tija ndani yake ambavyo vilipelekea Madaktari Bingwa kutoka Muhimbili kuja Zanzibar na kutoa ushirikiano mkubwa. Vikao hivyo sasa hivi havifanyiki kwa muda mrefu kidogo. Je, Serikali ina kauli gani kuhusu vikao hivyo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba Serikali ina mpango gani na vikao hivyo? Vikao hivyo havijawahi kufutwa na havitofutwa kwa sababu Wizara hizi mbili (Wizara ya Afya ya Jamhuri ya Muungano na Wizara ya Afya ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar) zimekuwa na utamaduni huo na zinaona utamaduni huo ni mzuri na zitauendeleza. Hivyo, tutaendelea kuvihuisha ili viwe active zaidi kuliko ilivyokuwa katika mwaka huu mmoja wa uchaguzi uliopita. Lakini kuanzia mwezi Januari tayari tumekwisha kufanya kikao kimoja, naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Ussi.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante kwa kunipa swali kwenye Wizara ya Afya. Suala linalotokea Hospitali ya Mnazi Mmoja ni sawasawa kabisa na masuala yanayotokea katika Hospitali ya Rufaa ya Ndanda, Mkoa wa Mtwara. Mheshimiwa Waziri atakubaliana na mimi alipotembelea alitoa ahadi ya wafanyakazi wasiopungua 85; hivi ninavyoongea sasa hivi hospitali ya Rufaa ya Ndanda inakaribia kukosa hadhi ya kuitwa Rufaa kwa sababu kuna Daktari Bingwa mmoja tu. Je, Wizara yake ina mpango gani wa kuwawezesha watu hawa ili waendelee kutoa huduma kwa sababu ni hospitali ambayo ina vifaa vingi lakini inakosa wataalam wa kuvitumia?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba mpango tulionao ni kusubiri kibali kutoka kwa wenzetu wa utumishi kitoke, kitakapotoka tutaajiri Madaktari Bingwa kwa kiasi ambacho tutakuwa tumekasimiwa na kuwatawanya kwenye hospitali zote za Rufaa za Mikoa nchini ikiwemo Hospitali ya Ndanda.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Changamoto za mahospitalini zimekuwa nyingi na moja kati ya kero kubwa ambayo wananchi wanaipigia kelele ni kile kitendo ambacho mwananchi akiuguza mgonjwa wake na hatimaye akapoteza maisha haruhusiwi kuchukua mwili wa marehemu mpaka alipe gharama za matibabu ambazo kimsingi hazikumsaidia mgonjwa wake mpaka amefariki dunia. Kitendo hiki kinatengeneza taswira mbaya kwa wananchi kuonesha kwamba Serikali haijali utu na haithamini utu wa wananchi wake.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba endapo mwananchi atafiwa na mgojwa wake lile deni la matibabu asamehewe ili familia ijikite tu katika kushughulikia suala la mazishi?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba kwanza nakanusha kwamba Serikali haithamini utu wa Watanzania, hapana Serikali ina thamini sana utu wa Watanzania wote na ndio maana ikaweka utaratibu mzuri sana wa kutoa huduma za afya kwa watu wote hata wasiojiweza. Tanzania ni miongoni mwa nchi chache sana ambazo zinawapa usawa wa huduma tena bure kwa kuwahudumia takribani asilimia 67 ya wagonjwa wote hapa nchini bure bila gharama yoyote ile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa wale wachache ambao wanatengeneza hiyo asilimia 33 ya wanaochangia huduma za afya, kama itajitokeza kwa bahati mbaya baada ya kuhudumiwa akafariki halafu Sheikh Mtolea unasema sasa pale ndio utu wake unaanza, sio sahihi. Utu wa Mtanzania upo akiwa anaumwa, akiwa anahudumiwa kwenye hospitali na hata ikatokea bahati mbaya umauti ukamkuta utu uko pale pale. Lakini gharama za mtu ambaye amekwishahudumiwa iwe alipona ama kwa bahati mbaya alipoteza maisha; zipo pale pale ni lazima ziwe compensated na Serikali haiwezi kuziondoa.
MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Kwako Mheshimiwa Naibu Waziri, pamoja na majibu hayo mazuri pia nikupongeze umekuwa champion mzuri wa vijana, watoto na wanawake na unatambua kuwa wanawake wengi hususani Mkoa wa Iringa wanakiu kubwa ya kujitafutia maendeleo ya kwao pamoja na watoto wao. Na kikwazo kikubwa kimekuwa upatikanaji wa hii mitaji na mikopo yenye riba nafuu. Pamoja na jitihada za Serikali za kufungua hivi vituo viwili pale Mkoa wa Iringa na kama ulivyokiri huu mchakato wa kufungua dirisha pale MUCOB umechukua muda mrefu, sasa ningeomba pia utupe kipaumbele na time frame ni lini sasa pale MUCOB tutegemee kituo hiki ili hawa akinamama waepukane nah ii adha ya kupata mitaji yao? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, namshukuru Mheshimiwa Rose Tweve kwanza kwa kunipa compliment, mara chache sana Wabunge huwa wanawapongeza Serikali wanapofanya vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, time frame ni mpaka tutakapopata fedha kwa ajili ya kutunisha mtaji wa benki yetu. Lakini jambo la faraja ni kwamba kwa ahadi niliyoitoa hapa hapa Bungeni kwake yeye mwenyewe na kwa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwamba tuna-cosider kufungua dirisha pale MUCOB bado iko pale pale na ndio maana tumeiingiza kwenye mpango mkakati wetu.
MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.kwa kuwa ni miaka mingi sasa kila tunapoulizia kuhusiana na suala hili la Benki ya Wanawake kuanzishwa Zanzibar, mimi mwenyewe nimeulizia mara nne mpaka leo tawi hili halijafunguliwa kule Zanzibar. Na kuna mara moja niliulizia Mheshimiwa Waziri Ummy alinijibu kwamba ilitakiwa Serikali ya Zanzibar ichangie shilingi milioni 10. Nataka niulize ile shilingi milioni 10 ishalipwa ili hii benki ianzishwe au kama haitolipa hiyo shilingi milioni 10 ndio basi wanawake wa Zanzibar hatutopata benki hii? Mchakato wake ukoje?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante! Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Faida kwa kuuliza swali hili mara nyingi sana. Nina uhakika ndio maana wanawake wa Zanzibar wameendelea kumchagua kuja kuwawakilisha hapa Bungeni kwa sababu amekuwa balozi wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jibu letu ni kwamba shilingi milioni 10 bado haijapatikana lakini azma yetu ya kufungua tawi Zanzibar iko pale pale na Mheshimiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan amejitolea kutupa eneo kwa ajili kufungulia tawi hilo la benki yetu pale Zanzibar; tutaendelea kufuatilia kwa ukaribu. Na nitakapofanya ziara kwa ajili ya kufuatilia tumekwama wapi kwa ajili ya tawi hili la Zanzibar nitamshirikisha Mheshimiwa Faida.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru
sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kujibu maswali hayo. Sasa nina maswali
mawili.
Kwa kuwa, MSD imetengewa fedha shilingi bilioni 251 kwa ajili ya kununua
madawa, kwa kuwa kuna upungufu mkubwa sana wa madawa katika hospitali
zetu wagonjwa wakienda hospitalini wanaandikiwa vyeti na Madaktari
wanawaambiwa mkanunue dawa maduka binafsi. Je, kwa nini hizo fedha bilioni
251 zisipelekwe moja kwa moja MSD badala ya kukaa Hazina na wanapelekewa
kidogo kidogo?
Swali la pili, kwa kuwa, katika Jimbo langu la Mpwapwa kuna Vituo vya
Afya, vya Mima, Mbori, Berege, Mkanana pamoja na Zahanati za Chamanda,
Igoji Kusini, Kibojane Lupeta, Makutupa, Majami, Nana, Mgoma havijakamilika
hadi sasa na ujenzi huu sasa umechukua zaidi ya miaka kumi. Je, Serikali ina
maelezo gani kwa wanachi wa vijiji hivyo, kwa sababu wananchi wa vijiji hivyo
hufuata tiba zaidi ya kilomita 15?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA
WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa fursa hii. Swali lake la kwanza
kuhusu kwa nini Serikali isipeleke pesa moja kwa moja kutoka Hazina kwenda
MSD moja kwa moja tayari nilikwishatoa maelezo ya msingi, kwenye jibu la
msingi; kwamba Idara za Serikali zinazopewa vifungu ni Serikali Kuu tu na Ofisi za
Wakuu wa Mikoa na pamoja na Wizara. Kwa hivyo, MSD hawezi kupewa pesa
moja kwa moja kutoka Hazina ambapo ni Serikali Kuu na bila kupitia Wizara ya
Afya, kwenye kifungu kile ambacho sasa tumepewa kinaitwa kifungu 2005 chini
ya Mfamasia Mkuu wa Serikali. Kwa hivyo, utaratibu huo ni lazima uzingatiwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie nafasi hii pia kukanusha kauli
yake ya kwanza aliyoisema kwamba kuna upungufu mkubwa wa dawa,
hapana, hakuna upungufu mkubwa wa dawa nchini. Kwa taarifa tulizonazo sisi
na ukweli ni kwamba upatikanaji wa dawa (Drug availability) kwa sasa ni wa
kiwango cha asilimia 84 kwa mujibu wa taarifa za wiki iliyopita.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili lina maelezo yake sipendi kupoteza muda
wako, naomba nisiyatoe hapa lakini huo ndiyo ukweli. Serikali katika Awamu hii
ya Tano imewekeza sana kwenye dawa na ndiyo maana tumepewa bilioni 251.5
ukilinganisha na bilioni 31 kwenye mwaka wa fedha kabla ya huu. Bilioni hizo
mpaka sasa tunavyozungumza kufikia Desemba tulikuwa tumeshapokea bilioni
84 kutoka Hazina kwa ajili ya manunuzi ya dawa. Kwa hivyo upatikanaji wa dawa
ni wa kutosha pengine hizo anazozisema Mheshimiwa George Malima Lubeleje ni
hadithi za zamani kidogo anapaswa kufanya utafiti wa kina.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kuhusu kukamilisha zahanati na
vituo vya afya kwenye jimbo lake, naomba nitoe rai kwake yeye mwenyewe,
Halmshauri yake pamoja na kwa Wabunge wengine wote na Halmashauri zote
nchini kuzingatia ukweli kwamba, ukamilishaji wa majengo ya zahanati na vituo
vya afya inapaswa kuwa kipaumbele cha Halmashauri husika. Kwa sababu miradi hii ya maendeleo kama ambavyo imewekwa kwenye Ilani ya Uchaguzi
kwamba tutajenga zahanati kila kijiji, kituo cha afya, kila kata hatuwezi kusema
sasa tunapewa pesa na Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli ili tujenge hapana. Sisi
sote tuna wajibu wa kutimiza.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima katika Halmashauri zetu tuweke
kipaumbele kwenye kukamilisha miradi ya zahanati ambayo imeanzishwa na
wananchi kwa kujitoa sana kwenye Halmashauri tukakamilishe zahanati hizo ili
ziweze kuanza kufanya kazi. Wala tusitarajie kwamba sasa Wizara ya Afya
itatuletea pesa ili tukamilishe. Pesa ile inapaswa kutoka kwenye ownsources za
Halmashauri na maamuzi ya kufanya hivyo wanayo Waheshimiwa Wabunge na
Waheshimiwa Madiwani kwenye Halmashauri zao.
MHE. HALIMA ALI MOHAMMED: Mheshimiwa Naibu Spika, asante sana.
Kwa kuwa, kwa mujibu wa taarifa ya CAG ya mwaka ulioshia Juni 2015,
inaonesha kwamba kuna bohari ambazo hazina viwango. Sasa, je, Serikali
inasema nini kuhusiana na hatari ya afya za wananchi wetu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA
WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwanza naomba nikanushe vikali
sana kwamba kuna bohari za dawa zisizo na viwango. Kwa sababu, hiyo ni ripoti
ya CAG, sasa hii ni taarifa ya Serikali. Kwa hivyo naongea kama Serikali kwa
mamlaka kamili niliyopewa. Kwamba bohari tulizonazo pale MSD ni bohari zenye
viwango vya hali ya juu. Viwango hivi vimethibitishwa kwa ISO standards na
standards hizi zinakaguliwa kila baada ya miaka mitano ili kuthibitisha viability
yake na kwa msingi huo hatuwezi kutunza dawa kwenye bohari zisizo na viwango
kwa sababu zitaharibika.
Mheshimiwa Naibu Spika, ifahamike kwamba dawa ni high value items,
hatuwezi kuzitunza hovyo hovyo kwa sababu tunazinunua kwa gharama kubwa
na ndio maana kuanzia utunzaji kwenda kwenye usambazaji mpaka kwenye
storage kwenye kituo cha afya kijijini kuna mnyororo uliokamilika unaozingatia
viwango vya ubora.


WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO:
Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake lakini
pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, niseme tumepokea swali na
tutalifanyia kazi na tutaleta majibu Bungeni.
MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Mheshimiwa Naibu Waziri amenijibu majibu mazuri sana na ndiyo kawaida yake. Pamoja na majibu mazuri, naomba kuuliza swali moja na nikipata baadaye hata la pili naweza kuongezea. Kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba Wizara ya Afya ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itashauriana na Wizara ya Afya ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ili kuona uwezekano wa kuwapatia posho wataalam hawa wanaotoka Chuo Kikuu cha SUZA ambao wanafanya kazi za vitendo katika maeneo mbalimbali ya hapa Tanzania Bara, nakubali atashauriana, lakini anaweza akasema kwamba atashauriana, lakini tukasubiri mwaka mzima umeisha; naomba kujua, ni lini hasa ushauri huu utaanza, natamani uanze hata leo.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri huyu ameonesha nia safi ya kusaidia suala hili na kwamba amesema atashauriana na Waziri mwenzake wa Zanzibar, naomba kushauri, akishauriana naye aweze kumweleza sheria kama hii ya huku iwekwe au mwongozo ili kuwaondoshea madhila wataalam wetu ambao wanafanya kazi kiuzalendo.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza napenda kumshukuru Mheshimiwa Faida Mohammed Bakar kwa kunipiga fagio zito kama alilonipa hapa siku ya leo.
Mheshimiwa Spika, kwamba ni lini tutashauriana na wenzetu wa upande wa Zanzibar, utaratibu tulionao kila baada ya miezi mitatu Wizara hizi mbili huwa zinakutana, kikao cha kwanza cha mwaka huu kimefanyika mwezi Januari na cha pili kitafanyika mwezi wa tatu kwa ajili ya mashauriano ya mambo mbalimbali na hili sasa litakuwa ajenda ya kikao cha Mawaziri kitakachofanyika mwezi wa Tatu.
Mheshimiwa Spika, ili kumtoa wasiwasi, na kuwatoa wasiwasi wahitimu wote wa kozi ya Environmental Health Sciences wanaotokea Zanzibar ambao wanapenda kufanya internship huku Tanzania Bara, ni kwamba kuna utaratibu ambao sio rasmi sana umewekwa ambao umekuwa ukiwasaidia kwa muda mrefu wahitimu wote ambao wanahitaji kufanya internship Tanzania Bara ambao wanaotokea upande wa Zanzibar.
Mheshimiwa Spika, kwa sababu utaratibu huo umekuwepo na haukuwa rasmi ndiyo maana leo hii ninavyoongea hapa Wizara ya Kazi ya Jamhuri ya Muungano imeita wadau kwa ajili ya kutengeneza kitu kinachoitwa National Framework on Internship Programme ambapo ndani yake utawekwa utaratibu wa namna ya kuwahudumia wanafunzi wanaotoka Zanzibar ambao wanataka kufanya internship huku Tanzania Bara.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Nataka kujibu sehemu ya pili ya swali la Mheshimiwa Faida kwamba ni kwa nini sasa na yeye anatushauri na sisi tukashauri Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar walifanyie kazi suala hili. Tunao Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi ndani ya Bunge hili, kwa hiyo, napenda kuwashauri walibebe suala hili walieleze pia katika Baraza la Wawakilishi ili liweze kupata nguvu, kwa hiyo litatoka katika Wizara ya Afya ya Jamhuri ya Muungano lakini pia litoke kwenye Baraza la Wawakilishi la Zanzibar mwisho wa siku watoto wetu wataweza kufanya internship bila shida.
MHE. LEONIDAS T. GAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kwa mheshimiwa Waziri kama ifuatavyo:- Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi sote tunajua kwamba tutakuwa wazee, hawa wazee hivi sasa wanateseka sana, hali zao za maisha ni ngumu, uwezo wao wa kupata huduma za dawa ni mdogo. Sasa nilitaka nijue katika mpango wetu tumepanga mpango wa kuhakikisha wazee hawa wanatibiwa bure. Je, ni lini Serikali itatoa uamuzi wa kuwatibu bure wazee ili angalau waondokane na matatizo waliyonayo? (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili, tulizungumza sana juu ya suala la wazee kupata pensheni ili ziwawezeshe kupata huduma muhimu. Mpango huu tumeuzungumza lakini hatujapata mwelekeo wa nini tunafanya kwa wazee ili waweze kupata pensheni zao. Sasa naomba nipate uhakika Serikali ina mpango gani na imejipangaje, lini tutaanza utaratibu wa kuwapa pensheni wazee ili waweze kujipatia huduma muhimu kama za matibabu, elimu na kadhalika?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la kwanza, kwamba ni lini Serikali itaanza kutoa huduma bure za afya kwa wazee, jibu letu ni rahisi tu kwamba tayari Sera ya Taifa ya Afya ya mwaka 2007 inatoa msamaha wa matibabu kwa wazee wote wenye umri wa kuanzia miaka 60 na kuendelea wasiojiweza; napigia mstari neno wasiojiweza. Kwa hivyo, taratibu za kuwahudumia wazee wasiojiweza zipo na zimewekwa wazi na Sera ya Afya ya Taifa lakini pia na miongozo mbalimbali ya kutoa huduma za afya nchini. Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakoelekea mkakati wetu kama Serikali ni kutafuta namna bora zaidi ya kuzihamasisha na kuziwezesha Halmashauri zetu nchini kuwakatia kadi za CHF wazee wote ambao wanakidhi vigezo hivyo. Tayari Waziri wa Afya mwezi wa 12 alitoa agizo hilo kwenye Halmashauri zote nchini na kuna baadhi ya Halmashauri zimeanza utekelezaji wa agizo hilo na ninaamini wazee wanafaidika na mpango huo. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la pensheni kwa wazee; Serikali inatambua mchango mkubwa uliotolewa na wazee wetu kwenye ujenzi wa Taifa hili, na ndiyo maana tunaweka mikakati mbalimbali ya kuwahudumia wazee wetu hususani katika kipindi ambapo wame-retire na hawawezi kuendelea kufanya kazi za nguvu za kuzalisha na kukuza kipato chao. Na kwa msingi huo ndiyo maana tumeanza mchakato wa kutengeneza mkakati ambao utatuwezesha kuwahudumia wazee. Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya kwanza tuliyoifanya ni kutazama takwimu za sensa na kuona kama tutakuwa na uwezo wa kuwa hudumia na kwamba tutakuwa tunabeba mzigo kiasi gani wa wazee ili tuweze kufikiria kama ni kitu tunachoweza kukitekeleza na pengine kukiingiza kwenye bajeti. Kwa sasa kamati ambayo iko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge inaendelea kutekeleza utaratibu mbalimbali wa kupitia takwimu hizo na kufanya tathmini na baadaye mchakato wa ndani ya Serikali utakapokamilika tutafanya utekelezaji wa mpango huo. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nitumie nafasi hii kuwahamasisha Waheshimiwa Wabunge wote tuliopo hapa na wananchi wote wakazi wa Dodoma kushiriki kwenye mazoezi ambayo yataongozwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu kesho asubuhi saa 12 kuanzia kwenye viwanja vya Bunge tutatembea kilometa 5.2 tukiongozwa na Waziri Mkuu wetu mpaka kwenye viwanja vya Jamhuri. Hii itatusaidia kuondokana na changamoto za kutumia sana dawa za shinikizo la damu, lakini pia dawa za kisukari kwa sababu tutakuwa na afya bora. Nakushukuru.
MHE. BHAGWANJI MAGANLAL MEISURIA: Mheshimiwa Spika, nashukuru Mheshimiwa Naibu Waziri amenijibu vizuri lakini nina maswali ya nyongeza. Ni kweli kabisa aliyosema, nakubali wazazi wote wapate haki kamili ya kumlea mtoto.
Ikiwa mtoto yupo kwa mama aruhusiwe kwenda na kwa baba. Hata hivyo, katika Tanzania yetu wananchi wengi hawampi baba haki ya kumlea mtoto au hata kumwona, je, Serikali inasemaje kuhusiana na suala hili? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili. Huyu mtoto
kuanzia miaka mitatu hadi saba yupo kwa mama, ikiwa mtoto huyo amefikisha miaka saba, je, baba anayo haki ya moja kwa moja kumlea, kumsomesha na kumuangalia kiafya? Kwa sababu watoto wengi wa Tanzania hawapati
nafasi ya kulelewa na baba. Kwa hiyo, baba apate nafasi ya kulea, baada ya miaka saba apewe mtoto.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Yaani kumtia mwanamke mimba haitoshi kukufanya uitwe baba. Ili kuwa baba kamili, pindi unapompa mimba mwanamke unapaswa kwanza kuitunza
mimba yenyewe, lakini baada ya hapo kumtunza mtoto baada ya kuzaliwa, muwe mnaishi pamoja ama hamuishi pamoja na huyo mwanamke. Hilo ni jukumu la kwanza unapokuwa mwanaume na imetokea umempa mimba mwanamke. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama kuna mgogoro wowote ule unaoweza kutokea katika mchakato huu kuna taratibu za kufuatwa. Moja ya taratibu ni za kimila ambapo yanaweza yakatokea mashauriano ya kimila kwenye jamii kati ya upande wa baba na upande wa mama na
wakaelewana kimila na kuna gharama za kutoa. Kwa mfano, kwa Wasukuma kuna ngwegwe na nafahamu kwenye makabila mengine pia kuna taratibu za kufuata. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kama ikishindikana kimila ndiyo unafuata huo mchakato wa kisheria niliousema ambapo utapaswa kwanza kumpa haki mama kumlea mtoto mpaka miaka saba ifike na katika kipindi hiki cha miaka saba unapaswa kuwa umemtunza yule mama. Pale mwanzoni
kama hukumuoa huyo mwanamke unapaswa
ukajitambulishe rasmi kwamba wewe unahusika na ile mimba, siyo umeikataa mimba halafu mtoto akizaliwa anafanana na wewe unasema mtoto ni wa kwako, hapana! (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwanza kwa mujibu wa sheria unapaswa ama ufuate taratibu za kimila ujitambulishe kwamba wewe ndiye uliyetia mimba, uilee mimba na mwisho wa siku umlee mtoto au kwa taratibu za kisheria ujitambulishe mahakamani kwamba wewe ndiye umetia mimba na utailea. Sasa ikifika ile miaka saba una haki ya kudai mtoto. Nadhani Mheshimiwa Meisuria amenielewa.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, nataka kuongezea hiyo sehemu ya pili.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto Na.21 ya mwaka 2009, presumption ni kwamba mtoto anatakiwa akae na mama in the best interest of the child lakini akifika miaka saba sheria inasema in the opinion of the court anaweza akakaa na mzazi yeyote pale mahakama
itakapojiridhisha kwamba mtoto huyu atapata matunzo na malezi mazuri.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimtoe wasiwasi
Mheshimiwa Bhagwanji kwamba kama mtoto amefikisha miaka saba siyo lazima akae na mama, mahakama itapima na kuona in the best interest of the child mtoto huyu atapata malezi mazuri wapi, kwa baba au kwa mama.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA: Mheshimiwa Spika,
ahsante sana. Nami naomba nimuulize Naibu Waziri swali
dogo la nyongeza. Kwa kuwa ongezeko la watoto wa
mitaani linachangiwa na akinababa kukataa mimba na
kukataa familia zao. Je, Serikali inaweza kusema mpaka sasa
hivi ni akinababa wangapi wameshatiwa hatiani na
kufunguliwa mashtaka ili kutunza familia zao?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII,
JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza hatuna takwimu sahihi za watu waliochukuliwa hatua kwa kukataa mimba. Hata hivyo, nimhakikishie tu kwamba tuko makini katika kufuatilia kesi za namna hiyo ili kuweza kuchukua hatua pindi inapojitokeza.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nami kwanza kabla ya yote niungane na Waheshimiwa Wabunge wote kwa kumtakia afya njema Mheshimiwa Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete pamoja na
familia yake kwa jinsi alivyotuongoza kipindi chake. Pamoja na hayo, naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.

MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Basi nitauliza swali moja la nyongeza lenye kifungu (a) na (b).
Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri na Waziri wake kwa kuwa makini wakati wa kujibu suala hili lakini kuna kadhia kama hii imetokea kwa baba kufariki na watoto kubaki na huyu mtu akaenda kulalamika Ustawi wa Jamii nao wakapendekeza kwamba
watoto hawa ikifika muda waende kwa babu yao na ukitazama chimbuko la hawa watoto ni babu. Leo kwa nini babu ananyimwa haki yake ya kuwasomesha watoto wale? La kushangaza, baadaye bibi huyo akakimbilia mahakamani
nayo ikaamua kuwa shule zikifungwa wakatembelee tu watoto asiweze kuwachukua. Haki ya mtoto iko wapi hapo katika vifungu ulivyotaja 21 na 7?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, Sheria ya Mtoto iko wazi katika kifungu cha 37 ambacho kinahusu custody of the child. Katika kifungu hicho utaratibu unawekwa kwamba pale mtoto anapokuwa amefika umri wa miaka saba utaratibu unabadilika badala ya kubaki tu kwamba atakuwa chini ya usimamizi wa mama yake sasa mahakama inaweza ikaamua mtoto ama aende kwa baba au kwa mama kwa kuzingatia mahali ambapo huyo mtoto atapata malezi bora.
Mheshimiwa Spika, lakini kama imetokea sasa mzazi ambaye ni baba amefariki, maana yake mzazi anayebaki automatically ni yule mmoja kwa sababu mtoto ni wa wazazi wawili. Kwa hiyo, kama mama yupo maana yake naturally tu mama anapata haki ya kumlea yule mtoto siyo tena kwa
babu mzaa baba, hapana! Kama mama yupo lakini baba amefariki haki inabaki kwa mama.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama inatokea
kwamba mama anaonekana hana uwezo wa kumlea yule mtoto ama mtoto hapati haki ama mtoto anafanyiwa vitendo vya ukatili kwa namna yoyote ile na wazazi na jamii ipo, basi hao wazazi kama babu wanaweza wakaenda mahakamani kwenda kushtaki na shauri hili likajadiliwa pale
na hatimaye mahakama itaamua kutafsiri kifungu hicho in the best interest of the child.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana; kwanza naomba nioneshe masikitiko yangu kwa kiwango cha juu kwa Waziri kijana kujibu majibu ambayo hayaendani na kasi ya Serikali kwa sasa hivi. Haya
mashirika ambayo ameyataja TRA, BOT, ANESCO, NHC na TPA mimi mwenyewe binafsi nilitembelea wakati nipo NHIF lakini ni tofauti ya anavyosema Waziri sasa hivi. Je, katika michakato ambayo imeshawahi kutokea nchini kwetu
mchakato mgumu ulikuwa wa kuhamia Dodoma, Rais alisema mwaka jana mwezi wa Saba lakini sasa hivi Mawaziri wote wamehamia Dodoma.
Swali la kwanza; je, ni nini kinashindikana mashirika haya ya umma kuhamia NHIF wakati ni kitendo cha muda mfupi tu?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ofisi yako ni
shahidi Wabunge tulipotoka mashirika ya private insurance kwenda NHIF tuliweza ku-save kiwango kikubwa cha pesa mpaka tukanunua madawati nchi nzima. Kumekuwepo na ubadhirifu mkubwa wa pesa za Serikali kwa haya mashirika ya umma through private health insurance. Je, Serikali
itakubaliana na mimi sasa hivi kufanya mchakato wa kuangalia kiwango gani cha pesa kinachopotea iwapo mashirika ya umma yataendelea kutumia private health insurance badala ya NHIF?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naweka sawa, mimi sio Naibu Waziri kijana, mimi nimeshavuka umri wa ujana mimi ni mtu mzima na yeye bado kijana mdogo wangu lakini mimi sio kijana, mimi ni Naibu
Waziri. Kumjibu ni kwamba, hakuna kinachoshindikana kwa mashirika kujiunga na Mfuko wa Bima ya Afya ya Taifa na kinachofanyika sasa hivi ndani ya Serikali ni mapatano baina ya shirika letu la NHIF na haya mashirika mengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, ambapo tunatarajia
watakapokubaliana kama ambavyo Katibu wa Bunge amekubaliana na Shirika letu la NHIF kuliingiza Bunge huko na haya mashirika mengine taratibu yataendelea kufanyiwa kazi kama ambavyo alikuwa akifanya yeye wakati ameajiriwa na NHIF. Aliendelea kuwashawishi kwa sababu
sio suala la kulazimishana. Yeye amekuwa akienda kule kuwashawishi miaka yote ambayo amekuwa akifanya kazi kule hakufanikiwa kuwa-convince wakajiunga na mfuko; leo hii anataka tu hii miezi miwili, mitatu tuwe tumeshawaconvince sisi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo pengine mfupa uliomshinda yeye anatarajia sisi tutauweza kwa haraka zaidi wakati yeye mwenyewe ulishamshinda. Kwa hiyo wataalam wetu, kama alivyokuwa yeye mtaalam wa NHIF – wanaendelea kupatana na haya mashirika taratibu
kuyashawishi yajiunge na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu yake ya pili; mpaka sasa hatujajua ni kiasi gani cha pesa ambacho pengine kinapotea kwa mashirika mbalimbali ya umma kuwa yamejiunga kwenye mifuko ya private health insurance na sio kujiunga katika Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya. Hata
hivyo, natoa rai kwa mashirika haya na Mawaziri ambao wanayasimamia mashirika haya kutoa maelekezo kwenye mashirika haya ili huu mchakato wa negotiations ambao unaendelea uweze kuongezwa kasi ili mashirika yote ya
Serikali hatimaye yajiunge na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya badala ya kuwa kwenye mifuko hiyo mingine.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nimshukuru sana Mheshimiwa Goodluck Mlinga, Mbunge wa Ulanga kwa maswali yake mazuri.
Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, nataka kuwathibitishia suala la mashirika ya umma kujiunga
na NHIF sio suala la hiari. Tayari kama Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wanatumia NHIF kwa hiyo hatuoni kisingizio kwa mashirika ya umma kutumia NHIF. Nimetoka kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha na yeye alipowasilisha mpango wa bajeti na mwongozo wa sera za matumizi, Serikali imetoa maelekezo tutumie huduma na bidhaa zinazozalishwa na Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tutakaa na
mashirika haya tuweze kuona, wengi tumeongea nao wana mikataba na mashirika haya ya bima binafsi kwa hiyo hatuwezi kukatisha lakini nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Mlinga, tutafanya kazi pamoja kuhakikisha mashirika yetu haya yote yanajiunga na bima ya afya NHIF. Nitoe wasiwasi, NHIF sasa hivi inakubalika katika hospitali kubwa zote, kama Wabunge wanatumia sioni ni sababu gani mtumishi wa TRA na BoT asitumie huduma
za NHIF. Mheshimiwa Mlinga, nakushukuru sana na tutafanya kazi pamoja kuhakikisha tunalitatua suala hili.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza. Hapo mwanzo Mfuko huu wa Bima ya Afya ulikuwa unatoa mikopo mbalimbali katika vituo vyetu vya afya, hospitali, kwa ajili ya ku-support matibabu kwa wateja wao, lakini tangu mwaka jana utaratibu huu wa kutoa mikopo katika hospitali zetu umekuwa sasa na urasimu kwa kupitia Hazina na tangu mwaka jana mwezi wa Tatu mikopo mingi imekwama Hazina. Naomba nifahamu, Serikali ina mpango gani
kurudisha utaratibu huu wa Mfuko wa Bima ya Afya katika Wizara husika ili hospitali zetu zipate mikopo ikiwemo Hospitali ya Mrara, Babati ambayo tumeomba mkopo tangu mwaka jana na hatujajibiwa? Naomba ufafanuzi.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Utaratibu wa mikopo ni kwamba ni lazima taasisi za Serikali zinapokopa ziwe zimepata kibali cha kutoka kwa Msajili wa Hazina (Treasury Registrar) na huo ni utaratibu wa
kawaida wa ndani ya Serikali. Kama ilikuwa ikifanyika hivyo huko nyuma maana yake taratibu zilikuwa haziko sawa lakini kwa mujibu wa circular ambayo ilitolewa na Msajili wa Hazina miezi takribani 24 iliyopita, utaratibu uliwekwa kwamba taasisi yoyote ile ya Serikali haitaruhusiwa kuchukua mkopo ama kutoa mkopo kwenye taasisi nyingine bila kuwa kuna kibali cha mwenye mali kwa maana ya Treasury Registrar ambaye anazishikilia mali zote za mashirika ya umma, kwa hiyo ni utaratibu wa kawaida wa kisheria ambao ni lazima ufuatwe.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Katika majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri amekiri kabisa kwamba tatizo hili la Kifua Kikuu ni kubwa sana na hasa
katika maeneo ya wachimbaji wa madini ikiwemo Geita. Ningependa kujua sasa kwamba Serikali ni lini itaweza kufanya utafiti wa kina hasa katika maeneo ya wachimbaji ili kubaini ukubwa wa tatizo hili katika maeneo haya na hatimaye kuweza kupatiwa ufumbuzi?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa
nchini Tanzania tatizo hili la kifua kikuu ni kubwa sana, katika takwimu za dunia inaonesha kwamba mwaka 2015 watu 160,000 waliweza kupata tatizo hili la kifua kikuu. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuwa na sera pamoja na mikakati ili kuweza kupambana kutokomeza ugonjwa huu wa kifua kikuu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza kwamba ni lini Serikali itafanya utafiti kwenye maeneo haya, naomba nimuahidi tu kwamba, Serikali itaendelea kutekeleza mikakati hii kama ambavyo imeweka
mpango wake wa bajeti wa kila mwaka na tutakapopata pesa mahususi kwa ajili ya tafiti mbalimbali, tutahakikisha tunatoa kipaumbele kwenye eneo hili la maeneo ya migodi kwenye magonjwa haya ya kifua kikuu pamoja na magonjwa ya silicosis.
Mheshimiwa Naibu Spika, sina tarehe mahususi
kwamba ni lini tunaweza tukafanya hivyo lakini dhamira yetu ni njema na kwamba tutakapopata pesa basi tutazielekeza kwenye tafiti kwenye maeneo haya ya migodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili kwamba kwa nini Serikali isilete sera kwa ajili ya Kifua Kikuu; naomba nimjulishe tu kwamba sera tunayo na infact mapitio ya sera yanatuelekeza sasa hivi ndani ya Serikali kutekeleza miradi
ya Kifua Kikuu, uchunguzi pamoja (case detection) mpaka kwenye ngazi ya jamii, kwenye ngazi ya kaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ufuatiliaji wa kesi mbalimbali za kifua kikuu kwa sera hii tuliyonayo sasa unafanyika mpaka kwenye ngazi ya community kwa maana ya kwamba tunakwenda mpaka kwenye kaya, kwenye household. Kwa hiyo sera tunayo na tunaendelea kuitekeleza na kwa kiasi kikubwa katika miaka ya karibuni maambukizi ya kifua kikuu yameendelea kupungua.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nimesimama kutoa msisitizo kwa swali la Mheshimia Lolesia Bukwimba, ni kweli tuna wagonjwa takribani 160,000 wa kifua kikuu nchini lakini changamoto yetu kubwa ni kuwafikia wagonjwa wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeweza kuwafikia
wagonjwa takribani 62,000 tu, kwa hiyo nitoe wito kwa Waheshimiwa Wabunge, tunapokwenda katika majimbo yetu tuwahamasishe wananchi kupima kifua kikuu, takribani wananchi 100,000 tunao katika majumba yetu, katika kaya zetu, katika shule zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo kubwa ambalo
tumelifanya, kila mama mjamzito na mtoto mwenye umri wa chini ya miaka mitano anayekwenda hospitali sasa hivi atapimwa kifua kikuu na watu ambao pia wana maambukizi
wa VVU. Kwa hiyo, nawaomba sana kifua kikuu kiwe ni agenda yenu ya kila siku mnapokuwa katika majimbo yenu. Mtu ambaye hajapata matibabu ana uwezo wa kuambukiza mpaka watu 20 kwa mwaka mmoja, tusipochukua hatua Kifua Kikuu kitakuwa ndicho kinachoongoza kuua kuliko Malaria au HIV/AIDS.
Mheshimiwa Naibu Spika, niliona nisimame ili
kuwahamasisha Waheshimiwa Wabunge kushiriki katika mapambano ya kifua kikuu.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kuniona. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, katika sheria hii na kwa mujibu wa watu wa TRA, magari ya ambulance yana-fall katika HS Code 87039010 ambayo kitaalamu kwenye kodi inakuwa zero rated yaani haina kodi isipokuwa inatakiwa kulipiwa kodi ya VAT. Sasa swali langu la kwanza, kwa kuwa kwa mwaka wa pili sasa mfufulizo Serikali haijaweza kutenga fedha za kununua magari ya wagonjwa, inaonaje Wizara ikaanzisha mchakato wa kubadilisha sheria kwa kuileta hapa Bungeni ili magari ya wagonjwa yaingie kwenye item no. 7 kusudi na yenyewe ya-enjoy msamaha wa kutolipa VAT? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Serikali
imekiri kwamba haitaweza kununua magari ya wagonjwa isipokuwa Halmshauri zenyewe zitafute fedha kwa ajili hiyo na Halmashauri nyingi hazijaweza kuwa na uwezo huo wa kununua hayo. Pia Waheshimiwa Wabunge wengi wanaomba misaada kutoka kwa watu mbalimbali jambo ambalo siyo guaranteed kwamba utapata gari. Je, Serikali iko tayari kwa wale Waheshimiwa Wabunge na Halmashauri ambazo zitapata magari ya misaada kuwalipia gharama za VAT?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza, mpaka sasa utaratibu ambao unatumika haujaleta usumbufu wowote ule kama Mbunge ama mwananchi yeyote yule mwenye nia ya kutaka kununua gari la wagonjwa atauelewa na kuufuata kwa kadiri ambavyo umewekwa. Sheria ya Kodi ya mwaka 2014 ambayo inasimamiwa na
wenzetu wa Wizara ya Fedha na Mipango imempa mamlaka Waziri mwenye dhamana ya afya kwa maana hiyo kwa sasa ni Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kutoa mapendekezo ya msamaha kwa Waziri mwenzake wa Fedha na Mipango kwa magari na vifaa mbalimbali ambavyo vimeainishwa kwenye Jedwali la Saba la sheria hiyo ninayoisema.
Mheshimiwa Spika, hakujawahi kuwa na utata/shida yoyote ile kama mtu atafahamu utaratibu huu na akatoa taarifa kwa Waziri wa Afya kwamba ana malengo ya kuagiza gari la wagonjwa ama vifaa mbalimbaliv ya hospitali na
Waziri wa Afya akiridhia basi atawasiliana na mwenzake Waziri wa Fedha na Mipango na mara nyingi kodi zote huwa zinakuwa waved (zinaondolewa). Kwa maana hiyo, hakuna haja ya kufanya mabadiliko yoyote ya kisheria.
Mheshimiwa Spika, lakini swali lake la pili la nyongeza kwamba Serikali ibadili utaratibu huu kwa sababu imeshindwa kuagiza ambulance, hapana. Kipaumbele cha kununua ambulance kwa kweli kinapaswa kutoka kwenye Halmashauri zenyewe husika na Halmashauri kama mamlaka za Serikali zinazojitegema, zinafahamu zaidi mahitaji yake na kipato chake. Halmashauri zinapaswa tu kuweka kipaumbele kwenye kununua magari ya wagonjwa na wakishirikiana na sisi hakuna kitakachoshindikana watapata magari hayo. Sisi kama Wizara ya Afya tunachokifanya kwa kuwa tuna-access na wadau mbalimbali wa maendeleo tumekuwa tukishirikiana nao kuwaomba watusaidie kununua
magari hayo ambayo mara kwa mara tumekuwa
tukiyatawanya kwenye Halmashauri mbalimbali nchini lakini sio jukumu letu la msingi kufanya hivyo.
MHE. RHODA E. KUNCHELA: Mheshimiwa Spika, nataka kuuliza swali kuhusiana na changamoto ya gari katika Hospitali ya Wilaya ya Mpanda. Hospitali hii imepandishwa hadhi kutoka kwenye Wilaya kwenda kwenye Mkoa, lakini
pia gari lililopo pale ni bovu na halikidhi haja ya Watanzania
waliopo katika Mkoa wa Katavi. Je, ni lini Serikali itaongeza
nguvu katika Halmashauri ili gari lingine lipatikane katika
Manispaa ya Mkoa wa Katavi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza Hospitali ya Mpanda haijapandishwa hadhi na kuwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ila kwa sasa inatumika tu kama Hospitali
ya Rufaa ya Mkoa lakini yenyewe bado ni Hospitali ya Wilaya ya Mpanda. Kwa sasa Mkoa wa Katavi unajenga Hospitali mpya ya Rufaa ya Mkoa, wapo kwenye mchakato huo.
Mheshimiwa Spika, kuhusu gari la wagonjwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda ni kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi kwamba utaratibu ni kwa Halmashauri yenyewe kuweka kipaumbele kwenye kununua gari la wagonjwa kama Halmashauri inaona inalihitaji kwa wakati huo. Sisi kama Serikali Kuu, wajibu wetu siyo kuwapangia vipaumbele Halmashauri zote nchini.
Halmashauri zenyewe zinapaswa ziweke vipaumbele vyao, watumie vyanzo vyao mbalimbali vya fedha na hata ruzuku inayotoka Serikali Kuu wanaweza wakaitumia kwa namna
yoyote ile watakavyoona wao wenyewe kwenye Halmashauri yao ili waweze kununua gari la wagonjwa.
Mheshimwa Spika, kwa hivyo kuhusiana na Mpanda mahsusi kama tutapata fursa ya misaada ya magari, nilikwishamuahidi Mheshimiwa Kakoso lakini pia Mheshimiwa Mhandisi Kamwelwe kwamba tutatoa kipaumbele cha kipekee kwa Mkoa huu mpya wa Katavi kwa sababu nilifanya ziara pale na nikaona kwa kweli miundombinu yake ipo katika hali mbaya. Nilisema kama kutatokea sisi tukapata ambulances pale Wizara ya Afya huu ni katika Mikoa ambayo tutaipa kipaumbele cha kwanza.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Naipongeza Serikali kwa mtazamo huo mpya na ninaamini sasa huo ndiyo mtazamko chanya ambao tunapaswa kwenda nao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa sasa hivi katika ununuzi wa vifaa tiba tumekuwa tukivinunua bila kuwa na mpango wa matengenezo kwa maana ya Plan Preventive Maintenance, kuwekwa katika mpango wa
manunuzi.
Je, sasa Serikali mtakuwa tayari kuhakikisha wakati mna-negotiate kununua zile mashine mnaweka mpango wa Preventive Maintenance kwa sababu sasa hivi gharama zinazotumika kutengeneza vifaa tiba ni za juu sana?
Swali la pili, kwa kuwa, gharama za utengenezaji wa vifaa hivi ni kubwa sana, kwa maana ya
Preventive Maintenance na pale vinapokuwa vinaharibika kwa hali ya kawaida:-
Je, Serikali haioni sasa ni muda muafaka kuingiza gharama za PPM ama Plan Preventive Maintenance katika gharama za vitendanishi, badala ya kutenga peke yake ambazo ni mabilioni ya hela ambapo mara nyingi Serikali inaishia kutozilipa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inakubaliana na wazo lake kwamba gharama za Planned Preventive Maintenance ni vema zikawa sehemu ya mkataba mkuu wa ununuzi wa vifaa tiba. Hivyo, ndiyo maana mikataba yote mipya ambayo itafungwa na Serikali na Private Contractors kwa sasa itahuisha uwepo wa section maalum ambayo ina Planned Preventive Maintenance katika costs zake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili pia tunakubaliana naye kwamba ni lazima tuziingize gharama za PPM kwenye manunuzi ya vitendanishi. Pia tunakubaliana naye kwamba ni wazo zuri, naomba nilichukue na nitalifanyia
kazi ndani ya Serikali.
MHE. MARTHA J. UMBULLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, kwanza nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa juhudi yake kubwa, amekuja mara nyingi katika Mkoa wetu wa Manyara kutatua kero mbalimbali za wananchi hasa katika sekta ya afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini naomba kutoa masikitiko yangu kwamba sijaridhika na majibu ya Serikali katika swali langu hili la namba 94.
Kama tatizo liko kwa asilimia 100 katika mkoa, ina
maana kwamba lazima kwa utafiti uliofanywa na Serikali kuna vigezo vilivyoonyesha kwamba lazima kuna takwimu ambazo zinaonyesha asilimia 100 imetokana na vitu gani, hasa vifo na adhari mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu (b) ya swali langu nilitaka kupata idadi ya vifo, siyo sababu zinazosababishwa na ukeketaji kwa sababu hizo tunazijua. Nilitaka kupata takwimu ni vifo kiasi gani na maeneo gani ili sisi viongozi wa Mkoa wa Manyara tuweze kupambana, tuongeze juhudi ya
Serikali kapambana na janga hili ambalo liko kwa asilimia 100 katika mkoa wetu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, nini kauli ya Serikali kufuatana na hali hii mbaya katika mkoa wetu wa Manyara?
Swali la pili, kwa maelezo ya Mheshimiwa Naibu Waziri, amesema tunatumia Maafisa Maendeleo ya Jamii na Afisa Ustawi wa Jamii ili kutoa elimu kupambana na janga hili, lakini Maafisa Maendeleo ya Jamii na Afisa Ustawi wa Jamii wako siku zote na hali imefikia asilimia 100.
Sasa je, Serikali ina mikakati gani ya ziada ili kupambana na tatizo hili specifically kwa Mkoa wa Manyara ili na sisi Manyara tubaki salama?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII JINSIA NA WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Namshukuru Mheshimiwa Martha Jachi Umbulla, kwa maswali yake ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu yetu ni kwamba
kwanza, asilimia 100 siyo kwamba ni watu wote. Ni kwamba tatizo hili lipo zaidi Vijijini kuliko maeneo ya Mijini, lakini kiwango hasa cha kitakwimu kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na
National Bureau of Statistics ni kwamba katika wanawake 100 wa Mkoa wa Manyara, basi wanawake 71 wamekeketwa. Idadi ya vifo hatukuweza kupata takwimu za idadi yake kwa
uhakikika kwa sababu vitendo vya ukeketaji vinafanyika gizani, vinafanyika kwa siri na utamaduni umebadilika, badala ya kuwakeketa kipindi kile cha usichana mdogo, sasa hivi wanakeketa watoto wachanga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna mbinu mpya
ambayo wamegundua, wanawakeketa watoto wakati wakifanya tohara kwa watoto wa kiume. Kwa hiyo, wanawachanganya, inakuwa kama ni sherehe ya tohara inayokubalika kisheria kwa watoto wa kiume wanawaunganisha na watoto kike. Kwa hiyo, kuna mbinu nyingi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika kujibu maswali yake, najibu tu yote kwa pamoja mawili kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Profesa Palamagamba Kabudi akizungumza hapa, aligusia Legal Anthropology. Sisi kwenye tiba tunazungumzia Medical Anthropology, sasa tunapo-approach tatizo pamoja na kuwa na sheria, pamoja na kuwa na mambo mengine, hatuwezi kujikita kwenye sheria peke yake, ni lazima tuitazame jamii nzima holistically, lazima tuitazame jamii nzima kwa ujumla wake. Tuzitazame mila na desturi za jamii husika, tutazame namna ya kupenya kwenye hiyo jamii ili kuufikisha ujumbe wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa msingi huo, tumekuja na mkakati mpya sasa wa kutumia mbinu inaitwa kwamba alternative right of passage. Kwa sababu kwenye mila za kukeketa, imebainika kwamba ni lazima zifanywe na jamii
zinazofanya mambo hayo kwa sababu wanataka kuwagraduate watoto wa kike kutoka kwenye status ya usichana na kwenda kwenye status ya uanamke. Sasa kama wasipokeketwa, wanaume wanakataa kuwaoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ili ku-address hili tatizo, huwezi kutumia sheria peke yake, ni lazima uelewe sababu hizo na sasa mbinu yetu mpya ya ARP (Altenative Right of Passage) tunaitumia kwa maana ya kuyafikia viongozi
wa kimila na watu mashuhuri kwa jamii husika ili kufikisha ujumbe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo namshauri Mheshimiwa Martha Umbulla na viongozi wote wa kimila na Kiserikali katika Mkoa wa Manyara kuanza kuhamasisha jamii yao kuachana na mila hizi kwa hiari na kwa kuwaelewesha kuliko kutumia zaidi nguvu. Ahsante.
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kutokana na majibu mazuri ya Serikali kuwa msamaha wa matibabu utatolewa kwa mtu mwenye ulemavu ambaye atabainika hana uwezo; ikumbukwe kuwa ugonjwa unampata mtu bila taarifa.
Je, Serikali ina utaratibu gani wa kuwabaini watu wenye ulemavu wasio na uwezo ili waweze kupata msamaha huu wa matibabu?
Swali la pili, je, Serikali ipo tayari kuziagiza mamlaka husika na kutoa waraka ili majibu yaliyotolewa hapa leo yaweze kutekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, maswali anayozungumzia Mheshimiwa Stella ni muhimu sana kama ulivyosema wewe mwenyewe na ni maswali yanayohusu uwiano na usawa kwenye jamii yetu, ambapo kama Taifa ni lazima tutoe uwiano sawa kwa watu wote bila ubaguzi wa aina yoyote ile kama ambavyo waasisi wa Taifa letu waliweka misingi kupitia sera yetu ya ujamaa na kujitegemea.
Mheshimiwa Spika, ni kwa msingi huo, Serikali kupitia
Sera yake ya Afya ya mwaka 2007 inatoa matamko ya kisera ya namna ambavyo makundi maalum kwenye jamii yanalazimika kuhudumiwa ikiwemo kundi hili la watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Spika, sasa utaratibu wa utekelezaji unawekwa na sheria na taratibu mbalimbali ndani ya Serikali. Katika awamu hii ya tano, tunakusudia kuleta hapa Bungeni mapendekezo ya Bima ya Afya ya lazima kwa watu wote ambapo ndani yake tutakuwa tumeweka utaratibu mahsusi wa kuhakikisha uwiano huu tunaouzungumza unatekelezeka kupitia Bima ya Afya ambapo tutaweka utaratibu sasa kwamba watu wanaopewa msamaha kwa mujibu wa sera, basi wawe na kadi ya Bima ya Afya kuliko ilivyo sasa. Kwa sababu inajitokeza katika nyakati mbalimbali ana msamaha anastahili kupata huduma bure, lakini anapofika kwenye kituo cha kutolea huduma, anakosa dawa ama anakosa vipimo fulani na analazima kwenda kwenye private. Kwa hiyo, hata ile bure inayokusudiwa na sera yetu inakuwa haipo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sisi ndani ya Serikali tunaamini kama tutafanikiwa kupitisha sheria hii ya Bima ya Afya kwa wote, utaratibu utakuwa mzuri. Kwa hiyo, anachokizungumzia sasa hivi tumekianzisha kwa mfano tu kwa kujaribisha kwenye kundi la wazee wenye umri wa zaidi ya miaka 60 wasiojiweza ambapo Halmashauri zinalazimika kuwabaini wazee wote katika eneo lao na kuwawekea utaratibu wa kuwapa kadi za CHF ili kujaribisha utaratibu tunaozungumza.
Mheshimiwa Spika, kwenye kundi la walemavu, bado hatujaanza.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa sasa MSD ina Bohari Kikanda. Je, Serikali ina mpango gani wa kufungua Bohari ya MSD kila Mkoa ili kurahisisha usambazaji wa madawa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; Serikali imejiandaaje kudhibiti upotevu, wizi wa dawa kwa watumishi wasio waaminifu katika zahanati na vituo vya afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Swali la kwanza kuhusu Serikali kujenga bohari za dawa kila mkoa; kwamba tuna mpango gani; kwa sasa hatujawa na mpango wa kufanya hivyo kwa sababu tunaamini utaratibu wa kuwa na bohari kwenye kila kanda bado haujakwama. Ni kwamba tunahitaji kufanya maboresho kidogo tu ili tuweze kuongeza tija na ufanisi kwenye kuhakikisha vituo vya umma vinapata dawa kadri ambavyo vinahitaji na kwa haraka kadri ambavyo inawezekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mfumo wetu wa sasa hivi wa Supply Chain Management, tunaamini bado haujakwama na ndiyo maana tumeendelea kuuboresha. Tulikuwa na changamoto kidogo za kifedha, ambazo kama ambavyo sisi Wabunge ni mashahidi na naomba nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa azma yake thabiti ya kuongeza upatikanaji wa dawa kwa kutuongezea bajeti kwenye eneo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, changamoto ya kifedha tuliyokuwanayo ambayo ilikuwa inashusha tija na ufanisi, sasa inaelekea kuondoka na mfumo wa upatikanaji wa dawa umeimarika sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuhusu udhibiti, naomba nitumie Bunge lako Tukufu kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wote, Madiwani wote na Viongozi wote kuanzia Viongozi wa Mikoa na Wilaya washiriki kikamilifu katika kusimamia udhibiti wa mfumo wa upatikanaji wa dawa kwenye vituo vyetu kwa sababu, jambo hili haliwezi kuwa ni la sisi tu tuliopo Fungu 52, kwa maana ya Wizara ya Afya pekee. Kwa sababu, mfumo wetu wa udhibiti upo, kwamba kwenye kila zahanati, kila Kituo cha Afya na kwenye kila hospitali, kuna Kamati ya Udhibiti wa Dawa, Vifaa, Vifaa Tiba na Vitendanishi ambapo ndani yake kuna viongozi wa kuchaguliwa na kuna watendaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo ni kwamba, mfumo huu hausimamiwi ipasavyo. Kama ungefanya kazi ipasavyo, kwa hakika, tungeweza kudhibiti wizi na ubadhirifu wa madawa ambao umekuwa ukitokea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu, kama kuna mtu ana taarifa yoyote ile ya mahali ambapo kuna wizi ama upotevu wa dawa ambao umejitokeza, atupe taarifa na sisi tutachukua hatua haraka.
MHE. ANNA J. GIDARYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Ugonjwa wa fistula ni ugonjwa ambao umeenea karibu Tanzania nzima. Ugonjwa huu unawadhalilisha akinamama, hususan mikoa yetu ambayo ina jamii ya wafugaji, watu ambao hawahudhurii mara nyingi kliniki. Je, Wizara ina mpango mkakati gani wa kutoa elimu hii kwa kila Wilaya, hasa kwa jamii hii ya wafugaji?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nakubaliana na Mheshimiwa Gidarya kwamba ugonjwa wa fistula unawadhalilisha sana mama zetu, shangazi zetu, dada zetu katika jamii. Ni jambo ambalo mwanaume yeyote ambaye anawapenda mama zetu na dada zetu hawezi kukubaliana nalo. Nami kama Balozi wa Wanawake nimhakikishie tu kwamba tutaendelea kuboresha huduma za uzazi kwa sababu ndiyo kisababishi kikubwa cha ugonjwa wa fistula ili kupunguza cases za fistula ambazo zimekuwa zikijitokeza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango tulionao kwa sasa ni kutumia kliniki zetu za uzazi ambazo zipo kwenye kila kituo cha kutolea huduma za afya, kuanzia ngazi ya zahanati kwenda ngazi ya kituo cha afya, ngazi ya hospitali ya wilaya mpaka ngazi ya hospitali za rufaa, kutoa elimu kwa akinamama wote na akinababa wote ambao wanafika kuhudhuria kliniki za uzazi salama katika vituo vyetu vya kutolea huduma za afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa changamoto zinazojitokeza za tiba zimekuwepo na tunaendelea kuzipunguza kwa kuendelea kutoa ujuzi, lakini pia elimu kwa umma juu ya kuwahi kupata huduma za uzazi ili wasipate madhara yanayotokana na mchakato wa uzazi.
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii nami niulize swali moja la nyongeza. Kwa kuwa, tatizo linalozikabili zahanati nyingi nchini siyo upungufu wa dawa tu, bali pia huduma kwa akinamama wajawazito, hususan katika wodi zao huduma ni mbaya, ni hafifu, vifaa stahiki hakuna: Je, ni lini Serikali itahakikisha inaboresha afya kwa akinamama wajawazito katika hospitali na zahanati zote za Mkoa wa Kagera?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nitoe majibu ya uhakika kwamba, kwanza nimkumbushe Mheshimiwa Halima Bulembo kwamba kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM katika vipaumbele vitano kwenye Sekta ya Afya ambavyo vimeandikwa mle ni pamoja na kuboresha huduma za akinamama wajawazito na watoto.
Kwa maana hiyo, naye kama Mwana-CCM mwenzangu lazima anafahamu kwamba jitihada za kupunguza matatizo na changamoto mbalimbali zilizopo kwenye huduma za akinamama wajawazito, zimekuwepo, zitaendelea kuwepo na ndiyo maana hata leo tutakapowasilisha bajeti yetu ataona tuna mikakati mahususi ambayo imejikita kwenye kuboresha huduma za uzazi kwa akinamama wajawazito.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli hili ni jambo ambalo Mheshimiwa Rais mwenyewe alilizungumza pia hapa Bungeni na sisi wakati anatukabidhi majukumu haya alituagiza tulisimamie kwa nguvu za kutosha. Kwa hiyo, ni jambo ambalo kwa hakika hatulifanyii mzaha hata kidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba huduma za uzazi zitakuwa bora na yeye atajifungua salama kadiri Mungu atakavyomsaidia.
MHE. MGENI JADI KADIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naipongeza Serikali kwa kuunda Tume ya Kupambana na Kudhibiti Dawa za Kulevya na kuongeza vituo vya tiba. (Makofi)
Swali langu la kwanza, Serikali baada ya kupiga marufuku uingizaji wa biashara za viroba na kuteketeza mashamba ya bangi, je, adhabu gani iliyowekwa kwa wale watakaoingiza viroba na wale watakaopanda mbegu za bangi katika mashamba yao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, je, ni Mkoa gani unaoongoza kwa idadi ya vijana walioathirika zaidi kwa dawa za kulevya? Na Serikali inawaangaliaje vijana hao baada ya kupona? Watawapa msaada gani ili waweze kujiendeleza na maisha yao?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, adhabu gani watapata; adhabu zimeainishwa kwenye sheria zetu, tuna sheria inayozuia matumizi ya vilevi, hususan dawa za kulevya (The Narcotic and Drug Abuse Act) kwa hivyo, ndani mle imeainishwa adhabu ya mtu anayetumia na mtu anayeingiza na mtu anayesaidia kuwezesha mambo hayo. Kwa hiyo, adhabu itatolewa kwa mujibu wa sheria hizo, sikumbuki ni adhabu yenye ukubwa kiasi gani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali lake la pili, ni Mkoa gani ambao unaongoza; Mkoa wa Dar es Salaam unaongoza kwa kuwa na wagonjwa wengi kuliko mikoa yote, ukifuatiwa na majiji mengine na sasa Serikali inachukua hatua gani kuwasaidia watu ambao wameathirika na dawa za kulevya. Mikakati tuliyonayo ni kama hii ya kuanzisha kliniki za kutoa dawa ya methadone. Hii dawa ya methadone inasaidia sana kwa wagonjwa kuacha kutumia hizi opioids kwa sababu methadone na yenyewe ni katika group hilo hilo la opioids, lakini uzuri wa methadone haisababishi utegemezi kama zile dawa nyingine. Kwa sababu dawa hizo nyingine kama heroin na cocaine zinasababisha utegemezi ambapo utegemezi ule unaweza ukaondolewa na dawa nyingine ambayo inafanya replacement ya dawa zile, kwa hiyo, mtu anaweza akaacha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hilo ni la kwanza, lakini la pili, ni kuwasaidia kwenye shughuli mbalimbali za kurudi kwenye jamii, kama kushiriki kwenye ufundi na kuwapa mafunzo mbalimbali, ili waweze kuwa intergrated kwenye jamii.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nichukue nafasi hii kuwapa pole wananchi wangu waliopotea na chombo baharini, leo ni wiki hawajaonekana, niwaombee Mwenyezi Mungu awajalie kama bado wako hai awafanyie wepesi na kama wamefariki awaweke pema peponi, Amina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiona azma nzuri ya Serikali katika kupambana na dawa za kulevya; na ninaisifu sana, naipongeza Wizara hii kwa usimamizi mzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kukinga ni bora kuliko kutibu, kwa muda mrefu imesemekana na ni ukweli usioshaka kwamba, Zanzibar imekuwa ni lango kuu la kupitisha dawa za kulevya. Tumeona juhudi ya Serikali pale inapowaonea huruma wananchi wake wa Zanzibar katika mambo tofauti mbalimbali yanapojitokeza. Je, ni lini Serikali itachukua kwa makusudi jitihada za kuiweka Zanzibar katika uangalizi maalum wa kukomesha kuwa corridor muhimu ya kupitisha dawa za kulevya ambazo uingiaji wake na matumizi yake makubwa inakuwa ni hapa Tanzania Bara?Ni lini Serikali itaonesha kujali na kuchukua hatua madhubuti kukomesha janga la Zanzibar kuendelea kuwa uchochoro wa dawa za kulevya? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niungane na yeye kumpa pole juu ya wananchi wake waliopotea na boti.
Lakini la pili, jibu lake kwenye swali lake ni kwamba nakubaliana na yeye Zanzibar kwa muda mrefu imekuwa ni corridor ya dawa za kulevya, lakini kwenye mikakati ya kupambana na dawa za kulevya kuna maeneo mawili; kuna supply reduction na kuna demand reduction, kwa hiyo, kwenye supply reduction wenzetu wa Tume ya Dawa za Kulevya ambayo inaongozwa na Kamishna Siang’a wanaongoza mapambano kweye eneo hilo na mikakati yao zaidi ni ya kiintelijensia na mambo mengi wanayoyafanya hayasemwi hovyo hovyo. (Makofi)
Kwa hivyo, nikuhakikishie tu Mheshimiwa Khatib, Tume kwa sasa kwa kweli imepunguza sana supply ya dawa za kulevya kwenye nchi yetu, ikiwemo kule Zanzibar. Na hilo wala halina shaka na huo mfereji unaousema kwa hakika kwa sasa umezibwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kwenye demand ni kutoa tiba na kuwasaidia kwenye impact reduction. (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa, Mheshimiwa Waziri alipokuwa anajibu majibu yake alisema kwamba, kwenye miji mikubwa kuna hiyo huduma inatolewa, lakini ukija kwenye miji midogo kwa mfano Iringa kuna vijana wengi sana wameathirika. Lakini tumshukuru sana Dkt. Ngala pale Iringa, ameweza kuhamasisha wananchi wamefungua vituo kama hivi, lakini sasa wananchi wanashindwa gharama imekuwa kubwa sana kwenda kwenye vituo.
Sasa je, Serikali iko tayari kutoa ruzuku kwa watu ambao wamenzisha vituo hivi ili viweze kusaidia kwenye miji midogo kama Iringa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nijibu maswali haya mawili, Mheshimiwa Waziri wa Nchi atamalizia kwa ujumla yanayohusu supply reduction.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la kwanza la Mheshimiwa Amina Mollel, kwanza nimpongeze siku ya jana aliniletea wageni kutoka Chama cha Wananchi ambao wanajihusisha na Afya ya Akili Nchini na katika mazungumzo tuliyoyafanya ni pamoja na hili suala la Madaktari Bingwa wa Afya ya Akili kwenye Mikoa nchini. Mkakati tulionao na ndio taarifa niliyowapa wale wananchi wenzetu ni kwamba Serikali ina-scale up huu mkakati wa kuwa na hizi kliniki kama iliyopo Muhimbili, Temeke na Mwananyamala kwa mwaka huu kwenye mikoa kumi ya Tanzania Bara na kwa mwaka ujao tutaongeza mikoa mingine kumi, tunakwenda kwa awamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, kila tutakapoanzisha hii kliniki ya methadone ni lazima awepo Daktari Bingwa anayehusika na ku-administrate hiyo dawa kwa sababu methadone inalindwa kwa taratibu maalum za kuitunza na kuitoa kwa wagonjwa. Kwa hiyo, ni lazima awepo Daktari Bingwa anayeweza kufanya hivyo kwa hivyo, kwa mwaka huu nimhakikishie Mheshimiwa Amina Mollel kwamba tutakuwa na Madaktari Bingwa kwenye mikoa kumi ncjini, pindi kliniki za methadone zitakapoanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni la Mheshimia Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kuhusu hizi kliniki na rehabilitation centres kwenye Mikoa; kwa sasa kweli, tuko Dar es Salaam peke yake, lakini kwenye mkakati wetu tunakwenda kwenye mikoa kumi kama nilivyosema. Na kwenye kila kanda tunakwenda kuanzisha rehabilitation centre ambapo tutakuwanazo nne sasa katika nchji nzima. Kwa hivyo, hii ni mikakati ambayo tunayo katika siku za usoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ruzuku, Serikali haina utaratibu wa kutoa ruzuku kwenye taasisi mbalimbali za binafsi, kwa sababu wao wanafanya kwa hiyari na tunawaomba na kuwatia moyo waendelee kufanya hivyohivyo kwa hiyari, lakini sisi kama Serikali tuna mikakati yetu ya kuwasaidia wenzetu ambao wameathirika na dawa za kulevya.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, ninaomba nijibu maswali ya nyongeza yaliyoulizwa kwa umoja wake, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwanza nianze kumpongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri wa Afya, kwa majibu mazuri aliyokwishakuyatoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze tena kwa kulipongeza Bunge letu Tukufu kwa sababu mwaka 2015, ndilo lililosababisha kufanyika kwa mageuzi makubwa ya mapambano dhidi ya dawa za kulevya nchini kwa kutungwa kwa sheria mpya ambayo imeunda hiyo mamlaka sasa ambayo tumemuona Kamishna Jenerali akifanya kazi kubwa sana kwa kushirikiana na makamishna wenzake kuhakikisha kwamba tunapambana na tatizo la dawa za kulevya nchini.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba niliarifu Bunge
lako Tukufu Kamishna Jenerali baada ya kuteuliwa na mamlaka kuanza kazi rasmi, ameshahakikisha ametengeneza Mpango Mkakati Maalum wa Taifa wa kuhakikisha kwamba tatizo hili la dawa za kulevya nchini linaondoka. Na mpango mkakati huo unashirikisha pande zote mbili za Muungano, upande wa Zanzibar na upande wa huku Bara. Kwa hiyo, Mheshimiwa Khatib wala usiwe na wasiwasi, tunafanya kazi hizi kwa pamoja, vyombo hivi vyote viwili vinafanya kazi kwa pamoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumegundua kwamba, wenzetu wa private sector wanafanya kazi nzuri sana kwenye mapambano dhidi ya dawa za kulevya nchini. Na hivyo nichukue nafasi hii kwanza niwapongeze wale wote ambao wameamua kujitolea kusaidiana na Serikali katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya katika nchi yetu ya Tanzania, tunawashukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika mwaka huu wa bajeti, Ofisi ya Waziri Mkuu imeamua kuweka bajeti kidogo ambayo itasaidia kushirikiana na hao wenzetu ambao wameonesha kwamba, wana nia ama ya kuanzisha sobber houses kwa ajili ya kuwasaidia hawa walioathirika na dawa za kulevya, lakini vilevile kufanya kampeni na kuleta uhamasishaji mkubwa wa kuwasaidia vijana wetu kuwaondoa kwenye tatizo hili.
Kwa hiyo, tuko pamoja tunafanya kazi hii kwa pamoja, mapambano yanaendelea na tunataka kuona kwamba tunaondoa tatizo hili katika nchi yetu. (Makofi)
MHE. OTHMAN OMAR HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nina maswala mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, pamoja na kuhamasishwa Halmashauri mbalimbali kununua dawa hizi zinazotengenezwa na kiwanda hiki, Wizara ya Afya ni mteja mkuu ambaye alitegemewa kununua dawa hii inayozalishwa na kiwanda hicho, lakini wameshindwa kutokana na kukosa pesa, jambo ambalo limepelekea kiwanda kutafuta wateja kutoka nchi za nje.
Mheshimiwa Naibu Spika, namuomba Naibu Waziri atueleze hapa imekuwaje Wizara kutokutenga pesa kwa ajili ya kuwanusuru Watanzania ambao wanasumbuliwa na ugonjwa huu wa malaria hapa nchini?
Swali la pili,kwa sababu teknolojia hii ya kuzalisha viuadudu vya kuulia viluilui vya mbu ni mpya hapa Tanzania na Bara zima la Afrika, Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza kutueleza ni maeneo gani katika Jamhuri yetu ya Tanzania wamewahi kuchukua angalau sampuli ya kiwanda kile na kuweza kuifanyia majaribio ili kuweza kujua ubora wa dawa hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba arudie swali la pili walikuwa wanapiga makofi, sikumsikia vizuri.

MHE. OTHMAN OMAR HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimemuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba kwa sababu teknolojia hii ya kuzalisha viuadudu vya kuulia viluilui vya mbu wanaoeneza malaria ni mpya hapa Tanzania na Bara zima la la Afrika.
Je, Wizara imewahi angalau kwenda kuchukua sampuli kule kiwandani na kuweza kuifanyia majaribio na kuweza kujua ubora wa hii dawa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nitaanza na swali la pili kwamba je, Wizara imewahi kwenda kuchukua sample kwenye kiwanda kile na kuzifanyia utafiti?
Kwanza naomba nimhakikishie kwamba teknolojia
ya biolarvicides kuingia hapa nchini na kukubalika kutumika kuna mchakato mrefu wa kisayansi ambao umefuatwa.
Kwa hivyo, katika hatua hii ambapo inazalishwa kwa wingi wala hakuna haja ya kufanya utafiti wa majaribio, kwa sababu pale mwanzoni wakati ugunduzi wa teknolojia unafanyika zilifanyika tafiti ambazo kisayansi zinajulikana kama clinical tries za kubaini efficacy ya biolarvicide ambayo inatumika lakini pia kubaini kama kuna any emergency ya resistance yaani usugu dhidi ya biolarvicide yenyewe ambayo inatumika na hatimaye ikafikiwa kuthibitishwa kwamba ni teknolojia ambayo ni effective.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano walipoanza kufanya tafiti hizi miaka hiyo ya zamani walitumia bacteria ambaye anajulikana kama bacillus sphaericus katika hatua za awali mpaka wakafikia mwisho wakakamilisha uchunguzi na ikaonekana kwamba bacillus sphaericus ana-develop resistance kiurahisi sana, wakahama wakaweka bacillus thuringiensis vara israelensis ambayo ni second generation.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kumuweka huyu bacillus wa aina ya pili yaani kwa kifupi BTI ikaonekana kwamba yeye ni effective zaidi kuliko yule wa kwanza. Kwa hivyo, ikaonekana kwamba sasa tutumie generaly BTI kwa ajili ya biolarvicide. Kwa hivyo ni teknolojia ambayo imethibitishwa na haina shaka, na sisi Tanzania tunapaswa kujivuna kwa kuwa tuna kiwanda hicho hapa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza kiwanda kile kitazalisha full capacity yake biolarvicides lita milioni sita. Malengo hasa ya kuanzisha kiwanda kile sio kwa ajili ya Tanzania peke yake, ni kwa ajili ya Tanzania na nchi nyingine za Afrika na dunia ambazo zitakuja kununua biolarvicide hapa nchini. Kwa mfano mpaka sasa tayari tuna nchi za Serbia, tuna nchi ya Cuba, yenyewe tuna nchi za Sweden, tuna nchi ya Niger ambazo zimenunua biolarvicide kutoka Tanzania, kwa sababu kuanzia hiyo mwezi Desemba, 2016 mpaka sasa tumezalisha lita milioni mbili na tumeuza kwenye hizo nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hapa Tanzania Halmashauri takribani tano zimeonesha nia ya kununua, Halmashauri mbili zimekwisha nunua japokua kwa kiasi kidogo na zimekwishatumia.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba niwapongeze Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe na Halmashauri ya Wilaya ya Geita ambao wao walikuwa ni wa kwanza kwa Halmashauri za hapa nchini kununua biolarvicide. Kwa hiyo swali lake la msingi linasema kwamba Wizara ya Afya tungepaswa tununue si sahihi kwa sababu malengo ni sisi kuwezesha kiwanda kile kuwepo na baada ya hapo Halmashauri ziweke kwenye bajeti zao wao wenyewe waweze kununua pale kadri ambavyo wanahitaji. Ndiyo maana tunaendelea na uhamasishaji wa Halmashauri zote nchini kununua biolarvicide kwa ajili ya control ya malaria.
MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Kwa kuwa ugonjwa wa malaria ni ugonjwa ambao unaongoza kwa kuua katika nchi hii na ninaamini kwamba Wizara imetenga fedha kwa ajili ya kupambana na malaria. Ni kwa nini Waziri asione kuna umuhimu wa fedha zote ambazo zimetengwa kwa ajili ya kupambana na malaria zikapelekwa kwenda kununua dawa za viuadudu Kibaha ili kupambana na malaria ikizingatiwa hicho kiwanda sasa hivi kimesimama kuzalisha kwa sababu ya kukosa soko la bidhaa zake?
NAIBU WAZIRI WA WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwamba kwa nini tusichukue fedha zote tukapeleka kwa ajili ya kununua biolarvicide pale Kibaha kwa ajili ya Halmashauri zetu nchini. Hatuwezi kufanya hivyo kwa sababu udhibiti wa malaria siyo kuua larva peke yake tunamu-attack adui mbu katika hatua nyingi tofauti tofauti, lakini pia tunamu-attack kile kijidudu chenyewe ambacho kinaambukiza malaria yaani plasmodium falciparum katika hatua nyingi tofauti. Kwa hivyo, mikakati ni mingi ambayo inamlenga adui mmoja kwamba yule vector ambaye ni mbu either wa aina ya anopheles ama tunamu-attack plasmodium mwenyewe akiishaingia kwenye damu ndiyo control inakuwa hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo hatuwezi kutumia njia moja kumu-attack adui kwamba tunaua tu mazalia yaani larvae halafu tunasema basi ndiyo tumemaliza, hapana! Lazima kuwe kuna tiba. Kwa hiyo, ndiyo maana tuna mkakati wa kusambaza ALU (Artemether na Lumefantrine combination) nchi nzima na tunagawa bure ili tuue plasmodium falciparum ambaye yumo kwenye damu. Ndiyo maana tuna mkakati wa wajawazito, tunatumia SP (Sulfadoxine Pyrimethamine) kwa ajili ya kumuua mdudu mbu ambaye anawa-attack akina mama wajawazito.
Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana tuna net kwa ajili ya kuzuia mbu ambao wanapenda kuishi ndani ya nyumba na wanauma saa sita usiku kuambukiza malaria. Sasa tuna mikakati mingi, tunatumia IRS – Indoor Residual Spraying kwa ajili ya kumu-attack mbu ambaye anapenda kubaki ndani ya nyumba, mchana hatoki nje anabaki ndani ili asiwepo. Kuna mikakati ya kumuua mbu kama atakuwa nje kwenye mzingira. Sasa hii ya kwenye mazingira ndiyo tunaona teknolojia hii mpya ya biolarvicides itatusaidia. Vinginevyo tungetumia DDT. (Makofi)
MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na ushirikiano mzuri wa ndugu zetu hawa wa Cuba katika mambo ya tiba Tanzania, kwa kule Zanzibar ndugu zetu hawa walikuwa na programu maalum ya kuwafunza vijana wetu Udaktari na kwa kweli tayari sasa hivi intake mbili zimeshatoka, moja madaktari wanaendelea na kazi zao na wengine wako katika internship sasa hivi. Kwa kweli inaonekana kwamba wana mafanikio makubwa.
Je, kwa hapa Tanzania Bara programu hii imeanzishwa au imeshafikiriwa kuanzishwa kwa kuwatumia hawa ndugu zetu wa Cuba? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza Cuba ni marafiki wa kihistoria wa Tanzania. Comradeship iliyotengenezwa na Fidel Castro na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ni ya muda mrefu na imezaa matunda mengi katika nchi zote mbili, zaidi sisi tukiwa wafaidika kuliko wenzetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika ushirikiano huo, Watanzania wengi, hususan kwenye fani hii ya afya wamepelekwa Cuba kwa ajili ya masomo na wamesoma masomo ya ubingwa lakini pia katika nyakati mbalimbali hata wanajeshi wetu ambao wanahusika na mambo ya tiba na uokoaji pia wamepelekwa Cuba kwa ajili ya kusoma.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 1986 ikaonekana kwamba isitoshe tu kuwa na exchange ya Watanzania kwenda kufundishwa kule Cuba mambo ya afya, ikaonekana kwamba tusaini mkataba mwingine ili waje hapa hapa watujengee uwezo. Kwa hivyo, harakati za kujenga uwezo zimekuwa zikifanyika kila mahali ambako madaktari wa Cuba wamekuwepo, pia wamekuwa wakifundisha katika vyuo vyetu hapa nchini, hivyo hata kwa Tanzania Bara tunao.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ninavyozungumza hapa, tuna Madaktari Bingwa kumi na moja wanaotokea Cuba ambao wapo katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Ruvuma. (Makofi)
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Natambua Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla wewe ni mtaalam na unafahamu kabisa kwamba katika prevention za malaria kuna primary prevention na kuna secondary prevention, nashukuru umeelezea vizuri sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Mheshimiwa Naibu Waziri kiwanda cha viuadudu kama tutaweza kufanikiwa, dawa ikasambaa vya kutosha tuka-control wale vector kwenye hiyo level ya wale wadudu kutafuna larva, huoni kwamba tutakuwa tume-eradicate kabisa malaria na ni wajibu wa kila Hamashauri kununua zile dawa ili kusudi kile kiwanda kifufuke na tuweze kuzuia malaria? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Anachokisema ni sahihi kabisa, tukitumia hii teknolojia ya biolarvicides effectively tunaweza tuka-control malaria na hatimae kuidhibiti kabisa katika muda mfupi zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaweza tukawa tupo constrained kibajeti na nadhani mkakati wetu kama nchi siyo kwa Wizara ya Afya kununua na kusambaza nchi nzima kwasababu majukumu yetu sisi kwakweli ni prevention, lakini pia tiba na mambo mengine na tuna support kwa kupitia pesa tunazozipata kutoka kwa wabia wa PMI pamoja na Global Fund.
Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana hili suala la biolarvicides tunawahamasisha Halmashauri zote nchini kwa kutumia mapato yao ya ndani washiriki kwa kutenga pesa kwa ajili ya kununua hizi biolarvicides na kuzisambaza na kuzitumia kwenye maeneo yao. Sisi kama Wizara ya Afya tumekwishakutengeneza mwongozo wa namna ya wao kutumia teknolojia hii ku-control hawa bio larvae kwa kutumia biolarvicides katika maeneo yao. Kwa hivyo, sisi kazi yetu ni hiyo tu, kutoa mwongozo na tumekwishatoa. Sasa Halamshauri zote including Halmashauri ya Maswa mnunue. Wenzenu wa Kondoa wameshaweka order, wenzenu wa Songwe, Namtumbo, Mbogwe na Geita pia wameweka order.
Waheshimiwa Wabunge, kwa hivyo Halmashauri nyingine na ninyi mhamasishe kwa kutumia mapato yenu ya ndani muweze kununua biolarvicides kwa ajili ya control ya malaria. (Makofi)
MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIBU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri, lakini nipende kumuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tathimini inaonesha kwamba kila mwaka akina mama zaidi ya 400 wanapoteza maisha kutokana na vifo vinavyosababishwa na kujifungua. Je, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza vifo hivi 400 kwa mwaka vinavyojitokeza wakati wa kujifungua? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, ni kwa
nini vituo vya huduma ya upasuaji katika Tanzania yetu ni vichache hasa ukizingatia maeneo ya vijijini?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze kwa hali aliyo nayo na nimtakie kila la kheri yeye na mwanaye na niwahakikishie kwamba watamaliza safari yao salama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kujibu maswali yake naomba niyajibu kwa pamoja tu kwamba tuna mkakati gani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mikakati tuliyonayo ni mingi na kwa kiasi kikubwa Serikali kwa sasa imewekeza nguvu zake zote kwenye huduma zijulikanazo kitaalamu kama Comprehensive Emergency Obstetric and Neonatal Care (CEmONC). Hizi ni package ya medical interventions ambazo zinahusisha kufanya upasuaji wa kumtoa mtoto tumboni, kumsaidia mama kwa kutumia njia za manual, lakini kumsaidia mama wakati wa kujifungua kama mtoto amekwama kwenye njia, pia kumuongezea damu mama mjamzito wakati wa kujifungua ama baada ya kujifungua, vile vile huduma za kutoa dawa ambazo zinajulikana kama urotonic ambazo zinasaidia ku-contract ile placenta wakati wa kujifungua ili kupunguza damu nyingi kupotea kwa mama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile huduma za dawa zinazopunguza magonjwa ya kifafa cha mimba, magonjwa kama eclampsia, pre-eclampsia, gestational hypertension na magonjwa yote yanayohusiana na akina mama wajawazito. Sasa hii package inapaswa kutolewa kwenye vituo vya afya nchini, inaitwa CEmONC. Huduma hizi kwa kweli zilikuwa za kiwango cha chini sana. Katika vituo vya afya takribani 484 tulivyo navyo nchini vinavyomilikiwa na Serikali tulikuwa na vituo 113 tu vinavyotoa huduma hizi; lakini kwa mujibu wa sera vituo vyote vingepaswa kutoa huduma hizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na ndiyo maana katika bajeti iliyopita hata kwenye bajeti hii tumejikita zaidi kwenye kuongeza idadi ya vituo ambavyo vitaweza kutoa huduma za CEmONC, na pia mkakati wetu umeendana sambamba na kuhakikisha hizo dawa nilizozisema kama oxytocin na magnesium sulphate zinapatika kwenye vituo vyote, hiyo ndiyo mikakati tuliyonayo. (Makofi)
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na Serikali kuweka mikakati mizuri ya kuhakikisha inapunguza vifo vya akina mama, nilikuwa naomba; wewe unatambua sasa hivi kuna Watanzania wengi walioko vijijini na mitaani wanaoteseka, wanaoumwa na kuugua maradhi yanayotibika lakini wamekosa fedha za kutibiwa hospitali mpaka wanagundulika na vyombo kama televisheni au redio au waandishi kwa sababu ya kukosa pesa.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia watu hawa? Kwa mfano kuna kijana mmoja anaitwa John ambaye ana maradhi makubwa ya moyo amegundulika na Clouds Television, je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia wagonjwa hawa? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwanza nivipongeze vyombo vya habari na Watanzania wote ambao wamekuwa katika nyakati tofauti wakichangia gharama za huduma kwa Watanzania wenzetu ambao wanakuwa wamekosa uwezo wa kufanya hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo niseme tu kwamba Serikali ina utaratibu wa kutoa misamaha kwa kila Mtanzania ambaye atashindwa kumudu gharama za huduma ya afya kwa sababu huduma za afya ni haki ya msingi ya kila Mtanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo nitoe rai, kama kuna Mtanzania ametozwa gharama ambazo hawezi kuzimudu, kuna utaratibu wa kufuata kueleza hali yake kwamba hana uwezo wa kumudu gharama hizo kupitia kwa Maafisa Ustawi wa Jamii waliopo kwenye Halmashauri zote na kwenye hospitali zote. Afisa Ustawi wa Jamii akifanya uchunguzi na akathibitisha kwamba kwa kweli Mtanzania huyu mwenzetu ameshindwa kumudu gharama za matibabu alizopewa basi Afisa Ustawi wa Jamii ata-write-off msamaha, ataandika msamaha kwenye fomu zake na Mtanzania huyu atapata huduma hizo bure bila gharama yoyote ile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo ni watu sasa wauelewa utaratibu huu na sisi Waheshimiwa Wabunge tuwaeleweshe Watanzania wenzetu, wanahabari pia wawaeleweshe Watanzania wenzetu, wala hakuna sababu ya kwenda kuchangishana kwenye vyombo vya habari ili ukapate huduma kwenye Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa sababu kama huduma hiyo ipo na huna uwezo wa kulipa muone Afisa Ustawi wa Jamii utapewa msamaha na utatibiwa bure hapo hapo Muhimbili.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Sambamba na kuokoa tatizo la akina mama katika uzazi salama bado akina mama hao wamekuwa wamachinga wa kubeba vifaa mbalimbali wakati wa kwenda kujifungua. Je, kama Serikali mnatambua tatizo hili ni lini Serikali mnahakikisha mnatenga bajeti ya kutosha katika hospitali zote za akina mama na akina mama wakifika kule kujifungua wapate huduma salama? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba kwanza nimesema kwenye jibu la msingi kwamba kuanzia mwaka wa fedha unaoendelea sasa hivi tuliweka bajeti ya kununua delivery packs ambayo itakuwa ina vifaa vyote vya kujifungulia kuanzia mackintosh kuja catgut na vitu vingine vyote vinavyopaswa kujifungulia, nguo zile za kujifungulia, sterile gown kwa ajili ya kumsaidia mama wakati wa kujifungua, na tutawagawia akina mama laki tano. Lakini pia kwenye bajeti ya mwaka huu tunavyo vifaa vingine (delivery packs) milioni moja, kwa hivyo katika akina mama 1,900,000 ambao wanajifungua kila mwaka tutakuwa tuna vifaa vinavyokaribia 1,500,000, lakini sio wote ambao watahitaji vifaa hivyo. Kwa hiyo, tutavigawa kwa watu ambao wana mahitaji kwa hivyo ni jambo ambalo tumekwisha kulitazama.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Serikali imekuwa ikitoa huduma bure kwa wagonjwa wa kisukari, kifua kikuu pamoja na UKIMWI, je, Serikali haioni sasa ni muda muafaka wa kuanza kutoa huduma bure kwa wagonjwa wa saratani ili kuwapunguzia wananchi gharama hiyo?
NAIBU WAZIRI WA WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma za saratani kwa mujibu wa Sera ya Afya ya mwaka 2007 nchini Tanzania ni bure katika ngazi zote na kwa maana hiyo kila mgonjwa wa saratani atapata huduma zote anazohitaji bure (free of charge) wala hakuna gharama yoyote ile, kwa hiyo sio kwamba tutaanza lini tayari sera inasema hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ila kama mgonjwa haijajulikana kwamba ana saratani wakati anafanyiwa uchunguzi, haijathibitika kwamba ana saratani anaweza akachajiwa vipimo na vitu vingine lakini kuanzia pale atakapogundulika kwamba ana saratani atapata huduma zote bure.
MHE. WILFRED M. LWAKATARE: Mheshimiwa Spika, yako makabila ambayo kwa jadi yamekuwa yanatumia bangi kama mboga na wakati mwingine kuvuta, je, Serikali inatambua hilo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili Mbunge Musukuma wa Geita aliwahi kutamka hadharani hapa Bungeni kwamba kule Geita vijana wanatumia bangi, wakivuta bangi wanalima kuliko trekta, sasa majibu ya Serikali ambayo yanasema kwamba vijana waweze kusaidiwa kuacha matumizi ya bangi, je, Serikali haioni kwamba tunakwenda kudumiza kilimo na uchumi wao wa vijana wa Geita? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba atambue bangi ni dawa za kulevya, ni katika dawa za kulevya na adhabu zake zote kwa mujibu wa sheria tulizotunga hapa nchini, inaunganishwa kwa pamoja na koka, heroin inaunganishwa pamoja na dawa nyingine zote za jamii ya opium na kwa msingi huo sisi kama nchi ambao tumesaini mkataba wa dawa za kulevya wa mwaka 1961, tumetunga sheria ambazo zinakataza matumizi ya bangi katika nchi yetu. Na kwa msingi huo sasa, hii anayoisema kwamba kuna makabila yanatumia bangi kwa asili kama chakula, kama mboga ni jambo ambalo sisi kama Serikali hatulitambui na ni jambo ambalo sisi kama Serikali tunasema ni kitendo cha uhalifu na watu hawa wakibainika kutumia majani ya bangi, ama maua ya bangi, ama magome ya bangi watachukuliwa hatua za kisheria. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kwamba bangi inaongeza nguvu, pamoja na Mheshimiwa Musukuma kumkana lakini naomba nilijibu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwamba bangi haiongezi nguvu kwa sababu bangi katika mwili wa binadamu inapoingia na kuwa metabolized, inavunjwa vunjwa kwenda kwenye kemikali zaidi ya 500 na katika hizo kemikali 500, kemikali 113 ni sumu kwa mwili wa binadamu zilizo kali zaidi na kwa wingi zaidi kwenye bangi ni pamoja na hiyo niliyoitaja wakati wa jibu langu la msingi inayoitwa THC au tetrahydrocannabinol lakini zipo CBD na zipo CBG na zipo CBE zote hizi kemikali ni hatari sana kwa afya ya akili na mtu akivuta hivi kemikali nilizozitaja 113 kwanza anadhoofu mwili wake, anakuwa na uchovu, kwa maana ya kupata refuge, lakini pili anachanganyikiwa kwa muda mfupi na kama hujawahi kuona mtu ambaye amepata kichaa cha ghafla, basi baada ya kujibu swali hili njoo uniulize nitakupa historia ya kijana mmoja ambaye tulisoma naye Kigoma secondary school, ambaye alijaribu kuonja bangi akiwa kidato cha tatu na alianza kuona barabara ikinyenyuka hivi, na kwa hiyo alikuwa akitembea kwa kunyanyua miguu kama mtu anayepanda ngazi. (Kicheko)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kusema kwamba bangi ambayo inadhoofisha mwili, inaongeza nguvu hilo nalikubali kisayansi.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, wakati Naibu Waziri anajibu alielezea ni jinsi gani moshi wa bangi unamuathiri si tu mtumiaji bali hata watu wa pembeni.
Mheshimiwa Spika, tumekuwa tukiona wakati Serikali inafanya operation ya kukata au kuzuia bangi, inavuna yale mabangi yaliyokwisha komaa, na wanaenda wanachoma zile bangi, sasa Naibu Waziri atueleze ni kwa kiasi gani Jeshi la Polisi wameweza kuathirika na ile bangi na je, hawaoni kwamba zile bangi zinawaathiri ndio maana wanatenda kinyume na wajibu wao wanavyowatakiwa kufanya?(Makofi/ Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwamba kwanza sio jambo la mzaha kuzungumzia masuala yanayohusu dawa za kulevya, kwa sababu zinaathiri vijana wetu, zinaharibu umakini na utimamu wa nguvu kazi ya Taifa letu.
Kwa hiyo, kujibu swali lake sasa ni kwamba wanapoenda kuchoma huwa wanakuwa wamejifunika vifaa maalum na hata kama hawajajifunika vifaa maalum, wakati wanateketeza bangi wakawa passive smoker wa cannabis bado ile bangi ikiingia kwenye mwili wao itakuwa catabolized na kupotea ndani ya miili yao ndani ya siku 30 kwa sababu metabolism ya bangi inadumu ndani ya mwili ndani ya siku 30 baada ya hapo inaisha kabisa inakuwa imekuwa katika form nyingine ya salt inatoka pamoja na mkojo.(Kicheko)
Mheshimiwa Spika, kwa hivyo hata kama wataathirika lakini madhara yake hayatakuwa ni ya kudumu unless huyo mtu atumie bangi leo, iingie kwenye damu atumie na kesho na kesho kutwa na mwezi ujao awe chronic smoker wa cannabis hapo anaweza akapata madhara. (Kicheko)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini Waheshimiwa Wabunge ambao wanashughulikia tatizo hili la kupambana na dawa za kulevya wanakumbuka, Mamlaka ya Udhibiti wa Matumizi ya Dawa za Kulevya, mara kadhaa imeenda kwenye kamati hiyo kuelezea matumizi ya sheria na kanuni zilizotungwa chini Ofisi ya Waziri Mkuu, ambazo pia zinaongoza utaratibu mzima wa kuteketeza dawa hizi za kulevya katika maeneo mbalimbali.
Mheshimiwa Spika, unapoona vikosi vile vinafanya
kazi ya uteketezaji wa bangi ziko technics ambazo wanazitumia katika kufanya kazi ya uteketezaji ikiwemo wakati wa uteketezaji pia, wanazingatia uelekeo wa upepo na uelekeo wa hewa. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa Wajumbe wa Kamati wanaelewa jambo hilo wanazingatia kwa mfano uelekeo wa upepo na maandalizi mengine ya aina ya matumizi ya vyombo vya uteketezaji ikiwepo aina ya moto utakaotumika katika uteketezaji na aina ya mafuta yatayotumika katika uteketezaji.
Kwa hiyo, naomba niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge si kweli kabisa na naomba Bunge lako liondoke hapa likijua kwamba si kweli eti kukitokea tatizo ndani ya Jeshi la Polisi ni kwa sababu wameshiriki katika kuteketeza bangi, na hivyo wameathirika na matumizi ya bangi, ninaomba hilo tuliweke wazi, kikosi kazi kimefundishwa vizuri, polisi wetu ni waadilifu na wanapofanya kazi ile wanafanya kitaalam na kwa kutumia uadilifu mkubwa na kwa kufuata utaratibu.(Makofi)
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii na nashukuru kwamba Serikali imetambua umuhimu wa Hospitali ya KCMC, na niseme tu kwamba hospitali hii ni ya rufaa na inahudumia zaidi ya watu milioni moja wa Kanda ya Kaskazini.
Mheshimiwa Spika, lakini kwa masikitiko makubwa sana hospitali hii iliomba Serikali zaidi ya shilingi bilioni nne mwaka jana kwa ajili ya huduma za cancer ambazo hospitali ile inaanza kuzitoa, lakini mpaka tunafika Machi bado Serikali ilikuwa haijatoa na Mheshimiwa Naibu Waziri mimi kama Mjumbe wa Kamati nalitambua hilo. Lakini je, ni lini sasa Serikali itatoa fedha hizo ili hospitali ile iweze kuwahudumia wananchi wa Kanda ya Kaskazini kutoka Singida mpaka Arusha na Tanga?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba mnafanya kazi na TAMISEMI ili kuhakikisha kwamba zile Hospitali za Rufaa za Mikoa kama vile Mawenzi na Mount Meru ziweze kutoa huduma ili kupunguza idadi kubwa ya watu wanaoenda Hospitali ya KCMC, lakini hapa ninavyoongea Hospitali ya Mawenzi Mkoa wa Kilimanjaro na Hospitali ya Mount Meru ziko katika hali mbaya sana, jamboambalo linafanya wagonjwa katika hospitali hizo waendelee kwenda KCMC hospitali ambayo pia Wizara bado imeshindwa kuipatia vifaa tiba kamaambavyo wameomba. Je, sasa mna mpango gani kuhakikisha kwamba hospitali hizi za Mikoa ya Mawenzi na Mount Meru zinakarabatiwa majengo yake na kutoa vifaa tiba pamoja na kuweka watumishi hasa ikizingatiwa kwamba watumishi wengi wa afya…
Mheshimiwa Spika, watumishi wengi wa afya wamekumbwa na tatizo la vyeti fake na kwa maana hiyo wameondolewa, je, Serikali ina mkakati gani sasa? ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpe pole na nimtie moyo kwamba asisikitike sana kuhusiana na hali ya Hospitali ya KCMC, mimi binafsi toka nimeteuliwa nimeshafika pale takribani mara tatu na hivyo ninafahamu vizuri sana namna ambavyo hospitali ile inatoa huduma zake na ina madaktari mahiri sana vijana wakiwemo marafiki zangu kina Kajiru, kina Urassa ambao ni mabingwa waliobobea. Tumewapeleka pale sisi kutoka Wizara ya Afya na wamekubali kukaa pale kwenye Kanda yetu ya Kaskazini kutoa huduma kwa Watanzania wenzetu wa eneo lile na nadhani angepongeza kwa jitihada hizo ambazo tumezifanya.
Mheshimiwa Spika, pili, kwamba lini tutapeleka fedha. Tutapeleka fedha pindi ambapo uwezo wa Serikali wa kufanya hivyo utakapohimili, lakini kwa sasa naomba atambue tu azma yetu ya kutenga shilingi milioni 500 ili kuchangia katika kukamilisha mradi wa kujenga bankers kwa ajili ya kufunga mashine za mionzi na naomba nimfahamishe kwambamradi ule wa kujenga bankers kwa ajili ya kutoa tiba ya mionzi sio wa Serikali peke yake wala sio wa KCMC peke yake tunaufanyakwa ubia na wadau wa maendeleo ambao tayari wamashajitolea baadhi ya vifaa kwa ajili ya kutekeleza mradi ule. Kwa hiyo, sisi kama Serikali lakini wenzetu wa KCMC tutashirikiana na huyo mdau kuhakikisha mradi ule unakamilika na sisi mchango wetu ni hizo shilingi milioni 500 ambazo tumeziweka kwenye bajeti.
Swali la pili, kwamba hospitali ya Mawenzi na Mount Meru ziko katika hali mbaya sana, si kweli ninaomba tuwe tunatumia maneno ambayo yanatia moyo wananchi kwa sababu hospitali hizi nimezitembelea zaidi ya mara mbili zote hizi na ninafahamu miradi mikubwa inayofanyika katika hospitali hizi. Na niwapongeze wenzetu wa TAMISEMI na wadau wa maendeleo ambao wametoa misaada mikubwa katika kuboresha eneo la maabara na eneo la huduma za mionzi na kwa kweli kwa pale Mawenzi kuna theatre nzuri sana ya kimataifa, zipo theatre karibu nne pale ndani na zote zinafanya kazi na ni za kisasa kabisa na ninadhani labda Mheshimiwa Mbunge uende ukatembelee maabara ya Mawenzi pamoja na theatre ili uone jinsi hospitali ile ilivyo katika hali nzuri kuliko unavyosema wewe. Nitoe rai kwa wananchi waendelee kuamini huduma bora zinazotolewa na hospitali zetu za Mawenzi, Mount Meru na hospitali ya KCMC.
MHE. MAULID S.A MTULIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. La kwanza, naungana naye katika umuhimu wa watu wetu kuchangia gharama, lakini anaonaje sasa Serikali dhana ya kuchangia gharama ikabaki katika kuchangia dawa pamoja na vipimo lakini wananchi wetu wakapata fursa ya kwenda kumwona Daktari bila kulipa pesa ya kumwona Daktari ili kuongeza idadi ya watu wanaokwenda kwenye vituo vya afya?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa kuna makundi yetu maalum ambayo kwa mujibu wa sheria yetu wanatakiwa wapate huduma za afya bure na kwa kuwa Wabunge wengi wamesimama hapa na mimi mmojawapo tunaonesha kwamba bado makundi haya hayapatiwi huduma ya afya bure. Je, Mheshimiwa Waziri atakuwa yuko tayari sasa kufuatana na mimi kwenda katika hospitali zangu za Jimbo la Kinondoni kwenda kusisitiza na kuhakikisha wananchi hawa wanapata huduma bure?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Swali lake la kwanza kuhusu wananchi kupewa ruhusa ya kwenda kununua dawa na vifaa tiba katika hospitali lakini wakaonwa bure na Madaktari, sisi kama Serikali hatuna utaratibu huo kwa sababu tunafanya kazi kwa mujibu wa sera lakini pia mipango mbalimbali ya kimkakati ya kuhudumia wananchi.
Mheshimiwa Spika, tunafuata Sera ya Afya ya mwaka 2007 pia Mpango wa Kimkakati wa Huduma za Afya Na.4 ambao unaanza 2015 - 2020. Pamoja na mikakati mbalimbali kama Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa na yote haizungumzii uelekeo huo.
Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, mwongozo ambao tunaufuata sisi kama Serikali ni kuwahudumia wananchi zaidi kwa kutazama mipango hiyo na uelekeo wetu kwenye mipango yote hii ni kuelekea kwenye universal health coverage ambapo kutakuwa kuna bima ya lazima ya kila Mtanzania. Tukianza kutekeleza mpango huo kama Bunge lako Tukufu litatupitishia sheria ambayo tunakusudia kuileta muda si mrefu basi kila Mtanzania atalazimika kuwa na kadi ya bima ya afya ya namna moja ama nyingine iwe ni CHF ama iwe ni Social Health Insurance kama NHIF.
Mheshimiwa Spika, kila Mtanzania akishakuwa na hiyo kadi yake maana yake sasa atakuwa anatibiwa kwa kutumia kadi ya bima ya afya. Huo ndiyo uelekeo na sio uelekeo anaouzungumzia Mheshimiwa Mtulia. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusu makundi maalum, hata hili suala la makundi maalum kuhudumiwa chini ya kiwango japokuwa tunalikubali, lakini dawa yake hasa ni huu mfumo wa kuwa na bima ya afya ya lazima kwa kila Mtanzanzia ambapo yale makundi maalum ambayo yanapewa msamaha kisera maana yake yatakuwa yanakatiwa bima kabla hayajaenda kutafuta huduma.
Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, wazee wote ambao wanastahili kupewa msamaha wa kupata huduma za afya basi wanakatiwa kadi za bima ya afya na Serikali kwa sababu wao wanapewa msamaha anapokwenda pale kutibiwa huwezi kubagua yupi ana kadi na yupi hana kadi, kila mtu ana kadi. Yupi kadi yake ni ya msamaha na yupi kadi yake ni ya kulipia, kila mtu atakuwa ana kadi na kila kadi itaheshimiwa na kituo chochote kile cha kutolea huduma za afya.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa msingi huo hata haya makundi maalum anayoyazungumzia yatapata huduma zilizo bora. Kwenye Ilani ya Uchaguzi kwa kuwa tunaelekezwa kufanya hivyo, namhakikishia miaka hii mitano haitakwisha kabla hatujaleta hapa Bungeni mapendekezo yetu ya Sheria ya Single National Health Insurance ambayo ni compulsory kwa kila Mtanzania.
Mheshimiwa Spika, kuhusu kufuatana naye, anajua yeye ni rafiki yangu halina shida, tutafute muda twende Kinondoni tukatembelee, japokuwa mimi nimeshafika Kinondoni mara nyingi sana. Ahsante.
MHE. HAMIDU H. BOBALI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Sera ya Taifa ya Wazee ya mwaka 2003 miongoni mwa privilege ambayo inawapa wazee ni kutibiwa bure lakini hivi sasa imekuwa kama ni uamuzi wa Daktari wa Kituo cha Afya husika ambaye anakuwepo pale. Kwa hiyo, mara nyingi wazee wamekuwa wakinyanyaswa kutokana na kukosekana kwa sheria. Mheshimiwa Waziri anatuthibitishia kwamba ni lini atatuletea Sheria ya Wazee ili kwenda sambamba na Sera ya Wazee ili wazee wetu waweze kutibiwa isiwe sasa ni privilege au maamuzi ya Daktari katika kituo husika?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ni lini tutaleta mapendekezo ya kutungwa kwa Sheria ya Wazee kwenye Bunge lako Tukufu, hatuna uhakika ni lini exactly, lakini tutaleta sheria hiyo. Hata hivyo, mpaka sasa kuna mchakato unaendelea ndani ya Serikali na pindi tutakapopata idhini ya Baraza la Mawaziri ya kuleta sheria hiyo hapa Bungeni basi itafika. Kwa sasa tuna mchakato ndani ya Serikali, sheria hii ni muhimu.
Mheshimiwa Spika, pamoja na kutokuwa na sheria hii, tayari tumeshaanza kutekeleza afua mbalimbali ambazo zinawahusu wazee hususan kwenye sekta ya afya. Kwa mfano, tuna mkakati niliusema hapa wiki iliyopita wakati nikijibu maswali wa ‘Mzee Kwanza, Mpishe Mzee Apite’ ambao tumeu--roll out nchi nzima na mkakati huu wazee wameupenda na wameufurahia sana.
Mheshimiwa Spika, pia tumetoa mwongozo kwa kila Halmashauri nchini kuhakikisha zinawakatia kadi za CHF wazee wote ili waweze kupata huduma za afya kwenye vituo vyao. Tunachokifanya sisi ni kufanya maboresho ya huu Mfuko wa Afya ya Jamii yaani CHF ili uwe na value zaidi, uweze kumsaidia mtu kupata huduma palepale kwenye zahanati yake kijijini ama kwenye kituo cha afya na kuzunguka mkoa mzima yaani awe anapata referral kwa kutumia kadi ya CHF.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama Halmashauri zita-comply kutekeleza mapendekezo yetu ya kuwa na kadi ya CHF kwa wazee wote ambao wanastahili kupewa kadi hizo za msamaha kwenye Halmashauri zao maana yake katika miaka hii miwili huduma za afya kwa wazee zitaboreka sana.
MHE. MARTHA J. UMBULLA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwanza nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake ya jumla kuhusu swali hili. Pamoja na hayo nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa takwimu za vifo vya akinamama vinavyotokana na uzazi katika Mkoa wa Manyara vinaongezeka mwaka hadi mwaka. Kwa mfano, mwaka 2015 tulikuwa na vifo 38, mwaka 2016 vifo 49 na nusu mwaka tu ya 2017 tayari vifo 23.
Kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri katika majibu yake amesema wameanzisha Benki ya Damu katika Mikoa ya Geita, Simiyu, Mara na Kigoma na sijasikia Mkoa wa Manyara; na kwa kuwa pia amesema wamejengea uwezo Wahudumu wa Afya nchi nzima bila kutaja Manyara. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri atakubaliana nami kwenda katika Mkoa Manyara kuangalia hali hii ikoje ili kupatia ufumbuzi wa haraka janga hili katika mkoa wetu?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa vifo vingi
vya watoto wachanga vinatokana na kukosa na huduma upasuaji na huduma ya damu kwa ajili ya akinamama wajawazito; na kwa kuwa pia amesema kwamba wamewezesha vituo 159 nchi nzima bila kutaja katika hivyo 159 vingapi vipo Manyara na katika vituo vya afya 106 vilivyojengewa uwezo kwa njia ya mafunzo hajataja Manyara. Je, anaweza akaniambia kwamba hali ikoje katika kuwezesha vituo vya upasuaji katika mkoa wetu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mama yangu mpendwa, Mheshimiwa Martha Umbulla kwa kufuatilia kwa ukaribu sana mambo yanayohusu Sekta ya Afya kwa Mkoa wa Manyara hususani mambo yanayohusu wanawake na watoto kwenye mkoa wake. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza, halikuwa
swali per se, nikubaliane naye niko tayari kwenda Manyara wakati wowote atakapoona inafaa. Nimkumbushe tu kwamba toka nimeteuliwa kuwa Naibu Waziri nimeshafika Mkoa wa Manyara zaidi ya mara tatu na nimefika mpaka anapokaa yeye, jirani na nyumba anayoishi pale Dongobesh.
Mheshimiwa Spika, bahati mbaya yeye hakuwepo
lakini nimefika mpaka Dongobesh, nimefika mpaka kwenye kituo cha afya ambacho yeye Mbunge wa Viti Maalum na rafiki yangu Mheshimiwa Flatei Massay wanajenga na nikawapongeza sana kwa jitihada wanazofanya za kujenga kituo kile cha afya na kuleta hizi huduma za upasuaji karibu zaidi na wananchi wa Dongobesh. Niwashukuru kwa kunipa Uchifu wa pale Dongobesh na kunivalisha yale mavazi yenu ya kimila. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nilipofika pale niliguswa na nikajitolea mimi mwenyewe bati 100 kwa ajili ya kuwasaidia kwenye jitihada hizo. Kwa hivyo, akiniambia specifically nitaje vingapi, sikumbuki ni vingapi tulivyonavyo pale, lakini nafahamu Mkoa wa Manyara wanafanya jitihada kubwa sana za kuboresha huduma za Mama na Mtoto hususani kwa kupandisha hadhi zahanati zao kwenda kwenye vituo vya afya na mimi mwenyewe nimefika pale nikashuhudia mradi wao huu wa pale Dongobesh.
Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo, niruhusu tu nifanye utafiti nitampa majibu ya statistics anazozitaka baadaye kwamba ni vituo vingapi hasa. Hata hivyo, azingatie agizo ambalo nililitoa mimi mwenyewe nikiwa Mwandoya kwa Mheshimiwa Mpina, ambapo nilisema kwamba, Halmashauri zote nchini wahakikishe wanapandisha hadhi vituo vyao vya afya ambavyo vilikuwa havitoi huduma za upasuaji sasa vianze kutoa huduma za upasuaji wa kumtoa mtoto tumboni. Hii ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuna damu salama na kuna huduma za uchunguzi wa magonjwa katika ngazi ya kituo cha afya.
Mheshimiwa Spika, nilisema pia kwamba kama kuna kituo ambacho kitakuwa hakijakidhi matakwa haya ya sera, maana yake tutakishusha hadhi kiende kuwa zahanati badala ya kukiita kituo cha afya jina tu wakati hakitoi huduma za kituo cha afya. Nilitoa miezi sita ambayo inakwisha sasa hivi. Miezi hii mitatu inayofuata, natuma timu yangu ya wataalam kwenda kukagua kwamba ni Halmashauri zipi zimetekeleza agizo lile, agizo la Mwandoya. Ma– DMO, Wakurugenzi na Wakuu wa Wilaya wote nchini wanajua.
Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, kituo ambacho kitakuwa hakijakidhi hayo masharti, nitakishusha hadhi. Kwenye lile agizo langu nilisema nitapeleka taarifa yangu kwa Mheshimiwa Rais mwenyewe kwamba hawa ndiyo wateule wake ambao wanakubaliana na vifo vya akinamama wajawazito kwa sababu hawataki kutekeleza agizo ambalo lingeokoa maisha yao. Nina uhakika Mheshimiwa Rais atachukua hatua. Nimejibu kwa upana ili kuwakumbusha.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusu upasuaji, kwa sehemu nimelijibu. Kuhusu damu salama, kwa Mkoa wa Manyara kwa ujumla wake kwenye bajeti hii inayokuja, tumeweka kama Mkoa wa kipaumbele kwa ajili ya kuanzisha Benki Salama ile kubwa.
Mheshimiwa Spika, nilipofika pale Manyara miezi sita iliyopita nilihakikisha wana damu ya kutosha, lakini niliona kuna RMO pale alikuwa anasinziasinzia hivi kutekeleza mpango huu, tulishauriana na wenzetu wa TAMISEMI na tulikwishamtoa.
MHE. HALIMA A. MOHAMMED: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba, je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba kwa kila Hospitali ya Halmashauri kunakuwepo huduma nzuri za watoto njiti kuliko ilivyo hivi sasa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mkakati tulionao kama Serikali tumetoa mwongozo sisi kama Wizara ya Afya, ambao unazitaka Halmashauri zote ambazo zinamiliki Hospitali za Wilaya kuhakikisha wana chumba maalum kwa ajili ya watoto njiti lakini pia wana chumba maalum kwa ajili ya Kangaroo Mother Care ambayo ni njia ya kisasa ya kuwalea watoto wachanga ambao wamezaliwa chini ya umri.
Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, mkakati ndio huo sasa Halmashauri kutekeleza hilo ni jambo lingine, lakini agizo letu kama Serikali ni kuzitaka Halmashauri zote kuhakikisha zinafuata mwongozo wa kuanzisha huduma za njiti katika hospitali zao.
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Spika, ahsante.
Kwa kuwa wanawake wanaoishi katika Manispaa ya Singida na maeneo yanayozunguka Manispaa hiyo wamekuwa wakipata huduma kwenye Hospitali ya Mkoa pamoja na Sokoine lakini idadi yao ni kubwa kiasi kwamba inawazidi wale watoa huduma hali kukiwa na Hospitali ya Rufaa ambayo imeshajengwa tayari lakini bado Wizara haijaleta huduma yoyote kuboresha pale ili huduma zianze na kuokoa maisha ya wanawake wengi. Ni lini sasa Serikali italeta huduma kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida ili kuokoa maisha ya wanawake? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nimpongeze yeye lakini pia nimpongeze RMO wa Singida rafiki yangu Dkt. Mwombeki kwa jitihada mbalimbali ambazo wanazifanya kuboresha huduma za wana Singida. Wamekuwa wakifanya mikakati mbalimbali ikiwemo kujenga hiyo Hospitali ya Rufaa mpya, nzuri na ya kisasa kabisa.
Mheshimiwa Spika, pia wamekuwa mkoa wa kwanza kuanzisha huduma za outreach, huduma za kuwafuata wananchi na kuwapa huduma za kibingwa kwenye vijiji vyote. Naona Mheshimiwa Spika sasa hivi hata hapa mkoani kwako zimefika na juzi zilikuwa pale Kongwa lakini waanzilishi ni Mkoa wa Singida. Niwaombe Wabunge wote wa-support mpango huu, wawasiliane na RMO wa Mkoa wa Dodoma ili waone ni namna gani wanaweza wakazipeleka hizi huduma kwenye mikoa yao.(Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya bashirafu hiyo, jibu langu ni kwamba tayari huduma zimeshaanza kwenye Hospitali ya Rufaa anayoizungumzia lakini tunakwenda kwa awamu. Katika hatua ya kwanza tumeanza kutoa huduma za outpatient lakini kadri tunavyoendelea kuboresha huduma na kupata pesa za kuweza kuijengea uwezo hospitali ile, ndivyo tunapanda ngazi na kuongeza huduma moja baada ya nyingine.
Mheshimiwa Spika, kuanzisha hospitali siyo jambo dogo, linataka muda, rasilimali na hatutaki kukurupuka kwa sababu tunataka tuitendee haki hospitali ile nzuri ambayo imejengwa chini ya usimamizi wa RC aliyekuwepo Mheshimiwa Parseko Kone. Ahsante.
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri anasema alishatuma wataalam wake toka katika Ofisi ya Mganga Mkuu wa Mkoa wa Pwani, kwenda katika Kituo cha Kibiti, ili watoe maelekezo sasa namna ya kutoa huduma kwa ngazi ya Hospitali ya Wilaya. Swali langu nataka kujua sasa ceiling ya kituo hicho imekuwaje, ni kwamba, tumeongezewa mgawo wa fedha wa uendeshaji ili ufanane na hadhi ya ngazi ya Hospitali ya Wilaya?
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali langu la pili; atakubaliana Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba, kutambulika kituo cha afya kuwa Hopsitali ya Wilaya kunasababisha kuongezeka mgawo wa fedha na ukomo wa bajeti. Hadi hivi tunavyozungumza Kituo cha Afya Kibiti kina changamoto kubwa ya ukosefu wa vifaa tiba muhimu kama X-Ray Machine na Ultra Sound. Nataka kujua sasa ni upi mkakati wa Serikali kuhakikisha tunapatiwa vifaa hivyo muhimu, ili kuimarisha afya ya wana-Kibiti? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma, binti yangu, kwa jitihada kubwa anayoifanya ya kupigania afya za wananchi wa Mkoa wa Pwani kwa ujumla. Kwa pamoja naomba nijibu swali lake la kwanza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa bado hatujapandisha hadhi Kituo cha Afya Kibiti kuwa Hospitali ya Wilaya na kwa msingi huo bado hatujaanza kuwapelekea mgawo wa fedha ambao unaendana na mgao ambao vituo vya kutolea huduma za afya vilivyo katika ngazi ya hospitali ya wilaya vinapata kwa hivyo mgawo wao bado ni wa kituo cha afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo nakubaliana na yeye kwamba, kama kituo cha kutolea huduma za afya kikipanda ngazi kutoka ngazi ya kituo cha afya kwenda kwenye ngazi ya hospitali ya wilaya ni wazi mgawo wa fedha utaongezeka, bajeti yake itaongezeka, idadi ya watumishi itaongezeka, lakini pia idadi ya vifaa tiba vya kufanyia uchunguzi wa magonjwa pia, itaongezeka ili kuendana na huduma zinazopaswa kutolewa katika ngazi husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kuhusu changamoto ya vifaa tiba, naomba nimtaarifu Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba changamoto hii tunaifahamu na ni kati ya changamoto kubwa tatu kwenye sekta ya afya nchini na mkakati wetu kama Serikali kwa sasa ni kutekeleza mradi unaojulikana kama ORIO ambapo tuko katika hatua za mwisho za kufanya utekelezaji wa mradi husika mkandarasi amekwishapatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, tutakapoanza tunakusudia kupeleka vifaa tiba kama Ultrasound, X-Ray Machines, CT Scans na vifaa tiba vingine mbalimbali kwenye hospitali nyingi nchini ambazo zipo katika ngazi tofauti tofauti; ngazi ya hospitali za rufaa za mikoa, ngazi ya hospitali za wilaya, lakini pia ngazi ya vituo vya afya. Kwa hivyo kwa sasa hivi sina kumbukumbu sahihi kama Kituo cha Afya Kibiti, kipo katika mgawo husika, lakini nitafutilia na nitampa taarifa.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza natangaza interest kwenye suala hili, binafsi. Pili, si kila anayetetea matetemeko ya ardhi kama nyumba yake imeanguka, la hasha; hapa kwenye meza yangu nina memo chungu nzima za Waheshimiwa Wabunge akiwemo Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mheshimiwa Selasini, Waheshimiwa wote wakielezea shida ya jambo hili. Kwa hivyo nikuombe pamoja na uchache wa muda uwape nafasi wenzangu, ili nao wajichawanye kwenye jambo hili. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali, hivi sasa kuna utitiri wa matangazo ya biashara ya dawa za kuongeza nguvu za kiume. Kuna matangazo mengi yanayosambaa nchini kutangaza dawa zinazosaidia tatizo hili, jambo ambalo linaashiria ukubwa wa jambo hili. Sasa, je, Wizara inachukua hatua gani, kwa sababu, utumiaji wa dawa kiholela unazidisha matatizo ya maradhi?
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kabila moja kila unayekutana naye huko njiani anauza dawa hizi, sijui vipimo hivi wanavipata wapi? Kwa hivyo naomba Wizara itoe tahadhari na kuchukua hatua juu ya dawa za tatizo hili ambazo zinasambaa kila siku ndani ya nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tendo la raha linahitaji furaha, na kuna taasisi ya World Happiness Report imeeleza kwamba Tanzania ni miongoni mwa nchi 10 duniani wananchi wake waliopoteza furaha. Je, Serikali miaka 50 ya Uhuru kwa nini bado nchi yetu bado iko kwenye nafasi ya 10 mwisho duniani kwa kupoteza furaha, mmekosea wapi? (Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kukubaliana na Mheshimiwa Khatib Said Haji, kwamba kwa hakika tendo la raha linahitaji furaha. Pia kwa msingi huo changamoto zinazowapata wanaume wa kisasa kwenye tendo hili zinatokana kwa kiasi kikubwa na ukosefu wa furaha, msongo, lakini pia mwongezeko mkubwa wa magonjwa yasiyo ya kuambikiza.
Mheshimiwa Naibu Spika, hizi ni sababu kubwa kuliko sababu nyingine yoyote, kwamba, ukiwa na stress, ukiwa na anxiety, ukiwa na uchovu wa kupitiliza kwa hakika huwezi kuwa na ile furaha na ile hamasa ya kushiriki tendo la ndoa ipasavyo na hii ni sababu mojawapo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana ashangaa sana watu ambao wanahangaika sana kutafuta dawa za kuongeza nguvu za kiume kwa hayo makabila aliyoyasema ambayo yamekuwa yakizunguka na ku-take advantage ya changamoto hii ambayo inawakumba wanaume wengi hapa nchini kwa sasa kwa sababu pengine hawajui tu changamoto hii inasababishwa na nini.
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto hii kwanza ni physical, ni changamoto ya kimwili. Kwa hivyo, lazima uwe na afya njema, uwe huna magonjwa, lakini pia hutumii madawa kwa muda mrefu, madawa ambayo yanaweza yakasababisha kupunguza nguvu za kiume, si dawa zote, lakini pia uwe umetulia, uwe una furaha, una amani kwenye moyo wako. Sasa huwezi kuipata hiyo raha unayoisema kama huna hiyo furaha kwa hiyo, nakubaliana na wewe Mheshimiwa Khatib Said Haji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, naomba nitumie jukwaa lako hili kutoa hamasa kwa mara nyingine tena kwa wanaume wote nchini na kwa wanawake vilevile kushiriki kwa kiasi kikubwa kwenye mambo yanayoendana na kulinda afya zetu. Kufanya mazoezi, kula vizuri, kupumzika, lakini pia kufurahi, kucheka, kushirikiana na wenzako, ili kuondoa msongo wa mawazo kwa sababu, msongo wa mawazo, sonono, wasiwasi, ni katika mambo makubwa sana yanayosababisha watu wapate erectile disfunction lakini pia hata wakose watoto wengine, kushika mimba inakuwa ngumu kwa hivyo, naomba nitumie fursa hii kutoa wito huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusiana na utitiri wa matangazo ya dawa za kuongeza nguvu za kiume, Mheshimiwa Waziri wa Afya yuko hapa na amekusikia. Ataamua kutupa mwongozo kama tutoe tamko ama tusitoe tamko, lakini kwa sasa nimetoa hayo maelezo. Niwahamasishe watu tule vizuri, tulale vya kutosha, tufanye mazoezi na naamini kwa kiasi kikubwa tutaepukana na changamoto hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na furaha, kwamba, Tanzania imekuwa miongoni mwa nchi ambazo hazina furaha kwa kiasi kikubwa, sina uhakika na taarifa hiyo kwa sababu, sijaisoma, lakini ukweli ni kwamba, furaha inahusiana na vitu vingi sana katika nchi. Kuna nchi nyingine kwenye katiba zao wameweka kwamba, pursuit of happiness, kuitafuta furaha, ni katika malengo makubwa katika nchi hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, na sisi ningependa sana tuwe ni wananchi ambao tunapenda kuitafuta furaha kwa kushiriki kufanya kazi za kujiletea kipato, kupunguza stress, kupunguza umaskini, lakini pia kwa kufanya maboresho kwenye sekta ya afya, ili watu ambao watajikuta kwa bahati mbaya wamepata magonjwa, basi waweze kutibiwa vizuri, waweze kupona, warudi kuwa na furaha kama ambapo hawakuwa na magonjwa. Kwa hiyo, ni mambo mengi yanayohusika, mambo ya umaskini, mambo ya afya, mambo ya kijamii, mahusiano na watu, yote haya yanahusiana na furaha kwenye nchi. Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Nikijibu sehemu ya pili ya swali la kaka yangu, Mheshimiwa Khatibu Kai Haji, Mbunge wa Konde; tuna Sheria ya Tiba Asili na Tiba Mbadala ya Mwaka 2002 na kanuni zake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa sheria hizo dawa zote za tiba asili au tiba mbadala ni lazima zisajiliwe na Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala baada ya kuwa zimethibitishwa na Mkemia Mkuu wa Serikali pamoja na TFDA kwamba hazina madhara.
Mheshimiwa Naibu Spika, tamko langu kwa nchi, yeyote anayeuza dawa za tiba asili ambazo hazijasajiliwa anavunja sheria; tutamkamata na tutamchukulia hatua, ikiwemo dawa za kuongeza nguvu za kiume. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ndiyo kauli ya Serikali, wanaofanya hivyo wanafanya kinyume na sheria. Naomba kutumia Bunge lako Tukufu niwatake Waganga Wakuu wa Mikoa na Wilaya kuwachukulia hatua wote wanaouza dawa za kuongeza nguvu za kiume ambazo hazijasajiliwa na Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. ANNA J. GIDARYA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Waziri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo. Kwanza, Mheshimiwa Waziri kwenye majibu yake amesema wameunda madawati 516, pamoja na madawati haya ni idadi ya watoto wangapi waliokufa kwa kukeketwa?
Pili; Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na takwimu zinazoonesha 2016/2017, ni hatua zipi na ni watuhumiwa wangapi ambao wamechukuliwa hatua za kisheria. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya kwanza, kuhusu takwimu za watoto waliokeketwa, mpaka sasa hatuna takwimu halisi za watoto ambao wamekeketwa, kwa sababu kwa kiasi kikubwa vitendo hivi vinafanyika katika zama hizi katika mazingira ya usiri mkubwa kwa sababu Serikali imetoa jicho lake kila kona kwamba vitendo hivi toka tumevi-criminalize kwenye Sheria ya Mtoto mwaka 2006. Mpaka sasa tumekuwa wakali, tumeanzisha hayo madawati, tumetoa mafunzo kwa Polisi na kwa kiasi kikubwa kila mtu sasa amekuwa aware kwamba hili ni tatizo na sio mila tu ambayo tunairuhusu katika nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, vitendo hivi sasa vimehamishwa kutoka utaratibu wa kizamani wa kimila ambapo vilikuwa vinafanyika wazi na kwa sherehe na sasa vinafanyika katika taratibu za usiri. Kwa hivyo imekuwa ngumu kwa kweli kuweza kutengeneza takwimu halisi za namba ya watoto ambao wamekeketwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, ni watu wangapi ambao wamewahi kukamatwa kwa vitendo vya ukeketaji. Mpaka sasa pia sina takwimu halisi mahsusi hasa za kuhusu wakeketaji, kwamba wangapi wamewahi kushtakiwa na wangapi wamewahi kuhukumiwa. Kwa sababu pia toka tumetunga hiyo sheria kama nilivyosema awali hata wale Mangariba ambao walikuwa ni mashuhuri kwa kukeketa nao pia hawakeketi waziwazi na hawakubali pia kukeketa kwa sababu wanajua ni kinyume cha sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tumeona kwa sababu bado vitendo vinaendelea kwa njia za kichini chini ni vema tukatumia njia mbadala za kufanya kazi na Mangariba kwa kuwaelimisha, kuwajengea uwezo lakini pia kuwapa tahadhari kwamba kitendo hiki ni kosa la jinai na kwamba akikutwa anafanya kitendo hicho, yeye, wazazi wa mtoto, ndugu wa mtoto na watu wote ambao wamesherehekea kitendo hiki kifanyike, wanachukuliwa hatua kali za kisheria. Kwa hivyo, hata Mangariba nao wamekuwa wanasita kushiriki kufanya vitendo vya ukeketaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, tumeanza mradi wa kufanya njia mbadala ya kufanya graduation ya watoto kwenda kwenye ujana ambayo inajulikana kama Alternative Rights of Passage (ARP) ambapo tunatumia sasa Viongozi wa Kimila zaidi, hao Mangariba pamoja na Viongozi wa Kimila kama Malaigwanan, Machifu na Watemi kwenye maeneo mbalimbali ili kuwaelimisha kuhusu jambo hili na kuwaambia kwamba mtoto anaweza akahitimu kutoka kwenye utoto kwenda kwenye utu uzima bila kukatwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa msingi huo, anapata mafunzo yote ambayo yanahusu mambo ya kiutu uzima kwa sababu sasa anakua bila kukatwa na tunapata mafanikio makubwa na ndio maana vitendo hivi vimepungua kwa kiasi kikubwa.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, napenda kumuuliza kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla, deni la MSD lilikuwa ni kiasi gani na kiasi gani kimeshalipwa?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, nataka kujua MSD tayari wameshapewa pesa, ni maboresho gani waliofanya kuhakikisha kwamba wananchi wanapata dawa kwa wakati? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza kwa jitihada anazofanya kuzungumzia masuala mbalimbali yanayohusu afya za wananchi wa Mkoa wa Njombe na ndiyo maana amenialika kwenye mkoa wake mara mbili ili kwenda kutatua changamoto zinazowakabili.
Mheshimiwa Naibu Spika, deni la MSD mpaka kufikia mwezi Juni, 2016 lilikuwa linafikia shilingi bilioni 143.4 na uhakiki ulikuwa bado unaendelea. Sehemu kubwa ya deni ilikuwa imehakikiwa na mpaka sasa bado uhakiki wa deni hilo unaendelea kufanywa na wenzetu wa Hazina. Tayari pia hatua mbalimbali za kuanza kulipa deni la MSD zilikwishaanza kuchukuliwa kwa wenzetu wa Wizara ya Fedha kutuletea pesa kwa ajili ya kulipa deni hilo kila baada ya muda wa miezi mitatu. Mpaka sasa tayari deni la MSD limeshapunguzwa kwa takribani shilingi bilioni 12 na linaendelea kuhakikiwa lakini pia kulipwa taratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tuna changamoto moja kwamba kuanzia 2016 - 2017 Juni, kipindi hiki cha mwaka mmoja hapo, deni pia limeongezeka tena kwa shilingi bilioni 11 na ni kwa sababu ya miradi misonge ambapo kwa kiasi kikubwa inafadhiliwa na taasisi mbalimbali za kimataifa ikiwemo Global Fund to Fights Malaria, HIV/AIDS and Tuberculosis. Kwa msingi huo, wanatupa dawa na vifaa tiba lakini tunatakiwa sisi tuingie gharama za ku-clear. Sasa pesa hizi zimekuwa zikichelewa kuja kutoka kwa wenzetu wa Hazina. Kwa hiyo, deni limeendelea tena kuongezeka mpaka kufikia tena shilingi bilioni 144 kufikia Julai, 2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye majibu ya swali ya msingi niliyoyatoa hapa nilieleza maboresho mbalimbali ambayo tumeendelea kuyatekeleza kufuatana na ushauri wa kitaalam tuliopewa na taasisi ya kutoa ushauri ya kimataifa ya Deloitte and Touche na mpaka sasa tunaendelea kufanyia kazi mapendekezo yao 21 ambayo yalitolewa. Kutilia msisitizo tu ni kwamba changamoto kubwa ambazo zilijionesha katika ripoti ile, pamoja na kuwepo changamoto ya deni, magari machache ya kusambaza dawa na mtaji wa MSD kwisha kutokana na madeni kuwa makubwa lakini pia kulikuwa kuna changamoto nyingine ya kukosekana kwa maoteo (quantification) kutoka kwenye Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, haya ni mambo ambayo tumekuwa tukiyaboresha kwa ukaribu sana katika kipindi hiki na sasa upatikanaji wa dawa kwa kweli imekuwa ni suala la kihistoria. Mimi nazunguka sana kwenye vituo vya afya, Hospitali za Wilaya nakuta upatikanaji wa dawa upo kwa zaidi ya asilimia 90 na mpaka sasa wastani umefika asilimia 80. Hakuna mtu atasimama leo hii na kulalamika kwamba kuna upungufu wa dawa kwenye eneo lake. Ukiona imejitokeza hivyo basi ujue DMO ama Mkurugenzi hawafanyi kazi yao ipasavyo na wala siyo suala la MSD ama Serikali Kuu. (Makofi)
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Awali ya yote nianze kuishukuru sana Serikali kwa sababu, swali hili leo ni mara ya nne naliuliza ndani ya Bunge lako.
Mheshimiwa Spika, nitakuwa mwizi wa fadhila nisipoishukuru Serikali kwa kazi kubwa ambayo inaendelea katika Kituo cha Wazee cha Kolandoto. Natumia fursa hii kuishukuru sana na kuipongeza Serikali kwa kazi ambayo wanaifanya, wamesikia kilio cha wananchi na wazee wa Kolandoto.
Mheshimiwa Spika, naomba nimwulize Naibu Waziri swali moja la nyongeza. Kwa kuwa, jengo hili linaonekana litapendeza sana baada ya kukamilika. Je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha wanawapelekea wazee hawa vitanda na magodoro ili waweze kuishi kwa raha mustarehe?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante.
Naona dada yangu Mheshimiwa Azza Hillal Hamad amefurahishwa sana na kazi inayoendelea pale Kolandoto mpaka amekosa swali la nyongeza la kuuliza.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeweza kujenga jengo jipya kubwa na la kisasa ambalo lina miundombinu yote kuanzia miundombinu ya malazi, kila mzee atakuwa na chumba chake, lakini pia kuna ukumbi wa television, kuna ukumbi wa burudani mbalimbali, wazee watakuwa wanapumzika pale, kuna majiko ya kisasa ya gesi, tumewanunulia Bajaj wazee wa Kolandoto na vituo vingine takribani 17 nchi nzima, ili waweze kupelekwa hospitali na kupewa huduma mbalimbali za kusafiri kutoka eneo moja kwenda eneo lingine. Nadhani ndiyo maana Mheshimiwa Azza amekosa swali la kuuliza kwa sababu hatuwezi kushindwa kununua magodoro kama tumeweza kujenga na kuweka vifaa vyote hivyo. (Makofi)
MHE. USSI SALUM PONDEZA AMJAD: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa majibu mazuri ambayo Mheshimiwa Naibu Waziri amenipatia, naomba kuulizwa swali, je, haoni sababu ya majibu ya vipimo kutoka Zanzibar ambako amesema huwa yanachukuwa muda mrefu kutokana na umbali yanapotoka. Lakini Zanzibar na Tanzania Bara, Dar es Salaam ambapo anapatikana Mkemia Mkuu kwa sasa hivi hakuna umbali, ni dakika 20 mpaka nusu saa inaweza kufika.Je, haoni kutoa kipaumbele kwa vipimo ambavyo vinatoka Zanzibar kupewa majibu ya haraka, kwa sababu watu wamekuwa wakipata matatizo ya kusubiri muda mrefu huku wengine wanakuwa wapo katika magereza kwa kusubiria criminal cases zao ziweze kupatiwa majibu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, tunaona kuna haja ya kutoa kipaumbele kwa sampuli za makosa ya jinai zinazotokea Zanzibar lakini ni ngumu sana kutoa kipaumbele kwa msingi huo kwa sababu kama ni kesi za jinai zipo nchi nzima na watu wa kila kona ya nchi hii wana haki ya kupata haki ya kusikilizwa kwenye mahakama zetu kwa wakati bila kucheleweshwa. Tunachokifanya kama Serikali kwa sasa, ili kupunguza ucheleweshwaji, ni kuongeza idadi ya mashine za kupima vinasaba ili kwa ujumla wake kupunguza ucheleweshwaji kwa sampuli zote kutoka kila kona ya nchi yetu, Zanzibar ikiwemo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka huu wa fedha, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, tumetenga bajeti ya kununua mashine tatu mpya za vinasaba lakini pia tunaanzisha kituo cha kupima vinasaba pale Mbeya ambacho pia kitatusaidia kupunguza wingi wa case files kutoka kwenye Kanda ya Nyanda za Juu Kusini pamoja na Kanda ya Kati ambazo zinaweza zikatumia huduma za maabara itakayokuwepo pale Mbeya badala ya kutumia maabara moja iliyopo kule Dar es Salaam.
Mheshimiwa Spika, ucheleweshwaji si wa makusudi, ucheleweshwaji ni wa kitaalam kwa sababu kuna vigezo vingi ambavyo vingepaswa kuwepo kabla sampuli hazijapatiwa majibu kutoka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali kwa haraka ikiwemo kujenga uwezo wa wachunguzi wetu wa makosa ya jinai kwa maana ya Jeshi la Polisi wa namna ya ku-navigate kwenye crime scene na kuchukua sampuli. Lakini pia namna ya kujua ipi ni sampuli ya maana na ipi sio sampuli ya maana kwenye kesi hii, lakini pia mlolongo wa mpaka sampuli kufika kwenye maabara nao ni mrefu sana.
Mheshimiwa Spika, kwa mfano kwa sampuli kutoka Zanzibar ni lazima wachunguzi wakamilishe uchunguzi wao, wakusanye sampuli, wazipeleke kwa Mkemia Mkuu wa Serikali kule Zanzibar naye aridhike kwamba sampuli zinajitosheleza ziweze kuletwa huku Dar es Salaam kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi.
Mheshimiwa Spika, kwa vyovyote vile lazima kuwe kuna ucheleweshwaji, majibu pia yana mlolongo huohuo kutoka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali Maabara, kwenda mpaka kule. Na wataalam tulionao pia ni wachache, kwenda kutoa ushahidi kwenye kesi mbalimbali nchi nzima nayo pia ni sababu nyingine ya ucheleweshwaji.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Kama vitabu vyetu vyote vya dini vinasisitiza tohara, na pia tafiti zinaonyesha katika maeneo ambayo hakuna tohara ya wanaume maambukizi ya UKIMWI ni makubwa kushinda viwango vya Kitaifa, sasa kwa nini Serikali inapata kigugumizi katika kulazimisha suala hilo? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili; kama magonjwa mengine yote yanapewa chanjo, yaani chanjo inakuwa ni lazima kwa ajili ya kukinga magonjwa haya, kwa nini tohara kwa upande wa wanaume isiwe lazima ili na yenyewe iwe kinga ya kupunguza maambukizi ya Virusi vya UKIMWI na kupunguza gharama kubwa kwa Serikali ya kuhudumia ugonjwa huo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwa nini Serikali inapata kigugumizi, Serikali haina kigugumizi chochote kwenye jambo hili. Tunachokifanya kwanza kwa ujumla ni lazima ieleweke dhana ya ridhaa, kwenye huduma za afya, kwenye huduma za tiba, kuna kitu kinaitwa consent, sasa kunaweza kukawa kuna ridhaa ambayo inatolewa kwa mtu moja kwa moja kwenda hospitali yeye mwenyewe kwa ridhaa yake kwa sababu anaumwa na amefika hospitali. Pale hatutamuuliza kama anaruhusu tukutibu kwa sababu yeye mwenyewe amekuja hospitali na kwa msingi huo anataka kutibiwa, kwa hiyo yule ameshatoa ridhaa ambayo ni ya yeye mwenyewe kutaka kwenda hospitali kwa sababu amefika hospitali kwa sababu anaumwa. Lakini kwenye mambo yote yatakayohusu upasuaji, vipimo, ni lazima pia kuwe kuna ridhaa kutoka kwa mgonjwa na kama mgonjwa hajitambui kutoka kwa ndugu zake, huo ndiyo msingi wa huduma za tiba duniani kote.
Mheshimiwa Spika, sasa kwenye suala hili la tohara, kwa sababu ni jambo la hiari kama vile ilivyo kwa matibabu mengine yote, ni lazima mtu atoe ridhaa yake ndiyo aweze kupatiwa huduma ya kufanyiwa tohara, na haiwezi hata siku moja kuwa ni jambo la lazima na kwa msingi huo, Serikali haina kigugumizi chochote kwenye jambo hili.
Mheshimiwa Spika, lakini nitumie nafasi hii kutoa rai kwa akina mama wote nchini kutumia fursa ya kuwashawishi wenza wao watafute…

Mheshimiwa Spika, natoa rai kwa akina mama wote nchini kutafuta wakati muafaka wakiwa na wenza wao kuzungumza nao kwa upole, kwa heshima na upendo wa hali ya juu wale akina baba ambao wanashiriki nao tendo la ndoa ambao hawajafanyiwa tohara. Hii itasaidia kuwashawishi wanaume wao wenyewe kwa hiari yao waende kwenye vituo vinavyotoa huduma za tohara ama kwenye huduma mkoba ambazo zinazunguka kwenye mradi wetu kama nilivyosema hapo, kwa sababu tohara inapunguza maambukizi ya Virusi vya UKIMWI kwa kiwango cha asilimia 60, sio kitu kidogo, ni kitu kikubwa. Lakini pia tohara inaepusha maambukizi ya vinasaba vya Human Papilloma Virus (HPV) ambavyo vimekutwa kwa zaidi ya asilimia 80 kwa akinamama ambao wana saratani ya shingo ya kizazi. Kwa hiyo, ni muhimu sana akina baba wakafanyiwa tohara. Na akina mama watumie fursa wakati muafaka wawasihi wenza wao waende wakafanyiwe tohara kwa hiari.
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa chanjo ni lazima why not tohara? Nafikiri majibu yangu kwenye jibu langu la awali yanajitosheleza. Tohara hata kama ni kitu ambacho kingesaidia kupunguza maambukizi ya Saratani kama hivyo nilivyosema ama kupunguza maambukizi ya virusi vya UKIMWI lakini bado ili kumfanyia mtu ni lazima kuwe na hiari yake na hatuwezi kufanya vinginevyo.
MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza. Kuna baadhi ya makabila wanatumia njia za kienyeji badala ya kwenda kufanyia tohara vijana wao katika hospitali njia ambazo zinasababisha wakati wa kuwafanyia tohara wakati mwingine kutokwa na damu nyingi na kupoteza maisha. Je, Serikali inatuambia nini kuhusu kuwapa elimu ili waweze kupeleka vijana wao katika hospitali zetu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ni rai yetu kwenye Makabila ambayo yana utamaduni wa kufanya tohara za kiasili maarufu kama kavukavu kama ulivyosema kuwaomba watumie huduma hiyo ya kutoa tohara kwa kwenda kwenye hospitali na kufanyiwa huduma ya tohara ya kitabibu yaani medical circumcision ili kuepukana siyo kutokwa damu nyingi, lakini pia kuepukana na uwezekano wa kuambukizwa magonjwa mbalimbali kwa sababu kule wanakofanya tohara ya kiasili kuna uwezekano mkubwa wakachangia vifaa vya kufanyia tohara yenyewe na hivyo kuhamisha vimelea vya magonjwa, kwa mfano homa ya ini ama virusi vya UKIMWI kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mtu mwingine kwahiyo, nitumie jukwaa lako hili kutoa rai kwa Mangariba wote kwenye makabila ambao wanatoa tohara ya kiasili kuanza kutumia tohara ya kitabibu kwenye hospitali zetu.
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nina swali moja tu la nyongeza, lakini naomba nitoe na ushauri kwa Serikali. Kwanza kabisa nitoe ushauri kwamba kuongeza vyuo haitakuwa msaada mkubwa sana, niombe sana sasa Serikali ione umuhimu wa kuboresha mafunzo katika hivi vyuo viwili. Dar es Salaam Institute pamoja na Arusha Technical kwa kuongeza vifaa vya kufundishia vijana hawa na kuboresha ufundi. Kwa sababu Serikali inaposema asilimia 24 itakuwa imefikiwa mwaka 2015 maana yake hali ni mbaya sana. Kwa hiyo niiombe sana Serikali iliangalie hilo iboreshe mafunzo katika vyuo hivi vilivyopo na wafundishe mpaka level ya degree.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na wataalam hawa kutengeneza vifaa vya tiba, lakini wako wataalam wa kupima kwa kutumia hivi vifaa wajulikanao kwa jina la Radiologists, Halmashauri ya Mji wa Njombe katika Hospitali yake ya Kibena ina wataalam hawa wawili lakini ni wa daraja la pili. Je, Serikali iko tayari kutuletea Radiologist Grade One ili aweze kutumia mashine ambayo Halmashauri tumeinunua pale katika Hospitali yetu ya Kibena?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ushauri wake tumeupokea, lakini kwa sasa tupo katika jitihada za makusudi za kuongeza idadi ya wadahiliwa kwenye fani mbalimbali za Uhandisi wa vifaatiba, lakini pia Serikali kupitia vyuo vyake vikuu, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) pamoja na Muhimbili University of Health and Allied Sciences (MUHAS) kwa ajili ya kutengeneza mtaala ambao utatumika kufundisha hao wanafunzi wa uhandisi kwenye eneo la vifaatiba kwa sababu tunakoelekea teknolojia ya vifaatiba itaendelea kuongezeka, kukua kwa kasi na tunaendelea kuingiza nchini kama nilivyotoa maelezo yangu hata jana hapa. Kwa msingi huo, mafundi hawa lazima tuwe nao wa kutosha. Kwa hiyo, tumeona tuanzishe degree ya Uhandisi wa Vifaatiba kwenye Vyuo Vikuu vya Muhimbili pamoja na kile cha Dar es Salaam. Malengo ni hayo ya kukabiliana na mahitaji ambayo yanajitokeza nyakati na nyakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia swali lake la pili kuhusu kupeleka mtaalam wa kupima mionzi (Radiologist) pale Kibena, naomba nilichukue ombi lake na pindi tutakapokuwa tunaajiri wataalam na kuwatawanya kwenye maeneo mbalimbali ya nchi yetu tutazingatia ombi la Mheshimiwa Mbunge.(Makofi
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa malengo makuu ya kuanzishwa kwa Benki ya Wanawake ni kumkomboa mwanamke wakiwemo wanawake wa Mkoa wa Singida. Swali la kwanza, je, Serikali haioni umuhimu wa kuanzisha dirisha maalum la wanawake kwenye benki ambazo inamiliki hisa kama NMB ili kuwawezesha wanawake wa Mkoa wa Singida kupata mikopo nafuu wakati Serikali ikiendelea kujipanga?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa wanawake wengi wamejikita katika shughuli za ujasiriamali lakini hawana dhamana za kukopa; Je, Serikali inatoa maelekezo gani kwa SACCOS na benki binafsi ili kuwawezesha wanawake wengi kupata mikopo? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Mwaka huu akinamama wa Singida wana bahati kwa sababu tunaanza hatua ya awali ya kufungua kituo cha kutolea huduma za Benki ya Wanawake. Singida ni katika mikoa mitatu ambayo tumeamua kuwekeza mwaka huu. Sambamba na mkakati huo tulionao, wazo lake tunalichukua, kwamba Benki yetu ya Wanawake Tanzania iangalie uwezekano wa kufungua madirisha maalum kwenye benki mbalimbali ambazo zipo katika maeneo mengi zaidi nchini. Ni wazo zuri, tunalichukua.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie, teknolojia ambayo imeingia sasa hivi kwenye huduma za kibenki hapa nchini ya kutumia mitandao lakini pia ya kutumia simu za mkononi, nayo itatusaidia kuwafikia Watanzania wengi zaidi na huduma za kibenki na hata huduma za kimikopo huko tunakoelekea.
Mheshimiwa Naibu Spika, tayari tuna management mpya ya Tanzania Women’s Bank ambayo imeanzisha mazungumzo na wenzetu wa TTCL pamoja na wa Halotel kwa ajili ya kutengeneza mifumo ya kibenki ambayo inatumia simu za kiganjani ili kuwafikia wananchi walio wengi zaidi na mikopo pamoja na huduma mbalimbali za kibenki katika nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusu SACCOS na benki binafsi; tunazishauri ziendelee kufanya kazi kwa ukaribu na wataalam wetu wa Benki ya Wanawake Tanzania ili waone ni namna gani wanaweza wakashirikiana kwa pamoja kuwahudumia wanawake ambao ni wajasiriamali.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi. Hivi Serikali ina mpango gani mahsusi wa kuwaangalia na wanawake wa vijijini, kwa sababu mipango mingine yote imefeli kwa wanawake wa vijijini kupata mikopo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa yeye pia ni Kada wa Chama cha Mapinduzi, naomba nimkumbushe kwamba kwenye Ilani ya Uchaguzi pamewekwa maelekezo kwamba kila Halmashauri nchini itenge asilimia tano ya bajeti yake kutoka kwenye Own Source kwa ajili ya kuwakopesha akinamama, huu Mfuko unajulikana kama Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake. Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo wanawake wote, wakiwemo wanawake wa vijijini, hata wale anaowapenda sana wa kule Same, nao wanaweza wakatumia fursa hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi yetu ssi Waheshimiwa Wabunge ni kuingia kwenye vikao vya Halmashauri wakati tunapanga bajeti na kushiriki kuhakikisha asilimia tano ya akinamama inatengwa, asilimia tano ya vijana inatengwa. Pia tusiishie hapo, pesa zinapopatikana tuziweke pembeni pesa za Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia Wabunge ni Wajumbe wa Kamati ya Maendeleo ambayo huwa inahusika kugawa hizi pesa kwenye vikundi mbalimbali. Kwa hiyo baada ya kuwahamasisha wananchi wetu waombe mikopo hii ya Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake, pia tushiriki kwenye vikao vile vya Halmashauri ambavyo vinagawa pesa hizi kwenye vikundi mbalimbali vya akina mama ili ziwafikie kwa uhakika wananchi hao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kupitia Benki ya Wanawake tunatengeneza mifumo sasa ambayo itawafikia Watanzania popote pale walipo, hata wa kijijini, sasa hivi matumizi ya simu ni kwa zaidi ya watu milioni 36 hapa nchini, kwa hiyo njia hii itawafikia watu wengi zaidi hapa nchini kwetu. (Makofi)
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa sababu nilikuwa nimefikiri atazungumzia wanawake tu kwa kuwa hii biashara ni ya watu wawili. Hata hivyo, nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa, pamoja na kwamba kunakuwa na biashara hiyo ya wanawake na wanaume, lakini pia sasa hivi kuna biashara ya homosexuals, wanaume peke yao au lesbians; je, hawa wanachukuliwa hatua gani?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hiyohiyo niliyoisema wakati natoa majibu ya msingi hapa inakataza pia vitendo vya watu wa jinsia moja kufanya mapenzi kinyume cha maumbile. Pia inakataza hata, kwa mfano kwa mwanaume kufanya vitendo ambavyo vinaashiria kwamba ni vya jinsia ya kike, yaani kufanya mambo ya kike wakati wewe ni mwanaume. Sheria hiyo inakataza na inayajinaisha na kuna adhabu kali ambayo inatolewa na sheria hiyo, ni zaidi ya miaka 30.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali tumekuwa tukipambana kwa nguvu zetu zote na makundi haya ambayo yamekuwa yakishiriki kwenye vitendo vya mapenzi ya jinsia moja ama kuyahamasisha ama kuyahalalisha ama kuyafanya yaonekane ni vitu vya kawaida kwenye nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumefanikiwa kwa kiasi kikubwa kwa sababu tuliendesha operesheni kubwa ya kudhibiti vitendo hivi lakini pia hata taasisi ambazo zilionekana zina mwelekeo wa kutekeleza afua mbalimbali za kinga kwenye sekta yetu ya afya tumezifuta, tumezibadilisha. Hata miongozo ambayo iliruhusu baadhi ya afua zinazohusiana na kupunguza maambukizi kutoka kwa watu wanaofanya mapenzi ya jinsia moja nayo tumeibadilisha, kwa hiyo tuko vizuri. Watakaofanya hivyo watakamatwa na Jeshi letu la Polisi na watachukuliwa hatua za kisheria.
MHE. LUCY S. MAGERELI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa swali langu lilirejea Taarifa ya Kamati ya Mambo ya UKIMWI iliyotolewa ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Februari mwaka huu, nilitarajia majibu ya Mheshimiwa Waziri yawe at least na takwimu ambazo sasa zitaunga mkono hoja ya Taarifa ya Kamati au zitatengua ile hoja ya Taarifa ya Kamati kwamba fedha za wafadhili katika eneo hili zimepungua sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali langu, Mheshimiwa Naibu Waziri anisaidie kwamba hao wadau aliowataja ni wadau gani ambao wameendelea kutoa support katika eneo hili? Kwa sababu tunafahamu fedha za mambo ya UKIMWI zimekuwa zikichangiwa kwa asilimia kubwa sana na PEFA na Global Fund ambao kwa sehemu kubwa wame-pull out.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa sijajua hao aliowazungumzia hapa Mheshimiwa Naibu Waziri ambao anasema wanachangia kwa kiasi kikubwa kinyume na Taarifa ya Kamati ni akina nani? Napenda kufahamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kumekuwa na maendeleo kadhaa ya kitabibu na kimaabara ambayo yanaonesha majaribio yaliyofanikiwa katika upatikanaji wa chanjo na hata tiba ya Virusi vya UKIMWI. Je, Serikali ina maelezo gani kuhusu maendeleo haya na taarifa hizi ambazo zinatokana na vyombo mbalimbali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwamba ni wadau gani? Kwa mujibu wa sheria ambayo inaanzisha Mfuko wa UKIMWI Tanzania, malengo makuu ya mfuko huu ni kukusanya pesa ambazo zitakwenda kuweka uendelevu wa pesa ambazo zitakuja kuwa zinatumika sustainably kwenye kununua dawa za UKIMWI kwa kiwango cha asilimia 60, lakini pia kutoa huduma za kinga kwa asilimia 25, pia kwa asilimia 15 kusaidia kwenye mwitikio wa UKIMWI kwa maana ya kujenga mazingira mbalimbali wezeshi hapa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mfuko huu una malengo ya kuwa endelevu na ulianzishwa kwa malengo kutokana na mabadiliko yaliyofanyika kwenye Sheria ya UKIMWI ambayo ilianzisha TACAIDS mwaka 2001 Sheria Namba 22 kwa ajili ya kutengeneza sustainability kwenye eneo la upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya HIV/Aids.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa mfuko huu bado ni mchanga sana na umezinduliwa mwaka 2016 tu mwezi Disemba na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano za Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan na kwa mwaka wa fedha uliopita tulitenga kiwango cha shilingi bilioni 5.5 na mwaka huu tumetenga shilingi bilioni tatu. Kwa hiyo, ndiyo tumeanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wadau ni akina nani? Wadau wa kwanza ni Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia bajeti yake, lakini pia tunatarajia mfuko huu utakusanya vyanzo vingine vya fedha kutoka kwa wananchi kwa ujumla ambao watajitokeza kuchangia kutoka kwenye sekta binafsi, asasi za kiraia, asasi za hiari, lakini pia wadau wa maendeleo hawazuiliwi pia kuchangia kwenye mfuko huo. Malengo yetu ni kwamba tuweze kufikia angalau asilimia 30 ya kujitosheleza kwenye fedha za dawa za kupunguza makali katika kipindi cha miaka mitatu ijayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, chanjo ya virusi vya UKIMWI bado inaendelea kufanyiwa utafiti duniani, jitihada bado zinaendelea. Nasi Tanzania ni washiriki katika tafiti mbalimbali ambazo zitapelekea kupatikana kwa chanjo kwa siku zijazo, lakini kwa sasa tuko katika hatua za awali sana za Kisayansi za kutafuta chanjo hiyo na bado hakujawa na mwangaza mkubwa sana kwamba labda katika kipindi cha miaka kadhaa tunaweza tukawa tumefikia hatima ya kuwa na chanjo ya virusi vya UKIMWI.
Kwa hiyo, tuendelee kuvumilia wakati wanasayansi wakifanya kazi yao kwenye maabara zetu. (Makofi)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri, lakini nimesimama kwa sababu Mheshimiwa Mbunge Lucy Magereli anazungumzia upatikanaji wa dawa za ARV.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie Bunge lako Tukufu kusema kwamba tunazo ARV ambazo kuanzia mwezi Oktoba, 2016 zinatolewa kwa kila Mtanzania atakayepima na kukutwa na maambukizi ya VVU.
Mheshimiwa Naibu pika, sasa kwa nini nimesimama? Kati ya watu wenye maambukizi ya VVU, wanawake wanaotumia ARV ni asilimia 73, wanaume ni asilimia 48 tu. Kwa hiyo, nitoe wito kwa wanaume wote Tanzania watumie dawa za ARV ili kwa pamoja tuweze kupunguza maambukizi ya VVU nchini. Acheni kujiona nyie mna misuli, ni wababe, dawa za ARV zipo, tumieni ili tuweze kupunguza maambukizi ya UKIMWI. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa kwa sababu kati ya maambukizi mapya ya vijana wetu wenye miaka 15 mpaka 24 kwa wavulana ni asilimia nane na wasichana ni zaidi ya asilimia 80. Maana yake hawa wanaume ndiyo wanarudi tena kwa watoto wadogo na hivyo kufanya kuwepo kwa maambukizi mapya ya VVU na UKIMWI.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona nitumie fursa hii Waheshimiwa Wabunge wakawahamasishe wanaume watumie ARV, zipo bure, zinapatikana na mtu yeyote akipima anapata bila shida. Ahsante sana. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU):
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ninampongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Afya kwa majibu ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa ili kuweza kulithibitishai Bunge lako kwamba mfuko huu ambao ulianzishwa kwa Sheria Namba 6 ya mwaka 2015 na unasimamiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, umeanza kufanya kazi nzuri sana pamoja na uchanga wake.
Mheshimwa Naibu Spika, maagizo ya Kamati kama alivyosema Mbunge aliyeuliza swali, yalikuwa na malengo ya kuhakikisha kwamba Serikali inasimamia mfuko huu na unaanza kufanya kazi.
Mheshimwa Naibu Spika, naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Waheshimiwa Wabunge wa Kamati inayohusika na masuala ya UKIMWI waliiagiza Serikali, kwa rasilimali ndogo iliyopatikana ni lazima sasa mfuko uanze kuhakikisha unatoa fedha kupeleka Wizara ya Afya ili kushughulika na dawa na kuongeza maisha ya Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Kifungu cha 6(1) cha Sheria hiyo, mfuko unakaribia kutoa, umeshapitisha kwenye Bodi jumla ya shilingi za Kitanzania bilioni 1.45 kwa ajili ya kununua dawa za septrine na kwa ajili ya kujenga Kituo cha Upimaji Mererani na kujenga kituo kingine cha upimaji kwenye Visiwa ndani ya Ziwa Victoria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba niwathibitishie Wabunge kwamba Kamati ilifanya kazi nzuri na Serikali imepokea maagizo hayo na tayari mfuko wetu umeanza kuonesha kwamba tunaanza kujitegemea ndani ya Serikali yetu ingawa wafadhili bado wanaendelea kutusaidia. (Makofi)
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.
Kwanza, ni lini Serikali itatoa ruzuku ya moja kwa moja kwa kinamama wanaojifungua ili kuondoa kadhia hii?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, Ilani ya Chama cha Mapinduzi ilielekeza kujenga vituo vya upasuaji kila kata. Je, ni lini Serikali itatekeleza agizo hili kibajeti? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Khadija Nassir Ali kwa kuuliza swali la kisera ambalo limetupa fursa ya kufafanua mambo mbalimbali ambayo ni kipaumbele kwa Wizara yetu kwa sababu yanahusu kupunguza vifo vya wakinamama wajawazito na watoto na yeye kama Mbunge mwanamama nadhani anaguswa na mtazamo wetu kwamba hiki ni katika vipaumbele vyetu pale Wizarani.
Mheshimiwa Spika, ruzuku kutoka Serikali kuu kwenda Serikali za Mitaa kwamba ni lini itatoka? Nadhani hakufanya mazingatio ya kutosha kwenye majibu yangu ya msingi kwa sababu tayari hapa hapa tu nimezungumza tuna zaidi ya bilioni 66 ambazo tunazipeleka kwenye Halmashauri mbalimbali nchini kwa ajili ya kufanya maboresho kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini. Na hiyo ni ruzuku kutoka Serikali kuu.
Mheshimiwa Spika, vilevile kwenye bajeti ya afya Fungu Namba 52 tumeweka bajeti ya dawa mbalimbali ambazo zinaenda kusaidia kupunguza vifo vinavyotokana na sababu mbalimbali za uzazi. Kwa mfano, tumeweka bajeti ya Uterotonic drugs kama Oxycontisin ambapo tunapeleka kwenye Halmashauri moja kwa moja, kwenye vituo vya kutolea huduma za afya.
Mheshimiwa Spika, pia tumeweka bajeti mahususi ya kutoa dawa za magnesium sulphate ambazo zinasaidia kutibu ugonjwa wa eclampsia (kifafa cha mimba) ambazo hizi ni katika sababu kubwa ambazo zinapeleka kupoteza maisha wakati wa uzazi.
Mheshimiwa Spika, pia Serikali Kuu inasaidia sana kwenye kuimarisha mfumo wa upatikanaji wa damu salama kwenye vituo vyote vya afya nchini na hii ni moja kwa moja tunatoa sisi tunapeleka msaada kule chini. Kwa hiyo, ruzuku tunatoa na tunatoa kwa kiasi kikubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba nisisitize hapa kwamba Wabunge wenzangu wote na Halmashauri zote nchini watambue jukumu la kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi ni la kwao wenyewe kwenye Halmashauri husika. Ni lazima tufanye uwekezaji kwenye vituo vya kutolea huduma za afya, hakuna namna nyingine. Sisi Serikali kuu tunasaidia tu kujenga uwezo wa vituo vyetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, la pili, Ilani ya CCM haizungumzii kujenga vituo vya upasuaji kwenye kila kata, Ilani ya CCM inazungumzia ujenzi wa vituo vya afya (health centers) kwenye kila kata na zahanati kwenye kila kijiji. Ilani ya uchaguzi inakwenda sambamba na Mpango wa Maendeleo wa Afya ya Msingi wa mwaka 2007/2017 ambapo Halmashauri zote nchini zinapaswa kujenga vituo vya afya kila Kata na zahanati kwenye kila kijiji.
Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo, jitihada bado zinaendelea kwenye Halmashauri mbalimbali nchini na sisi kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya awali, tunaendelea kujengea uwezo lakini pia ku-support halmshauri zetu kutimiza azima hii iliyowekwa kwenye Ilani ya uchaguzi ya CCM. (Makofi)
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwanza, niipongeze Wizara hii kwa maana ya MSD kwa kuwa sasa wanatoa dawa za kutosha katika hospitali zetu. Hata hivyo, kwa kuwa hospitali hizi zinapokuwa zinakosa hivi vifaa tiba, kama ambavyo amezungumza kwenye jibu lake la msingi, kwamba wanaruhusu kwenda kununua kwa wazabuni, haoni kwamba kitendo cha kwenda kununua kwa wazabuni bei ni kubwa mara mbili zaidi ya vile vifaa ambavyo wanakwenda kuvinunua kama vile dawa za amoxicillin pamoja na vile vifaa vya theater. Hawaoni kwamba sasa inakuwa ni gharama kubwa zaidi kuwahudumia hao wagonjwa ambao wanaokwenda kwenye hizi hospitali? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pili, kwa kuwa anasema kwamba mteja apewe ndani ya siku moja ili kwenda kununua kwenye haya maduka ya watu binafsi. Kwa nini isiwe ndani angalau ya wiki moja kuliko ile siku moja ili mtu apate nafasi nzuri ya kuweza kwenda kununua hizo dawa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza, ni kweli kwamba bei kwenye sekta binafsi zinaweza zikawa kubwa ukilinganisha na bei zilizopo kwenye maghala ya MSD. Sababu ni nyingi, mojawapo ikiwa ni kwamba kwenye MSD kwa sasa kwa sababu tunanunua dawa moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji tumeshusha gharama ya manunuzi ya dawa, vifaa, vifaa tiba na vitendanishi kwa asilimia takribani 40 na kwa hiyo bei ya dawa MSD iko chini sana ukilinganisha na kwenye sekta binafsi.
Mheshimiwa Spika, lakini kinachosababisha tushindwe ku-take advantage ya bei ya MSD kuwa chini ni kujaribu kuongeza ufanisi kwamba pale ambapo hatuna dawa kwa kiasi fulani tusicheleweshe wananchi kupata huduma ya dawa kwa sababu tu tunataka vituo vyetu vipate dawa kutoka MSD, basi tuwape fursa Halmashauri waende wakanunue dawa kwenye sekta binafsi ili dawa zisikosekane kwa wateja pale kwenye kituo cha kutolea huduma za afya. Haya yalikuwa ni malalamiko ya muda mrefu, kabla hata sisi hatujateuliwa kwenye nafasi hizi malalamiko ya dawa yalikuwa mengi sana na Waheshimiwa Wabunge wengi walitamani Halmashauri zao ziruhusiwe kwenda kununua dawa kwenye sekta binafsi, kwa sababu kisheria hairuhusiwi kabisa lakini tumeamua kufanya maboresho ambayo yanaongeza tija na ufanisi wa MSD ili kuhakikisha tunaharakisha upatikanaji wa dawa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya wakati ambapo Halmashauri zina pesa na MSD haina stock ya dawa fulani.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, niwathibitishie na kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote kwa ujumla kwamba baada ya kuongeza ufanisi wa MSD, kwa sasa upatikanaji wa dawa umeongezeka kwa zaidi ya asilimia 80. Kwenye Halmashauri nyingine ambazo natembelea nakuta upatikanaji wa dawa umekuwa mpaka katika kiwango cha asilimia 90, asilimia 95, dawa zote muhimu zinapatikana.
Mheshimiwa Spika, swali la pili, tunatoa saa 24 kile kibali cha Out of Stock (OS) kwa sababu tunataka kuongeza ufanisi kama nilivyosema. Kuliko kusema tutoe wiki nzima ndiyo tutoe kile kibali cha Halmashauri kwenda kununua dawa, maana yake tutakuwa tumewachelewesha wananchi kupata dawa kwa wiki nzima.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hii kwenda kwenye 24 hours maana yake tunataka ufanisi uwe ni wa hali ya juu na wananchi wasikose dawa.
MHE. KEMIREMBE J. LWOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kumekuwa na tatizo kubwa sana na uhaba mkubwa wa dawa ya morphine kwenye hospitali zetu ambayo inapelekea wagonjwa hususani wa cancer kuteseka na maumivu makali sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali langu, je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kuweka dawa hii ya morphine kwenye list ya dawa muhimu au National Essential Drug List ili ziweze kupatikana kirahisi na kuwaponya maumivu wagonjwa hawa wa cancer? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwamba dawa ya morphine iwekwe kwenye Essentials Medicine List ni kitu ambacho katika hali ya sasa ya nchi yetu hatuwezi kukikubali kwa sababu ni katika dawa ambazo ziko controlled na kwamba ili kuzitoa ni lazima kuwe kuna ujuzi fulani unaohitahijika kuwepo katika kituo hicho ndipo mtu aweze kuruhusiwa kutoa dawa hiyo. Ndiyo maana inatolewa kwa kibali maalum, inatunzwa kwa kibali maalum na hatuwezi kubadilisha hilo kwa sababu dawa ya morphine ina madhara kama ikiwa administered na mtu ambaye hata ujuzi wa namna ya kuitunza na namna ya kui-prescribe.
MHE. DKT. GODWIN A. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, hili suala la dawa linaonesha ni tatizo sugu na swali langu ni kwamba ukilinganisha vituo vya afya vya binafsi na hata maduka ya binafsi na MSD, dawa ambazo hazipatikani Serikalini mara nyingi zinapatikana kwenye vituo binafsi.
Mheshimiwa Spika, je, Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza kutuambia ni kwa nini vituo binafsi vinakuwa na dawa zote wakati Serikali inashindwa kuwa nazo na imekuwa ni tatizo sugu, tufanye nini kama nchi?
Mheshimiwa Spika, hapa amezungumzia suala la morphine pamoja na ku-control, lakini ni dawa ambayo kwa kweli inahitajika kwenye vituo vya Serikali kwa sababu watu maskini wanateseka sana. Pamoja na control hizo zote ambazo tunazisema lakini kwa kuzingatia hizo control ni muhimu hizo dawa ziwepo kwenye vituo vyetu. Unatuambia nini kwa sababu kwa kweli hili ni suala sungu na ni aibu kwa Seriali kwa sababu kwanza tunanunua kutoka kwa mtengenezaji, kwa nini hatuna dawa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mollel...
Mheshimiwa Spika, basi nachangua kujibu lile la kwanza, kwamba kwa nini kwenye baadhi ya vituo vya Serikali hakuna baadhi ya dawa wakati kwenye private zipo.
Mheshimiwa Spika, ukweli ni kama nilivyoeleza kwenye majibu yangu ya msingi lakini pia kwenye maelezo ambayo nimeyatoa kwenye maswali mbalimbali ya nyongeza ambayo yamekuwa yakiulizwa hapa Bungeni ni kwamba huko tunakotoka hali ya upatikanaji wa dawa ilikuwa chini sana na sababu zilikuwa nyingi.
Mheshimiwa Spika, sababu mojawapo ilikuwa ni hiyo ya maoteo kujua mahitaji ya Halmashauri zote nchini kabla mwaka haujaanza na hii ni kwa mujibu wa sheria kwamba inatakiwa kila Halmashauri kufikia Januari ya kila mwaka wawe wameleta maoteo yao ya mahitaji ya dawa MSD na MSD ijipange kununua kadri ambavyo itaweza na kadri ambavyo inajua kwamba mahitaji ya dawa yametathminiwa na Halmashauri husika. Sasa mwaka jana tulikuja kugundua Halmashauri nyingi hazikuwa zikileta maoteo kwa hivyo unakuta Halmashauri wana pesa, halafu MSD ana bajeti ndogo kiasi kwamba hawezi ku-meet mahitaji ya Halmashauri ambao wana pesa zao tayari. Ndiyo maana tukaanzisha hii saa 24 kutoa kibali cha kwenda kununua kwenye private sector.
Mheshimiwa Spika, sababu nyingine ni kwamba dawa nyingi hazipatikani hapa nchini kwenye viwanda na sisi tuna maelekezo ya Mheshimiwa Rais ya kununua dawa moja kwa moja kutoka viwandani na sasa ili tuweze ku-meet hayo maelekezo tulikuwa tunapaswa kufanya mambo yafuatayo; tutanue mtaji wa MSD na ndicho ambacho tumekifanya. Mheshimiwa Rais ametuongezea bajeti ya dawa kutoka shilingi bilioni 31 mwaka juzi mpaka shilingi bilioni 251.5 mwaka jana na mpaka shilingi bilioni 299 mwaka huu. Tatizo la fedha sasa limeanza kupungua kwa hivyo sasa tuna uwezo wa ku- order dawa kadri ambavyo tunaona mahitaj ya nchi yatakuwa katika mwaka husika na kupanga schedule ya supply kila baada ya miezi mitatu itakuwaje.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, baada ya kufanikisha hilo, ndiyo maana nimesema pale awali, mahitaji ya dawa sasa tuna uwezo wa kuya-meet katika nchi kwa wastani wa asilimia 80 na kuna baadhi ya Halmashauri ambazo zina viongozi wazuri ma-DMO wazuri, Wakurugenzi wazuri wanaweza kufika mpaka asilimia 90. (Makofi)
Kwa hiyo, tukisema kuna baadhi ya dawa hazipo Serikalini na kuna baadhi ya dawa zipo kwenye private sector ni kweli, lakini angalau sisi tumehakikisha kwenye ile list ya essential medicines, dawa 138 za muhimu zaidi tunazo na kuna zile tracer medicine 30 tunazo wakati wote. Kwa hiyo, kuongelea kwamba dawa fulani ipo huku private na huku Serikalini haipo linaweza likawa ni suala kidogo relative lakini objectivity yake ni kwamba angalau tuna uhakika makundi yote ya dawa yanapatikana, anti-biotics zipo, anti inflammatories zipo dawa zote essentials zinapatikana kwenye vituo vya kutolea huduma vya Serikali.
Sasa hivi mimi nazunguka sana pengine kuliko Mheshimiwa Mbunge, sijapata malalamiko ya dawa tena takribani mwaka mzima umepita. Nakushukuru.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, napenda kuuliza maswali mengine ya nyongeza kwa sababu swali la msingi kwa kweli Mheshimiwa limejibiwa kwa ujumla zaidi kiasi kwamba linaninyima matumaini.
Mheshimiwa Spika, swali langu niliuliza kuna mkakati gani wa kuharakisha, sasa suala la uzio wa mwaka 2011 nadhani hilo si sehemu ya kuharakisha ujenzi wa hiyo hospitali. Suala la kama Bima ya Afya pia wamekubali kusaidia katika ujenzi huo tumelisikia zaidi ya miaka miwili sasa.
Je, ni lini taratibu za ndani zitakapokamilika ambazo zilichukua zaidi ya miaka miwili?
Swali la pili, hivi majengo ya OPD peke yake yanatosha kuifanya kuwa ni Hospitali ya Rufaa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante.
Kwanza nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Dada yangu Hawa Abdulrahman Ghasia kwa ufuatiliaji wa karibu sana wa suala hili. Ninadhani wananchi wa Mtwara Vijiji wananisikia kwamba suala hili amekuwa akilifuatilia kwa ukaribu na hii ni mara yake ya zaidi ya tatu kuuliza suala hili.
Majibu ya swali lake la kwanza kwamba ni lini mchakato wa ndani utakamilika naomba nisitoe time frame mahsusi kwa sababu sina uhakika ni lini mchakato huu utakamilika lakini nimuahidi tu kwamba nitalifuatilia mimi mwenyewe kwa ukaribu na nitamjulisha pindi nitakapokuwa nimepata jibu la uhakika kwamba ni lini haswa mchakato wa ndani utakamilika kabla NHIF hawajatoa pesa kwa ajili ya kwenda kumalizia jengo la OPD.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili linalohusu mchakato wa kuanzisha hospitali yenyewe kwamba je, inatosheleza tu kwa kuwa na OPD ili iwe hospitali ya Kanda, hapana. Tunachokifanya ndicho alichokiuliza kwenye swali la msingi kwamba, tunataka hospitali walau ianze kutoa huduma sasa katika kuanza kutoa huduma ili ikamilike zinahitajika pesa nyingi sana. Kwa kuwa pesa zote hazipatikani siku moja na mahitaji ya hospitali hii ni makubwa na sote tunakubaliana kwamba kuna umuhimu wa kuwepo na hospitali hii na huduma hizi kuanza kwa haraka, ndiyo maana tumeona kuliko kusubiria mpaka hospitali yote ikamilike wakati tuna majengo ya awali yameshakaribia kukamilika kabisa na tunaweza tukaanza kutoa baadhi ya huduma, tumeona tuanze kutoa huduma kwa awali, lakini zitatoka katika kiwango hicho hicho cha ngazi ya Hospitali ya Rufaa ya Kanda.
MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Serikali inafanya kazi kama timu moja, kwa nini marekebisho ya Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 isibadilishwe ili itambue Mahakama ya Kadhi kama chombo cha kuamua hatima ya ndoa za kiislamu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa hili la Mahakama ya Kadhi nitaomba Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali anisaidie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sehemu ya kwanza ya swali lake, ufafanuzi ni kwamba Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 kile kifungu cha 13 na 14 kwa kiasi kikubwa vinahusu mambo ya nodal, hususan vinaruhusu mtoto mwenye miaka 14 kuolewa kwa sababu mbalimbali ambazo nitazitaja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi sheria ile ilitungwa katika zama ambapo mila na desturi za baadhi ya makabila yaliyopo katika nchi yetu zikizingatiwa. Pia sheria ile ilitungwa kwa kuzingatia pia misingi ya dini mbalimbali ikiwemo dini ya kiislamu ambapo katika imani hiyo inaruhusiwa mtoto kuolewa ama kuoa tu pindi anapobalehe ama anapovunja ungo. Kwa hiyo, haya ni mambo ambayo kama Serikali tunahitaji kuyachukua kwa utaratibu sana kwa sababu yanahusu imani, yanahusu mila na desturi za watu wetu na hivyo lazima ipatikane consensus ya kitaifa kabla hatujafanya uamuzi wowote wa mabadiliko ya suala hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nia ya Serikali ipo wazi na taratibu kadri tunavyojifunza kwa wenzetu kama nchi ya Kiislam ya Bangladesh, nasi tutaona ni njia ipi muafaka tuweze kupitia. (Makofi)
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa sheria hii imekuwa ikiwazungumzia sana watoto wa kike na tunapozungumzia watoto, wapo watoto wa kike na watoto wa kiume; na watoto wa kiume kwa sasa wanakabiliwa na janga kubwa la ulawiti:-
Je, Serikali inazungumziaje swali hili ili kuhakikisha kwamba inawalinda watoto hawa wa kiume ambao wamekuwa wakipatwa na madhara hayo?
NAIBU WAZIRI AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kinyume cha sheria za nchi yetu kwa mtu yeyote yule kumwingilia kinyume cha maumbile mtu mwingine yeyote yule. Makosa haya yanaelezwa kwenye Sheria ya Kanuni za Adhabu, Chapter 16 of the Law, nafikiri ni kwenye Kifungu cha 154 na vifungu vinavyofuata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msingi huo makosa haya yamekuwa criminalized. Mwaka nafikiri 2012 au 2013 hapa Bungeni tuliongeza ukali wa adhabu ya mtu yeyote yule ambaye atabainika kufanya hivyo. Changamoto inayojitokeza kwa kweli, vitendo vya ulawiti kwa kiasi kikubwa sana vinafanyika kwenye familia. Vinapofanyika kwenye familia, ushahidi unakosekana kwa sababu ndugu wanakuwa hawataki kuripoti vitendo vya namna hii kwa kuhofia ndugu mwingine kwenda kufungwa. Kwa hiyo, wanayamaliza mara nyingi kimya kimya kwenye familia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Serikali msimamo wetu uko wazi kwamba adhabu kali ya kifungo kisichopungua miaka 30 itampata mtu yeyote yule ambaye atathibitika bila shaka kwamba amefanya kitendo cha ulawiti kwa mtoto yeyote yule awe wa kiume ama wa kike. (Makofi)
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa, Serikali imekiri kwamba baadhi ya sheria tulizonazo zinadumaza maendeleo ya wanawake na hasa watoto wa kike na kwa kuwa, tatizo la watoto wa kike wa Mikoa ya Lindi na Mtwara kukatisha masomo yao kutokana na mifumo ambayo mingine imepaliliwa na Sheria hizi mbovu tulizonazo.
Je, Serikali inachukua hatua gani kuwanusuru hawa watoto ambao sasa wanaendelea kupoteza fursa ya kusoma na kufanikiwa katika masomo yao kutokana na sheria hizi mbovu tulizonazo?

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la msingi ni kwamba tatizo hili la watoto wa kike kutomaliza masomo yao au kukatisha masomo yao kwa Mikoa ya Lindi na Mtwara ni kubwa sana na hasa katika Jimbo la Mtama. Moja ya sababu kubwa ni hizi sheria tulizonazo ambazo zinapalilia matendo kama hayo ya watoto hawa kupewa mimba na kukatishwa masomo yao na wengine kuolewa wakiwa bado wanaendelea na masomo na mengine wazazi wanasukuma watoto wao wafanye vibaya ili wafeli waende wakaolewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa swali langu ni kwamba Serikali inachukua hatua gani kuwanusuru hawa watoto ambao kwa kweli wanaendelea kupoteza fursa katika maisha yao?
NAIBU WAZIRI AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba arudie swali lake kwa ufupi. Swali hasa analotaka nijibu.

NAIBU WAZIRI AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Vizuri!
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Namshukuru Mheshimiwa Nape kwa swali lake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu yetu kama Serikali ni kwamba, kama nchi tulipitisha Sheria hapa Bungeni mwaka jana tu, 2016 na tulifanya mabadiliko kwenye Sheria ya Elimu ya mwaka 1978, kwenye kile kifungu cha 60(A).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kifungu hicho tuliamua kupandisha umri wa mtoto kuolewa mpaka kufikia miaka 21, lakini pia kuzuia mtoto yeyote yule ambaye anasoma primary school ama secondary school asiolewe kwa mujibu wa sheria na tukaweka adhabu pale. Kwa maana hiyo, suala hili kama Serikali tunalichukulia kwa ukali kama lilivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, umuhimu wa suala hili hauwezi kupigiwa mfano kwa sababu, ni jambo linalohusu maisha ya kizazi cha nchi yetu huko tunakoelekea. Kwa hiyo, rai yangu ni kwamba wazazi wote washiriki kikamilifu katika kuwalea watoto wetu na kuwasomesha ipasavyo kwa mujibu wa sheria; na wa watambue kwamba ni kosa kisheria kumwoza binti ambaye anasoma ama ni kosa kisheria kumpa mimba binti ambaye anasoma. Yule atakayefanya hivyo, awe mzazi, awe ndugu, awe mlezi, atachukuliwa hatua za kisheria kama itathibitika kwamba imekuwa hivyo. (Makofi)
MHE. KEMIREMBE J. LWOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri inaonyesha dhahiri kabisa kwamba Serikali inabagua maeneo ambayo hayana Hospitali za Wilaya. Kwa mfano, Wilaya ya Sengerema kuna hospitali moja ya mission inahudumia wananchi wote wa Wilaya ya Sengerema na kuna ombi ambalo limetolewa na wilaya yetu miaka minne iliyopita la kujenga Hospitali ya Wilaya Sengerema ya Serikali.
Je, ni lini Serikali itatekeleza ombi hili na kujenga Hospitali ya Wilaya ili kuweza kuweka huduma ya vifaa tiba na dawa katika Wilaya yetu ya Sengerema? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimhakikishe tu kwamba Serikali haibagui Wilaya yoyote ile dhidi ya Wilaya nyingine kwa sababu Wilaya zote hizi mwisho wa siku ndiyo zinaunda nchi yetu Tanzania. Kwa hivyo, tunatoa huduma sawa kwa maeneo yote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kuhusu hospitali ya Sengerema, nimefika kwenye hospitali ile na nimeshuhudia maendeleo makubwa yanayofanywa kwa ushirikiano baina ya mission, Mheshimiwa Mbunge, rafiki yangu na Mwenyekiti wangu wa Bunge Sports Club Mheshimiwa Ngeleja pamoja na Halmashauri yake na wadau mbalimbali wakiwemo Vodacom Foundation na kuna miradi mizuri inayoendelea katika Wilaya ya Sengerema. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kujenga Hospitali ya Wilaya nimshauri Mheshimiwa Mbunge akishirikiana na Mheshimiwa Ngeleja kwa pamoja kwenye vikao vyao vya Halmashauri waweke kipaumbele cha kuanzisha mradi wa ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Nina uhakika Mheshimiwa Jafo anasikiliza vizuri hapa atashirikiana nao kuwapa ufundi na sisi tutawapa ufundi, lakini pia ikibidi kama kuna rasilimali fedha tutawasaidia. Hata hivyo, uamuzi wa kwanza uwe ni wao wenyewe kuweka kipaumbele cha kuanzisha Hospitali ya Wilaya, lakini kwa sasa inaonyesha wameridhika na huduma zinazotolewa na Hospitali ya Mission.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba niishukuru Serikali kule Katavi tuliweza kupatiwa kituo hiki cha MSD kwa msaada wa Mheshimiwa Waziri Mkuu, lakini mita chache kutoka kilipojengwa kituo hicho kipo Chuo cha Matabibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu, ni lini Serikali itatusaidia kuhakikisha chuo hicho kimeanza kazi kwa sababu ukarabati ushafanyika kwa asilimia 99?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni lini, sina hakika sana lini tunaweza tukawa tumekamilisha lakini chuo hiki ni katika vyuo vinne ambavyo tumevipa kipaumbele cha kufanyiwa ukarabati na kufanyiwa maboresho ili kuweza kutusaidia katika mpango wetu wa kuendeleza na kuzalisha rasilimali watu kwenye sekta ya afya. Kwa msingi huo, ndiyo maana yeye mwenyewe anasema kimekamilika kwa asilimia 99; kwa hivyo kwa sasa hivi sina taarifa sahihi kwamba lini tutakifungua rasmi lakini naomba nifuatilie na baada ya hapo naweza nikamshirikisha kwenye uvumbuzi wa majibu nitakayokuwa nimeyapata kutoka kwa watendaji wa Wizara yetu.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza niipongeze Serikali kwa mkakati wake wa kusambaza maduka ya dawa sehemu mbalimbali za nchi na nimpongeze Waziri wa Afya na Naibu wake kwa kazi nzuri ya kusimamia maduka haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa swali langu, kumekuwa na kauli ya kuwatia matumaini wazee kwamba wataendelea kupata tiba bure, lakini wazee wengi katika nchi hii hasa wazee wa Jimbo langu la Rombo bado kero ya matibabu ni kubwa sana kwao.
Ni lini Serikali basi itamaliza kero hii ili wazee waliotumikia nchi hii kwa shida sana waweze walau kumaliza maisha yao hapa duniani wakiwa na matumaini kwamba wanapendwa na Serikali pamoja na wananchi ambao wamekuwa wakiwahudumia miaka yao yote?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi tu nimshukuru Mheshimiwa Joseph Roman Selasini, Mbunge wa Rombo kwa swali lake kuhusu wazee na nimhakikishie tu kwamba Serikali yetu ya Awamu ya Tano kwa mara ya kwanza inaweka commitment kubwa sana kwenye masuala yote yanayohusu mambo ya wazee na ndiyo maana katika ngazi ya kitaifa Mheshimiwa Rais mwenyewe ametengeneza Wizara ndani yake ameweka mahsusi portfolio inayohusu mambo ya wazee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la wazee tuna vipaumbele sana sana cha kwanza ikiwa ni kwenye eneo hili la afya ambapo tunashukuru kwamba Sera ya Afya ya mwaka 2007 inatoa msamaha wa matibabu kwa wazee wote wenye miaka 60 (ambao hawana uwezo). Ili kutekeleza hilo, nakubali kumekuwa na changamoto kadhaa lakini kwa sasa tumeweka utaratibu wa kuzitaka Halmashauri zote ziweze kuwakatia kadi ya CHF wazee kuanzia mwezi wa 12. Kwa hiyo, Halmashauri zimeanza ku-respond na nikuombe na wewe kwenye Halmashauri yako uhamasishe wenzako kwenye Baraza lenu muweze kuwakatia kadi za CHF wazee ili waondokane na adha hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na mkakati huo, tumesema mzee kwanza na wazee wenyewe wanafurahi sana, juzi nimetoka kwenye mkutano wa wazee wanafurahi sana kwamba Serikali hii inawapa kipaumbele na kweli hospitali zote nchi zimeweka kibao kwamba mzee apite kabla ya mtu mwingine na hilo linatekelezeka. Kwa hiyo, tuendelee tu kwa pamoja kutekeleza mikakati hii.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na juhudi nzuri za Serikali, takwimu zinaonyesha kuwa, asilimia 60 ya wagonjwa wanaohudumiwa Hospitali ya Ocean Road wanatoka Kanda ya Ziwa, lakini katika huduma zinazotolewa kwa sasa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando zipo changamoto kubwa ikiwemo uhaba wa fedha wakati wa ku-service ile mashine. Hospitali yenyewe haijitoshelezi na kusababisha huduma hiyo kusitishwa wakisubiri fedha na kuendelea kuleta usumbufu kwa wagonjwa katika Hospitali ya Ocean Road. Je, Serikali haioni haja ya kupeleka ruzuku ya kutosha katika kitengo cha saratani kilichopo Bugando?
Swali langu la pili, tafiti zinaonesha kuwa maji yaliyoachwa kwenye gari lililopo kwenye jua na yakakaa kwa muda mrefu katika vyombo vya plastiki inaonyesha inapopata joto kuna chemical zinatoka kwenye plastiki aina ya dioxin ambazo zinaonyesha kuna uwezekano wa kupata saratani hususani saratani ya matiti. Je, Wizara ina mikakati gani ya kutoa elimu kwa wananchi?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII (K.n.y. WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO):
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwanza kuhusu ruzuku kuongezwa kwa ajili ya kituo cha tiba ya saratani kilichopo Kanda ya Ziwa kwa maana ya Hospitali ya Rufaa ya Bugando ndiyo kwanza kimeanza kufanya kazi, kwa hiyo, tunatarajia uwepo wa changamoto mbalimbali ambazo zitajitokeza mpaka pale ambapo kita-stabilize. Kwa hivyo, ninaomba niichukue hii kama changamoto na tutatazama changamoto hii inasababishwa na nini ili wakati wa mchakato wa bajeti inayokuja, tuone ni kwa kiasi gani tunahitaji kuongeza ruzuku kwenye kituo hiki ili kiweze kutoa huduma bora zaidi katika mwaka wa fedha unaokuja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na swali lake la pili ambalo linahusu plastics ambazo zinatumika kuwekea maji ambayo yakikaa kwenye jua kwa muda mrefu inasemekana yanaweza yakasababisha saratani, hili ni jambo ambalo limekuwa likisemwa kwenye mitandao mara nyingi lakini halina ukweli wowote ule na naomba niwatoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge pamoja na wananchi wote kwamba Serikali iko makini na haiwezi kuruhusu kitu chochote kile ambacho kinauzwa kwa ajili ya matumizi ya binadamu na kikawa na madhara kikaingia kwenye soko, kwa sababu tunafanya uchunguzi pia tunafanya udhibiti wa bidhaa zote ambazo zinaenda kutumika kwa wananchi kupitia taasisi yetu ya Tanzania Foods and Drugs Authority (TFDA) - (Mamlaka ya Chakula na Dawa) ambapo mambo yote haya yakisemwa ama yakizungumzwa kwenye jamii huwa tunayafanyia utafiti wa kimaabara na hatimaye kuthibitisha kama yana ukweli ama hayana ukweli ndani yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili analolisema Mheshimiwa Komanya tulikwishalifanyia kazi na tukabaini ni uzushi na halina ukweli wowote ule na kwa hivyo hakuna sababu ya kuendelea kuwatia wasiwasi wananchi.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.
Hospitali ya Ocean Road ambayo ndiyo maarufu na inafanya kazi kubwa ya kuhudumia wagonjwa hawa wa saratani ndiyo hospitali ya siku nyingi na miundombinu yake pia ni ya kizamani lakini idadi ya wanaopata huduma hapo imeongezeka maradufu. Mbali na hayo hospitali ile haifikiki kirahisi kwa sababu iko pembeni na vituo au barabara za usafiri wa umma kwa maana ya daladala. Hivyo, wananchi wanatakiwa kutembea umbali mrefu kwa zaidi ya kilometa moja kufika hospitalini pale umbali huu si rafiki kwa mgonjwa au watu wanopeleka wagonjwa hospitali. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga hospitali nyingine kubwa ya kisasa jijini Dar es Salaam ili kuzihamisha huduma hizi za magonjwa ya saratani ziweze kufanyika katika kituo kimoja kikubwa na cha kisasa?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII (K.n.y. WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO):
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hatuna mpango kwa kweli wa kujenga kituo kingine cha kutoa tiba ya saratani katika Jiji la Dar es Salaam, kwa sababu kituo cha Ocean Road kinajitosheleza na kinajitosheleza kwa maana ya kutoa huduma kwa Kanda nzima ya Mashariki na hata wagonjwa wanaotokea Kanda ya Kati wanaweza wakapata huduma zao pale Ocean Road.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ni moja kituo kile hakipaswi kuwa kama hospitali ya kwenda kila siku, kile kituo ni kituo cha rufaa. Kwa sasa kilikuwa ni kituo pekee cha rufaa cha Kitaifa lakini kwakuwa toka tumeingia Awamu ya Tano tumeanzisha utaratibu wa kufungua vituo vingine kwenye satelites/kwenye Kanda zote kwa maana ya Kanda ya Kusini pale Mbeya, Kanda ya Ziwa pale Bugando na Kanda ya Kaskazini pale KCMC ndio maana sasa tunakichukulia kituo hiki cha Ocean Road kama cha Kanda hii ya Mashariki na Kanda zozote zilizo karibu na Dar es Salaam.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma ile ya saratani inayotolewa pale ni ya rufaa ni huduma ya ngazi ya juu kabisa, kwa hivyo kwa vyovyote vile hatuwezi kusambaza huduma hizi kila sehemu kwamba tuweke na upande mwingine, hapana. Hospitali kubwa zipo nyingi Dar es Salaam ikiwemo ile mpya ya Mloganzila ambayo itatoa huduma nyingine zozote pembeni lakini siyo huduma za saratani kwa sababu gharama za kuanzisha kituo cha saratani ni kubwa sana. (Makofi)
niulize maswali mawili madogo ya nyongeza, lakini kabla ya hayo kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Afya, Dada yangu na Shemeji yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu pamoja na Naibu wake, pamoja na Wizara nzima kwa hatua za haraka walizochukua baada ya ugonjwa wa hatari kuibuka kule Wilayani Chemba, kwa kweli nawashukuru sana na wanafanya kazi yao vizuri sana.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, bei ya dawa za binadamu hasa kwenye maduka ya watu binafsi imekuwa ni kubwa mno, kiasi kwamba watu wenye kipato cha chini wanashindwa kumudu gharama. Je, chombo hicho cha kudhibiti dawa kitaundwa lini?
Swali la pili, katika maduka mengi ya dawa, hasa vijijini dawa nyingi hazina ubora, lakini nyingi zinauzwa zikiwa tayari muda wake wa matumizi umekwisha na inawezekana wananchi wetu wengi wanatumia dawa hizi zikiwa tayari zime-expire. Je, Serikali hili inaliona? Kama inaliona inachukua hatua gani?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika nakushukuru. Kwanza nimpe pole kwa kupatwa na madhila ya ungonjwa wa hatari ambao ume-claim maisha ya watu kwenye Jimbo lake, lakini Serikali inaendelea kulifanyia kazi suala hilo kama ambavyo yeye mwenyewe amesema.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza ni lini chombo hicho kitaanzishwa, bado tuko kwenye mchakato wa kutazama aina ya chombo ambacho tunakihitaji na namna ambavyo kitafanya kazi na pindi tutakapokamilisha utaratibu huo wa muundo wa chombo chenyewe na majukumu ya chombo hicho, kwamba yatakuwa ni yapi, ndipo tutaweza kusema ni lini chombo hicho kitaanza kufanya kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi zilizoendelea zina vyombo vya namna hiyo, kutokana na mifumo ya ku-finance mfumo wa afya kwa ujumla, zinaitwa health technology assessment na zinakuwa chini ya Wizara ya Afya, na sisi tumeona tuanzishe chombo kama hicho. Hivyo lini ni pale ambapo tutakamilisha utaratibu wa ndani wa utafiti kwamba tunahitaji chombo cha namna gani, chenye muundo upi na majukumu yapi.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, kwamba dawa saa nyingine zinakuwa zime-expire muda wake. Hili sidhani kama linaweza likajitokeza kwa kiasi kikubwa kwenye nchi yetu; kwa sababu Mamlaka ya Chakula na Dawa wakishirikiana na Kitengo cha Ukaguzi, kilichopo chini ya Wizara ya Afya, pia wakifanya kazi kwa ukaribu na Baraza la Madawa (Pharmacy Council) kwa ujumla wake, huwa tunafanya ukaguzi wa kushtukiza na pia tunafanya ukaguzi maalum wa Taasisi zote ambazo zinauza dawa ama zinatoa huduma za afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukaguzi ule tunaweza kubaini ni dawa kiasi gani zime-expire na nani anayeuza dawa ambazo zime-expire na huwa zinawekwa chini na zinawekwa sehemu maalum na zinakuwa labelled kwamba zime-expire. Kwa maana hiyo haziwezi kuuzwa kwa wananchi. Kwa maana nyingine ni kwamba dawa ambayo shelf life yake ime-expire haiwezi kuwepo kwenye shelf.
MHE. MARTHA J. UMBULLA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa vifo vya wanawake wanapokwenda kujifungua katika mikoa yetu tunaposomewa, kwenye RCC bado iko juu sana na tena kwa muda mrefu sasa na hii ni kutokana na kukosa vifaa tiba, vitendanishi na huduma stahiki kwa ajili ya kujifungua. Je, sambamba na ukarabati wa zahanati na vituo vya afya sasa hivi kama mkakati wa Serikali, nini kauli ya Serikali hasa kutokana na vifo hivi, takwimu hizi ambazo zipo kwa muda mrefu, mama kwenda kujifungua anafariki?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwenye Bajeti ya mwaka huu ambapo tumetenga takribani shilingi bilioni 183, mahsusi kwa ajili ya kununua dawa na vifaatiba, nina hakika kwenye mwaka huu wa utekelezaji utakaoanza Julai Mosi, mambo yatabadilika sana kwenye sekta ya afya, hususan kwenye eneo la dawa, vifaa, vifaatiba na vitendanishi na hivyo nimtoe shaka Mheshimiwa Umbulla.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ujumla wake niseme tu kwamba matatizo na changamoto ambazo zinawapata akinamama wajawazito na watoto, kipindi kile cha puerperium cha kujifungua na cha kunyonyesha, yatatatuliwa tu endapo tutafanya mabadiliko makubwa kwenye mfumo mzima wa afya, hususani kuwekeza zaidi kwenye mfumo wa afya ya msingi, kwa maana ya kuziwezesha zahanati na vituo vya afya ziweze kufanya kazi ipasavyo.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa matatizo ya bei za dawa yanaonekana yako maeneo ya mengi na kwa sababu tayari Serikali kupitia Wizara ya Afya imeanzisha maduka ya madawa MSD kwenye Hospitali zetu za Mkoa. Je, Serikali ina mpango gani sasa kupeleka maduka haya kwenye hospitali za Wilaya, kwa sababu ndiko kwenye watu wengi zaidi, lakini pia inaonekana ndiyo maduka yanayosaidia zaidi kwa dawa za gharama nafuu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, majibu ya swali la Mheshimiwa Mbunge ni kwamba, sisi kama Wizara ya Afya na Taasisi yetu ya Bohari ya Taifa ya Dawa, hatuna jukumu la kuuza dawa moja kwa moja kwa wateja kwa mujibu wa sheria iliyopo na kwa maana hiyo tumefuata maelekezo ya Kiongozi Mkuu wa nchi yetu kufungua maduka ya mfano katika Hospitali ya Taifa na Hospitali za Kanda na tutaishia hapo, naomba hili kwanza lieleweke.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mkakati wa kuyawezesha maduka ya Mikoa na Wilaya, ambayo yatatamani kuwa na maduka yanayofanana na yale ya MSD Community Outlets, kwenye maeneo yao, lakini yale maduka watayamiliki wao, watayaendesha wao. Sisi tutawasaidia ufundi (technical expertise), tutawasaidia namna ya kuyajenga, kuyakarabati kwamba yanatakiwa yakae vipi, tutawasaidia mifumo ya computer kwa ajili ya kuendeshea biashara hiyo ya kuuza dawa; na tutawasaidia expertise kwamba wafanyeje customer care yao ili yafanane kutoa huduma katika mfumo ule ambao tunatoa kwenye maduka ya MSD Community Outlets. Hata hivyo, chanzo hiki cha mapato kizuri na cha uhakika kwenye hospitali za Wilaya, hatuwezi kukiondoa kwenye hospitali za Wilaya tukakileta Serikali Kuu.
MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona, Mheshimiwa Waziri, katika gazeti la Mwananchi la leo imeandikwa kwamba dawa zote zinazotakiwa wagonjwa wapate kuanzia leo au kuanzia mwaka huu zitakuwa zinalipiwa. Sasa tunatambua kwamba kuna mpango wa Serikali hasa katika dawa za watu wenye UKIMWI, Kifua Kikuu na baadhi ya magonjwa, kwamba dawa hizi zinatolewa bure. Sasa nataka Mheshimiwa Waziri atuambie; je, hizi taarifa zilizotolewa leo kwenye gazeti ni za kweli? Kwanza, lakini pili kama zina ukweli ni dawa gani ambazo kuanzia sasa zitakuwa zinachajiwa, kwa maana ya kutoa pesa na dawa gani ambazo zitakuwa bure? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimtoe shaka yeye, Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwa ujumla kwamba pengine gazeti hilo litakuwa limekosea tu, limefanya misconception ya kilichosemwa pale Muhimbili. Sijalisoma binafsi, lakini kama Naibu Waziri kwenye Wizara ambayo inasimamia utekelezaji wa Sera ya Afya natoa maelezo yafuatayo:-
Kwamba hatujabadilisha sera ya kuwahudumia Watanzania kwenye eneo la kugharamia dawa. Kwa maana hiyo utaratibu ni ule ule, hakuna dawa za UKIMWI zitakazouzwa, hakuna dawa za Kifua Kikuu zitakazouzwa, hakuna mama mjamzito wala mtoto mwenye umri chini ya miaka mitano ama mzee mwenye umri zaidi ya 60 atakayeuziwa dawa, hiyo ndiyo Sera ya Afya kwenye mambo ya gharama. Kwa hiyo, kama gazeti limeandika hivyo pengine limem-miss quote aliyekuwa ametoa kauli inayofanana na kitu cha namna hiyo, hii ndiyo kauli ya Serikali.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nataka kuongeza nguvu kwamba tutaitaka, maana maneno hayo yameandikwa kwenye gazeti la leo la Mwananchi, kwa hiyo tutaitaka Muhimbili ituletee maelezo rasmi. Kwa sababu sera yetu kama alivyosema Naibu Waziri dawa ni bure kwa magonjwa ya UKIMWI, Kifua Kikuu na magonjwa yale ambayo yamesamehewa kwa mujibu wa sera. Kwa hiyo, nikitoka hapa tunatoa maelekezo kwa Muhimbili watuletee maelekezo rasmi na tutarudisha mrejesho hapa Bungeni.
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Kulelea Watoto Wenye Ulemavu Shule ya Mgeza Mseto, Bukoba Mjini na Kituo cha Kulelea Wazee cha Ibosa cha Bukoba Vijijini hawajapata matibabu bure kama Sera ya Serikali inavyosema. Je, Serikali inasema nini kurekebisha dosari hii? Hilo ni la kwanza.
La pili, katika mapambano ya VVU na UKIMWI, sisi Waheshimiwa Wabunge tulipitisha hapa sheria ya mapambano haya na tukatoa adhabu ambayo kwa wale wanaoeneza VVU na UKIMWI kutakuwa na adhabu maalum. Katika hili Serikali hadi sasa haijaweza kufuatilia kwa makini kuwagundua wale wanaoeneza VVU na UKIMWI kwa makusudi na mpaka sasa Serikali haijaweza kudhibiti hali hii kwa kutoa adhabu kali kwa wanaohusika. Je, Serikali kwa sasa inasema nini juu ya kudhibiti tatizo hili ambalo bado kuna watu wanaeneza UKIMWI kwa makusudi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Kituo cha Watoto pamoja na kile cha Wazee cha Bukoba Vijijini kwamba kuna dosari ya matibabu kwamba wazee hawapati, naomba niwafahamishe Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwa ujumla wanaonisikia kwamba huduma kwa wazee wasio na uwezo kwa mujibu wa Sera ya Afya ya mwaka 2007 ni bure and this comes automatic. Hii ni automatic, wala haina mjadala.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, kama ni mzee na hajiwezi, sera imempa msamaha automatically. Kwa hiyo, ni yeye sasa mzee kwenda kuidai huduma hiyo kwenye Kituo cha Afya ambacho anakwenda na ninakuhakikishia hawezi kudaiwa gharama za matibabu na kama ikitokea amegharamia pengine bila kujua ama pengine kwa kukosea ama yeye mwenyewe hakutaja umri wake vizuri, basi anaweza akalalamika kwenye mamlaka mbalimbali na mamlaka ya haraka kabisa ya kufikisha malalamiko hayo, ni kwa Afisa Ustawi wa Jamii ambaye anakuwepo kwenye hospitali hiyo. Kwa mfano, kama ni kwenye Wilaya, kila Hospitali ya Wilaya nchini ina Afisa Ustawi wa Jamii (Social Welfare Officer), lakini pia kila Halmashauri ina Ofisi ya Maafisa Ustawi wa Jamii na Maafisa Maendeleo ya Jamii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kama mtu anataka kuidai haki yake kwenye sekta ya afya, anaweza akawaona hao Maofisa na watamsaidia na hata kama amedaiwa naye anajua kwamba sera inampa msamaha, anaweza akaenda kwenye ile ofisi ya pale Wilayani akaomba apewe barua ya msamaha. Atapewa barua yake ya msamaha, atakwenda kwenye kituo chochote kile hapa nchini na atapata huduma hizo bure. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kuna watu wanaambukiza virusi vya UKIMWI kwa makusudi kwamba Serikali haijafuatilia; hapana. Bunge hapa tukishatunga sheria tukaiweka kwamba imekuwa ni sheria sasa katika nchi hii, ku-enforce kuna pande mbili zinazohusika na kuna ya tatu ambayo inaaangalia pande hizo mbili, pande ya mlalamikaji, pande ya mlalamikiwa lakini pia kuna wanaosikiliza mashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kama kuna mtu anahisi kwamba ameshuhudia mtu ambaye ameambukiza virusi vya UKIMWI kwa makusudi na anamfahamu, ni vyema mtu huyo akaenda ku-report kwenye mamlaka zinazohusika na usimamizi na ufuatiliaji wa utekelezaji wa sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya ku-report, sasa Serikali itachukua hatua, lakini kusema sisi tuanze kufuatilia, kuwatafuta watu wanaoambukiza virusi vya UKIMWI watu wengine kwa makusudi, itakuwa ni suala gumu sana. (Makofi)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri, lakini nataka kusisitiza jambo moja, Mheshimiwa Naibu Waziri alisema kwamba ni wajibu wa Halmashauri kuwapa wazee barua za matibabu bure, nilishaelekeza. Siyo kila siku mzee anapoumwa apewe barua. Halmashauri zinatakiwa kuwapa wazee wote wasio na uwezo vitambulisho vya matibabu bure.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilishasema kwamba itakapofika tarehe 30 Desemba, wazee wote wasio na uwezo wapewe vitambulisho vya matibabu bure. Otherwise hatuwatendei haki wazee, kila siku akiumwa anakwenda kwa Mtendaji wa Kata apewe barua. Kwa hiyo, tunataka vitambulisho vya matibabu bure na Halmashauri kama za Kasulu, Mbarali na Shinyanga Vijijini zinafanya vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimeona nitumie Bunge lako kusisitiza Halmashauri zote, Wakurugenzi wote kuwapa wazee wasio na uwezo vitambulisho vya matibabu bure ili wanapokwenda kwenye Vituo vya Afya waweze kupata matibabu bila usumbufu wowote. (Makofi). Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. MOHAMED R. CHUACHUA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa matibabu ya wazee yamekuwa siyo ya uhakika sana katika Zahanati zetu, katika Vituo vya Afya na Hospitali za Serikali.
Je, Serikali haioni sasa uwe wakati muafaka wa kufanya sensa na kuwapa Bima za Afya hawa wazee ili waweze kupata matibabu haya bure? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilishaliona hilo siku nyingi na jana nilipokuwa najibu maswali mengine nilieleza suala hili kwa mapana sana. Kwa sasa sera tu imetamka kwamba wazee wasiojiweza, maana yake siyo tu wazee wote, wazee wasiojiweza ndiyo wanaopaswa kupewa msamaha kwa mujibu wa Sera ya Afya ya 2007.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tamko la sera lipo, utekelezaji wake unahitaji sheria za ku-enforce lakini pia taratibu za namna ya kulitekeleza. Zamani huo utaratibu nilioueleza awali ndiyo ulikuwepo kwamba Maafisa wa Ustawi wa Jamii kwenye vituo wakishathibitisha kwamba mtu ni mzee, wanampa msamaha, wanagonga mhuri anapata huduma zote bure na katika hospitali zote hapa nchini. Mwezi Desemba mwaka jana Waziri wa Afya akatoa hilo agizo analolizungumzia hapa kwamba sasa wazee wapewe vitambulisho na Halmashauri zote. Baadaye tumeliboresha hilo agizo kwamba sasa kila mzee kwenye kila Halmashauri ambaye ana-qualify kupata msamaha alipiwe kadi ya CHF na Halmashauri yake ili anapoenda kutafuta huduma za afya azipate kiurahisi bila unyanyapaa wa aina yoyote. (Makofi)
Mheshimwia Naibu Spika, kwa hivyo, tunakoelekea ndiyo huko anakozungumzia Mheshimiwa Dkt. Rashid Chuachua kwamba tutakapotunga Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote ambayo ni ya lazima yaani Comprehensive Single National Health Insurance which is compulsory for every one ndipo sasa tutatengeneza utaratibu ndani ya sheria hiyo hapa Bungeni kwa mapendekezo yetu sisi ambapo wazee na makundi yote yanayopewa msamaha wa kupata huduma za afya basi wakatiwe kadi za Bima ya Afya na Serikali. Utaratibu wa kupata pesa kwa ajili ya kuwakatia hizo kadi za Bima ya Afya utatengenezwa kwenye sheria hiyo. Nadhani nimelijibu comprehensive. (Makofi)
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya matibabu kwa magonjwa ya UKIMWI na TB yanafanana sana na magonjwa ambayo yameibuka siku hizi, yale ambayo yanatokana na mtindo wa maisha hususani kisukari na shinikizo la juu la damu. Nataka kujua Serikali ina mpango gani wa kutoa ruzuku kwenye dawa za magonjwa hayo kwa sababu mgonjwa akishapata ugonjwa huo ataendelea kutumia dawa hizo mpaka mwisho wa maisha yake. Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa ruzuku au kutoa bure kabisa dawa za magonjwa hayo? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Chikota kwa kupunguza kitambi chake yeye mwenyewe. Kwa sababu alipokuja hapa alikuwa ana kitambi kirefu, lakini kadri siku zinavyoenda kitambi kimepungua. Sijui kama ni kwa changamoto za Ubunge ama ni kwa mazoezi makali anayoyafanya kwenye viwanja vya Jamhuri. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili nitoe rai kwa Waheshimiwa Wabunge wote ambao hawajajiunga na timu ya Mheshimiwa Ngeleja wafanye hivyo haraka kwa sababu wanatupunguzia gharama za matibabu ya magonjwa yasiyoambukiza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tuna mikakati ya kitaifa ambayo tumeizindua, Mheshimiwa Makamu wa Rais alituzindulia mwaka jana mwezi Desemba na nchi nzima sasa hivi kuna siku ya mazoezi kila mwezi na inafanya vizuri sana. Kwenye Serikali, tiba kwa magonjwa yote chronic yakiwemo magonjwa hayo yasiyoambukiza na magonjwa mbalimbali ambayo yanatokana na magonjwa yasiyoambukiza ni bure kwa mujibu wa Sera ya Afya.
Kwa hivyo, ukiugua ugonjwa wa hypertension ama waswahili tunapenda kuita pressure, kisukari na saratani unatibiwa bure kwa mujibu wa sera, kwa sababu magonjwa yote sugu ama chronic illnesses kwa mujibu wa Sera ya Afya ya mwaka 2007 yanapaswa kutibiwa bure kwa gharama za Serikali. Kwa hivyo, hakuna gharama yoyote kwenye matibabu ya magonjwa haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto inakuja pale unapoenda kwenye kituo cha kutolea huduma za afya kukawa hakuna baadhi ya dawa ambazo unazihitaji. Pale wenye kituo wanakuwa hawana namna zaidi ya kukuambia uende ukanunue mwenyewe kwenye private pharmacies. Hata hivyo, kwa mujibu wa sera matibabu ya magonjwa haya ni bure na tumeendelea kuboresha huduma zetu ili kama tutafikia uwezo wa kuwa na dawa zote ambazo watu wanazihitaji basi waweze kuzipata huduma hizo bure. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nisisahau kukupongeza wewe mwenyewe Mheshimiwa Naibu Spika kwa kuamka kila siku asubuhi kwenda kushiriki mazoezi pale Jamhuri. Pia nikupongeze kwa ku-keep figure yako kuwa ya kiingereza (english figure). Nasema haya kuwatia moyo Waheshimiwa Wabunge wengi zaidi waweze kutamani kuwa na figure ndogo kama ya Mheshimiwa Naibu Spika. (Kicheko/ Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sera ya Serikali ni kuhakikisha kwamba Wazee wanapata matibabu bure na Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya afya na Naibu wake, wamesisitiza kwamba Wakurugenzi waendelee kutoa kadi za Bima ya Afya kwa wazee wasiojiweza ili waweze kupata matibabu lakini hawa wazee kupewa Kadi ya Bima ya Afya tu siyo dawa tosha, endapo kama vituo vya afya watakavyokuwa wanaenda kutibiwa hawatapata dawa na vifaa tiba.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba inamaliza kabisa tatizo la upungufu wa dawa pamoja na vifaa tiba ili wazee hawa waepukane na kadhia ambayo wanaipata pindi wanapokwenda kutibiwa katika vituo vya afya katika Mkoa wote wa Ruvuma?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, mikakati ya kutosha tunayo ya kuhakikisha tunaboresha huduma za afya nchini. Tuna mkakati wa miaka mitano wa kutoa huduma za afya nchini yaani Health Sector Strategic Plan 2015-2020) na mle ndani tumeelekeza kila kitu. Kwa bahati mbaya sana hatuna uwezo tu wa kiuchumi wa kuweza kuutekeleza mpango ule kwa asilimia mia lakini tunajitahidi. Kwa mfano kwenye ule mpango, tungetakiwa kwa mwaka kwenye bajeti ya afya peke yake tutenge shilingi trilioni 4.5 ambayo imeandikwa katika ule mpango mkakati wa afya wa miaka mitano lakini sisi tuna uwezo wa kutenga shilingi trilioni 2.2. Kwa hivyo, lazima utaona kutakuwa na upungufu tu kwa sababu kadri tulivyotazama mbele kama nchi hatujaweza kufikia pale ambapo tunatamani kufika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie tu kwamba tuna suluhu ambayo ni kuanzisha Bima ya Afya ya lazima kwa kila Mtanzania. Kwa sababu Bima ya Afya ya lazima kwa kila mtu maana yake ni kwamba kila mtu atakuwa amechangia kiasi fulani kwenye mfuko wa kutolea huduma za afya lakini siyo watu wote watakaougua maana yeke zile pesa ambazo kila mmoja wetu amechangia zitakwenda kuwahudumia wale wachache miongoni mwetu ambao kwa bahati mbaya watakuwa wamepata madhira ya kuugua. Kwa hivyo, kadri ambavyo tutakapoleta mapendekezo ya sheria hapa na Mungu akajalia ikapita basi tunakoelekea pengine ni pazuri zaidi kuliko tunapotoka. (Makofi)
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, pamoja na majibu hayo ya Mheshimiwa Naibu Waziri na amekiri kabisa kwamba TFDA wanashindwa kukusanya wenyewe kwa sababu ya changamoto ya rasilimali watu pamoja na vitendea kazi vingine na Halmashauri inakwenda kukusanya tozo hizo kwa kutumia rasilimali watu zake, magari yake na muda lakini mwisho inapata asilimia 40 na yule ambaye amekaa tu maana ya TFDA anapata asilimia 60. Je, Serikali haioni kwamba kuna umuhimu sasa wa kubadilisha Halmashauri ibaki na asilimia 60 na TFDA apate asilimia 40? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kumekuwa na tabia chafu kati ya wanaouza na kuzalisha vyakula kwa maana vyakula vinapokuwa vinakaribia kumaliza muda wake wa matumizi, wanakwenda kuwauzia kwa nusu hasara watu wenye migahawa au hoteli ili waweze kuvitumia. Ndiyo maana imekuwa ni kawaida sasa kusikia mtu amekula sehemu fulani na amepata food poison, kwa sababu vyakula vinavyotumika kwa maana ya vyakula ghafi vinavyotumika kuandalia vyakula katika hoteli na migahawa mingi vinakuwa ama vime-expire au vimekaribia sana kumaliza ule muda wake wa matumizi. Je, TFDA inafanya jitihada gani kuhakikisha kila chakula ghafi kinachotumika kuandalia chakula hotelini kinakuwa ni salama? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza kuhusu tozo za makusanyo mbalimbali ya ukaguzi, usimamizi wa maeneo ya biashara zinazohusiana na sheria hii niliyoitaja Sura 219, kwa kawaida yanabaki kwenye Halmashauri kwa asilimia 100. Sijui wewe umeitoa wapi hiyo asilimia 60 lakini sheria ninayo hapa nimekuwa naiperuzi tu wakati unauliza swali lako, inasema mapato yote yanayokusanywa kwenye Halmashauri yanabaki kwenye Halmashauri wala hayachukuliwi na TFDA. Kazi ambazo zimekuwa delegated ni pamoja na kukagua groceries, restaurants, bar, mashine za kusaga na kukoboa na fees zote ambazo zinakusanywa zinabaki kwenye Halmashauri zenyewe. Kwa hiyo, wala hakuna cha asilimia fulani kwamba inaenda TFDA, hapana, sheria inasema hivyo, naomba uipitie ukitaka naweza nikakupa ukaitazama.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kuhusu usalama wa malighafi ambazo zinaenda kutengeneza vyakula kwenye restaurants kwamba ni mdogo, hapana, sikubaliani na wewe kwa sababu kiukweli kama kuna mamlaka iko makini katika nchi yetu, ambazo mimi na zifahamu vizuri ni pamoja na Mamlaka ya Chakula, Dawa na Vipondozi. Hawa watu wako makini sana na ni kwa sababu wanajua jukumu lao linahusu afya za Watanzania. Wakivurunda tu wao maana yake vyakula feki ama dawa feki zitaingia nchini na mwisho wa siku Watanzania wataumia na Watanzania wakiumia itakuwa kelele nchi nzima, kila mtu atajua kwamba sehemu fulani kuna chakula fulani kimeingizwa na ni kibovu na kinasababisha madhara kwa Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, kama kuna mamlaka haina compromise ni pamoja na TFDA. Kwa kweli hawana compromise, hata mimi leo nikisema nazalisha juice kuja kunikagua watanikagua kwa umakini wa ajabu na hawatabadilisha matokeo kwa sababu wakibadilisha matokeo tu itajulikana.
Mheshimiwai Naibu Spika, namhhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa usalama wa afya za Watanzania uko kwenye mikono salama ya TFDA. Kama inatokea food poisoning kwenye maeneo wanapouza chakula basi ni aidha uandaaji wa chakula ama uandaaji wa vyombo lakini sio zile ingredients ambazo zimekaguliwa na TFDA.
MHE. MARIA N. KANGOYE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa TFDA imekuwa na ucheleweshaji wa masuala mbalimbali ya kiukaguzi kutokana na ukosefu wa wafanyakazi wa kutosha. Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza wafanyakazi upande wa ukaguzi ndani ya shirika hili?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze yeye mwenyewe binafsi kwa jitihada zake za kijasiriamali anazoendelea nazo, anafanya social entrepreneurship, anakusudia kuleta sanitary pads kwa ajili ya watoto wa kike, mataulo masafi ya kurudia kufua kwa ajili ya watoto wa kike na ameamua badala ya kuya-import basi azalishe hapa nchini. Nakupongeza kwa hilo na naomba nikwambie kwamba sisi kama Serikali tunatambua jitihada zako na tutakuunga mkono kadri ambavyo inafaa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu ucheleweshaji wa vibali, nafahamu kibali chako kilichelewa mpaka ukakata rufaa kwa Waziri lakini ukweli ni kwamba TFDA kuna changamoto za kuwa na maabara chake na kuwa na bidhaa nyingi japokuwa uwezo wetu umekuwa ukiongezwa siku hata siku. Kwa mfano, sasa hivi TFDA tunaongeza uwezo kwa kuongeza maabara kwenye kila kanda hapa nchini. Kwa hiyo, kila mwaka tunatenga bajeti kwa ajili ya kujenga maabara mpya na kuanzisha kituo kwenye kila kanda. Nafahamu sasa hivi kwenye Kanda ya Ziwa tupo katika hatua za mwisho za kufungua huduma zetu pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, kadri tunavyozidi kutanua wigo wetu wa kuwafikia wananchi ndivyo ambavyo tutazidi kuongeza kasi ya kuwahudumia wateja wetu. Kwa msingi huo, huo ndiyo mkakati wetu kwamba tunaenda kwenye kanda sasa badala ya kubaki na TFDA makao makuu peke yake lakini changamoto ya kuchelewesha kwa kweli ilikuwepo.
MHE. LUCIA M. MLOWE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Naibu Waziri bado kuna malalamiko makubwa juu ya dawa hizo zilizopitwa na wakati na bado watu wanapata dawa zilizopitwa na wakati. Hapa katika jibu lake amesema kuna watu wanaofuatilia, je, ni nani anaeyefanya monitoring ya Kamati hiyo?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kuna wagonjwa ambao mpaka sasa hivi wanapata matatizo kwa sababu vituo vyao ni mbali, wanatembea umbali mrefu na wengine wanakata tamaa wanaamua kuacha dawa. Je, Serikali ina mkakati gani kuongeza vituo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza nani anayefanya monitoring ya Kamati hiyo. Kwanza hii Kamati ya Dawa ni Kamati ambayo ipo kwenye kila kituo na Kamati hii inahusisha Watumishi kwa maana ya wataalam kwenye kituo husika lakini pia inahusisha wawakilishi wa wananchi ambao wanaingia kwenye Kamati hiyo ili kulinda maslahi ya watumiaji wa huduma za afya kwenye kituo.
Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo, hii ni Kamati shirikishi na ushirikishi wake unaifanya Kamati hii ipate uhalali wa macho ya wananchi kwa sababu wananchi moja kwa moja wamewakilishwa na kwa msingi huo wanajua wanachokipokea na wanashiriki aidha, kwa kusaini ama kwa kushuhudia mtu ambaye anasaini nyaraka hizo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama kuna upungufu wowote ule ambao unaweza kuwa umejitokeza, basi ushiriki wa wananchi kwenye eneo hilo utakuwa ni mdogo. Nitoe rai kwa Mheshimiwa Mbunge ashiriki yeye pamoja na Baraza la Madiwani kufanya ufuatiliaji wa kazi inayofanywa na Kamati ya Dawa ya kila Kituo na kwa kufanya hivyo tutakuwa tumetimiza wajibu wetu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, jibu letu ni kwamba, wanaofanya Monitoring ni wenye mali, wenye mali ni wanaomiliki Kituo husika na wanaomiliki kituo husika, maana yake ni wananchi na wananchi wamehusishwa humo ndani na wawakilishi wa wananchi, ni wasimamizi wa vituo vyao vyote ndio maana wanaenda kufanya supportive supervision kila mwezi na kuna bajeti kwenye Halmashauri zote nchini ya kufanya hivyo.
Mheshimiwa Spika, swali la pili kuhusu mkakati ya Serikali kuongeza vituo, kwanza kusema umbali ni mrefu sana hapana, kwa sababu toka Alma-Ata declaration hata kabla ya hapo toka Afya kwa wote miaka hiyo ya 70 Serikali imekuwa ikiongeza idadi ya Vituo siku hata siku na mwishoni tumekuja kuweka hili Azimio kwenye Ilani ya Uchaguzi kwamba tutajenga Kituo cha Afya kwenye kila Kata na Zahanati kwenye kila Kijiji ambalo sasa hivi tuko mbioni kutekeleza kwa kiasi fulani.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, uwezo wetu wa kuwa na vituo ambavyo vipo karibu na wananchi umeongezeka sana toka miaka hiyo ambayo naisema ya Azimio la Afya kwa wote la miaka ya 1971 – 1972 na kwamba kuna umbali mrefu, hapana. Sema tumejiongezea malengo, sisi wenyewe tumeongeza target, targets za zamani zilikwishafikiwa na Serikali zilizopita, kwa hiyo tunachokifanya sasa hivi ni kuboresha huduma na kuongeza tena vituo vingi zaidi, lakini hakuna umbali mrefu.
Mheshimiwa Spika, nilitaka kukanusha hilo ili kuweka sawa. Pia mkakati wetu ni huo ambao nimeusema wa kujenga Kituo cha Afya kwenye kila Kata na Zahanati kwenye kila Kijiji.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni muda mrefu sasa wananchi wa Wilaya ya Lushoto hawapati mawasiliano hasa ya redio ya Taifa na hili swali nimekuwa nikiliuliza mara kwa mara.
Je, ni lini Serikali itajenga mitambo hiyo ili wananchi wa Wilaya ya Lushoto waweze kupata taarifa kama ilivyokuwa kwa wananchi wengine waishio mjini?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu kumuomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira swali linalokuja linaongelea masuala ya usikivu wa redio katika nchi ya Tanzania.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Tafsiri hii ni nzuri sana, lakini ni ya kitaalam zaidi. Je, sasa Serikali ina mpango gani kuwaelimisha wananchi juu ya tafsiri hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nimhakikishie tu Mheshimiwa Hija kwamba toka maambukizi ya virusi vya UKIMWI yalipotokea miaka ya mwanzo ya 1980 Serikali pamoja na wadau mbalimbali tumekuwa tukishirikiana kuelimisha wananchi juu ya virusi vya UKIMWI, UKIMWI, magonjwa nyemelezi, lakini pia madhara yanayotokana na UKIMWI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi hiyo imeendelea na imefanyika kwa ufanisi mkubwa na kwa mafanikio makubwa sana. Ndiyo maana leo hii ninavyozungumza hapa, kiwango cha maambukizi ya UKIMWI kimepungua sana mpaka kufikia sasa hivi tuna kiwango kama cha asilimia 4.6 tu (prevalence rate).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msingi huo tuna mafanikio makubwa sana kwenye eneo hili kuliko anavyofikiria. Vile vile tutaendelea kutumia mbinu ambazo tumekuwa tukitumia, lakini pia ubunifu wa taasisi mbalimbali tunazoshirikiana nazo kuweza kuzidisha uelewa wa wananchi juu ya maambukizi ya virusi vya UKIMWI na UKIMWI wenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda tu kwa ufupi nitoe elimu tu kidogo hapa kwamba virusi vya UKIMWI, yaani VVU ama HIV ama kitaalam Human Immunal Deficiency Virus, ni kirusi ambacho kipo katika familia ya retroviridae na viko virusi vingi vinavyosababisha magonjwa mbalimbali yanayosababishwa na virusi hiki nacho kimo katika kundi hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi kinayofanya ni kuingia kwenye chembe chembe ya mwanadamu ya aina ya white blood cell ambayo inahusika na kinga mwilini na kitakaa mle kwa miaka kati ya hiyo mitano mpaka 10 hadi 12 bila kujulikana na baada ya hapo sasa kama mtu alipima atajulikana, lakini kama hakupima, haitajulikana kwamba ana maambukizi. Kuanzia hapo zile cells za kinga zitapungua mwilini na mtu sasa ataanza kuonesha dalili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale mtu anapoanza kuonesha dalili kwamba amepungua kinga mwilini, ndiyo tunasema amepata UKIMWI. Hiyo ndiyo tofauti. Isipokuwa unaweza ukaishi na hicho kirusi kwa muda huo niliousema bila kuonesha dalili; na kwa maana hiyo, utakuwa na kirusi tu, lakini hauna UKIMWI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa UKIMWI maana yake ni ugonjwa unaokuja baada ya kuwa umeambukizwa virusi vya UKIMWI labda miaka mitano ama kumi huko nyuma, kinga ikashuka, sasa ndiyo unaanza kupata UKIMWI na kwa sababu kinga imeshuka, magonjwa ambayo kwa kawaida hayatokei kwenye watu wenye afya, yanaanza kutokea kwako kama magonjwa mbalimbali ya cancer mbalimbali, kama Kaposi’s sarcoma, magonjwa ya kukohoa kama Kifua Kikuu, magonjwa ya kifua kisichopona mara kwa mara; magonjwa ya ngozi kama herpes zoster na vitu vingine. Kwa hiyo, hapo tunasema sasa una UKIMWI.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Wote tunajua kwamba maambukizi ya virusi vya UKIMWI au UKIMWI yanatokana na sababu kubwa ya kuwa na sexual partners wengi; lakini kwa hapa Tanzania na duniani kote inaonekana wanawake ndio wanakuwa wengi kuliko wanaume. Je, Mheshimiwa Waziri anatuambia sababu hasa ni nini? Kwa nini wanawake wanakuwa na maambukizi kuliko wanaume? Je, tatizo ni kwamba wanaume ndio wanawaambukiza zaidi au wanawake wanakosa maadili? Tusaidie kwa hilo.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nitazingatia muda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kwamba wanawake wanaambukizwa zaidi kuliko wanaume; uwiano hauko mbali sana, tofauti ni ndogo, lakini ni kweli kwamba maumbile ya kibaiolojia ya wanawake ni tofauti sana na maumbile ya wanaume. Pia tabia za wanawake kuhusiana na ngono ni tofauti sana na tabia za wanaume kuhusiana na ngono.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanaume wengi wana tabia ya kuchepuka sana na mara nyingi wanaweza wakavitoa virusi nje wakavileta kwenye ndoa zao kwa wanawake ambao wametulia; hilo halibishaniwi. Kwa hiyo, nitoe rai kwa wanaume wenzangu kujipanga sana kwenye eneo hili la kuchepuka, kuachana na michepuko, lakini pia kupima afya zetu, kupima hali zetu lakini pia kupima hali za wenza wetu. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wale Waislamu wenzangu, tunapewa fursa ya kuoa wake hadi wanne; kuliko kuchepuka na watu usiowajua, unawakuta mtaani huko, ni bora ukapima na ukajiridhisha kwamba unayekwenda kumuoa yuko salama, ukatulia na wake zako wanne. (Makofi)
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Je, Serikali ina mikakati gani ya kupunguza maambukizi mapya ya virusi vya UKIMWI katika Jamii? Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Swali lake ni refu kidogo; tuna mikakati gani ya kupunguza maambukizi mapya? Mikakati tuliyonayo ni mingi sana. Mkakati mkubwa wa kwanza ni kinga, kuzuia watu wasipate maambukizi ya UKIMWI kwa kutoa Elimu ya Afya kwa Umma.
Mkakati wa pili, ni tiba ambapo tunatumia zaidi ya kliniki zaidi ya 2000 za CTC (Care and Treatment Clinics) ambazo zimetapakaa nchi nzima mpaka kwenye ngazi za Vituo vya Afya kwa ajili ya kutoa dawa za ART (antiretroviral therapy) dawa za kupunguza makali ya virusi vya UKIMWI, tukiamini kwamba watu ambao wanatumia dawa, wanapungua virulence, wanapungua kiwango ambacho wanaweza wakaambukiza. Kwa hiyo, hata ikitokea bahati mbaya akafanya ngono ambayo siyo protected anaweza asimwambukize partner wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, tuna mkakati wa kuongeza sasa idadi ya watu ambao tunawatibu, kwamba kila atakayepimwa na kubainika na Virusi vya UKIMWI kuanzia Oktoba, 2016 atatibiwa hapo hapo, ataanza kupata dawa za kupunguza makali ya Virusi vya UKIMWI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni mkakati mpya wa kisasa ambapo tumehama sana kwenye mikakati ambayo ipo preventive based tunahamia kwenye treatment based, kwamba badala ya kutoa tu kinga sasa tunatoa tiba zaidi. Kwa kufanya hivi, taratibu tutapunguza maambukizi mapya kwa kiasi kikubwa.
MHE. MGENI JADI KADIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Serikali ilitoa elimu na tamko kuwa wanaume ambao hawajafanyiwa tohara wana maambukizo zaidi. Je, ni Mkoa upi ulioelimika na wanaume wengi kufanya tohara kwa hiari zao ili kuzuia kuambukiza maradhi ya UKIMWI?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni kweli nakubaliana na yeye kwamba kumekuwa kuna makabila mengi nchini ambayo traditionally hawapendi kufanya tohara ya kukata, wana tohara nyingine ambazo wanafanya za elimu na vitu kama hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua hilo na ndiyo maana tumeweka msisitizo sana katika suala hili. Kwenye Country Operational Plan ya mwaka huu tumepewa takribani milioni 526 za Kimarekani na Mfuko wa UKIMWI wa Rais wa Marekani (PEPFAR). Hizo pesa ndani yake pamoja na kuongeza watu 360,000 kwa ajili ya kuwapa dawa za ART lakini pia tutahamasisha na kuimarisha mkakati wetu wa kuwafanyia tohara wanaume katika mikoa ambayo predominantly hawapendi kufanya tohara ya kukata.
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa niulize swali moja la nyongeza. Ugonjwa wa UKIMWI siyo tishio kwa maana ya kuua, tishio kubwa ni magonjwa nyemelezi. Kwa bahati mbaya Serikali imekuwa ikinunua dawa hasa hasa kwa ajili ya kufumbaza Virusi vya UKIMWI aina ya TLA (Tenofovir, Lamivudine na Efavirenz). Je, ni lini Serikali itaanza kununua dawa kwa ajili ya magonjwa nyemelezi (Opportunistic Infections -OI drugs) hasa hasa Azithromycin, Fluconazole na Co- trimoxazole?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inanunua dawa za Opportunistic Infections lakini siyo kwa kiwango ambacho tunanunua dawa hizi za UKIMWI za moja kwa moja kama hizo anazosema Mheshimiwa Mbunge za Tenofovir, Lamivudine, Zidovudine, Efavirenz na nyinginezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na upungufu tulionao sasa hivi tunaboresha kwa ujumla wake mfumo wa kutoa dawa nchini. Kwa hivyo, kadri mfumo wa dawa utakavyoboreka, dawa za kutibu magonjwa nyemelezi pia na zenyewe zitaongezeka kuwepo katika vituo vyetu. Kwa hivyo, ni lini, ni kadri tunavyoendelea kuboresha ndivyo ambavyo tutaendelea kuwa na dawa hizi kwenye vituo vyetu.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, Mwenyezi Mungu akupe wepesi katika siku hii ya leo kwa sababu Wabunge umewafurahisha sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuuliza swali dogo la nyongeza. Mheshimiwa Waziri, kuna watu wanafanya makusudi kabisa kuambukiza wenzao ugonjwa huu. Mtu anajua kama ni muathirika wa UKIMWI lakini anambukiza watu kwa makusudi hata watoto wadogo ambao ni wanafunzi wa vyuo. Je, Serikali ina mikakati gani kwa hawa ambao wanafanya maambukizi ya makusudi kwa wanafunzi wa vyuo na hata kwa ambao hawajaambukizwa maradhi haya? Naomba tamko la Serikali. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Katika Bunge lako Tukufu palitungwa sheria ambayo inatoa adhabu kwa watu ambao wataambukiza wengine Virusi vya UKIMWI kwa makusudi huku wakijua kwamba wana Virusi vya UKIMWI. Kwa hivyo, ili sheria hii iweze kufanya kazi ni watu kuripoti kwamba wameambukizwa Virusi vya UKIMWI kwa makusudi. Watakaporipoti, mkondo wa sheria utafuata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, kwanza watu wenyewe wapime, kwa mfano wewe unazungumzia mabinti, maana yake mabinti wapime wajue hali zao. Wakishajua hali zao hata ikitokea ameambukizwa na mtu ambaye hakupima naye anaweza akasema wewe ndiyo umeniambukiza kwa sababu mimi nilikuwa sina maambukizi. Kwa hivyo, wapime wajue hali zao na waweze kutumia kinga kama hawawezi kuacha kufanya ngono, lakini kama wanaenda kuoana basi wapime kila mtu ajue hali wakate wanaoana ili wasiambukizane bila kujua.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Nina swali dogo la nyongeza. Kwa nini Serikali isiwezeshe lishe kwa kaya duni ambazo zinatumia dawa za kupunguza makali ya UKIMWI?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hatuna mpango wa kuwezesha chakula kwenye kaya duni au kaya yoyote ile. Tunaamini wagonjwa na watu wengine wanapaswa kuhudumiwa na familia zao. Hata hivyo, tunatoa dawa ama kemikali ambazo zina nutritive effect, zina effect ya kuongeza lishe kwenye miili ya wagonjwa wanaotumia dawa hizi. Kwa hiyo, tunawapo multivitamins na dawa nyingine inatosheleza kwa kweli kuhimili mikikimikiki ya ART.
MHE. SAVELINA S. MWIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa ugonjwa wa TB unaenea kwa hewa na sanasana naona Wizara inahamasisha sana watu kujikinga na UKIMWI lakini sijaona wanaweka nguvu sana kwenye ugonjwa wa TB na umeenea kwa kasi sana. Ni lini Serikali itatoa hamasa na kuwajulisha watu ugonjwa wa TB kuwa ni mbaya sana kwa vile huenea kwa hewa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ugonjwa wa Kifua Kikuu ama Tuberculosis unaibuka tu kwenye mwili wa mwanadamu, pale ambapo kinga yake imeshuka. Ndiyo maana sasa unauona upacha wa maambukizi ya Virusi vya UKIMWI, UKIMWI pamoja na Kifua Kikuu, sio kwamba ugonjwa haupo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana hata sisi wazima na tuna afya tuna vimelea vya Mycobacterium tuberculosis kwenye miili yetu lakini havitajionyesha mpaka tutakufa navyo kama hatutoshusha kinga za mwili wetu. Kwa hiyo, kwanza tuepuke maambukizi ya Virusi vya UKIMWI, lakini pili tuwe na tabia ya kupima afya zetu kwa kweli ili tuweze kudhibiti magonjwa kama haya kabla hayajatokea.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mheshimiwa Waziri amesisitiza mara kadhaa kwamba tuwe na desturi ya kupima, ni kitu kizuri kwa sababu UKIMWI bado upo na sometime unaona kama umezoeleka hivi. Ni kwa nini sasa vile vipimo (disposable) haviko kwenye maduka ya dawa ya kawaida ili hayo maelekezo ya Waziri anayoyasema kwamba tuwe na desturi ya kupima iwe rahisi? Kwa sababu yale mambo ya kusema kwamba mtu atazimia ni ya kizamani. Ni vizuri vipimo vya UKIMWI viwe available madukani kama ilivyo kwa vipimo vya sukari, pressure na kadhalika ambavyo viko available madukani. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni swali zuri na nieleze tu kwamba, katika hizi USD milioni 526 tulizopewa na Serikali ya Marekani kwenye mwaka huu wa fedha unaokuja, tumeweka mkakati wa kufanya majaribio ya self-test hiyo unayoisema. Kwa hivyo, tutaanza majaribio hayo, tunakwenda kisayansi, hii siyo blaa-blaa ya siasa mzee, tunakwenda kisayansi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tunafanya majaribio tuone hasara na faida zake, tukijiridhisha kwamba ni kitu ambacho tunaweza tukakifanya ndiyo tuna launch sasa scale up project kwa nchi zima. Kwa hivyo, kwa mwaka huu tunafanya majaribio na ni hatua nzuri kwa sababu zamani tulikuwa hata tunaogopa kuruhusu watu kupimwa bila kuwa na ushauri nasaha kutoka kwa wataalam kwa kuepuka mambo mengine ambayo yangeweza kuibuka.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Nataka kutoa ufafanuzi kwenye swali la nyongeza la Mheshimiwa Khadija Nassir kwamba tuna mikakati gani ya kuzuia maambukizi mapya. Kati ya mkakati mkubwa ambao tumeutekeleza na tunaendelea kutekeleza katika kupunguza maambukizi mapya ya VVU ni kupunguza maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili tumefanikiwa sana, asilimia 92 ya vituo vyetu vya huduma takribani 5,200 vinatoa huduma ya kuzuia maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto. Takribani wanawake zaidi ya asilimia 90 wote wanaohudhuria katika kliniki ambao ni wajawazito wameweza kupata huduma wale ambao wamekutwa na maambukizi. Tumefanikiwa sana Tanzania, kwa sababu ya mkakati huu, tumepunguza maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto kutoka watoto 14,000 hadi watoto 6,500. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, huo ndiyo mkakati mkubwa na niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge katika maeneo yetu, katika majimbo yetu, tuwahimize wanawake wajawazito mara tu wanapojigundua kwamba ni wajawazito waende kliniki lakini pia wapime UKIMWI kwa sababu wataweza kuzaa watoto ambao hawatakuwa na maambukizi ya UKIMWI. Niliona nilisisitize hili. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa Manispaa ya Songea haina Hospitali ya Wilaya lakini pia katika Manispaa ya Songea, wakazi wengi wanategemea Kituo cha Afya cha Mji Mwema na kituo hicho hakina gari la wagonjwa. Je, Serikali ina mpango gani wa kuleta gari kwa ajili ya wagonjwa ili kurahisisha kutoa huduma pamoja na kurekebisha jengo la upasuaji ili kuweza kwenda sawasawa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Serikali ina mkakati gani wa kuweka Kituo cha Damu Salama katika Kituo cha Afya cha Mji Mwema?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Swali la kwanza kuhusu ambulance, kama ambavyo tumekuwa tukisema hapa Bungeni kila siku siyo jukumu la Wizara ya Afya. Kimsingi ni jukumu la Halmashauri husika kwamba katika vituo wanavyovimiliki na wanavyoviendesha, kama kuna mahitaji ya ambulance basi Halmashauri husika iweke katika vipaumbele vyake iweze kununua ambulance hizo na kuzipeleka kwenye vituo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachokifanya sisi Wizara ya Afya na naona sasa kinatuletea shida, tunaomba kwa wahisani watupe ambulance katika maeneo ya kipaumbele kama eneo la kupunguza vifo vya akinamama wajawazito na watoto, tukipata ndiyo tunatawanya kwenye Majimbo na kwenye Halmashauri kadri ambavyo tutaweza kufanya hivyo, lakini sio jukumu letu. Kwa hiyo, natoa rai kwake na kwa Halmashauri zote nchini kuweka kipaumbele cha kununua ambulace katika Halmashauri zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili linahusu damu salama. Mpaka sasa tuna upungufu wa kuwa na vituo vikubwa vya kanda vya damu salama katika mikoa saba nchini, Mikoa ya Geita pamoja na Arusha wameonesha uwezekano wa kujenga vituo vyao wenyewe. Mikoa ambayo imebaki tumeweka kwenye bajeti, mwaka jana tuliweka shilingi bilioni mbili bahati mbaya hatukufanikiwa kukamilisha, mwaka huu pia kwenye bajeti hii tumeweka tena shilingi bilioni mbili. Malengo yetu kwa kweli ni kuhakikisha mikoa hii ukiwemo Mkoa wa Ruvuma pale Songea tunajenga kituo kikubwa cha Damu Salama ili kuokoa Maisha ya Watanzania wenzetu.
MHE. ISSA A. MANGUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Hospitali ya Rangi Tatu, Mbagala ina upungufu mkubwa wa dawa na huwa zinachelewa kuletwa katika hospitali ile. Vilevile tunawadai MSD dawa zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 300. Je, Wizara itatusimamia dawa zile zipatikane ili tuweze kutoa huduma hasa ikizingatiwa tunatoa huduma mpaka maeneo ya Mkoa wa Pwani maeneo ya Mkuranga?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kituo hiki cha Rangi Tatu nakifahamu vizuri kwa sababu mdogo wangu pale ndiyo in charge wa kituo kile, sidhani kama Mheshimiwa Issa anajua, kwa hiyo nafahamu changamoto hiyo na kwamba kina wateja wengi sana, maana yake analalamika halali kwa kufanya kazi kwa bidii kuwahudumia Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakachokifanya, nitafanya kazi kwa ukaribu na Mheshimiwa Mangungu kufuatilia tuone kama kweli wanadai shilingi milioni 300 na kama wanadai basi waweze kupata huduma hiyo ya dawa.
MHE. RAISA ABDALLA MUSSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri wanayotoa Wizara ya Afya mara nyingi wanapoulizwa maswali hapa Bungeni nina swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la msingi ni kwamba kunahitajika vifaa tiba katika hospitali za Serikali. Sasa pamoja na vifaa tiba, kuna kitu muhimu ambacho kinatakiwa na Watanzania katika Hospitali hasa za Serikali nacho ni kauli nzuri ya wahudumu na wafanyakazi katika hospitali za Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimwambie Waziri na Naibu Waziri kwamba suala hili halipatikani katika katika Hospitali zetu za Serikali. Ama ukienda hospitali za binafsi jinsi wanavyofanya biashara zao wanawanyenyekea watu, lakini hospitali hizi za wanyonge hilo halipatikani. Je, Mheshimiwa Waziri anatuambia vipi kuhusu wafanyakazi ambao wanatoa kauli ambazo haziridhishi kwa Watanzania? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza natambua kazi nzuri na kubwa inayofanywa na wataalam wanaotoa huduma kwa watu wetu hapa nchini. Napenda sisi kama viongozi tutambue kazi kubwa wanayoifanya kwa kujitoa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia natambua kuwa kuna baadhi ya wafanyakazi ambao wana changamoto hizo anazozisema Mheshimiwa Raisa kwamba wana lugha mbaya, wanashindwa kuhudumia watu vizuri na customer care ni mbovu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai kwamba wataalam wote kwenye sekta ya afya wale wachache ambao bado hawajabadilika, huu ni wakati wa kubadilika. Kwa sababu kwa kweli tukipata taarifa za mtaalam ambaye amem-treat vibaya mteja wetu huwa tunachukua hatua bila kulaza damu. Kwa hiyo, nitoe rai wasiombe nikawakuta na tuhuma hizi kwa sababu nitawapeleka kwenye Baraza lao la Kitaalam waweze kuchukuliwa hatua za kitaaluma. Ahsante. (Makofi)
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa mimi Mbunge wa Jimbo la Nyang’wale niliweza kujitolea na kujenga zahanati na kuikamilisha katika Kijiji cha Mwamakiliga na kwa kuwa niliweza kujitolea na kujenga wodi mbili na chumba cha kuhifadhia maiti katika Kituo cha Afya ambayo ni Hospitali ya Wilaya ya Nyang’wale, nimeweza kuyafikisha majengo hayo kiwango cha asilimia 75 na nimekwama. Je, Serikali inasaidia vipi sasa kuweza kuifungua ile zahanati ya Mwamakiliga ili iweze kufanya kazi na kukamilisha majengo hayo yaliyo katika Kituo cha Afya Kalumwa ili yaweze kufanya kazi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Hussein Nassoro Amar kwa kujitoa kiasi hicho kwa ajili ya wananchi wa Nyangh’wale. Nimwombee dua Mungu apokee swaumu yake katika Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwa sadaka hiyo kubwa aliyoitoa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimhakikishie kwamba sisi tutakuwa pamoja naye, bahati mbaya sikufika pale Kalumwa wala Mwamakiliga nilipokuja kwenye ziara ya Mkoa wa Geita, lakini baada ya Bunge hili nina ziara tena ya kuzunguka mikoani na nitapita Mkoa wa Geita na mahsusi nitafika kwako na kwa Mheshimiwa Musukuma nina ahadi yangu naikumbuka. Nitakapofika pale, nitaongea na wataalam wale tujue ni nini cha kufanya kwa kushirikiana na wenzetu wa TAMISEMI ili kuweza kuunga mkono jitihada nzuri alizozionyesha. (Makofi)
MHE. DEVOTA M. MINJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona. Matatizo ya afya katika Mkoa wa Songea yanafanana kabisa na matatizo ya afya katika Hospitali ya Mkoa Morogoro ambapo licha ya kazi nzuri inayofanywa na Madaktari katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro lakini hospitali ile inaelemewa na wagonjwa wengi. Kwa mwezi mmoja Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro inatibu zaidi ya wagonjwa 15,000. Je, Serikali haioni sasa kuna haja ya kupeleka vifaa muhimu kama MRI, CT- Scan na X-ray machines za kisasa ili kuwapunguzia mzigo wagonjwa ambao wanalazimika hivi sasa kwenda Muhimbili kwa matibabu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mbunge wa Jimbo la Morogoro Mjini Mheshimiwa Mohamed Abood kwa kazi nzuri anayoifanya kwenye hospitali ile lakini pia kwa kutumia pesa zake za mfukoni kuweza kununua baadhi ya vifaa tiba ambavyo vinatumika katika Hospitali ya Mkoa wa Morogoro. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumwaga sifa hizo kwa Mheshimiwa Abood, naomba nijibu sasa swali la Mheshimiwa Devota Minja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango mkubwa kupitia mradi wake wa ORIO wa kupeleka vifaa tiba kwenye Hospitali za Mikoa nchini, Hospitali za Wilaya na baadhi ya vituo vingine maalum vya kutolea huduma za afya nchini. Mradi huo ulisuasua mwaka jana kwa sababu tulikuwa hatujalipa counterpart funds kwa Serikali ya Netherlands ambao ndiyo wafadhili wa mradi ule. Sasa tumeshaanza kukamilisha sehemu yetu ya fedha ambazo tunapaswa kulipa ili mradi uanze kutekelezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina hakika baada ya miezi mitatu mradi huu utaanza kutekelezwa. Mradi huu ukitekelezwa, tutaweza kupata CT-Scan, MRI, Ultra-sound, digital X-rays na vifaa vingine vingi vya kufanyia uchunguzi wa magonjwa kwa ajili ya hospitali zetu hapa nchini. Sina hakika mgao umekaaje mahsusi na Hospitali ya Rufaa ya Morogoro, lakini naamini kwa vile ni kati ya hospitali kubwa hapa nchini inawezekana ikapata badhi ya vifaa hivi vikubwa ambavyo vinatarajiwa kuja lakini nitaangalia na akipenda nimpe taarifa nitampa baadaye.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante wa majibu ya Serikali athari kubwa ya mgogoro huo ni kijiji cha Kikulyungu kuondolewa kwenye WMA ya Jumuiya ya Magingo na kwa majibu haya inaonekana mgogoro huu umefika mwisho.

(i) Sasa ni lini Serikali itakuja Kikulyungu kuwapa wananchi matokeo ya maamuzi haya na kuwapa kibali au kuwapa kibali au kuwapa hati ili waweze kurudishwa kwenye Jumuiya ya Magingo?

(ii) Na kwa sababu sisi tunaoishi kwenye maeneo ya hifadhi kumekuwa na uharibufu mkubwa sana wa mazao unaotokana na wananyama waharibifu kama tembo, nguruwe, na wananyama wengine waharibu. Na Serikali imekuwa ikitoa kitu kinachoitwa kifuta machozi sasa ni lini Serikali itakuja na marekebisho ya sheria ili badala ya kutoa kifuta machozi iwe wananchi wao wanapata fidia inayotokana na uharibifu wa mazoa ya mashambani?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zuberi Mohamedi Kuchauka Mbunge wa Jimbo la Liwale kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimuahidi kwa kuwa taarifa ya kamati ambayo ilienda kuhakiki mipaka imekamilika na ipo mezani kwangu, kwamba baada ya Bunge hili la Bajeti kuisha aidha nitaenda mwenyewe ama nitamtuma Mheshimiwa Naibu Waziri kwenda kuzungumza na wananchi wa kijiji cha Kikulyungu kwenda kuwapa matokeo ya taarifa ya kazi iliyofanywa na kamati iliyokuwa chini ya uzongozi wa Wizara ya Ardhi ambayo ili hakiki mpaka ule kwa hivyo ni lini baada ya Bunge la Bajeti kumalizika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili kuhusu Serikali kuachana na kulipa kifuata machozi ama pia na kifuta chasho kutokana na uharibifu wa unaofanywa na wanyama wakali na waharibifu badala yake tulipe fidia. Ngumu kwa Serikali kuji-commit kwamba itaanza kulipa fidia ya uhalibifu unaofanywa na wanyama wakali na wanyama waharibifu na sababu zipo wazi. Kwa mfano mnyama amesababisha umauti wa raia wa mwananchi huwezi kusema utalipa fidia ya mnyama kuua mwanadamu kwa sababu thamani ya mwanadamu haiweezi kulinganishwa na kitu chochote kile.

Kwa hivyo, hiyo ni bahati mbaya ambayo inakuwa imetokea tunachoweza kulipa pale ni kufuta machozi na sio fidia. Lakini thamani ya mazao vilevile ni ngumu kusema Serikali itaji- commit kulipa fidia balada ya kufuta jasho kwa sababu changamoto zilizopo ambazo zinahusiana na wanyama hawa kwenda kwenye maeneo ni nyingi wakati mwingine wananchi wanawafuata wanyama kwenye mapito yao ama kwenye mazalia yao ama maeneo ya mtawanyiko na wakati mwingine sisi viongozi tukiwemo Wabunge, madiwani tunahamasisha sana Serikali imege maeneo ya hifadhi ambayo kiuhasili ni lazima yatapitiwa na wanyama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, kusema Serikali itaji-commit kwa kweli kulipa fidia ni jambo gumu kwa sababu gharama itakuwa kubwa sana mwisho wa siku tutashindwa kutunza hizi maliasili ambazo sisi zote tunapaswa kuzilinda kwa mujibu wa katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 27.

Kwa hivyo ninawaomba sana wa kwa Waheshimiwa Wabunge wote na wananchi wote watambue kwamba wanyamapori ni maliasili ya Taifa, ni utajiri, ni urithi wa Taifa letu na hatuwezi kwamwe kuacha kuilinda kwa ajili ya matumizi ya sasa na vizazi vijavyo.
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri, ingawa katika maeneo aliyozungumza kuhudu REGROW hajaeleza kiuwazi kwamba itakuwa ni lini makumbusho yatakuwa yameanza. Nina maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza ni kwamba, wananchi wa Jimbo la Kalenga hasa katika Kata husika ya Kalenga hawanufaiki na chochote kupitia Makumbusho haya ya Mkwawa Mkwavinyika, zaidi wanapata zile fedha ndogo ndogo kupitia watalii ambao wanakuja kununua bagia, maandazi na mbogamboga. Sasa sijui Serikali ina utaratibu gani kuhakikisha kwamba wananchi wa Kalenga hasa katika Kata husika ya Kalenga wananufaika na Makumbusho haya ya Mkwawa Mkwavinyika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni kwamba, kutokana na utaratibu ambao umeanzishwa na Serikali kuhakikisha kwamba tunajenga au kuboresha barabara ya Iringa Mjini kuelekea Ruaha ambayo iko katika utaratibu wa REGROW ningependa kufahamu kupitia Mheshimiwa Waziri kwa sababu Ruaha National Park ni mbuga kubwa katika Bara la Afrika na Tanzania kwa ujumla. Ningependa sasa kufahamu, je, utaratibu wa ujenzi wa barabara hii ambayo inaenda Ruaha National Park ukoje ukizingatia kwamba Wizara ya Ujenzi imeshaeleza kwamba itaijenga barabara hii, lakini vile vile kwa sababu inakidhi mahitaji ya Wizara ya Maliasili, je, kuna mawasiliano yoyote kati ya Wizara hizi mbili kujua barabara hii itaanza kujengwa lini?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajibu maswali mawili ya Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa kwanza niwape salamu Wanayanga wote, kamwene, mnogage.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya salamu hizo kwa Wanayanga, naomba kujibu maswali ya Mheshimiwa Mgimwa kama ifuatavyo:

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza ni kwamba, Mtwa Mkwavinyika Mnyigumba Mwamuyenga ni shujaa wa Taifa, ni alama ya Utanzania wetu na ni miongoni mwa watu mashuhuri ambao sisi watoto wa Tanzania tunajinasibu nao. Pia hawezi kuwa mtu ambaye anaweza kutupa historia inayoleta faida kwa watu wa Kalenga peke yake, kwa hivyo mafanikio yatakayopatikana kutokana na Mtwa Mkwavinyika Mnyigumba kuwa ni Mtwa wa Wahehe na ngome yake kuwa pale Kalenga ni kuvutia watalii kuja katika eneo lile na hiyo multiplier effect anayoizungumza kwamba watalii watalala, watatembelea maeneo mbalimbali, watajifunza historia ya Wahehe, wataacha pesa pale, lakini sio lazima moja kwa moja kwa kuwa Mtwa Mkwavinyika alikuwa wa eneo lile, basi iwe tu ni kwa faida ya watu wa pale, huyu ameshakuwa alama ya Taifa. Kwa hivyo, kinachopatikana kutokana na utalii kinaingia kwenye taasisi za Serikali na wananchi wanafaidika na kodi inayotokana na Sekta ya Utalii kwa ujumla wake na pia wananchi wanafaidika kwa kufanya shughuli mbalimbali ambazo zinaendana na mnyororo mzima wa kazi au shughuli za utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuhusu barabara ya kutoka Iringa kwenda Msembe, ni barabara muhimu sana kiutalii na ni barabara ambayo tunaipa kipaumbele cha hali ya juu katika kuifungua circuit ya Kusini hususan kuitumia Hifadhi ya Taifa ya Ruaha kwa faida zaidi kiutalii. Pia ni barabara ambayo Serikali katika bajeti hii tutakapokuwa tukitoka hapa tuna uhakika itakuwa imepitishwa na katika mikakati yetu ni kwamba tutaanza sisi wenyewe kuijenga barabara hii japokuwa tayari tuna fedha kutoka Benki ya Dunia kwa ajili ya barabara hii kuunganisha pia na Mradi wa Kuboresha Uwanja wa Ndege wa Nduli. Kwenye uwanja wa ndege wa Nduli uliopo pale Iringa tayari Mkandarasi atatangazwa muda si mrefu, tunabaki na hii barabara ya kuunganisha Iringa Mjini na Hifadhi ya Taifa Ruaha kwenye eneo la Msembe. Kwa hivyo, hii barabara naijua vizuri japokuwa mimi sio Waziri wa uchukuzi wala wa Ujenzi kwa sababu ni barabara muhimu sana kiutalii kama anavyosema Mheshimiwa Godfrey Mgimwa.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza. Wananchi wa Urambo wanaoishi karibu na hifadhi za misitu wamekuwa na migogoro ya muda mrefu sana na hata kusababisha kuchomewa nyumba zao na mali zao hasa katika sehemu ya Kata ya Nsenga, Lunyeta, Ukondamoyo na Uyumbu. Je, Serikali inawaambia nini wananchi kuhusu lini watakwenda kutatua na hasa kwa vile ninavyokuwa na imani na Waziri husika. Lini anamaliza matatizo haya ili wananchi wafanye shughuli zao kwa raha?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margareth Simwanza Sitta, Mbunge wa Jimbo la Urambo, mama yangu, kwa ufupi tu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia maelekezo ya Mheshimiwa Rais aliyoyatoa Januari 15, 2019 kwa Mawaziri wa Wizara nane ambazo ni wadau wa migogoro ya ardhi, tumefanyia kazi jambo hilo kuhusiana na Lunyeta na maeneo mengine ya Mkoa wa Tabora na mikoa mingine hapa nchini na kwa sasa siwezi kusema nini itakuwa hatma yake, lakini kazi ya Mawaziri imekamilika na tumepeleka mbele ya meza ya Mheshimiwa Rais, tunasubiri mwongozo. Baada ya hapo Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote kwa ujumla watapata kujua ni nini itakuwa hatma ya ufumbuzi wa migogoro ambayo imedumu kwa muda mrefu kwenye Sekta ya Ardhi na Maliasili.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba nimuulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa, katika historia ya Wahehe, moja ya sifa ni kumpiga Mjerumani na Mjerumani alipigwa katika Kijiji cha Lugalo Iringa na ikasababisha kiongozi wao Zelewisky kupigwa na kaburi lake liko pale. Je, Serikali sasa haioni kwamba kile kilikuwa ni kivutio kizuri tosha mpaka sasa hivi kimetelekezwa kwa miaka yote na Waziri yuko tayari kufika pale?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Venance Mwamoto, kamwene bwana!

Mheshimiwa Mwenyekiti, niko tayari kufika katika eneo hili na wakati wowote muda ukipatikana tunaweza tukachomoka na Mheshimiwa Mwamoto tukaenda kuona eneo hili, lakini kwa ujumla wake tu maeneo yote ya malikale na maeneo ya makumbusho kwa kweli tumeyafanyia mkakati mzuri sana wa kuyaboresha kwa sababu Idara ya Malikale ambayo iko chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii ilikuwa ina uwezo mdogo sana wa kuyasimamia maeneo haya kifedha, kwa hivyo ilikuwa inayaendeleza kidogo kidogo. Kwa kuzingatia umuhimu wa maeneo haya, kihistoria lakini pia kama urithi kwa nchi yetu ambao unapaswa kudumu kwa vizazi na vizazi, tumeamua kuyakabidhi baadhi ya maeneo nyeti ikiwemo eneo la Kalenga na eneo la Isimila kwa taasisi za uhifadhi ambazo zina msuli mkubwa kidogo kifedha kwa mfano TANAPA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano eneo la Kalenga na eneo la Isimila na vivutio vyote vilivyoko Mkoa wa Iringa vya Malikale tumewakabidhi Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) ili waweze kuviendeleza na kuvisimamia.

Kwa hivyo tumegawa maeneo haya kutokana na shirika lipi ambalo lina msuli mkubwa kifedha, liko jirani na maeneo haya. Kwa hivyo, maeneo mengi kwa kweli kwa sasa yataendelezwa yatakuwa na hadhi ya kisasa na yatatoa huduma nzuri zaidi kwa watalii wa ndani na wa nje.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana nina maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nishukuru sana majibu mazuri ya Serikali, naomba tu utekelezaji uwe wa haraka kwa sababu msimu wa mvua karibu unafika. Katika operasheni zao mbalimbali, watu wa Maliasili wa Luafi Game Reserve wamekuwa wakiwafukuza wananchi usiku kwenye Vijiji vya King’ombe, Lundwe, Mlalambo, Kizumbi na Lupata: Je, utaratibu huo hauwezi kubadilika ili operesheni zao wafanye mchana ili sheria zifuate taratibu zake?

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii Mheshimiwa Kigwangalla alipofanya ziara Wilayani kwetu, aliahidi kutoa bati katika Kijiji China katika ujenzi wao wa zahanati: Je, bati hizi zitatolewa lini? (Makofi)
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba nijibu hili la bati, la kwanza atajibu Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Spika, naomba niwasiliane na Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge hili kwisha ili tuweze kuona hatua stahiki za kuchukuliwa ili ahadi hiyo iweze kutekelezwa mara moja. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza nimuhakikishie kwamba kama kuna Askari wetu wa Wanyamapori badala ya kufanya operation mchana anakwenda usiku kufungua nyumba za watu anafanya makosa, maelekezo ambayo ninayatoa hapa ni kwamba operation hizo zifanyike mchana na zisifanyike usiku kwa mujibu wa sheria.(Makofi)
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuwa kumekuwa na mgogoro wa muda mrefu katika Wilaya ya Arumeru katika kijiji cha Ngalinanyuki na hifadhi ya Taifa ya Mumera, na mpaka sasa hivi wananchi wale hawajafikia muafaka wa mgogoro huo.

Je, Serikali sasa ni wakati muafaka wa mimi na Mbunge aliyeapishwa leo na Mheshimiwa Waziri kuongozana mpaka Kijiji cha Ngalinanyuki kwenda kusikiliza wananchi wale ili kero yao ifikie muafaka?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri yaliyotolewa hapa Bungeni na Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kujibu swali na nyongeza na Mheshimiwa Catherine Valentine Magige kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwamba kwanza katika eneo la Arusha National Park ususani katika sehemu hiyo ya Momera hakuna mgogoro per se hakuna mgogoro unaoweza kuita mgogoro. Lakini kwa sababu wananchi walienda mahakamani na walishindwa, kwa hivyo eneo lote lile ambalo walikuwa wanalidai ni eneo la Serikali.

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na malalamiko ya wananchi na pamoja na kwamba wameshinda kesi mahakamani. Serikali imeona ikate sehemu ya eneo la Arusha National Park ambalo lilikuwa ni miongoni mwa mashamba yaliyokuwa ya settlers wa eneo lile ili kuwagaia wananchi waweze kuishi kwa raha na amani zaidi. Kwa hiyo, wakati process hiyo itakapokamilika wananchi wa Momera watapata eneo ambalo tunazungumzia.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kuongozana nae kwenda kutoa maelezo hayo nitaomba aongozane na Mheshimiwa Naibu Waziri baada ya Bunge hili.